Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Judith Salvio Kapinga (57 total)

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Pia nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri yenye matumaini kwa wananchi wangu wa Rorya, lakini ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; kwa kuwa Sheria ya Uthamini inatamka wazi kwamba thamani ya ardhi inapaswa kulipwa ndani ya miezi sita, lakini wananchi hawa wamedai malipo yao toka mwaka 2011 na hawajalipwa. Nataka nipate commitment ya Serikali itakapofika Novemba kama wananchi hawa hawajalipwa uthamini wa ardhi yao, je, Serikali itakuwa tayari sasa kurudia uthamini kwa mujibu wa Sheria inavyotamka kwamba wananchi wale walipwe ardhi kwa mujibu wa Sheria inavyotamka?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kwa kuwa jambo hili limekuwa ni la muda mrefu toka mwaka 2011 na sasa liko ndani ya Ofisi ya Mkurugenzi nataka nipate commitment ya Serikali hasa Ofisi ya Wizara ya TAMISEMI, je, ni lini watalipa fedha ili wathamini warudi site wakamilishe uthamini na upande wa TANESCO waweze kulipa fidia kwa wananchi hawa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jafari Chege, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusu kurudia zoezi ikifika Novemba, zoezi hili limeshachukua muda mrefu nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Serikali imeshatenga fedha kiasi cha milioni 350 ili wananchi 231 wanaodai fidia walipwe ikifikia Novemba, 2023. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba zoezi hili tunaenda kulikamilisha na kwa sababu limechukua muda tutafuatilia kwa ukaribu kuhakikisha kwamba linakamilika.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la pili kuhusiana na kutoa fedha, tayari Serikali kupitia TANESCO imeshatoa fedha kiasi cha shilingi milioni 15 kwa ajili ya kukamilisha zoezi la uthamini. Tutafuatilia kuhakikisha kwamba Halmashauri ya Rorya inakamilisha taratibu hizi kwa wakati ili zoezi hili liweze kukamilika kwa wakati kwa kadri ambavyo imepangwa, ahsante. (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba nitumie nafasi hii tena kumwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Rorya kuhakikisha kwamba fedha hizi ambazo wenzetu wa TANESCO wameshazipeleka kwenye halmashauri ile ziweze kutumika mara moja na kulipa fida hiyo. (Makofi)
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mradi wa Geita - Nyakanazi na Nyakanazi - Rusumo kuna baadhi ya wananchi wa Biharamulo ambao wanapitiwa na mradi ule katika Kata nne za Rusahunga, Kaninha na Nyakahula nao pia bado hawajalipwa pesa zao za fidia. Je, ni lini Serikali itaweza kukamilisha malipo hayo kwa baadhi ya watu ambao walikuwa hajalipwa pesa zao? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nijibu maswali ya Mheshimiwa Engineer Ezra Chiwelesa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na fidia ya Geita - Nyakanazi tayari Serikali ilishatenga fedha bilioni sita na tayari fedha bilioni 5.9 zilishalipwa kwa ajili ya wananchi na wananchi waliobakia ni wananchi 49 tu, tunaamini taratibu zikikamilika na wao wataweza kulipwa.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Nyakanazi -Rusumo pia Serikali ilishatenga fedha bilioni 3.8 na tayari bilioni tatu ilishalipwa, wananchi waliobakia ni 39 tu. Nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia na kwa sababu fidia hii imekamilika kwa zaidi ya asilimia 95, tutafuatilia kuhakikisha kwamba kidogo kilichobakia kinaweza kukamilika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri. Hata hivyo nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, tuna Kijiji cha Mlundelunde, Kitongoji cha Mchaka ambacho kina shule ya sekondari ambapo bahati mbaya umeme umepita juu yake na shule ile ya sekondari kama taasisi ya Serikali, haijapata ule umeme: Je, nini maelekezo ya Serikali kwa REA Mtwara ili waweze kufanya haraka kuunganisha umeme katika hiyo shule ya sekondari?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Tumepata changamoto kubwa kwa Jimbo letu la Masasi Mjini ambapo tuna Kata saba za Sururu, Mwengemtapika, Matawale, Chanikanguo, Temeke, Marika pamoja na Mmbaka ambazo ziko vijijini, lakini wanatakiwa kulipa shilingi 320,000/= kama sehemu ya ada ya uunganishaji wa umeme: Je, Serikali haioni ni wakati muafaka sasa, wananchi hawa wapate haki kwa maana wapo vijijini, waunganishiwe umeme kwa shilingi 27,000/= kama vijiji vingine?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Geoffrey Mwambe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na shule ambayo ameitaja, shule hii ipo katika moja ya kitongoji ambapo utaenda kutekelezwa mradi wa vitongoji 15 ambavyo tayari Serikali imeshatenga fedha kwa mwaka huu wa fedha. Tunaanza kufanya ufuatiliaji ili tuweze kuona ni namna gani tunaanza kutekeleza mradi huu wa vitongoji 15.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na swali lake la pili juu ya maeneo ya vijijini ambayo yanakataliwa kutozwa shilingi 27,000/=, tayari Serikali tumeshaya-identify haya maeneo na tuko katika mchakato wa mwisho ili kuweza kutolea maelekezo kwa maeneo kama haya ambayo yanaleta mkanganyiko wa bei.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza swali la nyongeza. Mkandarasi aliyekabidhiwa vijiji 15 vya Wilaya ya Hanang’ kasi yake inasuasua sana: Je, nini kauli ya Serikali juu ya Mkandarasi huyu ili kuwapa matumaini wananchi wa Wilaya ya Hanang’?

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asia Halamga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkandarasi aliyekuwepo Hanang’ Nakurwa Investment Company ni kweli alikuwa anasuasua lakini tumemsimamia na katika vijiji 15 ambavyo vimebakia, vijiji tisa ameshasambaza nguzo, na tuna imani mpaka ifikapo Desemba, 2023 atakuwa amekamilisha kuweka umeme vijiji vyote, ahsante.
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza naishukuru Serikali kwa majibu mazuri. Hali ya makali ya mgao wa umeme katika Wilaya ya Kahama pamoja na Halmashauri yake ni makali mno, hali ni ngumu, wafanyabiashara wanashinda wamekaa, umeme umekatika siku nzima. Sasa Mheshimiwa Waziri yupo tayari kufanya ziara katika Wilaya hii ya Kahama pamoja na Halmashauri zake ajionee hali ilivyo kwa wananchi hawa?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili. Je, Serikali ina mkakati gani sasa wa kuipa Mkoa wa ki-TANESCO Wilaya hii ya Kahama ambayo inakua kwa kasi kwa nchi hizi za maziwa makuu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Emmanuel Cherehani.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na mgao wa umeme, kwa sababu sasa hivi tumetengamaa na tumepunguza kidogo ule upungufu ambao ulikuwepo, niwaelekeze TANESCO na kituo chetu cha pamoja cha gridi (Grid Control Center) wahakikishe maeneo yote yanaendelea kupata umeme kulingana na jinsi ambavyo tunaboresha upatikanaji huo wa umeme.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na ziara, nitafika Ushetu Mheshimiwa Mbunge. Suala la pili kuhusiana na kuweka kituo cha kimkoa Ushetu, Mheshimiwa Mbunge tutaendelea kuangalia tathmini kama Wilaya ya Kahama inafaa kuwekwa kama Mkoa wa ki-TANESCO kwa ngazi ya mkoa, na kama itafaa, basi tutafanya hivyo, lakini kama haifai, tutaendelea kuboresha huduma ili wananchi wa Ushetu waendelee kupata huduma bora na stahili za masuala ya umeme. (Makofi)
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa. Hospitali mpya ya Wilaya ya Mabogini imeshaanza kutoa huduma, je, Serikali ina mpango gani kupeleka umeme katika Hospitali yetu hii mpya?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Hospitali ya Mabogini tayari tumeshaifanyia tathmini na tupo katika mchakato wa kupata fedha ili ifikapo Januari, 2024 tuweze kuhakikisha Hospitali hii ambayo tayari inafanya kazi iweze kupatiwa umeme wa uhakika, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Licha ya majibu mazuri ya Serikali, nina maswali madogo mawili.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza. Kata ya Mgambazi ipo kwenye Manispaa ya Morogoro, lakini mpaka sasa hivi Mtaa mzima wa Mgambazi pamoja na Chambilazi na Vilengwe hawajapatiwa umeme, licha ya kuwa kwenye Manispaa ya Morogoro: Je, ni lini watapata umeme? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kijiji cha Zongo ambacho kiko kwenye Kata ya Kisemo pamoja na Kijiji cha Bwakila Juu katika Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro Vijijini, hawajapata umeme. Ni lini vijiji hivi vitapatiwa umeme? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Dkt. Christine Ishengoma kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na umeme katika Mitaa ya Mungazi, Chambilazi na Vilengwe tayari tumeshaiweka kwenye Mpango wa fedha wa 2025 na mitaa hii itapatiwa umeme.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Vijiji vya Zongo na Bwakila Juu, tayari wakandarasi wamepatiwa site na muda wowote kazi itaanza, ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Serikali iliahidi kufunga umeme katika shule zote za sekondari na taasisi za dini, lakini zipo shule ambazo hazijaweza kufungiwa umeme; je, ni lini Serikali itafunga umeme katika Shule ya Sekondari Kimenyi, katika Halmashauri ya Kasulu DC? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Genzabuke, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tayari kuna miradi inaendelea kwenye vijiji vyote ya kupeleka umeme. Mwanzoni ilikuwa kilomita moja, tumeongeza kilometa mbili ili taasisi nyingi zifikiwe. Kwa shule hii ya Kimenyi kama haipo katika scope ambayo ipo sasa hivi, tutahakikisha kwamba tunaweka fedha kwenye mwaka ujao ili na wenyewe waweze kupatiwa umeme, ahsante.
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Wananchi wa Kilwa wamekuwa ni wanufaika wakubwa wa umeme wa gesi unaozalishwa katika Kituo cha Somanga.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kukiboresha kituo hiki ili kumaliza changamoto kubwa inayokabili wananchi wa Kilwa katika huduma ya umeme? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ndulane, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tayari tumeanza mkakati wa kurekebisha kufanya matengenezo kwenye visima vyetu ambavyo vinazalisha gesi na tumeshaanza Mnazi Bay, Songosongo pamoja na Madimba. Kwa Somanga pia tutahakikisha tunaweka kwenye mkakati ili tuweze kukiboresha na wananchi wa Kilwa waweze kupata umeme wa uhakika, ahsante.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa tatizo la kukatika umeme katika Manispaa ya Morogoro linafanana na tatizo lililopo katika Wilaya na Mkoa wa Kilimanjaro, hususan Kata ya Uru Kusini; ni lini sasa TANESCO itarekebisha tatizo hilo kabisa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shally Raymond, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tatizo la kukatika kwa umeme halipo tu Morogoro na Kilimanjaro, limekuwepo kwa Tanzania nzima. Serikali tumechukua hatua. Mwanzoni tulianza na upungufu wa Megawati 421 wastani hapo. Mpaka kufikia leo tumefanikiwa kupunguza upungufu kwa wastani wa Megawati 218. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tunachukua hatua.

Mheshimiwa Spika, nilieleza hapa kwamba Bwawa la Mwalimu Nyerere tumefikia 94.01% na tumeshaanza majaribio. Pia, nimesema hapa tumeongeza uzalishaji kwenye visima vetu vya Songo Songo pamoja na Madiba ili kuweza kuongeza gesi ili tuweze kupunguza changamoto hii ya upatikanaji wa umeme. Tayari tunafanya matengenezo kwenye mitambo yetu yote ili kuboresha hali. Nina uhakika Waheshimiwa mmeona hali ya upatikanaji wa umeme imeanza kutengemaa.

Mheshimiwa Spika, niwahakikishie tutaendelea kufanya kazi hii nzuri ili kuhakikisha tunaiondoa nchi katika changamoto ya umeme, ahsante. (Makofi)
MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Uyui Makao Makuu yake ni Isikizya, kilometa 35 kutoka Tabora Mjini, na lipo tatizo kubwa kweli la umeme. Watumishi pale; DC na Wakurugenzi hawafanyi kazi kutwa nzima, umeme unakatika zaidi ya mara tano kwa siku; je, Serikali ina mpango gani wa kuweka umeme wa kudumu pale Isikizya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Almas Maige, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tayari Serikali tumechukua hatua katika Halmashauri ya Uyui na katika Mkoa mzima wa Tabora. Tumechukua hatua na tuna mradi unaendelea wa kujenga vituo vya kupooza umeme na line za kusafirisha umeme. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, baada ya mradi huo kukamilika ndani ya miezi 18, tatizo la kukatikakatika kwa umeme unaotakana na line ndefu kutoka Tabora Mjini mpaka Uyui mpaka kwenye Jimbo la Mheshimiwa Sitta tutakuwa tumelipunguza.

