Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Marwa Ryoba Chacha (27 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nichukue nafasi hii kwanza kabisa niwashukuru wananchi wa Jimbo la Serengeti kwa kunichagua kuwa Mbunge wa Jimbo la Serengeti, Mbunge wa kwanza wa CHADEMA tangu Serengeti iwe Wilaya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo machache nahitaji kuchangia kwenye Mpango. Jambo la kwanza ni kuhusu mapato ya Serikali. Nimekuwa Diwani tangu mwaka 2010 katika vipindi vilivyopita ambapo Mpango wa kwanza ulianza, kwa kweli hali ya makusanyo ya mapato ilikuwa ni hafifu sana. Tangu niwe Diwani nimewahi kuona fedha za maendeleo kwa miaka miwili tu na hata hiyo miaka miwili fedha za maendeleo zinazokuja ni 20% au 22%. Sasa kwa namna hii haya malengo ambayo tumejiwekea hayawezi kufikiwa hata siku moja. Kama hatuwezi kukusanya kiasi cha fedha zinazotosha kwa ajili ya maendeleo yetu ni ngumu sana, tutaendelea kudanganyana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuhusu elimu. Kwanza niwashukuru sana wazazi wa nchi hii kwa moyo wao mkubwa wa kujitoa kujenga shule na madarasa mbalimbali. Natambua Serikali ya CCM inajinasibu kwamba wao wamejenga shule kila kona lakini ukweli wajenzi wa madarasa, wanunuzi wa madawati ni wazazi. Kwa hiyo, nawashukuru sana wazazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipofanya mambo yafuatayo bado hatuta-improve chochote kwenye elimu, mimi kitaaluma ni Mwalimu. Ukiangalia shule za binafsi zinafanya vizuri sana kuliko shule za Serikali, tatizo ni nini? Walimu walewale wanaotoka Serikalini wakienda kule private wanafanya vizuri kwa nini wakiwa Serikalini wanafanya vibaya? Nilichogundua ni kwamba hakuna motivation kwa Walimu wa Serikali. Mwalimu mshahara uleule anaoupokea ndio huohuo afanyie mambo yote, haiwezekani! Lazima ifikie sehemu Serikali iwatazame Walimu, iwa-motivate Walimu mkiwaacha hivi wanakuwa demoralized hawawezi kufanya kazi kwa moyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine Serikali imesahau elimu ya chekechea. Huwezi uka-base kuanzia darasa la kwanza mpaka la saba bila kuangalia elimu ya awali. Elimu ya awali tumeiacha kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni issue ya maabara, wazazi wetu wamejitahidi wamejenga maabara kila shule lakini sasa vifaa vya maabara hamna. Siamini kama Serikali hii miaka mitano itaisha ikiwa imepeleka vifaa kwenye shule zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu la Serengeti ni Jimbo ambalo sehemu kubwa ya Hifadhi ya Serengeti ipo. Serengeti ni mbuga ambayo inaongoza kwa kuwa na watalii wengi kuliko mbuga zote za wanyama zilizopo katika nchi hii. Hata hivyo, ukija katika Wilaya ya Serengeti, siongelei Serengeti National Park, naongelea wanapoishi binadamu, Mheshimiwa Maghembe nakumbuka mwaka jana umekuja pale, maji ya kutumia ni shida. Kilichosababisha nikawapiga CCM kwa muda mrefu maji hakuna. Tangu 2009 limejengwa Bwawa la Manchila mpaka leo hakuna chujio, hakuna usambazaji wa maji. Kwa hiyo, maji yale yako kwenye Bwawa la Manchila lakini namna ya kuyachukua yale maji kutoka pale kuyasambaza hakuna. Ingawa feasibility study ilishafanyika tangu mwaka 2009 mpaka leo implementation hakuna.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeupitia Mpango huu kwenye ukurasa wa 14, nilitegemea kuona Bwawa la Manchila lakini sijaona. Sijui huu Mpango ume-base kwenye nini. Ukiangalia kwenye huu Mpango ukurasa ule wa 14 kuhusu maji naona wame-base Dar es Salaam sijafahamu miji mingine itakuwaje. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango unapokuja ku-wind up tuambie kwamba mji mingine kwenye Mpango kwa nini haikuingizwa? Nimeona mme-base zaidi Dar es Salaam, je, miji mingine ambayo iko nje ya Dar es Salaam mnafanyaje?
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni barabara, kwenye ukurasa wa 10 - 12 wa Mpango, nilikuwa najaribu kuangalia barabara za mikoa, karibia mikoa yote nchi nzima imeunganishwa kwa miundombinu ya barabara isipokuwa Mkoa wa Mara. Sasa nikasema ngoja niangalie Mkoa wangu wa Mara kama umeunganishwa na Mkoa wa Arusha. Mwalimu Nyerere kabla hajaondoka madarakani ali-propose ujenzi wa barabara ya Musoma – Butiama – Isenye - Nata - Mugumu - Tabora B na kadhalika lakini mpaka leo zimepita awamu nne barabara ile haijajengwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mimi sijawa Mbunge nilikuwa natazama Bunge nasikia kwamba zimetengwa billions of money kwa ajili ya ujenzi wa barabara ile, lakini hata mita moja ya lami haijawahi kujengwa. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango unapokuja ku-wind up kwenye huu Mpango, hebu tuambie watu wa Mkoa wa Mara barabara ya kutuunganisha na Mkoa wa Arusha itaanza kujengwa lini na itakamilika lini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ni vizuri tufahamu kwamba Mkoa wa Mara na hususan Wilaya ya Serengeti kitega uchumi kikubwa tulichonacho ni Serengeti National Park na Game Reserve zilizopo lakini watalii ili waje Serengeti ni lazima tuwe na miundombinu mizuri ya barabara. Kwa mfano, barabara ya kuanzia Tarime - Mugumu, barabara ya Musoma - Sirori Simba - Magange - Ring‟wani - Mugumu, ni vizuri zikawekwa lami ili watalii wanapokuja basi waweze ku-enjoy sasa hivi ni za vumbi hata hazieleweki. Haiwezekani mji wa Mugumu ukakua kwa haraka. Ndiyo maana hata Mheshimiwa Rais wakati anafanya kampeni mwaka jana Serengeti hakuja kwa sababu ya tatizo la barabara. Barabara za Serengeti ni mbovu kuliko zote nchi nzima. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wa Mipango unapokuja ku-wind up hebu tuambie watu wa Serengeti ni lini barabara ya Musoma – Makutano –Butiama - Nata, Isenye - Tabora B - Clains na Loliondo itakamilika?
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kilimo. Serengeti kwa sasa chochote tunacholima tunatengenezea tembo. Ukilima mahindi, mihogo, jua unasaidia tembo kushiba. Tukakubaliana wananchi wa Serengeti tulime tumbaku lakini tumbaku tunayoilima haina soko. Sasa tukimbilie wapi watu wa Serengeti? Nyie CCM mmepewa nafasi na wananchi wa nchi hii kwamba muiongoze nchi hii, lakini nawaambia kama msiposimamia rasilimali za nchi hii fursa zikaenda kila eneo mwaka 2020 mtapigwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana Mheshimiwa Profesa Maghembe jana umetupokea na kwa kweli wananchi wangu wa Serengeti wamekushukuru sana. Naomba utusaidie wananchi wa Serengeti, tumesaidia tembo kutoka 3000 – 7000, sasa hivi tembo wanatutesa, hebu tusaidie basi hata gari moja. Serengeti nzima unapokuja hatuna gari hata moja ambalo mmetupa ninyi Wizara, gari moja tulilonalo alitupa mwekezaji, Grumeti Game Reserve ambalo kwa sasa limechakaa haliwezi kufukuza tembo hebu tusaidieni magari kwa ajili ya kufukuzia tembo. Namshukuru Mungu kwamba tumepata zile ndege (drones) najua zitasaidia lakini haziwezi kusaidia kama hawana magari. Tusaidiane magari ili tuweze kufukuzana na hawa tembo. Sisi watu wa Serengeti tumeamua ku-conserve mazingira ya SENAPA na tumeamua tushirikiane na watu wa Serengeti National Park hebu basi na nyie tuoneni majirani wenu kwamba tunaumia na tembo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine ni kuhusu madeni ya Walimu. Nimekuwa Mwalimu Serikalini, nimekuwa Mwalimu private, Walimu wana shida kubwa sana. Sijaona kwenye Mpango kama kuna sehemu yoyote ambayo mmekusudia kuwalipa Walimu. Mheshimiwa Waziri utakapokuja ku-wind up utuambie ni lini mtalipa madeni ya Walimu.
MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umeisha.
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)
Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kupata nafasi hii ili niweze kuchangia Mpango huu wa Miaka Mitano na Mpango huu wa mwaka mmoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na elimu; ukiangalia Mpango huu umejikita zaidi kwenye mambo ya viwanda ili kubadilisha uchumi wa Taifa letu na maisha ya wananchi wa Tanzania. Nilikuwa najaribu kupitia mpango wote kwenye suala la elimu sijaona kama tumewekeza vya kutosha kwenye suala la elimu. Ninapoongelea suala la elimu, elimu inayoendana na viwanda tumewekeza kwa kiasi gani, Mpango huu umetaja kiwango gani, kiasi gani cha pesa ambazo tumeziwekeza kwenye vocational training.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukichukulia kwa mfano Mkoa wa Mara, ndiyo Mkoa ambao umetoa Kiongozi mkubwa katika Taifa hili, ambaye ndiye amesababisha na ninyi mmekaa kwenye hivyo viti vya mbele hapo, Mwalimu Nyerere. Mkoa wa Mara hauna Chuo cha VETA hata kimoja, hauna Chuo Kikuu hata kimoja, Mkoa wa Mara watu wake ni maskini kweli, hakuna kiwanda cha kueleweka, Mkoa wa Mara hauna hospitali ya Wilaya, iko shida kweli kweli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashindwa kuelewa vizuri kwamba nilivyokuwa nasikia Tanzania ya Magufuli itakuwa ni nchi ya viwanda nilitegemea nitaona humu fedha za kujenga viwanda, sijaona! Sasa sijui ni viwanda vya namna gani maana nilitegemea Mkoa wa Mara tutapata pale kiwanda, vijana wetu watapata ajira, kumbe hamna ni blah, blah tupu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, iko hivi mmesema elimu bure 20,000/= sekondari, lakini wanaojenga madarasa ni wazazi, hawa wananchi wetu maskini ndiyo wanajenga madarasa, ndiyo wanajenga shule, asilimia 90 ya shule zinaendeshwa na wazazi, wewe umesema umeondoa 20,000/=. Iko hivi, wewe chukua asilimia 90 jenga madarasa, peleka madawati, acha wazazi walipe hiyo 20,000/=, hapo tutakuelewa lakini kama wazazi ndiyo wajenge madarasa wapeleke madawati, msiwadanganye Watanzania Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi natokea Serengeti, ni Mbunge wa Jimbo la Serengeti, Jimbo ambalo kwa miaka mingi limeongozwa na CCM lakini hakuna hata kipisi kimoja cha lami, hata mita moja ya lami hakuna, hospitali ya Wilaya hakuna, Wilaya ya Serengeti kuna wengine hawajui iko Mkoa gani, iko Mkoa wa Mara! Nimeangalia hapa hata kwenye miundombinu ya barabara wanasema mikoa yote imeunganishwa na barabara ya lami, nikajiuliza hivi Mkoa wa Mara na Mkoa wa Arusha umeunganishwa na barabara ya lami, barabara aliyoiasisi Mwalimu Nyerere ya kupita Butiama kwenda Arusha mpaka leo, Mheshimiwa Magufuli alikuwa Waziri wa mambo ya barabara, hata mwaka jana hakuja kuomba kura Serengeti maana barabara haijapita pale, lakini walimpa kura nyingi kuliko Lowassa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, walimpa kura nyingi eeh! walimpa kura nyingi wanataka kumpima waone kwamba uaminifu walioufanya kwake je, yeye atakuwa mwaminifu kwao, asipokuwa mwaminifu 2020 hawampi, habari ndiyo hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilichokuwa nasema ukienda kiuhalisia kwenye vijiji vyetu, kuna upungufu wa madarasa na baada ya kusema elimu bure watoto wamefurika mashuleni, madarasa hakuna, madawati hakuna, sasa nawauliza CCM fedha za kujenga madarasa ziko wapi humu, kwenye Mpango wenu mbona hausemi, ziko wapi? Mheshimiwa Waziri unisaidie utakapokuja hapa uniambie hela za madarasa na madawati ziko wapi humu au ndiyo zile za Bunge bilioni sita zitatosha? (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda vijijini kwenye shule za msingi, ninakotoka Serengeti nimeenda Shule ya Msingi Gwikongo haina dawati hata moja, mimi nimeamua kama Mbunge niwe mfano nisaidie angalau tupate madawati machache kwenye shule ile, lakini wamekuweko Wabunge miaka na miaka, dawati hata moja hakuna, ni shule hiyo! Wilaya ambayo imeongozwa na CCM muda mrefu, dawati shule ya msingi hakuna, halafu mnasemaje mipango, mipango gani hii! Upungufu wa Walimu ukienda shule za msingi, kuna shule moja ina walimu wawili tu, tangu uhuru mpaka leo wapo wawili, halafu mnasema wanafunzi wanafaulu wanakwenda wapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, CCM mnamsaidia shetani kazi nawaambia ninyi, maana mnatengeneza majambazi wengi, vibaka wengi, ambao baadaye watakuja kuwatesa ninyi wenyewe, maana ninyi ndiyo mtakuwa matajiri, watawaibia ninyi wenyewe. Unafikiri kama akimaliza darasa la saba, kamaliza form four hana ajira unafikiri atafanya kazi gani, atalala na njaa na wewe unashiba hapa, atakushughulikia!
Mheshimiwa Mwenyekiti, iko shida, ukienda sekondari Walimu wa sayansi ni kilio, hivi viwanda mnavyosema mnaanzisha siyo maana yake sayansi, Physics, Chemistry, Biology, Mathematics Walimu wako wapi? Walimu wa Sayansi wamekimbia Ualimu maana Ualimu haulipi, hata mimi ni mwalimu wa sayansi nimekimbia kwa sababu hali ni ngumu. (Makofi)
Walimu wanalia, walimu wa sayansi unakuta Mwalimu ni mmoja ana vipindi 50 kwa wiki, Mwalimu wa art ana vipindi vinne kwa wiki lakini mshahara unajua ni ule ule, hiyo biashara ngumu mzee! Kwa hiyo, walipeni walimu wa sayansi vizuri. Vijana wanapomaliza wamefaulu vizuri sayansi form four na form six wanaenda kwenye udaktari, wanaenda kwenye mambo mazuri na hata ninyi ambao mko hapa, wengi ambao mmesoma sayansi mmekimbia huko, wengi siyo walimu! Naomba Waziri unapokuja tuambie mmefanya nini kuhusu elimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu mapato. Serikali ya CCM ni ya ajabu sana, wakiona Halmashauri za Wilaya zimetengeneza vyanzo vizuri vya mapato wanabeba, kule Serengeti tulikuwa na bed fee wakabeba, nimesikia sasa hivi wanataka wachukue property tax.
MHE. MARWA R. CHACHA: Sasa ninyi kwa nini msitengeneze vyanzo vya kwenu huko Serikali Kuu, Halmashauri itengeneze vyanzo vya mapato, ninyi mbebe, halafu madawati sisi tutatoa wapi tuwapelekee wale watoto, yaani ninyi mnachukua fedha zote mnakula, eeh mnatumia zote, kwa mfano, mimi nimekuwa Diwani tangu 2010, miaka yote Capital Development Grant (CDG) 26 percent ndiyo inakuja, mnafanya nini? Hamuwezi kufanya chochote.
Nawaambia CCM pumzikeni tupeni CHADEMA hapa tuongoze nchi tuwaoneshe mambo, maana mmeshindwa! nenda kwenye pembejeo ni kilio, kila kitu ni kilio, ukija nimepewa mahindi ambayo mkulima wangu ameenda amepanda hayakuota, sasa hivi wanapaka rangi wanasambazia wananchi kule hiyo ndiyo Serikali ya CCM. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana. Naomba na mimi nichangie kwenye mpango huu mambo machache, lakini ya msingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna Wabunge huwa hawaielewi hii Serikali, mmojawapo ni mimi huwa siielewi, ninazo sababu za msingi mnisikilize wote mkae kimya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii ni ya wakulima na wafugaji, unapokuja kwenye mikoa iliyopo Kanda ya Ziwa, wafugaji waliopo kandokando mwa hifadhi na mapori ya akiba na misitu wana kilio kikubwa sana. Ng’ombe wa wafugaji wa mikoa ya Mara, Simiyu, Mwanza mpaka huko Kagera inataifishwa na Serikali hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi maskini ambao tegemeo lao ni mifugo, leo unapiga mifugo mnada, unamuacha mfugaji akiwa maskini akiwa ana watoto wanamtegemea yeye, akiwa na rundo la familia nyuma wanamtegemea yeye awalipie ada za chuo kikuu na shule za sekondari, leo mmepiga minada, watu wetu wamebaki maskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Serengeti ng’ombe wameuzwa, watu wanalia. Mama mmoja ng’ombe wameuzwa wote, mama akapigwa miaka mitatu jela na kulipa faini ya shilingi 800,000, ameacha familia haina chochote, mnatupeleka wapi ninyi Serikali ya CCM? Mnasema ninyi ni Serikali ya wanyonge, mnatesa wafugaji. Mimi nawaambia wafugaji wa Kanda ya Ziwa wale wa Mikoa ya Simiyu, Biharamulo, Serengeti na Mkoa wa Mara hii Serikali ya CCM 2020 ishughulikieni kweli. Haiwezekani wafugaji wetu waendelee kuteswa na Serikali hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashindwa kuwaelewa, njoo kwenye viwanda. Nchi hii tuna viwanda vya kuchakata mazao ya mifugo vingapi, kiwanda kipo kimoja tu, tena cha mjasiriamali mmoja Mtanzania yupo pale Mwanza, ndiye mwenye kiwanda kikubwa ambacho angalau. Tembea kokote huko hakuna wana bucha tu wanaita viwanda, hakuna kiwanda ni butchery. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka Waziri Mheshimiwa Mpango, tuambie mna mpango gani kuhusu viwanda vya kuchakata mazao ya mifugo, mtuambie hapa. Ukienda hata kwa yule ambaye ana kiwanda pale Mwanza analalamika kweli, kodi kibao, hakuna namna ya kumsaidia yule mjasiriamali, tumsaidie kwa ajili ya kusaidia wafugaji wetu wa Kanda ya Ziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka Mheshimiwa Mpango uniambie, mifugo ya nchi hii ambayo kimsingi tuna mifugo mingi, mna mpango gani maana kiwanda ni hicho cha huyo na kiwanda kingine kipo huku Rukwa yule Mbunge mstaafu yule Mzee Mzindakaya, kinakaribia kufa kile. Tumeshindwa kuwasaidia watu wetu ili wawe na viwanda vya kwao wenyewe. Kwa hiyo, nikisema siwaelewi, siwaelewi kweli na wananchi hawawaelewi kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye fedha za maendeleo, mwaka wa fedha uliopita zilitengwa shilingi trilioni 11.8 kwa ajili ya maendeleo, zikatoka shilingi trilioni
6.5 sawa na asilimia 55, fedha za maendeleo hizo. Kwenye bajeti ya mwaka huu, fedha zilizotengwa za bajeti ni kama shilingi trilioni 12 kwenye robo ya kwanza zimetoka shilingi trilioni 1.3 sasa piga zipo robo nne. 1.3 trilioni mara nne ni ngapi, utaona ni kama asilimia 44, hapo wanasema hapa kazi tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Jimbo langu la Serengeti, Mkoa wa Mara barabara ya lami inayounganisha Mkoa wa Mara na Mkoa wa Arusha, tangu Mheshimiwa Kikwete aliondoka mzee mpaka leo na aliyekuwa Waziri wa Ujenzi wa barabara ni Mheshimiwa Magufuli, tangu hapo barabara ya kuunganisha Mkoa wa Mara na Mkoa wa Arusha imekuwa ni ndoto. Kibaya zaidi aliyepewa tender kujenga barabara ile ni rafiki yake na Magufuli na ndiyo huyu amempa kujenga uwanja wa Chato sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka Mpango unapokuja tuambie yule mkandarasi mliyempa kilomita 50 miaka zaidi ya mitano ameshindwa kumaliza kilomita 50, bado mnaendelea nae? Barabara ya kuunganisha Mkoa wa Mara na Mkoa wa Arusha “baakerwa” wameshindwa! Barabara hiyo kipande cha Mugumu - Nata mwaka wa fedha 2016/ 2017 kilitengewa shilingi bilioni 12, mwezi wa 12 2016 wakatangaza tender mpaka leo wanatafuta mzabuni, sema hamna hela bwana msitudanganye hapa! (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye maji nako ni aibu. Mwaka jana zimetengwa zaidi ya shilingi bilioni 600 kwenye maji, zimetoka asilimia 18. Kwenye nchi hii shida kubwa ya watu wetu ni maji, ukienda vijijini ni maji na ukienda mijini ni maji, unatoa asilimia 18 tu halafu unasema hapa kazi tu, hapa kazi kwa kitu gani...mura nu tune ng’ana [unatafuta jambo]. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ni mbaya sana, barabara sasa hivi wameanzisha kitu kinaitwa TARURA.

TARURA sijui iko chini ya nani? Ukija kimsingi Madiwani na Mkurugenzi ndio wasimamizi ambao wapo karibu na wananchi, barabara zimeondolewa kwa wala barabara hazipo chini ya Mkurugenzi tena, hazipo chini ya Baraza la Madiwani wala Mbunge, zipo chini ya kitu kinaitwa TARURA. TARURA ina mapembe, wao wenyewe ndio wanajua walime barabara ipi na waache ipi, mimi sielewi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamekomba engineers waliokuwa kwenye Halmashauri za Wilaya na Manispaa wamekwenda TARURA, Halmashauri za Wilaya hazina wahandisi sasa hivi. Mheshimiwa Mpango unapokuja utuambie mpango wenu ni kuua Halmashauri au mna mpango gani? Kwa sababu kwenye mapato mimi sijawahi kuona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri zilikuwa zinakusanya mapato vizuri sana, property tax, ushuru wa mabango na ushuru mwingine mwingi walikuwa wanakusanya. Leo Serikali hii inayojiita Serikali makini imechukua mapato ya Halmashauri hata ushuru, ushuru unakusanywa unapelekwa Serikali Kuu halafu ushuru wenyewe umeshindwa kukusanya, Halmashauri zinakaa hata kuendesha vikao imeshindikana. Mtuambie mna mpango gani hizi Halmashauri, mna mpango wa kuziua Halmashauri kwa kuzinyng’anya vyanzo vya mapato? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaambia Madiwani nchi nzima, wawe wa CCM ama CHADEMA wote muungane pamoja, ninyi ndiyo mnatafuta kura za Wabunge na Rais. Madiwani wote wa CCM na CHADEMA unganeni muishughulikie hii Serikali ijue kwamba ninyi ndiyo wasimamizi wakubwa wa miradi ya maendeleo. Haiwezekani Baraza la Madiwani, haiwezekani Halmashauri zinyang’anywe mapato, haiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii Serikali inaitwa Serikali ya bomoa bomoa. Mmewakuta wananchi, enzi hizo mlikuwa hamuwapimii viwanja, walijenga kwenye squatters ndiyo utaratibu uliokuwepo, leo mnabomoa hovyo hovyo. Serikali makini, Serikali ya wanyonge! Mimi naangalia kilio, eti Rais anabomolea watu wa Dar es Salaam halafu anakimbilia Mwanza anasema, eti Mwanza ndiyo walimpa kura, hivi Mwanza ndiyo walimpa kura nchi hii nzima! Sasa kwa kuwa Mwanza ndiyo walimpa kura, aache mwaka 2020 uone maeneo mengine watamshughulikia kama hana akili. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ajira. Viwanda hakuna, ukija kwenye nchi hii, hivi wamemaliza wanafunzi wangapi vyuo vikuu, wapo wapi, ajira ziko wapi? Mnasema Serikali ya viwanda, hamjajenga vyuo vya kati vya ufundi, vyuo vya VETA, unakuja Mkoa mzima unaweza kukuta Chuo cha VETA kimoja au mikoa mingine haina. Mimi hata pale Serengeti nataka kufungua kiwanda, lakini ukitafuta hata fundi tu wa kuongoza ile mitambo hayupo, mkoa mzima hayupo! Hata nchi hii wa kuhesabu ni wachache, sasa tunaenda wapi? Elimu ya ufundi iko wapi tuambieni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mpango unapokuja hapa sema mpango unasema nini kuhusu VETA kila Wilaya, tungelikuwa na VETA kila Wilaya tungekuwa na vijana mafundi wazuri tu ambao wangekuwa wanachakata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nendeni hata Kenya hapo msiende mbali, msiende Ulaya, nenda hapo Kenya uone vijana wanavyofanya kazi, wana mafunzo mazuri na wanajiajiri. Leo unasema, kwa mfano hivi mwalimu ambaye amemaliza chuo kikuu ana Bachelor of Arts atajiajiri kwenye nini maana kazi yake ni kufundisha, anaenda kujiajiri wapi, akajenge shule, umempa mtaji? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye afya. Ninyi Serikali ya CCM nisikilizeni. Sera yenu ya afya inasema kila kijiji kiwe na zahanati na kila kata iwe na kituo cha afya. Njoo Serengeti tuna vituo vya afya viwili tu, Kituo cha Nata na Ilamba, hata hivyo vituo viwili bado havijakamilika vizuri vina mapungufu kibao, lakini sera yao inasema kila kata iwe na kituo cha afya, hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtuambie pesa mnayojidai mnasema mnakusanya zipo wapi? Mimi nataka waniambie wanasema wanakusanya matrilioni, tunataka kuona huko mtaani ukienda hakuna pesa wananchi wanalalamika, hata Wabunge wanalia. Wananchi wanalia kweli, sasa mtuambie hizo pesa mnakusanya mnalalia au mnafanyia nini! (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye Wizara hii. Nina mambo machache na ninamwomba ndugu yangu Mheshimiwa Kangi Lugola, Waziri wa Mambo ya Ndani anisikilize. Naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Kangi Lugola, ni moja ya Mawaziri wanaofanya vizuri sana, hilo halina ubishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya Askari ambao hawana nidhamu walikuwa wanajaribu kuharibu Wizara ya Mambo ya Ndani; na Mheshimiwa Kangi Lugola bila aibu amekuwa akisema wazi wazi. Nampongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo machache. La kwanza naomba Kituo cha Polisi cha Mugumu na nyumba za Askari ni za siku nyingi. Kwa mfano, nyumba ambayo anakaa OCS, OCCID imechakaa sana. Naomba kwenye bajeti hii tusaidieni Polisi Mugumu waweze kukarabatiwa kituo na nyumba za Polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kama Mbunge nimejitahidi, kulikuwa na shida ya choo, kupitia fedha zangu za Mfuko wa Jimbo niliwasaidia tukajenga choo na kibanda cha mlinzi. Halikadhalika Magereza walikuwa na nyumba zao tatu, mimi kama Mbunge niliwapa mabati na mbao wakapaua. Sasa Mheshimiwa Waziri niunge mkono tuwasaidie Magereza na Polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni Zimamoto. Mheshimiwa Waziri watu wetu wa Zimamoto pale hawana ofisi, hawana vitendea kazi. Gari walilonalo limechoka ni la miaka mingi. Kama tunaweza tukapata msaada pale Serengeti, gari la Zimamoto lenye uwezo la kisasa itapendeza zaidi, maana nyumba zinaungua lakini kwa sababu ya udogo wa gari lile haliwezi kuhimili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwa Mheshimiwa Kangi Lugola, Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani, ni kuhusu Wakisii wanaoishi Rwamchanga. Jamii hii ya Wakisii imekuwepo kabla ya Uhuru, lakini hawajapewa nafasi ya kuwa raia wa Tanzania, wanaishi kwa vibali na hawaruhusiwi kupiga kura. Namwomba Mheshimiwa Waziri, ifikie wakati hawa Watanzania wenzetu wapewe fursa ya kuwa Watanzania kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma biblia kuna andiko linasema, utawezaje kukitoa kibanzi cha ndugu yako ilhali wewe bado una kibanzi? Labda tu nisome eneo hili, anasema, “basi mbona wakitazama kibanzi kilicho ndani ya jicho la ndugu yako na boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe huiangalii? Au utawezaje kumwambia ndugu yako, ndugu yangu niache nikitoe kibanzi kilicho ndani ya jicho lako, nawe huiangalii boriti ya ndani ya jicho lako mwenyewe. Mnafiki wewe, itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe, ndipo utakapoona vyema kukitoa kile kibanzi kilichomo ndani ya jicho la ndugu yako.” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimewasikiliza kule ng’ambo…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema kuna ufisadi mkubwa ndani ya Jeshi la Polisi, CAG amekagua. Nami niwaulize, lile gari la CHADEMA mnafahamu ufisadi mlioufanya? Kama hamfahamu, acha niwaambie leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema kuna ufisadi mkubwa ndani ya Jeshi la Polisi, CAG amekagua. Nami niwaulize, lile gari la CHADEMA wanafahamu ufisadi walioufanya? Kama hawafahamu, acha niwaambie leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, gari linalosemwa alikopeshwa mwanachama fedha anunue gari ni uongo! Lile gari ni la CHADEMA, lile gari alipewa fedha Mbunge fulani yuko humu simtaji kwa sasa ila wakitaka nitamtaja; akapewa fedha kwamba yeye ndiyo anaenda kununua gari ili akwepe kodi. Kwa hiyo, chama kimekwepa kulipa kodi kwa kumtumia Mbunge kununua gari lile na ndiyo maana gari lile liko mpaka leo pale! Sasa niwaulize, mimi nimekuwa CHADEMA, ni lini chama kimekuwa na utaratibu wa kuwakopesha wanachama wake fedha? Lini? Eh, tuambiane hapa, wamekwepa kodi! (Makofi) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba…

T A A R I F A

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nampa mzungumzaji anayeeleza kwamba kuna hoja inatolewa humu kwamba askari wameshindwa kulipa mishahara. Sasa kama chama husika na watu husika wanakwepa kodi, mishahara ya watumishi wanaowasema itatoka wapi? Nataka nimpe Taarifa. (Makofi) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

MWENYEKITI: Ahsante. Endelea Mheshimiwa Ryoba.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ile Taarifa ya CAG ni ya kweli. Alikopeshwa Mbunge mmoja hapa wa Viti Maalum tena ananiangalia yuko pale, alipewa hela, akaenda kuinunulia CHADEMA gari. Wamekwepa kodi na mkileta mchezo nitamtaja hapa! (Makofi/Kicheko) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

MBUNGE FULANI: Mtaje.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwani si ni Sophia Mwakagenda?

MBUNGE FULANI: Kuhusu Utaratibu…

MWENYEKITI: Subiri Mheshimiwa Ryoba. Kanuni ya ngapi? Kanuni kwanza niambie. Nitajie Kanuni kwanza.

MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa Kanuni ya 64(1) kwamba Mbunge hatasema mambo ya uongo, yasiyokuwa ya ukweli ndani ya Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti…

MWENYEKITI: Elezea basi vizuri niweze kuridhika kama kweli ameenda nje maana wewe ndiyo unalijua zaidi hilo suala.

MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa ya CAG inaeleza vizuri kwamba katika moja ya queries ambazo zilitolewa kwam ba Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kilinunua gari ambayo imesajiliwa kwa jina la mwanachama wake mmoja, lakini aliyetoa fedha ni chama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukweli ni kwamba anachokieleza Mheshimiwa Mbunge anayechangia sasa hivi ni uongo kwa sababu ukweli hauko hivyo, vitabu vya CAG vipo.

Sasa sisi tunamwomba au mimi namwomba athibitishe, alete huo ukweli kwamba chama kilitaka kukwepa kodi ndiyo kikatoa hizo fedha kupitia kwa huyo mwanachama na kama hatafanya hivyo ili taratibu ziweze kutumika, kwa sababu anachosema ni uongo. (Makofi)

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, ni masuala ya kanuni haya 64(1)(a) uliyoisoma lazima uisome na kanuni ya 63 kwa sababu aliyekuwa anaongea alikuwa ni Mheshimiwa Ryoba, amesema kitu ambacho kikafanya wewe ujisikie kwamba usimame kwa mujibu wa Kanuni ya 63(3) Kuhusu Utaratibu kwamba yeye hajasema kitu kilicho sahihi. Wewe kwa mujibu wa Fasili ya (4), Mbunge anayetoa madai kwa mujibu wa Fasili ya Tatu ya Kanuni hii atakuwa na wajibu wa kutoa na kuthibitisha ukweli kuhusu jambo au suala hilo kwa kiwango cha kuridhisha Bunge. Sasa huo wajibu au ule mzigo wa kuthibitisha sasa ulihama kutoka kwa Mheshimiwa Ryoba kuja kwako. Umejaribu kuelezea lakini hukufikia sasa kile kiwango cha kutofautisha pale ambapo yeye yupo tayari kumtaja maana hoja hapa ni kwamba ilikuwa ni scheme ya kukwepa kodi. Sasa tusaidie hapo ili sasa nirejee kwake. (Makofi)

MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, source yake ni CAG kama alivyosema. Katika Taarifa ya CAG hakuna mahali popote ambapo CAG amesema CHADEMA ilitaka kukwepa kodi na CHADEMA imetoa maelezo kwamba kuna mwanachama ambaye aliagiza gari akashindwa kulikomboa, chama kikamkopesha fedha akalinunua na hilo gari liko pale kwenye Chama na CAG ameliona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo suala hapa ni kwa nini halijahamishwa kutoka kwa yule mwanachama aliyekopeshwa kuja kwenye chama, lakini hakuna suala la kukwepa kodi. Sasa hiyo ya kukwepa kodi anatoa wapi? Hiyo ndiyo tunataka athibitishe na akishindwa kuthibitisha afute hiyo kauli, vinginevyo atakuwa anasema kitu ambacho sio sahihi. (Makofi)

MWENYEKTI: Ahsante. Mheshimiwa Ryoba.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Komu yuko sahihi kabisa na bahati nzuri Mheshimiwa Komu na Mheshimiwa Kubenea wako kwenye matazamio chini ya Kamati Kuu, maana…

MWENYEKITI: Mheshimiwa, jibu tu hilo.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, amenisaidia. Ni kweli kwamba alikopesha mwanachama na alikwepa kodi, kwani si Sophia Mwakagenda, alilipa wapi? Kama mimi ni mwongo, gari hilo mpaka leo liko kwenye chama, ni la chama sio la mwanachama! Mwanachama katumika tu kukwepa kodi! Kama mimi mwongo thibitisha wapi mlilipa kodi. (Makofi) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme Komu na Kubenea walitoa tuhuma dhidi ya Mwenyekiti wa CHADEMA, Mbowe, kwamba anakula ruzuku!

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu.

MHE. MARWA R. CHACHA: … na wako chini ya Kamati Kuu kwa uangalizi na wakavuliwa nafasi zao zote! (Makofi)

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, naona huo sio utaratibu mzuri wa matumizi ya muda wetu wa Bunge. Ningependa sasa Mheshimiwa Ryoba, nisaidie tu kwa sababu na mimi lilikuwa linanisumbua sana hilo suala la kwamba kulikuwa na scheme ya kukwepa kodi. Sasa kama kwenye CAG Report hakuna kitu cha namna hiyo, nisaidie tu ondoa hiyo scheme ya kukwepa kodi, tubaki tu katika utaratibu wetu.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo haina shida kwa sababu jinsi gari lilivyoingia…

MWENYEKITI: Ondoa tu hiyo nanihii. Nisaidie ondoa hiyo ya kukwepa kodi.

MHE. MARWA R. CHACHA: Naondoa, lakini tutafuatilia zaidi. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru. Kwa hiyo niseme huwezi ukawa unanyoosha tu kidole, ondoa boriti ya kwako kwanza. Sasa wewe hujaondoa ya kwako unasema! Hapa ngoja nikwambie, hawa Wabunge wewe unaowaona kule ng’ambo wana shida! Mbunge wa Viti Maalum kila mwezi shilingi 1,500,000 na hawajui zinafanya kazi gani na tunavyoongea hata matumizi ya ruzuku niambieni Katibu gani wa CHADEMA wa Jimbo au wa Wilaya anayelipwa na ruzuku ya CHADEMA? Hela inaliwa na wachache pale Makao Makuu.

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nashukuru.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii niweze kuchangia Mpango ambao ni wa awamu ya pili kati ya Awamu Tatu za Mipango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kuishukuru sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Nilikuwa najaribu kupitia Mpango huu wa 2016/2017 - 2020/2021, nilikuwa najaribu kupita kwenye maeneo ambayo yamefanyiwa utekelezaji na kwa kiasi kikubwa naweza kusema tuipigie Serikali makofi kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo siri, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Bajeti, tunakaa tuna-negotiate mambo mbalimbali kwenye kikao, kwa kweli nchi yetu kwa miradi mikubwa ambayo inafanyika imetubeba sana. Na mimi niwaambie Wabunge wa CCM kama kuna wakati mmefanya mambo mpaka yamefilisi upande wa kule kwenye hoja ni kipindi hiki. Mambo mazito kweli kweli! Siku moja nilikuwa namsikiliza kiongozi mmoja anasema, unajua uamuzi wa kununua ndege; ziko ndege ngapi? Kununua ndege saba…

MBUNGE FULANI: Nane.

MHE. MARWA R. CHACHA: Nane eeh!

MBUNGE FULANI: Eeh!

MHE. MARWA R. CHACHA: Siyo mchezo! Ni maamuzi magumu, lazima mtu awe ameamua kweli kweli. Mtu mwepesi mwepesi hawezi. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa maamuzi yake. Nilikuwa nasikia asubuhi kwenye Ripoti ya Kambi ya Upinzani wanasema Mpango haufuatwi, haujatungiwa sheria, ni maamuzi ya mtu mmoja.

Mheshimiwa Spika, nikawa najiuliza, nikawa napita kwenye Mpango humu nione uamuzi wa mtu mmoja ambao umetekelezwa ambao uko nje ya Mpango ni upi? Nikakuta Bandari imo kwenye Mpango, reli iko kwenye Mpango, ndege ziko kwenye Mpango. Sasa nitamwomba rafiki yangu Mheshimiwa Silinde atuoneshe kitu hata kimoja tu ambacho humu hakimo ambacho kimefanyiwa maamuzi yaliyo kinyume na Katiba na Sheria za Nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ni-chip in kidogo baadhi ya maeneo ambayo ninadhani tuyarekebishe ambayo kimsingi kwenye utekelezaji wa Mpango nimeona yana shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia 70 ya Watanzania wanategemea kilimo. Ukisikia watu wanalia hawana hela mfukoni, ujue kwamba kuna shida kwenye Sekta ya Kilimo. Kama kuna eneo ambalo kiukweli tunahitaji kupeleka nguvu kubwa, kuwekeza ni kwenye kilimo. Mfano, kule ninakotokea Jimboni kwangu Serengeti, wananchi wa Serengeti walikuwa wanalima tumbaku. Kulikuwa na Kampuni ya Alliance One, wakilima tumbaku, wakivuna wakiuza, shilingi bilioni 20 zinazungua ndani ya Wilaya. Unakuta watu mifukoni wana pesa. Tangu kampuni ilivyoondoka, pesa hakuna. Kwa nini? Kampuni imeondoka. Kwa hiyo, jambo hili la kilimo lazima tulitazame kwa upya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Mpango huu tuna mikoa 17 inayolima pamba. Nimekuwa nikijiuliza, hivi ni lazima sisi Tanzania twende kuuza pamba ghafi nje? Kwamba mikoa 17 izalishe pamba, sisi tuwe watu wa ku-export pamba, hii itatuchukua mpaka lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka enzi za Mwalimu Nyerere kulikuwa na viwanda vingi sana vilivyokuwa vinachakata pamba, kwa mfano, MWATEX, KILTEX, MUTEX na vingine vingi. Sasa mimi nikadhani Serikali ukiiuliza inasema mambo ya viwanda ni Sekta Binafsi inatakiwa ijenge, lakini kuna viwanda vingine lazima Serikali iingilie kati kuangalia namna ya kusaidia Sekta Binafsi kujenga viwanda. Maana ukijenga kiwanda cha ku-process pamba, leo utaokoa wananchi wa mikoa 17. Siyo jambo dogo!

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Serikali inaweza kutoa mabilioni ya pesa ikajenga miundombinu kwa mfano, ukanunua ndege hata moja, ni billions of money lakini kumbe unaweza uka-finance sekta binafsi kwa kutumia Mfumo wa PPP ikasaidia kujenga kiwanda cha ku-process pamba ambacho kiwanda hicho kitaokoa wakulima wa mikoa 17.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mawaziri husika, jambo hili la kilimo cha pamba liangaliwe kwa upya, kwa undani. Kama ambavyo tumeingia PPP kwenye miradi mingine, tunaweza kuingia PPP kwenye kiwanda cha kuchakata pamba tukaleta ajira kwa wananchi wetu ambao wengi wanategemea pamba. Hilo lilikuwa wazo langu kwenye kilimo cha pamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwenye barabara. Unakumbuka kilianzishwa chombo kinaitwa TARURA kwa ajili ya kusimamia utengenezaji wa barabara mjini na vijijini na sababu ilikuwa ni kwamba wakati fedha zikienda kwenye Halmashauri zimekuwa hazitengenezi barabara zetu kwa kiwango kinachotakiwa. Iliamuliwa kwamba kingeundwa chombo hiki kikasimamia utengenezaji wa barabara za vijijini na mijini, barabara zingekuwa za kiwango, lakini hali imekuwa sivyo. Kwa nini hali imekuwa sivyo? Ni kwa sababu TARURA wanapata pesa kidogo, pesa wanayopata ni ile ile ambayo Halmashauri za Wilaya zilikuwa zikipata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumbuka kwa sasa TARURA hawako chini ya Halmashauri, wana Ofisi wamepanga mitaani, kwa hiyo, wanalipa bill za majengo. Wanatumia gharama kubwa kwa ajili ya bill za ku-rent majengo. Kwa hiyo, ni gharama kubwa kwanza kuendesha chombo hiki. La pili, pesa wanayopata ni ile ile. Kwa mfano, nchi nzima TARURA inahudumia kilometa zaidi ya 100,000, wanapewa shilingi bilioni 250, hazitoshi hata kidogo. Hizi shilingi bilioni 250 ni pamoja na barabara za lami kwenye Majimbo mbalimbali. Kwa hiyo, unaweza kuona ni hela kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nashauri, TARURA na TANROADS kutegemea Mfuko wa Barabara, shilingi 100 ya mafuta peke yake haitoshi, lazima Serikali ije na financing nyingine ya kuisaidia TARURA kusimamia barabara. Kwa wale Wabunge wa Majimbo tunaotokea huko Majimboni, hali ni mbaya kwenye vijiji kiasi kwamba mazao ya kilimo kutoka vijiji fulani kwenda sokoni inashindikana. Magari yanashindwa kwenda kuchukua mazao kwenye vijiji hivyo. Kwa hiyo, naomba Wizara, mbali na Mfuko wa Barabara tutafute chanzo kingine cha ku-finance TARURA ama tuongeze shilingi 50/= kwa ajili ya TARURA peke yake ili tuweze kuhudumia barabara za vijijini na mijini ambazo ziko chini ya TARURA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vinginevyo kama hakuna chanzo kingine cha kuisaidia TARURA ni bora Serikali ikubali kuchukua maamuzi magumu kwamba popote kila Wilaya ilipo, TARURA waruhusiwe ama wakopeshwe fedha wawe na vifaa vya kutengeneza barabara ili fedha ambayo ni ruzuku wanayoipata ya Mfuko wa Barabara watengeneze wenyewe, vinginevyo barabara zetu zitaendelea kuwa mbaya sana. Kwa hiyo, huo ni ushauri wangu ili TARURA ikae vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni Sekta ya Utalii. Sekta ya Utalii ni moja ya Sekta nzuri sana ambayo inachangia asilimia 24 ya mauzo ya huduma nje ya nchi. Ni moja ya Sekta ambayo inachangia kwenye GDP ya Taifa letu asilimia 17.2. Kwa hiyo, siyo sekta ya kubeza ni sekta ambayo inahitaji tuitazame kwa macho mangapi mangapi ili iweze ku-boom.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii na Naibu Waziri kama wako hapa, kwa kuamua kujenga uwanja wa Serengeti uliopo Mugumu kutoka kwenye ule wa Seronera. Ni jambo zuri sana kwa sababu ndege zilikuwa zimejazana sana mle hifadhini na mnafahamu mpaka ikatokea ile ajali ni kwa sababu ndege zimekuwa nyingi. Nawapongeza sana watu wa TANAPA na Bodi ya TANAPA kwa kuridhia kwamba sasa wahamie kwenye uwanja ambao uko Mugumu. Nasi kama Halmashauri tuna hatimiliki tayari, tuna kibali cha NEM na TAA kwa ajili ya ujenzi wa uwanja ule wa ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali, Mheshimiwa Mpango, kile kiwanja ni kiwanja kizuri sana kwa ajili ya kuhakikisha kwamba upande wa Magharibi wa Hifadhi ya Serengeti unakuwa kiutalii. Sasa ni vizuri Serikali itazame namna ya kuwasaidia TANAPA, namna ya kuisaidia Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti kuboresha ule uwanja uwe katika kiwango ambacho kinatakiwa kwa sababu ndege zinaruka almost zaidi ya 200 kwa siku, siyo kitu kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie barabara za kuunganisha mikoa na mikoa na hususan barabara ya kuunganisha Mkoa wa Mara na Mkoa wa Arusha, barabara ya Makutano - Sanzate – Nata - Mugumu - Tabora B, Kilensi – Loliondo - Mtu wa Mbu. Hii ni barabara muhimu sana ya kiutalii na barabara ya kuanzia Sirari – Tarime - Mugumu ni barabara nzuri za kiuchumi kwa sababu unakuta watalii wengi wanaoshukia Kenyatta International Airport lazima waingie Sirari, Tarime. Sasa ni vizuri barabara hizi ziboreshwe kwa kiwango cha lami maana ni barabara ambazo zina fursa ya kiuchumi ili ziweze ku-boost uchumi kwa wale watalii ambao wanatembelea Hifadhi ya Serengeti pamoja na Ngorongoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni maji. Maji bado financing yake pia haijakaa vizuri. Ni vizuri kwenye Mpango unaokuja, Mheshimiwa Mpango, mwangalia namna ya kupata fund nyingine ili kusaidia huduma ya maji vijijini. Maana huduma ya maji vijijini na yenyewe ikitegemea Mfuko wa Maji shilingi 50/=, haitoshi. La sivyo, tuongeze ziwe shilingi 100 ili ziweze kusaidia. Kwa hiyo, nadhani kwenye hili ni vizuri mkaliangalia ili kuwepo na upatikanaji wa maji vijijini, kwani bado maji vijijini hali yake siyo nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na nimpongeze Waziri wa Fedha kwa kazi nzuri, naipongeza Serikai ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri. Naona kila sehemu Wenyeviti wa Vijiji wanapita bila kupingwa. Naona wenzetu wanalialia tu hawasimamishi sijui kwa nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa niaba ya wananchi wa Serengeti naomba nichukue nafasi hii kuchangia Wizara hii ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
Mheshimiwa Mwenyekiti naomba nianze na Mawasiliano. Katika Wilaya ya Serengeti tuna maeneo mengi sana ambayo mitandao ya simu hakuna na tunavyoongelea Serengeti, ndiko kwenye mbuga ambayo inaingiza fedha nyingi katika nchi hii, yaani ndiyo mbuga ambayo inasaidia ku-finance watumishi wa TANAPA kwenye mbuga nyingine kama Mikumi na maeneo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mbuga hii kuna maeneo mengi ambayo hayana mawasiliano. Kwa mfano Robo ambako kuna Hoteli ya Robo hakuna mawasiliano kabisa, Bilila iko shida. Mheshimiwa Waziri nikuombe wakati wa ku-wind up hebu njoo na jibu la kueleweka kwamba sasa hoteli ambazo ziko ndani ya hifadhi watapata minara kwa ajili ya mawasiliano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni barabara. Sasa naomba niseme kuhusu barabara ya Makutano – Nata – Mugumu – Loliondo – Mto wa Mbu. Aliyeanza kuwa na maono ya kujenga barabara hii ni Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, wakati huo ikiitwa Makutano – Nata – Ikoma Gate.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baadaye alipokuja Mheshimiwa Benjamin William Mkapa ndipo wakaanza kuiweka kwenye Ilani ya CCM. Mkapa akaondoka, katika miaka yake kumi hakujenga barabara hii. Akaja Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, ikawekwa kwenye Ilani ya CCM, wakati huo Mheshimiwa John Pombe Magufuli akiwa ndiye Waziri wa Wizara ya Ujenzi. Ikapita miaka kumi wala hakuna chochote kilichofanyika. Sasa amekuja ambaye alikuwa Waziri wa wizara hiyo, Mheshimiwa John Pombe Magufuli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni barabara pekee inayounganisha Mkoa wa Mara na Mkoa wa Arusha. Wakati mwingine watu wa Mkoa wa Mara wanalalamika hawanufaiki na utalii, hawanufaiki na fursa zilizopo za utali, ni kwa sababu barabara hii haijafunguka kuunganisha mkoa wa Mara na mkoa wa Arusha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni aibu sana, barabara hii mwaka 2013 ilitengewa fedha kwenye bajeti ili ianze kujengwa na mwezi wa tatu mwaka 2013 ujenzi wa barabara ukaanza, ambapo wakandarasi wa ndani ndio waliokuwa awarded tender ya kujenga barabara hii. Na bahati nzuri mmoja wa wakandarasi anaitwa Steven Makigo, rafiki yake sana Magufuli, akapewa kazi ya kujenga barabara hii. Yeye na wenzake contractors kumi, tangu mwaka 2013 mwezi wa tatu mpaka leo ninavyoongea wamepewa shilingi bilioni 14 hawajajenga hata mita moja ya lami. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia; waliopewa kujenga barabara hii ya lami, Makutano – Nata – Mto wa Mbu ni contractors wa ndani wakiongozwa na Kampuni ya Mayanga ambayo Mkurugenzi wake ni huyu Steven Makigo, wako contractors kumi. Wakaisajili kwa jina moja wanasema Mbutu Bridge Contractors; ni wa kwetu ni wazawa. Tangu 2013 wamepewa shilingi bilioni 14 hata mita moja ya lami hakuna halafu mnasema hapa kazi tu, hapa kazi kwa issue gani? Kama mmewapa bilioni 14 wameshindwa wanyang‟anyeni, watumbueni majipu wale, anzeni na huyu mkandarasi, yaani hakuna chochote anachofanya lakini munampa mahela tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siku moja nimeuliza swali hapa Mheshimiwa Waziri hakulijibu na hiyo wamepewa kujenga 50 kilometers kuanzia Makutano mpaka Sanzate. Sasa hivi ninavyoongea mkataba wa kujenga barabara ile uliisha mwaka 2015 mwezi wa tano, baadaye wakaomba extension wakaongezewa mpaka Machi 2016, hivi huu ni mwezi gani? Mpaka leo bado hawajajenga hata mita moja, bado tunaendelea ku-entertain watu wa namna hii, si afadhali mtuwekee pale Mchina ajenge ile barabara ikamilike haraka.
KUHUSU UTARATIBU...
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee, kwa kanuni aliyoisoma; inasema hatatumia jina la Rais kwa dhihaka katika mjadala au kwa maudhui ya kutaka kulishawishi Bunge kuamua jambo lolote kwa namna fulani kwani mimi nimewashawishi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, naombo niendelee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi simuongelei Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli, namuongelea yule aliyekuwa Waziri wa Ujenzi wakati huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni aibu, kama watu wamepewa shilingi bilioni 14 hata mita moja ya lami hawajajenga halafu unaniambia nisiongee, I have to talk. Nimeletwa hapa kama Mbunge wa Jimbo la Serengeti niongee kwa niaba ya wananchi wa Serengeti. Tunachokiongea hapa si mambo ya chama, hata kama ingelikuwa kwako wewe wametumia shilingi bilioni 14 hawajajenga kilometa moja ya lami utasikia vizuri, au huyo malaika akiguswa mnasikiaje? Tulia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni yenyewe sasa hivi wanajenga daraja la Mto Kiarano, hata structural engineer hawana, material engineer hayupo! Hivi hii Wizara ikoje hii?
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, haina watu wa kwenda kukagua pale waone kwamba kuna structural engineer, material engineer? wataalamu wa namna hii hawapo? Sasa unajenga barabara ya kuunganisha mkoa na mkoa key personnel are not there, ninyi vipi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi nataka Waziri anapokuja atuambie hii barabara itakamilika lini? Kwa mwendo huu ndiyo mtatuambia hapa kazi tu, hakuna cha kazi hapa tunadanganyana. Na kama kweli Rais, Mheshimiwa John Pombe Magufuli anaipenda nchi hii, anawapenda wananchi wa Mkoa wa Mara, anawapenda wananchi wa Serengeti, aanze ku-deal na huyu mkandarasi. Kama mtu anaweza kutumia shilingi bilioni 14 halafu hakuna chochote alichofanya halafu watu wanaona sawa tu eti usimguse nitakugusa tu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mara tumesema ni mkoa ambao ni very potential, una mbuga ya wanyama, una migodi ya Nyamongo, tuna watalii na watalii wengi kama mnavyojua wanatokea uwanja wa ndege wa Jomo Kenyatta – Nairobi, wanapita Sirali, Tarime wanakuja Serengeti. Ninavyoongea kwa sasa barabara zote Serengeti zimekatika na tunaelekea kwenye high season, sijui hata hayo mapato tunayoyategemea kutokana na utalii tutayapata wapi kama barabara zimekatika inakuwa ni chaos kwa watalii?
Mheshimiwa Maghembe uko hapo unafahamu, watalii wengi wanatokea Nairobi, sasa kama hatutaki kujenga hata barabara ya Tarime - Mugumu watalii watakata tamaa. Kuna Barabara ya Musoma – Sirori Simba, Magange Ring‟wani ya kuingia Mugumu, barabara zote hizo hazina hata lami. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Serengeti ndiyo wilaya pekee ambayo mtoto anaweza akazaliwa akasoma Shule ya Msingi Ring‟wani akaenda sekondari ya Ring‟wani akamaliza akaenda form six pale Nata sekondari, akasoma Chuo cha Kisare hajawahi kuona hata lami. Ni Wilaya pekee ya kitalii ambayo haina hata mita moja ya lami…
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi namuomba Mheshimiwa Waziri…
MWENYEKITI: Muda wako umemalizika Mheshimiwa Marwa!
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana. Naomba nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kunipa neema ya kuondoka CHADEMA kuja CCM. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unajua nilikuwa kule ng’ambo kumbe nilikuwa sijui tulichokuwa tunakifanya kule, tulikuwa tunasema uwongo kwa kile tusichokiamini. Nimekuwa nikisawakiliza Wabunge wa CHADEMA na wa kule ng’ambo kwa ujumla wanasema Serikali ya CCM inafanya maendeleo ya vitu na siyo maendeleo ya watu, nawasikiliza nasema hawa vipi hawa au wamerogwa?(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma Ayoub 13:4 inasema “lakini ninyi hubuni maneno ya uwongo, ninyi nyote ni matabibu wasiofaa”. Isaya 9:15 inasema “Mzee mwenye kuheshimiwa ndiye kichwa na Nabii afundishae uongo ndiye mkia”, Manabii wafundishao uongo ndiyo mikia.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nina Ilani ya CHADEMA hapa. Nilikuwa Mbunge wa CHADEMA, niliinadi hii wakati nikiwa mgombea ninaijua na wanaijua. Leo nataka nipite humu tuangalie maendeleo ya vitu kwamba kweli Serikali ya CCM inafanya maendeleo ya vitu na siyo maendeleo ya watu, nitaangalia baadhi ya maeneo, naomba nianze na Bandari. Wao wanapinga ujenzi wa bandari na wanasema ukiangalia kwenye ukurasa wa 40 wa Ilani yao watafanya nini:

Kwanza ni kujenga reli mpya na kukarabati zilizopo kwa viwango vya kisasa kwa kuzingatia maslahi ya nchi. wanaopinga reli ya kisasa ya standard gauge ni akina nani?

WABUNGE FULANI: Wao.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, pili ni kuboresha zilizopo na kujenga mpya kama vitega uchumi vya Taifa. Tatu, ni kujenga Shirika la Ndege la Taifa linalojiendesha kwa misingi ya faida. Ndege zimenunuliwa wa kwanza kupinga ndege ni watu gani?

WABUNGE FULANI: Hao hao.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mikia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia ukurasa wa 41 unasema Shirika la Ndege la Taifa Air Tanzania…..

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Kuhusu utaratibu

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Marwa Ryoba Chacha subiri kidogo. Mheshimiwa Selasini naomba ukae kidogo. Mheshimiwa Marwa Ryoba Chacha pamoja na kwamba umenukuu kitabu cha dini kwamba kinawaita pengine watu wa aina fulani kwamba wao ni mikia na kitu kama hicho, lakini kwa kuwa sehemu hii Waheshimiwa Wabunge siyo kwamba vinakatazwa vitabu vya dini kunukuu, lakini pale ambapo ile lugha iliyotumika kwa sababu hatuna uwezo wa kuanza kutoa mahubiri na kutoa maana halisi ya hayo maneno humu ndani, yale maneno yako uliyoyachukua mwanzo, uliyoyanukuu kwenye kitabu cha dini Mheshimiwa Marwa Ryoba Chacha matumizi yake kwenye kusema nani ni mkia na nani siyo mkia hayataweza kutumika humu ndani kwa sababu siyo lugha ya Kibunge.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante nimekuelewa lakini maana yangu ni kwamba, Ilani ya CHADEMA iliongelea ndege lakini wakija humu ndani wanakataa kwa nini? Ni watu wa namna gani hawa, tuwaite jina gani? Mimi acha niende. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma ukurasa wa 41 wa Ilani yao inasema: “mizigo yote mizito kusafirishwa kwa njia ya reli na meli” leo wanageuka hapa, tuwaite jina gani? hawa watu wa ajabu sana. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma ukurasa wa 45 wa Ilani yao wanasema kupiga marufuku uuzaji wa korosho ambazo hazijabanguliwa na kuhakikisha kwamba asilimia 100 ya korosho zote tunazozalisha zaidi ya tani 200,000 zinabanguliwa hapa Tanzania. Rais Magufuli amesema hakuna kuuza nje Korosho nini? ambazo hazijabanguliwa na akasema Wanajeshi, bangua hata kwa midomo yenu kabangue tuuze korosho zilizokuwa processed wanakataa. Wewe ngoja nipite kwenye Ilani tulia kwani mnaisomaga basi ninyi! Hawa wanaambiwaga fanya hivi wanafanya hata bila kufikiria.(Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukurasa wa 53 unasema: “vipaumbele havijawekwa kwenye uendelezaji wa vyanzo vya uzalishaji wa umeme wa bei nafuu vilivyopo nchini, mfano Stigler’s kwenye Bonde la Mto Rufiji”. Wanasimama hapa wanapinga mradi wa umeme wa Stigler’s hawa tuwaite vipi, kwenye Ilani yao ipo hapa? (Makofi)

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. MARWA R. CHACHA: Tulia.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwakajoka nataka kuamini umezingatia matakwa ya Kanuni ya 68(8).

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimezingatia.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nafurahi sana kuona mzungumzaji pale anakubali kwamba kweli CHADEMA tumeandaa Ilani sahihi kabisa kwa ajili ya kuendesha Taifa hili na Serikali ya CCM imeyachukua na sasa hivi inayatumia kuhakikisha kwamba inatekeleza majukumu yote ambayo tulikuwa tumeweka kwenye Ilani yetu. Tunashukuru sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwakajoka, hapo sasa ni ufafanuzi wa jambo gani uliloeleza? Kila wakati nawakumbusha matumizi ya Kanuni.

Mheshimiwa Marwa Ryoba Chacha, endelea na mchango wako.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru leo baada ya kusoma hili andiko wamekubali kwamba CCM inafanya kazi, ahsante sana. Leo ndiyo wamekubali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukiangalia ukurasa wa 57 pia wameongelea, Serikali ya CHADEMA sio ya UKAWA, Serikali ya CHADEMA itaupa uzalishaji mkubwa wa umeme wa maji kipaumbele namba moja, yaani nyie vigeugeu kweli kweli sijawahi kuona. Imeandikwa kwamba kipaumbele cha kwanza cha uzalishaji wa umeme, cha kwanza maji, wameandika kwenye Ilani. Leo akisimama pale anasoma huwa nakaa nawaangalia hivi hawa wako sawasawa hapa kweli? Serikali ya CHADEMA itaupa uzalishaji mkubwa wa umeme wa maji kipaumbele namba moja, umeme wa makaa ya mawe kipaumbele namba mbili, umeme wa gesi asilia kipaumbele namba tatu, muende mkasoma Ilani yenu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi namshukuru Mungu kwa kuniipa neema ya kutoka kule. Unajua wale watu ukisema moja ongeza moja ni mbili, CCM akisema moja ongeza moja ni mbili wao watasema ni saba.

TAARIFA

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Goodluck.

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nataka nimpe taarifa Mheshimiwa anayeongea kuwa CHADEMA walikopa kwetu mgombea pamoja na Ilani. (Makofi)

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, hebu…

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee.

NAIBU SPIKA: Subiri kwanza Mheshimiwa Ryoba.

Waheshimiwa Wabunge, Kanuni hizi zinatutaka tutumie wakati wetu vizuri. Kwa hiyo, zinavyosema taarifa unakuwa unatoa ufafanuzi kwenye jambo analochangia mtu mwingine, kwenye hoja yake. Mheshimiwa Ryoba Chacha.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, unaona ukurasa huu kwenye hii Ilani, Mheshimiwa Mlinga alisema Lowassa ndiye aliyeandika Ilani wakakataa, ona kwenye huu ukurasa picha ya Lowassa hii hapa. Kwa hiyo, Lowassa alivyotoka CCM aliondoka na ile Ilani ya CCM aka- copy akapeleka kule.

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

MHE. MARWA R. CHACHA: Ndiyo, huo ndiyo ukweli.

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

MHE. MARWA R. CHACHA: Hii hapa, anayebisha asimame apinge, mimi ninayo hii hapa, hakuna wa kupinga wanajua ni ukweli. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya CHADEMA na UKAWA ilikuwa ni ufisadi, Mheshimiwa Magufuli ameshughulika na ufisadi. Unawasikia wanaongelea ufisadi sasa hivi, kimya, hola hamna kitu, yaani sasa hivi hawana hoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine wanasema ukurasa wa 37, sekta ya bandari imegubikwa na rushwa pamoja na utendaji mbovu kiasi kwamba mrundikano wa mizigo umekuwa mkubwa sana bandari na kupelekea mapato yake kuwa madogo kulingana na fursa za usafirishaji. Mheshimiwa Magufuli alivyoingia tu madarakani ziara zake za kwanza zile alienda wapi?

WABUNGE FULANI: Bandarini.

MHE. MARWA R. CHACHA: Bandarini akaenda akafumua, kuna watu walijifanya Miungu, eeh Mheshimiwa Magufuli ni mwanaume, haki ya mama. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, nilikuwa nataka kuwakumbusha tu kwamba waiunge mkono Serikali ya CCM maana inafanya mambo mazuri kama mimi nilivyofanya ukienda Serengeti sasa hivi mambo safi kabisa. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba niseme mambo machache na ninaomba Mheshimiwa Waziri unisikilize kwa makini kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza mwaka jana kuna vijana wamepotea katika Jimbo langu la Serengeti, walikamatwa porini vijana zaidi ya 20, mpaka leo ninavyoongea ndugu zao wamewatafuta hawajulikani waliko. Inasemekana wameuawa na askari wa wanyama pori, unapokuja hapa niambie wako wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, Mheshimiwa Waziri unakumbuka walikuja hapa Wajumbe wa WMA mwaka huu, walikuja Madiwani, walikuja Wenyeviti wa Serikali za Vijiji, walikuja na baadhi ya watendaji kwa ajili ya tatizo la single entry! Sasa tulikutana na wewe ukasema Kamati imekataa. Inawezekana Kamati imeamua, imechukua maamuzi haya kwa sababu haijafika Serengeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mapori ya akiba ya Ikorongo na Grumet Game Reserve pamoja na WMA ya Ikona, jiografia ya kwake ni tofauti kabisa na WMA ambazo ziko maeneo mengine.
Mimi ninakuomba Mheshimiwa Waziri tusaidiane wote na Kamati iende ikakutane na Wajumbe wa Ikona WMA, otherwise you want to kill WMA! Na WMA ikifa pale maana yake mapori ya akiba yale yote yataangamia. Maana kama yataangamia maana yake hakuna ajira. Vijana wataanza kuwinda, no conservation will proceed there. Kwa hiyo, ninakuomba Mheshimiwa Waziri fanya juu chini, Kamati yako itembelee Serengeti ili ikajiridhishe nini kilio cha watu wa pale Serengeti, lakini kama mkikaa hapa mezani mkaamua, kule mtaua yale mapori na hakuna kitakachoendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu, Serengeti National Park imeanzishwa kwa mujibu wa sheria na imekuwa Gazzeted kwenye Gazeti la Serikali tangu mwaka 1968 kwenye GN Na. 235; ukisoma ile GN iko clear, inataja mipaka ya Hifadhi ya Serengeti National Park. Kilichotokea Wizara yako imeendelea ku-extend mipaka kila kunapoitwa leo. Tangu GN itangazwe wame-extend mipaka zaidi ya mitano, wamechukua maeneo ya wananchi. Sasa sielewi nini maana ya GN? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama GN imetangaza mipaka, leo Wizara yako ina-violate, inachukua maeneo ya wananchi na bahati nzuri beacon zilipo zote tunazifahamu sisi watu wa Serengeti na Mheshimiwa Waziri ukitaka tutakuonesha. Naomba kitu kimoja, unapokuja naomba uniambie uko tayari wewe na Waziri wa Ardhi Mheshimiwa Lukuvi, kwenda kuhakiki mipaka ambayo ilitangazwa kwenye GN mwaka 1968? Ninataka hayo majibu wakati unapokuja kujumuisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni tembo na simba. Nimepiga kelele sana kwenye maswali na imefikia sehemu ninaitwa tembo. Iko hivi, hakuna watu wanaopata shida kama wananchi wa Serengeti dhidi ya tembo na simba. Tembo siku hizi anatembea tu kama binadamu wa kawaida, mnagongana naye kama binadamu wa kawaida, hakuna mtu anayechukua hatua dhidi ya tembo na simba. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, siku moja simba wamevamia kijiji cha Park Nyigoti, sasa wananchi siku hizi walishaelewa ili askari waje hawasemi simba amekamata mnyama, wanapiga simu wanasema tumeuwa simba hapa, dakika tano haziishi wameshafika. Kwa hiyo maana yake ni nini! Tembo, simba ni wa thamani kuliko binadamu. (Kicheko)
Sasa Mheshimiwa Waziri nataka pia unapokuja hapa utuambie katika Sheria ya Wanyamapori mko tayari ku-review, kuileta hapa Bungeni tuipitie upya vile viwango vya kifuta machozi na kifuta jasho? Maana tunajua hamtoi fidia. Mnatoa kifuta machozi na kifuta jasho ambavyo kimsingi haviendani na wakati tulionao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tembo wamekula mashamba ekari tano unampa mtu shilingi 100,000 for what? Shilingi 100,000 kwa eka tano shilingi 100,000 inatosha hata kwa mbegu? Mtu akiuawa mnampa shilingi 1,000,000 hata hiyo shilingi 1,000,000 ataomba miaka 10 ndiyo mnampa. Wewe ni shahidi unafahamu, hamjawahi kulipa. Pale Serengeti watu wameuawa wengi sana na tembo, sijawahi kuona mtu amelipwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nimeona wameleta wanalipa laki moja moja kwa baadhi ya watu, wengine wote walioathirika hakuna.
Sasa naomba unapokuja ku-wind up uniambie ni lini utaleta ile sheria tuipitie, kifuta machozi, kifuta jasho ili kiendane na wakati tulionao? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu barabara. Mimi sijawahi kuona, ninasikia sijatembea sana, lakini nasikia kuna Mbuga inaitwa Kruger iko Afrika ya Kusini, ukitembea kwenye ile mbuga na wanasema ndiyo mbuga inayoingiza watalii wengi na ndiyo mbuga inaingiza mapato mengi, lakini ukienda kwenye mbuga ile kuna lami. Wale ambao mmefika mtakuwa mashahidi, lakini kwenye Mbuga yetu ya Serengeti, hiyo hakuna! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Serengeti ukianzia Tarime, watalii wengi wanatokea Tarime, Sirari. Barabara ile watalii wanalalamika kila leo ingawa ninyi mnapuuza lakini watalii wanalalamika. Wanahitaji kutembelea Serengeti, lakini kutokana na barabara mbovu zilizopo wanaogopa.
Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri, gharama ambayo mnaitumia kila siku ku-maintain barabara za hifadhini ni afadhali mngeangalia zile barabara za msingi, zile ambazo zinatumiwa na magari mkaziwekea lami, hizo nyingine za kawaida kwa sababu hazina magari mazito, mnaweza kuzi-maintain kwa kutumia kifusi na kawaida. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ukija kwenye Mbuga ya Wanyama ya Serengeti National Park kuna hoteli lukuki, zaidi ya hoteli 100 ziko mle. Kuna camp nyingi lakini hayalipi service levy wamekimbilia mahakamani yet Serikali mko hapa, hamzisaidii Halmashauri zetu kupata mapato! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, unapochukulia Halmashauri kama Wilaya ya Serengeti kwa muda mrefu hatunufaiki na utalii. Inafikia sehemu watu wanakata tamaa. Sasa hakuna wananchi wenye nidhamu kama wananchi wa Serengeti kwenye conservation. Huwa wanakuja pundamilia (zebra), tunawarudisha, tunawapigia simu wanakuja wanawachukua. Wananchi wana nidhamu kweli, lakini itafikia sehemu tutachoka. Hebu tusaidie Mheshimiwa Maghembe tupate service levy! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, mkatunyang‟anya na bed fee, gate fee unajua ya kwamba Serengeti mizigo tunayoipata, vitu vya madukani tunavyovipata tunatoa Arusha, lakini mnawa-charge wafanyabiashara wa Serengeti kwenye mageti ya Ikoma Gate, wapi huko kwenda Ngorongoro wanachajiwa (charge) gharama kubwa! Vitu Serengeti ni bei ya juu kweli kweli. Mfuko wa saruji ninavyoongea sasa hivi ni shilingi 23,000 nadhani ndio inaongoza…
MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Chacha.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nimshukuru jirani yangu Mwita Gatere, Mbunge wa Bunda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na suala la tembo. Tembo ni tatizo Mkoa wa Mara. Tembo ni tatizo Serengeti ni tatizo Bunda, ni tatizo Tarime. Nichukue nafasi hii kutangaza janga la tembo Serengeti, Tarime na Bunda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, imefika sehemu tembo anaenda kutafuta chakula kwenye ghala, anabomoa ghala, juzi hapa, ameenda kwenye Kijiji cha Nyichoka, wakabomoa ghala wakala chakula isitoshe wananchi wakahamishia chakula ndani ya nyumba akaenda akabomoa nyumba akala chakula chote, wananchi wamebaki hawana chakula. Bahati nzuri amekuja Naibu Waziri, tumempeleka mpaka maeneo hayo amekuta nyumba zimebomolewa.(Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tembo anauwa wananchi kwa wingi sana sasa hivi, tembo amekuwa ni hatari sana kwenye ukanda wetu huo. Kama Serikali isipochukua hatua ni hatari kubwa mtasikia huko. Sasa hivi majambazi wanauwa tembo hawaendi kuwatafuta hifadhini wanakuja kuwavizia kwenye vijiji vya Serengeti nje kabisa. Juzi hapa nilimwambia Mheshimiwa Waziri wamekuja wakaua tembo sita katika kijiji cha Merenga, wakawapiga wakaua wakang’oa meno wakaenda. Kwa hiyo, sasa hivi majambazi hawasumbuki kwenda kutafuta tembo hifadhini maana tembo wanakuja huku kusambua wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambie Wizara ya Maliasili na Utalii chukua hatua ya ku-protect wananchi wa Serengeti, Bunda na Tarime dhidi ya tembo. Kama hamtafanya hivyo tembo wanaenda kuisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni WMA.WMA ni chombo cha wananchi, wananchi wameji-organize wakatoa maeneo ya wakaunda WMA. Leo Wizara ndiyo inakusanya mapato yanayotokana na WMA kwa nini? Kwa mfano, tumeenda Babati kwenye ile WMA ya Burunge Wizara inakusanya mapato, imekusanya shilingi bilioni sita inawapelekea milioni 800 for what? Unakusanya bilioni sita unarudisha milioni 800 itafanya nini? Kwa hiyo, mimi niiombe Serikali, suala la WMA ukusanyaji wa mapato, uendeshaji wa WMA waachie WMA wenyewe, waendeshe wenyewe, wakusanye mapato yao, wajiletee maendeleo wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine linalotesa WMA ni single entry. Tunaomba Serikali ifanye utaratibu wa kurekebisha bila kurekebisha issue ya single entry WMA zitakufa. Kule kwangu Serengeti WMA ya Ikona sasa hivi mahoteli yaliyokuwa ndani ya hifadhi wawekezaji wameanza kuondoka, kwa sababu hakuna wageni. Serikali naomba mrekebishe hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni mauaji, kwangu Serengeti wameuwawa watu 50 na askari wa wanyamapori, ninayo taarifa ambayo nimeandikiwa na Serikali za Vijiji, Watendaji wa Vijiji ambavyo viko kandokando mwa hifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba orodha hii nitakuletea uone askari wa wanyamapori wanauwa Watanzania wenzao kisa amekanyaga ndani ya hifadhi anapigwa risasi anauawa. Mimi binafsi Ryoba nimeshuhudia wameuwa, hivi huu ndiyo utaratibu au ndiyo maana Magufuli ameweka Katibu Mkuu mwanajeshi, Mwenyekiti wa Bodi Waitara mwanajeshi ili kuwaua Watanzania wanaoingia hifadhini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwangu wameuwawa vijana 50, huu ndiyo utaratibu wa Tanzania kuua vijana wake? Ndiyo utaratibu wa Serikali ya CCM? Hebu ninaomba Serikali chukua hatua, kama hamtachukua hatua nitawashughulikia mwenyewe. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine…
MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Ryoba dakika zako zimeisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Nina jambo moja. WMA ni sehemu ya ardhi ya vijiji kwa maana kwamba Serikali za Vijiji na wananchi wao walikaa wakatoa hayo maeneo wakaunda WMA ili wanyamapori wakiingia humo wao wawekeze wapate mapato. Ni vizuri Waziri afahamu sera na sheria iliyoanzisha WMA ilikusudia nini, ilitaka kugatua madaraka kuyapeleka kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa WMA zimeundwa lakini mmeanza kuziua kwa kuanzisha kitu kinaitwa single entry. Ikona WMA ambayo ndio WMA kioo ambayo ina-shine kuliko WMA zote, mmeiua. Camps zote na hoteli zilizokuwa zimewekeza kwenye ile WMA wameanza kuondoka kwa kukosa wageni. Mwaivaro ni camp ambayo ilikuwa inapata wageni 400 kwa msimu sasa hivi wameshuka mpaka 70. Camps nyingi pale zimeondoka kwa sababu ya issue ya single entry. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri Mheshimiwa Waziri afahamu kwamba ili uende Ikona WMA lazima utokee Arusha na ukitokea Arusha lazima u-cross Serengeti National Park, kwa ku-introduce mfumo wa single entry wageni hawaendi tena Ikona WMA, you kill it. Sisi tunasema ahsante, yeye aue tu lakini kwenye ardhi ile sisi tutafuga ng’ombe na tutalima tumbaku kwa sababu hawataki sisi tufanye conservation. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamekuja hapa Wenyeviti wa Serikali za Vijiji wa maeneo yanayounda Ikona WMA, wamekuja Madiwani na wajumbe wa WMA tukaenda mpaka kwa Mheshimiwa Waziri akasema ataishughulikia hii ya Serengeti ni very unique, baadaye akaniambia Kamati imekataa. Mimi nikachukua jukumu la kwenda kwenye Kamati ya Maliasili na Utalii hata hawana habari, sasa ni Kamati ipi ilikataa? Sasa mimi nataka leo kwa dakika hizi tatu ambazo nimepewa atakapokuja ku-wind-up aniambie yuko tayari kuangalia upya mfumo huu wa single entry au wapo tayari kuua hizi WMA?

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. MARWA R. CHACHA: Kama msipopitia upya kanuni hizi zilizounda WMA, you will kill it na sisi hatuna shida tutachunga tu ng’ombe mle.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kuwashukuru wananchi wangu wa Jimbo la Serengeti, lakini pia nichukue nafasi hii kuwapa pole kwa tatizo kubwa la njaa walilonalo. Nafahamu wana hali mbaya kweli kweli, lakini niwaambie tu Serikali imekubali kufanya tathimini ya mahindi yaliyopo Shinyanga kwenye ghala la Serikali na watapata mgao wa mahindi kwa ajili ya kupunguza mfumuko wa bei. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya mchango huo, sasa nijielekeze moja kwa moja kwenye Wizara husika. Naomba Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wako mnisikilize kweli kweli hapa.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2016 mmekuja ndani ya Wilaya ya Serengeti kuhusu barabara ya Makutano
- Mgumu - Mto wa Mbu. Ni barabara ambayo imeanza kujengwa tangu mwaka 2013 mwezi wa tatu. Kipande cha kilometa 50 kuanzia Makutano mpaka Sanzate, mwaka 2016 nimeongea hapa sana; sasa hivi ninavyoongea hapa wamepewa almost shilingi bilioni 26 kama sikosei, lakini mpaka leo miaka zaidi ya minne bado hata kilomita moja haijakamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri alipokuja Jimbo la Serengeti kutembelea ile barabara, bahati nzuri tulikuwa naye, tulikaa tukaongea na alitoa tamko kwenye vyombo vya habari kwamba ikifika mwezi wa nne, kama hata kilometa moja haijakamilika, hawa wakandarasi tunawatumbua. Mheshimiwa Waziri, huu ni mwezi wa ngapi? Hata kilometa moja bado.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka Mheshimiwa Waziri anapokuja ku-wind up aniambie lile tamko alilolitoa kwenye vyombo vya habari na huu ni mwezi wa nne umeisha, hata kilometa moja bado haijakamilika, umechukua hatua gani kulingana na maneno aliyoyasema ambayo kimsingi wananchi wa Mkoa wa Mara, Musoma, Bunda na Serengeti walimsikia akitoa tamko. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Waziri, barabara hii ilitakiwa itengenezwe kwa kiwango cha lami kuanzia Makutano mpaka mpaka wa Hifadhi ya Serengeti National Park pale Tabora B; naona mmekomea pale Mugumu Mjini. Kilometa 18 hazieleweki. Naomba Mheshimiwa Waziri anapokuja kusema, atuambie hizi kilometa 18 kutoka Mugumu mpaka mpakani mwa Hifadhi ya Serengeti kwa maana ya geti la Tabora B, wataitangaza lini?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye barabara hii mwaka 2016 imetengewa shilingi bilioni 20; upande wa Arusha shilingi bilioni nane na upande wa Mara shilingi bilioni 12. Sasa mwaka huu mpaka ninavyoongea kipande ambacho kimetangazwa cha kuanzia Mugumu kwenda Nata na Isenye bado mkandarasi hajapatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaenda sasa kupitisha bajeti ya Mheshimiwa Waziri na Mkandarasi hajapatikana, nitaomba aseme chochote kuhusu upatikanaji wa mkandarasi wa kujenga hii barabara. Na mimi namwomba Mheshimiwa Waziri, bahati nzuri yeye sio mwanasiasa, amekuja pale nimemwona, hana mambo ya ubaguzi ubaguzi kama wengine, nampongeza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri anisaidie ili barabara hii ikamilike. Kimsingi, tunawapenda wakandarasi wa ndani, lakini kama hawawezi kufanya kazi kwa mujibu wa mkataba, kwa nini tuendelee kuwa-entertain?
Mheshimiwa Naibu Spika, ni vizuri ukumbuke Mheshimiwa Waziri, hii barabara ilianza kuwekwa kwenye Ilani ya CCM tangu enzi za Nyerere. Nyerere akaondoka akaja Mwinyi, akaja Mkapa; na wakati wa Mkapa kumbuka pia Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Magufuli ndiye aliyekuwa Waziri wa Ujenzi. Akaondoka, amekuja Kikwete; Mheshimiwa Dkt. Magufuli huyo huyo ndiye alikuwa Waziri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikwambie tu kwamba wananchi wa Serengeti na wananchi wa Mkoa wa Mara, walimpa kura Mheshimiwa Dkt. Magufuli kwa sababu walijua akiwa Rais, hizi barabara zitakamilika upesi. Sasa tunaenda 2020 sijui mtasemaje kama zitakuwa hazijakamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, barabara ya Tarime - Mugumu inafanyiwa feasibility study. Wananchi wa Jimbo la Serengeti wanataka wajue ni lini barabara hii itaanza kulimwa? Kwa hiyo, utakapokuja naomba useme kuhusu barabara hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nilitaka niseme, tuna barabara ya Musoma inaitwa Nyankanga - Rung’abure ambayo kimsingi mkoa kwa maana ya TANROADS wameanza kujenga kilometa mbili, wameanza kidogo kidogo. Kwa hiyo, naomba kwa niaba ya wananchi wa Serengeti na wananchi wa Mkoa wa Mara, barabara hii iingizwe kwenye barabara za kufanyiwa upembuzi yakinifu.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka niseme, ni vizuri mfahamu kwamba Hifadhi ya Serengeti ambayo ndiyo hifadhi inayoongoza Afrika kwa kuingiza watalii wengi na watalii wengi wanaoingia Hifadhi ya Serengeti wanatokea Kenya, ni vizuri mfahamu umuhimu wa barabara hii kwamba ni kiungo kikubwa cha kiuchumi katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni vizuri mfahamu kwamba Serengeti National Park ambayo ina tembo na simba wengi, wanaathiri watu wa Serengeti, ni vizuri mkafahamu ni mbuga ambayo duniani inatambulika, lakini unapoenda Serengeti unatwanga vumbi kuanzia Bunda mpaka Mugumu; kuanzia Tarime mpaka Mugumu na kuanzia Musoma mpaka Mugumu, sidhani kama mnamtendea haki hata Baba wa Taifa ambaye jana tulikuwa tunamuenzi kwa sababu ya makubaliano ya Muungano walioufanya na Rais wa Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine naomba Mheshimiwa Waziri anisaidie, katika Jimbo la Serengeti, bado hali ya mawasiliano kwa maana ya minara ni shida kweli kweli. Mwaka 2016 nilisema hapa kwamba ukienda kwenye maeneo ya mbuga yetu ya Serengeti ambako kimsingi tuna population kubwa mle ya watalii na nini, mawasiliano ni shida kwa maeneo ya Robo, Birira, Seronera na maeneo mengine ya mbuga yanahitaji mawasiliano ya uhakika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika Wilaya ya Serengeti, kuna maeneo ambayo tunahitaji minara. Sasa namwomba Mheshimiwa Waziri, kwenye hili la minara, naomba uniambie, ni lini maeneo hayo yatapata minara ya simu, ama Vodacom ama Halotel? Kwa hiyo, ni jambo la msingi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwahiyo, nachukue nafasi hii kukuomba hayo mambo ya msingi ambayo wananchi wangu wa Serengeti wamenituma, wanataka kusikiliza kutoka kwako Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, nashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. MARWA R. CHACHA: Naomba nianze na hii ya ukurasa wa 173. Mheshimiwa Waziri kwanza nichukue nafasi hii nikupongeze wewe na Naibu wako, kwa kweli ni moja ya Mawaziri ambao mnajitahidi ila shida tu ni kwamba hamna hela, kwahiyo hapa hata tukiwaadhibu hakuna lolote. Sasa mimi niwashawishi Wabunge kwamba wakubali, wasikubali Wizara ya Fedha ile shilingi 50 iongezeke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Maji, hatuwezi kufanya hadithi hapa ya kuwafurahisha wananchi huko nje, lakini sisi Wajumbe wa Kamati ya Maji hukio ndani ndiyo tunafahamu uhalisia wa shida ya maji nchi hii sasa hiyo iongezeke, Mheshimiwa Waziri wewe furahi hiyo lazima iongezeke.

Sasa nilitaka wakati mnakuja kujibu Mheshimiwa Waziri hebu nisaidie, kwenye ukurasa wa 173 Mji wa Mugumu kwenye usambazaji wa maji kuna hizi fedha bilions almost 19 kutoka Serikali ya India. Nataka kujua na wananchi wa Serengeti wa Mugumu wanataka kujua ni lini zinakuja ili kazi ya usambazaji wa maji ianze, maana ile ya uchujio inaendelea vizuri na nikushukuru sana kwa kusukuma naona Yule mkandarasi anakwenda speed kweli kweli Mungu akubariki sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme moja tu, kwamba kuna hii Programu ya Maji Vijijini vimechimbwa visima vingi lakini wananchi wetu wa vijijini hawawezi kuendesha kwa kutumia majenereta na hata maeneo mengine ambayo yana umeme bado wnanachi wetu wanakuwa ni shida kuendesha miradi hii. Kwa hiyo mimi ningeomba Mheshimiwa Waziri kama jinsi tulivyoenda Shinyanga tukaona ule mradi wa Maganzo wanatumia solar, wanatumia na zile prepaid meter, naomba Wizara ichukue jukumu la kuhakikisha ya kwamba, miradi ya maji vijijini wanatumia umeme wa jua katika uzalishaji wa maji, hilo ni la msingi sana bila hivyo hii miradi itakuwa hapa tu na haifanyi kazi yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine ni kwenye umwagiliaji, unapokuja ku-wind up niambie mabwawa ya umwagiliaji ya maji ambayo tayari yamekwishatumia fedha za Serikali ya Bugerera kule Nata, Nyamitita kule kata ya Ling’wani, Mesaga kule kata ya Kenyamonta nataka kujua progress yake ikoje? Kwa hiyo, unapokuja ku-wind up note that, ninahitaji kusikia na wananchi wa Serengeti wanahitaji kusikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambi lingine nilitaka niseme, ukiangalia Sera ya Maji ya Namibia, wao kwenye sera yao wanaita Water For Survival. Wanatenga asilimia 60 ya bajeti yao kwa ajili ya maji kwa nini? Maji ndiyo chakula, bila maji hatuwezi kupata mazao ya chakula, leo Tanzania kila kona wananchi wanalia njaa. Lakini kama tungelikuwa na kilimo cha umwagiliaji kila kona naamini kungekuwepo na chakula cha kutosha; lakini leo tunalia. Ukiangalia kwenye takwimu maeneo ambayo ardhi inatumika kwa ajili umwagiliaji ni sehemu ndogo sana.

Kwa hiyo, mimi ningependekeza kwamba kwenye bajeti zinazokuja, kama kweli tunahitaji kufanya mapinduzi ya viwanda katika Taifa hili ni lazima tuwekeze kwenye miradi ya maji ya umwagiliaji. Kama hatuwezi kuwekeza kwenye miradi ya maji ya umwagiliaji hayo mapinduzi ya viwanda sijui viwanda vya namna gani, labda viwanda vya kuchomelea.
Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Malawi pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Amani na Usalama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nami niweze kuchangia Itifaki hii naomba nianze na hii Itifaki ya Amani na Usalama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimejaribu kuipitia vizuri na nimeilewa ni nzuri. Sisi kama nchi tunapaswa kuiridhia lakini kuna mambo machache ningetaka niseme, kwamba kuna nchi zimejiunga na zingine hazijajiunga na kwa kuwa Itifaki hii lengo lake ni kutatua migogoro ndani na nje ya nchi wanachama, kuzuia mauaji ya kimbari, kupambana na ugaidi, kupambana na uharamia na kadhalika ni jambo zuri sana. Hata hivyo, nchi hizi za Jumuiya ya Afrika Mashariki zinaongozwa kwa mujibu wa Katiba ya nchi zao na Katiba hizi zimetoa haki kadha wa kadha, lakini unakuta katika nchi hizi, viongozi ambao wako madarakani wanaamua kukanyaga Katiba ya nchi hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Katiba imetoa fursa ya demokrasia, Katiba imetoa fursa ya uhuru wa mawazo, Katiba imetoa fursa ya uhuru wa kujieleza, Vyama vya Siasa na kadhalika, anatokea mtu anakwenda kinyume na Katiba, huyu mtu siyo gaidi? Kwa hiyo, gaidi siyo wale wa kuvamia peke yake ni pamoja na viongozi wanaokwenda kinyume na Katiba ya nchi, wanaokwenda kinyume na sheria ya nchi. Kwa hiyo, nimefurahi kuona hii Itifaki kwamba pamoja na wale wanaozuia vyama vya siasa visifanye mikutano kwa mujibu wa sheria itawashughulikia, nimefurahi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ni vizuri mfahamu kwamba, amani siku zote ni tunda la haki. Kama viongozi wa nchi hizi ambao wako madarakani hawataki kutenda haki, hakutakuwepo na amani, ni vizuri tufahamu Muasisi wa amani ni Mungu mwenyewe. Kama viongozi wa nchi hizi ambao wako madarakani wanawaona wananchi wenzao hawana haki ambayo haki imetolewa kwa mujibu wa Katiba, Mungu atawahukumu siku moja na namshukuru Mungu ameanza kuwahukumu wengine leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi kama Mheshimiwa Ryoba ninaikubali hii Itifaki iko sawa sawa, Bunge liridhie ili wale viongozi wanaokwenda kinyume na Katiba ya nchi, kuzuia vyama vya siasa visifanye mikutano kwa mujibu wa sheria waweze kushughulikiwa na umoja huu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

T A A R I F A . . .

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, huyu mtu hata hajasoma Kanuni, kwanza hajui Kanuni, lakini la pili hii Itifaki inaongelea amani na ukisoma ndani yake kuna kuzuia ugaidi, mauaji ya kimbari, nini source ya mauaji ya Kimbari? Ni Viongozi walio madarakani kutokutenda haki. Fuatilia kule Rwanda na Burundi nini kilitokea? Viongozi waliokuwa madarakani hawakutenda haki. Msipotenda haki kunaweza kukatokea mauaji ya kimbari, kwa hiyo ni vizuri haki itendeke ili watu wote wawe na amani. Msipofanya hivyo haina maana, ndiyo maana nikasema hii ni nzuri sana, kwa sababu itawazuia wale viongozi ambao hawatendi haki kwa wenzao. (Makofi)

Jambo lingine nilitaka niongelee hii Commission ya pamoja ya Bonde la Mto Songwe. Pamoja na Mbunge wa Singida Mashariki Mheshimiwa Tundu Lissu ametoa tahadhari hapa kwa sheria iliyopitishwa. Pia niungane naye kwamba ni vizuri jambo hili liangaliwe vizuri ingawa maudhui ya Itifaki hii ni mazuri sana kwa sababu jambo hili kimsingi lilitakiwa lifanyike muda mrefu sana kwa ajili ya kutoa manufaa kwa wananchi wa maeneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo pia mabonde mengi sana, kuna Bonde la Mto Rufiji, kuna Bonde la Mto Mara na Mabonde mengine ambayo kama mabwawa yangetengenezwa, kilimo cha umwagiliaji kikafanyika, wananchi wa maeneo husika wangepata faida kubwa sana. Kwa hiyo, pamoja na weakness za kisheria ambazo zimeonekana, ambazo naamini kupitia Bunge hili mtazipitia mkaangalia nini kinaweza kufanyika ili Commission hii iweze kutekelezwa, lakini kimsingi maudhui yake ni mazuri lakini angalizo kubwa ni mgogoro wa mpaka.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017.
HE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana. Naomba niseme machache kuhusu Kamati hii ya Miundombinu na hii ya Nishati.

Mheshimiwa Naibu Spika, huwa naona kuna Wabunge wamejiuzulu Ubunge wao na Madiwani eti wanamuunga mkono Magufuli kwamba amefanya mambo mazuri sana katika nchi hii. Huwa nakaa najiuliza mpaka leo sijapata majibu, kwamba Magufuli amefanya mambo makubwa kwelikweli. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikachukulia sample ya Mkoa wangu wa Mara mpaka leo haujaunganishwa na barabara ya lami na Arusha ambayo Muasisi wake ni Nyerere mwenyewe. Nyerere akafa akawaachia wengine kuongoza nchi hii mpaka leo na Magufuli amekuwa na historia ya kuwa Waziri wa Wizara hiyo kwa muda mrefu sana. Mwaka 2013 wameanza kutengeneza barabara ya kuunganisha Mkoa wa Mara na Mkoa wa Arusha wakaanza na kilometa 50. Imepita miaka sita kilomita 50 hazijakwisha hata kilometa sita tu wameshindwa kumaliza. Hiyo ndiyo Serikali ya CCM, nijiuzulu leo nimuunge mkono wakati barabara imemshinda. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2016/2017 ikatengwa shilingi bilioni 20 kwenye barabara hiyo, upande wa Mara bilioni 12 upande wa Arusha bilioni nane. Upande wa Arusha wakatangaza tenda wameshaanza kulima. Upande wa Mara bilioni 12 kipande cha Mugumu - Nata mpaka sasa hivi wanaendelea kutangaza tenda, bajeti ya 2016/2017. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi Ryoba niko tayari kujiuzulu kuwaunga mkono, lakini mbona sioni sababu ya kuwaunga? Nipeni sababu ya mimi kujiuzulu kuwaunga kama barabara ndogo tu ya kuunganisha Mkoa wa Mara na Arusha imewashinda. Kwa hiyo, bado, bado sana. Kwa hiyo, niwaambie wananchi wa Mkoa wa Mara adui yao ni CCM na Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi leo mkoa ambao ametoka Muasisi wa Taifa hili Mwalimu Julius Kambarage Nyerere hata Uwanja wa Ndege hakuna. Hakuna uwanja wa ndege wa maana Mkoa wa Mara. Nani leo, Waziri gani, Mbunge gani wa CCM asimame hapa aniambie Mkoa wa Mara haustahili kuwa na Uwanja wa Ndege tena wenye hadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2016/2017 ilitengwa bilioni mbili kwenye Uwanja wa Chato, baadaye nikasikia bilioni 39.15 zimetokea wapi mbona hatujawahi kuziona kwenye bajeti mniambie! Kama kweli mnampenda Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, unachukua bilioni 39 unapeleka Chato kuna nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, samahani Mheshimiwa Waziri wewe ni rafiki yangu lakini naongea mambo ya kitaifa kidogo inauma. Pale ambapo anatokea Muasisi wa Taifa hata uwanja wa ndege na barabara hakuna. Leo Mkoa wa Mara kwa mfano hakuna Jimbo hata moja ambapo wanakunywa maji safi na salama, hakuna! Asimame yeyote hapa aniambie Mkoa wa Mara kuna Jimbo lenye chujio, wapi? Tarime wanakunywa matope, Musoma Mjini wanakunywa jinsi yalivyo, wanaugua amoeba na minyoo hivyo hivyo, sasa ninyi niwaunge kwa lipi, si mnisaidie? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, unajua nilikuwa napita kwenye hiki kitabu cha Kamati ya Miundombinu, ninyi Wajumbe wa Kamati mniambie, nimesikia mmeitisha mpewe taarifa ya Uwanja wa Chato, Waziri amegoma kuwaletea na umetumia bilioni 39! Kwenye kitabu humu naangalia naona viwanja vingine, hivi uwanja wa Chato unajengwa au haujengwi na kama unajengwa kwa nini haumo humu? Wajumbe wa Kamati nataka majibu, kwa nini hauko humu? Wabunge nataka majibu kwa nini hauko humu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halafu mkandarasi anayejenga huo uwanja unajua ni nani? Ni yule ambaye ameshindwa kumaliza zile kilometa 50 pale Mkoa wa Mara, ndiyo amepewa Mayanga nani mwingine si ndiyo huyo? Kisa rafiki yake na nani, Magufuli, ooh haya, twende kazi.

M W O N G Z O . . .

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Msigwa naomba ukae. Mheshimiwa Ryoba naomba ufute hayo maneno halafu uendelee na mchango wako.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nifute.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, katika nchi hii Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi, ni moja ya Wizara hewa. Katika Wizara hewa ambazo zimewahi kuundwa ni hii na nina sababu. Nenda ukurasa wa nane wa hotuba walitengewa development bilioni nne, ukisoma pale anasema hadi kufika mwezi Aprili 2018 hakuna fedha iliyokuwa imetolewa, yaani maana yake sifuri, walipewa sifuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa unajua mimi ni Mwalimu, ukisahihisha ukamwekea mtoto sifuri, maana yake hewa, hakuna kitu. Sasa najiuliza kwa nini waliamua kutoa hii Wizara iliyokuwa pamoja na kilimo ili iwe peke yake! Sasa nimejua kwamba ilikuwa ni kutafutia washikaji ulaji, haikuwa na maana yoyote. Kama Wizara ya Mifugo na Uvuvi huwezi kutenga fedha za maendeleo maana yake ni nini? Wabunge wote mko hapa maana yake ni nini? Maana yake ni kwamba hawataki kusikia biashara ya wafugaji, hawataki kusikia habari ya samaki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nami niwaeleze wafugaji, Serikali hii ya CCM haina mpango na nyie. Hivi can you imagine wafugaji wanaoteseka nchi hii, kwa wale wafugaji ambao wako kandokando ya hifadhi na mapori ya akiba, ng’ombe akikanyaga hifadhini, ng’ombe mmoja laki moja ndiyo Sheria inasema.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi hapa mfugaji mmoja kutoka Jimboni kwangu Serengeti, ng’ombe 300 wote wamepigwa mnada amebaki maskini. Ng’ombe akikanyaga hifadhini laki moja, tembo akila heka tano shamba la mahindi mtu anapewa laki moja, hii ndiyo Serikali ya CCM. Tembo akila shamba la hekari tano, laki moja; ng’ombe akikanyaga tu pale hifadhini akakamatwa, ng’ombe mmoja fine laki moja, hutaki kulipa wanapiga mnada Mahakamani, hiyo ndiyo Serikali ya CCM. Kwa hiyo, hii Wizara kazi yenu ni nini? Kama hamuwezi kutetea wafugaji wa nchi hii kazi yenu ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wafugaji wanateseka, unajua tumekaa hapa kuna watu wanakula nyama tu hawajui tabu ambayo wafugaji wanakula. Utakwenda pale canteen utakuta kuna Wabunge wanakula hata hajui ng’ombe anavyofugwa, lakini ukimkuta anavyopinga ng’ombe humu. Wafugaji wetu wanapata shida, sasa nilikuwa naangalia kwenye ule ukurasa sijui watafanya nini mwaka huu, watatoa wapi hela? Ulega atatoa wapi hela? Haya wanayosema watafanya hela watatoa wapi? Kama mwaka uliopita wameshindwa kupewa hata mia, afadhali waje hata naweza kuwafadhili, kama Magufuli ameshindwa kuwapa hela, waje nitawasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye uvuvi ni balaa, yaani Ulega na Mpina wanataka wananchi wa Kanda ya Ziwa wale nini? Tulizoea kula dagaa, kula samaki sasa hivi hawataki kabisa na mitego yote, nyavu zote wamechoma na kuteketeza. Hata zile ambazo ziko kwa mujibu wa Sheria walikuwa wameigiza, ziko pale mpakani Sirari Mpina amezikataa. Akija hapa atuambie kwanini zile nyavu ambazo ziko pale mpakani amezikataa. Nataka majibu leo toka kwa Mpina, kama hatatupa majibu, mimi nitakamata shilingi yake na Wabunge wote wa Kanda ya Ziwa tutamsulubu kesho.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunataka majibu, kwa nini nyavu za wafanyabisahara zile ambazo ziko pale Sirari amezikataa ambazo ziko kwa mujibu wa sheria. Sasa hivi dagaa wameadimika Kanda ya Ziwa hakuna dagaa, hakuna samaki. Nilikwenda pale naulizia samaki wananiambia elfu 30, samaki mmoja shilingi elfu 30. Hivi Mheshimiwa Mpina anatoka Kanda ya Ziwa au anatokea wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli niwaombe Wabunge wa CCM kama wataunga mkono hoja, uchumi wa Kanda ya Ziwa ni samaki, uchumi wa Kanda ya Ziwa ni ng’ombe, ng’ombe wamepigwa mnada wamekwisha, samaki nao hawataki, sasa wanataka wafanye nini, wakaibe? Mheshimiwa Mpina wakaibe?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kimsingi nashangaa Wizara hii, hivi kazi yao ni nini?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Leo nitaongelea jambo moja mahsusi kwamba hizi National Parks zote za Tanzania ambazo kwa sasa zipo 16, iliundwa TANAPA 1959 kwa Sheria, Cap Na. 412 na kwa mara ya kwanza kabisa mwaka 1959 ilianzishwa Hifadhi ya Serengeti. Hifadhi ya Serengeti na hifadhi zingine zilianzishwa kwa mujibu wa Government Notes (GN) ambapo GN wakati huo ilikuwa inataja mipaka, mabonde fulani, mlima, mto, jiwe iko specific GN. Tangu wakati huo mpaka leo haikuwahi kutengenezwa ramani ya Serengeti National Park na hifadhi zingine. Kitu ambacho kimetokea na kinaendelea ni kwamba Wizara ya Maliasili na Utalii inapanua mipaka ya Hifadhi kinyume na GN. Ni jambo la ajabu sana nchi hii, tunawaonea Watanzania, tunawaonea watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwe specific, Serengeti National Park katika Wilaya ya Serengeti inapakana na Vijiji vya Merenga, Mbalibali, Machochwe, Nyamakendo, Bisarara, Mbilikili, hivyo vijiji eti TANAPA wanakuja kuweka mipaka kwenye vijiji ambayo iko kinyume na GN. Sisi walivyofanya hivyo tukatafuta GN, tukatafuta na hiyo ramani yao tukaenda Mahakamani na tumewashinda Mahakamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jaji alihamia site na zile beacon zilizowekwa enzi zile pamoja na namba zake Jaji alienda akaona nyingine wameng’oa, bahati nzuri nyingine walisahau kung’oa tukaikuta Jaji akaiona. Hii ni kuonyesha jinsi gani ambavyo TANAPA wanavamia na kuwanyang’anya wananchi maeneo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekit, sasa hivi nimeona wamehamia Tarime, nyie watu wa Tarime nendeni Mahakamani, GN iko wazi, inaeleza. Haiwezekani leo mkapora maeneo ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kibaya zaidi vijiji hivi vimepimwa vina ramani na vimepimwa na Serikali hiyohiyo. Kibaya zaidi inakuweje TANAPA ndiyo wanaenda kuweka beacon? TANAPA ni nani? TANAPA ni Waziri wa Ardhi? TANAPA leo wamepoka madaraka ya Wizara ya Ardhi, wanaenda kupima wenyewe? Sisi Serengeti tumesema hapana na Mahakama imetutetea imesema hapana, nyie TANAPA mlifanya makosa. Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla amka, usilale kuna watu wanafanya mambo visivyo huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sawa, unajua naumia sana maana wananchi wananyang’anywa maeneo yao ambayo wanamiliki kihalali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafugaji wanapata shida leo wanakosa maeneo ya kuchungia mifugo yao, inawalazimu kuingiza ng’ombe kwenye hizo hifadhi kwa sababu wamenyang’anywa maeneo yao. Kwa mfano, Pori la Mkungunero wamepanua hekari na hekari kutoka square kilometer 10,300 mpaka square kilometer 20,000, mmemeza vijiji vya Watanzania, Wamasai wa watu ambao hawajui kula kimoro au nyumbu. Ingekuwa ni kama sisi Wakurya tunaishi na wale wanyama tungekuwa tushawamaliza lakini Wamasai watu wa watu hawajui, mmewanyang’anya vijiji, Kigwangalla wewe ni mtoto wa mfugaji, Mheshimiwa samahani . (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla ni mtoto wa mfugaji. Wengi humu mnafahamu wafugaji wanapata shida kweli kweli, sasa mnataka nchi nzima iwe National Parks au WMA’s. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Wizara naomba tuwasaidie wafugaji wapate maeneo ya malisho na…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. CHACHA R. MARWA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi. Naomba nami nisome Mithali 29:1-2, halafu nitaendelea, inasema: “Aonywae mara nyingi akishupaza shingo atavunjika ghafla wala hapati dawa. Wenye haki wakiwa na amri watu hufurahi, bali muovu atawalapo watu huugua.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hali ni mbaya. Ukienda mtaani hamna hela, mimi sijui kwenye majimbo yenu, lakini mimi kwa Serengeti hela hakuna, wamepeleka wapi hela? Mheshimiwa Dkt. Mpango amepeleka wapi hela? Yaani hela hamna, hivi nini kimetokea? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nishauri, wala mimi siwezi kumlaumu Rais Magufuli, wala siwezi kuilaumu CCM; maana angalia kwenye kilimo; ukisoma ukurasa wa 15 ile namba tatu inasema sekta ya kilimo inayojumuisha mazao, mifugo na uvuvi ambayo inaajiri asilimia 66 ya Watanzania inachangia asilimia 30 ya pato la Taifa. Inaendelea kukua kwa kasi ndogo ya wastani wa 3%, nani kasababisha ikue kwa asilimia ndogo?

