Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Kangi Alphaxard Lugola (25 total)

MHE. PETER J. SERUKAMBA (K.n.y. MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO) aliuliza:-
Athari za mazingira ni kubwa na vyanzo vingi vya mito (water sources) vimeathirika sana (mfano Mto Makere):-
Je, Serikali ina mpango gani wa muda mfupi na mrefu wa kukabili hali hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ruhusa yako, napenda nichukue fursa hii ya mwanzo kabisa kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuniamini na kuniteua kwenye Baraza lake. Nishukuru pia Wabunge wenzangu ambao wamenipa ushirikiano na wewe mwenyewe Mwenyekiti ulikuwa mjumbe mwenzangu wa Tume kwenye Utumishi wa Bunge, nakushukuru sana kwa ushirikiano ulionipa. Niwashukuru wananchi wa Mwibara pia kwa kunifanya Mbunge wao na Rais akaniona. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), sasa naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwako, Mbunge wa Kasulu Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukabiliana na uharibifu wa mazingira ya ardhi na vyanzo vya maji, Serikali ilipitisha Mkakati wa Kuhifadhi Mazingira ya Ardhi na Vyanzo vya Maji wa mwaka 2006. Mkakati huu umeainisha hatua za muda mfupi, muda wa kati na muda mrefu za kukabiliana na uharibifu wa mazingira ya ardhi na vyanzo vya maji. Aidha, mwaka 2008, Serikali iliandaa Mkakati wa Hatua za Haraka za Kuhifadhi Mazingira ya Bahari, Maziwa, Mabwawa na Mito ili kuhifadhi maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2012, Serikali ilipitisha kwa ajili utekelezaji Mkakati wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi. Aidha, mwaka 2016, Serikali ilielekeza utekelezaji wa Programu ya Kupambana na Kuenea kwa Hali ya Jangwa na pia Serikali inakusudia kuzuia matumizi ya kuni kwenye taasisi za umma ili zianze kutumia nishati mbadala. Mikakati yote hii inalenga kukabiliana na athari za uharibifu wa mazingira na vyanzo vya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua za muda mfupi zilizoainishwa na mkakati wa mwaka 2006 ni pamoja na kuwaondoa wafugaji waliovamia mabonde na maeneo ya vyanzo vya maji; kusimamisha shughuli zote za kilimo na kuwaondoa wavamizi kwenye maeneo yaliyoharibika sana; kuzitaka taasisi na watumiaji wengine wakubwa wa miti, kuni na mkaa kuwa na mshamba yao ya miti; kudhibiti shughuli za umwagiliaji usio endelevu na kuzitaka wilaya zote kubainisha vyanzo vya maji na kufanya tathmini ya hali ya mazingira yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua zingine ni kudhibiti matukio ya uchomaji moto wa misitu; kupiga marufuku upandaji wa miti isiyofaa katika maeneo ya vyanzo vya maji; kuendeleza Kampeni ya Taifa na Kupanda na Kutunza Miti; Kuendeleza Program ya Kitaifa ya Elimu ya Mazingira kwa Umma; kuwa na programu za hifadhi ya mazingira na mipango shirikishi ya matumizi bora ya ardhi kwa kila wilaya na kutekeleza na kupiga marufuku uchimbaji holela wa madini kwenye vyanzo vya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua za muda wa kati ni pamoja na kujenga na kuendeleza malambo, visima na mabwawa katika maeneo ya wafugaji na wakulima; kuhuisha na kusambaza kwa mpango kabambe wa matumizi ya ardhi ili uanze kutumika mara moja na kuianisha na kuondoa miti isiyofaa kwenye vyanzo vya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua za muda mrefu ni pamoja na kuendeleza teknolojia sahihi za kuvuna, kuhifadhi na kusambaza maji ya mvua na ya ardhini, kuharakisha matumizi ya njia mbadala za kuzalisha umeme ili kupunguza gharama za umeme kwa watumiaji na hatimaye kupunguza mahitaji ya kuni na mkaa. Aidha, Serikali imeanzisha Tuzo ya Rais ya Kuhifadhi Vyanzo vya Maji, Kupanda na Kutunza Miti. Lengo la tuzo hii ni kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika kuhifadhi mazingira ya ardhi na vyanzo vya maji. Tuzo hii hutolewa kila baada ya miaka miwili.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI Aliuliza:-
Suala la mabadiliko ya tabianchi ni mtambuka na linagusa sekta mbalimbali za kiuchumi na kijamii.
Je, ni mashirika ya umma mangapi yamepokea ruzuku kutoka Wizara/Idara au kwa wafadhili katika kipindi cha miaka mitano iliyopita? Je, nini madhumuni ya ruzuku hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) Alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Immaculate Sware Semesi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
– Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna mashirika ya umma yanayopata ruzuku kutoka kwenye Wizara, Idara au wafadhili.
– Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye kipengele (a), haiwezekani kuelezea madhumuni ya ruzuku ambayo haitolewi.
MHE. JANET Z. MBENE aliuliza:-
Mto Songwe umekuwa ukihama hama kwa sababu ya mabadiliko ya tabianchi huku ukiharibu rasilimali za wakazi wanaoishi karibu na mto huo na kingo zake kutokana na mafuriko.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kudumu kudhibiti uharibifu huo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) napenda kujibu swali la Mheshimiwa Janet Zebedayo Mbene, Mbunge wa Ileje kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mazingira na maumbile ya Bonde la Mto Songwe pamoja na mgawanyiko wa unyeshaji wa mvua katika bonde hilo ndio sababu kubwa inayofanya kuwepo kwa mafuriko ya mara kwa mara kila mwaka. Inakadiriwa kuwa takribani hekta 9,000 za ardhi huathiriwa na mafuriko katika kila msimu wa mvua na kufanya Mto Songwe kubadili mkondo wake mara kwa mara, hivyo kuathiri pia mpaka kati ya nchi za Malawi na Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hali hii, tatizo hili linakuwa kubwa zaidi kutokana na mabadiliko ya tabianchi na ongezeko kubwa la watu katika bonde. Aidha, matumizi mabaya yasiyo endelevu ya rasilimali zilizoko katika bonde husababisha uharibifu mkubwa wa ardhi, vyanzo vya maji, mifumo ikolojia na kutokewa kwa bioanuai zilizo katika bonde hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kushirikiana na Serikali ya Malawi imechukua hatua mbalimbali za kukabiliana na matatizo katika Bonde la Mto Songwe. Hatua hizo ni pamoja na kuanzisha Kamisheni ya Pamoja (Songwe River Basin Commission), ambayo itashughulikia masuala yote ya bonde hilo. Mpaka sasa kuna sekretarieti ya mpito iliyoanzishwa ambayo inaratibu shughuli ya bonge hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, tayari programu ya kuendeleza Bonde la Mto Songwe (Songwe River Basin Development Program) imeshaandaliwa kwa ajili ya utekelezaji. Masuala yaliyoainishwa kwenye programu kwa ajili ya utekelezaji ni kama ifuatavyo; kuendeleza kilimo endelevu, uzalishaji wa umeme kwa kutumia nguvu ya maji, kudhibiti mafuriko ya mto pamoja na kudhibiti kuhamahama kwa mto, uboreshaji wa upatikanaji na usambazaji wa maji, maendeleo ya uvuvi, kukuza utalii na uboreshaji wa mazingira na kuiwezesha kamisheni usimamizi wa pamoja wa rasilimali za Bonde la Mto Songwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na changamoto za mafuriko Sekretarieti ya Mpito ya Bonde kupitia programu hii (Songwe River Development Program) itajenga mabwawa matatu ambayo ni Songwe Chini, Songwe Kati na Songwe Juu. Pamoja na mabwawa hayo kutumika kudhibiti mafuriko pia yatatumika katika kuendeleza kilimo cha umwagiliaji, usambazaji wa maji na shughuli za uvuvi. Vilevile, kutakuwa na mradi wa mazingira ambao utadhibiti kingo za mto (River Banks Stabilization) ili kuufanya mto usihame hame.
MHE. MWANTUMU DAU HAJI aliuliza:-
Kilimo cha Tanzania hutegemea mvua za msimu ambazo kwa kiasi kikubwa zimeathiriwa na mabadiliko ya tabianchi na hivyo kuathiri shughuli za uzalishaji:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantum Dau Haji, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ili kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi katika sekta ya kilimo. Ofisi ya Makamu wa Rais iliandaa mpango wa Taifa wa kuhimili mabadiliko ya tabianchi wa mwaka 2007 na mkakati wa Taifa wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi wa mwaka 2012 katika sekta mbalimbali ikiwemo na sekta ya kilimo.
Mheshimiwa Spika, mipango hii kwa sekta ya kilimo imejikita katika kuendeleza kilimo cha umwagiliaji ikiwa ni pamoja na kutumia teknolojia zinazopunguza upotevu wa maji ili kuepuka kilimo cha kutegemea mvua, kubadili vipindi vya upandaji mazao ya misimu ili kuendana na mabadiliko ya misimu, ikiwa ni pamoja na kupanda mazao na mbegu zinazohimili ukame, kuboresha mbinu za kudhibiti wadudu waharibifu wa mazao na kuweka mifumo mbadala ya kilimo ili kuongeza uzalishaji.
Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Makamu wa Rais imekuwa inashirikiana na wadau wengine ikiwa ni pamoja na Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi katika suala zima la kuleta maendeleo endelevu, ikiwa ni pamoja na masuala ya mabadiliko ya tabianchi katika sekta ya kilimo kwa kuandaa mpango mahususi wa sekta ya kilimo katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, Mpango wa Taifa wa Kilimo Rafiki cha Mabadiliko ya Tabianchi na programu mbalimbali za uendelezaji wa kilimo. Katika utekelezaji wa mipango na programu mbalimbali za uendelezaji wa kilimo.
Mheshimiwa Spika, katika utekelezaji wa mipango na programu hizi katika sekta ya kilimo suala la kuhimili mabadiliko ya tabianchi katika kilimo limezingatiwa hasa kwa kusisitiza uwekezaji katika miundombinu ya kilimo, kuongeza tija kupitia kilimo cha umwagiliaji na teknolojia bora za uzalishaji kupitia kilimo shadidi, kuboresha mfumo wa upatikanaji wa mbegu bora, kuwekeza katika utafiti wa mazao ya kilimo, kutumia sayansi na teknolojia za kisasa katika kilimo kulingana na misimu na hali ya ukame na msingi mingine inayolenga kuweka mbinu mbadala za kuongeza uzalishaji wa mazao ya kilimo.
MHE. NAJMA MURTAZA GIGA aliuliza:-
Kwa muda mrefu sasa Serikali zetu zote mbili zimekuwa kwenye jitihada za kukabiliana na kero za Muungano:-
(a) Je, Serikali inawaambia nini wananchi wa Zanzibar kuhusu ushiriki wa Wizara zisizo za Muungano na Zanzibar kwenye Taasisi za Kimataifa zinazotambua utaifa wa wananchi katika uwakilishi wake?
