Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Deus Clement Sangu (26 total)

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, lakini tumekuwa tukiona taasisi mbalimbali kwa mfano TRA, Benki Kuu, Bandari na taasisi nyingine mbalimbali ambazo zinawapa vijana nafasi za kujitolea, lakini hakuna utaratibu maalumu ambao umewekwa wa kujua kwamba hawa vijana wanaenda kupata hizo nafasi namna gani na hii inaweza ikatokea ama boss ama mfanyakazi akaweza kumpa nafasi hiyo matokeo yake tunavyokuwa tunaomba vijana hawa wapate ajira kwa sababu wamejitolea unakuta unaweka mlolongo wa walewale ambao wako katika ofisi hiyo.

Sasa swali langu hapa, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba mna utaratibu maalumu wa kuwapata vijana wanaojitolea katika taasisi mbalimbali hata Serikalini?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, pamoja na kusema kwamba kuna mwongozo au taratibu ambazo mmeziweka, ni lini sasa mwongozo huu utatoka hara ili vijana wetu waweze kupata nafasi hizo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana naomba kujibu maswali mawili madogo ya nyongeza ya Mheshimiwa Grace Tendega, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa namna ambavyo amekuwa akiwasemea vijana wa kitanzania hasa awale ambao wamekuwa wakijitolea amepaza sauti sana kuwasemea.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali mawili yake ya nyongeza kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi kwamba Serikali inatambua na baada ya kuona changamoto hiyo hasa katika taasisi mbalimbali kwa namna ambavyo wanawapata vijana wa kujitolea. Tuko mbioni tunaandaa randama ambayo baada ya kukamilika tutatoa waraka namna na utaratibu wa kuwapata vijana hawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee Serikali imeona kwamba itaweka utaratibu wa ushindani ilikijana aende kujitolea sehemu tunaenda kuweka utaratibu kama tunavyofanya kwenye ajira za sasa ambazo zimetangazwa kwenye kada ya ualimu, kada ya afya na kada nyinginezo. Kwa hiyo, nimuondolee shaka Mheshimiwa Mbunge, Serikali inalitambua hilo na ndio maana imeingia kwenye mchakato huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lini tutatoa waraka huo, naomba nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kabla ya kukamilika kwa mwaka huu wa fedha tayari waraka huu utakuwa umetoka kuwaongoza Wakuu wa Taasisi namna ya kuwapata vijana wa kujitolea, ahsante. (Makofi)
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, nipongeze kwanza Serikali, wamesema sasa walau wameshusha kwa ngazi ya mkoa, lakini ninayo maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza: Je, Serikali haioni iko haja sasa ya kutambua mahitaji ya nafasi hizi za kazi kwa kila jimbo ili kutoa msawazo sawa na baadaye kuratibiwa kitaifa ili kulinda utaifa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, wako vijana ambao walihitimu vyuo mbalimbali kuanzia 2015 mpaka 2020 na kwa sasa kwa kutumia mfumo hawa vijana ni kana kwamba mfumo unawakataa. Je, Serikali haioni iko haja sasa ya kutoa upendeleo maalum kwa hawa vijana ambao kwa sasa kwa sababu ya umri unavyokwenda wanaachwa sasa kwenye mfumo wa ajira? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba kujibu maswali mawili madogo ya nyongeza ya Mheshimiwa Amandus kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza ametaka kujua kwamba Serikali ina mpango gani wa juu ya kushusha hizi ajira katika ngazi ya majimbo kwa maana hiyo. Bunge lako Tukufu lilitoa maelekezo kwa Serikali kwamba wahakikishe ajira hizi zinashuka katika ngazi za mikoa. Katika kutekeleza hilo na commitment ambayo Serikali ilitoa ndani ya Bunge hili, tayari utekelezaji huo umeanza ambao tumeanza katika ngazi ya mkoa na usaili utafanyika katika ngazi ya mkoa ambapo utahusisha Sekretarieti za Mikoa na Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, baadaye kwa kuwa safari ni hatua, tayari Serikali itaendelea kujipanga kwa namna ya kushuka katika ngazi ya wilaya. Kwa hiyo, nimwondolee shaka Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imekuwa ikisikiliza maelekezo ya Bunge na ushauri wa Waheshimiwa Wabunge na ushauri wake tunaupokea, tutaingiza katika utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ameuliza habari ya kwamba ni namna gani Serikali imejipanga sasa kuangalia wale waliohitimu kwa miaka ya nyuma. Ni kweli katika nyakati mbalimbali Serikali imetumia hiyo approach ya kuchukua wale wa miaka ya nyuma na ndani ya Bunge humu tulipata ushauri huo, lakini kiukweli ukiangalia wale wanaohitimu na namna ambavyo Serikali imekuwa ikitoa ajira nafasi zinakuwa ni chache. Kwa hiyo, ukienda kwa mtindo huo unaweza ukakuta tunakaa ndani ya mwaka mmoja.