Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. John John Mnyika (22 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Katiba na Sheria ina wajibu wa kuiwezesha nchi kuwa na mfumo mbalimbali wa Kikatiba na Kisheria katika kufanikisha Mipango ya Maendeleo ya Taifa. Pamoja na wajibu huu muhimu hotuba nzima ya Waziri haijazungumzia kabisa kuhusu mchakato wa Katiba mpya. Aidha, katika vitabu vya bajeti hakujatengwa fedha zozote/kiasi chochote kwa ajili ya kuendeleza mchakato wa Katiba mpya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali inadhihirisha kwamba Serikali ya Rais Dkt. John Magufuli lazima dhamira ya kuendeleza kwa wakati mchakato wa mabadiliko ya katiba. Hivyo ni vyema Serikali ikatoa kauli hii Bungeni ni kwa nini haijatenga fedha kwa ajili ya mchakato huu muhimu kwa maslahi ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika aya ya 20, 21, 22, Waziri wa Katiba na Sheria amezungumzia kuhusu utekelezaji wa mkakati wa kuboresha huduma za Mahakama ikiwa ni pamoja na kufanya ujenzi na ukarabati wa Mahakama mbalimbali nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika orodha hiyo imetajwa Wilaya mpya ya Kigamboni, hata hivyo Wilaya mpya ya Ubungo haijatajwa hivyo, Serikali itoe kauli ni kwa nini Wilaya mpya ya Ubungo haijajumuishwa na lini Mahakama ya Wilaya ya Ubungo itajengwa. Aidha, Mahakama hiyo ni vyema ikajengwa katika Jimbo la Kibamba yalipo Makao Makuu ya Wilaya mpya ya Ubungo kama ilivyopendekezwa kwa nyakati mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume ya kurekebisha Sheria ina wajibu na mpango muhimu ya maboresho ambayo yamependekezwa muda mrefu ni pamoja na matumizi ya lugha ya Kiswahili katika mfumo mzima wa Mahakama na utungaji sheria nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imeeleza kuwa imefanya uchaguzi kuhusu mabadiliko yaliyowasilishwa katika THUB.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiwa Mbunge wa Ubungo niliwasilisha malalamiko na madai ya kutaka, uchunguzi kuhusu ukiukwaji wa haki za binadamu na misingi yake ya utawala bora juu ya mgogoro wa muda mrefu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu matatizo ya maji katika Kata ya Goba naomba kupatiwa majibu juu ya hatua ambazo Tume imechukua na kupatiwa nakala ya ripoti ya Tume kuhusu uchunguzi huo. Aidha pamoja na uwekezaji mkubwa wa Serikali juu ya miradi ya Ruvu juu na Ruvu chini tume ielewe kwamba Goba bado imeachwa kama kisiwa kwa kuwa haina mtaro wa mabomba.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatia kugawanywa kwa Manispaa ya Kinondoni na kuanzishwa kwa Wilaya mpya ya Ubungo, Hospitali ya Mwananyamala kwa sasa inahudumia zaidi Manispaa ya Kinondoni. Hospitali ya Sinza Palestina iliyobaki katika Wilaya ya Ubungo haina hadhi na uwezo wa kutoa huduma kwa Manispaa nzima. Hivyo, Wizara ichukue hatua za haraka za kuboresha huduma katika hospitali hiyo ya Palestina ilingane na wajibu wa kutoa huduma kwa Manispaa mpya ya Ubungo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, hospitali hiyo iko mbali na Jimbo la Kibamba lenye Kata za Goba, Saranga, Msigani, Mbezi, Kwembe na Kibamba; na pia kimuundo Wilaya ya Ubungo inapanuka kuelekea Kata hizo za pembezoni makao makuu ya muda ya wilaya yakiwa kwenye Kata ya Kibamba na ya kudumu yakitarajiwa kujengwa kwenye Kata ya Kwembe. Kadhalika kuna ujenzi wa Mji Mpya wa Viungani (Satelite town) katika eneo la Luguruni hivyo, ni muhimu kukawa na mkakati wa kupandishwa hadhi kituo cha afya kuwa hospitali ya wilaya na zahanati kuwa, kituo cha afya katika kila mojawapo ya kata hizo za pembezoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua kwamba, kuna hospitali kubwa katika Chuo Kikuu cha Afya (MUHAS), Campus ya Mloganzila. Hata hivyo, hospitali hii hadhi yake itakuwa sawa na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili hivyo, haitakuwa rahisi kwa wananchi wa Jimbo la Kibamba kupata huduma za kawaida zinazotolewa na vituo vya afya na hospitali za wilaya. Hivyo, ni vyema Wizara ikafanyia kazi mchango huu na kunipatia majibu yanayostahili.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. JOHN J. MNYIKA: Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ina wajibu mkubwa wa kujenga Taifa linalohabarishwa, lililoshamiri kiutamaduni, lenye kazi bora za sanaa na lenye umahiri wa michezo. Hata hivyo, wajibu huu haujaweza kutekelezwa mpaka sasa na bajeti ya mwaka 2017/2018 haielekei kujenga msingi mzuri wa kuwezesha azma hiyo kutekelezwa ifikapo 2025.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa maendeleo ya Sekta ya Habari, Taifa linarudi nyuma kwenye kuwezesha uhuru na haki kwa mujibu wa ibara ya 18 na 30 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na ibara ya 19 ya mkataba wa kimataifa wa haki za kiraia na kisiasa wa mwaka 1966 ambao Serikali imeridhia. Hivyo, Serikali ifanye marekebisho ya Sheria zote zilizotungwa katika Bunge la Kumi na Bunge la Kumi na Moja zenye kukwaza uhuru na haki wa/ya habari. Aidha, Waziri katika majumuisho aeleze hatua ambazo Serikali imechukua kwa viongozi na watendaji wa Serikali walioingilia uhuru wa habari ikiwemo juu ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa kuvamia Clouds Media akiwa na watu wenye silaha.

Maendeleo ya utamaduni wa nchi yetu yanategemea sana ukuaji wa lugha ya Kiswahili na matumizi yake. Katika majumuisho Wizara ieleze Serikali imefikia hatua gani katika kuwezesha lugha ya Kiswahili kutumika katika ngazi zote za mahakama nchini. Aidha, Serikali inapoleta Miswada ya Sheria Bungeni inaleta Miswada hiyo kwa lugha za Kiingereza na Kiswahili ambayo inafanya kisheria lugha rasmi ya sheria hizo kuwa Kiingereza, Wizara ishawishi katika Baraza la Mawaziri na ngazi zote za Serikali ili Miswada yote iletwe ikiwa katika lugha ya Kiswahili pekee.

Mheshimiwa Spika, aidha, katika aya ya 45 ya Hotuba ya Waziri ukurasa wa 25 imetajwa Kamusi kuu mpya ya Kiswahili. Ni vyema Wabunge tukapatiwa nakala ya kamusi husika.

Mheshimiwa Spika, mkakati wa TFF kuandaa vituo vya ufundi vitakavyokuwa na vifaa stahiki kila mkoa kwa madhumuni ya kulea vipaji ni muhimu katika kuchangia maendeleo ya michezo. Hata hivyo, kwa Mkoa wa kiserikali wa Dar es Salaam idadi ya vijana wenye vipaji ni kubwa kwa mkakati kuweza kutekelezwa kwenye ngazi ya mkoa. Hivyo ni vyema mkakati huo ukatekelezwa kwenye ngazi ya Wilaya na nawasilisha rasmi ombi kwa TFF kwa kituo kuwekwa katika wilaya mpya ya Ubungo katika Jimbo la Kibamba.

Mheshimiwa Spika, aidha, kwa upande wa maendeleo ya soka la wanawake, TFF itoe majibu kwa Wizara ni kwa kiwango gani imeifaidia timu ya Mburahati Queens ambayo inatoa wachezaji wengi kwenye timu ya Taifa ya wanawake kama ilivyoahidi kwa nyakati mbalimbali.
TAARIFA YA KAMATI YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE KUHUSU SHAURI LA KUDHARAU NA KUDHALILISHA BUNGE LINALOMKABILI MHE. GODBLESS JONATHAN LEMA (MB)
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Wakati Mwenyekiti wa Kamati anawasilisha taarifa na mapendekezo kwa Bunge pamoja na mambo mengine amesema uamuzi huu unalenga kulinda heshima ya Bunge dhidi ya kudhalilishwa, kuzarauliwa na mambo kama hayo.

Mheshimiwa Spika, heshima ya Bunge lolote haiwezi kulindwa kwa kuwafukuza, kuwaadhibu, kuwadhalilisha na kuwahukumu Wabunge wake. Heshima ya Bunge lolote inalindwa kwa Bunge kutumia vizuri madaraka yake na kwetu yamewekwa kwenye Katiba, Ibara ya 63(2) mamlaka ya kuishauri na kuisimamia Serikali, kuwawakilisha na kuwatumikia wananchi, Bunge linalofanya kazi hiyo vizuri ndiyo Bunge lenye heshima kwa wananchi na siyo Bunge la adhabu, siyo Bunge la kudhalilisha. (Makofi)

SPIKA: Nadhani nilisahau kusema muda, kwa kawaida huwa tunatumia dakika tano, tano lakini kwa hili nitawapeni dakika kumi, kumi.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Katika mazingira kama hayo, mapendekezo ya adhabu zilizotolewa na taarifa yote ya Kamati yasikubaliwe na Bunge hili tukufu ili Bunge liachane na haya ambayo kimsingi badala ya kulinda heshima ya Bunge yanazidi kuendelea kudhalilisha heshima ya Bunge, Bunge lijielekeze kwenye kazi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuko kwenye Bunge la bajeti hakuna….

SPIKA: Unajua unaongea na mimi, sasa ukipandisha sana unakuwa unanifokea, ongea taratibu.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, naongea taratibu na kukuomba kwamba Kanuni 5 ambayo umeapa kuilinda ya Kanuni za Bunge inakutaka wewe Mheshimiwa Spika unapoliongoza Bunge uhakikishe Bunge linazingatia Katiba, Sheria na Kanuni. Kanuni ya 5(3) inakutaka wewe Mheshimiwa Spika pale ambapo ukiona Mbunge amekiuka utaratibu umtake huyo Mbunge anayekiuka utaratibu ajirekebishe. Vilevile Kanuni ya 8(a) inakutaka uendeshe Bunge hili bila chuki wala upendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nini kilitokea? Ndiyo maana nasema, mapendekezo yote ya Kamati yanapaswa kutupiliwa mbali na Bunge.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa kumbukumbu za Bunge (Hansard) kwa sababu ya muda sitarejea pale ambapo Mheshimiwa Lema alinukuu taarifa ya Kamati juu ya maneno ambayo Mheshimiwa Mdee aliyasema kuunga mkono kauli ya CAG. Ila nitanukuu kauli aliyosema Mheshimiwa Lema.

Mheshimiwa Spika, baada ya kunukuu maelezo yote hayo, Mheshimiwa Lema akasema, mimi ni Mbunge wa Vipindi viwili, nathibitisha Bunge hili ni dhaifu. Mara baada ya Mheshimiwa Lema kunukuu maneno hayo, Mheshimiwa Naibu Spika, kinyume na kanuni ya 5 (1) ya Bunge, kinyume na kanuni ya 5 (2) ya Bunge, kinyume na kanuni ya 8 (a) ya Bunge akasimama akasema, Mheshimiwa Lema kwa maneno hayo uliyoyasema, nawe unapelekwa kwenye Kamati ya Maadili na ukae na hakuna mchango kwa sababu tunajadili adhabu kuhusu maneno hayo hayo na wewe unasema unayathibitisha. Haya maneno muhimu sana “unayathibitisha.” Nawe utaelekea kwenye Kamati ili ukathibitishe. Nasisitiza “ukathibitishe” vizuri kule.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa sababu Mheshimiwa Naibu Spika alisema ukathibitishe kule; kwa kanuni zetu za Bunge, Mheshimiwa Naibu Spika alipokuwa hapa mezani alipaswa kuongozwa na kanuni ya 63 ya Kanuni za Bunge. Kanuni ya 63 ya Kanuni za Bunge inasema; maana yake hili jambo mlitofautishe kati ya kauli inayotolewa nje ya Bunge na kauli inayotolewa ndani ya Bunge. Kauli zinazotolewa ndani ya Bunge zina kinga ya Kibunge ya Ibara ya 100 ya Katiba, zina kinga ya Kibunge ya Kanuni za Bunge, zina kinga ya Kibunge ya Sheria ya Kinga, Haki na Madaraka ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukikubali leo Bunge likapitisha azimio la kumwadhibu Mbunge kwa kauli aliyosema Bungeni kwa kumpeleka Kamati ya Maadili bila utaratibu wa kikanuni, mkipitisha utaratibu huu maana yake mmetengeneza mazingira ya Bunge hili la Bajeti linaloanza leo kwa Hotuba ya Waziri Mkuu Wabunge kuminywa mamlaka na haki yao ya kikatiba ya kuishauri na kuisimamia Serikali, ambalo ndiyo lingelinda heshima ya Bunge.

Mheshimiwa Spika, sasa utaratibu ambao ulipaswa kufuatwa ni upi? Ibara ya 61, 63 (1)(a) inaweka makatazo kwa Mbunge, baada ya hapo, inaeleza nini ambacho Mbunge mwingine angefanya. Siyo Mbunge mwingine angefanya, ndiyo kusema kwamba hicho ulichosema siyo sahihi au ni uongo. Ibara ya 63 (5) inasema: “bila kuathiri masharti ya fasiri zilizotangulia za kanuni hii, Spika au Mbunge mwingine yeyote, baada ya kutoa maelezo mafupi ya ushahidi unaotilia mashaka ya dhahiri kuhusu ukweli wa kauli au usemi au maelezo juu ya jambo au suala ambalo Mbunge amelisema Bungeni, anaweza kumdai Mbunge huyo atoe uthibitisho wa ukweli au kauli au usemi au maelezo yake na kama atashindwa kufanya hivyo, afute kauli au usemi wake.

MBUNGE FULANI: Taarifa Mheshimiwa Spika.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Naibu Spika hakufanya hayo, badala yake…

MBUNGE FULANI: Taarifa.

SPIKA: Nawaombeni leo wala kusiwe na taarifa. Tuwaache waseme, watumie dakika zao 10, na wengine nao watasema, watatumia dakika zao 10. Leo sitaki fujo, anayeleta fujo leo, hamna cha taarifa wala nini. Endelea bwana, dakika zako 10.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kama utaratibu huo ungefuatwa, maana yake ama Mheshimiwa Lema angetakiwa afute kauli, au angetakiwa athibitishe hapa Bungeni. Kama angeshindwa kuthibitisha, utaratibu wa adhabu ambao ungefuatwa uko kwenye kanuni ya 63 (9) ambapo adhabu pekee zilizotajwa kama ni kosa la kwanza, vikao visivyozidi 10 kama ni kosa la pili, vikao visivyozidi 25 na kadhalika. Adhabu zimetajwa hapa.

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa adhabu ungekuwa tofauti na ilivyopendekezwa na Kamati, asingesimamishwa mikutano mitatu kwa mapendekezo mnayotoa ambayo ni kinyume kabisa na utaratibu, isingekuwa namna hii na utaratibu usingekuwa hivi.

Mheshimiwa Spika, sasa nasimama kusisitiza hili na nayasema haya na naomba taarifa ya Kamati isikubaliwe. Kwa sababu kama taarifa ya Kamati ikikubaliwa; Mheshimiwa Lema alikata rufaa baada ya uamuzi wa Naibu Spika kabla Kamati ya Kinga, Haki na Madaraka ya Bunge haijakaa. Alitumia haki ya kikanuni, kanuni ya 5 (4) akapeleka taarifa ya rufaa kwa Katibu, kama kanuni inavyosema, akaeleza nimesema hoja moja tu ya kasoro za jambo zima kama nitakuwa na muda nitakwenda kwenye nyingine, alikuwa na hoja tatu; akakata rufaa kabla. Akaenda mbele ya Kamati ya Kinga, Haki na Madaraka ya Bunge akaiambia Kamati, nimekata rufaa ipo kwa Katibu, nakala ya rufaa hii hapa. Kamati ikasema hatujapokea rufaa, hatuko tayari kuipokea kutoka kwako, sisi tunaendelea mbele. Kimsingi Kamati ilikuwa imesha-shape uamuzi.

Mheshimiwa Spika, kwa misingi ya haki, kwa kauli zako za jana tayari ulishatoa hukumu kabla ya Kamati kufanya kazi. Huu mchakato mzima ukiendelea, ni mchakato ambao ni batili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama uamuzi ukishafanywa na Bunge, hakuna mahali popote pengine pa kukata rufaa isipokuwa Mahakamani na Mahakama inaminywa kwa Sheria ya Kinga Haki na Bunge kushughulikia mambo ambayo yameamuliwa na Bunge. Sasa kama tukipitisha huu uamuzi leo, maana yake tuna-pre-empty Kamati ya Kanuni. Tuahirishe hii taarifa isijadiliwe kabisa, Kamati ya Kanuni ikakae kwanza kabla ya uamuzi wa Bunge ili taratibu za kikanuni zifuatwe.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda, nijielekeze kwenye eneo lingine haraka haraka. Amehukumiwa kwa kosa la kudharau Bunge wakati siyo kosa lake. Kwa kosa hilo, Ibara ya 33 kifungu cha 33 (1) cha Sheria ya Kinga, Haki na Madaraka ya Bunge kinasema: “Where any member commits any contempt of the Assembly whether specified in section 26 or otherwise, the Assembly may, by resolution, either direct Speaker to reprimand…” ungeweza wewe mwenyewe Spika kuamua kumwonya, kungeweza kuwa na adhabu ya onyo, lakini naendelea mbele. Kwa hiyo, kama Spika ukiamua kuondoa misingi yoyote ya mazingira ya kuonea au nini, unaweza kumpa onyo tu.

Mheshimiwa Spika, sentensi inaendelea, kama ukiamua kutoa suspension: suspend him from service of the Assembly for such period as it may determine. Sheria inaendea mbele inasema, sikilizeni: “provided that, such period shall not extend beyond the last day of the session next following that which the resolution was passed or of the session in which the resolution is passed as the Assembly may so detrmine.”

Mheshimiwa Spika, sheria imeweka ukomo wa kiwango cha adhabu kinachoweza kutolewa. Ninyi taarifa yenu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika ninyi taarifa yenu ya Kamati imekiuka sheria, imekiuka Katiba, imekiuka mambo yote ya msingi isikubalike.

SPIKA: Mheshimiwa Mnyika ahsante sana.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Kwa sababu mko wengi na mmeshaamua, kama mnataka kuamua, ninyi muamue kwenye Mahakama ambayo ninyi wenyewe ndio walalamikaji, ninyi wenyewe ndio watoa hukumu na kila kitu Mheshimiwa Spika na hatimaye mtaendelea kulidhalilisha Bunge kwa haya mnayoyafanya.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kama muda wangu umeisha. Kama bado, niendelee.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda nianze na hili suala la nyongeza ya fedha kwenye Bajeti ya Wizara ya Maji. Tunaweza tukakimbilia kufanya maamuzi, maamuzi ambayo yakawa na athari ya ongezeko la gharama za maisha kwa wananchi, kwa hiyo, badala ya kupunguza tatizo tukaongeza tatizo. Tatizo letu la msingi ambalo naliona katika Serikali hii inayoongozwa na Chama Cha Mapinduzi ni vipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi kama Serikali inaamua kununua ndege (Dreamliner) kwa quotation ya watu wa Boeing wanasema dola milioni 224 ambayo ni takribani shilingi bilioni 400 Serikali haitaki kusema walichokubaliana hasa ni kiasi gani wanasema ni pungufu ya shilingi bilioni 400. Kama tunaweza tukatoa pesa kununua ndege shilingi bilioni 400 hivi ni nini kinatushinda kutoa shilingi bilioni 400 kuongeza kwenye bajeti ya Wizara ya Maji? Kwa hiyo, ndiyo maana nimeanza kwa kusema kwamba, tatizo letu kubwa ni kipaumbele. Serikali ya CCM kwa awamu zote pamoja na kuwa inatamka kuwa maji ni kupaumbele number one katika nchi hii, lakini kwenye bajeti kwa nyakati mbalimbali maji hayajawahi kufanywa kipaumbele number one katika nchi hii.

Katika mazingira ya namna hii ya Serikali ya CCM kupuuza kero ya msingi ya wananchi, mimi kwa maoni yangu kwa muda ambao nimekaa Bungeni nianze na hili la kwanza, ufumbuzi hauwezi kupatikana katika huu mjadala tulioanza jana unaohitimishwa kesho. Ufumbuzi kwa maoni yangu unapatikana kwa Watanzania kutambua kwamba kwa miaka mingi wamedanganywa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi ufumbuzi ni kuindoa Serikali ya CCM madarakani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeyasema haya bila kusubiri Mheshimiwa Waziri atakapohitimisha hotuba kesho. Kwa sababu Mheshimiwa Waziri Mkuu amekwishazungumza leo na Mheshimiwa Waziri Mkuu ndiyo Kiongozi wa Serikali. Mheshimiwa Waziri Mkuu alipojibu maswali, swali mojawapo liliulizwa asubuhi leo kuhusu maji, nilitarajia Mheshimiwa Waziri Mkuu kuelezwa namna ambavyo hii bajeti ya maji imepungua, yaani mwaka jana bajeti ya maendeleo ilikuwa bilioni 915, leo bajeti ya maendeleo ni shilingi bilioni 623 yaani tumepunguza bajeti kwa shilingi bilioni 292; nilitarajia Mheshimiwa Waziri Mkuu kama Kiongozi wa shughuli za Serikali aliposimama hapa kujibu swali Bungeni angesema; kwa kweli nimesikia kilio cha Wabunge kuanzia jana na nimesikia vilevile swali nililoulizwa leo na naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba tutakaa tena katika Serikali, tutaongeza bajeti ya Wizara ya maji badala yake Mheshimiwa Waziri Mkuu ameshatoa kauli hapa Bungeni leo kwamba Wabunge tuipitishe bajeti kama ilivyo. Kwa maneno mengine mheshimiwa Waziri huyu wa Maji hatarajiwi kuja na jipya lolote kama Mheshimiwa Waziri Mkuu ameshatoa mwelekeo wa Serikali tayari.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mazingira ya namna hii Serikali hii ni vyema ikakiri tu kwamba imekwishashindwa kwenye suala la maji. Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2005 aya ya 67 iliahidi kwamba ikifika mwaka 2010 asilimia 65 ya wananchi vijijini watakuwa na maji na asilimia 90 ya wananchi watakuwa na maji mijini.

Mheshimiwa Nasibu Spika, kwa maneno mengine, wale wananchi wenzangu walionituma Bungeni wa Kata ya Kibamba, iwe ni Kiluvya na maeneo mengine ya pembezoni Kibwegere na kadhalika kule Kwembe kule iwe ni Kisopwa, iwe ni Kwembe Kati katiza mpaka Kata ya Msigani, Malambamawili, nenda Mbezi kule maeneo ya pembeni, Mpiji Magohe, Goba sijui Kinzudi, Matosa maeneo yote haya ya Saranga, King’ong’o, Mavurunza yaani kwa ahadi hii ya Serikali; Serikali ya CCM iliahidi mwaka 2010 asilimia 90 wangepata maji, mwaka 2010 ikafika hawakupata maji, Serikali ikaahidi tena kwenye ilani nyingine ya CCM ya mwaka 2010/2015 kwamba ikifika mwaka 2015 asilimia 90 watapata maji, asilimia 65 watapata maji, ahadi nyingine ya uongo miaka 10 ikapita ikafika 2015, Serikali ikarudia tena ahadi ile ile ya kuahidi tena mwaka 2020 ndiyo matatizo haya yatatauliwa na Mheshimiwa Waziri ulijibu uongo Bungeni naomba tu utakapohitimisha ujibu ukweli.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilipouliza swali Bunge hili, ukasema kwamba kwa sasa na hata katika kitabu chako umeonyesha tena kwamba kiwango cha maji kimeongezeka kutoka mita 300 mpaka 504 milioni na kwamba sasa kero kwa maneno yako mwenyewe umetumia maneno; “huduma ya maji imeimarika.” Wakati unanijibu swali Bungeni ulisema kuanzia sasa kilomita 12 huku, kilomita 12 huku kwenye barabara ya Morogoro, maeneo yote haya sasa yenye mabomba ya Mchina maji yatakuwa yanatoka. Ukaniahidi hapa Bungeni Mkutano huu huu ukasema maji yameshasukumwa tatizo ilikuwa ni umeme tu, maji yamesukumwa mpaka tanki pale Kibamba na sasa maji yatatoka, lakini Mheshimiwa Waziri ulisema maelezo ya uongo Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana nasema, kwa haya majibu ya Serikali ambayo kimsingi Waheshimiwa Wabunge na hapa nitaomba nafasi kwa mujibu wa Kanuni ya 69(1) kabla ya kuingia kwenye hatua ya Kamati, kama Mheshimiwa Waziri hatatumia Kanuni ya 58(5) kuindoa hii hoja ili Serikali ilete commitment ya kurudisha zile shilingi bilioni 300 zilizoondolewa, kama Mheshimiwa Waziri hatatoa commitment hapa, Wizara ya Fedha haitasema ni kwa nini mpaka sasa imetoa asilimia 19.8 na wakati mpaka sasa ilipaswa pesa zitoke asilimia 75, kama hakutakuwa na commitment ni afadhali mjadala huu tuuahirishe kimsingi ili Serikali ikajipange upya ili bajeti hii ya maji iweze kuletwa ikiwa ina marekebisho ya msingi pesa za maji ziweze kutolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa kuwa Serikali hii ni muendelezo tu wa kusema uongo Bungeni, ni muendelezo wa kutotekeleza ahadi, kama hamtayafanya haya ni wakati wa Watanzania kote nchini wenye kero kubwa ya maji, kero number one kujipanga kuindoa CCM madarakani.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninatambua kwamba mnaogopa haya yasiende kusemwa kwenye majimbo yenu ndiyo maana mnazuia mikutano ya vyama vya siasa. Lakini nawaambia mtatuzuia humu Bungeni, mtatuzuia majimboni, mtatuzuia maeneo mbalimbali lakini Watanzania wanauelewa ukweli wa kudanganywa na Ilani za CCM za toka miaka niliyoitaja. Bila kero ya msingi ya maji kuondolewa watachukua hatua mwaka 2019/2020.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika aya ya 33, ukurasa wa 15 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge amezungumzia kuhusu marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Siasa na utekelezaji wake ambao umeanza. Hata hivyo, Ofisi ya Waziri Mkuu haijazungumzia hatua iliyofikiwa katika kuandaa kanuni kufuatia marekebisho hayo ya sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili ni nyeti na tete, kwa kuwa wakati Muswada wa marekebisho ya sheria hiyo ulipotoka, Msajili wa Vyama vya Siasa aliwasilisha pia rasimu ya kanuni kabla hata ya sheria kutungwa. Baada ya kubaini kasoro hiyo, rasimu hiyo ilichukuliwa na Msajili. Hata hivyo, rasimu ya Kanuni hiyo ilionesha kwamba masharti mengi yaliyo kinyume na Katiba ya Nchi na ziada ya mambo yaliyokuwa katika Muswada na sheria yanakusudiwa kupenyezwa kupitia kanuni. Katika muktadha huo Waziri mwenye dhamana pamoja na Ofisi ya Msajili hawapaswi kujifungia na kuandaa rasimu, bali mchakato mzima wa marekebisho ya kanuni zinazohusu Sheria ya Vyama vya Siasa unapaswa kuwa shirikishi na vyama vya siasa viitwe kwa ajili ya majadiliano kuhusu suala hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika aya ya 36, ukurasa wa 17, Serikali imeeleza kuwa imekamilisha maandalizi ya Kanuni za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Hii ni katika hotuba ya tarehe 4 Aprili, 2019 wakati ambapo tarehe 1 na 2 Aprili, 2019 nimeshiriki mkutano baina ya Wizara ya TAMISEMI na Vyama vya Siasa ambapo wadau tulitoa maoni ya marekebisho kwenye vifungu na vipengele vingi vya rasimu ya kanuni zilizowasilishwa. Aidha, tarehe 3 Aprili, 2019 Wizara ya TAMISEMI, ilikutana na Asasi za Kiraia na wadau wengine kwa ajili ya kupokea maoni yao katika kikao ambacho kiliisha jioni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mazingira hayo inawezekanaje tarehe 4 Aprili, 2019 isemwe Bungeni kuwa maandalizi ya kanuni za uchaguzi huo yamekamilika? Hotuba hii ya Waziri Mkuu sio ushahidi wa kwamba vikao vya wadau vimeitwa kwa kujikosha wakati ambapo tayari Serikali imeshafanya maandalizi ya kanuni za uchaguzi huo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali hii inajitokeza pia katika aya ya 37 ambapo Waziri Mkuu ameeleza kuwa kanuni za uboreshaji wa daftari la kudumu la wapigakura zimeandaliwa na kutangazwa kwenye gazeti la Serikali Na. 792 na 793 ya tarehe 28 Desemba, 2018. Kanuni hizo ziliandaliwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) na kutangazwa bila kwanza wadau kupewa rasimu na kutoa maoni. Mwezi Machi, 2019 ndipo NEC ilikutana na vyama kupata maoni wakati tayari kanuni zilishatangazwa. Waziri Mkuu awasiliane na NEC kutoa majibu Bungeni ni lini marekebisho ya kanuni hizo yatafanyika kabla zoezi la uboreshaji haujafanyika nchi nzima. Aidha, naomba kupewa nakala ya Kanuni iliyotangazwa 28 Disemba, 2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Aya ya 92, ukurasa wa 44 wa hotuba ya Waziri Mkuu, Serikali imezungumzia kuhusu kuondoa msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam. Naunga mkono upanuzi wa barabara ya Kimara Mwisho – Kiluvya kilometa 19.2 kutoka njia mbili kuwa nane na ni vyema kiwango cha fedha katika bajeti kikaongezwa na kutolewa kwa wakati ili ujenzi ukamilike mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, pamoja na ujenzi huo kuendelea, bado nasisitiza haja ya Serikali kuwalipa fidia wananchi waliobomolewa kupisha ujenzi wa barabara hiyo. Ombi hili la wananchi niliwasilisha mbele ya Rais tarehe 19, Desemba, 2018, wakati wa uzinduzi wa ujenzi wa barabara hiyo. Rais alikataa ombi hilo kwa maelezo kwamba kesi ilishaamuliwa na Mahakama Kuu. Naomba Waziri Mkuu na Mawaziri wengine wenye dhamana wamkumbushe Rais kuwa kesi anayoirejea wananchi waliohusika ni wa Kimara pekee waliofungua kesi haikuhusu eneo lote linalohusika na ujenzi hivi sasa na haihusu substantive grounds bali wananchi walishindwa kwa technicalities.

Mheshimiwa Spika, baadaye wananchi wa Mbezi walifungua kesi nyingine mwaka 2005 kupitia shauri Na. 80 katika Mahakama Kuu, Kitengo cha Ardhi na hukumu ilitolewa tarehe 31 Mei, 2013 ambapo wananchi walishinda. Pamoja na mambo mengine, mahakama ilitamka kuwa the Highway Ordinance Cap 167, Government Notice No. 161 ya tarehe 5 Mei, 1967 ambayo hutumiwa na TANROADS kutwaa ardhi za wananchi bila fidia ni batili kwa kutofautiana na vifungu vya 15 na 16 vya Sheria ya Ardhi ya Vijiji Na. 5 ya 1999.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Rais alisema kuwa upana wa barabara wa toka mwaka 1932 uliingizwa kwenye Sheria ya Barabara mwaka 2007. Hata hivyo, ukipitia Sheria ya Barabara ya mwaka 2007 haina kifungu kinachotaja upana wa Barabara ya Morogoro. Upana unaolalamikiwa sasa uko kwenye Kanuni ya Barabara za mwaka 2009 ambazo zinakinzana na Sheria ya Vijiji Na. 5 ya mwaka 1999 na sheria nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia hayo, naomba Rais abadili uamuzi na kuwezesha wananchi hao kulipwa fidia. Kama Serikali haiwezi kulipa fidia kamili basi ifuate misingi ya haki na kuwalipa wananchi hao ex gratia kwa kuzingatia kuwa Serikali yenyewe ndiyo iliyoweka wananchi katika maeneo hayo toka wakati wa operesheni ya vijiji ambapo sasa imewaondoa bila ya kuwalipa fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande mwingine naamini Serikali imeona faida ya barabara za mlisho/ mizunguko/pete katika kupunguza foleni kupitia Barabara ya Mbezi – Goba, Temboni – Msingwa – Msigani – Malamba Mawili mpaka Kinyerezi. Kwa umuhimu huohuo, naomba Serikali itenge fedha kwa barabara za Mbezi – Mpiji Magohe, Kibamba – kibwegere, Malamba Mawili – Kwembe na zingine zilizoko kwenye mpango wa barabara za mlisho (feeder), mzunguko (ring) ambazo zitaisadia barabara ya Morogoro inayojengwa zikiunganisha Wilaya ya Ubungo na Wilaya za Kinondoni na Ilala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika aya ya 115 ya hotuba ya Waziri, ukurasa wa 55 ameeleza kwamba hadi Februari, 2019 upatikanaji wa maji safi na salama katika Jiji la Dar es Salaam na maeneo mengine yanayohudumiwa na DAWASA imefikia asilimia 85. Kiwango cha asilimia 85 hakina ukweli ukilinganisha na hali halisi ya matatizo ya maji ilivyo. Hivyo, katika majumuisho Mheshimiwa Waziri Mkuu aeleze ni vigezo gani vimetumika kupata takwimu hizo kwa kulinganisha baina ya idadi ya kaya na watu katika Jiji la Dar es Salaam na hali halisi ya upatikanaji wa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano wa Jimbo la Kibamba lenye kata sita ili Ofisi ya Waziri Mkuu ishirikiane na Wizara ya Maji na DAWASA kutoa majibu ya takwimu halisi na kuchukua hatua za kuongeza kwa haraka kiwango cha upatikanaji wa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mosi, katika Kata ya Goba, Mitaa ya Matosa Goba, Tegeta A na Kulangwa, maji hayatoki na uwekaji wa mabomba ya maji unakwenda kwa kusuasua. Hata katika maeneo ambayo wananchi walijitolea kuchimba mitaro na mabomba kuwepo, lakini maji hayatoki. Kwa hali hiyo upatikanaji wa maji Kata ya Goba hauwezi kuwa umefikia asilimia 85.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, Kata ya Msigani, Mitaa ya Malamba Mawili, Kwa Yusufu na mitaa mingine mambomba ya maji hayatoi maji kwa kuwa hayajaunganishwa na bomba lenye maji kwa madai kuwa hakuna vifaa. Mradi uko chini ya kampuni ya India ambayo nayo imeipa kazi kampuni ya kutoka China. Kampuni hizi mbili zinatupiana mpira kuhusu ukamilishaji wa kazi. Aidha, baadhi ya vifaa vinasubiriwa mpaka vitoke India, hali inayofanya mashimo yaliyochimba kuweka mabomba mengine kuanza kujaa mchanga/ udongo. Hivyo, kata hii nayo haijafikiwa kwa asilimia 85.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, Kata ya Mbezi Luis, Mtaa wa Makabe, mabomba ya inchi nane yamechimbwa ardhini toka 2017, lakini maji hayatoki na kuwa mtandao na mabomba kwenda barabara za ndani kwenda kuwafikiwa wananchi. Pia kuna ujenzi wa tanki ambao umesimama kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Mtaa wa Msakuzi hakuna mtandao wa mabomba. Mtaa wa Luis wameunganishwa walioko kwenye mita 50 kwa mkopo lakini maji hayatoki katika bomba kubwa. Pia maeneo manne katika mtaa huo hayajaunganishwa na Bomba Kuu. Kata hiyo nayo maji hayatoki kwa asilimia 85.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, Kata ya Kwembe, Mtaa wa King’azi B wanamaliza kufunga vizimba lakini maji hayatoki hata kwa walio pembezoni ya bomba. Hali iko hivyo maeneo mengi ya Mtaa wa Mji Mpya. Hivyo, kata hii nayo haina maji kwa asilimia 85.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tano, Kata ya Kibamba Mitaa ya Hondogo, Kibwegere na mingine hakuna maji. Kibwegere waliahidiwa toka 2016 kupelekewa bomba la inchi nane mpaka Daraja la Mpiji Magohe toka 2016 lakini kazi hiyo haijafanyika. Hivyo, napo haiwezi kuwa asilimia 85.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sita, Kata ya Saranga, Mtaa wa Saranga mabomba ndiyo kwanza yanatandazwa kwa kusuasua. Mtaa wa Kimara B, maji yakitoka ni mara moja kwa mwezi. Kwa ufupi kwa wastani huo haiwezekani Jimbo la Kibamba kama sehemu ya Dar es Salaam kuwa imefikiwa kwa asilimia 85. Hatua gani zitachukuliwa ili kufikia lengo hilo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Waziri Mkuu pia inapaswa kumshauri Rais kuweka kipaumbele maalum kwenye maendeleo ya vijana na kuongeza fursa za ajira kwa vijana. Tatizo la ukosefu wa ajira kwa vijana lisipodhibitiwa kwa haraka litaleta madhara makubwa kwa nchi. Katika aya ya 138, ukurasa wa 65, programu ya kuendeleza vijana imewezesha vikundi 755 tu ambavyo vimepatiwa shilingi bilioni 4.2 pekee.

Mheshmiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2019/2020 kiwango cha fedha katika mfuko wa maendeleo ya vijana kinapaswa kuongezwa. Katika kutumia mfuko huo, naomba Ofisi ya Waziri Mkuu itoe mikopo pia kwa vikundi vya vijana katika Jimbo la Kibamba. Katika mwaka wa fedha 2019/2020 Serikali inatarajia kuwezesha vijana kupata mafunzo ya ujuzi na stadi za kazi kwa vijana 46,950. Mpango huo wa mafunzo utekelezwe. Pia katika Jimbo la Kibamba na Ofisi ya Mbunge na Manispaa ya Ubungo tuko tayari kutoa ushirikiano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ya fursa za ajira, kiwango cha kutengeneza fursa hizo hakilingani na kiwango cha nguvu kazi ya vijana kinachoingia kwenye soko la ajira kwa mwaka. Aidha, kitendo cha jumla ya ajira 221,807 kuwa zimezalishwa kufikia Februari, 2019 huku ajira kwa sekta binafsi zikiwa 75,393, sawa na asilimia 34, kinadhihirisha kwamba programu ya kutengeneza ajira siyo endelevu. Mkakati endelevu wa kuibua fursa za ajira kwa vijana hauwezi kutegemea zaidi utekelezaji wa miradi ya Umma bali kutoa fursa kwa sekta binafsi hutengeneza ajira kwa wingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, katika hotuba yote ya Mheshimiwa Waziri Mkuu hakuna mahali ambapo amezungumzia kuhusu Baraza la Vijana la Taifa kama nyenzo ya kuwaunganisha vijana kuanzia ngazi ya chini mpaka ya Taifa katika masuala ya maendeleo ya vijana. Sheria ya Baraza la Vijana ilipitishwa mwaka 2015, lakini mpaka sasa miaka mitatu imepita bila baraza kuundwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali kisingizio kilikuwa kutokamilika kwa kanuni jambo ambalo haliwezi kuwa sababu tena kwa kuwa kanuni zilishachapishwa kwenye gazeti la Serikali. Hivyo, katika majumuisho Serikali ieleze mchakato na ratiba ya kukamilisha uundwaji wa Baraza la Vijana katika ngazi zote zilizojatwa katika sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande mwingine, kanuni zimeweka utaratibu wa Asasi za Kiraia na Mashirika yasiyo ya Kiserikali yanayolenga vijana kuwasilisha maombi ya kufanya kazi kwa baraza. Haya ni mashirika ambayo yamepitia mchakato wa makubaliano (compliance) kwa sheria nyingine zinazotawala mashirika yasiyo ya kiserikali. Kwa uwezo mdogo wa taasisi za vijana, kutakiwa kulipa gharama za usajili/kujiandikisha kwa mamlaka zaidi ya moja ni mzigo mkubwa. Hivyo ni vyema kanuni zirekebishwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Waziri Mkuu ina wajibu, pamoja na mambo mengine wa kushughulikia masuala ya Bunge na Wabunge kwa kushirikiana na Ofisi ya Bunge. Katika masuala hayo ni pamoja na ujenzi wa Ofisi za Wabunge. Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge zitoe maelezo Bungeni ni kwanini Ofisi za Wabunge hazijengwi katika Majimbo mbalimbali ambayo hayana Ofisi za Wabunge mpaka sasa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitendo cha Wabunge kupewa Ofisi kwenye majengo ya Wakuu wa Wilaya, kimefanya Wabunge kutokuwa kwa huru juu ya matumizi ya Ofisi hizo. Pia kupewa nafasi ndogo ya chumba kimoja ya Mbunge na Watendaji wake wote na hivyo kukosekana faragha ya kuwahudumia wananchi. Aidha, wapo Wakuu wa Wilaya ambao wamewanyang’anya Wabunge Ofisi kwa maelezo kwamba zinahitajika na Watendaji wengine walio chini ya Mkuu wa Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Jimbo la Kibamba, lipo katika Wilaya mpya ya Ubungo ambapo kumekuwa na mchakato wa kutenga viwanja/maeneo kwa ajili ya Makao Makuu ya Halmashauri na Mkuu wa Wilaya. Baadhi ya viwanja hivyo vimepatikana kutoka ardhi iliyokuwa chini ya National Housing Corporation (NHC).

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka kadhaa, nimeiomba Ofisi ya Waziri Mkuu iratibu mambo nyingine kuwezesha kiwanja/eneo kwa ajili ya ujenzi wa Ofisi ya Mbunge. Hata hivyo, mpaka sasa sijapatiwa majibu stahili. Hivyo katika majumuisho, Ofisi ya Waziri Mkuu inipe majibu, ni eneo gani hasa limetengwa kwa ajili ya ujenzi wa Ofisi ya Mbunge? Hata kama hakuna fedha za ujenzi kwa sasa, kiwanja kipatikane wakati huu kabla ardhi iliyo wazi haijaendelezwa kwa matumizi mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kutaka pia uratibu ufanyike kuwezesha kutengwa kwa eneo kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama jirani na panapojengwa Makao Makuu mapya ya Wilaya ya Ubungo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Leo asubuhi tulipoingia hapa, tulianza na dua, kwa hiyo tulianza na Mungu kwanza, sio kilimo kwanza au elimu kwanza, tulianza na Mungu kwanza na tulisali; “Ewe Mwenyezi Mungu Mtukufu, muumba mbingu na Dunia, umeweka katika Dunia Serikali za wanadamu na Mabunge ya Mataifa ili haki yako itendeke. Twakuomba ibariki nchi yetu idumishe uhuru, umoja, haki na amani. Umjaalie Rais wetu hekima, afya njema na maisha marefu ili pamoja na wanaomshauri wadumishe utawala bora.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaomba mchango wangu wa leo kwa kweli uongozwe na hii sala ambayo tumeisali leo. Kwa sababu tunachangia Ofisi ya Rais nitaomba bila kuvunja kanuni ya kujadili mwenendo wa Rais, nitaomba niguse maswali mbalimbali kuhusiana na Ofisi ya Rais, lakini ambalo naliomba sana Ofisi ya Rais, Utawala Bora na TAMISEMI, walitoleee kauli, hivi ilikuwa ni halali kwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora kusema kwamba anakwenda kufanya nini Mheshimiwa Selasini?

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Kumwomba Mungu amshukuru Rais.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, yaani anamwomba Mungu amshukuru Rais, hii ni kufuru!

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mnyika, ongea na kiti.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongee na kiti kwamba Ofisi ya Rais, Utawala Bora na Ofisi ya Rais, TAMISEMI ituambie hivi ni halali kwa Wakuu wa Mikoa na viongozi wa Kiserikali kukufuru na kufanya dhihaka dhidi ya Mwenyezi Mungu? Wengine utasikia wanajiita Mungu wa Dar es Salaam na mambo mbalimbali. Serikali itoe kauli juu ya jambo hii ndani ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imeelezwa hapa kwamba Mheshimiwa Rais atakuja kesho kuzindua Makao Makuu, ujenzi wa Mji wa Serikali. Ningeomba sana sana Ofisi ya Rais imshauri Rais kama ambavyo anapata wasaa wa kuzunguka kuzindua majengo pengine kupatikane wasaa wa siku moja wa Taifa letu na siku ya sala A National day of prayer tuiombee nchi yetu. Pengine tutaponya majeraha ya Kibiti, majeraha ya watu kupigwa risasi kama Mheshimiwa Tundu Lissu, majeraha ya miili kuokotwa Coco beach na mambo mengine ambayo kwa kweli, Mheshimiwa Selasini anasema kipindi cha Kwaresma yatatusaidia kutuweka pamoja kama Taifa, kwani Taifa linalokwenda pamoja ni Taifa linaloweza kwenda kwa kasi zaidi kuliko kasi tuliyonayo ya maendeleo ya nchi yetu kwa sababu kasi yetu tunapewa takwimu za uongo Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaambiwa kwamba uchumi wa nchi utakua kwa asilimia saba huku Shirika la Fedha Duniani linatoa taarifa kwamba hiyo asilimia inayosemwa na Serikali haiwezekani sanasana tukijitahidi ni asilimia nne. Taifa la namna hii linahitaji uponyaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ningependa kulizungumza, tumeapa kulinda Katiba, naelewa wenzetu tukisema kuhusu Katiba wanasema kipaumbele cha msingi cha wananchi ni maji, umeme na miradi mingine ya maendeleo, lakini tulipoapa na Mheshimiwa Rais aliapa cha kwanza tuliapa juu ya katiba kwa sababu Katiba ndiyo nyenzo ya kusimamia mambo yote na ndiyo nyenzo ya kuleta maendeleo ya nchi. Kwa hiyo, nasema Katiba ni jambo la pili muhimu sana kwa nchi yetu na kwa sababu Katiba ni jambo la pili ningependa kuwakumbusha Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Rais alipokuja kuhutubia Bunge wakati anazindua Bunge aliahidi hapa Bungeni kwenye hotuba yake kwamba ataendeleza na kukamilisha mchakato wa Katiba mpya. (Makofi)

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Hebu subiri tu Mheshimiwa Mnyika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimkumbushe mzungumzaji anayeongea kwamba siku Rais amekuja hapa kutoa maelekezo yake ya nchi yeye hakuwepo Bungeni, alijuaje hayo maneno? (Makofi)

MWENYEKITI: Endelea Mheshimiwa.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Mbunge wa wapi ambaye hajui kwamba kila kinachojadiliwa Bungeni kinawekwa kwenye kumbukumbu rasmi za Bunge? Kwa hiyo analiaibisha Bunge tu. Naomba niendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Rais akiwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwenye kongamano, kinyume na kauli yake ya Bungeni, Rais amesema eti hataki mchakato wa Katiba mpya kuendelea kwa sababu kuna watu wanataka wapewe posho ndani ya Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vyema Ofisi ya Rais ikamkumbusha Rais. Wao walikaa kwenye Bunge Maalum wakapitisha Katiba inayopendekezwa kinyume na Katiba na wananchi kwa Sheria ya Kura ya Maoni na Sheria ya Mabadliko ya Katiba, hatua inayofuata ni kura ya maoni dhidi ya hizi rasimu mbili uamuzi wa wananchi kufanyika, jambo hilo halihusu Wabunge kukaa kikao, jambo hilo halijusu Wabunge kupewa posho.

Kwa hiyo kauli ya Rais ilikuwa inataka kupotosha tu mjadala wa Katiba mpya ni muhimu katika majumuisho. Ofisi ya Rais ikasema ni kwanini katika Bunge hili hakijatengwa pesa kwa ajili ya kura ya maoni na kukamilisha mchakato wa Katiba mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusikubaliane kwa namna yoyote na kauli ya kwamba eti hakikuwa kipaumbele chenu wala kipaumbele cha Rais. Nimeisoma Ilani ya Uchaguzi ya CCM, Ilani ya Uchaguzi ya CCM imesema bayana, CCM itaendeleza na kukamilisha mchakato wa Katiba Mpya, tekelezeni Ilani yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitarudi kwenye haya mambo…

T A A R I F A

MHE. GEORGE B. SIMBACHAWENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimtaarifu mzungumzaji anayezungumza kwamba Katiba inayopendekezwa tulishiriki wote Wabunge tuliokuwepo Bunge lililopita na mchakato ule ulipofikia hatua, wenzetu wa upinzani hatukuwa nao mpaka hatua ya mwisho waliikataa. Leo hii wanakuja hapa kusema wanataka mchakato uendelee wa kupigia kura, Katiba ipi mpya inayopendekezwa wakati wao waliikataa na hawakushiriki zoezi mpaka mwisho? (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Mnyika taarifa.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Kura ya Maoni inasema Katiba inapendekezwa ikishapitishwa kwenye Bunge Maalum hatua inayofuata ni kura ya maoni bila kujali nani alikuwepo na nani hakuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuendelea. Nitaomba kupata ufafanuzi kutoka kwa Ofisi ya Rais, ripoti iliyopita ya CAG sio ya sasa, ripoti ya mwaka uliopita iliibua madudu mengi kwenye sekta mbalimbali na Wizara mbalimbali na kati ya mambo yaliyoibuliwa ni pamoja na suala la 1.5 trillion ambayo baadaye ilipanda mpaka kuwa 2.4 trillion. Katika ufafanuzi wa Serikali juu ya 1.5 trillion kuna taarifa zilitolewa toka 1.5 mpaka 2.4 kwamba bilioni 976.96 zilihamishwa kwenye Mafungu mbalimbali zikapelekwa kwa maana ya kibajeti reallocation zikapelekwa kwenye Fungu la 20 la bajeti ambalo ni sehemu ya hotuba yetu ya leo Ofisi ya Rais, Ikulu. Sasa mimi kama Mbunge naamini moja, Bunge halikupitisha uamuzi wa kufanya reallocation ya bilioni 976.96 kupeleka Fungu namba 20 Ikulu. Pili… [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mnyika, hebu nisaidie Sheria ya Bajeti kuhusiana na reallocation inasemaje? Nisaidie?

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya interests…

MWENYEKITI: Ni Bunge linafanya au mamlaka husika inafanya?

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa interest ya time nijikite zaidi kwenye hoja yangu.

MWENYEKITI: Hapana.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tukitaka kujadili hilo tuta…

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, utalinda muda wangu?

MWENYEKITI: Naulinda! Mheshimiwa Mnyika na Waheshimiwa Wabunge, tusifanye generalization ambazo huwezi kuzi-defend hapa. Sisi wote hapa tumeshiriki, baadhi yetu tumeshiriki katika utungaji wa sheria hiyo.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Shut up!

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Nawaombeni Waheshimiwa Wabunge, kiwango ambacho kimetajwa na Sheria ya Bajeti kama kuna Mbunge anataka ku-challenge hiyo, warrant ya reallocation inapowekwa na Serikali hapa wewe unapaswa sasa useme kwamba reallocation hiyo imezidi kiwango ambacho kimewekwa na Bunge, ukomo, lakini hatuwezi hapa kuja tunafanya generalization tu ili -m-get away na hiyo, hapana si kweli! Waziri wa Fedha, jamani Wizara hiyo ni makini sana. Endelea. (Makofi)

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuondoe utata kuhusu jambo hili la bilioni 976.96 kwa kuwa CAG anabanwa banwa kidogo kukagua Ikulu, Ofisi ya Rais ikija kwenye majumuisho hapa itueleze hizi bilioni 976.96 Ikulu zilitumika kwa matumizi gani? Tupewe mchanganuo wa kina…[Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kusubiri kuja kujibu kuwaachia Watanzania wanapotoshwa. Lazima watu wanaosema uongo ndani ya Bunge lako Tukufu wathibitishe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakiomba kiti chako kimwelekeze Mheshimiwa Mnyika aweze kuthibitisha kwamba CAG anabanwa banwa kukagua Fungu 20 la Ofisi ya Rais, kwa sababu kinachofahamika kila Fungu lina Resident Auditor kutoka Ofisi ya CAG including Fungu 20. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hiki kinachoelezwa kisiwapotoshe Watanzania kule nje. Naomba iwekwe wazi kwamba hakuna Fungu hata moja ambalo CAG anazuiwa kulikagua na Fungu hili lilikaguliwa na CAG hakuja na hoja hizi zinazoletwa kuwadanganya Watanzania humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kiti chako kitende haki kwenye jambo hili ili Watanzania wasiendelee kudanganywa na Mheshimiwa Rais wetu asiendelee kuchafuliwa bila sababu za msingi. (Makofi)

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini ulilinda muda wangu, lakini mimi bado naomba katika majumuisho Ofisi ya Rais ilete mchanganuo hizi pesa zimetumika kwenye kitu gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea. Hotuba hii ya…

MWENYEKITI: Una dakika mbili.

MHE. JOHN J. MNYIKA… Utumishi wa Umma inahusu maslahi ya wafanyakazi wa umma…

KUHUSU UTARATIBU

MWENYEKITI: Kanuni namba ngapi?

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kanuni ya 64(a).

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kanuni iliyovunjwa ni ya 64(a). Kanuni inasema hivi; Mbunge hatatoa ndani ya Bunge Taarifa ambazo hazina ukweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la 1.5 trillion limeendelea kuongelewa humu ndani ya Bunge tena limeongelewa kwa uongo. Kwa sababu nitahitajika kuthibitisha kuwa huo ni uongo, Ripoti ya PAC Mwenyekiti wake ambaye ni Mpinzani, Mheshimiwa mama Kaboyoka, Mbunge wa CHADEMA inasema hivi ukurasa wa 35; “Mheshimiwa Spika katika kuhitimisha suala la tofauti la 1.5 trillion kati ya mapato ya Serikali na makusanyo kwa mwaka 2016/2017, naomba kuweka kumbukumbu sahihi katika Bunge lako Tukufu kuwa tofauti hiyo haikuwepo baada ya marekebisho ya mahesabu kufanyika.” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Bunge lako limeendelea kutumika kama jukwaa la kuichafua Serikali kuwa imefanya matumizi ya 1.5 trillion na Bunge lako limekaa kimya bila kuwakemea hawa. Watanzania wameendelea kupotoshwa na Bunge lako limekubali. Naomba likemewe suala hili na utoe maelekezo. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mlinga, umesimama kuhusu utaratibu, umetaja hiyo Kanuni ya 64(1)(a)…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, please. How can you get to (a) without reading 64? (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, naendelea, hatatoa ndani ya Bunge taarifa ambazo hazina ukweli. Sasa Kanuni hii lazima uisome pamoja na Kanuni ya 63, Mbunge aliyekuwa anaongea hapa alikuwa ni Mheshimiwa Mnyika, kwa hiyo, ni Kanuni ya 63(2), inasema, Mbunge yeyote anapokuwa akisema Bungeni, hutachukuliwa unasema uongo kama unafanya reference. Fasisli ya (3) inasema, Mbunge mwingine yeyote anaweza kusimama mahali pake na kutamka “kuhusu utaratibu’, tumemsikiliza Mheshimiwa Mbunge kafanya hivyo na Mheshimiwa Mnyika kwa mujibu wa fasili ya (4), aliketi, lakini sasa huyu aliyesema wewe husemi ukweli anapaswa aseme kitu, atoe maelezo kwa kiwango ambacho kinaliridhisha Bunge kwamba kuna uongo umesemwa. Ameenda mbali zaidi amesema Taarifa ya Kamati ya PAC kuhusiana na amount hiyo, kwamba Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali ilisema suala hilo si hoja tena, kwa hiyo, hiyo ni rekodi ya Bunge. (Makofi)

Kwa maana hiyo Mheshimiwa, kwa mujibu wa Kanuni zetu, kwa sababu ya maamuzi ya Kamati ya Bunge ya PAC, kwa hayo iliyoyasema, wewe sasa ndiyo unatakiwa uthibitishe kweli au si kweli. Kwa maana hiyo, nakupa options mbili tu, ya kwanza, ufute tu kauli yako kuhusiana na hayo maelezo yako, yale uliyosema ya bilioni ambazo zilikuwa summarized zote, wewe umesema bilioni 900 lakini ukasema ni trilioni 2.4 kwa maana kwamba 1.5 trillion kujumlisha na hizo bilioni ndiyo unapata hiyo. Sasa maelezo ya 1.5 trillion yapo kwenye ripoti ya PAC. Maana wewe umefanya majumuisho, sasa nakupeleka ufute kauli yako au nikupe muda wa kuja kuthibitisha Bungeni hapa, chagua mojawapo.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshmiwa Mwenyekiti, kwanza niweke rekodi sawa, nimesema…

MWENYEKITI: Tunabishana tena?

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshmiwa Mwenyekiti, naomba niseme, naomba niweke rekodi sawa. Nimesema, nataka maelezo ya Serikali Bungeni juu ya shilingi bilioni 976.96 zimetumika kwa matumizi gani? Nimesema jambo hili liko outstanding na hili ndilo linasababisha mjadala wa 1.5 trillion na 2.4 trillion kuendelea. Kwa hiyo, kama ni uthibitisho, nitakiwe kutoa uthibitisho kuhusu suala la shilingi bilioni 976.96 za Vote 20 ya Ikulu. Nipewe nafasi ya kuzungumza kuhusu hilo. (Makofi) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mbunge, huna hoja yoyote, unatupotezea muda wetu wa Bunge. Kwa sababu kama issue yako ilikuwa ni 1.5 trillion kama ulivyoanza, usingekimbilia kutafuta 900 billion shillings. Ulifanya majumuisho ya 2.4 trillion na ndiyo maana Mheshimiwa Naibu Waziri akasimama. (Makofi)

Kwa hiyo, kama unataka tupitie Hansard ili tuone mtiririko wa argument yako. Mimi naagiza watu wa Hansard kabla ya sasa saba tupate Hansard hiyo halafu nitatoa uamuzi wangu kuhusiana na hoja ya Mheshimiwa Mnyika. Ahsante. (Makofi)

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshmiwa Mwenyekiti, naomba…

MWENYEKITI: Muda wako umekwisha, si nilikwambia dakika mbili.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshmiwa Mwenyekiti, muda wangu umekwisha wakati nimekuwa interrupted!

MWENYEKITI: Umekwisha!

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshmiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie muda wangu, nilikuwa nazungumza nikawa interrupted.