(b) Je, Serikali inapata ugumu gani kuwafahamisha wananchi kwa uwazi kabisa kila kero za Muungano zinazopatiwa ufumbuzi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Najma Murtaza Giga, Mbunge wa Viti Maalum, lenye vipengele (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo kweli kwamba Wazanzibari kwa muda mrefu wamekuwa na kero ya kutoshirikishwa katika medani za Kimataifa. Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 pamoja na mabadiliko yake, masuala ya mambo ya nje yapo chini ya mamlaka ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo Zanzibar ni sehemu yake. Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imekuwa ikishirikishwa kwa kiasi kikubwa katika taasisi za Kimataifa zinazotambua utaifa wa Tanzania kwenye Wizara zisizo za Muungano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imeshirikishwa katika mikutano ya Kimataifa na taasisi za Kimataifa, kama vile Mikutano ya mabadiliko ya Tabianchi, Mikutano ya Shirika la Kazi Duniani, Mikutano ya Kamisheni ya Hali ya Wanawake, Mikutano ya Shirika la Kazi Duniani, Mkutano kuhusu utekelezaji wa lengo Namba 14 la Maendeleo Endelevu linalohusu Uhifadhi na Matumizi Endelevu ya Bahari na Rasilimali zake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Viongozi wa Mashirika ya Kimataifa waliofanya ziara hapa nchini kwa mwaka 2017, walitembelea pia Zanzibar na kufanya mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ambao ni Wakurugenzi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Mkurugenzi wa FAO, Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Mkurugenzi Mtendaji wa UNAIDS.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kulieleza Bunge lako Tukufu kuwa, Serikali haijawahi kupata ugumu wala kugugumizi katika kuwafahamisha wananchi kwa uwazi kuhusu changamoto zilizopatiwa ufumbuzi na hata zile ambazo ziko katika hatua mbalimbali ya kutafutiwa ufumbuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mwenyewe nikiwa Waziri mwenye dhamana ya Muungano, nimefanya jitihada kubwa za kuwafahamisha wananchi kwa uwazi kabisa kuhusu jitihada za Serikali katika kutatua changamoto za Muungano kupitia vyombo vya habari mfano television, redio na magazeti, makongamano, hotuba za viongozi wakati wa maadhimisho ya Muungano na hata kupitia Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuza:-
Je, ni kwa nini mikakati ya dhati ya Serikali katika kunusuru na kuzuia uchafuzi wa mazingira ya Mto Rubana ambao unaingiza maji yake katika Ziwa Victoria na ni chanzo kikubwa cha maji katika Vijiji vya Tingirima, Kyandege, Mugeta, Mariwanda, Sarakwa, Kihumbu na Hunyari katika Jimbo la Bunda.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS – MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), napenda kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mto Rubana ulioko katika Halmashauri ya Wilaya ya Bunda ni chanzo muhimu cha maji kwa wananchi wa vijiji vilivyoko maeneo unakopita mto na pia kwa shughuli za uhifadhi. Maji ya mto huu hutumiwa na wananchi kwa ajili ya matumizi ya nyumbani, kunyweshea mifugo, kilimo na uvuvi. Aidha, maji ya Mto Rubana hutumiwa na wanyamapori kutoka Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na Pori la akiba la Grumeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia umuhimu wa Mto Rubana kama chanzo cha maji na shughuli za uhifadhi, Serikali imechukua hatu zifuatazo ili kunusuru na kuzuia uchafuzi na uharibifu wa mazingira katika mto huo:-
(i) Kuziagiza Halmashauri za Serengeti, Bunda na Bunda Mjini kuzingatia na kutekeleza kikamilifu Mkakati wa Kuhifadhi Mazingira ya Ardhi na Vyanzo vya Maji wa mwaka 2006 na Mkakati wa Hatua za Haraka za kuhifadhi Mazingira ya Bahari, Ukanda wa Pwani, Maziwa, Mito na Mabwawa wa mwaka 2008 katika maeneo yao ili kuzuia uharibifu wa Mto Rubana.
(ii) Kuendelea kutoa elimu ya uhifadhi wa mazingira kwa viongozi wa Halmashauri za vijiji na wananchi wote wa Kata za Hunyari, na Mugeta kuzingatia Sheria ya Usimamizi wa Mazingira Namba 20 ya mwaka 2004, Sheria ya Misitu Namba 14 ya mwaka 2002 inayozuia ukataji miti ovyo na Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori Namba 5 ya mwaka 2009.
(iii) Kufanya doria za mara kwa mara na kukamata wanaokaidi na kukiuka sheria na kusababisha uharibifu wa mazingira ya mto kwa kukata miti ovyo na uchomaji wa mkaa.
(iv) Kuendelea kujenga na kuboresha miundombinu ya kunyweshea mifugo ili kuzuia wananchi kunyweshea mifugo kwenye mto.
Mheshimiwa Naibu Spika, natoa wito kwa wadau wote ikiwemo viongozi katika ngazi ya Halmashauri, Waheshimiwa Wabunge, viongozi wa Kata na Vijiji na wananchi wote katika maeneo hayo kushirikiana katika kutekeleza mikakati ya Serikali ili jitihada za kunusuru Mto Rubana na kuzuia uchafuzi zifanikiwe kikamilifu.
MHE. JEROME D. BWANAUSI (K.n.y. MHE. HAWA A. GHASIA) aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati mifereji ya maji na matuta ambayo yalijengwa zaidi ya miaka 50 iliyopita katika Mji wa Mikindani ili kupunguza athari ya maji ya bahari kwenye mitaa na makazi ya watu hasa kipindi cha mvua kali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) sasa naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Abdulrahman Ghasia, Mbunge wa Mtwara Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali imeweka mipango ya ukarabati wa mifereji ya maji ya mvua na matuta katika Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Mikindani. Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Mikindani imekuwa ikifanya ukarabati wa mifereji ya maji ya mvua inayoingia baharini katika mji wa Mikindani kila mara mahitaji yanapojitokeza kwa kutumia fedha za mapato ya ndani na Serikali Kuu.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2017/2018 Halmashauri imetuma kiasi cha shilingi milioni tatu kutoka mapato ya ndani ya Halmashauri katika kufanya ukarabati wa mfereji uliopo Kata ya Magengeni. Aidha, kiasi cha shilingi milioni 37 zilitumika kufanya ukarabati wa mfereji katika Kata ya Mtonya, Magengeni na Mitengo kupitia fedha za Mfuko wa TASAF.
Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa ukarabati wa mifereji na matuta, Halmnashauri ya Manispaa ya Mtwara Mikindani imeendelea kutenga fedha kwa ajili ya ukarabati huo. Hivyo, kwa mwaka wa fedha 2018/2019 Halmashauri imetenga kiasi cha fedha shilingi milioni 50 kutoka mapato ya ndani kwa ajili ya kufanya ukarabati wa mifereji kata za Mtonya, Magengeni na Kisungule.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-
Uharibifu wa mazingira kwenye Msitu wa Chome (Shengena) umeleta athari kubwa ya uchafuzi wa maji hasa katika Mito mikubwa ya Yongoma na Saseni; mito hiyo kuanzia kwenye vyanzo vya maji imebadilika rangi na kuonesha rangi yenye matope. Kwa kuwa Wizara ya Maliasili na Utalii ilikanusha kwamba hakuna ushahidi unaoonesha kwamba athari za mazingira katika msitu huo zinatokana na uchimbaji wa madini ya bauxite.
• Je, Serikali ipo tayari kuunda Kamati ya kuchunguza chanzo cha uharibifu huo katika Msitu wa Shengena?
• Je, Serikali ipo tayari kuwapatia wananchi miti ya asili inayoongeza maji ili kudhibiti upungufu wa maji katika vyanzo vya maji mito hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, uharibifu wa mazingira kwenye msitu wa Chome - Shengena unachangiwa na sababu mbalimbali ikiwemo shughuli za kilimo katika maeneo jirani yanayozunguka mlima Shengena na wachimbaji wadogo wa madini ya dhahabu waliovamia msitu huo miaka ya nyuma kati ya mwaka 2008 na 2010. Katika kutatua changamoto hii Serikali iliunda timu ya watalaam kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Baraza la Taifa la Hifadhi ya Mazingira yaani NEMC, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Ofisi ya Madini Mkoa wa Kilimanjaro na Bodi ya Mto Pangani ambayo ilitembelea eneo hilo kwa nyakato tofauti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, timu hiyo ya wataalam ilibaini changamoto za uharibifu wa mazingira katika eneo hilo na kupendekeza hatua za kuzuia uharibifu huo ambazo zimetekelezwa ikiwa ni pamoja na kuzuia shughuli za uchimbaji wa madini ndani ya msitu kwa kuweka ulinzi ambao unafanywa na Jeshi la Kujenga Taifa (SUMA JKT).
Hivyo, Serikali itapitia upya mapendekezo ya timu ya wataalam na kuhakikisha kuwa ina…
hivyo, Serikali itapitia upya mapendekezo ya timu ya wataalam na kuhakikisha kuwa yanatekelezwa kikamilifu na iwapo itaonekana ni lazima kuunda Kamati, Serikali haitasita kufanya hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, Serikali kupitia Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) imeanza kuchukua hatua za kuwapatia wananchi miti ya asili na rafiki kwa mazingira kwa ajili ya kuhifadhi vyanzo vya maji katika Mito ya Yongoma na Saseni. Aidha, katika jitihada za kutunza vyanzo vya maji katika eneo hili, Serikali kupitia TFS imepanda miti ya asili takribani 2500 kati ya mwaka 2012 mpaka 2017 ndani ya eneo la Msitu wa Chome lililoharibiwa na shughuli za uchimbaji wa madini ya dhahabu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nitumie fursa hii kuwasihi viongozi na watendaji wa Serikali katika ngazi zote kuchukua hatua kadri itakavyowezekana kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ili kudhibiti uharibifu wa mazingira nchini.
MHE. MARTHA M. MLATA (K.n.y. MHE. CATHERINE V. MAGIGE) aliuliza:-
Je, Serikali ina mikakati ipi kisheria kushughulikia suala la ulinzi wa maeneo ya vyanzo vya maji ili kunusuru maeneo hayo dhidi ya uvamizi na matumizi mengine yasiyokusudiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Catherine Valentine Magige, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Usimamizi wa Mazingira Na. 20 ya mwaka 2004 katika Ibara ya 7 imeweka misingi ya kisheria ya ulinzi na usimamizi wa mazingira ikiwemo mazingira ya vyanzo vya maji.
Aidha, kifungu cha 57(1) kinaweka katazo la kufanya shughuli za binadamu ndani ya mita 60 kutoka kwenye vyanzo vya maji na kifungu cha 60(3) kinaelekeza Bodi za Maji ya Bonde kuhakikisha kunakuwa na maji ya kutosha kwa mazingira.
Aidha, Sheria ya Usimamizi wa Rasilimali za Maji Na. 11 ya Mwaka 2009 inaelekeza umuhimu wa kutunza na kulinda vyanzo vya maji na rasilimali za maji. Vilevile Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015 – 2020 Ibara ya 152(d) nayo inasisitiza kuhusu umuhimu wa kutunza vyanzo vya maji kwa kuendelea kufanya tathmini ya vyanzo vya maji vilivyohifadhiwa, kubaini vyanzo vipya na kufufua vilivyopotea ama kuharibika ili kuwa na uhakika wa kuwa na maji safi na salama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa kuzingatia sheria hizi na maelekezo haya, Serikali imeweka mikakati mbalimbali ikiwa ni pamoja na mkakati wa kuhifadhi mazingira ya ardhi na vyanzo vya maji kwa mwaka 2006 na mkakati wa hatua za haraka za kuhifadhi mazingira ya bahari ukanda wa Pwani, Maziwa, Mito na Mabwawa wa mwaka 2008.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia mikakati hii, Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo kuhamasisha jamii zinazozunguka vyanzo vya maji; Serikali za Mitaa na Vijiji kushiriki kikamilifu katika jitihada za kuhifadhi vyanzo vya maji; kutoa elimu juu ya umuhimu wa kutunza vyanzo vya maji; kuvitambua vyanzo vya maji na kuviweka mipaka; kuondoa watu waliovamia vyanzo vya maji; kupiga marufuku au kusitisha shughuli zisizo endelevu katika maeneo ya vyanzo vya maji; kuondoa miti isiyo rafiki kwa mazingira; kuondoa mifugo katika maeneo ya vyanzo na kuandaa mipango ya matumizi endelevu ya ardhi katika maeneo ya mabonde.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Tanzania ni mwanachama wa Makataba wa Kimataifa wa Ardhi Oevu (Ramsar Convention) kwa mwaka 1971 na Mkataba wa Kimataifa wa Baioanuai wa mwaka 1992 ambayo moja ya lengo lake ni kuhakikisha vyanzo vya maji vinalindwa ili kuwa na maji ya kutosha kwa kizazi cha sasa na cha baadaye.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa Serikali itaendelea kuhamasisha shughuli za hifadhi ya mazingira hususan kutunza vyanzo vya maji kwa kuendelea kutoa miongozo ya utekelezaji wa sheria na mikakati inayohusiana na kutunza vyanzo vya maji. Aidha, Sekta Binafsi na Mashirika yasiyo ya Kiserikali wataendelea kuhamasishwa kutekeleza mikakati inayolenga kuhifadhi mazingira ya vyanzo vya maji kwa vizazi vya sasa na vya baadaye. (Makofi)
MHE. MBAROUK SALIM ALI aliuliza:-
Pamoja na jitihada za Serikali katika kutatua kero za Muungano bado kuna manung’uniko mengi kuhusiana na Muungano huu:-
Je, ni kero ngapi mpaka sasa zimeshapatiwa ufumbuzi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, sasa napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbarouk Salim Ali, Mbunge wa Wete, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijamjibu napenda nielezee kidogo maneno mawili ambayo kwenye Muungano yanachanganywa. Suala la kero na suala la changamoto. Sisi ambao tunashughulika na masuala ya Muungano, Muungano huwa una changamoto, huwa hauna kero. Kwa hiyo mara nyingi maswali yanayokuja Waheshimiwa Wabunge wanapenda kutumia neno kero, nawaomba tuwe tunatumia neno changamoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya kuwepo kwa changamoto chache za Muungano, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge, Bunge lako Tukufu na Watanzania kwa ujumla kuwa Muungano wetu uko imara na changamoto ambazo zimekwishapatiwa ufumbuzi hadi sasa ni (11).
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA aliuliza:-
Milima ya Uluguru ni chanzo kikubwa sana cha maji katika mito na vijito vingi ambavyo husaidia kwa kiwango kikubwa upatikanaji wa maji safi na salama katika Mkoa wa Morogoro, Pwani na Dar es Salaam. Hata hivyo, kutokana na uharibifu wa mazingira uliosababishwa na ujenzi holela, kilimo na ufugaji, mito hiyo imeanza kukauka hivyo kusababisha adha kubwa ya upatikanaji wa maji kwa wananchi:-
Je, Serikali ina mipango gani ya kimkakati ya kuilinda milima hiyo isiendelee kuharibiwa na kuhakikisha miti iliyokatwa inapandwa mingine ili kuhifadhi vyanzo vya maji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, sasa napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Jasmine Tisekwa Bunga, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Tisekwa ambaye amekuwa akifuatilia sana masuala ya mazingira. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hilo sasa; Milima ya Uluguru ni mojawapo ya Milima ya Tao la Mashariki (Eastern Arc Mountains) yenye ikolojia ya kipekee na bioanuai adhimu; ni mojawapo ya vyanzo vikuu vya maji ya Mto Ruvu unaohudumia wakazi wa Mkoa wa Dar es Salaam, Pwani na Morogoro. Kwa kuzingatia umuhimu huo, Serikali kupitia taasisi zake na kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo imeendelea kuchukua jitihada mbalimbali za kuitunza na kuihifadhi Milima ya Uluguru. Jitihada hizo ni pamoja na:-
Kwanza, kuanzisha Mfuko wa Hifadhi ya Tao la Mashariki (Eastern Arc Mountains Conservation Endowment Fund) wa mwaka 2002 kwa lengo la kusaidia juhudi za uhifadhi wa Milima ya Tao la Mashariki ikiwemo Milima ya Uluguru. Jumla ya dola za kimarekani milioni 2.4 zilitumika kuanzisha na kuendesha shughuli za mfuko huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi sasa Mfuko huu ni mojawapo ya vyanzo vikuu vya fedha kwa taasisi za Serikali, Mamlaka za Serikali za Mitaa, Asasi za Kiraia na vikundi vinavyojihusisha na juhudi za uhifadhi wa Milima ya Tao la Mashariki. Kila mwaka kiasi cha shilingi milioni 50 hutolewa kwa wadau wa uhifadhi wa mazingira kwa njia za ushindani.
Pili, mwaka 2008, Serikali ilitangaza kupitia gazeti la Serikali namba 296 eneo lenye jumla ya hekari 24,115 kuwa hifadhi asilia (nature reserve) na kuanzisha mamlaka rasmi ya kusimamia eneo hilo la Milima ya Uluguru. Kupitia mamlaka hiyo, uhifadhi wa Milima ya Uluguru umeendelea kuimarika kwa kuanzishwa na kuimarishwa kwa Kamati za Maliasili na Mazingira katika vijiji vyote 62 vinayozunguka hifadhi hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, juhudi nyingine ni pamoja na kuweka upya alama za mipaka (beacons), kufanya tafiti mbalimbali, kuimarisha utalii, kupanda miti na kuingia makubaliano ya ushirikiano wa uhifadhi wa vijiji hivyo.
Tatu, kupitia Mamlaka ya Bonge la Wami – Ruvu ambalo linahusisha Mlima Uluguru, Serikali inaendelea na utekelezaji wa mradi wa miaka mitano (2016-2021) uitwao Securing Watershed Services Through Sustainable Land Management.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia mradi huu, Serikali imetenga jumla ya dola za kimarekani 22,000,000 huku wafadhili wengine (UNDP na GEF) wakichangia jumla ya dola za kimarekani 5,648,858 na kufanya mradi huu kuwa na gharama ya dola za kimarekani 27,648,858. Sehemu ya fedha hizi zinatumika katika juhudi za uhifadhi katika maeneo yaliyo nje ya hifadhi asilia (Uluguru Nature Reserve). (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI aliuliza:-
Mataifa makubwa duniani yanayoongoza kwa kuharibu mazingira, kwa kushirikiana na Umoja wa Mataifa na mifuko kama vile Climate Investment Funds (CIF), Global Environment Facility (GEF), Green Climate Fund (GCF) na kadhalika wamekuwa wakitenga fedha kwa ajili ya kusaidia nchi zinazoendelea kukabiliana na madhara ya mabadiliko ya tabianchi. Je, Taifa limejipangaje kunufaika na fedha za mifuko hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote niombe radhi kwa sauti, lakini pia kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kusimama kwenye Bunge lako tukufu naomba nichukue fursa hii kutoa shukrani zangu za dhati.
Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pia nimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuniamini na kuniteua kuwa Naibu Waziri kwenye Ofisi ya Makamu wa Rais kushughulikia Muungano na Mazingira. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimshukuru Makamu wa Rais Mama yetu mama Samia Suhulu na wafanya kazi wote wa Ofisi yetu ya Wizara yetu kwa ushirikiano mkubwa wanaouonesha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Waziri Mkuu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano mkubwa ambao anauonesha kwetu. Lakini nisisahau kuwashukuru wananchi wa Jimbo langu la Singida Mjini pamoja na familia yangu kwa ushirikiano wanaouonesha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa baada ya shukrani hizo kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira nijibu swali la Mheshimiwa Cosato David Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuendeleza kunufaika na fedha kutoka katika Mifuko ya Kitaifa ya Mabadiliko ya tabianchi, Serikali imejipanga kwa kuandaa mkakati wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi wa mwaka 2012 na inakamilisha Mpango wa Taifa wa kuhimili mabadiliko ya tabianchi, kukamilika kwa mkakati huo kwa mpango huo utaiwezesha nchi kunufaika na fedha kutoka mifuko hiyo. Mkakati wa mpango huo umeainisha maeneo ya kipaumbele kwa ajili ya kuandaa miradi ya kukabiliana na mabaliko ya tabianchi ambayo imeombewa fedha na utekelezaji kutoka katika mifuko hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kutumia fursa hii kulifahamisha Bunge lako Tukufu kuwa Tanzania tayari imeanza kunufaika na fedha za mifuko hiyo kupitia mfuko wa GEF, tunatekeleza miradi mbalimbali ikiwa ni pamoja na miradi ya kurejesha ardhi iliyoharibika na kuongeza usalama wa chakula katika maeneo kame ya Tanzania ambapo tumepata dola za Kimarekani 7,155,963 na mradi wa kuhimili mabadiliko ya tabianchi kupitia mfumo ikolojia katika maeneo ya vijiji nchini Tanzania tuliopata dola za Kimarekani 7,571,233.
