Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula (19 total)

MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, kwanza niruhusu nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa fursa ambayo nimeipata kuja kuuliza swali hapa. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa imani yake kubwa kwa kuniamini, nimefanya kazi na nimetua kijiti kwa Mheshimiwa Silaa na niko tayari kutoa ushirikiano wakati wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina swali la nyongeza. Kwanza natambua kwamba Serikali imeweka katika bejeti yake kuongeza chanzo kingine cha maji katika Jiji la Mwanza, hususan Manispaa ya Ilemela kutokana na changamoto kubwa ya maji katika mji ule: Je, ni lini utekelezaji wa mradi huo wa chanzo kipya cha maji utaanza kutekelezwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Angeline Mabula Mbunge wa Ilemela kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nipende kumpongeza kwa sababu suala hili amesha lileta mara kadhaa katika ofisi zetu na niseme tu jitihada zako zimesababisha Mheshimiwa Waziri Jumaa Hamidu Aweso kukuletea Mkurugenzi wa mamlaka mpya mwanamama, mchapakazi. Jitihada zako zimesababisha kuileta task force ya wataalam kuona kwamba Mwanza sasa inaenda kupata suluhu.

Mheshimiwa Spika, chanzo hiki kipya Mheshimiwa Dkt. Angeline Mabula naomba nikupe amani kwamba kadri wataalam wetu watakapo kamilisha kazi waliyopewa na Mheshimiwa Waziri Jumaa Hamidu Aweso, chanzo hiki mara moja kinakwenda kufanyiwa kazi ndani ya mwaka huu wa fedha.
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, ningependa kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, wamejenga barabara ya kilometa 2.5 ya breweries kwa kiwango cha lami kwa kilometa 1.7 na kimebaki kipande kidogo cha mita 750. Je, ni lini watakamilisha ujenzi huo kwa maana sasa ujenzi umesimama?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nitakaa na Mheshimiwa Mabula kuona ni namna gani ambavyo Serikali inaweza ikaliratibu hili na kukamilisha kipande hiki cha barabara ambacho kimesalia kwa kuwasiliana na Meneja wa TARURA, Mkoa wa Mwanza na Meneja wa TARURA, Wilaya ya Ilemela kuona ni kiasi gani kinahitajika ili kuweza kukamilisha ahadi hiyo.
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, naomba kumuuliza Naibu Waziri, kwanza kwa kuwashukuru namna ambavyo wanatatua kero ya maji katika Jiji la Mwanza hususani Wilaya ya Ilemela. Wamekuja na mkakati wa matokeo ya muda mfupi, wameanza kusambaza sim tank katika maeneo yenye changamoto.

SPIKA: Swali Mheshimiwa, mmesimama Wabunge wengi.

MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, swali langu ni kwamba walishafanya survey katika maeneo ambyo wanaweza kuchimba visima kwa ajili ya ku-save maji hapo;

Je, ni lini visima vitajengwa katika Kata ya Kayenze Mtaa wa Lutongo ambako tayari feasibility study imeshafanyika na maji yalipatikana?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Angeline Mabula kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tumeshafanya survey na baadhi ya maeneo katika vijiji hivyo alivyovitaja tumepata maji. Katika eneo la kata aliyoitaja tumepata maji kidogo lakini maji hayo tutahakikisha tutayatumia kujenga vichotea maji vichache ili wananchi wale waweze kupata huduma ya maji.
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ninashukuru kwa kunipa fursa na mimi niulize swali la nyongeza. Kwanza, ninashukuru kwa huduma tuliyoipata miundombinu katika Ziwa Victoria. Wilaya ya Ilemela asilimia 87 ni eneo la maji, na wanawake na vijana wengi wanashughulika na mazao ya samaki hususani dagaa lakini miundombinu yao ya kukausha samaki si mizuri hasa kwa afya ya binadamu. Ni lini Wizara itasaidia kuweka miundombinu kwa ajili ya kukausha samaki kwa wafanyabiashara hao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimesema kwamba Serikali imeshaanza na katika Ziwa Victoria tumeshaanza kuwasaidia Wavuvi namna ya kuvua zile samaki lakini pia kuhifadhi samaki. Hili wazo la Mheshimiwa Mbunge tumelichukua tutakwenda kulifanyia kazi kuwasidia Wavuvi wakanda ya ziwa. (Makofi)
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa nami niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Manispaa ya Ilemela katika kuunga mkono uwekezaji ilitenga eneo la ekari 52 katika eneo la Nyamungoro, eneo lenye miundombinu yote; maji, barabara na liko kwenye main road ya kwenda Musoma kwa ajili ya kuweka industrial park na tayari andiko lilishafika katika Ofisi za Serikali; ni lini mradi huu utatekelezwa ili tuongeze ajira na kukuza TEHAMA kwa watu wa Mwanza na ukizingatia ni ukanda wa maziwa makuu ni hub katika eneo hilo? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, maendeleo ya Industrial Park tunafanya pamoja na Wizara ya Viwanda, ipo chini ya EPZA. Nalifahamu hili eneo na nilishafika na tayari lipo katika Taasisi yetu ya EPZA wakilifanyia kazi, linaenda kwenye bodi na baada ya hapo tutalitolea maelekezo maalum kwamba ni lini hasa ratiba itatoka ya utekelezaji. Naamini katika mpango na bajeti ambao tutawasilisha kwenye Mkutano ujao, tutaeleza mpango maalum kuhusu Industrial Park ya Manispaa ambayo Mheshimiwa Angeline Mabula ameieleza.
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kinipa fursa na mimi kuuliza swali la nyongeza. Naomba kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Nyamhongolo katika Manispaa ya Ilemela walitoa eneo la square meter 6,339 kwa ajili ya kujenga miundombinu ya kituo cha polisi zikiwemo nyumba 12 pamoja na kituo chenyewe. Tayari nyumba sita zimekamilika na askari wapo, nyumba sita hazijakamilika na kituo kimefikia asilimia 75 kwa nguvu za wananchi.

Je, ni lini Serikali sasa itakamilisha miundombinu hiyo ili kituo hicho cha polisi kiweze kuanza kazi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mabula, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza kwa namna ambavyo anavyofuatilia kwa karibu na kuhakikisha kwamba ujenzi wa kituo kicho unakamilishwa. Kwa kweli kwa maendeleo makubwa yaliyofanyika katika Wilaya ya Ilemela, hasa kwa kuwa kituo hiki kiko karibu na Kituo Kikuu cha Mabasi cha Nyamhongolo; ni kipaumbele chetu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa Jeshi la Polisi kukipa fedha ili kiweze kukamilika. ninamwahidi Mheshimiwa, tutafuatilia maelekezo tuliyoyatoa ili ujenzi wa kituo hicho ukamilishwe, ahsante.
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa na mimi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Airport – Nyanguge yenye urefu wa kilometa 46 imekuwa ikiingia katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa vipindi viwili mfululizo na mwaka huu Serikali ilitangaza kujenga kilometa 10.

Je. Ni lini ujenzi huo sasa utaana ili kurahisisha by pass ya kwenda Serengeti kutoka Mwanza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, habari njema kwa Mheshimiwa Mbunge tender ilishatangazwa ya kilometa hizo 10 zilizokuwa zimehaidiwa. Nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge mara tutakapokuwa tumekamilisha kazi za tender ujenzi utaanza kwa sababu tunatambua pia ndiyo barabara ambayo itapunguza foleni. Ni kama by pass ya Mji wa Mwanza kuelekea Simiyu na Mara kupitia Barabara ya Airport.
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya Nyanguge – Airport yenye urefu wa kilometa 46, Serikali ilipanga kuijenga kwa kilometa 10 na tayari mkandarasi alipatikana. Je, ni lini mkandarasi huyu atakabidhiwa site ili aanze kazi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tumetangaza na Mkandarasi amepatikana, lakini kutokana na ukubwa wa barabara imehamishiwa, badala ya kusimamiwa na mkoa sasa itasimamiwa na TANROADS, Makao Makuu. Kwa hiyo, ni suala linalosubiri kumkabidhi mkandarasi hiyo site ili aanze kazi ya ujenzi. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, wananchi waishio katika Visiwa vya Besi na Tefu hawana maji safi na salama kwa maana ya maji ya bomba. Ni lini Serikali itawapelekea maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Angelina Mabula, Mbunge wa Ilemela, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kisiwa cha Base ni moja ya visiwa vidogo vidogo ambavyo viko katika Ziwa Victoria, lakini Ofisi ya Bonde la Ziwa Victoria walifanya tathmini na kugundua kwamba hakuna maji ardhini. Tunachokifanya kwa sasa kupitia Mamlaka ya Maji Mwanza, MWAWASA wanaenda kuanzisha mradi mdogo ili waweze kuchakata maji kutoka Ziwa Victoria kwenda katika kisiwa hicho ambacho zaidi kinakaliwa na wavuvi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Mbunge aendelee kushirikiana na Serikali kuhakikisha katika mwaka huu wa fedha 2024 tutaanza mradi huo na hatimaye wananchi wa kisiwa hicho watapata maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali iliweka minara katika maeneo ya visiwa base ambako kulikuwa hakuna mawasiliano, sasa hivi mawasiliano wanapata, changamoto waliyonayo hawana zile voucher za kukwangua na si wote waliozoea kununua kwa kutumia simu. Ni lini voucher hizo zitapatikana ili mawasiliano yao yawe mazuri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza kuhusu vocha za kukwangua, naomba niseme nimelipokea nitalifikisha kwa watoa huduma lakini kama Serikali tunaendelea kutaka kuboresha kuondokana na hizi hard copies na kuingia kwenye voucher moja kwa moja kupitia mtandao.
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu hili sasa naliuliza kwa mara ya tatu na Serikali inaahidi, lakini hakuna kinachofanyika. Naomba nimwulize Mheshimiwa Waziri kwamba, wananchi wamefanya kila juhudi kuweza kujenga boma na limefikia kwenye lintel, lakini tayari kuna maboma sita pale kwa ajili ya Askari: Je, ni lini watakamilisha kazi hii ili kituo kile kianze kufanya kazi na tayari kuna nyumba sita ambazo zina Askari, lakini wanakwenda mbali na kituo hakijaanza kutumika?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nawapongeza wananchi wa Jimbo la Ilemela kwa kazi kubwa walioifanya ya ujenzi wa maboma kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kazi ambayo wananchi walishaianza, Serikali inaunga mkono na nitapata fursa ya kukaa na Mheshimiwa Mbunge baada ya kipindi hicho niweze kuzungumza naye kuona namna bora ya kumalizia maboma haya ambayo tayari wananchi wameshayajenga.
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, Hospitali ya Rufaa ya Bugando inazidi kukua siku hadi siku na pale kuna Chuo Kikuu cha Afya na kuna Chuo cha Afya. Je, Serikali ipo tayari sasa kuhamisha Chuo cha Afya katika Manispaa ya Ilemela ambayo imetenga eneo la ekari 20 karibu na hospitali mpya ya wilaya ambayo Serikali imejenga? (Makofi)
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli Mheshimiwa Dkt. Angeline Mabula nimpongeze sana kwa jinsi anavyowapambania wananchi wa Ilemela na ni kweli nataka kukiri kwamba chuo chetu cha afya ambacho kipo katika Hospitali ya Rufaa Bugando kipo ndani ya hospitali, lakini hospitali nayo wana Chuo cha Afya Kikuu, kwa hiyo Wizara tayari ilishaliona hili la kukihamisha Chuo cha Afya cha Mafunzo ya Kati kilichopo Bungando. Kwa hiyo, kwa sababu umekuwa ni Mbunge wa kwanza wa Mkoa wa Mwanza kutupa ofa ya eneo naomba nikuahidi kwamba tutakuja Ilemela ili kujenga Chuo cha Afya Ilemela, tuwaachie Bugando waweze kufanya upanuzi wa majengo. (Makofi)
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Serikali. Napenda kuiuliza Serikali, ni sababu zipi ambazo zimefanya wabadili uamuzi wa awali ambapo ilikuwa wanatoa eneo la meta 700 kutoka kwenye njia ya kurukia ndege na sasa wanachukua eneo lote mpaka nje ya milima upande wa pili ambapo hapahitajiki kwa upanuzi wa Uwanja wa Ndege? Hilo ni swali la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, naishukuru pia Serikali kwamba zoezi la uthamini limeanza na lilipangwa kufanyika kwa siku 55, mpaka sasa hivi siku 38 zimekamilika, ni mitaa miwili tu ambayo imefikiwa ambayo ni Mtaa wa Bulyanhulu na Shibula bado mitaa mitatu; mtaa wa Kihili, Monze na Nyamwilolelwa. Je, ni lini kazi hiyo itakamilika kwa mitaa yote mitano ili wananchi waweze kupata haki yao?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge kuhusiana na eneo ambalo awali lilikuwa limepangwa, lakini baada ya tathmini ya kina na tukiangalia kwamba Serikali ina mpango mkubwa wa kufanya Uwanja wa Ndege wa Mwanza kuwa wa Kimataifa, vipo vigezo mbalimbali, kimojawapo ni usalama. Tathmini ya kiusalama ilipofanyika, ilidhihirika kwamba ni muhimu na ni lazima wananchi wa eneo lote lile wapishe ili tuweze kuwa na uwanja ambao siyo tu ni mkubwa, lakini pia unakidhi takwa la kisheria pamoja na la ukubwa kwa maana ya kiusalama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, kuhusiana na muda. Pendekezo la Mkoa kupitia Mkuu wa Mkoa la kuwatoa wananchi katika eneo lile kwa sababu za kiusalama lilipokamilika lilibidi liwasilishwe Serikalini na baada ya kupata idhini, tayari uongozi wa Mkoa pamoja na Kamishna wa Ardhi wa Mkoa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege wameshaanza mchakato kwa ajili ya uthamini. Mara tu tutakapokamilisha, tutaanza zoezi la kulipa.
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kutokana na mabadiliko ya tabianchi, barabara nyingi zimekuwa zikiharibika na kuifanya Serikali iwe na matengenezo ya mara kwa mara. Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kutumia rasilimali ya mawe tuliyonayo hasa katika maeneo ya miji ili kuwa na barabara imara ambazo hazitasumbua wakati wa mvua? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. ZAINAB A. KATIMBA): Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya Mheshimiwa Mbunge ni hoja ya msingi sana, kwa kutambua hilo, Serikali tayari imeshaanza kutumia teknolojia mbadala katika ujenzi wa barabara zetu hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tayari imeanza kutumia teknolojia ya barabara ambazo tunaziita eco roads ambazo zenyewe zina gharama nafuu katika ujenzi lakini pia zina life span kubwa zaidi, zinakaa kwa muda mrefu haziharibiki kama hizi barabara zetu zingine za kawaida. Pia teknolojia aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge ya kutumia mawe, kwa hiyo Serikali inatambua umuhimu mkubwa sana wa kutumia teknolojia hizi mbadala na tayari imeshaanza majaribio kwenye baadhi ya maeneo ili kuona ufanisi na ubora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuthibitika, baada ya hicho kipindi cha majaribio, Serikali inaona umuhimu mkubwa sana wa kujenga barabara hizi ambazo zitakuwa na gharama nafuu lakini zitaweza kuishi kwa muda mrefu zaidi na kupunguza adha ya wananchi kuharibikiwa na barabara na kupata changamoto kutokana na barabara zetu hizi kuharibika na hasa kipindi cha mvua. (Makofi)
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumwuliza Naibu Waziri kwa sababu sasa hivi Mwanza imekuwa ikisahaulika sana kwenye michezo kwa kutokuwa na timu ambayo imeingia kwenye Premier League na sasa hivi Pamba FC Wanatipilindanda wako katika Premier League. Ni lini uwanja wa CCM Kirumba utakarabatiwa ikiwa ni pamoja na ule wa mazoezi ya AFCON wa Ilemela utakuwa tayari?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nilijibu kwenye jibu la msingi, kwa sasa mpango uliopo ni kuanza kujenga kiwanja kipya cha Ilemela lakini hata Uwanja wa CCM Kirumba uko katika viwanja vitano ambavyo tunaanza navyo kuvikarabati ambavyo viko chini ya Chama cha Mapinduzi kama ambavyo nilishasema. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, asiwe na wasiwasi Wanatipilindanda watakuwa na sehemu ya kuchezea michezo yao ya Ligi Kuu kuanzia msimu ujao ambapo kitakuwa kimekarabatiwa na kitakuwa katika kiwango cha kupendeza.
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, napenda kuiuliza Serikali, ni nini mkakati wao kuhakikisha kwamba mazao yetu kwa zile mbegu za asili yanaendelea kuimarishwa katika vyuo vya utafiti ili kuepuka adha wanayoipata sasa hivi kwa kutumia mbegu za kisasa ambazo mkulima anakuwa tegemezi, kila mwaka lazima anunue mbegu mpya badala ile ya zamani ambayo ilikuwa unaweza ukapanda hata misimu sita hadi saba? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Mabula, Mbunge wa Ilemela, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama Serikali sasa hivi tumeshakusanya aina 330 za mbegu zetu za asili na tumeanza kuzifanyia mchakato wa kuzisafisha na kufanyia characterization. Vilevile tumefanya mabadiliko ya Kanuni ya Sheria ya Mbegu ili kuruhusu mbegu zetu za asili ziweze kuingia madukani kama certified seeds kama nyingine zilivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaamini kwamba baada ya mwaka mmoja kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu mbegu zetu za asili zitakuwa madukani kama zinavyoonekana hybrid seed au OPV seed. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wataalamu wetu wa TARI tayari wameshakusanya mbegu zaidi ya 300 zinafanyiwa characterization, zinasafishwa na tutaanza kuzifanyia multiplication na kuzigonga muhuri wa TOSCI na kuziingiza madukani ili Mtanzania aweze kuzipata kama anavyohitaji mbegu nyingine zozote.
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwanza nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuwa champion katika matumizi ya nishati safi. (Makofi)

