Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. John Wegesa Heche (9 total)

MHE. JOHN W. HECHE aliuliza:-

Tathmini ya Mgodi wa Nyamongo (ACACIA) kwa wakazi wa Vijiji vya Nyakunguru, Kewanja, Nyangoto, Matongo kupisha upanuzi wa uzalishaji wa mgodi ilifanyika kuanzia mwaka 2012 ambapo wananchi walizuiwa kuendeleza maeneo yao:-

(a) Je, Wananchi hao watapewa lini fidia kutokana na maeneo yao kulingana na bei ya sasa?

(b) Je, fidia hiyo itaendana na usumbuu na hasara waliyoipata hadi sasa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa John Wegesa Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba wananchi hawajaanza kulipwa fidia, ukweli ni kwamba fidia imeanza kutolewa na imelipwa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kijiji cha Nyakunguru, awamu namba 24, awamu namba 34 na awamu namba 35 kijiji hiki kina ukubwa wa hekta 35. Makadirio ya fidia ilikuwa shilingi bilioni mbili, lakini ziliongezeka hadi kufikia bilioni ishirini na saba kutokana na ujenzi holela na upandaji wa mazao unaofanywa na baadhi ya wananchi wasio waaminifu wakati wa fidia ikifanyika maarufu inaitwa mtegesho.

Mheshimiwa Spika, kutokana na hali hiyo, mgodi umeamua kuliacha eneo hilo na kutumia njia ya uchimbaji wa chini ya ardhi yaani underground mining method. Aidha, awamu namba 22 mheshimiwa spika, 23, 25, 28, 29, 33 na 44 yenye ukubwa wa eneo la hekta 90.4 ambao fidia yake ni shilingi bilioni 12 ililipwa kati ya mwaka 2012 na 2014.

Mheshimiwa Spika, kijiji cha Kewanja, awamu namba 30. Ukubwa wa kijiji hiki ni hekta 8.10. Makadirio ya fidia yalikuwa shilingi milioni 250 lakini kwa sababu ile ile ya ujenzi holela na upandaji wa mazao unaofanywa na baadhi ya wananchi wasio waaminifu, fidia pia iliongezeka kutoka shilingi milioni 200 hadi kufikia shilingi bilioni 8.3. Mgodi umeamua kuliacha eneo hilo kwa sababu hauna fedha ya kuwalipa, aidha awamu namba 26, 27 na 31 jumla ya hekta 26.8 zililpwa fidia ya shilingi bilioni 8.8.

Mheshimiwa Spika, kijiji cha Nyangoto, awamu namba 20, namba 36, namba 37, namba 38, namba 40, 41, 42 na 44, kijiji hiki kina ukubwa wa eneo wa hekta 115.79, jumla ya fidia iliyolipwa kwa mgodi huu ilikuwa ni shilingi bilioni 41.14.

Mheshimiwa Spika, ieleweke pia katika awamu ya 20, jumla ya hundi 157 zenye thamani ya shilingi bilioni 3.7 bado hazijachukuliwa na wafidia, baada yao kusingizia kwamba pesa hiyo waliyolipwa ni kidogo mno.

Mheshimiwa Spika, kijiji cha Matongo, awamu namba 39, mgodi ulihitaji eneo kwa ajili ya kinga ya kiusalama tu ambao ni Bufferzone ya mita hasa 200 wakati wa ulipuaji baruti kati ya eneo la mgodi na wananchi, lakini kwa sababu ya tegesha ile ile, mgodi uliamua sasa kuachana na eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, fidia husika hulipwa kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi Na. 4 na Sheria ya Ardhi ya Vijiji Na. 5 zote za mwaka 1999. Fidia hii ni kulingana na thamani ya kipindi ambacho tathmini ilifanyika, lakini pia fidia hizi zilizingatia usumbufu na uharibifu wa mali za wadai husika. Aidha, wananchi wa maeneo hayo wanatakiwa kujua kwamba viwango vya fidia vinavyotolewa na mgodi wa North Mara ni vikubwa zaidi ya viwango vinavyowekwa na Serikali. Kutokana na ukweli huo, wananchi wote wanaotakiwa kuchukua fidia na kupisha shughuli za uchimbaji wanashauriwa sasa wachukue fidia ili kupisha shughuli za uchimbaji.
MHE. JOHN W. HECHE aliuliza:-
Wakati wa kampeni ya Urais mwaka 2015, Mheshimiwa Rais John Pombe
Magufuli aliwaahidi wananchi wa Mji wa Nyamwaga kuwa ataanzisha
mchakato wa kuwalipa wazee pensheni zao kwa wakati:-
Je, mpango huo muhimu utatekelezwa lini?
MHE. ANTONY P. MAVUNDE - NAIBU WAZIRI (SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA,
VIJANA NA WALEMAVU) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri Mkuu, napenda kujibu swali
namba 77 la Mheshimiwa John Wegesa Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini, kama
ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais ana dhamira ya dhati ya kuhakikisha Wazee wote nchini wanapata pensheni ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi na ahadi ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa kwenye mikutano ya kampeni Serikali imejipanga kutekeleza mambo yafuatayo:-
(i) Kuainisha idadi ya wazee nchini watakaohusishwa katika mpango wa pensheni kwa wazee nchi nzima;
(ii) Kuainisha viwango vya pensheni; na
(iii) Kuandaa utaratibu utakaotumika kulipa pensheni pamoja na taratibu za kiutawala na kupokea maoni ya wadau kuhusu mpango wa pensheni kwa wazee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha wa 2015/2016 Serikali ilitenga kiasi cha shilingi milioni 130 kwa ajili ya maandalizi ya mpango huo.
MHE. JOHN W. HECHE aliuliza:-
Mgodi wa North Mara (Acacia Gold Mine) umeanza uchimbaji wa ardhini (underground) sasa yapata mwaka mzima bila kuweka wazi kama kuna mabadiliko ya kimkataba na kitendo hiki ni hatari kwa usalama wa kijiografia kwa wakazi wanaozunguka mgodi huo:-
Je, kwa nini Serikali isizuie zoezi hili mpaka mikataba iridhiwe na Serikali za Kijiji na kuanza upya bila kuwepo makandokando?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa John Wegesa Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba uchimbaji wa madini chini ya ardhi (ungerground mining) katika mgodi wa North Mara (Acacia Gold Mine) ulianza mwaka 2015 katika eneo la Gokona baada ya Tathmini ya Kimazingira kufanyika na kibali kutolewa tarehe 23 Aprili, 2015. Aidha, mgodi haukuwahi kuwa na mkataba wa uchimbaji baina yake na vijijii vinavyozunguka eneo hilo. Kifungu cha 48(1)(a) cha Sheria ya Madini ya mwaka 2010 kinamtaka mmiliki wa leseni ya uchimbaji mkubwa (Special Mining Licence) kubadili njia ya uchimbaji madini (mining method) pale inapohitajika kufanya hivyo hasa kwa lengo la kufanya uchimbaji kuwa endelevu kulingana na uwepo wa mashapo na jiografia yake. Mabadiliko hayo ya uchimbaji yalihusisha pia kufanya Tathmini ya Mazingira (Environmental Impact Assessment) zinazoweza kujitokeza wakati wa kutekeleza mabadiliko ya uchimbaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, mgodi wa North Mara una mikataba na vijiji saba vinavyozunguka mgodi inayohusu namna ya kunufaika na uwepo wa shughuli za uchimbaji kwenye mgodi huo. Vijiji hivyo ni Kerende, Kewanja, Matongo, Ngenkuru, Nyakunguru, Nyamwanga na Nyangoto. Mikataba hiyo haihusiani kabisa na namna mgodi unavyowajibika katika kutekeleza sheria wakati wa uendeshaji wa shughuli za uchimbaji. Hivyo, mgodi haulazimiki kuomba ridhaa ya Serikali ya Vijiji husika wakati wa kubadili aina ya uchimbaji yaani kutoka mgodi wa wazi kwenda mgodi wa chini ya ardhi. Hata hivyo, pamoja na mgodi kubadilisha aina ya uchimbaji, mikataba yote iliyopo kati ya vijiji hivyo pamoja na wadau wengine itaendelea kuwepo kwa mujibu wa mikataba yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kusimamia uchimbaji huo kwa mujibu wa sheria husika na kuchukua tahadhari ili kuhakikisha kwamba uchimbaji wa madini chini ya ardhi katika mgodi huo hauhatarishi usalama wa wananchi wanaozunguka mgodi huo.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE (K.n.y. MHE. JOHN W. HECHE) aliuliza:-
Barabara ya Tarime - Nyamwaga - Serengeti inapita kwenye Mgodi wa Nyamongo na pia ndiyo tegemeo kuu la uchumi wa Wilaya ya Serengeti na Tarime kwa kutoa mazao kwa wakulima na kuyasafirisha hadi sokoni Musoma Mjini:-
Je, ni lini barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa John Wegessa Heche, Mbunge wa TarimeVijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Tarime – Nyamwaga – Mugumu - Serengeti ni barabara ya Mkoa yenye urefu wa kilometa 85 na ni kiungo muhimu sana kiuchumi na kijamii kwa Wilaya za Tarime na Serengeti. Barabara hiyo pia ni kiungo muhimu kwa watalii wanaotokea nchi ya Kenya kupitia Sirari kuelekea katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia umuhimu wa barabara hiyo, Serikali imeanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami kwa awamu kutoka Tarime kuelekea Mugumu Serengeti. Hadi sasa jumla ya kilometa sita za barabara hiyo zimekamilika kwa kiwango cha lami katika eneo la Mji wa Tarime. Pia ujenzi wa kilometa mbili unaendelea na unatarajiwa kukamilika kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha 2015/2016.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2016/2017, Serikali imetenga shilingi 430 milioni kwa ajili ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara ya Tarime, Nyamwaga hadi Mugumu yakiwa ni maandalizi ya kuijenga barabara yote kwa kiwango cha lami. Aidha, katika mwaka wa fedha 2016/2017, Serikali imetenga shilingi bilioni moja kwa ajili ya ujenzi wa daraja la Mara katika barabara ya Tarime, Nyamwaga hadi Mugumu.
MHE. JOHN W. HECHE aliuliza:-
Mji wa Sirari unakua kwa kasi kubwa sana kutokana na kuwa na mapato mengi yatokanayo na ushuru wa forodha na bandari kavu. Hata hivyo Mji huo una tatizo la ujenzi holela kutokana na Halmashauri ya Wilaya ya Tarime kukosa fedha za kupanga mji na kulipa fidia stahiki kwa wananchi wanaotakiwa kuhamishwa:-
Je, Serikali itatoa lini fedha za fidia ili kazi ya ujenzi wa Mpango wa Mji huo ifanyike?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa John Wegesa Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wa Sirari ni miongoni mwa Miji midogo inayokua kwa kasi nchini Tanzania kutokana na fursa za kibiashara kati ya Tanzania na Kenya pamoja na uwepo wa bandari kavu katika eneo hilo la mpakani. Mji wa Sirari umetangazwa kuwa eneo la mpango yaani Planning Area kwa tangazo la Serikali Na. 176 la tarehe 9 Agosti, 1996.
Mheshimiwa Naibu Spika, upimaji wa makazi wa Sirari unafanyika kwa njia shirikishi ambapo wananchi wenyewe kwa kushirikiana na wataalam wataamua kuhusu upimaji wa mji huo yaani informal settlement upgrading. Hivyo, hakuna fedha zilizotengwa kulipa fidia kwa sababu hakuna wananchi watakaohamishwa katika zoezi hili ili kuboresha Mji. Wakazi wachache ambao watapisha maeneo ya umma kama barabara na huduma za jamii kwa makubaliano yao watapatiwa viwanja mbadala katika maeneo ya Lemangwe, Ng’ereng’ere na Gwitiri ambako vitapimwa viwanja 2,644.
MHE. JOHN W. HECHE aliuliza:-
Kwa mujibu wa tafiti, uchimbaji mdogo ndio unaotoa ajira kwa wingi katika sekta ya madini:-
(a) Je, ni lini Serikali itajenga maeneo maalum kwa ajili ya wachimbaji wadogo katika eneo la Nyamongo?
(b) Je, kwa kutokuwatengea vijana maeneo ya uchimbaji, Serikali haioni kuwa inazidisha chuki ya vijana dhidi ya mgodi wa Acacia North Mara?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa John Wegesa Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2015 Serikali ilitenga eneo lenye ukubwa wa hekta 598 katika eneo la Nyamongo, Kitongoji cha Kerende kuwa eneo maalum kwa ajili ya wachimbaji wadogo; kadhalika katika eneo hilo ilitoa leseni 96 za uchimbaji mdogo kwa wananchi katika mwaka 2014, kadhalika Serikali ilitenga eneo la ukubwa wa hekta 49.18 katika Kijiji cha Nyakunguru linaloweza kutoa leseni tano za uchimbaji ambapo hivi sasa leseni nne zimeshatolewa kwa Kampuni ya Itandura Miners Cooperation Limited ambayo ipo katika eneo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo mengine ambayo yametengewa eneo ni pamoja na eneo la Gorong‟a ambayo ilitenga eneo la hekta 82.52 lenye leseni nane za uchimbaji mdogo ambapo leseni tatu kati ya hizo zimetolewa kwa wananchi wa eneo hilo. Katika eneo la Msege, Serikali pia ilitenga leseni tisa za uchimbaji mdogo kwa wananchi wa eneo hilo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa wananchi wanapokosa maeneo ya uchimbaji wanaweza kuwa na chuki na wawekezaji wakubwa. Kwa kutambua hilo basi, Serikali imeendelea kuitekeleza azma hii ya kuwatengea maeneo wananchi ili wananchi wapate mahali pa kufanyia kazi na kuondoa chuki kati yao na wawekezaji wakubwa.
MHE. MWITA M. WAITARA (K.n.y MHE. JOHN W. HECHE) aliuliza:-
Mazingira ya ufundishaji kwa Walimu walio wengi nchini ikiwemo Wilaya ya Tarime yamekuwa siyo rafiki, ambapo Walimu wamekuwa wakibebeshwa mzigo wa gharama za vifaa vya kufundishia kama maandalio ya somo, chaki na kadhalika:-
Je, matumizi haya yatarekebishwaje katika mfumo huu wa elimu bure ulioanzishwa na Serikali ya Awamu ya Tano.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwanza naomba kwa ruhusa yako, nimpe pole Mheshimiwa John Heche na wote ambao wamefiwa, Serikali ipo pamoja nao katika misiba hiyo.
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa John Wegesa Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini, ambapo marekebisho yake madogo naomba yaingie katika Hansard kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kupitia Waraka wa Elimu Na.5 wa mwaka 2015, uliotoa mwongozo wa Serikali kuhusu Elimu Msingi bila malipo, majukumu ya Serikali, jamii, wazazi, walezi, wakuu wa shule, Kamati au Bodi za shule, yamefafanuliwa vizuri sana kwenye Waraka huo. Miongoni mwa majukumu ya Serikali ni kutoa ruzuku ya uendeshaji wa shule, inayogharamia chakula kwa wanafunzi wa bweni, ununuzi wa vitabu vya kiada na ziada, vitambulisho, mitihani endelezi, mitihani ya Taifa, shughuli za michezo, maandalio ya somo, chaki na vifaa vingine. Hivyo siyo sahihi kwa Walimu kutumia fedha zao kugharamia maandalio ya somo na vifaa kama chaki.
Mheshimiwa Spika, nawaagiza Wakurugenzi wote wa Halmashauri, Maafisa Elimu wote wa ngazi zote na Walimu Wakuu kusimamia vizuri Mpango wa Utoaji Elimu Msingi bila malipo kama ulivyofafanuliwa katika waraka nilioutaja, kuanzia sasa Walimu wasikubali kubebeshwa mizigo ya gharama isiyowahusu.
MHE. JOHN J. MNYIKA (K.n.y. MHE. JOHN W. HECHE) aliuliza:-
Wilaya ya Tarime ni miongoni mwa Wilaya zinazoongoza kwa wakazi wake kuwa na kesi za kubambikiwa hasa za wizi wa kutumia silaha na mauaji, kitendo kinachokuwa na sura ya kumpa mtuhumiwa wakati mgumu sana kupata msaada wa kisheria.
Je, ni kwa nini Serikali isisaidie upatikanaji wa msaada wa kisheria kwa mahabusu hao ambao kitakwimu ni wengi katika Gereza la Tarime kuliko mashauri mengine yoyote?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. ATHONY P. MAVUNDE K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria napenda kujibu swali la Mheshimiwa John Wegesa Heche, Mbunge wa Tarime Vijijii kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa utoaji wa msaada wa kisheria kwa watu walioko vizuizini. Kwa kutambua hilo, Sheria ya Msaada wa Kisheria ya mwaka 2017 imetamka wazi kuwa Jeshi la Polisi na Magereza yanapaswa kuweka mazingira ya kuwezesha upatikanaji wa msaada wa kisheria kwa watu walioko vizuizini. Vile vile, kanuni za Sheria hiyo (GN.No. 92018) zimeweka utaratibu wa kufuatwa na Wakuu wa Vituo vya Polisi katika kufanikisha suala hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufanikisha upatikanaji wa huduma hii, Wizara imefanya vikao vya mashauriano na Wizara ya Mambo ya Ndani kwa nyakati tofauti tangu mwaka 2017 kwa lengo la kuweka utaratibu mzuri wa kutekeleza matakwa ya sheria. Hadi kufikia leo tayari rasimu ya mwongozo wa kutoa huduma katika Vituo vya Polisi na Magereza umeandaliwa na utawasilishwa kwa wadau. Pia hivi karibuni Wizara ya Katiba na Sheria itasaini hati ya makubaliano na Wizara ya Mambo ya Ndani kwa ajili ya kushirikiana katika eneo hili. Jitihada hizi za Serikali zinalenga kuondoa changamoto ya upatikanaji wa msaada wa kisheria katika magereza yote nchini pamoja na gereza la Tarime.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua fursa hii kumwomba Mheshimiwa Mbunge avute subira, pindi Mwongozo huu utakapokamilika yamkini Wilaya ya Tarime inaweza kuwa miongoni mwa wilaya ambazo zitanufaika na huduma hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Magereza kwa upande wake yamekuwa na utaratibu wa kutoa huduma ya msaada wa kisheria kwa muda mrefu sasa kwa makubaliano yaliyofanyika kati yao na Shirika la Envirocare ambalo lilikuwa likitoa msaada wa kisheria kwa mahabusu na wafungwa katika baadhi ya mikoa hapa nchini.
MHE. JOHN W. HECHE aliuliza:-

