Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Hassan Selemani Kaunje (1 total)

MHE. HASSAN S. KAUNJE:
Mheshimiwa Spika, nishukuru kupata nafasi ya kuuliza swali la moja kwa moja kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwanza tunafahamu kwamba maji ni uhai na Sera ya Taifa ya Maji inahitaji kila mwananchi kuweza kuyafikia maji ndani ya umbali wa mita 25. Je, Serikali ya Awamu ya Tano imejipangaje kuhakikisha maji haya yanawafikia wananchi especially
wananchi wa Mkoa wa Lindi ambao wanatatizo kubwa sana la maji?
WAZIRI MKUU:
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kaunje, Mbunge wa Lindi Mjini kama ifuatavyo:-
Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Kaunje, amekuwa anafuatilia sana mwenendo wa maji na hasa alipoweka kule mwishoni hasa wananchi wa Mkoa wa Lindi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Sera ya Maji nchini imetamka wazi kwamba Serikali itasambaza maji kwa wananchi wake kote nchini mpaka ngazi za vijiji tena kwa umbali usiozidi mita 400 hiyo ndiyo sera na wakati wowote Wizara ya Maji inapofanya kazi yake inafanya kazi kuhakikisha kwamba sera hiyo inakamilika. Iko mipango mbalimbali na nadhani Wizara ya Maji itakuja na bajeti hapa ikiomba ridhaa yenu muipitishe Waheshimiwa Wabunge ili tukaendelee kutekeleza hiyo sera ya kusambaza maji, na mikakati yetu sisi, maji
lazima yawe yamefika kwenye ngazi za vijiji kwa asilimia mia moja ifikapo mwaka 2025 na ikiwezekana kufikia mwaka 2020 hapa kwa zaidi ya asilimia tisini huo ndiyo mkakati wetu. Mkakati huu utatokana tu kama tutaendelea kupata fedha nyingi Serikalini na kuzipeleka Wizara ya Maji ili Wizara ya Maji waendelee na mkakati ambao wanao.
Kwa hiyo, niseme tu kwamba kwa malengo haya tunakusudia kusambaza maji kwenye maeneo yote ya vijiji na maeneo ya miji ili wananchi wetu waweze kupata tija ya maji kwenye maeneo haya. Kwa miradi ambayo ipo, ambayo imeelezwa kwamba ipo inaendelea kutekelezwa, tunaamini miradi hiyo kwa watu wote ambao tumewapa kazi hiyo wataendelea kutekeleza kadri ambavyo tunawalipa fedha zao ili waweze kukamilisha.
Waliokamilisha wakamilishe miradi ambao hawajakamilisha tunaendelea kuwapelekea fedha ili waweze kukamilisha ili maji yaweze kutolewa na kila mwananchi aweze kunufaika na sera hiyo ya Serikali.