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka mmoja, kwa mfano waliohitimu 2015 tunakaa tunaajiri ndani ya miaka sita, kwa hiyo, tatizo litakuwa pale pale, ndiyo maana tumerejea kufuata kwenye Sera ya Ajira na Utumishi kwamba sasa waende kwenye ushindani na katika ushindani ili kuzingatia pia waliomaliza kwa miaka ya nyuma, Serikali imeweka utaratibu mzuri wa kwamba kama endapo waliokuwa kwenye ushindani wamefungana kwa marks na yule ambaye ana umri mkubwa atapewa kipaumbele, nashukuru. (Makofi)
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nilitaka nimwulize Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba je, wapo tayari kutoa hadharani vigezo wanavyotumia kwa vijana kupata ajira ili kuondoa usumbufu wa vijana wanaoomba ajira, kusumbua Wabunge wakidhani kwamba ukituma message kwa Mbunge atakuombea ajira ili wajue kwamba ajira inatolewa kwa haki na mtu atakayeomba ana sifa atapata nafasi hiyo, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Ni wazi kwamba kupitia Sekretarieti ya Ajira, vigezo vyote viko wazi na kwa namna ambavyo tunafanya usaili, matokeo yanatoka wazi na wale ambao wanatokea kukosa wanapewa sababu. Hata hivyo, tumetoa fursa ya kwamba yule ambaye anadhani hakutendewa haki, amepewa fursa ya kukata rufaa. Kwa hiyo, vigezo vyote viko wazi na kila Mtanzania yuko wazi kuomba kwa kadri ya nafasi anayotaka, nashukuru. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Tulikuwa tunajadili suala la wale vijana ambao wanajitolea kwenye shule zetu kufundisha au kutoa huduma kwenye vituo vya afya. Serikali imekuwa inaahidi kwamba itatoa kipaumbele wakati wa kutoa ajira kwa hawa wanaojitolea. Je, Serikali imechukua hatua gani angalau kuchukua kuunda kanzidata ya hawa vijana wanaojitolea? Mimi najua kwamba watu wa Jimbo la Vunjo iliwasilisha orodha ndefu tu ya vijana wanaojitolea, naomba kupewa jibu.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali hilo la Mheshimiwa Dkt. Kimei kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeweka utaratibu mzuri katika ajira safari hii. Kweli vijana wanaojitolea katika sehemu zetu huko katika Serikali ni wengi, tumechukua kanzidata na tukaona kwamba suala la wanaojitolea halitakuwa automatic, nao wataingia kwenye mfumo wa ushindani, lakini mwishoni yule aliyejitolea atakuwa na added advantage ukilinganisha na yule asiyejitolea.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, Serikali inaandaa mfumo mzuri ambao tutawabaini kwanza namna ya kuwapata hao wanaojitolea na pia hawa wanajitolea wamekuwa wakifanya kazi pia kuona namna hata ya kuwapatia stahiki ili waweze kupata morali ya kuweza kujitolea. Kwa hiyo, Serikali ina utaratibu mzuri na tumeshauandaa hivi karibuni tutau-submit. (Makofi)
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, kwa sababu tatizo la ajira mpya kuhama kwenye Halmashauri zile za pembezoni limekuwa ni kubwa sana, nini kauli ya Serikali juu ya watumishi hawa ambao wanaajiriwa baada ya miaka mitatu wote wanakuwa wameondoka kabisa kwenye vituo vyao vya kazi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imeweka utaratibu mzuri kwamba mtumishi anapoajiriwa anatakiwa kukaa kwenye kituo cha kazi miaka isiyopungua mitatu. Hata hivyo, kuna taratibu mbalimbali ambazo ni miongozo kwamba hata kuomba uhamisho na sasa hivi tumeanzisha mfumo mzuri ambao waajiri wanaomba uhamisho kupitia kwenye mfumo unaitwa e-Uhamisho.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge na hata katika ajira hizi tulizotangaza zimetangazwa kimkoa. Naomba niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba baadhi ya kada za afya hasa mikoa ile ya pembezoni zimekosa wanaoomba, nafasi ni nyingi lakini wanaoomba wamekuwa wachache hasa mikoa ya pembezoni mfano Mtwara, Kigoma na Mkoa wa Lindi.

Mheshimiwa Spika, natoa rai kwa waombaji wasikimbilie tu kuomba nafasi hizi sehemu za mijini kwa sababu huko kuna ushindani mkubwa. Niwaase pia waombe huko kwa sababu pia Serikali imeweka vizuri miundombinu kama vile maji na huduma nyingine za kijamii. Kwa hiyo, wasihofu kuomba ajira katika sehemu za mikoa ya pembezoni, nakushukuru.
MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa takwimu zinaonesha kwamba kumekuwa na ongezeko kubwa la ndoa nyingi zinazovunjika baada tu ya miaka miwili ya kufungwa kwake. Kufuatia takwa la Sheria za Ndoa la mwaka 1971, Serikali haioni haja ya kuondoa au kupunguza takwa hili au kigezo hiki cha miaka mitatu kwa waajiriwa wanaotafuta uhamisho kwa kigezo cha kufuata wenza wao? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa ni ukweli usiopingika kwamba malezi mazuri ya watoto na kuwepo kwa familia imara na bora kunategemea malezi ya wazazi wote wawili na sasa hivi nchini tumekuwa na changamoto kubwa sana ya mmomonyoko wa maadili kwa watoto. Hatuoni haja au Serikali haioni haja ya kuondoa kabisa kigezo hiki cha miaka mitatu kwa watu wanaotafuta uhamisho? Au kuwaweka moja kwa moja waajiriwa ambao ni wanandoa sehemu moja ya ajira? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Kamani kwa namna ambavyo anafuatilia masuala ya haki za watumishi ikiwemo uhamisho.

Mheshimiwa Spika, katika kujibu swali lake anasema kwamba kigezo cha miaka mitatu kuondolewa, Serikali iliweka kigezo hiki cha miaka mitatu kwanza ili kuweka stability ya taasisi, kwa maana ya kwamba ukiruhusu watumishi wakakaa kwa muda mfupi namna ya ku-retain na performance ya taasisi inaweza kushuka. Hii imeoneshwa katika Mikoa ya Pembezoni baada ya kuweka muda mfupi watumishi wengi wanachukua check number na kuondoka na baadaye kupelekea uhaba wa watumishi.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, Serikali imeendelea kutoa vibali vya uhamisho kwa wale watumishi hasa wanaotaka kuungana na wenzao. Kwa mwaka wa fedha 2023/2024, maombi yalikuwa takribani 3,374 na Serikali imetoa vibali 1,136. Kwa hiyo, Serikali itaendelea na jitihada hiyo bila kuathiri haki na maombi ya hawa watumishi wanaoomba kufuata wenza wao. (Makofi)
MHE. MUNIRA MUSTAPHA KHATIB: Mheshimiwa Spika, je, Serikali haioni haja ya kuongeza kigezo cha ‘mwenza wako’ wakati wa kuomba ajira ili kuwarahisishia watumishi kuwapangia mkoa ambao alikuwa anatoka mwenza wake na kuweza kupunguza gharama za kuhamisha watumishi hawa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, Serikali imetambua jambo hilo na ndiyo maana katika mwaka huu ajira zilizotangazwa 47,404, Serikali imewapa uhuru waombaji wa ajira hizo kuomba mikoa hiyo wanayotaka na lengo kubwa ni wao kwenda sehemu wanazotaka ili kuzuia wimbi hili la kuomba uhamisho kila wakati. Nakushukuru.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niulize swali. Kwenye halmashauri nyingi ambazo sisi tunakutananazo Kamati ya LAAC kumekuwa na watumishi wanaokaimu muda mrefu kiasi kwamba wanashindwa kufanya maamuzi sahihi kutokana na kukaimu. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha mnajaza nafasi kwenye halmashauri zote nchini ili kuwe na ufanisi na utendaji kazi ambao unaridhisha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, suala la kukaimu ni kweli limelalamikiwa na Serikali tumelichukua kwa uzito mkubwa. Hivi sasa kupitia Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, tuna zoezi la kufanya assessment nchi nzima kuona wale watumishi wanaokaimu katika nafasi mbalimbali. Wale watakaokuwa wamekidhi vigezo, tayari Serikali imeandaa utaratibu wa kuwa-confirm na wale ambao watakua hawajakidhi vigezo basi utaratibu mwingine wa kujaza nafasi zile utafanyika. Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na vilevile namshukutu na kumpongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu haya mazuri ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na changamoto ya muda mrefu ya kusomana kwa mifumo ambayo Mheshimiwa Waziri ameitaja na mifumo mingine ya Serikali. Kwa kuwa kuna ahadi na mapendekezo mbalimbali ambayo yametolewa ndani ya Bunge na nje ya Bunge ya kwamba mifumo hii inakwenda kuunganishwa, sasa nataka kujua, katika utekelezaji huu Serikali imefikia wapi ili kuongeza uwazi, uwajibikaji na ufanisi kazini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwanza, nampongeza Mheshimiwa Bakar Hamad kwa kufuatilia habari ya mifumo kusomana. Kwa kweli hili ni agizo la Mheshimiwa Rais katika nyakati mbalimbali kuhakikisha mifumo inasomana. Vilevile, katika kuchukua hatua, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, kupitia taasisi yake ya e-GA ikishirikiana na Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, imejenga mfumo wa kuwezesha mifumo kusomana ambao unaitwa Government Enterprises Service Bus. Mfumo huo mpaka kufikia tarehe 30 Septemba, 2024 umesaidia taasisi zaidi ya 175 mifumo yao kusomana na kubadilishana taarifa, ikiwemo ile mifumo muhimu ya Hakijinai, Polisi, Mahakama na PCCB. Nakushukuru.
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa vile mifumo hii pia inatumika kupima utendaji kazi wa watumishi, je, Serikali ina mpango gani kwa wale watumishi ambao wako pembezoni ambako hakuna mitandao na pia wale wenye kazi kubwa ili zile asilimia wanazowapimia kufika waweze kupanda vyeo na shughuli nyingine? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Dkt. Alice Kaijage kwa kufuatilia masuala yanayohusu watumishi. Naomba nimhakikishie kwamba, tulipoanza zoezi la kuwapima watumishi, hatukupata malalamiko ya watumishi kushindwa kuingia kwenye mfumo wa PEPMIS kwa maana ya kujipima.