Hospitali ya Wilaya ya Tarime imeelemewa na Wagonjwa kwa sababu inapokea Wagonjwa wengi kutoka Wilaya ya Tarime na Rorya, pamoja na uchache wa Vituo vya Afya, Zahanati na Vifaa katika maeneo mengi ya Wilaya hizo.

Je, ni kwa nini Serikali isipandishe hadhi Hospitali hiyo na kuwa Hospitali ya Mkoa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa John Wegesa Heche Mbunge wa Tarime Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi 367,985 wa Halmashauri ya Wilaya ya Tarime wanapata huduma za afya katika Hospitali ya Wilaya ya Tarime iliyoko Tarime Mjini pamoja na Vituo vya Afya vinane ambavyo vitano vinamilikiwa na Serikali na vitatu vinamilikiwa na Watu Binafsi na Zahanati 23 za Serikali zikiwa 16 na 7 Watu binafsi. Vilevile, Hospitali hiyo inahudumia wilaya za jirani ambazo ni Rorya, Musoma na Bunda na wagonjwa kutoka nchi jirani ya Kenya na kusababisha msongamano wa wagonjwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haina mpango wa kupandisha hadhi Hospitali ya Wilaya ya Tarime kuwa Hospitali ya Mkoa kwa kuwa Mkoa wa Mara una Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mara iliyoko Musoma Mjini. Ili kutatua changamoto ya utoaji wa huduma za Afya katika Mkoa wa Mara, Serikali katika Mwaka wa Fedha 2018/2019 imetenga kiasi cha shilingi bilioni 4.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali tatu za halmashauri katika Halmashauri za Wilaya ya Bunda, Rorya na Musoma.

Tayari fedha zote zimepelekwa kwenye Halmashauri husika kwa ajili ya kuanza ujenzi. Vilevile, Serikali inaendelea na Ukarabati na ujenzi wa Vituo sita vya Afya katika Mkoa wa Mara vinavyogharimu jumla ya shilingi bilioni 2.4. Ujenzi wa Hospitali tatu za halmashauri na Vituo sita vya Afya utaimarisha huduma katika ngazi ya msingi na kupunguza msongamano wa Wagonjwa katika Hospitali ya Wilaya ya Tarime.