Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Eng. Ezra John Chiwelesa (1 total)

MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, je, Serikali imefikia wapi taratibu za ujenzi wa Barabara ya Mtwara Pachani kwenda Lusewa – Magazini mpaka Nalasi – Tunduru? Maana Mwenyekiti mmoja wa kijiji…

SPIKA: Mheshimiwa hiyo ni barabara moja?

MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ndiyo, ni barabara moja, ila inapitia kwenye Kata za Lusewa - Magazini...

SPIKA: Haya, uliza swali lako sasa.

MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ni lini Serikali itajenga Barabara ya Mtwara – Pachani – Nalasi ambayo inapitia katika kata hizo?

Mheshimiwa Spika, juzi nilielezwa na Mwenyekiti wa Kijiji kimoja kwamba mwezi wa Nne niwe nimeanza kuijenga barabara hiyo au watanishughulikia. Je, Serikali inawaeleza nini? (Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa...

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, ngoja kwanza. Mheshimiwa Mbunge maelezo ya sehemu ya pili ya swali lako kidogo yatakuwa nje ya utaratibu wa yale anayoweza kujibu Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwa hiyo, ili umweke sehemu nzuri, hebu mwulize swali lako kwa yale anayoweza kuyajibu yeye kama Naibu Waziri wa Ujenzi. Ile sehemu ya pili mwondolee ili asilazimike kukujibu.

MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, je, Serikali imefikia wapi kuhusu utaratibu wa kuijenga barabara ya Mtwara - Pachani mpaka Nalasi – Tunduru ambayo inapita kwenye Kata za Mkongo, Ligera, Lusewa, Magazini mpaka Tunduru? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna uhitaji mkubwa sana wa kuijenga hii barabara kwa kiwango cha lami. Tulichofanya kama Serikali, kwanza ni kuisanifu barabara yote wakati tunatafuta fedha kuijenga hiyo barabara ambayo ina urefu wa kilomita 300.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, tulichomwahidi Mheshimiwa Mbunge ni kwamba, wakati tunaendelea kutafuta fedha, maeneo yote korofi katika hiyo barabara ambayo huwa yanaleta changamoto tutahakikisha kwamba tunayaimarisha kwa kuyajenga kwa zege ama lami ili wananchi hao wasikwame wakati Serikali inatafuta fedha. Hivyo, mpango huo upo, ndiyo maana tumefanya usanifu kwa barabara yote, ahsante.