Mheshimiwa Spika, pia nimwelekeze Meneja wa TANESCO Mkoa wa Tabora ahakikishe ratiba wanazozipanga zinazingatia maeneo ambayo yanatoa huduma kwa wananchi hususan maeneo ambayo yanatoa hospitali, vituo vya afya pamoja na shule na maeneo mengine ambayo yanatoa huduma kwa wananchi, ahsante.
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, wakati wa Bunge la Bajeti, Serikali iliahidi kupeleka turbine ya megawati 20 kule Mtwara kama hatua za dharura za kupunguza tatizo la upungufu wa umeme ambalo linasababisha kukatikakatika kwa umeme; je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anastazia Wambura kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli tuliaahidi kupeleka hii taibai kutoka Ubungo kwenda Mtwara. Baada ya tathmini ya kina tulijirididha mtambo huu hautafanya kazi vizuri pale Mtwara. Tumeshaongea na Kampuni ya CSI juu ya kuzalisha umeme hapo na tumeshakamilisha, na tuna kituo cha kupoza umeme tunakijenga hiyari ambacho tunategemea kitakamilika ndani ya mwezi huu. Kikikamilika basi, umeme ambao utatolewa na Kampuni ya CSI utaweza kwenda kwenye Mkoa mzima wa Mtwara na Lindi na hivyo tutakuwa tumeondoa kabisa changamoto ya umeme kwa Mikoa miwili.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunawaomba Waheshimiwa Wabunge na wananchi wa Mtwara na Lindi watuvumilie kidogo mpaka mwishoni mwa mwezi huu tutakuwa tumekamilisha na kuwapatia umeme wa uhakika, ahsante.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ipo dhamira ya Serikali ya kupeleka umeme vijijini kote na umeme kufika maeneo ya mbali kabisa kutoka Mkoa wa Singida ambako ndio sub-station kubwa ilipo eneo la Rungwa, lakini umeme unafika ukiwa faint na Serikali ilikuwa na dhamira ya kujenga kito cha kupoza umeme kwa maana ya sub-station katika eneo la Mitundu. Je, Serikali inaanza lini kujenga kituo cha kupoza umeme Mitundu, ili kusaidia wananchi, ili waweze kujiwezesha na viwanda vidogo vidogo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yahaya Massare, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli mpango huo upo, na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tunatafuta fedha na pili, mchakato huo wa upatikanaji wa fedha ukikamilika basi tutaanza kujenga kituo hiki cha kupoza umeme, ahsante.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Spika, kwa kuniona. Naomba kuuliza swali. Je, ratiba ya mgawo wa umeme katika Jimbo letu la Temeke umekuwa ni wa muda mrefu sana na ratiba yake haifuatilii kadiri ya ratiba zinavyokuja kwamba, umeme utakatika kuanzia muda fulani mpaka muda fulani, sasa umekuwa ni wa muda mrefu sana. Kuanzia jana mpaka leo saa hizi Temeke hatuna umeme, je, una tamko gani Waziri, ili kule Temeke waweze kutuletea umeme kulingana na mgawo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dorothy Kilave, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyotangulia kusema, kidogo tumetengemaa kwenye suala la upatikanaji wa umeme, na kwa Mkoa wa Dar es Salaam tunafahamu maeneo mengi kwa sasahivi yanaweza yakapitisha hata siku mbili mpaka tatu bila kukatika kwa umeme. Kwa hili ambalo ambalo ameniambia Mheshimiwa Mbunge inaonekana ni suala ambalo ni specific, yaani ni mahususi. Naomba nilifuatilie, Mheshimiwa Mbunge, nikitoka hapa na nitakupatia majibu, ahsante. (Makofi)
MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, tarehe 10 Agosti, 2021 TANESCO na STAMICO waliasaini makubaliano ya kuzalisha megawati 200 kutoka kwenye Mgodi wa Makaa ya Mawe Kiwira; je, mpango huo umefikia wapi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Jumbe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mpango huu bado upo na tunautekeleza kulingana na upatikanaji wa fedha, ahsante.
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa swali la nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, nini mpango wa Serikali katika kupeleka umeme katika Shule ya Sekondari ya Tawa katika Halmashauri ya Morogoro Vijijini.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Kalogeris, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tayari tuna miradi ambayo inaendelea kwenye kila Mkoa kuhusiana na kupeleka umeme. Nitafuatilia kuona kama Shule ya Sekondari Tawa ipo katika mipango ambayo tunayo, na kama hamna, basi tutafanya jitihada za ziada, ili kuhakikisha Shule ya Sekondari Tawa inapatiwa umeme, ahsante.
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Spika, ahsante, je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha maeneo ya uzalishaji pamoja na hoteli za kitalii kama za Mkoa wa Arusha hazipati adha ya ukatikaji wa umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zaytun Swai, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimeshatangulia kusema hapo awali, Serikali tunafanya jitihada mbalimbali kuhakikisha tunapunguza adha ya upatikanaji wa umeme. Na kwa kadiri ya mipango hii, nimhakikishie, maeneo haya ya uzalishaji yataendelea kuendelea kupata umeme wa uhakika kwa kadiri ambavyo tunaboresha upatikanaji wa umeme. Ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru sana Serikali kwa majibu mazuri, nami nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza: Je, ni mikoa mingapi hapa nchini hadi sasa haijaunganishwa na Gridi ya Taifa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili: Nafahamu kwamba Kigoma nayo ipo katika mpango wa kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa kupitia vituo vya Urambo na Ipole Sikonge. Sasa swali ni kwamba wananchi watalipwa lini fidia kwenye ile njia ya kutoka Tabora kwenda Ipole?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kakunda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na mikoa ambayo haijaunganishwa kwenye Gridi ya Taifa, mikoa miwili ya Katavi na Rukwa ndiyo ambayo haijaunganishwa kabisa kwenye Gridi ya Taifa. Mikoa ya Mtwara, Lindi, Kigoma na Kagera imeunganishwa kidogo kwa Msongo wa kilovolt 33, lakini miradi inaendelea ili tuiunganishe kwa Msongo Mkubwa wa Kilovolt 220 na Kilovolt 400. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na fidia ambayo ameuliza Mheshimiwa Mbunge, tayari tumeshafanyia kazi na tunategemea ifikapo tarehe 30 mwezi huu wa Novemba, 2023 wananchi wataanza kulipwa, ahsante.
MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Spika, naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza; kwa kuwa Mvomero ni miongoni mwa Wilaya ambazo ziko vijijini; na kwa kuwa, Kijiji cha Madizini, Lusanga, Manyinga, Turiani, Kilimanjaro na Kichangani, havikuwahi kupata hadhi ya kisheria kuwa miji midogo; Mheshimiwa Naibu Waziri, huoni sasa kuna haja ya kutoa maelekezo wananchi wa vijiji hivi walipie umeme kwa shilingi 27,000 badala ya kulipia umeme kwa shilingi 321,000? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Wananchi wa Tarafa ya Turiani wamekuwa wanapata adha kubwa sana ya kukatika kwa umeme: Je, Mheshimiwa Naibu Waziri, huoni sasa ni wakati muafaka kutenga bajeti ya kwenda kuboresha miundombinu hii inayotoka Morogoro kuelekea Turiani ya kupeleka umeme kwa sababu miundombinu hii ni ya muda mrefu na imechakaa kwa kiwango kikubwa sana? Nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jonas Zeeland, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Vijiji vya Madizini, Lusanga, Manyinga, Kilimanjaro, Kichangani na Turiani, vilitolewa tangazo, lakini havijaidhinishwa kama miji midogo. Kwa hiyo, niwaelekeze TANESCO Mkoa wa Morogoro kuendelea kuwa-charge wananchi 27,000 kwa maeneo haya yote ambayo hayajaidhinishwa kama miji kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la pili la line ya umeme inayotoka Turiani kwenda Kilosa na Gairo, mwaka huu wa fedha tumetenga bajeti ya matengenezo. Nikuahidi, kama matengenezo hayatakamilika, mwaka ujao wa fedha tutaendelea kutenga bajeti ili kuhakikisha tunaboresha miundombinu hii ili wananchi waendelee kupata umeme wa uhakika, ahsante. (Makofi)
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona; ni lini Serikali itapeleka umeme kwenye vitongoji zaidi ya asilimia 70 katika Wilaya ya Kyerwa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oliver Semuguruka, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tayari Serikali tumeanza mpango wa kupeleka umeme kwenye vitongoji vyote vilivyobakia 36,000. Kwa kuanza, tumeanza kwa miradiya ujazilizi ambayo tumeshaweka wakandarasi na vilevile tunategemea kuendelea kutafuta wakandarasi kwa Mradi wa Vitongoji 15 kwenye kila jimbo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, vitongoji katika Jimbo la Kyerwa na vyenyewe vitafikiwa, ahsante. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujua, lini wananchi wa Jimbo la Bunda watapata umeme wa REA II C kwa vijiji 147?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mradi wetu wa II C tumetenga vitongoji 17 na kwa mradi ujao pia, vitongoji 15 Jimbo la Bunda litapata. Kwa hiyo, kwa kuanzia wataanza na vitongoji 32, ahsante.
MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa, tulisema mpaka mwezi wa 12 mwaka huu, vijiji vyote vitakuwa vimepata umeme na bado kuna vijiji kama Kiteto hatujapata umeme. Nini kauli ya Serikali kwa mpango huu wa mwezi wa 12 vijiji vyote vipate umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Edward Olelekaita, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli, Wakandarasi wote ambao tumewapatia mikataba ya kwisha Desemba 30, kupeleka umeme kwenye vijiji vyote, lazima wakamilishe kupeleka umeme kulingana na mikataba yao. Wale ambao walipewa ziada mpaka Juni, 2024 wata-cross kwenda 2024. Niwaelekeze Wakandarasi wote, yeyote ambaye hatahakikisha anamaliza mkataba wake kwa muda, bila sababu za msingi, hatutasita kuchukua hatua na kuweza kutokuendelea na mkataba wake ikifika Desemba, 30 mwaka huu, ahsante.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa kuwa vitongoji vinavyopewa umeme ni vile ambavyo line za umeme kubwa tayari zilishapita, lakini kwenye jimbo langu kuna Kitongoji kama Nindi na Songeapori ambavyo viko mpakani na kuna changamoto kubwa za kiusalama.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuvisaidia vitongoji hivi viwili kwa jicho la kipekee? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Stella Manyanya, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, vitongoji hivi viwili kwa kweli, vimekaa kimkakati. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa awamu hii ya ujazilizi utaweka addition scope ili vitongoji hivi viweze kufikiwa na umeme kwa umahususi wake, ahsante.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi ya swali la nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, usambazaji wa umeme wa REA katika Kata ya Nanjirinji na Kata ya Likawage, umekwama kwa sababu ya mgogoro kati ya TFS pamoja na mkandarasi. Nini Kauli ya Serikali katika kutatua mgogoro huu ili wananchi wapate umeme huo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Kassinge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge nikuahidi, nitafuatilia suala hili ili kuhakikisha linatatuliwa kwa wakati na wananchi waweze kupata umeme katika maeneo yao, ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, je, ni lini Serikali itapeleka umeme kwenye vijiji sita vilivyobakia kwenye Tarafa ya Mikumi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christine Ishengoma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mkandarasi katika vijiji hivi yuko site anaendelea na kazi. Nimhakikishie tu, ifikapo Juni, 2024 vijiji hivi vyote vitakuwa vimepatiwa umeme, ahsante.
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kufanya rejea kwenye zana nzima ya local content ambayo imeweka takwa la kisheria kwamba, katika miradi wakandarasi kwa maana fursa za zabuni pamoja na ajira ziweze pia kupatikana kwa wale wanaotoka kwenye maeneo ya mradi (host community). (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa msingi huo nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, katika hao 42 waliowasilishwa hapa na Serikali ambao amesema kwamba ni wakandarasi pamoja na watoa huduma. Ukweli ni kwamba hao 42 ni watoa huduma (local suppliers) na siyo wakandarasi (local contractors). (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, swali langu la kwanza. Je, Serikali ipo tayari kufanya tathmini ya kina, kuweza kuainisha maeneo na fursa ambazo wakandarasi wa Mkoa wa Kagera wanaweza wakapewa kinyume na ilivyo hivi sasa? Fursa zingine wamepewa wakandarasi kutoka mikoa mingine, kama Mwanza ili hali Mkoa wa Kagera wanao wakandarasi wanaoweza kufanya kazi hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, je, Serikali kupitia Wizara ya Nishati wapo tayari kuja Mkoa wa Kagera ili kukaa na Uongozi wetu wa Mkoa wa Kagera chini ya Mkuu wa Mkoa wetu Mheshimiwa Fatma Mwasa, kujadili na kuona namna bora ya kuhakikisha kwamba Wakandarasi wa Mkoa wa Kagera wanapata fursa (local contractors), jambo ambalo litaweza kuhakikisha ulinzi wa mradi (host community) kinyume na ilivyo hivi sasa jambo ambalo linasikitisha, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Neema Kachiki Lugangira, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na kufanya tathmini, kwa kuwa Mradi huu wa Ujenzi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima Uganda mpaka Chongoleani Tanga umefikia 32.6%. Nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge tunavyoendelea kwenye utekelezaji wa mradi, tutahakikisha wakandarasi wadogo ambao wanatokea maeneo ambapo mradi unatekelezeka wanaendelea kupewa fursa, kadri ambavyo tunaendelea na utekelezaji wa mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na kutemebelea Mkoa wa Kagera Mheshimiwa Mbunge nikuhakikishie, tutakuja ili kuweza kuona ni namna gani tunaweza tukashirikiana kwenye masuala haya ya msingi ambayo tunaamini yanagusa jamii ya watu wa Kagera. Lakini vilevile kwa kwa jamii zote ambazo mradi unatekelezeka tutahakikisha tunafanya hivyo kwa maslahi ya wananchi vile vile kwa maslahi ya utekelezaji wa mradi, ahsante.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, ukizingatia kwamba Bandari ya Dar es Salaam ni bandari ya nchi nzima siyo Dar es Salaam peke yake, lakini tumeona kwamba mafuta kwa maana ya petroli na dizeli zimekuwa rahisi zaidi Dar es Salaam kuliko maeneo mengine ya pembezoni. Kwa mfano, kwa Taarifa ya EWURA ya jana petroli Dar es Salaam ni 3,257 na dizeli 3,210 lakini ukienda Songwe ni 3,374 na dizeli ni 3,227 na maeneo mengine hali kadhalika.

Mheshimiwa Spika, maswali yangu mawili ya nyongeza; la kwanza; je, Serikali inategemea kumaliza lini tathmini hiyo ili utekelezaji huu uanze mara moja na wananchi walioko nje ya Dar es Salaam waepuke hiyo changamoto? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Serikali imejipangaje kuhakikisha kwamba inatatua changamoto za nyuma kama ambavyo imezisema kwenye majibu yake ya leo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kuhusiana na kumaliza tathmini yalikuwa ni maelekezo ya Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, kufanya tathmini hii kwa haraka sana ili kuweza kujua kama tunaenda kwa mfumo huo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge suala hili ni la kipaumbele na tathmini itakamilika hivi karibuni na kisha tutaweza kufanya tathmini, ili kuweza kujua kama kweli tunaweza kwenda kwenye mfumo huo. Kwa hiyo, ni suala la kipaumbele kwa upande wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile tathmini itatueleza namna ambavyo tulipata changamoto huko nyuma na kwa sasa tujipange vipi ili kuelekea kuwa na mfumo huu kama tathmini itatuelekeza hivyo. Ahsante.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, naomba niulize swali moja dogo lenye sehemu (a), (b), (c), (d) kama ifuatavyo: -

SPIKA: Mheshimiwa ni (a) na (b) pekee. Kwa hiyo, katika hayo manne chagua mawili.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante.

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuongea na wadau ili waweze kuondoa gharama kubwa iliyopo ya ununuzi wa mtungi wa gesi na gesi yenyewe, wakati mchakato wa kupunguza au kuweka ruzuku kwenye nishati ya gesi unaendelea kwa Serikali?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Shule ya Ufundi Mtwara Tech. imefunga mfumo wa gesi asilia suala ambalo limepunguza gharama kubwa ambayo ilikuwa inatumika wakati wakitumia nishati mbadala ya kuni na mkaa. Wakati wakitumia nishati hiyo walikuwa wanatumia shilingi milioni saba. Sasa baada ya kuweka mfumo wanatumia shilingi milioni 1.8.

(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka mfumo huo kwenye Taasisi zote za Serikali ikiwemo Chuo cha Ualimu Matogolo na Shule za Sekondari zote katika Mkoa wa Ruvuma na nchi yote ya Tanzania? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa namna anavyofuatilia matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la ruzuku, ajenda ya nishati safi ya kupikia ni ajenda ya Mheshimiwa Rais mwenyewe. Wote mnakumbuka wakati wa mkutano wa COP28 Dubai, alizindua Mkakati wa Nishati ya Kupikia kwa Wanawake Afrika. Kwa hiyo, jambo hili tumelibeba kwa uzito sana.

Mheshimiwa Spika, kuhusu ruzuku tayari tuna programu na miradi kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya tunayo programu ambapo mawakala wanawezeshwa kifedha ili kupunguza bei ya mitungi kwa wale wanunuaji wanaonunua gesi kwa mara ya kwanza. Tutaendelea kubuni miradi na kutafuta fedha ili kuhakikisha wananchi wanapata mitungi ya gesi kwa gharama rahisi zaidi.

Mheshimiwa Spika, la pili, kuhusiana na kuwekeza mifumo ya gesi katika taasisi; kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) tumeshaanza mradi kwa ajili ya kuweka nishati hii safi ya kupikia ya gesi kwenye magereza, kambi za Jeshi pamoja na shule za msingi na sekondari. Tutaendelea kutafuta fedha ili kuhakikisha tumefikia taasisi nyingi zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwa taasisi alizosema za Mkoa wa Ruvuma tutazingatia pia, ili kuhakikisha wanawekewa mifumo hii, ahsante.
MHE. JESCA D. KISHOA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Julai mwaka huu mkataba huu unatakiwa kusainiwa, nataka kujua majadiliano haya yatakamilika lini?

