Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru tena kwa kupata nafasi ya kuchangia leo Wizara ya Utumishi na Utawala Bora. Kwanza kabisa, nitoe shukrani kwa Waziri na Wasaidizi wake wote kwa namna ambavyo wanawajibika na kutekeleza majukumu ambayo wamekabidhiwa na Mheshimiwa Rais kwa niaba ya Watanzania. Hongereni sana, kazi mnazozifanya tunaziona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nina mambo machache sana. Jambo la kwanza, nina hakika kabisa jukumu la kupanga na kutumia rasilimali watu ni jukumu la Wizara hii japo wamekasimu majukumu haya kwenye Wizara ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa kuwa jukumu mama la kupanga na kusimamia masuala ya kiutumishi yanakuwa kwao, japo wanayapeleka kule TAMISEMI kwa niaba ya kuwasaidia kusimamia, kuna mambo machache ningewaomba wayatazame kwa kina na waweze kutoa maelekezo ikiwezekana au kusaidiana na Wizara ya Utumishi kwenye kuyarekebisha ili mambo yakae vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza ambalo ningependa kabisa kulizungumza ni suala zima la kuwapanga watumishi kwenye vituo vya kazi. Leo nchi hii ina tatizo kubwa la watumishi kuwa wachache kuliko mahitaji yanayotakiwa nchini. Bado ukienda kwenye utaratibu mzima wa kupanga, yapo maeneo ya watumishi wengi zaidi kuliko maeneo mengine na madhara haya yanatukuta sana sisi wenye Halmashauri zinazoitwa za vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, unaweza ukaenda ukakuta vijijini huduma zile ambazo wanatakiwa wapewe wananchi katika maeneo yale, watumishi walio kwenye maeneo hayo ni wachache zaidi kuliko watumishi walioko kwenye maeneo mengine. Hii ni kwa sababu ya namna ambavyo wanapangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni imani yangu kwamba pamoja na uchache uliopo wa watumishi nchini, kama Wizara mbili hizi zitakaa chini na kupitia vizuri ikama za watumishi kwenye nchi yetu, wanao uwezo wa kuwapanga kwa mahitaji yalivyo na kukawa na uwiano unaoweza kufanana na ukasaidia utendaji wa kazi na hii kasi ya kuonekana kuna watumishi wachache ikawa ndogo sana. Kwa hiyo, naomba sana, kwa kuwa tunawaamini, ni imani yetu kabisa kwamba hili jukumu lao mama, kwa maana ya Utumishi wanaweza wakakaa chini wakaliweka vizuri na likaondoa changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli vibali vinatolewa na watumishi wanaajiriwa, lakini kila siku Wabunge tukisimama tunalia namna gani watumishi hawa bado wanaendelea kuonekana wachache kwenye maeneo yetu. Kwa hiyo, niwaombe sana watazame. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kwenye suala zima la kuwapanga, hapa ndugu yangu Naibu Waziri anaweza akawa na ushahidi. Wapo watumishi wanapangwa kwenye maeneo tofauti na skills walizonazo. Ushahidi huu Naibu Waziri anao, aliwahi kuja kufanya ziara jimboni kwangu, alikutana na vitu hata yeye alishangaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kumkumbusha Naibu Waziri, lile ambalo alilishangaa Kibaha la kupangwa mtumishi ambaye kwa kweli mwenyewe ameona amepata taabu kufanya kazi kwenye halmashauri, walitazame na waweze kusaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nje ya hili la huyu wa Kibaha, nina hakika litakuwa lina watu wengi katika nchi hii ambao watakuwa wamewa-site katika maeneo ambayo hawawezi kuyafanyia kazi. Kwa hiyo, ni vizuri wawasikilize watumishi. Kama mtu wanamwona, maana unaweza ukafikiri kama mtu amepelekwa kwa adhabu, lakini mtu anaonekana ni mtaalamu wa masuala mazima ya manunuzi, anatolewa, anapelekwa kwenye eneo lingine ambalo hata ukimwuliza anashindwa kulifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni vizuri tunapozungumzia suala zima la kupanga watumishi, ni vema Wizara hii ya Utumishi kama jukumu lao mama, wawasilisane vizuri na TAMISEMI, wawapange watumishi kwenye maeneo ambayo wanaweza kuyafanyia kazi. Ipo mifano mingi na tunaweza tukaieleza hapa, na kwa kuwa bahati nzuri huu mfano ninaoutoa Mheshimiwa Naibu Waziri anaufahamu, basi ni vizuri akaufanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo kwa kweli linaondoa morali ya kazi, ni Serikali na Wizara hii ya Utumishi inayowashauri watumishi wajiendeleze kielimu. Mtumishi anaamua kujiendeleza kielimu, anajitoa kwenye sifa za kuwa mtumishi wa kada fulani, kwenda kada nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, anatakiwa afanyiwe recategorization, lakini ukirudi kwenye muundo mtu huyu kama atalazimika kufanyiwa recategorization analazimika kurudi madaraja ya chini hata kama ameshalitumikia Taifa kwa muda mrefu. Matokeo yake anapoteza sehemu ya maslahi yake, kwa sababu tu ameamua kubadilisha kada ya utumishi kwa sababu ya elimu aliyoamua kujiendeleza nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni vizuri kwa sababu shughuli nzima ya Wizara ya Utumishi ni kulinda maslahi, nao ndio walitoa huu mwamko wa watumishi kuamua kusoma vitu vingine ili waweze kujibadilishia kada. Kwa hiyo, ni vizuri wakapitia ile sheria waone ni namna gani wanaweza wakairekebisha ili