Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. George Mcheche Masaju

Sex

Male

Party

Ex-Officio

Constituent

None

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 – Wizara ya Fedha na Mipango

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kupata fursa hii ya kuchangia, nikushukuru wewe Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia na nianze kusema tu kwamba naunga mkono hoja hii kwa sababu mbili kubwa zifuatazo; kwanza hoja yenyewe iliyoletwa mbele yetu ya bajeti imeandaliwa vizuri kukidhi matarajio na matakwa ya wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili ni kwamba bajeti ndiyo interface kwa kiingereza, wanaita interface yaani kiunganishi kati ya wananchi na Serikali yao. Kwa hiyo, mkutano wa bajeti ni mkutano muhimu sana na wananchi wanaufuatilia wanataka kuona kile ambacho Serikali iliahidi kinatekelezwa na kwa sababu hiyo mimi naunga mkono hoja hii na ni kwa sababu ya bajeti hakuna mkutano ambao ni mrefu kuliko mikutano yote isipokuwa mkutano wa bajeti. Katiba ambayo imetoa jukumu kwa Wabunge la kuisimamia na kuishauri Serikali inapokuwa inatekeleza wajibu wake pia imetoa jukumu kwa Wabunge kujadili utekelezaji wa kila Wizara wakati wa bajeti na ninawapongeza sana Waheshimiwa Wabunge, mmefanya kazi kubwa sana ya kuisimamia Serikali yenu na kuishauri ili matarajio ya wananchi mnaowawakilisha yaweze kutekelezwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, muda mfupi uliopita tumewasikiliza Mawaziri wakitoa mchango wao namna gani watatekeleza zile hoja ambazo zimezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge. Kwa hiyo, nichukue fursa hii kuwapongeza sana Waheshimiwa Wabunge.
Mheshimiwa Naibu Spika, imezungumzwa hoja hapa kwamba, kwamba sasa hivi hakuna mgawanyo wa Serikali. Hii siyo kweli kwa sababu sisi wote tuna katiba Ibara ya 4 imeweka mgawanyo wa dola, kuna Serikali, inaitwa vyombo vya utendaji, kuna Bunge na mahakama, halafu Katiba hiyo imeendelea kutoa ufafanuzi wa kazi wa kila mhimili na ndiyo maana leo tuko hapa Bungeni, sisi leo hapa tunajadili bajeti ya Serikali na ndiyo jukumu la Bunge, yes hapa atuhumu kwa sababu hukumu ni mambo ya mahakama.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia Bunge hili unaweza kujiuliza, kama Katiba imeweka utaratibu katika Ibara ya 26 kwamba kila mmoja lazima aifuate na kutii Katiba hii na sheria za nchi na kwamba imetoa fursa mtu yeyote kwenda mahakamani kulinda hifadhi ya Katiba na sheria hiyo iweje leo iseme kwamba kama kungekuwa na hiyo fursa yenyewe au mwanya au viashiria tu kwamba sasa mgawanyo wa madaraka katika hii mihimili mitatu imevunjwa mpaka sasa hivi hakuna kesi yoyote iliyokwishakufunguliwa mahakamani na kwa hiyo, kama kungekuwa na viashiria hivyo mtu yeyote ana haki ya kwenda mahakamani. Kwa hiyo, hii ni hoja ambayo haina msingi na haiwezi ikawa na maana tu kwa sababu kwamba hakuna matangazo ya hadharani.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshasema ndani ya Bunge hili kwamba Ibara ya 100 imetoa huru na haki kwa Wabunge huru wa kujadili bila hata mipaka yoyote, siyo uhuru wa kutangazwa, haiwezekani yasipokuwa matangazo ya moja kwa moja ukasema kwamba madaraka ya Bunge yanapokwa au Wabunge wanazuiliwa kujadili, Wabunge wangeweza kuwa wanazuiliwa kujadili leo wasingeweza kujadili wakaishauri Serikali mpaka Serikali ikatoa maelezo kiasi hiki. Ninaloweza kusema pia kwamba kumekuwepo na hoja hapa kwamba Bunge limegeuzwa kuwa rubber stamp haiwezekaniki, kwa sababu kwanza mfumo wenyewe Bunge ambalo limepewa mamlaka kwa niaba ya wananchi kuisimamia Katiba litawezaje kuwa rubber stamp haiwezekaniki kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha pili kwa hiyo Serikali haiwezi ikapitisha bajeti yake bila Bunge kushiriki na kuamua kwa hiari yao. Lakini mfumo wenyewe wa maandalizi ya bajeti na utendaji wa Serikali ni kwamba ni shirikishi kwanza unaona katika Katiba yenyewe Ibara ya 63(2)(3) lakini pia sheria kwa sababu hiyo ikatungwa sheria ya bajeti na Sheria ya Bajeti ni shirikishi na kanuni zenyewe unaweka ushirikishi kati ya Serikali na Wabunge kuhusu bajeti. Kwa hiyo, kifungu cha tano na cha sita kinatoa mamlaka kwa mfano kifungu cha tano fiscal policy object, halafu cha sita microeconomic policies na kifungu cha saba kinasema kutakuwa na uanishaji wa mpango mfupi na mpango mrefu na bajeti sasa inaandaliwa kwa ajili ya mpango wa mwaka mmoja, mmoja. Kwa hiyo, bajeti katika mpango ambao umegawanyika katika kipindi cha mpango mrefu wa miaka mitano inakuja kutekelezwa kupitia mpango wa mwaka mmoja ambao ndiyo unaandaliwa bajeti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana nahoja za Wabunge wana kiu kwa ajili ya maendeleo ya majimbo yao kwa sababu ndiyo hasa, lakini pia kuwakumbusha tu ni kwamba kiu itatimizwa au itakidhiwa haja pale ambapo kila mwaka tunaleta mapendekezo kwa ajili ya utekelezaji huo. Kwa hiyo, yale ambayo hayakutekelezwa mwaka huu yatatekelezwa mwaka mwingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo niseme tu kwamba kanuni zenyewe zinaweka ushirikishi na Bunge lenyewe limepewa mamlaka chini ya kifungu cha nane na Kamati ya Bajeti imepewa mamlaka chini ya kifungu cha tisa namna ya kuangalia hivyo. Kwa hiyo, hoja ya kwamba Bunge limebaki rubber stamp haiwezekani ikawa ni ya kweli. Kwa hiyo, mimi nimeshiriki mle kwenye Kamati ya Bajeti, nimeshiriki humu Bungeni mnajua mimi siyo Mbunge mtoro, nakuwepo karibu muda wote humu ndani nimeona jinsi ambavyo Wabunge wamechangia sana, wameshauri Serikali yao na Serikali imeitikia vizuri, tumempigia makofi mengi sana hapa Mheshimiwa Mwijage muda mfupi uliopita kuonyesha kwamba Wabunge wametekeleza sana jukumu lao la Kikatiba.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na nikushukuru Mheshimiwa Naibu Spika na hili ni la msingi sana, kwenye jambo la msingi sana kama la bajeti linalowaunganisha wananchi na Serikali yao ambayo ndiyo interface yao, Bunge hili linahitaji kwa kweli kuendeshwa kwa namna ambayo italiwezesha Bunge lifanikishe utekelezaji wa majukumu yake. (Makofi)
Kwa hiyo, tunapofanya maamuzi haya chombo kinachoendeshwa kwa majadiliano kinahitaji kizingatie Katiba, sheria na kanuni zilizojiwekea. Kwenye hili mimi nakuomba na umefanya vizuri sana kuendelea kulisimamia hivi vizuri kusudi matarajio ya wananchi yaweze kutekelezwa, tunafanya reform ambazo lazima ziendane na kuzingatia Katiba na sheria za nchi. Mwanasheria Mkuu wa Serikali wakati hoja ya kumthibitisha Waziri Mkuu alisema juu ya umuhimu wa kuzingatia Katiba na sheria tunapotekeleza majukumu yetu hapa. Kwa hiyo, mimi naomba sana usikatishwe tamaa, umefanya vizuri na ndio maana Bunge hili linakuja na mapendekezo mazuri sasa. Bunge kama hili la bajeti ambalo ndiyo kiungo cha wananchi na Serikali yao likianza kuvurugwa matarajio ya wananchi yanaenda wapi? Kwa hiyo, usikate tamaa, uwezo unao, nia ya kufanya vizuri unayo na sababu za kuongoza Bunge hili unalo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.