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Mkataba wa Songas kwa takriban miaka 20 umekuwa una changamoto kubwa sana eneo la shareholding structure. Sasa, kwa lengo la kuongeza uwazi na uwajibikaji pamoja na kwamba tuna TEIT, Je, serikali haioni kuna umuhimu wa ku-list shares zake kwenye stock market kwa sababu kule kuna scrutiny ya hali ya juu na hesabu zinawekwa wazi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na lini majadiliano yatamalizika, majadiliano haya tunategemea yatamalizika ifikapo mwezi wa tatu mwishoni. Kuhusiana na suala la pili la Serikali kuweka shares zake kwenye stock market, tumezingatia ushauri wa Mheshimiwa Mbunge na tutafanyia kazi wakati tunaendela na majadiliano, ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa vijiji 29 vilivyopo Jimbo la Ludewa vinahudumiwa na mzalishaji binafsi wa umeme na vinakabiliwa na changamoto ya bajeti kwa wazalishaji binafsi; na kwa kuwa Serikali imeshafanya kazi kubwa ya kutambua gharama za kufikisha umeme kwenye vitongoji na kuwasha umeme Mawengi na Milo: Je, nini ahadi ya Serikali kwa wananchi wale ikizingatiwa sasa tunaenda kwenye bajeti?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali moja la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na uzalishaji wa umeme kwenye vijiji hivyo 29, nafahamu kuna changamoto ya umeme kwa sababu ya wazalishaji ni wawezeshaji binafsi, lakini Serikali kupitia REA tunao mpango wa kuwawezesha wazalishaji binafsi wa umeme na utaratibu upo. Vilevile, tutaendelea kushirikiana nao kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata umeme wa uhakika. Pia, tunao mkakati wa kuhakikisha wananchi hawa wanapata umeme kupitia miradi ya Serikali ambayo tunayo na tutahakikisha hilo linafanyika haraka iwezekanavyo ili wananchi waondokane na kadhia hiyo, ahsante.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza hapa. Kwanza, ningependa kujua katika maeneo haya ambayo yanafanya utafiti wa gesi na mafuta ni leseni ngapi zimetolewa kwa ajili ya uchimbaji wa gesi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, napenda kujua Serikali ina mkakati gani wa kuendelea kunadi vitalu hivi ili kupanua wigo wa uwekezaji na kuweza kuthibitisha zaidi kiasi cha rasilimali hizi ambazo tunazo nchini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, hadi sasa kwa maeneo haya 84 ambayo tunafanya tafiti, tunazo jumla ya leseni 11 ambapo leseni nane ni za utafutaji na leseni tatu ni za uzalisahaji wa gesi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili, kwa sasa hivi Wakala wa Udhibiti wa Mkondo wa Juu Wa Petroli (PURA) akishirikiana na Wizara tunao mkakati wa kuendelea kufanya maandalizi ya kunadi zabuni za vitalu kwa ajili ya kuleta wawekezaji zaidi ili kufanya tafiti na kuthibitisha rasilimali hii, ahsante.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, ukizingatia kwamba Bandari ya Dar es Salaam ni bandari ya nchi nzima siyo Dar es Salaam peke yake, lakini tumeona kwamba mafuta kwa maana ya petroli na dizeli zimekuwa rahisi zaidi Dar es Salaam kuliko maeneo mengine ya pembezoni. Kwa mfano, kwa Taarifa ya EWURA ya jana petroli Dar es Salaam ni 3,257 na dizeli 3,210 lakini ukienda Songwe ni 3,374 na dizeli ni 3,227 na maeneo mengine hali kadhalika.

Mheshimiwa Spika, maswali yangu mawili ya nyongeza; la kwanza; je, Serikali inategemea kumaliza lini tathmini hiyo ili utekelezaji huu uanze mara moja na wananchi walioko nje ya Dar es Salaam waepuke hiyo changamoto? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Serikali imejipangaje kuhakikisha kwamba inatatua changamoto za nyuma kama ambavyo imezisema kwenye majibu yake ya leo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kuhusiana na kumaliza tathmini yalikuwa ni maelekezo ya Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, kufanya tathmini hii kwa haraka sana ili kuweza kujua kama tunaenda kwa mfumo huo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge suala hili ni la kipaumbele na tathmini itakamilika hivi karibuni na kisha tutaweza kufanya tathmini, ili kuweza kujua kama kweli tunaweza kwenda kwenye mfumo huo. Kwa hiyo, ni suala la kipaumbele kwa upande wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile tathmini itatueleza namna ambavyo tulipata changamoto huko nyuma na kwa sasa tujipange vipi ili kuelekea kuwa na mfumo huu kama tathmini itatuelekeza hivyo. Ahsante.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa mkakati wake wa kuhakikisha kwamba sasa tunakwenda kupata nishati safi na salama ya kupikia. Ni jambo kubwa, tunampongeza sana na wananchi wa Mkoa wa Dar es Salaam wamelipokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu ni kwamba, kwa kuwa wananchi wa Mkoa wa Dar es Salaam wamehamasika na wako tayari katika matumizi ya nishati safi ya gesi ya kupikia, lakini kwa kuwa changamoto kubwa ni gharama ya hiyo gesi na Serikali imeonesha mipango ya kusambaza gesi hiyo ambayo ina gharama nafuu kwa wananchi, je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuelekeza nishati hiyo au mabomba hayo kwenye maeneo yenye wananchi wengi kama Kawe, Mwenge, Mbagala, Manzese na maeneo mengine, badala ya ku-base kwenye eneo hilo hilo la Mbezi Beach na Mikocheni peke yake?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Tunao mpango wa kuhamasisha matumizi ya gesi asilia nchini, na kwa sasa hivi tunao mkakati wa kupeleka gesi kwenye nyumba takribani 10,000. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba maeneo hayo ambayo ameyataja yenye watu wengi yatafikiwa na huduma hii ili waweze kutumia gesi kwa gharama nafuu zaidi kwa sababu gesi hii inayounganishwa majumbani ina unafuu zaidi kuliko gesi ile ya LPG ya mitungi. Ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, Serikali imehamasisha matumizi ya nishati safi na Watanzania wengi hasa wa vijijini wamehamasika, lakini bei, kwa maana ya gharama ya ujazaji wa gesi ni kubwa sana. Nataka kujua, nini mkakati wa Serikali katika kuhakikisha inatoa ruzuku ili kupunguza gharama za gesi kusudi wale wananchi maskini wa kijijini waache kutumia kuni na mkaa, watumie gesi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, tunao mkakati wa matumizi ya nishati safi ya kupikia ambao tunaenda kuukamilisha hivi karibuni ili kuweka mkakati wa kukabiliana na changamoto zote ambazo zinawazuia wananchi wasiweze kutumia gesi katika kupikia. Kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge, baada ya mkakati huu kukamilika, tutakuwa na mikakati madhubuti wa kuwawezesha wananchi wote kutumia gesi safi ya kupikia ili kupunguza matumizi ya mkaa na kuni.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kule Tunduru Kusini na Jimbo langu la Nanyumbu tunao madereva pamoja na mafundi sanifu ambao sasa hivi wapo katika ajira za muda kati ya miaka mitano na miaka saba. Je, wizara ipo tayari sasa katika ajira zinazokuja kuwafikiria madereva hawa ambao wamekuwa muda mrefu katika shirika? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, jukumu la kupeleka umeme vijijini lipo chini ya REA. REA jukumu lake ni kupeleka umeme vijijini na baadaye kuwaachia TANESCO kuwaunganishia wateja. Je, Serikali haioni wakati umefika REA baada ya kupeleka umeme vijijini iwaunganishie wateja ndipo iwakabidhi kwa TANESCO wateja wote badala ya kuwaachia TANESCO kufanya kazi ya kuwaunganishia wateja hao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na ajira kwa ajili ya madereva, kwanza niwapongeze Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Mhata na Mheshimiwa Mpakate, kwa kazi nzuri wanazofanya katika majimbo yao. Kuhusiana na ajira za vibarua hawa, kama wizara tunathamini sana mchango wa wafanyakazi wetu vibarua hususani mafundi na madereva. Nataka niwahakikishie kwa kuwa ni wafanyakazi wetu ambao wanafanya kazi kwa jitihada kubwa sana kulitegemeza shirika letu, tutahakikisha ajira zinapotoka wanazingatiwa ipasavyo kulingana na sheria na taratibu za utumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na suala la REA kuendelea na kuunganisha wateja pale ambapo miradi inakamilika. Ushauri wa Mheshimiwa Mbunge tumeupokea na tutauchakata kuona kama unatekelezeka na kama unatekelezeka hatutasita kuufanyia kazi, ahsante. (Makofi)
MHE. AGNESTA L. KAIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wanaotumia umeme wa REA vijijini wamekuwa wakipata changamoto kubwa sana za huduma za haraka pale inapotokea hitilafu ya umeme na hii ni kwa sababu ya mafundi wengi wanakaa Makao Makuu. Swali langu, je, Serikali haioni umuhimu sasa wa kuajiri mafundi hawa maalum kwa ajili ta kitengo cha dharura na kuwasambaza huko vijijini ili wananchi hawa waweze kupata huduma za haraka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa mawazo mazuri. Nataka nimhakikishie kuhusiana na suala la huduma kwa wateja tayari tumeshaanza kufanyia kazi kuhakikisha tunakitegemeza kitengo hiki ili kiweze kuwa na huduma nzuri kwa wateja. Kuhusiana na suala la mafundi tayari tumekuwa tukiongeza viunga kwenye maeneo ya mbali ili wananchi waweze kupata huduma za uhakika. Kwenye suala la mafundi, kuongeza mafundi Mheshimiwa Mbunge tumelipokea na tutaendelea kulifanyia kazi kuhakikisha wananchi wanapata huduma nzuri. (Makofi)
MH. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali yenye kutupa matumaini naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; baada ya Serikali kutupatia katika kipindi hiki hiyo mitaa 15, vipi sasa kuhusiana na ile mitaa ambayo haikutajwa hapo ambayo imebaki mfano Chora, Damai, Ngereli pamoja na Hurumbi na yenyewe mpango wao ukoje?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; je, ni lini Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari kufuatana na mimi twende Kondoa kwa ajili ya kuona yale mazingira na namna watu wanavyohitaji huo umeme. Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri anayoifanya kwenye jimbo lake. Katika mitaa ambayo ameitaja Mheshimiwa Mbunge tutazingatia katika bajeti inayofuata kuona kama mitaa mingine imebakia tunaweza kuiingiza baadhi ili kuweza kuwafikishia wananchi huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na kuambatana na yeye jimboni, tutapanga na Mheshimiwa Mbunge siku za hivi karibuni ili tuweze kwenda kuona utekelezaji wa miradi katika jimbo lake, ahsante. (Makofi)
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru swali langu la msingi linauliza ni lini mradi huu utakamilika?

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nina maswali mawili ya nyongeza; swali la kwanza narudia, ni lini mradi huu utakamilika?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, nini mpango wa Serikali katika kunusuru Mji wa Mpanda dhidi ya katikakatika ya umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kuendelea kufuatilia mradi huu wa kufikisha umeme wa Gridi ya Taifa Katavi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na lini mradi huu utakamilika? Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Wana-Mpanda na watu wa Katavi wote kwa ujumla. Suala la kupeleka Gridi ya Taifa Mpanda na Katavi ni suala la kipaumbele chini ya Awamu ya Sita kuhakikisha mikoa yote ambayo haijaunganishwa na Gridi ya Taifa inaunganishwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunamwomba kwa niaba ya watu wa Katavi watuvumilie kidogo, mradi unaenda vizuri na kwa maelekezo ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati tunasimamia kwa weledi mkubwa sana na nina imani miezi michache ijayo tutakuwa tumekamilisha hii njia ya kusafirishia umeme, uzuri kituo cha kupooza umeme kimeshafikia 98%. Kwa hiyo, ni njia tu hii ya kusafirishia umeme itakamilika hivi karibuni na watu wa Katavi watapata umeme wa Gridi ya Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, tunaelewa umuhimu wa umeme wa uhakika Mpanda na Katavi kwa sababu wananchi wa Katavi ni wafanyakazi wazuri sana. Sasa kwa hatua za haraka, kwa maelekezo ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati leo mafundi wetu watafungua mtambo wa megawati moja Biharamulo ili kuweza kuupeleka Mpanda pale ili kuweza kuongeza uzalishaji kwa sababu mahitaji ni megawati saba, lakini tunazalisha karibia megawati 6.15 tutaongeza megawati moja ili tuweze kupunguza mgao Katavi pamoja na Mpanda, ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, Serikali inatambua kwamba njia hiyo ya umeme haiwezi kukamilika bila kuwalipa wananchi wa Sikonge fidia ya shilingi bilioni 2.2 ambayo bado Wizara ya Fedha haijaipa Wizara ya Nishati hizo hela.

Sasa ni lini Wizara ya Fedha itatoa fedha hizo ili Wizara ya Nishati walipe fidia hiyo ili kukamilisha huo mradi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, suala la fidia la wananchi hawa wa Sikonge tayari tunalifanyia kazi. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tupo kwenye hatua za mwisho kwa ajili ya kufanya malipo haya na uzuri Wizara ya Fedha wameshaji-commit kwamba wanatoa fedha kwa ajili ya kulipa fidia wananchi hawa. Tunaomba wananchi wa Sikonge, Tabora na yale maeneo ambayo wanadai fidia katika mradi huu wa njia ya kusafirisha umeme kutoka Tabora hadi Mpanda waendelee kutuvumilia, tutalipa fidia hiyo kwa sababu tayari tulishaji-commit kwamba tutalipa, ahsante.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali kwa majibu yake.

Kwa kuwa maeneo yote ya mitaa iliyotajwa na Mheshimiwa Naibu Waziri maeneo mengi makazi ya watu yamerukwa na uingizaji wa umeme; je, Serikali haioni kuwa sasa ni wakati mwafaka wa kuingiza yale maeneo ya huduma ya afya, elimu na maeneo ya makanisa kuingizwa kwenye mradi huu wa kuingiza umeme kwa shilingi 27,000?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa tayari katika eneo la Mbulu Mjini, maeneo mengi yaliyopelekewa huduma ya umeme yamekuwa na changamoto nyingi ya wananchi kushindwa kuingiza umeme kwa yale yaliyofikiwa.