Mhshimiwa Spika, hata hivyo, kwa kutambua kwamba maeneo mbalimbali ya nchi yanakumbana na changamoto ya mitandao, Ofisi ya Rais, Utumishi imeendelea kushirikiana na Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, katika programu yao ya Tanzania ya Kidigitali, kuhakikisha minara inajengwa nchi nzima na mawasiliano yanakuwepo ili watumishi wa umma nao watakapokuwa wanatumia mifumo yao katika kujipima, wasiweze kupata changamoto, nakushukuru. (Makofi)
MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa takwimu zinaonesha kwamba kumekuwa na ongezeko kubwa la ndoa nyingi zinazovunjika baada tu ya miaka miwili ya kufungwa kwake. Kufuatia takwa la Sheria za Ndoa la mwaka 1971, Serikali haioni haja ya kuondoa au kupunguza takwa hili au kigezo hiki cha miaka mitatu kwa waajiriwa wanaotafuta uhamisho kwa kigezo cha kufuata wenza wao? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa ni ukweli usiopingika kwamba malezi mazuri ya watoto na kuwepo kwa familia imara na bora kunategemea malezi ya wazazi wote wawili na sasa hivi nchini tumekuwa na changamoto kubwa sana ya mmomonyoko wa maadili kwa watoto. Hatuoni haja au Serikali haioni haja ya kuondoa kabisa kigezo hiki cha miaka mitatu kwa watu wanaotafuta uhamisho? Au kuwaweka moja kwa moja waajiriwa ambao ni wanandoa sehemu moja ya ajira? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Kamani kwa namna ambavyo anafuatilia masuala ya haki za watumishi ikiwemo uhamisho.

Mheshimiwa Spika, katika kujibu swali lake anasema kwamba kigezo cha miaka mitatu kuondolewa, Serikali iliweka kigezo hiki cha miaka mitatu kwanza ili kuweka stability ya taasisi, kwa maana ya kwamba ukiruhusu watumishi wakakaa kwa muda mfupi namna ya ku-retain na performance ya taasisi inaweza kushuka. Hii imeoneshwa katika Mikoa ya Pembezoni baada ya kuweka muda mfupi watumishi wengi wanachukua check number na kuondoka na baadaye kupelekea uhaba wa watumishi.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, Serikali imeendelea kutoa vibali vya uhamisho kwa wale watumishi hasa wanaotaka kuungana na wenzao. Kwa mwaka wa fedha 2023/2024, maombi yalikuwa takribani 3,374 na Serikali imetoa vibali 1,136. Kwa hiyo, Serikali itaendelea na jitihada hiyo bila kuathiri haki na maombi ya hawa watumishi wanaoomba kufuata wenza wao. (Makofi)
MHE. MUNIRA MUSTAPHA KHATIB: Mheshimiwa Spika, je, Serikali haioni haja ya kuongeza kigezo cha ‘mwenza wako’ wakati wa kuomba ajira ili kuwarahisishia watumishi kuwapangia mkoa ambao alikuwa anatoka mwenza wake na kuweza kupunguza gharama za kuhamisha watumishi hawa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, Serikali imetambua jambo hilo na ndiyo maana katika mwaka huu ajira zilizotangazwa 47,404, Serikali imewapa uhuru waombaji wa ajira hizo kuomba mikoa hiyo wanayotaka na lengo kubwa ni wao kwenda sehemu wanazotaka ili kuzuia wimbi hili la kuomba uhamisho kila wakati. Nakushukuru.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niulize swali. Kwenye halmashauri nyingi ambazo sisi tunakutananazo Kamati ya LAAC kumekuwa na watumishi wanaokaimu muda mrefu kiasi kwamba wanashindwa kufanya maamuzi sahihi kutokana na kukaimu. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha mnajaza nafasi kwenye halmashauri zote nchini ili kuwe na ufanisi na utendaji kazi ambao unaridhisha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, suala la kukaimu ni kweli limelalamikiwa na Serikali tumelichukua kwa uzito mkubwa. Hivi sasa kupitia Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, tuna zoezi la kufanya assessment nchi nzima kuona wale watumishi wanaokaimu katika nafasi mbalimbali. Wale watakaokuwa wamekidhi vigezo, tayari Serikali imeandaa utaratibu wa kuwa-confirm na wale ambao watakua hawajakidhi vigezo basi utaratibu mwingine wa kujaza nafasi zile utafanyika. Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. OMAR ALI OMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwenye Jimbo langu la Wete kuna wananchi ambao wametolewa katika mfuko huu kimyakimya. Je, Serikali inafahamu mpango huo?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; Mheshimiwa Waziri yuko tayari kuongozana nami baada ya kumalizika kwa Bunge hili ili kwenda kuona na kutatua changamoto ambazo zimejitokeza katika jimbo langu kwenye Mfuko huu wa TASAF?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Omar Ali kwa namna ambavyo amekuwa akifuatilia masuala haya yanayohusu TASAF.