Aidha, kwenye mfuko wa GEF katika mzunguko wake wa sita zilitengwa dola za Kimarekani milioni mbili ambazo zinatumika kwa ajili ya kutekeleza miradi midogo midogo ya nchi. Mfuko wa GCF ulianzishwa mwaka 2011 na ulianza kutoa fedha mwaka 2015. Kwenye mfuko huo Tanzania ilitarajia kupata dola za Kimarekani 124 kwa ajili ya mradi wa maji wa Simiyu unaotekelezwa chini ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha Tanzania inakamilisha utaratibu wa kupata dola za Kimarekani 300,000 kutoka GCF; ambazo zinatumika kujenga uwezo kwa Taasisi zetu ili ziweze kuandaa miradi itakayofadhiliwa na mfuko huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Climate Investment Fund inajumuisha mifuko miwili iliyoanzishwa mwaka 2008, mifuko hiyo ni Clean Technology Fund na Strategic Climate Fund. Mdhamini wa mifuko hii ni Benki ya Dunia, mifuko hii hutoa mikopo yenye riba nafuu kwa nchi zinazoendelea na kwa ajili kutekeleza miradi ya kupunguza uzalishaji wa gesi joto ambayo siyo kipaumbele cha nchi za Afrika ikiwemo Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Makamu wa Rais itaendelea kukuza uelewa na kuhamasisha sekta mbalimbali kutekeleza mkakati wa mabadiliko ya tabianchi kwa kuandaa miradi ambayo inakidhi vigezo vya vifuko hii ili Taifa liendelee kunufaika na fedha hizi. Aidha, Serikali kupitia taasisi zake mbalimbali imefanya tijihada za kujisajili yaani accreditation na Mfuko wa Mabadiliko wa Tabianchi ili taasisi hizi ziweze kuwasilisha maombi ya fedha hizo moja kwa moja kutoka mifuko hiyo. Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
MHE. PAULINE P. GEKUL aliuliza:-
Ziwa Babati limejaa magugu maji na Halmashauri haina bajeti ya kusafisha ziwa hilo kwa maana ya kuondoa magugu hayo. Je, ni lini Serikali itasaidia kuondoa magugu hayo ili kulinusuru ziwa hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Pauline Gekul, Mbunge wa Babati Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, magugu maji ni moja ya viumbe vamizi wageni (Invasive Alien Species) ambayo ni moja ya changamoto kubwa inayokabili mazingira yetu nchini. Baadhi ya maeneo yaliyoathirika na mimea ya aina hi ni pamoja na Ziwa Jipe, Ziwa Victoria, Hifadhi ya Bonde la Ngorongoro. Athari za mimea vamizi wageni kama magugu maji ni kusambaa kwa kasi katika eneo lilivamiwa pamoja na kusababaisha kutoweka kwa baionuai asili katika eneo husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kubaliana na tatizo hili, nchini Ofisi ya Makamu wa Rais imeitisha mkutano wa wadau uliofanyika terehe 4 Septemba, 2018 ili kushirikiana na wadau katika kutafuta ufumbuzi wa kukabiliana na tatizo hili kitaifa ikiwa ni pamoja na Ziwa Babati. Mkakati huu utakuwa ni muendelezo wa mkakati wa Kitaifa wa kuhifadhi mazingira ya pwani, bahari, maziwa, miti, mabwawa wa mwaka 2008.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mkutano huo wa wadau umeandaa mapendekezo ya hatua za kuchukua kitaifa kukabiliana na nchangamoto za uharibinfu wa mazingira unaotokana na mmea vamizi wageni katika magugu maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua juhudu za Halmashauri ya Babati na Bonde la Maji la Kati ambapo imeandaa andiko la mradi unaoihusu uhifadhi wa mfumo wa ikolojia wa Ziwa Manyara ambapo Ziwa Babati ni moja ya sehemu ya mfumo wa ikolojia hiyo. Katika andiko hilo, uondoaji wa magugu maji katika Ziwa Babati ni moja ya shughuli za mradi huo. Serikali inaendelea na utaratibu stahiki kuwashirikisha washirika wa maendeleo kupata fedha za kutekeleza mradi huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, juhudi izngine zilizochukuliwa na Halmshauri ya Mji wa Babati ni pamoja na kuweka mabango ya makatazo ya shughuli za binadamu ndani ya mita 60 ya eneo la ziwa. Mabango 20 yaliwekwa maeneo yaliyozunguka Ziwa Babati, kutoa elimu ya hifadhi ya mazingira na kuhimiza kilimo cha makingamaji katika maeneo ya Kata za Bagala, Babati, Mangala, Singe na Bonga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kudhibiti shughuli za kilimo na ufugaji katika eneo la Ziwa Babati na vilevile Halmashauri ya Mji wa Babati imepata Muwekezaji wa shughuli za kitalii karibu na eneo la Ziwa Babati na moja ya makubaliano ni kuondoa magugu maji katika eneo la ziwa hilo. Taratibu za kufikia makubaliano zinaendelea na Ofisi ya Makamu wa Rais itashirikiana na Halmashauri husika kwa kutoa wataalam wakati wa kuondoa magugu maji katika ziwa hilo.
MHE. MWATUM DAU HAJI aliuliza:-
Kilimo cha Tanzania hutegemea mvua za msimu ambazo kwa kiasi kikubwa zimeathiriwa na mabadiliko ya tabianchi na hivyo kuathiri shughuli za uzalishaji.
Je, Serikali ina mpango gani wa kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, (Muungano na Mazingira), napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwatum Dau Haji, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi katika Sekta ya Kilimo, Ofisi ya Makamu wa Rais iliandaa Mpango wa Taifa wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi wa mwaka 2007 na Mkakati wa Taifa wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi wa mwaka 2012 katika sekta mbalimbali ikiwemo na sekta ya kilimo. Mipango hii kwa sekta ya kilimo imejikita katika kuendeleza kilimo cha umwagiliaji ikiwa ni pamoja na kutumia teknolojia zinazopunguza upotevu wa maji ili kuepuka kilimo cha kutegemea mvua.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, mipango hii inaelezea namna ya kubadili vipindi vya upandaji mazao ya misimu ili kuendana na mabadiliko ya misimu ikiwa ni pamoja na kupanda mazao na mbegu zinazohimili ukame, kuboresha mbinu za kudhibiti wadudu waharibifu wa mazao na kuweka mifumo mbadala ya kilimo ili kuongeza uzalishaji. Aidha, Ofisi ya Makamu wa Rais ipo katika mchakato wa kukamilisha kuandaa mpango endelevu wa Kitaifa wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi (National Adaptation Plans). Mpango huu utakapokamilika utawezesha nchi kuwa na mipango itakayowezesha kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi katika sekta muhimu ikiwemo sekta ya kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Makamu wa Rais imekuwa inashirikiana na Wizara ya Kilimo pamoja na Wizara ya Maji na Umwagiliaji katika kuandaa mipango ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi katika Sekta ya Kilimo. Mipango iliyoandaliwa ni pamoja na:-
Moja, Mpango Mahususi wa Sekta ya Kilimo katika Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi (Tanzania Agriculture Climate Resilience Plan); pili, Mpango wa Kitaifa wa Kilimo Rafiki cha Mabadiliko ya Tabianchi (National Climate Smart Agriculture) na programu mbalimbali za uendelezaji wa kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika utekelezaji wa mipango na programu hizi katika sekta ya kilimo, suala la kuhimili mabadiliko ya tabianchi katika kilimo imezingatiwa hasa kwa kusisitiza uwekezaji katika miundombinu ya kilimo (suala la kuongeza kilimo cha umwagiliaji).
MHE. HAWA A. GHASIA aliuliza:-
Je, Serikali inaweza kutuambia ni nini hasa kinachosababisha uharibifu wa mazingira kwa kiwango kikubwa kati ya sheria na usimamizi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Abdulrahman Ghasia, Mbunge wa Mtwara Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Usimamizi wa Mazingira, Sura ya 191 Kifungu cha 11(1), 13(1), 14, 16(1) na 30 imeainisha mfumo wa kitaasisi wa usimamizi wa mazingira nchini. Ofisi ya Makamu wa Rais ina jukumu la kuratibu na kuna wasimamizi mbalimbali wa utekelezaji katika ngazi tofauti. Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) linasimamia utekelezaji na uzingatiaji wa sheria kwa ujumla. Aidha, Wizara za Kisekta na Serikali za Mitaa zina jukumu la kusimamia hifadhi ya mazingira kulingana na wajibu na maeneo wanayosimamia.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunazo sheria za kutosha zinazohusu usimamizi wa mazingira. Pamoja na Sheria Mama ya Mazingira Na.20 ya mwaka 2004, pia tunazo sheria zifuatazo ambazo ni muhimu katika hifadhi ya mazingira. Sheria ya Madini (2010); Sheria ya Usimamizi wa Rasilimali za Maji (2009); Sheria ya Afya ya Jamii (2009); Sheria ya Afya na Usalama Mahala pa Kazi (2003); Sheria ya Viwanda vya Kemikali na Wanunuzi wa Kemikali (2003); Sheria ya Uvuvi (2003); Sheria ya Chakula, Dawa na Vipodozi (2003); Sheria ya Misitu (2002); Sheria za Ardhi Na.4 na Na.5 (1999); Sheria ya Ulinzi wa Mimea (1997); na Sheria ya Hifadhi ya Bahari na Maeneo Tengefu (1994). Hivyo, tunahimiza usimamizi wa sheria hizi ili kulinda mazingira.
Mheshimiwa Naibu Spika, uharibifu wa mazingira kwa kiwango kikubwa unasababishwa na kukosekana kwa usimamizi thabiti wa shughuli za hifadhi ya mazingira katika ngazi za halmashauri unaochangiwa na kutokuwa na GFS Code kwa ajili ya kutenga fedha za hifadhi ya mazingira katika bajeti za Serikali za Mitaa. Aidha, uelewa wa wananchi kujua wajibu wao wa kuhifadhi mazingira bado ni tatizo. Pia uharibifu wa mazingira huchangiwa na ongezeko la idadi ya watu linalopelekea kuongezekana kwa mahitaji ya rasilimali kama vile matumizi ya ardhi katika vyanzo vya maji, ukataji wa misitu na pia uelewa mdogo wa jamii kuhusu Sera, Sheria na Kanuni za Hifadhi ya Mazingira.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nitumie fursa hii kuwaagiza watendaji wa ngazi zote kuchukua hatua kadri itakavyowezekana kusimamia utekelezaji na uzingatiaji wa sheria hizi ili kudhibiti uharibifu wa mazingira kwa ujumla.
MHE. SAADA MKUYA SALUM aliuliza:-
Kati ya mambo yaliyokubalika katika mkakati wa kutatua changamoto za Muungano ni pamoja na kugawana ajira zilizopo katika Taasisi za Muungano kwa asilimia 21 (Zanzibar) na asilimia 79 (Tanzania Bara):-
Je, ni kwa kiasi gani mkakati huo umetekelezwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saada Mkuya Salum, Mbunge wa Welezo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwongozo wa ajira katika Taasisi za Muungano wa asilimia 21 kwa Zanzibar na asilimia 79 kwa Tanzania Bara unatekelezwa kwa mujibu wa waraka wa Serikali Kumb.Na.CDA279/350/01/D/95 wa tarehe 10 Mei, 2013. Tangu kutolewa kwa mwongozo huo, umetekelezwa kwa asilimia 82.7 kwa Tanzania Bara na asilimia 18 Tanzania Zanzibar.
Changamoto iliyopo katika kupata taarifa sahihi za Wazanzibari wanaopata ajira katika Taasisi za Muungano ni kutokana na anuani zao za Zanzibar badala ya wengi wanaotumia anuani za Mikoa ya Tanzania Bara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Taasisi zote za Muungano zina mwongozo wa utekelezaji wa makubaliano hayo na zinaendelea kuzingatia utaratibu huo pindi wanapopata fursa ya kuajiri.
MHE. MWATUM DAU HAJI aliuliza:-

