Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Abdul Yussuf Maalim (6 total)

MHE. ABDUL YUSUF MAALIM: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwa kiasi gani TARI (Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania Bara) na ZARI (Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Zanzibar) zinashirikiana katika kutatua changamoto za kilimo kwa pamoja kupitia TEHAMA? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ni tafiti za aina gani mpaka sasa zimefanyika katika teknolojia ya habari na mawasiliano ili kutoa matokeo chanya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA K.n.y. WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nijibu maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia kuhusiana na matumizi ya TEHAMA na hasa ushirikiano wa taasisi zetu za utafiti kwenye kilimo kwa maana ya TARI kwa upande wa Tanzania Bara na ZARI kwa upande wa Zanzibar. Taasisi zetu, ikiwemo hizi zimekuwa zikishirikiana sana katika maeneo mbalimbali katika utafiti, kupeana na kujengana uwezo kati ya wataalamu kutoka ZARI na TARI.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali hayo kwa pamoja, hivi karibuni mwaka 2022 taasisi hizi zilifanya tafiti kwa ushirikiano katika mazao ya mihogo na mpunga ambapo moja kupitia Wakala wa Kimataifa wa Atomiki waone namna gani tunaweza kupunguza athari ya maradhi ya mihogo kwa maana ya michirizi kahawia ambayo inaathiri sana zao la muhogo ambalo linalimwa Tanzania Bara lakini pia na kule Visiwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia katika mpunga (mchele) ambapo wameweza kufanya utafiti ili kuona namna gani ya kuongeza uzalishaji wa mpunga (mchele) ambao unalimwa kati ya Tanzania Bara na kule Visiwani ili kupunguza baadhi ya athari au kuboresha mavuno yanayotoka katika maeneo haya ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo moja, tunashirikiana sana kama Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa taasisi zote kama nilivyosema TARI na ZARI. Pili, tafiti zote ambazo zinatumia TEHEMA zimefanyika kwa kushirikiana na tutaendelea kuboresha ushirikiano huu kadiri muda unavyoendelea, nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. ABDUL YUSSUF MAALIM: Mheshimiwa Spika, ahsante, je, ni lini Serikali itatatua changamoto za magari, pikipiki na vifaa vingine kwenye Kituo cha Polisi cha Ng’ambo – Unguja? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, tayari tumeshagawa pikipiki 105 mpaka sasa na tunazigawa kwa awamu. Kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge pia kituo chako ulichokisema tutaweka kwenye mpango ili tuweze kupata polisi kwa ajili ya kutoa huduma katika eneo lako ulilotaja.
MHE. ABDUL YUSSUF MAALIM: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi. Naomba kuuliza masuala madogo mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa muktadha wa mabadiliko ya Katiba ya TFF hususan kipengele Na.2. Je, ni vipi ZFF itanufaika na mabadiliko ya Katiba hiyo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kiasi gani itasaidia kuinua viwango vya ubora wa waamuzi kutoka Zanzibar kuelekea kimataifa ukizingatia Zanzibar tuna upungufu wa waamuzi wa kimataifa?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na mabadiliko ambayo Mheshimiwa Mbunge anayasema kwenye Katiba ya TFF, Zanzibar bado itakuwa inaendelea kunufaika na programu zote za maendeleo ya mpira wa miguu zinazofanywa na TFF, zikiwemo programu zinazoendeshwa kupitia CAF na FIFA kama ambavyo imekuwa ikitokea huko nyuma. Hakuna chochote ambacho kinakwenda kubadilika kwenye programu za maendeleo ya michezo na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Zanzibar itaendelea kunufaika.

