United Republic of Tanzania
Parliament of Tanzania
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Job Ndugai amewahamasisha Waheshimiwa Wabunge wote kujiandaa kwa ajili ya kwenda kuipa hamasa Timu ya Taifa wakati wa fainali za Mataifa ya Afrika zinazotarajiwa kuanza mwezi Juni 21 mwaka huu nchini Misri.
Akizungumza Bungeni Mhe. Spika amesema kuwa itakuwa ni jambo la aibu iwapo Wabunge
wa nchi nyingine za Afrika Mashariki ambao timu zao za Taifa zimefuzu
watajitokeza kwa wingi alafu Wabunge kutoka Tanzania wasionekane.
“Ni fusra ya pekee
ambayo haijawahi kutokea kwa hivyo nawaombeni tujitahidi kujiandaa kwenda na
mimi nitaangalia kama kuna uwezekano wa kupunguza baadhi ya gharama ili muweze
kwenda kwa wingi,” alisema Mhe. Spika.
Mhe. Ndugai aliongeza kuwa mawasiliano yanaendelea kufanyika
na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ili iweze kuratibu safari ya
Waheshimiwa Wabunge kwenda huko Misri kwa
kwa ajili ya fainali za AFCON.
“Mpaka sasa inaonekana ukiwa na dola za Kimarekani kuanzia 1,500
unaweza kugharamia safari pamoja na malazi,” alisema Mhe. Spika nakusisitiza
kuwa angependa Wabunge wote waende kwani watapata pia fursa ya kufanya utalii
wakiwa huko nchini Misri
Timu ya Taifa ilifuzu kwenda kucheza fainali za Mataifa ya
Afrika kwa mara ya kwanza baada ya miaka 39 kwa kushika nafasi ya mbili katika
kundi lao mara baada ya kuifunga Uganda magoli 3-0 katika mchezo wake wa
mwisho.
Katika fainali hizo za mataifa ya Afrika Timu ya Taifa imepagwa katika kundi C pamoja na timu za Taifa za Senegal, Algeria na Kenya.