Kuna baadhi ya Askari Polisi kupandishwa vyeo lakini hawapati stahili zao kama inavyotakiwa:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia askari hao stahiki zao?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwatum Dau Haji, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa upandishaji vyeo kwa Askari Polisi hutekelezwa kwa kufuata sheria, kanuni na taratibu za Jeshi la Polisi ikiwemo kupandishwa vyeo baada ya kuhudhuria na kufaulu mafunzo stahiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe kuwa Jeshi la Polisi kama ilivyo kwa Wizara na Idara nyingine za Serikali lilihusika na zoezi la uhakiki wa watumishi, zoezi ambalo pia lilisitisha marekebisho yoyote kwenye daftari la mishahara, ajira mpya pamoja na upandishwaji vyeo kwa Watumishi wa Serikali. Baada ya zoezi hilo kukamilika tayari Maofisa, Wakaguzi na Askari wa vyeo mbalimbali zaidi ya 8,440 waliokuwa na madai mbalimbali yakiwemo stahiki za kupandishwa vyeo wamesharekebishiwa mishahara na stahili zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Maofisa, Wakaguzi na Askari wa vyeo mbalimbali wapatao 2,143 kati ya 3,089 waliopandishwa vyeo mwezi Juni, Septemba na Disemba, 2018 wamerekebishiwa mishahara yao. Hata hivyo taratibu za kukamilisha kuwarekebishia Askari waliobaki zinaendelea ili kuhakikisha kuwa Askari wote waliopandishwa vyeo wanarekebishiwa mishahara yao kulingana na vyeo vyao vipya.
MHE. ANNA R. LUPEMBE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga Gereza la Wilaya ya Mlele?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa nchini kuna wilaya 51 ambazo hazina Magereza ya Mahabusu ya Wilaya ikiwemo Wilaya ya Mlele. Lengo la Serikali ni kuhakikisha kila Wilaya nchini inakuwa na Gereza la kuhifadhi wahalifu wa wilaya husika. Vilevile ujenzi wa Magereza kwenye kila wilaya utapunguza gharama za kuwasafirisha wahalifu kutoka Wilaya moja kwenda nyingine kusikiliza kesi zao pamoja na kuhakikisha usikilizwaji wa kesi zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa Serikali inaendelea na ujenzi wa Magereza mapya kwa awamu kwenye wilaya zisizokuwa na Magereza. Hivyo, ni lengo la Serikali kuendelea na ujenzi huo kwenye Wilaya zote zisizokuwa na Magereza ikiwemo Wilaya ya Mlele kadri hali ya bajeti itakavyoruhusu.
MHE. FELISTER A. BURA aliuza:-

Kituo cha Polisi Chipanga kilijengwa kwa nguvu za wananchi takribani miaka 18 iliyopita:-

Je, ni lini kituo hicho kitafunguliwa na kutoa huduma kwa wananchi?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Felister Aloyce Bura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Kituo cha Polisi Chipanga kilichopo Wilaya ya Bahi Mkoa wa Dodoma kilijengwa muda mrefu kwa nguvu za wananchi wa eneo hilo, lakini baadaye jengo hilo lilipangiwa matumizi mengine ya makazi ya Walimu hadi ilipofika mwezi Februari, 2017. Baada ya jengo hili kutumika kama makazi kwa muda mrefu, maeneo mengi yanahitaji marekebisho ili kuweza kukidhi mahitaji ya kutumika kama Kituo cha Polisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tathmini ya maeneo yanayohitajika kufanyiwa ukarabati ni milango, madirisha kuvuja na nyufa katika paa, vyoo, vyumba viwili vya ofisi, chumba cha mahabusu na chumba cha kuweka silaha kwani kwa sasa kilivyo hakiwezi kutumika na kutoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wananchi maeneo mbalimbali nchini wana mwamko wa kujenga Vituo vya Polisi ambayo kwa namna moja au nyingine Serikali imekuwa ikivimalizia na kwa kuwa mahitaji ya kufanya ukarabati wa vituo nchini ni makubwa, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa Serikali kupitia Jeshi la Polisi, itaendelea kufanya juhudi mbalimbali ili kuweza kukimalizia kituo hicho na kianze kutoa huduma kwa wananchi wa Chipanga.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB aliuliza:-

