Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Kiteto Zawadi Koshuma (13 total)

MHE. KITETO Z. KOSHUMA aliuliza:-
Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni akiwa Mkoani Mwanza aliahidi kuifanya Mwanza kuwa Geneva; lakini Mwanza Mjini kuna barabara zenye urefu wa kilometa 546.1 ambapo kilometa 43.67 zina lami na kilometa 3.556 zimejengwa na mawe:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza barabara zenye kiwango cha lami?
(b) Je, Serikali itashirikiana vipi na Halmashauri za Ilemela na Nyamagana ili kuboresha barabara zilizopo chini ya halmashauri hizo kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kiteto Zawadi Koshuma, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaboresha barabara za Jiji la Mwanza kwa hatua kulingana na upatikanaji wa fedha. Katika mwaka wa fedha 2015/2016 jumla ya shilingi milioni 500 zilitengwa kwa ajili ya ujenzi wa kilometa 1 ya barabara ya Nyakato - Buswelu -Mhonze kwa kiwango cha lami na taratibu za kumpata mkandarasi atakayejenga barabara hizo ziko katika hatua za mwisho. Aidha, katika mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 1.16 kwa ajili ya kujenga kilometa 1.4 kwa kiwango cha lami katika barabara hiyo hiyo ya Nyakato - Buswelu - Mhonze yenye urefu wa kilometa 18.2.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imepanga pia kujenga barabara ya Sabasaba –Kiseke- Buswelu yenye jumla ya kilometa 9.7 kwa kiwango cha lami kama ilivyoahidiwa na Mheshimiwa Rais. Aidha, Serikali inaendelea na upanuzi wa barabara ya Airport - Pansiasi na kujenga daraja la Furahisha, huu ukiwa ni mpango wa kuboresha barabara za Jiji la Mwanza na kupunguza msongamano wa magari uliopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu ndiyo yenye dhamana ya barabara zote nchini. Hivyo kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI na Halmashauri za Ilemela na Nyamagana itaendelea kuhakikisha kuwa fedha zinatengwa mwaka hadi mwaka ili kuhakikisha barabara za Jiji la Mwanza zinajengwa kwa kiwango cha lami kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA aliuliza:-
Shule nyingi katika Wilaya ya Ilemela hususani shule za msingi zina upungufu mkubwa wa madawati:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa hakuna mwanafunzi anayekaa chini wakati wa masomo?
(b) Je, Serikali haioni umuhimu wa kuweka karakana kwa kila shule ya msingi katika Wilaya ya Ilemela na kutumia vijana wazawa kutengeneza madawati ili kuepuka tatizo hili sugu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiteto Zawadi Koshuma, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, upungufu wa madawati kwa shule za msingi katika Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela ni madawati 13,080. Ili kukabiliana na upungufu huo Serikali katika bajeti ya mwaka wa fedha wa 2015/2016, imetenga jumla ya shilingi 228.5 kwa ajili ya upatikanaji wa madawati. Kati ya fedha hizo shilingi milioni 25.69 zinatokana na Mfuko wa Kuchochea Maendeleo katika Jimbo la CDCF.
Naomba kuchukua fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Ilemela kwa uamuzi wake wa kuelekeza fedha hizo katika upatikanaji wa madawati. Aidha, natumia fursa hii kuwakumbusha Wakuu wa Mikoa wote kuhakikisha agizo la Serikali la kumaliza tatizo la madawati ifikapo tarehe 30 Juni, 2016 liwe limekamilika kikamilifu.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, mazingira ya shule yanahitaji utulivu na usalama wa watoto katika kujisomea bila kuwa na bughudha, hivyo hatushauri karakana hizo kuanzishwa katika maeneo ya shule za msingi badala yake Halmashauri zinashauriwa kuimarisha karakana za Halmashauri chini ya Mhandisi wa Halmashauri ili kujenga uwezo wa kutengeneza madawati kwa gharama nafuu. Mfano mzuri ni Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali ambao wametumia karakana ya Halmashauri kutengeneza madawati yote yanayohitajika. Natumia fursa hii kuwahamasisha vijana kujiunga katika vikundi vya ujasiriamali katika fani ya useremala ili waweze kukopesheka na kushiriki katika shughuli za utengenezaji wa madawati na shughuli nyingine katika Halmashauri.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA aliuliza:-
Huduma za afya bila malipo kwa wamama wajawazito, wazee na watoto chini ya miaka mitano ni Sera ya Afya ya Taifa lakini utekelezaji wake umegubikwa na rushwa na urasimu mkubwa.
(a) Je, Serikali imejipangaje kuhakikisha utekelezaji wa sera hiyo ili kupunguza vifo kwa makundi hayo mijini na vijijini?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha upatikanaji wa huduma za upasuaji wa kupanga na ule wa dharura kwa akina mama wajawazito hasa wa vijijini ili kupunguza vifo vya mama na mtoto?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kiteto Zawadi Koshuma, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutumia Sera ya Afya ya mwaka 2007 iliyoainisha makundi maalum ya watu, (wanawake wajawazito, watoto chini ya miaka mitano, wazee wanaozidi miaka 60, watu wenye ulemavu na wasiojiweza) kwa kuzingatia sheria zilizopo ili kutekeleza mikakati ya kuleta unafuu kwa huduma za afya kwa watu wote wanaotakiwa kupewa huduma za afya bila malipo. Aidha, Wizara inaendelea na maandalizi ya utaratibu ambao utawafanya wananchi wote wawe wanachama wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya. Hatua hii ikifikiwa, changamoto nyingi zinazowapata watu walio katika makundi maalum wanaotakiwa kupewa huduma za afya bila malipo zitakuwa historia. Vilevile Wizara kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, TAMISEMI, inaendelea na kuimarisha uongozi katika vituo vya kutolea huduma za afya ili kuhakikisha kuwa watoaji wa huduma kwa makundi haya wanazingatia sera, sheria, mikakati, miongozo na maelekezo mbalimbali yanayolenga kuboresha huduma za afya kwa wananchi kwa ujumla wake.
(b) Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha kuwa wananchi, hasa wanaoishi vijijini, wanapata huduma za upasuaji za kupanga na zile za dharura, Wizara inaendelea kutekeleza mkakati wa kuvijengea uwezo vituo vya afya, hasa vilivyopo vijijini ili viweze kutoa huduma za upasuaji hasa wa dharura. Vituo hivyo vimeonesha kuwa na uwezo huo na vinaokoa maisha ya wananchi, hasa wanawake wanaohitaji upasuaji wa dharura. Katika kuvijengea uwezo vituo hivyo, Wizara ikishirikiana na wadau mbalimbali inaboresha miundombinu, watumishi, upatikanaji wa dawa, vifaa, vifaa tiba na vitendanishi.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA aliuliza:-
SIDO pamoja na majukumu mengine inatoa huduma kwa viwanda vidogo na vya kati kwa kutoa mikopo, mafunzo na vitendea kazi.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuiwezesha SIDO kutimiza majukumu yake?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kiteto Zawadi Koshuma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa SIDO katika ujenzi wa uchumi wa Taifa letu imekuwa na mipango na mikakati mbalimbali ya kuliwezesha Shirika hili kutimiza majukumu yake. Kupitia Bajeti Kuu ya Serikali, SIDO inatengewa fungu kwa ajili ya kujenga miundombinu ya ofisi ya maghala ya viwanda (industrial sheds). Kwa mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali imetenga jumla ya shilingi bilioni 7.04 kwa ajili ya kujenga miundombinu tajwa hapo juu katika Mikoa ya Katavi, Manyara, Kagera, Geita na Simiyu. Nafurahi kutamka kuwa tayari shilingi bilioni tano kati ya bilioni saba zilizopangwa kufanikisha jukumu hilo hapo juu zimeshatolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali hutoa fedha za mitaji kwa SIDO kupitia Mfuko wa Kuendeleza Wajasiriamali (NEDF). Mfuko huu uliainzishwa mwaka 1994 kwa mtaji wa shilingi milioni 800 na mpaka sasa Serikali imechangia shilingi bilioni 5.5 ambazo zimezungushwa na wajasiriamali na kufikia shilingi bilioni 62.8 kwa mwaka wa fedha 2017/2018; na kwa mwaka huu sasa tumetenga shilingi bilioni 7.14 kwa ajili ya mfuko huu; na mahususi tutaelekeza juhudi zetu katika uanzishaji wa viwanda vidogo sana na viwanda vidogo chini ya mkakati wa Wilaya Moja, Bidhaa Moja (ODOP).
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali pia ina mkakati wa kuwatafutia SIDO wabia wa nje ili waweze kuwasaidia kufikisha huduma kwa wananchi hasa wafanyabiashara na wenye viwanda vidogo. SIDO inashirikina na Shirika la viwanda la India (National Small Industry Corporation of India) katika masuala ya kukuza teknolojia. Ushirikiano huo unahusisha uanzishwaji wa kiatamizi cha teknolojia za aina mbalimbali katika Mitaa ya Viwanda eneo la Vingunguti Dar es Salaam.
Mheshimiwa Naibu Spika, SIDO imewezesha kuingia ubia na Shirika la maendeleo la Sweden na wamepatiwa shilingi bilioni 1.8 kuanzisha Kongano. Vilevile SIDO imewezeshwa kuingia Ubia na Shirika la Maendeleo ya Uchumi la Canada (Economic Development Associates) ambao unawezesha kutoa mafunzo ya kuimarisha na kuendesha biashara katika ukanda wa Mtwara na Lindi na ukanda wa Morogoro mpaka Arusha.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA aliuliza:-
Vifo vya mama katika Mkoa wa Mwanza pamoja na mambo mengine huchangiwa na kukosa huduma za upasuaji, damu salama na upungufu wa watumishi.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kupunguza vifo vya mama na mtoto?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiteto Zawadi Koshuma, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, vifo vinavyotokana na uzazi bado ni changamoto nchini. Tafiti zilizofanyika mwaka 2015/ 2016 zinaonesha kwamba kuna idadi ya vifo 556 kwa kila vizazi hai 100,000. Kulingana na sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012 Mkoa wa Mwanza ulikuwa na vifo 305 kwa kila vizazi hai 100,000. Katika kukabiliana na tatizo hili Wizara yangu imeandaa mpango mkakati wa kuboresha huduma ya afya kwa wanawake wajawazito wa mwaka 2016 mpaka 2020 na mpango maalum wa kutekeleza afua muhimu zenye matokeo makubwa ambao umezinduliwa mwezi Novemba, 2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, mambo muhimu yaliyomo katika mpango mkakati huu ni pamoja na kuimarisha huduma kwa wanawake wajawazito ikiwemo huduma ya dharura wakati wa ujauzito wakati wa kujifungua hadi wiki sita baada ya kujifungua. Sanjari na hiyo tumeimarisha mifumo ya afya ikiwemo kuwa ajili watumishi wenye ujuzi vifaa tiba pamoja na dawa ili kuhakikisha kwamba huduma inayotolewa ina ubora unaokidhi viwango.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imepata ufadhili wa World Bank na Canada kwa ajili ya kujenga na kuboresha miundombinu katika vituo vya afya ili kuwezesha kutoa huduma za dharura za uzazi ikiwemo upasuaji wa kumtoa mama mtoto tumboni. Katika Mkoa wa Mwanza vituo vya Kome (Buchosa), Karume (Ilemela), Kahangara (Magu), Malya (Kwimba), Kagunga (Sengerema) na Bwisya (Ukerewe) vimepata jumla ya bilioni 2.6 kwa ajili ya ukarabati wa au kujenga vyumba vya upasuaji, wodi ya wazazi, chumba cha kijifungulia, maabara ya damu na nyumba za watumishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kibali cha ajira cha watumishi wa afya takribani 3152 kilichotolewa mwezi Disemba, 2017 Mkoa wa Mwanza umepokea jumla ya watumishi 78. Aidha Wizara imeupatia Mkoa wa Mwanza magari ya wagojwa manane kwa ajili ya huduma za rufaa za wajawazito kwenye vituo vya afya, vilevile tunaendelea kuhamasisha akina mama wajawazito kujifunguliwa katika vituo vya kutolea huduma za afya.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA aliuliza:-
Uzalishaji wa pamba Mkoani Mwanza umepungua kutoka tani 350,000 kwa mwaka 2009 hadi tani 120,000 kwa mwaka 2016:-
Je, Serikali inachukua hatua gani za makusudi ili kulifufua zao hilo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kiteto Zawadi Koshuma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, uzalishaji wa pamba umekuwa ukishuka katika miaka ya hivi karibuni, sio kwa Mkoa wa Mwanza tu, bali pia katika maeneo yote yanayozalisha pamba nchini. Miongoni mwa sababu ambazo zilichangia kushuka kwa uzalishaji ni bei ndogo ya pamba kwa wakulima, kukosekana kwa mfumo bora wa usimamizi wa ununuzi wa pamba ambao ulisababisha baadhi ya wakulima kukopwa, matumizi madogo ya pembejeo hususan viuadudu, mbegu bora na mbolea. Aidha, kutozingatiwa kwa kanuni bora za kilimo cha pamba na matumizi madogo ya zana bora za kilimo vimeathiri uzalishaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekusudia kuinua kilimo cha zao la pamba kwa kuimarisha usimamizi kuanzia ngazi ya kijiji hadi ngazi ya kitaifa. Katika usimamizi huo, mkazo umewekwa katika upatikanaji wa taarifa na takwimu sahihi za wakulima, eneo wanalolima, kiasi cha pembejeo hususan viuadudu, mbegu bora na mbolea. Aidha, Serikali inasimamia kikamilifu vyama vya msingi ili viwe imara na pale ambapo havipo vianzishwe ili huduma za pembejeo na masoko zipatikane kupitia vyama hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na uhamasishaji na usimamizi imara, msimu wa 2017/2018, uzalishaji wa pamba unategemewa kuwa zaidi ya tani 600,000. Hii ni kutokana na wakulima kuhamasika na Serikali kupeleka pembejeo hususan viuadudu ambapo chupa milioni 7.3 zenye thamani ya shilingi bilioni 29.2 zimenunuliwa na kupelekwa kwa wakulima ikilinganishwa na chupa 700,000 katika msimu uliopita. Aidha, vinyunyizi 16,500 vyenye thamani ya shilingi milioni 495 vimenunuliwa. Pia vinyunyizi vibovu 6,000 vilivyokuwa kwa wakulima vimekarabatiwa bila malipo pamoja na wakulima kufundishwa namna ya kupulizia viuadudu hivyo ili kudhibiti visumbufu vya zao hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati wa muda wa kati na mrefu kuongeza uzalishaji wa pamba kutoka tani 121,639 mwaka 2016/2017 hadi kufikia tani milioni moja ifikapo mwaka 2020. Lengo hilo litafikiwa kwa kuongeza matumizi ya mbegu bora ambapo katika msimu wa 2018/2019, bodi itazalisha tani 40,000 za mbegu aina ya UKM08 ambayo ni zaidi ya mahitaji ya tani 25,000 kwa mwaka. Mbegu mpya aina ya UKM08 ina sifa za kipekee ikiwemo tija kubwa ya uzalishaji ikilinganishwa na mbegu ya zamani aina ya UK91.
Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati mwingine ni kuongeza uzalishaji wa mbegu mpya aina mbili zilizothibitishwa kwa ajili ya kuzipeleka kwa wakulima na kutenga maeneo maalum ya kuzalisha mbegu bora. Aidha, maeneo yaliyoainishwa na Serikali kupitia Bodi ya Pamba katika kutekeleza mpango wa uzalishaji wa mbegu bora aina ya UKM08 ni Wilaya za Igunga, Uyui, Urambo, Nzega na Meatu.
MHE. STANSLAUS S. MABULA (K.n.y. MHE. KITETO Z. KOSHUMA) aliuliza:-
Hospitali ya Rufaa ya Bugando inatoa huduma kwa Mkoa wa Mwanza na Mikoa jirani ikiwemo Simiyu na Mara lakini Hospitali hiyo haina CT Scan:-
Je, ni lini Serikali itapeleka CT Scan katika Hospitali hiyo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiteto Zawadi Koshuma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara inatambua umuhimu wa kuimarisha huduma za uchunguzi katika hospitali za Kibingwa ngazi ya Kanda na Taifa ikiwemo hospitali ya Bugando. Hii ni pamoja na kuhakikisha hospitali hizi zinakuwa na vifaa vya kisasa vya uchunguzi vikiwemo kuwa na CT Scan na MRI. Wizara ipo katika hatua za utekelezaji wa mradi wa usambazaji wa vifaa vya uchunguzi kupitia mradi wa ORIO ambapo Hospitali ya Bugando ilipangiwa kupata MRI na CT Scan.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, wakati Wizara ikiendelea ukamilishaji wa mradi huu, Hospitali ya Bugando nayo ilinunua CT Scan kupitia mipango yake ya hospitali na tayari ilishasimikwa, kuzinduliwa na kuanza kazi tangu tarehe 26 Januari, 2018. Wizara inaipongeza Hospitali ya Bugando kwa juhudi hiyo. Serikali kwa sasa itaendelea na mpango wa kuitafutia Hospitali ya Bugando mashine ya MRI.
MHE.KITETO Z. KOSHUMA aliuliza:-
Katika vikao vya Ushauri vya Mkoa wa Mwanza (RCC), moja ya kipaumbele kwa mwaka wa fedha 2017/2018 ni ujenzi wa jengo la ghorofa tatu katika Hospitali ya Mkoa linalohitaji shilingi bilioni nne na laki mbili (4.2 bilioni):-
Je, Serikali imetenga kiasi gani cha fedha kinachohitajika katika mwaka huu wa fedha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) (K.n.y. WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Kiteto Zawadi Koshuma, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuupongeza uongozi wa Mkoa wa Mwanza kwa jitihada zake za kuimarisha upatikanaji wa huduma bora za afya kwa kuanzisha ujenzi wa jengo la ghorofa tatu katika hospitali ya rufaa ya Mkoa Sekou Toure ikiwa ni jengo mahususi kwa ajili ya kutoa huduma ya Mama na Mtoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali ilitenga jumla ya shilingi bilioni mbili na hadi sasa kiasi cha shilingi bilioni moja kimeshatolewa na kulipwa kwa Wakala wa Majengo Tanzania kwa maana ya TBA ambaye ndiye msimamizi Mkuu wa jengo hili. Vilevile katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni mbili kwa ajili ya uendelezaji wa ujenzi huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatia tamko la Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kuagiza hospitali za Mkoa kuwa chini ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na watoto, Wizara imetenga kiasi cha shilingi bilioni 30 kwa ajili ya kuimarisha utoaji wa huduma za afya katika hospitali za rufaa za mikoa ikiwa ni pamoja na hospitali ya Mkoa wa Sekou Toure.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali italeta sheria ya kuwataka wananchi wote kujiunga Mifuko ya Taifa ya Bima ya Afya?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiteto Zawadi Koshuma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto inaendelea na maandalizi ya utaratibu wa kuhakikisha Watanzania wote wanakuwa katika mfumo wa bima na hivyo kuwa na uhakika wa kupata huduma wakati wote wanapohitaji bila ya kuwa na kikwazo cha kifedha. Katika kulitekeleza jambo hili Wizara imeandaa mapendekezo ya kuanzisha bima ya afya moja, kwa maana ya Single National Health Insurance na kuwasilisha katika ngazi mbalimbali za maamuzi Serikalini. Pindi Serikali itakaporidhia mapendekezo haya suala hili litawasilishwa Bungeni.

Mheshimiwa Spika, endapo Bunge lako litaridhia muswada huo kutakuwa na ulazima wananchi wote kujiunga na bima ya afya. Matarajio ni kuanza kutekeleza mwaka huu 2019. Kwa sasa Wizara inaendelea kutekeleza mikakati ya kuhamasisha wananchi kujiunga na bima ya afya na CHF iliyoboreshwa. Nitoe rai kwa Waheshimiwa Wabunge kuendelea kuwahimiza wananchi kujiunga na bima ya afya na CHF zilizoboreshwa wakati tunasubiri muswada huo kupitishwa.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA aliuliza:-

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuelekeza taasisi zote nchini kuwa sifa mojawapo ya kuajiriwa iwe ni umri wa miaka 21- 35 ili kuwezesha Vijana wengi wanaotoka vyuoni kupata ajira?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. ANTONY P. MAVUNDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kiteto Zawadi Koshuma, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mijibu wa Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini Na. 6 ya Mwaka 2004, Kifungu cha 5 kimekataza mtoto chini ya umri wa miaka 18 kuajiriwa isipokuwa katika mazingira maalum yaliyotajwa katika kifungu hiki. Kwa msingi huo, umri wa kuajiriwa ni miaka 18 na kuendelea pamoja na masharti yaliyotajwa katika kifungu cha 5 cha Sheria Na. 6 ya mwaka 2004. Hivyo nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kuendelea kuwahimiza waajiri wote kutii Sheria za kazi na kuhakikiahsa vijana wote wenye sifa wanapomaliza mafunzo yao na kutimiza umri wa kuajiriwa wanaajiriwa kwa kuzingatia fursa zilizopo kwa waajiri na masharti ya kazi husika.
MHE. STANSLAUS S. MABULA (K.n.y. MHE. KITETO Z. KOSHUMA) aliuliza:-

Bodi ya Utalii pamoja na mambo mengine ina jukumu la kutunza utalii wa ndani ya nchi:-

Je, Serikali inasimamiaje Bodi hiyo ili kuhakikisha Mkoa wa Mwanza unatangazwa kama Mji wa Kitalii?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimisha Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiteto Zawadi Koshuma, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha kuwa vivutio vya utalii vilivyopo Mkoani Mwanza vinatangazwa ipasavyo, Wizara inayo ofisi ya kanda ya Idara ya Utalii Jijini Mwanza na mwaka 2011 ilielekeza Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) kufungua Ofisi ya Kanda jijini Mwanza. Aidha, Wizara imeelekeza Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania - TANAPA kufungua Ofisi ya kanda ya kaskazini magharibi Mkoani Mwanza. Lengo likiwa si tu kusogeza karibu huduma kwa wadau wa sekta ya utalii lakini pia kuhakikisha vivutio vya utalii na fursa za uwekezaji katika sekta ya utalii Mkoani Mwanza na maeneo yote ya kanda ya Ziwa zinatangazwa kikamilifu.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo Wizara yangu kwa kushirikiana na Sekta binafsi imekuwa ikishiriki na kuratibu matukio na matamasha yanayolenga kutangaza vivutio vya Mkoani Mwanza ikiwemo; Maadhimisho ya Siku ya Utalii Duniani, Tamasha la Bulabo na Afro Calabash, Tamasha la Urithi (Urithi Festival), Rocky City Marathon na Mashindano ya Urembo. Lengo ni kuvutia wageni na watalii wa ndani na nje kutembelea mikoa hiyo.

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inatambua kuwa Mkoa wa Mwanza ni miongoni mwa maeneo machache yenye rasilimali nyingi za utalii ikiwemo fukwe nzuri za Ziwa Viktoria, visiwa vinavyovutia, Hifadhi ya Taifa ya Saanane, wanyamapori, utamaduni, miamba ya mawe yenye kuvutia na mandhari nzuri ya jiji. Vivutio hivi kwa miaka ya karibuni vimekuwa vivutio wageni wengi kutembelea mkoa huo.

Mheshimiwa Spika, Kwa sasa Wizara inaendesha zoezi la kubainisha vivutio vya utalii kwa dhumuni la kuviendeleza na kuvitangaza. Katika mwaka wa Fedha 2019/2020 Wizara imelenga kutekeleza zoezi hilo katika Mikoa sita ikiwemo Mkoa wa Mwanza. Kazi hii inatekelezwa kwa kushirikiana na Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), uongozi wa mkoa, Wilaya, Vijiji na wadau wa sekta ya utalii.

Mheshimiwa Spika, aidha, tarehe 16 na 17 Machi, 2019 Wizara ilifanya kikao na wadau wa utalii kanda ya ziwa na magharibi ikiwa ni jitihada za kuimarisha utalii Mkoani Mwanza na Kanda ya ziwa kwa ujumla. Katika kikao hicho kilichofanyika Mkoani Mwanza kilihusisha viongozi kutoka Mikoa ya Mwanza, Geita, Simiyu, Mara, Kagera, Shinyanga na Kigoma. Vilevile Wizara inaendelea na jitihada zingine za kuhamasisha uwekezaji kwenye shughuli za utalii na vijana kujifunza uongozaji watalii katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, Sekta ya utalii ni mtambuka, hivyo kazi ya utangazaji na uendelezaji sekta hii inahitaji juhudi za pamoja za wadau wa sekta ya umma na binafsi. Nitoe wito kwa Mheshimiwa Mbunge na Uongozi wa Mkoa wa Mwanza kuendelea kufanya kazi kwa karibu na Wizara yangu katika jitihada za kuendeleza na kutangaza vivutio vya utalii vya Mkoa wa Mwanza.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA aliuliza:-

Serikali imeziagiza halmashauri zote nchini kutenga asilimia tano ya vijana na asilimia tano ya wanawake kutoka mapato ya ndani ili kuchangia mfuko wa maendeleo wa wanawake na vijana:-

Je, Serikali inachukua hatua gani kwa halmashauri ambazo hazizingatii takwa hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMIESEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiteto Zawadi Koshuma, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, hapo awali utekelezaji na usimamizi wa mfuko wa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu, ulikuwa na changamoto kutokana na kutokuwepo kwa sheria na kanuni. Baadhi ya Halmashauri zimekuwa zikitenga asilimia 10 kutoka katika mapato yake ya ndani bila kujali vyanzo lindwa na fedha zenye maelekezo maalumu kama vile CHF na fedha zenye maelekezo maalumu.

Mheshimiwa Spika, mwezi Juni, 2018, Serikali ilifanya marekebisho ya Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa sura Na. 290 kwa kuongeza kifungu cha 37(a) ambacho kimeelekeza namna bora ya kusimamia fedha hizo. Kufuatia marekebisho ya sheria hiyo, Ofisi ya Rais (TAMISEMI) imeandaa kanuni ambazo zimefafanua namna bora ya kutenga fedha hizo, kutoa mikopo na kusimamia utekelezaji wake. Kwa mujibu wa kanuni hizo, asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa ajili ya mikopo ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu itatengwa baada ya kutoa vyanzolindwa.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Ofisi ya Rais (TAMISEMI) itaendelea kuzismamia halmashauri kuhakikisha zinatekeleza sheria hii na kanuni zake za mfuko wa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu na hatua za kinidhamu na kisheria zitachukuliwa kwa halmashauri zitakazoshindwa kutekeleza sheria hiyo na kanuni zake. Ahsante.
MHE. DKT. HADJI H. MPONDA (K.n.y MHE. KITETO Z. KOSHUMA) aliuliza:-

Ili kuelekea Tanzania ya viwanda, Watanzania wanapaswa kuandaliwa vema ili kushiriki kikamilifu katika viwanda vya ndani.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuandaa wataalam mbalimbali watakaotumika katika kuendesha viwanda nchini?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNLOJIA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kiteto Zawadi Koshuma, Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2016 Serikali kupitia Wizara Elimu, Sayansi na Teknojia ikishirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu na wadau wengine ikiwa ni pamoja na sekta binafsi na washirika wa maendeleo ilikamilisha na kuanza utekelezajii wa mkakati wa Taifa wa kukuza maarifa (National Skills Development Strategy – NSDS 2016). Mkakati huu ni wa kipindi cha miaka kumi na unaorodhesha mahitaji mbalimbali ya maarifa ambayo wataalam wake wanahitajika ili kuifikisha nchini yetu katika uchumi wa kati wa viwanda tunaoukusudia.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha Watanzania wanaandaliwa vema kushiriki uchumi wa viwanda, Serikali inaendelea kutekeleza mipango mbalimbali ikiwemo kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia kama vile ujenzi na ukarabati wa maiundombinu ya shule na kusambaza vifaa vya maabara na kemikali katika shule za sekondari.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Serikali inaendelea na mpango wa ukarabati, ujenzi wa miundombinu, ununuzi wa vifaa vya kisasa vya kujifunzia na kufundishia na kuboresha mitaala katika vyuo na taasisi za elimu. Kwa mfano, ukarabati wa vyuo vya maendeleo ya wananchi, ujenzi na ukarabti wa vyuo vya VETA katika Mikoa na Wilaya pamoja na Vyuo Vikuu nchini. Aidha, katika mwaka 2019/ 2020 Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknojia itaanza ujenzi wa chuo kipya cha ufundi cha Dodoma (Dodoma Technical College) pamoja na kujenga vyuo vya ufundi stadi katika Wilaya 25 ili kuongeza udahili wa wanafunzi katika fani mbalimbali za ufundi.