Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru (1 total)

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Waziri Mkuu ni Sera ya Serikali kulinda usalama wa watu na mali zao. Mheshimiwa Waziri Mkuu, mwezi wa Saba Jeshi la Polisi lilifanya shambulio Msikitini katika Jimbo langu na ikasababisha kifo cha Sheikh Ismail Bweta na kuondolewa jicho kwa Sheikh Abdallah Nakindabu, lakini Serikali iko kimya. Je, Serikali iko tayari kulipa fidia kwa watu hawa? Ahsante.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vedasto, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza sina uhakika kama Jeshi la Polisi lilimshambulia huyo unayemtaja kwa jina na kumtoa jicho, kama ambavyo umedai, lakini jukumu la vyombo vya dola, Jeshi la Polisi likiwemo, ni kulinda usalama wa raia wake na mali zao. Sio jukumu la Polisi kwenda kumshambulia mtu na hatimaye sasa tuanze kufikiria kulipa fidia kwa sababu ya shambulio lililofanywa na Polisi.

Mheshimiwa Spika, kama kuna askari au yeyote kutoka chombo cha dola ambaye ametenda tendo hilo yeye mwenyewe, ikiwa ni nje ya majukumu yake ya kila siku, hilo atakuwa ametenda kosa binafsi na atachukuliwa hatua za kisheria kama yeye aliyetenda kosa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali haiwajibiki kulipa fidia ikiwa si sehemu ya maagizo na wala si jukumu la majeshi ya vyombo vyetu vya dola, bali ikithibitika kama mmoja kati ya watumishi wetu wa vyombo vya dola ambaye ametenda kosa hilo na ikathibitika yeye mwenyewe atawajibika kuchukuliwa hatua kali ili sasa kama kutakuwa na fidia itakuwa ni moja kati ya hukumu ambazo atapewa na vyombo vinavyotoa hukumu kutokana na tendo ambalo limeshatendwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niseme tu kwamba, Serikali wala vyombo vyake vya dola havilengi kufanya kazi ya kuweza kwenda kuwatendea makosa wananchi, bali kulinda kama ambavyo nimesema, kulinda amani na mali zao ili tuweze kufanya kazi kama ambavyo tumejipanga kufanya kazi zetu vizuri. Ahsante sana.