Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Kangi Alphaxard Lugola (54 total)

MHE. ALBERT O. NTABALIBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Uharibifu wa vyanzo vya maji katika Taifa letu la Tanzania ni mkubwa mno. Namshukuru Mheshimiwa Waziri amesema vizuri kwamba sheria tunazo lakini namna ya kusimamia hizo sheria ili vyanzo visiharibike ndiyo hafifu. Je, Wizara sasa inajipambanua vipi kuhakikisha vyanzo vya maji vinalindwa kwa nguvu zote hapa nchini Tanzania?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna wakati ambao Serikali ya Awamu ya Tano imejipambanua kulinda vyanzo vya maji kwa nguvu zote ni Serikali ya Mheshimiwa Magufuli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuhakikishie wewe na Watanzania wote wanaotusikiliza, Mheshimiwa Makamu wa Rais aliunda Task Force ikaenda kwenye Great Ruaha ambako walikuwa wanaharibu vyanzo vya maji kuhakikisha kwamba wanafanya usimamizi, kutoa mafunzo na kuwaelekeza wananchi. Pia tumeenda Bonde la Usangu na Ihefu, tumeondoa wafugaji wote kwa maana ya kutumia nguvu kubwa kuhakikisha kwamba vyanzo vya maji vinaimarika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wangu Mheshimiwa Januari Makamba, ule Mto wa pale Katavi ambao ulikuwa umeziba kabisa, Mto Kachima, alienda pale akakuta mkulima mmoja ameweka banio amezuia maji viboko wanataka kufa njaa na watumiaji wengine hawana maji, akazibua na sasa maji yanaendelea kutoka. Kwa hiyo, tutaendelea kutumia nguvu na sheria kuhakikisha kwamba hakuna atakayevunja sheria. Yeyote atakayevunja sheria hatasalimika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenu ninyi nitoe darasa la MEMKWA kwa wale walioikosa yaani Mpango Maalum kwa Walioikosa. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria niliyoisema Na.20 ya mwaka 2004, kifungu cha 57, Waziri anaweza akatoa kibali kwenye maeneo ya mita 60 kutokana na changamoto aliyoiona. Ndiyo maana wakati mwingine mnaona hoteli zinajengwa ndani ya mita 60 ni kutokana na vibali. Kwa hiyo, Rais wetu hajavunja sheria na ninyi mtakapowachochea wananchi kuvunja sheria, sheria ya Rais Magufuli itapambana na ninyi. Ahsante sana. (Kicheko/Makofi)
MHE. PETER J. SERUKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majawabu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina swali moja la nyongeza. Mto Makere hali yake ni mbaya sana pamoja na Mto Malagarasi, lakini sababu kubwa kuna mifugo mingi sana imeingia huko na hakuna anayeitoa. Nataka kujua ni lini sasa Serikali tutakwenda kutoa mifugo iliyovamia kwenye vyanzo vya Mto Makere pamoja na Mto Malagarasi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabla sijajibu swali la nyongeza, nitoe maelezo ya utangulizi. Wananchi wote nchi nzima kwa mujibu wa Sheria yetu ya Na.20 ya mwaka 2004 ya Usimamizi wa Uhifadhi wa Mazingira kila Mtanzania ana wajibu wa kutunza na kuhifadhi mazingira. Sheria yetu pia inatoa haki kwa kila Mtanzania aishi katika mazingira safi, salama na ya kiafya. Kwa hiyo, sheria inazuia watu wengine wasiwakere watu wengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mto Makere ni kweli kabisa kwamba mto ule kwenye vyanzo vyake ulivamiwa lakini uvamizi ule ulikuwa unafanywa na wale wahamiaji haramu ambao wanakuja kule Kasulu, wanawakodi wananchi wa Kasulu halafu wengine wanaenda wanakata miti usiku wengine wanalima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kwa kushirikiana na Mamlaka za Serikali za Mitaa, Halmashauri ya Mji wa Kasulu na Wilaya ya Kasulu tumeweza kuhakikisha kwamba yale maeneo ambayo yamevamiwa na kama nilivyosema kwenye majibu ya msingi mifugo yote tumeiondoa na hata hivyo kuhusu miti; Nyarugusu, Makere yenyewe, Kwamba, Mwadivano na Kalimungoma, katika maeneo yote yale wamepanda miti zaidi ya 50,500,000. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wako Watanzania pamoja na vyombo vya habari wameanza kupotosha kauli ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa jana kule Kagera kwamba sasa wananchi ni ruksa kwenda kuvamia maeneo oevu, maeneo ya vyanzo vya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe kauli ya Rais isije ikapotoshwa wananchi wakaenda kuvamia maeneo ya mito na kuanza kulima. Kauli aliyoitoa Mheshimiwa Rais Watanzania waelewe vyanzo vya maji ndivyo uhai wetu, mito yote itakauka, hakuna anayeruhusiwa kwenda kwenye chanzo cha maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kwa mujibu wa Sheria ya Mazingira, Rais ametumia kifungu cha 57 cha sheria hiyo kwamba pale ambapo kunakuwa na changamoto, wananchi wale ambao wako Karagwe wamekuwepo pale hawana ardhi, Rais ametuomba tushirikiane na uongozi wa mkoa kuhakikisha wale wananchi wanapatiwa maeneo mengine lakini siyo kuwaondoa.
Kwa hiyo, hamruhusiwi na msije mkasema kwamba Rais amewaruhusu wananchi kinyume na sheria. Ahsante.
MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwanza kabisa niipongeze Wizara imekuwa mara nyingi ikihamasisha tutunze mazingira na sisi kama wawakilishi wa wananchi tumekuwa tukifanya hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sisi kama wawakilishi wa wananchi tumsikilize Rais au tumsikilize Waziri? Mara nyingi tumeambiwa Rais akisema ni sheria. Rais jana amewatangazia wananchi kwamba walime, waingie kwenye mabonde mpaka mvua itakapowatoa na hii sheria ya Rais anayoisema Mheshimiwa Waziri inahusu tu Kanda ya Ziwa na ni sheria namba ngapi kwa sababu anazungumza kila siku kwenye Kanda ya Ziwa, analeta upendeleo wa wazi. Je, tumsikilize Rais au tumsikilize Waziri? Kwa nini kila wakati Rais akienda Kanda ya Ziwa…
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Msigwa ambaye alikuwa commissioner mwenzangu sasa nime-retire, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu haiongozwi kwa kupendelea wananchi wa eneo moja. Nchi yetu inaongozwa kwa mujibu wa sheria na Katiba. Nimhakikishie na nirudie tena, alichokisema Rais wetu kule Kagera hajavunja sheria nimekwambia kifungu cha 57 kasome ambacho kinatoa mamlaka ya kuruhusu na hata wewe Mheshimiwa Msigwa kama una shughuli zako unataka kuzifanya kando kando ya ziwa au mto lete Ofisini kwetu utapata kibali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu Mheshimiwa Msigwa mimi nimeenda Kihansi nimekuta wananchi kule Kihansi pamoja Mufindi na Ifakara wanalima kwenye bonde la Mto Kihansi na tumewasaidia kabisa wananchi wale kwenye mradi wetu ili waendeleze lile bonde kwa kilimo. Hii inaonyesha dhahiri kwamba hatubagui, wananchi wote wako sawasawa.
heshimiwa Mwenyekiti, narudia tena, wananchi ambao wamezoea kuchezea sheria, Serikali ya Awamu ya Tano haitamfumbia macho yeyote ama kwa kuchochea wananchi wavunje sheria ama yeye mwenyewe kuvunja sheria watapambana na mkono wa sheria na sheria hii inatoa adhabu kwa wanaochochea. Ahsante sana. (Makofi/ Vigelegele)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri ambayo yamedhihirisha kwamba katika kipindi kifupi ambacho ameshika nafasi hii kwa kweli amejua mambo kwa haraka na kwa uzuri kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongezee mambo mawili, kwanza, Serikali kupitia Ofisi yetu iliziagiza lakini napenda nirudie kutoa agizo tena upya kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa na Halmashauri zetu kuorodhesha vyanzo vyote vya maji katika maeneo yao na kuvileta kwetu na kuelezea hatua ambazo zinachukuliwa katika kuvilinda, hilo la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba kifungu cha 57 cha Sheria ya Mazingira, Na.20 ya mwaka 2004, kipengele cha (1) kinaweka zuio la kufanya shughuli mita 60 kwenye kingo za mito, fukwe na maziwa lakini kifungu kinachofuatia cha (2) kinasema, Waziri anaweza kuweka miongozo ya kuendesha shughuli za binadamu ndani ya maeneo yaliyoelezwa kwa mujibu wa kifungu hiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, baada ya maelekezo mahsusi ya eneo mahsusi alilokuwepo Mheshimiwa Rais, kazi yetu sisi sasa ni kutengeneza mwongozo wa namna ya kufanya shughuli ile katika eneo lile lakini hapo hapo kwa kuzingatia hifadhi ya mazingira. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba niliweke sawa kwa namna hiyo kwamba kutokana na maelekezo yaliyotolewa, sisi sasa sheria inatuelekeza kuweka mwongozo wa pale mahali ambapo wale watu waliomba kufanya ile shughuli namna ya kufanya ile shughuli bila kuathiri mazingira. Kwa hiyo, hakuna blanket permission ya kuvamia vyanzo vya maji na kingo za mito kote nchini. Tutaendelea kufuata sheria kwa sababu sheria bado ipo. Ahsante.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuweka kumbukumbu sawa kwenye jambo moja huku nikipongeza majibu yaliyotolewa na Naibu Waziri pamoja na Waziri mwenye dhamana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo hili lililosemwa kwamba Rais anapendelea Kanda ya Ziwa, nataka niweke kumbukumbu sawa kwamba Mheshimiwa Rais siyo kwamba anapendelea Kanda ya Ziwa, isipokuwa Rais amekuwa akisikiliza vilio vya wananchi pale anapokuwa katika eneo husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya jambo ambalo nataka nitumie kumbukumbu, Mheshimiwa Rais alipokuwa Bagamoyo, wananchi walipolilia eneo la Magereza alilitoa hapo hapo huku sheria ikiwa inataka eneo lile litumike kwa ajili ya Magereza, lakini kwa kuwa kilio cha wananchi kilikuwa kikubwa na huko siyo Kanda ya Ziwa ni Pwani, hapo hapo wala hata hakusubiri maelekezo ya Wizara kukaa kama alivyosema Kanda ya Ziwa, pale aliamua hapo hapo akasema wananchi hawa wapewe eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo ndivyo ambavyo nasemea ni kwamba anakuwa anatolea utatuzi changamoto za wananchi na hicho ndicho kilichomfanya achaguliwe na yuko kwa ajili hiyo. Siku atakapokuwa Ruvuma atatoa majibu hayo hayo kwenye kilio cha wananchi, siku akiwa Arusha atatoa majibu hivyo hivyo na maeneo mengine mengi ameshafanya shughuli za aina hiyo, hivyo tusije tukapotosha utekelezaji wa kazi za Mheshimiwa Rais. (Makofi)
MHE. MWANTUM DAU HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Namshukuru Waziri kwa majibu yake mazuri ambayo ameyatoa hapa hivi sasa, lakini nina maswali mawili ya nyongeza nataka kuuliza. Je, Serikali inasema nini katika kuboresha kilimo cha umwagiliaji maji kwa kupitia mito mikubwa, maziwa na mabwawa? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sambamba na kilimo cha umwagiliaji maji, je Serikali ina mpango gani wa kutoa elimu kwa wakulima juu ya kilimo hicho. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Spika, kama ambavyo tumejibu kwenye swali letu la msingi ambapo Serikali imeweka mipango mikakati ya kuhakikisha kwamba kilimo cha umwagiliaji na hasa pale ambapo tunakuwa na matatizo ya ukame; matatizo ambayo yanasababisha mvua zisijulikane sana. Ndio maana mipango ambayo nimeisema katika majibu yangu ya msingi, inabidi izingatiwe.
Mheshimiwa Spika, vilevile wakulima wanashauriwa katika kilimo hiki cha kutumia maji vizuri, kikiwemo na kilimo hiki ambacho tunaita drip irrigation. Kilimo ambacho kinatumia matone ya maji na hivyo kuweza kuwa na maji mengi kwa ajili ya watumiaji wengine.
Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la pili ambalo ni la elimu kwa wakulima. Ofisi ya Makamu wa Rais kupitia Baraza la NEMC tumekuwa na mikakati mbalimbali ya kuwapa wakulima elimu. Vilevile kwenye Sikukuu ya Wakulima ya Nane Nane tumekuwa tukichapisha majarida mbalimbali; majarida mengine ambayo ninayo hapa ambayo baada ya hapa nitampatia Mheshimiwa Mbunge. Wadau mbalimbali na wakulima wamekuwa wakitembelea mabanda yetu na kupata vipeperushi pamoja na majarida mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pia mikakati ambayo tumeizungumzia hapa, nitampatia Mheshimiwa Mbunge kuna hii ya National Climate Change Strategy ambayo tumeizungumzia ya mwaka 2012 halafu vilevile tunayo miongozo ambayo ni ya kisera kuhusiana na suala la sekta ya kilimo.
Mheshimiwa Spika, niseme pia kwa faida ya Watanzania wote, masuala ya mazingira ambayo yanaathiri kilimo yameanzia kwenye Biblia ukisoma Mwanzo 10:15 ambapo Mungu alianzisha utaratibu kwenye ile mito minne akamwambia mwanadamu nakuagiza ukalime na kuitunza.
Mheshimiwa Spika, hivyo, vyanzo vya maji ni asili yake kwenye Biblia. Hii ndio maana na sisi kwa kutunga Sheria hii namba 20 ya 2004, vilevile tumechukua kipengele hicho tukaweka kifungu cha sita (6) ambacho kinatoa wajibu wa kisheria kwa kila mtanzania kutunza na kuhifadhi mazingira.
Mheshimiwa Spika, Ahsante sana. (Makofi)
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Tanzania hivi sasa tunaelekea katika uchumi wa viwanda. Na moja ya ajenda/ suala muhimu ambalo linazingatiwa hivi sasa ni ujenzi wa viwanda. Na kwa kuwa viwanda ni miongoni mwa mambo ambayo yanachangia uharibifu wa mazingira, kwa mfano nchi ya China pamoja na Marekani ni miongoni mwa nchi ambazo hazikukubali kusaini Mkataba wa Kyoto kutokana na viwanda. Sasa ninachotaka kujua tu ni kwamba, Tanzania kwa sababu tunahitaji viwanda.
Je, tunajiandaaje ili kuhakikisha kwamba viwanda vitakavyojengwa hapa nchini haviwi sababu ya uharibifu wa mazingira? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kulikuwa na baadhi ya nchi matajiri ambao walikuwa hawataki kusaini Mkataba wa Kyoto lakini mkutano niliouzungumzia ambao mpaka sasa wanaendelea kule Bonn, Ujerumani. Mkutano huu umekuwa wa mafanikio makubwa kwa sababu makubaliano yaliyofanyika Mjini Paris kila nchi wanatakiwa sasa wasaini mkataba ule wa mabadiliko ya tabianchi. Ka hiyo, hakutakuwa na nchi hasa hizi tajiri ambazo ndizo zinazalisha hewa ya ukaa ambayo inakuja kuathiri nchi zetu maskini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Tanzania ya viwanda ambayo sasa tunakwenda nayo, sheria yetu ya mazingira ambayo niko nayo hapa, Sheria Namba 20 ya mwaka 2004 ya Usimamizi wa Mazingira. Sheria hii inavitaka viwanda vyote kuhakikisha kwamba kabla hawajaanza uzalishaji wawe katika ile Environmental Impact Assessment pamoja na Environmental Management Plan zao, namna ambavyo watakwenda ku-manage emissions zote ambazo zinaharibu mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio maana kupitia Baraza la Hifadhi la Taifa la Mazingira (NEMC) tumekuwa tukikagua mara kwa mara kuhakikisha viwanda hivi vina-comply masharti yale ambayo hayaharibu mazingira. Ndio maana viwanda ambavyo vinakaidi tunavipiga fine na vingine tunavifungua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuwahakikishia Watanzania, katika Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Jemedari Dkt. John Pombe Magufuli hakuna wazalishaji wa viwanda wanaoharibu mazingira watakaotumia nguvu za fedha kuhakikisha kwamba wanaendelea kuharibu mazingira halafu na sisi tunawatazama, lazima sheria hii itawashughulikia. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na athari kubwa ambazo zimetokana na mabadiliko ya tabianchi, wakazi wa Mkoa wa Iringa wamekuwa wakihamasishwa sana namna ya kupanda miti na wamejitahidi sana kupanda miti ili kuokoa hii hali ya mabadiliko ya tabianchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali, kuna wakati wakazi hawa walikuwa wameambiwa kwamba jinsi wanavyoendelea kupanda miti watapata fidia kutokana na jinsi wanavyopata miti kutoka kwenye mashirika mbalimbali duniani. Je, hili limeishia wapi? Ningeomba nipate majibu kutoka Serikalini.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba nchi yetu imeanza kuwa na dalili za kuwa na jangwa, nchi yetu inakuwa na ukame na hatuna option, lazima Watanzania kote nchini tuweze kuwa na tabia ya kupanda miti. Na kama nilivyosema juzi, ni wajibu wa kila Mtanzania kushiriki katika Ilani hii ya CCM, ukurasa wa 212 mpaka 213 unazitaka Halmashauri zote nchini wapande miti kila mwaka isiyopungua 1,500,000.
Kwa hiyo, kwa kuwa, Wananchi wa Iringa wameanza juhudi hii sisi tuko tayari kuhakikisha kwamba, hewa ya ukaa ambayo inaharibu ozone layer yaani tabaka la ozone na kusababisha miale mikubwa ya jua ule mnururisho uweze kuleta joto jingi duniani, ni kweli mashirika ya kimataifa yananunua kitu tunaita karadha, kwa jinsi ambavyo miti ile ndio inayosaidia kufyonza hewa ya ukaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa kuwa wananchi wa Iringa wameanza na wananchi wengine wameanza, Ofisi ya Makamu wa Rais itaanzisha utaratibu wa kuona ni kiwango gani wananchi wameweza kupanda miti ili watalaam sasa waweze kuona kiwango cha karadha ya ufyonzaji wa hewa ya ukaa, ili waweze kupata fidia kwenye mashirika ya kimataifa. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: MheshimiwaMwenyekiti, nashukuru. Nimepata masikitiko makubwa sana kutika kwenye Wizara husika ambayo inasimamia shughuli za mazingira nchini. Kwa kuwa Wizara hii ndio iliyoshikilia au inaongoza Sheria yetu ya Mazingira ya mwaka 2014; na kwa kuwa Wizara hii ndio iliyoshikilia Mfuko wa Mabadiliko ya Tabianchi; na kwa kuwa ni Wizara hii ambayo inasimamia Mfuko wa Mazingira Nchini; na kwa kuwa ni Wizara hii ambayo ina fedha kutoka mashirika mbalimbali nchini na duniani kote inayosimamia shughuli zote za mazingira nchini, inanijibu kwamba haitoi, haihangaiki, haina chochote, hamna jibu linalohusu shughuli za kusimamia fedha za ku- address issues za climate change nchini na tunaona dhahiri kwamba mabadiliko ya tabianchi yameleta madhara makubwa, majira ya mvua hayajulikani, kuna ukame, na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka kujua, hii Wizara ipo au haipo? Na kama ipo, mbona imenyamazia kimya issue ya mabadiliko ya tabianchi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa ninamheshimu sana Dkt. Sware ambaye Ph.D yake ameisoma kule Stockholm, Sweden, Masters yake ameichukulia Norway, namheshimu sana, lakini kwa sababu anashindwa kutofautisha kati ya maneno mawili ambayo ni rahisi sana, yeye ameuliza swali la ruzuku na ruzuku kwa kiingereza kwa faida yako Dokta tunaita subsidies, lakini kuna kitu kingine tunaita misaada, misaada ni grants.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama yeye ameuliza ruzuku, ndio nimemjibu sisi hatuna ruzuku. Lakini haya aliyoyasema leo kama angejiongeza akauliza hayo, kwa faida ya Watanzania, kwa ajili ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi na nchi yetu mpaka leo kuanzia tarehe 6 mpaka 17 wako Bonn, Ujerumani wanashiriki mkutano mkubwa wa kimataifa kujadili masuala ya mabadiliko ya tabianchi. Na sisi Tanzania ni nchi wanachama ambao tulisaini Mkataba wa Mabadiliko ya Tabianchi kule Mjini Paris na tunayo mifuko ifuatayo ambayo sisi tunakabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfuko wa kwanza unaitwa Adaptation Fund, yani kwa maana kwamba ni mfuko wa kuhimuli mabadiliko ya tabianchi. Mfuko wa pili, unaitwa ni Least Developed Countries Fund, yaani kwa maana Mfuko wa Nchi Maskini Duniani. Na mfuko mwingine ni GEFT ambao ni Global Environmental Facility. Mfuko mwingine ni Mfuko wa Mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tumepata grants hizi ambazo sasa tunapambana na athari za mabadiliko ya tabia nchi maeneo mbalimbali hapa nchini. Tuna mradi mkubwa sana ambao Ocean Road pale kwa sababu kina cha bahari kimeongezeka tunajenga ukuta mkubwa wa kilometa moja, ili kingo za bahari zisije zikasombwa na kuharibu makazi ya watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Chuo cha Mwalimu Nyerere, Kigamboni tunajenga ukuta mkubwa ili kudhibiti kingo zisiendelee kubomoka. Vilevile kupitia grants hizo kule Rufiji tunarudishia mikoko ambayo ilikuwa imekatwa na mradi unaendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kule Zanzibar Kisiwapanza, kule Zanzibar Kisakasaka pamoja na Kilimani mifuko hiyo inaendelea. Kule Pangani tunajenga ukuta pamoja na kurudishia mikoko. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Bagamoyo tunajenga visiwa 28 kwa wananchi wa Bagamoyo, zikiwepo na sekondari mbili mojawapo inaitwa Kinganya ambayo ni ya Mheshimiwa Dkt. Kawambwa. Mifuko hiyo, tunaitumia kwa ajili ya kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. NAJMA MURTAZA GIGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu aliyoyatoa Mheshimiwa Naibu Waziri kwa niaba ya Waziri bado nina swali moja la nyongeza. Je, kwa nini Serikali haioni umuhimu wa kutuletea taarifa zote pale ambapo changamoto za Muungano zinapopatiwa ufumbuzi ndani ya Bunge hili ili sisi Wawakilishi wa Wananchi tuweze kumsaidia Mheshimiwa Waziri kuzifikisha kwa wananchi kwa wepesi zaidi? (Makofi). Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais(Muungano na Mazingira) napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Najma Murtaza Giga ambaye ni nyara ya CCM na tegemeo kubwa la CCM kule Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wazo hilo ni zuri kwamba iko haja ya kuleta taarifa zote kwa namna ambavyo Ofisi ya Makamu wa Rais wanavyoweza kupitia Kamati yetu ya pamoja ya kero za Muungano hapa Bungeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali yetu imekuwa ikitoa taarifa hizi kila wakati kama nilivyosema kwenye majibu yetu ya msingi. Zile taarifa ambazo zinatolewa kwenye maeneo hayo ya siku ya Muungano kwenye televisheni Mheshimiwa Waziri wetu tunatekeleza amekuwa akiongelea mambo haya, hata hapa Bungeni ambapo anasema ni vema tukazileta. Naomba nimhakikishie hizi Hansard hizi zimesheheni taarifa mbalimbali kuhusu namna ambavyo Serikali imekuwa ikitatua kero za Muungano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapa, Mheshimiwa Najma nitakupatia hizi Hansard hizi na tayari nimeonesha maeneo yale ili usipate usumbufu ili uweze kuona namna ambavyo Serikali yeu inavyotoa taarifa hiyo. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya ndugu yangu Kangi Lugola nuru ya wanyonge, Jimbo la Mwibara, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, kwa kuwa chanzo kikubwa cha maji ya binadamu, mifugo na wanyamapori katika eneo hili la vijiji tisa ni Mto Rubana, na kwa kuwa hakuna chanzo kingine mbadala kwa wananchi wa maeneo hayo, na kwa kuwa ardhi haiongezeki na watu wanaongezeka na mifugo inaongezeka. Je, ni lini sasa Serikali kwa kupitia Wizara yake ya Mazingira itapeleka mradi mkubwa wa maji katika vijiji hivi viwili ili kuviokoa na tatizo la maji?
Swali la pili, kwa kuwa Mto Rubana, ndiyo mpaka kati ya vijiji tisa vinavyopakana na pori hilo la akiba, la Grumeti. Je, ni lini agizo lako ulilolitoa miezi miwili iliyopita, ulipotembelea maeneo hayo kwamba mita 500 za eneo la wazi kutoka eneo la mpaka kwenda vijijini na mita 500 kutoka eneo la mpaka kwenda porini wataweka beacon?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana Mheshimiwa Getere wapiga kura wako wanakuita Tingatinga la maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikiri kwamba baada ya uteuzi wangu nilitembelea Jimbo la Mheshimiwa Mbunge na kuweza kufanya mikutano miwili Maliwanda pamoja na Hunyari, ninamhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali yetu tayari kwa kuzingatia kwamba wananchi walikuwa wanatumia maji ya Mto Rubana kunyweshea mifugo, uvuvi pamoja na matumizi ya nyumbani, tayari katika Kijiji cha Kyandege, Kijiji cha Mugeta na Kijiji cha Mariwanda Serikali tulishawajengea malambo ya kunyweshea mifugo na mabirika ya kunyweshea mifugo yanafanya kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna taasisi inaitwa Rubana Corridor Invironmental Development Strategy wako mbioni na wamekamilisha mchoro wa kujenga bwawa moja kubwa katika Kijiji cha Kihumbu. Pia Halmashauri ya Wilaya Bunda, katika mwaka wa fedha wa 2017/2018 wametenga jumla ya milioni 30 kukarabati lambo la Kihumbu na pia Foundation for Civil Society kushirikiana na asasi niliyoitaja mwanzo, tayari wanataka kujenga visima viwili vya maji katika Kijiji cha Kihumbu, ikiwa ni pamoja na kuongeza lambo moja kubwa kwa ajili ya kunyweshea mifugo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuhakikisha uvuvi uliofanyika Rubana usiendelee na kuchafua mazingira, tayari Foundation for Civil Society wameendesha mafunzo ya vijiji vinne kwa ufugaji wa nyuki na sasa watasambaza mizinga 100 kwa ajili ya kuwafanya wananchi wasiende kuchafua mto.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili kuhusu changamoto ya mita 500. Ni kweli kabisa Sheria namba 5 ya mwaka 2009 kifungu cha 74 kinazungumzia kuweka buffer zone ya mita 500 kwenda kwa wananchi. Nimhakikishie Mbunge tayari Ofisi ya Makamu wa Rais, imeshawasiliana na Mkurugenzi Mkuu wa TAWA pamoja na Wizara ya Maliasili na Utalii, kwamba wanashughulikia masuala ya beacon. Pia nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba beacon zinazohusu wanyama na wanadamu ni beacon ambazo siyo endelevu, leo utaweka beacon ya mita 500 kwa wananchi, na hawa wanyama wao hawajui kama kuna beacon ya mita 500, baadae watasogea tena kwenye mita 500, baadae wananchi watasema wanyama wamesogea tuweke tena beacon za mita 500, mwishowe vijiji vyote vitaisha kwa kuwa beacon ya hifadhi. Hiyo ndiyo changamoto iliyopo. (Makofi)
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru.
Tatizo lililopo katika Jimbo la Bunda linafanana kabisa na tatizo lililopo katika Jimbo la Tabora Manispaa, chanzo cha maji cha Mto Gombe kinasumbuliwa sana na tatizo la mazingira katika eneo hilo.
Je, Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira ina mpango gani wa kusaidia wananchi wale kunusuru afya zao za maji ambayo wanatumia wakati tukisubiri maji ya Ziwa Victoria?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba nchi yetu ina changamoto ya uharibifu na uchafuzi wa mazingira, kwenye vyanzo vingi vya maji. Ndiyo maana mkakati mmojawapo wa kunusuru vyanzo vya maji nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa January Makamba alishatoa agizo kwa Halmashauri zote nchini kuhakikisha wanaorodhesha vyanzo vyote vya maji katika maeneo yao, vikiambatana na changamoto ambazo zinakabili vyanzo hivyo ili Serikali ijipange katika kunusuru vyanzo hivyo, hili la kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, katika Ilani hii ya CCM ambayo naamini Mheshimiwa Hawa Mwaifunga anaiamini na kuisimamia itekelezwe katika maeneo yake, katika ukurasa wa 212 mpaka 213 Ilani hii inaagiza Halmashauri zote katika nchi yetu, kuhakikisha kila mwaka wanapanda miti ya kuhifadhi mazingira na kwenye vyanzo vya maji isiyopungua milioni 1.5.
Hivyo kupitia swali hili, naziagiza Halmashauri zote nchini, zitekeleze Ilani hii na baada ya Bunge hili wajue wana deni ambalo dawa ya deni ni kulipa nitaenda kukagua kuona sasa miaka miwili kwamba wana miti si chini ya milioni tatu.
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa uchafuzi wa mazingira ni pamoja na uchomaji misitu hovyo unaosababisha uzalishaji hewa ya ukaa, na kwa kuwa tayari Halmashauri ya Wilaya ya Ngara kupitia Mbunge wao tulishandaa andiko la mradi kwa ajili ya kupambana na uchomaji moto Mradi unaoitwa Participatory Community Based bush Fire Management and Livelihood Improvement na tukawasilisha Wizara ya Muungano na Mazingira kwa ajili ya kuanza na vijiji 15 kati ya vijiji 75.
Je, ni lini Wizara yenye dhamana itawezesha ili Halmashauri tuweze kutekeleza mradi huu ambao unaonekana kuwa na tija, kwa sababu tutapanda miti ni macadamia na ufugaji wa nyuki vitakavyopelekea kutoa ajira lakini na kudhibiti mazingira, ni lini Wizara yenye dhamana itawezesha mradi huu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Mheshimiwa Alex Gashaza amekuwa akifuatilia sana juu ya andiko lake katika ofisi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwakikishie Waheshimiwa Wabunge na nitoe wito kwa Watanzania wote na hasa ambao wanamiliki viwanda, suala la hewa ya ukaa ambalo Mheshimiwa Mbunge amelizungumzia ambalo ndio msingi na chimbuko la andiko lake, mabadiliko ya tabianchi ambayo yanatokea sasa yanaanza kuandama nchi yetu, ni kutokana na hewa ya ukaa inayozalishwa kwenye nchi zilizoendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa katika nchi yetu tumeanza kuwa na maendeleo ya viwanda, kwa hiyo viwanda vihakikishe vinadhibiti hewa ya ukaa isije na vyenyewe vikaendelea kuongeza ukubwa wa tatizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Gashaza hewa ya ukaa, pamoja na kwamba upandaji wa miti utasaidia sana kwa sababu mchana miti inavuta hewa ya ukaa, kwa hiyo, ni kweli kwamba tukipanda miti kwa wingi tutaweza kudhibiti uzalishaji wa hewa ya ukaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hewa ya ukaa ni bidhaa ambayo ni adimu sana inauzwa kupitia Mfuko wa Mazingira Duniani. Ukiwa na hewa ya ukaa ukaivuna takwimu zile ukizipeleka kule ni fedha nyingi sana.
Kwa hiyo andiko lako Mheshimiwa Gashaza, Ofisi yetu inaendelea kulifanyia kazi, ili kuhakikisha maandiko ambayo tumeomba fedha kwenye mifuko ya Mazingira Duniani itakapopatikana basi andiko lako ambalo wataalam wetu wameliona ni zuri sana tutakwenda kulitekeza. Ahsante sana.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kama Mheshimiwa Waziri atafuatilia na naamini ataunda hiyo Kamati maana najua bado mazingira ni machafu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la nyongeza ni kwamba; kwa kuwa hii mito mikubwa minne ya Yongoma, Saseni, Hingilini na Nakombo imejaa magogo ambayo yameletwa kutoka misituni na hivyo kufanya maji yatuame na yasiwafikie watu walioko mabondeni.
Je, Waziri atatusaidiaje au Serikali itatusaiaje kufundisha wananchi na kuwapa vifaa ili waweze kufanya usafi wa ile mito yaani Kiingereza wanaita dredging ili watoe yale magogo ili maji yaweze kufikia wananchi walioko bondeni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa kwamba Mito ile ya Hingilini, Saseni, Yongoma pamoja na Nakombo ni kweli imeathiriwa na shughuli za kibinadamu yakiwemo hayo mdgogo aliyoyasema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa kifupi tutauma tena timu ya wataalam ili waende waone ukubwa wa lile tatizo na baada ya kuona ukubwa wa lile tatizo watatupa taarifa ambayo tutawashirikisha wananchi wenyewe katika maeneo yale ikiwa ni pamoja na kuwaelimisha juu ya matatizo haya ambayo yanafanyika katika vyanzo vya maji. Kwa hiyo, Mheshimiwa Kaboyoka usiwe na wasiwasi na kama utakuwa tayari kuambatana na mimi nitakapokuja kule, mimi nitakuwa tayari pia kuambata na wewe, ahsante sana.
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya ya Iramba, Tarafa ya Ndago, Kata ya Ndago kwenye Magereza ya Ushora ambayo yana “A” na “B”, Ushora pamoja na Mirungu kulikuwa na msitu mkubwa na miti mikubwa ambayo ilikuwa ni chakula cha tembo lakini wafungwa wale wamemaliza ile miti hadi wale wanyama wamehama kule. Waziri ananiambia nini kuwapelekea miti wale wafungwa wakapande waturudishie msitu wetu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Martha Mlata, alipokuwa kwenye Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira alikuwa anazungumzia sana juu ya ukataji wa miti hovyo kwenye Gereza la Ushora. Mimi niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote na niwakumbushe kwamba suala kulinda, kutunza na kuhifadhi mazingira kwa mujibu wa kifungu namba sita cha Sheria Namba 20 ya mwaka 2004 sote tunawajibika kufanya hivyo. Tuendelee kuhakikisha kwamba zile taasisi ambazo ziko kwenye maeneo yetu yakiwemo magereza, shule, hospitali wahakikishe kwamba wanatumia nishati mbadala kama ambavyo Mheshimiwa Waziri alivyoelekeza.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Martha Mlata kupitia swali lako hili, naendelea kuzitaka taasisi zote ambazo tulishazielekeza wasiendelee kukata miti kwa ajili ya nishati, waendelee kutumia nishati mbadala na katika siku ya Mazingira Duniani ambayo tunaanza tarehe 30 Mei mpaka tarehe 5 Juni, 2018 kutakuwa na maonesho ya…

…watu mbalimbali katika kutumia nishati mbadala. Mheshimiwa Martha Mlata nitakuwa tayari kuambatana na wewe kwenda Gereza la Ushora, ahsante sana.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Waswahili wanasema usipoziba ufa utajenga ukuta. Imekuwa ni tatizo linaloendelea na ni maneno kila siku yanazungumzwa kuhusiana na uharibifu wa vyanzo vya maji na hususani Chemchemi.
Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuhakikisha inatoa elimu kwa wananchi wote wanaozunguka maeneo ya vyanzo vya maji ili kuhakikisha kwamba wao ndio walinzi lakini hao hao wawe ndiyo watunzanji wa mazingira wa maeneo yale?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Sera yetu hii ya Taifa ya Hifadhi ya Mazingira pamoja na Sheria ya Mazingira tayari Mheshimiwa Waziri alishatoa miongozo na maelekezo kwa Halmashauri zote 185 Tanzania watuletee orodha ya vyanzo vyote vya maji ikiwa ni pamoja na changamoto. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge tuko katika harakati za kuhakikisha kwamba tunaweka mikakati ya utoaji wa elimu kwa wananchi ambao wako kwenye vyanzo vya maji ikiwa ni pamoja na kutangazwa kwenye Magazeti ya Serikali. Ahsante sana.
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nampongeza Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri.
Kwa kuwa amezungumzia mikakati ya Serikali katika kuhakikisha inatunza na kuhifadhi vyanzo vya maji, ninaomba kujua, kwa kuwa Ofisi ya Makamu wa Rais ilishawahi kutoa maelekezo kwa Wakurugenzi wote nchi nzima iweze kubaini vyanzo vyote vya maji na kupeleka orodha ili Serikali sasa ije na mkakati wa kutekeleza, siyo kwa ajili ya kuweka mikakati ya kufikiria kuanza; je, mkakati huo na agizo hilo limetekelezwa kwa kiwango gani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa sababu Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba Serikali ina mpango wa kufufua vyanzo; kuliko kusubiri kuja kufufua vyanzo ambavyo vilishakufa, Singida tuna maziwa mawili, Singidani pamoja na Kindai na ukienda Singidani lile ziwa limeshaanza kujaa tope. Je, kuna mkakati gani sasa wa kuja pale Singida ili mje muondoe lile tope, kina cha maji kibaki kama kilivyokuwa mwanzo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze swali la msingi Mheshimiwa Catherine Magige kwa namna ambavyo anawakilisha Mkoa wake wa Arusha na wananchi wa Arusha wanadhani yeye ndiye Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa Ofisi ya Makamu wa Rais ilishatoa agizo kwa Wakurugenzi wote nchi nzima kubaini na kuorodhesha vyanzo vya maji na tuliwapa muda wa kutosha, lakini mpaka sasa ni mikoa mitatu tu kati ya mikoa yote ambao wamewasilisha orodha ya vyanzo vya maji pamoja na changamoto zake. Sasa mikoa mingine wameshindwa kutekeleza agizo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachofanya sasa ni kuhakikisha kwamba orodha ya Halmashauri zote nchini ambazo hazijawasilisha orodha ya vyanzo vya maji, tunaiwasilisha kwa Waziri Mkuu wa nchi yetu ili aweze kuamua hatma ya Wakurugenzi hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Mheshimiwa Martha Mlata naye amekuwa akifuatilia sana kero za Mkoa wa Singida hasa upande wa mazingira. Napenda nimhakikishie Mheshimiwa Martha Mlata kwamba maziwa mengi katika nchi yetu likiwemo hilo la Singidani yamekuwa yakijaa tope kutokana na shughuli za kibinadamu. Sasa nitamwagiza Mkurugenzi wa Mazingira wa nchi yetu aambatane na timu yake washirikiane na Halmashauri ya Wilaya ya Singida na ya Mji wa Singida ili waweze kuona ni mikakati gani tunayoweza kuifanya kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunadhibiti hali hiyo. Ahsante sana. (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri kuhusu vyanzo vya maji katika Halmashauri zote, napenda kulipa taarifa Bunge hili kama nyongeza ya majibu kwamba mwaka 2006 wakati wa kuandaa Programu ya Maji nchi nzima ilifanyika stadi ya vyanzo vya maji nchi nzima. Kwa hiyo, kwa Wakurugenzi siyo kazi mpya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa agizo kwa Wakurugenzi wote, ndani ya mwezi mmoja waweze kuwasilisha Ofisi ya Makamu ya Rais hivyo vyanzo vya maji vyote kwa sababu wanavyo katika vitabu vyao. (Makofi)
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Hivi vyanzo vya maji kuvihakiki ni kwingine, Ziwa Tanganyika hakuna kazi inayofanyika, watu wanajenga majumba mpaka yanagusa Ziwa Tanganyika, lakini hakuna operation iliyofanyika, hakuna chochote. Hivi vyanzo vya maji ni kwingine tu, Ziwa Tanganyika mbona hakuna chochote kinachofanyika katika nchi hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye swali letu la msingi, ni kwamba katika maziwa yote, mito yote pamoja na bahari ni kweli kabisa kwamba Sheria yetu Na. 20 ya 2004 ya Usimamizi wa Mazingira inakataza shughuli za binadamu kufanyika ndani ya mita 60.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto iliyoko Ziwa Tanganyika ni sawa na changamoto ambazo ziko kwenye maeneo mengine. Ndiyo maana tumesema tunataka tubaini ili tujue ukubwa wa tatizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo wale wanaofanya shughuli za binadamu kwenye mita 60 katika Ziwa Tanganyika. Inawezekana wanafanya kwa mujibu wa kifungu cha 57(2) lakini tutatuma timu ya wataalam chini ya Mkurugenzi wa Mazingira kwenda kuona kama hao aliowasema Mheshimiwa Keissy wanaruhusiwa kwa mujibu wa kifungu cha 57(2) au la ili tuweze kuchukua hatua stahiki. (Makofi)
MHE. MBAROUK SALIM ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Kwanza nisikitike sana kwamba swali langu halikujibiwa na pamoja na kwamba Naibu Waziri amesema kwamba si kero, lakini Majaji wanasema ni kero. Kwa hiyo hizi ni kero za Muungano ambazo zinatambulika na kwa hiyo naomba na yeye atambue kwamba hizi ni kero za Muungano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba niulize maswali yangu mawili ya nyongeza. Kulingana na makubaliano ya Muungano ambayo yaliasisiwa na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Baba wa Taifa pamoja na Baba wa Taifa wa Zanzibar Abeid Amani Karume ni kwamba miezi 12 tu iundwe tume ambayo itapanga mambo ya Muungano. Hata hivyo ni jambo la kusikitisha kwamba mpaka mwaka 1991 ndipo tume hiyo ikaundwa na Tume ya Jaji Nyalali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la kusikitisha, pamoja na kuundwa hiyo tume hakuna lolote lililofanyika mpaka hivi leo. Swali la kwanza, je, uko wapi huo uhalali wa Muungano?
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili; hiyo Tume ya Jaji Nyalali iliainisha kero 40 za Muungano, lakini mpaka sasa Naibu Waziri anasema kwamba kuna kero 11 tu ambazo zimepatiwa ufumbuzi. Je, kuna nia safi kweli hapo ya Muungano?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbarouk ni rafiki yangu wa karibu sana. Sasa anaposema kwamba swali lake halijajibiwa vizuri si kweli, naamini alikuwa ananitania kwa sababu swali lake ameuliza ni kero ngapi ambazo zimekwishatafutiwa ufumbuzi, tumemjibu kwa idadi hiyo ni kero 11. Kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge anavyokuja kimaswali na sisi kimajibu ndivyo tunavyokwenda kwake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Tume ya Jaji Nyalali, ni kweli kabisa kwamba Tume ya Jaji Nyalali iliweza kufanya kazi zake katika kuangalia masuala ambayo yanahusiana na Muungano na hasa masuala pia ya changamoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala la Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni suala ambalo si la kukimbizwa haraka haraka katika kutatua changamoto zake. Ndiyo maana baada ya Tume ile baadaye Kamati ya Pamoja ya pande zote mbili ya kutatua changamoto za Muungano iliweza kuundwa ambapo inahusisha Zanzibar na Tanzania Bara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali ya Muungano inayo nia na dhamira ya dhati kuhakikisha kwamba yale yote ambayo yaliweza kubainika yanafanyiwa kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kwamba kero 40 na kwamba sasa zimetatuliwa kero 11 tu, kwamba Serikali ya Muungano haina dhamira ya dhati. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kero za Muungano pamoja na zile 40 ambazo zilibainika; kadri tunavyokwenda kila kukicha kuna baadhi ya changamoto zingine ambazo huwa zinajitokeza, sisi kama Serikali kadri ambavyo zinaibuka na kuongezeka na sisi tunaendelea kushughulika nazo na kuhakikisha kwamba tunazipunguza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa zilikuwa zimebaki kero 15 tu na katika kero 15, tayari 11 sasa zimepatiwa ufumbuzi na zilizobaki ni changamoto nne tu ambazo bado zinafanyiwa kazi yakiwemo masuala ya vyombo vya moto pamoja na haya masuala ambayo ni ya double taxation. Katika double taxation tayari tumeshafikia hatua ya turn fees kuhakikisha kwamba mifumo ya bara na kule visiwani na yenyewe inawekwa na inafanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbarouk kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inashughulika na changamoto za Muungano na kuhakikisha kwamba zinakwenda vizuri pasipo kwenda kwa pupa au kwa uharaka. Hata dereva barabarani anawekewa alama za barabarani hapa uende 50, hapa uende 80; sasa kama yeye anataka katika kutatua hizi kero twende zaidi ya zile speed ambazo zinatupa usalama, basi chombo cha Muungano kinaweza kikapata ajali halafu Watanzania wakafa na wengine wakajeruhiwa. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri, ila nataka niweke record kidogo sahihi ili Mheshimiwa Mbunge awe na taarifa sahihi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume ya Jaji Nyalali haikuja na orodha ya kero 40 za Muungano. Ile namba 40 katika Tume ya Jaji Nyalali ni sheria ambazo zilipendekezwa zifanyiwe mabadiliko na baadhi nadhani zilichukuliwa katika mfumo wa Tume ya Marekebisho ya Sheria (Law Reform Commission) ambayo iliundwa na kuanza kuzifanyia mabadiliko ya sheria hizo 40, kwa hiyo hakukuwa na kero 40 zilizoainishwa na Tume ya Jaji Nyalali.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa miaka 54 sasa Serikali hizi mbili za Chama cha Mapinduzi zimeshindwa kutatua kero za Muungano na Tume ya Warioba ilileta pendekezo katika mchakato wa Katiba ambao ungeondoa hizi kero za Muungano kwa kuunda Serikali tatu. Sasa je, ni lini Serikali watarejesha ule mchakato wa Katiba ili kuweza kupata Katiba ambayo itaondoa kero za Muungano?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Baba Paroko, Mheshimiwa Selasini. Si kweli kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inaongozwa na Chama cha Mapinduzi kwamba imeshindwa kutatua changamoto za Muungano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema hapa katika majibu ya kumjibu Mheshimiwa Mbarouk kwamba mpaka sasa changamoto ambazo tunashughulika nazo zimebaki nne tu katika nyingi zilizokuwepo. Sasa kusema kwamba Serikali imeshindwa katika uwiano huo nafikiri Mheshimiwa Selasini itabidi tukae mahali fulani tufundishane mahesabu yale ya wingi na uwiano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa wapo baadhi ya Watanzania na Waheshimiwa Wabunge hata yale masuala ambayo si changamoto za Muungano, wamekuwa wakitumia nguvu kubwa kuonesha kwamba masuala hayo ni changamoto za Muungano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niwasihi Mheshimiwa Selasini (Baba Paroko) tusifike mahali ikawa kama Kanisani ambapo kanisani kila siku lazima tunahubiri kwamba shetani yupo, tuendelee kupambana naye. Sisi kwenye masuala ya kisiasa yapo mambo tunapambana nayo yakiisha, hayo yameisha hayapo tena si kama tunavyopambana na shetani. (Makofi). Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante Naibu Waziri kwa majibu mazuri, napongeza Serikali kwa mpango mzuri ambao wameueleza. Hata hivyo, kama alivyozungumza kwenye majibu yake, ameonesha kabisa kwamba milima hii ina ikolojia ya pekee, bioanuai adhimu, lakini kuna mifuko ambayo imeanzishwa kwa Hifadhi ya Tao la Mashariki na utekelezaji wa mradi wa miaka mitano kuanzia 2016 – 2021 pamoja na vijiji vinavyozunguka, napongeza kwa hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia sasa kwenye hii Milima ya Uluguru, kwa sababu uhifadhi sio lazima uwe pale kwenye chanzo, maana yake pamoja na hills yaani vijilima vyake. Lakini ukiangalia kwa sasa hivi pale Manispaa ya Morogoro ile milima iliyozunguka kuanzia maeneo ya Kilakala, Bigwa, Kigurunyembe na Pangawe ambayo hapa kuna vyanzo vikubwa sana vya maji ambao wakazi hawa wote niliowataja wa Bigwa, Kigurunyembe na Kola tunategemea maji kutoka kwenye milima hii, lakini mito hii imekauka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inasababishwa na uharibifu mkubwa ambao unaendelea sasa hivi kwenye milima hii ya Bigwa, Kigurunyembe, Pangawe ambapo sasa watu wanajenga kwa kasi kubwa sana ndani ya ile misitu, wanakata ile misitu yaani… (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba kwa sababu pia pale kuna Mbega wale weupe na ndege ambao ni adimu. Je, Serikali imechukua hatua gani kusimamisha na kudhibiti ujenzi huu holela ambao unaendelea katika milima hii ambayo ni vyanzo vikubwa vya maji? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa tarehe 5 Aprili, nilifanya ziara ya kukagua uharibifu wa mazingira kwenye maeneo ambayo Mheshimiwa Mbunge ameyasema. Maeneo hayo ndiyo ambayo Mheshimiwa Mbunge kwa juhudi kubwa aliweza kuyafuatilia na wakashirikiana na Serikali ya Mkoa na Serikali ya Wilaya wakawaondosha wale watu ambao walikuwa wanajenga kiholela.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maagizo ambayo niliyatoa kwa Manispaa ya Morogoro ni kuhakikisha kwamba wanatengeneza mpango mkakati wa namna ambavyo watashughulikia uharibifu huu wa mazingira. Mheshimiwa Tisekwa ile climate change strategy niliyomwahidi, nitampatia hapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ambalo ningependa Wabunge waelewe, masuala ya uharibifu wa mazingira au uchafuzi wa mazingira wamekuwa wakidhani ni vyanzo vya maji kuviharibu au kukata miti, ni pamoja na upigaji wa makelele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi hapa, Hajji Manara wakati anatangaza kwamba mechi yao na Simba wacheze ili mapato yale yatakayopatikana waweze kuisaidia Yanga watu walipiga makelele sana, nikaulizwa haya makelele kwa mujibu wa mazingira yana mahusiano gani. Nikasema kwa mujibu wa kifungu cha 106, makelele yanazuiwa lakini yale makelele ya kushabikia kama matamko ya Hajji Manara yale yanaruhusiwa kwa mujibu wa mwongozo. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Spika, nakushukuru lakini nasikitika na majibu haya kwani ni majibu yale yale ya muda mrefu ambayo yamekuwa yakitolewa hapa Bungeni na imekuwa kidogo hayaleti taswira nzuri kwa pande mbili za Muungano. Nina maswali mawili ya nyongeza:-
Mheshimiwa Spika, katika majibu yake anasema kwamba Tume ya Pamoja haijaanza kufanya kazi kwa kuwa majadiliano kati ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu mapendekezo ya Tume hayajakamilika. Miaka yote hiyo mapendekezo wanajadiliana kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, sasa mpewe muda gani? Mtuambie wananchi wanataka kusikia leo, mupewe muda gani mtaweza kukamilisha hayo mapendekezo? Ni miaka 33 ya Tume lakini tangu mapendekezo mwaka 2003 ni miaka kadhaa sasa, lakini hakuna kitu na wakati huo mnaendelea kutumia bilioni 31 point; mtuambie mnataka muda gani hasa, nusu karne au karne moja?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, majibu ya Serikali yanasema kwa makini sana, Tume ya Pamoja ya Fedha imeandaa rasimu ya Mwongozo wa uendeshaji wa Akaunti ya Fedha ya Pamoja ambao unatarajiwa kutekelezwa mara baada ya majadiliano ya pande mbili za Muungano yatakapokamilika. Wameandaa rasimu sasa, miaka yote hiyo.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri atuambie maeneo machache ya rasimu hiyo, maana hakuna anayeamini tunaona ni kiini macho, kizungumkuti, tuambie hayo maeneo machache.
Mheshimiwa Spika, maeneo machache ya rasimu yaliyotayarishwa ni yapi? Kwa sababu tayari wameshaandaa rasimu lakini hakuna anayeamini, tunaona haya ni majibu tu ya kizungumkuti, kiini macho, kusadikika, tuambie hilo.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Spika, napenda kuongezea majibu ambayo yamejibiwa na Mheshimiwa Naibu Waziri. Majibu ambayo sisi kama Serikali tunaamini yalikuwa ni majibu mazuri, majibu yanayojitosheleza, lakini kwa kiu ya Mheshimiwa Masoud anasema bado Serikali haina dhamira ya kuhakikisha kwamba hiyo Akaunti ya Fedha ya Pamoja inaanza kufanya kazi.
Mheshimiwa Spika, katika bajeti yetu ambayo ilipitishwa na Bunge hili, Serikali kupitia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, aliliarifu Bunge lako Tukufu kwamba mwezi wa Aprili, tarehe 22, Kamati ya Pamoja ambayo inahusu Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na ya Muungano watakaa kwa ajili ya kuchambua mapendekezo ambayo yametoka kwenye Tume ya Fedha.
Mheshimiwa Spika, kwa bahati mbaya Mheshimiwa Rais wa nchi yetu ilikuwa ahudhurie Mkutano wa Commonwealth kule London, Uingereza, lakini akawa amemtuma Mheshimiwa Makamu wa Rais ambaye ndiye Mwenyekiti wa hicho kikao cha Kamati ya Pamoja, kwa hiyo, matokeo yake kikao kile hakikufanyika. Aliporudi wakati kikao kile kilikuwa kimeandaliwa tena, akatumwa na Mheshimiwa Rais kwenda kwenye Mkutano wa SADC.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba yale yote aliyoyasema tuko katika hatua nzuri. Mapendekezo yalishawasilishwa kwenye ile Kamati, ni uchambuzi tu ambao ukishafanyika yale maeneo ambayo alikuwa anasema ni maeneo gani yataweza kufanyiwa kazi na Mheshimiwa Mbunge atayafahamu. Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Jambo hili ni la muda mrefu na limekuwa likijitokeza kila mara. Si aibu wala si ajabu kwa lile linalotushinda tukawa wakweli na tukafanya lingine tunaloliweza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, haikuwa aibu kumuondoa Rais wa Zanzibar kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na hilo limefanyika; na hili la Akaunti ya Pamoja kama linatushinda ni kwa nini lisiondolewe na tukatafuta njia nyingine au utaratibu utakaotuwezesha kuliendesha jambo hili katika mustakabali huo, badala ya kuendelea kuvunja Katiba kwa kutotimiza takwa hili la kikatiba? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Khatib, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, masuala ya Muungano na zile changamoto zake tulishasema hapa Bungeni, changamoto zile 15 ambazo tulikuwanazo tayari 11 zimeshapatiwa ufumbuzi tumebaki na nne tu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hii Akaunti ya Fedha ya Pamoja anayoizungumzia tusipokuwa makini na jambo hili, tusipokuwa na maridhiano, tunaweza tukaingia kwenye matatizo ambayo yatasababisha Watanzania kuanza kusema kwamba, afadhali hata hiyo Akaunti tusingekuwanayo.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tuko kwenye uendeshaji wa gari, tunapokuta kuna kibao kimeandikwa hapa uendeshe speed 50 au 80 na sisi hatuna budi kufanya hivyo. Katika jambo hili kuna umakini mkubwa ambao unatakiwa.
Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Khatib Serikali ina dhamira ya dhati na wala hatuna kigugumizi na hatuna sababu yoyote ya kuuaibisha Muungano kwa sababu tulishaungana, haya mambo mengine yote haya tutayashughulikia vizuri. Atupe nafasi kwa sababu tumesema kile kikao kitafanyika, asiwe na haraka. Ahsante sana.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi pamoja na maelezo hayo mazuri na jitihada hizo za Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza ninaona hapa ni mamilioni mengi sana yamekuja katika nchi yetu ninauliza Serikali. Je, ni lini maeneo mahususi kama ya Mufindi, Njombe na Ruvuma ambako wananchi wana mwamko wa hali ya juu katika kupanda miti ambayo inasaidia kwa kiasi kikubwa ku- regulate mambo ya tabianchi. Lini wananchi hawa nao wataanza kunufaika na fedha hizi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili umeeleza kuhusu accreditation, kati ya tatizo kubwa ambalo linasababisha Taasisi zetu hapa nchini hususani za kijamii kama NGO’s kukosa fedha kutoka mifuko hii ni kwa sababu sisi kama Taifa bado hatujafanya accreditation katika huo mfuko ambao umeutaja.
Je, ni lini Serikali itakamilisha utaratibu huo ili pamoja na fedha hizi ambazo Serikali inazipata moja kwa moja taasisi pia za kiraia kama ma NGO’s yanayojishughulisha na mazingira yaweze pia kuanza kunufaika na fedha hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Chumi ametaka kujua ni lini fedha hizi zina tutazipata ama tutaweza kuzitumia hasa kwa watu ambao wanawajibika na suala la kutunza mazingira kwa kupanda miti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Chumi kwamba kwa sababu sisi focal point, sisi ndiyo waratibu wa mifuko hii hasa GEF, kwa hiyo wakati wowote tutakapokuwa tumepata fedha hizi hasa GEF7 maana yake tutatangaza ili kuhakikisha kwamba tunaweka vipaumbele kwenye eneo hili la wenzetu ambao wanashughulisha kutusaidia kwa ajili ya kutunza mazingira kwa kupanda miti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kupitia NGO’s na tuliposema kuhusiana accreditation maana yake tunatarajia fedha zitakapokuja tutaweka bayana na NGO’s zote na vikundi vyote ambavyo vimesajiliwa vipata fursa ya kuomba fedha hizo na sisi tutawapa kipaumbele, ahsante sana.
MHE. YUSSUF SALIM. HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri katika nchi yetu kuna mazoea ya kwamba miradi hii ya hifadhi ya mazingira inafadhiliwa fedha nyingi kutoka kwa wafadhili lakini wanapoondoka tu miradi yenyewe inakufa kwa mfano HADO, HASHI, katika ile miaka ya mwishoni mwaka miaka ya 1980.
Je, Mheshimiwa Waziri unatuhakikishiaje fedha hizi zitakazokuja sasa kwa ajili kukabiliana na tatizo la tabianchi zitatumika vizuri na zitakuwa endelevu ili kukidhi kile kiwango cha kupotea kwa misitu ya hekta laki 350,000 kila mwaka katika nchi yetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, na tumeanza utaratibu wa kuwashirikisha wananchi moja kwa moja katika miradi yote ambayo inakuja na miradi hii wananchi wenyewe wanatengeneza utaratibu wa kuweza kusimamia. Kwa hiyo, ni imani yetu kwa kupitia watalaam wetu na wananchi kuwashirikisha moja kwa moja na nimuombe Mheshimiwa Mbunge na yeye awe sehemu ya kuhakikisha kwamba hili suala linakuwa endelevu. Ahsante.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro inategemea sana upandaji miti wa wananchi wanaozunguka Mlima Kilimanjaro na unyevunyevu wa ile miti ndiyo unasaidia theluji mlimani iweze kuendelea kukaa na ikae kwa muda mrefu. Sasa nataka nimuulize Mheshimiwa Waziri au Serikali, fedha hizi zitakapopatikana maeneo muhimu kama haya yenye Hifadhi za Taifa kama mlima wetu, mko tayari hizi fedha zisaidie wananchi wale ili waweze kupanda miti kwa wingi kwa ajili ya kuhifadhi theluji katika ule mlima wetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kifupi ni kwamba tuko tayari kutoa fedha kwa kushirikiana pia na wezentu wa Maliasili hasa Wakala wa Misitu ambao pia watatusaidia kupata miti inayoweza kuhimili maeneo hayo. Ahsante.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijauliza maswali yangu ya nyongeza naomba tu nimsahihishe Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba tuna Kata ya Nangara na siyo Mangara lakini pia tuna Kata ya Bagara siyo Bagala, kwa hiyo nafikiri uta-capture hayo msahihisho. Naomba niulize maswali haya yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kwa mara ya kwanza niko disappointed kwa mara ya kwanza, hii ni essay siyo majibu na umenikumbusha wakti nipo Chuo Kikuu nilikuwa nikikosa jibu naandika the whole topic kama ni democracy and election naandika…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea…
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri haya uliyoandika ya Ziwa Jipe umeanzia Kenya, ukaja Ziwa Manyara kwanza lipo Mto wa Mbu hili andiko la Ziwa Manyara wala halihusiani na Babati na hakuna ulichojibu naomba sasa nikushauri; ni kwa nini usiongee na watu wa TANAPA watoe fedha, wasafishe Ziwa Babati kwa sababu sisi tuliomba mtupatie fedha wewe hapa hujasema unatupa fedha.
Sisi tunawalindia viboko wao, wanaua watu wetu, hakuna fidia basi nenda TANAPA wakupe fedha tusafishe Ziwa Babati otherwise msituachie Halmashauri sisi hatuna vyanzo hata ushauri huo naamini unaupokea. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepokea ushauri. (Makofi)
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Wizara kwa hatua inayochukua. Tatizo linaloikumba Ziwa Babati kadhalika linaikumba Ziwa Tawi katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu na kwa kuwa tatizo hili ni tatizo mtambuka kwa nchi nzima.
Je, Serikali haioni umuhimu sasa wa kuunda wataalam kwa nchi nzima na baadae kuzitafutia fedha za kunusuru maziwa hayo ili yaweze kuendelea kutoa huduma kwa jamii na viumbe wengine hai?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika majibu yangu kwenye swali la msingi nimeeleza tarehe 4 Septemba kimefanyika kikao cha wadau ambapo Waziri alikuwa amekisimamia na moja ya mambo ambayo wamejadili ni mkakati wa kuhakikisha kwamba wanaondokana na tatizo hili la magugu maji.
Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba utaratibu huu tutaendelea nao na baada ya kuweka ule mkakati basi tutahakikisha kwamba tunaweza kuondoa tatizo hilo.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
Mheshimiwa Spika, zipo sheria nyingine ambazo kuchelewa kuletwa Bungeni zina-cost maisha ya watu moja kwa moja. Kwa mfano, Sheria hii ya Usalama Barabarani, suala la sasa hivi Bodaboda ku-overtake kushoto linasababisha ajali nyingi sana na watu wengi wanapoteza maisha. Sheria inasema overtake kulia, lakini wewe una- overtake kushoto na ajali nyingi zinatokea kwa utaratibu huo.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa maisha ya watu yanapotea kila siku, Serikali haioni haja ya kuleta sheria hii kwa fast-track Bungeni ili kuokoa maisha ya watu wanaoteketea kila siku kwa sababu ya Sheria ya Barabarani kuwa imepitwa na wakati?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama ndani ya Bunge hili tukufu nikiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, nichukue fursa hii kuendelea kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuniamini kwamba ninatosha na ninaweza kumsaidia kazi hii ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Pia nakushukuru wewe kwa ushirikiano ambao unanipatia. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nampongeza Naibu Waziri, Mheshimiwa Mavunde namna ambavyo amejibu swali la msingi.
Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa katika kupambana na ajali za barabarani, na sisi tunajua kabisa bodaboda kama alivyosema Mheshimiwa Sakaya limekuwa ni tatizo kubwa. Tayari hivi tunavyozungumza, majibu mazuri kabisa ya Mheshimiwa Mavunde ni kwamba marekebisho ya Sheria ya Usalama Barabarani yako katika hatua za mwisho. Aiamini Serikali kwamba tutaileta hapa Bungeni kwa ajili ya Bunge hili kuweza kuipitisha. Ahsante. (Makofi)
MHE. SUSAN L. KIWANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante mimi siko mbali…
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Waziri Kangi Lugola ni awamu yake ya kwanza ya kuwa katika nafasi hii, na kwa kuwa mara nyingi nikimsikia na hata ndani ya Bunge amethibitisha ya kwamba atakomesha hiyo hali ya wananchi kuonewa, kuwekwa mahabusu muda mrefu bila utaratibu wowote.
Mheshimiwa Spika, je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari sasa kwenda kwenye mahabusu ya Wilaya ya Ifakara na Mlimba kwenda kuangalia hali halisi, mahabusu wanavyowekwa ndani muda mrefu lakini hata chakula hawapewi, mara nyingi nimeenda kuwanunulia chakula na kuwapa mahabusu haki zao zinavunjwa kabisa za kibinadamu, hilo wa kutowapa mahabusu chakula unalizungumziaje?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza wananchi wa Tanzania nataka niwahakikishie kwamba siyo nia wala lengo la Jeshi la Polisi kuwatesa mahabusu wanapokuwa wamekamatwa na wako ndani. Mahabusu wote wanapata chakula na wapo watu ambao wanapewa tender hizi za kuleta vyakula kwa mahabusu, hilo la kwanza.
Mheshimiwa Spika, pili kumekuwa na wananchi pia ambao wana vyakula wanavyohitaji kuwaletea wananchi mahabusu wao. Vyakula hivyo pia tumekuwa tukiwaruhusu kuwapatia mahabusu na kwa kuwa amelenga Mlimba, kwamba kuna matatizo nimeishasema kwamba kutokana na tatizo la baadhi ya askari wachache ama kuwabambikiza kesi wananchi ama kuwatesa nimesema jambo hilo halitakuwa na nafasi na litakomeshwa. Nimesema nitaanza ziara mikoa yote hivi karibuni na hizo kero nitazishughulikia. (Makofi)
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante.
Mheshimiwa Spika, katika siku za karibuni kumejitokeza tabia chafu, mbaya na ovu kabisa ya mahabusu kufia kwenye Vituo vya Polisi. Mahabusu anapelekwa, wanashikiliwa, wanapata mateso ambayo yanapelekea vifo vyao. Hivi karibuni tu kuna baadhi ya jamii zimekataa kupokea maiti kwenda kuzika kutokana na kufia ndani ya Vituo vya Polisi.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri anatoa kauli gani kali ya kukemea tabia hii ambayo inatia aibu nchi yetu ambayo ni ya haki na demokrasia?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa mwananchi kufa, anakufa wakati wowote, mahali popote na ndiyo maana sijui kwenye Qurani, ila kwenye Biblia ukisoma Muhubiri 9:12 ni kwamba kifo ni mtego, kifo humnasa mtu wakati wowote, mahali popote. Kwa hiyo, mwananchi anaweza akafa akiwa polisi, anaweza akafa akiwa anafanya mapenzi, anaweza akafa akiwa kwenye gari anasafiri, anaweza akafia hata humu ndani ya Bunge. Kwa hiyo, isije ikachukuliwa kwamba anayefia kwenye Kituo cha Polisi ni kwamba ameteswa. (Kicheko)
Mheshimiwa Spika, ninakiri kwamba kumekuwa na matukio ambapo wananchi wanafia mikononi mwa polisi na pale ambapo matukio hayo yanajitokeza tumekuwa tukifanya uchunguzi na pale inapobainika kwamba polisi wamehusika tumekuwa tukichukua hatua, ndiyo maana tunazuia wananchi wasichukue sheria mikononi za kuanza kuvamia vituo kwa sababu mtu amefia mikononi mwa polisi. Nimekuwa nikihoji huyu anayekufa akifanya mapenzi mbona hawaendi kuchoma kitanda na nyumba kwamba amefia mikononi mwa kitanda? Ahsante sana. (Makofi/Kicheko)
MHE. MWATUM DAU HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri aliyoyatoa yenye kila aina ya vinjonjo. Napenda kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa programu hizi katika sekta ya kilimo linahusiana na suala la kuhimili mabadiliko ya tabianchi; je, Serikali ina mkakati gani kutoa elimu kwa wakulima ili waende sambamba na mabadiliko ya tabianchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Mwatum ambaye amekuwa akifuatilia sana masuala ya mazingira na hasa mambo haya ya mabadiliko ya tabianchi. Namhakikishia kwamba pamoja na mipango hii ambayo Serikali tumekuwa tukiifanya, hata kule Unguja na Pemba tunashirikiana na Taasisi za Kimataifa USAID pamoja na FAO katika miradi ya kilimo ya kuhimili mabadiliko ya tabianchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa kutoa elimu, nimhakikishie Mheshimiwa Mwantum tayari mpaka sasa Serikali ilishatoa mwongozo pamoja na mafunzo kwa watu wapatao 192 wakiwemo Maafisa Kilimo, Maafisa Uvuvi, Maafisa Mifugo pamoja na Maafisa Mipango kutoka kwenye Halmashauri za Wilaya na kuwaelekeza kwamba katika mipango wanayoipanga Wilayani pamoja na bajeti waweze kushirikisha mipango hiyo ya kilimo himilivu cha mabadiliko ya tabianchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, elimu hii tayari tulishaipeleka kwa wananchi na bado tunaendelea katika mpango huu tuliosema endelevu wa kuhimili mabadiliko ya tabianchi, ni element ambayo pia inahusishwa. Pamoja na kwamba Mheshimiwa Rais alizindua juzi hapa ASDP II, vilevile kuna element ya kutoa mafunzo ya kilimo himilivu kutokana na mabadiliko ya tabianchi.
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali.
Mheshimiwa Naibu Spika, mapema mwaka 2017 niliwasilisha andiko la mradi ujulikanao kama Commitment Bush Fire Management and Livehood Improvement kwa lengo la kudhibiti uchomaji moto ovyo. Ni lini Wizara yenye dhamana itaweza kuwezesha mradi huu kwa kutoa fedha ili tuweze kutekeleza kikamilifu kwa kuanzisha zao ambalo ni rafiki na mazingira lakini pia na ufugaji wa nyuki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, mapema katika Mkutano uliopita Mheshimiwa Gashaza aliuliza swali la nyongeza kuhusiana na mradi wake huu.
Napenda nimhakikishie kwamba sasa hivi Ofisi ya Makamu wa Rais inaandaa maandiko mbalimbali kwa ajili ya kuomba fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunahamasisha Halmashauri za Wilaya waweze kuandika maandiko ambayo watayaleta Ofisi ya Makamu wa Rais ili tuweze kuwatafutia fedha katika kutekeleza miradi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Gashaza, andiko lake tumelipitia ni muhimu sana. Pia aliweza kuwahusisha wananchi wa Jimboni kwake kupitia michezo wakiwa na kauli mbiu ya kwamba mazingira ni uchumi ili waweze kucheza ligi ile na kauli mbiu hiyo waweze kuhakikisha kwamba wanajihusisha na ufugaji wa nyuki pamoja na kilimo ili wasiendelee kuchoma misitu ambayo inaendeleza uharibu wa mazingira.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Gashaza kwamba hata hiyo ligi yake, baada ya kupata fedha mimi mwenyewe nitaenda kumsaidia kuizindua ili iwe kichocheo kwa nchi nzima ili wananchi wengine nao wafanye hivyo. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, napenda kuuliza maswali ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa nini Serikali kama inaona umuhimu wa mazingira inashindwa kutenga fedha kwa ajili ya kutengeneza GFS Code? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, je, Wizara inao mkakati wa kusimamia hizi sheria kwa sababu sheria ni nyingi na zinajitosheleza lakini kinachoonekana hapa ni udhaifu katika usimamizi wa sheria. Je, mkakati upo wa kuzisimamia hizo sheria? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hawa Abdullahman Ghasia, Mbunge wa Mtwara Vijijini na kule kwao Naumbu karibu na Mkunguni wanamuita mama ambaye hakubali kushindwa, mama ambaye tunaamini kwa namna anavyowawakilisha Mtwara huyu mama mpaka mwenyewe atakaposema kwamba sasa basi nipumzike lakini anawawakilisha vizuri wananchi wa Mtwara Vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana wakati mwingine yeye kama mchezaji huwa ana-overlap anasaidia mpaka Jimbo la Mtwara Mjini. Juzi juzi ameuliza maswali ambayo yalikuwa yanahusu mifereji pale Mtwara Mjini, anamsaidia rafiki yetu ndugu Mheshimiwa Nachuma. (Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kulikuwa na tatizo la kupanga bajeti au kuanzisha code maalum (kasma) kwenye Halmashauri zote katika nchi yetu lakini Mheshimiwa Waziri amekwishatoa mwongozo na kuomba Halmashauri hizi waweze kuanzisha hiyo kasma na kutenga fedha. Hii ni sambamba na Wizara zote za kisekta kuanzisha kitengo maalum ambacho pia kinatakiwa kwa mujibu wa sheria kusimamia mazingira.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili, kwamba tuna mikakati na pengine anadhani ni udhaifu wa usimamizi wa sheria. Nimhakikishie Mheshimiwa Hawa Ghasia, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuanzia Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 27 imetoa wajibu kwa kila Mtanzania kulinda na kuhifadhi rasilimali za nchi yetu. Pia tuna Sera hii ya Usimamizi wa Mazingira ya Mwaka 1997 na yenyewe ni sera ambayo inahakikisha kwamba mazingira yetu yanalindwa vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Ghasia tuna sheria hii hapa Sheria Mama Na.20 ya 2004 ambapo Kifungu cha 6 kimewapa wajibu wananchi waweze kulinda na kuhifadhi mazingira. Tuna Ilani ya CCM hapa Ibara ya 152 ambapo tunakwenda kupambana na uharibifu wa mazingira ikiwa ni pamoja na kupambana na mabadiliko ya tabianchi. Ndiyo maana sasa kutokana na yote haya hata juzi hapa nilielezea tulivyo na mikakati ya 2007 ya kitaifa ya kuhimili katika masuala ambayo ni ya uharibifu wa mazingira. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge ni mashahidi hapa, suala ni mindset ya wananchi, tuna sheria nzuri na mikakati lakini mindset ya wananchi ndiyo tatizo. Mungu amemuumba mwanadamu kwa mfano wake lakini bado wanadamu hawahawa wanamuangusha pamoja na kwamba Mungu alimweka kuanzisha mazingira kwenye bustani ya Eden. Kwa hiyo, nitoe wote kwa wananchi wote na Wabunge, sisi wenyewe tuhakikishe kwamba tunalinda na kuhifadhi mazingira, ahsante.

MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye majibu ya msingi Naibu Waziri amesema kwamba tatizo ni pia uelewa mdogo wa wananchi kuhusu kutunza mazingira. Kwa kuwa sasa Mlima Kilimanjaro ile theluji inaendelea kuyeyuka na mazingira yamekuwa kame muda wote lakini wanawake na vijana wa Kilimanjaro wapo tayari kuungana na Wizara hiyo katika kuboresha mazingira hayo. Ni lini sasa hii Wizara ya Mazingira itawezesha wanawake na vijana wale kiuchumi ili wapate miche waweze kuotesha miti kwenye mashamba yao kuzunguka mipaka na pia kwenye barabara inayoelekea Mlima Kilimanjaro?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la shemeji yangu Mheshimiwa Shally Raymond, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa kwamba katika Mlima Kilimanjaro kutokana na athari za mabadiliko ya tabianchi ambapo maeneo mengi yameathirika ni pamoja na theluji ambayo imekuwa ikipamba ule mlima kule juu unakuwa ni kivutio katika masuala ya utalii. Pia tumeendelea kusisitiza kupitia Halmashauri za Hai, Rombo, Moshi Vijijini pamoja na Moshi Mjini kuhakikisha kwamba wanapanda na kuhifadhi miti. Hawa akina mama ambao amesema mimi nipo tayari kabisa kuja kwa hao akina mama japo hakuwasema ni wengi kiasi gani ili na mimi pengine niambatane na akina baba wengi kidogo kuja kuonana na hao akina mama.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Shally, baada ya Bunge hili, naye ni shahidi nilipokuwa Kilimanjaro nilimpa taarifa na kukupigia simu kwamba aje tushughulike na mazingira. Aliweza kuja na akanipa msaada ambao kwa kweli mpaka leo bado naukumbuka. Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza swali moja dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, inaonesha kwamba ukataji wa miti kwa ajili ya nishati ya mkaa umekuwa ni chanzo pia kikubwa sana cha kusababisha uharibifu wa mazingira. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba inaondoa VAT katika nishati ya gesi ili wananchi waweze kununua gesi hiyo kwa matumizi ya nyumbani kwa bei ndogo ili kuondokana na adha ya uharibifu wa mazingira inayosababishwa na ukataji wa miti ambalo ni tatizo kubwa katika nchi yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa katika Ilani ya CCM, ukurasa wa 212 - 213, sehemu ndogo ya (e) tumeelekezwa na chama sisi kama Serikali kwamba lazima tuhakikishe kwamba tunaongeza kiwango cha watumiaji wa nishati mbadala kutoka asilimia 30 mpaka asilimia 50 katika kipindi cha miaka mitano. Ndiyo maana katika Wiki ya Mazingira Duniani ambapo tulikuwa na siku tano pale Dar es Salaam tuliweza kuwaalika wadau mbalimbali ambao sasa wanakuja na teknolojia ya nishati mbadala. Wananchi waliweza kwenda pale wakashuhudia namna ambavyo hizi taka ngumu zikiwemo randa za mbao pamoja na vinyesi vya mifugo, wameweza kuja na teknolojia na kubana na kutengeneza mkaa. Kwa hiyo, tunaamini kwamba tutapunguza ukataji wa miti kwa sababu ya teknolojia mbadala.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwenye upande wa gesi kulikuwa na ORYX wanaonyesha kutumia gesi tutatumia fedha kidogo sana ambapo huwezi kulinganisha na mkaa. Ndiyo maana Mheshimiwa Waziri wa Nishati tayari wameshahakikisha kwamba usambazaji wa gesi katika Jiji la Dar es Salaam kwa kupitia mabomba sasa umeanza. Ni lengo la Serikali kwamba tutaenda na miji mingine na miji ndiyo inayotumia mkaa zaidi kuliko vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Msongozi, naamini wewe kama mdau wa mazingira jambo hili ambalo lipo kwenye ilani tutakwenda kufanya mageuzi makubwa ya kuhakikisha kwamba tunatumia nishati mbadala badala ya kuendelea kukata miti. Ahsante.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Nimuulize mtani wangu kama anavyotaka. Mwishoni mwa miaka ya 80 kulikuwa na uharibifu mkubwa wa mazingira ambao ulipelekea mmomonyoko mkubwa wa ardhi katika Mikoa ya Dodoma na Shinyanga na kukawa na miradi ya uhifadhi wa mazingira ambayo ilikuwa inaitwa HADO kwa Dodoma na HASHI kwa Shinyanga. Je, Serikali ina mkakati gani sasa wa kufufua miradi ile ambayo ilipelekea Mikoa husika kuwa na hali nzuri kama ilivyo Dodoma sasa? Serikali ina mpango gani wa kuhuisha miradi kama ile katika mikoa mingine ambayo imeathirika zaidi kwa uharibifu wa mazingira?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la mtani wangu wa kisiasa Mheshimiwa Yussuf, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe 19 wakati tunajibu swali la Mheshimiwa Mwantumu Dau Haji tulieleza mikakati mbalimbali ambayo tunayo katika kuhakikisha kwamba tunapambana na uharibifu wa mazingira katika masuala ya vyanzo vya maji lakini pia kwenye ardhi kama ambavyo Mheshimiwa Yussuf amezungumzia. Tulisema mkakati ule tumehusisha wasomi na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na utakuwa tayari hivi karibuni, unaonesha namna gani ambavyo katika nchi yetu maeneo yalivyoathirika, si tu kwa Dodoma huku ambako tunasema kuna ukame lakini pia maeneo yale ya wafugaji ambapo ardhi imeharibika kwa kiasi kikubwa. Mkakati ule tunauita ni Mpango Maalum Endelevu wa Matumizi Bora ya Ardhi pale ndipo ambapo tutakwenda kutekeleza mambo hayo kwa sababu mikoa yote ambayo ina shida kubwa zaidi ya mmomonyoko wa udongo imeanza kubainishwa katika mkakati ule. Nakushukuru sana.
MHE. IGNAS A. MALOCHA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kuniruhusu niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Ziwa Rukwa linatoa ajira kwa wananchi wengi kutoka katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Vilevile ni ziwa ambalo imegundulika gesi aina helium lakini ziwa hilo hilo linatabiriwa kukauka kwa miaka ijayo. Nini mkakati wa Serikali katika kunusuru ziwa hilo lisikauke? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Malocha, Mbunge wa Kwela, shemeji huyu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ufupi sana, tayari Ofisi ya Makamu wa Rais kupitia Waziri wa Nchi (Muungano na Mazingira), Mheshimiwa January Makamba alishatoa maelekezo kwa Halmashauri zote nchini kuhakikisha kwamba wanawasilisha ofisini kwetu vyanzo vyote vya maji pamoja na changamoto zake. Ziwa Rukwa ni miongoni mwa vyanzo vikubwa vya maji ambavyo hata bila kutuletea jina hilo tayari kitaifa tunafahamu kwamba Ziwa Rukwa ni chanzo cha maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Malocha na Mheshimiwa Mulugo, baada ya mkutano huu mimi pamoja na wataalam tutakuja kwenye Ziwa Rukwa ili kujionea sisi wenyewe namna gani mazingira yalivyoharibiwa ili tuweze kuchukua hatua stahiki na za haraka. Kwa hiyo, Mheshimiwa Malocha pale kwa shemeji yangu Movu pale wapelekee salamu waanze kufanya maandalizi ili wanipokee twende nao Ziwa Rukwa tuweze kufanya kazi hii ya Serikali. ahsante sana. (Makofi)
MHE. SAADA MKUYA SALUM: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu. Kabla sijauliza maswali yangu mawili ya nyongeza, nilikuwa nimepata confusion kwa sababu Mheshimiwa Waziri anasema kwamba, mwongozo umetekelezwa kwa asilimia 82.7 kwa 18 ambayo inawezekana ikawa ni jambo nzuri sana. Vile vile anasema kuna changamoto, kwa hivyo hizi statement zenyewe zina-contradict.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, huu mchanganuo wa asilimia 82.7 kwa Tanzania Bara na asilimia 18.3 umetumia vigezo gani? Maana yake huu mchanganuo yaani success, hii rate umetumia vigezo gani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, as far as I understand kwamba, ni karibuni tu hivi kumetolewa kumbushio kutoka Wizara inashughulika na Utumishi wa Umma kwamba baadhi ya Taasisi hazitekelezi agizo hilo. Kutokana na miongozo hii kutolewa bila kuwa na utaratibu wa kisheria, je, ni lini Serikali itakuwa inaandaa miongozo hii ikiambatana na utaratibu wa kisheria ili tuone kwamba hizi taasisi pamoja na mambo mengine zinatekeleza hii miongozo kwa mujibu wa sheria?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, NA MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Saada Mkuya Salum ambaye amekuwa akifuatilia sana masuala ya Muungano na hasa changamoto za Muungano. Ni Mheshimiwa Mbunge ambaye kwa akinamama tunasema ni mama wa nguvu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, majibu tuliyoyatoa hayana confusion, ni majibu ambayo yamenyooka kwa sababu mwongozo ule unazungumzia asilimia 21 Zanzibar na asilimia 79 Tanzania Bara. Sasa kilichokuja kutekelezwa ambapo kwa Zanzibar ni asilimia 18.3 halafu Bara ni asilimia 82.7 ambapo pengine yeye anadhani ule ndiyo mkanganyiko, tumetoa sababu Mheshimiwa Saada Mkuya, kwamba tumepata ugumu sana wa kujua Wazanzibar ambao wanaajiriwa kwenye Taasisi za Muungano kwa sababu wengi wanatumia anuani za Bara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani, miaka miwili tulikuwa na zoezi la kuhakiki watumishi hewa na vyeti hewa. Kwa hiyo, Serikali haikuweza kuajiri, ndiyo maana hizi asilimia hazikwenda juu sana. Hata hivyo, nimpe mfano mmoja; Wizara ya Mambo ya Nje, katika ajira za mwaka wa fedha 2014/2015, waliajiri watumishi 28, lakini kati ya 28 watumishi saba (7) wote ni Wazanzibar na ukipiga asilimia ni asilimia 25 ambayo iko juu zaidi asilimia 21 kwenye mwongozo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili anasema baadhi ya Taasisi hazizingatii, hazitekelezi mwongozo huo na kwamba na ili utekelezaji uwe na nguvu kwa nini kusiwe na sheria. Wazo lake ni nzuri kwamba, pengine mwongozo unaweza usitekelezeke, lije suala la sheria. Nimhakikishie kama ziko taarifa ambazo Mheshimiwa Mbunge anaweza akatuletea ofisini kwamba Taasisi zifuatazo hazitekelezi bado Serikali tuna uwezo wa kuzitaka zitekeleze hata kama Sheria haijatungwa. Kwa hiyo mawazo yake ni mazuri. (Makofi)
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona, nina swali moja dogo tu la nyongeza. Je, ni lini Zanzibar kutakuwa na Ofisi au Kurugenzi inayoajiri kwa shughuli za Muungano badala ya kuzifuatilia Bara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Fakharia alikuwa Kamishna mwenzangu kwenye Tume ya Utumishi wa Bunge, najua kabisa uwezo wake wa kuwawakilisha Wazanzibari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli hoja aliyoitoa ya kuwa na Kurugenzi kule Zanzibar siyo jambo baya, lakini nimhakikishie kwamba mpaka sasa tunavyokwenda na ndiyo maana tukaja na utaratibu wa huu mwongozo ambao tuliamini kama Serikali kwamba tunaweza tukatatua changamoto. Kikubwa ni kile ambacho Mheshimiwa Saada amesema kuzibana taasisi zinazohusika zihakikishe kwamba wanazingatia ule mwongozo katika kuajiri. Hata hivyo, wazo lake pia siyo baya.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Mpaka sasa hivi Mkoa wa Njombe kuna tatizo kubwa sana la kuuawa watoto wadogo. Sasa Serikali inasemaje kuhusiana na hili, maana wananchi wa Njombe sasa hivi wana wasiwasi mkubwa na wazazi wanawapeleka watoto wao shuleni. Je, Serikali inasemaje kuhusiana na mauaji haya yanayoendelea katika Mkoa wa Njombe?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kumekuwa na sintofahamu na kuzuka kwa taharuki katika Mkoa wa Njombe kutokana na vitendo vya baadhi ya Watanzania wenzetu ambao wamekuwa wakiwachukua watoto wadogo na kuwaua. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kuanzia juzi Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Injinia Hamad Masauni yuko kule Mkoa wa Njombe anafanya vikao na Kamati za Ulinzi na Usalama za Wilaya pamoja na Mkoa kuhakikisha kwamba vitendo hivi vinakomeshwa, lakini taarifa za awali zinaonesha ni imani za kishirikina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Wabunge watupe ushirikiano
kwa sababu Waheshimiwa Wabunge maeneo yale wanayafahamu vizuri. Nitoe onyo siyo kwa Njombe peke yake bali kwa Watanzania wote kwamba wasitingishe kiberiti cha Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, wasipoacha vitendo hivyo watakipata cha mtema kuni na tunaanza na kule Njombe ambako tumeshabaini majina kwa ajili ya kuwachukulia hatua za kisheria.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nimpongeze sana Mheshimiwa muuliza swali Mheshimiwa Mwatum Dau. Kwa kweli hawapati stahili zao Polisi na waliojenga Vituo vya Polisi pamoja na Ofisi zao. Swali la Msingi linahusiana na kwamba hawapati stahili zao, karibu mwaka wa sita au wa saba….

