Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami niungane na wote waliotangulia kusema, kwanza, kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutujalia afya iliyo njema na hata leo tupo mbele yako ukituongoza, tukiwasilisha kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wangu Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Comrade Mheshimiwa George Boniface Simbachawene, GBS. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwangu mimi binafsi nianze pia kwa kukushukuru wewe, kwanza kwa kuongoza kikao chetu vizuri. Pia kwa upekee kabisa namshukuru Mheshimiwa Spika kwa kuongoza Bunge hili vizuri, ameendelea kuwa Spika wa mfano, Spika anayetupa heshima na kwa kweli Spika wa viwango vikubwa. Nasi kwa kweli tunaendelea kumshukuru sana kwa uongozi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo, nami niungane na waliotangulia kusema kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri ambayo ameendelea kuifanya. Ni wazi kabisa kutokea kwenye michango ya Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia wamedhihirisha kabisa kwamba Mheshimiwa Rais wetu ni Rais wa mfano wa kuigwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nirudi katika maneno mazuri yaliyosemwa na ndugu yangu Mheshimiwa Mohamed Said Issa, Mbunge wa Konde, ambaye alisema, kwa kweli akipata nafasi ya kupiga kura atamchagua Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Maneno haya ni maneno mazito, maneno ambayo hayapaswi kupuuzwa, na pia ni maneno ambayo yanaonesha wazi kwamba naye anakubali kazi nzuri inayofanywa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Kwa kweli huu ni mfano wa wazi kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo, nawashukuru sana wote ambao wanamsaidia ambao kwetu sisi; mimi na Mheshimiwa Waziri wangu wamekuwa ni viongozi wetu. Nikianza na Mheshimiwa Makamu wa Rais, Dkt. Philip Isdor Mpango, yeye pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu, Dkt. Doto Mashaka Biteko, kwa kweli kazi nzuri inayofanyika ni wazi kabisa nchi yetu imepiga hatua kubwa ya kimaendeleo toka sehemu moja kwenda sehemu nyingine na hili linashuhudiwa kwa vitendo kutokea kwenye kazi zao, usimamizi wao na maelekezo ambayo kila siku wamekuwa wanayatoa, nasi Mawaziri wao tunatekeleza kazi hizo kwa juhudi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siwezi katika salamu za shukurani nikamsahau Waziri wangu, ndugu yangu, Doctor…

MBUNGE FULANI: He, amekuwa Doctor?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Bado.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimetaja madaktari hapa nimeona, nikampa naye Mheshimiwa Dkt. George Boniface Simbachawene. Mwenyezi Mungu atamjalia atafika huko. Kwa kweli Mheshimiwa Waziri mimi binafsi kwa niaba ya wenzangu wote ndani ya Wizara. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nitumie nafasi hii kabla sijaingia kwenye michango hii mizuri ya Waheshimiwa Wabunge, kumshukuru sana, kwanza kwa uongozi wake, na pia mazingira mazuri ambayo anatengeneza ndani ya Ofisi yetu. Amefanya Ofisi imetulia, anatoa ushirikiano mkubwa, maelekezo yake, maangalizo yake, kwa kweli ni Waziri wa mfano na Mwenyezi Mungu amjalie katika safari yake ya uongozi, basi ampandishe madaraja. Mwenyezi Mungu ampe na mengineyo ndani ya nyumba yake ili tuweze kuyaona na sisi tulio chini yake tuendelee kufaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mchango wa leo, tumepata bahati ya Waheshimiwa Wabunge 23 kuchangia hotuba ya bajeti ya Wizara yetu ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. Michango yote imejikita katika maeneo ya kimsingi kabisa ambayo yameelekezwa kuwa ndiyo kazi yetu ya msingi kabisa sisi ndani ya Ofisi ya Rais, inayosimamia Utumishi na Utawala Bora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, nataka kuanza kwa kulikumbusha Bunge lako kwamba, msingi mkubwa wa ofisi yetu ni usimamizi wa sheria, sera na taratibu ili kuweza kuisadia nchi katika kuhakikisha kwamba Utawala Bora na Utumishi wa Umma unaendelea kustawi.

Mheshimiwa Naibu Spika, yote yaliyozungumzwa hapa kwa mfano kwenye upande wa Utawala Bora, Waheshimiwa Wabunge wameeleza juu ya mambo ya msingi ambayo wao wanayaona kwamba yana changamoto kwa upande wao; siyo huko tu, pia hata katika eneo la Utumishi wa Umma, nalo pia wameeleza mambo ya msingi ambayo wanaona kwamba yana changamoto kwa upande wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo, pia katika michango yao wametumia nafasi hiyo kuishauri Serikali juu ya maeneo ya kimsingi ambayo wanadhani yakifanyiwa kazi, yakiwekwa vizuri au yakiangaliwa kisera na kisheria mambo yatakuwa mazuri zaidi kuliko ilivyokuwa jana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niendelee kuwakumbusha Waheshimiwa Wabunge kwamba, sisi ndani ya Serikali tukiongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na Mheshimiwa Waziri wetu, Mheshimiwa George Boniface Simbachawene, kazi ya kuendelea kuangalia sera, sheria na taratibu kuendelea kuongoza nchi yetu, tumeshaanza kuifanya na tunaendelea kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo maeneo ambayo kutokea kwenye michango ya Waheshimiwa Wabunge, imejidhihirisha wazi kwamba tunayo kazi ndani ya Wizara yetu ya kuendelea kutoa elimu kwa Waheshimiwa Wabunge, kwa sababu yapo mambo yanafanyika ndani ya Wizara na kwa michango ya Waheshimiwa Wabunge ni wazi kabisa yanaonekana mawasiliano kutoka kwenye Wizara yetu kuja kwa Waheshimiwa Wabunge kwa maana ya wananchi, bado yamekuwa ni hafifu. Katika mchango wangu au katika uchambuzi wangu nitayagusia maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nianze kwa hoja ambazo zimeelezwa na Waheshimiwa Wabunge hasa katika eneo hili la TASAF. Katika hoja ambayo imeelezwa na Waheshimiwa Wabunge iliyochangiwa ni kwamba, Serikali iharakishe upatikanaji wa vitambulisho vya Taifa ili kuwawezesha wananchi wenye sifa za kunufaika na mradi wa TASAF kupata fursa hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nilihakikishie Bunge lako kwamba, TASAF imeingia kwenye mkataba wa makubalino (MOU) kwa kushirikiana na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) kufanya mazoezi maalum ya kusajili na utoaji wa Namba za Vitambulisho vya Taifa kwa wanufaika wa mradi huo. Mpaka sasa wanufaika wa TASAF 680,816, wameshasajiliwa na kupokea ruzuku zao kwa njia ya elektroniki, kigezo kikubwa kikiwa ni kupatikana kwa hivyo vitambulisho vya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge Omar Ali Omar yeye ameeleza na amesikitika sana juu ya utaratibu ambao unaonekana kwamba kuna baadhi ya watu wapo juu ya sheria, miongozo na taratibu zinazosimamia miradi miradi ya TASAF.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naliambia Bunge lako kwamba, kama malalamiko hayo yapo, namwomba Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako kwa ujumla waendelee kutuletea ili tuyashughulikie. Isitoshe katika hilo, miongozo inayosimamia mradi wa TASAF inaelekeza wazi njia ya ku-deal na malalamiko ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kama inatokea kuna tatizo katika ngazi ya shehia, basi kwanza malalamiko yanatakiwa yapelekwe katika Kamati ya Uchambuzi kwamba, sijafanyiwa haki na ninahitaji kufanyiwa haki hiyo, lakini kama ataona pale katika shehia ambapo ndiyo matatizo yametokea labda wale watu wamekusanyana kwa pamoja dhidi yake, basi utaratibu unaelekeza kwamba, malalamiko yapelekwe katika ngazi ya wilaya, hasa kwa Wakurugenzi ili waweze kusimamia na kuchambua vizuri malalamiko hayo. Pale watakapoona kweli mtu huyu ana haki, lakini hakupendekezwa katika mradi, basi uamuzi wa kumrudisha ili awe sehemu ya wafaidika utafanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, endapo mtu huyu ataona pia Mkurugenzi katika ngazi ya wilaya hajafanya haki, basi utaratibu wa kukata rufaa kwenda Makao Makuu inabidi ufanyike ili mfaidika huyu aweze kupata haki anayostahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na Bunge lako kwamba, utaratibu huo unafanyika na uko wazi. Naomba yeye aendelee na kama ataona mambo yanakwenda hovyo, basi Ofisi ya Waziri na Ofisi ya Naibu Waziri zipo wazi, tuletee tuyashughulikie.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia 4R alizosema Mheshimiwa Rais, moja ya kazi kubwa ni kuhakikisha kwamba sisi wasaidizi wake tunawafikia mara moja wananchi wetu na tunakutana na changamoto wanazokabiliana nazo ili kuweza kuzitatua. Katika kufanya hilo, nataka kulieleza Bunge lako kwamba, tumepokea malalamiko 52,376 na baada ya kudodosa kaya hizo, tumeridhika kwamba kaya 7,412 zinajitosheleza katika vigezo na zimerudishwa katika mpango, lakini kaya 44,964 ambazo hazijajitosheleza katika vigezo, zimetolewa baada ya rufaa zao kushindwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri mwingine ni Serikali ihahakikishe matokeo ya rufaa za waombaji wa kujiunga na mradi wa TASAF yanatolewa mara moja. Ushauri umepokelewa na kuzingatiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kulieleza Bunge lako kuwa Serikali inaendelea kufanyia kazi rufaa zilizopokelewa kama ambavyo nimeeleza na ambapo sasa tunapozungumza kaya zile ambazo nimezitaja 7,412 ambazo zimeleta rufaa zake na kusikilizwa, zimeshajulishwa. Hapa tunapozungumza, watu wapatao 1,300,000 kutoka kwenye kaya hizo wanaendelea kufaidika na mradi huu wa TASAF.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo pia wapo baadhi ya wajumbe ambao walizungumza na kuitaka Serikali iendelee kuimarisha misingi ya utawala bora pamoja na kuboresha mifumo ya utendaji kazi katika utumishi wa umma, sambamba na kuboresha mishahara na maslahi ya watumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa ninataka nizungumzie eneo la watumishi na mishahara. Serikali imepokea ushauri huo na inaendelea kusimamia misingi ya utawala bora kwa kuzingatia uwajibikaji, uwazi na ushirikishwaji. Katika kuboresha mifumo ya utendaji kazi, Serikali imejenga mifumo ya kielektroniki katika maeneo mbalimbali kwa ajili ya kusimamia utendaji katika utumishi wa umma, ukiwemo Mfumo wa PEPMIS na PIPMIS ambao unawezesha kupima utumishi na ufanisi wa kazi wa watumishi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, kwa sasa mambo yote yanayohusu utumishi wa umma yanapimwa kwa kupitia vigezo ambavyo vimeainishwa na PEPMIS na PIPMIS. Kupitia Mfumo wa PEPMIS na PIPMIS wafanyakazi wanaweza kuorodhesha majukumu yao na vigezo vya kuwapima watumishi hawa vinatumika kwa kupitia vigezo vilivyowekwa katika utaratibu huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia wajumbe wengi wamezungumzia jambo la msawazo wa watumishi wa umma, hasa katika maeneo ambayo yanaonekana kwamba kuna shida kubwa ya watumishi wa umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa maneno mazuri ambayo yameelezwa na Naibu Waziri, Mheshimiwa Katambi wakati anatoa mchango wake kuhusiana na hoja iliyowekwa Mezani. Nawahakikishia Waheshimiwa Wabunge kuwa Serikali katika utaratibu wa kusimamia utendaji kazi, imebuni mfumo unaoitwa HR Assessment. Mfumo huu unaiwezesha Serikali kujua idadi ya watumishi katika maeneo yao, ni wapi ambapo kuna upungufu mkubwa na ni wapi pana uhitaji mkubwa ili kuwezesha mipango na misawazo ya utumishi wa umma kuweza kukaa vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kueleza jambo hili, nataka nirudi katika maneno au hoja iliyoelezwa na Mheshimiwa Yahaya Massare, Mheshimiwa Francis Isack Mtinga na Mheshimiwa Lujuo Mohamed Monni ambao wamezungumza hasa katika eneo la hitaji la walimu na upungufu mkubwa wa watumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawahakikishia Waheshimiwa Wabunge na Bunge lako kuwa, pamoja na changamoto hiyo, Serikali kupitia Mfumo wa HR Assessment inaendelea kupanga na kukamilisha zoezi la tathmini ya rasilimali watu ili kubaini upungufu au ziada ya walimu na watumishi wa kada mbalimbali katika Halmashauri zetu. Katika kufanya hivyo, Wilaya ya Mkalama na Wilaya ya Iramba zimetengenezwa nafasi za ajira mpya 86 na 70 za msawazo wa kada ya ualimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo, pia nalikumbusha Bunge lako kwamba, katika mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali ilitarajia kuajiri walimu 10,505 ili kupunguza changamoto ya upungufu wa walimu, lakini katika mwaka wa fedha 2024/2025, Serikali imetenga jumla ya nafasi za ajira mpya 10,590 za kada ya ualimu ili kuendelea kujaza nafasi katika maeneo yenye upungufu wa watumishi wa kada hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kwa upande wa Wilaya ya Mkalama na Iramba katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka 2021/2022 hadi sasa, walitengewa nafasi za ajira mpya 192 na 175 za mtawala wa kada ya ualimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi ameeleza masikitiko yake, hasa katika eneo la malimbikizo ya mishahara ya watumishi na kwamba bado kuna maeneo hawajalipwa malimbikizo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kulikumbusha Bunge lako juu ya kazi kubwa ambayo inafanywa na Serikali, hasa baada ya muundo mpya wa mfumo wa taarifa ambao unaitwa HCMIS. Mfumo huu unaiwezesha Serikali siyo tu kupata taarifa za watumishi, lakini pia katika kupanga vizuri mishahara.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo, pia napenda kulieleza Bunge lako kwamba, mfumo huu kwa namna moja au nyingine umewezesha watumishi kutokuwa na malimbikizo ya madai kutokana na kupandishwa vyeo kutokana na mabadiliko ya miundo kwa sababu sasa, kupitia mfumo huu mfanyakazi au mtumishi wa umma anapopanda daraja pale pale mabadiliko ya mishahara na taarifa zake, ikiwemo posho zake anazostahili nayo pia yanabadilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kueleza mbele ya Bunge lako kwamba, kwa mwaka 2021/2022 hadi 2023/2024 Serikali imelipa zaidi ya shilingi bilioni 193.15 kwa watumishi 118,584 wenye madai. Aidha, Serikali inaendelea na uhakiki wa madeni yaliyowasilishwa kwa waajiri kwa ajili ya malipo. Hadi sasa madai ya malimbikizo ya watumishi 21,660 yenye jumla ya shilingi bilioni 45 yamehakikiwa na yanasubiri kulipwa na Serikali kulingana na uwezo wa bajeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Joseph Kakunda amehimiza na kuikumbusha Serikali kufuatilia uzingatiaji wa maadili ya watumishi wa umma sehemu za kazi. Kwanza nalihakikishia Bunge lako kwamba mawazo mazuri yaliyotolewa na Mheshimiwa Mbunge tunayabeba na kwenda kuyafanyia kazi, lakini katika kufanya jambo hilo, Serikali inaendelea kutoa mafunzo ya maadili kwa watendaji na watumishi wa umma ili kuwakumbusha wajibu wao wa kazi pamoja na kutekeleza mipango na malengo ya Serikali. Mpaka sasa tunapozungumza jumla ya watumishi 24,922 wamepatiwa mafunzo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya taasisi 92 zimefanyiwa ufuatiliaji na kubaini maeneo yenye upungufu katika kuzingatia maadili na kuchukua hatua stahiki. Jibu hili ninalotoa hapa ni sanjari na mazungumzo au kumbusho lililotolewa na Waheshimiwa Wabunge kwamba, Tume yetu ya Watumishi wa Umma siyo tu isubiri kesi na kufuatilia mienendo, pia iende katika taasisi na Idara za Serikali ili kuweza kujua ni nini ambacho kinatokea hasa katika stahiki na haki za watumishi hao?

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo, pia Mheshimiwa Kakunda ameeleza kuwa kuna wakati uanzishwaji wa OPRAS ulipigiwa debe sana, lakini hajui kiutendaji OPRAS hiyo imepimwa vipi na ni lini imefanyiwa tathmini?

