Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 15 Sitting 42 Works and Transport Maswali kwa Waziri Mkuu 6 2024-06-06

Name

Aysharose Ndogholi Mattembe

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kumuuliza swali Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mkuu, kutokuzingatia kwa sheria za barabarani na uzembe wa madereva wa bodaboda inatajwa kuwa ni sababu inayosababisha vifo vingi kwa Watanzania wengi hususan vijana ambao ndiyo nguvu kazi ya Taifa.

Je, Serikali ina jitihada gani za makusudi kuhakikisha kwamba vijana wote waliojisajili katika vijiwe wanapata mafunzo sahihi ya usalama barabarani?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aysharose Mattembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nikiri kwamba tunao wajasiriamali ambao wanaendesha bodaboda ambao wanasaidia sana katika kuchangia pato la Taifa pale ambapo wanafanya biashara zao, lakini pia wanasaidia sana Watanzania kupata usafiri wa haraka wa maeneo mafupi mafupi. Wafanyabiashara hawa wameratibiwa kwenye maeneo mbalimbali, lakini pia wengine wako kwenye vijiwe.

Mheshimiwa Spika, nini Serikali inafanya ili kuondoa au kupunguza sehemu kubwa ya ajali na kuwafanya wafanye shughuli zao kwa usalama?

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Jeshi la Polisi na Usalama Barabarani wanaendelea kutoa elimu kwenye makundi haya ya bodaboda kwenye makundi ambayo yameratibiwa na yamesajiliwa na kwa miongozo ambayo imetolewa LATRA sasa wamepewa mamlaka ya kusajili vikundi vyote vya vijana wa bodaboda ili kuwezesha kuwafikia na kuwapa elimu ya usalama barabarani, lakini pia kuwasaidia katika kufanya biashara zao kwa usalama zaidi.

Mheshimiwa Spika, pia uko mpango unaoratibiwa na kila halmashauri kupitia Idara ya Maendeleo ya Jamii kwa kuwaanzishia SACCOS na ushirika wao mdogo kwa ajili ya kuendesha biashara zao kwa usalama zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali itaendelea kuratibu kundi hili la madereva bodaboda kwa lengo la kupeleka elimu zaidi, lakini pia kuwaanzishia ushirika mdogo mdogo ambao utaweza kuwasaidia kuchangia fedha na kuwaonesha maeneo ya kupta mitaji na kupanua wigo wa shughuli zao za kibiashara na za usafirishaji.

Mheshimiwa Spika, pia nitoe wito kwa madereva wetu wa bodaboda popote walipo, ni vema sasa wakaamua kukaa maeneo ambayo yako rasmi na yameainishwa na halmashauri ili iwe rahisi sasa kwa taasisi yetu ya LATRA kuwafikia na na kuendesha elimu pamoja na kuwapa fursa mbalimbali za kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kuwahakikishia Watanzania kwamba, eneo hili ambalo limeonekana kuwa na ajali nyingi linaendelea kuratibiwa vizuri kama ambavyo nimesema na Wizara ya Mambo ya Ndani, Kitengo cha Usalama Barabarani kwa lengo la kuwafanya waweze kufanya shughuli zao kwa usalama mkubwa zaidi, ahsante. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister