Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Alexander Pastory Mnyeti (49 total)

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa majibu hayo ya Serikali yenye kuleta matumaini kwa wananchi wa Lindi Manispaa. Hata hivyo, naomba sasa niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Lindi Manispaa tumeshatenga ekari moja na nusu kwa ajili ya ujenzi wa soko hili la samaki, vilevile tuna wavuvi 2,193 ambao wamesajiliwa na wachuuzi wadogo wadogo 470 ambao wanakosa mahali pa kufanyia shughuli zao za biashara. Naomba Serikali itupe majibu ya uhakika na ya kueleweka ya kuwapa wananchi wa Lindi Manispaa matumaini; ni lini sasa mtaanza kutenga bajeti kwa ajili ya ujenzi wa soko la Samaki?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake kwa wavuvi kwa kuwakopesha maboti, pamoja na nyavu na injini ili wavuvi hawa sasa waendeleze uvuvi wao kwa vifaa hivi vyenye uhakika na usalama wa kutosha? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kama Mheshimiwa Mbunge alivyouliza swali lake la nyongeza kuwa tayari Halmashauri ya Manispaa ya Lindi tayari wameshakupata eneo, namwomba baada ya Bunge hili twende na wataalamu pale Lindi tukahakiki hilo eneo na wataalamu na tukishajua eneo hilo lililopatikana lina ukubwa gani na linafaa kwa matumizi hayo, Wizara iko tayari kuanza ujenzi wa soko hilo mara moja.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ameuliza kuhusu zana. Tathmini tayari imeshafanyika, wataalamu wameshafanya tathmini ya zana gani zinafaa kwa maeneo hayo ya wavuvi, namwomba baada ya hili, kwa sababu tayari kila kitu kimeshafanyika, basi baada ya Bunge hili tuambatane naye kama nilivyosema hapo awali, twende kwa wavuvi hao kuhakiki ni aina gani ya zana zinazohitajika ili Serikakli ione namna ya kuanza kuwakopesha wavuvi hao hizo zana, ahsante.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipatia fursa ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Ni lini Serikali itaanza mpango wa kujenga soko jipya la kisasa la samaki katika Wilaya ya Kigamboni?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, swali la nyongeza Mheshimiwa Ndugulile, anataka kujua ni lini Serikali itaanza ujenzi wa soko jipya Kigamboni. Ujenzi wa soko jipya Kigamboni utategemea uwezekano wa kibajeti. Kama Serikali itapata bajeti, basi iko tayati kuanza ujenzi wa soko hilo jipya pale Kigamboni, ahsante sana. (Makofi)
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, swali dogo la nyongeza. Hali ya soko la samaki Tanga ni sawa sawa kabisa na hali ya soko la samaki Lindi; je, ni upi mkakati wa Serikali katika kuhakikisha linapatikana soko la samaki la kisasa kwenye Jiji la Tanga?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kama alivyouliza Mheshimiwa Mbunge katika swali lake, wako wataalam wanafanya tathmini ya kuyatambua hayo masoko yote nchi nzima. Tunaomba nafasi ili wataalam hao waendelee na tathmini hiyo, na wakishamaliza, Serikali itatoa utaratibu wa namna gani masoko hayo yanakwenda kujengwa katika nchi yetu. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Miundombinu ya soko la samaki katika Manispaa ya Mtwara Mikindani ni mibovu na mibaya hasa sehemu ya jiko pamoja na ofisi. Nini mkakati wa Serikali kuboresha miuondombinu hiyo? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, soko la Mikindani ni kama masoko mengine ambayo nimeshatoa maelekezo, kwamba tutatuma wataalam kuja kuangalia upungufu uko wapi, halafu baada ya kuyajua huo upungufu, Serikali iko tayari kuanza kufanya marekebisho ya maeneo hayo. (Makofi)
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Serikali naomba kuuliza maswali mawili madogo nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, sasa ni mwaka wa tano tangu 2018 maktaba ilipokamilika, thamani zake ziko wapi?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, maabara ilipanga kukamilika Oktoba, 2022 na kwa sasa imefikia asilimia 35, nini tamko la Serikali?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwamba Wizara ilikuwa inasubiri ukamilishaji wa maktaba na maabara na baada na ukamilishaji huo, Serikali inakwenda kuweka samani zote. Kwa kuwa tayari maktaba imeshakamilika, bado maabara, Wizara ilikuwa inasubiri vyote vikamilike kwa pamoja ili samani hizo zote ziende kwa pamoja. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Mbunge avute Subira, jambo hili tunalifuatilia. Leo jioni tukutane mimi na yeye twende pale Wizarani tufuatilie tuone jambo hili linafika mwisho kwa kiwango hiki, ahsante. (Makofi)
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa Shirika la CARMATEC limebobea katika kutengeneza mitambo ya biogas; je, Serikali inajishughulishaje na shirika hili karika mambo ya utengenezaji wa biogas?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kwa kuwa nchi ya China inaongoza kwa uzalishaji wa biogas kwa kiwango cha cubic meters 15,000,000 kwa mwaka; je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka wananchi wetu wakasome wapate ujuzi wa hali ya juu wa kutengeneza biogas; kwanza kwa sababu tunahitaji kufuga zaidi kisasa kuliko kuswaga ng’ombe; na pili itapuguza uharibifu wa mazingira kwa ajili ya mmomonyoko wa udongo unaoletwa na ng’ombe wengi ambao wanachungwa badala ya kufungwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mheshimiwa Mbunge anataka kujua namna ambavyo Serikali na Wizara yetu inavyoshirikiana na mashirika haya ikiwa ni pamoja na wadau wetu wa China. Wizara imepokea ushauri huo wa Mheshimiwa Mbunge. Tutakwenda kulifanyia kazi jambo hili la mashirikiano yetu na kupeleka wanafunzi wetu kwenda kujufunza nchini China.

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, jambo hili tumelichukua na ushauri huu tumeupokea na tutakwenda kulifanyia kazi.
MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana pia nashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wa sekta hii ya uvuvi kwenye Pato la Taifa kwa kiwango cha asilimia 1.8, tunakubaliana kwamba mchango huu bado ni mdogo sana, lakini nafahamu kwamba ipo mipango ya Serikali kununua meli kwa ajili ya uvuvi wa Bahari Kuu. Nataka kufahamu ni stage gani tumefikia kwenye uagizaji wa meli hizi kwenda kuvua kwenye Bahari Kuu?

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nataka kujua ni kwa namna gani mipango hii ya Serikali kwenye Wizara hii ya Uvuvi inaishirikisha Zanzibar katika kukuza Uchumi wa Bluu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Bakar Hamad Bakar. Swali lake la kwanza anataka kujua kuhusu mchango.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba mchango huu ni mdogo, mchango wa asilimia 1.9 ni mchango mdogo na ndiyo maana Serikali imekuja na mikakati mbalimbali ambayo itakuja kusaidia sana kuinua kipato hiki. Moja ya mikakati ambayo Serikali imekuja nayo ni pamoja na ujenzi wa Bandari ya Uvuvi. Tunakwenda kujenga Bandari ya Uvuvi pia kuhamasisha ujenzi wa viwanda vya kuchakata mazao ya samaki, pia kufufua viwanda ambavyo tayari vimeshakufa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa kwamba asilimia 1.9 ni asilimia ndogo na Serikali iko na mkakati wa kufanya kazi hiyo ikiwa ni pamoja na kufufua Shirika la TAFICO ambalo tayari limeshakufa. Kwa hiyo, tunayo mikakati kama Serikali kwamba mikakati hiyo ambayo tumeiweka tukiitimiza vizuri tunaweza tukaongeza pato kutoka 1.9 kwenda juu zaidi. Kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Mbunge avute subira kwamba iko mikakati Serikali inajipanga kwa ajili ya kwenda kuimarisha jambo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ametaka kujua ni lini ununuzi wa meli hiyo utakamilika. Mchakato wa ununuzi wa meli upo unaendelea lakini umesimama kidogo kwa sababu za kibajeti. Kwa hiyo, mara Serikali itakapopata fedha ununuzi wa meli hiyo utaweza kufanyika mara moja. Ahsante.
MHE. ANNA R. LUPEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya ucheleweshwaji wa mradi huu masika ikakuta mradi umecheleweshwa na mvua za masika, lakini Mkandarasi alichukua muda mrefu sana kuingia site katika kujenga mradi huu na mradi huu unajengwa na Wizara, haushirikishi Halmashauri ambayo wako katika eneo husika la mradi.

