Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Amina Nassoro Makilagi (18 total)

MHE. AMINA NASSORO MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa khanga hii ni vazi ambalo mwanamke wa Kitanzania analivaa akiwa nyumbani, ni vazi ambalo analivaa akiwa shambani analima, ni vazi ambalo analivaa anapokuwa kwenye shughuli za kijamii kwenye misiba na kwenye shughuli za harusi, ni vazi ambalo mama anakuwa nalo hata anapokwenda leba. Ni vazi ambalo linampokea mtoto hata anapotoka leba. Ni vazi rasmi la Mwanamke wa Kitanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, kanga ambazo zinatengenezwa katika viwanda vyetu vya Tanzania kwa kiwango kikubwa hazikidhi mahitaji ya wanawake wa Tanzania na hasa kwa kuzingatia kwamba vipimo vinavyotumika na ukilinganisha upana na viwango walivyonavyo wanawake wa Tanzania. Wanawake wa Tanzania wanaishi kwa amani na utulivu wako sawa katika afya zao, kanga wanazozivaa haziwatoshi kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna baadhi ya viwanda hata hizi sentimita zilizozungumzwa hawafikii; unakuta urefu ni wa mita 100, sentimita 120 kwa kweli ukiangalia hata wewe mwenyewe haikutoshi hata kwa urefu peke yake. (Kicheko/Makofi)
Sasa swali langu la kwanza, kwa kuwa vazi hili kwa kweli ni vazi la mwanamke wa Kitanzania. Matokeo yake wanawake wameanza kuvaa kanga zinazotoka India na China, wanawake sasa wamehamia kwenye madera, jambo ambalo kwa kweli hawakuzoea, ningependa kujua sasa Serikali inamkakati gani wa kuhakikisha inaielekeza TBS (Shirika la Viwango Tanzania) ili kufuatilia vazi hili, liendane na ubora halisi wa maumbo ya wanawake wa Kitanzania na hasa kwa kuzingatia kwamba kanga hii hata ukiivaa inateleza haifungiki sasa hivi; kwa hiyo hata malighafi wanayoitumia siyo pamba. (Makofi)
Swali la pili, ningependa kujua sasa kwa sababu hili vazi la kanga limekuwa ni dogo, na wanawake wameamua kuachana nalo kwa kuwa na India. Ningependa sasa kujua Serikali ina mkakati gani kwa sababu sasa vazi la dera limekuwa likiwapendeza wakina mama na ni vazi la heshima, ina mkakati gani sasa la kuhamasisha viwanda vya hapa nchini vitengeneze dera badala ya kuwanufaisha mataifa ya mbali? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI (K.n.y. WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Amina Makilagi, Mbunge maalum na machachari kwa akina mama kama ifuatavyo:- (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikiri kama Serikali ni kweli, kwanza nitambue viwanda tulivyonavyo hapa nchini vingi kabisa tulivirithi toka ukoloni na vichache tulivijenga miaka ya 1970 na vingine miaka ya 1980. Viwanda ambavyo tunavyovitambua kama Mwatex, Murutex, Urafiki, ni vya Nida ndiyo vimeongezeka hivi karibuni. Kwa hiyo ni kweli kabisa viwango vyake ni vya chini na hiyo ninakubali.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hatua ambazo Serikali imechukua sasa kwa kutambua mabadiliko ya maendeleo siyo mabadiliko ya uchumi tu hata makuzi ya binadamu. Kwa hiyo ninatambua size za kina mama na hata akina baba, akina baba na nyie mko wapi? Na zenyewe zinakuwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ya kwanza ambayo Serikali imechukua viwango vilivyowekwa na TBS vinavyotumika sasa kwa upande wa nguo za kanga kama nilivyosema ni urefu wa sentimita 165 na upana sentimita 116. Lakini kwa upande wa vitenge urefu wa sentimita 200 na upana wa sentimita 116; lakini ni viwango vya mwaka 2009. Kwa hiyo sasa TBS mkakati wa kwanza kabisa inafanyia maboresho viwango hivyo, akina mama sasa mkae tayari kuvaa viwango vikubwa vya nguo. Viwango vinapitiwa na vitaanza kutumika mwezi Juni, mwakani.
Kwa hiyo akina mama Mheshimiwa Mwakilagi nikupongeze sana; Mheshimiwa Naibu Spika hata wewe nadhani unaendelea kukua utavivaa mwaka 2016.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mpango wa Pili ambao sasa Serikali inafanya, imetenga maeneo maalum kwa ajili ya viwanda vitakavyokuwa vinazalisha sasa nguo aina mbalimbali, vikiwemo vitenge vya kuvaa lakini hata ambavyo vimeshonwa, wametenga hekta 2100 kule TAMCO - Kibaha, pamoja na hekta 431 kule Kigamboni. Kwa hiyo Waheshimiwa akina mama taratibu za kiserikali zinafanyika kuwahakikishia sasa mtavaa nguo bila wasiwasi.
Kuhusiana sasa na madera ni kweli kabisa hata sisi akina baba tunashangaa, unaona akina mama wanavaa madera kila sehemu, kumbe ni kwa sababu hata nguo za kuwabana sasa siyo fashion tena. Sasa hatua za Serikali za makusudi kabisa ambazo imezichukua, sasa hivi vipo viwanda vitatu vinavyozalisha nguo za kuvaa, kiwanda cha kwanza ni cha TUKU ambacho kipo pale Mabibo, lakini viwanda vingine pamoja na Sunflag, pamoja na kile kiwanda cha Mzava karibu na maeneo ya Dar es Salaam.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mavazi aina ya madera Serikali imekaribisha wawekezaji wa Kichina na Kihindi ili waje wawashonee nguo sasa aina ya madera akina mama mnayoyataka. Kwa hiyo Serikali imeshachukua hatua asante sana Mheshimiwa.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri Tizeba kwa kuchaguliwa kuwa Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi na pia kumshukuru kwa majibu mazuri sana pamoja na kwamba ameanza kazi leo. Sasa naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa zao la mwani limekuwa likikabiliwa na changamoto nyingi sana ikiwemo kutofahamika kwa zao lenyewe lakini vilevile kukosa soko, pembejeo na hivyo kufanya wakulima wa mwani na hasa wanawake kuhangaika kutafuta masoko na pembejeo. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha zao hili la mwani linaongezewa thamani kwa kujenga viwanda katika maeneo yote yanayozunguka ukanda wa bahari ili zao hili lilete tija kwa wanawake na hasa ikizingatiwa kwamba zao hili limekuwa linachukuliwa tu na Wachina na soko lake liko China, Korea na maeneo mengine? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa vikundi vya ujasiriamali kwa asilimia kubwa vimekuwa vikitegemea mabenki ya kibiashara ambayo kwa kweli riba yao imekuwa kubwa sana na hivyo kufanya vikundi vya wanawake na vijana kushindwa kabisa kumudu kwenda kukopa katika mabenki hayo. Serikali ina mkakati gani kupitia upya mabenki yote na vyombo vyote vya fedha ili kuangalia hizi riba zinazotozwa na kulinganisha na hali halisi ilivyo ili wanawake na vijana waweze kunufaika na mabenki haya? Ahsante.
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kwa sasa hili zao la mwani soko lake siyo zuri sana hapa nchini. Kama alivyosema yeye mwenyewe, wakulima wa mwani wanauza kwa makampuni ya kutoka huko Korea, China na India.
Mheshimiwa Naibu Spika, Sababu kubwa ya msingi ya kutoongeza thamani ya zao hili hapa hapa nchini ni uzalishaji mdogo ambao uko katika zao hili kwa sasa. Ili uzalishaji uweze kuwa na tija kwa mwekezaji mwenye kiwanda kwa uchache zinahitajika tani 12,000 kwa mwaka au zaidi, ndiyo mtu akiwekeza kwenye kiwanda cha kuchakata mwani anaweza kupata faida. Sasa hivi uzalishaji tulionao ni tani 600 tu kwa mwaka.
Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana sasa Serikali, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, kupitia huu mradi wa SWIOFish tunajipanga kupitia vikundi vya uzalishaji wa mwani ili viweze kupatiwa mikopo. Nitoe wito kupitia nafasi hii kwamba Halmashauri zote ambazo ziko katika Ukanda wa Pwani watie jitihada kubwa katika kuviorodhesha hivi vikundi ili hizi fedha ambazo zinatolewa na Benki ya Dunia ziweze kutumika vizuri kwa vikundi hivyo vya akina mama na hata wasio akina mama kwa sababu zao hili siyo kwa ajili ya akina mama na vijana peke yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, ziko fedha ambazo Serikali imeshapata kutoka Benki ya Dunia, Dola za Kimarekani milioni 36. Dola za Marekani milioni 17 zitatumika kwa Tanzania Bara na Dola milioni 11 zitatumika kwa Tanzania Zanzibar na Dola milioni 8 hivi zitatumiwa na taasisi zinazohudumia utafiti katika eneo hili la uzalishaji viumbe katika Ukanda wetu wa Pwani.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kujibu swali lake la pili la nyongeza, hivi vikundi vijiorodheshe. Hizi fedha hasa ndiyo zimelenga kuwakomboa hawa watu wa vikundi kuondokana na mikopo ambayo siyo rafiki sana wakati mwingine kutoka kwenye taasisi za fedha kwa sababu, watapewa msaada wa pembejeo, ruzuku za dawa na vitu vingine ili kuwawezesha kuongeza uzalishaji wao. Tutakapofika tani 12,000 au zaidi, watu wengi wanayo nia ya kuwekeza katika viwanda hapa nchini vya kuchakata hizi mwani na ndiyo hapo sasa hata thamani ya hili zao itaweza kuongezeka.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Tatizo la nyumba na ofisi katika Halmashauri mpya ya Wilaya ya Nyang’hwale ni sambamba na matatizo katika Halmashauri nyingi zilizoanzishwa hapa nchini ambazo ni mpya. Sasa napenda kujua, je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha inatenga fedha za kutosha kwa ajili ya kujenga ofisi mpya na nyumba mpya katika Halmashauri zote nchini zilizoanzishwa ikiwemo na Halmashuri ya Butiama ambako ndiko alikotoka Baba wa Taifa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa mama yangu na wamama wa Tanzania, Mheshimiwa Mama Amina Makilagi kama ifuatavyo:- (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali hili ni lazima nilijibu taratibu sana kwanza. Kweli hoja aliyoitoa Mheshimiwa Mama Makilagi ni ya msingi sana, ndiyo maana siku tulipokuwa tukihitimisha bajeti yetu ya TAMISEMI nilisema kwamba Halmashauri zile mpya lazima tuhakikishe tunaweka miundombinu na ni lazima nyumba zijengwe. Ndiyo maana katika kipaumbele chetu sisi cha TAMISEMI katika bajeti yetu ya mwaka huu, tuliziorodhesha zile Halmashauri ambazo ujenzi unaanza, lakini Halmashauri nyingine mpya hata ujenzi haujaanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu swali hili ni kubwa na zito na limetolewa na Mbunge mzito, niseme yafuatayo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuliona hili tunaweka kipaumbele; kuna Halmashuri mpya zipatazo 20 tumezitengea kila moja shilingi bilioni 2,140,000,000 kila Halmashuri moja! Halmashauri hizo ni Buchosa, Bunda TC, Chalinze DC, Handeni TC, Ifakara TC, Itigi DC, Kasulu TC, Kibiti DC, Kondoa TC, Madaba DC, Mafinga TC, Malinyi DC, Mbinga TC, Mbulu TC, Mpimwa TC, Nanyamba TC, Newala TC, Nzega TC, Songwe DC na Tunduma TC. Hizi kila moja tumezitengea shilingi bilioni 2,140,000,000.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, kuna Halmashauri zipatazo 44 tumezitengea kati ya shilingi milioni 500 na shilingi milioni 850. Hii maana yake ni nini? Wajumbe mbalimbali inawezekana wakasimama hapa kutaka kujua juu ya hoja hiyo.
Nakala hii iko hapa, mtu anaweza akafanya reference katika Halmashauri yoyote ambapo mwaka huu tumeweka kipaumbele, lazima Ofisi ya Rais, TAMISEMI ihakikishe inajenga miundombinu katika maeneo hayo, ili mradi wafanyakazi waweze kupata huduma bora na waweze kupata mazingira rafiki ya kufanyia kazi.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri na kuipongeza Serikali kwa kuleta Muswada na Bunge lililopita Wabunge tukatunga sheria kali sana ambayo itawabana wale wote waliokuwa na tabia ya kuwaoa watoto. Ningependa kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni hivi karibuni Mahakama Kuu ya Tanzania iliiagiza Serikali iifanyie marekebisho Sheria ya Ndoa ya Mwaka 1971, kama kweli dhamira ni nzuri kama ambavyo Mheshimiwa Waziri ameeleza, ningependa kujua, ni kwa nini Serikali iliamua kukata rufaa badala ya kutekeleza maamuzi ya Mahakama? (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa sheria nyingi sana ambazo zinawakandamiza wanawake na watoto, bado zipo katika nchi yetu ya Tanzania, zikiwepo hata sheria za kimila na nyingine na nyingine. Ningependa kujua sasa, Serikali ina mkakati gani na hasa Wizara ya Katiba na Sheria, kuhakikisha inaleta sheria zote kandamizi zinazowabana wanawake na watoto ili sheria hizi tuweze kuzifanyia marekebisho? (Makofi)
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Amina Makilagi kwa kupigania haki za akinamama bila kuchoka, matunda ya juhudi zenu, wewe mwenyewe Mheshimiwa pamoja na wanawake wenzako yanaonekana.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kuhusu kesi iliyokuwepo Mahakamani na kwa nini Mwanasheria Mkuu wa Serikali imebidi akate rufani, nimeeleza katika jibu langu la msingi kwamba Serikali inaona tatizo katika Sheria ya Ndoa, si kwamba haioni tatizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kilichotupeleka Mahakama ya Rufani ni vitu viwili. Kwanza, Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971, tayari iko katika mchakato chini ya Wizara yangu na utaratibu tunaoutumia tulidhani itakuwa vyema kwa mshikamano wa Taifa letu tukaendeleza majadiliano kama tulivyofanya wakati wa kuitunga hii sheria ya mwaka 1971. Sisi tunataka tu kupata busara za Mahakama ya Rufani kuhusu suala hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, haki ya kukata rufani si tu ya wananchi, lakini vilevile hata Serikali pale ambapo inaona kuna kitu ambacho kinahitaji kupewa msimamo madhubuti zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii anaweza akatokea Jaji mwingine wa Mahakama Kuu akatoa uamuzi tofauti kwa sababu wote wako katika maamuzi. Sasa tunachotafuta na anachotafuta Attorney General ni kupata sasa maamuzi kwenye Mahakama yetu ya juu katika nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu, ni kweli kabisa bado kuna baadhi ya sheria zinamkandamiza mwanamke lakini naomba nimhakikishie Mheshimiwa Amina Makilagi na wanawake wenzake kwamba tumepiga hatua kubwa mno toka uhuru katika kuhakikisha kwamba mwanamke anapata haki sawa kama ambavyo Katiba yetu inavyosema chini ya Ibara ya 13.
Mheshimiwa Naibu Spika, tukumbuke, tumefanya mabadiliko ya sheria nyingi, tukumbuke Sheria ya Ardhi namba Nne (4) na namba Tano (5) imeondoa kabisa ubaguzi uliokuwepo kwa mwanamke. Sasa hivi mwanamke ana haki sawa chini ya sheria hizo. Leo si kawaida tena kwa mume akatoka tu asubuhi akauza nyumba, akauza kiwanja bila kupata ridhaa ya mama na mama akienda Mahakamani hiyo sale ama mauzo hayo hayana maana kabisa. Leo hii akinamama talaka haitokei akaondoka hivi hivi lazima kugawana matrimonial property, hizo zote kwa kweli ni faida ambazo tumezipata katika mabadiliko mbalimbali ya sheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii nenda Jela; wafungwa wengi wanaotumikia vifungo virefu katika nchi hii ni wale ambao wana makosa ya kunyanyasa akinamama. Namshukuru Mheshimiwa Makilagi ameelezea kuhusu sheria tuliyobadilisha juzi tu hapa Sheria ya Elimu ambapo leo hii mtoto wa kike aliye sekondari, aliye shule ya msingi, akipata mimba ole wako wewe uliyefanya hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, yote hii ni kulinda na baada ya muda si mrefu tutaleta Muswada hapa wa Huduma ya Msaada wa Sheria ambayo nakuhakikishia utakuwa mkombozi mkubwa hasa kwa akinamama walioko vijijini ambao katika mfumo tulionao usiojali mtu kutokujua sheria; kwamba ignorance of the law is not defence, akinamama wengi watafaidika sana. (Makofi)
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali moja la nyongeza. Kwa kuwa, wanawake wa Tanzania kwa kiwango kikubwa walio wengi ndiyo wakulima; na kwa kuwa wanawake wa Tanzania hawana fursa za kiuchumi zitakazowafanya wafikie Benki hii ya Wakulima kwa sababu ya kukosa dhamana. Napenda kujua Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha wanawake wengi ambao ni wakulima waishio vijijini wanafikia fursa hii ya kupata mikopo katika Benki ya Wakulima kwa lengo la kuwakomboa kiuchumi?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli wanawake wengi wa Tanzania ndiyo wanaojihusisha katika kilimo hapa nchini. Serikali kwa kutambua hilo imeweka mipango mbalimbali ikiwemo ukopeshaji wa vikundi vya akinamama katika uzalishaji kupitia Halmashauri zao lakini pia tunatoa kipaumbele katika Mfuko wa Pembejeo. Wanawake wanaokwenda kukopa katika Mfuko wa Pembejeo wanapata kipaumbele kwa sababu wao wanafahamika ndiyo wanaoshiriki zaidi katika shughuli za kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sio Benki ya Kilimo tu inayotoa mikopo katika sekta ya kilimo, benki nne hapa nchini kwa sasa zinatoa fedha katika shughuli za kilimo. Utoaji wa fedha hizi hauko katika shughuli yenyewe ya kilimo tu, isipokuwa benki zinatoa fedha katika mnyororo mzima wa thamani katika kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano Benki ya NMB mwaka huu pekee wa fedha imetenga shilingi bilioni 500 kwa ajili ya shughuli za kilimo na akinamama wana kipaumbele. Masharti ya mikopo katika benki ambazo tumezungumza nazo za NMB, Commercial Bank of Africa, CRDB, wote wamepunguza masharti katika mikopo ya kilimo ili kuwawezesha Watanzania wengi na hasa wale wasio na dhamana kuweza kupata mikopo hii kwa urahisi.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana na Ajira napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri amethibitisha kwamba kweli ziko sheria ambazo zimeshapitwa na wakati na Tume ya Kurekebisho ya Sheria ya Serikali inaendelea kuzifanyia marekebisho. Ningependa kujua ni sheria gani hizo sasa ambazo ziko katika huo mchakato na pia ningependa kujua hizi sheria zinaletwa hapa lini ili Bunge lako tukufu liweze kuzipitisha? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa kumekuwa na kilio cha muda mrefu na hata leo Mheshimiwa Mwenyekiti imethibitisha kwamba kumekuwa na kilio cha muda mrefu cha Waheshimiwa Wabunge Wanawake na Wabunge wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kumekuwa na kilio kikubwa sana cha wanawake na vijana juu ya kutungwa sheria ya mfuko wa wanawake na vijana na walemavu. Lakini pia kumekuwa na kilio cha muda mrefu cha wakulima wadogo wadogo kwamba kilimo chao hakiwaletei tija kwa sababu hakuna sheria inayoweka mfumo mzuri wa wakulima wadogo waweze kuletewa tija. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kujua sasa. Serikali ina mkakati gani wa kuleta hizi sheria Bungeni. Hili suala la kuwa kila siku tunaambiwa Serikali itaweka msukumo kuhakikisha asilimia 10 ya wanawake na vijana inatengwa ili tuweze kufikia mahali panapohitajika. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa namna ambavyo amekuwa mstari wa mbele kutetea maslahi ya akina mama nchini na ni kazi kubwa amekuwa akiifanya kwa ajili ya akina mama wa nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza anauliza ni sheria gani zipo katika mchakato. Kama nilivyosema, kazi kubwa ya Tume ya Kurekebisha Sheria ni kupitia sheria na baadaye kutoa mapendekezo kupitia taarifa mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka huu wa fedha Tume inafanya kazi ya mapitio ya sheria za mambo ya jinai (criminal justice) wanafanya pia mapitio ya sheria ya mambo ya evidence law, utoaji wa ushahidi mahakamani, lakini pia wanafanya mapitio ya sheria ya ufilisi (insolvency law) na vilevile wanafanya mapitio ya sheria ya huduma za ustawi wa jamii. Kwa hiyo, hizo ndiyo kazi ambazo zinafanyika katika mwaka huu wa fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika swali lake la pili ameuliza kuhusu lini Serikali italeta sheria mahsusi kwa ajili ya utungwaji wa uundwaji wa mifuko hii maalum kwa ajili ya akinamama na vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema Naibu Waziri kutoka Ofisi ya Rais, TAMISEMI, mifuko ya akina mama na vijana ipo na inaongozwa na miongozo yake tayari na imekuwa ikifanya kazi katika utaratibu huo wa kuchangia asilimia 10 hizo za mapato ya ndani ya Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mwongozi tayari upo. Labda ambacho kinaweza kikafanyika ambapo Serikali imekuwa ikijibu hapa ni kuboresha na kuona namna bora ya kuweza kuwafikishia kwa urahisi zaidi akina mama na vijana huduma hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la wakulima wadogo wadogo kutungiwa sheria. Kama Serikali tunaichukua na tutaona umuhimu wake hapo baadaye wa kuweza kulifanyia kazi.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri na jitihada za Serikali za kuongeza zana za uvuvi katika sekta hii ya uvuvi na pamoja na kupongeza jitihada zinazoendelea. Ningependa kujua, pamoja na mwanzo huu mzuri uliofanywa na Serikali, je, Serikali ina mkakati gani sasa wa kuongeza wigo zaidi ili zana hizi zipatikane katika bahari yote ya Tanzania? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa sekta ya uvuvi ni miongoni mwa sekta ambazo zinaweza zikaleta tija katika Taifa letu na kuongeza Pato la Taifa, tumeshuhudia miaka iliyopita wakati Mheshimiwa Rais, Dkt. Joseph Magufuli, akiwa Waziri wa Uvuvi, alikamata meli moja tu na ikaleta tija kwa Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujua Serikali ina mkakati gani wa kutengeneza meli za kutosha ili ziweze kwenda kuvua katika kina kirefu na kuongeza Pato la Taifa katika Taifa letu? (Makofi). Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana kwa kazi nzuri anayoifanya wakati wote ya kuwapambania wavuvi wa nchi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, anataka kujua juu ya mkakati wa Serikali wa kusambaza teknolojia hii. Katika jibu langu la msingi nimeeleza kwamba Taasisi yetu ya Utafiti ya TAFIRI inafanya utafiti wa kujiridhisha juu ya ufanisi wa teknolojia hii katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Mara tu baada ya kuwa tumefanikiwa na kujiridhisha kwamba teknolojia hii inaweza kutupatia tija, naomba nimhakikishie tutaisambaza kwa kiasi kikubwa katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu ikiwemo katika maeneo mengine ya bahari yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili, anataka kujua juu ya mkakati wa Serikali wa kupata meli kubwa kwa ajili ya kuweza kuvua na kupata faida kubwa kwa ajili ya nchi yetu. Naomba nimhakikishie kwamba Serikali tumejipanga vizuri na tupo katika programu ya kuhakikisha tunapata meli hiyo, hivi sasa tupo katika hatua kabla ya kwenda katika ununuzi wa meli hiyo, tuanzishe na kulifufua Shirika letu la TAFICO ambalo hili ndilo litakalokwenda kuwa msimamizi mkuu wa hata hiyo meli ambayo tunatarajia kuinunua.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba aendelee kuvuta subira na kutuunga mkono ilimradi tuweze kufikia katika hatua hii tunayoifikiria. (Makofi)
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, hapa nitoe ombi kwamba ni vizuri akatuletea takwimu hizi kwa maandishi kwa sababu tatizo la kutelekeza watoto ni kubwa sana katika nchi yetu, na mfano ni pale Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaama alipofanya zoezi la kuwatambua watoto waliotelekezwa. Nilikuwa naomba hapa atuletee kwa maandishi.
Mheshimiwa Spika, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa viwango vilivyowekwa vya kutunza watoto waliotelekezwa ni vidogo, lakini hata nilipopitia hii sheria haioneshi kwamba mzazi anayeacha watoto wake anatakiwa apeleke kiasi gani kwa mwezi au kiasi gani kwa mwaka badala yake ni busara ya Mabibi Maendeleo ya Jamii, badala yake ni mahakama zinatumia busara wanalipisha kiwango cha shilingi 2,000 kwa mwezi kiwango ambacho hakitoshi kabisa kutunza watoto.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuweka utaratibu wa kisheria utakaowafanya wazazi wanaotelekeza watoto waweze kubanwa kisheria na waweze kutunza watoto?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa sababu baadhi ya wazazi walio wengi katika jamii yetu wanatekeleza watoto kwa kisingizio kwamba si watoto wao, na kwa sababu katika vituo vyetu vya afya na katika zahanati zetu hapa nchini hakuna vipimo vya kupima DNA.
Mheshimiwa Spika, ningependa kujua sasa Serikali ina mkakati gani ili kupeleka vifaa hivi na kuweza kuwabana wazazi wote wanaokwepa kulea watoto wao kwa visingizio kwamba si watoto wao? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, mwitikio wa swali hili unaonesha kwamba suala hili la utelekezaji wa watoto ni changamoto kubwa hata ndani ya nyumba yako. (Kicheko)
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Amina Makilagi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taratibu tulizonazo ni kwamba, kiwango na gharama za matunzo ambazo zinatolewa yanapatikana baada ya kufanya assessment ya yule mhusika kuona hali yake ya kipato na hali ya maisha na umri wa yule mtoto na pale ndipo mahakama inaweka utaratibu wa kiwango ambacho kinatolewa. Mimi niseme tu kwamba katika suala hili sisi kama Wizara tunaendelea kufanya mapitio ya sera zetu na vilevile kuja na sheria ambayo itajaribu sasa kufanya mapitio ya yote haya kuangalia sasa ni utaratibu gani mzuri tunaweza tukaweka kuhakikisha kwamba wale wote wanaotelekeza watoto basi wanabanwa vizuri zaidi na sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili Mheshimiwa Makilagi ameuliza kuhusiana na kupanua huduma za upimaji wa DNA. Niseme tu kwamba upimaji wa DNA unafanywa na ofisi au taasisi ya Mamlaka ya Mkemia Mkuu wa Serikali. Upimaji huu si upimaji ambao holela mtu anaweza akanyanyuka akaenda na sampuli yake pale anapojisikia kwenda kufanya upimaji. Kuna taratibu ambazo zimewekwa kwamba ni mamlaka ikiwa ni pamoja na Mahakama, Maafisa Ustawi wa Jamii au Polisi ambao wanaweza wakaagiza na si kila mtu ambaye ukiwa na sampuli yako unafikiri kwamba mtoto si wako unaweza ukaenda pale ukafanya, hatufanyi upimaji, request zote zinapatikana kupitia mamlaka husika.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali moja la nyonge. Pamoja na kuishukuru Serikali kwa kazi nzuri sana iliyofanya ya kujenga miundombinu katika Mji wa Musoma kiasi kwamba maji sasa hivi yanapasua mpaka mabomba na maji yanayozalishwa kwa saa ni takribani lita elfu 12, lakini maji yale yanaweza kupelekwa mpaka Wilaya ya Butiama, Kata za Bukaga, Mkanga, Makatende mpaka Bisuma. Vile vile maji haya yanaweza kufika mpaka Jimbo la Musoma Vijijini katika Kata za Etalo, Nyakatende, Nyigima pamoja na Nyamimange. Ningependa kujua, je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha wananchi wa maeneo hayo ambako chanzo cha maji yaliyoleta maji ya Musoma wanaweza kupata na wenyewe huduma ya maji safi na salama kutokana na chanzo hicho cha maji? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nimpongeze Mheshimiwa Makilagi kwa kazi nzuri ya kuwatetea Wanamara, lakini kikubwa Serikali imefanya kazi kubwa sana ya kuwekeza mradi zaidi ya bilioni 45 pale Musoma. Kwa hiyo changamoto kubwa ni suala zima la usambazaji, sisi hilo tumeliona na tutahakikisha tunawekeza fedha ili tusambaze maji ili maeneo hayo aliyoyataja yaweze kupata maji safi salama na yenye kutosheleza.
MHE. AMINA N. MAKILLAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri na pamoja na kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri sana inayoifanya ya kujenga miundombinu ya maji, kiasi cha kufikia kiwango cha asilimia 80 mijini na asilimia 64.8 vijijini, napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Kwa sababu Mkoa wa Mara ni Mkoa ambao umezungukwa na Ziwa Victoria na una Mto Mara, Mto Robana, Mto Simiyu na Mto Suguti; lakini Mkoa wa Mara bado ipo changamoto kubwa ya upatikanaji wa majisafi na salama, kwa upande wa vijijini ni asilimia 50.7 na mijini ni asilimia 60. (Makofi)

