United Republic of Tanzania
Parliament of Tanzania
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Job Y. Ndugai anasikitika kutangaza kifo cha Mbunge wa Jimbo la Songea Mjini (CCM), Mhe. Leonidas Tutubert Gama aliyefariki usiku wa kuamkia leo katika Hospitali ya Peramiho iliyopo Songea Mkoani Ruvuma.
Kabla ya kifo chake Marehemu alirejea kutoka Nchini India Novemba 11,2017 ambapo alikuwa akitibiwa. Aidha, Novemba 21 alitokea Dar es Salaam na kurejea Songea kupitia mkoani Dodoma ili kushiriki mapokezi na ziara ya Mheshimiwa Waziri Mkuu Mkoani Ruvuma iliyoanza ya jana tarehe 23/11/2017.
Aidha, Novemba 22, 2017 majira ya saa 6 usiku Marehemu aliugua ghafla ambapo alikimbizwa katika Hospitali ya Peramiho kwa ajili ya Matibabu.
Ofisi ya Bunge baada ya kupata taarifa hizo iliandaa ndege maalum kwa ajili ya kumsafirisha kwenda Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa matibabu zaidi ambapo Madaktari wa Hospitali ya Peramiho walishauri asisafirishwe hadi hali yake itakapotengemaa. Hata hivyo Novemba 24, 2017 saa 6 usiku Marehemu aliaga dunia.
Marehemu Leonidas Tutubert Gama anatarajia kuzikwa siku ya Jumatatu tarehe 27 Novemba 2017 katika Kijiji cha Likuyu Fusi Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma. Ofisi ya Bunge, Serikali na familia ya Marehemu inaendelea kuratibu taratibu za mazishi ambapo taarifa zaidi zitaendelea kutolewa.
Mwenyezi Mungu ailaze Roho ya Marehemu mahali pema peponi.