Mheshimiwa Spika, hali kama hiyo pia inakwenda mpaka kwenye suala la waamuzi, kwa vile course zote za waamuzi ikiwemo mitihani ya kupata beji ya FIFA ambazo zinaendeshwa na TFF zinahusisha pia upande wa waamuzi kutoka Zanzibar. Kwa hiyo, fursa ya kufanya mitihani kwa ajili ya kupata beji ya FIFA bado itaendelea kuwepo kama ambavyo imekuwa ikitokea kama nyakati zote.
MHE. ABDUL YUSSUF MAALIM: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza; je, Serikali inatumia njia gani kuelimisha wananchi juu ya athari ya mifuko hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Abdul kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, baada ya sheria hii kuwepo, kwa sababu sheria imeelekeza tuwe tunatoa elimu kwa wananchi kupitia njia mbalimbali. Kwa hiyo, zipo njia mbalimbali za vyombo vya habari tunazotumia ikiwemo televisheni, redio, magazeti na namna nyingine. Pia, tumekuwa tunawakusanya wadau hasa wamiliki wa viwanda tunakutana nao kwa pamoja na kuwapa elimu namna ambavyo wanaweza wakapunguza, au ikiwezekana wakaondoa kabisa changamoto ya kuzalisha mifuko ya plastiki kwa sababu imekuwa inaleta athari kubwa kwa jamii. (Makofi)
MHE. ABDUL YUSSUF MAALIM: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Je, Serikali ina mikakati gani wa kuweza kuimarisha sheria ya udhibiti wa uchafuzi wa mazingira unaosababishwa na meli baharini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, hivi karibuni tumeanza, ama tumekuwa na mchakato wa kufanya marekebisho madogo ya Sheria ya Mazingira Sura 191. Miongoni mwa mambo ambayo tunataka tuhakikishe kwamba tunayafanyia kazi ni jambo la uchafuzi wa vyanzo vya maji ikiwemo jambo la uchafuzi wa masuala ya mazingira kwenye maeneo ya bahari.

Mheshimiwa Spika, nimwambie tu Mheshimiwa, itakapokamilika sheria hii, hayo mambo ambayo ameyashauri na amependekeza yawemo, basi tutahakikisha kwamba yanakuwemo ili kuendelea kunusuru mazingira, hasa mazingira ya Bahari, nashukuru.
MHE. ABDUL YUSSUF MAALIM: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Naomba kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza. Kwa kuwa fedha hizi za Mfuko wa TASAF huwa zinachelewa, je, Serikali ina mkakati gani wa kuharakisha fedha hizi ili ziweze kunufaisha wananchi kwa wakati?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza wanufaika wa Mfuko huu wa Maendeleo wa TASAF ili kuweza kuwanufaisha wananchi wakiwemo wa Jimbo la Amani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwanza nimpe pole Mheshimiwa Abdul kwa matatizo aliyoyapata, lakini namshukuru Mwenyezi Mungu, amerudi akiwa salama na anaendelea kupambana kuwatetea wananchi wake wa Jimbo la Amani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali yake mawili ya nyongeza, kwanza ameuliza habari ya fedha za Miradi ya TASAF kuchelewa. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa, siyo kwamba fedha hizi zinachelewa, isipokuwa utekelezaji wa miradi hiyo unahusisha wadau mbalimbali. Kwa mfano, tunapopeleka fedha zile zinakwenda kuhudumia sekta ya elimu, maji na afya. Sasa pale kuna wadau kama Wizara ya Elimu, Wizara ya Afya na Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na michakato mingi, lakini sisi pamoja na hawa wadau tumekaa, tumeweza ku-stream line na baada ya hapo tumeboresha zaidi kupunguza urasimu ili fedha hizo zifanye kazi kwa wakati na kuwanufaisha wananchi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge nikuondoe shaka, tutahakikisha jambo hilo linafanyika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kuongeza wanufaika ni kweli baada ya programu hii kukamilika mwitikio umekuwa mkubwa na kila mahali watu wanataka kunufaika na mpango huu wa TASAF. Nakuhakikishia kwamba, baada ya awamu hii ya pili kukamilika, mwezi Septemba mwaka huu tunakuja na awamu ya tatu, na awamu hii Serikali imejipanga vizuri kuhakikisha wanufaika wanakuwa wengi zaidi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)