Je, Serikali ina mkakati gani kushirikisha kwa ukamilifu Halmashauri ya Nsimbo ili kuendelea kusimamia mradi huu?

Swali la pili, Serikali inachelewesha malipo ya Mkandarasi, Mkandarasi anashindwa kutekeleza mradi kutokana na kukosa kulipwa pesa. Je, ni lini Serikali itamlipa Mkandarasi pesa zake ili aweze kukamilisha mradi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza miradi hii ni miradi ya Serikali, haijalishi mradi unatekelezwa na Wizara ama unatekelezwa na Halmashauri, miradi hii yote ni ya Serikali. Miradi hii inapokuja huku kwenye Halmashauri maana yake mamlaka zote za Serikali zinapaswa kushiriki katika kutekeleza mradi huo, kwa sababu miradi hii haimaanishi kwamba inapojengwa na Wizara ni kwamba Serikali nyingine haihusiki, Hapana! Sasa hii ni dhana ya uelewa katika Halmashauri zetu kwamba miradi inapokuja kwa namna moja au nyingine ni lazima watumishi wa Halmashauri washiriki kwa namna moja ama nyingine katika kusimamia mradi huo ili kuleta tija na ubora wa miradi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili Mheshimiwa Mbunge ametaka kujua namna ya ucheleweshaji wa malipo. Malipo ya Serikali yoyote yanalipwa kulingana na certificate ya utekelezaji wa mradi alipofikia huyo Mkandarasi. Serikali inalipa fedha kutokana na certificate alizo-raise ambazo zinatokana na kazi aliyoifanya kwa kiwango hicho na huyu mkandarasi mpaka sasa ameshalipwa zaidi ya asilimia 70 ya malipo yake kwa sababu jumla ya shilingi milioni zaidi ya 270 amekwishalipwa kati ya milioni 510.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Mkandarasi huyu anakwenda vizuri na ukiona mradi unachelewa ni kwa sababu ya upatikanaj wa fedha lakini ni pamoja na kwamba kazi anayoifanya ndiyo itakayo-determine analipwa fedha kiasi gani, kwa hiyo, huyu analipwa kulingana na kazi anayoifanya. Naomba kuwasilisha.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali yaliyotolewa. Ninaomba kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo jitihada kubwa ambazo zilishafanywa huko nyuma na wananchi kupitia utaratibu wa Vijiji vya Ujamaa na nguvu za wananchi kuhakikisha kwamba wanachimba mabwawa katika kipindi cha nyuma. Hapa miaka ya 90 mpaka 2000, Serikali iliweza kuchiba baadhi ya mabwawa, lakini mabwawa yale ni kama yalitelekezwa na baadaye yakawa yameharibika. Kuna uhitaji ama umuhimu wa kuyafufua yale mabwawa ambayo yalichibwa nyakati hizo, kabla ya kuweka mkakati wa muda mrefu ule wa kujenga mabwawa haya.

Je, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha mabwawa yaliyopo katika maeneo hayo yanafufuliwa kwanza?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza natumia nafasi hii kumpongeza sana Mbunge wa Kishapu, Mheshimiwa Boniphace Nyangindu, kwa kazi kubwa anayoifanya ya kufatilia namna ambavyo wafugaji wake wanatakiwa wawe na maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyouliza swali lake la msingi, ni kweli kwamba Serikali ipo na mipango mingi ya kufufua mabwawa yote yaliyokufa. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge, baada ya Bunge hili tutatuma wataalam kuja kufanya tathmini katika jimbo lake. Tujue tathmini hiyo, mabwawa yako mangapi na yanahitaji nini ili Wizara kamaSerikali Wizara iweze kutuma namna ya kuyafufua haya mabwawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua mabwawa ambayo yanahitaji kufufuliwa na Serikali yapo maeneo mengi. Serikali tunamuahidi Mheshimiwa Mbunge Serikali imejipanga vizuri. Tukishapata kujua gharama za shilingi ngapi inatakiwa kwenda kuyafufua hayo mabwawa tupo tayari kwenda kuyafufua mabwawa hayo kwenye Jimbo la Kishapu. (Makofi)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru sana kwa kunipatia nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na migogoro mikubwa kati ya wafugaji na wakulima. Ndani ya Jimbo langu la Nanyumbu wakulima wa Kata ya Lumesule wana mgogoro mkubwa na wafugaji wa eneo hilo. Hii imepelekea kuhatarisha hata maisha yao. Hivi ninavyozungumza wakulima wako katika hali mbaya sana ya usalama kati yao na wafugaji.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri upo tayari mara baada ya kuahirishwa Bunge letu kesho kutwa, mimi na wewe tukafuatana tukaenda kwenye Kata husika kutatua mgogoro uliopo kati ya wakulima na wafugaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge anataka kujua kama Wizara iko tayari kuambatana naye baada ya Bunge hili. Wizara iko tayari kuandamana na Mheshimiwa Mbunge. Tuko tayari kwenda kuona mgogoro huu na kuutafutia ufumbuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla Wizara haijaenda kutafuta ufumbuzi wa mgogoro huu Serikali hii ni kubwa, wapo viongozi ambao wanapaswa kuanza kuhangaika na migogoro hii kabla Wizara haijafika huko. Yupo Mheshimiwa DC, nitoe wito sana, Mheshimiwa DC na wataalam wote waliopo huko wa Mifugo na Kilimo kwenda kutatua mgogoro huu kabla Wizara haijafika huko kutafuta ufumbuzi wa kudumu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ina Wataalam wa Kilimo na Mifugo, ina Mheshimiwa DC ambaye ni Kamisaa wao. Tunaomba kabla Wizara haijafika huko nitoe wito kwa wakuu wote waende kutatua mgogoro huu kabla hatujafika huko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. MAIMUNA A. PATHAN: Mheshimiwa Spika, ahsante, nina maswali mawili ya nyongeza.

Je, ni lini tathmini hiyo itakamilika ili Watanzania wafanye kazi zao kwa ufasaha ili kuleta tija? Swali la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; je, kwa kuchelewesha kukamilisha taratibu hizo hatuoni kwamba tunawanyima Watanzania fursa katika kumiliki rasilimali zao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema katika jibu la msingi kwamba mchakato wa kubadilisha sheria ama kanuni ni mchakato unaofanyika mara kwa mara. Kama nilivyosema mwaka 2019 mchakato huo ulifanyika tukabadilisha sheria mbalimbali, mwaka 2020 tukabadilisha. Kwa hiyo, sheria ambazo zinaonekana pengine ni kandamizi kwa wadau wa uvuvi, Serikali iko tayari kuendelea kuzibadilisha mara kwa mara kadri ya mahitaji.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tathmini zinaendelea kulingana na sheria, jiografia na uhitaji wa maeneo husika. Lengo la Serikali hasa ni kuhakikisha kwamba sheria zinazotumika kumsaidia huyu mvuvi ama mtumizi wa sekta hiyo kurahisisha shughuli zake.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tathmini zinaendelea. Sheria ambazo ni kinzani na mahitaji ya watumiaji wetu, zinaendelea kubadilishwa siku hadi siku kama ambavyo zimekuwa zikibadilishwa mara kwa mara. Kwa hiyo, wataalamu wanaendele kufanya tathmini, lakini sio tu wataalam wa Wizara, ni pamoja na watumiaji wa sheria hizi wanaendelea kufanya tathmini siku hadi siku kama ambavyo sheria na kanuni zimekuwa zikibadilika, naomba kuwasilisha. (Mkofi)
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Kwanza ni kweli Serikali ilisitisha zoezi hili la utambuzi wa mifugo kwa kutumia hereni za kieletroniki mwaka jana 2022, Novemba tarehe kama hii, ili kuipa Wizara kufanya tathmini ya upungufu. Kutokana na umuhimu wa zoezi la utambuzi wa mifugo ambacho ndicho kinachoweza kuondoa migogoro kati ya wafugaji, na kusababisha mifugo kuhamahama na kuingiliana pamoja na wizi wa mifugo; changamoto ambayo iko kwa wafugaji wadogo zaidi kuliko wa mashamba makubwa, ambapo ufugaji kule uko salama na idadi yake inafahamika: Ni lini sasa Serikali itafanya zoezi hili kwa wafugaji wa kawaida na wadogo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, kuna changamoto ya takwimu ya uhakika ya mifugo. Ni lini Serikali itafanya sensa ya mifugo ili tuwe na takwimu halisi ya mifugo katika nchi yetu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, kwanza nianze na hili la hereni kwamba ni kweli Serikali ilisitisha na sasa mwaka mmoja umepita. Serikali imesitisha baada ya zoezi hili kulalamikiwa sana na wadau, hasa wafugaji wadogo wadogo. Sasa Serikali ilichokifanya ni kuainisha changamoto zile ambazo wafugaji wanazilalamikia na kutafuta majawabu sahihi. Baada ya kupata hayo majawabu sahihi, na kwa kuwa zoezi hili lilizuiliwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu, tulichokifanya Wizara ni kumwandikia Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba sasa tunashughulikia changamoto zote ambazo wafugaji wameziainisha, kwamba majibu yake sasa tayari tunayo na Mheshimiwa Waziri Mkuu tayari amesharuhusu tuendelee na zoezi hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba zoezi hili litaanza mara moja, hivi punde kadiri ambavyo maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu yalivyotolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili amelisema hapa kuhusu sensa. Ni kweli kwamba sensa hii huwa inafanyika kila baada ya miaka mwili. Sensa ya mwisho ilifanyika mwaka wa fedha 1920 na mwaka huu sasa tutafanya sensa 2023 kwa ajili ya kubaini idadi halisi ya mifugo tuliyonayo katika Taifa letu. Sensa hii tunashirikiana na watu wa NBS, wanaoshughulika na masuala ya takwimu kuhakikisha kwamba takwimu tunazozipata zinalenga kwenye kuleta tija katika Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. VINCENT P. MBOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Nina maswali mawili ya nyongeza. Ziwa Tanganyika, Wilaya Nkasi hakuna vizimba hata kimoja . Ni lini Serikali mtapeleka vizimba Wilaya ya Nkasi hasa Jimbo la Nkasi Kusini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la namba mbili, lini Serikali itamalizia ujenzi wa Bwawa la Kacheche la kunyweshea mifugo pamoja na ujenzi wa majosho mawili Chala B, Kata ya Chala pamoja na Kijiji cha Kitosi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaanza na hili la vizimba, tumeshatoa maelekeza kwamba mvuvi yeyote ama mwananchi yeyote ambaye ana shida na vizimba ama boti au nyenzo zozote zinazohusiana na uvuvi, aombe haraka iwezekanavyo milango ipo wazi kwa Watanzania wote. Kwa kweli Mheshimiwa Rais, ametufungulia njia kama mnavyokumbuka Tarehe 30, aligawa kule Mwanza vizimba na boti za kutosha na Wizara ipo katika mchakato wakutafuta vizimba vingine ili kuwagawia wananchi watakaohitaji kwa awamu ya pili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge aendelee kuhamasisha Wananchi wake wenye uhitaji. Tupo tayari kupeleka Ziwa Tanganyika na tayari tumeshaanza Ziwa Victoria na kwa kweli vijana wote na wavuvi wote wenye shida na wenye uhitaji wa nyenzo za uvuvi Serikali ipo tayari kuwagawia. Ahsante. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la pili, kuhusiana na lini bwawa litakamilika na majosho. Hapa katikati tulisimama kidogo kwa sababu ya upatikanaji wa fedha. Mara tu Serikali itakapopata fedha tutakwenda kukamilisha ujenzi wa majosho hayo. Mheshimiwa Mbunge atakumbuka katika Wilaya yake tumemtengea jumla ya shilingi bilioni 1.6 kwa ajili ya ujenzi wa soko la samaki katika eneo hilo. Tukapopata fedha nyingine tutakwenda kukamilisha ujenzi wa majosho hayo na mabwawa ambayo yapo katika Wilaya yake, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ninashukuru kwa kunipa fursa na mimi niulize swali la nyongeza. Kwanza, ninashukuru kwa huduma tuliyoipata miundombinu katika Ziwa Victoria. Wilaya ya Ilemela asilimia 87 ni eneo la maji, na wanawake na vijana wengi wanashughulika na mazao ya samaki hususani dagaa lakini miundombinu yao ya kukausha samaki si mizuri hasa kwa afya ya binadamu. Ni lini Wizara itasaidia kuweka miundombinu kwa ajili ya kukausha samaki kwa wafanyabiashara hao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimesema kwamba Serikali imeshaanza na katika Ziwa Victoria tumeshaanza kuwasaidia Wavuvi namna ya kuvua zile samaki lakini pia kuhifadhi samaki. Hili wazo la Mheshimiwa Mbunge tumelichukua tutakwenda kulifanyia kazi kuwasidia Wavuvi wakanda ya ziwa. (Makofi)
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwenye orodha ya masoko ya Samaki yatakayojengwa katika mpango ambao ameusema Mheshimiwa Naibu Waziri kwa mwaka wa fedha 2023/2024 ni pamoja na Nyamikoma, Jimbo la Busega. Mpaka sasa soko hili halijaanza kujengwa na imebaki miezi minne kukamilika kwa mwaka wa fedha. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa soko hili la Nyamikoma? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaanza ujenzi wa Soko Nyamikoma mara tu fedha zitakapokuwa zimepatikana. Tayari Serikali imeshaanza ujenzi wa masoko katika maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na Tunduma, Muleba, Momba, Ludewa, Busega, Nkinga na Kalambo. Kwa hiyo, mara tu tutakapopata fedha Serikali itaanza ujenzi haraka sana iwezekenavyo katika Kijiji cha Nyamikoma. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza na naishukuru Serikali kwa kuchimba Bwawa la Kihumbu. Sasa nataka kuuliza, kwa sababu bwawa limechukua muda mrefu kidogo pamoja na kwamba jitihada zipo.

Je, ni lini sasa hilo bwawa litakamilika ili wananchi watumie maji ya bwawa hilo na mifugo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli bwawa halijakamilika; Serikali tayari imeshakutana na mkandarasi na imeshampa deadline juu ya lini bwawa linatakiwa kukamilika na tayari tumeshakubaliana. Mara tu mkataba utakapokuwa umekamilika bwawa hilo litakuwa limekamilika na atatukabidhi Serikallini kwa ajili ya kuendelea kulitumia.
MHE. ABEID R. IGHONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Hali ya upatikanaji wa maji katika Jimbo la Manyoni Magharibi ni mbaya, eneo lile ni kame. Pamoja na juhudi hizi za Serikali, sasa Naibu Waziri haoni umuhimu wa kuongeza kasi ya kupeleka mabwawa zaidi pamoja na majosho katika Jimbo la Manyoni Magharibi ili kuwasidia wakulima wetu pamoja na wafugaji ambao mifugo yao inapata tabu kwa kipindi cha kiangazi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika Jimbo la Singida Kaskazini katika bajeti ya mwaka 2023/2024, Serikali ilitupatia miradi ya majosho manne katika Kijiji cha Minyenye, Ghalunyangu, Muhamo na Mangida. Kwa bahati mbaya fedha hazikuja kwa ajili ya kutekeleza miradi hii pamoja na kuwa wananchi tayari walishaanda upande wa nguvu kazi.

Je, sasa ni lini Serikali italeta fedha kwa ajili ya kukamilisha miradi hii ambayo inasubiriwa kwa hamu kubwa na wananchi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na hili swali la kwanza la Mheshimiwa Mbunge kwamba, mabwawa ambayo yaliahidiwa kwenye bajeti ya mwaka 2023/2024. Kwanza nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba, mwaka wa fedha wa bajeti bado haujaisha. Namhakikishia kwamba, jinsi ambavyo upatikanaji wa fedha utakavyokuwa unapatikana, tutakwenda kuyajenga hayo mabwaka kama ambavyo bwawa tulilokwishalikabidhi tayari limekwishajengwa katika jimbo lake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili kuhusu kuongeza kasi ya ujenzi wa haya mabwawa, ni kweli kama nilivyokwisha jibu kwamba, tumeshakabidhi bwawa la kwanza na Serikali sasa inaendelea kutafuta fedha zingine kwa ajili ujenzi wa mabwawa mengine. Tunakiri kwamba, Wilaya ya Itigi ni miongoni wa wilaya kame ambazo zinahitaji kuongezewa mabwawa na majosho kwa ajili ya kuisaidia mifugo yetu iliyoko katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali inaendelea kufuatilia na inaendelea kutafuta namna ambavyo inaweza kusaidia ujenzi wa mabwawa katika Wilaya hii ya Itigi, ahsante. (Makofi)
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nataka kuuliza ni lini sasa Serikali ina mpango wa kutekeleza ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mashimba Ndaki, alipokuja kwenye Jimbo la Msalala na kuahidi bwawa la kunyweshea mifugo.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahadi ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo, Mheshimiwa Mashimba Ndaki, Mheshimiwa Waziri wa Mifugo Mstaafu ambayo aliitoa katika Jimbo la Msalala, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, ahadi za viongozi wote walizokwishazitoa tunazo kama Wizara. Tuna database muhimu ya ahadi hizo. Nimhakikishie, mara ambapo tutapata fedha kwa ajili ya utengenezaji wa mabwawa hayo tutakuja kujenga katika Jimbo lake la Msalala. (Makofi)
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi. Wilaya ya Liwale tulipata shilingi milioni 400 kwa ajili ya kujenga bwawa pale Kijiji cha Kimambi lakini wale wataalamu badala ya kujenga bwawa walijenga Karo. Ni nini kauli ya Serikali juu ya ufisadi ule?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, concern ya Mbunge tumeshaipokea na tayari Wizara inajipanga kupeleka wataalam kwa ajili ya uchunguzi wa jambo hili. Mara tutakapojiridhisha kwamba kuna tatizo katika mradi huo tutachukua hatua stahiki kwa mujibu wa sheria za utumishi. (Makofi)
MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na nimshukuru Mheshimiwa kwa majibu mazuri, hata hivyo nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 Kata hizo Nane zina jumla ya wananchi 26,582. Je, kwa idadi hiyo ya boti mbili Mheshimiwa Waziri atakubaliana na mimi kwamba Serikali inatakiwa iongeze boti?

Swali la pili, wavuvi wa Jimbo lile wana changamoto nyingi na wana maoni mengi ambayo wangetamani wakae na Mheshimiwa Waziri. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri uko tayari kutangulizana na mimi baada ya Bunge hili kwenda kukaa na wavuvi wa Jimbo la Ludewa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, zoezi la ugawaji wa boti lilianza kwa zoezi la awali Mheshimiwa Rais amekwishatoa maelekezo kwamba tuangalie maeneo yote yenye uhitaji wa kuongeza boti hizo na tayari tumeshaainisha maeneo ambayo yana umuhimu wa kuongeza boti na sasa Wizara iko tayari kuongeza boti kulingana na mahitaji ya maeneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ni kuhusu kuwatembelea, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Kamonga kwa jinsi ambavyo anafuatilia sana shida za wananchi wake na kuwatatulia, kwa kadri hiyo na sisi Wizara tuko tayari kufika katika eneo lake kwenda kuzungumza na wavuvi hao kuona namna sahihi ya kutatua changamoto wanazopitia wavuvi hao.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya vyuo katika taasisi hizo kama vile Mtwara–Mikindani, Kibirizi–Kigoma, Gabimori–Rorya mameneja wake wamekaimu kwa kipindi kirefu sana kuanzia miaka saba mpaka kumi na moja;

i. Je, Serikali haioni inafifisha malengo ama maelekezo ya Chama cha Mapinduzi katika vyuo hivyo kutoa mafunzo kwa sababu havina mameneja wa kudumu?