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mpango ameandika yeye, aliyesababisha kasi ya ukuaji wa kilimo ikue kwa 3% ni nani? Ni yeye kwa sababu gani? Njoo kwenye bajeti, kwenye kilimo mwaka 2016/2017, walitengewa bilioni 100.5 wakapewa bilioni mbili, asilimia mbili aliyesababisha sekta ya kilimo isikue ni nani, ni yeye ambaye hakupeleka fedha. Mwaka 2017/2018, ilitengewa bilioni 150, akapeleka bilioni 16, sawa na asilimia 11, nani kaua sekta ya kilimo, ni yeye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye Mifugo mwaka 2016/2017, ilitengewa bilioni nne, akapeleka 150 milioni yaani ni sawa na Landcruiser moja, sawa na 3%, nani kaua hii sekta ni yeye. Mwaka 2017/2018, mwaka huu wa fedha tulionao tulitenga sisi Bunge bilioni nne, amepeleka shilingi ngapi, sifuri. Nani kaua sekta ya kilimo na uvuvi na mifugo ambayo inaajiri 66% ya Watanzania? Ni yeye Mheshimiwa Dkt. Mpango na huyo Mheshimiwa ambaye wamekaa naye hapo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tusitafute mchawi kwamba kwa nini hela haiko mtaani, hela haiko mtaani kwa sababu hatujawekeza kwenye kilimo, mifugo na uvuvi. Kama tunataka hela iwe mtaani tupeleke pesa huko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo wanasema viwanda; kama kuna viwanda ambavyo tungewekeza vikaisaidia nchi cha kwanza ni Kiwanda cha Mbolea. Hebu aniambie Mheshimiwa Waziri wa Fedha tuna viwanda vingapi vya mbolea? Kila leo tuna-import mbolea kwa ajili ya nchi yetu, tunatumia pesa nyingi za kigeni kwenda kununua mbolea nje, pesa ambazo zingefanya mambo mengine. Mheshimiwa Waziri Mkuu yuko hapa, kwa nini Tanzania tusijenge kiwanda cha mbolea? Nini tunashindwa? Yaani kama kweli kiwanda tu cha mbolea cha kuwasaidia wakulima wetu tunashindwa sasa tunaongelea viwanda, viwanda gani? Maana kama kuna kiwanda cha kujenga ni cha mbolea.

Mheshimiwa Spika, maana tukisema tuna viwanda, viwanda gani? Kama mbolea hakuna una-import kila kitu unategemea nini? Kwa hiyo, haya mambo yanauma sana, hebu tusaidie wakulima wa Tanzania. Tuache mambo ya vyama, mimi ni CHADEMA lakini ninachoangalia hapa Utanzania wetu kwanza. Kule mtaani hamna hela, Mheshimiwa Jenista kuna hela kule? Hamna. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hebu niambieni.

Mheshimiwa Spika, ahsante. Mazao ya biashara; hivi katika mazao ya biashara ya nchi hii ni mangapi, tumbaku iko wapi? Serengeti tulikuwa
tunalima tumbaku, pale Serengeti tumbaku ilikuwa inaleta bilioni kumi na sita mpaka bilioni ishirini. Wananchi unakuta bilioni kumi na sita ikimwagika kwenye ile wilaya, wilaya inachangamka. Sasa hivi Alliance One kampuni pekee iliyokuwa inafanya biashara ya tumbaku imeondoka. Unategemea hela itakuwepo, mzunguko wa hela utakuwepo, hakuna.

T A A R I F A . . .

MHE. CHACHA R. MARWA: Yuko sawa, si kwamba Watanzania wanashindwa kuzalisha tumbaku, wamezalisha nyingi imekosa soko, yuko sawa. Watanzania wamezalisha nyingi imekosa soko, nani alaumiwe? Wamevuruga wenyewe makampuni ya kununua. Watanzania wako tayari kulima tumbaku, kule Serengeti wamehama na maeneo mengine Songea huko walikuwa wanalima tumbaku, maeneo mengine wamevuruga. Nenda pamba, Mheshimiwa Waziri Mkuu namshukuru sana. Hebu tumpigie makofi Waziri Mkuu kafanya kazi kubwa. (Makofi)

T A A R I F A . . .

MHE. CHACHA R. MARWA: Mheshimiwa Spika, Serengeti wanalima tumbaku. Duniani yako makampuni manne yanayonunua tumbaku na Tanzania yako manne. Kwa hiyo, nadhani sijui anaongea nini, Watanzania hawajashindwa kuzalisha tumbaku, wanazalisha kwa wingi hata Serengeti ipo mpaka leo, imeshindwa kununuliwa.

Mheshimiwa Spika, pamba Mheshimiwa Waziri Mkuu amefanya kazi nzuri, ndiyo maana nikasema tumpigie makofi amefufua zao la pamba, tatizo soko. Mpaka leo ninavyoongea Serengeti hakieleweki, wananchi wamekaa na pamba yao hawajui nini cha kufanya. Mheshimiwa Waziri Mkuu aangalie hawa wataalam wa Wakuu wa Mikoa sijui watu gani wanawadanganya. Ukienda kwa wananchi, mimi Mbunge wao napigiwa simu na si mimi peke yangu, Wabunge wengi wanaotoka kanda ya ziwa wanasumbuliwa na wananchi wao kuhusu ununuzi wa pamba, ni tatizo.

Mheshimiwa Spika, alizeti; mimi nimshukuru Waziri Mheshimiwa Dkt. Mpango huyu, wamepandisha ile kodi ya ku-import mafuta safi ili tuzalishe alizeti kwa wingi tuwe na viwanda vyetu. Hata hivyo, Mheshimiwa Dkt Mpango nikitaka kujenga kiwanda cha kuchakata alizeti kodi kwenye zile mashine ninazo-import si aondoe.

Mheshimiwa Spika, mimi siyo Mwanauchumi lakini ili u-import kuna VAT 18%. Sijui kuna import duty, sijui kuna nini, si waondoe. Kama kweli wanataka tujenge uchumi wa viwanda waondoe kodi kwenye mashine ambazo tuna- import kwa ajili ya viwanda, kama Ghana walivyofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna issue ya corporate tax sijui na nini, naomba nihame hapo niongelee mambo ya wakandarasi. Wakandarasi sasa hivi wa Kitanzania wana hali ngumu, sijawahi kuona. Wakandarasi wana hali ngumu, ndiyo hiyo naomba kwenye wale wanaofanya mambo ya ujenzi, vifaa hivi vya ujenzi wanavyo-import, wapunguze kodi. Tutengeneze wazawa ambao watafanya miradi yetu wenyewe. Tunao vijana wazuri wenye makampuni lakini…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, sijui niseme nini hali ni mbaya kweli kweli, naomba tuwasaidie Watanzania.

Mheshimiwa Spika, nakupenda sana, nikwambie na ukisimama vizuri hawa jamaa watanyooka hapa, nchi itaenda vizuri, simama, mimi nakuunga mkono. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI anisikilize kwa makini maana Jumatatu nitaondoka na shilingi yake. Mheshimiwa Waziri wa Afya alinipa barua inayoonesha Kituo cha Iramba, Kijiji cha Nyagasense, Kata ya Kenyamonta inapata milioni mia saba; na Waziri wa Afya alituma wataalam wakaenda kule wakahamasisha wananchi wakachangia viashiria wakapeleka mchanga wanasubiria milioni mia saba. Mpaka leo TAMISEMI wamepindua milioni mia saba wamepeleka kwenye jimbo lingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kenyamonta walimpa Mheshimiwa Magufuli kura, wanataka kutwambia 2020 wasimpe, si ndiyo? Kwa hiyo, nataka majibu Jumatatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, mwaka jana Mheshimiwa Jafo ulikuja Serengeti tukampeleka Hospitali yetu ya Wilaya ya Serengeti tunayojenga kwa nguvu za wananchi na wadau mbalimbali na tumemaliza wing ya kwanza; akatuahidi na akaniahidi tutapata milioni mia saba, lakini hatukupata. Mwaka huu tena sijaona chochote ingawa ameniahidi kwamba ameweka vizuri na kwamba tutapata milioni mia tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, amekuja pale Mheshimiwa Waziri, tumempeleka kwenye ile hospitali na ameona jitihada zetu. Amekuja Mheshimiwa Makamu wa Rais tumempeleka pale akaahidi kutusaidia; juzi tumempeleka Mheshimiwa Waziri Mkuu, sijaona chochote. Hebu naomba Mheshimiwa Waziri aseme kwamba katika Hospitali ya Wilaya ya Serengeti ambayo itahudumia mpaka watalii hawaoni sababu ya kutenga chochote kwa ajili ya wilaya ile? Kwa hiyo, nataka majibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niingie kwenye elimu, naomba niongelee elimu bure. Serikali ya CCM sasa hivi kila mtu akisimama anasifia elimu bure. Wametenga na wanapeleka shilingi bilioni mia moja sabini na mbili kwenye elimu. Ukienda kuna matatizo chungu nzima kwenye shule zetu za msingi, watoto kwenye darasa moja wamerundikana, hakuna madarasa ya kutosha. Tuna upungufu nchi nzima wa madarasa laki 264,594.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya vyumba vya madarasa ni mbaya. Kwa nini wasingetumia pesa hizi kujenga madarasa? Ukienda kwenye shule zetu hali ya elimu ni mbaya, hakuna Walimu, wameamua kutoa Walimu wa sekondari wanawapeleka katika shule za msingi, kweli wataweza ku-deliver? Wata-deliver nini? Watafundisha nini? Hali ya Walimu ni mbaya na ukienda kwenye hali ya Walimu wa sayansi ni tatizo kweli kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba tumpigie makofi Mheshimiwa Kikwete, alifanya kazi kubwa sana. Mimi ni mojawapo ya matunda ya Mheshimiwa Kikwete, nilienda crush program baada ya kumaliza form six, nikasoma mwezi mmoja nikaenda kufundisha. Baada ya miaka miwili nikaenda chuo kikuu nikafanya Bachelor of Science and education nikamaliza nikaenda kufundisha, nilikuwa nafanya vizuri na nina wanafunzi wangu sasa hivi ni madaktari; nilifanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kikwete alikuwa very creative kwenye suala la ualimu; ndipo Mheshimiwa Kikwete alipoona kwamba kuna tatizo la Walimu wa sayansi akaanzisha program maalum chuo kikuu cha UDOM ili kukabiliana na tatizo la Walimu wa sayansi. Serikali ya CCM; yuko hapa ndugu yangu Mwalimu wangu Mheshimiwa Ndalichako, hivi kweli wanawapenda watoto wa nchi hii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekondari ukienda hakuna Walimu wa hesabu hakuna wa fizikia, hakuna wa kemia, hali ni mbaya, are you serious, mko serious kweli? Mimi ni
Mwalimu, wakati wa likizo nakwenda kufundisha kule, hali ni mbaya. Wanasema Serikali ya viwanda wanatoa wapi Walimu? Lazima muwe na special program kwa ajili ya Walimu wa sayansi, lazima watengeneze incentives za kuwavutia wanafunzi kusoma sayansi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hata ukiwa Mwalimu wa sayansi haina maana, ndiyo maana hata mimi niliondoka huko, mimi ni Mwalimu wa kemia na baiolojia. Yaani Mwalimu wa sayansi ukienda kwenye shule za sekondari, Mwalimu kwa mfano wa kemia ni Mwalimu mmoja, labda kemia na baiolojia; unafundisha kuanzia form one mpaka form four, wanafunzi karibu 2,000, wewe mwenyewe, hakuna incentives yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, akina Mheshimiwa Jafo washauri Mheshimiwa Rais aje na special program kwa ajili ya sayansi. Ndugu zangu tunawashauri bure mkiona ni la muhimu chukueni mkiona halina maana... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kama kuna wakati Serikali ya CCM imewahi kupigwa upofu na Mungu basi ni wakati huu. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, maji ni siasa, maji ndiyo kila kitu nchi hii; na kama ukitaka uendelee kuwepo madarakani, hakikisha ya kwamba umewapelekea Watanzania maji. Ukienda vijijini wananchi wanalia, wanalalamika maji, ukienda mijini wananchi wanalia wanalalamika maji. Lakini unashangaa watu hawa hawaoni, hawasikii, hawaelewi! Fedha nyingi wamepeleka sijui wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilitamani Waziri wa Fedha awepo hapa, naona hayupo, maana huyu ndiye tatizo. Nilikuwa Mjumbe wa Kamati ya Kilimo na Maji, kilio kilikuwa ni hiki hiki tangu niingie Bungeni mpaka leo, fedha haziendi.

Mheshimiwa Spika, walitenga zaidi ya shilingi bilioni mia sita haziendi, leo wanaleta tena. Shida si hawa Mawaziri waliokaa hapo, shida ni huyu Waziri wa Fedha na Naibu wake, hawa ndio tunatakiwa tuwasulubu kweli kweli. Kwa hiyo, mimi niwashukuru sana Waziri wa Maji na Naibu wake, wanajitahidi, wanafanya kazi nzuri ila wanaangushwa na huyu mtu huwa anakaa hapa. Sasa amekimbia ngoja nimuache. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri alikuja Serengeti, akauona ule mradi wa maji pale Mugumu, una zaidi ya miaka mitano. Kama asingekuja kwenye mradi ule maana yake hakuna chochote ambacho kingekuwa kinaendelea pale, lakini ujio wake umesababisha mambo sasa yaende vizuri. Ni ushauri tu kwamba jitahidini, kwa sababu ninyi ndiyo mnatoa fedha, jitahidini iwezekanavyo, nendeni kwenye miradi yote nchi nzima. Ni bahati mbaya sana hamna chombo kinachosimamia kwa niaba yenu. Ulikuja Serengeti, ulienda kwenye ule Mradi wa Mugumu. Kuna Mradi wa Maji Nyagasense, ulitumia zaidi ya shilingi bilioni 500 mpaka ninavyoongea hakuna maji! Imetulazimu kama Halmashauri tuutangaze upya, lakini fedha za wananchi zilishatumika pale.

Mheshimiwa Spika, kuna Mradi wa Maji Kata ya Kibanchebanche, Kijiji cha Kibanchebanche, mradi ule umetumia shilingi milioni 557 na kampuni iliyokuwa inajenga mradi ule inaitwa Gross Investment Company, wamejenga DP, wamejenga tank, power house lakini chanzo cha maji hakuna, na mkandarasi alishatokomea na ndiyo maana nilikuwa nalia Mheshimiwa Waziri ungefika pale Serengeti nikakupeleka mwenyewe ukaona pesa zimechukuliwa, lakini chanzo cha kuleta maji kwenye tenki hakipo mpaka leo na hakuna chochote kinachoendelea.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nikuombe wa hili Mheshimiwa Waziri, ama wewe ama naibu wako, naomba aje twende Serengeti akajionee mwenyewe, lakini wakati anakuja aje na wataalam wake na hatua ya nini kifanyike kwa ajili ya ku-rescue hizi shilingi milioni 557 ambazo zimetumika lakini hakuna maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, pia niombe wakati unapokuja kujibu, kuna zile fedha ambazo ni mkopo kutoka Serikali ya India, nataka kujua zimekwamia wapi? Maana tangu bajeti ya kwanza tulianza kuzungumzia fedha za mkopo kutoka Serikali ya India, imepita miaka hiyo mpaka leo hazijulikani. Kwa hiyo naomba unapokuja ku-wind up ueleze wananchi wa Mugumu ni lini watasambaziwa maji maana Mradi wa Maji Mugumu ni moja ya miradi ambayo ilikuwa inapata hizi fedha za kutoka India.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine ninaomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja pia aje na ufafanuzi. Mradi wa maji Mugumu uko class gani. Najua uko class C, je, unastahili kupewa ruzuku kwa ajili ya kulipia umeme? Na kama unastahili kupewa ruzuku, nani yuko responsible na kulipa hiyo fedha maana wananchi wanapata shida, kila siku tunachangishana tu kwa ajili ya kulipia maji lakini ni mradi ambao unastahili kupewa ruzuku na Serikali kwa ajili ya kulipia bill.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri, mimi niwashukuru mnafanya kaz nzuri lakini mnatakiwa kwenda mradi mmoja baada ya mwingine. Ahsante sana nashukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru. Naomba niseme mambo machache kwenye Wizara hii ya Madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania ina madini mengi sana na pengine Tanzania ingekuwa Korea ya Kusini ingekuwa ni nchi tajiri sana. Nahisi kuna kitu ambacho kama nchi hatujakiona. Tunapambana kuwekeza kwenye vitu ambavyo havina faida, tunaacha kuwekeza kwenye madini ambayo nchi kama Tanzania tungekuwa ni miongoni mwa nchi tajiri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kila kona ya nchi kuna madini, leo nikimuliza Mheshimiwa Waziri ana-enroll wanafunzi wangapi wanaoenda kusomea madini? Chuo cha Madini kipo hapa Dodoma kina-enroll wanafunzi 70 kwa mwaka kwa ajili ya diploma, mpo hapa Mawaziri watatu kina-enroll wanafunzi 70. Kwa hiyo, hatujawekeza vya kutosha kwenye madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niishauri Serikali kwamba nchi hii kama kuna sehemu tunaweza tukawekeza na tukatoka haraka ni kwenye madini na tuanze na elimu, Watanzania wengi hawajui madini. Hata humu ukiuliza Wabunge wengi dhahabu inafananaje inawezekana physically hawajawahi kuona dhahabu ikoje. Wanaona tu kwenye mikufu labda na kwenye Siwa hapo lakini yenyewe kama yenyewe hawajawahi kuiona lakini dhahabu iko kila kona. Kwa hiyo, niiombe Wizara hebu wekeni fedha za kutosha kwenye elimu inayohusu madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, nchi kama Afrika ya Kusini imeendelea sana kwa sababu waliokuwa wanachimba dhahabu Afrika ya Kusini, wale Makaburi ni wa palepale. Faida yote waliyokuwa wanaipata walikuwa hawapeleki Uingereza walikuwa wanawekeza Afrika ya Kusini. Sisi kama Taifa tumewasaidiaje wazawa kumiliki migodi mikubwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna wachimbaji wadogowadogo ukiangalia namna wanavyochimba yaani ni aibu. Kama Taifa tunahangaika kwenda kuwekeza billions of money kwenye bombardier, lakini fedha hizo tungepeleka tukawasaidia wachimbaji wadogowadogo wakawa na migodi mikubwa, wakawa kama Acacia, wakawa kama GGM, Taifa tungeondokana na umaskini tulionao. Kwa hiyo, namtaka Mheshimiwa Waziri anapokuja kujibu, hebu watusaidie kama Serikali wanawasaidiaje wachimbaji wadogo ili waweze kufikia kiwango cha kuwa wachimbaji wenye migodi mikubwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu ambalo pia nataka mje mnipe majibu. Tangu Serikali hii ya Awamu ya Tano iingie madarakani imevuruga soko la madini hususan gemstone. Wale mnaofahamu pale Arusha wanunuzi wakubwa walikuwa wanakuja kununua gemstone pale Arusha, baada ya hii purukushani ya Serikali ya Awamu ya Tano wamekimbilia Nairobi. Sasa hivi wachimbaji wadogo wanavyochimba hizi gemstone wanaenda kuuza Nairobi, kama Taifa tunakosa mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri akija atuambie wana mpango au mkakati gani kwa sababu tangu mlivyoingia madarakani mwaka wa kwanza 2016 mpaka leo soko la gemstone halieleweki, soko la madini halieleweki? Leo gemstone za kwetu zinawanufaisha watu wa Kenya, kama Taifa hatulioni hili? Ni miaka mingapi mmesema mnaandaa soko la pamoja pale Arusha ili wanunuzi wanunue hapo, utekelezaji mpaka lini au mpaka Yesu arudi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka nipate majibu, tuliambiwa kwamba tunaibiwa sana na ikaundwa Tume ikakuta kwamba tumeibiwa shilingi trilioni 424, hivi ziko wapi? Baadaye nikaona wale Wazungu wamekuja, tukaambiwa eeh, tutawapa shilingi bilioni 700, ziko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu haya makinikia, Mungu anajua hata kama mkijifanya hamjui, mimi najua haya makinikia ndiyo yalisababisha Mheshimiwa Tundu Lissu kupigwa risasi. Watu walijaa jazba wakasema Mheshimiwa Tundu Lissu ni kibaraka cha Wazungu, kesho yake tunaona Wazungu hao hao mmekaa nao Ikulu. Sasa nataka mtuambie hizi fedha mlisema tunaibiwa na mkatoka kwenye vyombo vya habari pale, ziko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumetengeneza sheria ni kweli na ni sahihi kulinda rasilimali zetu za madini, lakini mmekwishakaa na haya makampuni makubwa ya uchimbaji wa madini tuliyonayo hapa Tanzania mkasikia changamoto zao? Mmeshakaa nao? Maana huko pembeni ukipitia wako hapo, mimi nimejaribu kupita nawasikilizia, wanalia, wanalalamika, sasa kwa nini msikae nao? Kaeni nao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri nikuombe Mheshimiwa Waziri hawa watu wenye haya makampuni na pengine wana chama chao, waje watupe elimu nasi angalau tujue. Hivi unadhani Wabunge wanajua nini hapa, wengi hawajui, sehemu kubwa ya sisi Wabunge hatujui haya mambo ya madini. Kwa hiyo, ni vizuri mkatafuta hata semina kwa Wabunge wote wakajua kuhusu mambo ya madini, lakini mkikaa ninyi wenyewe, tunatunga Sheria ya Madini, madini yenyewe hatuyajui, utatungaje sheria hata hujui unachokitunga? Unatunga Sheria ya Madini, madini yenyewe huyajui, utaratibu wa kuchimba madini huujui. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni vizuri mkawa- empower Wabunge ili wawe na elimu wajue undani kuhusu haya madini, ili wanavyotunga sheria wanajua wanachotunga. Bila hivyo watatunga sheria ya kukomoa, mwisho wa siku utadhani unawakomoa hawa Wazungu kumbe unawakomoa na Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana na kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kusimama nikiwa upande huu wa pili, naomba nichukue nafasi hii kumshuruku Mungu kwa neema aliyonipa kuwa upande huu. Ni bahati sana unajua kuwa Mbunge wa pande zote wakati kama huu nimekuwa upande wa kule ng’ambo na leo niko hapa, I can taste the difference. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kitu nimejifunza na nitaomba nikiseme, kazi ya Bunge au kazi ya Mbunge ni kuikosoa, kuishauri na kuisimamia Serikali. Lakini nimegundua kumbe kipindi nikiwa ng’ambo ile nilikuwa nakosoa tu nilikuwa sishauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nitakosoa, nitashauri na naomba nianze kwa kunukuu maneno aliyoyasema Mwalimu Julius Kambarage Nyerere mwaka 1969 alisema hivi; “Taifa lisilokubali kutaabika kwa maendeleo yake lenyewe, bila shaka Taifa hilo litataabika kwa maendeleo ya mataifa mengine, anasema maendeleo ni mtoto wa taabu.” (Makofi)

Naomba nirudie hawajasikia vizuri; “Taifa lisilokubali kutaabika kwa maendeleo yake lenyewe, bila shaka Taifa hilo litataabika kwa maendeleo ya mataifa mengine, maendeleo ni mtoto wa taabu.” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuendelea kwa kutegemea donors, kama ingelikuwa mataifa yanaendelea kwa kutegemea donors tungeona kwa China, tungeona kwa Amerika na mataifa mengine. Lakini ni mataifa ambayo yaliamua kutumia rasilimali zao wenyewe na leo wako hapo walipo wanasaidia watu wengine na nampenda sana Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli yeye hataki tujiite sisi maskini na kweli sisi siyo masikini, Tanzania siyo masikini. (Makofi/ Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kuna maeneo naomba nishauri eneo la kwanza…

T A A R I F A

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa leo niongelee mwenendo wa thamani ya shilingi. Ukiangalia kwa mujibu wa taarifa ya Kamati ambayo mimi pia ni Mjumbe wa Kamati thamani ya shilingi inashuka na kuna mapendekezo yametolewa nini kifanyike ili ku- stabilize shilingi yetu. Sasa kama nilivyosema leo nitakosoa kwamba ni kweli tumeendelea kushuka shilingi yetu imeendelea kushuka, lakini nini kifanyike ili shilingi yetu iendelee kuwa stable.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kwanza, lazima tukubali kama Bunge kuisimamia Serikali ipeleke fedha za kutosha kwenye kilimo. Kwenye kilimo wenzangu wameshauri kwenye yale mazao ya kimkakati kwa mfano tumbaku, korosho na mazao mengine ambayo yanatuingizia fedha za kigeni lazima tuhakikishe tunawekeza huko, sasa huo ndio ushauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili, nina kiatu hapa, hebu kiangalie vizuri kwanza, hiki hapo, kiangalie vizuri hicho kiatu, hiki kiatu ukikiangalia utadhani kimetoka Ulaya, kinatengenezwa hapa Dodoma.

MBUNGE FULANI: Nyoosha juu tukione. (Makofi)

MHE. MARWA R. CHACHA: …hapa Dodoma, hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tu-discourage importation ya vitu tunavyoweza kuvitengeneza wenyewe. Leo tuna ng’ombe kila kona, tuna ngozi ya kutosha, lazima Serikali ichukue hatua ikiwezekana ya kuondoa kodi kabisa kwenye mashine za uchakataji wa ngozi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukienda kwa huyu mtu ambaye anatengeneza hivi viatu, yuko hapo karibu na Chuo cha Mipango, ni mjasiriamali mdogo tu, lakini unaweza ukaangalia ukadhani kimetoka Ulaya. Sasa tutawawezeshe tuwasaidie watu wetu wazalishe vitu vyetu, soko la ndani ni kubwa. Badala ya kuagiza nje tuzalishe vya kutosha na tuuze nje shilingi yetu itakuwa imara kwelikweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ushauri mwingine ni kwenye mafuta. Tupige kodi kubwa kwenye mafuta ya kutoka nje ili watu wetu walime alizeti, walime michikichi, tuzalishe mafuta yetu wenyewe. Haiwezekani shilingi yetu ikawa stable kama mafuta tunatoa nje, haiwezekani. Hivi ni kweli tumeshindwa kulima alizeti? Tumeshindwa kuzalisha mafuta ya alizeti? Haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, lazima tuchukue mkakati wa makusudi na mimi namshukuru sana Rais John Pombe Magufuli, alisema kama hamlimi sitoi chakula, umesikia watu wanalia njaa saa hizi? Wamenyooka, watu wanalima, watu wanalima, hakuna cha dezo kila mtu afanye kazi fursa zipo. Kwa hiyo lazima tukubali kuzalisha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine, tuwasaidie wachimbaji wadogowadogo wa madini. Nichukue hatua hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Madini, Mheshimiwa Doto Biteko ameanza vizuri. Nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kukubali kukaa na wachimbaji wadogo wadogo na wachimbaji wakubwa, ni hatua nzuri, tumuunge mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tuwasaidie wakandarasi wa ndani kwa sababu hapa ndipo pia tunalipa fedha nyingi za kigeni kwenda nje. Leo tungekuwa tumewezesha watu wetu wakandarasi wa ndani kufanya miradi yetu fedha zinabaki humu ndani, zinazunguka humuhumu. Kwa hiyo, tuendelee kuwawezesha wakandarasi wa ndani. Nimshukuru pia Mheshimiwa Rais Magufuli kwa sababu ndiye mwanzilishi wa kusaidia wale wakandarasi wa ndani waliojenga Daraja la Mbutu kule Igunga, na sasa hivi wako kule wanatengeneza barabara, wanaenda vizuri na wametengeneza Daraja la Mto Mara ambalo liko mpakani kati ya Jimbo la Serengeti na Jimbo la Tarime na Mheshimiwa Heche anafahamu. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Chacha.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namalizia, naomba nimalizie. Nilikuwa naomba nishauri kwenye eneo lingine ni TARURA, tumeunda chombo hiki TARURA ili kusaidia barabara za vijijini, tunaomba Serikali ilete chanzo kingine cha kui-finance TARURA ili ifanye kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda nashukuru, lakini niseme nilimsikia mtu mmoja anasemasema pale ni Mchungaji, sijui mchungaji? Are you a Pastor or Poster?
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana. Nianze kwa kunukuu kifungu cha Biblia kinasema, nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana, dunia na wote wakaao humo. Sehemu nyingine Biblia inasema Mungu ndiye anayetawala katika falme za wanadamu na yeye huamua kumpa mtu awaye yote amtakaye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kuwakumbusha Waheshimiwa Wabunge mwaka 2015 ulifanyika Uchaguzi Mkuu na kulikuwa na miamba miwili iliyokuwa inamenyana; alikuwepo Mheshimiwa Magufuli na Mheshimiwa Lowassa. Mimi nilikuwa Upinzani wakati huo; kwa kweli niwaambie Mheshimiwa Lowassa alipata umaarufu mkubwa sana hususani kwa wafugaji kwamba kwa kuwa yeye ni Mmasai anatokea Umasaini kwa wafugaji angekamata nchi hii wafugaji wangepata neema sana, lilimpa umaarufu mkubwa sana na hata huko nakotoka wafugaji walimwanini sana.

Mheshimiwa Spika, nataka niwambie kama kuna jambo ambalo Mheshimiwa Rais Magufuli amelifanya la kihistoria katika nchi hii ni jambo la kukubali kupitia upya GN ili wafugaji na wakulima wapate maeneo kwa ajili ya kulisha mifugo yao. Kwa wale ambao si wafugaji hawawezi kujua kwa sisi tunaotokea maeneo ya ufugaji, tunafahamu taabu ambayo wafugaji wanaipata katika nchi hii. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naipokea taarifa hiyo, nilikuwa sijui, ahsante. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati nikiwa pale ng’ambo mwaka 2018, nilitoa shilingi kwa ajili ya kusimamisha zoezi la kuweka vigingi kwenye vijiji vilivyozunguka hifadhi mbalimbali ikiwemo hifadhi ya Serengeti. Wakati ule zoezi lilikuwa likiendelea kule Tarime kwenye vijiji vya kando kando ya hifadhi vikiwemo Vijiji vya Serengeti, Merenga, Machochwe, Nyamakendo, Mbalibali, Visarara, Bonchugu, Pakinyigoti, Miseke na kadhalika. Kama kuna wananchi wamefurahi baada ya tamko la Rais, ni Wananchi ambao wanazunguka maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, ukikumbuka, Hifadhi za Serengeti na hifadhi nyingine zilianzishwa kwa mujibu wa Sheria na GN na kilichokuwa kinatokea katika maeneo haya, walikuwa wanapanua mipaka na kwa kweli kulikuwa na confusion kati ya TAMISEMI na Wizara ya Maliasili na Utalii, kwamba mipaka inawekwa kwenye vijiji, wananchi wanyang’anywa maeneo yao. Kwa kweli wananchi wamefarijika sana. Kwa hiyo, nina kila sababu ya kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli kwa hiki alichokifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaambie, Tanzania tumepata neema ya kuwa na Rais ambaye pengine akiondoka madarakani ndio Watanzania watakuja wakumbuke. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaambie, wakati nikiwa ng’ambo ile, Mheshimiwa Rais, Dkt. Magufuli alikuwa anatunyima usingizi kweli kweli. Ndiyo ukweli! Kwa sababu kule ng’ambo tulikuwa tumezoea ufisadi. Yaani ikitokea issue ya ufisadi, tunapiga kelele kweli kweli. Sasa jamaa amekuja amekaba hakuna cha ufisadi tena; na amekaba kweli kweli. Ukijulikana umefanya ufisadi anatumbua, hana mswalie Mtume, hata wao wanajua. Kwa hiyo, niwaambie tumepata Rais…

MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Taarifa.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Spika, wakati mwingine niseme ni maombi ya Watanzania, wewe ni shahidi.

T A A R I F A

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Spika, napokea taarifa yake, ni kweli, si tulikuwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba unilindie muda wangu. Kwa hiyo, ukweli ni hivi, 2010 Watanzania walikuwa wanaomba, yaani unajua inatakiwa tupate Rais wa kufanya maamuzi magumu.

Mheshimiwa Spika, unakumbuka ilifikia sehemu, sisi ambao tulikuwa huko duniani hatujaja humu, wananchi walikuwa wanasema, yaani tunatakiwa tupate Rais kichaa ili hii nchi inyooke. Nchi sasa hivi imenyooka. Nchi imenyooka Mura, wewe vipi? (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ngoja niwaambie, hivi kwa mfano, nani angeweza kuanzisha Bwawa kwenye Stiegler’s Gorge? Tuseme ukweli, nani? Yaani nchi za Ulaya hazitaki, Marekani haitaki, sijui nani hataki, nani? Huyu jamaa ana maamuzi magumu, tumuunge mkono. Umeme wa Stiegler’s Gorge ni kwa ajili ya maslahi ya Watanzania. Tutapata umeme kwa cheap price, wewe hutaki hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unajua wanasiasa wengi wanapenda kitu kinaitwa cheap politics. Mheshimiwa Dkt. Magufuli hapendi cheap politics anafanya hard politics. Hakuna ambaye angeweza kujenga reli, hakuna ambaye angenunua ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unajua wanasiasa wengi, hususan wa ng’ambo ile wangependa wajenge madarasa, vitu vidogo vidogo tu, lakini mambo mazito yenye kulinufaisha Taifa kwa miaka mingi, hakuna ambaye angethubutu kufanya. Kwa hiyo, ukiona tumehamia upande huu, tumeona mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ile hoja yako ya miaka saba, ile tumpe Magufuli hata miaka saba aendelee. Hivi…

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, wanaoafiki!

WABUNGE FULANI: Ndiyoooooo.

SPIKA: Hapana, hiyo futa kwenye Hansard. Endelea Mheshimiwa. (Makofi) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, naona wamekaa kimya, wanaelewa ndiyo ukweli.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nilitka niongelee ni jambo la cultural tourism. Cultural tourism kwa maeneo ya Serengeti inakuwa affected na single entry. Naomba kupendekeza kupitia Kamati ya Maliasili na Utalii, ongezeni jambo la single entry, is a big challenge kwa watu wetu. Watalii wanaishia hifadhini. Watalii wanatakiwa wakifika hifadhini, waende kutembea kwenye vijiji.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Naomba nimshukuru Mungu kwa kunipa nafasi ya uzima tena. Nianze kwa nukuu ya mstari kwenye Biblia, Mithali 10:15 inasema, “Mali ya mtu tajiri ni mji wake wa nguvu, uangamivu wa masikini ni umasikini wao.” Waswahili wanasema, “mtaji wa masikini ni nguvu zake mwenyewe.” (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru sana Mungu kwa kutupa Rais, Mheshimiwa Dkt. Magufuli. Ni kiongozi mwenye uthubutu na vision, anayetupeleka kule kunakotakiwa. Kwa mtu wa kawaida anaweza asielewe, kwa mtu mwenye macho ya hapa (short sighted) anaweza asione tunapoenda. Miradi anayoifanya Rais Mafufuli ni miradi mikubwa (heavy) ambayo mtu mwepesi asingeweza kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi leo unaweza ukaanza kuhoji ndege kwamba hujaona faida ya ndege? Watanzania tu kwenda hapa Uganda unafikiria labda uende Kenya upate ndege ya kwenda Uganda au kwenda nchi nyingine. Leo Air Tanzania inaenda Uganda, Kenya na karibia nchi nyingi za Afrika inaenda sasa hivi. Kwa hiyo, ukisema huoni manufaa ya ndege ni wewe, lakini sisi Watanzania tunahitaji ndege ziendelee kununuliwa zaidi na zaidi kwa ajili ya uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo vinajengwa viwanja vya ndege kila mkoa. Sasa unajenga kiwanja kila mkoa halafu unaendaje huko kama huna ndege? Kwa hiyo, namshukuru Rais, Mheshimiwa Dkt. Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, Stiegler’s Gorge, umeme wa maji ndiyo umeme wa bei ya chini kuliko sources zozote zile unazojua. Leo mtu anasimama anasema tungeenda kwenye gesi, sijui kwenye vitu gani, atuchanganulie gharama za kila source. The cheapest source of electricity ni maji. Tangu nchi hii iumbwe haijawahi kuwa na umeme wa Megawatt 2,115; tunaenda kupata umeme wa Megawatt 2,115 kupitia Stiegler’s Gorge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaambie Waheshimiwa Wabunge, hakuna atakayetuhurumia Watanzania. Hayupo wa kutuhurumia sisi, tutajikomboa kwa resources zetu tulizonazo wenyewe. Wazungu wangependa mpate umeme wa teknolojia kubwa ambayo mtaendelea ku-depend kwao. Ndiyo wanataka! Hawapendi kile kitu ambacho ni rahisi kwetu, wanataka everyday tuendelee ku-import kutoka nje. Ndicho wanachotaka sisi lini tuta-export? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namshukuru sana Rais, Mheshimiwa Dkt. Magufuli. Sisi Wabunge wa CCM na Wabunge wa Upinzani tumuunge mkono Rais, Mheshimiwa Dkt. Magufuli, songa mbele na Stiegler’s Gorge. Stiegler’s Gorge ilipingwa tangu enzi za Mwalimu Nyerere. Leo watu wanasema miti, miti; inatusaidia nini Mura kama haituingizii faida? Sisi tunataka umeme wa uhakika. Ukienda leo kila kona unakuta umeme unakatikakatika, hatuna umeme ambao ni stable. Mheshimiwa Rais anasema tunataka umeme wa haraka na wa haraka ni wa Stiegler’s Gorge…

MHE. AHMED ALLY SALUM: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Marwa Ryoba Chacha kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Ally Salum.

T A A R I F A

MHE. AHMED ALLY SALUM: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba Mheshimiwa Makamu wa Rais anapambana katika hii nchi kuhakikisha kwamba miti inapandwa kwa wingi sana. Wewe unasema miti inatusaidia kitu gani? (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Chacha, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, sasa taarifa gani hiyo? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niingie kwenye suala la elimu. Naiomba Serikali yangu na nimwombe Waziri Mkuu na vile vile naomba Mawaziri ambao wapo chini ya Waziri Mkuu wanisikilize vizuri, hususan kwenye elimu. Tunahitaji kubadili Sera ya Elimu. Kwenye suala la vyuo vya ufundi, lazima tuliangalie vizuri kwa upya. Tunahitaji vyuo vya ufundi kila Wilaya kwa sababu tunaenda kwenye uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, tusipokuwa na vyuo hivi, tutafeli. Kwa nini Mataifa mengi yanakimbilia kuwekeza China? Ni kwa sababu ya manpower ambayo ni skillful kwenye eneo hili la ufundi. Kwa hiyo, ili tuendelee na tuendelee kupata viwanda, unaweza ukasema unafungua kiwanda hapa ukakosa wataalam wenye uelewa wa eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili kwenye elimu, tunahitaji kuangalia kwa upya mitaala yetu. Kwa mfano, somo la ujasiliamali ni vizuri lifundishwe kuanzia Shule ya Msingi na kuendelea ili mtoto anapomaliza Shule ya Msingi, Sekondari au Chuo asifikirie kwenda kutafuta ajira Serikalini. Leo tuna mamia wame-graduate wanafikiria kwenda kuajiriwa, hiyo hapana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine niongelee kidogo kuhusu tourism. Kwenye tourism Wilaya ya Serengeti, pale katikati Seronera wanapanua uwanja wa ndege. Tunahitaji uwanja wa ndege uwe nje ya hifadhi. Ukiwa nje ya hifadhi, utakuwa na multiplier effect.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba iangaliwe issue ya single entry ambayo ina-affect sana cultural tourism. Leo watalii wanapoingia hifadhini hawawezi kutoka sababu akitoka anaambiwa alipe tena. Kwa hiyo, imeathiri sana cultural tourism. Wale ambao mpo maliasili na utalii, single entry siyo nzuri kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni kwenye uzalishaji. Naiomba sana Serikali, kwenye eneo la kilimo, mifugo na uvuvi kama kuna vitu tunaweza kuvitengeneza sisi wenyewe Tanzania, ni bora kuzuia importation ili kusababisha uchumi wetu kukua ili tuweze kuuza nje. Tumeona kwenye suala la korosho ambapo watu wa nje wanatuchezea. Kama tungekuwa na viwanda vyetu, tuna-process korosho, tunasafirisha, tunaenda kuuza huko, inaingiza fedha nyingi za kigeni. Kwa hiyo, nilitaka niseme hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, ni maji. Naomba Waheshimiwa Wabunge wenzangu mniunge mkono kwenye hili. Mwaka huu kwenye Finance Bill tumwombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha tuongeze shilingi 50/= kwenye maji ili kukamilisha miradi ya maji vijijini.

Naomba Waheshimiwa Wabunge mniunge mkono kwenye hili, tuungane tumwombe Mheshimiwa Waziri Mpango shilingi 50/= iingie kwenye maji. Ndiyo nakuona Mheshimiwa Mpango unatikisa kichwa lakini hii ni muhimu sana. Kama Mheshimiwa Mpango amegoma kuingiza, atuletee chanzo mbadala cha kwenda ku-finance miradi ya maji. Hiyo tu akituletea sisi tunakubali. Kama hajatuletea chanzo mbadala, tunakula sahani moja naye, shilingi 50/= iingie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kusema, ninamshukuru Mungu sana, tena ningelijua ningewahi siku nyingi kwenda CCM. (Kicheko/Makofi)

Kabisa! Yaani nimekuja kugundua kumbe nimechelewa sana. Aisee! CCM kuzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, si unaona sina mawazo sasa hivi, nipo vizuri. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru sana. Naomba nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kunipa uzima niweze kuchangia leo tena hapa kwenye hii hoja ya TAMISEMI. Kwanza, nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Jafo, ni moja ya Mawaziri ambao wako very humble and mobile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipindi nikiwa ng’ambo ile, Mheshimiwa Jafo alitutembelea Wilaya ya Serengeti akaona jitihada zetu kwenye Hospitali ya Wilaya ya Serengeti, Jafo hakusita akatuletea fedha na hospitali inaendelea vizuri. Nikushukuru sana kwa mwaka huu Mheshimiwa Jafo umetupa shilingi milioni 500, Mungu akubariki sana lakini pia naomba unifikishie salamu hizi kwa Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma Biblia Zaburi ya 11:3 Biblia inasema,”Kama misingi ikiharibika, mwenye haki atafanya nini?” Hakuna ubishi kwamba nchi huko nyuma ilikokuwa inaenda ilikuwa inaenda kubaya kweli kweli. Upande wa kule ng’ambo walikuwa na nguvu sana kwa sababu kwa kweli mambo hayakuwa mazuri. Nakumbuka kabla sijawa Mbunge, nikiwa Diwani na wanasiasa wengi waliojifunzia upande wa kule kama mimi, hoja kubwa waliyokuwa wanaitumia ni ufisadi. Ufisadi ulikuwa ni tiketi ya wewe kuhakikisha unaing’oa CCM. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ndugu zangu tukubaliane ukweli, kwa mfumo ambao Mheshimiwa Rais Magufuli amekuja nao, kwanza kwa kuanzisha kitu kinaitwa Treasury Single Account ni mfumo bora ambao hakuna kiumbe yeyote anaweza ku-temper nao kirahisi. Unalipa kila mtu anaona; Serengeti wamelipa hiki, wamefanya hiki na kinakuwa evaluated. Kwa hiyo, namshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemsikiliza Mbunge mmoja ng’ambo ile anasema kwamba, decision making iliyofanywa na Chama cha Mapinduzi, chini ya Mwenyekiti, Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Magufuli kununua ndege kwamba ni maamuzi mabaya. Ngoja niwaambie, wakati wengine tukiwa nje ya Bunge hili kipindi kilichopita, waliokuwa wanaipinga Serikali kwa nini hakuna ndege za nchi, mmojawapo alikuwa Mheshimiwa Mch. Msigwa. Akasema nchi gani hii hatuna ndege! Alikuwa Mheshimiwa Mch. Msigwa huyu. Ndege zimenunuliwa anaanza kupiga kelele. Hawa watu vinyonga hawa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukikaa ukamsikiliza Mheshimiwa Mch. Msigwa, kila siku anaongelea uwanja wa Nduli, hivi uwanja wa Nduli uko Jimbo gani? Si Iringa? Anasema watengeneze uwanja wa Nduli. Sasa watapeleka ndege gani? Hawa ndege wanyama au! Ndege wa angani ndiyo wataenda kwenye uwanja wa Nduli! Si lazima tununue ndege ziende kule ili kuleta watalii watakaoenda Ruaha National Park. Watalii wataendaje Ruaha National Park bila ndege? Kwa hiyo, lazima tununue ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mtu anapinga Stieglers Gorge. Hivi jamani, si tumeona kila siku, sisi tunaijua hapa, si tunaelewa! Mheshimiwa Rais amesema tunataka umeme rahisi. Umeme rahisi ni wa maji. Labda ile Kambi wangesema sisi Kambi ya Upinzani tumefanya utafiti, tumegundua umeme rahisi ni wa gesi. Hizo tafiti mlizofanya ziko wapi Mheshimiwa Mch. Msigwa? Serikali ya Chama cha Mapinduzi imefanya utafiti wa vyanzo vyote vya umeme, imegundua umeme rahisi ni wa maji. Leo utatokea wapi? Ni Stieglers Gorge, yaani unapinga na hiyo? Aaaah mura! (Makofi/Kicheko/ Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambie Serikali ya Chama cha Mapinduzi ni Serikali sikivu. Kweli kabisa ni sikivu. Issue ya kikokotoo, ni kweli ilipita sheria hapa, tulipitisha Wabunge wote, si na wewe!