MWENYEKITI: Swali swali.

MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge hili limeahidi kwa kampuni ya Albertina kumlipa pesa zake milioni 200 kwenye bajeti iliyopita ya nyuma yake na mpaka leo hajalipwa na Mheshimiwa amekuwa akitembea na ilani ya chama cha Mapinduzi. Je, ni lini stahili hizi atapata kwa ajili ya kituo hiki cha…
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Mheshimiwa Jaku amekuwa akifuatilia sana suala la huyu Askari ambaye amezungumzia. Nimuhakikishie kwamba yale ambayo nimeyajibu kwenye swali la msingi, huyu anayemsema ni baadhi ya wale Askari ambao wako katika hatua za mwisho mwisho kumaliza matatizo yao. Ni kweli kabisa katika Ilani hii ya CCM, Ibara ya 146 imezungumzia stahiki za askari na ndiyo maana sisi kama Wizara tunawajibika kuhakikisha kwamba stahiki za askari hazichezewi kwa namna yoyote ile.
MHE. MWATUM DAU HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa jibu lake zuri ambalo alilolitoa hapo, lakini naomba kuuliza swali la langu la nyongeza. Tunaelewa kuwa Serikali inawajibika vilivyo katika kushughulikia na kutatua matatizo hayo. Je, ni lini hasa Serikali itafikia ukomo wa suala hili kwa kuwa imekuwa ni kero kubwa kwa Askari wetu, kwani kufanyiwa hivyo pia kunawanyima haki zao na vilevile itawapelekea kutokufanya kazi kwa ufanisi na uadilifu? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi ni kwamba Maofisa, Wakaguzi pamoja na Askari wa vyeo mbalimbali wa Jeshi la Polisi na hata vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama vilivyoko chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi mishahara yao inaendelea kurekebishwa. Hata hivyo, pale ambapo kutorekebishwa kwa mshahara kwa askari yeyote kutatokana na uzembe wa makusudi kwa Afisa ambaye anashughulika na mishahara ya Askari nimeshatoa maelekezo kwamba ifikapo mwezi wa Tano mwaka huu asiwepo Askari, wala Afisa wala Mkaguzi anayelalamikia stahiki yake. Pia nimewaelekeza kwamba wasicheze na maslahi na stahiki za Askari. Kufanya hivyo ni sawa na kushika mboni ya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niulize swali moja tu dogo la nyongeza. Kwa kuwa tunazungumza habari za stahiki za Maaskari Wilaya ya Kilolo toka imeanzishwa sasa hivi takribani miaka 17 Askari wamekuwa wakiahidiwa kuwa na Ofisi ya Wilaya ya Kilolo na nyumba za Maaskari, mpaka leo ni kila mwaka tumekuwa tukiahidiwa. Sasa nataka nijue kutokuwa na nyumba na Ofisi si wanakosa stahiki zao la halali?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Venance Mwamoto kwa jina la utani mzee wa vinungu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba siyo Jeshi la Polisi pekeyake tuna tatizo la ofisi pamoja na makazi kwa Askari. Hata hivyo, nimhakikishie kwamba tunaendelea kutenga fedha ili kupunguza kama siyo kumaliza kabisa suala la makazi na ofisi kwa ajili ya Jeshi la Polisi. Nitumie fursa hii pia kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye amekuwa akitupatia fedha kwa ajili ya kujenga nyumba za Askari na mpaka sasa kuna nyumba za Askari ambazo zinaendelea kujengwa kwenye mikoa mbalimbali. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Venance Mwamoto na baada ya Bunge hili nilimwahidi nitakwenda Kilolo kwa ajili ya kujionea hali ilivyo. Ahsante
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri kwamba kuna Maaskari Polisi waliopandishwa vyeo, alipandishwa kutoka private kuja Koplo ametumikia Koplo kwa miaka minne, mpaka ameenda Sajenti hajapata mshahara ule wa Koplo na wengine mpaka wanafikia kustaafu wanakosa stahiki zao analipwa kwa mshahara ule aliotokea nao. Je, Mheshimiwa Waziri Askari kama hawa atawa-consider vipi katika zoezi analoendelea nalo ili wapate haki zao kulingana na Utumishi wao walivyotumikia nchi hii?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudie kusema kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, kwamba mishahara inaendelea kurekebishwa kwa Maofisa, Wakaguzi pamoja na Askari. Hata hivyo, kama kuna suala ambalo linamhusu Askari ambaye amemsema kwamba alipanda cheo na nirekebishe kidogo, Jeshi la Polisi hatuna private, tuna constable kuanzia constable akaenda Koplo, Sajenti na hajarekebishiwa, namwomba Mheshimiwa Yussuf anipe jina la Askari huyo ambaye amemsema ili nifuatilie nijue kwa nini apande vyeo vyote hivyo pasipo kurekebishiwa mshahara wake. Ahsante.
MHE. ANNA R. LUPEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Wilaya ya Mlele inakaa Mahabusu kidogo sana, wanakaa watu takribani kumi, lakini kutokana na uhaba wanakaa watu kuanzia 30 mpaka 40 na wale ni binadamu na sisi binadamu tuna maradhi mengi wanaambukizana, wanakula mle ndani. Kwa nini Serikali wale watu wenye makosa madogo madogo wanaotakiwa kupewa dhamana, wasipewe dhamana ili waende kufanya shughuli zao zingine ili Mahabusu isikose watu kwa sababu mhalifu anajulikana na mhalifu ni Mtanzania anajulikana katika maeneo anayoishi. Je, ni kwa nini wasiwe wanapenda kutoa dhamana ili Mahabusu hizi zisiwe na watu ili msongamano uweze kupotea?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, Wilaya ya Mlele katika kile Kituo cha Polisi hakuna magari, hakuna magari sasa unakuta Mahabusu wale wanakaa wiki nzima wakibanana mle ndani; je, ni lini Serikali itatununulia magari kwa ajili ya uboreshaji zaidi kwa sababu wanatolewa Mlele wanapelekwa Mpanda? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anna Richard Lupembe Mbunge wa Viti Maalum ambaye ni Mtumishi wa Mungu. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Anna Lupembe ambaye ni Mtumishi wa Mungu kwa namna ambavyo amekuwa akiwahamasisha Watanzania na waumini katika kulinda amani na kufanya doria za kiroho. Kwa hiyo nimpongeze sana kushiriki kwenye ujenzi na ulinzi wa amani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba pale Mlele kuna tatizo la Gereza na kama nilivyojibu kwenye jibu la msingi kwamba Serikali iko kwenye mchakato wa kuhakikisha hizi Wilaya mpya tunajenga Magereza na Magereza mengine kwenye mikoa mipya. Tatizo ni kwamba ni kitu ambacho hakiwezekani kupangisha Gereza kwamba unaweza ukaenda kwenye nyumba ya mtu ukasema tumekuja tupangishe kwa ajili ya Gereza. Kwa hiyo kwa vyovyote vile lazima sisi kama Serikali tuendelee na mipango yetu ya kuhakikisha kwamba tunajenga Gereza. Ndiyo maana tumeanza kupunguza msongamano kwa kutumia Sheria mbalimbali ikiwa ni pamoja na mawazo yake aliyoyasema ya dhamana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye swali la gari, Wilaya zote tumezipa gari kwa ajili ya kuhakikisha kwamba gari zile zinasaidia kubeba Mahabusu. Kwa kesi ya Mlele Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Katavi nichukue fursa hii kumpongeza ameshaanza juhudi kwa kushirikiana na Mkuu wa Wilaya kuhamasisha wananchi na tayari ameshatoa mifuko 200 kwa ajili ya kuanza kujenga Gereza la Mlele na tayari tumeshampatia ramani. Kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa anayoifanya tutakapokwenda Mlele tutashirikiana pamoja na wananchi. Ahsante.
MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo nyongeza. Tangu mwaka 2017 mwezi wa Pili, huu ni mwaka wa tatu jengo hili halijawahi kutumika baada ya kulikabidhi kwa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Wananchi wanatoka kilometa 30 kufuata huduma Dodoma Mjini badala ya kwenda Bahi ambayo ndiyo Wilaya iliyopo Tarafa ya Chipanga. Wananchi wanateseka kwa sababu hawana mahali pa kupeleka wahalifu wanapokamatwa. Je, Serikali iko tayari sasa kufanya ukarabati kwa mwaka huu wa fedha katika jengo hili ambalo tulikabidhi litumike kama Kituo cha Polisi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, je, Mheshimiwa Waziri yupo tayari sasa aandamane pamoja nami baada ya Bunge hili twende akaongee na wananchi ambao wamekaa kwa muda mrefu wakisubiri jengo lile litumike kama Kituo cha Polisi?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Bura kwa namna ambavyo anachapa kazi kwa umahiri na juhudi kubwa kwa wananchi wa Mkoa wa Dodoma. Ndiyo maana Mheshimiwa Bura namfananisha na kumlinganisha na mama mmoja kwenye Biblia naitwa Ester. Mama huyu akiwa bikira alipata kibali machoni pa Mfalme Ahasuero wa kule Shushani Ngomeni. Kwa hiyo, Mheshimiwa Bura amepata kibali kwa wananchi wa Mkoa wa Dodoma katika kuwafanyia kazi iliyotukuka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, ni kweli kwamba Kituo hiki cha Polisi cha Chipanga kina matatizo ambayo tumeyafanyia tathmini. Namhakikishia Mheshimiwa Bura awe na amani, kwamba kituo hicho baada ya kufanya tathmini, tutatenga fedha kwa ajili ya kwenda kukikarabati ili kianze kutoa huduma kwa wananchi wa Chipanga katika Wilaya ya Bahi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Felister Bura nikukuhakishie kwamba huko unakotaka twende labda wewe ndio umechelewa, mimi niko tayari hata leo hii ukitaka tutakwenda wote kule Bahi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nitoe wito kwa Mabaraza ya Madiwani kote nchini kwamba katika Ilani hii ya CCM, Ibara ya 146 chama kimeelekeza Serikali zake mbili kwa maana ya Serikali za Mitaa na Serikali Kuu. Nawaomba Waheshimiwa Madiwani, kwenye makusanyo ya ndani watenge pia fedha kwa ajili ya kujenga Vituo vya Polisi pamoja na nyumba za askari ili tuweze kuhakikisha kwamba tunatoa huduma bora kwa wananchi hapa nchi. (Makofi)
MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nimpe pole sana Mheshimiwa Waziri kwa kuvamiwa Kituo chake cha Polisi cha Madema…

MWENYEKITI: Waheshimiwa, muda wetu umekwisha. Mheshimiwa Jaku.

MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Tarehe 25 Julai, 2017, naomba kunukuu Hansard, “taratibu hizo zilishafanyika kama nilivyokwambia sasa. Tarehe 9 Novemba, “Serikali inatambua deni hilo.” Tarehe 8 Novemba, 2017 mwaka wa Fedha 2017, “Jeshi la Polisi limetenga jumla ya shilingi bilioni 2.2 kwa ajili ya kupunguza madeni ikiwemo mkandarasi.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naona ni aibu kwa Serikali yangu kupata aibu na hili deni ni la muda mrefu. Je, Mheshimiwa Waziri, hesabu hata ulipochaguliwa wewe Jimboni kwako ulianzia kwa kura moja ukafika hapa. Kama mimi, Serikali yangu kupata aibu nami ninaipenda niko tayari…

MWENYEKITI: Mheshimiwa, uliza swali.

MHE. JAKU HASHIM AYOUB: …niko tayari kuanza kuchangia shilingi milioni moja kwa ajili ya kituo. Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kuchukua shilingi milioni moja, kupokea mchango huu ili tufuatane kupeleka deni hilo na hizi hapa? Maana yake deni limeshakuwa la muda mrefu. Yuko tayari kupokea shilingi milioni moja kufuatana nami kupeleka hizi fedha za deni?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Ilani hii ya CCM ujenzi wa vituo vya Polisi na makazi ya Askari tumeweka utaratibu kwamba tutahusisha wadau. Ninashukuru sana wewe Bungeni kujitokeza kuwa mdau kwa mujibu wa ilani hii. Hivyo naomba mchango wako uuwasilishe kwa Inspekta Jenerali wa Polisi ili tuendelee na ujenzi wa vituo vya Polisi hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ni kweli kabisa kwamba deni la huyu Mkandarasi limekuwa la siku nyingi. Nimhakikishie Mheshimiwa Jaku, ambaye najua akifuatilia jambo lake ni king’ang’anizi, ni moto wa kuotea mbali; na kwa kweli siku siyo nyingi hatutakubali jambo analolisema kwamba Serikali yetu inatiwa aibu. Ndiyo maana Wakandarasi wengi nchini wanapenda kufanya kazi na Serikali na Serikali yetu inalipa madeni yake na deni lake limeshahakikiwa, awe na subira wakati wowote tutaweza kumlipa Mkandarasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. JUMA S. NKAMIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Naomba niulize swali moja dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Chemba ni moja kati ya wilaya mpya. Tumeanza kujenga kituo cha Polisi kwa sababu huduma nyingi za Polisi zinapatikana kwenye Wilaya mama ya Kondoa: Je, Serikali ina mchango gani kuhakikisha kwamba tunakamilisha ujenzi wa Kituo cha Polisi pale Chemba ambao tayari tumeuanza?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Juma Selemani Nkamia, Mshabiki wa Simba namba moja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi katika muundo wake na utoaji wa huduma, tunayo Mikoa 35 ya Kipolisi, tunazo Wilaya 182 za Kipolisi na pia tunazo Tarafa 610 za Kipolisi na tuna Kata na Shehia 4,410. Kwa hiyo, tunao mpango mkakati kuhakikisha kwamba huduma hizi zinakwenda kwenye maeneo yote hayo; na bado tuna mikoa mipya na wilaya mpya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Juma Nkamia kwamba Wilaya ya Chemba ni miongoni mwa wilaya ambazo mikakati yetu ndani ya Jeshi la Polisi tunakwenda kujenga kituo cha Polisi katika Wilaya ya Chemba.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza, nimshukuru Mheshimiwa Waziri na kumpa pongezi kwa majibu yake ambayo yanaonyesha nia ya dhati ya Serikali kuwasaidia wafungwa wanawake. Maswali yangu mawili yanyongeza ni kama ifuatavyo:-

(a) Je, Serikali inawasaidiaje watoto ambao wapo gerezani na mama zao kielimu na kisaikolojia kwa kuzingatia haki za watoto husasan wanapotumikia kifungo hicho ambacho watoto wao hawahusiki nacho?