Je, Serikali haioni kuwa ni wakati mwafaka kutazama upya nchi nzima maeneo yote ambayo wananchi wameshindwa kuingiza umeme kwa gharama kubwa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge, kwanza, kwenye upande wa maeneo ambayo yamepitiwa na umeme, lakini taasisi hazina umeme, tayari nimeshajibu kwenye jibu la msingi kwamba, mitaa ile 12 iliyobakia tunao mkakati wa kupelekea umeme kupitia mradi wa vitongoji kwa mwaka ujao wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile niwasihi REA waweze kufanya tathmini kwenye maeneo haya na kuweza kuona kama maeneo haya yanaweza yakaingizwa kwenye Mradi wa Peri Urban na kisha taasisi zilizopo katika maeneo haya na yenyewe yaweze kupata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili la Mheshimiwa Mbunge, kwenye maeneo yenye sura ya vijiji lakini yapo mijini tayari Wizara ya Nishati kupitia Shirika la Umeme (TANESCO) tumeshafanya mapitio kwenye maeneo 1,570 ya maeneo ambayo yana sura ya vijiji, lakini yapo mijini ili kuweza kuona uwezekano wa kutoka shilingi 320,000 hadi shilingi 27,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, maeneo yake ambayo yana picha hiyo na yenyewe tutayapitia kuweza kuona kama yanakidhi vigezo vya kuingia kwenye utaratibu huu wa shilingi 27,000. Ahsante. (Makofi)
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru. Katika Jimbo la Tarime Vijijini maeneo ya Vijiji vya Nyangoto, Kerende, Mjini Kati, Nyabichune na Nyamwaga wananchi wangu wanalipia umeme shilingi 320,000 kinyume na sera ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nini kauli ya Serikali wananchi wapate umeme kwa bei nafuu ambayo imeelekezwa vijijini? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye maeneo haya ambayo ameyataja Mheshimiwa Mbunge, tutayapitia kuona kama yapo kwenye yale maeneo 1,570 ambayo tumeshayaainisha na kama hayapo tutayafanyia tathmini kuweza kuona kama na yenyewe yanaweza kuingia katika mpango huo ili wananchi waweze kupata huduma ya kuunganisha umeme kwa shilingi 27,000. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, je, ni lini Serikali itawapatia umeme wananchi waliopo katika Mtaa wa Msisina, Msalagala na Kisowele, Iringa Mjini kwa sababu maeneo hayo yalikuwa katika Jimbo la Ismani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, mitaa hii ambayo ameitaja Mheshimiwa Mbunge ya Msisina, Msalagala na Kisowele itaenda kupatiwa umeme kupitia mwaka wa fedha 2024/2025. Ofisi yetu ya TANESCO - Mkoa wa Iringa, imeshaweka kwenye mpango huo, lakini vilevile katika mitaa hiyo kuna Mtaa mmoja pia wa Kipululu na wenyewe hauna umeme. Tulishawaelekeza TANESCO kupitia Ofisi ya Mkoa waweze kutenga special fund ili mitaa yote hii minne ambayo haina umeme waweze kupatiwa umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, mitaa hii tayari ipo kwenye mpango na yote itapata umeme kwa mwaka ujao wa fedha, ahsante. (Makofi)
MHE. JESCA D. KISHOA: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nishukuru Serikali kwa kutupatia umeme kwenye vijiji vyote 70, lakini changamoto kubwa iliyopo ni size ya transformer zilizofungwa. Wamefunga size ya transformer kVA 50 na mahitaji ni makubwa, wananchi wana viwanda vya alizeti na viwanda vya kuchomelea. Swali la kwanza; je, Serikali haioni kuna haja ya kufunga transformer za kVA 200 mpaka 345 ili kupata umeme wa uhakika?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; nimesikia Serikali kwamba wako kwenye hatua za kutafuta wakandarasi kwa ajili ya kutengeneza kwenye vitongoji. Kumekuwa kuna kasumba miaka yote ya kupata wakandarasi wasiokuwa na sifa. Nataka kujua Serikali wamejipanga vipi kuhakikisha katika eneo la due diligence hawafanyi makosa? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante, tumepokea maoni ya Mheshimiwa Mbunge na maoni ya Waheshimiwa Wabunge wengi na kwa hivyo tumefanyia kazi, kuanzia mwaka huu unaokuja wa fedha 2024/2025, tutaongeza ukubwa wa transformer. Zitakuwepo transformer za ukubwa wa KVI 50, KVI 100 na KVI 200 na zitafungwa kulingana na mahitaji ya eneo husika. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge, jambo hilo tumelipokea na lipo tayari kwenye utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na wakandarasi wanaosuasua kwenye miradi; maelekezo ya Serikali, kupitia Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, yalishatoka. Hatutawavumilia wakandarasi wote wanaotekeleza miradi kwa kusuasua na kutoendelea mbele, kupitia Taasisi zetu za TANESCO na REA hatutawapatia kazi wakandarasi wanaosuasua katika miradi yetu, ahsante.
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, ahsante, Wilayani Rungwe vijiji saba mpaka sasa hivi havijafikiwa na umeme wa REA. Vijiji hivyo ni Mpindo, Kata ya Bulyaga; Isumba Kata ya Kinyala; Kyobo Juu, Kata ya Ikuti; Ngumbulu, Kata ya Isongole; Mpombo, Kata ya Lupepo; Isabula, Kata ya Kisiba; na Kasanga, Kata ya Mpombo. Je, ni lini vijiji hivyo vitapata umeme wa REA? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nimwambie Mheshimiwa Mbunge, katika vijiji vyote hivi saba vilivyopo katika Jimbo la Rungwe mkandarasi yuko site. Namhakikishia kwamba, tutaongeza usimamizi kuhakikisha vijiji hivi vinapatiwa umeme kulingana na mikataba yetu ambayo ni Juni, mwaka huu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge, tutasimamia vizuri na tutahakikisha wananchi wa Jimbo la Rungwe wanapata umeme katika vijiji hivi saba, ahsante.
MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Spika, naishukuru Serikali kwa kumaliza kuweka umeme katika vijiji vyote 70 vya Mkalama. Naomba commitment ya Serikali kuhusu vitongoji 15 ambavyo nimeviombea umeme, ni lini umeme utawashwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, vitongoji hivi 15 katika Jimbo la Mkalama na katika majimbo yote, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge na ninalitaarifu Bunge lako Tukufu kuwa, tupo katika hatua za manunuzi. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa, hivi karibuni tutakamilisha na tutaenda kwenye utekelezaji wa kupeleka umeme kwenye vitongoji 15 katika kila jimbo, ahsante.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, je, ni lini Serikali itasambaza umeme kwa bei ya vijiji katika Kata ya Katindiuka, kama ilivyokuwa imeahidi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, katika maeneo yote ambayo tunatekeleza miradi ya kupeleka umeme vijijini bei ya kuunganisha umeme ni 27,000. Katika maeneo ya vijiji-miji ambako bei ni zaidi ya hiyo, tunaendelea kufanya mkakati wa kuona namna ambavyo tunaweza tukaenda kwa ajili ya ku-incorporate hata wananchi ambao hawana uwezo wa kulipa 321,000, lakini katika maeneo yote tunayotekeleza miradi yetu ya vijiji bei ya kuunganisha umeme ni 27,000 na tutaendelea kufanya hivyo, ahsante.
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, je, ni lini Serikali itamaliza kusambaza umeme katika vijiji vilivyobaki katika Mkoa wa Singida?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, katika vijiji ambavyo vimebakia katika Mkoa wa Singida wakandarasi wanaendelea na kazi ya kufikisha umeme kwenye vijiji hivyo. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge tutaendelea kusimamia kwa weledi mkubwa sana ili vijiji vilivyobakia viweze kupata umeme kwa wakati. Ahsante.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, zipo shule za sekondari ambazo bado hazijapata umeme. Pamoja na shule hizo, mwaka jana, 2023 niliomba Shule ya Sekondari Kimenyi ipatiwe umeme, lakini mpaka sasa shule hiyo iliyopo Kata ya Kagera Nkanda haijaweza kupatiwa umeme. Ni lini sasa sekondari hiyo ya Kimenye itapelekewa umeme? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili. Mkoa wa Kigoma una wilaya saba. Kati ya wilaya hizo, ni wilaya nne tu ambazo zimepatiwa umeme wa gridi ya Taifa. Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika wilaya zilizosalia kwa maana ya Kigoma Vijijini, Kigoma Mjini na Uvinza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na kupeleka umeme katika Shule ya Kimenyi iliyopo katika Kijiji cha Kagera Nkanda, tayari mkandarasi ambaye anatekeleza mradi wa kupeleka umeme katika Kijiji cha Kagera Nkanda yupo site. Sasa nimwelekeze Meneja wa Mkoa wa Kigoma ahakikishe anatenga fungu la ziada kwa sababu shule hii ipo mita 900 kutoka kwenye njia ya umeme anayojenga mkandarasi. Kwa hiyo, pale ambapo njia hii itakamilika, basi watenge fungu la nyongeza kwa ajili ya kuunganisha umeme kwenda kwenye shule hii ya sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na kupeleka umeme wa gridi katika hizi wilaya tatu, Serikali inatekeleza mradi wa kupeleka umeme wa gridi katika Mkoa wa Kigoma ambapo mradi huu kwa sasa umefikia asilimia 94. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa mradi unaendelea vizuri sana na tunajenga njia ya umeme ya kilovoti 400 kutoka Nyakanazi hadi Kidahwe. Umeme ukifika Kidahwe utaenda Kigoma Mjini pamoja na Uvinza kwa kadiri ya utekelezaji wa mradi ambao upo kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwahakikishie wananchi wa Kigoma kuwa mradi wa kupeleka gridi ya umeme Kigoma unaendelea vizuri sana na utamalizika kwa wakati. (Makofi)
MHE. MAIMUNA A. PATHAN: Mheshimiwa Mwenyekiti, je, ni lini Serikali itakamilisha zoezi la kupeleka umeme katika shule na taasisi zote zikiwepo za dini katika Mkoa wa Lindi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika miradi ambayo inaendelea, ni maelekezo ya Serikali kwamba shule na taasisi ambazo zipo mita chache katika maeneo ambayo tunapitisha njia za umeme, basi taasisi hizi ziweze kuunganishwa. Zile ambazo zipo umbali wa zaidi ya mita 900 kwenda nyuma, ni maelekezo kwamba Ofisi zetu za Mikoa na Ofisi za TANESCO za kimkoa zihakikishe zinatenga bajeti ya ziada na nyongeza kuhakikisha zinapeleka umeme katika taasisi hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni maelekezo ya Serikali kuhakikisha taasisi zote za msingi zinapata umeme kwa ajili ya ustawi wa watu wetu na shughuli za maendeleo za wanajamii.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Mwenyekiti, je, ni lini umeme unaopita eneo la Uhasibu utakamilika ili Jimbo la Temeke tuweze kupata umeme usiokatikakatika tena?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la Kurasini ni kweli limekuwa lina changamoto ya umeme, lakini tuna ujenzi wa laini ya chini ya umeme kwa ajili ya kuboresha umeme katika Wilaya ya Ilala. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba mradi unaendelea vizuri sana na upo katika hatua za mwisho za umaliziaji. Pindi utakapokamilika, wananchi wa jimbo lako watapata umeme wa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuhakikishia tunasimamia mradi huu kwa weledi mkubwa sana kuhakikisha unakamilika kwa wakati.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, je, ni lini Serikali itapeleka umeme kwenye vijiji vilivyobakia kwenye Wilaya ya Kilosa pamoja na Morogoro Vijijini? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI:Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya ya Kilosa na Morogoro Vijijini wakandarasi wapo site. Tunaendelea kuwahimiza wakandarasi kutekeleza miradi hii kwa weledi kuhakikisha wananchi wanapata umeme kwa wakati na kuhakikisha wanakamilisha majukumu yao kulingana na mikataba yao, ahsante.
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Jimbo la Muleba Kusini ina vijiji vitatu ambavyo havijapata umeme; Kijiji cha Kiholele, Burungura na Bihanga. Ni lini Serikali itapeleka umeme katika vijiji hivyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hivi vijiji vitatu kwenye Jimbo la Mheshimiwa Dkt. Kikoyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mkandarasi yupo site. Tutaendelea kumsimamia ili aongeze kasi kuhakikisha vijiji hivi vinawaka umeme.
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri yaliyotolewa na Serikali nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa hii gesi asilia (CNG) sasa inatumika kwenye gari nyingi, je, hamuoni kuwa sasa ni wakati mwafaka wa kufungua vituo njiani ili mtu anapokuwa anasafiri kutoka Dar es Salaam kuja hapa kuwe na vituo maalumu kabisa vya gesi asilia ambako mtu anaweza kujaza kwenye gari lake?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kwa swali zuri la Mheshimiwa Askofu Josephat Gwajima. Ni kweli kwamba Serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi tumeanza mkakati wa kutafuta namna ya kuwa na vituo kwa gari binafsi kuanzia Dar es Salaam mpaka Dodoma kwa awamu ya kwanza. Tayari tumekwishaanza kuwa na mkakati huo na tayari wadau wa sekta binafsi wameshaanza kujitokeza kwa ajili ya kuwekeza kwenye ujenzi wa vituo barabarani kutoka Dar es Salaam kwenda Dodoma. Hata kwa upande wa magari ya Serikali tayari TPDC imeanza kuongea na Bohari za GPSA ili kuongeza vituo vya CNG kwenye hivi vituo vya bohari kutoka Dar es Salaam hadi Dodoma ili pia hata magari ya Serikali nayo yakiwa yamekwishabadilishwa yaweze kujazwa gesi kutokea Dar es Salaam – Dodoma ambapo ndiyo njia kuu ya magari haya kwa kiasi kikubwa yanapopita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa kwa pande zote mbili za magari binafsi pamoja na magari ya Serikali tumekwishaanza kulifanyia kazi suala hili ili kuongeza idadi ya magari ambayo yanatumia CNG, ahsante.
MHE. MUNIRA MUSTAPHA KHATIB: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa kuwa Serikali ina mpango kuwa ifikapo mwaka 2030/2034 wananchi wote wawe wanatumia nishati safi na salama.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha wanasambaza mabomba kwenye nyumba ili ifikapo mwaka 2030/2034 wananchi wote wawe wanatumia nishati safi na salama? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, na nimshukuru Mheshimiwa Munira kwa swali zuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari Serikali tulikwishaanza awamu ya kwanza ya majaribio kwa ajili ya kuweka miundombinu kwenye maeneo ya Mikocheni pamoja na Mbezi. Aidha, kwa sasa tayari tumeanza mchakato wa kuendelea kuwekeza katika miundombinu hii kwa maeneo mengi zaidi hususan kwa Mkoa wa Dar es Salaam kwanza ili wananchi wengi waweze kutumia gesi nyumbani, kwa sababu ni ukweli kwamba gesi ya nyumbani kwa miundombinu ina bei nafuu kuliko ile ya mitungi. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa tayari mikakati ipo ya kuendelea kuongeza miundombinu nyumbani ili wananchi wengi waweze kutumia gesi nyumbani na tufikie azma ya Mheshimiwa Rais ya kuhakikisha 80% ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034. (Makofi)
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali kwa juhudi zake za kuleta teknolojia ya gesi katika gari, lakini sasa hivi teknolojia imepanda sana kiasi kwamba kuna magari ya kutumia umeme.

