Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 12 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Wizara ya Kilimo 147 2022-02-16

Name

Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Primary Question

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha wakulima wa mazao ya viungo kama Iliki, mdalasini, pilipili manga na karafuu wa Kata ya Kigongoi, Mhindano na Bosho Wilayani Mkinga ili waweze kuongeza uzalishaji wa thamani ya mazao hayo?

Name

Hussein Mohamed Bashe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Mjini

Answer

WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dunstan Luka Kitandula, Mbunge wa Mkinga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mazao ya viungo yanayojumuisha Karafuu, Pilipilimanga, Pilipili Kali, Mdalasini, Hiliki, Tangawizi na jamii hiyo ya mazao ya viungo, hulimwa zaidi katika Mikoa ya Tanga, Morogoro, Mbeya, Kilimanjaro, Kigoma na Ruvuma. Aidha, katika Mkoa wa Tanga Wilaya ya Mkinga na katika Kijiji cha Kigongoi na vijiji vidogo jirani yake ndiyo wanazalisha mazao ya viungo zaidi ikiwemo Hiliki, Mdalasini na Pilipilimanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa kuendeleza mazao ya bustani yakiwemo mazao ya viungo, inatekeleza Mkakati wa Kuendeleza Mazao ya Bustani wa Mwaka 2021 - 2031 wenye lengo la kuongeza uzalishaji kwa kutumia teknolojia bora na kuimarisha usimamizi na uratibu. Aidha, mikakati mingine ni pamoja na kutoa mafunzo ya wataalam na wakulima kuhusu kanuni za uzalishaji wa mazao ya viungo, kuunganisha wakulima na wanunuzi wakubwa, na kuanzisha vitalu vya kisasa vya miche ya viungo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kushirikiana na chama cha wasindikaji wa viungo (TASPA) na wasindikaji wa mazao ya viungo wameanza kuwashirikisha wakulima wa viungo Wilaya ya Mkinga kwa kuanzisha vitalu vya kisasa vya viungo. Mfano, Kampuni ya Trianon Investment Ltd yenye Kiwanda cha Viungo Lusanga – Muheza tayari imeanza kununua mazao kwa wakulima wa viungo Mkinga na imedhamiria kugawa miche bora kutoka katika bustani bora ya kuzalisha miche iliopo kiwandani.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Tume ya Maendeleo ya Ushirika imeanza kuhamasisha wakulima kuanzisha na kujiunga na Vyama vya Msingi vya Ushirika ili kukuza uwezo wao wa kifedha kupitia mikopo na kuwa na nguvu ya pamoja katika soko; na pia Serikali kuweza kuwapatia mafunzo ya uzalishaji bora na uongezaji thamani wa mazao yao. (Makofi)