Mheshimiwa Spika, kuhusu wananchi wake kuondolewa kimyakimya, utaratibu uliopo ambao umewekwa na TASAF ni kwamba, wale wanaohitimu na kuimarika kiuchumi, kabla hawajaondolewa, kwanza wanapewa mafunzo na kuwaandaa na baadaye kupewa taarifa rasmi kwamba sasa mmefikia kwenye ukomo. Kama jambo hilo limetokea jimboni kwake, naomba kuchukua fursa hii kumwelekeza Mtendaji Mkuu wa TASAF afuatilie jambo hili na kama hawa hawakutaarifiwa, waweze kupata taarifa kufuatana na taratibu tulizoweka.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kufuatana naye kwenda jimboni, hili halina shaka, tukimaliza Shughuli za Bunge hapa tutaenda huko Pemba ili tukaone namna ya kuzungumza na kutatua changamoto hizi kwa pamoja. Ninakushukuru.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa TASAF haiwezi kugusa maskini wote wa Tanzania na kwa kuwa maskini waliopo ni wengi sana sana wakiwemo vijana waliomaliza vyuo ambao hawana kazi bado wanategemea wazazi; wakiwemo wanawake ambao wanangoja kuguswa tu ili waweze kufanya miradi, wakiwemo pia hata akinababa ambao hawawezi kumudu chakula kwenye nyumba zao. Je, Serikali haioni sasa ni wakati wa kutoa miradi midogomidogo kwa makundi hayo niliyotaja badala ya kusema wote wakaguswe na TASAF? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana. Kama Programu ya TASAF ilivyo, ina programu ambayo tulianza 2012 – 2019 na tuko awamu ya pili katika kunusuru kaya maskini ambayo itaenda 2019 mpaka 25 Septemba, mwakani. Serikali ina utaratibu mzuri, kuna namna ambavyo inawezesha haya makundi kwa mfano kupitia halmashauri kuna mikopo ya 4:4:2 na yote hii ni namna ambayo Serikali imejipanga namna ya kuwakwamua wananchi katika umaskini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo na pamoja kwamba kuna Programu ya TASAF, bado pia Ofisi ya Waziri Mkuu ina programu ya mikopo kwa vijana ambayo inafanya ushirikiano pia pamoja na TASAF ambao wale vijana wanaotoka kaya maskini, wanaoshindwa, wanamaliza darasa la saba na kutokufanikiwa kwenda kidato cha kwanza, wameunganishwa na programu ya kwenda Ofisi ya Waziri Mkuu kupata mikopo ya kusomeshwa VETA bure. Ninashukuru. (Makofi)
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, TASAF kwa kweli bado ni tatizo kubwa katika jimbo langu. Wengi waliomo mle hawastahili na walioachwa ndiyo wanastahili. Ninaomba kama akipata nafasi tuweze kuongozana naye kwenda Mwibara ili kuondoa hili tatizo ambalo limejitokeza, je, yuko tayari? Ninakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Kajege kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, utaratibu wa kuwapata wanufaika wa kaya maskini ulifanyika kupitia mikutano ya vijiji. Kwa hiyo vijiji na wananchi ndiyo waliamua nani anufaike na nani asiingie kwenye kunufaika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo TASAF kwa maana ya TASAF waliletewa watu ambao tayari wamepitia katika michakato ya kijiji. Kama kuna tatizo kwenye jimbo lako Mheshimiwa Kajege, kupitia Bunge hili ninaomba kumuahidi tutafika huko ili tuone namna ya kutatua changamoto hii.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini pamoja na majibu hayo kuna ukweli kwamba kuna baadhi ya matatizo kwa watumishi wetu yanasababishwa na uzembe au kukosa weledi kwa baadhi ya Maafisa Utumishi. Kwa mfano, kuna walimu walioajiriwa mwaka 2018 mwezi Aprili, wamepandishwa madaraja mwaka 2021/2022, lakini mwaka huo huo kuna baadhi ya walimu wamepandishwa madaraja mwaka 2023/2024.