Kumekuwa na kilio cha uchakavu wa vituo vya polisi kwa upande wa Unguja na Pemba:-

(a) Je, ni vituo vingapi vipya vya polisi vilivyojengwa kwa upande wa Unguja na Pemba?

(b) Je, vituo hivyo vimejengwa na kampuni gani na ni vigezo gani vilivyoangaliwa katika ujenzi wa vituo hivyo?

(c) Je, ni lini Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara watafuatana nami kwenda kuviona vituo hivyo vilivyochakaa?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jaku Hashim Ayoub, Mbunge wa Baraza la Wawakilishi, lenye sehemu (a), (b) na (c), kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mikoa ya Unguja na Pemba vituo vingi vimejengwa au kukarabatiwa katika miaka tofauti, vikiwemo Vituo vya Mwembe Madafu na Mbweni katika Mkoa wa Mjini Magharibi, Kituo cha Mchanga Mdogo Mkoani Kaskazini Pemba, Vituo vya Chwaka na Jambiani Mkoa wa Kusini Unguja na Vituo vya Chakechake na Mtambile Mkoa wa Kusini Pemba. Aidha, kuna ujenzi unaoendelea kwa sasa wa Vituo vya Chukwani, Dunga na Mkokotoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, majengo mengi ya vituo hivi vya polisi ujenzi ulikuwa ni wa ushirikiano wa wananchi na Jeshi la Polisi. Hata hivyo, tunatambua mkandarasi aitwaye Albatina Construction Company Ltd anayejenga Kituo cha Polisi Mkokotoni ambaye kazi yake bado inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua kuwepo na uchakavu wa vituo vingi vya polisi katika Mikoa ya Unguja na Pemba kama vile vituo vya Mkoani Pemba, Kengeja, Micheweni, Konde, Mahonda, Nungwi, Kiwengwa na Kiboje ambapo hali ya kifedha ikiruhusu vitakarabatiwa. Viongozi wa Wizara wataambatana na Mheshimiwa Mbunge Jaku Hashim Ayoub tarehe 3/7/2019 kwenda kuviona vituo hivyo vilivyochakaa.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA aliuliza:-

Baadhi ya wanawake huingia gerezani wakiwa na ujauzito na hivyo kujifungulia gerezani.

