Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Abdul Yussuf Maalim (2 total)

MHE. ABDUL YUSSUF MAALIM aliuliza:-

Je, tathmini ipoje juu ya utatuzi wa changamoto zitokanazo na Mashirikiano yaliyopo kati ya ZFF na TFF?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa sasa mashirikiano kati ya ZFF na TFF hayana changamoto zozote kwani kazi zinaendelea kwa pamoja kwa manufaa ya pande zote za Muungano kwa maendeleo ya mpira wetu. Mathalani mashirikisho haya yanashirikiana katika kuendesha soka la vijana, mashindano yote ya kitaifa ya vijana under 15 na under 17. Aidha, katika mashindano ya CAF na FIFA wawakilishi wetu Taifa Stars, Twiga Stars, na Serengeti Boys hushirikisha wachezaji kutoka katika pande zote mbili za Muungano kulingana na vigezo vya Mwalimu katika uteuzi wa wachezaji husika.

TFF na ZFF pia wamekuwa wakishirikiana vema katika kuendesha mafunzo ya waamuzi pamoja na walimu wa soka kwa kozi zote za CAF na FIFA zinazoendeshwa ndani na nje ya nchi kwa kuzingatia mahitaji yaliyopo.

Mheshimiwa Spika, fauka ya hayo, mashirikisho haya yameendelea katika uandaaji wa mashindano ya kimataifa mathalani mashindano ya African Schools Football Championship ambayo yalifanyika mwezi Mei mwaka 2024 katika uwanja wa Amaan Complex, Visiwani Zanzibar na timu ya wavulana ya Taifa kuchukua ubingwa.

Mheshimiwa Spika, TFF kwa kushirikiana na ZFF zimekuwa zikipeleka mashindano mbalimbali Visiwani Zanzibar. Pia fainali za kombe la Shirikisho (FA Cup) kati ya Yanga dhidi ya Azam FC na nusu fainali ya Kombe la Ngao ya Jamii mwaka 2024, mchezo kati ya Coastal Union dhidi ya Azam FC yote ilifanyika katika uwanja wa Amaan. Hali kadhalika, misafara mingi ya Timu ya Taifa ya Tanzania - Taifa Stars imekuwa ikiongozwa na Rais wa ZFF kama Mkuu wa msafara, kuonesha ushirikiano mkubwa uliopo kwa sasa baina ya TFF na ZFF.
MHE. ABDUL YUSSUF MAALIM aliuliza: -

Je, tathmini ipoje juu ya maendeleo ya kaya maskini zilizodhaminiwa na TASAF kwa upande wa Zanzibar?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, tathmini kubwa ya Kipindi cha Kwanza cha Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini ilikamilika Mwaka 2019 na kipindi cha pili itakamilika mnamo Juni, 2025. Kwa upande wa Zanzibar, Tathmini kubwa ya kipindi cha kwanza cha Mpango ilionesha mafanikio makubwa katika maeneo mbalimbali kama vile, walengwa wanapata mahitaji ya msingi ya maisha kama vile chakula, vifaa vya skuli kwa watoto na makazi ya kuishi kuboreshwa; kuongezeka kwa mahudhurio ya watoto shuleni kufikia 95% na pia, viwango vya ufaulu; wazazi kupeleka watoto kliniki kwa zaidi ya 95%, kwa ajili ya ushauri wa kitaalam; na kuongezeka kwa mzunguko wa fedha katika shehia hivyo, kuchochea ukuaji wa shughuli za uchumi katika maeneo hayo.