Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 15 Sitting 14 Natural hazards and Disasters Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2024-04-25

Name

Twaha Ally Mpembenwe

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kibiti

Primary Question

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu. Ni kweli kwamba Taifa limekutwa na janga la mafuriko na mikoa mbalimbali imeathirika na mafuriko haya ambayo yanaendelea.

Mheshimiwa Spika, pale kwenye Jimbo la Kibiti tuna kaya takriban 6,150 zimeathirika, idadi ya watu takriban 31,900, lakini sambamba na hilo ekari zilizokuwa zimesambaratishwa na mafuriko haya ni takriban ekari 71,366. Tukizingatia kwamba wananchi hawa wanategemea sana kilimo; je, nini mkakati wa Serikali mara baada ya hali hii ya mvua kuwa imepungua, kuweza kuwasaidia wananchi hawa wa Jimbo la Kibiti pamoja na Rufiji kuweza kupata mbegu ili kuendelea na masuala ya kilimo? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Twaha Mpembenwe, Mbunge wa Kibiti, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nampa pole, miongoni mwa wilaya ambazo zimepata athari kubwa ni Wilaya ya Kibiti, eneo la delta. Kwa bahati nzuri eneo lile nalifahamu, nimeishi pale, nimefanya kazi pale na athari hii tumeitembelea na tunazo taarifa ofisini kwetu. Kwa hiyo, pole sana Mheshimiwa Mpembenwe na wananchi wote ambao wamepata athari kwenye eneo lile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati Serikali kuanzia ngazi ya wilaya, mkoa na Taifa zikiendelea kuratibu utoaji misaada kwenye maeneo yote ikiwemo Kibiti bado pia tumeweka mpango imara wa kuhakikisha kwamba baada ya utulivu wa hali ya hewa sekta zetu zote ambazo zinaguswa na maafa yale; miundombinu, Wizara ya Kilimo, mashamba na maeneo ya mifugo, sekta ya afya kama kulitokea mlipuko wa magongwa baada ya uwepo wa maji mengi yaliyopita katika maeneo mbalimbali. Wizara hizi zina mpango kazi kupitia Kamati ya Kitaifa ya Maafa.

Mheshimiwa Spika, moja kati ya jukumu ambalo sasa lipo kwa Wizara ya Kilimo kwa wakulima wale ni kwamba tumeshaandaa mbegu. Tulitoa taarifa kwa Mheshimiwa Rais kiwango cha tani ambazo tumeamua tuzipeleke kwenye eneo lile. Rufiji tumeona mazingira hayo wakulima walikuwa wanalima mazao gani, tumeandaa mbegu za kutosha kwa ajili ya kuwawezesha kuanza kulima tena. Kwa kuwa eneo lile ni chepechepe, tunaamini bado wanaweza wakalima mazao ya muda mfupi na yakaiva. Tumeamua kupeleka mpunga ili waweze kurudisha mashamba ya mpunga kwenye maeneo hayo chepechepe, mazao kama mahindi na mazao mengine ambayo ni ya muda mfupi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, utaratibu wote umeandaliwa na timu yetu iko pale Kibiti, Rufiji na maeneo mengine ambayo yamepata athari, wanaendelea kuratibu na kufuatilia mwenendo huo. Mwisho, kila hatua inayofikiwa wale watakuwa wanatupa taarifa. Kwa hiyo, tutaendelea kuwasiliana na Mheshimiwa Mbunge na yeye atakuwa anatupa mrejesho wa huduma zinazoendelea kutolewa pale ili tushirikiane na wananchi wale waweze kurudi kwenye hali yao ya kawaida. Huo ndiyo Mpango kazi wa Serikali. Ahsante. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister