Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Katiba na Sheria. Nianze kwa kukupongeza kwa kukaa kwenye kiti hicho; umependeza na naamini utatutendea haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maelekezo yake na nia yake njema juu ya nchi yetu juu ya masuala ya utawala bora, mambo ya sheria pamoja na Katiba. Nimpongeze sana pia Mheshimiwa Waziri Pindi Chana, Naibu wake pamoja na timu yao kule chini kwa usimamizi mzuri juu ya Wizara hii, wanafanya kazi nzuri sana. Sisi kama Kamati tumepata ushirikiano mzuri kutoka kwao kwenye mambo mengi tuliyokutana, kuanzia kwenye kutembelea miradi mpaka kwenye kujadili bajeti zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze pia Mheshimiwa Jaji Mkuu na Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu ambaye yuko humu ndani, pia Mtendaji Mkuu wa Mahakama Mheshimiwa Ole Gabriel, mtumishi wa Mungu. Pia niwapongeze sana timu zote zinazoongoza Mafungu ya Katiba na Sheria. Kwa sababu kwa kweli kazi yao ni nzuri sana, wamehusika sana katika kutuelimisha kama Kamati ili tujue kila fungu linahusika na nini na majukumu na kazi zao. Wamekuwa na bidii sana ya kukutana na Kamati ili kutuelimisha na sisi kwa sehemu kubwa tumeelewa na ndiyo maana nimegeuka kuwa mwanasheria mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze sana Serikali kwa kuanzisha Vituo Jumuishi vya Mahakama (ICJ). Vituo hivi kwa kweli vinatufaa sana sisi wananchi kwa sababu vina mambo mengi. Ukikuta kituo kinaitwa kituo maana yake hapo kuna Mahakama ya Mwanzo, kuna Mahakama ya Wilaya, kuna Mahakama ya Mkoa, kuna Mahakama Kuu na wakati mwingine Mahakama ya Rufaa inaweza ikatumia vituo hivi jumuishi kufanya sessions za Mahakama ya Rufaa. Niipongeze sana Serikali kwa approach hii. Naamini wananchi wataendelea kupata haki zao kwa karibu na gharama nafuu kuliko ilivyokuwa hapo mwanzo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetembelea vituo hivi Mwanza, Njombe, hapa Dodoma na mahali pengine, vituo hivi vimejengwa vimekamilika kabisa na ni vituo ambavyo vinajitosheleza. Niiombe tu Serikali iongeze watumishi kwenye vituo hivyo, mahakimu wa Mahakama za ngazi zote hizo wawepo kwenye vituo hivyo ili kwamba wananchi wetu wakienda pale waweze kuhudumiwa na mambo yao yaweze kuishia hapo badala ya kusafiri kuelekea mbali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze pia Serikali kwa ajili ya Wakili Mkuu wa Serikali kwa kuokoa fedha nyingi za Serikali, hasa kwenye mashauri haya ya nje na hata haya ya ndani. Niipongeze sana Serikali kwa sababu kupitia Wakili Mkuu wa Serikali, Serikali imeokoa fedha nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri alipokuwa anasoma hotuba yake, tumesikia alivyotaja mabilioni na matrilioni ya fedha yaliyookolewa, lakini sisi pia kwenye Kamati na hata taarifa yetu imetaja kwamba, Wakili Mkuu wa Serikali ameokoa fedha nyingi sana za Serikali ambazo zingepotea kama isingekuwa weledi na utaalam wa ofisi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niombe ofisi hii iweze kuongezewa wafanyakazi ili wawepo wafanyakazi wa kutosha, pia mafunzo juu ya masuala ya upatanishi (arbitration). Nadhani ni field mpya kwetu kama tunaweza kuanza kuwa na chuo cha kwetu hapa, tukafundisha wataalamu wa kutosha kuhusiana na jambo hili, litakuwa jambo jema. Kama hatuna, basi kama kuna vyuo kule nje, basi wataalam wetu wapelekwe wajifunze juu ya masuala haya ili watuwakilishe vizuri sisi Serikali. Dunia ya leo ya utandawazi na tunapokaribisha uwekezaji mwingi namna hii na unapofurika kuja Tanzania, tunahitaji ofisi hii ifanye kazi yake vizuri ikiwa na wataalamu walio na weledi kwenye mambo mbalimbali ili Taifa letu tusipate hasara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo nizungumze mambo mawili na la tatu nitamalizia la Jimbo langu. La kwanza, ni mchakato wa kupata haki baada ya kushinda kesi, Mheshimiwa OIelekaita amezungumza kidogo. Mchakato huu kusema kweli baada ya mchakato wa kesi kuisha na mtu anatakiwa sasa apewe haki yake, mchakato ni mrefu sana. Inabidi afungue tena kesi kwa Msajili wa Mahakama kupata hiyo haki yake, aweke tena wakili kama ana uwezo wa kufanya hivyo au aanze kusafiri kupata haki yake aliyopata mahakamani kwenda mahakamani tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mlolongo wote huu naambiwa uko kisheria, lakini hii sheria si inaweza ikabadilishwa? Kwa sababu kusema ukweli mlolongo huu unawanyima haki wananchi wetu wengi mno. Kwanza, wananchi wetu akishashinda kesi hajui kama kuna mambo ya kukazia hukumu na hata huo utaratibu akielezwa wa kukazia hukumu, utaratibu wake na namna ambavyo upo kisheria ni mrefu mno, kiasi kwamba inaingiza gharama na inakatisha tamaa na wananchi wetu wengi wameshindwa kupata haki yao na wengine hata wameaga dunia hawapo, lakini haki yao walishinda mahakamani kwa sababu tu ya kipengele hiki cha kutokukazia hukumu ili kupata haki yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana Serikali ijaribu kuangalia sheria inayoongoza masuala haya ni sheria ya namna gani, iletwe hapa Bungeni tuweze kuirekebisha. Kama pengine labda tu ni bureaucracy za kimahakama, sasa utaratibu huo unaweza kufupishwa? Tukizungumzia masuala ya kidijiti ambayo Mheshimiwa Mwenyekiti wetu ameyazungumza vizuri. Masuala ya kidijiti yakienda vizuri huu utaratibu unaweza ukafupishwa ili mtu apate haki yake? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa najiuliza, mimi nimeshinda kesi, ng’ombe wangu walikamatwa kwenye hifadhi, nikashinda kesi. Hivi Mahakama inashindwa nini sasa wakati huo huo kwa sababu imeniona nina haki, inashindwa nini kunipa haki wakati huo huo? Mpaka tena nianze utaratibu mwingine, nikasajili, nitafute mtu wa kunisaidia, kwa kweli utaratibu huu si mzuri sana na nadhani sisi kama Wabunge tunahitaji kuuangalia upya na kama ni sheria, iletwe hapa Bungeni tuibadilishe ili utaratibu huu uweze kutoa haki kwa watu wetu mara mtu anaposhinda kesi mahakamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ninalotaka kuzungumzia ni juu ya documentation za ushahidi. Ushahidi unapokwenda mahakamani, unatakiwa upeleke documents ambazo ni original. Kwa mfano, kama ni mkataba, nina kesi na ndugu yangu hapa Mheshimiwa Mpembenwe, labda za madai, nipeleke mkataba wangu ambao ni original, nipeleke malipo yangu ambayo nilifanya original. Sasa, kama nina kazi nazo zingine zinasimama kwa sababu hizi documents ziko kule mahakamani. (Makofi)
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ndaki, muda wako umeisha, hitimisha.

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ooh! Ahsante naunga mkono hoja. (Makofi)