Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Kangi Alphaxard Lugola (22 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana Mtemi wa Kabila la Wasukuma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo machache tu ya kushauri. Pengine nianze na hili la retention ambalo limezungumzwa na Mbunge aliyepita Mheshimiwa Rwamlaza. Retention kwa mapendekezo ya Serikali ni jambo zuri kwa sababu uzoefu unaonesha sisi ambao tumekuwa tukishughulika na mahesabu ya Serikali, ziko taasisi ambazo wanatumia fedha hizi vibaya. Kwa hiyo, Mpango huu wa Serikali ni mzuri, waendelee nao, isipokuwa Halmashauri zote nchini pamoja na Mifuko ya Hifadhi za Jamii, hao wasiwekwe kwenye kundi la kupeleka fedha kwenye Mfuko Mkuu wa Hazina, waendelee kubaki na makusanyo. Bahati nzuri Mheshimiwa Rwamlaza tuko Kamati moja nadhani kule tutaendelea kushauriana vizuri ili Halmashauri zetu zisije zika-suffocate.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la kilimo. Iko mikoa ambayo kila mwaka inakumbwa na njaa na haipungui mikoa 12 lakini kwenye Mipango yetu hapa sijaona mipango mahsusi na ya makusudi ya kuhakikisha kwamba mikoa hii wanaiwekea miundombinu ya umwagiliaji. Mikoa mingi upande wa Kanda ya Ziwa tuna maji ya uhakika, tunahitaji miundombinu ya umwagiliaji, tumechoka kuletewa chakula kila mwaka. Labda tuambizane hapa kwamba mikoa ile ambayo inakuwa na njaa kila mwaka tumeitelekeza na kwamba tutaendelea na Kamati za Maafa ili tuwe tunaendelea kuwapelekea tani za chakula ilhali wao ndiyo wamebahatika kuwa na maji ya uhakika, wanaweza wakamwagilia na tukapata chakula tukajitosheleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano pale Bunda tayari eneo la EPZ limetengwa zaidi ya hekari 1,350. Naishauri Serikali kwenye Mpango huu, hebu sasa mikoa ile ya Kanda ya Ziwa kwa kuanza na maeneo hayo ya EPZ watuwekee miundombinu ya umwagiliaji ili tusiendelee kuombaomba chakula. Kila mmoja hapa anajua madhara ya njaa, watu wenye njaa hawatawaliki, watu wenye njaa hawatulii na watu wenye njaa hawawezi wakashiriki kwenye maendeleo ya huu Mpango tunaouweka hapa. Utashirikije kwenye maendeleo wakati una njaa? Wakati mwingine hatutulii humu ndani, hakuna amani na utulivu kwa sababu watu wana njaa za aina mbalimbali humu. Wengine wana njaa ya pesa, wengine wana njaa ya kushika madaraka, huwezi kutulia humu ndani, ni mifano ya njaa ukiwa na njaa huwezi kutulia. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la reli. Kwenye Mpango huu nishauri jambo moja na hii itakuwa ni hatari kwa Serikali. Kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais, ukurasa wa 12 ameelekeza kujenga reli ya kutoka Dar es Salaam - Rwanda na kwa kwenye Mpango Serikali inasema itajenga reli ya kati kwa standard gauge. Sasa kitendo cha kunyamaza au cha kuwa na kigugumizi sijui kimetoka wapi cha kutotaja reli yetu ya kati ya kutoka Dar es Salaam kwenda Kigoma na michepuko yake ya kwenda Kalema kwenda Msongati, michepuko ya kwenda Mwanza na baadaye twende Dutwa kule kwa ajili ya nickel. Serikali inaweza kutumia uchochoro huo na kwa sababu wanamshauri vibaya Mheshimiwa Rais, kama wameweza kutaja michepuko ya kutoka Mtwara kwenda Liganga na Mchuchuma, michepuko ya reli kutoka Tanga kwenda Arusha na Musoma na michepuko ya Minjingu na Engaruka kuna kigugumizi gani cha kutotaja reli ya kati kwamba ndiyo inayoenda kujengwa kwa standard gauge? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Mpango huu kuna eneo la kukarabati reli ya kati. Kwa hiyo, tunaweza kukuta ule mtandao wetu wa reli ya kati ukaishiwa kukarabatiwa halafu tusiwe na standard gauge matokeo yake wanampelekea Rais Kagame. Nani asiyejua Kagame anatamani Bandari ya Dar es Salaam? Nani asiyejua Kagame aliwahi kusema akipewa mwezi mmoja atakusanya fedha za Bandari ya Dar es Salaam kuendesha Rwanda kwa mwaka mzima? Nani asiyejua Kagame alianzisha UKAWA ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki wakamtenga Rais wetu ili waweze kujenga reli ya Mombasa mpaka Rwanda na sasa wanavuka Naivasha. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye utalii. Tunahitaji kuinua pato la Taifa na ili tuliinue ni lazima tushughulike na ujangili ambao unatishia wanyamapori na ujangili unaotishia watalii kuja Tanzania.
Naomba Mheshimiwa Maghembe haya mambo ya kuandika humu kwamba tunataka kuboresha miundombinu, kununua zana za kupambana na majangili, mpaka sasa zana za kupambana na majangili unazo, tulikuwa na helkopta juzi majangili wameitungua, hizo ndizo zana za kupambana na majangili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama majangili wameanza kutungua ndege ambazo ndizo zana za kupambana na majangili maana yake tukiendelea kukupa hizi zana za kupambana na majangili wataendelea kuzitungua. Idara yako ya Wanyamapori na Hifadhi yako ya Ngorongoro ndiko kwenye wafanyakazi wasiowaaminifu kwenye Idara ya Intelejensia ambao wanaazimisha silaha za kivita, wanawapa majangili halafu wanatungua ndege. Waheshimiwa Wabunge, hizi ndege zinaendelea kuanguka kwenye hifadhi hata ile ya Marehemu Filikunjombe ilianguka kwenye Hifadhi ya Selous. Kwa nini nisiamini kwamba inawezekana kwa sababu walikuwa kwenye Hifadhi ya Selous ambako ujangili wa tembo ni mkubwa, ni majangili hawa hawa waliangusha ndege ya Mheshimiwa Filikunjombe? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, inakuwaje ninyi katika kuajiri askari wa wanyamapori na kwenye Kikosi cha Intelejensia hamuwa-vet? Watu wengine wamefukuzwa polisi ndiyo hao mnawachukua, mnawachukua kwa sababu ya ubinamu, ujomba na mwingine ameshiriki kuangusha ndege ya Rubani Gower, maskini Mungu aiweke roho yake mahali pema. Mtu huyu ameajiriwa wakati alifukuzwa ni mhalifu, ni jambazi matokeo yake ameshiriki kwenye tukio hili.
Mheshimiwa Maghembe unafanya kazi gani na yule Mhifadhi pale ambaye ndiye anashughulika na ajira za watu wa namna hii? Tutaendelea kuwa na majangili hata ukileta zana za kupambana nao kama wafanyakazi wa Idara yako hautawa-vet na kuwasimamia vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme jambo moja. Mpango huu ni mzuri sana na katika uzuri wake ndiyo maana tunaomba kuendelea na mapendekezo haya ili Serikali ije na rasimu ikiwa inaonesha sasa Mpango huu unatekelezeka. Nakuhakikishia Mpango huu ukirudi jinsi ulivyo mkadharau mapendekezo ya Wabunge hautatekelezeka, zitabaki ni hadithi, zitabaki ni porojo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kutaja maeneo ambayo reli yetu inaenda kujengwa kwa standard gauge kwa kisingizio kwamba hamuwezi kutaja kila kitu, kama hamuwezi kutaja kila kitu mbona maeneo mengine mmetaja? Kama mtakuja hapa bila mwelekeo wa reli ya kati, nitakuwa mtu wa kwanza kusema kwamba rasimu hii hatuikubali, nitakuwa mtu wa kwanza kutokubaliana na bajeti ya kupitisha mpango ambao hauna dhamira nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kule pembezoni Kanda ya Ziwa mfuko mmoja wa simenti shilingi 20,000 wakati Dar es Salaam ni shilingi 12,000, Watanzania hawa watajenga lini nyumba? Misumari, nondo, gharama za usafirishaji zinakuwa kubwa lakini tunaendelea kupiga chenga zaidi ya miaka 15. Hayo makelele yenu mliyonayo huko kwenye mambo ya tender, sisi hatutaki vurugu zenu huko, endeleeni kukaa vizuri, tunachotaka ni kujenga reli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo taarifa, reli hii Waheshimiwa Wabunge…
MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa muda wako umekwisha.
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Ahsante sana Mtemi wa Wasukuma. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kuchangia kwenye bajeti ya Serikali ya Awamu ya Tano, kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza mtumbua majipu Rais wa nchi yetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa namna ambavyo ameonesha kwa vitendo na kwa kumuenzi Mwalimu Julius Nyerere kwa kauli yake aliyosema kwamba Ikulu ni mahali patakatifu, Ikulu haiwezi kugeuzwa kuwa pango la walanguzi. Ndiyo maana kwa ushupavu kabisa na bila kupepesa macho aliamua kumtumbua Katibu Mkuu Kiongozi ambaye alikuwa Ikulu mahali ambapo ni patakatifu. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Waziri wa Kilimo na Naibu wake wanafanya kazi nzuri, ni wachapakazi hodari na ndiyo maana kukiwa na tatizo kwa wakulima Mheshimiwa Mwigulu huyo na Naibu wake, kukiwa na tatizo kwa wavuvi, Mheshimiwa Mwigulu huyo na Naibu wake, kukiwa na tatizo la mifugo Mheshimiwa Mwigulu huyo na Naibu wake. Mheshimiwa Mwigulu tutaendelea kukupa support katika Bunge hili ili uweze kushughulika na Wizara hii nyeti, Wizara ambayo asilimia 80 ya Watanzania wanaitegemea katika maisha yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kauli mbiu yako inasema kwamba kama tunaitaka mali tutaipata shambani. Mheshimiwa Mwigulu Nchemba hatuwezi tukapata mali shambani kama Wizara yako hautatumbua majipu ambayo yameota sehemu nyeti na Wizara yako ni sehemu nyeti. Kama Kanuni zinaruhusu, kuna majipu nje pale uyaruhusu yaingie humu ndani yaulize kila Mbunge ni mahali gani ya wote kwenye mwili wake, hakuna Mbunge atakayekubali jipu limuote sehemu nyeti. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina maana gani? Mheshimwia Rais ametumbua jipu la watumishi hewa, Mheshimiwa Mwigulu Wizara ya Kilimo kama Wizara nyeti ina wakulima hewa na wakulima hewa hawa ni jipu ambalo inabidi ulitumbue. Jimboni kwangu na nchi nzima hizi voucher za pembejeo ni jipu la wakulima, wanasajili wakulima hewa, wanasajili wengine wamekufa halafu wanalipa fedha za Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jimboni kwangu kwenye kata moja ya Namhula, voucher za pembejeo zenye thamani ya shilingi 46,320,000 wamewapa wakulima ambao hawapo. Kuna mmoja anaitwa Belita Mnyabwilo yuko Kayenze Mwanza wamemuandika Mwibara kule Mkoa wa Mara kwamba ni mkulima wakati siyo kweli. Kuna Mangasa Mfungo na mdogo wake Ally Mfungo wako Kata nyingine ya Chitengule wameorodheshwa kwenye Kata ya Namhula. Mheshimiwa Mwigulu Nchemba tumbua jipu la wakulima hewa vinginevyo hatutapata mali shambani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jipu lingine la kutumbua Mheshimiwa Mwigulu Nchemba ni la mbegu za pamba zisizoota aina ya quton. Ukiangalia jedwali ukurasa wa 23 wa hotuba ya bajeti, zao la pamba limeshuka mwaka hadi mwaka na sababu kubwa ni mbegu ya quton, mbegu ya kampuni ya mwekezaji fake. Wabunge tumepiga kelele kwenye Bodi ya Pamba wanamkumbatia, hili ni jipu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba ikiwezekana ukitoka hapa ukatumbue jipu hili la Kampuni hii ya Quton. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jipu lingine ni la viwanda vya samaki. Wavuvi wanaokwenda kuuza samaki kiwandani, wakifika pale wamefoleni msururu wa magari saa nne, ina bei yake, saa tano bei inashuka, saa sita bei inashuka mpaka kuja kufika saa 12 Wahindi wenye viwanda wanaendelea kushusha bei kwa wavuvi hawa.
Mheshimiwa Mwigulu Nchemba nenda Mwanza pale ukastukize viwanda hivi utaona kilio cha wavuvi wanapunjwa bei, samaki kwa sababu wanaoza wanakosa mahali pa kupeleka. Majipu haya yako sehemu nyeti ya Wizara hii nenda uyatumbue Mheshimiwa Mwigulu Nchemba. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni mbolea. Kama kweli Serikali imekuwa committed kwamba itakuwa Serikali ya viwanda na katika nchi yetu tayari tuna Kiwanda cha Mbolea cha Minjingu, kwa nini Serikali isikitazame kiwanda hiki kwa jicho la huruma kuhakikisha kwamba wanajengewa uwezo wa kuzalisha mbolea kwa wingi ambayo ita-stabilize soko la mbolea na tutaweza kuagiza mbolea kidogo sana kutoka nchi za nje na hatutahitaji dola nyingi za kimarekani. Mheshimiwa Waziri, wewe ni mchapakazi, nenda pale Minjingu angalia matatizo yao, viwanda ambavyo tayari vipo tuanze kuvijengea uwezo hivi kabla hatujajenga vingine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la leseni za uvuvi. Wavuvi hawa wakilipa leseni leo Halmashauri ya Wilaya ya Bunda samaki wanahama wanakimbilia Wilaya ya Busega wavuvi wanawafuata wakifika Busega wanatozwa fedha za leseni nyingine. Samaki wanakimbia wanaenda Ilemela kwa Mheshimiwa Angeline Mabula wanatozwa fedha za leseni kwamba wako Halmashauri nyingine. Samaki wanaogopa upepo siyo rafiki wanakimbilia Ukerewe wakifika kule wanatozwa fedha za leseni. Ndani ya wiki moja, wavuvi hawa maskini wanatozwa leseni kwenye Halmashauri zaidi ya tano na ushahidi tunao.
Mheshimiwa Mwigulu Nchemba hili ni jipu lingine, leseni hizi zinatozwa kitaifa. Kwa nini magari yetu unatoka Songea unakwenda Kagera, unakwenda Lindi…
MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa muda wako ndiyo huo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia hotuba ya bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Naomba nianze na mambo haya ili kuweka mambo vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wale ambao tulibahatika kucheza mpira wa soka, kuna wachezaji wa aina mbili, kuna mchezaji ambaye ana uwezo wa kutumia mguu mmoja tu wa kulia na kuna mchezaji mwingine anatumia miguu yote kulia na kushoto. Kwa wale tunaotazama mpira tunajua siku zote mchezaji anayetumia mguu mmoja tu wa kulia maadui wakishamgundua wakambana wakamfanyia tight making kwenye mguu wa kulia hawezi akacheza mpira uwanjani, sana sana atatolewa nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitendo cha Kamati ya Kanuni kukaba mguu wa kulia wa hotuba ya Kambi ya Upinzani wameshindwa sasa kutumia mguu wa kushoto na ndiyo maana wamejiondoa na kutoendelea kusoma hotuba yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna aina mbili ya wazungumzaji, kuna mzungumzaji mwingine ukishamdhibiti kusema uwongo, ukamdhibiti kutoa lugha ya matusi atajitoa kwenye mazungumzo kwa sababu hana uwezo tena wa kuendelea kuongea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika sana Mheshimiwa Lema kunizulia mambo ambayo mimi sijawahi kuyasema, hii inatokana na kukabwa mguu wa kulia akashindwa namna ya kuendelea kutumia mguu wa kushoto. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge hili lipo kwa ajili ya Watanzania, kwa ajili ya kutenda haki na ndiyo maana hakuna kiti wala Kamati ya Kanuni iliyozuia Mheshimiwa Lema kutozungumzia jambo la Lugumi, hakuzuiwa ameambiwa arekebishe maneno fulani yeye anasema amezuiwa, hajazuiwa ni kwa sababu anashindwa kuchangia hoja…
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye ripoti ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama suala la Lugumi limeongelewa kwenye ukurasa wa 12 na ukurasa wa 13 na Kamati hiyo Mwenyekiti huyo hakuzuiwa na ndiyo ripoti tuliyonayo mezani na hapo ndipo ninapozungumzia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niheshimu busara za kiti chako, niende moja kwa moja..
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurasa wa nne wa Hotuba ya Mheshimiwa Waziri amezungumzia majukumu ya msingi ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Kwangu mimi majukumu hayo hayawezi yakafanyika kwa ufanisi endapo hatutakuwa na jeshi lenye nidhamu, endapo hatutakuwa na jeshi lenye makazi bora ya askari, endapo hatutakuwa na askari wenye afya bora, hatutakuwa na askari wenye moral ya kazi, ufanisi ndani ya majukumu haya hautatokea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie makazi ya askari, sisi ambao tupo kwenye Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama tumekuwa tukipata fursa ya kukagua na kutembelea nyumba za askari vyombo vyote hivi vya ulinzi na usalama si Magereza, si Uhamiaji, si Zimamoto, si Jeshi la Polisi, makazi yao ni duni. Alichosema Mheshimiwa Kawambwa kwamba ukiingia kwenye makazi ya Polisi, makazi ya Askari Magereza na vyombo vingine vya ulinzi na usalama amesema unaweza ukatoka ukiwa na masikitiko. Ninayo picha hapa nilikutana nayo kwenye gazeti la uhuru tarehe 17 Novemba, 2015 inahusu ukaguzi wa nyumba za askari uliofanywa na Mheshimiwa Waziri Kitwanga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, picha hii ambayo nitaileta kwako, utayaona makazi haya ni makazi duni na picha inamwonesha Mheshimiwa Waziri Kitwanga alipokuwa anatoka kwenye nyumba hiyo alishindwa kupita akainama akapindisha mgongo haikutosha ikabidi akunje na miguu ndipo akatoka kwenye nyumba hii. Nyuma yake kuna AGP Mangu analia ametoa na kitambaa mfukoni anapangusa machozi, picha hii inasikitisha sana. Kwa nini AGP ndani ya dakika chache anaingia kwenye nyumba analia? Je, askari ambaye amekaa kwenye nyumba hiyo miezi nenda rudi, miaka nenda rudi, amelia kwa kiwango gani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii picha nitaileta kwako uone jinsi ambavyo AGP analia kwa sababu ya uduni wa makazi ya askari. Mheshimiwa Kitwanga kutuambia kwamba kuna fedha za Wachina kujenga nyumba za askari lazima pia tutumie vyanzo vyetu vya ndani tujenge nyumba badala ya kusubiri Wachina. Katika bajeti yakehakuna mahali popote ambapo ametenga fedha za ndani kwa ajili ya kujenga nyumba bora za askari. Ndiyo maana nikasema askari mwenye nidhamu ambaye anatakiwa apatikane kwa urahisi ikitokea dharura ni yule ambaye yupo kwenye nyumba ambazo ni za askari kwenye kituo anachofanyia kazi. Kwa hiyo, kwa stahili hii Wizara ya Mambo ya Ndani itakuwa katika kipindi kigumu sana kama hawatatenga fedha za ndani kwa ajili ya makazi ya askari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la posho ya chakula kwa vyombo vyote hivi vya ulinzi na usalama. Nilishasema hapa kwamba posho hii inayoitwa ya chakula ni posho ya lishe kwa ajili ya kuwatengeneza askari, wanatakiwa wapate lishe. Hii elfu kumi kwa siku ni lishe gani ambayo askari anaweza akabajeti akapata lishe halafu akaweza kuhimili kufanya doria, kufanya kazi zenye shuruba. (Makofi)
Nimeshangaa sana Kamati ilishasema viwango hivi vya posho ya chakula ya lishe iwe inahuishwa kila mwaka, lakini mwaka huu Mheshimiwa Kitwanga ameshindwa kuhuisha posho hizi. Ndiyo maana juzi hapa Waheshimiwa Wabunge getini kwetu hapa askari ambaye ameshindwa kupata lishe bora amevamiwa na mama mmoja akamchoma kisu yule askari kwa kukosa lishe bora, hana nguvu alishindwa kuhimili kumtoa yule mwanamama aliyekuwa amemchoma kisu. Tunalipeleka wapi jeshi hili, Wizara ya Mambo ya Ndani Mheshimiwa Kitwanga angalia lishe ndiyo inawapa moral askari hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye OC bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani imekatwa bilioni nane kutoka ile ya mwaka wa fedha uliopita. Hapa tunasema jeshi lazima liwe na fedha za kutosha OC kwa ajili ya kufanya doria kwenye maziwa, kwenye bahari wakiwa na marine police watu wa Uhamiaji waweze kudhibiti mipaka yote kwa ajili ya doria, wakimbizi waweze kushughulikiwa, magereza waweze kufanya shughuli yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini inakuwaje Wizara ya Mambo ya Ndani, fedha za OC mnadhani na zenyewe ni fedha za maandazi, mnadhani ni fedha za soda, za biskuti. Fedha hizi ni kwa ajili ya shughuli za kutoa huduma kwa ajili ya Watanzania. Sasa mnapunguza fedha mpaka zile za kununulia taarifa za wahalifu ambazo ma-RCO wote wanakuwa nazo zikitoka kwa DCI yaani Criminal Investigation Fund, watafanyaje kazi bila fedha hizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara ya Mambo ya Ndani, fedha zake za OC zinafanana na fedha za maendeleo kwenye Wizara zingine kwa sababu huduma hizi zinatakiwa zifanyike kila wakati, magari yanahitajika kwenye vyombo vyote, mafuta yanahitajika. Kwa hiyo, msifikiri kwamba OC ni fedha za kukata kata tu kila wakati, wakati kwenye vyombo vya ulinzi na usalama fedha hizi ni sawa na zile ambazo zipo kwenye miradi ya maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la vituo vya polisi. Kadiri siku zinavyokwenda mahitaji makubwa ya vituo vya polisi kwenye nchi yetu yanaongezeka. Ndio maana Jeshi la Polisi walikuwa wana utaratibu wa kujenga vituo vya polisi vya tarafa ili kila tarafa iwe na vituo vya polisi. Hata hivyo, matokeo yake ni nini? Tumekuwa tukisubiri fedha zingine hizi za maendeleo ndipo zikajenge vituo hivi vya tarafa, hatutaweza kuvijenga mpaka tuhakikishe zile fedha ambazo wanazikusanya kwenye maduhuli, Bunge hili liwaruhusu fedha hizi wanapozikusanya wapate ile asilimia ambayo moja kwa moja itakwenda kujenga vituo vya polisi. Vinginevyo tutaendelea kuwalalamikia kwamba uhalifu unatokea polisi ukiwaita hawafiki kwa wakati na hata vile vituo ambavyo vipo maeneo hayo wako kwenye nyumba za kupanga, hawana magari, wengine hawana hata pikipiki, tutaendelea kuwalaumu kama jambo hili hatutalifanya kwa umakini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie magereza kwenye suala lao lenye mahitaji maalum na ndiyo maana Mheshimiwa Kitwanga katika hili naomba angalau ufungwe siku moja tu ndani ya magereza yetu ili uweze kuona jinsi wafungwa na mahabusu na hawa mahabusu nadhani kuna wakati itabidi tubadilishe sheria kwa sababu ni mahabusu lakini ukienda kule nao wanakula mlo mmoja, ukienda kule na wao mahali pa kujisaidia ni shida. Nimekwenda kule wanakwenda kujisaidia kila mmoja anawaona, tufike mahali Mheshimiwa Kitwanga tusidhani kila mtu aliye…
MWENYEKITI: Ahsante.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia bajeti hii ya Serikali. Kwanza kabisa nimpongeze Dkt. Mpango na watu wake kwa kuleta bajeti ya kihistoria katika Bunge lako Tukufu, bajeti ambayo tunaamini kwa kiwango kikubwa itakwenda kutoa majibu ya mapambano dhidi ya umaskini ambao umekithiri miongoni mwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kupoteza muda hotuba yangu ya leo itajikita katika kuwaelimisha wenzangu ambao pengine wanadhani wao ndiyo wanajua sana mambo kuliko wengine ili tuweze kuelewana na Watanzania waweze kutuelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kabisa na hotuba aliyoitoa rafiki yangu Mheshimiwa David Silinde ninayemheshimu sana katika ukurasa wa 158 wakati anahitimisha alisema, nimalizie kwa kuwakumbusha Watanzania kuwa Serikali hii ya CCM inayoongozwa na Mwenyekiti wa CCM Mheshimiwa John Pombe Magufuli imekuwepo madarakani miaka mingi toka Taifa letu lipate uhuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshangaa sana kama kweli hii kauli ndiyo ya bajeti mbadala. Mheshimiwa Magufuli tunayemzungumzia leo ni tofauti kabisa na Mheshimiwa Magufuli aliyekuwepo jana. Mheshimiwa Magufuli wa jana alikuwa ni Waziri tu katika Serikali ya Awamu ya Nne lakini Mheshimiwa Magufuli wa leo tunamzungumzia Kikatiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katiba hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inamzungumzia Magufuli ni mtu wa namna gani. Ukienda Ibara ya 33 (2) inasema Magufuli ni Rais ambaye ni Mkuu wa nchi, ni Kiongozi wa Serikali, ni Amiri Jeshi Mkuu. Hiki pekee yake kinaonesha utofauti wake na alivyokuwa Magufuli wa jana, inakuwaje leo watu wawe na mashaka juu ya maamuzi na utendaji wa Rais John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Menyekiti, Mheshimiwa Magufuli wa leo kwa mujibu wa Katiba hii ana madaraka ya kutangaza hali ya hatari katika nchi Ibara ya 32. Magufuli wa leo ni tofauti na Magufuli wa jana, Magufuli wa leo Ibara 44 ya Katiba ana madaraka ya kutangaza vita dhidi ya nchi nyingine ambayo inaweza kuvamia mipaka yetu. Magufuli wa leo ni tofauti na Magufuli wa jana, Magufuli wa leo ana uwezo wa kutoa misamaha, Magufuli wa leo ndiye ambaye ni mlinzi mkuu wa rasilimali za nchi yetu. Inakuwaje ndugu zetu kama mnasoma Katiba hii leo mumlinganishe Magufuli wa jana na Magufuli wa leo? Huyu ni Magufuli tofauti na ndiyo maana ameanza na kushughulika na rasilimali za Watanzania na Watanzania sasa tunapaswa kumuunga mkono Rais wetu ambaye amejitoa muhanga ili Watanzania tuondokane na umaskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa rafiki yangu Tundu Lissu ninayemheshimu sana wakati tunampongeza Rais hapa, mimi nilidhani yeye kama Rais wa TLS, angetuambia kwamba sasa ameshajipanga kupitia TLS kuleta mapendekezo mazuri hapa ambayo tutakwenda sasa kutazama mikataba na lile agizo la Rais ambapo amemwambia Spika kwamba inawezekana akatuongezea muda ili Sheria hizi ambazo zina wizi ndani yake tuje hapa tuzibaddilishe. Badala yake Mheshimiwa Lissu anasema kwamba hakuna chochote na yeye sasa hajajiandaa. Anaonesha vitabu hapa vya Kamati zilizopita, nilitazamia pia aoneshe na book lililosheheni la Wanasheria kwamba tayari sasa wana kitu kizuri watakachotuletea hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, rafiki yangu Mheshimiwa Lissu anapenda sana kukimbilia MIGA (Multilateral Investment Guarantee Agency). Mimi ninayo hiyo Convention hii hapa, ambayo Mheshimiwa Lissu kila wakati anaisema tu lakini hana mimi ninayo hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hii convention ukiangalia article ya 12(3) ambacho kinazungumzia Eligible Investments kinasema hivi:

“Uwekezaji wowote utakuwa eligible pale ambapo utakuwa na yafuatayo:- Namba 3 unasema compliance of the investment with host Countries laws and regulations.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu uwekezaji wa wezi hawa hauko eligible, kwa hiyo MIGA hii haitawatetea hata siku moja, wanatakiwa...

TAARIFA . . .

MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Lissu ambaye namheshimu sana na ambaye ni msomi, atalifanya Bunge hili lishindwe kuamini kauli zake. Mheshimiwa Tundu Lissu huyu kila wakati yeye ndiye alikuwa anazungumzia hii MIGA na MIGA hii ndiyo nimemletea ili nimwelimishe, katika kumwelimisha nimemsomea kipengele cha tatu ambacho kinasema wazi kwamba wale Wawekezaji lazima wafuate sheria za nchi, kama hawafuati sheria za nchi, matokeo yake MIGA haiwezi ikawaunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata Walimu huwa wanafundishwa na Walimu wengine, mimi leo ni Mwalimu wa Tundu Lissu akae kimya ili niweze kumfundisha. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshauri Rais wa nchi yangu katika hilo, kwa kuwa hawa watu, ripoti imesema bayana ikiwa na Wanasheria na Wachumi kwamba hawa watu vitu vitatu; moja ni wezi, mbili wametoa taarifa za uwongo na tatu ni wahujumu uchumi. Mheshimiwa Rais wangu John Pombe Magufuli bado anasubiri nini kuchukua hatua juu ya wezi hawa na nashangaa Mawaziri wanaomsaidia Mheshimiwa Rais yeye tayari amekwishawapa majukumu haya, leo ningetarajia Mheshimiwa Mwigulu kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani angekuwa anashughulika na kule Buzwagi kule Bulyanhulu. Nilitarajia Mheshimiwa Mwinyi ambaye yuko kwenye Majeshi, angekuwa anashughulika na maderaya yanayoenda kwenye migodi kwa sababu migodi hawa watu ni wezi, wanasubiri nini mpaka Rais ndiye aende tena Bulyanhulu kule. Tungesubiri sasa wakati huu akina Majembe Auction Mart wameshakwenda ku-cease ile migodi kwa sababu hawa ni wezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wao bado wanahangaika na hawa wawezeshaji tu, vinginevyo mimi nitakuwa mtu wa mwisho kuamini report hii, kama hawa watu ni wezi, bado tunasubiri nini, kama kweli hawa watu ni wahujumu uchumi, tumekwisha kuwa na Mahakama ya Mafisadi, matokeo yake popo wanakojoa mle, hakuna washtakiwa, mafisadi tumewapata leo, bado hawapelekwi. Nitashangaa sana! Kama wananchi hawana maji, wananchi wa Mwibara wanasota, leo tumepata matrilioni bado tena tunataka ku- negotiate tuna-negotiate na wezi, mwizi tuna-negotiate naye kwa sababu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge hapa, sasa hivi tunapeleka mzigo wa Sh.40/= kwenye mafuta kwa ajili ya wananchi wapate maji ilihali matrilioni ya pesa tumekwishayapata kwa wawekezaji hawa, lakini bado tunasema tunataka ku-negotiate, tunataka ku- negotiate, ku–negotiate huku watakuwa nao Bahari Beach au Kilimanjaro Hoteli kwenye viyoyozi, wanakunywa juice na wakati hawa ni wezi! Namwomba Mheshimiwa Rais aende mbele zaidi ili achukue hatua kwa ajili ya watu hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye hii tozo ya Sh. 40/= kwenye mafuta, ndugu zangu tusitake kuwadanganya na kuwapotosha Watanzania. Kwanza tumefuta road license, road license tumeifuta haipo tena, tulichofanya ni kuhakikisha tunaongeza Sh.40/= kwenye lita ya mafuta ili Watanzania wote waingie gharama ili Serikali yetu iweze kutupatia maji, kwa hiyo mtu anaposema kwamba Sh.40/= haimsaidii mtu ambaye hana gari, hatuzungumzii gari pale, tunazungumzia kukusanya pesa kwenye mafuta ili zile fedha tuzipeleke kwa Watanzania wote ambao wanahitaji maji. Kila mtanzania lazima achangie na hata nauli hizi wanazosema zitapanda Serikali yetu inavyo vyombo vya kudhibiti nauli, SUMATRA wapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoomba Mheshimiwa Rais huyu SUMATRA ambaye hasimamii nauli hizi zinazopanda kiholela, SUMATRA ndiye mtu wa kwanza kutumbua huyu. Sisi tunaongeza pesa kwenye mafuta, hatumaanishi kwenda kupandisha nauli kwa wananchi bila kupitia SUMATRA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie hili la mwisho, kuna suala ambalo limetusumbua kwa muda mrefu, hili suala la ukusanyaji wa mapato. Kila wakati Mheshimiwa Mpango, mapato haya tunaambiwa wanakusanya vizuri wamefika kwenye trilioni lakini mapato haya hatuyaoni, sasa kama hatuyaoni na leo tunaenda kwenye trilioni 32 na zaidi, tunataka atakapokuja kuhitimisha hapa, atuondolee wasiwasi na sisi tusiwe tunaendelea kila wakati, tunapitisha bajeti za makaratasi, tunapokwenda kwenye utekelezaji pesa haziendi, pesa hazionekani halafu wanakuja na lugha nyingine vilipanda, vilishuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitakuwa mtu wa mwisho sasa, bajeti ya mwaka jana ilikuwa ni ya kwanza ya Mheshimiwa Rais, alikuwa anajipanga, sasa imekuja bajeti ya pili, bajeti ya pili namhakikisha Mheshimiwa Mpango kama hatapeleka pesa kwenye Halmashauri zetu za Wilaya, kama hatuta–finance miradi, nitakuwa mtu wa kwanza bajeti yake inayokuja kuikataa kwa sababu nitaamini ni wale wale waliokuwa wanatusumbua kwenye Serikali ya Awamu ya Nne kwa hiyo fedha hizi zikakusanywe, fedha hizi zipelekwe kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri hajaziondolea uwezo wa kuendesha Halmashauri zao, haya makusanyo ambayo wanayafanya sisi kama Wabunge hatuwezi kuwa sehemu ya kuua Halmashauri, kwa hiyo anayesema Halmashauri tunakwenda kuziua si sahihi. Halmashauri zitaendelea kuwepo, Halmashauri wataendelea kutekeleza miradi, hata hizi kodi ambazo tunasema kwamba wanaenda kutozwa watu kwenye nyumba za tope, huu ni uwongo wanataka kuwadanganya wananchi, hakuna mwananchi ambaye nyumba yake ya tope inaenda kutozwa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyumba ambazo zinaenda kutozwa kodi tumeanza na mjini na hizi nyumba za mjini kwenye Halmashauri baadaye ndiyo tutaenda kule vijijini kuangalia zile nyumba ambazo zina viwango, siyo kila nyumba ya mwananchi ambaye amejenga nyumba ya tope na yenyewe inaenda kutozwa, huu ni uwongo ambao wanataka wenzetu kutuchonganisha na wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge hili ni Bunge la kihistoria, hili ni Bunge ambalo Rais wetu tunayemfahamu kwa mara ya kwanza wakati anapiga pushapu, Watanzania wengi hawakumwelewa hizo push-up alizopiga alikuwa anamaanisha yeye ana nguvu, yeye ana afya njema, yeye ana uwezo, ndiyo maana anasema tumwombee Watanzania. Mheshimiwa Rais tuko nyuma yako tutaendelea kukuombea na ndiyo maana nawaomba Wabunge kupitia Bunge hili tusimame tumwombee. Eee Baba yetu uliye Mbinguni tunakuomba Rais huyu ambaye ulituletea umuwekee mkono wako, umwepushe na ajali, umwepushe na mikono ya watu ambao wanamnyemelea, wengine wako humu... (Makofi/Kicheko)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Azimio la Bunge la Kuridhia Makubaliano ya Paris chini ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu spika, nishukuru kwa kunipa fursa na mimi kuweza kuchangia hoja hii ya Azimio letu la makubaliano ya Paris chini ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa juu ya mabadiliko ya tabianchi. Mheshimiwa Waziri wangu atawatambua wale wote ambao wamechangia kwenye Azimio letu, mimi nigusie baadhi ya maeneo ambayo wachangiaji wameyasema.

Kwanza kabisa chimbuko la azimio hili ni mkutano ambao ulifanyika kule Stockholm na ulikuwa unahusu binadamu na mazingira. Kwa hiyo, utaona ni kwa kiasi gani jinsi umuhimu ulivyo kati ya binadamu na mazingira jinsi wanavyotegemeana. Sheria yetu namba 20 ya mwaka 2004 ya Usimamizi wa Mazingira imesheheni mambo ambayo Watanzania wakiyafuata bila shuruti tutakwenda kutunza, kuhifadhi na kulinda mazingira ya nchi yetu na tutakuwa ni nchi ya mfano katika ukanda mzima wa Afrika na dunia nzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nasema hivyo katika sheria yetu mazingira yametajwa kwamba ni urithi katika msingi wa ile sheria kwamba mazingira ni urithi wa kizazi hiki ambacho tunaishi sasa na vizazi vinavyokuja kwa hiyo, wananchi wakielewa umuhimu huo watakuwa katika fursa nzuri ya kujali katika kutunza vyanzo vya maji katika nchi yetu, watajali katika kutunza miti, watajali kila wakati kupanda na kutunza miti na hivyo urithi huu ndio hoja ambayo Mheshimiwa Saleh alikuwa anazungumzia masuala ya urithi, namna ambavyo baadhi ya ndege wanatoweka, baadhi ya miti inatoweka, theruji kwenye Mlima Kilimanjaro inapungua kwa hiyo tutakapokuwa katika fursa hii ya kujitambua kwamba mazingira tunatakiwa uwe ni urithi kwa sasa na baadaye Watanzani tutakuwa katika mazingira mazuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, amezungumzia suala la kufanyika tafiti hasa kuwatumia wataalamu tafiti hii ya mimea, tafiti ya miti sheria yetu ya mazingira inaanzisha mfuko wa Taifa wa dhamana ya mazingira na mojawapo ya matumizi katika mfuko ule ni katika masuala ya tafiti, ni katika masuala pia ya kuwafadhili Watanzania waweze kusoma katika maeneo haya ya mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni imani yetu Ofisi ya Makamu wa Rais kwamba bajeti hii inayokuja tuombe Waheshimiwa Wabunge wapitishe tuweze kuwa na fedha za kutosha katika mfuko wa Taifa wa dhamana ya mazingira ili kupitia mfuko huo tuweze kuhakikisha kwamba tunakuwa na wataalam wanaofanya hizi tafiti ikiwa ni pamoja na kuwasaidia wananchi katika kusoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria yetu ya mazingira kifungu cha sita kimetoa wajibu kwa Watanzania wote kuhakikisha kwamba wanatunza na kuhifadhi mazingira, kwa hiyo sio suala tu la Ofisi ya Makamu wa Rais au NEMC kwamba sisi ndio tunawajibika kuhakikisha kwamba wananchi wanatunza mazingira ni wananchi wote.

Niwaombe Waheshimiwa Wabunge nyinyi ndio mko majimboni kule ambako ndiko kuna halmashauri zetu kuanzia Halmashauri za Wilaya, za Miji za Manispaa na Majiji na amezungumzia Mheshimiwa Richard Mbogo masuala ya uelewa kwenye Vitongoji, kwenye Vijiji Waheshimiwa ninyi ndio Madiwani kwenye Halmashauri zenu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawaomba kwa kuwa sheria hii kuanzia kifungu cha 36 mpaka 41 kinazungumzia kuwepo kwa Kamati za Mazingira kwenye ngazi za Vitongoji, Vijiji, Mitaa, Kata mpaka Wilaya na kuwepo kwa Maafisa Mazingira hakikisheni kwamba Kamati hizo zipo na zinafanya kazi pale ndipo tutakuwa katika nafasi nzuri ya kulinda na kuhifadhi mazingira kwa sababu mazingira yako kule chini kabisa kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala lililozungumzwa sana la hasa kuanzia Kambi ya Upinzani kwamba kuwabana zile nchi ambazo zinachafua mazingira ili waweze kuleta fedha.

Katika Azimio hili kwenye mkataba imewekwa bayana kabisa namna ambavyo hizi nchi zinawajibika kusaidia fedha na tumetaja Mifuko mbalimbali na Mashirika ya Kimataifa ambako sisi hupata fedha. Tumewaonesha miradi mbalimbali, mingine ambayo Mheshimiwa Lubeleje amesema itaenda kwenye Wilaya yake na baadhi ya Wilaya za Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni matumaini yetu kwamba sisi tutakapotenga fedha za ndani na tukaendelea kupata fedha hizi kutoka kwa wafadhili, ni imani yetu kwamba tutakwenda kuhifadhi na kutunza mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na wasiwasi Mheshimiwa Mbogo. Anasema kweli, kwenye Ilani yetu ukurasa wa 213 tumezungumzia kwamba kila Halmashauri hapa nchini lazima kila mwaka wawe na miradi ya kupanda miti isiyopungua 1,500,000 na kwamba, ni kweli hiyo miti ipo?

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie kwamba mimi na Mheshimiwa Waziri tumekuwa tukizunguka nchi nzima ikiwa ni pamoja na kutumia Sikukuu za Mazingira Duniani, tumekuwa tukizunguka na kuhimiza Halmashauri waweze kupanda hiyo miti na kutuonesha kwa macho. Tunajipanga kama sehemu ya mkakati wa Kitaifa ili kuanzia mwakani, kama ilivyokuwa kwa Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Magufuli, akiwa Waziri wa Uvuvi, alikuwa na uwezo wa kujua idadi ya samaki kwenye bahari na kwenye maziwa na mito; nasi tutakuwa na sensa ya miti ili tujue kwamba hii miti tunayoambiwa kwenye taarifa mbalimbali wamepanda, je, hii kweli hii miti ipo, ili tuwe na uhakika kwamba mazoezi haya yanakwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mita 60 na wamezungumzia kwenye Kambi ya Upinzani vinyungu kule Iringa na Njombe; wamezungumzia kule milimani kule Kilimanjaro. Niseme tu kwamba Mheshimiwa Waziri alishatoa mwongozo kwamba Halmashauri zote nchini walete orodha ya vyanzo vyote vya maji, pamoja na milima na vilima ili wachanganue kwamba vyanzo hivyo vya maji vina changamoto gani ili sisi Ofisi ya Makamu wa Rais tuweze kutengeneza mkakati wetu wa Kitaifa ambao unaendelea kwenye task force ili tuweze kuwabana hao ambao wanaharibu na kuchafua vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba nchi hii ambayo tumekuwa tukisema Mataifa yanayochafua na kuharibu mazingira, hasa kwenye hewa ya ukaa ambayo inakuja mpaka huku na kuleta athari za mabadiliko ya tabianchi kwamba tuzibane zilete fedha; sisi kwa kutumia Sheria ya Mazingira tunawabana wananchi watumie fedha katika kuhifadhi na kutunza mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunawabana wawekezaji na hasa wenye viwanda kuhakikisha kwamba katika uwekezaji wao, nao wasiangalie tu sehemu ya faida, waangalie pia kuweka mifumo rafiki ambayo itahakikisha kwamba wanalinda na kuhifadhi mazingira ili siku ya siku Tanzania ya viwanda ambayo Mheshimiwa Rais ni champion kuhakikisha kwamba Tanzania ya Viwanda inaenda sambamba na kuzingatia sheria za kutunza na kuhifadhi mazingira. Kwa hiyo, tutaendelea sisi Ofisi ya Makamu wa Rais kuwa wakali sana kusimamia sheria hii ili Watanzania wote wahakikishe kwamba wanatunza na kuhifadhi mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye suala aliloligusia Mheshimiwa Lubeleje. Mheshimiwa Lubeleje amegusia suala la Mpwapwa. Mheshimiwa Waziri wangu alishaniagiza niende Mpwapwa ambako wananchi wanaendelea kukata miti ovyo kwenye vilima, wanaharibu vyanzo vya maji na kuchoma moto ovyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna shule moja ya sekondari ambayo inasemekana kuna mwananchi mmoja alienda akakata miti ya shule ambayo wao walikuwa wameipanda kwa ajili ya kuhifadhi mazingira. Kwa hiyo, nitoe wito kwa nchi nzima, siyo Mpwapwa tu kwa Mheshimiwa Lubeleje, kwamba suala la kisingizio cha kwamba tunatumia kuni, tunatumia mkaa, vijijini kule wananchi wengi hawatumii mkaa, mkaa mwingi unaenda mijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi Serikali imeshajipanga kuhakikisha kwamba kupitia Wizara ya Nishati wanaanza kusambaza gesi katika Mji wa Dar es Salaam ambapo tunaamini sasa tunaenda kuwa na nishati mbadala kwa njia ya gesi ili tuanze kupunguza matumizi ya kuni na mkaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, taasisi nyingi za Serikali yakiwemo Magereza, Hospitali na shule, tumeshawapa mwongozo na maelekezo kwamba waache sasa kutumia kuni na mkaa, waende kwenye nishati mbadala. Wazo zuri alilolitoa hapa Mheshimiwa Mbogo, kuwa shuleni kwenye bio- gas, kuna baadhi ya shule ambazo tayari tumeanza kuzitembelea kwamba wana-recycle, wana bio-gas ili sasa kupitia Bunge lako tutakapopata uwezeshaji wa kibajeti, tuanze kupita kwenye shule na taasisi nyingine ambazo nimezitaja kama majeshi na shule ili waanze kuwa na nishati hii ya bio-gas ili tupunguze ukataji wa miti.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mungano na Mazingira kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS,MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa nafasi niweze kuchangia na kutoa baadhi ya ufafanuzi kwenye hoja ambazo Kamati zote mbili pamoja na Wabunge wameweza kuziwasilisha. Kwanza kabisa nianze kuunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa namsikiliza Mheshimiwa Kigwangalla Dkt. na Mheshimiwa Sware Dkt. wanatunishiana misuli ya kiudokta kwenye suala la Stiegler’s Gorge, sasa nikasema mimi ambaye ni Naibu Waziri wa mambo haya ya mazingira nikiingia hapo nafikiri tutaelewana vizuri. Hata hivyo, namshukuru Dkt. Kigwangallla amemaliza masuala yote ya Stiegler’s Gorge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri wangu mtoto wa baba January namshukuru kwa sababu tangu alivyonipokea kwenye Ofisi ya Makamu wa Rais amekuwa msaada mkubwa sana na hivyo kunifanya niweze kukimbia haraka katika kumsaidia masuala haya ya mazingira katika nchi yetu. Kwa hiyo, Mheshimiwa mtoto wa Mzee Makamba, nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru Katibu Mkuu wa Wizara yetu, Ofisi ya Makamu wa Rais, Jemedali Engineer Joseph Malongo na Naibu Waziri Mwanasheria Butamo wamenisaidia sana katika kuhakikisha kwamba nafanya shughuli hizi za mazingira kwa raha mustarehe kwa sababu kila nilichokuwa nikiwaelekeza wamekuwa wakitekeleza ninachokihitaji wamekuwa wakifanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwashukuru wafanyakazi wote, Ofisi ya Makamu wa Rais namna ambavyo wamekuwa nami muda wote katika kunipa msaada na kuweza kupata uzoefu kwenye Ofisi ya Makamu wa Rais. Vile vile nimshukuru sana Dkt. Makotha ambaye ni Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NEMC pamoja na timu yake wamekuwa wakifanya kazi nzuri kazi ambayo imetukuka, wamekuwa watu wa msaada sana katika kunifanya mimi niweze kutekeleza majukumu yangu pasipo wasiwasi wala vikwazo vyovyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ambazo zimeibuliwa na Kamati zipo nyingi, lakini wamejikita katika kutushauri. Naomba kupitia Bunge lako Tukufu kuwaondolea wasiwasi Wajumbe wote chini ya Mwenyekiti Saddiq na Makamu wake Bashungwa kwamba yale yote ambayo wametushauri juu ya mazingira tutayafanyia kazi na nitagusia machache juu ya mazingira na nitagusia machache ambayo wameyasisitiza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wako Wabunge wengi ambao wamechangia kwa maandishi kwenye masuala ya mazingira na pia wamechangia kwa kusema hapa Bungeni kwa sababu ya muda nitakwenda kugusia masuala machache ambayo yamewasilishwa katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kufafanua hizi hoja, kwa nafasi ya pekee nimshukuru Mheshimiwa Rais ambaye aliniteuwa na hii ni bajeti yangu ya kwanza na Mheshimiwa Rais ameendelea kuniamini nami namuahidi kwamba sitamwangusha, nitaendelea kuifanya kazi hii katika kasi yake ya hapa kazi tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa pia niendelee kumtia moyo Mheshimiwa Rais kwamba baadhi ya Watanzania wenzetu na baadhi ya Wabunge wenzetu humu ndani wamekuwa wakimkebehi na kumkejeli kwamba Rais huyu amekuja na mambo ambayo sasa Taifa hili linaenda kuangamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo haya ni ya upotoshaji na siyo ya kweli. Kati ya Rais ambaye katika bara la Afrika na duniani kote ambaye amejibainisha kwamba sasa atakwenda kulinda kwa nguvu zote rasilimali za Watanzania ni Rais Dkt. John Pombe Magufuli, Rais Dkt. John Pombe Magufuli ni miongoni mwa Marais ambao hawazaliwi mara kwa mara na hawapatikani kila mahali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais anapokuwa anawaambia Watanzania kwamba katika shughuli zetu hizi tumtangulize Mungu mbele, wananchi wengi wanashindwa kuelewa maana yake ni nini. Maana yake ni kwamba Rais Dkt. Magufuli ni chaguo la Mungu na ndiyo maana anapotamka maneno hayo Mungu anamwambia kwamba hapo hapo uliposhikilia hapo usibadilishe gia endelea kulitetea Taifa la Watanzania na ndiyo maana.

T A A R I F A . . .

NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Gekul namheshimu sana, lakini napenda nimkumbushe kwamba hii kazi niyayofanya hapa nimeteuliwa na Rais na nafanya kazi ya Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama yeye hataki kusikia maneno ambayo nayasema juu ya aliyeniteua, basi avute subira pale ambapo vizazi vinavyokuja inawezekana na wenyewe wakawa Rais ambao watampatia majukumu ili aweze kuwazungumzia. Hata hivyo, nimhakikishie kwamba yeye na chama chake kuingia madarakani ni vigumu sana.

Na ni rahisi sana ngamia kupenya kwenye tundu la sitando. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze sasa kujibu hoja za Wabunge najua wana kiu ya kusikiliza. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wengi kwa kusema hapa na kuchangia kwa maandishi wamezungumzia kwa uchungu sana juu ya uchafuzi na uharibu mkubwa unaofanyika kwenye vyanzo vya maji. Vyanzo vya maji katika nchi yetu vina uhusiano mkubwa sana na maisha yetu na uhai wetu. Pia vyanzo hivi vya maji vina uhusiano mkubwa sana ndoto ya Mhesimiwa Rais ya Tanzania ya viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kuwa na viwanda lazima tuwe na umeme wa uhakika; ili tuwe na umeme wa uhakika lazima tulinde vyanzo vya maji kwa gharama zote na kwa nguvu zote. Ndiyo maana katika nchi yetu vyanzo vya maji ambavyo vinazalisha umeme kwa kutumia maji tuna Kihansi, Kidatu, Mtera, Maporomoko ya Pangani, Hale, Nyumba ya Mungu, Uwemba, Tulila, Mwenga, Darakuta pamoja na Iyovi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi yote hii wanazalisha kwa ujumla megawatt 560.6, kwa kuwa sasa tunakwenda kuwa na mradi mkubwa huu wa Stiegler’s Gorge ambao utazalisha megawatt 2100. Maana yake ni nini kwenye vyanzo vya maji maana yake ni kwamba sisi Ofisi ya Makamu wa Rais tusiposaidiana na Watanzania katika kuhakikisha kwamba tunalinda vyanzo vya maji katika nchi nzima, uzalishaji wa umeme ambao unatumia maji hautaweza kufanikiwa kwa kiwango ambacho tunakihitaji. Ndiyo maana Ofisi ya Makamu wa Rais tunayo mikakati kuhakikisha kwamba tunalinda vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wengi walikuwa wanaulizia tuna mikakati gani? Tuna mkakati wa mwaka 2006 ambao unahusu uhifadhi wa mazingira na vyanzo vya maji na ndiyo maana katika mkakati huu Ofisi ya Makamu wa Rais iliwaandikia barua Wakurugenzi wote wa Halmashauri nchini kuhakikisha wanabaini vyanzo vyote vya maji pamoja na changamoto zake ili wawasilishe Ofisi ya Makamu wa Rais ili vyanzo vingine viwe protected viweze kuwekewa utaratibu wa kuvitangaza kwenye gazeti la Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kupitia Bunge lako Tukufu muda tuliowaongeza wa hadi tarehe 20 mwezi huu unakaribia kwisha na kama nilivyosema juzi kwenye Bunge hili. Wakurugenzi ambao watakaidi na kutotekeleza agizo hili hakika Ofisi ya Makamu wa Rais itaorodhesha majina yao na kumpelekea Mheshimiwa Rais ambaye ndiye amewateuwa ili aweze kutafakari na kuona vitumbua vyao ama vitiwe mchanga ama laa! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuna mkakati mwingine wa mwaka 2008, mkakati huu ni wa kuhifadhi mazingira katika hatua za haraka kwenye bahari na kwenye ukanda wa Pwani pamoja na mito, maziwa na mabwawa makubwa. Tuna mkakati mwingine wa 2012, huu ni wa kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Kwa hiyo, mikakati yote hii pamoja na wananchi kuwataka watekeleze sheria ya mazingira tuna uhakikika tunakwenda kulinda vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana tuliweza kufanya mazoezi makubwa kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais kunusuru bonde la Mto Ruaha Mkuu, Task Force ambayo Mheshimiwa Makamu wa Rais aliiunda. Ndiyo maana maeneo yote ambayo yana mabonde, maeneo yote ambayo yana shughuli za binadamu lazima tutoe miongozo namna ya kufanya agriculture ambayo ni ya kihifadhi yaani conservation agriculture.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo limezungumziwa sana ni jambo hili la upandaji wa miti na hasa Kamati pamoja na Wabunge kwamba tumekuwa na kawaida ya kupanda miti ikiwa ni pamoja na uzinduzi wenye sherehe, lakini siku ya siku miti hiyo tukiihesabu haifiki idadi ile ambayo inakuwa inapandwa; Kamati ilitaka kujua tuna mpango gani Ofisi ya Makamu wa Rais. Kwenye ilani ya CCM ukurasa wa 212 hadi 213 halmashauri zote nchini wanatakiwa kupanda miti isiyopungua milioni moja na laki tano, lakini ni pamoja na kuweka sheria ndogo zitakazosimamia masuala hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba kuanzia mwakani Ofisi ya Makamu wa Rais inaandaa utaratibu wa kufanya sensa kubwa itakayokwenda kujua miti ambayo imepandwa imekuwa mingapi na mingapi imekufa. Ili tuweze kutoa miongozo ambayo itatusaidia kuwa na Tanzania ya kijani na hiyo imeenda sambamba, Mheshimiwa Makamu wa Rais alipohamia Dodoma alianza na mradi mkubwa wa kuijanikisha Dodoma na kwa utaratibu huo tunaendelea kujanikisha maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikakati mingine ni pamoja na siku ya mazingira duniani, tumekuwa tukihamasisha wananchi wapande miti ikiwa ni pamoja na kuomba shule, Taasisi za Dini pamoja Taasisi Zisizo za Kiserikali katika upandaji wa miti. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge niwatoe wasiwasi kwamba nchi yetu itakwenda kuwa na mkakati huo kuhakikisha kwamba miti tunayoipanda tunaitunza na kukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni hili la UDART kwamba NEMC ilikuwa wapi; nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, mwaka 2009 UDART waliweza kupata cheti cha tathmini ya athari kwa mazingira na walipewa masharti ambayo watakuwa wanayazingatia katika kuhakikisha kwamba wana-mitigate na kuepuka athari ambazo zingeweza kutokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba, kutokana na athari za mabadiliko ya tabianchi ambazo mara kwa mara tunawaambia mojawapo ya madhara ni mafuriko makubwa ndiyo maana katika eneo hilo mafuriko ambayo hayakutarajiwa yamechangia kwa kiasi kikubwa kuhakikisha kwamba UDART inakuwa kwenye mafuriko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shughuli za binadamu ambazo zinafanyika kando kando ya Mto Msimbazi na zenyewe zimechangia kwa kiasi kikubwa na ndiyo maana tuna mpango wa kupitia mito yote na miji yote kuhakikisha kwamba hawa ambao wako ndani ya mita 60 na wengine wamejenga mpaka kwenye kingo tuweze kuotoa mwongozo wa namna gani wanaweza wakaepusha mambo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nitoe mchango wangu kwenye hoja za Kamati, hususan kwenye taarifa ya Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru na kumpongeza sana Mwenyekiti wa Kamati, Mheshimiwa Zungu pamoja na Makamu wake na Wajumbe wote wa Kamati kwa kazi nzuri na kubwa ambayo wameifanya na kuweza kuainisha maeneo yenye changamoto na kutoa maoni pamoja na mapendekezo. Mheshimiwa Mwenyekiti na Kamati yake, nataka niwahakikishie kwamba maoni na mapendekezo waliyoyatoa katika Wizara yangu mara moja nitaanza kuyachambua na kuyashughulikia moja baada ya lingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii pia kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya tangu amekuwa Rais wa nchi hii. Mambo yote ambayo aliyaahidi kwenye Ilani hii ya CCM na hususan kwenye eneo la Ibara ya 4 na Ibara ya 146 inayohusu vyombo vya ulinzi na usalama. Nataka niwathibitishie Watanzania kwamba Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na Serikali yake ya Awamu ya Tano wamewahakikishia Watanzania kwamba wamekuwa na amani, wamekuwa na usalama, wamekuwa na utulivu, mali zao zinalindwa pamoja na maisha yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba kuna baadhi ya Watanzania ambao wanabeza, wanakejeli juhudi za Mheshimiwa Rais, nataka nimthibitishie kwamba hao hawajitambui na hawajui kwamba yeye yuko na Mungu. Isaya 54, mstari wa 17 inasema: “Kila silaha itakayonyanyuliwa juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa,” kwa sababu Mheshimiwa Rais yuko na Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe ufafanuzi wa baadhi ya hoja ambazo zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge. Katika uchambuzi wa Kamati, ukurasa wa 20 wamezungumzia masuala mbalimbali, lakini moja ambalo nitakwenda kulitolea ufafanuzi ni lile linalohusu kuchelewesha upelelezi wa kesi na hivyo wakati mwingine kusababisha magereza kuwa na mrundikano hasa wa mahabusu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango uliotolewa na Mheshimiwa Ruth Mollel ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati, ameelezea sana kwa hisia na uchungu mkubwa kwamba kesi nyingi zinachelewa, zingine miaka minne mpaka sita kwa mifano aliyoitoa. Nakubaliana naye, lakini sababu zinazosababisha kuchelewa kwa upelelezi wa kesi sio sababu moja, ni sababu nyingi kadha wa kadha. Kuna sababu zingine ni kutokana na kesi yenyewe jinsi ilivyo, inahitaji utaalam, wakati mwingine inahitaji kusafiri, tunahitaji fedha. Hata hivyo, pia nakubali kwamba, upelelezi mwingine unachelewa kwa sababu ya uzembe wa askari, kwa sababu ya askari kutowajibika na hivyo kuchelewesha upelelezi wa kesi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sababu nyingine ambayo ni kubwa na naomba Mheshimiwa Ruth Mollel anisikilize vizuri, pamoja na upande huo wanisikilize vizuri, kuna kesi ambazo zinachelewa upelelezi wake kwa sababu ya kutelekezwa. Baadhi ya kesi ambazo zinatelekezwa, nitolee mfano wa kesi maarufu ya Mheshimiwa Tundu Lissu. Kesi ya Mheshimiwa Tundu Lissu imetelekezwa. Katika mazingira ya kawaida kesi inapotelekezwa Jeshi la Polisi hawana namna nyingine ya kufanya uchunguzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika tukio lile lililotokea tarehe 7 Septemba, 2017, lile gari lilikuwa na watu wawili tu. Baada ya tukio lile, sisi wapelelezi na uendeshaji wa kesi kuna wale tunaowaita key witnesses; key witnesses ni pamoja na victim, Mheshimiwa Tundu Lissu na yule dereva aliyekuwa kwenye gari. Katika mazingira ya kutatanisha na ambayo mpaka sasa hatuelewi; ni kwa nini dereva ameitelekeza kesi hii na kutotoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi…

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: …ili atueleze hao ambao waliwafuatilia walikuwa ni watu wa aina gani?

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: …wembamba, wanene; warefu, wafupi, walivaaje …

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, analipotosha Bunge, taarifa.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: … ili kusaidia Jeshi la Polisi liweze ku…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Selasini, taarifa nilishazikataa tangu Mheshimiwa Stanslaus Mabula aliposimama, kwa hiyo naomba ukae tafadhali; Mheshimiwa Kangi Lugola.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni vyema wakatulia ili niwape darasa la mambo ya upelelezi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kukosa ushirikiano wa key witness ambaye ni dereva mpaka sasa, kesi hiyo tumeshindwa kuendelea nayo katika mazingira ya kawaida.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini namba mbili; niendelee kutoa maelezo kwa nini kesi zinachelewa. Mheshimiwa Tundu Lissu baada ya kutoka hospitali tulitarajia kwamba angekuja kwa uchungu wa kesi yake ili aje atoe maelezo kusaidia Jeshi la Polisi ili tuweze kuchunguza na kuanzisha ushahidi ambao tunaweza tukapeleka kesi mahakamani. Kwa hiyo katika mazingira ya namna hiyo tunashindwa kuendelea na baadhi ya kesi kwa sababu wanaohusika wanatelekeza kesi zao na wanashindwa kutoa ushirikiano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni matarajio yangu na niwaombe Watanzania wote ambao mnakuwa na kesi zenu za jinai, lazima mtoe ushirikiano kwa Jeshi la Polisi, lazima kesi hizi muwe na uchungu nazo ili kuondoa lawama kwa Jeshi la Polisi kwamba wanachelewesha kupeleleza ilhali ninyi mnatelekeza kesi zenu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kutoa mchango wangu… ninyi ndio mnaumiza Jeshi la Polisi kutoendelea kupeleleza.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Selasini, naomba utulivu tafadhali.

Mheshimiwa Selasini nimekutaja tena, naomba utulivu na wewe ndio Chief Whip kwa sasa, naomba utulivu.

(Hapa Mheshimiwa Selasini aliendelea kuhitaji nafasi ili atoe mwongozo)

NAIBU SPIKA: Siwezi kukupa nafasi kwenye miongozo wakati nimekataa.

Mheshimiwa Kangi Lugola, ongea na Kiti.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwenye kipengele hicho kwamba katika mazingira ambayo mashahidi muhimu hawatoi ushirikiano kwa Serikali, wasitumie ndimi zao kupotosha wananchi kwamba Serikali inahusika katika vitendo kama hivyo ilhali wao hawataki kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye suala la wahamiaji haramu; Waheshimiwa Wabunge wametoa michango yao juu ya wahamiaji haramu hasa katika Mikoa ya Kigoma, Kagera pamoja na Katavi. Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli inawahakikishia Watanzania kwamba wahamiaji haramu, hasa ambao wanatoka kwenye Nchi za Congo, Burundi, Rwanda pamoja na Uganda, kupitia Uhamiaji tunaendelea kufanya misako pamoja na doria na kuwabaini wahamiaji haramu wote wengine tunawarudisha kwao wengine tunawashtaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo katika kushughulika na suala hili la wahamiaji haramu, kuna maeneo mengine yana changamoto kubwa kama ambavyo Mheshimiwa Oliver Semuguruka amezungumzia maeneo ya Kyerwa kule. Nilipokwenda kule Isingiro, nikaenda Ruambaizi, pia kuna lile ziwa ambalo amelizungumzia ambapo wahamiaji haramu wanapenda kutumia mitumbwi na kuvuka kuja upande huu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na Uhamiaji tutaendelea kufanya doria ikiwa ni pamoja na kutafuta uwezekano wa kuwa na boti katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika suala la wahamiaji haramu Serikali imeielekeza Idara ya Uhamiaji kuhakikisha kwamba wanasirikiana na Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa hiyo niliyoitaja kuhakikisha kwamba wanafanya operesheni maalum ya kuwabaini na kuwachukulia hatua mahamiaji haramu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye suala la vitambulisho vya Taifa ambavyo vinatolewa na NIDA kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wametoa michango yao. Nataka niwathibitishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwamba Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa wanaendelea kubaini na kusajili na kutoa vitambulisho vya Taifa na wale ambao hawajafikiwa, wale ambao hawajapata vitambulisho wasiwe na wasiwasi, vitambulisho hivi lazima kila Mtanzania ambaye ana miaka 18 na kuendelea atapata na vitambulisho hivi vinatolewa bure. Kwa hiyo wale ambao hawajafikiwa wasidhani kwamba kuna ukomo na kwa sababu hajapata kitambulisho kwa hiyo sasa hatapata kitambulisho.

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Kangi, muda wako umwekwisha.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe ufafanuzi wa hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge kutokana na hotuba yangu ya taarifa ya utekelezaji wa mpango na Bajeti kwa Mwaka 2018/2019 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya fedha kwa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2019/2020 niliyoiwasilisha hapa Bungeni tarehe 24 Aprili, 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba yangu imechangiwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama ambayo imetoa maoni na ushauri kwa Wizara na Serikali kwa ujumla katika maeneo mbalimbali. Kwa dhati kabisa naishukuru Kamati hii kwani imekuwa ikitoa maoni ya msingi kwa Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya Waheshimiwa Wabunge 92 wamechangia hotuba hiyo, kati ya hao Wabunge 45 wamechangia kwa kuongea na Waheshimiwa Wabunge 47 wamechangia kwa maandishi. Pamoja na maelezo ya ufafanuzi nitakayoyatoa, hoja zote za Waheshimiwa Wabunge zitawasilishwa rasmi kwa maandishi katika Ofisi ya Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima na taadhima nianze kutoa majibu kutokana na ushauri mbalimbali ambao umetolewa na Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, lakini kwa sababu ya muda nitagusia maeneo machache na ushauri mwingine ambao umetolewa na Kamati naomba uingie kwenye Hansard kwa sababu Wizara ushauri wote uliotolewa tumeuzingatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wametoa ushauri kwamba Serikali itenge shilingi bilioni nane ili kuendeleza Makao Makuu ya Jeshi la Zimamoto pale Mchicha, Dar es Salaam. Tumezingatia ushauri wa Kamati kwamba kwa kuwa tumehamia Dodoma na sasa tumeanza kujenga Makao Makuu ya Jeshi la Zimamoto na uokoaji Mjini Dodoma, lile jengo tumeunda Kamati Ndogo ya Wataalam ili waweze kutushauri kwa ajili ya kubadilisha matumizi na kwa sababu tuna chuo, tunaweza tukafanya kuwa Tawi la Chuo chetu cha Jeshi la Zimamoto na Uokoaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Kamati yako ilishauri kwamba mchakato wa kukamilisha Sheria ya Usalama barabarani umechukua muda mrefu. Nikuhakikishie pamoja na Bunge lako tukufu kwamba katika Mwaka huu wa fedha, sheria hii iko katika hatua nzuri tutakuwa tumeiwasilisha kwenye Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwewnyekiti, pia ushauri mwingine ambao tumeuzingatia ni kuendelea kutumia utaratibu wa Bodi ya Parole ya kupata adhabu mbadala kwa ajili ya kupunguza msongamano kwenye Magereza wa wafungwa pamoja na mahabusu. Si hilo tu, ni pamoja na kuendelea kutumia msamaha wa Mheshimiwa Rais ikiwa ni pamoja na kujenga magereza hapa nchini kama ambavyo tunaelekea kumaliza Gereza la Ruangwa pamoja na Chato pamoja na ukarabati na kupanua mabweni kwenye magereza mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri mwingine ambao ni vyema nikaugusia ni kwamba Kamati ilishauri Serikali itoe fedha za maendeleo bilioni 5.79 zilizoidhinishwa kwa ajili ye ujenzi wa Ofisi za Uhamiaji za Mikoa, Wilaya na vituo, hata hivyo fedha hizo kwamba hazikutolewa. Ni kwamba Wizara imeendelea kuwasiliana na Hazina na mpaka sasa tunaendelea na mawasiliano kuhakikisha kwamba hizo fedha kabla ya mwaka wa fedha haujakwisha zinatolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ushauri walioutoa ambao ni vyema nikaugusia ni huu wa wahamiaji haramu kwamba wahamiaji haramu wapatao 3,260 wako kwenye magereza yetu hapa nchini na wametoa ushauri, tumezingatia na hasa ikizingatiwa kwamba Tanzania, Ethiopia pamoja na Kenya tumefanya mkutano wa pamoja, yako mambo ambayo tumekubalina kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunatatua tatizo la wahamiaji haramu. Kwa hiyo ushauri wote ambao Kamati imetupatia sisi Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi tumeuzingatia na tutaufanyia kazi na hatutakuwa na mzaha. Naamini ninavyozungumza hapa, Naibu Waziri anajua, Naibu Katibu Mkuu na Katibu Mkuu wote wamesikia na Wakuu wote wa vyombo wamesikia, tutafanya kazi kama mchwa usiku na mchana kuhakikisha kwamba yote haya tunayatekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende sasa kugusia hoja mbalimbali za Waheshimiwa Wabunge zingine ambazo zimetolewa kwa maandishi, zingine kwa kusema na zinahusu vyombo vya ulinzi na usalama mbalimbali ambavyo viko chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Kabla sijafikia hatua hiyo, nataka niwathibitishie Waheshimiwa Wabunge na nataka niuthibitishie umma wa Watanzania kwamba mkiona vyaelea vimeundwa. Amani na usalama na utulivu wanaouona katika nchi hii ni kwa sababu ya kazi nzuri, kazi ambayo imefanywa na vyombo vya ulinzi na usalama na hususan Jeshi la Polisi kuhakikisha kwamba nchi yetu inaendelea kuwa nchi yenye heshima duniani na kuheshimika kwa kuwa na amani na usalama wa hali ya juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, nataka niwafahamishe Wabunge; kazi namba moja kabisa ya Jeshi la Polisi ni kumlinda Mheshimiwa Rais pamoja na Taasisi yake na ndiyo maana alipo Mheshimiwa Rais, Jeshi la Polisi tupo. Hainiingii akilini baadhi ya Waheshimiwa Wabunge kusimama na kubeza kazi nzuri zinazofanywa na Jeshi la Polisi na kulibatiza majina mengine ya kejeli, kitu gani ambacho unakifanya wewe mpaka uone kwamba Jeshi la Polis linahitaji kubatizwa majina ya namna hii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi, siku mia tatu sitini na tano na robo hawana cha Jumamosi, hawana cha Jumapili, hawana cha Sikukuu, hawana cha mvua, hawana cha jua. Askari hawa wanafanya kazi kubwa halafu humu ndani anaibuka Mbunge anasema hata Askari kung’atwa na mbu hiyo ni kazi yao, ni majukumu yao na maneno hayo yanazungumza na mtu ambaye anaheshimika, Mheshimiwa ambaye ni Mchungaji na sisi waumini hatumwiti tu Mchungaji, tunamuita Baba Mchungaji, lakini anasema maneno ya namna hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wako watu hapa wanasema Jeshi la Polisi wanatumia lugha ambazo ni za kuudhi, za kejeli, hazina staha. Nataka nikuhakikishie; wakati ule CAG aliposema Bunge hili ni dhaifu wapo baadhi ya Wabunge hapa walitetea kauli hizo ambazo ndizo za kejeli, kauli ambazo zinadhalilisha Bunge lakini leo Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Dodoma, Kamanda ambaye amefundishika, Kamanda ambaye anajua kutumia lugha za Kibunge anasema “ole wao watakaoandamana kesho, watapigwa na watachakaa” hiyo ni lugha ya kufundishwa Askari ambaye amefundishika, hiyo ndio lugha ya kipolisi”. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikuambie sisi Jeshi la Polisi tunazo lugha nyingi ambazo tukiongea hapa wengine hamtatuelewa. Kwa mfano, wewe unaitwa Mheshimiwa Zungu sisi Polisi tunakuita Zulu uniform Novemba uniform ndivyo tunavyokuita sisi, hawa hawatatuelewa. Tunaposema kwamba tunatumia lugha hizi, lugha hizi zinatokana na preemption model. Preemption model kwenye Jeshi maana yake nini, nifungue darasa kwa wale walioikosa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi linapoona kwamba kuna mambo ambayo yanataka kufanyika, mikusanyiko isiyoruhusiwa, Jeshi la Polisi tunajiandaa kwenye vifaa ndiyo maana mtaona askari wanamwaga mahali wanatembea kikakamavu, wanafanya hivi kuona kesho uandamane uone cha mtema kuni. Wakati mwingine tunatumia lugha hizi kwamba ole wake na wale tunaowaambia lugha hizi ni wale watakaokuwa wahalifu, hii ni lugha ya kushughulikia wahalifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwa Mheshimiwa Msigwa mara kwa mara namuona ananyanyua Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Niende kwenye hiyo hoja ya mikutano ili tumalizane na akina Mheshimiwa Msigwa na Mheshimiwa Ruth Mollel na wote wale ambao mmekuwa mkiuliza ni sheria gani inawanyima haki ya mikutano ya ndani, inawanyima haki ya mikutano ya hadhara na mnisikilize vizuri ili leo tumalizane hapa. (Makofi)

WABUNGE FULANI: Aaaaa.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais alipo apa kwenye Uwanja wa Taifa aliapa kuilinda, kuhifadhi na kuitetea Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mheshimiwa Rais anapokuwa analinda na kuitetea ni kuhakikisha yale yote yaliyoandikwa humu yanatekelezwa na hayavunjiwa na mtu yeyote na yeye kama Mkuu wa Nchi anasimamia hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 20(1) unayoinua inasema hivi: “Kila mtu anao uhuru wa kukutana na watu wengine kwa hiari yake na kwa amani, kuchanganyika, kushirikiana na watu wengine na kwa ajili hiyo kutoa mawazo yake hadharani na kuanzisha na kujiunga na vyama au mashirika yaliyoanzishwa kwa madhumuni ya kuhifadhi au kuendeleza imani au maslahi yake au maslahi mengineyo”. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 20(3) inasema hivi: “Bunge laweza kutunga sheria inayoweka masharti yatakayohakikisha kuwa vyama vya siasa vinazingatia mipaka na vigezo vilivyowekwa na masharti ya ibara ndogo ya (2) kuhusu uhuru na haki ya watu kushirikiana na kujumuika.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 30 ya Katiba inaweka masharti ya mipaka na inasema hivi: “Ifahamike kwamba masharti yaliyomo katika sehemu hii ya Katiba hii, yanayofafanua misingi ya haki, uhuru na wajibu wa binadamu, hayaharamishi, naomba nirudie, hayaramishi sheria yoyote iliyotungwa wala kuzuia sheria yoyote kutungwa au jambo lolote halali kufanywa kwa mujibu wa sheria hiyo kwa ajili ya-

(a) Kuhakikisha kwamba haki na uhuru wa watu wengine au maslahi ya umma haviathiriwi na matumizi mabaya na uhuru na haki za watu binafsi. (Makofi/ Vigelegele)

(b) Kuhakikisha ulinzi, usalama wa jamii, amani katika jamii, maadili ya jamii, afya ya jamii, mipango ya maendeleo mijini na vijijini haviathiriwi”. (Makofi)

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati umefika sasa, Mheshimiwa Rais alipopiga marufuku mikutano hii ni kwa mujibu wa Katiba hii kwenye vifungu nilivyovieleza kwa maana kwamba mikutano hii…

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Order, order.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Sikiliza basi Mheshimiwa Msigwa.

MWENYEKITI: Order, order.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana kwamba mikutano hii isije ikavuruga mipango ya maendele, nimesoma Ibara hii.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Msigwa Mbunge ukitaka kuongea unafuata utaratibu.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Heche.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri hebu ngoja kwanza. Waheshimiwa Wabunge, kama Serikali inajibu watu wote tukae kimya.

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Hapana, ndiyo muda wake wa kujibu.

MBUNGE FULANI: Anadanganya.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri, anajibu ndiyo muda wake, sasa mnapoanza ku-provoke, mnakifanya Kiti kianze kuwa…

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Endelea Mheshimiwa.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye Sheria ya Vyama vya Siasa, kifungu cha 11(1) kinasema hivi: “Kila chama chenye usajili wa muda na usajili wa kudumu kitakuwa na hadhi ya-

(a) Kufanya mikutano katika sehemu yoyote ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania baada ya kutoa taarifa kwa Afisa Msimamizi wa Polisi wa eneo husika kwa ajili ya kujitangaza kwa umma na kutafuta wanachama. (Makofi)

(b) Kupata ulinzi kwa ajili ya usalama wa mikutano ingawa vyama vyenye usajili wa muda havitaruhusiwa kuweka mgombea au kufanya kampeni katika uchaguzi wowote wa Ubunge, Uwakilishi au Urais au Uchaguzi wa Serikali za Mitaa”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu cha (2) kinasema: “Bila kuathiri sheria nyingine, vifungu 43, 44, 45 na 46 vya Sheria ya Jeshi la Polisi na Polisi Wasaidizi, Sura ya 322 vitatumika katika mikutano yote itakayofanyika ndani ya Jamhuri ya Muungano na chama chochote hata kama kina usajili wa kudumu au usajili wa muda”.

MBUNGE FULANI: Vifungu hivyo vinahusu ulinzi.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu cha (3) kinasema: “Kila chama chenye usajili wa kudumu kitakuwa na hadhi ya kuweka mgombea na pia kufanya kampeni kwa ajili ya mgombea yeyote katika uchaguzi wa Wabunge, wawakilishi wa Urais au uchaguzi wa Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu cha (4), Mheshimiwa Ruth Mollel sasa unisikilize vizuri ili uone ni sheria gani tunatumia ya kuzuia mikutano yako ya ndani. Kifungu cha (4) kinasema: “Pale ambapo chama cha siasa kinapokuwa na nia ya kufanya mikutano au maandamano katika eneo lolote la wazi, hiyo ndiyo ya hadhara, au sehemu yoyote, maana yake sehemu ya ndani au wapi, kinatakiwa kutoa taarifa si chini ya saa 48 kabla mkutano husika kufanyika. Taarifa hiyo ni lazima iwe kwa maandishi itakayowalishwa kwa Afisa wa Polisi Msimamizi wa eneo husika ambapo mkutano husika unatarajiwa kufanyika. Ikitokea chama cha siasa kimewasilisha taarifa kulingana na kifungu kidogo cha (4) chama hicho kinaweza kuendelea na mkutano kama ulivyopangwa isipokuwa kitakapopokea amri kutoka kwa Afisa wa Polisi Msimamizi wa eneo husika kutoendelea na mkutano husika, mkutano huo hautafanyika”. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zuio hili ambalo linahusisha Sheria ya Vyama vya Siasa limeenda kutafsiriwa kwenye Sheria ya Jeshi la Polisi. Sheria ya Jeshi la Polisi, kifungu cha 42 kinasema hivi: “Mtu yeyote atakayekaidi amri au kudharau au kutekeleza amri iliyotolewa katika kifungu kidogo cha (1) hapo juu atakuwa ametenda kosa na atakamatwa bila hati ya ukamataji na endapo atatiwa hatiani anaweza kuuhukumiwa kulipa faini au vifungo au vyote”. (Makofi)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kinaendelea kusema: “Pale ambapo mtu atawalisha taarifa ya maandishi kama ilivyoelezwa kwenye kifungu kidogo cha (1) anaweza kuendelea kuandaa au kukusanya watu au kuandamana kama ilivyopangwa isipokuwa tu pale anapopokea amri kutoka kwa Afisa wa Polisi Msimamizi wa eneo husika juu ya kusanyiko hilo au maandamano kutofanyika kama ilivyoelekezwa.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilichotaka kuwaambia hawa Wapinzani ni nini? Tatizo la wenzetu hawa hawataki kutekeleza na kufuata Katiba. (Makofi)

WABUNGE FULANI: Aaaaa.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la wenzetu hawa hawataki kufuata sheria za Vyama vya Siasa na Jeshi la Polisi. Sasa mimi niwaambie, najua haya yote yanawasumbua kwa sababu mmekosa hewa ya oxygen upande mliopo. Ushauri wangu wa bure kwenye chama kingine cha siasa bado kuna oxygen ya kumwaga na kutosha, kama mnaona kufanya siasa huko hakuwezekani nendeni kwenye vyama vyenye oxygen. (Makofi)

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe maelekezo kwa Jeshi la Polisi na naamini IGP unanisikia kwamba vyama vyote vya siasa na najua uchaguzi unakuja Novemba, najua kuna watu wanaokaidi na kutotaka kuzingatia sheria na najua sikio la kufa halisikii dawa, endeleeni kuhakikisha kwamba mikutano isiyoruhusiwa ni kweli hairuhusiwi na wale watakaokaidi waendelee kukamatwa. (Makofi)

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila utaratibu)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye hoja za Mheshimiwa Msigwa, mimi nakuheshimu sana. Mambo mengi sana yamesemwa humu kuhusiana na watu kupotea, kuuwawa, kutekwa lakini Mheshimiwa Msigwa alienda mbali zaidi akawa ananitaka mimi Waziri kwa niaba ya Serikali nitoe majibu kuhusiana na upigwaji risasi wa Mheshimiwa Tundu Lissu, kutoonekana kwa kina Ben Saanane na wengine aliowataja. Maneno yote haya yanaletwa kwa sababu moja tu na sababu yenyewe ni kutaka Serikali na wananchi kuchonganishwa. (Makofi)

WABUNGE FULANI: Aaaa.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Serikali pale ambapo tunaona Mheshimiwa Mbunge anatoa maneno ambayo kila kukicha tunapotoa maelezo lakini hataki kusikia, anabaki na kazi moja tu. Kazi moja hiyo kwa sababu ni Mchungaji, ukisoma kwenye Kutoka 23:1 inasema: “Usivumishe habari za uongo; usitie mkono wako pamoja na mwovu, kuwa shahidi wa udhalimu”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu ambaye ni mchonganishi ana shetani ndani yake. Biblia inasema mtu ambaye ni mchonganishi anakuwa ni mmiliki halali wa ibilisi shetani. Biblia inasema mtu ambaye ni mchonganishi anakuwa ni mtumwa wa shetani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo naomba Bunge hili mnisikilize vizuri, nimekuwa nikieleza hapa nyakati mbalimbali kwamba taarifa zote za watu kupotea, kutekwa, kuuwawa, ambazo zimeripotiwa kwenye vituo vya Polisi zote hizi zina mafaili na upelelezi unaendelea. Katika mazingira ambayo upelelezi unaendelea, sisi tuna Jeshi la Polisi lenye weledi na teknolojia katika kufuatilia uhalifu ambao umetokea wa watu niliowataja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulaumu Jeshi la Polisi na kutaka kuonesha kidole kwamba matukio hayo yanafanywa na Serikali, sisi kama Serikali hatutakubali. Ziko nchi nyingi ambazo wananchi wake tena wengine maarufu wamepotea, wameuwawa lakini mpaka leo waliofanya matukio hayo hawajapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano, nchi ya Marekani ambayo ina FBI, Central Intelligence Agency pamoja na taasisi nyingine 24 za Serikali kwa ajili ya usalama kuanzia mwaka 1947, miaka zaidi ya 72 alikufa pale Elizabeth Short aliyekuwa anataka kujiunga na Hollywood kwa ajili ya movie, mpaka leo pamoja na vyombo vyote hivyo wanaendelea kuchunguza, hawajampata aliyehusika na tukio hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Marekani hapo hapo, kuna mwanamuziki Tupac Shakur, leo ni miaka 23 wanaendelea kuchunguza lakini hawajampata nani amefanya tukio hilo. (Makofi)

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, leo sisi Tanzania ambao tunaendelea na uchunguzi pale ambapo hatujapata mtuhumiwa aliyefanya tukio, kwa nini baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wanaonesha kidole kwa Serikali? Hii yote wanafanya kwa sababu ya kuchonganisha Serikali na wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niseme bayana matukio mengine kama nilivyowahi kusema upelelezi unachukua siku nyingi na sisi Jeshi la Polisi tunashindwa kuunganisha dot za upelelezi kwa sababu baadhi ya wahusika hawataki kutoa ushirikiano. Umezungumzia kesi ya Mheshimiwa Tundu Lissu, Mheshimiwa Msigwa nilikilize vizuri, unataka kusikia Serikali inasema nini kuhusu nani aliyempiga risasi Mheshimiwa Tundu Lissu, nataka nilihakikishie Bunge lako Tukufu baada ya tukio hili kutokea Polisi tulianza uchunguzi na hata kabla hatujaanza uchunguzi Madaktari wa Serikali kwa nia njema ya kunusuru uhai wa Mheshimiwa Tundu Lissu walikuwa mstari wa mbele kabisa na baada ya hapo kupitia Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Dodoma alimtaka dereva aliyekuwa na Mheshimiwa Tundu Lissu aje kwenye kituo cha Polisi atoe maelezo. Polisi hawa sio Mungu, Polisi hawa wanahitaji binadamu ambaye alikuwa kwenye tukio aje atoe maelezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu wakati huo dereva wa Mheshimiwa Tundu Lissu kwa jina Adam amekimbia na hataki kuonekana kuja kutoa maelezo kwenye kituo cha Polisi. Sasa sisi Jeshi la Polisi huwa tunaangalia na mazingira yanayozunguka tukio lililotokea. Kwa kuwa risasi zilizopigwa ni nyingi zaidi ya 38; na kwa kuwa risasi hizo zilimpiga Mheshimiwa Tundu Lissu kutokea alikokuwa amekaa kuelekea upande alikokuwa dereva lakini dereva alitoka akiwa hana kovu hata ukucha wake kupigwa risasi.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hali hii inatia mashaka na ndiyo maana Jeshi la Polisi wanamtaka Adam aje atoe maelezo nini kilitokea. Pili kwenye gari mule walikuwa wawili tu dereva Adam na Mheshimiwa Tundu Lissu, yeye ni mtu muhimu sana wa kusaidia Jeshi la Polisi.

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Sisi Jeshi la Polisi tunakosa usaidizi…

WABUNGE FULANI: Mwongozo, mwongozo.

MWENYEKITI: Waheshimiwa wote mnaofanya fujo nawaona na nawa-note.

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Hapana, Serikali inajibu na kama mtu ana hoja baadaye atatoa siyo sababu ya kufanya fujo ndani ya Bunge.

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Unapomkatisha Waziri unakifanya Kiti kichukue hatua za Kikanuni. Nimekuona hapo Mheshimiwa. Endelea Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Wewe Mheshimiwa Heche tulia, hizi ajali gani kuanzia Chacha Wangwe dereva anatoka mzima, anakuja Mheshimiwa Tundu Lissu anatoka mzima halafu tusiseme?

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

WABUNGE FULANI: Kakae huko.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri, endelea.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo…

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Toa dozi, toa dozi Mheshimiwa Kangi.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo baadhi ya watu wamekuwa wakitaka Jeshi la Polisi litumie sheria inayoitwa Mutual Assistance on Criminal Matters kwamba tunaweza tukam-summon mtu yeyote ambaye yuko nje ya nchi akaja akatoa ushahidi. Hata hivyo, katika kesi hii matumizi ya sheria hii yangelenga kwa mtu ambaye anajificha asiweze kuja kwa hiari yake, kwa hiyo, tunatumia vyombo na nchi nyingine kumlazimisha huyo mtu aje lakini kwa dereva wa Mheshimiwa Tundu Lissu na Mheshimiwa Tundu Lissu wenyewe wanatakiwa waje kwa hiari yao na hivyo hatulazimiki kutumia sheria ya namna hiyo. Kwa hiyo, katika mazingira ambayo Mheshimiwa Tundu Lissu ametekeleza kesi yake, katika mazingira ambayo Adam hatakuja kutoa ushahidi, isitokee tena Jeshi la Polisi kulaumiwa katika mazingira ya namna hii.

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye eneo lingine, niende kwenye ufisadi ambao umeelekezwa kwenye Jeshi la Polisi. Wako Waheshimiwa Wabunge hapa wameelezea kuwepo kwa ufisadi ndani ya Jeshi la Polisi lakini taarifa za ufisadi huu wamezipata kwenye Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Serikali na kama Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi tunahakikisha kabisa kwamba hakuna chombo chochote cha ulinzi na usalama ambacho kitakuwa na matumizi mabaya ya fedha, kitafanya ufisadi na ndiyo maana pale ambapo tunabaini kwamba ufisadi umefanyika tumekuwa tukichukua hatua ikiwa ni pamoja na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria ambao wanahusika na ufisadi huu. Ufisadi mwingine ambao umetajwa kwenye taarifa ya CAG lazima niwe bayana CAG pamoja na mambo mengine amelihusisha Jeshi la Polisi na kashfa ya sare hewa na kwamba sare hewa hizi ni za shilingi bilioni 16.6.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima na taadhima, kwa moyo mkunjufu, kwa mikono yangu myeupe nikiwa kama Waziri makini, nikiwa kama Waziri ambaye ninaitakia mema nchi hii, nikiwa kama Waziri ambaye ninatetea rasilimali za Watanzania na tumuogope Mungu, sijawahi kuona mtu muongo kama CAG katika nchi ya Tanzania. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani sare zinazodaiwa kuwa hewa mimi Waziri ambaye nimekwenda kwenye ma-container na ma-godown ya Jeshi la Polisi. Ambapo nimekuta sare nyingi ambazo zimeletwa halafu CAG anapeleka taarifa kwa Mheshimiwa Rais ya uwongo kwamba, hakuna sare za Jeshi la Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nanyanyua mikono juu, itakapofika jioni kama mimi nasema uwongo kwamba, hakuna sare hewa, kama nasema uwongo najivua nguo. Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama tukiwa tumeambatana na maafisa wa CAG twende main store akaangalie ma-container zaidi ya 15 yenye futi 40, ma- godown matano ambayo yamesheheni sare za vitambaa, viatu, kofia na mikanda, halafu CAG anapeleka taarifa mbele ya Rais kwamba, Jeshi la Polisi wamepokea sare hewa na kulipa shilingi bilioni 16.6 na ninaweka uwaziri wangu rehani kama nasema uwongo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumuogope Mungu. Na kama tutaendelea kuwa na mtu anayefanya ukaguzi halafu anaenda anasema uwongo kwamba, kule kuna sare hewa, huyo mtu tumuogope kama ukoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilianza kuwa na wasiwasi inakuwaje Jeshi la Polisi liwe na Sare hewa? Sare ambazo nimeziona kwa macho yangu mimi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumuogope Mungu, sare hizo zipo, hakuna hewa…

MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu Utaratibu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Heche kaa chini, mda wetu mdogo.

MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kanuni.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Heche kaa chini.

MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kanuni na Katiba zinavunjwa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Heche utaratibu maamuzi yote ni ya Kiti. Kaa chini.

MBUNGE FULANI: Aaah!

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, liligusiwa pia, suala la Lugumi. Kwamba, suala la Lugumi lilianza nikalichukua, sasa limeishia wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nilitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba, baada ya kubaini kwamba, chombo kingine cha Serikali (TAKUKURU) kwamba, wameanzisha uchunguzi na wakati ule nilikuwa tayari nimeshamuita Lugumi kwa ajili ya kuchukua hatua, suala hilo nililiacha mikononi mwa TAKUKURU, ili waendeleenalo na pale ambapo watakuwa wamelimaliza, jambo hilo litawekwa hadharani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwathibitshie kwamba, wale wote waliokuwa wamekwapua fedha za NIDA. Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi tuliweza kuyaita makampuni tukanusuru fedha aslimia 84 ya fedha ambazo zilikuwa zimekwapuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ziko hoja mbalimbali pia za Wabunge ambazo ni vema nikazigusia, hasa Vitambulisho vya Taifa:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema jana wakati umeelekeza mwongozo wa Mheshimiwa Felister Bura kwamba, kutakuwa na usajili wa simu na watanzania wanayo hofu. Napenda niendelee kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba, usajili wa Vitambulisho vya Taifa tunaendelea vizuri na ni lengo letu itakapofika Disemba mwaka huu malengo yetu ya kufikia milioni 24 ya Watanzania tutakuwa tumefikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ndio maana nikasema kwa kuwa mpaka sasa tumekwishafikia katika kusajili na kuweza kuandaa namba ya utambulisho wa Taifa, tumefika milioni 16 ambapo Watanzania milioni 16 wana uwezo wa kwenda kusajili simu zao kwa mujibu wa masharti ya TCRA. Wale ambao hawataangukia kwenye hiyo milioni 16 sisi kama Serikali tumesema kwamba, si makosa ya wanaomiliki simu, tutaweka utaratibu maalum wa kuhakikisha kwamba, hakuna Mtanzania ambaye simu yake itakapofika Disemba itazimwa kwa sababu hajawa na namba ya utambulisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jingine ambalo ni vema nikagusia, Naibu Waziri amezungumzia masuala ya ujenzi wa vituo vya Polisi, makazi ya askari kwenye Jeshi la Polisi:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ninavyozungumza tayari tumekwishaanzisha The Police Force Cooperation Soul, yaani hili ni shirika ndani ya Jeshi la Polisi. Tayari mkurugenzi mkuu tumemteuwa na wale wakurugenzi wa idara tumewateuwa, tayari wajumbe wa bodi tumewateuwa. Ni imani ya Wizara kwamba, watakwenda kukusanya fedha nyingi sana ambazo ni imani yetu kwamba, watakwenda kumaliza tatizo la makazi na vituo vya Polisi ndani ya Jeshi la Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kwenye Jeshi la Magereza. Kwenye Jeshi la Magereza pia nigusie kwamba, tunaendelea kuhakikisha kwamba, ule mfumo wa ujenzi wa nyumba bunifu wa kila gereza tunauendeleza vizuri, ili kila mwaka kila gereza tumeshalielekeza lazima liwe na nyumba zisizopungua tatu mahali ambapo kuna gereza ili kuhakikisha kwamba, askari wetu wanapata nyumba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Naibu Waziri amezungumzia stahiki mbalimbali za askari, posho:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahakikishie askari wote kwenye vyombo vya ulinzi na usalama, najua mnanisikiliza; la kwanza ambalo tumelifanya ni kuhakikisha kwamba, tunapitia sheria zote pamoja na kanuni zote, ili kubaini na kuorodhesha posho zote ambazo ni stahiki ya askari kwa sababu, kuna baadhi ya posho ambazo ziko kwenye kanuni au kwenye sheria, lakini askari hawajaanza kuzipata. Ni imani yangu kwamba, tutakapokuwa tumekamilisha zoezi hilo lazima tuhakikishe kwamba, askari wanapata hizi posho ambazo zipo kwa mujibu wa sheria na kwa mujibu wa kanuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, nijielekeze kwenye madeni ya wazabuni mbalimbali, Waheshimiwa Wabunge wengine kwa maandishi mmezungumza hapa:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahakikishie Serikali ya Dkt. John Pombe Magufuli inaendelea kulipa madeni ya wazabuni na watoa huduma. Na ndio maana wapo wazabuni kwenye vyombo hivi vya ulinzi na usalama tumeanza kuwalipa fedha. Wale ambao madeni yao yamekwishahakikiwa naomba waendelee kuamini kwamba, madeni yao yatakwenda kulipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye hoja ya Mkoa wa Kigoma na Mkoa wa Kagera, hususan kwenye suala la uhalifu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba, Mheshimiwa Waziri Mkuu alifanya ziara kwenye Mkoa wa Kigoma, alipofanya ziara kwenye Mkoa wa Kigoma, pamoja na mambo mengine na taarifa ya Ulinzi na Usama aliyoipata ni kweli kabisa kwamba, mazingira ya Mkoa wa Kigoma na sehemu ya Mkoa wa Kagera hali ya uhalifu wa kushtukiza na hasa wenye silaha za moto kutoka nchi jirani ya Rwanda au Burundi wamekuwa wakiingia. Na ni kweli kabisa tukiweza kufunga milango ya mipakani ni kweli tutapunguza uhalifu wa silaha ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba, tayari tumeanza kutekeleza agizo la Mheshimiwa Waziri Mkuu ambapo Jeshi la Polisi wanaendelea na mchakato wa kutathmini na kuangalia vigezo ambavyo vinasababisha maeneo gani ambayo yanaweza yakatengwa, halafu tukayatafutia mkoa maalum wa kipolisi au kanda maalum ya kipolisi. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge mnaotoka maeneo yale naomba muwe na amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie jambo lingine la wahamiaji haramu. Wahamiaji haramu Mheshimiwa Kitandula amegusia, Wataita pamoja na Wakamba maeneo ya Mkinga wana maingiliano na nchi ya Kenya na kwamba, kuna usumbufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge. Na ndio maana hata juzi Waheshimiwa Wabunge kutoka Kigoma mliweza kutusifia Immigration kwamba, sasa ile kero ya kutumia pua au kuimba wimbo wa Taifa kwamba, huyu ni Mrundi au sio Mrundi imeanza kupungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahakikishie Wabunge kwamba, tutaendelea kudhibiti mipaka na tutaendelea kupambana na uhamiaji haramu mpaka tutakapoutokomeza. Na ndio maana wahamiaji haramu wengine ambao tayari tumekwisha wakamata tunafanya mpango wa kuwarudisha makwao. Na ndio maana katika kuwarudisha makwao tumeendelea pia kupata taarifa za madalali au watu wengine Watanzania wenzetu ambao wanashiriki katika kuwatafutia usafiri ama kuwahifadhi, ili tuweze kuvunja mitandao hii ya uhamiaji haramu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie suala kwa ujumla la usalama barabarani ikiwa ni pamoja na kero ya bodaboda:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahakikishie na niwathibitishie Waheshimiwa Wabunge, kama kuna eneo ambalo sasa tunafanya vizuri ni kwenye kikosi cha usalama barabarani ndani ya jeshi la Polisi. Sasa hivi kikosi cha usalama barabarani zile rushwa zile ambazo zilikuwa zinatuhumiwa sasa zinaenda kwisha. Na ninyi Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi kwa sababu, wengine pia mlikuwa mkiombwa, lakini siku hizi hamusemi kwa maana hali inaendelea kuwa nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, ajali zimepungua kwa asilimia 38.7. Na kielelezo kwamba, tunafanya vizuri ni kupungua kwa ajali na hasa ambazo zilikuwa zinachukua vifo vya watu wengi ikiwa ni pamoja na watu kupata vilema, pamoja na uharibifu wa mali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ndio maana huko mbele tunakokwenda, hilo shirika la Polisi nililolisema litaenda mbele zaidi kuhakikisha kwamba, wanapata wawekezaji ambao wana fedha na sisi Serikali hatutoi hata senti tano kwa ajili ya kuanzisha vituo maalum vya ukaguzi wa magari katika nchi nzima. Tutakapokuwa tumemaliza hilo ni imani yangu kwamba, magari mabovu yote yatatoka barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bodaboda nimeshatoa maelekezo na hayo maelekezo ni vema nikayarudia. Ibara ya 4 ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi inazungumzia kwamba, Serikali zote mbili zitatumia nguvu zake zote kuhakikisha kwamba changamoto kubwa nne zinafanyiwa kazi. Changamoto ya kwanza ni kuondoa umasikini. Changamoto ya pili ni kutatua tatizo la ajira hasa kwa vijana na changamoto ya tatu ni vita dhidi ya rushwa na ubadhirifu wa mali na ya nne ya mwisho ni kuendelea kudumisha amani, usalama, utulivu na kulinda maisha ya watu na mali zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bodaboda ni eneo ambalo wamejitokeza kama kujiajiri na hawa ni vijana wanajiajiri. Nimetoa maelekezo kwa Jeshi la Polisi kwamba, bodaboda hawa kwanza lazima wafuate sheria za usalama barabarani kama chombo kingine chochote ambacho kiko barabarani. Hawaruhusiwi kubeba mshikaki, hawaruhusiwi kutokuwa na leseni, hawaruhusiwi kutovaa kofia lazima wavae, lazima waende speed inayotakiwa, sheria zote na watengeneze bodaboda zao. Lakini tumepiga marufuku namna walivyokuwa wanakamatwa na nikaelekeza kwamba, bodaboda za aina tatu tu ndizo zitakazokamatwa na kupelekwa kwenye kituo cha Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kundi la kwanza la bodaboda ni bodaboda ambayo imehusika kwenye uhalifu. Bodaboda ya pili ni iliyohusika kwenye ajali na bodaboda ya tatu ni ile ambayo ni ya kuokota, haina mwenyewe. Bodaboda ambazo haziko kwenye makundi hayo zisikamatwe na kupelekwa kituoni, tunachofanya ni nini, na nimetoa maelekezo; pale ambapo Askari wa Usalama Barabarani hakumuonya, akaamua kumpiga fine, atampiga fine na yeye atakwenda atafute fine yake kwa muda wa siku saba sawa na wenye magari. Na atakaposhindwa ndani ya siku saba nimeelekeza namna ya kuwapata hawa bodaboda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimewaambia kwa kuwa Sheria ya Jeshi la Polisi na Polisi Wasaidizi Sura ya 322 inawataka pia, halmashauri wawe na hawa Polisi auxiliary. Ma-DTO wote nchi nzima washirikiane na wakurugenzi wa halmashauri zote nchi nzima. Hizi halmashauri zina viongozi kuanzia vitongoji, vijiji na kwa mijini kwenye mitaa yote, kila bodaboda hapa nchini lazima aisajili kwa kiongozi wake mahali anapoishi. Atasajili namba ya bodaboda yake, jina la dereva au mmiliki wa bodaboda, baadaye orodha zile zitakusanywa ndani ya ile halmashauri, mkurugenzi ataingiza kwenye database halafu atazalisha database ile ataipeleka kwa DTO, yani Mkuu wa Traffic katika wilaya ile. Na asubuhi askari wa usalama barabarani watakapokuwa wanaenda kazini mojawapo ya kitendea kazi ni orodha ya bodaboda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, bodaboda atakapokuwa ametenda kosa ataangalia namba, akiangalia kwenye orodha yake bodaboda haipo atajua huyu hajasajiliwa mahali kwa hiyo, hilo nalo tutadhibiti wizi wa bodaboda. Na bodaboda hiyo ambayo haijasajiliwa lazima atoe maelezo na ile ambayo ataikuta kwenye orodha ata-indicate kwamba wewe tarehe fulani unatakiwa uwe umelipa fine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mtindo huo katika nchi yote ya Tanzania hakuna bodaboda atakayetuchenga na hatutahangaika na bodaboda kwa sababu tutakuwa tunajua mahali walipo na namna ambavyo tunaweza tukawasaidia kwa sababu, lengo sio kuwasumbua bodaboda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwa wafanyabisahara ndogondogo, almaarufu mamantilie au mamalishe. Vijana wanachoma chips wanakaanga chips:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na sintofahamu wakati mwingine, Ilani hii inasema waondoe umasikini; sasa kama mamantilie anasumbuliwa biashara zake, babalishe anasumbuliwa biashara zake. Lazima Jeshi la Polisi mahali walipo watafute namna bora ya kuwalea hawa wafanyabiashara ndogondogo. Na pale ambapo wanajihusisha na makosa ya kipolisi ya kijinai, waweze kuwaelekeza namna bora ya kuendesha biashara yao na sio kila wakati kuwafunga mashati halafu wanashindwa kufanya biashara zao watu masikini hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la kusisitiza kesi za kubambikiza pamoja na dhamana. Wamesema Waheshimiwa Wabunge hapa kwamba, kweli kwenye magereza zetu hapa nchini kuna baadhi ya kesi ndogondogo ambazo watu wako mahabusu kule magereza au kesi ndogondogo mtu amefungwa yuko kule magereza:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliarifu Bunge lako Tukufu tumeishakubaliana na Waziri wa Katiba na Sheria namna ambavyo tutakwenda kutumia hizi Mobile Courts, namna ambavyo ushauri uliotolewa na Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, ya kuhakikisha kwamba, tunatengeneza kamati za kutembelea magereza kila wakati kwenda kuwabaini wale ambao kwa kweli wako kule, lakini hakuna sababu za msingi kuendelea kulundikana kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na nimuombe Mheshimiwa Esther Matiko katika hili wewe ni shuhuda mzuri, kuna watu walikuwa wanasema msongamano magerezani wengine wanatoka na ukurutu, wengine wanatoka na vifua, lakini tumeshuhudia Mheshimiwa Esther Matiko na Mheshimiwa Mbowe wametoka kule wako vizuri tu kwa hiyo, magereza yetu wanakula vizuri na wanalala vizuri na wanatoka wakiwa na afya njema kama mnavyomuona Mheshimiwa Esther Matiko anavyong’ara. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala alilolisema Mheshimiwa Esther Matiko. Mheshimiwa Esther Matiko mpaka sasa bado mimi Waziri haijaniingia akilini kwamba, kwenye kituo cha Polisi na ukavitaja baadhi ya vituo vya Polisi kwamba, wako Polisi wetu ambao wanalawiti watuhumiwa kinyume na maumbile, watuhumiwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hilo kama kweli litakuwa na ushahidi kwa sababu, kuna mambo yanaweza kufanyika, lakini yakiwa na ushahidi. Nimuombe Mheshimiwa Esther Matiko aligusia wakati anachangia kwamba, kuna RCO alienda magerezani pale kwa hiyo, niombe unisaidie jina la huyo RCO, ili tupate mahali pakuanzia, pengine tunaweza tukaona kwamba, jambo hili lilitokea kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wengi mmehitaji vituo kwenye maeneo yenu, mmehitaji magari au pikipiki akiwemo na ndugu yangu Mheshimiwa Suzan Kiwanga, Mbunge wa Mlimba. Changamoto ya Mlimba pale naifahamu. Nawaomba Waheshimiwa Wabunge na ndiyo maana nimekuwa nikiongea na Halmashauri zilizopo kule; Halmashauri za Wilaya, Miji, Manispaa na Majiji, kwamba sisi Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi tunapokuwa hapa Bungeni, tunagawana sungura mdogo huyu. Tunapomaliza kugawana, baadhi ya Wizara wanakwenda kule kwenye Halmashauri zao wanagawana sungura mwingine tena. Sisi Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi tunakosa fursa kama hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba Waheshimiwa Wabunge, ninyi ni Madiwani kwenye Halmashauri zetu. Nimezunguka, kuna baadhi ya Halmashauri kwa kweli wanatenga fedha. Kuna maeneo ambapo wananchi wameshaonyesha nguvu zao, yapo maboma; nawaomba kwenye hizo Halmashauri pia, vyombo hivi vya ulinzi na usalama na vyenyewe vinatoa huduma kama ambavyo darasa linatoa huduma. Kama ambavyo kwenye elimu mwalimu anahitaji nyumba; nasi Askari tunahitaji nyumba. Mahitaji ni yale yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa naomba Waheshimiwa Wabunge kwenye Halmashauri zenu mjaribu kushawishi, nami nitaendelea kuwasiliana na Waziri mwenzangu wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuone namna ambavyo tunaweza tukasaidia maeneo hayo. Mheshimiwa Suzan Kiwanga ahadi yangu ya kuja Mlimba bado iko pale pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Mkuchika, masuala yanayohusu mishahara, maslahi pamoja na vyeo, ametoa kauli ya Serikali hapa leo. Pia niwahakikishie Askari wote kwenye vyombo vyote vya ulinzi na usalama na katika hotuba yangu nimeeleza, nimeeleza…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Malizia Mheshimiwa Waziri, muda wako umekwisha.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeeleza kwamba Askari wapo ambao tumewapandisha vyeo hivi karibuni na wapo wale ambao mchakato wa kuwabaini na kuwapandisha vyeo unaendelea. Kwa hiyo, wafanye kazi bila kuchoka kwa sababu mchakato wa kuangalia maslahi ya vyeo unaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia, nataka niwahakikishie Watanzania na Bunge hili kwamba pamoja na kasoro ndogo ndogo ambazo zinajitokeza kwa baadhi ya askari, endeleeni kuliunga mkono Jeshi la Polisi na vyombo vingine vya usalama, wanafanya kazi kubwa. Hatuwezi kukata tamaa, na ndiyo maana wale wachache ambao wanataka kuharibu taswira ya Jeshi la Polisi, tumeonyesha kwenye hotuba yetu kwamba tumekuwa tukichukua hatua za kuwashusha vyeo na wengine kuwafukuza kwa aibu. Kwa hiyo, nasi hatuvumilii na kukaa na watu kama hao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana, kwa heshima na taadhima, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Muswada wa Sheria ya Upatikanaji wa Habari wa Mwaka 2016
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kukushukuru sana kunipa fursa ya kwanza kabisa kuchangia mjadala huu wa Watanzania kuwa na haki ya kupata taarifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Sheria mama, ndiyo ambayo msingi wa Mtanzania yeyote bila kujali cheo chake, hadhi yake, bila kujali kazi anayoifanya, anayo haki ya Kikatiba ya kupata taarifa. Pia upo msemo wa Kiingereza unaosema information is power. Ili Mtanzania aweze kuwa powerful katika sekta ya kilimo, katika kuzalisha, katika sekta ya uvuvi, katika sekta ya biashara, katika sekta ya utafiti, sekta ya elimu na sekta nyingine zote, lazima awe informed; lazima awe na taarifa mbalimbali zitakazomsaidia yeye katika shughuli ambazo anazifanya hasa shughuli za kimaisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuzungumzia uhusiano wa wakulima wangu kule Mwibara na wakulima wote nchini na namna ambavyo taarifa zinazohusu kilimo chao, uvuvi wao, ufugaji wao zinavyoweza kuwanufaisha katika maisha yao. Tunayo Taasisi ya Takwimu ya Taifa (Tanzania Bureau of Statistics), Idara hii kwa muda mrefu wamekuwa hawafanyi tafiti zinazohusiana na masuala ya kilimo, uvuvi, ufugaji ili kuweza kukusanya taarifa ambazo zinaweza zikawasaidia wakulima kule vijijni waweze kunufaika na kilimo, uvuvi na ufugaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nashauri kwamba badala ya kusema tu kwamba leo tunatunga sheria inayompa haki mwananchi ya kupata taarifa anayoitaka, pengine inahusu masoko au kilimo au ufugaji, sheria hii pia ingeweka wajibu kwenye hizi taasisi za umma zote ambazo zinapata fedha ili wawe na wajibu ikiwezekana on a monthly or quarterly basis wawe wanatoa taarifa muhimu kupitia vyombo mbalimbali vya habari, magazeti, redio, televisheni, ili wananchi waweze kuwa informed juu ya taarifa mbalimbali ambazo zinaweza zikawasaidia katika kilimo chao kuwa cha tija zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tukisema tu kwamba mwananchi leo ndio tunamtungia sheria ya yeye kupata habari, lakini taasisi hizi za umma ambazo zinapata fedha lakini hatuziwajibishi kuhakikisha kwamba wanajitokeza kwa wananchi na kuwapa taarifa mbalimbali, sheria hii na yenyewe inaweza isimsaidie mwananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye eneo lingine ambalo pengine kwenye taarifa ya Kamati walijaribu kuligusia na kwenye sheria yenyewe ya ule muda ambao mhusika wa kutoa taarifa kwa mwananchi anayohitaji, muda wa siku 30.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siku hizi naona ni nyingi, kwa sababu inategemea na taarifa ambayo huyu Mtanzania anaihitaji. Kunaweza kukawa na taarifa ambayo ni very urgent ambayo ingeweza kumsaidia, sasa kama huyu Afisa atajiona kwamba muda alionao ni mwingi anaweza akakaa tu matokeo yake kuja kumpa ile taarifa huyu mwananchi inakuwa imeshapitwa na wakati, anakuwa haihitaji tena. Kwa hiyo, inakuwa ni kama alikuwa anapoteza muda wake.
Kwa hiyo, naomba kwenye sheria hii tungeweka kipengele ambacho pia kinajaribu kuainisha categories za taarifa, ni taarifa gani ambayo inaweza ikachukua muda wa siku 30 au ni taarifa gani ambayo ni very urgent ambayo mwananchi huyu anaihitaji? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kuna siku moja nilikuwa nahitaji mkopo benki kwa ajili ya kumlipia ada mwanangu na vinginevyo hataweza kusoma, lakini kwa sababu benki wanasema wana siku 15 za ku-process mkopo, na mimi mkopo nilikuwa nauhitaji kwa muda usiozidi siku tano, lakini baada ya wao kuwa wamechukua muda mrefu, nikaenda kukopa kwa mtu binafsi akanipa hela. Baada ya siku 15 ndiyo wakaniambia mkopo wako uko tayari. Nikawaambia mkopo wenu umeshapitwa na wakati. Kipindi ambacho nilikuwa nauhitaji, sasa hivi hauna tija yoyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namuomba Mheshimiwa Waziri anayehusika ajaribu kuhakikisha kwamba tunaingiza aina za taarifa na tukazitengenezea schedule kwamba taarifa fulani ikiwa kwenye first schedule hii inaweza ikachukua siku fulani, taarifa ambayo ipo kwenye second schedule inaweza ikachukua siku fulani mpaka pengine na kwenye third schedule. Vinginevyo mwananchi atakuwa ametungiwa sheria ya kupata tu haki lakini katika zile siku ambazo mtumishi anajisikia ile taarifa isiweze kumsaidia sana mwananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye eneo lingine ambalo linahusu vyanzo vya taarifa. Ukumbuke hata sisi wanasiasa pia ni vyanzo vya taarifa. Sisi wanasiasa kama Wabunge, ni vyanzo pia vya taarifa. Kama Wabunge pia tunatumia fedha za umma kama taasisi, yaani Mbunge kama taasisi. Wananchi wanaweza kuwa wanahitaji taarifa kutoka kwa Mbunge ama kwenye Ofisi ya Mbunge au kwa Mbunge mwenyewe kupitia mkutano, wanahitaji taarifa ambayo wanaweza wakajua nini kinaendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wakati sisi Wabunge kama wanasiasa ambao ni vyanzo vya taarifa, utaratibu huu wa sisi Wabunge kuwekewa siku kumi za Jimboni kufanya mikutano, sisi kama wanasiasa ambao ni vyanzo vizuri vya taarifa, siku hizi zinakuwa ni kidogo sana kwa Mbunge kuweza kuzunguka Jimbo zima kwa muda wa siku kumi kwa ajili ya kuwapa taarifa wananchi. Kwa sababu haitakuwa rahisi; wananchi wanamwandikia Mbunge na wenyewe wana-request, Mbunge naye anaambiwa baada ya siku fulani kwa sababu ni taasisi ya umma na anatumia fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nashauri eneo hili pia tuliangalie vizuri. Mbunge kama chanzo cha taarifa; je, anaweza aka-deliver taarifa muhimu kwa wananchi kabla ya kusubiri wananchi wenyewe ndio wa-request kutoka kwa Mbunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye eneo la vyombo vya habari ambavyo ni taasisi binafsi, vingine ni vya Serikali na vyombo vya habari vingine vya Serikali vinapata fedha za umma, magazeti ya Serikali, Daily News, Habari Leo na magazeti mengine ya Uhuru; na sisi kama chama tunapata ruzuku ya Serikali; magazeti mengine ya Tanzania Daima ambayo nayo ni ya chama kingine wanapata ruzuku kuendesha magazeti haya…
MWENYEKITI: Mjadala uelekeze kwa kiti.
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Ndiyo Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mchungaji Msigwa anadhani anafukuza mapepo kwa mtu aliyepandwa na mapepo. Hatuko Kanisani hapa. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nazungumzia vyombo vya habari na nikawa najaribu tu kuvitolea mfano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi vyombo vya habari ambavyo vinapata fedha, najaribu kumshauri Mheshimiwa Waziri anayehusika kwamba vyombo hivi pia kuna haja ya kuviwekea wajibu, kwa kuwa ni vyombo vinavyopata fedha zikiwemo na televisheni za Serikali kama TBC ambazo zinapata fedha; kwamba wafike mahali wawajibike kutoa taarifa kwa wananchi, wawe ni wakulima, wawe ni wavuvi, kuhusu vipindi mbalimbali; kwa mfano zamani kulikuwa na kilimo cha kisasa, masuala ya masoko yako wapi, badala ya kuviacha vyombo hivi vikawa vinaweka Mabango ya Chereko, maharusi sijui vitu gani na vinatumia fedha za umma badala ya kurusha taarifa ambazo zinawahusu wananchi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata magazeti pia yasiachwe yakawa yanaandika habari nyingi ambazo zinahusu mambo ambayo hayawasaidii sana wananchi wanaposoma kuwa informed ili waweze kutumia taarifa hizi katika shughuli zao za uzalishaji. Wanakuwa na mambo mengi mno, hasa hasa ya siasa ndiyo wanaweka front page; leo akitokea mwanasiasa tu pale kaenda pale mfano Mheshimiwa Mrema, au kaenda pale sijui Mheshimiwa Mbowe, akisema tu jambo, utakuta magazeti haya ambayo ndiyo yanapata fedha za umma, front page yanaruka na vichwa vya habari juu ya hao watu; badala ya kuruka na taarifa zinazozungumzia kwamba mwananchi fulani kule Mwibara ameibiwa nyavu zake, majambazi wamepora mashine ili wananchi hawa taarifa hizi ziweze kufika kwa wanaohusika ili wazifuatilie na kuzifanyia kazi.
Sasa tukiacha hali hii ikaendelea bila sheria hii kuvibana vyombo hivi, matokeo yake vitakuwa ni vyombo vinavyotoa taarifa kwa wananchi ambazo haziwasaidii sana, ni vyombo vya kifedha zaidi kwamba wakiweka hii kwenye front page ndiyo wanaweza wakauza magazeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, vyombo vya habari kama redio na magazeti ni vyombo muhimu sana kwa wananchi na kuna redio nyingi siku hizi zinaanzishwa kule vijijini, Wilayani; sasa redio kama hizi inabidi Serikali izisaidie sana kwa sababu unakuta Redio ya Taifa au redio hizi nyingine binafsi ambazo wanarusha matangazo, matangazo haya hayafiki kule kwa wananchi.
Kwa hiyo, redio hizi ambazo wanawekeza kule Wilayani au vijijini, redio hizi wazisaidie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi juzi hapa niliona mlolongo wa orodha ya redio nyingi zimefungwa, zimeondolewa kwa kisingizo kwamba wengine hawalipi kodi, kwa kisingizio kwamba wengine wameenda kinyume na ethics za utangazaji. Sasa kitendo hiki kinawafanya wananchi wetu vijijini wanaotegemea vyombo hivi kutopata habari na matokeo yake watu wa mjini ndio ambao wanaweza waka-access kwenye hizi taarifa ambazo wao huzipata kupitia vyombo vya habari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namshauri sana Mheshimiwa Nape. Mimi nilikuwa shabiki sana wa redio hii inaitwa Magic FM ya akina Salum Mkambala sijui na watu gani wale wana sauti nzuri za bass zile. Sasa ghafla juzi juzi hapa nikaona umeweka gate valve pale. Mheshimiwa Waziri hebu vyombo hivi uvitazame vizuri, vyombo hivi vinatusaidia sana na wanapokuwa wanachambua taarifa zao wanasaidia sana Watanzania kuelewa, ni wachambuzi, wanachambua sana. Kwa hiyo, kama kunakuwa na hizi kasoro nyingine ndogo ndogo Mheshimiwa Nape, ni wa kuwapa maonyo. Siamini kama kuna maonyo ambayo Mheshimiwa Waziri ulishawapa hawa Magic FM, lakini ukawawekea tu gate valve.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kupitia Bunge hili, badala ya kuwafungia; ni wachambuzi wazuri sana kama kuna mahali waliteleza, Mheshimiwa Waziri ajaribu kuwafungulia pengine na kuwapa adhabu ya onyo badala ya kuwafungia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru sana Serikali kwa kuja na muswada huu ambao ni mzuri sana ambao nafikiri kwamba haya mapendekezo yaliyotolewa na Kamati yetu pamoja na michango ya Wabunge itaweza kuuboresha zaidi na hatimaye tuwe na sheria nzuri sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye lile eneo ambalo pengine wanazungumzia taarifa za kiusalama, nitoe mfano kwenye Jeshi la Polisi. Mwananchi anaweza kuwa amekamtwa yuko ndani, lakini ndugu zake wanakwenda kituoni kufuatilia kujua tu angalau huyu mtu kwa nini amewekwa ndani na sababu ni ipi? Hata hiyo yenyewe wanaweza wakasema kwamba ni nani wewe tukupe taarifa ya huyu ndugu yako kuwa humu ndani? Kwa hiyo, tuangalie taarifa hizi mnazosema za kiusalama, msije mkadhani kwa kuwa Jeshi la Polisi ni suala la usalama, basi hata mtu kupata taarifa ya kwa nini ndugu yake yuko ndani na yenyewe…
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali wa Mwaka 2016
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kunipa nafasi na mimi kuchangia miswada miwili iliyowasilishwa leo asubuhi. Lakini mimi kwa sababu ya muda ntajikita kwenye Muswada wa Sheria ya Kuanzisha Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali. Kama ntapata muda nitaingia kwenye professional ya hawa wakemia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa niishukuru Wizara, Mheshimiwa Waziri Ummy Mwalimu na Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Hamisi Kigwangalla kwa kuona umuhimu na haja ya kuharakisha muswada huu muhimu na kuuleta mbele ya Bunge lako Tukufu.
Lakini pia nimshukuru sana in-charge ambaye ni Mkemia Mkuu wa Serikali na watumishi walio chini yake ambao wamesukuma muswada huu, kwa sababu kwa miaka mingi wamefanya kazi katika mazingira magumu, mazingira ya kudakiadakia sheria nyingine zilizopo halafu wanafanya shughuli zao. Na ndiyo maana kwa mazingira magumu hayo hata vyombo vingine vilivyopo kama Jeshi la Polisi waliokuwa wanamtegemea wanapopeleka sampuli wamepata shida sana, na katika kupata shida hiyo magereza yetu yamekumbwa na wimbi kubwa la msongamano wa mahabusu. Wengine wana kesi za mauaji wana miaka kumi, wengine wana kesi za robbery wana miaka kumi; tatizo ni kwa sababu bado uchunguzi kwa Mkemia Mkuu wa Serikali haujakamilika. Kwa hiyo mimi nipongeze jambo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na mazuri yote hayo ninayo mambo ambayo ningependa kuboresha muswada huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nianze na changamoto iliyopo kwenye jina la muswada wenyewe, kwamba ni wa Kuanzisha Mamlaka ya Maabara za Serikali. Sasa jina hili linanifanya nikumbuke kwamba majukumu yaliyoainishwa katika kifungu cha tano, majukumu ambayo yatakuwa ya mamlaka hii hayaendani au hayaendi sambamba na jina ambalo liko kwenye muswada huu. Kwa nini nimesema hivyo, kama hivyo ndivyo kwamba ni Mamlaka ya Maabara za Serikali, mamlaka maana yake ni chombo ambacho kinavisimamia vyombo vingine ambavyo ndivyo vinatenda, kwamba Serikali inazo maabara zake mbalimbali lakini lazima kuwe na chombo chenye mamlaka kwa ajili ya kusimamia vyombo hivyo, na ndiyo maana wana-set standards za vyombo hivyo; standards za wataalamu, standards za vifaa ili waweze kuvifikia kwa ajili ya kuleta ufanisi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa sisi ambao ni waumini kuna kitu kinaitwa Mungu Baba, Mungu Mwana, Mungu Roho Mtakatifu. Ukiangalia kifungu cha tano kinasema mamlaka itakuwa maabara ya rufaa. Inakuaje mamlaka hiyo hiyo tena ndiyo iwe maabara, kwa maana kwamba mamlaka ni chombo kinachosimamia maabara chenyewe hicho hicho tena ndicho kina-operate? Kwa hiyo, tayari kunakuwa na conflict of interest, jambo ambalo litaleta ugumu sana katika kutekeleza sheria hizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo lazima tukubaliane, ama tunatunga Sheria ya Government Chemist au tunatunga Sheria ya Authority (ya mamlaka). Na ndiyo maana hata juzi tulipitisha sheria hapa ma-valuer, ma-valuer hawa wamo mpaka ma-valuer binafsi ambao wanasimamiwa na chombo ambacho tulikipitisha hapa juzi. Sasa mimi nadhani kwamba Wizara ingekuwa na upana zaidi kwa sababu kutakuwa na maabara za watu wengine ambao wangeweza kutaka ku-invest kwenye masuala ya hizi maabara, sasa itakuwa ni shida sana kuwa accommodated chini ya sheria kama hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tuna chombo kinaitwa TCRA. TCRA hawawezi wakawa na kampuni ya simu; sisi tuna chombo kinaitwa EWURA, EWURA hao hao hawawezi wakawa na kituo cha mafuta; sisi tuna chombo kinaitwa TCAA (usafiri wa anga) haohao hawawezi wakamiliki ndege waka-operate; tuna TIA (Mamlaka ya Viwanja vya Ndege), haohao hawawezi na wao wakasajili, wakaandikisha viwanja vya watu wengine. Kwa hiyo, lazima mamlaka hii iwe ni mamlaka ambayo ni independent. Na inapokuwa independent tunaipa majukumu ya kumsimamia Chief Government Chemist, kulisimamia Jeshi la Polisi ambalo nalo lina maabara zake maana yake Jeshi la Polisi nao wana DNA, wana forensic pale, awasimamie, pamoja na maabara nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, na ndiyo maana mimi sijawahi kuona rufaa ya maabara, maabara inakuwa na rufaa sijawahi kuiona. Tukiruhusu maabara kuwa na rufaa hatutakuwa na ufanisi kwenye maabara yoyote. Na ndiyo maana mambo haya ni ya kisayansi. Inakuwaje uende kwenye zahanati ya Bunge kupima malaria unaambiwa negative, unaenda Benjamin Mkapa - UDOM unaambiwa una positive malaria, unaenda General Hospital unaambiwa huna, unakimbia Lacent unaambiwa unayo, kwa kutumia kipimo hichohicho cha darubini, jambo ambalo haliwezekani. Kwa hiyo, tunachotafuta hapa ni kwamba kama tuna darubini iliyoko kwenye maabara zote, darubini hiyohiyo lazima iseme una malaria, lazima iseme huna malaria kwenye darubini zote.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa inakuaje wapeleke mtoto kumpima kama si wa Mheshimiwa Shabiby! Ah, samahani Mheshimiwa Shabiby. (Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama sio mtoto wake wanabishania wanampeleka kwenye DNA ya Polisi halafu baadaye Mheshimiwa huyu analalamika anasema aah, kumbe maana yake kwa sababu tumetunga sheria hii inaonesha kuwepo maabara ya rufaa wanaenda kwenye maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali. Kufika pale DNA inasema huyu mtoto sio wa Mheshimiwa Shabiby, tutaleta machafuko makubwa sana katika nchi hii. Tutaleta machafuko kwa sababu kipimo fulani kinasema ni wa kwako, sikuridhika nikakata rufaa kumbe kuna kingine cha kukata rufaa kinasema huyu sio wa kwako hivi kweli hao watu wataishi katika mazingira gani?
Mheshimiwa Naibu Spika, maana yake lile tatizo huo mgogoro hautaisha kwa sababu kila mmoja anaamini mbona mimi mahali fulani niliambiwa ni wa kwako, na huyu anasema mbona mimi mahali fulani nimeambiwa sio wa kwangu. Lazima tuwe na standards. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, maabara hizi zote ambazo ni za Serikali, ni za wadau hawa ni labaoratory operators. Kwa hiyo, kutegemea na pale sampuli itakapopelekwa maana yake matokeo ya uchunguzi yaliyopo pale ndiyo matokeo kwa sababu mamlaka inayosimamia maabara hizi imejihakikishia kwamba pale kuna wataalam kutokana na standards tulizoweka, pale kuna DNA machine ambayo tumeweka standards, kwa hiyo jambo hili litakuwa handled vizuri sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi lilikuwa na kitu kinaitwa modernization. Sasa kama Jeshi la Polisi tumesema liwe la kisasa lina maabara zake za DNA, za forensic, lakini leo humu Mheshimiwa Ummy Mwalimu kuna sheria mbalimbali ambazo unazitunga chini ya sheria hii, ambapo katika hotuba yako umesema kwamba sheria hii haitaleta mgongano, lakini kuna mgongano mkubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi kwa mujibu wa sheria zao wanayo database yao, wanayo masijala ya kumbukumbu ambapo wanatunza kumbukumbu za wahalifu, lakini kwenye sheria hii unasema wale laboratory operators wapeleke taarifa zao kwa Mkemka Mkuu wa Serikali, tayari sheria hizi zinaanza kugongana. Kuna sheria za ushahidi ambazo zinazungumzia expert opinion, huku nako unasema kuna mambo ya conclusive na finality. Mambo kama haya pia yatakwenda kuleta mgongano mkubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika nimemsikia mchangiaji mmoja, nadhani ni Mheshimiwa Susan Lyimo, anasema kuna polisi hapa kwenye bodi anakwenda kufanya nini. Polisi hawa ndio wanaohusika na upelelezi wa kesi za jinai katika nchi yetu, na mojawapo ya jukumu la msingi kwenye Jeshi la Polisi ni investigation, na ndiyo maana sasa katika investigation hii ya sayansi ya jinai pamoja na kemia lazima polisi hawa; na ndiyo sababu sheria imemuweka polisi ambaye ana cheo cha juu ambaye ni Inspekta anakwenda juu, ndio maana akienda katika ile Bodi ataleta connection nzuri sana kati ya Jeshi la Polisi ambacho ni chombo pia cha kisheria ambacho kinahusika na makosa ya jinai na wao pia wana maabara zao, kwa hiyo ni kiungo muhimu sana ndiyo maana umeona na watumishi wengine wako pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye hizi sampuli ambazo wanasema kwamba zitasimamiwa na Mkemia Mkuu wa Serikali. Jambo hili litakuwa ni gumu sana, lazima hizi maabara zote kuanzia hiyo ya Mkemia Mkuu wa Serikali na hizi nyingine ambazo zote zinatakiwa ziwe chini ya mamlaka moja katika kusajiliwa, lazima kila maabara ipewe uwezo wa kufanya managemet ya sampuli zake, management ya records zake ili mradi katika regulations ambazo wataziweka wanakuwa wame-set standards. Vinginevyo huyu ambaye ni Mkemia Mkuu wa Serikali ambapo kuna maeneo mengine anatoza fedha kwa maana anafanya biashara, yeye huyo huyo; kwanza anajisajili kwa sheria hii yeye huyo huyo, halafu kuna element ya kufuta wengine, sijui kama atajifuta yeye huyo huyo, ni jambo ambalo halitawezekana. Kwa hiyo, lazima tuziache hizi laboratories nyingine za Serikali ziweze ku-manage sampuli zao, waweze ku-manage na records zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, halafu kuna element ya mchunguzi kwenye definition. Kama sheria hii itapita jinsi ilivyo Jeshi la Polisi watapata taabu sana kwa sababu na wao ni wachunguzi, wana maabara zao, lakini kwenye sheria hii imejaribu kumuonesha kwamba yule ambaye atakuwa ni mchunguzi kwa mujibu wa sheria hii ni yule ambaye ameteuliwa au ametangazwa na Mheshimiwa Waziri wa sheria inayohusika ambayo ni Wizara ya Afya; lakini yule Police Officer ambaye yuko kwenye maabara ya polisi, yeye sasa atakosa hadhi ile hata mahakamani wanaweza wakam-question kwamba wewe unatoa hii expert opinion kama nani. Kwa hiyo, lazima sheria hii isije ikaenda ikafifisha upande wa Jeshi la Polisi halafu wakapata taabu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la professionals. Nishukuru sana kwamba sasa tunakwenda kutunga sheria ya professionals. Lakini professionals hawa kwa mujibu wa muswada huu uwajibikaji wao utakuwa wa shida sana kutokana na namna ambavyo Mheshimiwa Waziri anayehusika amekuwa na mamlaka makubwa sana juu ya watu hawa. Kwa hiyo, kule kwenye utumishi wao, kwenye utendaji wao itakuwa ni sekeseke, wengi watakuwa wanafukuzwa, wengi watakuwa wanafutwa kwa sababu sheria hii ambayo tumempa mamlaka watakuwa mahali pa kukimbilia inakuwa ni shida, mara baadaye wakakate rufaa mahakamani. Kwa hiyo mwisho wa siku, sheria hii badala ya kuwa rafiki itatuletea shida sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nilikuwa naomba pamoja na schedule of amendements ambazo nitaleta, Mheshimiwa Waziri ajaribu kulitafakari jambo hili, jambo hili ni muhimu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hii pia tunasema kwamba inatekelezwa Tanzania Bara, lakini sheria hii iko kwenye Wizara ambayo si ya Muungano, Wizara ya Afya. Sasa mimi nilikuwa najiuliza, Jeshi la Polisi ambalo linafanyakazi ndani ya mipaka ya Jamhuri ya Mungano wa Tanzania; Pemba, Unguja, Geita, Musoma pale Mwibara pale kote kule inakwenda kwa sababu ni Wizara ya Muungano. Lakini sheria hii ambayo tunaitunga leo msimamizi wake mkubwa ni Wizara isiyokuwa ya Muungano lazima kwa vyovyote vile nilivyosema kutatokea mgongano mkubwa sana kati ya hizi sheria ambazo chombo cha Jeshi la Polisi kinatumia ikiwemo ile nyingine ambayo mwenzetu amezungumzia, road traffic act, sheria ya ushahidi, Sheria ya Jeshi la Polisi; kwahiyo kutakuwa na shida sana.
Kwa hiyo nilikuwa namshauri Mheshimiwa Waziri yale maeneo yale ambayo kwa dhahiri yanahusu au kuonesha kwamba kutakuwa na migongano, maeneo hayo…
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa mabadiliko ambayo nimeyapendekeza na nitaleta schedule of amendments, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. KANGI A. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kutoa mchango wangu kwenye hotuba ya bajeti, ambayo iko mbele yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda pengine nianzie alipomalizia Mheshimiwa Shonza, amenikumbusha, hii hoja ya kwamba UKAWA wananyanyaswa vyuoni, ni bahati nzuri sana nimkumbushe Mheshimiwa Ally Saleh na Mheshimiwa James Mbatia, nikiwa pamoja na mimi, tulikuwa Chuo Kikuu, tukaonekana tunashiriki mambo ya siasa, tukashughulikiwa na Serikali, hatukuwa UKAWA. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, suala la Serikali kushughulika na wanafunzi kwenye vyuo, ni jambo linguine na suala la kushughulikia wanafunzi kivyama si sahihi kulihusisha na chuo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nishukuru sana hotuba nzuri ya Mheshimiwa Ndalichako.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti imekuja katika wakati ambao ni muafaka, wakati ambao tunataka kuzungumzia suala la elimu kwa Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na ukurasa wa 24 wa hotuba. Ukurasa wa 24 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri, imejaribu kutoa majibu, kwenye hoja ambayo Mheshimiwa Chumi aliiwasilisha Bungeni hapa kama hoja binafsi, juu ya wanafunzi 489 ambao wanaonekana kwamba hawana sifa za kudahiliwa kusoma kozi ya Ualimu wa Sayansi katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu Joseph.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimwambie ukweli Mheshimiwa Waziri na Waheshimiwa Wabunge naomba mnisikilize kwa makini, Wizara ya Elimu imekuwa na tatizo la kubomoa na kufumuafumua mifumo ya elimu katika Taifa letu. Mambo haya yanafanywa, kila Waziri anayekuja, anafumua mifumo iliyotengenezwa na Mawaziri wengine. Ni lini tutakuwa na mifumo ambayo inaheshimika? Ina maana kwamba, kwenye Wizara ya Elimu, hawa ambao ni Maprofesa wameshindwa kabisa kuja na mitaala, mifumo ambayo itatupeleka miaka mingi bila kufumuliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Uingereza tunasema kuna Cambridge, mpaka leo Cambridge haifi, hivi Tanzania tumeshindwa kuwa na Cambridge ya Watanzania; kila anapokuja Waziri anafumua mifumo ya elimu. Kwa nini nasema mifumo ya elimu inafumuliwa? Inaniuma sana baada ya kuwa na matatizo ya Walimu wa sayansi katika nchi yetu, tukaona kwamba kwa sababu wanafunzi wanapomaliza kidato cha nne, wanapokwenda kidato cha tano, wale ambao wanachukuliwa wamefaulu sayansi, wakimaliza forms six, hawataki kwenda kwenye kozi za Ualimu wa sayansi au kozi za Ualimu, wanaenda engineering, wanaenda kuchukua kozi zingine. matokeo yake shule zetu za Kata na shule za Serikali tumeshindwa kuwa na mikakati ya kuzalisha Walimu wa sayansi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuhakikishie tu hawa wanafunzi waliomaliza kidato cha nne, wale ambao wana credit nzuri kuanzia C, ndio wanaofaulu kwenda kidato cha tano, wale wanaobaki na alama za D, ndiyo wanaonekana wamefeli. Sasa kukawa na utaratibu, kwamba kwa nini kama wanafunzi wanakwepa kusoma Ualimu wa sayansi, kwa nini tusianzishe utaratibu maalum, ambao waliuita five years integrated bachelor degree program, ili mtaala huu, uweze kuwachukua wanafunzi wa kidato cha nne, ambao wana alama za D, waweze kusoma miaka mitano na siyo miaka mitatu. Katika kipindi cha miaka mitano wawalee, wawanoe, wawapike, iwe kama wamesoma certificate, diploma mpaka degree na wanakuwa wamechujwa hapa katikati, wale wanaofeli wanaondoka, kumaliza miaka mitano tunakuwa na Mwalimu tuliyemfundisha sayansi ili wafundishe shule zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake Mheshimiwa Waziri anakuja hapa anatuambia kwamba hawakustahili, hawana sifa, wakati wamekuwa na sifa ndani ya mtaala maalum ambao umewasilishwa na Chuo cha Mtakatifu Joseph; kuna nini hapa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, huko nyuma tulipokuwa na mahitaji ya Walimu, tulianzisha Walimu wa UPE na wenyewe hawakuwa na sifa, lakini tukawa-qualify na ndiyo wametufundisha sisi, nimefundishwa na Mwalimu wa UPE mimi. Vile viel tulipoona kuna mahitaji ya Walimu, tulianzisha programu miezi mitatu, kumfundisha Mwalimu, wakabatizwa jina la yeboyebo, sijui voda fasta, yote hiyo ilikuwa ni kwa sababu ya mahitaji ya Walimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tulipokuwa na mahitaji ya Walimu tulianzisha combination ambazo unasoma HG Education, PC Education, CB Education, yote hiyo ilikuwa ni kutatua matatizo ya Walimu. Sasa leo kupitia mtaala maalum mnawaita hawa watoto ni vihiyo haiwezekani, hawa siyo vihiyo. Mheshimiwa Ndalichako, kuniambia kwamba wengine walikuwa arts, kwa nini wameenda kusoma, kwenye arts wanasoma biology pamoja na mathematics masomo mawili hayo ni sayansi hata kama wako arts, wakienda kusoma masomo hayo wamesoma sayansi, leo unasema ni vihiyo; matokeo yake umewafukuza wanafunzi 489. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii haiwezekani, huu ni ukatili, unyama na kama umesema umemshirikisha Mheshimiwa Rais, umemshirikisha kwa kumpotosha. Umemweleza mambo ambayo si sahihi na ndiyo maana, Mheshimiwa Ndalichako anataka tucheze muziki anaotulazimisha kucheza sisi, haiwezekani!
Niliwahi kusema hapa kwamba, hatuwezi kukubali kuchezeshwa kama Joyce wowowo hapa. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Ndalichako wanafunzi hawa wamedahiliwa na TCU, wamepewa mikopo na Serikali, itakuwaje wawe wahanga, muwafukuze. Hatutakubali, utakapokuja kuhitimisha, tunataka majibu kwa nini wanafunzi hawa umewafukuza, lazima muwarejeshe hatuwezi kukubali, tumepoteza fedha za Serikali kwa sababu ya matatizo yenu huko TCU, matatizo yenu yasije yakatuletea uhanga kwa wanafunzi hawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye ada elekezi. Hii ada elekezi mnaelekeza kitu gani? Mkitaka shule za binafsi wapunguze ada, mkitaka shule za binafsi zife ni shule za Serikali kuwalipa Walimu vizuri, kuwa na madarasa, kuwa na nyumba za Walimu, kuweka msosi yaani chakula, hakuna mtu binafsi atakayepandisha ada na ninyi kama mtaendelea kuhakikisha mazingira haya hamyajengi kila mtu ana uchaguzi kupeleka mtoto Ulaya, kupeleka mtoto shule binafsi. Shule binafsi mmezirundikia kodi nyingi sana, mara wapake magari rangi, mara sijui wafanya nini, sasa watarudishaje hizo fedha mnazowaambia wapake rangi magari, kodi kede kede, tunakwenda wapi! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, CCM ni gari kubwa na Serikali yetu ya Awamu ya Tano ni gari kubwa tukiacha gari ku….
MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Kangi Lugola muda wako umemalizika.
MHE. KANGI A. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo mambo machache sana ya kuchangia kama ifuatavyo:
Kwanza kabisa ni wavuvi wamekuwa wakichomewa nyavu zao ambazo ni haramu, nyavu hizo zimeendelea kwa kiasi kikubwa kuzalishwa na viwanda na kusambazwa na wanafanya biashara kila kona hapa nchini. Kwa kuwa, hali hii inaendelea kuwafanya wavuvi kuwa maskini, wengi wa wavuvi wanachukua mikopo benki na taasisi zingine za fedha kama PRIDE, FINCA, SACCOS na kadhalika. Kwa muda mrefu sasa Wabunge tumekuwa tukitaka Serikali ya Awamu ya Tano kukomesha uzalishaji na usambazaji wa nyavu hizo ili zisiwafikie wavuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua ni mkakati gani uliopo kuhakikisha kwamba, nyavu hizo haramu hazizalishwi na kusambazwa ikiwa ni pamoja na kudhibiti uingizaji wa nyavu hizo kutoka nje ya nchi? Naomba maelezo ya kina juu ya kuwepo kwa mkakati huo kama upo au la.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili; kwa kuwa nchi yetu ilianzisha mpango mahsusi wa uwekezaji wa EPZ wa kutenga maeneo ambapo baadhi ya maeneo Serikali ililazimika kuwaondoa wananchi. Je, mpaka sasa kwa nini eneo la EPZ Wilayani Bunda Mkoa wa Mara halijatekelezwa? Ni vema tukajua utaratibu wa uwekezaji katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuchangia hayo machache naunga mkono hoja!
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. ALPHAXARD K. N. LUGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nina kila sababu ya kumpongeza Waziri Profesa Sospeter Muhongo na Naibu wake Mheshimiwa Kalemani kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuhakikisha nchi yetu inapata umeme. Aidha, nawapongeza kwa usimamizi mzuri wa Sekta ya Madini, nawatakia kila la kheri chapeni kazi bila wasiwasi kwani Wabunge tuko nyuma yenu kuhakikisha mnakuwa katika mazingira rafiki ya kufanya kazi. Pia nawapongeza kwa kuwasilisha bajeti nzuri yenye kuleta matumaini kwa Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri Serikali juu ya mpango wa umeme vijijini unaotekelezwa na Wakala wa Umeme Vijijini (REA). Yapo maeneo hapa nchini ambayo yana changamoto kubwa sana katika usambazaji wa umeme. Maeneo hayo ni yale ya visiwa vingi ambavyo viko katika maziwa na bahari.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri kwamba ili kupunguza gharama za kutumia marine cable kupeleka umeme katika visiwa, basi REA wasambaze umeme huo kwa njia ya solar (umeme jua) Jimboni kwangu nina visiwa katika Ziwa Victoria vya Nafuba, Sozia, Namuguma, Machwela, Rwiga, Buyanza, Kwigali, Bwenyi na Nyakalango.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa shughuli kubwa za kiuchumi katika visiwa hivi ni uvuvi, umeme huu utasaidia sana kuhifadhia mazao ya samaki pamoja na viwanda vidogovidogo vya kuchakata samaki na kutengenezea boti na mitumbwi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa haya machache, naunga mkono hoja. Ahsante.
Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dokta John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hatua anazochukua kukabiliana na Upotevu wa Mapato ya Serikali katika Sekta ya Madini
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami niungane kuunga mkono Azimio hili la kumpongeza Rais John Pombe Magufuli. Watanzania tulimwomba Mungu atuletee Rais ambaye ni jasiri, Rais ambaye ana uthubutu, Rais ambaye atakuwa mlinzi wa rasilimali za nchi yetu na Mungu akasikia kilio chetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya watu ambao wanasimamia kauli zao ni Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. Mheshimiwa John Pombe Magufuli kabla hata hajawa Rais wa nchi hii, alitoa kauli kwamba atakapokuwa Rais atahakikisha mchanga wa dhahabu hautasafirishwa tena kwenda nchi za nje. Mheshimiwa Magufuli kabla hajawa Rais alisema, ole wao Watanzania watalimia meno endapo atakuwa Rais wa nchi hii. Leo tunashuhudia Watanzania aliowalenga kulimia meno ni mafisadi wanaoiba rasilimali za nchi hii na sasa wanaanza kulimia meno. Namwomba Rais wetu hata wale wanaoshabikia na kuunga mkono mafisadi na wenyewe awaweke katika kulimia meno kwa sababu na wao wanashabikia kuibiwa rasilimali zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi zote duniani huwezi ukampata mtu wa aina ya Magufuli ambaye amezaliwa kila wakati, ambaye anazaliwa kila mahali na ndiyo maana hata nchi zingine wanaanza kumlilia kwamba huenda na sisi tungekuwa na mtu kama huyu mtu ambaye ana uchungu na watu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wetu wakati anapokea Ripoti ya Makinikia alitaka kulia, nilimwona ameshika shavu la kushoto, anasema kama na yeye ana damu Rais wetu analia na rasilimali za Watanzania. Leo kuna watu hawataki tumpongeze Rais wetu wakati amejitoa mhanga, kuna watu wanajitoa mhanga kulipua ndege, kuna watu wanajitoa mhanga kulipua hata Mabunge leo Rais anajitoa mhanga kufa kwa ajili ya rasilimali za Watanzania kwa nini tusimuunge mkono mtu kama huyu? Ndiyo maana ukisoma Isaya 54:17 unasema, kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu hauta… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. KANGI A. LUGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, na kabla sijafika mbali Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango naomba masuala mawili haya ambayo kwenye hotuba yako hujayazingatia nipate ufafanuzi; sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi, kuna ushuru na tozo mbalimbali ambazo toka Bunge lililopita tunapiga kelele kwamba wakulima katika sekta hiyo hawatafika mbali kwa sababu ya ushuru na tozo ambazo hazina tija.
Mheshimiwa Naibu Spika, na kwenye hotuba yako hapa umebaki tu kutaja kwamba kuna hizo changamoto, lakini hujatuletea hizo sheria mbalimbali kwa ajili ya kuzifuta ili wakulima waweze kuifanya Tanzania yetu kuwa nchi ya viwanda. Na wewe Mheshimiwa Mwijage hivyo viwanda unavyovihubiri havitakuwepo kama sekta hii ya kilimo tunafanya nayo mzaha wa namna hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni suala la maji. Maji vijijini tulitenga Shilingi 50 kila lita ya mafuta ya petrol na diesel kuanzia Bunge lililopita kuwekwa kwenye mfuko wa maji, lakini zile fedha zikapelekwa maji mjini matokeo yake mpaka leo vijijini bado kunashida ya maji. Wabunge hapa tulisema na tukashauri tuongeze kutoka shilingi 50 kwenda shilingi 100, lakini kwenye hotuba yako ya bajeti unasema itabaki hivyo hivyo shilingi 50. Tunaomba tuweke shilingi 50 kwenye mafuta ili tuweze kuwa na mfuko mzuri wa maji vijijini; na hakutakuwa na mfumuko wa bei. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais, John Pombe Maghufuli, kwa juhudi zake anazozifanya za kutumbua majipu katika nchi yetu na nimshukuru kwamba analeta Mahakama ya Mafisadi na zile rushwa kubwa za manyangumi. Lakini juhudi hizi za Mheshimiwa Rais, hatazifikisha mwakani endapo atabaki peke yake mtumbua majibu wakati mtambua na mbaini majipu ambaye ni CAG ataendelea kuwa na fedha shilingi bilioni nne katika bajeti hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kitendo cha kupunguza bajeti ya CAG ambapo mwaka jana alikuwa na shilingi bilioni 74; wakati fedha za miradi ya maendeleo zilikuwa ni kidogo kuliko mwaka huu, tuna trilioni 11 halafu ndipo mnampa shilingi bilioni 44. Hii ni dalili kwamba bajeti hii inataka kukumbatia mafisadi kwa sababu CAG ndiye anayekagua miradi na mikataba ambayo ni ya kifisadi. Kitendo cha kuminya Ofisi ya CAG, nakuambia Mheshimiwa Waziri Mpango, utumbuaji wa majibu utaishia mwaka huu; Rais hatakuwa na majipu ya kutumbua tena kama bajeti ya CAG haitaongezwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi niseme bayana, hata hawa watumishi hewa ambao sasa wanatumbuliwa, juhudi kubwa zilifanywa na CAG Bunge lililopita akawa anabaini watumishi hewa, miradi hii ambayo mingine tunapigwa kwenye barabara na sasa tunapeleka asilimia 40 kwenye miradi ya maendeleo, kama CAG ofisi yake itaminywa haya majipu yakifisadi nani atayabaini na hizi fedha mnazosema mnawezesha TAKUKURU; TAKUKURU atawachunguza mafisadi gani ambao hawajabainiwa na CAG?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kwangu mimi bila kumwongeza fedha CAG ambaye ndio jicho, ambaye ndiye ameikomboa nchi hii kwa kubaini mafisadi, nakuhakikishia Mheshimiwa Rais wetu, mwakani hatakuwa hata na kijipu uchungu; hata kipele cha kuweze kutumbua, kwa sababu CAG atakuwa hajafanya kazi yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye hii hoja iliyowasilishwa na Mheshimiwa Mpango ya kuondoa msamaha kwenye mafao ya Wabunge. Mheshimiwa Mpango naomba nikuulize, hawa Wabunge ambao unaondoa msamaha kwenye mafao yao unajua kwamba hawana pensheni? Unajua kwamba Wabunge hawa sio pensionable?
Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge sisi hufanya kazi yetu miaka mitano tu hapa, hatuna pension, matokeo yake tunaambulia hicho kidogo; fedha nyingine ni nauli, mizigo, vifedha vingine ndio vile ambavyo tumevidunduliza kwenye mshahara tunawekewa kila mwezi. Sasa wewe unataka kuondoa msamaha. Nataka nikuhakikishie kuanzia utawala Mkapa, Wabunge walikuwa wanaomba hata watumishi wengine mafao yao yasije yakakatwa kodi kwa sababu wamefanya kazi miaka 30, 40 watumishi wanakatwa fedha, wanaenda wengine wanakufa kesho yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa tumefika pazuri baada ya kuondoa kundi la Wabunge. Tulitarajia katika Bajeti hii sasa unatuletea sheria ya kwenda hata kufuta hizo kodi za mafao ya watumishi wengine Serikalini, sasa matokeo yake unatuletea tena kufuta za Wabunge. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge ninyi ni mashahidi, akiwepo Mheshimiwa Makinda hapa alisema amechoka kusumbuliwa Wabunge ambao walishastaafu wamekuwa wakija ofisini wanamwomba hela, wamekuwa ombaomba.
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge leo maslahi yetu tumedunduliziwa na kila mwezi tunakatwa kodi ya mapato halafu tena mafao yetu ambayo yamelimbikizwa na yenyewe yakakatwe kodi mnataka turudi mtaani halafu muanze tena kutucheka. Lazima Wabunge tulinde maslahi yetu, Mheshimiwa Waziri usicheze na maslahi yetu, lazima tulinde maslahi yetu. Hatuwezi kukubali fedha ambazo sisi kila mwezi tunakatwa kodi Pay as You Earn na nyingine ile tunawekewa pale halafu baada ya kutoka hapa uanze tena kututoza kodi. Waheshimiwa Wabunge tusikubali sisi hatuna pensheni lazima kodi hii isiwekwe kwenye fedha za Wabunge. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka nimwambie Mheshimiwa Waziri Mpango, sisi Wabunge mshahara wetu ni mdogo sana kuliko wa kwako, wewe mshahara wako ni mkubwa. Sisi Wabunge kule mtaani ndio ATM hata sasa hivi humu kila simu ya Mbunge sijui kuna msiba wapi, kuna kisima kimeharibika, kuna darasa upepo umeezua, ndipo hapo hapo tunapotoa pesa. Halafu Mheshimiwa Mpango unataka kucheza na maslahi ya Mbunge na wewe hapo ulipo wewe Jimbo lako ni Mheshimiwa Rais, sisi Jimbo letu ni wananchi kule. (Makofi)
Waheshimiwa Wabunge tumekuwa tukiomba fedha hata za kukarabati chuma kidogo tu kwenye pampu ya maji kutoka Halmashauri unaambiwa wewe Mbunge saidia. Tunaomba Halmashauri kuna kadaraja pale kamekatika kidogo pelekeni fedha wanasema kazi ya Mbunge, kazi ya mwenge. Halafu leo hata hicho kidogo na ndiyo maana unanikumbusha lile tangazo kwenye TV walikuwa wameweka kakuku pale linakuja lile kama fisadi mara ya kwanza likakata robo tatu ya kuku haaam! Halafu kakabaki karobo likamalizia tena haamm! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mpango asitupeleke huko, fedha zetu ni kidogo sana matokeo yake unaanza kuzikwangua tena, je, tutakapofika mwakani utakuja tena na ajenda gani?
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mtu wa CHADEMA hapa alikuwa anawasilisha bajeti hapa nikaona mhh! Huyu ndiye Silinde kweli? Anashabikia kwamba eti na sisi tunaunga mkono hii kodi wakatwe.
Mheshimiwa Mpango wewe ni mchumi kuna kitu kinaitwa free rider problem, huyu pamoja na kuipiga panga kwamba haitaki wanajua sisi tukiitetea na wao pia watapata free rider problem. Asidanganye wananchi hapa UKAWA wata-enjoy free rider problem baada ya sisi kuitetea na wewe ni mchumi unajua maana ya free rider problem, hatutakubali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, anazungumzia masuala ya sitting allowance, leo, mimi nadhani alikuwa anachomekea tu kwa sababu wana ugomvi na mama yetu pale wanachomekea chomekea vitu na sisi hivi vitu vya kuchomekea hivi mama wala usiwe na wasi wasi wewe ndiye Naibu Spika na wao walikuchagua na sisi tumekuchagua hicho kiti utakikalia mpaka wewe mwenyewe utakaposema sasa basi. (Makofi)
Mheshimiwa Mpango utakapokuja kutoa majumuisho fedha hizi za CAG bila kupanda na bila kutoa kauli hapa kwamba hicho ulichojaribu cha kutu-beep juu ya maslahi yetu hatutaelewana. Na ninashukuru umetu-beep na sisi tumeamua kukupigia. Tunakwenda wapi? Na watumishi wengine wote wale tulishasema fedha zao zile msizikate kodi zile.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. KANGI A.N. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru pia kunipa nafasi ya mwisho katika kuchangia hoja ya Mpango wa Maendeleo ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kabisa kuwakumbusha Waheshimiwa Wabunge wenzangu, sisi ni binadamu husahau, sisi ni binadamu ambao wakati mwingine hatuwezi tukaukubali ukweli hata kama ukweli utabaki kuwa ukweli. Niwakumbushe Wabunge wenzangu kwamba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alizindua Bunge hili pamoja na mambo mengine aliliomba Bunge hili, alituomba Wabunge kwamba ameomba kazi ya kutumbua majipu tumsaidie ahakikishe anatumbua majipu katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia aliliomba Bunge hili limsaidie pale anapoleta mipango yake ya Serikali tumsaidie ili mipango hiyo iweze kutekelezeka, tuweze kuijenga nchi yetu. Hata hivyo, Bunge hili sasa linapoteza mwelekeo, limepoteza kumbukumbu limebaki sasa ni Bunge la kumlaumu Rais, limebaki ni Bunge la kulialia. Bunge hili litakuwa halimtendei haki Mheshimiwa Rais wa nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, najua Mheshimiwa Rais ana nia njema na Taifa, najua Mheshimiwa Rais kwa kauli mbiu ya hapa kazi tu inasababisha watu ambao walikuwa wanaishi kwa mazoea waweze kumlaumu na kumlilia kwamba anaharibu nchi yao. Tunamtia moyo, tunamwunga mkono aendelee kushika na kukandamiza mahali ambapo amekandamiza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mazoea ni ya ajabu sana, tulizoea kwa makundi, wako wafanyabiashara walizoea kukwepa kodi, leo wameshikwa pabaya wanaanza kulia kwamba sasa biashara imekufa. Watumishi tulizoea posho za hapa na pale, tulizoea kusafiri, sasa wameshikwa pabaya wanaanza kulialia. Wabunge tulizoea kwenye Kamati tunapata chai nzuri, tunakula andazi la inchi kumi na nane leo tunakula andazi la sentimita mbili, tumeshikwa pabaya tunaanza kulialia. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge sasa tunaanza kulialia kwa sababu tumeshikwa pabaya na kuwaingiza wananchi wanyonge kwamba wao ndiyo wanaonewa kwamba wao ndiyo hawana fedha. Mambo mengine ni ya ajabu sana, mpaka unajiuliza huyu ndiye Mheshimiwa Mbowe? Mbowe naye leo anailaumu Serikali imefilisika! Hivi ni Mbowe huyu kweli ambaye analipiwa gari na Serikali, shangingi, mafuta yamejaa, kiyoyozi kiko masaa 24, anasema Serikali imefilisika? Huku ni kuwatumia wananchi vibaya, ni kutaka kuwachonganisha wananchi na Serikali yao na Rais wao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Msigwa kwa bahati mbaya leo hayupo, Mheshimiwa Msigwa yeye kama Mchungaji nilitarajia atatumia taaluma yake kuwashauri wenziwe kwamba hata wakati ule kwenye Biblia wakati Musa anawachukua wana wa Israel kutoka Misri awapeleke kwenye nchi ya ahadi, nchi yenye maisha mazuri jangwani walipata shida, hawana maji, wanang’atwa na nyoka lakini hatimaye kwa kuwa walikuwa na Mungu, Musa aliwafikisha salama na wakaishi maisha mazuri. Mheshimiwa Msigwa awashauri wenzake kwamba katika safari hii kutakuwa na misukosuko ya hapa na pale, lakini Musa wetu Mheshimiwa Rais Magufuli anatupeleka nchi ya Kaanani twende kuishi maisha ya asali. (Makofi/Vigelegele)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo pia machache ya kumshauri Rais wetu wa nchi hii. Rais wetu alituahidi kwamba sisi Watanzania ambapo yeye ni dereva na sisi ni abiria wake anatusafirisha kutoka mahali tulipopandia basi atupeleke kwenye nchi ya ahadi. Namshauri Mheshimiwa Rais barabarani yeye kama dereva kuna matuta lazima ajue matuta haya akiendesha vibaya yataleta ajali na Watanzania hatutafika mahali anapotupeleka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimshauri pia anapoendesha gari kuna zebra cross, wanafunzi wana-cross, ng’ombe wanapita, aendeshe vizuri Watanzania atufikishe salama. Naomba nimshauri pia anapoona wameandika speed 50 na yeye aende speed 50 ili Watanzania atufikishe salama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huu Mpango nimeusoma, Mpango huu ni mzuri, yako maeneo ya kushauri. Tunayo dira yetu ya Taifa ya Maendeleo 2025, tunayo Ilani ya CCM, vitabu hivi viwili ndivyo vinavyomsaidia Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango katika kuja na mapendekezo mazuri ambayo yanaenda sambamba na utekelezaji wa Ilani ya CCM. Mheshimiwa Waziri yako maeneo humu ambayo inabidi nimshauri, kwenye Ilani yetu kuna mambo ya kilimo, kwenye mambo ya kilimo mpango wake umeacha kabisa mazao ya biashara kama vile pamba, tumbaku, kahawa, katani na pamba pamoja na mazao mengine imeshuka sana. Nimpe mfano, mwaka 2012/2013, tulizalisha pamba tani 356,000 na 2016/2017 imeshuka mpaka tani 120,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni nini? Kama leo watoto wetu wa maskini wanakosa mikopo ya elimu ya juu…
Kimbilio lao ni kwa wazazi wao ambao wanalima pamba. Kama wazazi wao wanalima pamba na humu hajaweka mpango wa kusaidia zao la biashara la pamba, watoto wa maskini hawatasoma, watoto hawa watakuwa wa mitaani. Namshauri atakapoleta Februari rasimu yake isheheni masuala ya kilimo cha mazao ya biashara, masuala ya mbolea ili watoto wa maskini waweze kupata elimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, humu ndani Mheshimiwa Waziri ameweka kanda maalum za kiuchumi. Kanda maalum za kiuchumi Mheshimiwa Mpango tuna Ziwa Viktoria katika nchi yetu, zawadi ambayo tumepewa na Mwenyezi Mungu. Hata hivyo, maji ya Ziwa Viktoria yamebaki kunufaisha Sudan na Misri wakati sisi wa Mikoa ya Kagera, Geita, Tabora, Shinyanga, Mara na Mwanza tunatakiwa tuwe na miradi mikubwa ya uzalishaji kwa sababu tuna maji na ardhi nzuri. Kwa hiyo, Ziwa Viktoria liwekwe kwenye kanda maalum za kiuchumi ili tuweze kuzalisha kwa wingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni eneo la elimu ya juu. Kwenye Ilani tulisema tutajenga Chuo Kikuu cha Kilimo cha Mwalimu Nyerere, Wilaya ya Butiama. Sasa kama mpaka leo Waziri analeta mpango hauoneshi kwamba tutajenga Chuo Kikuu cha Mwalimu Nyerere Butiama na ujenzi wa chuo kikuu ni miundombinu mikubwa, chuo hicho kitajengwa lini Mheshimiwa Mpango? Namwomba kwenye rasimu yake aje na mpango wa kujenga Chuo Kikuu cha Kilimo cha Mwalimu Nyerere pale Butiama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mwana CCM ambaye niliapa kabisa nitasema kweli daima. Ninyi Mawaziri wa Serikali yangu ya CCM na ninyi ni abiria kwenye basi analoendesha Rais wetu na ninyi mmekaa siti za mbele, wakati mwingine abiria ndiyo humchochea dereva kwamba mnataka kufika mapema. Baadhi ya Mawaziri msimdanganye Rais, msimpotoshe Rais…
Asije akatuletea matatizo kwa sababu Rais anatakiwa ashauriwe vizuri, Rais wetu siyo mchumi. Hivi kweli mtamshaurije Rais kwamba kupotea kwa pesa ni kwa sababu watu wameficha kwenye magodoro, haiwezekani!
Pesa zimepotea kwa sababu Benki Kuu wamezichukua kutoka kwenye mabenki maana yake hazionekani. Pesa zimepotea, mshaurini ni kwa sababu madeni ya ndani hayalipwi, mumshauri vizuri. Itakuwaje mnamshauri Rais kununua ndege kwa cash wakati…
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Mkataba wa Ubia wa Uchumi baina ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Umoja wa Ulaya.
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Spika naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kwanza kabisa kuwa mchangiaji wa siku ya leo kuhusu mkataba wa Ubia wa uchumi baina yetu ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki pamoja na Jumuiya ya Nchi za Ulaya.
Mheshimiwa Spika, mkataba huu ambao mimi nimeushika hapa mkononi ni miongoni mwa mikataba ambayo ni mibovu, ni miongoni mwa mikataba ambayo ni mibaya, ni miongoni mwa mikataba ambayo inanikumbusha enzi za miaka ya zamani. Mikataba kama hii ndiyo ambayo tulisoma kwenye historia ya akina Carl Peters na kwamba Wazee wetu wakiwemo wakina Mangungu waliweza kusaini mikataba mibovu na ya ajabu kama huu.
Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu, Jemedari John Pombe Magufuli ambaye kwa kutumia mkono wake alikataa kabisa mkono wake usitumike katika kusaini mkataba mbovu huu katika Ikulu ya Tanzania, mjini Dar es Salaam.
Mheshimiwa Spika, kwa nini nasema mkataba huu ni mbovu? Niliwahi kuja Bungeni hapa nikiwa na semi-trailer ambalo nilishindwa kuliingiza humu ndani nikaliacha pale nje lilikuwa limesheheni bidhaa mbalimbali vikiwemo vijiti vya kutolea nyama kwenye meno, chaki, vikiwemo vitambaa, zikiwemo peremende.
Mheshimiwa Spika, kama nchi yetu imekuwa na bidhaa ambazo zimezagaa na kusababisha sisi tusiweze kuimarisha na kujenga viwanda vyetu, tukisaini mkataba wa namna hii nchi yetu itakuwa ni dampo la bidhaa nyingi za ajabu na matokeo yake dhamira njema ya Mheshimiwa Rais ya kutaka nchi hii sasa iwe ni nchi ya viwanda hakika hatutaweza kufanikiwa kama tutasaini mkataba wa namna hii.
Mheshimiwa Spika, mkataba huu ambapo katika aya zake 146 zaidi ya vifungu 20 ni vifungu ambavyo vina matatizo, na Waheshimiwa Wabunge mtakuwa mashahidi kwa sababu ya muda sina sababu ya kuvipitia tena. Vifungu hivi vina matatizo, vifungu hivi vinatufanya tukisaini mkataba nchi yetu ya Tanzania haitakuwa na nafasi ya kujitanua katika ku-negotiate tutakuwa tumefungwa. Tukisaini mkataba huu kwenye vifungu ambavyo vinahusu masuala ya kilimo, masuala ya mifugo, masuala ya miundombinu tutakuwa tunasaini mkataba ambao kwa kweli nchi yetu itaingia kwenye matatizo makubwa.
Mheshimiwa Spika masuala haya ya nchi za Ulaya kuwinda nchi zetu katika umoja wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, wanajua kabisa kwamba nchi ya Kenya ambayo wamepiga hatua kiviwanda, sote tunajua viwanda vya nchi ya Kenya viwanda vingi ndivyo hawa hawa ambao wanatoka kwenye Jumuiya ya Ulaya. Kwa hiyo, leo hii tukisaini mkataba kama huu ambapo tunashirikiana na nchi ya Kenya kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa vyovyote vile tutaingia katika matatizo makubwa.
Mheshimiwa Spika, kuna mifano ambayo iko hai. Sisi tulipoanzisha General Tyre wakati ule tulijua kabisa kwamba tutakuwa na soko zuri na tutaweza kuwa na viwanda ambavyo vitatusaidia, lakini Kenya hawa hawa ambao walitumiwa na nchi za Jumuiya ya Ulaya waliweza kuanzisha Kiwanda cha Fire Stone, leo hii kiwanda chetu cha General Tyre kimekufa. Kwa hiyo, tukisaini mikataba kama hii kwa kweli tutaendelea kuwa na matatizo makubwa sana.
Mheshimiwa Spika niseme, wenzetu wa Kenya ndiyo hata miaka ya nyuma wakati wa Jumuiya ya Afrika Mashariki walikuwa ni chanzo cha kuua Jumuiya ya Afrika Mashariki ambayo tuliianzisha wakati ule. Leo nina wasiwasi tukiendelea na Mkataba huu tukiwa tunashirikiana na Wakenya kwa vyovyote vile Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki ambayo tumeianzisha kwa nguvu kubwa, kwa nia njema lazima Jumuiya hii matokeo yake itaenda kuvunjika tena. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo viongozi wetu wa Serikali, Wizara ya Afrika Mashariki, Wizara ya Viwanda na Biashara na Uwekezaji, hakikisheni kwamba wataalam wetu waendelee kuuchambua mkataba huu ili maeneo yote yale ambayo yana matatizo yaweze kufanyiwa kazi. Na niseme bayana, lazima katika negotiation nchi yetu itakapofanya uchambuzi waweze kuwa na negotiation framework ambayo imetokana na mawazo ya Wabunge waweze kuboresha mkataba huu.
Mheshimiwa Spika, tunajua kwamba mkataba huu kuna maeneo ambayo ni mazuri, lakini kwa sababu maeneo makubwa yana matatizo, hatuwezi tukaingia kwenye risk kwa sababu tu kuna mambo ambayo ni mazuri wakati mambo makubwa ndiyo mabaya. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Jumuiya ya Afrika Mashariki ambapo sisi tuna Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki kwenye EALA lazima Wizara ya Mambo ya Nje na Afrika Mashariki iweze pia kushirikisha Wabunge kwa Chapter ya Tanzania na wenyewe wajaribu kuchambua katika Bunge lao, waende kupiga marufuku muswada kama huu kuendelea kusainiwa ukiwa mbovu namna hii. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tuna Mabunge mawili, Bunge letu hili kwa leo mimi kama Mbunge wa CCM, Mbunge ambaye naamini Serikali yetu inahitaji mkataba wa kufanya biashara na nchi za Ulaya, lakini hatuwezi kukubali Serikali ya CCM ikaingia mkataba ambao ni mbovu, ambao ni fake kama huu.
Ninawaomba Waheshimiwa Wabunge wenzangu, bila kujali itikadi zetu, lazima nchi hii tuitendee mema, lazima mkataba huu tuukatae, Mkataba huu ni mbovu, urudi uchambuliwe halafu lazima Bunge hili baadaye lishiriki tena kuangalia ile negotiation framework ili tuone kwamba sasa tunaweza tukaenda kusaini mkataba ambao ni mzuri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mikataba mingine kama hii, humu humu ndani mimi nimesoma vifungu vingine vinajaribu kuwa na mwelekeo pia wa kutuletea mambo mengine ya ushoga kama ambavyo mikataba mingine inaleta mambo ya ushoga. Kwa hiyo, lazima Wabunge tuwahurumie Watanzania na hasa Watanzania ambao ni wanaume. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tusipokuwa macho, sehemu zao nyeti zinaweza zikaingiliwa kwa sababu ya mikataba mibovu kama hii. Hatuwezi sisi tukakubali. Lazima tulinde haki za binadamu sisi kama Wabunge wa Bunge hili. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Spika, mimi ninakushukuru sana. Nitawashangaa Wabunge wenzangu ambao tumepata semina hapa nzuri ya maprofesa na madokta waliobobea halafu matokeo yake Mbunge unasimama, unakuja kuupongeza na kusema tupitishe mkataba wa namna hii. Nitakushangaa sana, na ndiyo maana hii mbingu mnayoiona hii yuko Mwenyezi Mungu anatutazama, analitazama Bunge hili namna gani mlivyo na huruma na uchungu na wananchi ambao ni watu wa Mungu. Mkisaini mkataba huu nawaambieni itakuwa ni vigumu sana hata ninyi kuuona ufalme wa Mungu.
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana. Siungi mkono kupitisha mkataba huo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, majeshi yetu ya Polisi, Magereza, Uhamiaji pamoja na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ni majeshi ambayo yamesahaulika, ni majeshi ambayo yanachukuliwa kama ni ya kawaida, ni majeshi ambayo yanadhaniwa watendaji walioko mle hawana professionalism ya aina yoyote. Ndiyo maana majeshi haya yamefanywa kama majeshi ya miujiza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Yesu peke yake Mwana wa Mungu aliye hai ambaye ni bingwa wa miujiza, ambaye alikufa akafufuka, ambaye alimfufua Lazaro, ambaye alitembea juu ya maji. Hivi kweli kama majeshi haya hatutawekeza, hatuwezi tukapunguza uhalifu katika nchi yetu, hatuwezi tukajenga nidhamu ya majeshi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwakumbushe kidogo Waheshimiwa Wabunge, hima himaaa, Tanzania sauti hii ukiona vyaelea vimeundwa, msidhani magwaride haya mnayofurahi jinsi majeshi wanavyopiga mguu chini, jinsi wanavyotoa sauti yao ya kutoa heshima ya utii kwa Amiri Jeshi Mkuu, mkadhani sauti hii imekuja hivi hivi. Sauti hii inatengenezwa na lishe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inakuwaje askari wetu tunawapa shilingi 10,000, shilingi 10,000 hii aiache kwa familia, shilingi 10,000hii aende nayo kwenye lindo la benki, shilingi 10,000 hii aende nayo doria, asubuhi mpaka jioni haitawezekana. Ndiyo maana Waziri anapotuambia katika

ukurasa wake wa 21 katika hotuba yake kwamba Serikali inaendelea kuboresha maslahi ya watendaji wa vyombo vya usalama kwa kuwapatia ration allowance za kila mwezi. Mheshimiwa Waziri unasema unaendelea kuboresha ration allowance mbona kwenye kitabu chako humu hujaboresha, umeweka maneno tu yasiyoboresha? Tunahitaji uboreshe maslahi haya ili askari wetu waweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, askari hawa mnaosikia wengine wanatekwa kwenye mabenki, wengine wanavamiwa kwenye doria, wakati mwingine wanakuwa kwenye stress, hajui leo familia yake itakula nini, hajui yeye atakula nini, anabaki askari wa kupiga miayo tu kwenye benki matokeo yake wanamnyang’anya bunduki. Tunahitaji kuboresha maslahi ya Jeshi la Polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye mafunzo, Mheshimiwa Mwigulu ulipokuwa Wizara ya Kilimo ulikuwa na kauli mbiu mkitaka mali mtaipata shambani. Sasa leo uko Wizara ya Mambo ya Ndani nataka nikushauri, ukitaka kupunguza msongamano magereza, siyo kujenga mabweni ni kupunguza uhalifu katika nchi yetu. Ukitaka kupunguza uhalifu katika nchi yetu lazima uzingatie mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya miaka kumi sasa hakuna traffic courses kwenye Jeshi la Polisi, imebaki tu wewe askari kesho unapigiwa simu unakuwa traffic na ndiyo maana ghafla mnaona traffic anachoropoka kwenye vichaka kwa sababu hawana mafunzo ya aina yoyote. Mnagombana na askari traffic hawana mafunzo, tunataka mafunzo ya askari wa usalama barabarani wasomee magari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna masuala ya CID. Msongamano utaendelea kwa sababu upelelezi uko kiwango cha chini sana, kesi zinachukua muda mrefu kwa sababu ya kutokuwa na mafunzo katika kupeleleza, kwa sababu ya kutokuwa na fedha ya kutosha kwenye Criminal Investigation Fund, mfuko ambao unatumika kuwapatia watu wanaoleta taarifa, taarifa ni za kununua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la CRO wenzangu ambao hamkupita kwenye Jeshi kama hilo maana yake mimi nimepita huko nina-declare interest. Pale mnapoita kaunta pale, pale ni CRO pale kulikuwa na mafunzo ya CRO, lazima anayekuwa in charge pale awe amefundishwa namna ya kupokea mashitaka, namna ya kujua hili ni kosa la jinai au ni kosa la civil, matokeo yake kunakuwa na malalamiko mengi ndani ya Jeshi la Polisi, kwa sababu hakuna kozi kama hizi za CRO.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuomba Mheshimiwa Mwigulu kozi hizi zirudi na wafundishwe Askari ili wajue kupokea mashtaka, tunaposema watu wanabambikizwa kesi ni pamoja na kutokujua hii ni ya criminal au ni ya civil kwa sababu hawajapata mafunzo ya CRO muda mrefu.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye vitendea kazi. Kwenye PGO lazima askari anapopanga ile duty roster pale kituoni, kunakuwa na askari wa standby…

(Hapa Kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Mheshimiwa Mnyika nataka nikuhakikishie kwamba ni vyepesi sana ngamia kupenya tundu la sindano kuliko upinzani kuiondoa CCM madarakani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na kumpongeza Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa jitihada kubwa anazozifanya kwa kuwatetea wanyonge wa Tanzania na kutetea maslahi ya nchi hii. Ninampongeza kwa sababu amejitoa mhanga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unaweza ukawa Rais lakini usijitoe mahanga kwa ajili ya kupigania maslahi ya watanzania na kuziacha rasilimali zikiporwa na kutumiwa na watu wachache; ninampongeza sana Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli na ndiyo maana zile pushapu alizopiga, na yale majina ya tingatinga tuliyompa na zile nyimbo tulizokuwa tunaimba za Kisukuma ling’ombe lyamapembe, lyekumakinda mumbazu ndiyo maana sasa matunda tunaanza kuyaona, ndiyo maana amewanyima pumzi mafisadi, wakwepa kodi amewanyima pumzi hawapumui, wenye vyeti fake hao nao na wenyewe sasa ndio wanakandamizwa, ninakuomba Mheshimiwa Rais uendelee kukandamiza hapo hapo na wala usibadilishe gear. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge nianze kwa kuwapa nukuu zifuatazo, nianze na ukurasa wa 30 wa kitabu cha hotuba ya Mheshimiwa Waziri, anasema; “Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli amekuwa ndiye msemaji mkuu (champion) wa masuala yanayohusu maji Barani Afrika.” Na kwamba Waziri mwenyewe ni Rais wa Baraza la Mawaziri wa maji Afrika kwa kipindi cha miaka miwili. Waheshimiwa Wabunge, u- champion huu naomba niwakushe, u-champion wa maji wa Mheshimiwa Rais wetu aliuanza wakati ule alipopiga push up kwenye kampeni, na aliponyanyuka kutoka chini kwenye push up aliwaambia Watanzania kwamba najua Watanzania akina mama mna tatizo la maji, ninakwenda kutatua tatizo la maji na ole wake Waziri wa Maji nitakayemteua asipowaleteeni maji nitamgeuza kuwa maji na Watanzania waweze kumnywa. Mheshimiwa Waziri, bajeti hii jiandae sasa unaenda kugeuzwa maji endapo tozo ya shilingi 50 haitakubalika na kuongeza pesa kwenye bajeti hii, kwa ajili ya kutatua kero ya maji kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini champion mkuu wa maji Waheshimiwa Wabunge ni Yesu Kristu Mwana wa Mungu. Ukisoma Yohana 19:26-28 Yesu alipopata maumivu msalabani anateswa wakati mama yake yuko pembeni, alimwambia; “mama tazama mwanao” na baadaye alipoona kwamba lazima haya yakamilike akasema; “naona kiu.” Hakuna kitu kingine ambacho Yesu alikiona ni isipokuwa kiu, kiu ni maji na ndiye champion mkuu wa maji kwa ajili ya akina mama katika Taifa letu. Tatizo la maji kwa akina mama, huu ni mwaka wa saba nilipoingia Bungeni humu niliingia na nyoka ya shaba, nikawaambia akina mama msichague Wabunge ambao watapitisha bajeti isiyotatua kero ya maji. Leo ni mwaka wa saba maji bado ni kero kwa wananchi hasa Watanzania akina mama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwaambie Wabunge wenzangu atakaye kwenda kupitisha bajeti hii kwa ndiyo! Ndiyo! Ndiyo! Ndiyo! Wakati Bajeti hii, haijaongezwa pesa ya tozo ya shilingi 50, niko tayali na mimi kuanzisha mwenge, mwenge wa sauti nitachukua kwenye Hansard sauti za Wabunge za ndiyo nitazikimbiza nchi zima kuwaambia akina mama sikilizeni Wabunge wanavyowasaliti na nyinyi hampati maji katika nchi yenu. Lazima tuwe na huruma kwa akina mama. Waheshimiwa Wabunge ni nani ambaye hakunyonya mtindi kwenye ziwa la mama yake katika nchi hii? Waheshimiwa Wabunge ni nani ambaye hakuishi miezi tisa kwenye tumbo la mama yake halafu leo inakuja bajeti ambayo haitatui tatizo la maji tunaendelea kufanya ushabiki katika suala la msingi la bajeti ya maji, hatutakubali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule vijijini kule Mwibara kule, miradi ya Buramba, miradi ya Kibara, Bunda Mjini amesema Mheshimiwa Ester Bulaya hapa, zaidi ya miaka kumi akina mama hawapati maji, kwa nini, ni kwa sababu ya Bunge hili lenye uwezo wa kutatua kero ya maji kwa akina mama tunafanya ushabiki na kupitisha bajeti ambazo hazitekelezeki. Naomba Waheshimiwa Wabunge tukatae. Nitashangaa kwa kweli Mbunge atakayepitisha bajeti hii ambayo haijaongezwa pesa za maji. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, ngoja ni waambie, kule vijijini wako wanaume ambao sasa hivi ni vilema ambao akina mama wanawaacha vitandani saa kumi usiku na kurudi saa tano ilhali wanadhani wana wivu kwamba akina mama wanakwenda kufanya mambo mengine wanapanda juu ya miti, matokeo yake wanadondoka wanakuwa ni vilema, leo tunakuja kufanya mzaa hapa. Waheshimiwa Wabunge, kule vijijini wanaoga kwa zamu maji hayatoshi. Aoge baba, aoge mwanafunzi aende shule, lakini hata wale wanaopata maji ya kuoga na wao wanachagua sehemu nyeti tu za kuoga kwa sababu maji hayawatoshi, halafu tunakuja tunafanya mzaa hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye umwagiliaji. Nilishasema hapa Bungeni. Kule Mwibara kuna bonde zuri kwenye Ziwa Victoria kuanzia Musoma Vijijini kule Bugwema linakuja linapita kwenye kata ya Butimba maeneo ya Kabainja linaenda Karukekele, Namhula, Bulendabufwe, Igulu matokeo yake linaingia mpaka Genge, Kisolya mpaka Nansimo lakini hatuna umwagiliaji. Tumechoka kuletewa mahindi ya msaada ya kilo nne kwa familia ilhali tuna maji ya Ziwa Victoria. Tunaomba miundombinu ya umwagiliaji. Nimeangalia kwenye kitabu hiki hakuna kabisa, lazima tutende haki kwa Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwenye mgawanyo wa fedha za maji. Nilikuwa nasoma humu unakuta kuna Halmashauri nyingine zina kata sita wana shilingi bilioni nne za maji. Kuna Halmashauri nyingine wanakata 20 mpaka 30; kuna Halmashauri nyingine zina majimbo mawili lakini wanapata shilingi milioni 800 tutakwenda wapi sisi, tutawambia nini wananchi wetu kwenye mgawanyo kamba huu? Tunasema tunagawana sungura mdogo, haiwezekani Halmashauri nyingine; niliona ya Mheshimiwa Kitwanga hapa ana shilingi bilioni nne wengine tuna shilingi 500,000,000 au kwa sababu anatishia kung’oa mitambo ya maji ndiyo sababu mnapatia maji? Haiwezekani, huyu sungura mdogo lazima tugawane hapa pasu kwa pasu; haiwezekani kabisa Halmashauri ipate shilingi milioni 500 wengine wana shilingi bilioni nne; haiwezekani tukamla kuku wengine wakachukua mapaja, wengine wakachukua mnaita chenye mafuta mafuta kile, halafu wengine mafuta mafuta yale, kakiuno kana mafuta na haka kakiuno kenye mafuta ndiko ambako wewe Waziri umechukua, ndiko wewe Naibu Waziri umechukua na sisi tunakataka hako, na sisi tunataka mafuta haiwezekani…(Makofi/Kicheko)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. ALPHAXARD K. N. LUGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia kwenye hoja muhimu na mahsusi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Kwanza kabisa naunga mkono hoja hii. Ni hoja ambayo imesheheni mambo ya msingi kwa Watanzania na hivyo ninashangaa sana watu ambao wanabeza juhudi ambazo Mheshimiwa waziri Mkuu anazifanya. Hilo ni kusema tu kwamba washindwe na walegee.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninayo mambo mawili yanayohusu masuala ya mazingira. Kuna mambo mengi ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyazungumzia yanayohusu uharibifu wa vyanzo vya maji, uchafuzi wa mazingira kwenye vyanzo vya maji likiwemo suala la ukataji miti hovyo na suala la mkaa. Nataka niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge jambo moja ambalo wanadamu huwa tunajisahau. Mwanadamu anapomuona mwenzake anakufa hakumbuki kwamba na yeye ni marehemu mtarajiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwanadamu anapomuona mwenzake ni mlemavu hakumbuki kwamba na yeye ni mlemavu mtarajiwa. Vivyo hivyo, wako Waheshimiwa Wabunge ambao wanadhani kwamba mazingira yanahusu tu wanyama watatoweka, miti itatoweka, ndege watatoweka, wanasahau kwamba hata sisi wanadamu vilevile tutatoweka endapo hatutalinda na kuhifadhi mazingira ya nchi yetu. Kwa hiyo, na sisi wanadamu ni watoweka watarajiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria yetu ya mazingira inazungumzia namna ambavyo tunatakiwa kutoa miongozo kwa Halmashauri zote nchini pamoja na wadau wengine wa mazingira kuhakikisha wanaorodhesha vyanzo vyote vya maji pamoja na milima na vilima wakionesha changamoto za vyanzo vya maji kwenye maeneo yao pamoja na milima na vilima.

Mheshimiwa Naibu Spika, miongozo hii inatuhitaji sisi baada ya kupata orodha hizo tuweze kuona changamoto za kila vyanzo vya maji ili vyanzo hivi tuweze kuvitengenezea miongozo ya kuvilinda ikiwa ni pamoja na kuvitangaza kwenye Gazeti la Serikali. Sasa kuna baadhi ya Wakurugenzi katiaka nchi hii ambao tangu Ofisi ya Makamu wa Rais imetoa agizo hili la kuwasilisha orodha hizi, muda ulishapita na juzi nikiwa Morogoro nimetoa muda mwingine wa mwisho kwamba tarehe 20 Aprili, 2018 Wakurugenzi wote nchi nzima wawe wamewasilisha Ofisi ya Makamu wa Rais orodha za vyanzo vya maji kwenye maeneo yao, vilima pamoja na milima.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wakurugenzi ambao wataendelea kukaidi agizo hili na kutolitekeleza, Mheshimiwa Waziri Mkuu najua mamlaka ya uteuzi Mheshimiwa Rais, kazi yetu sisi Ofisi ya Makamu wa Rais tutaorodhesha Wakurugenzi wote katika nchi nzima ambao wamekataa kutekeleza agizo hili ili mamlaka ya uteuzi itafakari na kuona kama vitumbua vya Wakurugenzi hawa vinastahili kutiwa mchanga ama laa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vyanzo vya maji vina uhusiano mkubwa sana na ndoto yetu ya Tanzania ya viwanda. Vyanzo vya maji vina uhusiano mkubwa na suala la uzalishaji wa umeme. Niwape mfano mdogo Waheshimiwa Wabunge, Mtera inazalisha megawati 80, Kihansi inazalisha megawati 180, Kidatu inazalisha megawati 204 na vyote hivyo vinahitaji sisi tulinde na kuhifadhi vyanzo vya maji na hasa maeneo ya Bonde la Mto Ruaha Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawataka Watanzania ambao wanalima kwenye bonde hilo wazingatie masharti ya kulima kilimo cha uhifadhi (conservation agriculture) na wasijihusishe na uharibifu wa Bonde la Mto Ruaha Mkuu. Hata wake rafiki zangu akina Mheshimiwa Mwamoto, akina Mheshimiwa Chumi, Mheshimiwa Ritta Kabati ambao wana kilimo maarufu kinaitwa vinyungu, kilimo hiki cha vinyungu lazima kiende sambamba na kuhifadhi mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye suala lililojitokeza la shule ama vyuo ama taasisi ambazo zinatoa mafunzo kutokuwa na matundu ya vyoo na hivyo kusababisha ama wanafunzi, ama wafanyakazi kujisaidia porini na hivyo kuchafua mazingira; pamoja na kwamba kuna baadhi ya shule ambazo hazina matundu ya vyoo lakini hata shule ambazo zina matundu ya vyoo vikiwemo na vyuo vya kati na vyuo vikuu wana tabia ya kutapisha vyoo na kupeleka kwenye mifumo ya mito ambayo wananchi wanatumia kwa kumwagilia mbogamboga pamoja na matunda. Nimeenda Dar es Salaam pale, kuna vyuo pale ambavyo vinatiririsha maji kwenda Makuburi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo natoa tahadhari, shule zote ambazo nimefanya ukaguzi na kuwaambia watoe mabomba yanayotiririsha kwenye vyanzo vya maji wayaelekeze DAWASCO, na tutafanya ukaguzi nchi nzima. Yale mabasi ambayo bado hawataki kutekeleza agizo la Mheshimiwa Mwakyembe la kuchimba dawa, tutaanza kuorodhesha kutumia maafisa mazingira wa wilaya mabasi ambayo wanachimba dawa porini na kuchafua mazingira ili na wao tuwapige faini kama wale wengine.
Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Ununuzi wa Umma ya Mwaka 2016
MHE. KANGI A. LUGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye huu Muswada wa Sheria ya Ununuzi wa Umma.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo Yanga inacheza TP Mazembe pale Dar es Salaam na haya marekebisho tunayoyafanya leo ya sheria hii nina imani kama Yanga itashinda na marekebisho haya yatakuwa mazuri zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kulikumbusha Bunge lako tukufu kwamba, katika Bunge la Kumi Serikali iliwasilisha Muswada wa Sheria ya Ununuzi na tukatunga Sheria Namba 7, 2011 kwa kufuta kabisa Sheria Namba 21 ya mwaka 2004. Ilionekana ile sheria tulioifuta ilikuwa na mapungufu makubwa sana na hivyo Wabunge tukajiridhisha kwamba sheria tuliyoitunga kwenye Bunge la Kumi ingeweza kuondoa matatizo katika sekta ya ununuzi wa umma.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ni kwa bahati mbaya leo Serikali inawasilisha tena Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Ununuzi wa Umma na marekebisho ambayo tunaenda kuyafanya leo. Nilikuwa naangalia muswada wenyewe, tunakwenda kubadilisha vifungu 40 na vifungu 40 ni vingi sana, ni vifungu ambavyo tunaenda kuvibadilisha katika hati ya dharura, kwa hiyo ninayo mambo ambayo ningependa niitahadhalishe Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwenye ukurasa wa 11 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Tulipotunga Sheria Namba 7 ya 2011 tuliangalia kwamba sekta ya ununuzi wa umma kwenye Halmashauri zetu lazima tuweke sharti ambalo linamtaka Mkurugenzi wa Halmashauri kuwasilisha mbele ya Kamati ya Fedha na Mipango maamuzi yaliyofanywa na Bodi ya Zabuni ili Kamati ile iweze kuchambua na kuridhia juu ya utoaji wa tuzo kwa mzabuni aliyeshinda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tulifanya vile kwa sababu ndipo sasa dhana ya D by D (ugatuaji wa madaraka) kwenda vijijini ulikuwa unajidhihirisha. Kamati ya Mipango na Fedha ndiyo inayofanya ziara kwenye eneo lao la Halmashauri na kukagua miradi yote ya maendeleo ambako wazabuni hawa wanakuwa wanatekeleza zile zabuni walizoshinda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa masikitiko makubwa, leo muswada unaoletwa mbele ya Bunge lako tukufu. Mheshimiwa Waziri anapendekeza kwa lugha ya kusema kuboresha kwa kufuta kabisa na kuondoa sharti la Kamati ya Fedha na Mipango kutopokea tena taarifa ya maamuzi ya utoaji wa zabuni. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi kweli kamati hii kupitia na kuchambua uamuzi huu ni kasoro na ni upungufu? Mimi nilidhani kuendelea kuwapa lungu zaidi Kamati ya Mipango na Fedha.Ndipo pale ambapo watahakikisha fedha za wananchi katika manunuzi ya umma kwenye miradi inatumika ipasavyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ndio maana kamati hii inapokuwa inapokea taarifa hii na kuichambua.Wao hawaiambii bodi kwamba mpeni huyu zabuni, hapana! Wao jukumu lao ni kuangalia inawezekana katika kaguzi walizofanya za miradi wakakuta kuna mzabuni. Kampuni ya ukandarasi imechakachua mradi, imejenga mradi chini ya kiwango, wanayo mamlaka ya kuiambia bodi kwamba huyu mkandarasi ana matatizo ili waweze kuiangalia upya zabuni ile. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ninamtahadhalisha sana Waziri wa Fedha na Mipango alitazame hili ili tuhakikishe kwamba sharti hili la kuipa Kamati ya Fedha na Mipango liendelee kama lilivyokuwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwenye suala hili la bei ya soko. Sababu nyingi zinazotolewa na hasa katika muswada huu za kwamba Serikali imekuwa ikiingia hasara kwa sababu zabuni hizi wanaweka bei ya juu tofauti na bei ya soko. Na hivyo leo tufanye marekebisho kwa kutazama kwamba wazabuni hawa wawe wanaleta zabuni zao kwa kuangalia bei ya soko.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimtahadhalishe Mheshimiwa Waziri amejipanga vipi kuhakikisha kwamba yale mambo yaliyokuwa yanawafanya ghawa wazuni kuweka bei ya juu Serikali inayatazama.
Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza wazabuni hawa wanapokuwa wanaleta bei zao Serikali hii imekuwa haiwalipi kwa wakati! Na hivyo wamekuwa wakiingia hasara, wanafuatilia madai yao miaka nenda rudi Serikali haiwalipi na matokeo yake hata zile fedha wanazofatilia zinakuwa haziwasaidii.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kampuni nyingi zimefilisika, watu wanalisha shule, wanalisha magereza lakini malipo kutoka Serikali inakuwa ni kizungumkuti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, leo mnaposema kwamba walete bei za soko na wakati ninyi Serikali hamjabeba jukumu katika sheria hii hii kwamba na ninyi muwalipe kwa wakati, nina imani kwamba sheria hii tunayoibadilisha leo haitaleta mafanikio, wazabuni hawa hawa mtaendelea kupata bei za juu na vinginevyo hamtawapata wazabuni mtarudi kule kule kuanza kufanya manunuzi nyinyi wenyewe. Ndiyo maana leo hii Mkurugenzi ambaye ana cash money ukimtuma kwenda kwenye duka ana uwezo wa kununua bei ya soko lakini Mkurugenzi huyo huyo akienda kwa kauli ya kukopa alipe baadaye bei ile lazima haitakuwa hiyo ambayo mnaiita ni bei ya soko. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo lingine Serikali imejipangaje kwenye suala la rushwa kwenye hizi tenda za zabuni? Kwa sababu rushwa ndiyo husababisha wazabuni hawa wanaleta bei ambazo ziko juu na wamekuwa wakifanya mawasiliano na wazabuni kwamba katika kujenga barabara hii au katika kuleta jenereta, katika kuleta fridge, katika kulisha shule ndizi moja lazima ulete bei fulani kwa ajili ya kushindana na hao wengine. Wanafanya hivyo kwa sababu wazabuni hawa au wakandarasi ili waweze kulipa ile 10 percent ambayo ni ya corruption lazima waweke bei za juu, hawawezi wakatumia hela zao za mfukoni katika kulipa hawa kwa njia ya rushwa. Kwa hiyo, nilitaka kujua Serikali imejipangaje, haya mambo ya kuwaambia wazabuni wanapoleta zabuni zao wawe wameandika kwamba hawatajihusisha na rushwa, yale yamekuwa ni maandishi tu ni makaratasi lakini bado kumekuwa na matatizo kwenye zile zabuni.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo namtahadharisha ambalo inabidi pia walichukue kwa makini, katika masuala haya ambayo tumesema kwamba tujaribu kupunguza muda wa hizi tenda ambapo mwanzoni walikuwa wanatumia muda mwingi sana, lazima ule muda tungeuoanisha na huu muda ambao tunataka kuboresha wa manunuzi ya dharura. Tusipooanisha muda huu na yale manunuzi ya dharura, nina uhakika lazima Bodi ya Zabuni watakuwa hawatengenezi ule mpango wa manunuzi kwa mwaka, watakuwa wanasubiri wajifanye kila kitu wananunua kwa dharura na watakuwa wanasubiri pia waweze kuzigawa zile tenda. Kwa sababu kwenye Sheria ya Manunuzi kuna kile kiwango ambacho hawaruhusiwi katika tenda moja Mkurugenzi kutoa maamuzi kwa ajili ya manunuzi lazima waende kwenye tenda. Kwa hiyo, ule muda tusipouoanisha vizuri na hizi zabuni za kawaida pamoja na haya manunuzi ya dharura, tunaweza tukarudi kule kule tukasema kwamba sheria tuliyoipitisha lazima tuirekebishe tena.
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho. Leo tunakwenda kufanya maboresho 40 kwa Sheria ya Manunuzi na tunafanya maboresho haya…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kangi, naomba umalizie sekunde 10 muda wako umekwisha.
MHE. KANGI A. LUGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, haya, naunga mkono hoja.