Mheshimiwa Naibu Spika, unakuta kwamba walimu wameajiriwa mwaka mmoja lakini wanatofautiana sana kimuundo na kimaslahi. Je, Serikali haioni kwamba inawakatisha tamaa walimu hawa na kwa hiyo ina wajibu wa kuchukua hatua kufanya marekebisho hayo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kuna walimu walioajiriwa kabla ya mwaka 2018, lakini wana sifa zilezile sawa na wale walioajiriwa mwaka 2018 kuendelea na wamepandishwa madaraja, wale walioajiriwa kabla hawajapandishwa madaraja. Serikali inasemaje katika kuwarekebishia muundo walimu hawa walioajiriwa kabla ya mwaka huu? Ninashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ninachukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Joseph Mkundi kwa namna ambavyo anawasemea walimu wa Tanzania, lakini kipekee walimu wake katika Jimbo la Ukerewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali yake yote mawili kwa pamoja, kwanza ninaomba nimwondoe shaka, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan, haina nia na wala kwa wakati wowote haitawakatisha tamaa walimu wa Tanzania kwa sababu wanafanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jitihada kubwa imefanyika, kwa Mwaka huu wa Fedha 2024/2025, Serikali imetenga bajeti ya shilingi bilioni 252.7 kwa ajili ya kutatua changamoto hizo ikiwemo kuwabadilishia miundo wale waliocheleweshewa na wale ambao walistahili kupandishwa vyeo ambapo Maafisa Utumishi hawakuleta taarifa Ofisi ya Rais Utumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kupitia Bunge hili, nichukue nafasi hii kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, kuwaelekeza waajiri kwa maana ya Wakurugenzi, wakishirikiana na TSC, kuhakikisha walimu wote waliosahaulika kwenye suala la miundo na promotion, walete taarifa hizo Ofisi ya Rais Utumishi ili tuweze kutatua changamoto hii. Ninashukuru. (Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kutokana na jibu lake la msingi Mheshimiwa Waziri anasema, walimu wanaenda kujiendeleza bila mwajiri kujua ndiyo maana inakuwa ngumu kwa Serikali kuweza kuwapandisha. Hamwoni kama mnawakatisha tamaa kwa kuwa Serikali haina fedha ya kuwasomesha au kuwaendeleza walimu hao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru. Nitoe ufafanuzi, kwenye hili, walimu ninaowaongelea ni wale ambao hawakuomba ruhusa wakajiendeleza bila mwajiri kufahamu, lakini hata hivyo baada ya kujiendeleza Serikali inatambua jitihada kwa kuwa tunaamini mwalimu anapojiendeleza anakuwa na tija katika kazi yake. Kwa hiyo ninaomba nimwondoe shaka Mheshimiwa Sophia kwamba hata hawa baada ya kutambulika, tayari Serikali kama nilivyosema imeandaa bajeti nao watapewa kipaumbele, hakuna mwalimu atakayesahaulika.
MHE. ABDUL YUSSUF MAALIM: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Naomba kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza. Kwa kuwa fedha hizi za Mfuko wa TASAF huwa zinachelewa, je, Serikali ina mkakati gani wa kuharakisha fedha hizi ili ziweze kunufaisha wananchi kwa wakati?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza wanufaika wa Mfuko huu wa Maendeleo wa TASAF ili kuweza kuwanufaisha wananchi wakiwemo wa Jimbo la Amani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwanza nimpe pole Mheshimiwa Abdul kwa matatizo aliyoyapata, lakini namshukuru Mwenyezi Mungu, amerudi akiwa salama na anaendelea kupambana kuwatetea wananchi wake wa Jimbo la Amani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali yake mawili ya nyongeza, kwanza ameuliza habari ya fedha za Miradi ya TASAF kuchelewa. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa, siyo kwamba fedha hizi zinachelewa, isipokuwa utekelezaji wa miradi hiyo unahusisha wadau mbalimbali. Kwa mfano, tunapopeleka fedha zile zinakwenda kuhudumia sekta ya elimu, maji na afya. Sasa pale kuna wadau kama Wizara ya Elimu, Wizara ya Afya na Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na michakato mingi, lakini sisi pamoja na hawa wadau tumekaa, tumeweza ku-stream line na baada ya hapo tumeboresha zaidi kupunguza urasimu ili fedha hizo zifanye kazi kwa wakati na kuwanufaisha wananchi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge nikuondoe shaka, tutahakikisha jambo hilo linafanyika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kuongeza wanufaika ni kweli baada ya programu hii kukamilika mwitikio umekuwa mkubwa na kila mahali watu wanataka kunufaika na mpango huu wa TASAF. Nakuhakikishia kwamba, baada ya awamu hii ya pili kukamilika, mwezi Septemba mwaka huu tunakuja na awamu ya tatu, na awamu hii Serikali imejipanga vizuri kuhakikisha wanufaika wanakuwa wengi zaidi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, tulipokuwa tunahamasisha sensa, tulikuwa tunawahakikishia wananchi kwamba kati ya matumizi ya takwimu zile, ni kutathmini upya zile orodha za watu wanaonufaika na TASAF, na kulikuwa na maswali mahsusi kuhusiana na hali ya umaskini kwenye kaya.

Mheshimiwa Spika, nataka nimwulize Mheshimiwa Waziri, je, ni lini sasa watatumia zile takwimu ili kuhakikisha kwamba kaya kadhaa za wananchi wa Vunjo ambazo wanaendelea kulalamika wanapata haki yao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Kimei, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli katika utekelezaji wa awamu ya pili ya TASAF kulikuwa na changamoto na malalamiko mengi. Baada ya kutambua hilo, ili kuboresha zaidi, Ofisi ya Rais, Utumishi tukishirikiana na taasisi nyingine kama Wizara ya Fedha kupitia Ofisi ya Takwimu, tumekaa pamoja na tayari tumefanya tathmini.