iweze kuwapa morali watumishi, anayeamua kubadilisha fani, aende kwenye fani ile kwa mshahara ambao alikuwa nao ili maisha yake yaendelee katika kiwango kile kile, kwa sababu suala zima la mtu kubadilisha kada, anaweza akafanya hivyo kwa maana ya yeye kuangalia career yake anapendelea wapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, kama mtu anakwenda katika career ambayo atafanya vizuri, siyo vibaya akienda huko na akaendelea kulindwa mshahara wake ili aendelee kufanya kazi vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningependa kulizungumza kwenye maeneo haya ya utumishi, tunasikia Wabunge wengi tunalalamika juu ya suala zima la watumishi waliostaafu kupata tatizo la kufungashiwa mizigo kurudi makwao. Nazungumza kwenye Wizara hii kwa sababu tu wao ndio wana jukumu zima la utawala bora. Mambo haya yanawaumiza watumishi wengi kwa matendo wanayofanyiwa kule wanapofanyia kazi kwenye Wizara ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, utakuta mtumishi amefanya kazi halmashauri fulani, anafikia umri wa kustaafu, anafanikiwa kupata mambo yake mengine, lakini suala la kuondoka kurudishwa kwao, ambako ndiko alikoandika alijaza kwenye fomu ya ajira ni mtihani. Matokeo yake, mtu anakata tamaa, anabaki ugenini, anakuwa mzee wa ugenini, anashindwa kurudi kwao, mambo yanakuwa magumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna mifano mingi ya kutosha. Hata kwangu Kibaha Vijijini kuna orodha kubwa ya watumishi ambao wamestaafu na hawajasafirishwa kurudi makwao. Imekuwa ni kazi wakiamka kuja kwenye Ofisi ya Mbunge kumwambia tusaidie Mkurugenzi atulipe.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa unajaribu kujiuliza, kwani wakati anaajiriwa mtu huyu Serikali haikujua imemtoa wapi? Serikali haikujua anapaswa kurudi wapi? Kwa hiyo, mimi nalizungumza kwenye Wizara ya Utumishi nikiwa na maana kwamba wao ndiyo wasimamizi wa masuala ya utawala bora, ni vema wakasimama na wakawatazama waliowakasimia majukumu kama jukumu lao hilo wanalitenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo napenda kulielezea hapa ni la TASAF. Nimezungumza na hapa kwanza nitoe pongezi kwa Wizara na Naibu Waziri naomba pongezi hizi uzifikishe kwa Waziri kama ambavyo uliagizwa na Wazee wa Kibaha Vijijini. Ulipofanya ziara pale walikushukuru sana namna ambavyo uliwasaidia kufanya ukarabati wa ukumbi wao. Pia wakawa na ombi mbele yako, nafikiri unakumbuka. Ni imani yangu wakati utakapokuwa unatoa majibu, utaniambia ni namna gani wazee hawa hili ombi lao unaenda kulitekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, waliomba uwasaidie namna ya kumalizia kufanya ukarabati wa jengo ambalo kwao ni kitega uchumi. Hapa naomba nitoe ushauri kidogo kwa Wizara hii. Tunawahudumia wazee hawa sasa hivi katika ule mfumo wa kufanya yale majukumu mepesi, kwenye ile miradi ya barabara, miradi ya kupanda miti na miradi mingine ambayo inakuwa imechaguliwa kwenye maeneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukumbuke wale ambao wanaenda kuifanya ile kazi tayari tuliwatambua ni wazee ambao wameshaishiwa nguvu. Kwa hiyo, tunapokwenda kuwapa majukumu ndiyo wapate fedha, bado tunafanya kosa ambalo kwa kweli haliko katika dhana ile ambayo tumewasaidia. Ni vizuri tungeendelea kuwajengea msingi wa kuwatengenezea maeneo ya vitega uchumi ili kitega uchumi kiwe kinawaingizia kipato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nitatoa ule mfano wa pale Kibaha. Nafikiri ameuona Naibu Waziri alipokuja. Wale wazee mliwajengea ukumbi wa mikutano kwenye ile miradi ya mwanzo kabisa. Pamoja na uzee wao, ule ukumbi unafanya shughuli mbalimbali na wanaingiza kipato.

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri tungeweza kufikiria kufanya hivi kwenye maeneo mengi kuliko kuwapa majukumu ya kwenda kulima barabara na wakati mnajua kwamba tunaowasaidia ni watu wazima ambao pia wameshaishiwa nguvu. Kwa hiyo, wanakwenda asubuhi saa kumi na mbili, saa moja wanaisha. Matokeo yake barabara wanazozitengeneza ukienda kwenye hesabu ya kawaida zinatumia gharama kubwa, afadhali zile gharama zinazotumika kule zingesimamiwa na TARURA zingekuwa na uwezo mkubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, wazee wetu kwa lengo la kuwatunza tuendelee kuwatafutia utaratibu mzuri wa kuwasaidia katika hizi fedha za Mfuko wa TASAF ili waweze kubadilisha hali yao ya kimaisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hili, ningeweza kutoa ushauri ufuatao; nimezungumzia suala zima la recategorization, nawaomba sana, ipitieni vizuri tena ile sheria, kwani inaondoa morali kwa wale watu ambao wanaamua kwenda kujiendeleza na wanapokuwa wanaondoka morali, mtu yeyote yule ambaye hamu ya kazi ikimwondoka kwa sababu ya ugumu fulani wa utendaji anapoteza uwezo wa kuifanya ile kazi kwa ubora aliyonao. Kwa hiyo, nawaomba sana, tuzingatie mambo haya ili tuweze kuwasaidia watumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno haya, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)