MBUNGE FULANI: Eeh!

MHE MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ilipitishwa hapa. Mheshimiwa Rais alivyo msikivu, Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi akasikiliza wafanyakazi akasema, hakuna, hii rudisha huko. Sasa hiyo nayo unapinga tena kwamba eti ni maamuzi mabaya! Aaah mura! (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemsikiliza mwingine anasema, Serikali ya Chama cha Mapinduzi waongo, waliahidi mwaka jana shilingi bilioni 29 za maboma, ziko wapi? He, unaishi wapi wewe? Mheshimiwa Dkt. Magufuli alishatoa hela, yaani huko madarasa yanafunikwa, madarasa yanakamilishwa na hakuna watoto watakaoshindwa kwenda shule. (Makofi/Kicheko/Vigelegele)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Mfumo wa elimu Tanzania umezeeka, umechoka na umechakaa. Ukiangalia sheria iliyoanzisha sekta ya elimu ni sekta ambayo tunalingana umri. Mimi sasa hivi ni mzee. Mfumo wa elimu ambao hauwezi kujibu matatizo ya nchi, huo mfumo umezeeka, umechoka lazima uangaliwe kwa upya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kitabu cha Kamati, ukurasa wa 12, nitanukuu baadhi ya maneno wanasema: “Mheshimiwa Spika, uchambuzi wa Kamati umebaini kuwa baadhi ya maoni yanaendelea kutekelezwa na baadhi bado hayajatekelezwa kabisa. Baadhi ya masuala ambayo Kamati inaona yana umuhimu lakini bado hayajatekelezwa ni pamoja na; mimi nachukua ile (c), kuangalia upya mfumo wa elimu yetu nchini ni jambo ambalo Kamati inaona halijafanyiwa kazi kwa zaidi ya miaka mitatu sasa.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma Biblia sehemu fulani inasema watu wangu wanaangamia kwa kukosa maarifa. Sehemu nyingine Biblia inasema mkamate sana elimu usimwache aende zake, mshike sana maana yeye ndiye uzima wako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka tu twende vizuri kama Waheshimiwa Wabunge. Watoto wanaomaliza darasa la saba ni wangapi ambao hawaendelei na sekondari? Watoto wanaomaliza form four ambao hawaendelei na form six ni wangapi? Watoto wanaomaliza form six ambao hawaendi vyuo vikuu ni wangapi? Mfumo wetu wa elimu ni mfumo unaowaandaa watu kwenda kuajiriwa si mfumo unaowaandaa watu kujitegemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tuchukulie tu takwimu ya 2017/2018, waliofeli mwaka 2017 darasa la saba ni 247,915 sawa na asilimia 27. Mwaka 2018 waliofeli ni 210,215 sawa na asilimia 22. Hawa wanaenda wapi na wana ujuzi gani? Kwa hiyo, ni lazima mfumo wetu wa elimu tuupitie upya. Mataifa yote duniani ambayo tunasikia ni matajiri kamaMarekani, China, Finland na Uingereza lakini utajiri walionao sio raw materials bali ni brain na brain inahitaji uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu moja kwenye Biblia inasema bora hekima basi jipatie hekima, naam, kwa mapato yako yote jipatie ufahamu. Narudia, kwa mapato yako yote jipatie ufahamu. Maana yake uwekezaji kwenye elimu ni gharama na halikwepeki. Ili nchi yetu iweze kubadilika lazima mfumo wetu wa elimu tuubadili. Hiyo hatuwezi kuikwepa ni lazima tubadili mfumo wetu wa elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunasema kwa mfano asilimia zaidi ya 70 ya Watanzania ni wakulima, hivi tunawafahamu hao wakulima? Unadhani wakulima ni wale wanao-graduate, ni wenye PhD au ni maprofesa? Wakulima ni hawa waliofeli darasa la saba na form four, tumewapa skills gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni shahidi wakati naanza darasa la kwanza nilijifunza kupalilia na kutengeneza bustani shule ya msingi. Leo shule zote za msingi watoto anamaliza la saba hajui kushika jembe, tunamwandalia mazingira gani? Leo tunataka tupate wafugaji bora, kule shule ya msingi tunajua wafugaji ni darasa la saba, uongo? Wanaofuga ni darasa la saba, wana skills za ufugaji na agriculture?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri masomo ya kilimo yako wapi, tume-concentrate na masomo mengine masomo ya kilimo hakuna, masomo ya biashara hakuna, tumeondoa. Wakati umefika tuko kwenye karne ya viwanda lazima watoto wetu wapate masomo ya usindikaji, kilimo na ujasiriamali kuanzia shule za msingi and so forth kinyume na hapo haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaomba sana unilindie muda wangu, samahani. La pili ni lugha ya kufundishia na hapa naomba ninukuu abstract kidogo kutoka kwenye blog moja ya Science Direct kuhusu lugha ya kufundishia. Wanasema: “The importance of learning a foreign language in childhood. Among philosophers, empiricism and the psychologist, behaviourists believe that language is a social creature and like other social behaviours are aquired. Language learning is natural. Babies are born with ability to learn it and that learning begins at birth. Many experts believe that learning the language before the age of ten years allow children to speak correct and fluent as an indigenous person. Therefore, whatever the earlier children become familiar with the foreign language, he/she have better chance to speak proficiency. Research suggests that from birth through age ten is the best time to introduce new languages to a child.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, lugha ya kujifunza shuleni lazima ianzie utotoni, lazima Tanzania tujue sisi siyo kisiwa. Hii biashara ya Kiswahili kuanzia darasa la kwanza then sekondari imeshapitwa na wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua wapo wanaosema twenda kwenye Kiswahili, mimi niwaambie kama tunachagua kwamba ni Kiswahili tujuulize maswali, who are we trading with, tunafanya biashara na akina nani? Kama unataka kufanya biashara na China, Marekani, Rwanda, lugha sahihi siyo Kiswahili bali ni Kiingereza.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Ahsante, mengine uandike.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba dakika moja tu nimalizie.

MWENYEKITI: Haya malizia sekunde kumi.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nikiuliza hapa Wabunge, Mawaziri na watu wengine wenye pesa wangapi watoto wao wanasoma shule za Kiswahili kama sio English Medium, kama siyo shule za private.

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. MARWA R. CHACHA: Kwa hiyo, English is the solution.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana. Naomba nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayofanya katika Wizara hii. Anafanya kazi kubwa sana Mungu ambariki sana. Niseme Mheshimiwa Waziri kuna jambo atakumbukwa sana ni jambo la ujenzi wa barabara ya kuanzia lango la Loduare kule Ngorongoro mpaka pale Golini Serengeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii barabara ya Ngorongoro ni barabara ambayo Waziri anafahamu udongo wake ni volcanic, katika matengenezo ya kawaida ilikuwa imeshindikana. Kwa hiyo niseme, Mungu ambariki sijui nimpe nini? Wamefanya kitu kikubwa ambacho watakumbukwa milele na milele, kujenga barabara ya lami katika eneo hili na tena kizuri zaidi wameruhusiwa na UNESCO. Niseme Mheshimiwa Waziri Mungu ambariki yeye pamoja na Ndugu Kijazi. Maana ilikuwa sio kazi rahisi kuruhusiwa na UNESCO kujenga barabara hii, lakini niseme Mungu ambariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kidogo, kwenye eneo hili la barabara kilomita 88, ni bora waka-extend ikafika Ikoma gate kwenye ile gate la Serengeti ili ikae vizuri. Hata hapa niseme wamefanya jambo kubwa na Mungu awabariki sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni mapendekezo nimesoma kwenye kitabu cha Waziri ukurasa wa 33, ile namba 75 kuhusu masharti ya wajumbe wanaounda WMA, nimeisoma vizuri kwamba kwenye kanuni ambazo zilikuwa zimetengenezwa, kwamba wale wajumbe ambao ni darasa la saba walikuwa hawaruhusiwi kugombea na kwenye maelezo ya kitabu cha Waziri amesema imeleta mgongano, sintofahamu kidogo na nimeona Wizara wapo tayari kufanya marekebisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri alisimamie, wafanye marekebisho kwa sababu kanuni hii kimsingi inapingana na katiba ya nchi. Katiba ya nchi inasema mtu ajue kusoma na kuandika ndio achaguliwe sasa tukiweka kwa wale Wenyeviti wa WMA, bahati nzuri tuna kina Musukuma hapa ni Mbunge, lakini si darasa la saba? Kwa hiyo, nadhani ni vizuri kanuni ile irekebishwe ili darasa la saba na wao wapate fursa ya kugombea kuwa Wajumbe wa WMA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni mgogoro wa mipaka kati ya vijiji ambavyo vipo Serengeti na Serengeti National Park, tunafahamu, tumeongea mara nyingi mimi na yeye na ameonesha positive response na aliahidi kwamba tutaenda na yeye Serengeti. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, nimwombe sana rafiki yangu akipata nafasi hebu twende kwenye Vijiji vya Merenga, Machochwe, Mbalibali, Tamkeri, Bisarara, Bonchugu angalau aone uhalisi wa kile kinachozungumzwa, kwa sababu kuna maeneo vigingi vimewekwa kwenye maeneo ya vijiji kabisa katikati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kibaya zaidi kuna siku moja nimekwenda kwa Mheshimiwa Waziri, akikamatwa na ng’ombe kwenye maeneo hayo anafilisiwa ng’ombe na anafungwa. Kwa mfano kuna mama mmoja alikamatwa ni mjamzito, ngo’mbe walitaifishwa wameunzwa wote, amefungwa, amepigwa faini na sasa hivi amejifungulia yupo magereza. Nimwombe Mheshimiwa Waziri yeye anatokea maeneo ya wafugaji na bahati nzuri mwenyewe ni mfugaji anafahamu ninachokiongea, sio vyema kuwafanya watu wetu kuwa maskini, ni vema tuwasaidie watu wetu kujali Hifadhi ya Serengeti, kwa sababu kama una jirani ni lazima uishi naye vizuri, sio kwa kugombana. Kwa hiyo nimwombe twende Serengeti akaone.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambao nataka niongee ni jambo la utafiti umefanyika, inaonekana kama Serengeti hoteli kama zinakuwa nyingi vile. Huku nje hakuna hoteli, nimwombe pamoja na tatizo la single entry, ni bora tusaidie watu wajenge hoteli nyingi nje ya hifadhi, kukiwa na utitiri wa hoteli ndani ya hifadhi kutakwamisha migration ya wanyama kwenda kule Masai Mara. Kwa sababu kutakuwa na utitiri wa hoteli, tuweke nje hoteli zitasaidia wananchi wanaozunguka hayo maeneo kukua kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa najaribu kuangalia kwenye kitabu cha hotuba ya Kambi la Upinzani, ukurasa wa tano ile namba 13; wanasema Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kufuta agizo lake la kuzuia biashara ya viumbe hai nje ya nchi na iwalipe fidia wafanyabiasha kwa hasara na usumbufu waliowasababishia wafanyabiashara hao. Maana yake kambi ya Upinzani inasema Serikali iruhusu wanyama wauzwe nje ya nchi. Sasa nakumbuka mwaka fulani tukiwa nje ya Bunge waliokuwa wanapiga kelele wanyama kuuzwa nje ya nchi walikuwa ni Kambi ya Upinzani au nasema uongo jamani?

WABUNGE FULANI: Kweli.

MHE. MARWA R. CHACHA: Walikuwa wanapiga kelele twiga amepandishwa kwenye ndege, walikuwa ni akina nani, si ni akina Msigwa hawa?

WABUNGE FULANI: Kweli.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Mheshimiwa Msigwa anakuja na maoni hapa kwamba wanyama wauzwe, maana yake leo Upinzani wangepewa nchi hii wangeuza wanyama wote wakaisha. Mheshimiwa Waziri asiingie kwenye huo mkenge, akatae hiyo biashara, azuie wanyama wasiuzwe, kwa ajili ya manufaa ya vizazi…

T A A R I F A

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Marwa.

MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemsikia mchangiaji nilikuwa nadhani angechukua muda kidogo kujielimisha. Wanyama tunaozungumza warudishwa hawa wananchi wanaouza ni tofauti kabisa na hao wanyama anaosema twiga, tembo. Wanaozungumziwa ni mijusi, konono, vipepeo ambavyo havihusiani kabisa na wanyama anaosema.

MWENYEKITI: Ahsante. Taarifa hiyo Mheshimiwa Ryoba.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa huyu Mchungaji nini asichoelewa, wewe si unasoma maandiko unalewa vizuri. Mmesema inataka kufuta agizo lake kuzuia biashara ya viumbe hai, viumbe hai ni wapi? Sasa ungekuwa unamaanisha konono, ungekuwa unamaanisha mijusi ungetaja lakini hujataja. Kwa hiyo hapo usijifiche hapa, nilikuwa najaribu kushangaa nimwombe Mheshimiwa Waziri, wasamehe maana hawajui walitendalo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni jambo la KfW, Mheshimiwa Waziri na hususan Mheshimiwa wa Fedha naomba anisikilize, tumepata msaada kutoka Ujerumani, kwa ajili ya kusaidia Ngorongoro na Serengeti kwenye barabara kwenye afya na maji. Leo kuondoa exemption miradi hii ifanyike imekuwa ngumu, mpaka leo tunaongelea mwaka wa tano miradi haijafanyika. Nimwombe Mheshimiwa Waziri bado asichoke, nimwombe Waziri wa Fedha jamani wakae waangalie hili jambo, hivi mtu anakuletea msaada wewe unaukata eti alipe kodi, hiyo ya wapi jamani, hiyo haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo sikuwa na mambo mengi. Ahsanteni sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana. Naomba na mimi nichangie kwenye Wizara hii ya Nishati na Madini. Nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Waziri wa Nishati kwa kazi nzuri anayofanya; Mungu akubariki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niseme, kama taifa tunahitaji umeme mwingi, na kama ingewezekana leo tukawa na uwezo wa kuzalisha megawatt 10,000 ingelipendeza zaidi. Mimi nimpongeze sana Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambaye ni muasisi wa taifa letu. Mwalimu Nyerere alikuwa na maoni ya kama Taifa la Tanzania tuwe na utoshelevu wa Nishati ya umeme na Mwalimu Nyerere wakati ule alikuwa na maono ya Stiegler’s Gorge. Sasa bahati mbaya sana wakati ule kama Taifa tulikuwa tunahitaji megawatt 100 na uwekezaji kwenye Stiegler’s Gorge usingewezekana kwa sababu gharama ilikuwa kubwa. Lakini wakati ambao tunao ni wakati mwafaka wa kuwa na umeme unaotokana na Stiegler’s Gorge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna watu wana hoja dfhaifu sana. Hivi wanataka watuambie kwamba Mwalimu Nyerere alikuwa mjinga, kwamba hakuwa na maono sahihi? Mimi nikuambie, kama kuna mtu anapingana na maono ya Mwalimu Nyerere huyo mtu amelaaniwa. Mwalimu Nyerere alikuwa ni mtu wa principle, mwalimu Nyerere alikuwa ni mtu wa maono, amekufa mzee wa watu hana chochote hana lolote kwa sababu alikuwa na uzalendo mkubwa na nchi hii. Leo nani anayeweza akasema mimi ni mzalendo kuliko Nyerere? Leo watu wanasema issue ya mazingira, mazingira kitu gani? Wananchi wa Tanzania wangapi wanatumia kuni na mkaa? Misitu mingapi inafyekwa kwa ajili ya mkaa na kuni? Tuambizane hapa kwa kuja na takwimu. Mimi huko ninakotoka kila mtu anatumia mkaa, kila mtu anatumia kuni, misitu inafyekwa kila leo. Leo sehemu ambayo inafyekwa kwa ajili ya kuwekeza ni sehemu ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, umeme wa maji ni umeme wa gharama ndogo. Unajua mimi kitu siwaelewi watu wa kule upinzani, hawaji na statistics, research. Leo tuambieni umeme wa gharama ndogo ni upi kwa research ni upi? Umeme wa gharama ndogo ni umeme wa maji; shilingi 36. Sasa ukiwasikiliza hivi hawa wako sawasawa kweli? (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini bahati nzuri unajua mimi nimetokea kule unajua kule ili mtu achangie mpaka ale ile kitu ya kwao Heche kule Tarime.

Mheshimiwa Naibu Spika, wanasema waemacha gesi, wameacha gesi wapi? Kwa taarifa yako asilimia 50 ya umeme tunaoutumia unatokana na gesi. Hawasemi hilo, hawasemi kabisa. Leo nimepigiwa simu, kuna watu wana magari yanatumia gesi, hiyo hiyo gesi yanatumia, na kesho Mheshimiwa Waziri amesema wayalete hapa Bungeni Wabunge waone magari yanayotumia gesi yetu. Sasa labda hawajui master plan ya nishati yetu. Our master plan is power mix, energy mix. Labda tu niwaamabie kwa dondoo kidogo ili waelewe. Upepo kwa research iliyofanyika utazalisha megawatt 500, solar 500, maji megawatt 5,000. Sasa uache umeme wa maji 5,000 uende kwenye nini? Wewe tulia, huelewi! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uwekezaji wa umeme huu wa Stiegler’s Gorge ndio rahisi kulingana na mazingira ya kiuchumi tuliyonayo. Huwezi kujigamba kwenda kuwekeza kwenye umeme wa ghali ilhali tuna shida nyingine. Tuwekeze kwenye huu ambao ni very cheap lakini umeme mwingi halafu utashuka bei; unajua hofu ni 2020 inawatesa wale jamaa wa kule ng’ambo. Ikifika 2020 wataenda kusema nini? Sasa hivi REA kila kijiji watakuwa wamepata umeme au nasema uongo? Kila kijiji watakuwa wamepata umeme, kwa hiyo wanahaha, wenzenu wana shida kweli kweli, hawalali! Sasa wewe unafikiria mtu kama yule Mnyika, atarudi wapi? Au yule Sugu, anarudi wapi? He! (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nikwambie kinachowatesa ni hofu ya kutokurudi 2020; na kwa kazi ambayo anaifanya Rais Magufuli mimi nasema Rais Magufuli kamua twende. Nilikuwa nasoma kwenye kitabu cha Kambi ya Upinzani yaani ni kituko. Yaani kweli, taarifa gani hii? Uongo mtupu!

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilikuwa najua Mnyika ni Padri kumbe anasema uongo. Hebu sikiliza hii, eti Mnyika anaema TANESCO ina madeni inashindwa kujiendesha sijui kitu gani. Hebu sikiliza, TANESCO enzi za nyuma ilikuwa inapewa kila mwaka bilioni 143 ruzuku ya Serikali, mwanaume Magufuli alipoingia akasema hakuna cha ruzuku mtajiendesha wenyewe; kwa kuwa ninyi ni Shirika la Serikali, lazima mzalishe faida. Mwaka 2017 TANESCO mapato ambayo imekusanya ziada 1.5 ziada! Na wanalipa kila wiki 9 billion TPDC, wewe unasema nini? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Chacha, ahsante sana muda wako umekwisha. Ahsante sana. Muda umeisha.

MHE. CHACHA M. RYOBA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. Mheshimiwa Kalemani songa mbele, ahsante sana. (Makofi)