Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Primary Question

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA aliuliza:- Je, lini majiko yanayotumia gesi yataanza kutumika katika Shule za Sekondari kote Nchini?

Supplementary Question 1

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru kwa majibu mazuri na ninaipongeza Serikali kwa kuliona hili. Kutokana na juhudi za kumuunga mkono Mheshimiwa Rais kuhusiana na nishati safi ya kupikia, Serikali haioni haja ya kupanua wigo kupitia REA kutoa majiko haya na kujenga hii miundombinu ya gesi kwenye hospitali, vituo vya afya na magereza kama ilivyofanya katika sekondari na shule za msingi kwa sababu changamoto kubwa kwenye shule za msingi kwa utoaji wa chakula shuleni ni hii miundombinu ya kupikia (mkaa au kuni bei iko juu sana). Je, Serikali haioni sasa kuna haja ya kuongea na REA, kwamba badala ya kutoa hii mitungi ya gesi kwa wajasiriamali ielekeze kwenye hizi taasisi za Serikali?

Name

Judith Salvio Kapinga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali tayari inatekeleza mkakati huo. Kama mtakumbuka Mheshimiwa Rais aliagiza taasisi ambazo zinalisha watu zaidi ya 100 ziwezekufungwa mifumo ya nishati safi ya kupikia. Pia tayari Wizara ya Nishati kupitia REA tumeanza kufanya hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna mradi wa kufunga mifumo ya nishati safi ya kupikia kwenye Jeshi la Polisi na Magereza, takribani mikoa 24; Jeshi la Zimamoto pamoja na huduma za Wakimbizi. Hapa tunapoongea tuna mkakati na mradi tayari unaendelea wa kufunga nishati safi ya kupikia katika taasisi zilizopo chini ya Wizara ya Afya; Hospitali za Mikoa, Rufaa na Kitaifa takribani 21.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika taasisi za Maendeleo ya Jamii vilevile tunafunga mifumo kwenye Vyuo vya Maendeleo ya Jamii takribani 13. Kwa hiyo, Serikali inatekeleza mkakati huo kuhakikisha kwamba, zile taasisi ambazo zinahudumia kuanzia watu 200 – 100 na zenye watu wengi basi zinafungiwa hiyo mifumo. Tayari tumeshaona matokeo katika baadhi ya magereza, kwa mfano, wameshapunguza gharama ya uendeshaji takribani nusu. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge mkakati unaendelea na tutaendelea kufanya hivyo hivyo kwa taasisi nyingi zaidi, ahsante.

Name

Tunza Issa Malapo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA aliuliza:- Je, lini majiko yanayotumia gesi yataanza kutumika katika Shule za Sekondari kote Nchini?

Supplementary Question 2

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka kujua mkakati wa Serikali, kuna mkakati gani wa kuhakikisha taasisi zote mpya ikiwemo shule, zahanati na vituo vipya vya afya ambavyo vinajengwa wanafunga kabisa mfumo wa gesi badala ya kwenda kuhama baadaye kwa sababu ni gharama? Ninakushukuru. (Makofi)

Name

Judith Salvio Kapinga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia mkakati wetu wa nishati safi ya kupikia ambao sasa tumeshaanza utekelezaji wake, kwa kweli huo ndio mtazamo ambao hata sisi wenyewe tunautazamia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Serikali tumejipanga kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, wenzetu wa Mazingira na taasisi zote ambazo kwa pamoja tunashirikiana katika kutekeleza mkakati huu kuhakikisha yale maeneo ambayo tayari yalishatolewa mwongozo yanayotoa huduma za kijamii na yanayotumia nishati nyingi sana katika kupikia yanafungwa mifumo hii ya nishati safi ya kupikia. Kwa hiyo, tunao mkakati na unatekelezeka vilevile. Ahsante.