Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 – Wizara ya Fedha na Mipango

WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nami napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutupa fursa ya kuchangia kwenye hoja muhimu ya Serikali iliyoko mbele yetu. Kabla ya yote, napenda kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Wabunge wengi wamechangia, hasa kuhusu miundombinu, kwani Wabunge wengi wanafahamu bila miundombinu nchi yetu haiwezi kuingia katika uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikianzia na Mheshimiwa Hawa Ghasia, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Miundombinu, ametoa hoja ifuatayo: katika Mpango wa Maendeleo wa Mwaka Mmoja Serikali imeainisha miradi saba ya kielelezo itakayohitaji mtaji mkubwa wa uwekezaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Miradi hiyo ni ujenzi wa Reli ya Kati kwa kiwango cha standard gauge, ununuzi na ukarabati wa meli kwenye Maziwa Makuu, kuboresha Shirika la Ndege Tanzania, ujenzi wa Barabara ya Kidahwa – Kanyani, Kasulu – Kibondo – Nyakanazi na Barabara ya Masasi – Songea – Mbaba Bay pamoja na mradi wa makaa yam awe na Mchuchuma na mradi wa chuma wa Liganga.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati inataka Serikali kuainisha miradi itakayotekelezwa kwa mfumo wa Public Private Partnership, muda wa kukamilisha na gharama za mradi husika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu hoja hiyo, kama ifiuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kutekeleza miradi ya barabara kwa kushirikisha sekta binafsi kwa utaratibu wa PPP.
Kwa sasa mradi pekee wa barabara ambao umepangwa kutekelezwa kwa utaratibu huu ni ujenzi wa Barabara ya Dar es Salaam – Chalinze Express Way. Barabara hii inatarajiwa kuwa na urefu wa kilometa 140 itakapokamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, upembuzi yakinifu wa mradi huu upo katika hatua za mwisho za kukamilishwa. Mara baada ya hatua hii kukamilika gharama za awali na muda wa utekelezaji wa mradi huo utajulikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Ghasia alikuwa na hoja ifuatayo; ushauri kwa Serikali kuhakikisha inahusisha Sekta binafsi kwa kugharamia mradi kwa njia ya ushirikishi yaani PPP pamoja na kutumia fedha zake za ndani ili kuwa na uhakika wa upatikanaji wa fedha za kutekeleza miradi ya maendeleo. Ushauri umepokelewa, Serikali imepanga kutekeleza miradi mingi iwezekanavyo ya miundombinu ya usafiri kwa njia ya PPP kila inapowezekana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja ya Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge kama ifuatavyo; kwanza ushauri kwa Serikali kuhakikisha sekta wezeshi zinatekeleza miradi kikamilifu kwa bajeti iliyotengwa kwa miradi hiyo. Miradi hiyo ni pamoja na ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara ya Chunya hadi Itigi, na barabara ya Ipole hadi Ikoga. Ushauri umepokelewa kwa barabara ya Chunya hadi Itigi upembuzi yakinifu na usanifu wa kina umekamilika kwa barabara yote yenye urefu wa kilometa 413 na barabara hii itajengwa kwa awamu. Katika mwaka wa fedha 2016/2017 zimetengwa shilingi bilioni 5.84 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa kiwango cha lami wa sehemu ya Itigi - Mkiwa yenye kilometa 35. Kwa sehemu iliyobaki Serikali itaendelea kujadiliana na washiriki wa maendeleo ili zipatikane fedha kwa ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara yote.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa barabara ya Ipole, Koga hadi Mpanda hatua za ununuzi wa Wahandisi Washauri watakapofanya mapitio ya usanifu na usimamizi, pamoja na mkandarasi atakayejenga barabara hiyo zinaendelea. Ujenzi umepangwa kuanza katika mwaka wa fedha 2016/2017, jumla ya shilingi bilioni 103.93 zimetengwa kama inavyooneshwa kwenye kitabu changu cha bajeti ukurasa 223.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna hoja kutoka kwa Mheshimiwa Josephat Kandege, Mbunge wa Kalambo kama ifuatavyo; kwanza anatoa pongezi kwa Serikali, pongezi hizo zimepokelewa, pia anatoa ushauri kwa Serikali kuwathibitishia au kuondoa wataalam wanaokaimu nafasi mbalimbali za uongozi katika taasisi na Serikali Kuu ili kuboresha uwajibikaji wa watumishi husika.
Kwanza ushauri huo umepokelewa, pili Serikali inaendelea na utaratibu wa kuhakikisha kuwa wataalam wote ambao sasa hivi wanakaimu wanafanyiwa confirmation ili wawe na muda wa kutosha wa kufanya kazi hiyo. Kwa kuanzia tu wiki iliyopita tulitangaza Bodi ya TPA ambayo sasa imeanza kufanya kazi, hatua inayofuata sasa hivi ni kumchangua Mtendaji Mkuu wa Bandari au Mamlaka ya Bandari ili aweze kuendelea na kazi hiyo ya kuendesha bandari zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna hoja ya Mheshimiwa Mbaraka Kitwana Dau wa Jimbo la Mafia ambapo hoja yake inasema kama ifuatavyoa; Serikali itoe mchanganuo wa muda wa utekelezaji yaani timeframe ya miradi yote ya maendeleo pamoja na gharama zake na siyo tu kwa ujumla kwa mfano ujenzi wa kiwango cha express way wa barabara ya Dar es Salaam hadi Chalinze.
Kwanza ushauri umepokelewa Mheshimiwa Mbunge, muda halisi wa ujenzi wa barabara ya Chalinze express way utajulikana baada zabuni kutangazwa na mwekezaji kujulikana. Kwa sasa mtaalam elekezi anakamilisha upembuzi yakinifu wa mradi huo na wakati huo utakapofika muda maalum utaelezwa kwa Waheshimiwa Wabunge na wananchi wa ujumla.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia alikuwa anahoja Serikali ijengwe….
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa muda wako umekwisha naomba umalizie.
WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, narejea tena naomba kuunga mkono hoja asilimia moa moja.