Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Victor Kilasile Mwambalaswa (25 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili nami nichangie hoja iliyo mbele yetu.
Kwanza, napenda kutumia fursa hii kuwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Lupa waliokichagua chama changu kwa kura nyingi sana, kuanzia Rais, Mbunge na Madiwani, kura nyingi sana nawashukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema na kama alivyosema Mheshimiwa Rais, hatutawaangusha. Uchaguzi umekwisha, sasa iliyobaki ni kufanya kazi, ni kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, ni kutekeleza ahadi ambazo wagombea tuliahidi kwenye
majukwaa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Jimboni kwangu kuna genge limeibuka linaeneza uongo kwamba barabara ya lami kutoka Chunya kwenda Makongolosi aliyoahidi Mheshimiwa Rais haitajengwa! Eti haitajengwa kwa sababu kuna watu wamekula hela na hao watu wamekimbilia nje ya nchi!
Mheshimiwa Naibu Spika, wale ni waongo, ni watu ambao kwenye uchaguzi walishiriki na walikuwa wanatamba kwamba wangeshinda kwa kishindo! Wameshindwa kwa kishindo! Wanashindwa pa kutokea, wanaeneza uongo! Hilo wananchi wa Lupa ni jipu, mtajua namna
ya kulitumbua wakati ukifika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikiangalia Hotuba ya Mheshimiwa Rais nalinganisha sana na maneno, yaani nikiangalia hotuba yake na matendo yake, nalinganisha sana na maneno na matendo ya Yohana Mbatizaji zaidi ya miaka 2000 iliyopita. Kwa ruhusa yako, naomba nisome
paragraph moja aliyosema Yohana Mbatizaji kwenye Injili ya Luka 3:7-14. Siyo maneno yangu haya, maneno ya Yohana Mbatizaji:
“Basi aliwaambia makutano ya wale waliomwendea ili awabatize. Enyi wazao wa nyoka, ni nani aliyewaonya ninyi kuikimbia hasira itakayokuja? Basi toeni matunda yapatanayo na toba, wala msianze kusema mioyoni mwenu tunaye baba, ndiye Ibrahimu, kwa maana nawaambia kwamba katika mawe haya Mungu aweza kumuinulia Ibrahimu watoto. Na sasa hivi shoka limekwisha kuwekwa penye mashina ya miti na kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa na kutupwa motoni.
Makutano wakamuuliza, tufanye nini basi? Akawajibu akiwaambia, mwenye kanzu mbili na ampe asiye na kanzu na mwenye vyakula na afanye vivyo hivyo. Watoza ushuru nao wakaja kubatizwa wakamuuliza, Mwalimu tufanye nini na sisi? Akawaambia, msitoze zaidi kitu zaidi
kuliko mlivyoamriwa. Askari nao wakamuuliza wakisema, na sisi tufanye nini? Akawaambia, msidhulumu mtu wala msishtaki kwa uongo tena mtoshewe na mishahara yenu.”
Mheshimiwa Naibu Spika, haya maneno ni ya miaka 2000 iliyopita! Ni maneno ambayo yako kwenye Hotuba ya Mheshimiwa Rais Magufuli, yanafanana; anawaambia Watendaji wa Serikali, Mawaziri, Makatibu Wakuu, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi, wote timizeni wajibu wenu, vinginevyo shoka liko shinani. Mti usiozaa matunda utakatwa! (Makofi)
Sasa msianze kulalamika, aah mimi, hapana! Timizeni wajibu wenu. Yohana Mbatizaji alikuwa anawaambia hawa, ili warithi Ufalme wa Mbingu. Mheshimiwa Rais Magufuli anawaambia Watendaji wa Serikali ili tuondoe umasikini kwa Watanzania, ili tulete maendeleo kwa Watanzania. Kwa hiyo, timizeni wajibu wenu, vinginevyo shoka liko shinani, mti usiozaa utakatwa na kutupwa motoni. Ninaomba hotuba hii hasa pale kwenye vipaumbele ambavyo ameweka Rais, Serikali mhakikishe Wakuu wa Mikoa wanayo, Wakuu wa Wilaya wanayo, Watendaji wanayo waangalie Rais ameweka vipaumbele gani kwenye hotuba yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hotuba hii anasema wakulima na wavuvi, hasa wakulima, wataletewa pembejeo kwa wakati, watawekewa huduma za ugani, watatafutiwa masoko panaposumbua! Jimboni kwangu mwaka uliokwisha wakulima wa tumbaku wamesumbuka sana, soko la tumbaku halipo. Naomba sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo hili ni jipu lako la kwanza, uhakikishe wakulima wa tumbaku wa Jimbo la Lupa na hasa nchi nzima, watafutiwe soko la zao lao kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, iko nchi ya Zimbabwe ambayo yenyewe imeingia ubia na Jamhuri ya Watu wa China kwamba tumbaku yote ya Zimbabwe inanunuliwa na China. Unajua Wachina wako wengi sana, wako watu 1.6 billion kwa hiyo, chakula kinahitajika kingi, vinywaji
vingi, hata tumbaku ya kuvuta inahitajika nyingi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, naomba jipu hili ulishike vizuri ili wakulima wa tumbaku wa Jimbo la Lupa na nchi nzima mwaka huu wapate soko la uhakika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Hotuba hii ya Mheshimiwa Rais aliongea kwamba anataka kuleta Muswada Bungeni kubadilisha vipengele fulani vya Sheria ya Manunuzi, ili iharakishe, ilete unafuu wa kuleta huduma kwa Watanzania. Nawaambia wadau wote, nimeongelea Sheria ya Manunuzi miaka 10 Bungeni hapa kwamba jamani eeh, bajeti yetu inatakiwa ni trilioni 20! Ujue kwamba 70% ya hela hizo inaenda kwenye manunuzi! Sasa mkiona Rais mwenyewe wa nchi ameshtuka anasema tuongelee manunuzi, muichukulie very positively watendaji wote, ili mlete mapendekezo mazuri ya kuirekebisha sheria hiyo, ili iweze kuharakisha kupeleka huduma kwa Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, pale ambapo muda wa tender ni siku 60, kwa nini, inachelewesha kupeleka huduma kwa Watanzania. Pale ambapo tender sum ya kujenga barabara kutoka hapa kwenda Iringa ni shilingi milioni 200, lakini variations zinazotolewa hapo inafika milioni 600, ni vitu vya kuviangalia hivyo. Pale ambapo Mtendaji au Accounting Officer kwenye Wizara, kwenye Idara, anasema ikifika shilingi milioni 50 lazima akapate kibali kwa Accountant General! Hilo ni la kuliangalia, ili hiyo nayo threshold iongezwe kutoka milioni 50 iende 500 au bilioni moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia, sera ya magari; nimesema sana Serikali iwe na sera ya magari. Kuwe na sera ya magari siyo kwamba huyu ananunua hili, huyu ananunua hili, hapana, kuwe na sera ya magari kabisa. Kenya, Rwanda, Zambia na Malawi wana sera ya magari!
Kwingine kote kuwe na Sera ya Magari! Hiyo Sera mkiiandika vizuri na mkaitia kwenye Sheria, kuna kitu Watendaji wa Serikali wanafanya sana hapa, una-acquire property ya Serikali by tender, lakini sasa katika kui-dispose sheria inasema u-dispose by tender! Magari wanajiuzia!
Hiyo naomba isimamishwe kwenye mapendekezo ambayo yataletwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, mwaka jana Serikali yetu nzuri ilitangaza kupitia kwa Rais na kwa Waziri Mkuu kwamba Mkoa wa Mbeya utagawiwa kuwe na Mkoa wa Songwe na wa Mbeya na kwamba Wilaya ya Chunya itagawiwa kuwe na Wilaya mbili; Wilaya ya Songwe na ya Chunya. Namwomba sasa Mheshimiwa Simbachawene atekeleze ahadi hiyo haraka, ili kila Wilaya katika hizo Wilaya mbili itengeneze Halmashauri yake ili kuharakisha kuwapelekea huduma wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, kuna kitu kinanisumbua sana, kinanisumbua kweli, consistency! Nimeshindwa namna ya kusema Kiswahili, consistency! Wakati wa mjadala wa kusema Jamhuri yetu ya Tanzania tuwe na Serikali ngapi, mbili, tatu! Wanasema aah, hapana,
Zanzibari bwana wakae mbali kule, wakae mbali! Hapana, hapana, kuwe na Serikali yao huko! Sawa bwana! Wakati wa uchaguzi, wanasema aah, wale ndugu zetu bwana, lazima tuwasaidie wale, consistency! Nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii kuniwezesha na mimi kuweza kutoa mchango wangu kwenye hoja iliyo mbele yetu. Naomba nichukue nafasi hii vilevile kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya Wizara hii, kwa mawasilisho yake mazuri sana aliyoyafanya kwenye hotuba yake. (Makofi)

Vilevile kuwasilisha hotuba nzuri ina maana hotuba hii ilitayarishwa na timu ya wataalam wenye weredi mkubwa sana, napenda nichukue nafasi hii, kumpongeza Naibu Waziri, Makatibu Wakuu na wataalam wote kwenye Wizara hii kubwa ambao wamewezesha kutengeneza hotuba nzuri kama hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile napenda kuipongeza na kuishukuru Serikali hii ya awamu ya tano ambayo kwa makusudi mazima imeamua kuwekeza karibuni asilimia 40 ya bajeti yetu kwenye miundombinu. Ukiwekeza kwenye miundombinu sawasawa na kuweka akiba kwa ajili ya vizazi vijavyo, kwa sababu miundombinu inachochea maendeleo na uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo naomba nije kwenye barabara yangu ya Mbeya - Chunya - Makongorosi. Napenda nimfahamishe Mheshimiwa Waziri kwa sababu yeye anaifahamu sana hii barabara. Kwanza ninamsifu sana ametoka Mbeya mpaka Itigi anaikagua barabara. Hii barabara zamani ndiyo ilikuwa njia ya The Great North Road inayotoka Cape kwenda Cairo, ilipita Chunya, Itigi ikaja Manyoni kwenda Arusha - Nairobi mpaka Cairo. Serikali kwenye miaka ya 1960, 1961, 1962 ndio waliibadilisha route hiyo ya Great North Road kwa kutumia GN kwa kuifanya itoke Mbeya - Iringa - Dodoma - Babati kwenda Cairo, lakini originaly ilikuwa ni hiyo ya Chunya, Itigi, ndiyo hii The Great North Road kwa hiyo Mheshimiwa Waziri nakusifu sana umeikagua unaifahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali imejenga barabara hii kwa kiwango cha lami kutoka Mbeya mpaka Chunya, kilometa 72 tunawashukuru sana wananchi wa Chunya, mmetupunguzia sana matatizo. Sasa hivi kutoka Mbeya kwenda Chunya ni shilingi 3,500 au 4,000 ambapo ilikuwa shilingi 10,000 au shilingi 12,000 sasa hivi mazao tunayolima Chunya yanafika haraka kwenye masoko, kwa hiyo mimi napenda kuishukuru sana Serikali kwa jambo hili kubwa ambalo wamelifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mwaka huu Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 22 barabara hii kujengwa kwa lami kutoka Chunya kwenda Makongorosi hadi Mkola kilometa kama 42. Kwenye kitabu chake nimeiona na ninajua kwa sababu niko karibu sana na Mheshimiwa Waziri na Naibu wake, tender imetangazwa sasa hivi wako kwenye evaluation, najua ujenzi utaanza siku za karibuni, ninawawashukuru sana. Naomba barabara hii ambayo ni ya muhimu sana tuiendeleze mpaka ifike huko inakohitajika kufika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona vilevile kwenye kitabu kwamba, barabara hii hii kwa mwaka huu inaanza kujengwa kutoka Mkiwa kwenda Itigi ili mwaka ujao itoke Itigi kuja tukutane katikati na Mheshimiwa Massare, kwa hiyo naishukuru sana Serikali kwa niaba ya wananchi wa Chunya.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile niongelee barabara ndogo ambayo inatoka kijiji cha Kiwanja inakwenda kwenye kijiji cha Mjele kwenye Mkoa mpya wa Songwe, Wilaya mpya ya Songwe Barabara hii inashughulikiwa na Halmashauri ya Chunya, lakini kwa kuwa sasa hivi Mkoa wa Songwe ni Mkoa mpya na Chunya iko Mkoa wa Mbeya kwa hiyo hii barabara inaunganisha mikoa miwili, inaunganisha Mkoa wa Mbeya na Mkoa wa Songwe. Kwa hiyo, naomba Serikali na Wizara muichukue barabara hii iweze kushughulikiwa na TANROADS badala ya kushughulikiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Chunya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudi kidogo kwenye hii hii barabara ya Mbeya - Chunya - Makongorosi. Barabara hii ina matatizo makubwa mawili, naleta kilio kwako Mheshimiwa Waziri. Tatizo la kwanza barabara hii baada ya kujengwa kilometa 72 ukipita sasa hivi kama ulivyoona ulivyopita kumeanza kuonekana matobo mawili, matatu, manne; kwa barabara ambayo haijamaliza hata miaka mitano siyo vizuri, haina afya hii. Kwa hiyo, naomba sasa hivi mnavyofanya evaluation kwa kuiendeleza barabara hii kutoka Chunya kwenda Makongorosi na Mkola, kandarasi ambaye alijenga huku nyuma ambaye hata miaka mitano haijapita mashimo yanaonekana asipewe kazi tena. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili hili labda tungechukua mfano wa barabara ambayo inajengwa na Serikali kutoka Ruaha ambayo sasa hivi imefika mpaka Mafinga imekwenda Igawa, barabara imejengwa kwa kiwango cha juu sana. Labda wakandarasi wengine wa barabara hapa nchini wangekwenda kujifunza kwa mkandarasi huyu anayejenga barabara kutoka Ruaha kwenda mpaka Igawa kwenda mpaka Tunduma. Kwa hiyo hilo ni tatizo la kwanza, kwamba kumeanza kujitokeza mashimo madogo madogo, kwa hiyo naomba Mheshimiwa Waziri na viongozi wako mlielewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo la pili, Chunya tunalima tumbaku, sasa wasafirishaji wa tumbaku wanaobeba tumbaku kutoka Chunya kuleta Morogoro kutoka Chunya kuja Mbeya wanapakia malori ya rumbesa kwa sababu wanajua kwamba kule sijui hakuna mizani; wanapakia malori ya rumbesa ili akifika Mbeya ndipo anagawa hilo lori yanakuwa malori mawili. Sasa hiyo rumbesa inaiumiza sana barabara ya lami ambayo mmetujengea inaumizwa vibaya sana. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri nipewe hata weighbridge moja au mbili hata mobile weighbridges ili tuweze kuilinda hii barabara, nakuomba sana Mheshimiwa Waziri katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niongee kidogo kuhusu uwanja wa Songwe. Naishukuru Serikali kwa awamu zilizopita na awamu hii, mmejenga uwanja wa ndege wa Songwe ambao unainua sana uchumi wa Mikoa ya nyanda za juu Kusini; Mikoa ya Iringa, Mbeya, Ruvuma, Katavi, Rukwa, majirani wa Zambia wa Congo tunatumia uwanja wa Songwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tumeona hapa karibuni wakati wa masika huu, ndege zinatoka Dar es Salaam kufika Songwe kama kuna ukungu zinashindwa kutua, kwa hiyo naomba katika hii bajeti tunayoimalizia mwaka huu, Serikali iweke taa kwenye uwanja huo ili madhumuni ya Serikali ambayo ilikuwa imepanga kwa ajili ya uwanja huu yaweze kutimia. Vilevile naomba Serikali imalizie jengo la abiria kwenye uwanja wa Songwe, naomba tafadhali sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niongelee reli ya TAZARA, reli ya Uhuru ambayo walijenga Waasisi wa Taifa hili. Serikali inafanya jambo jema sana kuwekeza kwenye miundombinu, kutengeneza bandari, kujenga reli ya kati kwa standard gauge, bandari za Mtwara, Dar es Salaam, Tanga Serikali inawekeza ili iweze kuvuna kwenye uchumi wa jiografia wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hatuwezi kukamilisha jambo hili kama tutaelekeza tu kwenye reli ya kati na bandari zile basi bila kuingalia reli ya uhuru. Reli ya uhuru yenyewe haihitaji kujengwa, reli ya uhuru inahitaji kukarabatiwa kidogo ifanye kazi, nadhani ni sheria ambazo zimeiweka reli ya uhuru. Naomba Serikali ishirikiane na Serikali ya Zambia tuangalie sheria hizo ni sheria gani ambazo zinaikwamisha reli hii bila sababu, ili bandari zikikamilika, reli ya kati ikikamilika na reli ya uhuru ikikamilika nchi iweze kuvuna kutumia uchumi wa jiografia ambao Mungu ametuwezesha.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwenye reli ya kati zimeanza block trains ambazo zinabeba mizigo inayokwenda Isaka au inayokwenda Burundi au Rwanda na reli ya TAZARA nayo ingeweza kufanya hivyo, tungeweza kufanya bandari kavu ikawa Mbeya au Makambako au Tunduma tukawa tunatoa block trains kwenda Dar es Salaam, Tunduma, Mbeya au Makambako. Naomba sana, tunapotaka kuboresha miundombinu ya kutumia uchumi wa Jiografia wa nchi hii basi tuiangalie na reli ya TAZARA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kwa barabara ya mchepuko (bypass), Mheshimiwa Mwanjelwa aliiongelea jana; ya kutoka Uyole kwenda Mbalizi. Sasa hivi congestion ni kubwa mno kutoka Uyole kwenda Mbeya Mjini na kuelekea Mbalizi. Barabara ni ndogo, ni ya siku nyingi, biashara ni kubwa mno, fursa ziko nyingi sana za biashara kwenye Mkoa wa Mbeya. Kwa hiyo, hii hadithi ya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina kila mwaka, naomba barabara hii ya bypass iweze kujengwa ili tuweze kuuokoa Mkoa wa Mbeya kwa uchumi ambao unaweza kudidimia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuru sana kwa kunipa nafasi hii, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana Serikali kwanza kwa kubuni mradi huu wa shilingi milioni hamsini kwa kila kijiji lakini pia kwa kutambua kuwa pesa hizi pekee hazitoshi na kuongeza fedha za ushauri na usimamizi. Hili jambo jema sana. Kila Wilaya kuwe na desk la consultancy na kuwe na wataalam wa kilimo, biashara, utafiti na kadhalika. Nashauri fedha nyingi katika hii shilingi milioni hamsini ikopeshwe vikundi vya kilimo. Washauriwe vizuri, walime vizuri, kitaalam na baadaye vikundi hivi visindike mazao hayo na kutafutiwa masoko. Tanzania ya viwanda itakuwa rahisi sana kama mapinduzi ya kilimo yatatangulia kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Wizara ilete mageuzi sana kwenye masoko ya wakulima. Wakulima katika maeneo mengi wanauza mazao kwa walanguzi kwa bei ya chini sana. Vyama vya Ushirika viimarishwe, masoko ya uhakika yatafutwe. Utaratibu wa stakabadhi ghalani uenee maeneo yote Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Lupa, Maafisa Ushirika wa Wilaya na Mkoa wanakwamisha juhudi za wananchi kuanzisha Vyama vya Ushirika. Nina mfano wa Vijiji vya Lola na Lyesero, hawa wanakataliwa kuanzisha AMCOS kwa sababu ambazo hazina mashiko.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Wizara itafute wanunuzi wa tumbaku wengine toka China waliopo wameanza maringo na ukiritimba.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia kwenye hoja iliyo mezani kwetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kuchangia nataka nitoe ushauri wa bure kwa Mheshimiwa Waziri. Pamoja na juhudi kubwa za kuweza kutatua maji katika jiji la Dar es Salaam kwa kuongeza uzalishaji kwenye Mto Ruvu na kuchimba Bwawa la Kidunda. Kimbiji ilikuwa ndiyo lango la Mto Rufiji kuingia baharini, pale Kimbiji chini kuna maji takribani cubic kilometre moja ambayo wakazi wa Dar es Salaam pamoja na kukua kwake wanaweza wakatumia kwa zaidi ya miaka 50. Kwa hiyo, namshauri Mheshimiwa Waziri kwamba anapotafuta vyanzo vingine vya kupeleka maji Dar es Salaam na Kimbiji aifikirie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu alivyoibariki Mwenyezi Mungu pamoja na madini na kila kitu alichotupa ametupa vyanzo vingi vya maji, ukiacha bahari inayoanzia Tanga, Pemba, Zanzibar mpaka Mtwara; mito mingi, maziwa mengi. Lakini pamoja na mito yote tuliyonayo ukiangalia idadi ya watu waliokuwepo wakati wa uhuru na tuliopo sasa hivi tumeongezeka sana, wanyama wameongezeka sana, kilimo kimeongezeka sana, mito inapungua kwa sababu ya mabadiliko ya tabianchi. Ukiuangalia Mto Ruaha ulivyokuwa miaka ya 2006 - 2007 ukaungalia na leo inasikitisha, maji yanakauka ina maana mito yetu yote inakauka. Nashauri hizi Mamlaka za Mabonde ya Mito zote ambazo zimeunda naomba zipewe uwezo zaidi wa kusimamia vyanzo na kuboresha vyanzo vya mito hii vinginevyo vitakauka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa Mbunge miaka mingi sijawahi kuona mara moja ambapo mawazo ya Serikali, mawazo ya Kamati, mawazo ya Kambi ya Upinzani yanafanana, lakini safari hii naomba ninukuu kwa ruhusa yako. Mheshimiwa Waziri kwenye kitabu chake ukurasa wa 8 anasema kuhusu maji vijijini, Waziri anasema; “miradi ya maji vijijini inatekelezwa chini ya Programu Ndogo ya Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini kwa kuzingatia mpango wa Tekeleza kwa Matokeo Makubwa (BRN), idadi ya watu wanaopata huduma ya maji vijijini imeongezeka kutoka milioni 15 sawa na asilimia 40 ya wananchi waishio vijijini mwezi Julai, 2013 hadi kufikia watu milioni 21.9 sawa na asilimia 72.” Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu anasema; “aidha, Mfuko wa Taifa wa Maji umeonyesha mafanikio makubwa katika kuwezesha upatikanaji wa fedha za kugharamia miradi ya maji vijijini, ambapo kiasi cha shilingi milioni 90 zilizotengwa zimeonyesha kutokidhi mahitaji ya miradi ya maji yaliyopo.” (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani anasema; “uanzishaji wa Wakala wa Maji Vijijini, katika Bunge la Kumi yalitolewa maoni kadhaa ndani ya Bunge lako Tukufu kuhusu uanzishwaji wa Wakala wa Maji Vijijini (Rural Water Agency) ikiwa ni lengo la kuongeza utoaji na usimamiaji wa huduma ya maji kwa wananchi katika maeneo ya vijijini.” Wote watatu wamekubaliana kwa hoja hii moja, ina maana Bunge lako lote linasimamia kwamba tuanzishe Wakala wa Maji Vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona Wakala wa Barabara ilivyofanikiwa kutengeneza mtandao wa barabara nchini, tumeona mafanikio ya Wakala wa Umeme Vijijini sasa umefika wakati wa kuanzisha Wakala wa Maji Vijijini. Kwa hiyo, namuomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja kwenye majumuisho aoneshe dhamira na nia yake kwamba katika Muswada wa Fedha wa Bajeti hii tunayoizungumzia apeleke mapendekezo ya kuanzishwa kwa Wakala wa Maji Vijijini ili vyanzo vya fedha vijulikane na viwekewe uzio ili Wizara ya Fedha isiweze kuvichezea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kwetu Chunya. Katika kitabu chako hiki Mheshimiwa Waziri kuhusu orodha ya Halmashauri zilizotengewa fedha za maendeleo kutekeleza maji vijijini kwa mwaka 2016/2017 sina matatizo, nimeiona Wilaya ya Chunya ipo kuhusu fedha zinazotoka nje kwa ajili ya maendeleo ya maji vijijini na mijini sina matatizo, tatizo langu ni mgawanyo wa fedha ukurasa wa 153 zilizotengwa kwa ajili ya kuboresha huduma ya maji (Quick wins katika Miji Mikuu ya Wilaya na Miji Midogo kwa mwaka 2016/2017. Nikiangalia pale naona Mbeya kuna Kyela- Mbeya, Mbarali - Mbeya, Tukuyu - Mbeya, Kasumulu - Mbeya – Mbozi, sijaona Chunya, najua ni makosa ya uandishi, kwa hiyo nakuomba Mheshimiwa Waziri utakapokuja kuleta majumuisho yako hapa na Wilaya ya Chunya uiweke kwenye hizo Quick wins.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu Mji wa Chunya ni katika miji mikongwe nchini au wilaya kongwe, nitaichukua Bagamoyo, Ujiji na Chunya. Visima vya maji ambavyo viko Chunya pale vilianzishwa mwaka 1938 wakati huo wananchi pale Chunya walikuwa 2000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi pale Chunya wananchi wanaelekea kuwa 20,000. Tunachimba kisima hiki, hakitoshi, tunachimba kisima kingine hakikidhi. Hata Mheshimiwa Rais alipokuja kuomba kura Chunya alikuta shida kubwa ya pale Mjini Chunya ni maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, fedha za quick wins zije ili tuweze kutatua matatizo ya maji Chunya Mjini na kwenye mji mdogo wa Makongorosi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niishukuru sana Serikali kwa kujenga bwawa la maji la Matwiga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wa tumbaku wanapitia kipindi kigumu sana kuhusu masoko na bei ya zao hili. Najua kuwa Serikali inafanya kila njia kuwasaidia wakulima katika hili. Pamoja na hayo wawakilishi wa wakulima wa tumbaku Kusini mwa Ikweta walikaa Lilongwe nchini Malawi na kutoa azimio la pamoja lenye maslahi ya kuwalinda wakulima. Serikali italeta azimio hilo Bungeni lini ili Bunge liweze kuridhia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali ifanye haraka kuleta azimio hilo Bungeni. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia kwenye hoja iliyo mezani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza jana tulipewa kitabu, pamoja na cha bajeti, kitabu kingine kidogo chenye taarifa ya utekelezaji wa miradi ya Mfuko wa Mawasiliano kwa wote hadi Aprili 16. Kwenye ukurasa wa 17, naomba ninukuu, kwenye Wilaya yangu ya Chunya, wanatoa taarifa ya minara iliyoweka inayofanya kazi ya mawasiliano na ambayo haifanyi kazi, kwenye Wilaya ya Chunya:
“Kata ya Kambikatoto mtoa huduma Vodacom, ruzuku dola 51,000, mnara haujawaka. Kata ya Lualaje, mtoa huduma TTCL, ruzuku dola 62,000, mnara haujawaka. Kata ya Mafyeko, Vodacom, ruzuku dola 121,000, mnara haujawaka. Kata ya Makongorosi, Vodacom, mnara haujawaka. Kata ya Matwiga, Vodacom, haujawaka”
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa napenda tu rekodi iwe wazi kwamba minara haipo, kwa hiyo wanavyosema haujawaka ina maana upo lakini haujawaka, hii minara haipo. Kwa hiyo, kama ruzuku wameshapewa wapeleke minara, kama hawajapewa ruzuku basi wapewe ambao watapeleka minara. Minara haipo!
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Awamu ya Tano imejipambanua na mambo makubwa, mazuri yanayoonekana. Jambo la kwanza, bajeti ya maendeleo, Serikali ya Awamu ya Tano wameitoa kutoka asilimia 20 kwenda asilimia 40 ya maendeleo, jambo zuri sana, imejipambanua. Pia akiongea Mheshimiwa Rais ukimtazama usoni amejipambanua sana na wanyonge, watu wa chini. Ukimwangalia anavyoongea unasema huyu kweli inamuumiza, ukiwaangalia Mawaziri wanavyoongea na wanavyofanya kazi vijijini unaona kwamba kweli hawa wanataka kumkomboa mnyonge, wanataka kumkomboa Mtanzania, lakini kwa kuanzia na mnyonge. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hawa wanyonge ambao wanatuumiza, bajeti tunayoipitisha hapa inakwenda kutatua matatizo yao, ndiyo bajeti hii ambayo Bunge linapitisha. Hakuna kitu kinaumiza au kinakera kama Bunge hapa linapitisha bajeti iende kwenye Wizara hii kiasi kadhaa, Wizara hii kiasi kadhaa, zikija Kamati kupitia bajeti mwaka unaofuata mwezi wa Tatu au wa Nne, unaambiwa Wizara hii imepewa asilimia 10, Wizara hii asilimia 17, Wizara hii asilimia 15. Sasa Serikali yetu nzuri, Serikali ya Chama cha Mapinduzi tunawapa KPI hiyo sasa, hiyo ndiyo tutawapima. Mwaka kesho tukifika mwezi wa Nne tunataka tuone bajeti ambayo tunapitisha hapa ya kuwakomboa wanyonge ikifika mwezi wa Nne imepita asilimia 80, asilimia 90. Tutawapima mwezi wa Nne mwaka kesho. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hilo, naomba niongelee barabara ya Mbeya- Chunya- Makongorosi. Mnyonge mnyongeni haki yake mpeni, kwanza napenda kuishukuru sana Serikali kwa kujenga angalau kutoka Mbeya kufika Chunya, nawashukuru sana. Barabara hii ina historia ndefu sana, hii ndiyo ilikuwa zamani ambayo Cecil Rhodes alisema ni barabara ya kutoka Cape kwenda Cairo ilipita toka Zambia- Mbeya- Chunya- Itigi- Manyoni- Babati- Arusha kwenda Cairo, ingawaje Serikali yetu baadaye ilipitisha sheria, Government Notice, kwamba itakuwa inatoka Mbeya- Iringa- Dodoma, lakini asilia ilikuwa Mbeya- Chunya- Itigi- Manyoni- Singida- Babati- Arusha, ndiyo Great North Road ilikuwa inapita hapo. Sasa naishukuru sana Serikali kwa kujenga angalau mpaka Chunya.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi nauli kutoka Chunya kwenda Mbeya, kutoka Sh. 10,000/=, 15,000/= sasa hivi ni Sh. 3,500/=. Sasa hivi mazao kutoka Chunya kwenda Mbeya yanakwenda kwa urahisi. Ndiyo uzuri wa kuweka miundombinu mizuri kwa ajili ya wananchi, nashukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye mwaka huu sasa barabara hii imepangiwa Shilingi bilioni 45.8 lakini zaidi ya asilimia 80 ya hela hizi zinalipa madeni, kwa hiyo, itakayojenga barabara kutoka Chunya kuelekea Makongorosi ni karibu bilioni tisa. Kama alivyosema Mheshimiwa Massare, jirani yangu, kipande kingine cha kutoka Mkiwa kwenda Itigi, bilioni sita. Yote katika hiyo 45 billion itakwenda kwenye kulipa madeni.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ilianza kujengwa kabla ya barabara ya Iringa- Dodoma haijaanza, kabla ya barabara ya Msata- Bagamoyo haijaanza, hii itakwisha lini! Naomba sana Mheshimiwa Waziri aongezewe fedha kwa ajili ya kumalizia barabara hii kufika Makongorosi ili iendelee kutoka Makongorosi kwenda Rungwa na mwishoni kwenda Mkiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii kwa watu wa Chunya ni lulu, ni mboni ya jicho, sana, tena sana. Sasa imejengwa juzi nimetoka Chunya mwezi wa pili nimekwenda TANROADS Mkoani kuwaambia kuna sehemu mbili zimeanza kubomoka sababu kuna malori yanabeba tumbaku, kuna malori yanabeba mbao ambayo yanaweka rumbesa, kutoka Chunya kuja Mbeya, lakini yakifika Mbeya yanagawa kwa sababu kuna weigh bridges, kwa hiyo, naiomba sana Serikali iweke mizani ya kupima hiyo mizigo ya malori ili tuweze kuilinda hiyo barabara yetu, hata mkiweka temporary au mobile weigh bridge itasaidia sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mwakibete ameongelea Uwanja wa Songwe na mimi nitaongelea Uwanja wa Songwe huo huo. Uwanja wa Songwe ulianza kujengwa miaka kumi na nne iliyopita, Uwanja wa Kigoma umeanza kujengwa miaka minne iliyopita, Uwanja wa Bukoba miaka minne iliyopita, Uwanja wa Tabora miaka minne iliyopita, Uwanja wa Mafia miaka minne iliyopita, huu wa Songwe miaka kumi na nne iliyopita. Mara tatu, mara nne ndege zinatoka Dar es Salaam kwenda Mbeya zinageuza zinashindwa kutua, hasa mwezi wa Tano, wa Sita kwa sababu ya ukungu, kwa sababu uwanja hauna taa. Kwa hiyo, naomba uwanja huu nao uishe tunahitaji sasa hivi kuweka taa za kuzielekeza ndege kutua, kuweka fensi na kumalizia jengo la abiria. Sasa mwaka huu tumetenga bilioni 10 sijui kama zitatosha. Naiomba Serikali Uwanja wa Songwe ni gateway kubwa sana kwa Mikoa ya Kusini na nchi jirani, naomba uishe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kiongozi mmoja wa nchi jirani…
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Hivi karibuni Mheshimiwa Rais alifanya ziara Mkoani Mbeya, akiwa Wilayani Chunya, aliombwa na wananchi fedha za kukarabati Hospitali ya Wilaya. Mheshimiwa Rais aliahidi shilingi 200,000,000/= kwa ukarabati huo. Naiomba Wizara ifuatilie na kutekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye hoja iliyo mbele yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii na mimi kumpongeza kwa kweli Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Makatibu Wakuu kwa bajeti hii ya mwaka huu ambayo ni nzuri sana, ni bajeti ambayo imezingatia maoni ya wadau mbalimbali. Maoni ya Waheshimiwa Wabunge, maoni ya wasomi, maoni ya watu wote wafanyabiashara na ni bajeti ambayo imeepukana na bajeti za mazoea ya kupandisha bei ya sigara, bei ya bia na bei ya soda. Ni bajeti ambayo imekwenda kihalisia, nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kitabu cha Mpango hiki hapa ambacho alisoma asubuhi Mheshimiwa Waziri, Serikali imesema inapanga kuendelea kuboresha na kukarabati shule za msingi na shule za sekondari, ni jambo jema sana hili.

Mimi nimewahi kutembelea Sekondari ya Pugu ninaiona ilivyokarabatiwa inafurahisha sana. Mwanafunzi anaposoma kwenye mazingira, kwenye miundombinu ambayo ni rafiki anasoma vizuri na anaelimika vizuri. Mimi naipongeza sana Serikali kwa jambo hili, naiomba sasa Serikali ikishakarabati shule zote za msingi na sekondari sasa ikarabati walimu, iwakarabati walimu vizuri na kuwapa motisha ili wafanye kazi vizuri kwenye miundombinu ambayo imekarabatiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili mimi naomba niiombe Serikali, Chuo cha Ualimu cha Mkwawa ilikuwa sekondari, naomba Mheshimiwa Waziri wa Elimu unisikilize; Chuo cha Elimu cha Mkwawa ilikuwa ni sekondari ilikuwa inaitwa Mkwawa High School, ilikuwa na maabara ya fisikia sita, maabara ya kemia sita, maabara ya biolojia saba. Ilikuwa mkienda Chuo Kikuu cha Dar es Salaama one third ya wanafunzi wanaosoma sayansi wametoka Mkwawa High School. Sasa kulikuwa na umuhimu wa kuwa na walimu wengi ndio maana wakaibadilisha iwe Chuo cha Ualimu. Sasa hivi tuna walimu wa ziada naomba Mkwawa High School irudishwe ya zamani ili tuweze kutengeneza wanafunzi wa sayansi pale, naiomba sana Serikali ifanye katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kati ya hilo Serikali inatoa ruzuku vizuri sana kwenye sekta ya afya inatoa madaktari, inatoa walimu, inatoa madaktari walimu na madawa. Ruzuku kwenye sekta ya afya naiomba Serikali ikimaliza huko igeukie kwenye elimu, itoe ruzuku vilevile kwenye elimu, huwezi kuwa na maendeleo bila kuelimika. Kwa hiyo naiomba Serikali itoe ruzuku kwenye vyuo au shule za watu binafsi ili tuweze kuelimisha jamii ya Watanzania vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye mpango huu hapa Serikali inasema inanedelea kuboresha na kukarabati reli ya kati na reli ya TAZARA wakati huo ikijenga standard gauge, ni jambo zuri sana. Tunatumia uchumi wetu wa jiografia vizuri, tunaitumia hali ambayo Mwenyezi Mungu alituweka vizuri. Lakini reli ya TAZARA inasuasua kwa sababu ni reli ya kati ya nchi mbili ndio maana mimi naiomba Serikali ikiwezekana sheria iliyounda reli ya TAZARA irudishwe tena hapa Bungeni tuweze ukikarabati vizuri ili kila nchi ishughulikie sehemu yake ya reli, ile reli ya TAZARA ambayo ilikuwa reli ya uhuru wakati huo sasa hivi ni reli ya biashara ili Tanzania tunufaike na reli hiyo na uchumi wa jiografia ambao Mwenyezi Mungu ametupa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais alipotembelea Malawi hivi karibuni suala kuu kati ya yeye na kiongozi mwenzie ilikuwa ni reli ya TAZARA, ilikuwa ni Malawi Cargo Centers ambazo zimekufa, ndio sasa naiomba Serikali ifuatilie sana tufufue Malawi Cargo Centers ambazo ziko Dar es Salaam na Mbeya tuifufue vizuri sana reli hii lakini vilevile tujenga bandari kavu Inyala ili mizigo ya Malawi iishie pale Iny’ara pamoja na Malawi Cargo Centers, ikitoka hapo naishauri Serikali ijenga reli kutoka hapo Inyala kwenda mpaka Itungi Port ili tupunguze mizigo ambayo inapita barabarani na kuzifanya barabara zetu ziishi muda mrefu.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikitoka kwenye reli nije kwenye barabara, Mheshimiwa Rais alipokuwa ziarani Mbeya tumshukuru sana Mheshimiwa Rais amekaa Mbeya siku tisa bila kutegemea, tunamshukuru sana ahsante sana Mheshimiwa Rais. Aliiongelea barabara ya Tanzam High Way hasa hasa kipande cha pale Mbeya ambayo kuna conjunction kubwa sana, Mheshimiwa Rais akasema Serikali itatoa fedha ya kujenga bypass ya kutoka Mlima Nyoka kwenda mpaka Songwe. Naomba katika bajeti hii Serikali ilifikirie hilo la kujenga bypass ya kutoka Mlima Nyoka kwenda mpaka Songwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba niishukuru Serikali kwa barabara ya Mbeya - Chunya ambayo sasa hivi imeisha Mheshimiwa Rais aliifungua akiwa ziarani, namshukuru sana. Lakini kwetu sisi wana Chunya barabara hii ni mboni ya jicho letu, tunataka kuilinda kwa kila hali, kwa hiyo, naomba Serikali iweke mobile bridges za kuweza kuilinda barabara hiyo na mizigo ambayo ya lumbesa ambayo inaharibu barabara. (Makofi)

Vilevile Mheshimiwa Rais alifungua aliweka jiwe barabara ya kutoka Chunya kwenda Makongorosi, naomba Serikali isimamie kwa karibu barabara hiyo ili kama ilivyo kwenye mkataba barabara hii ujenzi wake uishe mwezi Februari, 2020 ili tukienda kwenye uchaguzi tuwe na mambo ya kusemea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nisome ukurasa wa 91 wa kitabu cha bajeti; malengo ya bajeti hii amesema Mheshimiwa Waziri makubwa yapo manne nalisema lengo la tatu ambalo linasema kuimarisha kilimo (uzalishaji wenye tija na masoko ya mazao, ufugaji, uvuvi na misitu) kwa kuzingatia umuhimu mkubwa wa sekta hii katika uchumi wa Taifa (chakula, ajira, kipato cha wananchi, michango katika fedha za kigeni na muunganiko wa sekta hii na maendeleo ya viwanda). Katika hili niongelee tu zao moja tu ambalo tunalima Nyanda za Juu Kusini tumbaku.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumbaku nchi ya Malawi ilikuja kuchukua mbegu Chunya mwaka 1966, leo nchi ya Malawi inatengeneza kilo milioni 200 kwa mwaka za tumbaku wanauza nje, sisi mwaka 2010 tulifika kilo milioni 120 mwaka huu projections ni kilo milioni 54 tunashuka. Naomba Wizara ya Kilimo ijiulize kuna nini kwa nini production zinashuka naomba tutumie Chuo Kikuu cha SUA watafiti wako pale wazuri sana kwa nini kilimo chetu kinashuka, kwa nini hatupati masoko ya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Serikali, Wizara ya Kilimo tujiulize mazao mengi mwenzangu alisema asubuhi hapa tumbaku, pamba, korosho inashuka production badala ya kuongezeka kuna tatizo gani? Naomba Serikali ilifikirie sana hilo hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi katika hilo zao la tumbaku mwaka huu kuna kampuni nne ambazo zinanunua tumbaku. Kampuni moja imekataa kutoa makisio, kwa hiyo, ina maana kuna wananchi wa sehemu za Tabora, Chunya, Mpanda na Ruvuma, kwa hiyo, wananchi na vyama vya msingi vitakosa kulima na kuuza tumbaku yao. Naiomba Serikali ilichukue jambo hili kwa muhimu sana ili wananchi wa sehemu hizi wapate kulima na kuuza tumbaku na kuinua hali zao za maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme la mwisho, Mheshimiwa Rais alipokwenda Afrika Kusini, nchi ya Afrika Kusini imesema inaanza kufundisha Kiswahili, nchi nyingi, hata nchi ya Kongo nayo imesema wataanza kufundisha Kiswahili, ina maana Tanzania itaanza ku-export kama zao Kiswahili, lakini vijana wetu tulionao hawajaiva kama tulivyoiva baba zao wa zamani ambao tulikuwa tunapitia JKT na tuna maadili ya kutosha. Naomba hawa vijana watakuwa ni mabalozi wetu huko wanakoenda kwa hiyo, naomba Wizara, Serikali, mnapowachagua vijana hawa wa kwenda kufundisha Kiswahili nje ya nchi, iwe ni Afrika Kusini, iwe ni Kongo, iwe Zambia, kwanza tuwafundishe itifaki, tuwafundishe ubalozi kwa hiyo, wasije wakaenda kule wakaenda kututia aibu Tanzania ambayo ni nchi ambayo inasifika duniani kote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja na ahsante kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana nami kunipa nafasi hii niwe mchangiaji wa pili kwenye hoja ambazo zimeletwa na wenyeviti wa Kamati. Kamati hizi mbili zimefanya kazi nzuri sana na wenyeviti mmetuletea taarifa ambazo zipo kamili, nawashukuru sana na nawapongeza sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nianze kwa kutoa mifano kama miwili hivi au mitatu. La kwanza kuna mkoa hapa nchini ambao miaka ya 70 nyani walikuwa wengi sana mkoani huko na walikuwa wanashambulia sana mahindi kiasi cha kuleta njaa kwa wananchi. Wananchi wa Mkoa huo wakaamua sasa kwamba nyani ni kitoweo, wakaanza kula nyani; wanakamata nyani wanakula, nyani wakatoweka kabisa na chakula chao kwa miaka iliyofuata kikawa salama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano wa pili kuna mkoa mwingine miaka hiyo hiyo ya 70 ilivamiwa sana na nzige; wananchi wa mkoa huo wakaamua kwamba nzige ni chakula wakawa wanakamata sana wanakaanga, wanakula; nzige wakatoweka. Maana yangu ni kwamba kukitokea maovu zipo njia nyingi za kuyashambulia ili yaishe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano madawa ya kulevya ni ovu, yanaharibu wananchi na society; kwa hiyo, inaweza kutumia njia zozote kushambulia mpaka ziishe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wizi ni dhambi; mwenye mamlaka ya kukamata mwizi ni polisi; sasa mtu akija shambani kwako anaiba mahindi unaogopa kukamata kwa sababu sio kazi yako kumkamata unasema ni kazi ya polisi utavuna mabua. Nadhani tutumie njia zote ili kuhakikisha kwamba maovu kama madawa ya kulevya yanatoweka nchini kwetu. Anakamata nani ni suala lingine, nani anayekamata ni kwenye vyombo vinavyohusika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka baada ya hapo niongelee masuala mawili tu machache ambayo Mwenyekiti wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii ameweka mezani. Nianze na Hospitali ya Rufaa ya Benjamin Wiliam Mkapa ambayo ipo hapa Dodoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali za rufaa hapa nchini zipo tano au sita; Muhimbili, Bugando, KCMC, Mbeya na Benjamin Wiliam Mkapa. Hiyo hospitali ya Benjamin Wiliam Mkapa ni kama Jakaya Kikwete Heart Institute; ina vifaa vya kisasa kweli kweli lakini watumishi hakuna. Ile hospitali ilikuwa na madaktari wanajitolea; vijana kutoka vyuoni wanajitolea wako pale kama saba au nane, wamejitolea kwa zaidi ya mwaka mmoja; wanasubiri Serikali itakaporuhusu ajira waweze kufikiriwa nao, sio kulazimisha Serikali kuwaajiri bali waweze kufikiriwa kuajiriwa. Mkurugenzi wa hospitali hiyo baada ya vijana kutumika pale amewaondoa, halafu baada ya miezi miwili baada ya kuwaondoa amewarudisha baadhi yao wengine amewaacha huko mitaani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wenyeviti wa Kamati mlishughulikie suala hili, naona kama si haki hata kama Serikali imesitisha ajira lakini hawa vijana wamejitolea kuokoa maisha ya wananchi; na hawasemi kwamba utakapokuwa tayari kuajiri waajiriwe wao, hapana; wanajitolea tu na uwape posho kidogo, naomba Wenyeviti mlichukue hilo na mlishughulikie ili muweze kuishauri Serikali vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye hospitali hiyo hiyo kama nilivyosema ina vifaa vya kisasa kweli kweli, sasa hapo mimi huwa naenda kutibiwa; kuna mashine ya MRI (Magnetic Reasoning Imaging) ya kisasa kweli kweli, haijafungwa bado ipo pale imekaa tu na mtu anayetaka kipimo cha namna hiyo inabidi umpeleke Muhimbili au kwingine lakini mashine iko hapa, kwa nini haifungwi? Tunahitaji lazima Mheshimiwa Rais atoe amri ya kufunga hiyo mashine?
Mheshimiwa Mwenyekiti, iko mashine ya CT Scan ya kisasa kwelikweli, haijafungwa; iko mashine ya X- Ray, sasa hivi wanatumia mobile mashine ya X-Ray; iko mashine ambayo ni fixed, kubwa, ya kisasa kweli haijafungwa; tunahitaji nani aje atuambie tufunge hizo mashine? Mheshimiwa Mwenyekiti na Kamati yake naomba sana walishughulikie suala hili, waishauri Serikali iweze kufunga vifaa hivi na kutoa huduma kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye Hospitali ya Muhimbili, kama alivyosema Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii; Taasisi ya Jakaya Kikwete inafanya kazi nzuri sana, imepunguza Watanzania kwenda kutibiwa nje; unafanya vipimo na unatibiwa hapa hapa, naipongeza sana Serikali kwa hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge mwenzangu aliyetangulia, tuiangalie taasisi hiyo, ipewe pesa ya kutosha ili lengo lake la kupunguza kabisa na kuweka sifuri ya Watanzania kwenda kutibiwa nje litimie. Kwa hiyo, namwomba Mwenyekiti wa Kamati waliangalie vizuri hilo na kuweza kuishauri Serikali; hilo la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiwa hapo hapo, kuna Mturuki ambaye ametoa fedha kwa Muhimbili; amejenga maabara pale Muhimbili, Maabara ya Hermatology ya kupima kwa ndani sana vipimo vya mwili na damu mpaka kwenye details za vinasaba. Ameijenga maabara ile, iko pale, ame-train Watanzania sita au saba wa kuweza kui-manage hiyo maabara ili Serikali, Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na hospitali nyingine ziachane na kupeleka sampuli Nairobi, Afrika Kusini, Uingereza na Marekani ambako tunatumia fedha nyingi sana. Hiyo maabara ipo tayari na naambiwa Kamati wamepita hapo na kuna vifaa vingine amevituma vipo njiani vinakuja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Hospitali ya Muhimbili haipeleki hizo sampuli kwenye maabara hiyo ambayo ipo mlangoni hapo, bado inapeleka Afrika Kusini, Uingereza na Marekani, kwa nini? Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati naomba hilo alishughulikie aishauri Serikali vizuri. Maabara iko pale, mtu wa Mungu ameijengea Tanzania; tuitumie hiyo ili iwe kama ilivyo Taasisi ya Jakaya Kikwete kupunguza kupeleka fedha zetu nje ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii, naomba kuunga mkono hoja za Kamati zote mbili.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sandiangu wa ukulu kabisa, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia hoja hii iliyo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kuunga mkono hoja hii mia kwa mia. Nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Makatibu Wakuu na wataalam wote waliotayarisha Bajeti ya mwaka huu. Ahsanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijachangia, kuna jambo moja dogo linanikera sana, naomba niliseme hapa hewani. Terehe 2 Juni, kwenye Bajeti ya Wizara ya Nishati, Mheshimiwa Saed Kubenea alisimama hapa akinituhumu mimi Mwambalaswa kwamba kwanza ni Mkurugenzi kwenye Kampuni ya Umeme ya Upepo ya Singida na kwamba Ukurugenzi wangu huu nina mgongano wa maslahi (conflict of interest) kwa sababu nilikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na vilevile nilikuwa Mjumbe wa Bodi ya TANESCO. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna project nyingine ya umeme wa upepo, kule kuna concept, kuna idea na idea hii imeanza mwaka 2000. Mimi nimekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati mwaka 2013, hii imeanza mwaka 2000. Mgongano wa maslahi unatoka wapi? Nimekuwa Mjumbe wa Bodi ya TANESCO mwaka 2008. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kubenea alienda mbali zaidi, akasema Mheshimiwa Mwambalaswa alizuia kutekeleza Ripoti ya Richmond ya Mheshimiwa Mwakyembe. Mimi Mbunge nitazuiaje ripoti? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, huyu Mheshimiwa ananisemea maneno ya uwongo bila sababu yoyote. Ananishambulia bila sababu! Kule kuna concept, is not a company! Is not a project, is a concept. Ni ya waswahili fulani, sisi na walimu wa Chuo Kikuu tumeacha wazo hilo, lakini linapigwa vita na watu kama yeye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani yeye Mheshimiwa angeona hii concept ni ya mzungu angeunga mkono kama vile ambavyo Mheshimiwa Rais amezuia makontena ya makinikia, amempinga, lakini angezuia mzungu, angemuunga mkono. Jamani tusitembee na Ph.D mifukoni za mitaani. Ph.D (Pull him Down). Tuinuane waswahili kwa waswahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kubenea namfahamu sana, ni mdogo wangu, rafiki yangu wa miaka mingi. Alipoanzisha Kampuni ya Jarida lake la Mwanahalisi, mimi na wenzangu tulimchangia computer yake ya kwanza tulinunua sisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulimnunulia, lakini unaona anakonipeleka! Mheshimiwa Kubenea alimwagiwa tindikali machoni; amelazwa hospitali, Mheshimiwa Rais Kikwete, Rais wa Awamu ya Nne ameenda kumwona hospitali na amemchangia pamoja na sisi aende akatibiwe India, akageuka na magazeti yake anamshambulia Mheshimiwa Kikwete. Huyo! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya, Mheshimiwa Kubenea amechukua miaka kama nane anamshambulia Mheshimiwa Lowassa kila siku, ona! Lowassa katika kashfa mpya, hilo hapo; Rostam Hajaandika, hilo hapo; Wanaomsafisha Lowassa Hawa Hapa, hii hapa; Genge Laundwa Kumkabili JK, hili hapa; Rostam Aziz Hashikiki, hili hapa; Mabilioni Yatengwa Kumsafisha Lowassa, hili hapa; Lowassa Kutinga Kortini, hili hapa; kila siku! Leo anamsujudia Mheshimiwa Lowassa, huyo huyo! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi lile ni wazo, sina con- flict of interest yoyote, ni wazo. Kama ana matatizo na mimi aje tuongee. Mimi ni rafiki yangu, namfahamu huyu kijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hilo, nasema hivi, sijui kama anatumwa na dhamira yake au analipwa. Sijui.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuwapongeza Wataalam na Mheshimiwa Waziri kuhusu bajeti iliyo mbele yetu, bajeti nzuri sana, mti wowote wenye matunda unapigwa mawe. Kwa hiyo, mawe tunayategemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefurahi sana kwamba barabara yangu ya Mbeya - Chunya - Makongolosi imefika Chunya kilometa 72, ahsante sana Serikali ya JK na Serikali ya Mheshimiwa Magufuli ahsanteni sana. Nimefurahi kwamba kwenye bajeti hii ambayo iko mbele yetu, sasa wanaanza kujenga Chunya kwenda Makongolosi na Mkola na wanafanya kama alivyoagiza Mheshimiwa Rais kwenye kampeni kwamba tuanze Makongolosi kuja Chunya. Wataalam wako pale kwenye manunuzi, ninashukuru sana na nimefurahi sana. Najua huku kutoka Mkiwa kwenda Itigi iko kwenye bajeti, itaanza kujengwa ili baadaye tukutane katikati hii barabara ambayo zamani ilikuwa the Great North Road iwe kwa kiwango cha lami barabara nzima. Nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, reli ya TAZARA, kama ilivyo reli ya kati ambayo sasa inaboreshwa na Serikali hii ili tutumie uchumi wetu wa jiografia, tutumie nchi yetu kijigrafia kuweza kuzihudumia nchi ambazo ziko landlocked, ili tuweze kuinua kipato na uchumi wa nchi yetu; na reli ya TAZARA iko hivyo hivyo. Reli ya TAZARA yenyewe iko zaidi ya meter gauge, ndiyo maana matreni ya Afrika Kusini yanaweza kupita kwenye reli hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, haihitaji maboresho ya makubwa sana, inahitaji tu labda kuweka umeme ili treni za umeme zipite. Ile ya Kati inapokuwa imekamilika na ya TAZARA nayo iwe imekamilika tuweze kuihudumia Zambia, Zimbabwe, Malawi na Kongo ya Kusini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwanja wa ndege wa Songwe, nashukuru sana Serikali za awamu zote kwa kujenga uwanja wa ndege pale Songwe, Mkoa wa Mbeya. Uwanja ule uko very strategic kwa kutega uchumi kwenye Mikoa yote ya Nyanda za Juu Kusini na nchi zote majirani zetu, lakini sasa hivi taa hazipo za kuongoza ndege. Ndiyo maana mara moja, mbili, tatu ndege inakwenda, inakuta ukungu, inarudi Dar es Salaam hasa wakati wa mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba bajeti ya mwaka huu hii ambayo iko mbele yetu, najua fedha imo, tukamilishe kuweka taa kwenye uwanja ule ili tuweze kupata fursa zote za kiuchumi kwenye uwanja huo wa Songwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii bajeti ni nzuri mno, siyo ya kuisemea sana, ni ya kuunga mkono moja kwa moja. Naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Napenda nichukue nafasi hii nimpongeze Waziri wa Fedha na Mipango, Naibu Waziri na wataalam wote kwa kazi nzuri. Nia ya kuuleta Mpango hapa Bungeni ni kuujadili na kuuboresha ikiwezekana, kwa hiyo, sidhani kama kuna Mbunge yeyote ambaye anaudhihaki na kuukejeli, kazi yetu ni kuuboresha na kuujadili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna Mbunge mwenzangu ambaye hajui tunu za Tanzania nataka nirudie mimi. Tunu za Tanzania ya kwanza ni lugha yetu ya Kiswahili, ya pili Muungano wetu, ya tatu ni utu na udugu wetu na ya nne ni amani na utulivu. Hizi tunu hazikuja Tanzania kwa bahati mbaya, viongozi/waasisi wetu walitumia nguvu na resources nyingi sana kuzi-inculcate kwa Watanzania na ndiyo maana Tanzania imekuwa mfano wa kuigwa duniani kwa sababu ya hizo tunu nne. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa zinapoanza kutokea kauli za kutugawa kwa majimbo na ukanda humu ndani zinasikitisha sana. Unajua sisi Wabunge ni viongozi na kiongozi kwenye jamii yoyote watu unaowaongoza wanapenda kuiga lile unalosema na unalotenda. Kwa hiyo, tunayoyasema humu watu wetu kule wataiga. Naomba Bunge lako hizi tunu nne tuzilinde kwa nguvu zetu zote, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niongelee kidogo Mpango aliouleta Mheshimiwa Mpango. Ameanza na miundombinu kwamba inasaidia kuchochea maendeleo kwenye nchi kama Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye umeme. Nimeona miradi mingi ya kuongeza uzalishaji wa umeme kwa sababu umeme ni driver kubwa ya kuchochea maendeleo ya uchumi. Stiegler’s Gorge itazalisha megawati 2,100 ikikamilika, na source kubwa ya maji ya mto unaokwenda kulisha Stiegler’s Gauge ni Mto Ruaha. Ukiuona Mto Ruaha ulivyokuwa mwaka 2008 na ukiuona leo, inasikitisha.

Kwa hiyo, naiomba Serikali inapopanga kwenda kuweka mtambo wa kuzalisha umeme pale Stiegler’s Gorge iweke mpango kabambe sana wa kufanya conservation ya The Great Ruaha, vinginevyo tutakuwa hatuna maji ya kuzalisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tumejaliwa kuwa na vyanzo vingi vya umeme, wengine wamesema asubuhi jotoardhi, jua, upepo, naomba Serikali iangalie kote huko ili tuweze kuwa na umeme mwingi wa kutosheleza viwanda vyetu na umeme mwingi wa ku-export.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wa China wameendelea mpaka kufika hapo walipo walikoanzia ni mbali sana. Kwanza walikuwa na revolution ya kilimo, lakini baadaye wakaona waanze viwanda vidogo vidogo, wakawapeleka vijana wao kwenda kusoma kokote kule nje kwa gharama yoyote na waliporudi kwa fani ile aliyosomea, walikopeshwa fedha na vifaa waende kufanya hiyo shughuli ambayo walisomea; hao ndio wameanzisha viwanda ambavyo sasa hivi China ina mabilionea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani hata sisi, juzi Mheshimiwa Rais alikuwa Kagera, Kiwanda cha Kagera Sugar kinafanya vizuri sana; kimeajiri vijana wa Kitanzania wanafanya kazi pale. Serikali inaweza ikafanya vivyo hivyo, ikawachukua vijana wa Kitanzania waliosoma, kama ni kilimo, iwawezeshe, iwakopeshe, iwape ardhi waanzie kule tuwe na mapinduzi ya kilimo kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye maji, wenzangu wengi wamesema, miaka mitano, sita ijayo maji yatakuwa ni crisis sana duniani. Naomba Serikali ianzishe Wakala wa Maji Vijijini na Mijini kama ilivyo kwa Wakala wa Barabara, kama ilivyo kwa Wakala wa Umeme na kama ilivyo TANROADS. Ni muhimu sana Serikali ianzishe Wakala wa Maji Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika miundombinu ambayo nilikuwa nimesema, nije kwenye reli ya kati ya SGR, reli ya Tanga kwenda mpaka Musoma, reli ya kutoka Mtwara kwenda mpaka Liganga, lakini reli ya TAZARA ni reli ambayo tayari ni standard gauge, inahitaji kuboreshwa tu na kuwekewa umeme. Naomba Serikali iangalie sana reli hii kwa sababu nayo itaifungua nchi yetu kwa nchi ambazo zipo kusini mwa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile reli hii itakuwa inapita kwenye dry port ambayo itaanza kujengwa pale Mbeya, kwa hiyo tunakuwa na block trains za kutoka Dar es Salaam kwenda Kigali na Bujumbura. Kutakuwa na block trains kutoka Dar es Salaam kwa reli ya TAZARA kwenda Mbeya, kwenda kuwasaidia wenzetu wa Zambia, wa Malawi na wa Zimbabwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nirudie, tunu za Tanzania ni hizo nne nilizozisema, nimesema Muungano, Lugha ya Kiswahili, utu na udugu na amani na utulivu. Bunge lako lizienzi na kuzilinda tunu hizi kama mboni za macho yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia kwenye taarifa hizi mbili ambazo zimewasilishwa na Wenyeviti. Napenda niwashukuru Wenyeviti wamewasilisha taarifa zao hizi kwa weledi na umakini mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Bunge la Tisa tulifanyiwa semina na watu wa Usalama wa Taifa, kuna mfano mmoja walileta wale watu wa Usalama wa Taifa, Kiongozi mmoja wa nchi hapa Tanzania amepelekewa zawadi ya Qurani, kitabu cha Mungu cha Qurani kapelekewa. Kwa kuwa ni Kiongozi mkubwa watu wa katikati waliingilia kuifungua kwanza ile Qurani, kumbe lilikuwa ni bomu tulioneshwa hapo. Sasa juzi Mheshimiwa Spika Mbunge mwenzetu amepigwa risasi moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, mbili, Jenerali mmoja Mstaafu wa Jeshi kapigwa risasi hicho ni kiashiria kwamba silaha zipo ‘bwelele’ nchini kwetu. Zipo bwelele kwa sababu tuna changamoto nyingi sana, hali ya majirani zetu Sudan, Somalia, Congo vita iliyoko huko inafanya na mipaka yetu ipo porous, silaha nyingi zipo nchini hapa sana; pia utandawazi uliopo duniani; tatu, kukosa ajira kwa vijana wetu ambao wanarubuniwa na watu wanaopigana vita huko na kuwafundisha ugaidi. Hizi ni changamoto ambazo zinaonesha kwamba usalama wa Viongozi hapa Tanzania is an issue of the sense kwa sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuomba sana Bunge lichukue hatua madhubuti kuhakikisha Wabunge, Wabunge ambao ni baadhi ya Viongozi, Wabunge ambao hapa Bungeni tunaongea mambo ambayo yanawagusa wengine huko nje ambao wana uwezo wao kifedha na kigaidi, wawekewe usalama. Usalama hapa Dodoma kwenye makazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nasema kwamba, naliomba Bunge lichukue hatua madhubuti sana kuhakikisha usalama wa Wabunge kwa sababu ni Viongozi. Kwa sababu mambo ambayo wanaongea Wabunge hapa ndani yanawagusa watu wengine huko nje ambao wana uwezo wa kifedha na uwezo wa kigaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge la Kumi lilianzisha mchakato wa kuwa na Kijiji cha Wabunge hapa, naomba wazo hilo liendelee, nyumba zijengwe Wabunge wote wake sehemu moja ili waweze kupatiwa ulinzi. Huko kwenye Majimbo yetu Wabunge wapewe ulinzi kama anavyopewa ulinzi Mkuu wa Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nne, Wabunge magari yao yatambuliwe, yawe na namba ambazo zipo sawasawa na zinajulikana kwamba huyu ni Mbunge wa Lupa, namba yake ipo pale, vinginevyo Wabunge wengi wataanza kupigwa risasi, Viongozi wengi wataendelea kupigwa risasi. Usalama wa Wabunge, usalama wa Viongozi wote nchini Tanzania sasa hivi ni issue ambayo ipo top of the agenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na mimi kunipa fursa hii niweze kuchangia hoja yetu ambayo iko mezani. Napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, Waziri wa Nchi katika Ofisi hiyo, Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu wote na watendaji wote wa Wizara hiyo wanavyochapa kazi katika Awamu hii ya Tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hii naona imejipambanua sana imeweka kipaumbele katika miradi ya miundombinu; miradi ya barabara, bandari, viwanja vya ndege, reli, miradi hiyo ya miundombinu. Miradi hii ni miradi ambayo inachochea ukuaji wa uchumi. Kwa hiyo, ninawapongeza na kuwapa moyo muendelee kuwekeza katika miradi hiyo kwa sababu inachochea sana ukuaji wa uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendeleze pale ambapo aliishia Mheshimiwa mwenzangu Mheshimiwa Oran Njeza Mbunge wa Mbeya Vijijini. Uwanja wa Songwe sawasawa na Serikali mmekula ng’ombe mzima tunashindwa kumalizia mkia, uwanja umejengwa ni mzuri sana, bado kuweka taa za kuongoza ndege, bado uzio na kumalizia jengo la abiria. Mbeya, Nyanda za Juu kote huko kuna fursa nyingi sana ya mazao. Kuna ndizi, kuna maua, kuna viazi, kuna mpunga anaolima Mheshimiwa Haroon, vyote vinahitaji usafiri wa kwenda nchi za nje.

Kwa hiyo, naomba uwekezaji uliobaki ni mdogo sana, kuweka taa kuweka na uzio na kumalizia uwanja wa ndege ni mdogo mno. Naomba Serikali katika bajeti hii ionyeshe nia ya kwelikweli kwamba inamalizia uwanja wa ndege wa Songwe ili biashara iendelee kama kawaida. Inauma sana pale ambapo ndege inatoka Dar es Salaam inafika Songwe inakuta kuna ukungu inageuza kurudi Dar es Salaam ni hasara kubwa sana. Kwa hiyo, naomba Serikali imalizie mradi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa Stiglers Gorge ni mzuri sana utaongeza nguvu kwenye uchumi, utaongeza umeme karibu megawati 2100, lakini mradi huu unategemea maji, maji ya Mto Ruaha, Mto Kilombero, Mto Rufiji, mto huu unakauka. Mto Ruaha, Kilombero, Rufiji inakauka seriously. Ukiuona mto huu ulivyokuwa mwaka 2008 na leo utalia. Mheshimiwa Makamu wa Rais ameenda Iringa kutembelea Bonde la Mto Ruaha akashtuka, ameunda Tume ya kufuatilia mto huo. Mheshimiwa Waziri wa Maliasili ameenda Kilombero ameona Kilombero, ameona mto unavyokauka na vijito vyake ambavyo vinaingia kwenye mto huo vinakauka naye akaunda tume ya kufuatilia mto huo.

Naomba Wizara zote zinazohusika zikae pamoja ziunganishe vichwa pamoja na Chuo Kikuu cha SUA, tuunganishe vichwa na kuurejesha mto huu uweze kuweze kuleta maji kwenye Bwawa la Stiglers isije ikawa white elephant.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee barabara ya Mbeya - Chunya - Makongorosi. Naishukuru sana Serikali imejenga barabara hiyo imefika Chunya kilometa 72, sasa hivi bei ya usafiri kutoka Mbeya kwenda Chunya ni shilingi 3,500 kama ilivyo kwingine kutoka Mbeya kwenda Tukuyu, na wananchi wangu wanaanza kusafirisha mazao kwa haraka kutoka Chunya kwenda Mbeya. Sasa hivi Serikali inaanza mwaka huu kujenga barabara hiyo kutoka Chunya kwenda Makongorosi, naishukuru sana. Wakati huo huo inaanza kujenga kutoka Mkiwa kwenda Itigi ili tukutane katikati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina ombi; mara nyingi nimeongea hapa kwamba barabara hii ya Mbeya Chunya imekamilika lakini malori yanayobeba mbao yanayobeba tumbaku Chunya - Mbeya yanabeba lumbesa. Wakifika Mbeya ndiyo wanagawa yanakuwa malori mawili, kwa hiyo, barabara inaumia. Hii barabara sasa hivi kwetu sisi ni mboni ya jicho inaumia, naomba Serikali iweke weigh bridge hata mobile weigh bridge tuweze kuilinda barabara hii, naomba sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la maji vijijini. Naunga mkono Wabunge wenzangu wengi wameongelea suala hili na wameiomba Serikali kwamba kama Serikali ilifanya vizuri iliunda TANROADS inajenga barabara vizuri, ikaunda REA inaweka umeme vijijini vizuri, imeunda TARURA imeanza kazi vizuri ya kuweka barabara za vijijini na mijini, umefika wakati wa kuweka Wakala wa Maji Vijijini. Naunga mkono sana hoja hiyo.

Pamoja na hiyo namshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuja Chunya alitukuta tuna shida ya maji kwenye Mji wa Chunya akaidhinisha fedha zimetoka na kinajengwa kisima kikubwa sana Chunya na nadhani katika mwezi huu na mwezi ujao kitakamilika, kwa hiyo wananchi wa Chunya kwa asilimia 80 watapata ahueni ya maji. Naomba fedha iliyobaki itolewe kwa muda ili tutatue tatizo la maji kwa wananchi wa Chunya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile wananchi wa Mji wa Makongorosi nao wanachimba kisima, kuna wananchi zaidi ya 20,000 wana shida sana ya maji, naomba Serikali nayo ielekeze macho kwa wananchi hawa wa Makongorosi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Bwawa la Matwiga Serikali imetoa fedha nyingi sana kujenga Bwawa la Matwiga. Bwawa hili likikamilika litaweza kuhudumia kata zaidi ya sita, sasa limechimbwa limejaa maji liko tayari, linasubiri miundombinu ya mabomba, matanki ili tuweze kupeleka maji kwenye kata hizo. Naomba Serikali itoe fedha haraka kwenye bajeti hii ili tukamilishe mradi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Chunya ni moja kati ya Wilaya kumi ambazo ziliteuliwa na Serikali kwamba wajenge Vyuo vya VETA. Tukakubali tumetenga eneo lakini mpaka sasa hivi chuo hakijajengwa, naomba Mheshimiwa Waziri wa Elimu atakapokuja hapa atuambie ni lini watatoa fedha za kuanza kujenga Chuo cha VETA kwa Wilaya ya Chunya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo la mwisho, kuna Watendaji wa Vijiji na wa Kata. Watendaji hawa wamekuwa wana sakata refu sana na Serikali. Serikali ilisema watendaji ambao waliajiriwa wakiwa darasa la saba walidanganya vyeti waliondolewa kuanzia mwaka 2004, lakini wale ambao walioajiriwa kabla ya hapo waliendelea kufanya kazi. Mwaka huu Serikali inawaondoa hawa watendaji kuleta watendaji wengine, inasema walipewa muda wa kujiendeleza hawajafanya. Sasa watendaji hawa ndio wamesaidia kujenga shule za sekondari, wamesaidia kujenga vituo vya afya, wamesaidia kujenga zahanati, walikuwa hawana muda wa kujiendeleza, naiomba sana Serikali hawa watendaji wengi karibu wanaelekea muda wa kustaafu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba watendaji hawa waachwe wamalizie muda wao wastaafu kwa amani hawakutenda kosa lolote, hawakusema wako form four hapana, waliajiriwa wakiwa darasa la saba.

