Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Zainabu Nuhu Mwamwindi (6 total)

MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante ka kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa zipo tafiti nyingi muhimu zilizokwishafanyika, ikiwemo tafiti ya uyoga pori kwa matumizi ya chakula, je, Wizara imejipanga vipi kufikisha matokeo ya tafiti hizo kwa wananchi walio wengi, hasa ambao wako vijijini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Mheshimiwa Waziri anaweza kuahidi nini kwa vyuo vikuu vilivyoko mkoani Iringa kuhusiana na ongezeko la bajeti yao ya tafiti katika mwaka ujao wa fedha?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimshukuru sana Mheshimiwa Mwamwindi kwa kuweka kipaumbele katika maeneo haya ya utafiti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa tafiti inapofikia katika nafasi ya uendelezaji (commercialization) inakutana na changamoto kubwa ya kuendeleza kutokana na kutokuwa na fedha zinazoweza kuondoa utafiti huo katika awamu ya awali na kufikisha katika hatua ambayo sasa inaenda kwenye matumizi. Vilevile Wizara imeliona hilo, lakini pia, hata wanasayansi wengine wa nchi za SADC wameliona hilo na hivi jitihada iliyopo ni kuona kwamba katika kila nchi, fedha za utafiti angalau ziwe ni asilimia moja ya bajeti ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa upande wa Chuo cha Iringa kwanza niwapongeze kwa hatua mbalimbali wanazozifanya, lakini niwasisitize kuwa wanachotakiwa ni kuandika hayo maandiko mazuri, ili sasa Wizara iweze kutoa kipaumbele katika ku-support bajeti za utafiti za chuo hicho.
MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Issue siyo kujenga ukuta kuzuia mwingiliano kati ya wananchi wanaokwenda hospitali na magereza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vikao vya RCC Mkoa wa Iringa, makubaliano na Wizara ya Mambo ya Ndani ilikuwa kupatiwa eneo mbadala ili Hospitali ya Mkoa wa Iringa ambayo sasa ni Hospitali ya Rufaa iweze kupanuliwa. Halmashauri ya Manispaa ya Iringa ilitekeleza agizo la vikao vya RCC, Magereza walipewa eneo mbadala ambalo liko katika eneo la Mlolo na Serikali kuanzia mwaka 1998 na 2000 imelipa fidia kwa wananchi wote waliokuwa wanamiliki eneo lile. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa swali, kama Serikali imeshawalipa wananchi fidia na eneo liko pale kubwa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kuhamishia matumizi ya Gereza pale, eneo lile ni dogo, Hospitali ya Rufaa inatakiwa iendelezwe na TANROADS waliokuwepo pale wameshaondoka, wamepisha eneo hilo kwa ajili ya eneo la Hospitali. Ni lini Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi itaondoa Jeshi la Mageraza pale ambapo ni eneo linalowatunza wafungwa pale?
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, akubaliane na mimi kwamba Mheshimiwa Mwigulu amekuja Iringa ameona hali halisiā€¦
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujua, ni lini sasa magereza wataondoa matumizi yao pale na kuachia Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, anachokisema Mheshimiwa Mbunge ni kweli, na sisi kama Wizara tunakubaliana naye kwa asilimia 100 ya mapendekezo yake aliyoyasema. Niweke sawa sawa hivyo, maana yake nilikuwa naona Mheshimiwa Ritta Kabati hapa anajiandaa kusimama; sasa ili alielewe ni kwamba Wizara inaelewa kwamba kati ya hospitali na gereza kinachotakiwa kuondoka pale mjini ni gereza na siyo hospitali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa hospitali ile inahitaji upanuzi, Wizara inakubaliana na gereza kuhama pale na kwenda kwenye eneo lingine ambalo na lenyewe liko ndani ya mji lakini pembeni kidogo kilometa kama saba kutoka pale mjini ili kuweza kuwa na nafasi ambayo hata kiusalama itaruhusu mazingira yale kuwa salama zaidi ya kutunza wafungwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, alichojibu Mheshimiwa Naibu Waziri ni kwamba wakati jambo hilo halijafanyika, kuna hatua za mpito ambazo tunazifanya zikiwemo hizo za barabara ile kupitika kwa dharura pamoja na masuala ya ukuta aliyoyasemea. Kadri bajeti inavyoruhusu na taratibu nyingine za ndani ya Wizara ya kutumia nguvu kazi inayoendelea, mpango ni huo huo kuhamisha gereza na kuacha fursa kwa Hospitali ya Mkoa kuweza kuwa na nafasi ya kutosha.
MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ninaomba kuuliza swali moja dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa kwamba Zahanati ya Mangalali imefunguliwa Februari. Zahanati hii ipo katika Kata ya Ulanda na katika vijiji ambavyo bado vinaendelea kupata huduma kutoka kwenye Zahanati ya Kalenga ni Kijiji cha Makongati ambacho kutoka pale Zahanati ya Kalenga pana kilometa karibu 15, lakini pia Zahanati ya Kalenga ipo jirani kabisa na Makumbusho ya Chifu Mkwawa, lakini pia iko karibu kabisa na Barabara Kuu iendayo Hifadhi ya Taifa ya Ruaha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu, kwa kuwa mpango wa Serikali ni kila Kata kuwa na Kituo cha Afya, je, Serikali iko tayari kuunga mkono jitihada za wananchi wa Kalenga walio tayari kutoa eneo lao na sehemu ya nguvu kazi kwa ajili ya kupatiwa Kituo cha Afya? (Makofi). Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jibu langu la msingi nimeelezea jinsi ambavyo hakuna uwezekano wa kuongeza majengo katika Zahanati ya Kalenga kutokana na eneo lile kwamba lina makazi na tayari yameshapimwa kiasi kwamba uwezekano wa kutoa compensation Halmashauri haina uwezo huo.
Mhesimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza niungane na Mbunge kwa kumpongeza kwa jinsi ambavyo anapigania suala la kuhakikisha wananchi wanapata afya iliyo bora, lakini pia na Mbunge wa Jimbo Mheshimiwa Mgimwa kwa jitihada zake. Kwa taarifa nilizopata ni kwamba mpaka sasa hivi ameshachangia mabati 100 na mifuko 80 ya saruji ili kuhakikisha kwamba Kituo cha Afya kinajengwa Kalenga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba Vituo vya Afya vingi vinajengwa ili kupunguza msongamano ambao unajitokeza katika
Hospitali ya Mkoa wa Iringa kwani kutoka Kalenga kwenda Iringa ni kilometa 15 na pale kuna lami kiasi kwamba wananchi wana option ya kwenda hata kule, lakini lengo ni kuhakikisha kwamba wanapata huduma kwa urahisi zaidi.
MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa mahitaji ni walimu 17, kwa sasa wapo walimu 7, je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha ikama ya walimu inakamilika katika Shule ya Msingi Kipela? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, watumishi wasio walimu wapo 7, mahitaji ya shule ile ni watumishi 13. Je, Serikali haioni wakati sasa umefika wa kuhakikisha idadi ya watumishi wasio walimu inakamilika kutokana na uhitaji wa shule? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zainabu Mwamwindi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba uniruhusu nimpongeze Mheshimiwa Mwamwindi kwa jinsi ambavyo amekuwa akiwapigania wananchi wake wa Mkoa wa Iringa katika kuhakikisha kwamba wanapata huduma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la kutaka kujua Serikali ina mkakati gani, kwanza naomba nitumie fursa hii kuagiza Wakurugenzi wote kwa sababu umeshatoka Waraka kutoka Ofisi ya Rai, TAMISEMI ukiwataka Wakurugenzi wahakikishe kwamba wale walimu ambao wamejifunza elimu maalum wanapelekwa kufundisha katika shule maalum kwa sababu wana ujuzi nao. Kwa hiyo, ndani ya Mkoa wa Iringa na maeneo jirani ni vizuri Wakurugenzi wakahakikisha stock inachukuliwa ili wale walimu wote ambao wana ujuzi maalum waweze kupelekwa kabla huo mkakati wa pili wa ajira haujatekelezwa kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la msingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na upungufu wa watumishi ambao siyo wa taaluma ya elimu, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba watumishi hawa wanapatikana kwa mujibu wa ikama lakini pia itategemea bajeti itakavyoruhusu.
MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, pamoja na jitihada kubwa za Serikali ambazo zinafanyika lakini bado tatizo la utapiamlo katika mikoa ambayo inazalisha chakula kwa wingi bado linaendelea kukua. Sasa je, Serikali ina mpango gani mkakati wa kuajiri watoa huduma za lishe katika vijiji?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli ukiangalia mikoa ambayo inazalisha chakula kwa wingi nchini ndio mikoa ambayo nayo inaoongoza sana kwa utapiamlo. Na siku zote nimeendelea kusema bado tuna changamoto watanzania kula bora chakula kuliko kula chakula kilicho bora. Na hii tunaiona katika mtiririko mzima kwa maana ya udumavu vilevile tuna tatizo la Tanzania kuwa na lishe iliyopitiliza zaidi ya asilimia 10 ya watanzania wana lishe ambayo imepitiliza kwa maana ya wanaviriba tumbo, kina mama wana vitambi na kina baba wote wana vitambi, vyote hivyo nayo inaonyesha kwamba ni lishe ambayo siyo sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo sisi kama Serikali tumeliona hilo na ndio maana tulifanya uzinduzi wa mpango mkakati wa masuala haya ya lishe na mpango mkakati huo ulizinduliwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu mwaka juzi hapa Dodoma na lengo ni kuweka msisitizo katika masuala haya ya lishe na katika sekta zote. Na mpango mkakati huu unaratibiwa pale chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu na sisi kama Wizara tuna nafasi yetu kubwa katika maeneo haya kuhakikisha kwamba tunapunguza udumavu kwa watoto wadogo lakini tunaanza kupambana na lishe iliyopitiliza kwa sababu nayo ina mahusiano ya karibu sana na magonjwa yasiyo ambukizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niendelee tu kumsisitiza kwamba kuhusiana na suala ambalo Mheshimiwa Mbunge ameliuliza kwamba tunaendelea kutoa elimu kwa njia mbalimbali katika mikoa ile kuhakikisha kwamba watu katika mikoa ile wanapata elimu sahihi kuhusiana na masuala ya lishe. Sambamba na hilo tutaendelea kuajiri watumishi, maafisa lishe kadri uwezo wa Serikali utakapokuwa unaruhusu.
MHE. ZAINAB N. MWAMWINDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Leo nasimama mara ya tatu katika Bunge lako Tukufu nikiikumbusha Serikali kuhusu barabara hii itokayo Iringa kwenda Ruaha National Park.

Mheshimiwa Spika, barabara hii urefu wake ni kilometa 104 na kama majibu ya Naibu Waziri alivyosema kwamba imetengenezwa kwa kiwango cha lami kilomita 14. Kwa masikitiko makubwa ninasikitika kwamba barabara hii kwa hizo kilomita 14 imejengwa na Marais wote wanne. Upembuzi yakinifu ulishafanyika na kila mwaka Serikali inapanga fedha za ujenzi wa barabara hii. Je, ni kwanini Serikali inapata kigugumizi kuikamilisha barabara hii?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Ruaha, barabara zote za ndani ni mbovu na wakati wa masika ni mahandaki, kiasi kwamba upitaji wake na watalii wanapata shida inapunguza pato la Taifa. Swali ni lini Serikali itapanga pesa kwa ajili ya kutengeneza barabara hii? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza nakiri kwamba katika jibu langu la msingi nimesema tumekwisha jenga kilometa 14 kati ya kilometa 130 ambazo zipo katika barabara hiyo, na barabara hiyo tayari imekwisha fanyiwa upembuzi yakinifu. Mheshimiwa Mbunge anafahamu juhudi za kilometa 14 ambazo zimekwisha fanyika sio haba. Lakini anafahamu yeye ni mjumbe wa Kamati ya Maliasili, tumekuwa naye katika ziara juhudi za Wizara yetu katika kuhakikisha kwamba barabara hizo zinajengwa ni kubwa, nimuombe awe na imani na Serikali kama yalivyo maeneo mengine barabara hii itajengwa.

Mheshimiwa Spika, swali lake kuhusu ubovu wa barabara zilizopo ndani ya Ruaha ni kweli, pamekuwa na tatizo la ubovu wa miundo mbinu mbalimbali katika hifadhi ya Ruaha. Lakini nimesema katika jibu la msingi tunao mradi mkubwa REGROW, ambao tayari tulikwisha saini mkataba na umeanza kutekelezwa, Barabara zote pamoja na miundo mbinu mingine katika hifadhi ya Ruaha imo katika mkataba huo.

Mheshimiwa Spika, na nimhakikishie kwamba wakati kutengeneza mkataba huo maeneo yote haya ambayo yamekuwa yakisababisha hifadhi hii kushindwa kutumika wakati wa masika yatakuwa yamefanyiwa matengenezo makubwa na moja ya eneo ambalo Wizara yetu imehakikisha kwamba inaipa kipaumbele kufungua utalii maeneo hayo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge ninafahamu juhudi zake kubwa za kupingania utalii maeneo ya Mkoa wa Iringa na kusini kwa ujumla lakini nimhakishie kwamba Serikali inalitilia maanani suala hilo.