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kulieleza Bunge lako kuwa, kwanza Mfumo wa OPRAS kwa sasa haupo. Sasa hivi mfumo unaotumika kupima utendaji kazi unaitwa PEPMIS na matokeo ya mtendaji mmoja mmoja wa PEPMIS ndiyo unaitwa PIPMIS kwa maana ya taarifa ya taasisi au ofisi ambayo inasimamia watumishi wa umma. Mfumo huu umeanza kutumika katika kupima utendaji kazi wa Watumishi wa Umma katika mwaka wa fedha 2023/2024, baada ya Serikali kutoa waraka na kufuta mfumo ule wa zamani wa OPRAS.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango mwingine umeelezwa na Mheshimiwa Dkt. Alice Kaijage, ambaye ametaka mtumishi anapobadili kada asianze katika cheo kipya au mshahara wake uweze kusomeka kama ulivyokuwa zamani, na kwamba, watumishi wa umma ambao wamejiendeleza kielimu ndiyo ambao wanakabiliana sana na changamoto hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nitumie mfano mmoja, hasa watu ambao wamesomea shahada ya kilimo. Kwa mtumishi wa umma ambaye ana Stashahada ya Kilimo ambayo ndiyo imemfanya aajiriwe katika kazi, pale anapokwenda kujiendeleza na kutunukiwa Shahada ya Kilimo kwa maana kwamba sasa ametoka katika stashahada, ameingia katika shahada, mara nyingi miundo ya kazi nayo hubadilika, kwa sababu, sasa huyu anakuwa ni Bwana Kilimo, lakini yule mwenye stashahada ya kazi kwa mujibu wa vyeo vya kimuundo anakuwa ni Afisa Kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu hawa wawili wote wana vyeo tofauti, lakini anapofika kwenye ngazi ya juu kabisa katika ngazi ya cheti, kwa maana ya mtu mwenye stashahada, maana yake ni mshahara wake unaweza kuwa juu ya mshahara ambao akiwa na shahada anaenda kuanzanao.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kulieleza Bunge lako kwamba, inapotokea mtu ana mshahara mkubwa katika nafasi ya cheo anachoomba kubadilishwa, basi maombi kwa ajili ya kumwezesha kuondoka na mshahara wake ule ulio juu, yanafanyika kupitia Ofisi ya Katibu Mkuu Utumishi. Kibali kinapotolewa, utaratibu wa kumhamisha mtu huyo na mshahara wake unafanyika ili aweze ku-enjoy uwepo wa Serikali ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge pamoja na Bunge lako kwamba, taratibu zipo wazi. Tunachoomba ni watumishi wa umma mfuate taratibu ili mambo yaende vizuri katika stahiki zenu zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hoja nzuri zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge, lakini wapo baadhi yao ambao wametaka kujua juu ya mifumo mipya ya Sekretarieti ya Ajira inavyofanya kazi katika eneo zima la usaili wa vijana wetu. Mheshimiwa Francis Mtinga ameeleza kwamba, utaratibu uliopo unafanya baadhi ya vijana wasafiri umbali mrefu, kwa mfano, wapo ambao wanatoka Kigoma, Mwanza, Bagamoyo, Lindi na Mtwara kuja kufanya usaili katika Mji wa Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelekezo yaliyotolewa na Kiti chako ya kutaka Sekretarieti ya Ajira iangalie tena utaratibu wa jinsi ambavyo watumishi wapya wa umma wanapatikana, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri George Boniface Simbachawene, naomba kuliarifu Bunge lako kwamba, tumeanza usajili kwa njia ya kidijitali ambapo sasa online aptitude test imeanza kufanya kazi na mara ya kwanza ilipotumika usaili ulifanyika Tanzania nzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kulitaarifu Bunge lako kwamba, katika siku ulipofanyika usaili kwa mara ya kwanza kupitia utaratibu huu mpya, hatukupata lalamiko lolote. Baada ya utaratibu huu kuonekana umefanikiwa, malengo ya Serikali ni kuhakikisha taratibu nyingine za usaili wa vijana wetu katika kada zote unaingia katika utaratibu huu wa online aptitude test system ili waweze kupata nafasi ya kufanya usaili katika maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako kwamba, kwa wale vijana wanaotokea Singida, kwa utaratibu huu mpya maana yake ni watafanya usaili Singida. Hivyo ndivyo itakavyokuwa pia kwa watu wote wanaotokea katika kona zote za Tanzania, ikiwemo wale wenzetu wanaotokea upande wa Visiwani au Zanzibar.