Kwa hiyo, naomba Serikali iwe na moyo wa huruma, kwenye human face iwaache watendaji hawa wamalizie muda wao wastaafu kwa amani kwa sababu wameifanyia kazi Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi niweze kuchangia hoja ambayo ipo mezani. Napenda kuchukua nafasi hii kuwapongeza sana Mheshimiwa Profesa Mbarawa na timu yako yote, Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu wote; Wizara yenu kubwa sana lakini mnachapa kazi kweli kweli. Nimewahi kukuona Profesa Mbarawa unasafiri kutoka Mbeya kwenda mpaka Itigi kwa barabara ambayo ni mbaya sana ili uione barabara ile ilivyo, uje utujengee, hongereni sana na endeleeni kuchapa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na wahenga wanasema mfinyanzi huulia gaeni, lakini kwa hapa Dodoma Area D Site II TBA angalieni pale maana yake barabara ya kuingia pale ni mahandaki, gari limezima, naomba TBA mtengeneze barabara ile ya kwenda Site II. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru sana Serikali kwa kujenga barabara ya lami kutoka Mbeya kwenda Chunya kuelekea Makongorosi, barabara imekamilika nauli zimeshuka na usafiri upo siku nzima kati ya Mbeya na Chunya, nawashukuru sana kilometa 72 zimekamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi Serikali imetenga fedha za kuanza ujenzi kutoka Mbeya kwenda Makongorosi kilometa 43, asanteni sana. Pia mmetenga fedha za kuanza ujenzi kutoka Mkiwa kwenda Itigi ili baadaye Chunya mtapopanda na Itigi wanashuka tukutane katikati, naishukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo lipo moja, hii barabara ya Mbeya – Chunya kwetu sisi ni tunu (master piece) imeturahisishia maisha mno, lakini sasa bahati mbaya Chunya kuna mazao mawili ambayo yanaharibu barabara; kuna mazao ya miti (mbao) na kuna tumbaku. Wachukuzi wanaochukua mizigo hiyo wanabeba malori ya lumbesa ili wakifika Mbeya ndio wagawe yawe magari mawili, wanaharibu barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba Mheshimiwa Waziri utuwekee weight bridge hata kama ni mobile weigh bridge tuweze kuyadhibiti magari hayo maana yanasafiri usiku, ahsante sana najua utatufanyia hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ninaipongeza Serikali kwa kuiboresha Tanzania – Zambia highway, mmejenga vizuri sana kuanzia Makuyuni mmekwenda mpaka Igawa sasa hivi ni barabara nzuri sana. sasa hivi kutoka Igawa kwenda Mbeya iko kwenye usanifu na kutoka Mbeya kwenda Tunduma ipo kwenye usanifu. Kama alivyosema Mheshimiwa Mwakibete, ninaomba mtakapokuwa mnajenga sasa kutoka Igawa kwenda Mbeya mkifika Mlima Nyoka mfanye bypass ya kwenda kutokea Mbalizi tujaribu kupunguza congestion katika Jiji la Mbeya. Tuiboreshe hiyo barabara ya katikati ya Mbeya lakini hiyo ya Mlima Nyoka kwenda Mbalizi iwe bypass, naomba muifikirie hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nataka niongelee kama walivyoongea wenzangu Mheshimiwa Njeza na Mheshimiwa Mwakibete, Uwanja wa Songwe. Kwanza ninaiomba Serikali Mkoani ianze mchakato wa kubadilisha jina kwamba isiitwe Uwanja wa Songwe, tutafute jina lingine maana yake Songwe ni Mkoa mwingine, kwa hiyo, tutakuwa tunatangaza mkoa mwingine. Samahani Mheshimiwa Naibu Waziri wa Michezo sikubagui, lakini ni mkoa mwingine, tuite jina lingine lakini uwanja huo umekamilka upo vizuri. Sasa hivi ndege wakati wa mvua zinakwenda pale wakati mwingine zinashindwa kutua pale zinarudi kwa sababu hakuna taa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hela imetengwa humu, ninaomba taa za kuongoza ndege na ukuta ujengwe naomba jengo la abiria likamilike. Ninajua Serikali imevunja mkataba na mkandarasi aliyekuwepo kwa sababu za kiufundi, ninaomba mteue mkandarasi mwingine haraka ili tukamilishe uwanja huo uanze kusaidia wana Mbeya kwa kiuchumi, tuna mazao mengi, parachichi, ndizi, viazi, mpunga na kila kitu, tuutumie uwanja huo vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mashirika mengi ya nje kama Emirates yapo tayari kwenda kuchukua mizigo Uwanja wa Songwe, lakini mpaka taa ziwepo na uzio wa uwanja uwepo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ninaiomba sana Serikali katika bajeti hii ya mwaka huu ikamilishe vitu hivyo vitatu; taa za kuongoza ndege, jengo la abiria na uzio katika uwanja huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana kunipa nafasi hii, ninaunga mkono hoja, ahsante sana.
Azimio la Bunge la Kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa SADC na kuendesha vyema Mkutano wa 39 wa Jumuiya hiyo
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Nami kama wenzangu waliotangulia, naunga mkono azimio hili lililowekwa mezani. Azimio hili linatukumbusha historia ya ukombozi katika Afrika. Tanzania iliongoza nchi za Kusini mwa Afrika ili nchi ambazo hazijapata uhuru zipate uhuru Mwalimu Nyerere akiwaongoza. Tulianza na Mlungushi Club ambayo alikuwa anaiongoza Mwalimu Nyerere, lakini Mabeberu wakaipiga vita nchi nyingine zikawa zinajipendekeza kwa mabeberu, ndiyo Mwalimu akaanzisha nchi za mstari wa mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bahati mbaya nchi za mstari wa mbele zipo nchi zilikuwa zinajitegemea Afrika Kusini kiuchumi. Kwa hiyo, Mwalimu akaona afadhali aache mstari wa mbele, ndiyo ikaazishwa Southern African Development Coordination Conference ili hizi nchi za Kusini mwa Afrika zisianze kujitegemea kijuchumi, ziachane na Afrika Kusini. Baada ya kuanzisha hii Southern African Development Coordination Conference, nchi za Ulaya na Marekani zikaanza kutambua kundi hili, likaanza kumpa pressure Afrika Kusini iachane na ubaguzi. Ndiyo ikakua ikaanza Southern African Development Community yote hii ikiongozwa na Mwalimu Nyerere. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vijana wa sasa wakitaka kuelewa Mwalimu Nyerere alikuwa champion wa uhuru katika Afrika, wasome kitabu chake cha Crusade for Liberation, utaona Mwalimu alivyojitoa ili Afrika yote ipate uhuru. Kuwepo kwa Southern African Development Community ndiyo kumeleta ukombozi Zimbambwe na Afrika Kusini.

Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Rais. Marais hawa waliokuja kwenye mkutano wa juzi, Rais Cyril Ramaphosa na Rais Mnangagwa angalau wanatambua umuhimu wa Tanzania kuleta mkombozi Kusini mwa Afrika.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado kwenye mkutano huo Tanzania ikiongozwa na Rais wetu pamoja na Waziri wa Mambo ya nchi za Nje inaendeleza mapambano ya kuikomboa Zimbabwe ili vikwazo viondolewe na Zimbambwe. Bado Tanzania iko… (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Azimio hili ni nzuri sana linatukumbusha Champion wa Tanzania katika kuikomboa Afrika. Yote haya ni mazuri, naunga sana mkono, nasema, boseaga maswano muno muno munze yetu. Muaha yalumbwe. Sendenyi. (Makofi/Kicheko)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Nishati
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia hoja iliyo mbele yetu hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote. Wizara yenu ni nyeti sana na mzigo mnapiga kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi Mheshimiwa Waziri amenishtua, Jumamosi alikuwa Mkoa wa Songwe kwenye Wilaya ya mdogo wangu Mheshimiwa Mulugo na kwa Dada yangu Ileje ya Udinde kilometa 300 kutoka Mbeya. Jumatatu namsikia yuko Mtwara anafungua umeme, kwa kweli mnapiga kazi hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Wizarani kwako kuna watu zaidi ya watano (5) wanakaimu, siyo vizuri. Maana anapokaimu anafanya kazi kukufurahisha wewe ili usije ukamnyima cheo lakini ukim-confirm anafanya kazi kwa mujibu wa sheria, kwa hiyo, naomba wawe-confirmed haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, REA I Wilayani kwangu Chunya ilipeleka umeme kwenye vijiji vingi sana lakini iliruka shule za sekondari zaidi ya saba. Mimi kama Mbunge na kama mzazi nilikopa hela benki nikaenda kulipa TANESCO niweze kupeleka umeme kwenye sekondari hizo. Nililipa pale TANESCO Chunya, Waziri anaweza ku-cross check na Meneja wa Chunya, nililipa pesa ndefu siwezi kuisema hapa kwa sababu sitaki kujisifu, kwa sababu vitabu vya dini vinasema mkono huu ukitoa sadaka huu usijue. Tatizo ni kwamba REA II imeruka Kituo cha Afya cha Kata ya Mtanila, cha zamani sana ambacho Mwalimu Nyerere alienda kuweka saini kwenye kitabu cha wageni mwaka 1966. Mheshimiwa Waziri sina uwezo tena wa kwenda kukopa benki kwa sababu bado nalipa ile ambayo nilikopa ya kupeleka umeme katika shule za sekondari. Naomba sana hii REA III inapoenda basi Kituo cha Afya cha Mtanila, Kata ya Mtanila ambacho kinachohudumia Tarafa nzima ya Kipambawe kipelekewe umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru sana Wizara kwa kupelekea hiyo REA III ya sasa hivi, Jimboni kwangu iko kwenye Kata ya Ifumbo, Vijiji vya Ifumbo, Soweto, Mawelo na vijiji vingine. Kuna kijiji kinaitwa Itumbi, Wizara ya Nishati inataka kujenga kituo cha kuwahudumia wachimbaji wadogo (Center of Excellence) nikamuomba Mheshimiwa Waziri kwamba hii REA III Itumbi wapeleke umeme.

