Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. NG'WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Katiba na Sheria. Nianze kwa kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa ya kuhakikisha kwamba, Watanzania wanaishi kwa haki, demokrasia, umoja na wanaishi kulingana na sheria zinavyotaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani nitakuwa nipo sahihi nikisema kwamba, mwanahaki za binadamu namba moja Tanzania kwa sasa ni Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Kwa hili kwa kweli amefanikiwa kwa ukubwa sana, ameanzisha Tume ya Haki Jinai ambapo maoni ya Watanzania yamechukuliwa na yanafanyiwa kazi. Bunge hili hili tumepitisha Sheria za Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani, tunaendelea kufanya mabadiliko mbalimbali ya sheria kuhakikisha kwamba, demokrasia na haki za binadamu Tanzania zinaendelea kulindwa. Naipongeza sana Wizara kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaendelea kufanya kuhakikisha kwamba Watanzania wote haki zao zinalindwa na kuangaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mchango wangu wa leo utajikita kwenye Fungu Namba 59 la Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania. Tume hii imeanzishwa chini ya Sheria ya Tume ya Kurekebisha Sheria, Sura Na. 171 ambayo tulianzisha tangu mwaka 1983. Kati ya majukumu makuu kabisa ya Tume hii, ilikuwa ni kuhakikisha kwamba, inaziangalia na kuzitazama Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili ziendane na mazingira ya wakati huo na kuhakikisha kwamba, zinaendana na mabadiliko endelevu ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka uliopita taarifa zinatuonesha Tume hii ilitengewe shilingi bilioni 5.1, lakini mpaka tunavyozungumza Tume hii imepewa fedha kwa 53% tu ambayo ni sawa na shilingi bilioni 2.6. Changamoto ya ukosefu wa fedha katika Tume hii ya Kurekebisha Sheria ndiyo ambayo inatufanya mpaka sasa tunakuwa na sheria nyingi ambazo zimepitwa na wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria nyingi sana amezitaja Mheshimiwa Noah, akionesha kuna Sheria ya Ndoa ambayo mpaka sasa haijarekebishwa na Bunge hili, kuna Sheria za Ardhi ambazo zina migogoro, kuna Sheria za Wanyamapori ambazo zina migogoro kwa wananchi. Sheria hizo zingeweza kubadilishwa kwa wakati kama tungeipatia fedha za kutosha Tume hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili naomba kushauri, tuipatie fedha za kutosha Tume hii ili mabadiliko yafanyike kwa wakati. Nitatoa mfano, leo hii kwenye Sheria zetu za Utumishi wa Umma, tuna mifumo ambayo ni centralized. Tumeianzisha mifumo hii kwa sheria za zamani na sera tunayoitumia sasa pia ni ya muda mrefu sana, sheria hii imeshakuwa na upungufu mkubwa sana kulingana na mazingira tuliyonayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii tuna mfumo centralized wa kupata waajiriwa wote Serikalini. Ajira zinatangazwa, watu wanaomba na tunakuwa na mfumo mmoja wa kuchakata nafasi hizi za ajira, lakini tumeona na tafiti mbalimbali zimefanyika zinazoonesha Tanzania ya sasa inahitaji mfumo decentralized. Inahitaji ajira zinapotangazwa zishushwe kwenye maeneo yetu, kama ni mikoa au wilaya ili watu wote Watanzania waweze kugawana nafasi hizi za ajira kwa usawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana Serikali ya Chama Cha Mapinduzi kwa Sera yake ya Elimu Bure na kwa kuendelea kuongeza mikopo kwenye elimu ya juu. Sasa hivi hakuna mkoa usio na wasomi, hakuna wilaya isiyo na wasomi, hakuna kata isiyo na wasomi. Wasomi wametapakaa kila sehemu. Tunahitaji mabadiliko ya sheria na sera zetu ili zinapotangazwa ajira zishushwe kwenye mikoa na wilaya zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakupa mfano, kuna nafasi hapa zimetangazwa kama nafasi 46,000 tukigawana kwa mikoa 