Swali langu ni kwamba, je Serikali haioni ni wakati mwafaka wa kutoa ruzuku katika matumizi ya mitungi ya gesi ili wananchi wengi watumie gesi na waachane na masuala ya kutumia mkaa na kuni ili kulinda mazingira kama ambavyo Serikali inahamasisha? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Mabula, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, tunatekeleza mkakati mahususi wa Taifa juu ya nishati safi ya kupikia ambapo tumeanza mwaka huu 2024 hadi 2034. Moja ya eneo lililopo ndani ya mkakati huu ni kuona jinsi gani Serikali itaweza kushusha bei na unapoongelea kushusha bei ni pamoja na utoaji wa ruzuku ili bei iweze kushuka na Watanzania wengi waweze kufikia kwenye matumizi ya nishati safi na salama ya kupikia. (Makofi)
DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa uwezo wa Manispaa ya Ilemela ni mdogo kukabiliana na athari za mafuriko. Je, Serikali haioni sasa ni muda mwafaka wa kutenga fedha kwa ajili ya kukamilisha mto huu ambao ni kilometa 4.9 badala ya kutegemea pesa za wafadhili ambazo hazina uhakika?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwenye jibu lake la msingi ameongea kwamba ujenzi unaendelea; je, Mheshimiwa Waziri anatambua kwamba wataalamu wamemdanganya kwa kuwa ujenzi ule umesimama toka 2018, yuko tayari kuambatana na mimi ili akajionee mwenyewe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mabula.