ii. Je, Serikali itakapokamilisha mchakato huo wa kujaza hizo nafasi kwa muundo uliokamilika tangu Novemba 2022, iko tayari kuwalipa mameneja hao wanaokaimu akiwemo meneja wa Mtwara-Mikindani aliyokaimu kwa miaka 11 kwa nafasi hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza nampongeza sana dada yangu Agnes kwa jinsi ambavyo amekuwa akifuatilia sana chuo hiki na kwa kweli kama Wizara tunatumia nafasi hii kumpongeza sana kwa jinsi ambavyo anafuatilia habari hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, ni kweli kwamba kuna makaimu katika vyuo vingi vinavyohusiana na masuala ya uvuvi. Napenda kutumia nafasi hii kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba makaimu hao sasa watakwenda kuthibitishwa, wale wenye vigezo. Jambo hili liko kwenye upekuzi na upekuzi upo katika hatua za mwisho namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba linakwenda kufanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili alilosema kuhusu mameneja waliokaimu kwa muda mrefu taratibu za kiutumishi zinafahamika. Kama watakuwa na sifa za kulipwa basi watalipwa, Serikali iko tayari kuwalipa na kama watakuwa hawana sifa za kulipwa basi hawatalipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi. Kwanza kabisa, naomba nichukue fursa hii kuishukuru Wizara kwa majosho matano. Nina swali moja tu la nyongeza. Nataka kujua kama Wizara inajua kwa uhakika katika vijiji vyetu vyote 114, mahitaji ya majosho ni kwa kiwango gani, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Ni kweli kwamba Wizara ina Database ya kujua wapi panahitajika josho lipi, kwa size gani na kwa umuhimu gani? Pia, Mheshimiwa Mbunge kama anaona kuna sehemu ambapo sisi kama Serikali tunapaswa kwenda kujenga josho, alete taarifa zake tuweze kufanyia kazi kwenye maeneo hayo. Hata hivyo, mpaka sasa database ya vijiji ambavyo majosho yanatakiwa kujengwa, Serikali ina hiyo database, ahsante. (Makofi)
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na nina maswali mawili ya nyongeza. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwapatia Wavuvi wa Bwawa la Nyumba ya Mungu zana na nyenzo za uvuvi kama vile nyavu, boti na vizimba, kama ilivyofanya hivi karibuni kwa wenzao wa Lake Victoria?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; uvuvi haramu ni chanzo kikubwa cha kuzorotesha uchumi wa Samaki; na Maafisa Uvuvi wa hapa nchini na hata kule Nyumba ya Mungu, wameweka mkazo kwenye kuwakamata wavuvi na kuwapiga faini badala ya kutoa elimu endelevu ya namna bora ya kufanya uvuvi: Je, Serikali haioni umuhimu wa kuchukua hatua kupambana na hali hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nianze na hili la kwanza. Kwanza ugawaji wa nyenzo za uvuvi kama boti, nyavu na kadhalika, kama ambavyo Mheshimiwa Rais alifanya juzi kule Mwanza, Ziwa Victoria, hii ni fursa kwa Watanzania wote kwenye maziwa na mabwawa mbalimbali, wanaruhusiwa kuchukua nyenzo hizi kwa njia ya kukopa kupitia TADB, benki yetu ya kilimo ambapo ukiwasilisha andiko lako vizuri kwa kupitia wataalamu wetu, unaweza kupata ushauri na baadaye ukakopeshwa nyenzo hizo ukafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hii ni fursa kwa Watanzania wote ikiwemo wavuvi wa Bwawa la Nyumba ya Mungu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge, kwanza nikupongeze sana kwa ufuatiliaji na namna ambavyo unaendelea kufuatilia. Umekuwa msumbufu sana kwenye hili. Tunakupongeza kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri. Kwa kweli tupo tayari kukupa ushirikiano ili wavuvi wako waweze kupata nyenzo hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni kweli kwamba Maafisa Uvuvi kazi yao ni kuhakikisha wanasimamia shughuli za uvuvi kwenye maeneo yao pamoja na kutoa elimu kwa wavuvi wetu. Natoa wito na rai kwa Maafisa Uvuvi wote nchini kuhakikisha kwamba wanajikiza zaidi kwenye kutoa elimu na kusimamia shughuli za uvuvi na siyo kujigeuza kuwa Maafisa Masuuli na Maafisa wa Mapato, kukatisha ushuru na mambo mengine ambayo hayawahusu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunatoa wito kwa Maafisa wote kwamba sasa wajielekeze kwenye kazi yao ya msingi ambayo wanatakiwa kufanya kwenye maeneo yao huko wanakofanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali langu la kwanza; tumekuwa na chanjo nyingi ambazo sisi kama Serikali tunapeleka. Tumepeleka chanjo za surua tunatoa bure. Tumepeleka pepopunda tunatoa bure. Ni kwa nini sasa, Serikali isipeleke chanjo za mifugo na zikatolewa bure na wataalam wetu wakatumika kutoa hizo chanjo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; tumekuwa na chanjo ambazo zinaendelea katika halmashauri zetu na majimbo yetu, lakini hizi chanjo zinatolewa tender na wazabuni wana-tender wanakwenda kuchanja kule, lakini mfugaji akipata athari kwenye mifugo yake hakuna msaada wowote ambao anaweza kuupata kupitia hao watoa huduma. Je, Serikali haioni haja ya kupeleka madawa na wataalam wetu wakaenda kuwachanjia wafugaji wetu ili ziweze kuwasaidia direct na wakipata matatizo wajue wapi wanakwenda? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama anavyosema Mheshimiwa Mbunge kwamba, chanjo nyingi zimekuwa zikitolewa bure, chanjo za binadamu na maeneo mengine. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama nilivyosema katika jibu la msingi kwamba Mwaka wa Fedha 2024/2025, tayari Serikali imekwishatenga bajeti ya jumla ya shilingi bilioni 29, kuanza kutoa chanjo bure kwa mifugo yetu ambayo wananchi wetu wanamiliki katika maeneo yao. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, mwaka huu katika bajeti hii itakapokuja aipitishe kwa kishindo ili twende kutekeleza jambo hili ambalo na yeye yamekuwa ni maono yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili tumepokea ushauri na ushauri huu tutakwenda kuufanyia kazi tuone namna ambavyo Serikali kupitia Wizara inaweza kuutekeleza ushauri huu. Ahsante. (Makofi)
MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Katika Kata ya Mkindi kuna Kijiji cha Kihwenda ambapo panajengwa bwawa kwa ajili ya wafugaji. Ni takribani mwaka wa pili sasa Mkandarasi ameondoka site na bwawa lile ni muhimu sana kwa maji kwa ajili ya wafugaji pamoja na wananchi. Je, nini mpango wa Serikali kuhakikisha kuwa, Mkandarasi anarudi na bwawa lile linakamilika? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli bwawa hilo limesimamishwa ujenzi wake. Nimhakikishie Mbunge tutakwenda kufuatilia, tutaangalia mimi na yeye twende kule, tuangalie na wataalam tuone namna ambavyo tunamrudisha Mkandarasi site ili aweze kukamilisha bwawa hilo na wananchi waweze kupata huduma katika eneo hilo. Ahsante. (Makofi)
MHE. SYLVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa majibu mazuri. Vile vile naomba nitumie nafasi hii kumpongeza Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia. Wote ni mashahidi, tumeona juzi amefanya kazi kubwa sana ya kukabidhi boti zaidi ya 160, haijawahi kutokea! Hakika hii ni kubwa na Mama apewe maua yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa maelezo ya Mheshimiwa Waziri utaona kabisa Ziwa Tanganyika wamewezeshwa boti tisa, na Ziwa Tanganyika linahudumia mikoa mitatu; Kigoma, Katavi na Rukwa. Uwiano huu ni mdogo sana: Je, nini mkakati wa Serikali wa kuongeza boti katika ukanda wa Ziwa Tanganyika? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Ziwa Tanganyika tuna uhaba wa vizimba; je, ni nini mkakati wa Serikali wa kuwapatia wavuvi wa Ziwa Tanganyika vizimba ili kuboresha Sekta ya Uvuvi? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze na hili la mpango wa Serikali wa kuongeza vizimba na maboti yote yanakwenda kwa pamoja. Ni kweli kwamba Ziwa Tanganyika ni Ziwa kubwa linalohudumia mikoa mingi na idadi ya boti zilizotoka mpaka sasa ni chache. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tumeshatoa maelekezo kwamba wale wote wanaohitaji boti na vizimba waendelee kuomba na Mheshimiwa Waziri ameshatoa maelekezo waendelee kuomba Wizarani na Wizara iko tayari kuwahudumia, kuwagawia boti hizo kupitia benki yetu ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wale wenye uhitaji, wanahamasishwa kwenda kuonana na Maafisa Uvuvi, wawasaidie kuandika maandiko mazuri yatakayowawezesha kupata hiyo mikopo ili waweze kujiendeleza kwenye Sekta yao ya Uvuvi. Ahsante.
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Rais, kwa kazi kubwa ambayo ameendelea kuifanya kwenye sekta ya uvuvi. Hata hivyo nina swali moja la nyongeza. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia wananchi wa Kata yangu ya Nyatwali na Bunda kwenye suala la ufugaji wa samaki wa vizimba? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwamba Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi, tayari imesharuhusu waombaji waendelee kuomba vizimba na hata maboti. Kwa hiyo, kwa kesi ya Mheshimiwa Maboto, nimshauri awahamasishe Wavuvi wake waonane na Maafisa Uvuvi, wawasaidie kuandika maandiko mazuri yatakayowasaidia kupata mikopo hiyo ili waweze kupata hizo nyenzo za uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Maboto, baada ya Bunge hili tuonane nimwelekeze, nimpe mawasiliano ya wanaohusika na habari hii ili waweze kumsaidia kuandika maandiko mazuri yatakayomsaidia kupata mkopo.
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mkakati gani wa kudhibiti uvuvi haramu katika Wilaya ya Kilwa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika jibu la msingi kwamba Serikali inakusudia kuanzisha chombo maalum kitakachosimamia, kwa sababu habari hii ya uvuvi haramu imekuwa ni suala mtambuka, kila maeneo, kila sehemu uvuvi haramu umetamalaki, sasa Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi, tumekuja na mkakati maalum wa kuanzisha chombo maalum kitakachosimamia wavuvi na shughuli zote za uvuvi ikiwa ni pamoja na uvuvi haramu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwenye eneo la Wilaya hiyo, Serikali itakapoanzisha chombo hiki kitakuwa na mamlaka ya kusimamia maeneo yote nchi nzima yanayohusiana na masuala ya uvuvi, ahsante.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa kwangu Wilaya ya Rorya tayari zaidi ya vikundi nane vimeshaandika andiko kwa ajili ya kupewa vizimba na boti; je, ni lini vikundi hivi vitapatiwa mahitaji haya?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kama vikundi hivyo tayari vimeshaomba na tayari vimeshafanyiwa assessment, awamu ya kwanza alifanya Mheshimiwa Rais hivi majuzi, awamu ya pili tunaenda. Kama tayari wameshakidhi vigezo watapatiwa vizimba hivyo.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kama ambavyo amezungumza Naibu Waziri kuhusiana na suala la kuomba vizimba na maboti, sisi kama Jimbo la Mchinga, tumeshaomba vizimba na tumeshaomba maboti; je, Serikali inatuambiaje juu ya jambo hili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maeneo ambayo tayari wavuvi wameshaomba vizimba, sasa tunakwenda kwenye mgao wa awamu ya pili ambao hivi karibuni tutaanza mgao huo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kama vikundi vyake tayari vimekidhi vigezo na masharti yaliyowekwa na Benki yetu ya Kilimo, tutaenda kuwapatia vizimba hivyo.
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Je, ni lini Serikali itatoa mafunzo kwa vikundi vya BMU (Beach Management Unit) kwa ajili ya kuwa na nguvu ya kuzuia uvuvi haramu?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, tayari Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeshaanza kutoa mafunzo kwenye vikundi vya BMU. Kama Mheshimiwa Mbunge ana kikundi ambacho pengine kinahitaji mafunzo hayo, tuko tayari kwenda kumfundisha, ahsante.
MHE. AGNESS E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ninayo maswali mawili ya nyongeza.

(a) Je, kwa nini Serikali haiwalipi Mameneja wanao kaimu katika Vyuo vya Uvuvi pamoja na Wakurugenzi ambao wamekaimu kwa miaka zaidi ya 12?

(b) Wizara haioni imedumaza maendeleo ya Vyuo vya Uvuvi nchini ikiwemo Mikindani Mtwara kwa kuwakaimisha mameneja wake na kutokuwa na taratibu za uendelezaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nianze na hili la kwanza kwamba haiwalipi makaimu; utaratibu wa Serikali uko wazi kwamba mtumishi yeyote anaweza akakaimishwa nafasi yoyote kama ana vigezo na upekuzi ukikamilika anataeuliwa kushika nafasi hiyo rasmi kulingana na maelekezo ya Serikali yalivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa kesi hii ya Mikindani, tumekuwa tukifanya upekezi kwa muda mrefu wenye sifa wanakosekana lakini tumeendelea kutafuta watu wenye uwezo wa kushika nafasi hizo katika maeneo hayo na sasa Serikali inaelekea mwishoni kukamilisha taratibu za uteuzi ili apatikane Mkurugenzi atakayekuwa ameshika nafasi katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na kwamba anafuatilia sana kwa karibu jambo hili kwa muda mrefu, nimhakikishie kwamba ndani ya muda mfupi tutakwenda kukamilisha jambo hili. Lengo la Serikali ni kuweka watu wenye weledi, wenye uwezo wa kushika nafasi hizo na si lengo kudumaza vituo hivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo naomba kuwasilisha.
SPIKA: Mheshimiwa Waziri, nadhani kulikuwa na swali la pili linalohusu kudumaa kwa wale wanaokaimu, kwamba wanashindwa kuendelezwa.

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi tumeendelea kutoa mafunzo mbalimbali kwa wataalam wetu, kwa hivyo wataalam wale wanapopata mafunzo wanaojiendeleza wanakuwa na sifa za kushika nafasi hizo, kwa hiyo tumekuwa tukiangalia katika hao tuliowapa mafunzo, Je, wapi wana uwezo wa kushika nafasi hizi za kukaimu nafasi za juu katika uongozi?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tumeendelea kutoa mafunzo, mafunzo hayo yamezidi kuwasaidia wataalam wetu kujipatia uwezo wa kushika nafasi hizi na lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba wale wote wenye uwezo wa kushika nafasi hizi wanapewa nafasi hizo.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, amekiri kila kata, kila Kijiji ni lazima kuwepo na Maafisa Ugani, pamoja na kutoa ajira na kuajiri, kwa nini Maafisa Ugani wanakwenda kuwekwa sehemu ambayo hawana uhitaji? Kwa mfano, unampeleka Afisa Ugani Kata za Dar es Salaam, Kata za Arusha, kwa nini wale wa kule msifanye reshuffle mkawapeleka vijijini ili wakawasaidie wafugaji wetu ambao ng’ombe wao wanapata adha kubwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, kumekuwa na tozo nyingi kwa wafugaji wetu kwa sababu ya kukosa elimu na Maafisa Ugani. Je, kama Serikali hamuoni kwamba mtengeneze mkakati mziondoe zile tozo, msaidie wale wafugaji ili sasa wafurahie matunda ya Serikali yao?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nianze na hili la kuwaweka Maafisa Ugani maeneo ya Mijini. Kwanza tukiri kwamba Maafisa Mifugo wetu walioko katika Taifa letu wanahitajika mahali pote kwa sababu hata huko Mjini ambapo Mheshimiwa Mbunge anapasema pia kuna wafugaji. Kama si wafugaji wa kufuga ng’ombe wa kuchunga kama vijijini wako wafugaji wanafuga ndani kwa ajili ya kuzalisha maziwa. Kwa hiyo Maafisa Ugani tukubali kwamba wanahitajika maeneo yote.

Mheshimiwa Spika, issue hapa ni upungufu wa Maafisa Ugani tulionao katika nchi yetu, hii inatokana na uwezo wa kifedha wa kibajeti ambao kama tungepata fedha za kutosha maana yake tungekuwa tunaajiri Maafisa Ugani wa kutosha katika Taifa letu, mijini na vijijini kwa sababu kote panahitaji Maafisa Ugani.

Mheshimiwa Spika, hili la pili kuhusu tozo. Sisi Wizara ya Mifugo hatuna tozo nyingi kiasi hicho. Tozo nyingi ziko katika Halmashauri ambako Mheshimiwa Mbunge ni Mjumbe wa Kamati ya Fedha na Mipango, nafikiri kule wakikaa kwenye vikao vyao sasa waende kupunguza tozo kwa wafugaji wetu ili wafugaji wetu waweze kufuga ufugaji watija.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kama ambavyo imeelezwa katika swali la msingi, zao hili ni muhimu sana. Sasa ili kiwanda kipate malighafi kwa maana ya maua, kiwanda kile kiko kwenye mazungumzo na Wizara ya Mambo ya Ndani kupitia Jeshi la Magereza ili kukodi eneo katika Gereza la Isupilo ili waweze kuzalisha maua kama sehemu ya malighafi.

Je, Wizara ya Kilimo iko tayari kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Ndani kuhakikisha kwamba mpango huo unakuwa fast trucked ili eneo hilo lipatikane kwa wakati? (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kama ambavyo imeelezwa katika swali la msingi, zao hili ni muhimu sana. Sasa ili kiwanda kipate malighafi kwa maana ya maua, kiwanda kile kiko kwenye mazungumzo na Wizara ya Mambo ya Ndani kupitia Jeshi la Magereza ili kukodi eneo katika Gereza la Isupilo ili waweze kuzalisha maua kama sehemu ya malighafi.

Je, Wizara ya Kilimo iko tayari kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Ndani kuhakikisha kwamba mpango huo unakuwa fast trucked ili eneo hilo lipatikane kwa wakati? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Wizara ya Kilimo kwenye jambo lolote jema na lenye tija ya kuongeza uzalishaji kwenye zao la pareto, tuko tayari kushirikiana na Wizara yoyote ikiwemo Wizara ya Mambo ya Ndani kupitia Jeshi la Magereza ili kuhakikisha tunapata eneo na kuongeza uzalishaji katika zao la pareto, ahsante.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, moja, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Katika majibu ambayo Mheshimiwa Naibu Waziri ametoa, ameunganisha skimu mpya zinazotarajiwa kuanzishwa na skimu ambazo zipo sasa.

Mheshimiwa Spika, hoja yangu kubwa ni kwamba, Skimu ya Murwazi, Ruhwiti na Katengera zipo. Tatizo ni miundombinu yake imeharibika na hivyo hazifanyi kazi inavyostahili. Swali langu, ni lini Serikali itapeleka fedha hizo kwa haraka ili kuhakikisha skimu hizo zinakarabatiwa na ujenzi unafanyika ili wananchi waweze kufaidi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari sasa baada kikao hiki twende pamoja ili kuhakikisha kwamba anaiona skimu hizi ili kutoa suluhisho haraka sana? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza nimthibitishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, moja ya maelekezo ambayo tumeyapata kutoka kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ni kuhakikisha kwanza tunakarabati skimu zote ambazo zilikuwepo na zimeharibika. Pili, tujenge maeneo mapya na kutambua maeneo yanayofaa kwa kilimo cha umwagiliaji. Hayo ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, sasa katika maelekezo yake, sasa hivi tunapotaka kufanya maboresho ya hizi skimu zilizoharibika, ni lazima tufanye upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ili tupate gharama halisi, tofauti na ule utaratibu uliokuwa unatumika zamani, mtu akiona tu dharura anapeleka shilingi milioni 500, lakini hajui kuna gharama kiasi gani zinahitajika. Ndiyo maana kulikuwa na mwendelezo wa matatizo mengi katika skimu zetu nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hilo kwa sasa hivi lipo katika utekelezaji na tukimaliza tu tutatenga fedha kwa ajili ya kuzikarabati na kuzijenga. Kuhusu kwenda, niko tayari mara tu baada ya Bunge lako Tukufu kumalizika.
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi; je, ni lini Serikali itampata mkandarasi katika Jimbo la Singida Kaskazini kwenye Skimu ya Umwagiliaji Msange.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, Mradi wa Isange, nafikiri Tume ya Umwagiliaji ipo katika mchakato. Pia, mnafahamu kwamba mchakato ni hatua, ukishakamilika tu maana yake tutatangaza mkandarasi ambaye anahusika katika ujenzi wa Skimu ya Msange, ahsante.
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Nami nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa Serikali imeshawekeza gharama kubwa kwenye Skimu ya Dongobeshi shilingi bilioni 2.5 kwa maana ya kukalimisha tuta na torosho la maji. Je, Serikali haioni sasa ni wakati wa kuweka kipaumble kukamilisha miundombinu iliyobaki kwa maana ya banio, vitorosha maji pamoja na kusakafia mifereji mikubwa?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; Serikali inawekeza gharama kubwa sana kujenga miundombinu ya umwagiliaji, lakini haitoi mafunzo kwa wakulima pamoja na viongozi wa Tume ya Maji. Je, kwa ajili ya kudumisha uendelevu wa miradi ya umwagiliaji, Serikali sasa haioni umuhimu wa kuwapa mafunzo viongozi wa Tume ya Maji kabla na baada tu ya kuimarisha miradi ya umwagiliaji? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI K.n.y. WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, jambo moja ni kwamba, ndiyo maana atakapomaliza kazi Mshauri Mwelekezi Mwezi Mei ni kwamba kitakachofuata baada ya hapo ni kuweka huu mradi kwa ajili ya mwaka wa fedha unaokuja ili uanze kujengwa. Kwa hiyo, ni sehemu ya vipaumbele vyetu sisi kama Wizara kuhakikisha Mradi wa Dongobeshi katika mwaka wa fedha ujao unaanza kutekelezwa. Kwa hiyo, lipo katika kipaumbele chetu.