MWENYEKITI: Sasa kama hutumii vizuri muda wako, umekwisha. Nimekulindia muda nikakwambia zilikuwa zimebaki dakika mbili, umeongezewa nyingine mbili.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kwanza natumia fursa hii kutoa pole kwa jumuiya nzima ya wafanyabiasha, wadau wa habari, wadau wa viwanda na familia ya mzee wetu, Mheshimiwa Reginald Mengi. Mwenyezi Mungu amlaze mahali pema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa kimya toka Wizara hii imeanza kuchangiwa, nilikuwa nasikiliza michango ya Waheshimiwa Wabunge wenzangu na nilikuwa napitia kumbukumbu za Bunge kuangalia michango ya mwaka 2018, nimekuta kwa sehemu kubwa malalamiko yetu Wabunge ni yale yale yanajirudiarudia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiit, kwa sababu mwaka 2018 tulilalamikia juu ya ubadhirifu kwenye miradi ya maji, kuwepo na miradi ya maji isiyotoa maji na mambo kama hayo; na Serikali ikaahidi yafuatayo, naomba kunukuu maneno ya Mheshimiwa Waziri aliyoyasema: “Kuna haja ya kuunda timu ya wataalamu watakaopitia miradi yote iliyotekelezwa kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge mnapendekeza. Mlipendekeza kwamba iingie Kamati ya Bunge, lakini kabla hamjafika hapo, sisi tayari tumeshaunda na kamati hii itasimamiwa na Profesa Mbwete wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali iliacha au ilikataa Wabunge tusiunde kamati ya kuchunguza ubadhirifu na miradi ya maji ambayo haitoi maji kwa kisingizio cha kwamba Serikali imeunda Kamati ya Profesa Mbwete, lakini Mheshimiwa Waziri alipokuja kutoa hotuba yake Bungeni, hajaeleza hiyo Kamati ya Profesa Mbwete imebaini yapi, watu gani wamechukuliwa hatua mpaka sasa na nini kinaendelea? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hiyo, naomba baada ya kuhitimishwa hoja hii nitoe notice kabisa ya kupendekeza kuundwe Kamati Teule ya Bunge ili ipitie taarifa ya Profesa Mbwete lakini iende mbali zaidi kushughulikia ubadhirifu na ufisadi wote ulioko kwenye miradi ya maji hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hilo la kwanza. Niliomba nianze nalo. La pili ni juu ya takwimu zinazotolewa na Serikali hapa Bungeni kuhusiana na hali ya upatikanaji wa maji. Serikali inasema, kwa wastani hivi sasa, vijijini maji yanapatikana kwa asilimia 65 na mijini kwa asilimia 80. Sasa nawaomba Wabunge wenzangu, hizi takwimu za Serikali zisikubalike kwa sababu hazilingani na hali halisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe ushuhuda tu wa majibu ambayo yametolewa na Serikali hapa Bungeni na Mheshimiwa Naibu Waziri, mwezi Aprili, 2019, Naibu Waziri, juu ya upatikanaji wa maji Jimbo la Kibamba ambapo alisema upatikanaji wa maji ni asilimia hii hii 80, lakini alitoa majibu ya uongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sitaki kuingia kwa undani katika hili kwa sababu ya muda, naipa nafasi Serikali pengine wakati wa majumuisho, irekebishe hii kauli. Kwa sababu Kambi Rasmi ya Upinzani kwenye hotuba yake ukurasa wa nane, sehemu ya tano, wameeleza kiunagaubaga kuanzia aya ya 27 mpaka aya ya 35 ushahidi wa namna ambavyo maelezo ya Serikali hayakuwa ya kweli kwa kueleza kata kwa kata, mtaa kwa mtaa, hali halisi ya upatikanaji wa maji. Nami nafahamu kwa takwimu za ukweli, upatikanaji wa maji kwa Jimbo la Kibamba haujavuka asilimia 65 mpaka sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali ije ieleze ukweli na Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri wafike Jimbo la Kibamba washughulikie hayo matatizo ili upatikanaji ufike hizo asilimia ambazo wanazieleza hapa Bungeni. Hilo ni jambo la pili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa sababu hali hii siyo ya Kibamba peke yake, ni maeneo mengi nchini takwimu zinatolewa siyo za kweli, hiyo Kamati Teule ya Bunge itakapoundwa, pamoja na mambo mengine ikachunguze ili zipatikane takwimu sahihi za hali ya upatikanaji wa maji hapa nchini, Bunge liweze kuchukua hatua kwa niaba ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu, tunaitwisha hii Wizara mzigo mkubwa ambao kwa kweli ni mzigo wa Wizara ya Fedha. Mzigo wa fedha kutokutolewa kwa wakati kwa ajili ya miradi ya maji. Tunavyozungumza hivi sasa, mpaka mwezi Aprili, ukilinganisha kiwango tulichopitisha kwenye bajeti na kiwango cha fedha kilichotolewa, fedha ambazo Serikali haijatoa bado kwa ajili ya Wizara ya Maji, kwa miradi ya maendeleo peke yake ni shilingi bilioni 329. Kati ya hizo, fedha za ndani ambazo Serikali haijatoa mpaka hivi sasa ni shilingi bilioni 288. Sasa kama Serikali hii ina uwezo wa kujigamba inalipa fedha taslimu kwa ajili ya kununua ndege, kwa nini haitoi fedha kwa ajili ya miradi ya maji? (Makofi)

T A A R I F A

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kusainiwa kwa fedha za Washirika wa Maendeleo hakujibu haja na hoja ya fedha za ndani ambazo Bunge lilipitisha ambazo Serikali inapaswa ilieleze Bunge, kwa nini fedha hizi hazijatoka? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Mheshimiwa Waziri wa Fedha atakapokuja kuchangia hii hoja hatatoa maelezo ya kuridhisha, nitaomba nafasi kutoa hoja kwa mujibu wa Kanuni ya 69(1) ili bajeti hii isogezwe mbele mpaka kwanza Serikali itimize matakwa ya kutekeleza bajeti ambayo imekusudiwa na Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kwenye hizi fedha za wahisani, mwaka 2018 tuliambiwa maneno kama haya haya juu ya fedha za India. Tuliambia Serikali imesaini mkataba wa dola milioni 500. Ninao ushahidi hapa wa Hansard wa kiwango kilichosainiwa. Hata kwenye hizo fedha za wahisani vilevile, kwa mujibu wa utekelezaji wa bajeti, kiwango cha fedha kilichotolewa hakijakamilika kwa idadi ya kiwango cha fedha ambacho kilipitishwa na Bunge. Kwa hiyo, hapa napo ipo hoja ya kujadili na Bunge lifanye kazi ya kuisimamia Serikali ili hatua ziweze kuchukuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Serikali haiwezi kutekeleza Bajeti, ni kwa nini mwaka huu vilevile Serikali imeleta hoja, ikitaka fedha nyingi zitengwe, mabilioni yale yale, safari hii imepunguza kidogo; fedha za maendeleo zimepungua kutoka shilingi bilioni 673 mpaka 610, pungufu ya shilingi bilioni 63, lakini bado fedha ziko kule kule juu. Kama Serikali inajijua haina uwezo wa kupeleka fedha, basi ilete bajeti inayolingana na mahitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu, Serikali hii ingeamua kipaumbele kiwe maji badala ya ndege fedha zingetengwa kwa ajili ya maji na wananchi wangekombolewa; na kwa sababu Serikali hii inajigamba wazi wazi kabisa kuleta maendeleo ya vitu, kama ndege, badala ya maendeleo ya watu kwenye miradi kama ya maji, tiba siyo ninyi kwa sababu hamsikii tena, tiba ni Watanzania, kujiandaa kuiondoa Serikali ya CCM madarakani kuanzia kwenye uchaguzi wa mitaa, kwenye vijiji, kwenye vitongoji, kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2020 ili kuingiza kwenye uongozi wa nchi Serikali ambayo itajali maslahi ya watu. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo maeneo ya kimkakati ndiyo biashara ya ndege ambayo Shirika la Ndege linaendeshwa kwa hasara, kwa mujibu wa ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kushindwa tu kujua namna ambavyo maji ni kipaumbele. Maji ni kipaumbele, siyo kwa sababu tu ni huduma kwa wananchi, maji ni kipaumbele vilevile kwa sababu ni huduma ya kiuchumi ambayo ingewezesha uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maji ni kipaumbele. Naomba vilevile Wizara itakapokuja kwenye majumuisho, ieleze ni kwa nini fedha za kujenga mradi wa Kidunda mpaka sasa hazijapatikana? Kwa mujibu wa kumbukumbu za Bunge, ninazo kumbukumbu za Bunge hapa, Mheshimiwa Naibu Waziri akijibu Bungeni kuhusiana na hoja ya Kidunda, kwa sababu ya muda naomba nisiende kwenye ukurasa, lakini alilieleza Bunge kwamba Serikali iko kwenye majadiliano na NSSSF kwa ajili ya kutoa fedha za ujenzi wa mradi wa Kidunda na kwamba akaahidi ifikapo mwezi Julai, 2018 zabuni ya Bwawa la Kidunda ingetangazwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inashangaza sasa hivi Serikali hii isiyowekea kipaumbele miradi ya maji, inasema kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri, ndiyo kwanza fedha za Mradi wa Maji wa Kidunda, zinatafutwa, mradi ambao ukitekelezwa, siyo tu utanusuru watu wa Dar es Salaam na Pwani; kwa sababu pamoja na kupanua Ruvu Juu na Ruvu Chini, kwa sababu ya mabadiliko ya nchi, wakati wa kiangazi, maji Dar es Salaam hayatakuwa yanapatikana ya kutosha, ndiyo maana tunahitaji fedha kwa ajili ya mradi wa Kidunda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo tu mradi huu utasaidia kwenye maji ya viwanda na majumbani, mradi huu ungeweza kuzalisha megawatts…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante. Ahsante sana.

MHE. JOHN J.MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, lakini suluhu ni kuiondoa Serikali madarakani. Ahsanteni sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, katika aya ya 185 ukurasa wa 136 Mheshimiwa Waziri ameeleza kuwa ili kuhakikisha haki za wazee zinalindwa, Wizara imeendelea kuratibu uanzishwaji wa Mabaraza ya Wazee katika ngazi mbalimbali za Halmashauri ambapo hadi kufikia Machi, 2019, jumla ya Mabaraza ya Wazee 9,083 yameanzishwa katika Halmashauri mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Mabaraza hayo yameanzishwa huku kukiwa hakuna Sheria ya Wazee nchini wala sheria ya kuwezesha kuanzishwa kwa Mabaraza hayo. Hivyo katika majumuisho Mheshimiwa Waziri aeleze ni lini Sheria ya Wazee italetwa Bungeni ambayo pamoja na mambo mengine itaeleza kuweka muundo na majukumu ya Mabaraza ya Wazee nchini. Aidha, sheria hiyo itawezesha kuundwa kwa Mfuko wa Maendeleo ya Wazee Nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande mwingine, ipo hoja ya kutungwa kwa Sera ya Maendeleo ya Wanawake Nchini. Sera hiyo ifuatiwe na kutungwa Sheria ya Baraza la Wanawake la Taifa na kusimamiwa kwa Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake nchini na wanawake wenyewe kupitia Baraza lao. Naomba kupata maelezo ya Serikali kuhusu hatua iliyofikia katika kuunda Mabaraza ya Watoto katika Jimbo la Kibamba. Haya yatawezesha watoto kujijenga ikiwemo Stadi za Uongozi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara imewezesha kuandaliwa kwa kanuni za mashirika yasiyo ya kiserikali za mwaka 2018 na kutangazwa katika Gazeti la Serikali Na. 609 la tarehe 19 Oktoba, 2018. Baadhi ya vifungu na vipengele vya kanuni hizo umekamilika na wadau yakiwemo mashirika yasiyo ya kiserikali. Hivyo, Wizara ikae tena na mashirika yasiyo ya kiserikali kupitia vifungu na vipengele vilivyolalamikiwa na kufanya marekebisho. Aidha, Wizara iharakishe kuweka kanzidata ya mashirika yasiyo ya kiserikali kwa kuwa suala hili limechukua muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Vituo vya Maendeleo ya Jamii na Vituo vya Ustawi wa Jamii unaweza kuwa na malengo makubwa kwenye maendeleo na ustawi wa jamii. Vituo hivyo vilianzishwa wakati ambapo mazingira ya kisiasa, kiuchumi na kijamii ni tofauti na sasa. Hivyo Wizara ifanye tathmini ya Mitaa na mazingira ya vituo hivyo na kuja na mapendekezo ya maboresho kwa kuzingatia hali halisi iliyopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mitaala ya vituo hivyo ilenge kujibu changamoto zinazokabili jamii yetu kwa sasa na baadaye. Kadhalika Wizara itoe maelezo ya athari za fedha za maendeleo kutolewa kidogo katika Fungu la 53, Idara Kuu ya Maendeleo ambapo hadi kufikia mwezi Februari, 2019 kiasi cha shilingi bilioni 1.13 tu sawa na asilimia 23.0 tu ya fedha iliyotengwa kilikuwa kimepokelewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ina wajibu wa kuzisimamia kwa karibu mashirika na taasisi yaliyoko chini ya Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) alikagua Bohari Kuu ya Dawa MSD na kubaini kuwa vifaa tiba ya shilingi bilioni 3.55 vilivyonunuliwa kwa mfumo wa manunuzi maalum vilivyorudishwa kutokana na kuzidi kiasi walichoagiza wateja. kutokuwa na sifa zilizotakiwa na wateja au kuzidi kiasi walichoagiza wateja. Baadhi ya vifaa tiba vilivyorudishwa vilikuwa vikikaribia kikomo cha muda. Hivyo, mfumo unapaswa kuboreshwa kuhakikisha kuwa hali kama hii haijirudii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia CAG alibaini katika mwaka 2017/2018 malipo ya shilingi bilioni 480 yalifanywa na Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) kwa vituo vya tiba ya afya kwa wateja ambao hawakuchangia mfuko. Hali hii kama ni kweli ni hatari kwa mustakabali wa mfuko.

Mheshimiwa Naibu Spika, kadhalika, yapo madai kwamba malipo ya shilingi bilioni 13.99 yalifanyika kwa wanaodaiwa kuwa watoto wategemezi, lakini ukweli ni kuwa wamevuka miaka 18, hali ambayo inahitaji NHIF kuharakisha kuanzisha kanzidata ya umri wa wategemezi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri Wizara itumie majumuisho kueleza sababu ya madeni yasiyolipika (bad debts) katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kutoka shilingi milioni 941.32 kwa mwaka wa fedha 2016/2017 mpaka shilingi bilioni 1.44 kwa mwaka wa fedha 2017/2018.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2013 na 2016 palifanyika uthamini (actual valuation) mara mbili kwa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF). Uthamini wa mwaka 2013 ulionyesha kwamba uendelevu bora na mfuko kwa maana ya mfuko kuanza kupata hasara ulikuwa mwaka 2040. Hata hivyo, uthamini wa mwaka 2016 ambao ripoti yake ilitolewa mwaka 2018 unaonyesha kwamba kiwango kimeshuka mpaka mwaka 2025. Hii ni kutokana na uwiano wa malipo ya huduma za afya kukua kila mwaka ukilinganisha na malipo ya Bima za Afya. Wizara inapaswa ieleze nini chanzo cha hali hiyo na ni ufumbuzi upi wa kukabiliana na hali hiyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua hizo zihusishe pia kuboresha mfumo wa Bima ya Afya kwa wastaafu kwa kuwekeza kiwango cha michango ya wanachama ili makato hayo yaje kusaidia malipo ya wanachama katika kipindi cha kustaafu kwao.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuanzishwa kwa Manispaa mpya katika Jiji la Dar es Salaam, Hospitali za Mikoa za Amana, Mwananyamala na Temeke zinapaswa kuhudumia Manispaa za Ilala, Kinondoni na Temeke mtawalia. Hivyo, kuna haja ya kuanzishwa kwa hospitali za mikoa kwa Manispaa mpya za Ubungo na Kibamba. Kwa upande wa Wilaya ya Ubungo Makao Makuu mapya ya Wilaya yanajengwa katika Kanda ya Kwembe eneo la Luguruni.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia patakuwa na ujenzi wa mji mpya wa pembeni (satellite town) eneo la Luguruni. Hivyo, mji unapanuka kuelekea eneo la Kibamba. Kwa mantiki hiyo, napendekeza badala ya kupandisha hadhi Hospitali ya Wilaya ya Sinza, Palestina, mchakato uanze wa kujenga Hospitali ya Mkoa Kibamba na Kwembe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa upande wa Sekta ya Afya, ina jukumu la kuboresha utoaji wa huduma za afya kwa kutekeleza afua mbalimbali. Kwa upande wa Hospitali ya Mloganzila, nimetembelea hospitali hiyo hivi karibuni na kubaini kwamba vipo vipimo ambavyo wagonjwa wanalazimika kwenda kuvipata kwenye Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika majumuisho, Mheshimiwa Waziri wa Afya alieleze Bunge, ni vipimo na huduma zipi ambazo wagonjwa wanalazimika kutoka Mloganzila au vipimo vyao kuchukuliwa kupelekwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na ni mpango gani umewekwa wa kuhakikisha vipimo na huduma hizo zinapatikana katika Hospitali ya Mloganzila?

Mheshimiwa Naibu Spika, katika maeneo niliyopita ni kwamba hata huduma ya CT-Scan wagonjwa kwa sasa wanalazimika kwenda kupata kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande mwingine, utaratibu wa rufaa kutoka Hospitali za Mikoa ya Dar es Salaam zinapaswa kuboreshwa. Kwa sasa hauangalii umbali toka wagonjwa wanapoishi au wanaowahudumia wanapotoka katika kupanga kama mgonjwa husika apelekwe Muhimbili au Mloganzila. Hii inasababisha mathalan mgonjwa wa Ilala kupelekwa Mloganzila wakati ambapo ingekuwa ni rahisi zaidi kwa mgonjwa kama huyo kupelekwa Muhimbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika majumuisho, Wizara ieleze ni utaratibu gani umewekwa wa rufaa kuhakikisha kwamba wagonjwa na wanaowahudumia hawaendi umbali mrefu? Aidha, utaratibu wa rufaa uzingatie uwiano ili kuwe na urari wa idadi ya wagonjwa kati ya Muhimbili na Mloganzila kwa kuzingatia miundombinu, watumishi na huduma zilizopo katika hospitali tajwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli alitoa maelekezo mbalimbali tarehe 3 Oktoba kuhusu uendeshaji wa Hospitali ya Mloganzila. Kati ya maelekezo aliyoyatoa ni pamoja na kuagiza wagonjwa kutoka Muhimbili kutohamishiwa katika Hospitali ya Mloganzila. Wakati Mheshimiwa Rais anatoa maagizo hayo, natambua kwamba wapo wagonjwa ambao tayari walikuwepo kwenye wodi za Mloganzila na pia Hospitali haikuwa na watumishi na huduma kwa kiwango kilichopo sasa. Matokeo ya maagizo hayo ni madai ya wagonjwa waliohamishiwa wengine kufariki kutokana na udhaifu wa huduma. Aidha, wapo wagonjwa ambao walihamishwa wakiwa katika hali mbaya na kupoteza maisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika majumuisho, Mheshimiwa Waziri aeleze ni wagonjwa wangapi walifariki katika kipindi hicho cha mpito na ni hatua gani zimeweza kuchukuliwa kupunguza idadi ya vifo vilivyotokea?

Mheshimiwa Naibu Spika, panakuwepo pia mgogoro wa mipaka baina ya Mkoa wa Dar es Salaam na Mkoa wa Pwani kuhusu wapi hasa ipo Hospitali ya Mloganzila? Naomba katika majumuisho au katika mjadala, Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana na suala hili, atangaze kuwa Hospitali ya Mloganzila ipo katika Jili la Dar es Salaam Manispaa ya Ubungo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba katika majumuisho Wizara ya Maliasili na Utalii itoe maelezo ni kwa nini mpaka sasa haijawezesha Pori la Akiba la Pande kugeuzwa kuwa bustani ya wanyama na kivutio cha utalii? Suala hili Serikali imekuwa ikinipa ahadi toka mwaka 2011. Mwaka 2015 Serikali ilijibu Bungeni na kuomba ipewe mwaka mmoja tu, huu ni mwaka 2017, miaka miwili imepita.
Aidha, baada ya Mkutano huu wa Bunge Wizara iandae ziara ya kikazi pamoja na Mbunge kutembelea pori husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha kati ya mwaka 2011 mpaka 2015, nilihoji kuhusu Kiwanda cha Tembo Chipboard kilichopo Mkumbara ambacho kiko chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Wizara ilijibu kuwa kulikuwa na matatizo katika ubinafsishaji, hali iliyosababisha kiwanda kuacha kufanya kazi. Wizara iliahidi kwamba itaingilia kati kuwezesha kiwanda kuweza kufanya kazi ipasavyo. Hata hivyo, mpaka sasa kiwanda hakijarejea katika hali ya kawaida.