Je, Serikali ina juhudi gani katika kuangalia vilevile uwezekano wa kuhamasisha kuleta magari ya umeme nchini ili kuendelea kupunguza matumizi ya mafuta na gesi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na nishukuru kwa swali zuri la Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali inaangalia njia mbalimbali kwa ajili ya kuhamasisha matumizi mbadala, kwa sababu tunaamini ajenda zote hizi zinalenga kwenye kuongeza jitihada za kupambania suala la mazingira. Kwa hiyo, kama ambavyo tunawekeza kwenye nishati ya gesi kwenye magari ndivyo ambavyo tumeshaanza mikakati ya kuweka pia mazingira wezeshi kwa ajili ya kuleta magari yanayotumia umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge jambo hili pia Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu kuanzia mwaka jana alishalianza na sisi tunaendelea nalo ili kuhakikisha kwamba tunaweka mazingira wezeshi kwa ajili ya matumizi ya magari ya umeme, ahsante.
MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, hapa katika majibu yake ya msingi Mheshimiwa Naibu Waziri anasema Serikali inahamasisha kwa kupunguza kodi magari ambayo yanatumia gesi, lakini magari yaliyopo nchini ni mengi sana na yanahitaji kutumia gesi. Gharama za ku-install mitambo ya gesi kwenye magari ni kubwa sana, ni takribani shilingi milioni 2.5. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba gharama hizi zinashuka?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nishukuru kwa swali zuri la Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama hizi ziko juu kidogo ndiyo maana Serikali tumeendelea kuhamasisha watu wengi zaidi na kampuni nyingi zaidi ziweze kuwekeza katika kuwa na karakana. Tunakubali mwanzo huwa ni mgumu sana, lakini tunakoelekea ni kuzuri kuliko tulikotoka. Mwaka 2021 wakati tunaanza kuhamasisha matumizi ya gesi kwenye magari, kwa wastani tulikuwa tuna-convert takribani magari 1,159, leo tunavyoongea tuna magari 5,100 katika mwaka huu wa 2022/2023. Hii ni kwa sababu karakana zimeongezeka kutoka ile moja ya DIT hadi nane. Kwa hiyo, wawekezaji wengi wanavyokuja ndivyo ambavyo gharama inavyoendelea kushuka kutokana na ushindani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa tunaendelea kuhamasisha sekta binafsi kuwekeza zaidi na kuja na teknolojia bora zaidi. Tukiwa na karakana nyingi zenye teknolojia ambayo ni bora gharama zitapungua. Kwa hiyo, tunaendelea kulifanyia kazi ili kuhakikisha kuwa gharama hizi zinapungua, ahsante.
MHE. REHEMA J. MIGILLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na kwanza tuipongeze Serikali kwa kuanzisha hii teknolojia ya kutumia gesi kwenye magari yetu, lakini magari mengi yanayotumia hii gesi ni magari ya petroli tu.

Je, Serikali ina mpango upi wa kuhakikisha kwamba magari yanayotumia dizeli nayo yaanze kutumia gesi kwani tunaona Kampuni ya Dangote magari yake yanatumia dizeli, lakini wamefanya installation ya mitungi ya gesi, mpango ni upi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu tumeanza programu hizi na kwa sasa hivi tulikuwa tuna vituo vitano tu, lakini ili kuelekea kuwa na vituo vingi zaidi tumeanza mazungumzo na hao wawekezaji wa kwenye sekta binafsi ili kuhakikisha wanaona namna ya kuwa na mifumo yote miwili, yaani petroli pamoja na dizeli. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa tunaendelea kulifanyia kazi ili kupata namna ya kuyafanya magari yanayotumia dizeli nayo kuweza kubadilishwa mfumo.