Mheshimiwa Spika, katika mpango mwingine, kwa maana ya awamu ya tatu ya TASAF itakayoanza baada ya Septemba, 2025, tutahakikisha tunatumia hizi taarifa ambazo tunashirikiana na Ofisi ya Takwimu kuhakikisha kwamba yale manung’uniko na lawama zote tunazimaliza kwa kuhakikisha wale walengwa sahihi wananufaika na mfuko huu, ahsante. (Makofi)
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza; katika miaka minne ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Serikali imeajiri takribani watumishi 140,000. Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba inatoa mafunzo elekezi ya awali kwa watumishi wapya ambao wanaajiriwa katika utumishi wa umma?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba taasisi zinapanga bajeti ya mafunzo kwa watumishi kazini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Simon kwa namna ambavyo amekuwa akifuatilia mambo ya watumishi hasa wa Jimbo lake la Busega. Nikianza na suala la mafunzo elekezi kwa waajiriwa wapya, ni kweli Serikali kwa kipindi hiki cha miaka minne imeweza kuajiri watumishi takribani 140,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, mwaka 2011 Serikali ilitoa waraka kwa taasisi zote za umma kuhakikisha watumishi wanaoajiriwa kwa mara ya kwanza wanapewa mafunzo elekezi ndani ya miezi sita.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kutumia Bunge hili Tukufu kukumbusha waajiri wote, wanapowapokea waajiriwa kwa mara ya kwanza wahakikishe wanawapa mafunzo hayo elekezi ili waweze kujua taratibu, misingi ya utumishi wa umma, kanuni na sheria na pia utendaji bora katika utumishi wa umma. Hii imeelezwa wazi kwamba wale wanaoajiriwa Serikali Kuu na mashirika ya umma watapewa mafunzo na Chuo chetu cha Utumishi wa Umma; wale wanaoajiriwa kwa maana ya Serikali za Mitaa jukumu hilo kimepewa Chuo cha Serikali za Mitaa pale Hombolo; na wale wanaoajiriwa kwa kada za sheria watatakiwa kupata mafunzo elekezi na Chuo cha Uongozi wa Mahakama kwa maana ya Lushoto. Ninashukuru sana.

NAIBU SPIKA: Ahsante.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, anataka kujua juu ya bajeti, tayari Serikali tulishatoa waraka kwa maana Ofisi ya Rais, Utumishi, kuhakikisha waajiri wote kwa mwaka huu wa fedha wanatenga bajeti ya kutosha kwa ajili ya mafunzo na mwishoni mwa mwaka huu wa fedha tutafanya tathmini tuone utekelezaji wa jambo hilo kwa kuwa ni muhimu katika ufanisi wa watumishi wetu wa umma, ninakushukuru.
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, hata hivyo ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa Wilaya ya Muleba ina kata tano ambazo ziko katikati ya Ziwa Victoria ambako huduma nyingi za Serikali hazijafika. Je, Serikali ina mkakati gani wa kutupatia angalau ambulance kwa ajili ya kuharakisha usafiri hasa walimu na wafanyakazi wengine wanapopata matatizo ya afya? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa kuna taasisi za Serikali ambazo zinatoa motisha kwa wafanyakazi wake; je, Serikali haioni haja ya kuharakisha huo mwongozo ambao imeusema hapa kwa ajili ya kuwaboreshea maisha wafanyakazi hasa walimu na manesi ambao wako pembezoni kabisa mwa nchi ambako hakuna umeme na nyumba za kuishi ili waweze kutumikia Serikali kwa moyo wao wote? Ninashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Kikoyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; nimpongeze kwa namna anavyowasemea wananchi wake wa Jimbo la Muleba Kusini. Suala la kwanza, ameongelea juu ya ambulance. Nimhakikishie Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuboresha huduma za afya katika maeneo yote nchini na hivi karibuni Mheshimiwa Rais alitoa ambulance nchi nzima, na anaendelea kufanya hivyo kutokana na mazingira mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Dkt. Kikoyo jambo la kupeleka ambulance katika kata hiyo yenye changamoto tutawasiliana na wenzetu wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI kuona namna ya kupeleka ambulance katika eneo hilo na hiyo ndiyo nia ya Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la motisha kwa watumishi hili ni jambo la jumla. Mheshimiwa Rais alionesha nia ya dhati na hata juzi alipokuwa anazindua Sera ya Elimu ya 2014, Toleo la Mwaka 2023 amesema wazi tunaenda kupitia upya maslahi hasa maslahi ya walimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nikuhakikishie pia, suala hili la motisha ni kati ya mambo ambayo tunayapa kipaumbele kama Serikali na kutokana na hali ya uchumi na upatikanaji wa fedha nikuhakikishie jambo hili tutalitekeleza na hasa kwa watumishi wako wa Jimbo la Muleba Kusini. Ninakushukuru sana.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kukagua au kutoa ripoti ni suala muhimu sana katika kuwasimamia wafanyakazi, lakini kada ya afya ni kada muhimu sana ambayo inaokoa maisha ya watu. Hamwoni kuna namna kwa kada hii pekee ikapewa nafasi ya kutoa kwa mwezi badala ya kila siku, kwa sababu saa 24 ni saa za kuangalia wagonjwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, ninaomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakagenda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa upimaji watumishi kupitia PEPMIS tumeweka kwa muda kwa wiki kwa makusudi maalum kwamba tuweze kutambua tatizo kwa muda mfupi na kulitatua. Kuweka muda wa mwezi mmoja haitaweza kutusaidia kwa sababu tutakosa kupata consistency ya majukumu aliyoyafanya mtumishi kwa sababu itakuwa ni muda mrefu. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Mbunge na tangu tumeanza zoezi hili hatujapata malalamiko ya hawa watumishi moja kwa moja, kwamba jambo hili linawasumbua, wameendelea kujaza hiyo PEPMIS kwa wakati na mpaka sasa zoezi hili linaendelea vizuri. Ninakushukuru.