Hivyo, ni vema Wizara ikafanya utaratibu mkataba uliokuwepo uvunjwe na kiwanda kirejee katika hali yake ya awali ya kufanya kazi. Wizara izingatie kuwa Serikali ilishatoa ahadi Bungeni kwamba viwanda vyote ambavyo vilibinafsishwa lakini waliopatiwa wameshindwa kutimiza masharti ya kimkataba, vitarejeshwa Serikalini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka imepita toka Bunge lipitishe maazimio kuhusu Operesheni Tokomeza. Nilitarajia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri angeeleza hatua ambazo zimechukuliwa katika kutekeleza maazimio husika ya Bunge.

Hivyo basi, katika majumuisho Mheshimiwa Waziri aelezwe hatua ambazo Wizara imechukua kutekeleza maazimio ya Bunge kuhusu Operesheni Tokomeza.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, katika aya ya 21 ukurasa wa tisa na 10 ya hotuba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, imeelezwa kwamba hali ya upatikanaji wa maji katika Jiji la Dar es Salaam imeimarika baada ya kukamilika kwa maboresho ya mitambo ya Ruvu Juu na Ruvu Chini. Hata hivyo, Wizara izingatie kuwa hali haijaimarika katika maeneo yanayohudumiwa na Ruvu Juu kwa upande wa Jimbo la Kibamba katika kata za Kwembe, Mbezi, Msigani, Saranga na Kibamba.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni vema kufanya ziara ya haraka ya kikazi yenye kumhusisha Waziri wa Maji, Mbunge, DAWASA na DAWASCO ili kukagua maeneo yote ya mabomba ya Mchina ambayo nilipowasilisha hoja binafsi tarehe 4 Februari, 2013 Bungeni Serikali iliahidi kwamba baada ya kukamilika kwa upanuzi wa mtambo wa Ruvu Juu na ujenzi wa bomba maji yangekuwa yanatoka. Aidha, kwa upande wa maeneo katika kata hizo za Kibamba, Kwembe, Mbezi, Msigani na Sarange ambayo hayana mtandao wa usambazaji wa maji, kasi ya kuwaunganishia wananchi ni ndogo sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kwamba katika aya ya 135 ukurasa wa 72 na 73, Wizara imetaja maeneo ya Mbezi hadi Kiluvya na maeneo ya Kibamba, Msakuzi, Makabe, Malamba Mawili na Msigani. Upanuzi wa mfumo wa kusambaza maji katika maeneo hayo unasuasua, kadhalika yapo maeneo mengine katika kata hizo hayajatajwa katika orodha hiyo. Hivyo naomba Wizara inipatie orodha ya maeneo yote ambayo hayana mfumo wa kusambaza maji safi katika kata hizo tano na ratiba yenye kuonyesha ni lini maeneo hayo yatasambaziwa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Ruvu Chini ieleweke kwamba katika Jimbo la Kibamba kata pekee inayopata maji kutoka chanzo hiki ni kata ya Goba, katika aya ya 135 ukurasa wa 73 yanatajwa maeneo ya Kinzudi, Matosa na Mtaa wa Goba. Hata hivyo mtandao wa mabomba ya maji katika maeneo hayo haulingani kabisa na mahitaji. Aidha, ipo mitaa mingine katika kata ya Goba ambayo haipo katika orodha ya kusambaziwa maji katika mradi huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo naomba kupewa orodha ya maeneo yote ya kata ya Goba yasiyokuwa na mtandao wa mabomba ya maji yenye kuonyesha ratiba ya lini yatawekewa mabomba ya maji. Naomba Wizara inaposhughulikia miradi ya maji ya Ruvu Chini kwa upande wa DAWASA na DAWASCO itoe kipaumbele maalum kwa kata ya Goba.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika aya ya 133 ukurasa 71, Serikali imeeleza kwamba inaendelea kutekeleza mradi wa Bwawa la Kidunda unaogharimu dola za Marekani milioni 215. Hata hivyo, kimsingi hakuna utekelezaji unaoendelea kwa kuwa pamoja na usanifu kukamilika muda mrefu, mpaka sasa Serikali inaendelea kutafuta fedha. Mradi huu ni wa kutoka wakati wa Mwalimu Nyerere mwaka 1980 na sasa ni wa dharura kutokana na mabadiliko ya tabianchi.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, katika Bunge la Kumi niliwasilisha Bungeni maelezo binafsi kuhusu tathmini ya ukusanyaji wa kodi ya majengo Jijini Dar es Salaam uliokuwa unafanywa na Mamlaka ya Mapato (TRA) kwa kulinganisha na wakati ambapo ukusanyaji huo ulikuwa ukifanywa na Halmashauri. Maelezo hayo yalieleza bayana kwamba kodi ilikusanywa kwa ufanisi zaidi na Halmashauri zaidi ya TRA.

Aidha, maelezo hayo yalipendekeza hatua za kuchukuliwa kuboresha kasoro ndogo katika Halmashauri ili kuongeza ufanisi. Wizara ya Fedha irejee maelezo hayo na kuleta marekebisho wakati wa Muswada wa Sheria ya Fedha ili kurejesha ukusanyaji wa mapato hayo kwa Halmashauri. Kitendo cha TRA kukusanya shilingi bilioni 20.2 tu wakati makadirio yalikuwa shilingi bilioni 47.6 pekee ni ushahidi kuwa yale niliyoyaeleza kwenye maelezo binafsi kwa TRA haiwezi kuwa wakala bora wa ukusanyaji wa kodi hizi.

Mheshimiwa Spika, izingatiwe kuwa hata makadirio ya shilingi bilioni 47.6 kwa nchi nzima ni madogo kwa kuwa hata Halmashauri na Jiji la Dar es Salaam ikiwemo ya kwetu ya Ubungo zingepewa mamlaka ya kukusanya kodi ya majengo zingevuka malengo yaliyowekwa na TRA. Hatua hii ya kurejesha kodi ya majengo ichukuliwe pia kwenye ada za mabango na vyanzo vingine vya mapato ambavyo Serikali Kuu imeamua kuvihodhi/kuvitwaa. Kitendo cha kuminya vyanzo vya uhakika vya mapato vinafanya Halmashauri kushindwa kutumia ipasavyo dhamana za Serikali za Mitaa (Municipal bonds) kujipatia fedha za vitega uchumi na miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, Serikali inapaswa kuchukua hatua za haraka za kurejesha Tume ya Mipango na kufanya marekebisho ya sheria kuipa mamlaka zaidi kuwa chombo huru. Hatua ya sasa ya masuala ya mipango kuwa kama sehemu ya Wizara ya Fedha kumefanya masuala ya mapato na matumizi kupewa kipaumbele bila mipango thabiti.

Mheshimiwa Spika, hali hii imeathiri pia bajeti za Wizara kwa Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano na Dira ya Taifa kutokuzingatiwa kwenye vipaumbele. Aidha, ni muhimu Kitabu cha Mapato (Volume 1) kipewe kipaumbele na utengwe muda wa kutosha na Bunge kujadili kuhusu mapato kabla ya kujikita katika matumizi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, Wizara ya ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ina majukumu yanayogusa sekta kama tatu zenye kuwezesha maendeleo ya nchi na wananchi. Katika aya ya 26 ukurasa wa 15, Waziri ameeleza ujenzi wa barabara ya Dar es Salaam – Chalinze, kilomita 144 haujaanza kutokana na maamuzi ya Serikali kusogeza mbele utelekezaji wa mradi huu ili kukamilisha kwanza miradi hii inayoendelea, ni vyema katika majumuisho Serikali ikaeleza imesogeza mbele mradi huu mpaka lini.

Mheshimiwa Spika, aidha, ni kwa nini Serikali imeamua kusogeza mbele wakati ambapo imesema mara kadhaa kwamba mwaka 2011 kwamba mradi huu ungetekelezwa kwa ubia kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP) na ungekuwa na barabara za kulipia ili kurejesha gharama za ujenzi ambazo zingeingiwa na sekta binafsi katika ujenzi.

Mheshimiwa Spika, katika aya ya 44, ukurasa wa 24, Serikali ieleze sababu ya barabaa za Kimara - Korogwe Maji Chumvi (kilomita tatu) na sehemu ya Goba - Madale (kilomita tano), ujenzi wake kwenda taratibu. Aidha, ni kwa nini Serikali imechukua kipande kidogo tu cha Mloganzila – Kisopwa (kilomita moja) kati ya kilomita 14.66 za barabara ya Kibamba – Kisopwa – Kwembe - Makondeko. Kwa kasi hii ndogo itachukua miaka takribani 14 kwa barabara hiyo kukamilika.

Mheshimiwa Spika, katika aya ya 54, ukurasa wa 30, imeelezwa kuwa ujenzi wa barabara ya juu (interchange) katika barabara ya Ubungo umefika asilimia 28. Hii inaonesha kwamba kasi ya ujenzi ni ndogo sana. Wizara ikumbuke kwamba mwezi Machi, 2017 wakati na uzinduzi wa ujenzi Mheshimiwa Rais aliagiza kwamba ujenzi wa barabara ya juu ya Ubungo ukamilike ndani ya miezi 30. Kwa agizo hilo ujenzi unapaswa kukamilika mwezi Agosti, 2019, hivyo kwa asilimia 28 mwezi Mei ni kiwango cha chini sana cha utekelezaji. Hivyo Wizara itoe maelezo ni mikakati gani imewekwa kuharakisha ujenzi ili ukamilike kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, kwenye aya ya 60, ukurasa wa 33, Waziri ameeleza kuwa upanuzi wa barabara kwa njia nane kwa sehemu ya Kimara - Kiluvya (kilomita 19.2) unaendelea ambao utarahisisha pia upanuzi wa Madaraja ya Kibamba, Kiluvya na Mpiji. Hata hivyo, Waziri hajaeleza ujenzi wa barabara umefikia hatua gani, eneo ambalo ni vyema akalieleza katika majumuisho. Katika kipindi cha uzinduzi uliofanywa na Rais ambapo walishiriki, kasi ya ujenzi kabla na baada ilikuwa kubwa. Hata hivyo, kwa sasa kasi imepungua, hivyo ni vyema Wizara ikafuatilia kwa karibu kuwezesha ujenzi kufanywa kwa haraka.

Mheshimiwa Spika, aidha, naomba mkandarasi kama alivyofanya kwa eneo la Kibamba CCM kusawazisha eneo kwa ajili ya kituo cha muda cha daladala afanye hivyo katika eneo la Kiluvya. Eneo la kusimama daladala lilishawekwa, Wizara ihakikishe SUMATRA inasimamia daladala zifike Kiluvya badala ya kuishia Kibamba CCM na kufanya wananchi wa Kiluvya waingie gharama kubwa za kupanda mabasi yanayokwenda Kibaha, Mkoani Pwani.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu ya Rais kuhusu fidia ya wananchi kupisha ujenzi wa barabara hii, naomba Wizara irejee hukumu ya kesi ya wananchi wa Mbezi ambao walifungua kesi Mahakama Kuu Kitengo cha Ardhi ambapo mahakama ilitamka wananchi wanastahili fidia.

Mheshimiwa Spika, katika aya ya 73, ukurasa wa 40, kwenye hotuba ya Waziri amezungumzia kuhusu miundombinu ya mabasi yaendayo haraka awamu ya pili hadi ya tano. Naomba majibu ya Serikali katika majumuisho ni awamu ipi hasa ya ujenzi itahusisha ujenzi wa miundombinu ya mabasi yaendayo haraka kwa kipande cha kutoka Kimara mpaka Kiluvya?

Mheshimiwa Spika, ili kutoiingiza nchi kwenye gharama kama iliyotokea katika maeneo mengine ambapo lami na miundombinu mingine imelazimika kuvunjwa kuwezesha kujengwa kwa miundombinu ya mabasi yaendayo haraka, ni vyema upanuzi wa sasa wa barabara ya Morogoro kutoka Kimara mpaka Kiluvya ukahusisha pia ujenzi wa miundombinu ya mabasi yaendayo haraka.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2018/ 2019, Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) umekuwa ukikabidhiwa ujenzi wa majengo mbalimbali ya Serikali. Kati ya kazi ambazo TBA imefanya hivi sasa ni pamoja na ujenzi wa Makao Makuu ya Wilaya Mpya ya Ubungo. Naomba TBA iharakishe kukamilisha ujenzi wa Makao Makuu ya Wilaya. Aidha, naomba TBA izishauri mamlaka zinazohusika ili ujenzi huo unaofanyika katika Kata ya Kwembe, Mtaa wa Luguruni uhusishe pia ujenzi wa Ofisi ya Mbunge ambayo katika michoro ya sasa haijawekwa.

Mheshimiwa Spika, TBA pia ikutanishwe na Shirikia la Nyumba (NHC) kujadiliana kuhusu uendelezaji wa Mji wa Viungani (Satellite Town) wa Luguruni ili majengo ya Serikali na nyumba za viongozi katika eneo hilo TBA ifuatilie kwa karibu ujenzi uanze. Serikali ililipa muda mrefu fidia katika eneo hilo lakini shughuli za uendelezaji zimesimama.

Mheshimiwa Spika, juu ya kasma 4138 ya kupunguza msongamano katika Jiji la Dar es Salaam (De-congestion of Dar es Salaam Roads) kipande cha Goba - Makongo kilomita nne kimetengewa milioni 310 tu ilihali kuna kipande cha barabara ambacho kwa muda mrefu hakijawekewa lami. Naomba kiwango cha fedha kiongezwe kuwezesha eneo lote lililobaki kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, kwenye kasma 4161 kuhusu Madaraja ya Juu (Dar es Salaam Road Flyovers) kwa upande wa Ubungo Interchange zimetengwa milioni 145 tu kwa upande wa fedha za ndani. Napendekeza kiwango kiongezwe kwa kuzingatia mahitaji yaliyopo kwenye mkataba.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kasma 4132 juu ya fedha za Mfuko Mkuu wa Serikali katika kutekeleza miradi ya mkoa barabara ya Kimara – Bonyokwa – Kinyerezi yenye kilomita mbili umetengewa katika bajeti milioni 60 peke yake wakati barabara hii ina hali mbaya. Naomba TANROADS watembelee barabara hii na kufanya matengenezo yanayostahili. Hali iko hivyo pia kwa barabara ya Goba – Matosa - Temboni.

Mheshimiwa Spika, katika kasma 2326 kumetengwa milioni 150 kwa ajili ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina (feasibility study and design) kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya juu (interchange) Mbezi mwisho kuelekea eneo kutakapojengwa kituo cha mabasi ya mikoani. Naomba mchakato huu uharakishwe ili uende sanjari na ujenzi wa kituo unaoendelea pamoja na upanuzi wa barabara kuwa njia nane.

Mheshimiwa Spika, fedha za Mfuko wa Barabara zitatumika pia kuboresha kwenda DSD barabara ya Kunguru - TATEDO (kilomita tano) ambapo kumetengwa milioni 120. Naomba hatua hiyo iende mbele zaidi kwa kujenga daraja katika eneo la Muungano, Kata ya Goba katika sehemu inayounganisha na Salasala.

Mheshimiwa Spika, katika kiambatisho namba 5(B-2), ukurasa 381, Waziri ameeleza barabara ambazo zitafanyiwa marekebisho ya muda maalum (period maintenance) kwa kutumia fedha za Mfuko wa Barabara. Hata hivyo, katika orodha hiyo hakuna hata barabara moja ya Jimbo la Kibamba kwenye Kata sita za Kwembe, Msigani, Mbezi Luis, Goba, Saranga na Kibamba. Hivyo ni vyema Wizara ikaongeza katika orodha hiyo barabara muhimu za Jimbo la Kibamba zenye kuunganisha Mkoa wa Dar es Salaam na Mkoa wa Pwani na zenye kuunganisha Wilaya ya Ubungo na Wilaya za Kinondoni na Ilala katika Jiji la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, kati ya barabara ambazo ni muhimu TANROADS ikazichukua na kuzifanyia matengenezo ya haraka ni Temboni kwa Msuguri – Msingwa ambayo inaunganisha mpaka Wilaya ya Ilala. Kihistoria, barabara hii TANROADS iliwahi kuitengeneza lakini baadhi ya wananchi wakaenda mahakamani miaka mingi nyuma hali iliyofanya TANROADS kuacha kuihudumia kwa muda mrefu. Mgogoro huo umemalizika lakini TANROADS na TARURA bado wanarushiana mpira mpaka sasa kuhusu kuihudumia. Pamoja na kuwa TARURA wameanza matengenezo madogo, naomba barabara hii ichukuliwe na TARURA ili ifanyiwe matengenezo makubwa na hatimaye ijengwe kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, kwenye sehemu (b) juu ya barabara za mikoa za changarawe/udongo. Matengenezo ya barabara zilizopo kwenye Jimbo la Kibamba yamekuwa yakifanyika lakini sio kwenye kiwango cha kuridhisha. Barabara hizo baadhi zimetajwa kwenye ukurasa wa 39o za Kibamba Shule – Magoe Mpiji na Makabe Junction – Mbezi Msakuzi. Naomba katika majumuisho, Serikali ieleze ni lini itafanya matengenezo yenye kiwango. Pia kwa barabara kutoka Mbezi kupitia Mpiji Magoe – Mabwepande mpaka Bunju. Barabara ina vipande kadhaa ambavyo viko kwenye hali mbaya ikiwemo kipande cha barabara kilichomo ndani ya Pori la Akiba la Pande.

Mheshimiwa Spika, Wakaguzi watembelee barabara hii na matengenezo yafanywe. Kwa upande mwingine, Serikali ieleze ni lini barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami kama ambavyo Serikali iliahidi miaka ya nyuma.

Mheshimiwa Spika, kwenye kiambatisho namba 5(D- 2) juu ya matengenezo makubwa ya madaraja na makalavati (bridge major repair) kwa kutumia fedha za Mfuko wa Barabara. Nashukuru kwa kalavati (box culvert) la Msakuzi katika barabara ya Kibamba Shule – Mpiji Magohe limejumuishwa na kutengewa milioni 340. Naomba ujenzi wa box culvert hilo ufanyike kwa haraka. Aidha, naomba maelezo ya Serikali ya sababu za Kibwegere box culvert kutengewa shilingi milioni 10 tu.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Sekta ya uchukuzi, Serikali ihakikishe ujenzi wa reli kwa kiwango cha kisasa (SGR) unatumia kwa kiasi kikubwa malighafi kutoka ndani ikiwemo matumizi ya chuma kutoka Mchuchuma na Liganga ili kuhakikisha sehemu kubwa ya fedha zinabaki katika mzunguko wa ndani. Kamati za Kisekta zinazohusika zipewe nafasi ya kuangalia Mikataba mikubwa ya Ujenzi na Uchukuzi ili kuhakikisha maslahi ya kiuchumi ya nchi yanalindwa kikamilifu.
Itifaki ya Nagoya ya Kusimamia Upatikanaji na Mgawanyo Sahihi wa Faida zitokanazo na Matumizi ya Rasilimali za Kijenetiki.
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mkataba mmoja pamoja na Itifaki mbili na nimepata wasaa wa kuzisoma soma hapa, lakini kwa kuwa kuna dakika tano nitajielekeza kwenye mambo machache tu.

Mheshimiwa Msigwa aliposema Bunge dhaifu husababisha Serikali dhaifu amenikumbusha kauli ambayo niliisema Bungeni hapa tarehe 19 mwaka 2012. Na kinyume chake, Serikali dhaifu vilevile husababisha Bunge kuwa dhaifu na ndiyo hali ambayo tunayo hivi sasa. Bunge letu limefanywa dhaifu sana na limefanywa dhaifu na Serikali na Serikali hii ingekuwa na nguvu ingejiamini sana, isingefanya Bunge kuwa dhaifu, lakini kwa sababu Serikali ni dhaifu ni lazima na Bunge nalo liwe dhaifu.

T A A R I F A . . . . .

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namwombea Mwenyenzi Mungu Mheshimiwa Mlinga aweze kubadilika hiyo tabia yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge hili limekuwa dhaifu kwa kiwango ambacho miswada, mkataba mmoja na Itifaki mbili zinaletwa zote kwa siku moja wakati ambapo Bunge lenye nguvu lingesema kwamba siku hii tunajadili mkataba huu, tunaujadili vizuri vinatafakari hoja umetolewa. Siku hii tunajadili mkataba huu, siku hii tunajadili mkataba huu. Kwa udhaifu huu wa Bunge unaoendelea anasema sikuwepo siku nyingi. Hii siku nyingine sikuwepo si Mwenyekiti unajua mlinitoa ndiyo maana sikuwepo. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya udhaifu huu Wabunge Mheshimiwa Halima Mdee hatakuwepo kwa muda wote ambao hatakuwepo, akija kurudi mtamwambia maneno haya haya. Mheshimiwa Ester Bulaya hatakuwepo hakirudi mtamwambia maneno haya haya. Sasa hii hoja ya uchafunzi wa mazingira upande wa bahari nizungumzie kwa niaba ya Mheshimiwa Mdee wa Jimbo la Kawe ambaye bahari inazunguka eneo lake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikataba hii Serikali iliisaini muda mrefu, lakini hakuna kinachofanyika kuzuia uchafuzi, hakuna kinachofanyika cha kutosha kunufaisha wavuvi. Nataka kusema nini hapa, kuridhia mikataba hii peke yake na Kambi ya Upinzani hapa inairidhia inaunga mkono kuridhiwa kwa hii mikataba haitoshi kama mwisho wa siku masharti ya msingi yaliyoko kwenye Itifaki, masharti ya msingi yaliyoko kwenye mikataba hayatekelezwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tutaruhusu Serikali kuendelea kuwa dhaifu na Bunge kuendelea kuwa dhaifu ni wazi siku zote tutapitisha mikataba na sheria lakini utekelezaji hakuna. Tuna Mkataba muhimu sana hapa, huu mkataba unahusu rasilimali za kijenetiki ambao nchi iliuingia mwaka 2010 tumeletewa leo kuridhia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matajiri unaowakuta duniani iwe ni akina Bill Gates, iwe ni tajiri wa Apple aliyefariki matajiri mnawakuta duniani walipata utajiri kwa sababu ya ubunifu. Wenzetu wana ubunifu wa kiteknolojia sisi tunawabunifu wengi sana ambao wangeweza kunufaika na rasilimali za kijenetiki kwenye ugunduzi wa dawa, tiba, vitu na mbalimbali lakini kwa sababu mambo haya hatuyafanyi vile inavyostahili ndiyo maana hatufiki pale ambazo tunafika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tumeingia katika sekta ambayo wengine ndiyo tunadhani ina manufaa zaidi ya madini. Kumbe huku kuna madini kwenye jenetiki, lakini hatufanyi ipasavyo. Hata kwenye madini tumewaambia muda mrefu leteni mikataba hapa Bungeni tumewaambia muda mrefu leteni mikataba leteni mikataba, tumeimba kwa miaka mingi leteni mikataba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mnatuletea hoja mnasema kwamba tunaleta sheria ya kulipa Bunge mamlaka juu ya mikataba halafu mnataka propaganda kama vile sisi ambao ndiyo tulikuwa tunasema mikataba iletwe tunakataa, sisi tunachokataa ni kwamba ninyi wa kuzileta sheria kwa Hati ya Dharura mnatunga sheria mbovu ambazo mwisho wa siku hazileti tija ambayo inasukudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kweli ninyi mnataka kuisaidia nchi kwenye masuala ya madini, hata kama tukianzia na hapo ambapo nilisema Rais angekuwa makini asingeanzia na makinikia angeanzia na madini. Hata kama tukiamua kuanzia na makinikia cha kwanza ambacho Bunge ingetaka kwenye Bunge hili kabla hata kuletewa miswada kusoma kwa mara ya kwanza zile ripoti mbili zile, zile ripoti alizokabidhiwa Mheshimiwa Rais, ipaswa ziwasilishwe hapa Bungeni Mawaziri wazisome tuzijadili Wabunge halafu tuseme sasa Serikali kaandae mapendekezo ya muswada ya kuhusu hiki, kuhusu hiki, kuhusu hiki, iletwe hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nachotaka kusema hapa ni kuwa, badala ya kuanza kujadili Miswada ya Sheria kwa Hati ya Dharura, Bunge hili liletewe kwa udharura huo huo ripoti mbili za Rais kuhusu makinikia, zisomwe hapa Bungeni, zijadiliwe hapa Bunge msipofanya hivyo ile kauli niliyosema kwamba Rais makini alipaswa kuanza na madini kabla ya makinikia kuna siku itakuja kuwatafuna.

Mheshimiwa Lema amesema kwamba kama hamtasikia maoni yetu basi ni afadhali mfike hatua mfute Kambi ya Upinzani. Mheshimiwa Lema kabla hawajafuta Kambi ya Upinzani kama wataendelea kutosikiliza maoni yetu imefikia hatua Watanzania waiondoe hii Serikali madarakani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mnadhani tumechelewa, kama mnashindwa tu kuwadhibiti wale watu wa Kibiti, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, kama mnashindwa kuwadhibiti watu wa Kibiti wanaotumia silaha, ndugu zangu hamuwezi kuwadhibiti Watanzania hawa wakiamua kutumia silaha yao, kadi yao kupigia kura kwenye sanduku la kura. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza kwa niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, naomba kutoa pole kwa Chama cha Mapinduzi, hususan Chama cha Mapinduzi Zanzibar kwa kifo cha Mzee wetu Shamhuna, Mwenyezi Mungu amlaze mahali pema na msiba wake unaendelea kutukumbusha kwamba, sisi wote ni udongo na tutarudi kuwa udongo. Kwa sababu hiyo, tuenende kwa unyeyekevu na hekima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, nieleze tu kwa sababu nina dakika 10 kwamba, naunga mkono Mapendekezo ya Kambi Rasmi ya Upinzani kuhusu zao la korosho kuanzia aya ya 80 mpaka aya ya 92 na mapendekezo yote hayo kuanzia ukurasa wa 23 na 26, yahesabike vilevile kama ni sehemu ya mchango wangu ili nijielekeze kwenye nini sasa tufanye baada ya kadhia nzima ya korosho ambayo kwa ukubwa wake, hii kashfa ya korosho inafanana na EPA, inafanana na Escrow, inafanana na Richmond, inafanana na kashfa zenye sura ya namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika mazingira ya namna hii tunapaswa turejee kwenye Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo Ibara ya 63(20), imetamka kwamba, Bunge ndio chombo kikuu ambacho kwa niaba ya wananchi kina wajibu, sio tu wa kuishauri Serikali bali pia, kuisimamia Serikali. Hapa tunahitaji kuisimamia Serikali na kutaka uwajibikaji wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tunapotaka uwajibikaji wa Serikali Kiongozi wa Shughuli za Serikali hapa Bungeni, kwa Katiba ya nchi yetu, Ibara ya 52 inamtamka kwenye Ibara Ndogo ya (2) kwamba, ni Waziri Mkuu na Ibara Ndogo ya (1) inasema, sio tu hapa Bungeni Waziri Mkuu atakuwa na madaraka juu ya udhibiti, usimamiaji, utekelezaji wa siku kwa kazi za shughuli za Serikali za kila siku.

Mheshimiwa Spika, sasa kama hili suala la korosho kwa siku zote hizo limeendelea na kashfa ya uozo wa namna hii, ni wakati sasa Waziri Mkuu katika majumuisho ya Wizara hii afike Bungeni atangaze kujiuzulu yeye mwenyewe nafasi yake kabla hajawajibishwa. Hii ndio italinda dhana ambayo Mheshimiwa Mwakyembe alisimama siku chache zilizopita akimjibu Mheshimiwa Msigwa wakati aliposema Waziri Kabudi anatakiwa kujiuzulu, Waziri Mwakyembe alisimama kwa niaba ya Serikali, kwa niaba ya Waziri Mkuu akasema jambo hili ni la uwajibikaji wa pamoja, sasa uwajibikaji wa pamoja uonekane ukitanguliwa na Waziri Mkuu mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili la uwajibikaji wa pamoja linaongozwa na Katiba yetu, Ibara ya 53(2), nitanukuu inasema:

“Serikali ya Jamhuri ya Muungano chini ya mamlaka ya Rais itakuwa ndio itakuwa na uwezo wa kufanya maamuzi juu ya sera za Serikali kwa ujumla na Mawaziri,” Mawaziri nasisitiza, “Mawaziri chini ya uongozi wa Waziri Mkuu watawajibika kwa pamoja Bungeni kuhusu utekelezaji wa shughuli za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kadhia hii imewagusa Mawaziri wengi kidogo, imewagusa wale walioondolewa mwanzoni, wakati Rais alipotoa kauli akafikia hatua mpaka kusema wale mashangazi kule Kusini watapigwa, wakaondoka baadhi ya Mawaziri. Wakaingia wengine, lakini hawa walioingia badala ya kurekebisha tatizo wamelikuza na kuliendeleza tatizo mpaka hivi sasa tunavyozungumza. Ndipo yanapokuja masuala kama ya Indo Power ambayo pamoja na kuwa Mheshimiwa Profesa Kabudi ndio anaonekana kwenye picha pale mbele, mstari wa mbele, Mawaziri wanaohusika ni Waziri wa Fedha ndio maana Gavana wa Benki alikuwepo, anatakiwa awajibike, Waziri wa Viwanda na Biashara anatkiwa awajibike, Waziri wa Kilimo naona tunamkwepakwepa Waziri huyu eti kwa sababu ni mpya wakati mkataba umesainiwa yeye akiwepo anatakiwa kuwajibika, Waziri wa Mambo ya Nje anatakiwa kuwajibika, Waziri wa Utawala Bora ambaye Usalama wa Taifa uko chini yake wenye wajibu wa kuishauri Serikali anatakiwa kuwajibika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwa mzigo wote huu wa uwajibikaji, lazima Waziri Mkuu ndio awe minara wa kwanza wa kuwajibika kutangaza kujiuzulu nafasi yake ya Uwaziri Mkuu. Waziri Mkuu akishajiuzulu maana yake… (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa John Mnyika kwa mtu ambaye hajui nini kimekuwa kikiendelea, ikiwa ni pamoja na mimi mwenyewe, tungependa kujua wawajibike kwa sababu gani? Endelea tu.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze na hili la Indo Power ambalo mnataka kusema as if kwa sababu, hawajauziwa korosho sio shida. Kwenye uchumi kuna kitu kinaitwa opportunity cost, gharama ya fursa; yaani kwamba, walituahidi kununua korosho laki moja na tukasaini na hawakununua na korosho zikakaa kwenye maghala mpaka zimeoza, tunavyozungumza hivi sasa tumekosa mapato ya nje. Hii gharama ni kubwa ni ya yale makosa yanayopelekwa Mahakamani unasikia, huyu awajibike kwa uzembe na kuisababishia hasara Serikali kwa uhujumu uchumi, hao wanatakiwa kuonesha uwajibikaji, ili sasa wale walioishauri Serikali vibaya, kama kuna watu nyuma walioishauri ukiondoa hawa Mawaziri, nyuma ya Serikali hawa nao wanapaswa kuwajibika.

Mheshimiwa Spika, hili ni suala la Kikatiba tena…

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

T A A R I F A

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, bahati nzuri nazungumza nikiwa nimetoka Ruvuma, Mtwara na Lindi kwenye shughuli za chama na nimekutana na wakulima. Wanapozungumzia korosho huwa zina muda wake, muda ukipita korosho zinasinyaa, zikishasinyaa zinakosa soko na ndiyo maana Serikali…

WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, taarifa…

MHE. JOHN J. MNYIKA: imeanza kuwarudishia wananchi, naomba niendelee…

WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, mimi naomba niendelee kwa sababu anani…

SPIKA: Mheshimiwa Mnyika pokea taarifa hiyo.

MHE. JOHN J. MNYIKA: …wananipotezea tu muda wangu.

Mheshimiwa Spika, ninachokisema ni kwamba kuna wakulima wanarudishiwa korosho zao wanaambiwa Serikali haizitaki tena zipo chini ya kiwango kwa sababu Serikali inajua haziuziki nje inaanza kuwarudishia wakulima. Kuna wakulima hawajalipwa, kuna mambo mengi nisipotezwe nje ya mstari naomba niendelee…

MHE. KATANI A. KATANI: Taarifa.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Katiba ya nchi…

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Spika, taarifa…

SPIKA: Naomba tumuache aendelee, endelea Mheshimiwa…

MHE. KATANI A. KATANI: Tuweke clarification hili…

SPIKA: Dakika zako zitavurugika, endelea.

MHE. KATANI A. KATANI: Nilitaka nijibu korosho wapi zimeoza maana najua.

SPIKA: Mheshimiwa Katani muachie, za kwako ulizitumia vizuri, ungeongea.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, Katiba ya Nchi yetu Ibara ya 54 inayozungumza kuhusu Baraza la Mawaziri ibara ndogo ya 3 inasema bila kuathiri masharti yaliyomo Ibara ya 37 ya Katiba hii, Baraza la Mawaziri litakuwa ndicho chombo cha kumshauri Rais juu ya masuala yote yanayohusika na utekelezaji wa madaraka yake. Inaendelea mbele, kwa ajili ya muda nisiinukuu yote.

Mheshimiwa Spika, maana yake ni kwamba huu uozo wote wa korosho, kuanzia ushauri wa kwanza wa kumshauri Rais kwamba korosho zikusanywe na zibebwe na jeshi na kuleta azimio hapa Bungeni la kumpongeza Rais; huu uamuzi Baraza la Mawaziri lilimshauri Rais vibaya, Baraza la Mawaziri linastahili kuvunjwa. Mpaka uamuzi wa kwenda mbele kuitafuta hiyo Kampuni ya Kenya ya Indo Power kwamba itanunua korosho…

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA): Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. JOHN J. MNYIKA: …za laki moja. Baraza la Mawaziri limemshauri Rais vibaya, Baraza la Mawaziri linastahili kuvunjwa na ili livunjwe Waziri Mkuu ajiuzulu…

SPIKA: Mheshimiwa Mnyika…

MHE. JOHN J. MNYIKA: …na kama hajiuzulu tutaleta hoja ya kutokuwa na imani naye ili kuiwajibisha Serikali.

SPIKA: Mheshimiwa Mnyika pokea taarifa ya Mheshimiwa Innocent.

T A A R I F A

MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA – NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mnyika tunamsikiliza lakini ukiangalia…

SPIKA: Mheshimiwa Mnyika bado dakika zako, hii ni kengele ya kwanza eeh, endelea.

MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA – NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, ukiangalia hoja anayojenga Mheshimiwa Mnyika anai-deduct kutoka kwenye kuoza kwa korosho. Taarifa tumempa kwamba hakuna korosho iliyooza kwa hiyo kwa sababu ana-deduct hoja yake kutoka… (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA – NAIBU WAZIRI WA KILIMO: kwenye kuoza kwa korosho na si kweli, hoja yake haipo-valid ni void. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nilitaka nimpe taarifa, una-derive hoja yako kutoka kwenye kuoza kwa korosho lakini hakuna korosho ambayo imeoza.

SPIKA: Ahsante sana, wanasemea neno kuoza, Mheshimiwa Mnyika unapokea hiyo taarifa? Bado dakika zako mbii.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Hivi mtu akileta korosho yenye kiwango halafu hiyo korosho ikawekwa kwenye maghala ikaharibika ikawa chini ya kiwango, anarudishiwa amefanya nini?

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, naomba niendelee. Hoja yangu siyo ishu ya kuoza peke yake na kuna taarifa hapa…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mbona taarifa za huku unazikataa, taarifa za huku unazikubali? Hiyo ni double standard, mkaribishe tu huyu anatoka kwenye eneo la korosho aseme kama korosho haziozi au la atoe ufafanuzi. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. JOHN J. MNYIKA: naomba umpe taarifa basi, pokea taarifa hiyo kuhusu korosho kuoza kutoka kusini.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, naomba kuendelea. Hoja siyo jambo la korosho tu kuwa chini ya kiwango ambayo tunakubaliana na kwamba CAG akachunguze tasnia nzima ya korosho…

SPIKA: Mheshimiwa Mnyika…

MHE. JOHN J. MNYIKA: …lakini hoja nyingine hapa kadhaa…

SPIKA: Subiri Mheshimiwa Mnyika. Nilikuwa nalinda dakika zako, nakulinda wewe mwenyewe nikiamini una cha kusema. Nilifanya hivyo kwa sababu huyo unayetaka atoe taarifa amepata dakika zake saba za kuzungumza hapa, unanielewa eeh?

Eeh subiri, amepata dakika zake za kuzungumza. Kuna kuhusu utaratibu huku sijui upande gani, Mheshimiwa Naibu Waziri.

KUHUSU UTARATIBU

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwa Kanuni ya 64(1) (a); kuhusu kudanganya. Kwanza mimi ni mkulima wa korosho, yeye si mkulima wa korosho. Korosho ina utaratibu wake, ina muda wake maalum unaofikiwa na kuitwa kwamba imesinyaa, tulisema na tukaiweka katika utaratibu ukaitwa unyaufu. Katika muda huo ambao tumezikusanya korosho mpaka hii leo, hamna uwezekano wa kusema korosho imeoza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, narudia tena, mimi ni mkulima wa korosho, ninazo kwangu korosho na ninazo za kwangu mwenyewe pia vilevie korosho. Kwa hiyo suala la kusema kwamba korosho imeoza, huo ni uongo mkubwa na aache kupotosha na urongo wake huo. (Makofi)

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, kuhusu utaratibu.

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika…

SPIKA: Mheshimiwa Selasini nimekuona Chief Whip.

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, kuhusu utaratibu.

SPIKA: Mheshimiwa Mwambe ukishamuona Mheshimiwa Selasini amesimama au unashinda naye? Kaa Mheshimiwa Selasini aongee Mheshimiwa Mwambe. (Kicheko)

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika…

SPIKA: Mheshimiwa Selasini ni bosi wako bwana anaposimama mnatakiwa kuheshimiana kidogo, ahsante Mwambe.

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, tumemuomba.

Mheshimiwa Spika, tusipotoshe hili jambo, tukiwa sisi kwenye kamati tumeletewa malalamiko, wanasema kwamba wanaomba kujenga maghala ya kuhifadhia korosho kwa sababu storage facilities zetu ni transit. Kwa hiyo, korosho ukiweka muda mrefu kwenye hayo maghala zinaharibika, they go bad. Na kwa kuthibitisha hili SIDO Mtwara waliamua kutunza korosho zilizobanguliwa ili wapate ile room temperature (AC) walikuwa wanawasha, wamewatoa wafanyakazi wote wakawa wanawasha AC, ninaweza kuthibitisha ndani ya hili Bunge na tulipowaambia wakazitoa. Wanasema wanajenga maghala ya kuhifadhia korosho zilizobanguliwa Dar es salaam, Kurasini, kazi hiyo haijafanyika. Ndiyo maana tunaomba CAG aende akakague aje atueleze hapa. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Mwambe tumeshakusikia. Issue ni kwamba anasema waliambiwa kwenye Kamati kwamba ukiweka korosho kwa muda mrefu katika maghala zinaweza kuharibika, kitu chochote ukikiweka katika muda mrefu kitaharibika. Anachosema ni kwamba katika muda huu tangu zimechukuliwa mpaka sasa hazijaharibika, katika muda huu, lakini katika muda mrefu huo mnaosema inaweza hilo likatokea.

Na kinachozungumzwa hapa ni terminology tu ya neno kuoza, kwa hiyo msemaji anaweza akarekebisha neno lake akaweka sawa na kwa sababu hakuna zilizooza, kwa hiyo maana yake hoja ya Mnyika imekufa, ndiyo wanachosema wenzako. Nakurudishia umalizie maana bado dakika moja tu hapo. (Makofi)

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, kama hilo neno linawakera sana naliondoa lakini hoja yangu mimi si suala la kuoza peke yake; nimesema kuhusu mkataba wa Indo Power, kuhusu Serikali kukosa mapato nje (forex), kukosa mapato kwa ujumla wake ambayo tungeyapata kwenye mauzo ya korosho. Mambo ni mengi kweli kweli ambayo kwa pamoja yanataka kama CAG hamumruhusu kuchunguza basi Kamati Teule ya Bunge iundwe iende kuchunguza na hatua zichukuliwe. Wakati tukiendelea na uchunguzi wa Bunge, Serikali iwajibike Waziri na Mawaziri wajiuzulu na kama hawajiuzulu tutaleta hoja ya kutokuwa na imani na Serikali, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, katika majumuisho naomba majibu ya Serikali kuhusu masuala yafuatayo mahsusi ya Jimbo la Kibamba.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja, Kata ya Goba kuna shida ya maji mitaa yote. DAWASCO/DAWASA waliahidi kwamba maji yatapatikana baada ya ujenzi wa matenki ya maji Sabasaba na Changanyikeni. Hata hivyo, ukweli ni kuwa maji hayajapatikana kwa wakati kwa kuwa mabomba ya maji hayajaanza kabisa kusambazwa. Wizara ieleze lini mabomba yataanza kusambazwa kwenye Kata nzima ya Goba.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Msigani ina mitaa mitano; mitaa ya Msingwa, Malambamawili, Temboni, Msigani na kwa Yusuph yapo mabomba ambayo yalijengwa awamu ya kwanza (maarufu kama mabomba ya Mchina) na ya sasa (maarufu kama mabomba ya Kihindi) ambayo mpaka sasa hayatoi maji. Ni lini yataanza kutoa maji? Aidha, yapo maeneo katika mitaa hiyo ambayo hakuna kabisa mabomba. Ni lini maeneo hayo mabomba yatasambazwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Saranga, mitaa saba ina mabomba ya maji lakini si maeneo yote maji yanatoka. Hivyo, DAWASCO ifuatilie katika maeneo ambayo maji hayatoki. Hata hivyo katika kata hiyo kuna mitaa miwili ya Saranga na Ukombozi ambayo hayana kabisa mabomba ya maji. Wizara ieleze ni hatua gani ya haraka zinachukuliwa kuhakikisha kwamba mabomba ya maji yanasambazwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Kibamba miradi ya maji inasuasua, kuna maeneo mabomba yamerundikwa bila kuchimbiwa kwa muda mrefu na mitaro imeachwa wazi. Hivyo, hatua zichukuliwe kuhakikisha mabomba hayo yanachimbwa na pia maeneo ambayo hayana mabomba nayo mabomba yatandazwe kwa haraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Mbezi mitaa ya Msakwi na Msakwi Kusini hali ya maji ni mbaya. Yapo mabomba ambayo kwa muda mrefu hayatoi maji. Aidha, mitaa ya Mpiji Magohe na Msumi haina kabisa mabomba ya maji hivyo Wizara ieleze ni lini mabomba ya maji yatasambazwa katika maeneo hayo. Wizara ihakikishe fedha zilizopaswa kupelekwa kwa Manispaa ya Ubungo zinafikishwa kwa haraka kupunguza ukubwa wa tatizo. Lakini izingatie kuwa misaada hiyo hailingani na ukubwa wa mahitaji na kasi ya ukuaji wa maenezo ya wakazi katika mitaa hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kunajitokeza tatizo katika eneo linalojengwa barabara ya lami kutoka Mbezi kwenda Goba ambapo TANROADS walijenga juu ya mabomba bila tahadhari hivyo mabomba yamepasuka wananchi kukosa maji na miundombinu kuharibika hasa karibu na Mazulu Kanisani na Njiapanda ya Goba na Makabe. Hali hiyo iko pia Mbezi mwisho round about.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Kwembe ipo mitaa ambayo mabomba yamewekwa lakini mpaka sasa maji hayatoki, ni lini maeneo hayo yatatoka maji? Aidha, limejitokeza tatizo katika maeneo hayo la mkandarasi kutoshindilia vya kutosha na kuweka kifusi mwaka baada ya kuchimba mitaro na kuwekwa mabomba. Matokeo yake ni kuwa mvua zimenyesha na udongo kuondoka na mabomba kubaki wazi na miundombinu ya barabara kuharibika. Kabla ya wakandarasi kumaliziwa malipo yao watakiwe kwenda kurekebisha miundombinu hiyo. Aidha, kuna mitaa kwenye kata hiyo ambayo haina kabisa mabomba, ni lini yatasambazwa? Kwa ujumla kuchukua hatua kamili DAWASCO ikutane.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa dharura na madiwani na wenyeviti wa mitaa na watendaji wa Jimbo la Kibamba mapema mwezi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, upatikanaji wa maji katika eneo linalohudumiwa na Ruvu Chini si wa uhakika pamoja na uwekezaji mkubwa uliofanyika kwenye mitambo ya Ruvu Chini. Hali ni tete zaidi wakati wa ukame ikilinganisha na kipindi cha mvua. Hali itakuwa mbaya zaidi kutokana na mabadiliko ya tabianchi (climate change). Hivyo, ujenzi wa Bwawa la Kidunda unapaswa kuharakishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya Waziri pamoja na taarifa ya Kamati zinajenga matumaini hewa kwamba ujenzi unakwenda kuanza. Hata hivyo, ukweli ni kuwa randama ya Wizara inaonesha kuwa ili mradi ukamilike kinahitajika kiasi cha dola za Marekani milioni 215. Taarifa nilizonazo ni kuwa mpaka sasa Serikali imeshindwa makubaliano na masharti ya kupata mkopo kuhusu mradi huo. Hivyo Wizara ieleze katika majumuisho ni namna gani fedha za mradi huo zitapatikana kwa kiasi cha kutosha katika mwaka huu wa fedha na ni lini mradi huo utakamilika? Wizara izingatie kuwa miaka nane iliyopita tumehoji kuhusu mradi huo na Wizara imekuwa ikitoa majibu ya kutoa matumaini bila utekelezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, juu ya mchakato unaoendelea wa kuunganisha DAWASA na DAWASCO, naomba Wizara katika majumuisho itoe maelezo ya kina juu ya mchakato huo. Aidha, kama Mbunge wa Jiji la Dar es Salaam naomba kupatiwa nakala ya taarifa zilizoombwa na Kamati kuhusu mchakato huo hasa kwa kuzingatia pia suala hilo linapaswa kuhusisha marekebisho ya sheria au kutungwa kwa sheria mpya ya kusimamia masuala ya maji katika Jiji la Dar es Salaam na maeneo ya jirani ya Mkoa wa Pwani yanayohudumiwa na mabomba ya Ruvu Juu na Chini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Bunge la Kumi kutokana na ukubwa wa matatizo ya maji nchini na haja ya Wabunge kupata majibu ya kina nilitoa hoja na Serikali ikakubali kwamba kwenye kila Mkutano wa Bunge Serikali ilikuwa ikiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa miradi ya maji. Kwa hali ilivyo kwa sasa ya wastani wa upatikanaji wa maji vijijini wa asilimia 56 tu kwa vijiji na asilimia 69 kwa mijini pamoja na hoja ya nyongeza ya fedha, upo umuhimu wa Bunge hili la Kumi na Moja Serikali kuweka utaratibu wa Wizara ya Maji kutoa taarifa ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika kila Mkutano wa Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, fursa ya maswali ya Wabunge pekee haitoshi ndiyo maana kwenye Mkutano wa Bunge, Wabunge husimama kutaka maswali ya nyongeza bila kupata nafasi. Katika kujibu michango ya Wabunge, Serikali ieleze itakavyotekeleza utaratibu huo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Toka jana nimekuwa nikisikiliza michango ya Waheshimiwa Wabunge wenzangu pamoja na leo na nimepitia taarifa ya Kamati na nimetafakari katika miaka niliyokaa Bungeni, nimekuja kugundua kwamba kwa miaka nane kwa kweli Bunge hili linajadili mambo yale yale, yaani ukiwa umeingia Bungeni leo tu au jana ukawa hujasikiliza Bunge huko nyuma, unaweza kufikiri sasa kuna Chama na Serikali mpya katika Bunge hili inajaribu kurekebisha mambo ya zamani. Kumbe ni chama kile kile na Serikali ile ile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sentensi moja ambayo iko bayana katika haya ni kwamba ninyi mmeshindwa kutekeleza na kutimiza matakwa ya wananchi kwenye masuala ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kabla sijaendelea mbele nisisitize ninachoendelea kusisitiza kwamba tiba ya kudumu ya haya matatizo tuliyonayo ni wananchi wa Tanzania kuwaondoa Serikali ya CCM madarakani na kuweka Serikali nyingine katika utawala wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wewe utakuwa unakumbuka vizuri kwa sababu ulikuwa kwenye kiti hicho hicho wakati ukiwa Naibu Spika. Tarehe 4 Februari, 2013 nilipoleta hoja Bungeni hapa juu ya maji Dar es Saalam na maji vijijini na namna ambavyo Wabunge wa CCM wakati huo Mheshimiwa Rais akiwa ndani ya Bunge, akiwa Waziri wa Ujenzi naye akisikiliza mlivyoshabikia kwa pamoja kwamba mambo yapo kwenye mkondo sahihi, kila kitu kipo sawasawa, hoja hii iondolewe isijadiliwe, hatimaye maji yakasababisha vurugu kubwa sana hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa miaka mitatu au miwili na ushee, toka mwaka 2016 hadi 2017 na mpaka sasa mlinyamaza kimya kusema kuhusu maji, nikifikiri kwamba Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli kwa sababu alikuwa Mbunge anayajua vizuri matatizo haya ya maji na kwa sababu alikuja hapa Bungeni akaahidi kwamba ifikapo mwaka 2020 asilimia 95 ya wananchi mijini ikiwemo Dar es Salaam watakuwa na maji na asilimia 85 wa vijijini watakuwa na maji, nikafikiri kwamba kutakuwa na tofauti. Nimekuja kugundua kwamba Mheshimiwa Magufuli ni yule yule na CCM ni ile ile, mambo ni yale yale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa huwa tunajengewa matumaini sana. Mwaka 2006, mwaka 2007 katika Bunge la Bajeti Waheshimwia Wabunge walisema mambo haya haya ambayo wanasema sasa tukajengewa matumaini wakati wa majumuisho ya Serikali kwamba kutakuwa na mabadiliko. Safari hii mmekuja na mkakati huo huo; na sasa kuna debate ya tozo ya mafuta ya shilingi 50 ili ikishafika hatua ya majumuisho Serikali iki-coincide kutoa tozo ya shilingi 50 watu walainike wote, bajeti ipite, halafu mambo yaendelee kuwa yale yale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kamati inasema mpaka mwezi Machi Serikali imetoa asilimia 22 tu ya pesa za maendeleo. Hizi asilimia 22 za pesa maendeleo ni katika bajeti ya maji ambayo imepunguzwa badala ya kuingezwa kutoka bajeti iliyotangulia. Halafu kwenye umwagiliaji haIi ni mbaya zaidi asiliamia 12 na kati ya hiyo 12 pesa za ndani ni 0.8. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika suala la sukari ulisimama ukataka kuonesha ukali. Maji katika maisha ya wananchi ni zaidi ya sukari kwa sababu ukikosa sukari unaweza ukanywa chai bila sukari. Katika suala la mafuta umeonesha ukali, maji ni zaidi ya mafuta, kwa sababu ukikosa mafuta unaweza ukapika bila ya mafuta. Ila ukikosa maji huwezi kunywa bia, ukikosa maji huwezi..., ni uhai. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, onesha ukali wako katika hili. Na mimi nakuomba ukubali, kwa sababu tumeishauri Serikali vya kutosha sana, lakini haisikii. Sasa nani wakati Bunge kutumia mamlaka yake ya Kikatiba kuisimamia Serikali. Mamlaka hayo yanaanza kwa kukubaliana kwamba hii bajeti ya Wizara ya Maji tusiipitishe sasa. Tukubaliane kwamba hii bajeti ya Wizara ya Maji tusiipitishe sasa. Sasa najua kwamba Waheshimiwa Wabunge wenzangu wana shauku sana ya kuchangia.

Mheshimiwa Spika, ingekuwa siyo shauku ya Waheshimiwa Wabunge wenzangu, ningesema nasimama sasa hivi kwa mujibu wa Kanuni ya 69(1) ambayo inaruhusu Mbunge kusimama wakati wowote kutoa hoja ya kwamba mjadala uahirishwe. Ningeweza kabisa kusema kwamba mjadala uahirishwe, sasa ni mwezi Mei na kuna bajeti zinajadiliwa mpaka mwanzoni mwa mwezi Juni, tungesema mjadala uahirishwe mpaka mwishoni mwa Mei ili Serikali katika makusanyo yake ya mwezi huu wa Serikali iingize pesa katika Wizara ya Maji, tuvuke kutoka hii asilimia 22, tufike juu ya asilimia 22.

Mheshimiwa Spika, tuna uwezo kabisa wa kufanya hivyo kwa kanuni za Bunge na tuna haki hiyo. Kwa sababu Waheshimwia Wabunge wenzangu wana shauku ya kuendelea kuchangia, bado tunayo nafasi hiyo.

Mheshimiwa Spika, ruhusu Wabunge wengine waendelee kuchangia lakini wakishamaliza kuchangia kesho, Serikali isiruhusiwe kuhitimisha, mjadala uahirishwe na nipewe nafasi ya kutoa hoja hiyo kesho, mjadala uahirishwe mpaka tarehe ngapi kwa mujibu wa kanuni.

T A A R I F A . . .

MHE. JOHN J. MNYIKA. Mheshimiwa Spika, nilisema awali kwamba ni mbinu tu ya kukwepesha hii bajeti ipite.

Mheshimiwa Spika, tulishapitisha bajeti hii ambayo Serikali imetoa asilimia 22. Serikali ikishapitisha Bajeti ni wajibu wa Serikali kutoa pesa. Nasema tuahirishe mjadala ili Serikali ilazimishwe kutoa hizo pesa. Sasa masuala ya tozo ni masuala ya kwamba tunakwendaje mbele? Tukifika huko napo hata katika tozo, kuna tozo zinatozwa na bado pesa nyingine haziendi vilevile. Kama ilivyo kwenye maji, kama ilivyo kwenye umeme, kwenye REA, hiyo ni jambo lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee, Waheshimiwa Wabunge mbalimbali wameeleza na kwa miaka kadhaa tumeeleza kuhusu ufisadi katika sekta ya maji na miradi ya ambayo kimsingi ni miradi ambayo imejengwa lakini maji hayatoki na matumizi mabaya ya fedha katika masuala ya miradi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hali hii imeendelea, ipo katika sura nyingi hata mtu akisoma kitabu hiki cha Mheshimiwa Waziri, ukiangalia tu uchimbaji wa visima vya DCCA kuanzia ukurasa wa 267 utaona jinsi ambavyo Mheshimiwa Waziri anavyojipendelea katika Mkoa wa Katavi na katika Jimbo lake. Mimi nazungumzia kipengele cha matumizi mabaya ya fedha za miradi ya maji katika maeneo mbalimbali ya nchini na miradi ya maji kutokufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, katika mazingira ya kero nyingi za ufisadi wa namna hii unaozungumzwa, nitaomba nafasi na ninaomba nitoe notice kabisa kwa mujibu wa Kanuni ya 120 ya Kanuni za Bunge 2A kwamba baada ya mjadala huu kukamilika, nipewe nafasi ya kutoa hoja ya kuundwa kwa Kamati teule ya kwenda kuchunguza masuala ya ufisadi na miradi mibovu katika masula ya maji maeneo yote nchini na katika maeneo mbalimbali nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wewe umeonesha kutaka kuunda Kamati za kiuchunguzi, umeunda Kamati ya Gesi, umeunda Kamati ya Tanzanite, umeunda Kamati ya Almasi na umeunda Kamati mbalimbali, lakini hizi Kamati zako ambazo taarifa zake hazijadiliwi humu Bungeni na Wabunge wote, sasa katika hili kwa sababu ya uzito wake iiundwe Kamati Teule ili ikachunguze na taarifa iletwe Bungeni ijadiliwe na hatua zichukuliwe. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora aya ya 37(xii), madai ya malimbikizo ya mishahara ya watumishi wa Umma 34,346 yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 79 inaonyesha hayajalipwa mpaka sasa. Hata ya shilingi bilioni 29 ambayo yamehakikiwa nayo hayajalipwa mpaka sasa. Serikali iache kutumia kisingizio cha uhakiki mwingine wa Wizara ya Fedha kuendelea kuchelewa kuwalipa wafanyakazi madai yao ya mishahara. Hivyo katika majumuisho, Mheshimiwa Waziri alieleze Bunge, ni lini hasa madai hayo ya wafanyakazi yatalipwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, katika aya ya 51 na 78 zinazohusu Bodi ya mishahara na masilahi katika utumishi wa Umma, zinaonesha kwamba Serikali haijafanya maamuzi ya kupandisha mishahara ya watumishi wa Umma. Bado Serikali inajificha katika kivuli cha kufanya utafiti wa hali ya maslahi ya watumishi wa Umma na kuandaa taarifa za gharama za maisha, kukwepa kupandisha mishahara ya watumishi wa Umma. Visingizio kama hivi vimetolewa katika hotuba za 2016/ 2017, 2017/2018 na 2018/2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo ni vyema ripoti ya utafiti iliyotajwa kwenye aya ya 51 na taarifa mbili za gharama za maisha ziwasilishwe Bungeni na Bunge katika majumuisho ya mjadala wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora itangazwe kwamba mishahara ya watumishi wa Umma itaongezwa katika bajeti hii ya mwaka wa fedha 2019/2020. Pia ili kukabiliana na gharama za maisha, ni vyema Serikali ikawapunguzia mzigo wafanyakazi wote wa Sekta ya Umma na Binafsi kwa kupunguza kiwango cha kodi ya mapato kwa wafanyakazi (PAYE) kama ilivyowaahidi wafanyakazi kwa nyakati mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kuhusu agizo la Serikali la watumishi wa Umma wa Wizara na Taasisi zake kuhamia Dodoma. Kuna umuhimu kwa Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na wakala zilizo chini yake kufanya utafiti juu ya athari za maamuzi hayo yaliyofanyika bila maandalizi ya kutosha kwa maisha ya watumishi wa Umma. Watumishi wa Umma walipokuwa Dar es Salaam wapo ambao wenzi wao wanafanya kazi katika sekta binafsi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Dodoma Sekta Binafsi haijapanuka kwa kiwango cha kuwezesha wenzi wa wafanyakazi hao nao kuweza kuhamia Dodoma kwa haraka haraka. Matokeo yake ni kuwa, kuna familia nyingi zimetenganishwa hali ambayo italeta athari za muda mrefu na kuathiri utendaji wao kwa kipindi cha muda mfupi. Aidha, kwa wafanyakazi wa kada ya chini na kati, hali hii ya kuwa na Miji miwili; Dar es Salaam na Dodoma kwa mishahara yao midogo, imeleta madhara ya kiuchumi kwa watumishi wa Umma.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, Wizara ya Mifugo na Uvuvi inapaswa kushirikiana na Wizara ya Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuhakikisha kwamba mipango kabambe (master plan) za kila Jiji, Manispaa na Wilaya zinalenga maeneo ambayo ufugaji na uvuvi unaweza kufanyika ili kuepusha migogoro na kuhakikisha uendelevu. Katika muktadha huo niombe katika majumuisho Wizara ieleze iwapo ilipewa nakala ya master plan ya Jiji la Dar es Salam na iwapo imeshatoa maoni ya kuboresha master plan ya Jiji mintarafu masuala na mipango ya mifugo na uvuvi.