Mheshimiwa Spika, kuhusu mafunzo, tunafanya hivyo kwa sababu katika kila mradi tunaweka bajeti kwamba, baada ya mradi kukamilika, wale watumiaji wa maji kwa maana mradi mzima lazima wapatiwe mafunzo ya namna bora ya kutumia, na vilevile, kuutunza ule mradi husika. Kwa hiyo, jambo hilo lipo na kikubwa tu tutaongeza kasi ili tuweze kuwafikia watu wengi, ahsante sana.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itakarabati Skimu za Umwagiliaji za Nyendara, Muhambwe, Kumbanga na Kugorogondo katika Jimbo la Muhambwe?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI K.n.y. WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nimthibitishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba moja ya wajibu mkubwa wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ambayo inafanya kazi sasa hivi, ni kufanya upembuzi yakinifu na ufafanuzi wa kina kwa miradi yote ya umwagiliaji, maana yake, malengo tuliyonayo sasa hivi ni kujenga mabwawa pamoja na schemes zikiwemo hizi ambazo Mheshimiwa Mbunge amezitaja za Garara, Muhambwe na miradi mingine ambayo ameitaja hapa. Kwa hiyo, tuko katika kazi na tukishamaliza hapo, maana yake tutatenga fedha katika bajeti yetu ili tuanze kuzijenga na nyingine kuzikarabati, ahsante.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha na kupelekea udongo wenye rutuba kwenda mabondeni, je, Serikali haioni kuwa kuna haja ya kujenga mabwawa katika Kata ya Makanya, Gare, Kwayi pamoja na maeneo mengine katika Jimbo la Lushoto?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI K.n.y. WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Mpango wa Serikali ni kujenga Mabwawa katika maeneo yote ambayo tunaweza tukakusanya maji yakatumika katika kipindi chote cha mwaka ili Watanzania waweze kuingia katika kilimo kinachotumia maji badala ya kutegemea msimu mmoja wa mvua.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mpango wetu ni pamoja na kutumia ikiwemo Bonde la Makanya, lipo katika mpango. Ndiyo maana mwaka huu wa 2022/2023 tuliomba Serikali itupitishie bajeti kwa ajili ya ujenzi wa mabwawa 100. Kwa hiyo, hilo ndilo lengo la Serikali na tutafanya hivyo. Ahsante sana.
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naishukuru sana Serikali kwa ahadi ya kunipatia madume 20 ya ng’ombe katika mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la kwanza. Kiasi hiki cha madume 200 ambayo Serikali inanunua ukilinganisha na idadi ya ng’ombe tuliyonayo ni hatua kidogo sana. Kwanza, hata hayo madume yenyewe tunayachosha kwa maana ya wingi wa majike yaliyopo. Je, Serikali haioni kwamba badala ya kununua madume 200 tuongeze tufike angalau hata 1,000 ili nchi nzima katika maeneo ya wafugaji tuweze kupata madume mengi na kwa uhakika?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Dodoma tuna Kituo cha Utafiti wa Malisho pale Mpwapwa na hapa Kongwa, lakini ukija katika Wilaya yangu ya Bahi kwenye kata za wafugaji ukianzia pale Chifutuka, Chipanga na Chikora, hakuna hata nyasi moja ya utafiti ambayo imeletwa katika wilaya yetu. Je, Serikali ina mpango gani wa vituo hivi ambavyo vina miaka mingi, lakini taarifa zake na matunda yake hayafiki katika wilaya zinazovizunguka? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na hili la madume 200. Ni kweli madume 200 ni wachache na mpango wa Serikali ni kuongeza kadri ya upatikanaji wa bajeti. Tunamhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tuko tayari kuongeza madume hao kadri ambavyo bajeti inapatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu hili la nyasi, tayari wataalam wetu wanaendelea na utafiti katika maeneo mbalimbali ya nchi, ukiwemo Mkoa wa Dodoma. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, mara tu utafiti utakapokamilika, basi mbegu za nyasi bora zitakwenda katika Jimbo lake la Bahi. Kwa sasa watafiti wetu wanafanya utafiti katika maeneo mbalimbali ikiwa ni Mkoa wa Morogoro, Mkoa wa Dodoma na maeneo mengine, na Bahi pia watafika kwa ajili ya kukamilisha utafiti huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, tutakuja Bahi kwa ajili ya kukamilisha utafiti huo na majibu yatakapopatikana, wataalam wetu wako tayari kutoa elimu kwa wafugaji wetu ili waweze kutumia nyasi hizo zinazotakiwa. Ahsante.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, je, ni lini Serikali itajenga Kiwanda cha Nyama na Malighafi za Mifugo Wilayani Ngorongoro kwa kuwa 80% ya wananchi katika wilaya hii ni wafugaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ujenzi wa Kiwanda cha Nyama, Serikali inaendelea kuhamasisha wawekezaji mbalimbali katika maeneo mbalimbali ili kuwekeza katika sekta hii kwa sababu imeonekana viwanda hivi vina tija katika mazingira hayo. Kwa hiyo, tunamwomba Mheshimiwa Mbunge pia kama ana mawasiliano na wadau mbalimbali katika maeneo mbalimbali wanaoweza kuwekeza katika sekta hii, pia tuko tayari kushirikiana nao katika kuhakikisha kwamba viwanda hivi vinapatikana katika Taifa letu. Ahsante.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Je, nini mpango wa Serikali kwa vikundi vya wafugaji wa Simanjiro, Kiteto na Hanang kuleta mbegu ya madume bora?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika jibu la msingi, ni kwamba madume bora yapo na katika bajeti ya mwaka huu pia tutaongeza idadi ya madume bora, na Wilaya ya Hanang, Kiteto, Simanjiro na maeneo mengine kote ambako wanahitaji madume bora, tuko tayari kuwapelekea. Ahsante.
MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa kuwa bei ya madume bora wamekuwa ni ghali sana hasa kwa hawa wa Serikali, kwa nini Serikali isipunguze bei sana ili wafugaji waweze kununua?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli madume hawa bei yake ilikuwa iko juu. Ilikuwa ni shilingi 4,000,000/= mpaka shilingi 6,000,000/=, lakini kwa concern hiyo ya Mheshimiwa Mbunge, pia madume hao wameshashuka bei. Sasa madume hao wanapatikana kwa shilingi 1,000,000/= mpaka shilingi 1,500,000/=. Kwa hiyo, Serikali inaendelea kupokea ushauri kama bei hiyo pia itakuwa bado inawatatiza wafugaji wetu, tuko tayari kuishusha na kuona namna ambavyo tutawasaidia wafugaji wetu katika maeneo mbalimbali. Ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mpango mzuri wa Serikali wa kuhakikisha kwamba, madume bora wanapatikana, lakini ni ukweli usiopingika kwamba wapo ng’ombe wa asili, kwa mfano wenye asili ya Wafipa ambao wanapatikana ndani ya Mkoa wa Rukwa ambao size yake ni kubwa na wanafanya vizuri kama wanyamakazi. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba hatupotezi specie hii ambayo ni nzuri?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inaendelea kuhamasisha ufugaji wa kisasa, na hawa ng’ombe wa asili anaowasema Mheshimiwa Mbunge kama wataonesha kuwa na tija, tuko tayari kuwalinda, lakini kusema kweli kwa sasa Wizara inajikita zaidi kwenye kuhamasisha ufugaji wa kisasa, wenye tija, wenye kutumia eneo dogo na kwa faida kwa ajili ya wafugaji wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wataalam wanaendelea kufanya uchunguzi wa jambo hili na ikionekana mbegu hizi za Wafipa zina faida kwa wafugaji wetu, tuko tayari kuzilinda na kama zinaonekana hazina faida, ni vizuri wafugaji wetu wakajifunza kufuga kisasa kwa ajili ya faida yao ya baadaye. Ahsante. (Makofi)
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, Serikali haioni haja kwenye mabwawa saba yaliyotengwa katika Mradi wa ASDP II ukiwemo Mkoa wa Simiyu, likajengwa katika Jimbo la Meatu kwa sababu ndio wilaya yenye mifugo mingi, ndio wilaya yenye ukame mkubwa na maeneo yapo mengi, wafugaji wapo tayari kuyatoa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; je, ni lini Serikali itakipelekea shilingi milioni 6.8 Kikundi cha Mwamalole cha kupanda nyasi kwa kuwa, mvua nazo zinaeleka kwisha? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naanza na hili la kwanza la mabwawa saba; tumepokea maombi ya Mheshimiwa Mbunge na ushauri wake. Tutatazama tuone namna ambayo inafaa zaidi kwenye Jimbo lake hili la Meatu. Kwa kuongezea katika hilo ni kwamba, Wizara ya Mifugo, Wizara ya Kilimo pamoja na Wizara ya Maji tumekubaliana yale malambo yanayojengwa kwa ajili ya shughuli za kilimo cha uwagiliaji ambayo yanajengwa na Wizara ya Kilimo pamoja na mabwawa makubwa yanayojengwa na Wizara ya Maji ambayo yanafanya shughuli za kuhifadhi maji, tumekubaliana sasa yawe na mabirika kwa ajili ya wafugaji ili yaweze kutumika kwa shughuli za mifugo katika maeneo yetu. Kwa hiyo, tutaangalia katika malambo saba ambayo yanajengwa na pia, tutaangalia katika Wizara ya Kilimo na Wizara ya Maji, kama kuna uwezekano wa kutengeneza mabirika kwa ajili ya wafugaji wetu ili waweze kupata huduma hiyo ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili la pili, la shilingi milioni sita kwenda kwa vikundi vyake. Namwomba Mheshimiwa Mbunge kwamba, leo nitalifuatilia jambo hili na baada ya hapo nitakupa majibu halisi juu ya namna gani ambayo tunakwenda kusaidia vikundi vyetu hivyo katika maeneo yetu. Ahsante. (Makofi)
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, kwanza naipongeza Serikali kwa hatua hii ambayo tumefikia, lakini mpaka jana tunaongea, mkandarasi amepokea shilingi milioni 50 tu kati ya fedha zote hizo alizoomba. Sasa swali langu la kwanza ni hili; ni lini sasa Serikali itakuwa serious kuhakikisha kwamba, fedha zote anazohitaji mkandarasi zinaenda kwa sababu wananchi wa Igamba wanakisubiri kwa hamu sana chuo hiki?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; je, Mheshimiwa Naibu Waziri, yuko tayari sasa kuongozana na mimi kwenda Igamba, Mkoa wa Songwe, akaangalie kinachoendelea pale? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, sisi Wizara ya Mifugo tumetimiza wajibu wetu. Tumeomba fedha Wizara ya Fedha na tayari documents zote ziko Wizara ya Fedha na mara tutakapopata fedha, tutapeleka kwenye ujenzi wa chuo hicho. Kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba, fedha zitakapokuwa tayari tutazipeleka kwa ajili ya ujenzi wa chuo hicho.