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, lakini hawa watumishi waliokumbwa na miaka minne na watumishi wa miaka mitatu sasa wamewapandisha kwa pamoja, wote wamekuwa kwenye position moja. Swali la kwanza; ninaomba Serikali inielezee ni utaratibu gani watachukua kuleta seniority kati ya wale waliokumbwa miaka minne na hawa wa miaka mitatu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; walimu waliajiriwa mwaka 2012 walisahaulika, sasa walivyokuja kupandisha vyeo wamepandisha wa mwaka 2013, 2014 na kuendelea. Sasa ni utaratibu gani watachukua ili hawa sasa waonekane kuwa ni ma-senior kwa hawa waliongia miaka iliyofuata? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Janejelly kwa namna anavyofuatilia mambo ya watumishi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu hawa walioathirika na miaka minne, Serikali tumechukua hatua ambako mpaka sasa tumebaki na kiasi kidogo cha watumishi hao ambapo jitihada ambayo inafanyika sasa, katika bajeti ya Mwaka wa Fedha 2024/2025 tutahakikisha watumishi wote walioathirika na kupanda vyeo miaka minne wanapandishwa kwa mserereko ili waweze kuwa sawa na wengine wale waliowatangulia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu walimu walioajiriwa mwaka 2012 na watumishi wengine ambao walitakiwa kupanda vyeo mwaka 2016 na promotion zilisitishwa kwa sababu ya uhakiki. Ninaomba nimtoe shaka Mheshimiwa Mbunge, hawa mpaka sasa tuna idadi ya watumishi 6,559 ambayo kwa mwaka huu wa fedha tumepanga bajeti na kama kuna wachache watakaosalia tutawakamilisha katika mwaka wa fedha utakaofuata kwa maana ya 2025/2026. Ninakushukuru sana.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kuna watumishi wamestaafu toka mwaka 2020 mpaka sasa bado hawajapata mafao yao na kwa kuwa waajiri hawakupeleka fedha kwenye mifuko. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha watumishi hao wanapata mafao yao? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, ninaomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zodo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwa na changamoto kwa baadhi ya watumishi wanaostaafu wanacheleweshewa kulipwa mafao kwa sababu moja tu baadhi ya waajiri wamekuwa wazembe wa kufikisha taarifa zao katika Ofisi ya Rais, Utumishi ili tuweze kuwa-process kwa wakati na Mheshimiwa Zodo ni moja ya mtu aliyeniletea kero hiyo ofisini na tunaishughulikia.

Mheshimiwa Spika, ninaomba nitumie Bunge lako kuwataka waajiri wote kwamba wastaafu wanapomaliza muda wao hili jambo sio la dharura, ni jambo ambalo linafahamika, watimize wajibu wao wa kuleta taarifa kwa wakati ili Ofisi ya Rais, Utumishi tuweze kushughulikia suala hilo kwa wakati. Kama kuna wengine watabainika na tulipitisha sheria hapa ndani ya Bunge tutawachukulia hatua kwa sababu kama Serikali hatutaki kuona wastaafu wa nchi hii wananyanyasika wakati wamefanya kazi yao kwa uadilifu kwenda kutumikia Taifa lao. (Makofi)
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, je, Serikali inazungumza nini kuhusu watumishi wanaojitolea katika kada mbalimbali hususani kada ya elimu ambapo kuna watumishi wapo huko wamejitolea kwa zaidi ya miaka sita na kumi sasa hivi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana na ninaomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mchungahela, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwa mara kadhaa ndani ya Bunge hili mjadala huu umeibuka juu ya vijana wetu wanaojitolea katika sehemu mbalimbali siyo tu kada ya ualimu, lakini tulitoa commitment kama Serikali ndani ya Bunge kwamba tutaenda kufanyia mchakato jambo hili.

Mheshimiwa Spika, ninaomba nilihakikishie tena Bunge lako, mchakato huu umefika katika hatua ya mwisho na tutaomba ruhusa yako (kibali) pia tukishirikishana na Kamati ili tuweze kuliboresha vizuri na baadaye tutatoa sasa mwongozo katika mwaka huu wa fedha namna ambavyo tuta-accommodate vijana wetu wanaojitolea. Kama Serikali tunatambua kujitolea kwao na tunathamini.