Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 15 Sitting 42 Public Service Management Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2024-06-06

Name

Mariamu Nassoro Kisangi

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, katika nchi yetu kumekuwa na sheria, sera, kanuni, taratibu na miongozo mbalimbali kwa watumishi wa Serikali na taasisi zake kuzingatia muda wa kuingia kazini na muda wa kutoka kazini, lakini kumekuwa na changamoto kwenye baadhi ya watumishi wa kada moja kutofautiana muda wa kutoka kazini, kwa mfano, walimu wa shule za msingi mijini wanatoka kazini saa 8.30 mchana lakini wale wa vijijini wanatoka mpaka saa 10.30 alasiri.

Je, Serikali haioni haja ya kupitia upya utaratibu huu ili kuweka sawa?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetuwezesha leo kuwa na uhai, uzima na hatimaye leo asubuhi hii tunaanza programu zetu kwa kipindi hiki.

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mariam Kisangi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nchi yetu inayo sheria ya kazi ambayo inaainisha pia muda wa kuingia kazini na muda wa kutoka kazini na kwa mujibu wa sheria zetu muda wa kazi Kiserikali ni saa zisizopungua nane, kuanzia saa 1.30 asubuhi mpaka saa 9.30 alasiri.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge amezungumzia utofauti wa muda wa kutoka kwa walimu wa shule za msingi wa mijini na vijijini, kwa bahati nzuri na mimi pia ni mwalimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kinachopelekea utofauti wa muda wa kutoka ni mazingira ya maeneo hayo ya miji na vijijini. Maeneo ya mijini mara nyingi ofisi za elimu na kwa kupata kibali kutoka TAMISEMI wanafunzi wakiingia asubuhi na walimu wakiingia asubuhi mchana hawapati muda wa kwenda kupumzika na kwa hiyo, wanaunganisha mpaka saa 8.30 mchana, lakini vijijini muda wa mchana wanapata nafasi ya kurudi nyumbani kwenda kula.
Kwa hiyo, ule muda wa kula ndio unaokuja kulipiwa pale mbele na kufanya muda wa kutoka uonekane kuwa ni mrefu zaidi, lakini saa za kazi ni zile zile. Kwa hiyo, huu ni mpango kazi uliowekwa kulingana na mazingira yaliyopo ya mijini na vijijini.

Mheshimiwa Spika, kwa nini huku mijini wanaamua kuunganisha moja kwa moja? Kwanza kuna shida ya usafiri, huwezi kuruhusu mwanafunzi mchana arudi nyumbani, aende shule utaona mazingira kama Jiji la Dar es Salaam mazingira yale mwanafunzi kutoka nyumbani kwenda shuleni peke yake shida, ukimruhusu mchana saa moja arudi nyumbani, halafu arudi tena saa saba bado ni shida vilevile, kwa hiyo wanaamua kuunganisha moja kwa moja na ndio sababu wanaonekana wanaingia saa 1.30 asubuhi na kutoka saa 8.30 mchana.

Mheshimiwa Spika, lakini vijijini kwa sababu hakuna tatizo la usafiri na shule za msingi ziko vijijini, kwa hiyo, ni kiasi cha kutembea kwenda nyumbani anapumzika, anakula, anarudi shule na ule muda alioutumia kwa kula unasogezwa mbele na kwa hiyo, muda wa kuondoka shuleni unaongezeka na kwa hiyo, hata walimu nao wanatoka muda huo huo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ni mpango kazi ambao pia umeridhiwa na TAMISEMI, kwa hiyo tuchukue hiyo tuipeleke TAMISEMI waone kama kuna umuhimu wa hata vijijini kuunganisha muda bila kuruhusu wanafunzi wetu kupata chakula, hiyo pia inaweza kuamriwa na Wizara kulingana na mahitaji na mazingira yalivyo, nakushukuru sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister