United Republic of Tanzania
Parliament of Tanzania
Mhe. Job Y. Ndugai, (Mb.), Spika wa Bunge amepokea kwa huzuni na masikitiko makubwa taarifa za kifo cha Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kilichotokea tarehe 17 Machi, 2021, Saa 12:00 Jioni katika Hospitali ya Mzena, Jijini Dar es Salaam na kutangazwa na Mhe. Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan.
“Tumempoteza Rais wetu kipenzi aliyejitoa kuwatumikia Watanzania wote kwa uadilifu, umahiri, bidii na moyo wa uzalendo wa hali ya juu. Kwa niaba ya Bunge, natoa pole kwa Mama Janeth Magufuli na familia ya marehemu, Makamu wa Rais pamoja na Watanzania wote kufuatia msiba huu mzito wa kitaifa.”
Kufuatia msiba huu mkubwa, Mhe. Spika ameagiza Kamati zote za Bunge zilizokuwa katika ziara za ukaguzi wa miradi ya maendeleo mikoani kurejea Dodoma mara moja.
Raha ya milele umpe ee Bwana na mwanga wa milele umuangazie, apumzike kwa amani. Amina.