26 tunapata karibu kila mkoa nafasi 1,700. Kwa Mkoa wangu wa Mwanza ambao una wilaya saba tukigawana hizo nafasi 1,700 kila wilaya inaondoka na nafasi zaidi ya 250. Itakuwa ni ngumu sana kwa kijana yeyote au mtu yeyote aliyeomba ajira kulalamikia mfumo wa upatikanaji wa ajira ilihali hata kama hajapata yeye anajua katika wilaya yake au kata yake kuna watu kadhaa wamepata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii itatuondolea sana migogoro mingi kati yetu sisi na wale ambao tunawaongoza. Pia, katika hili hili la kurekebisha sheria, nimshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuona kwamba kuna haja ya kufanya mapitio katika ile mikopo ya 10%. Naipongeza sana Serikali katika bajeti ambayo imesomwa na TAMISEMI hapa wiki iliyopita, wametuambia kwamba tunarudisha ile mikopo ya 10% kwa halmashauri kadhaa kwa mfumo mpya na halmashauri nyingine kwa mfumo ule ambao utaangaliwa kwa umakini zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mikopo hii tuliipitisha kwa Sheria ya Bunge. Tunahitaji Sheria iletwe hapa Bungeni ili tubadilishe kuruhusu mikopo hii kuanza kupitia benki. Leo hii tumetoa tamko hapa lakini tutakuwa challenged tunapitiaje benki bila kurekebisha sheria? Tutenge fedha kwa Tume hii ya Kurekebisha Sheria ili walete mabadiliko ya Sheria ya Fedha katika halmashauri zetu tuweze kuanzisha huu mfumo mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, tumekuwa tunapiga kelele sana kwamba, tunahitaji sheria iletwe kwa ajili ya kuwapa kipaumbele wale wanaojitolea katika halmashauri zetu wapewe kipaumbele pale ambapo ajira zitatangazwa. Sheria hii imekuwa ya muda mrefu sana tunajua itakuja lakini haiji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sasa Wizara hii na chini ya Tume hii iangalie sheria tulizonazo izirekebishe ili mtu yeyote anayeomba kujitolea kupata mentorship kwenye ofisi zetu, kwanza waruhusiwe. Kwa sababu kwa mfumo uliopo sasa hivi, mtu anaomba kujitolea kama vile anaomba kulipwa mshahara. Anaomba kufanya kazi bure, anaomba kujitolea kwa muda wake, lakini ataongeza pia uzalishaji na utoaji wa huduma lakini wanapata usumbufu sana. Tuletewe sheria watu waruhusiwe kujitolea, lakini wale wanaojitolea wapewe kipaumbele kwenye ajira zinapotangazwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yote haya yatawezekana kama tukiiwezesha Tume hii ya Kurekebisha Sheria chini ya Fungu hili 59 kupata fedha zake kwa asilimia zote 100. Sheria zetu zianze kuendana na mazingira tuliyonayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, misingi ya umoja, amani na uhuru tuliyonayo katika nchi yetu hii ilijengwa, haikutokea tu na ilijengwa kuanzia katika ngazi za familia. Tuna haja ya kuilinda sana taasisi ya familia. Kwa takwimu zilizopo sasa hivi inaonekana kwamba divorce rate kwenye nchi yetu inaongezeka kwa kasi na ni kwa kasi ambayo inatia mashaka ya ustahimilivu wa taasisi hii ya familia. Moja ya sababu ambazo zimeonekana zinaongeza rate ya divorce au talaka kwenye nchi yetu, ni umbali wa waajiriwa wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baba ameajiriwa Mwanza, mama kaajiriwa Mpanda, mama kaajiriwa Mara, baba kaajiriwa Rukwa. Hii ndiyo inaongeza wingi wa talaka. Kama tunataka kuhakikisha watoto wetu wanalelewa katika malezi bora tuhakikishe kwamba misingi ya mila na tamaduni zetu katika nchi hii zinalindwa, tuhakikishe kama Serikali inalinda taasisi hii ya familia. Tupitishe sheria hapa, tuzipitie sheria zetu za utumishi ili kuwepo na misingi inayobana utumishi wa umma katika kulinda familia. Kama baba ameajiriwa Mwanza hata kama ni wilaya tofauti, mama naye asogezwe karibu ili kulinda familia na taasisi hii kuhakikisha kwamba tunakuwa na kesho ya watoto wetu iliyo bora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)