Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Bupe Nelson Mwakang'ata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nachukua nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye bajeti hii muhimu iliyoko mbele yetu, Bajeti ya Kilimo ya 2024/2025. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uzima na kuweza kuchangia katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kazi yake ni njema na nzuri hasa kwenye suala zima la kilimo. Mama amefanya mapinduzi makubwa sana. Tukiangalia 80% ya Watanzania ni wakulima. Mama amefikiria, ameweza kuweka ruzuku kwenye suala zima la pembejeo za kilimo. Hongera sana Mama, umeupiga mwingi, tumpe mama maua yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii pia kumpongeza kaka yangu Mheshimiwa Bashe na Naibu wake, kaka yangu Mheshimiwa Silinde kwa kazi nzuri na ubunifu mkubwa kwenye sekta hii ya kilimo. Hongereni sana, nami namwomba Mwenyezi Mungu aendelee kumpa kibali mama na aendelee kuwapa nafasi ili muweze kuwatumikia Watanzania kama mlivyowatumikia kwenye suala zima la sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza Katibu Mkuu na Wakurugenzi Watendaji wote wa Taasisi za Wizara ya Kilimo, tukianza na TFC, NFRA, CPB, ASA, Kahawa, Korosho, Tumbaku, TOSCI na Tume ya Umwagiliaji. Kwa pamoja wameweza kufanya kazi nzuri na ndiyo maana Wizara ya Kilimo na sekta ya kilimo sasa hivi imekuwa ni nzuri sana na ni kimbilio la Watanzania. Wakulima wengi zamani walikuwa wanaonekana ni maskini, lakini kwa sasa mkulima ni tajiri na tunakwenda kupata mabilionea kwenye sekta ya kilimo. Yote hii inatokana na uongozi mzuri kuanzia kwa Rais, Waziri na Watendaji wote wa sekta hii, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naingia kwenye hoja yangu ya msingi, kwanza ni suala la BBT. Nimesoma ukurasa wa 10, kwanza kabisa naipongeza Wizara, nampongeza Waziri kwa mawazo mazuri ya kuleta wazo hili la BBT, ni wazo zuri sana. Mwanzoni watu walibeza, lakini hili wazo linakwenda kumkomboa Mtanzania, hasa vijana, wanawake na Watanzania kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusoma hapa, nimeona mpango wa program ya BBT umelenga kwenye mikoa ya Dodoma, Kigoma, Mbeya, Singida, Pwani, Tanga, Njombe na Kagera, lakini sijaona Mkoa wa Rukwa. Mkoa wa Rukwa ni miongoni mwa mikoa ambayo inalima sana na inaweza kulisha Tanzania nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe mwenyewe na Mheshimiwa Waziri ni mashahidi kwamba Mkoa wa Rukwa tunalima sana, lakini kwenye suala la BBT, hapa sijaona jina la Mkoa wa Rukwa. Naomba sana Mkoa wa Rukwa tuna vijana wengi wakulima wanaoweza kulima vizuri, lakini hawana pa kulima. Tunaomba hii BBT na Mkoa wa Rukwa pia tuwemo kwenye mikoa hii ambayo mmeitaja hapa. Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapo naomba arekebishe na Rukwa iwemo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naingia kwenye suala la pembejeo. Naipongeza sana Serikali kwamba katika Mkoa wangu wa Rukwa tumepata pembejeo za kutosha, pembejeo zenye ruzuku. Wakulima wanamshukuru sana Rais na Mhesimiwa Waziri kwa kuwa tumeona na tumeshuhudia tumepata pembejeo na mbolea ya kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua unapomaliza msimu, msimu mwingine unaanza. Basi mwaka huu mbolea ziwahi kufika na kwa kiwango cha kutosha. Mbolea inapokuja kwa mfano, kwa mwaka huu mbolea ya CAN imekuja nyingi, lakini mbolea ya UREA imekuja kidogo. Muda wa kuweka mbolea ya UREA ulipofika ikawa kidogo, kwa hiyo, tunaomba msimu huu mbolea zote zije kwa kiwango sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mtovu wa shukrani nisipompongeza Mkurugenzi wa Taasisi ya TFC, kaka yangu Samwel Mshote na Watendaji wote wa TFC, wamefanya kazi nzuri. Pia wameweza kuleta mbolea na pembejeo kwa wingi katika Mkoa wa Rukwa. Mkoa wetu wa Rukwa tunakwenda kuvuna mahindi kwa wingi na changamoto yetu itakuwa ni soko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Wizara izingatie sana, mmehamasisha wakulima wameweza kulima kwa wingi, sasa tatizo litakuja kwenye suala zima la soko, nasi mnajua kabisa tumepakana na nchi jirani ambazo tayari zina majanga ya njaa. Tunaomba mtakapojiridhisha kwamba sasa NFRA imenunua mahindi ya kutosha, basi mtupe kibali cha kufungua zizi, ili tuweze kuuza kwenye nchi jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la NFRA. NFRA pia wamefanya kazi nzuri sana, wamenunua mazao yetu kwa wingi, lakini changamoto ilikuwa ni kidogo tu, marekebisho kwenye suala zima la mizani. Mizani ilikuwa ni changamoto kubwa sana. Kwa hiyo, tunaomba safari hii mrekebishe mizani iweze kutenda haki, mkulima atakapokwenda pale amepima kilo zake 100 kutoka huko nyumbani kwake, lakini akifika pale akipima, kilo tano au kumi zinapungua. Kwa hiyo, muweze kurekebisha suala zima la mizani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, niongelee suala la mbegu. Tumeshuhudia kabisa wakulima wengi wanapenda sana mbegu za wenzetu wa Zambia, sijajua za kwetu tatizo ni nini? Ninachoomba ni kwamba, mfanye utafiti ili mbegu zetu ziweze kuingia kwenye ushindani wa masoko. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee pia suala la kuleta mbolea. Mbolea isiishie tu wilayani, iende mpaka vijijini, lakini pia mbolea hiyo iweze kuuzwa kwenye viroba vya kilo tano tano, kilo 50 na kilo 25 kwa sababu, kwenye Mikoa na wilaya zetu kuna wakulima wadogo na wakubwa ambao wana uwezo wa kununua kilo tano wanunue kilo tano, wenye uwezo wa kununua kilo 25, wanunue kilo 25. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, niongelee suala la ushuru. Suala la ushuru limekuwa ni changamoto huko, kwa sababu mkulima anapotoa mahindi yake shambani, tayari wataalamu wanafika pale kumtoza ushuru. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Bupe, muda wako umeisha.

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)