Mheshimiwa Spika, Jiji la Dar es Salam ni mtaji mkuu wa uvuvi kwa upande wa nchi yetu ya Tanzania, hata hivyo yamekuwepo malalamiko ya kuletwa kwa samaki wa sato na aina nyingine kutoka nje ya nchi ambao wamekuwa chini ya kiwango. Aidha, hata kwa samaki ambao wamekuwa wakifugwa kwenye mabwawa wamekuwa wakipewa muda wa wengi na kuwa baadhi ya kuku aina ya broilers. Hivyo, Wizara iwe na mikakati thabiti ya kudhibiti ubora wa samaki kutoka nje ya nchi na ubora wa samaki wanaofugwa katika mabwawa.

Mheshimiwa Spika, katika hotuba ya Waziri yametolewa maelezo kuhusu utatuzi wa migogoro baina ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi ambayo yanaonyesha bado Serikali haijawezesha utatuzi kamili na endelevu wa migogoro hiyo. Hivyo, katika majumuisho ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi iwasilishe Bungeni taarifa juu ya utatuzi wa migogoro yenye kuorodhesha migogoro iliyopo na kwa maeneo ambayo migogoro haijatatuliwa bado iwekewe road map ya utatuzi wa migogoro hiyo ambayo pamoja na mambo mengine itaeleza ni lini migogoro hiyo ikatatuliwa. Pia Wizara ya Fedha kwa kuwa suala hili ni mtambuka ieleze ni lini itaongeza fedha kwa Wizara zote zenye mipango ya upimaji wa ardhi ili kuwezesha ardhi ya nchi yetu kupimwa na kupangwa kwa ajili ya maendeleo endelevu ikiwemo ya mifugo na uvuvi nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa upande mwingine naomba kupitia mchango huu Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) itenge eneo katika ardhi yake ya Mkoa wa Pwani kwa ajili ya vijana wa Jimbo la Kibamba kulitumia kwa ajili ya ufugaji ikiwa ni sehemu ya mchango wake katika kuongeza ajira kwa vijana.

Mheshimiwa Spika, suala lingine muhimu kupewa kipaumbele ni nafasi ya Bodi ya Maziwa katika kuhamasisha unywaji wa maziwa ikiwemo kwa wanafunzi wa shule mbalimbali. Hivyo, naomba Bodi itekeleze kampeni maalum katika Shule za umma za msingi na sekondari katika Jimbo la Kibamba ya kuhamasisha wanafunzi kunywa maziwa kwa kushirikiana na wasindikaji mbalimbali wa maziwa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, mradi wa umeme Kinyerezi, Dar es Salaam- Arusha kupitia Kibaha- Chalinze, wakazi wa Kata ya Kinyerezi kwenye mitaa ya Kiboga na Kifuru walifanyiwa tathmini kwa ajili ya kupisha mradi wa njia ya umeme tangu mwezi Septemba, 2016, lakini mpaka sasa mwaka wa tatu wamesimamisha shughuli za maendeleo na Serikali hawaelezi chochote. Katika majumuisho yake Mheshimiwa Wizara ieleze ni lini hasa wananchi hao watalipwa fidia?

Mheshimiwa Spika, pia Wizara ieleze katika Kata za Jimbo la Kibamba za Kwambe, Mbezi, Msigani, Goba, Saranga na Kibamba yapo maeneo mpaka sasa umeme haujafika. Ni lini TANESCO itahakikisha maeneo yote yanafikishiwa umeme? Katika kata hizo kuna kawaida pia ya umeme kukatikakatika na kupungua nguvu (low voltage). Serikali katika swali langu Bungeni iliahidi ufumbuzi lakini mpaka sasa tatizo hilo limeendelea.
Muswada wa Sheria ya Mamlaka ya Nchi kuhusiana na Umiliki wa Maliasili wa Mwaka 2017.
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Asubuhi ulianza kutuongoza na Dua; Ewe Mwenyezi Mungu Mtukufu, Muumba Mbingu na Dunia, umeweka katika Dunia Serikali za wanadamu na Mabunge ya Mataifa ili haki yako itendeke. Ni kwa bahati mbaya sana tunasali tunataja jina la Mungu kwamba haki itendeke lakini haki haitendeki kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunalitaja jina la Mungu, huku haki haitendeki, maana yake tunalitaja bure jina la Mungu na tunatenda dhambi. Siku chache zilizopita tumetoka kwenye mwezi Mtukufu wa Ramadhani, Mwezi wa toba, lakini badala ya kutubu, mnarudia makosa yale yale ya kulitaja bure jina la Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwenyezi Mungu ameiumba nchi hii ikiwa na rasilimali nyingi sana. Ukiitazama ile nembo ya Taifa pale, unaweza kuona rasilimali moja baada ya nyingine zikiwakilishwa na rangi mbalimbali na kauli mbiu ya Taifa letu ikiwa ni Uhuru na Umoja lakini bahati mbaya wenzetu ninyi wa CCM, hamna uhuru kwenye Chama chenu na matokeo yake mmesababisha Bunge halina umoja kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, dhambi hii ya kulitaja bure jina la Mungu maana yake ni kwamba ni wazi inaambatana na matumizi mabaya ya rasilimali ambazo Mwenyezi Mungu amejalia Taifa letu. Kwa bahati mbaya, badala ya kurekebisha hali hiyo kwa kuleta sheria bora na kufikiria kwa muda mrefu tukae tuzijadili kwa umakini, mmeamua kutenda dhambi ile ile ya kuleta Miswada kwa Hati ya Dharura; miwili ijadiliwe kwa siku moja na matokeo yake hatutafanya kazi ya maana inayotajwa kwenye sala hii. Hii ni dhambi mbele ya Mwenyezi Mungu. (Makofi)



Mheshimiwa Naibu Spika, leo ulituambia tukipita hapa, tuwe tunainama, maana mjadala huu umeibuka kutokana na report ya Rais ya masuala ya Makinikia kuhusu dhahabu na pale kuna siwa inayofanana kidogo na dhahabu, lakini siyo dhahabu, kwa maneno mengine inawezekana ni sehemu ya makinikia.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hali ya mjadala tulionao, ilipaswa kabla hatujajadili Miswada hii, Bunge liletewe report zote mbili za Rais juu ya makinikia tuzijadili kwa kina, tuielekeze Serikali ikafanye nini, Serikali ndiyo ilete Miswada inayofikiri miaka 50 ijayo, inayofikiri miaka 500 ijayo inayofikiri mbele sana juu ya mustakabali wa Taifa letu, lakini ninyi mmeleta Muswada wa kufikiria miaka mitano tu ya kuelekea uchaguzi. Kuna mtu aliwahi kusema, Politicians think about election; Leaders, think about generation. Ni bahati mbaya sana Mheshimiwa Rais ameamua kuwa mwanasiasa badala ya kiongozi, anafikiria uchaguzi.

KUHUSU UTARATIBU...

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Juu ya Muswada wa Sheria ya kuhusiana na Umiliki wa Maliasili, nitaomba muda wangu ambao umeuchukua, ulindwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Sheria hii imetoa mamlaka makubwa sana kwa Rais kuhusiana na masuala ya umiliki wa rasilimali za nchi. Sheria hii imedhihirisha ni kwa nini sisi Wapinzani na wananchi tulioungana pamoja kutaka rasimu ya Warioba ili kupunguza mamlaka ya Rais kwenye masuala mbalimbali.

KUHUSU UTARATIBU...

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Ukiangalia ile Nembo ya Taifa kuna rasilimali yetu mojawapo, zile pembe za ndovu zina rangi nyeupe. Ndiyo maana nasema ninyi, samahani sana, kuna miongoni mwenu mnaabudu miungu badala ya Mungu. Mimi nawashauri mtubu, msafishike muwe weupe kama theluji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. (Makofi)

Kuhusu Muswada wa Sheria ya Mapitio na Majadiliano kuhusu Masharti katika Mikataba ya Maliasili kwa nchi ya mwaka 2017, sisi tumedai mikataba mara nyingi sana, tumedai mikataba muda mrefu sana. Sasa mmeleta sheria ya kuleta mikataba lakini sheria hiyo mmeleta kwanza mmetumia neno “may” kwa maana ni hiari lakini pili mnaileta mikataba siyo kwa majadiliano kwa mapitio ya moja kwa moja kwa sababu mikataba hii hamjaweka kifungu chenye
kuonesha kwamba Bunge linapaswa kuiridhia mikataba hiyo. Kwa maneno mengine kifungu hiki kitafanya mambo yawe yale yale kama ya miaka 50 iliyopita na Taifa litakuwa pale pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mwaka 2008 kwenye Maazimio ya Bunge kuhusu Richmond kulikuwa na Azimio ambalo lilisema bayana toka mwaka 2008 kwamba kuanzia mwaka 2008 Kamati za Bunge za Kisekta na hili nililikumbushia wakati wa mjadala wa Escrow nilileta mapendekezo ya marekebisho, Kamati za Bunge za Kisekta ziwe zinapewa mikataba na Serikali kabla ya Serikali kwenda kuridhia mikataba husika. Hata hivyo, kwenye marekebisho ya sheria hii hamjaleta kifungu cha namna hiyo na kwa bahati mbaya mmetubana tusilete marekebisho, mmekataa marekebisho yetu asubuhi tulivyoyaleta, kwa hiyo mmeamua kabisa kutunga sheria hovyo hovyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, marekebisho yameletwa machache, mengi yamekataliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mazingira ya namna hii, namkumbuka Mzee wangu Dkt. Emmanuel Makaidi, kabla hajafariki tarehe 30 Machi, 2014 tukiwa kwenye Bunge la Katiba alinikabidhi Emma’s Encyclopedia Tanzania of National Records, aliweka records za toka mwaka 1497 mpaka mwaka 1995; za miaka 498 ambazo nyingine zimegusa masuala ya rasilimali nchi yetu inaelekea wapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Viongozi, kati ya mambo ambayo yalitokea katika Taifa letu ni Vita ya Majimaji ya mwaka 1905 mpaka 1907 wananchi wakikataa kuporwa rasilimali zao. Kama ninyi mnasema mmeanzisha vita ya kiuchumi basi ni wakati sasa wa kuwa na Vita ya Majimaji ya kuwaondoa ninyi madarakani. (Makofi)

Kwa sababu katika hali iliyopo Watanzania hawawezi tena kuitegemea CCM hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tofauti na vita ya silaha, hii itakuwa ni vita ya kisiasa na kiuchumi, wananchi wakihamasishwa kutumia silaha yao kuu (sanduku la kura) kuiondoa CCM madarakani mwaka 2019 na mwaka 2020. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu mmeonesha wazi hamtaki kutuletea Katiba Mpya, mmeikataa Rasimu ya Warioba iliyotaka maadili, iliyotaka uadilifu, iliyotaka wananchi wanufaike na rasilimali, mmekataa na hamtaki kuwa na Katiba Mpya.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa maneno ambayo yameandikwa katika Biblia ya Mfalme Nebukadneza ambaye yeye aliamua kuisifu miungu iliyotengenezwa kwa fedha, dhahabu, shaba, chuma, miti na mawe. Miungu ambayo haioni wala haisikii, haijui lolote lakini Mungu ambaye uhai wako uko mkononi mwake na njia zako zi wazi mbele yako hukumheshimu basi Mungu ametuma mkono uandike maandishi haya, maandishi yenyewe ni haya; “Mene Mene Tekeli Peresi” na hii ndiyo maana yake. Mene maana yake Mungu amehesabu siku za ufalme wako na kuukomesha. Tekeli maana yake wewe umepimwa katika mizani nawe ukaonekana huna uzito wowote. Peresi maana yake ufalme wako umegawanywa kati ya Wamedi na Waajemi.
Muswada wa Sheria ya Mapitio na Majadiliano kuhusu Masharti Hasi katika Mikataba ya Maliasili za Nchi wa Mwaka 2017.
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Asubuhi ulianza kutuongoza na Dua; Ewe Mwenyezi Mungu Mtukufu, Muumba Mbingu na Dunia, umeweka katika Dunia Serikali za wanadamu na Mabunge ya Mataifa ili haki yako itendeke. Ni kwa bahati mbaya sana tunasali tunataja jina la Mungu kwamba haki itendeke lakini haki haitendeki kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunalitaja jina la Mungu, huku haki haitendeki, maana yake tunalitaja bure jina la Mungu na tunatenda dhambi. Siku chache zilizopita tumetoka kwenye mwezi Mtukufu wa Ramadhani, Mwezi wa toba, lakini badala ya kutubu, mnarudia makosa yale yale ya kulitaja bure jina la Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwenyezi Mungu ameiumba nchi hii ikiwa na rasilimali nyingi sana. Ukiitazama ile nembo ya Taifa pale, unaweza kuona rasilimali moja baada ya nyingine zikiwakilishwa na rangi mbalimbali na kauli mbiu ya Taifa letu ikiwa ni Uhuru na Umoja lakini bahati mbaya wenzetu ninyi wa CCM, hamna uhuru kwenye Chama chenu na matokeo yake mmesababisha Bunge halina umoja kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, dhambi hii ya kulitaja bure jina la Mungu maana yake ni kwamba ni wazi inaambatana na matumizi mabaya ya rasilimali ambazo Mwenyezi Mungu amejalia Taifa letu. Kwa bahati mbaya, badala ya kurekebisha hali hiyo kwa kuleta sheria bora na kufikiria kwa muda mrefu tukae tuzijadili kwa umakini, mmeamua kutenda dhambi ile ile ya kuleta Miswada kwa Hati ya Dharura; miwili ijadiliwe kwa siku moja na matokeo yake hatutafanya kazi ya maana inayotajwa kwenye sala hii. Hii ni dhambi mbele ya Mwenyezi Mungu. (Makofi)



Mheshimiwa Naibu Spika, leo ulituambia tukipita hapa, tuwe tunainama, maana mjadala huu umeibuka kutokana na report ya Rais ya masuala ya Makinikia kuhusu dhahabu na pale kuna siwa inayofanana kidogo na dhahabu, lakini siyo dhahabu, kwa maneno mengine inawezekana ni sehemu ya makinikia.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hali ya mjadala tulionao, ilipaswa kabla hatujajadili Miswada hii, Bunge liletewe report zote mbili za Rais juu ya makinikia tuzijadili kwa kina, tuielekeze Serikali ikafanye nini, Serikali ndiyo ilete Miswada inayofikiri miaka 50 ijayo, inayofikiri miaka 500 ijayo inayofikiri mbele sana juu ya mustakabali wa Taifa letu, lakini ninyi mmeleta Muswada wa kufikiria miaka mitano tu ya kuelekea uchaguzi. Kuna mtu aliwahi kusema, Politicians think about election; Leaders, think about generation. Ni bahati mbaya sana Mheshimiwa Rais ameamua kuwa mwanasiasa badala ya kiongozi, anafikiria uchaguzi.

KUHUSU UTARATIBU...

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Juu ya Muswada wa Sheria ya kuhusiana na Umiliki wa Maliasili, nitaomba muda wangu ambao umeuchukua, ulindwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Sheria hii imetoa mamlaka makubwa sana kwa Rais kuhusiana na masuala ya umiliki wa rasilimali za nchi. Sheria hii imedhihirisha ni kwa nini sisi Wapinzani na wananchi tulioungana pamoja kutaka rasimu ya Warioba ili kupunguza mamlaka ya Rais kwenye masuala mbalimbali.

KUHUSU UTARATIBU...

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Ukiangalia ile Nembo ya Taifa kuna rasilimali yetu mojawapo, zile pembe za ndovu zina rangi nyeupe. Ndiyo maana nasema ninyi, samahani sana, kuna miongoni mwenu mnaabudu miungu badala ya Mungu. Mimi nawashauri mtubu, msafishike muwe weupe kama theluji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. (Makofi)

Kuhusu Muswada wa Sheria ya Mapitio na Majadiliano kuhusu Masharti katika Mikataba ya Maliasili kwa nchi ya mwaka 2017, sisi tumedai mikataba mara nyingi sana, tumedai mikataba muda mrefu sana. Sasa mmeleta sheria ya kuleta mikataba lakini sheria hiyo mmeleta kwanza mmetumia neno “may” kwa maana ni hiari lakini pili mnaileta mikataba siyo kwa majadiliano kwa mapitio ya moja kwa moja kwa sababu mikataba hii hamjaweka kifungu chenye
kuonesha kwamba Bunge linapaswa kuiridhia mikataba hiyo. Kwa maneno mengine kifungu hiki kitafanya mambo yawe yale yale kama ya miaka 50 iliyopita na Taifa litakuwa pale pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mwaka 2008 kwenye Maazimio ya Bunge kuhusu Richmond kulikuwa na Azimio ambalo lilisema bayana toka mwaka 2008 kwamba kuanzia mwaka 2008 Kamati za Bunge za Kisekta na hili nililikumbushia wakati wa mjadala wa Escrow nilileta mapendekezo ya marekebisho, Kamati za Bunge za Kisekta ziwe zinapewa mikataba na Serikali kabla ya Serikali kwenda kuridhia mikataba husika. Hata hivyo, kwenye marekebisho ya sheria hii hamjaleta kifungu cha namna hiyo na kwa bahati mbaya mmetubana tusilete marekebisho, mmekataa marekebisho yetu asubuhi tulivyoyaleta, kwa hiyo mmeamua kabisa kutunga sheria hovyo hovyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, marekebisho yameletwa machache, mengi yamekataliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mazingira ya namna hii, namkumbuka Mzee wangu Dkt. Emmanuel Makaidi, kabla hajafariki tarehe 30 Machi, 2014 tukiwa kwenye Bunge la Katiba alinikabidhi Emma’s Encyclopedia Tanzania of National Records, aliweka records za toka mwaka 1497 mpaka mwaka 1995; za miaka 498 ambazo nyingine zimegusa masuala ya rasilimali nchi yetu inaelekea wapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Viongozi, kati ya mambo ambayo yalitokea katika Taifa letu ni Vita ya Majimaji ya mwaka 1905 mpaka 1907 wananchi wakikataa kuporwa rasilimali zao. Kama ninyi mnasema mmeanzisha vita ya kiuchumi basi ni wakati sasa wa kuwa na Vita ya Majimaji ya kuwaondoa ninyi madarakani. (Makofi)

Kwa sababu katika hali iliyopo Watanzania hawawezi tena kuitegemea CCM hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tofauti na vita ya silaha, hii itakuwa ni vita ya kisiasa na kiuchumi, wananchi wakihamasishwa kutumia silaha yao kuu (sanduku la kura) kuiondoa CCM madarakani mwaka 2019 na mwaka 2020. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu mmeonesha wazi hamtaki kutuletea Katiba Mpya, mmeikataa Rasimu ya Warioba iliyotaka maadili, iliyotaka uadilifu, iliyotaka wananchi wanufaike na rasilimali, mmekataa na hamtaki kuwa na Katiba Mpya.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa maneno ambayo yameandikwa katika Biblia ya Mfalme Nebukadneza ambaye yeye aliamua kuisifu miungu iliyotengenezwa kwa fedha, dhahabu, shaba, chuma, miti na mawe. Miungu ambayo haioni wala haisikii, haijui lolote lakini Mungu ambaye uhai wako uko mkononi mwake na njia zako zi wazi mbele yako hukumheshimu basi Mungu ametuma mkono uandike maandishi haya, maandishi yenyewe ni haya; “Mene Mene Tekeli Peresi” na hii ndiyo maana yake. Mene maana yake Mungu amehesabu siku za ufalme wako na kuukomesha. Tekeli maana yake wewe umepimwa katika mizani nawe ukaonekana huna uzito wowote. Peresi maana yake ufalme wako umegawanywa kati ya Wamedi na Waajemi.