MWENYEKITI: Swali.

MHE. AMINA N. MAKILLAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujua, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha Mkoa wa Mara ambao unazungukwa na Mito na Miji unapelekewa maji safi na salama na kufikia kiwango ambacho kimetajwa kwenye Ilani ya CCM?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Kwa kuwa kuna kazi nzuri sana inayofanywa na Serikali ya kutafuta fedha na kuwalipa Makandarasi wa miradi ya maji, lakini kwa Mkoa wa Mara tunalo tatizo kubwa sana. Kuna tatizo la kutolipa Wakandarasi. Wilaya ya Serengeti kuna miradi miwili, milioni 500 tayari wamesha-raise certificate hawajalipwa; Musoma Vijijini miradi mitatu, tumesha-raise certificate bilioni 1.6 hawajalipwa, Serengeti tuna miradi mitatu, shilingi milioni 500 haijalipwa na hata Butiama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujua Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha, kwa kuwa tumeshapeleka certificate, Wakandarasi waweze kulipwa fedha na miradi iweze kuendelea kwa sababu miradi yote imesimama na sasa ni mwezi wa nne? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda nimpongeze Mheshimiwa Amina Makillgi, amekuwa ni mtetezi mkubwa sana hususan suala linalohusu haki za huduma ya jamii ikiwemo katika suala zima la maji. Sisi kama Wizara Maji ni jukumu letu kuhakikisha Watanzania wakiwemo wana Mara wanapata majisafi, salama na yenye kuwatosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikakati katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji, Serikali imefanya jitihada kubwa sana. Ukienda Musoma, zaidi ya shilingi bilioni 45 za mradi mkubwa tumewekeza, kazi iliyobaki ni kwenda kusambaza maeneo ambayo hayana maji wapate maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati uliopo sasa hivi, tuna miradi zaidi ya 26 ambayo hivi karibuni tunataka tuitekeleze. Tupo katika hatua ya utangazaji wa tender kwa maana ya manunuzi. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika miji 26 kupitia fedha za India, dollar takribani zaidi ya milioni 500 katika miji ya Tarime pamoja na Mgumu kwa kaka yangu Mheshimiwa Ryoba nao watapatiwa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tupo katika hatua za mwisho sasa za kumpata Mkandarasi katika kuhakikisha tunaanzisha mradi ule mkubwa wa Mgango – Kyabakari mpaka Butiama katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji kwa Mheshimiwa Muhongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa na cha msingi kabisa kuhusu suala zima la kuwalipa Wakandarasi, sisi kama Wizara ya Maji, wapo baadhi ya Wakandarasi wanafanya kazi nzuri. Sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo katika kuhakikisha Wakandarasi wote waliofanya kazi nzuri za kutekeleza miradi ya maji, tutawalipa kwa wakati, lakini kwa wale wababaishaji, lazima tuwashughulie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa namwomba Mheshimiwa Makilagi tukutane baada ya saa 7.00 tuone certificate zake na tuweze kujiridhisha ili tuweze kuwalipa Wakandarasi wake na wananchi wake wa Mara weweze kupata majisafi na salama na yenye kutosheleza. (Makofi)
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2018 katika bajeti tulipisha sheria kwamba kila Halmashauri ni lazima kutenga 10% ya wanawake na vijana watu wenye ulemavu. Hivi sana ninavyozungumza zipo Halmashauri hapa nchini, ikiwemo Wilaya Butiama hawatoi mikopo kama ambavyo sheria tulivyoipitisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujua, nini kauli ya Serikali katika kuhakikisha Wakurugenzi wanatekeleza maagizio ya Bunge kutenga 10% ya wanawake, vijana na walemavu ili kusaidia katika vikundi na kuleta tija kwa wanawake, vijana na walemavu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA):
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ni kweli kwamba sheria imeshatungwa na kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi ni kwamba huko nyuma hatukuwa na sheria, sasa sheria ipo in place inafanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwapongeze Wajumbe wa Kamati ya Wizara ya TAMISEMI, walikumbusha Wajumbe, walitoa maelekezo kwenye mikoa na Halmashuri zote nchini na wakatoa masharti kwamba kipindi kijacho, kama kuna Halmashauri ambayo haijapeleka fedha hizo kwa mujibu wa sheria, hao watapata taabu sana katika Kamati ile wakati wanaleta bajeti yao mwaka ujao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maelekezo ni kwamba kama umekusanya shilingi 100/=, baada ya kuondoa yale makato ya kisheria kabla ya kupeleka zile fedha kwenye makundi muhimu yaliyotajwa, ni lazima 10% ya fedha hiyo ipekwe kwenye vikundi na igawanywe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama Halmashauri ya Butiama haijapeleka fedha, najua walipokuja kwenye Kamati ya Bunge walikuwa wameweka asilimia ndogo karibu 15% au 25% ambayo wakikuwa wamepeleka, lakini tumepata manung’uniko ya hapa na pale; Mheshimiwa Mbunge najua ni mwenyeji mkaazi wa Mkoa wa Mara, naomba nitoe maelekezo tupate taarifa mahsusi kwa Halmashauri ya Butiama kama kweli hawajapata fedha hizi. Mkurugenzi, ikifika kesho saa 7.00 tupate taarifa kama amepeleka fedha kiasi gani; vikundi gani vimepelekewa? Ili tuweze kumaliza jambo hili. Ahsante.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri na kazi nzuri inayofanywa na Serikali katika kuhakikisha inatokomeza ukatili wa watoto na wanawake, nina maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada hizo lakini ni ukweli usiopingika masuala ya ukatili wa wanawake na watoto bado ni ya kiwango kikubwa sana. Tumeshuhudia watoto wanafanyiwa ukatili na Mheshimiwa Waziri Mkuu juzi alikuwa anazindua tuliona hata zile takwimu wanawake wajane wananyang’anywa mali zao hasa viwanja na mali nyingine lakini watoto yatima na wanawake majumbani na hata kwenye familia zao bado wanafanyiwa ukatili…

MBUNGE FULANI: Kubakwa.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Ndiyo, kubakwa na halikadhalika na hata kufanyiwa ulawiti.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba Serikali imefanya kazi nzuri ya kutunga sheria inayotoa fursa kwa watu wanaofanyiwa ukatili kwenda kupata haki yao bila kujali anacho au hana, kazi hii imekuwa ikifanywa na mashirika yasiyo ya Kiserikali. Napenda kujua Serikali imejiandaaje kutenga bajeti kwa ajili ya kutekeleza mpango huu ili kutuachia peke yake mashirika yasiyo ya Serikali ambayo na yenyewe yanategea misahada kutoka nje? Hilo swali la kwanza.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, napenda kujua ni mkakati gani sasa umewekwa na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto wa kuratibu na kuona hao wanawake na watoto wanaopata msaada wa kisheria ni matokeo gani yamepatikana na changamoto zilizopo na Serikali inajiandaaje na kukabiliana na changamoto hizo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Amina Nassoro Makilagi kwa kazi kubwa ambayo anaifanya ya kufuatilia masuala mbalimbali yanayohusiana na ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto.

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba suala hili sisi kama Serikali tunalichukulia kwa kipaumbele kikubwa sana na ndiyo maana tumeanzisha Mpango Mkakati wa Kutokomeza Ukatili wa Kijinsia dhidi ya Wanawake na Watoto.

Mheshimiwa Spika, kupitia mkakati wetu huu imetusaidia sana maana matukio haya yanakuwa reported kwa kiasi kikubwa sana, kwetu sisi kama Serikali inatupa faraja kubwa sana. Kati ya Januari na Desemba, 2017 matukio 41,000 yaliripotiwa ndani ya nchi yetu na kati ya hayo 13,000 yalikuwa ni ukatili ya kijinsia dhidi ya watoto. Kwa hiyo, mwamko katika jamii umekuwa mkubwa sana.

Mheshimiwa Spika, nikiri kwamba Serikali imepitisha Sheria ya Usaidizi wa Kisheria, Namba 1 ya mwaka 2017 na kwa kiasi kikubwa sasa hivi usaidizi huu wa kisheria umekuwa unapitia katika taasisi zisizo za kiserikali, Serikali imeliona hilo na iko katika hatua mbalimbali za kuhakikisha kwamba tunaanzisha Legal Aid Fund ambapo sasa Serikali itatenga fedha kwa ajili sasa ya usaidizi wa kisheria pale mashauri haya yatakapokuwa yanajitokeza.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, Serikali imeendelea na hatua mbalimbali na iko katika hatua za mwisho za kuandaa Sera ya Ardhi, umilikiwa ardhi ulikuwa ni changamoto kubwa sana kwa wanawake. Sasa hivi Sera hii ya Ardhi inaenda kuweka utaratibu mzuri kuhakikisha kwamba wanawake nao wanakuwa na sauti katika masuala ya umiliki wa ardhi ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sisi kama Wizara tunaendelea kufuatilia utekelezaji wa Sera hii ya Kutokomeza Ukatili wa Kijinsia dhidi ya Wanawake na Watoto. Kwa kiasi kikubwa mwamko umezidi kuwa mkubwa lakini niendelee kutoa rai tu kwa jamii kueleza kwamba masuala mengi ya ukatili wa kijinsia yanafanywa na watu ambao wapo karibu na familia. Tuendelee kutoa taarifa na niombe sana masuala haya tusiyamalize ndani ya familia badala yeke tuhakikishe kwamba vyombo vya dola vinapewa fursa ya kuweza kuyashughulikia badala ya familia kuyamaliza ndani ya familia.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Mara ni miongoni mwa mikoa ambayo Serikali ya Chama cha Mapinduzi imeipa miradi mikubwa ya barabara ya kutoka Kisolya mpaka Bunda na barabara ya kutoka Makutano Butiama mpaka Mugumu. Barabara hizi zimekuwa zikijengwa kwa kusuasua, napenda kujua ni lini ujenzi wa barabara hizi utakamilika maana sasa ni miaka sita (6) tangu ujenzi uanze?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Makilagi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuna ujenzi wa barabara unaendelea katika Mkoa wa Mara na Mheshimiwa Mbunge anafahamu na mara nimpongeze tu amekuwa akifuatilia sana hizi barabara. Mradi unaoendelea sasa hivi ni barabara kutoka Bulamba kwenda Kisolya.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Mbunge anafahamu kwamba Mheshimiwa Rais, Dkt. Magufuli alipofanya ziara katika Mkoa wa Mara alitoa maelekezo ili tuweze kujenga barabara hii kutoka Bulamba – Bunda -Nyamuswa kilometa 56. Utaratibu wa hatua ya manunuzi unaendelea na wakati wowote tutapata mkandarasi ili barabara hii ijengwe. Mheshimiwa Mbunge pia anafahamu tunajenga barabara kutoka Makutano – Sanzate, ni kweli kuwa barabara hii na mimi nimeitembelea ilikuwa inasuasua kidogo lakini tumechukua hatua ili kwa haraka hii iweze kukamilishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara nyingine ambayo itakuwa inashughulikiwa kwa maana ya kutangaza kupata mzabuni kutoka Sanzate - Nata. Kwenye mpango huu wa bajeti ambao tumepitishiwa na Waheshimiwa Wabunge juzi tutatoka tena kutoka Nata - Mugumu lakini tutatazama pia kujenga barabara kutoka maeneo ya Mugumu - Tabora B ili tuunganishe kwenda mpaka Loliondo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, iko mipango mizuri tu, nimwombe Mheshimiwa Mbunge avute subira lakini kwa Mkoa wa Mara tumejipanga vizuri yale maeneo ambayo wananachi walikuwa na shida sasa neema inakuja. Ahsante sana.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, Kaka yangu Kandege, pamoja na kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri sana iliyofanya ya kuboresha hiki kituo muhimu cha Kiagata ambacho sasa kinatoa huduma kwa kiwango cha ufanisi, na pia kuishukuru Serikali kwa kazi nzuri sana iliyofanya ya kujenga vituo zaidi ya tisa katika Mkoa wa Mara, nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuayavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; kwa kuwa kituo cha Kiagata na hata hospitali ya Wilaya ya Butiama ina upungufu wa wataalam kwa kiwango cha asilimia 70, kwamba pia lipo tatizo kubwa la wataalam wa mionzi lakini vilevile hakuna x-ray kwa Wilaya nzima ya Bitiama ikiwemo hospitali ya Wilaya na hata kituo cha Kiagata.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha inapeleka wataalam katika hospitali ya Butiama na Kituo cha Kiagata na hasa kipaumbele kikiwa ni wale watalam wa mionzi kwa ajili ya wakina Mama?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa Wilaya ya Butiama kwa mujibu wa sensa ina watu zaidi ya 200,003 na Butiama ni Wilaya ya kazi, watu wanakula wanashiba, population ya watu inaongezeka.

Vilevile kwa kuwa Wilaya ya Butiama ina kata 18 na ina vitongoji 370 lakini Kituo cha Afya ni kimoja tu cha Kiagata ambacho kinahudumia hata wananchi wote wa Wilaya y Butiama; Tarafa ya Makongoro iko mbali na Kiagata, Wananchi wa Makongoro wanapata shida sana kwenda Kituo cha Afya cha Kiagata;

(i) Ni mkakati gani sasa wa Serikali wa kuboresha Kituo cha Bisumwa ili kiwe sasa kituo cha afya, ili kisaidie Kata saba?

(ii) Serikali ina mkakati gani wa kuboreshga Zahanati ya Kirumi ili sasa isaidie Kata sita?

(iii) Na Serikali ina mkakati gani wa kuboresha Zahanati ya Buhemba ili iweze kusaidia wananchi wa Wilaya ya Butiama?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Amina Makilagi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba uniruhusu nipokee pongezi ambazo ametoa kwa Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi inayofanya ya kupeleka huduma za afya jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza, anaongelea suala zima la uharaka wa kuhakikisha kwamba wanakuwepo wataalam, na hasa wataalam wa mionzi, ili kazi nzuri iliyofanyika Kituo cha Kiagata iweze kutoa matunda. Naomba nitumie fursa hii kumuagiza Mganga Mkuu wa Wilaya, miongoni mwa wataalam waliopo ateue angalau mtaalam mmoja akasomee kazi ya mionzi ili huduma ianze kutolewa ili huduma ianze kutolewa wakati Serikali inafikiria kupeleka wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ametaja kituo cha afya lakini na zahanati kama tatu, sina uhakika kama ni swali moja lakini naomba itoshe tu nimambie Mheshimiwa Makilagi, kazi kubwa, nzuri ambayo anaipigania kuhakikisha hasa akina mama wanapata huduma ya afya, sisi kama Serikali tuko pamoja na yeye.