Mheshimiwa Spika, la pili la kutembelea chuo hiki; Wizara iko tayari, mimi au Mheshimiwa Waziri tuko tayari, kutembelea chuo hicho na kama kuna mapungufu ama changamoto zozote tuko tayari kwenda kuzitatua, ahsante.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, naipongeza Taasisi ya Uvuvi na Utafiti kwa kuweza kuendelea na mchakato wa kubaini maeneo yanayofaa kwa ajili ya ufugaji wa samaki wa vizimba. Swali langu la kwanza; ni lini Serikali itamaliza mchakato huo ili wananchi wa Ludewa wapate fursa ya kuendelea na biashara hiyo?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; Wizara ina mkakati gani wa kufanya utafiti katika maeneo ambayo ni mazalia ya samaki kwa lengo la kuhifadhi na kufanya samaki waendelee kuwa wengi katika Ziwa Nyasa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema katika jibu la msingi kwamba, tumepokea concern ya Mheshimiwa Mbunge, tutaiweka katika bajeti ya 2024/2025 ili kwenda kufanya tathmini katika eneo hilo analolizungumza Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Spika, hili la pili, namna gani ya kuongeza uzalishaji wa samaki; kama nilivyosema katika majibu ya msingi kwamba, Serikali sasa imekuja na mpango wa vizimba na tunazidi kuhamasisha wavuvi wajikite zaidi katika vizimba kwa sababu, uvuvi huu wa sasa umebadilika duniani kote, kwamba sasa tunakwenda katika hali ya kutengeneza vizimba ili kuleta tija zaidi katika uzalishaji wa samaki.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu katika Maziwa yetu yote makubwa Nyasa, Victoria na Tanganyika, ukweli ni kwamba, mazalia ya samaki yanapotea kwa sababu ya wingi wa watu na uvuvi haramu. Kwa hiyo, ni lazima tuje na mkakati mpya ambao utawezesha watu wetu kuendelea na uvuvi wa kisasa zaidi, hasa kwenye vizimba, ahsante.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwa kuwa kwa kiasi kikubwa upungufu wa samaki unachangiwa na uvuvi haramu: Je, Serikali imejipangaje katika kuhakikisha inapambana na uvuvi huu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Kwa kuwa, mwitikio wa umuhimu wa ufugaji kwa kutumia vizimba katika Ziwa Tanganyika upo chini sana: Je, Serikali ipo tayari kwa kushirikiana na Wabunge wanaotoka ukanda wa Ziwa Tanganyika kutoa elimu kwa wananchi ili waweze kuchangamkia fursa hii?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza na hili swali la kwanza. Ni kweli, uvuvi haramu unachangia kwa kiasi kikubwa sana kupungua kwa samaki katika maziwa yetu, siyo tu Ziwa Tanganyika, bali maziwa yote yanayozunguka nchi yetu. Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi tayari imeshaweka mikakati madhubuti kuhakikisha uvuvi haramu unakwenda kukomeshwa katika maziwa yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikakati ipo mingi na nisingependa sana kuisema kwa sababu mingi inahusisha masuala ya kiintelijensia. Tayari vijana wetu wa kijeshi wameshaanza kufanya operation katika maeneo mbalimbali kuhakikisha tunadhibiti uvuvi haramu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mzuri ni kule Bahari ya Hindi. Wale Wabunge wanaotoka katika maeneo hayo, tayari wameona jitihada za Serikali kukomesha uvuvi kwa njia ya mabomu kama ambavyo Serikali imechukuwa hatua stahiki zinazotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuhusiana na vizimba. Ni kweli, tumeshaanza kutoa elimu, na elimu haina mwisho, tunaendelea kutoa elimu kupitia wataalamu wetu. Mimi na Mheshimiwa Waziri tayari tumeshafika katika maeneo hayo kuendelea kutoa elimu kwa wavuvi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tupo tayari kushirikiana na Waheshimiwa Wabunge tunapopata nafasi, siku za weekend tunakwenda kutoa elimu. Hata baada ya Bunge, tupo tayari kushirikiana na Waheshimiwa Wabunge kwenda kutoa elimu kwa wavuvi wetu ili waweze kuelewa namna sahihi ya kuchukua vizimba na boti kwa ajili ya mikopo ya riba nafuu ambayo Wizara imekuwa ikiendelea kuitoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ipo tayari kushirikiana na Waheshimiwa Wabunge kuhakikisha tunakwenda kutoa elimu kwa kusaidiana na Serikali, ahsante.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri anajua kwamba Ziwa Tanganyika sisi tunaotoka maeneo yale ndiyo shamba letu na ndiyo duka letu, hivyo unapopumzisha hilo ziwa kwa miezi mitatu, ningependa kufahamu, Serikali mmetenga kiasi gani kwa ajili ya kuwapatia wavuvi kwa kipindi hicho cha mpito?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi hiki cha miezi mitatu ni kweli, kama anavyosema Mheshimiwa Mbunge kuwa Ziwa Tanganyika kwa asilimia kubwa wanaozunguka eneo hilo, ndiyo shamba lao. Kwa kutambua hilo, Wizara imekuja na mkakati wa kuwakopesha wavuvi hao vizimba. Vizimba hivi vitasaidia kuongeza uzalishaji ambao umekuwa ukifanyika katika hilo Ziwa Tanganyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiukweli wavuvi wa Ziwa Tanganyika wamepokea jambo hili kwa mikono miwili na wapo tayari. Pia tayari tumeshapokea maombi mengi na tarehe 5/5/2024 Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi anakwenda kukabidhi vizimba kwa wale wote walioomba katika eneo la Ziwa Tanganyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tupo tayari kuendelea kutoa vizimba kwa wale watakaoomba na milango ipo wazi waendelee kuomba. Huu ndiyo utakuwa mbadala pekee wa kuwasaidia wavuvi katika eneo hilo la Ziwa Tanganyika.