(a) Je, ni huduma gani wanazopata ili kuhakikisha wanajifungua salama?

(b) Je, ni jitihada gani zinafanywa ili kuwapatia akina mama hao vyakula vinavyopendwa na wajawazito?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Angelina Adam Malembeka, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Magereza limekuwa likihifadhi wafungwa wa aina zote wakiwemo wafungwa wa kike wajawazito. Katika kuhakikisha kwamba wafungwa wajawazito wanajifungua salama, Jeshi la Magereza limekuwa likitoa huduma za afya, chanjo na kuhakikisha wanahudhuria kliniki za mama wajawazito katika vituo vya afya vya magereza na pale inapobidi kuwapeleka hospitali za Serikali.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Magereza limekuwa likiwapatia wafungwa wajawazito vyakula wanavyovihitaji kiafya kwa kuzingatia maelekezo na ushauri wa Daktari wa gereza ili kuhakikisha afya ya mama na mtoto inalindwa. Aidha, Serikali inazidi kuboresha bajeti ya huduma hizo ili kuhakisha kwamba wafungwa wajawazito wanapata huduma hizo inavyostahili.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-

Mgogoro wa ardhi kati ya Jeshi la magereza na wananchi wa Kata ya Ukondamayo hususan Kijiji cha Tumaini umedumu kwa muda mrefu sasa.

Je, Serikali inachukua hatua gani kutatua na kumaliza mgogoro huu?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI (K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukujulisha kwambakwa sasa hakuna mgogoro wa ardhi kati ya kata ya Ukandamoyo hususani kijiji cha Tumaini na gereza la ilimo Urambo. Ni kweli hapo awali ulikuwepo mgogoro baina vya vijiji vinne mojawapo kijiji cha tumaini, Mgogoro huo ulitatuliwa na kuhitishwa mwaka 200 kwa kuhutimishwa mwaka 2000 kwa kushirikishwa viongozi kutoka wizira ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Wizara ya Ardhi, Jeshi la Magereza, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya Urambo na Serikali ya vijiij vyote nine vilivyokuwa na mgogoro kikiwemo Kijiji cha Tumaini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hitimisho la mgogoro huo ni baada ya Jeshi la magereza kukubali kuotka eneo la jumla ya ekari 3,218 kwa vijiji vilivyokuwa na mgogoro mojawapo kijiji cha Tumaini wakapewa ekari 505, Imalamakoye ekari 195, Nsendakanoge ekari 1,655 na Itebulanda ekari 860.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha hati ya makubaliano ya hitimisho la mgogoro ilisainiwa na viongozi wa vijiji vyote vinne vilivyokuwa na mgogoro kikiwemo kijiji cha Tumaini na mawe ya mipaka yaani beacons yakawekwa upya kwa utambulisho wa namba Uv 66, Uv 69, Uv 107, Uv 35 na Uv 108.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB aliuliza:-

Kituo cha Polisi cha Malindi kilichopo Unguja ni kituo cha kihistoria na cha mfano, lakini kituo hicho tangu kimejengwa na wakoloni hakijawahi kufanyiwa ukarabati na kwa sasa kiko taabani:-

(a) Je, ni lini Kituo hicho kitafanyiwa ukarabati?

(b) Je, ni bajeti kiasi gani inahitajika kwenye ukarabati wa kituo hicho?

(c) Je, Serikali haioni kuwa kituo hicho kitavunjiwa hadhi yake ya kihistoria?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jaku Hashim Ayoub, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, jengo linalotumika kama Kituo cha Polisi Malindi ni moja ya majengo ya zamani yaliyojengwa enzi za mkoloni ambayo yanasimamiwa na Idara ya Mamlaka ya Hifadhi na Uendelezaji wa Mji Mkongwe ambayo inapata msaada kutoka Shirika la UNICEF. Jeshi la Polisi linashirikiana na wataalamu wa Idara ya Mamlaka ya Hifadhi na Uendelezaji wa Mji Mkongwe kuona ni namna gani ukarabati wa jengo hilo utafanyika kwa kuzingatia Sheria ya Uhifadhi na kuendeleza Mji Mkongwe.

Mheshimiwa Spika, tathmini ya ukarabati wa jengo hilo inatarajiwa kufanyika hivi karibuni baada ya makubaliano ya wataalamu wa Jeshi la Polisi na wataalamu wa Idara ya Mamlaka ya Hifadhi na Uendelezaji wa Mji Mkongwe.

Mheshimiwa Spika, ili kulinda historia ya jengo hili taratibu na kanuni za Idara ya Mamlaka ya Hifadhi na Uendelezaji wa Mji Mkongwe zitafuatwa na kutekelezwa.
MHE. ALHAJ ABDALLAH M. BULEMBO aliuliza:-

Mnamo tarehe 20 Mei, 2019 Kampuni ya Ultimate Security iliuzwa kwa asilimia mia moja kwa kampuni ya Garda World nchini Canada.

Je, Kampuni ya Garda World inatumia leseni ya kampuni ya ulinzi ya Ultimate Security au imeomba kubadili leseni ili isomeke kampuni mpya?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Alhaji Abdallah Majura Bulembo, Mbunge wa Kuteuliwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa Kampuni ya Garda World ya Canada imeinunua Kampuni ya Ulinzi ya Ultimate Security. Aidha, kwa kuwa Garda World imeinunua Ultimate Security kwa asilimia mia moja na kwa kuwa kibali cha Ultimate Security bado kipo hai, Garda World wanaendelea kukitumia kwa mujibu wa taratibu na kanuni zinavyoelekeza.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa jina la Garda World linatumika kama chapa (brand) ya kibiashara tu na limesajiliwa BRELA kama taratibu zinavyoelekeza.
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati Gereza Kuu Kitai lililopo Wilaya Mbinga?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Martin Msuha, Mbunge Wa Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Gereza Kuu Kitai ni miongoni mwa Magereza ya wazi lililojengwa kwa lengo la shughuli za kilimo na mifugo. Hata hivyo, Serikali inatambua tatizo la uchakavu hususani uzio wa Gereza uliozungushiwa kwa waya (Barbed Wire Fence) na nguzo za miti ambazo zimekuwa zikishambuliwa mara kwa mara na mdudu mchwa.

Mheshiwa Spika, katika kutambua tatizo la uchakavu huo, Serikali ina mpango wa kuyafanyia ukarabati mkubwa majengo na miundombinu ya magereza nchini likiwemo Gereza Kuu Kitai kwa kuzungushia Uzio kwa tofali na ukarabati wa mabweni ili kuboresha huduma za wafungwa na mahabusu.

Mheshimiwa Spika, aidha, ukarabati na uboreshaji wa miundombinu hiyo imepangwa kutekelezwa kwa awamu kwa kutegemea na upatikanaji wa rasilimali fedha.