Naomba nitoe wito kwa halmashauri kuhakikisha kwamba maombi yote ambayo Mheshimiwa Amina Makilagi ameyatoa hapa yanazingatiwa katika bajeti hii ambayo inaandaliwa na sisi Serikali Kuu hakika hatutamuangusha. (Makofi)
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuishukuru Serikali kwa kazi nzuri inayoendelea ya kujenga hiki Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, mawazo ambayo mwenyewe aliyaasisi na yakapokelewa na Mbunge wetu Mheshimiwa Mkono ambaye alitoa hata maeneo ningependa kuuliza swali moja la nyongeza kama ifuatavyo:-

Kwa kuwa, kutokana na changamoto ya radhi, Serikali ilishajipanga na tukaainisha maeneo kupitia kikao cha RCC Mkoa wa Mara, kwamba kuna majengo ambayo yapo katika Chuo cha Kisangwa-Bunda na kuna majengo mengine ambayo yako katika Chuo cha Shirati, na kuna majengo ambayo yako katika Chuo cha Wananchi-Bweri; na yale majengo yaliyopo yanaweza hata kupokea watoto.

Ningependa kujua, kwa kuwa Serikali bado inaendelea na mchakato na kwa kuwa pale kuna wafanyakazi sasa ni takribani miaka mitatu hawana kazi ya maana ya kufanya, ni lini sasa Serikali itawapanga watoto waende kuanzisha masomo pale wakati tukisubiria sasa fedha nyingi kwa ajili ya kuongeza majengo na maeneo mengine, ikiwa ni hatua muhimu sana ya kujenga mawazo ya Baba wa Taifa ambaye kwa kweli alijitoa, alitoa mpaka eneo, alijenga mpaka na Bwawa la umwagiliaji ambalo wananchi wameendelea kulilinda kwa muda mrefu sana?

SPIKA: Mheshimiwa Amina kwahiyo unapendekeza ihamishwe Butiama iende Bunda…

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Inabaki pale pale…

SPIKA: …na huko ulikotaja; hebu weka vizuri swali lako.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Spika, kwa mawazo yaliyokuwepo ni kwamba chuo kitaanzia pale na watoto watakuwa pale na majengo ya kusomea yapo, watakapokuwa…

SPIKA: Pale una maana ya Butiama?

MHE. AMINA N. MAKILAGI: …ni Butiama ila wanapkwenda field kwa ajili ya masomo kwa vitendo kuna maeneo mengine ambayo yako ambapo wangekwenda kufanya practice.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Makilagi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kumekuwepo na mapendekezo mbalimbali ya namna ya kuanzachuo kile wakati tunasubiri ujenzi uanze. Hata hivyo Wizara imekuwa ikiangalia vilevile athari ambayo inaweza ikatokea kama tutatumia majengo ya vyuo vilivyopo ambavyo navyo vina umuhimu Kitaifa katika chuo ambacho tunaanzisha. Kwahiyo busara ambayo sisi tumeifikia ni kwamba hatuna haraka sana tusije tukavuruga utaratibu uliopo kwenye vyuo vingine kama hivyo anavyotaja lakini tusubiri mpaka hiki tuanze kujenga.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuhisiana na maeneo ya kufanya mazoezi, kwasababu Chuo kile sehemu kubwa itakuwa ni kwa ajili ya kuwasaidia wakulima kuweza kufanya mafunzo mafupi ya kilimo, Wizara inaendelea kutafuta ardhi katika maeneo ya jirani ikiwemo pamoja na Wilaya ya Serengeti ili tuweze kuwa na sehemu ya kufanyia mazoezi. Kwahiyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba nia ya Serikali iko pale pale, chuo kile kitaanza na naomba wavute subira, lakini naomba wote kwa ujumla wao tusaidiane kuondoa changamoto za upatikanaji wa ardhi pale kwenye Chuo cha Uhamilishaji lakini vilevile katika kuweza kupata eneo lile la Oswald Mang’ombe tuweze kupata hati ili hatimae chuo kiweze kumiliki.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri na kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri inayoifanya kwa ajili ya kuimarisha ushirika, nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa huko nyuma tulikuwa na Mara Corp, tulikuwa na SHIRECU, tulikuwa na Nyanza, tulikuwa na KCU. Viongozi wake walikuwa na nguvu, weledi na uwezo, lakini vyama vile vya ushirika vilikuwa na mitaji kiasi kwamba vile vyama vya ushirika ndiyo vilivyonunua mazao ya wakulima na siyo kununua peke yake, hata kusindika na mfano ni Mkoa wa Mara, tulikuwa na Kiwanda cha Mwatex na Mwanza walikuwa na Mutex na Mwanza, lakini tulikuwa na Mgango Ginnery, tulikuwa na Ushashi Ginnery, tulikuwa na taasisi mbalimbali kwa ajili ya kusindika mazao ya wakulima. Sasa ushirika huu umeanza, viongozi wake hawana weledi, hawana mafunzo, lakini ushirika hawana mitaji na viwanda vile vya kusindika mazao vingi vimekufa.

MWENYEKITI: Uliza swali sasa.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kujua Serikali ina mkakati gani kuhakikisha inapatia ushirika mitaji ili vyama hivi viweze kujiendesha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa tulianzisha Benki ya Kilimo kwa ajili ya kuwakomboa wananchi na hasa wanawake na kwa kuwa vipo vikundi vingi vya wanawake vilivyoanzishwa kwenye SACCOS kwa ajili ya kilimo, ningependa kujua Benki ya Kilimo itafika lini kwa ajili ya kuwakopesha wanawake vijijini katika ushirika wao wa kilimo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mfumo wa ushirika wa SHIRECU na vyama vingine vya ushirika wakati ambao anaongelea Mheshimiwa Mbunge, mfumo wa uchumi ambao nchi ilikuwa inaenda nao ulikuwa ni mfumo hodhi. Kwa hiyo mfumo ule wa ushirika wa wakati ule ulikuwa ni compatible na zama zile na wakati ule. Sasa hivi ni mfumo wa soko, hatuwezi kurudi katika mfumo uliokuwepo wakati wa nyuma. Lakini tunachokifanya sisi kama Serikali sasa hivi ni kupitia upya Sheria ya Ushirika ya mwaka 2002 wakati huohuo kupitia Sheria ya Ukaguzi ya Vyama vya Ushirika ya mwaka 1985 na kupitia mfumo mzima wa uendeshaji wa ushirika ili vyama vya ushirika viweze kuwa vya kibiashara na vijiendeshe kibiashara zaidi na kuwa competitive katika soko ambalo ni soko huria linaloruhusu watu binafsi kufanya biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu suala la ushirika kupewa mitaji na Serikali; hili jambo haliwezekani. Kisera ya kiuchumi hatuwezi Serikali kuwapelekea vyama vya ushirika kupewa mitaji ya kujiendesha, lakini Serikali inachoweza kukifanya ni kuvifanya vyama vya ushirika kuwa strong na viweze kukopesheka na viweze kufanya biashara ili viwe vina sura ya kuendesha na kutengeneza faida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la Benki ya TADB; TADB ni development bank na wala siyo commercial bank kama benki zingine, haiwezi kufungua matawi nchi nzima, lakini pale ambapo ama chama cha ushirika au wananchi ambao wanaendesha miradi ya kilimo ya kimkakati wana business plan wanaweza kwenda ku-access mikopo katika Benki ya Maendeleo ya Kilimo ili tuweze kuendeleza infrastructure ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri Waheshimiwa Wabunge wakaelewa, Tanzania Agricultural Development Bank ni development bank na siyo commercial bank, haiwezi kufanya kazi za commercial bank, inafanya kazi za kuwekeza kwa miradi ya muda mrefu kwenye sekta ya kilimo. Kwa hiyo hawawezi kwenda kufungua matawi katika wilaya na mikoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu akina mama; akina mama Tanzania Women Bank imeunganishwa na Postal Bank na facilities za akina mama kuweza kukopeshwa mikopo midogo midogo inapatikana kupitia Benki ya Posta kwa akaunti maalum ambayo imeanzishwa kama product kupitia benki ile.

