Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 15 Sitting 42 Education, Science,Technology and Vocational Training, Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2024-06-06

Name

Kenneth Ernest Nollo

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Bahi

Primary Question

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi hii ya kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali ya Awamu ya Sita imefanya kazi kubwa ya kujenga madarasa kwenye shule zote za msingi na sekondari na wakati mwingine imejenga shule iliyokamilika, kutokana na kufanya kazi hii tumeongeza wanafunzi wengi na kutokana na kuongezeka kwa wanafunzi tumeongeza upungufu wa walimu.

Mheshimiwa Spika, ziko halmashauri na majiji ambayo yanakusanya fedha nyingi, lakini nao wanasubiri mgao wa ajira hususan kama ya walimu waweze kupata sawa na halmashauri zingine ambazo hazina mapato.

Je, Serikali haioni kama ni busara na ni vyema kwamba halmashauri na majiji ambayo yana uwezo wa kuajiri walimu waweze kuajiri ili inavyokuja ule mgao wa kitaifa hawa wengine ambao hawana tuwe tumewapunguzia mzigo huo na kufanya hivyo ni kwamba maeneo yale tayari tutakuwa tumeondoa tatizo la walimu? Ahsante sana.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nollo, Mbunge wa Bahi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu imesimamia mifumo ya ajira na ajira zote za kudumu ziko chini ya Serikali Kuu ikiwemo na sekta ya elimu kwa walimu. Nikiri kwamba tunao upungufu wa walimu kwenye shule zetu za msingi hata sekondari na upungufu huu unatokana na vipindi vya ajira, lakini hapa katikati kabla ya ajira kunakuwa na vifo kunakuwa na kustaafu lakini pia hata mpango usiokuwa mzuri wa kwenye halmashauri zenyewe kwa sababu walimu wengi wanaonekana wanajaa sana mijini kuliko vijijini, nitalisema baadae.

Mheshimiwa Spika, kwa nini ajira zote zimepelekwa Serikali Kuu? Lengo ni kuwa na mfumo mmoja wa kuajiri na kupata kanzidata yaani takwimu ya idadi ya waliopo kazini wanaoajiriwa, lakini pia kuweza kusambaza kwa usawa kwenye halmashauri zote ili kusiwe na halmashauri moja kuwa na mlundikano mkubwa kwa sababu tu wana uwezo wa wao kuajiri. Kwa hiyo, Serikali Kuu inasimamia kusambaza walimu nchini kote kulingana na mahitaji, kulingana na fani walizosomea, kwa mfano, masomo ya sayansi na masomo ya sanaa hiyo. Kwa hiyo, mahitaji yanakwenda nchini kote.

Mheshimiwa Spika, tunajua ziko halmashauri zenye uwezo, lakini kuna halmashauri ambazo hazina uwezo. Tukiruhusu halmashauri zenye uwezo ziajiri kuna hatari ya halmashauri ambazo zinapata pato chini ya uwezo wake hakutakuwa na walimu hakutakuwa na wafanyakazi na kwa hiyo, hakutakuwa na usawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali hatuwezi kuruhusu hili na ndio sababu ajira zote tumeweka za Serikali Kuu yenyewe inaajiri walimu 4,000 tunawagawa nchi nzima kulingana na idadi, uwiano wa masomo kwa maana ya fani, lakini na mahitaji ya hizo halmashauri. Tutaendelea kufanya hivi inatusaidia pia Serikali katika kulipa stahiki zao pamoja na mafao yao ya mwisho wa kustaafu, lakini pia inatusaidia kuwa na takwimu.

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo, sasa nitoe agizo kwa Maafisa Elimu na Wakurugenzi wa Halmashauri kufanya mapitio ya ikama zao. Hapa ndipo tatizo lilipo kwamba halmashauri inaruhusu eneo fulani kuwa na walimu wengi halafu kule vijijini hakuna walimu na kusababisha kuwa na upungufu mkubwa wa walimu, kumbe kama wangekuwa wamewasambaza vizuri ingekuwa na walimu wanaotosha kwenye fani zao. Kwa hiyo, wapitie ikama yao ili wajaribu kuona mlundikano wa walimu kwenye maeneo ya miji na barabarani ili wawapeleke pia na vijijini kuwe na utoshelevu halafu ile kanzidata isaidie pia katika kufanya kila shule kuwa na idadi nzuri ya walimu, hizi ndio sababu ambazo zinapelekea Serikali Kuu kuajiri centrally, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister