Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Mwanne Ismail Mchemba (9 total)

MHE. MWANNE I. MCHEMBA aliuliza:-
Hali ya kipande cha barabara ya kutoka Chaya - Tabora ni sehemu ya barabara ya kutoka Urambo – Kaliua:-
Je, ni lini ujenzi wa barabra hizo utakamilika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwanne Ismail Mchemba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Chaya – Nyahua na Urambo – Kaliua ni sehemu ya barabara ya Manyoni – Tabora – Urambo – Kaliua – Malagarasi – Uvinza - Kigoma yenye jumla ya kilometa 843.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa Serikali ni kuunganisha Mkoa wa Singida, Tabora na Kigoma kwa barabara ya kiwango cha lami. Katika kutimiza azma hiyo, tayari ujenzi kwa kiwango cha lami wa sehemu za Manyoni – Itigi – Chaya yenye urefu wa kilometa 89.3 pamoja na Tabora – Ndono yenye kilometa 42, Kigoma – Kidahwe yenye kilometa 28, Kidahwe – Uvinza yenye kilometa 76.6 pamoja na daraja la Malagarasi na barabara unganishi zenye urefu wa kilometa 48 umekamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, ujenzi kwa kiwango cha lami unaendelea kwa sehemu ya barabara zifuatazo na utekelezaji umefikia asilimia kama nitakavyoieleza. Sehemu za Tabora - Nyahua yenye urefu wa kilometa 85.4 ujenzi umefikia 90%. Sehemu ya Ndono - Urambo yenye urefu wa kilometa 52 ujenzi umefikia 87%. Sehemu ya Kaliua - Kazilambwa yenye kilometa 56 ujenzi umefikia 63%.
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi kwa kiwango cha lami sehemu ya Nyahau - Chanya yenye urefu wa kilometa 85.5 na Urambo - Kaliua yenye urefu wa kilometa 28 utaanza katika mwaka wa fedha wa 2016/2017 kufuatia kukamilika kwa usanifu wa kina wa barabara hizo.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA aliuliza:-
Wakulima wa tumbaku wamekuwa wakilipwa kwa dola pindi wanapouza mazao yao:-
(a) Je, nani huwapigia hesabu za kitaalamu?
(b) Je, wakulima wote wamefunguliwa akaunti benki?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwanne Ismail Mchemba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo wa kuwalipa wakulima wa tumbaku kwa dola kupitia Vyama vya Msingi ulipendekezwa, ukafanyiwa utafiti na kukubaliwa na wadau wote wa tasnia ya tumbaku. Vyama vya Msingi vya Ushirika vimeajiri Katibu, Meneja na Mhasibu wa kila chama kwa ajili ya usimamizi wa mali na stahiki za kila mkulima mwanachama. Watumishi hawa wana jukumu la kutunza hesabu na madeni pamoja na mauzo ya tumbaku. Ili kuongeza ufanisi katika kazi zao watumishi hao hupewa semina mbalimbali ikiwemo kushawishi bei nzuri ya kubadilisha fedha. Katibu, Meneja na Mhasibu wa Vyama vya Msingi ndiyo wanaohusika katika kubadilisha fedha kutoka dola na kwenda katika shilingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Serikali imekuwa ikipokea malalamiko kutoka kwa wakulima kwamba watumishi hawa kwa kushirikiana na mabenki wamekuwa wakiwapunja wakulima hasa katika mchakato wa kubadili dola kwenda kwenye fedha za Kitanzania. Wizara yangu inaendelea kuchunguza suala hili na ilipobaini ubadhirifu huchukua hatua stahiki ikiwemo kuwaandikia hati ya madai wahusika.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakulima wengi hawana akaunti binafsi za kupokea malipo ya tumbaku yao waliyouza na badala yake Vyama vya Msingi ndivyo vyenye akaunti. Baada ya vyama hivyo kupokea malipo ya tumbaku za wakulima hutoa fedha hizo kama fedha taslimu na kuzisafirisha hadi katika makao ya vyama hivyo kwa ajili ya kuwalipa wakulima waliouza tumbaku yao. Jambo hili ni hatari na linachochea sana wizi na upotevu wa fedha za wakulima. Hivyo, Serikali inavitaka vyama vyote vya ushirika kuhamasisha kila mkulima kufungua akaunti ili kukabiliana na tatizo hilio na ikiwezekana kufungua akaunti ya dola.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA aliuliza:-
Ugonjwa wa sickle cell umejitokeza kwa wingi hapa nchini na watu wengi hawajui sababu zinazosababisha ugonjwa huo, huku wengine wakiamini kuwa unasababishwa na kurogwa au imani za kishirikina.
(a) Je, ugonjwa huo unasababishwa na nini?
(b) Je, dalili zake ni zipi?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ahsantem kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwanne Ismail Mchemba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, naomba kuuhakikishia umma kwamba ugonjwa huu ni wa kibaiolojia na hauna mahusiano yoyote na imani za kishirikina. Ugonjwa wa sickle cell ambao kwa lugha ya kiswahili huitwa ugonjwa wa selimundu ni ugonjwa wa kurithi wa kupungukiwa na damu, ambapo mgonjwa huwa hana damu ya kutosha kwa sababu ya seli zake za mwili sio imara kiasi cha kubeba hewa ya oxygen kwenda sehemu mbalimbali za mwili wa binadamu.
Mheshimiwa Spika, ili mtoto aweze kupata ugonjwa huu ni lazima wazazi wawe na vimelea vya ugonjwa huo. Chanzo halisi cha ugonjwa huu ni kubadilika kwa mfumo wa mwili wa kutengeneza vimelea vya kutengenezea damu yaani haemoglobin. Hii husababisha seli zinazotengenezwa kuwa na shape ya seli kujikunja mithili ya mundu ambayo siyo ya kawaida. Mgonjwa hupata vimelea vya ugonjwa huu kutoka kwa wazazi wote yaani baba na mama kitaalamu tunaita carriers. Mama na baba wanaweza kuwa hawana dalili yoyote lakini wamebeba vimelea vya ugonjwa huo kwenye damu zao na kumzaa mtoto ambaye ana ugonjwa huu.
(b) Mheshimiwa Spika, mgonjwa wa selimundu yaani sickle cell haonyeshi dalili yoyote mpaka afikishe miezi minne ya umri tangu kuzaliwa na huanza na dalili zifuatazo; Kuishiwa damu, kuvimba vidole, kuchelewa kukua kwa watoto, kutoona vizuri na kusumbuliwa na mashambulio ya maumivu mara kwa mara sababu ya kukwama kwa seli hizo na kuzuia oxygen kwenda sehemu ya viungo vya mwili.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA aliuliza:-
Fomu ya PF3 hutolewa na polisi tukio linapotokea na kumletea usumbufu mgonjwa kwani anatakiwa kuwa na uthibitisho wa fomu hiyo ili daktari atoe ushauri wake na pia mgonjwa hawezi kupatiwa huduma yoyote mpaka awe na fomu hiyo hata kama ana maumivu makali au hali yake ni mbaya;
Je, Serikali haioni sasa umuhimu wa kufanya marekebisho ya utaratibu ili kuwaondolea usumbufu wagonjwa?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumjibu mama yangu Mwanne Ismail Mchemba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshmiwa Naibu Spika, Serikali iliweka utaratibu wa mtu anapokuwa ameumia apate Police Form No. 3 kwa mujibu wa Kifungu cha 170 cha Kanuni za Kudumu za Jeshi la Polisi ili aweze kupokelewa na kupewa matibabu katika hospitali zetu. Msingi mkubwa wa hiyo fomu ni kutaka kujua mazingira ya mtu huyo aliumia wapi na alikuwa anafanya nini.
Mheshimiwa Naibu Spika, PF3 inatumika pia kama kielelezo Mahakamani kama mtu ameshambuliwa ama amepigwa ili Mahakama ijue ameumia kiasi gani na kwa kuwa rahisi kutoa adhabu stahiki. Hata hivyo, kuna matukio mengine yaliyo wazi ambayo PF3 hupelekwa hospitali kwa urahisi wa matibabu na kwa msingi huo PF3 bado inakidhi matakwa yaliyokusudiwa kwa mujibu wa kifungu nilichokitaja hapo juu.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA aliuliza:-
Mkoa wa Tabora upo tayari kwa ajili ya uwekezaji wa EPZ uliotengewa eneo katika Wilaya ya Uyui.
Je, ni lini Serikali italeta wawekezaji katika Mkoa wa Tabora?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwanne Ismail Mchemba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchakato wa kutenga eneo la uwekezaji Mkoa wa Tabora kwa ajili ya EPZA ulianza mwaka 2010 baada ya Wizara yangu kuelekeza uongozi wa Mkoa kutenga eneo lisilopungua ukubwa wa hekta 2000. Uongozi wa Mkoa ulipendekeza eneo ulipokuwa Mgodi wa Resolute lenye ukubwa wa hekta 866. Baada ya ukaguzi wa eneo hilo ilibainika kuwa sehemu kubwa ni mashimo yaliyofunikwa hivyo kutofaa kwa ajili ya miradi ya EPZA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa ushauri kwa Mkoa wa Tabora na kwa Mikoa mingine waendelee kubaini na kutenga maeneo ya uwekezaji. Watenge maeneo kwa malengo ya Special Economic Zone - SEZ au Export Processing Zone - EPZ kulingana na ushauri utakaotolewa na wataalamu wangu, lakini pia watenge maeneo kwa ajili ya uwekezaji usiokuwa wa SEZ wala wa EPZA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na maelekezo ya hapo juu, Wizara yangu inakamilisha uandaaji wa mwongozo utakaosaidia Mamlaka za Mikoa na Wilaya kutenga maeneo ya uwekezaji na namna ya kuvutia wawekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kuleta wawekezaji Tabora, nitoe taarifa kuwa hivi sasa Mamlaka ya Biashara Tanzania (Tan Trade) kwa kushirikiana na Mkuu wa Mkoa wa Tabara wanaandaa kongamano la kutangaza vivutio vya Mkoa wa Tabora.
Mheshimiwa Mwenyekiti,niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na wananchi wa Tabora kuwa Wizara na mimi mwenyewe tutaendelea kuitangaza Tabora kwa lengo la kuvutia wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA aliuliza:-
Mkoa wa Tabora umepata usafiri wa uhakika wa ndege ya ATCL na kwa kuwa Tabora ina historia mbalimbali na kumbukumbu za mambo ya kale.
Je, Serikali ipo tayari kuutangaza Mkoa wa Tabora kwa utalii?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwanne Ismail Mchemba, Mbunge wa viti maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Tabora umo katika Kanda ya Kati inayounganisha Mikoa ya Dodoma, Singida na Kigoma. Ni kweli kabisa kuwa Mkoa wa Tabora kama sehemu ya Kanda ya Kati una historia mbalimbali na kumbukumbu za mambo ya kale ikiwa ni pamoja na Tembe lililokaliwa na missionary Dkt. Livingstone, ambaye ni mpinga biashara ya utumwa kutoka Uingereza mwaka 1871 akiwa njaini kuelekea Ujiji - Kigoma. Pia kuna kituo cha njia ya kati ya biashara ya utumwa na vipusa vilivypo Ulyankulu eneo la Mtemi Mirambo na Gofu lililokuwa hospitali ya kwanza ya Kijerumani katika Mkoa wa Tabora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tembe la Dkt. Livinstone limekarabatiwa na kuna Watumishi ambao wanatoa maekelezo kwa wageni wanaotembelea kituo hicho. Katika mwaka wa fedha 2013 hadi 2017 kituo kilitembelewa na wageni 1,642 na jumla ya shilingi 2,292,000 zilikusanywa kutoka kwa watalii wa ndani na nje. Aidha, mipango ya usimamizi wa maeneo mengine niliyoyataja hapo juu imeandaliwa ili yaendelezwe kuwa vituo vya kumbukumbu na taarifa kwa matumizi mbalimbali yakiwemo ya utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufanisi wa utangazaji, utalii wa Mkoa wa Tabora juhudi za utangazaji zinahusu vivutio vingine zaidi ya vivutio vya mambo ya kale vinavyopatikana katika eneo hilo. Juhudi hizo zinahusu utamaduni, wanyamapori, mazao ya nyuki na historia pana ya harakati mbalimbali za kijamii za nchi yetu zilizofanyika Mkoani Tabora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa juhudi za kuendeleza na kuutangaza Mkoa wa Tabora kiutalii zimekuwa zikiendelea hata kabla ya kuwepo kwa usafiri wa ndege ya ATCL. Kwa kuwa sasa Mkoa umepata usafiri wa uhakika wa ndege ya ATCL, Serikali itaongeza juhudi za kuutangaza Mkoa wa Tabora nje na ndani ya nchi ili kuhakikisha wageni wengi wanatembelea Mkoa huo kwa lengo la kukuza utalii na kuongeza pato la Taifa.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA aliuliza:-
Hali ya nyumba za Polisi na Magereza nchini ni mbovu sana. Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga nyumba za askari hao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwanne Ismail Mchemba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli hali ya makazi kwa Askari wetu siyo nzuri, hata hivyo Serikali imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo na kwa kutumia rasilimali zilizopo katika maeneo husika kujenga makazi mapya na kufanya ukarabati wa majengo yaliyopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya mwaka 2017/2018 Serikali imetenga jumla ya shilingi bilioni 12.3 fedha za maendeleo kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa makazi ya askari wetu katika maeneo mbalimbali nchini.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA aliuliza:-

Tabora Manispaa kuna Zoo ya Wanyamapori ambayo ilijengwa muda mrefu na mpaka sasa wanyama wanapungua na kuifanya kukosa maana:-

Je, Serikali iko tayari kupeleka wanyama hao katika zoo hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwanne Ismail Mchemba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, bustani ya wanyamapori ya Tabora ina ukubwa wa ekari 35.67 ambapo ekari 28.15 ni eneo la wanyamapori na ekari 7.52 ni eneo la makazi. Bustani hii ilianzishwa na Idara ya Wanyamapori mwaka 1967 ikiwa na aina mbalimbali za wanyamapori wakiwemo chui, simba, duma, fisi, pundamilia nyumbu, swala na ngiri. Kwa sasa, bustani hiyo ina jumla ya wanyamapori 256 wa aina tofauti 16.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1972 bustani hii ilikabidhiwa kwa Mkoa wa Tabora ili kuisimamia kwa ukaribu. Mwaka 2001, Ofisi ya Mkoa wa Tabora ilikabidhi shughuli za usimamizi wa bustani hii kwa Manispaa ya Tabora. Manispaa ya Tabora iliisimamia hadi mwaka 2012 ilipoirejesha kwa Idara ya Wanyamapori kutokana na kuongezeka kwa gharama za uendeshaji. Katika Idara ya Wanyamapori, bustani hii ilisimamiwa na Mfuko wa Wanyamapori Tanzania (Tanzania Wildlife Protection Fund). Mwaka 2018 bustani hii ilihamishiwa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori-TAWA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuongeza tija katika bustani ya wanyamapori, TAWA inaandaa mkakati wa kusimamia bustani ya wanyamapori zilizopo chini yake ikiwemo hii ya Tabora. Mkataba kati ya TAWA na mtaalam mwelekezi wa kuandaa mkakati huo umeshasainiwa ambapo mtaalamu huyo ataanza kazi hivi karibuni. Mkakati utakapokamilika utaainisha aina na idadi ya wanyama watakaowekwa katika bustani, aina ya huduma zitakazotolewa kwa wageni na kiwango cha tozo.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA Aliuliza:-

Serikali ya Awamu ya Tano imekaribisha wawekezaji wa nje na ndani kuwekeza sehemu mbalimbali hapa nchini:-

Je, Serikali ipo tayari sasa kuelekeza wawekezaji hao kuwekeza katika Mkoa wa Tabora?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (UWEKEZAJI) Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwanne Ismail Mchemba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kukuza uwekezaji katika sekta mbalimbali na kujenga uchumi wa kati wenye kuongozwa na Sekta ya Viwanda ni suala linalotekelezwa katika mikoa yote ukiwemo Mkoa wa Tabora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua fursa hii kuupongeza Mkoa wa Tabora na uongozi wake na Mikoa mingine kwa kuwa mfano mzuri katika kutekeleza mikakati ya kuvutia uwekezaji ikiwemo uandaaji wa makongamano ya uwekezaji kama lile lililofanyika mwaka 2013 Dar es Salaam na lililofanyika mwezi Novemba, 2018 katika mjini Tabora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia makongamano hayo, tumeendelea kuhamasisha kila Halmashauri kuandaa mradi wa kimkakati ambao utakuwa dira kwa wawekezaji wengine. Aidha, katika kutekeleza agizo la Serikali la kutenga maeneo ya uwekezaji, Mkoa wa Tabora umetenga ekari 42,053.71 katika Halmashauri zake zote nane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kama sehemu ya matokeo ya jitihada za Serikali, takwimu zilizopo katika Kituo chetu cha (TIC) zinaonesha kwamba tangu mwaka 1997, jumla ya miradi ya uwekezaji 55 imesajiliwa Mkoani Tabora katika Sekta za Kilimo, Viwanda, Ujenzi, Utalii Mawasiliano na Usafirishaji. Wilaya ya Tabora Mjini inaongoza kwa kusajili miradi 19, Urambo 13, Nzega miradi tisa, Igunga 11, Sikonge miradi miwili na Uyui mradi mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kati ya miradi hiyo, miradi 30 ni ya Watanzania, miradi tisa ni ya wageni na miradi 16 ni ya ubia. Hivyo, napenda kipekee kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inautambua Mkoa wa Tabora kama mojawapo ya maeneo ya kimkakati yenye fursa za uwekezaji katika sekta mbalimbali na tutaendelea kuwaelekeza wawekezaji kuja kuwekeza Tabora na katika Mikoa mingine nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kuwahamasisha Waheshimiwa Wabunge wote kushirikiana kwa karibu na Mamlaka za Serikali za Mitaa, Kituo chetu cha Uwekezaji (TIC), Mamlaka ya EPZA na Taasisi nyingine katika kuibua miradi inayokidhi vigezo (bankable projects) na pia kuboresha mazingira ya uwekezaji kwenye maeneo yao. Lengo la hili ni kufanikisha malengo ya Serikali ya kuvutia uwekezaji wenye tija nchini kote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Mikoa inashauriwa sasa kuanza kutenga katika bajeti zake fedha kwa ajili ya kujenga miundombinu ya msingi kama vile maji, barabara, umeme na kadhalika. Lengo ni kuelekea kwenye maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya uwekezaji. Hatua hizi zitasaidia katika kuharakisha uendelezwaji wa maeneo maalum ya uwekezaji kwa kukamilisha hatua muhimu za awali na hivyo kuvutia wawekezaji na hata ushiriki wa sekta binafsi katika kuendeleza maeneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, napenda kuzihamasisha Mamlaka za Serikali za Mitaa kufanya kazi kwa karibu na Taasisi za Serikali zinazotoa huduma za ushauri wa kuwezesha uwekezaji nchini ili kuweka mikakati ya pamoja ya kutambua vivutio na fursa za wawekezaji wa ndani na nje pamoja na kuwasilisha miradi ya kutafutiwa wawekezaji na kushirikiana na TIC katika kuandaa makongamano ya uwekezaji katika Mikoa husika.