(b) Je, Serikali haioni umuhimu sasa wa wanawake wafungwa ambao ni wajawazito wakatumikie kifungo hicho nje ili waweze kuwalea watoto wao katika familia huru badala ya kuwa gerezani?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Malembeka kwa jina maarufu Nyoka wa Kijani, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba wapo akina mama wafungwa ambao wanajifungua watoto wakiwa magerezani. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Nyoka wa Kijani, Nyara ya CCM kwamba utaratibu wa Jeshi la Magereza kupitia kanuni za Jeshi la Magereza watoto ambao wamekwishazaliwa magerezani wanpofikia umri wa kuanza awali wamekuwa wakisoma kwenye shule za awali zilizopo kwenye magereza zetu. Pia kwa kupitia watumishi wa magereza ambao wana utaalamu wa masuala ustawi wa jamii wamekuwa wakiwapa elimu pamoja na kuwafariji watoto hawa ili wajione wao siyo wafungwa ndani ya magereza isipokuwa wamezaliwa katika wakati ambao mama zao wapo magerezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kwamba kwa nini wafungwa ambao wanajifungua magerezani wasipate adhabu nyingine badala ya kuwafunga magerezani. Tunao utaratibu kupitia sheria yetu ambayo inaitwa Probation for Offenders pamoja na Community Services, wale ambao wana vifungo chini ya miaka mitatu tumekuwa tukiandaa utaratibu wa kuwaondoa magerezani ili wawe na vifungo mbadala. Hata hivyo, kuna utaratibu watoto wanaokuwa magerezani wanapofikia umri ambao wanaweza wakaishi uraiani bila kuwa na mama zao ndugu zao wamekuwa wakishirikishwa ili waweze kutoa malezi kwa watoto ambao mama zao wapo magerezani. Ahsante sana.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimwia Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi. Katika Gereza la Morogoro Mjini kuna msongamano mkubwa sana wa mahabusu na wafungwa hasa kwa upande wa wanawake. Je, kuna mkakati gani wa kupunguza msongamano huu wa wafungwa na mahabusu hasa wanawake kwenye Gereza la Morogoro?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christine Ishengoma, Mkuu wa Mkoa Mstaafu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kuna msongamano kwa wafungwa na mahabusu katika magereza mbalimbali katika nchi yetu. Gereza alilolisema Morogoro ni mojawapo ya magereza yenye msongamano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali kupitia sheria mbalimbali tumekuwa tukijaribu kuzitumia ili kuwaondoa wafungwa ambao wana vifungo vifupi. Pia tumekuwa tukitumia Sheria yetu ya Parole kupunguza msongamano. Vilevile Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amekuwa akitoa msamaha kwa wafungwa ili kupunguza msongamano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kuwataka Watanzania popote pale walipo wasijihusishe katika uhalifu utakaowasababishia wawe wafungwa ama mahabusu. Waelewe kwamba watakapofanya uhalifu wataenda kwenye magereza ambazo zina msongamo. Kwa hiyo, nichukue fursa hii kuwasihi wasijihusishe katika uhalifu. Ahsante sana.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa ujauzito ni kawaida kwa mwanamke yeyote kwa mfungwa au mtu aliyepo uraiani. Kwa hawa wafungwa ambao tayari ni wajawazito, kuna wakunga standby ili wawasaidie? Kwa sababu uchungu unakuja time yoyote na wapo ndani ya gereza, je, mnawawekea wazalishaji/wakunga standby wa kuwasaidia uchungu unapowajia?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, kwamba kwenye Jeshi la Magereza, tunazo Zahanati na Vituo vya Afya ambapo wapo Madaktari wanaotoa utaalam wao kuhakikisha kwamba yale mahitaji yote ya akina mama katika kuhudhuria kliniki na kufuatilia siku za kujifungua wanazifanya kama kawaida. Pia tunao wakunga ambao siku zao zikifika wanawazalisha kama kawaida na hata vifaa vya kujifungulia wanavipata kama kawaida; na hata vile vyakula ambavyo akina mama, vinachochewa na mahitaji ya ujauzito; iwe ni udongo au chakula chochote kile wanaletewa kama kawaida. Ahsante sana.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mwuliza swali alitaka kujua msaada unaopatikana kwa hawa mama zetu wanaokuwa wajawazito Magerezani na kujifungua. Zipo taarifa kwamba wako baadhi ya wanawake wanaoingia wakiwa sio wajawazito lakini wakapata ujauzito ndani ya Magereza. Inaeleweka kwamba walinzi wa wafungwa wa kike ni wanawake, mimba hizi wanazipataje Mheshimiwa Waziri?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa hakuna mimba ambazo zinatokea Magerezani. Hilo la kwanza. La pili, mimba tunazozizungumzia ni mimba ambazo mfungwa ama mahabusu anaingia gerezani akiwa tayari kule uraiani anakotoka ameshapata ujauzito.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana kulitokea jaribio hapa kwa Wabunge wakiwa wanataka tuweke sheria au utaratibu wa kuruhusu wenza wa mfungwa anayekuwa Gerezani ili waweze kupata fursa ya kwenda kufunguka wakiwa Gerezani, ya kwenda kujinafasi wakiwa Gerezani, lakini tulisema kwamba kwa sheria zetu na mila zetu, hatuwezi tukaruhusu hali hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. REHEMA J. MIGILLA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini naona majibu haya yamejibiwa kisiasa kuliko uhalisia wenyewe ulioko huko kwa waendesha bodaboda.

Mheshimiwa Spika, ni ukweli ulio hai kabisa bodaboda hawa wamejiajiri wenyewe na wanafanya kazi katika mazingira magumu na wamekuwa wakisumbuliwa sana na polisi especially hawa PT. Wanawakamata na wakishawakamata hata uchunguzi wa kina haufanyiki na sometimes wanawabambikizia makosa. Wanapowabambikizia makosa wanawaaambia watoe hela, wasipotoa zile hela pikipiki zao zinapelekwa polisi. Zikifika polisi, pindi wanapotaka kuzichukua wanakuta baadhi ya vitu kama betri, mafuta na hata wakati mwingine wanakuta hadi gamba zimebadilishwa na tunaelewa kabisa polisi ni mahali ambapo pana usalama wa kutosha na hakuna mtu ambae anaweza akaenda kubadilisha kitu chochote pasipo kukamatwa.

Mheshimiwa Spika, sasa je, Mheshimiwa Waziri, unataka kutuambia wanaohusika na hili zoezi la kuchomoa vitu au vielelezo ni Polisi au akina nani na tunajua kabisa pale ni mahali salama?

Mheshimiwa Spika, swali la pili nataka kufahamu pia pamekuwa na mrundikano mkubwa sana wa pikipiki katika vituo vya polisi na ukizingatia chanzo cha kukamatwa kwa hizi pikipiki na mrundikano huo ni hawa hawa polisi wanazikamata na kuwataka hao watu walipe…

SPIKA: Sasa swali.

MHE. REHEMA J. MIGILLA: … swali langu; Je, Serikali ina mpango gani kuwarudishia hawa watu pikipiki zao ambapo kwa kuendelea kukaa pale zinaidi kuharibika?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza kwa pamoja ya Mheshimiwa Rehema, Mheshimiwa Mbunge ambaye kwa muda mfupi tangu alipoingia Bungeni ni Mbunge machachari na nimekuwa nikimpa ushirikiano kwa masuala ya Mkoa wa Tabora.

Mheshimiwa Spika, mwanzoni nilikuwa najiuliza kwanini watu wanaoagiza magari bandarini vitu vinachomolewa au watu kwenye viwanda vya ndege kunakuwa na pilferage lakini baadaye nikaja kushangaa hata kwenye vituo vya polisi vitu vichomolewe nikaona ni jambo ambalo linashangaza sana.

Mheshimiwa Spika, nilichofanya, kama Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, kwenye ilani hii ya CCM Ibara ya Nne, CCM imeamua kwamba katika changamoto zile nne za Ibara ya 4 za kupunguza umaskini, za kutatua tatizo la ajira tena tukataja bayana vijana, nataka nilihakikishie Bunge lako tukufu kwamba bodaboda ambazo nimetoa maelekezo ili wapambane na umaskini na tatizo la ajira ni bodaboda za makundi manne tu zitakazochukuliwa kupelekwa kituo cha polisi na hata kwenye bajeti hapa nilisema.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, kundi la kwanza, ni bodaboda ambayo imehusika kwenye uhalifu, kwa sababu bodaboda zinatumika kufanyia uhalifu. Hiyo ikikamatwa itapelekwa kituoni. Kundi la pili ni bodaboda ambayo inahusika na kesi na kesi yenyewe, moja ni kama bodaboda hiyo imehusika kwenye ajali ya barabarani ama bodaboda iliyoibiwa sasa katika recovery ikawa imekamatwa, ni kielelezo. Kundi la tatu na la mwisho ni bodaboda ambayo haina mwenyewe sisi (found and unclaimed property) sasa polisi kwa sababu wanalinda mali za raia wataichukua ikae kituo cha polisi, ikipata mwenyewe ichukuliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, boda boda zingine zozote ambazo hazipo kwenye kundi hilo, sijui huyu hana helmet, huyu hana side mirror, huyu amepakia mshkaki, hakuna bodaboda itakayokamatwa kupelekwa kwenye kituo cha polisi. Nimewapata utaratibu wa kuwapa siku saba kama ni faini watalipa na nimeelekeza bodaboda ambazo ziko kwenye makundi matatu ztakazopelekwa kituo cha polisi na zenyewe wataandikiwa hati inayoonesha vitu ambavyo viko kwenye bodaboda ile ili atakapokuja huyu mtu a-cross check na hati aliyopewa ili yule aliyechukua kama kuna upotevu aweze kushughulikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sasa hivi bodaboda nchi nzima wanakula raha mstarehe, wanajinafasi. Kama Tabora suala hilo bado linaendelea, Mheshimiwa Rehema nikuhakikishie itakapofika jioni kama Tabora pale kuna pikipiki ambayo haiko kwenye makundi hayo, ama zao ama zangu. Ahsante sana. (Makofi/Kicheko)
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Kwanza nisikitike sana kwa majibu yaliyotolewa na Mheshimiwa Naibu Waziri hayaendani kabisa na maeneo ya Jimbo langu la Geita.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa bahati nzuri Waziri mhusika Mheshimiwa Kangi Lugola familia yake maana yake Mama yake na Dada zake wanaishi kwenye Jimbo langu, na Mheshimiwa Kangi Lugola mwenyewe ameishi kwenye Jimbo langu anayajua mazingira na majibu yaliyotolewa siyo sahihi. Kwa mfano, ukichukulia kituo cha Nyarugusu, Nyakagwe, Buziku, Bwanga na Chato Vijijini haya yote ni mazingira ambayo karibia tunafanana lakini wenzetu tayari wana Askari wa Kike. Sasa ninataka kujua ni lini Serikali itanipatia Askari wa Kike kwa kuwa majibu waliyotoa ni ya uwongo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Centre ya Nkome ni centre ya tatu kwenye Mkoa wetu wa Geita kwa ukubwa. Kituo kilichopo pale kinaongozwa na Inspekta na nimekijenga mimi kama Mbunge. Tatizo linaloonekana hapa kwamba hakuna makazi ya kuweza kumuweka Askari wa Kike, wajibu wa kujenga makazi bora ya askari ni ya Wizara.

Je, ni lini Serikali itachukua dharura ya kwenda kujenga hiyo nyumba anayotakiwa kukaa Askari wa Kike? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa kwamba taratibu hasa zinazohusu upekuzi ni lazima Askari wa Kike ampekue mtuhumiwa wa kike. Majibu mazuri kwenye swali la msingi ameyasema Naibu Waziri wangu, kwamba hata pale ambapo kunakuwa na changamoto ya kutokuwepo Askari wa Kike upo utaratibu ama wa kumtumia mgambo wa kike ama kumtumia Mke wa Askari ambaye yuko jirani na mahali ambapo kuna mtuhumiwa. Najua suala la Mheshimiwa Musukuma nimeshamwagiza tayari Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Geita kupeleka Askari wa Kike kwenye Kituo cha Polisi cha Nkome. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wapo Waheshimiwa Wabunge wengi ambao wamekuwa wakiomba tuwapelekee Askari wa Kike kwenye vituo vya Polisi. Ninajua Waheshimiwa Wabunge Askari wa Kike wanapokuwa katika maeneo mbalimbali ni faraja kwa wananchi kwa sababu Askari wa Kike wao wanaruhusiwa hata kuwapekua watuhumiwa wa kiume. Kwa hiyo ninajua kwamba Mheshimiwa Musukuma anatarajia kuona Askari wa Kike katika maeneo mbalimbali ya vituo vya Polisi. Kwa hiyo nimpe faraja kwamba pale ambapo kuna changamoto kama hiyo na juzi tumepata Askari kutoka Chuo chetu cha Polisi Moshi, tutawapelekea Askari wa Kike.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi/ Kicheko)
MHE. ALHAJ ABDALLAH M. BULEMBO: Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, ni kanuni namba ngapi zinazoelekeza kampuni ikiuzwa asilimia mia iendelee kutumia kibali cha kampuni nyingine na jina tofauti la kampuni nyingine?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa nini brand ya Garda World itumike kama nembo badala ya kutumika kama kampuni nyingine na kwa hali hii hamuoni haki za watumishi wa kampuni ya zamani zinapotea kwa kuhalalishwa na Serikali yenyewe?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu Maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Alhaj Abdallah Majura Bulembo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa usahihi kilichouzwa ni hisa. Hivyo wamiliki wa hisa wamebadilika lakini kampuni inabaki kama ilivyo. Hivyo Ultimate Security Company iko palepale, kwa usajili uleule na watumishi walewale na mikataba yake ileile na mali zake zote na vibali vyake vilevile na biashara yake yote. Hivyo uhalali wa kutumia vibali unapatikana na sheria iliyotumika ni Companies Act, No.12 kama ilivyorejewa 2002, Cap. 212, section 74 - 83. Hicho kinachoitwa jina lingine ni “brand name” ambalo inaruhusiwa chini ya Sheria ya Trade Marks, No.12 ya 1986, Cap.326 na Trade Mark hiyo imesajiliwa na BRELA chini ya sheria hiyo.

Mheshimiwa Spika, haki za watumishi zinabaki kama zilivyo na kilichonunuliwa ni hisa. Hivyo, kampuni na vyote vilivyomo ikiwa ni pamoja na watumishi na haki zao zinabaki kama zilivyo kwa mujibu wa mikataba yao.