Kwa hiyo, ninataka niwaombe Waheshimiwa Wabunge watusubiri wakati tunapitia Sheria ya Ushirika na kubadilisha mfumo wa uendeshaji wa ushirika ili uweze kuendana na mahitaji ya sasa na kuwajengea imani wananchi. Nashukuru. (Makofi)
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali moja la nyongeza, pamoja na kazi nzuri iliyofanywa na Serikali yetu ya chama cha Mapinduzi kujenga mradi mkubwa wa maji na kufikia kiwango cha asilimia 90 wananchi wanapata maji. Pamoja na mipango iliyopo ya kupeleka maji Mji wa Mgumu, Mji wa Rorya na Mji wa Tarime na Mganga Kiabakari Butiama, Mkoa wa Mara bado unazungukwa na ziwa lakini changamoto ya maji ni kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, ningependa kujua Serikali imejipangaje kuhakikisha Mkoa wa Mara katika Vijiji vyote vya Mkoa wetu ambavyo vinazungukwa na ziwa za Victoria vinapelekewa maji, safi na salama? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimimiwa Spika, nipende kumpongeza Mheshimiwa Mbunge mama yangu mama Kilagi kwa kazi kubwa anayoifanya kuwapigania wakinamama wa Mara si mara moja na wala si mara mbili na amewekuwa mfuatiliaji mkubwa sana hususani katika suala hili.

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wizara kwa kutambua changamoto hii ya maji tumetenga fedha au tulizopewa na Mheshimiwa takribani dola milioni 500 katika kuhakikisha kwamba tunatatua tatizo la maji zaidi ya Miji 28 na tumesha saini mkataba. Nataka nimuhakikishie katika Miji ya Mgumu pamoja na Tarime ile kazi inaenda kufanyanyika kwa haraka.

Mheshimiwa Spika, lakini kingine tunaenda kusaini sasa wa mkaba wa kupeleka maji Mganga Kiabakari Butiana katika kuhakikisha tuna tatua tatizo hili la maji. Kazi hizi tutazifanya kwa haraka pia bajeti yako umetuidhinishia wizara yetu ya Maji zaidi ya bilioni 610 katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. Nataka nimuhakikishie sisi kama viongozi kwa kushirikiana na Mheshimiwa Mbunge tutafanya kila linalowezekana katika kuhakikisha tutatatua tatizo la maji katika Mkoa wa Mara. (Makofi)
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba niipongeze Serikali kwa kazi nzuri inayoifanya ya kuhakikisha inaboresha huduma za afya kwa ajili ya kupunguza vifo vya wanawake wanaojifungua. Pamoja na pongezi hizi nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza; moja ya sababu inayofanya wanawake wengi wanafariki kwa kujifungua ni kutokana na kutokwa damu nyingi wakati wakijifungua, lakini lipo tatizo kubwa sana la ile Benki ya Damu katika Hospitali za Mikoa. Kwa mfano, Kanda ya Ziwa Mikoa yote sita tunategemea Bugando. Damu inatolewa Serengeti, Bunda, Simiyu, Geita, Kagera, Shinyanga mpaka Tabora na Kigoma lakini inatakiwa iletwe Bugando kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi.

Mheshimiwa Spika, wakati huo huo damu ikishatolewa kwenye mwili wa Mwanadamu inatakiwa ikae siku 30 baadaye ina-expire. Kwa hiyo, unakuta kutokana na tatizo na ule msongamano ulioko Bugando, damu inachelewa kurudi kule kwenye Vituo vya Afya na kwenye Hospitali za Mkoa na kwenye Hospitali za Wilaya. Ningependa kujua sasa, Serikali ina mkakati gani wa kujenga vituo vya Benki ya Damu katika Hospitali za Rufaa zote nchini pamoja na Hospitali za Wilaya na ikiwezekana hata Vituo vya Afya? Hilo swali la kwanza.

Mheshjimiwa Spika, swali la pili; moja ya sababu ya wanawake wanaofariki kwa kujifungua ni pamoja na kutoa mimba au mimba kutoka. Siku hizi humu mitaani kwenye maduka ya pharmacy kuna dawa zinaitwa misoprostol, Madakrati mtanisaidia kuijua vizuri maana mimi siyo Daktari. Vijana wa kike na wanawake huko mtaani wanafundishana siku hizi ndiyo wanazotolea mimba na hasa zile mimba ambazo hazikutarajiwa.

Mheshimiwa Spika, napenda kujua, Serikali ina mkakati gani wa kudhibiti hali hiyo? Kwa sababu wanapokunywa zile dawa, mimba inatoka lakini wakati mwingine kile kiumbe kinabaki ndani kinasababisha maambukizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningependa kujua Serikali ina mkakati gani wa kudhibiti hali hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Afya, naomba nimjibu Mheshimiwa Mama yangu Mheshimiwa Amina Makilagi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza ni kwamba kweli akina mama wanapojifungua wakati mwingine damu nyingi hutoka na kuweza kupoteza maisha yao. Ushauri wangu tu ni kwamba akina mama wafuate masharti wanapokwenda kwenye kliniki wakati wa ujauzito, kuna elimu wanapewa wakati huo. Vilevile wakati wa kujifungua na hasa mimba ya kwanza ni kwamba akina mama ni vizuri wakajifungua kwenye Vituo vya Afya. Wakati mwingine wanapokuwa wanajifungua nje ya Vituo vya Afya au hospitalini hasa kwa ule ujauzito wa kwanza, inakuwa ni hatari sana, kwa sababu huwa wanafanyiwa kitu kinaitwa Episiotomy ambayo ni kuongeza njia wakati wa kujifungua. Sasa ile inafanya damu zinatoka nyingi, usipo-repair vizuri kwa wakati, mama huyu anaweza kupoteza maisha yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la kuwa na blood bank ni kwamba huu ni mkakati ambao kila hospitali inatakiwa iwe na blood bank hata kama ni kiasi kidogo, wanahifadhi damu kwa ajili ya matumizi, pale inapotokea kuna dharura, basi waweze kumpa mgonjwa waweze kuokoa maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile kuhusiana na suala la hizi dawa ambazo ni Misoprostol, hizi dawa huwa zinatumika katika kuondoa au kutoa mimba. Dawa hizi huwa zinatakiwa zitolewe chini ya usimamizi wa daktari, yaani daktari ndiye anayetakiwa aandike dawa hiyo. Mgonjwa anapokwenda pharmacy, basi aende na cheti cha kuweza kupewa dawa hiyo. Hizi dawa huwa zina matumizi mengine.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna dawa hizo zimeanza kuzunguka ziko kwenye ma-pharmacy na dawa hizi ni za kazi maalum kwa kuzuia damu zisitoke, lakini wanazitumia vibaya kwa sababu side effect ya hiyo dawa ni kuweza kutoa mimba. Kwa hiyo, tunawashauri watu wote wenye pharmacy wasitoe dawa hizi bila prescription. Lazima dawa hii daktari athibitishe, aandike cheti, ampeleke kwenye pharmacy na mgonjwa aweze kupewa dawa hiyo. Kwa maana tunafahamu kabisa madaktari wanapotoa dawa hizo wanazitoa kwa sababu maalum.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)