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, pia Mheshimiwa Mbunge Dkt. Alice Kaijage amezungumzia eneo la Sekretarieti ya Ajira, anapenda aone uwezekano wa kutoa kipaumbele kwa waombaji kazi waliohitimu vyuo muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, uendeshaji wa michakato ya ajira katika utumishi wa umma unazingatia Sera ya Menejimenti ya Ajira ya Mwaka 2008, Sheria ya Utumishi wa Ajira Sura ya 298, na Kanuni ya Uendeshaji wa Shughuli za Sekretarieti ya Ajira ya Mwaka 2021. Aidha, kanuni ya 18 (2), (c) inampa kipaumbele msailiwa mwenye umri mkubwa kupangiwa kazi pale inapoonekana amepata alama za ufaulu. Kwa hiyo, nalihakikishia Bunge lako kwamba, utaratibu huu unaendelea, lakini najua kwamba hapa kinachozungumzwa hasa ni watu ambao wamemaliza shule muda mrefu na hawajapata ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nataka kulikumbusha Bunge lako kwamba, ndani ya vikao vya Bunge hili tumekubaliana kwamba, ajira zote ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa mujibu wa sheria, zitatolewa kwa njia ya ushindani. Kwa hiyo, sisi ndani ya Sekretarieti ya Ajira au ndani ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma tunachokifanya ni kusimamia sheria, sera na taratibu tulizokubaliana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawahakikishia Waheshimiwa Wabunge, mijadala juu ya hao wenzetu ambao wamemaliza shule muda mrefu na hawajapata nafasi za kuajiriwa inaendelea kujadiliwa ndani ya ofisi yenu. Katika kufanya hivyo, chini ya uongozi wa Mheshimiwa George Boniface Simbachawene, ninaamini kabisa kwamba majibu yatakapokuwa tayari tutayaleta mbele ya Bunge na huenda yakachagiza kubadilishwa kwa sera, sheria na mambo mengine. Haya yote yanayozungumzwa na Waheshimiwa Wabunge tunayachukua na tunakwenda kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho lakini siyo kwa umuhimu, ninazungumza juu ya ujenzi wa mifumo. Mheshimiwa Yahaya Massare amekuwa na tamaa ya kutaka kujua sana na ninadhani hili ni kwa Bunge lako lote, kwamba mifumo imekuwa inalalamikiwa kwamba haisomani. Hili limekuwa ni changamoto kubwa sana lakini pia Bunge lako limezungumza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nikuhakikishie wewe na Bunge lako kwamba juhudi kubwa sana zimeendelea kufanyika ndani ya Serikali. Moja ya eneo kubwa ambalo limefanyiwa kazi ni kutengenezwa kwa mfumo wa kubadilishana taarifa ambao unaitwa Government Enterprise Bus au kwa lugha ya ki-TEHAMA inaitwa GovESB. Hadi sasa taasisi 122 ambazo zinatumia mifumo 132 zimeweza kuunganishwa na zinabadilishana taarifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuthibitisha hili, nataka nitoe mfano wa Mfumo wa Haki Jinai ambapo wenzetu wa Jeshi la Polisi, Mahakama, Ofisi ya DPP na wenzetu wa TAKUKURU, mifumo yao inabadilishana taarifa kwa sasa. Sasa hivi likifunguliwa jalada katika ofisi, labda katika Jeshi la Polisi, basi jalada lile likiwekwa tu ndani ya utaratibu, Ofisi ya DPP itapata taarifa, wenzetu wa TAKUKURU watapata taarifa, pia Mahakama nayo itapata taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hilo tu, pia mfumo huo umewezeshwa na mfumo mwingine wa malipo wa Serikali ambao unaitwa GePG ambapo mfumo huo umeunganishwa na mifumo yote ya watoa huduma wa simu. Ikiwemo hawa wenzetu wa Vodacom, Tigo, Halotel, TTCL na wengine wote ili kuwezesha mifumo yote kusomana. Leo hii mimi ninayetumia simu fulani ya kampuni fulani, nikitaka kufanya malipo kwa simu ya kampuni nyingine kupitia Mfumo wa GePG, malipo yanawezekana na mambo yanakwenda vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, niendelee tena kuishukuru Serikali yangu. Pili, namshukuru Mheshimiwa Rais pamoja na wasaidizi wake wote wakiongozwa na Mheshimiwa Makamu wa Rais, kwa kazi nzuri inayoendelea kufanyika ya kuwahudumia Watanzania; kuwahudumia watu wote ambao wana mahitaji bila kusahau kaya masikini zinazohudumiwa na TASAF ambapo Serikali imeendelea kuongeza pesa kila siku kuhakikisha kwamba tunawaondoa Watanzania katika umaskini, huku ikibuniwa miradi ya mfano wa kipekee kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)