Mheshimiwa Spika, kutokana na athari kubwa iliyojitokeza ya maji, maji ambayo yameenda kuharibu miundombinu ya school, maji ambayo yameenda kuharibu makazi ya wananchi lakini baadhi ya shughuli nyingine pia zimeathirika. Nimwahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba katika bajeti ya fedha ijayo tutahakikisha ujenzi wa Kingo za Mto Msuka tunahakikisha tunatenga fedha kwa ajili ya kuupa kipaumbele. Hilo asiwe na wasiwasi nalo na tutahakikisha kwamba tunaenda kuondoa changamoto hiyo.

Mheshimiwa Spika, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba nipo tayari kuambatana na yeye kwenda kuona athari ambayo imejitokeza na kuona namna ambavyo tunaweza tukawasaidia wananchi. Baada ya Bunge hili nimwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakwenda pamoja kwenda kuona ahari iliyojitokeza, nakushukuru.
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, Kituo cha afya Sangabuye kilipandishwa hadhi mwaka 1999 kutoka zahanati na kuwa kituo cha afya. Kituo hicho mpaka leo kina wodi moja ambayo inatumika na wanawake, wanaume pamoja na watoto. Je, ni lini Serikali itakamilisha miundombinu ya pale ikiwa ni pamoja na kujenga uzio? (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Angelina Mabula, watoto, wanawake na wanaume wanalazwa kwenye wodi moja?

MHE. ANGELINA S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, ndiyo.

SPIKA: Wanawezaje kulazwa wodi moja?

MHE. ANGELINA S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, ndivyo ilivyo.

SPIKA: Mheshimiwa Mbunge, napata wasiwasi, wanalazwaje wanaume na wanawake kwenye wodi moja? Yaani wameweka mapazia au ni nini?

MHE. ANGELINA S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, katika kituo hicho cha afya unaweza ukakuta kitanda hiki amelazwa mwanamke, kitanda kinachofuata kuna mwanaume, kingine kuna mwanamke ana mtoto ndani ya wodi moja. Pia ni toka mwaka 1999 miundombinu hiyo haijakamilika na nilishauliza hilo swali. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa utaratibu na sera ya Wizara ya Afya, hairuhusiwi kulaza wagonjwa kwa maana ya wanawake na wanaume katika wodi moja. Kwa hiyo, kwa taarifa hii, Ofisi ya Rais, TAMISEMI tunaipokea taarifa kwamba kuna tatizo katika Menejimenti ya hospitali hiyo na Manispaa yenyewe.
Mheshimiwa Spika, naomba niichukue hoja hii mapema iwezekanavyo, kwanza nimwelekeze Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala kwa niaba ya Waziri wa Nchi.

MBUNGE FULANI: Halmashauri ya Ilemela.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni Halmashauri ya Ilemela; leo hii afike pale mara moja na atupatie taarifa rasmi Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kuona namna nzuri ya ku-manage wagonjwa katika wodi zile kwa sababu haikubaliki kulaza wanaume na wanawake katika wodi moja.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, Manispaa ya Ilemela ina uwezo angalau wa kuanza ujenzi wa wodi. Nimwelekeze Mkurugenzi, kupitia mapato ya ndani kwa dharura, wafanye reallocation waanze ujenzi wakati Ofisi ya Rais, TAMISEMI ikitafuta fedha kwa ajili ya kuwaunga mkono, kwa ajili ya ujenzi wa wodi hiyo muhimu, ahsante.(Makofi)