Mheshimiwa Waziri alinikubalia namshukuru sana Mungu ambariki, lakini naona bado Wahandisi wa REA hawajapewa hiyo taarifa kutoka kwake. Naomba anapowapelekea taarifa ya ombi langu la Kituo cha Afya cha Mtanila basi awapelekee na hii ya Kijiji cha Itumbi ambako itajengwa Centre of Excellence.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee kidogo umeme wa maporomoko ya Mto Rufiji, ni wazo zuri sana litaikomboa nchi yetu naliunga mkono sana. Mto Ruaha unakauka, haukauki kwa sababu ya tabianchi hapana unakauka kwa sababu ya matumizi ya maji (management), unakauka kwa sababu wakulima wanachukua maji hawayarudishi, unakuka kwa sababu ya wafugaji, unahitaji tu utawala. Ndiyo maana Mheshimiwa Makamu wa Rais alienda Iringa akaliona tatizo hilo akaunda Tume ya kulishughulikia. Mheshimiwa Waziri wa Maliasili alienda Kilombero aliona Mto Kilombero nao unaenda kwenye Mto Rufiji unakauka naye akaunda Tume. Rai yangu ni hii kwa Mheshimiwa Waziri, naomba yeye ambaye ndiye mwenye dhamana ya Nishati awe ndiyo kinara, achukue Wizara yake ya Nishati, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Maliasili na Wizara zote zinazohusika muweze ku-manage mito hii miwili (2); Mto Ruaha na Mto Kilombero ili tupate maji mengi ya kwenda kwenye umeme wetu wa Stiggler’s Gorge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imeishauri Wizara inasema, Kamati inaendelea kusisitiza Serikali kuwekeza zaidi katika nishati jadilifu (renewable energy). Mheshimiwa Waziri wakati anajibu maswali hapa alisema kwamba Tanzania ina-potential ya megawatt 5,000 katika geothermal, naomba nguvu ambayo Mheshimiwa Waziri ametumia kuunadi mradi wa Stiggler’s Gorge nguvu hiyo anadi hii geothermal, megawatt 5,000 ni nyingi mno. Tena hahitaji fedha nyingi Mheshimiwa Waziri, anahitaji tu anunue rig moja au mbili azileta hapa nchini na kuikabidhi hiyo Kampuni aliyounda ya Geothermal Development Company, yenyewe inatoboa mahali ambapo kuna potential inaleta juu kwenye well-head mnatangaza tenda waje wakezaji kuweka mitambo hapo. Kwa hiyo, naomba sana hii megawatt 5,000 potential ya Tanzania ni kubwa sana, naomba Mheshimiwa Waziri aishughulikie hii kama alivyoshughulikia Stiggler’s Gorge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba niongelee kidogo miradi miwili ya Kiwira megawatt 200 na Mchuchuma megawatt 600 ya makaa wa mawe. Mheshimiwa Waziri ulipoingia Wizarani ulisikia kuna mradi wa Kiwira megawatt 200 Mchuchuma megawatt 600. Ulipokuwa Mwanasheria Mkuu wa Wizara, Kiwira megawatt 200, Mchuchuma megawatt 600. Umekuwa Naibu Waziri Kiwira megawatt 200, Mchuchuma megawatt 600, sasa umekuwa Waziri bado Kiwira megawatt 200, Mchuchuma megawatt 600, Mheshimiwa Waziri do something, weka alama. Hii historia ya kwamba Kiwira, Mchuchuma iishe, fanya kitu, weka alama ili vizazi vijavyo viseme kwamba Mheshimiwa Dkt. Kalemani alikuwa Waziri wa Nishati alifanya kazi Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye hoja hizi mbili ambazo ziko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Naibu Makatibu Wakuu, kazi ni ngumu sana lakini wanaiweza, ni kazi ngumu kweli kweli. Hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kutoa hoja moja ambayo hailingani sana na hoja hii iliyo mbele yetu. Ziwa Rukwa miaka ya 60 na 70 mpaka 80 mwanzoni ilikuwa inatoa samaki wengi sana aina ya tilapia ambayo inaitwa ngege, walikuwa maarufu sana kwa Nyanda za Juu Kusini mpaka Zambia tulikuwa tunakula samaki hao. Miaka hii sasa hivi hao samaki hawapo, tumebaki tudogo hata huu mkono hauenei. Hata Serikali ikisimamisha uvunaji, miezi mitatu, miezi sita samaki havikui vinabaki pale pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina hofu, kwamba kwa sababu katika Wilaya ya Chunya ambako ndio Mto Rupa unatokea ambao unaingia kwenye Ziwa Rukwa kuna uchimbaji mkubwa sana ambapo hapo zamani walikuwa wanatumia zebaki kusafisha madini ya dhahabu, nina wasiwasi kwamba samaki hawa wamekuwa contaminated na zebaki ndio maana havikui. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali ifanye utafiti haraka, ifanye utafiti tujue kama ni zebaki ipo basi tujue tiba ni nini tusije tukaharibu afya za watu. Kama imeshindikana basi Serikali ifanye mpango wa kupandikiza samaki wengine katika ziwa Rukwa ili tuendelee kuvuna kama tulivyokuwa tunavuna zamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili naliunganisha na hoja ya kodi, tax measures ambazo Mheshimiwa Waziri ameweka mojawapo. Mheshimiwa Peter Serukamba juzi akichangia alidadavua sana kitaalam akiipongeza Serikali kwa kuanzisha electronic tax stamps, alidadavua kitaalam. Mimi nataka niiseme ki-layman, Watanzania tumekuwa tunanyweshwa mapombe makali, magongo kwa miaka mingi sana kwa sababu ya tax stamps ambazo zinaweza kuigwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilifika mahali hapa Tanzania ilikuwa nusu ya consumption ya konyagi hapa nchini nusu ni original na nusu ni fake. Sasa ukinywesha population ya Watanzania gongo kwa muda wa miaka minne, mitano utapata watu wa ajabu sana. Kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kuweka hii electronic tax stamp ambayo haiwezi kuigwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na faida zote ambazo watapata za ku-count real time kupata kodi kuongezeka kwa mara dufu, lakini hili la Watanzania kunyweshwa gongo mimi namsifu sana kwa hilo Mheshimiwa Waziri na siyo gongo tu kwa konyagi hata kwenye brand hata kwenye vitu vingine wanaiga tax stamps wananywesha Watanzania. Aliwahi kusema Mheshimiwa wa Jimbo fulani hapa kwenye jimbo lake watu wanaume walikuwa wanashindwa kuhudumia ndoa, wanakwenda nchi nyingine kwa sababu ya mambo kama haya. Kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niipongeze Serikali kwa kutumia uchumi wa jiografia kuweza kukuza mapato ya economy ya nchi, kupanua bandari ya Dar es Salaam, kujenga bandari ya Bagamoyo, kupanua bandari ya Mtwara, kujenga SGR na kuirekebisha meter gauge. Kwa hiyo, tutakuwa na reli mbili kwa upande wa kaskazini standards gauge ambayo ina mita 1.067 na meter gauge ambayo ni mita moja kamili. Vilevile reli ya TAZARA ambayo yenyewe ni cap gauge yenyewe upana wake ni mita 1.067, tutakuwa na aina tatu za reli. Hizi za Kaskazini zitaungana za Kenya, Uganda lakini hii ya TAZARA itaungana na South Africa na Zambia na Nchi zote za SADC huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pamoja juhudi zote ambazo tunafanya za kujenga reli mpya na kukarabati ya zamani reli ya TAZARA tusiisahau katika uchumi wa jiografia. Yenyewe inahitaji tuiweke umeme ibaki hivyo hivyo ni cap gauge tuiwekee umeme ili tuweze kuweka ma-train ya kwenda kwa kasi. Vilevile Serikali inaponunua mabehewa sasa, mabehewa ya hii reli mpya ya standard gauge inunue mabehewa na vichwa ambavyo ni adjustable ili viweze kutumika katika reli zote tatu. Vitumike kwenye SGR, vitumike kwenye meter gage na vitumike reli ya TAZARA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo naomba niisihi sana Serikali, imejenga uwanja wa ndege wa Songwe, ni jambo nzuri sana, inahudumia Southern Highlands yote pamoja Nchi za Kusini mwa Afrika jambo nzuri sana. Hata hivyo, huu uwanja wa ndege hauna ukuta wa usalama, jengo la abiria halijakamilika, taa za kuongoza ndege hazipo, ni kama Serikali imekula ng’ombe wote, lakini mkia imebakiza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara mbili nimeruka na ndege kutoka Dar es Salaam kwenda Mbeya tumeshindwa kutua tumerudi Dar es Salaam. Ni hasara sana kwa shirika la ndege lakini vile vile inamuumiza yule abiria sana kwenye mwili wake. Naomba sana Serikali ifanye juhudi zote ili kukamilisha kujenga ukuta wa usalama, waweke hizo taa za kuongozea ndege na wakamilishe ujenzi wa jengo la abiria ili uwanja wa ndege wa Songwe uendelee kuhudumia Southern Highlands kama ilivyopangwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeongea kwa kifupi inatosha, lakini naomba sana kusisitiza sana kwamba, napongeza sana hizi juhudi za Serikali za kuweka Electronic Tax Stamps ambazo zitakuza mapato ya Serikali mara dufu na zitapunguza wananchi kuweza kuathirika kwa kunywa gongo na product nyingine za ajabu ajabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia hoja yetu ambayo iko mezani.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Manaibu Waziri wote wawili na Watendaji wote Wizarani kwa kazi kubwa wanayofanya kwenye sekta hii ya madini iweze kuchangia maendeleo ya Watanzania. Mnachapa kazi kweli kweli, nimeona mnafika kila mahali, hata kwangu Chunya mmefika na huko mnatimiza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwa ruhusa yako nisome sehemu moja kwenye Kitabu cha Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 22, anasema, “Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia GST na STAMICO chini ya mradi wa usimamizi endelevu wa rasilimali madini, ilikamilisha utafiti wa kina wa kijiosayansi uliohusisha uchorongaji na ukadiriaji wa mbale katika maeneo ya wachimbaji wadogo kwenye maeneo sita ya ujenzi wa vituo vya umahiri vya Katente huko Bukombe, Itumbi Chunya kwangu, Kona - Tanga, Kapanda – Mpanda, Buhemba – Musoma na Kyerwa. Vituo hivyo vitatumika kwa ajili ya mafunzo ya uongezaji thamani madini na uchimbaji salama pamoja na kuongeza uzalishaji, tija na hivyo kuongeza mapato kwa wachimbaji wadogo.” (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana Wizara kwa jambo hili. Naomba kwenye kituo changu na vituo vingine vyote ambavyo mmevisema, mkivijenga na kuvianzisha, muweke mitambo ya kukodisha wachimbaji wadogo wadogo. Kwa sababu sehemu kama Chunya kwangu Wilaya nzima ni mwamba, dhahabu iko chini ya mwamba. Kwa hiyo, wachimbaji wadogo wadogo wanashindwa kupata vifaa vya kuweza kuchoronga hiyo miamba na kuweza kuifikia dhahabu. Kwa hiyo, naomba kwenye vituo hivi muweke mitambo yote ya kuweza kukodisha ili wachimbaji wadogo waweze kupata huduma hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nilimwomba Mheshimiwa Waziri wa Nishati kwamba kwenye kituo changu cha Itumbi ambako anaweka hii Center of Excellence wapeleke umeme kwenye awamu hii ya tatu ya REA. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri wa Nishati apeleke umeme kwenye kituo hiki cha Itumbi ili wachimbaji wadogo wadogo waweze kunufaika na kituo hiki ambacho mnawachimbia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuishukuru Serikali na Wizara, wamenijengea mtambo wa kuchakata na kuvunja miamba na mawe kwenye Kituo cha Matundasi ili kuwasaidia wachimbaji wadogo wadogo. Naishukuru sana Serikali, naomba mwendeleze mpango huu kwa sehemu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya nzima ya Chunya, hata kwenye nyumba ya Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya ni leseni za utafutaji. Wilaya nzima ya Chunya imejaa leseni za utafutaji ambapo wenye leseni hizo wako Dar es Salaam, siyo wachimbaji wadogo wadogo wa Chunya. Leseni yake ikiisha kwa mujibu wa sheria, huyu mtu anakwenda Wizarani kama anarudisha nusu, lakini hairudishi, anaomba kwa kutumia kampuni nyingine ya mtoto wake au ya mjomba wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Wizara kwa huu moto mlioanza nao, kupitia Tume ya Madini, mpitie upya leseni zote katika Wilaya ya Chunya. Kuna watu ambao wana leseni ya utafutaji kutoka mwaka 2007/2008 mpaka leo anayo yeye mwenyewe, wakati sheria inasema ikifika miaka minne hujapata chochote, unarudisha nusu kwa Kamishna wa Madini, unabaki na nusu, hawajafanya hivyo. Naiomba sana Wizara ipitie upya kupitia Tume ya Madini ili leseni hizi zirudishwe wapate wachimbaji wadogo wadogo waweze kujiongezea kipato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana hili lifanyike kwa sababu kuanzia Chunya Mjini kwenda Makongolosi, Malangamilo kwenda Ngwala mpaka Mbikatoto, maeneo yote hayo ni leseni za utafutaji na waliokamata leseni hizo ni wajanja ambao wako Dar es Salaam (speculators), wana- speculate kwamba atapata lini. Naomba sana Serikali ilishughulikie suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri Mkuu alikuja Chunya nawe ulikuwepo, nashukuru sana kwa ziara ile. Mlitembelea kampuni fulani ya uchimbaji ambayo mliona inatii sheria, hata hii Sheria mpya ya Madini ya 2017 kampuni hiyo inatii. Hiyo kampuni ikaomba iwemo kwenye mchakato wa kujenga smelter nchini. Naomba sana Wizara hii ya Madini iifikirie kampuni hiyo ambayo iko Chunya ili smelter ya kuweza kuchakata makinikia ijengwe Chunya ili yasiende nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee pia ruzuku kwa wachimbaji wadogo wadogo. Wizara imeanza na ni jambo jema sana. Kwangu Chunya mmetoa kwa wachimbaji wawili, watatu, naomba Wizara iendelee kutoa ruzuku kwa wachimbaji wadogo zaidi ili waweze kuinua kipato cha nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia kwenye hoja hii ambayo iko mbele yetu. Napenda kuwapongeza Mheshimiwa Waziri na Manaibu Waziri, Katibu Mkuu, Watendaji wote kwa kuitayarisha hoja hii vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, nataka niongelee zao la tumbaku peke yake. Nchi ya Malawi ilikuja Tanzania kuja kuomba mbegu ya tumbaku mwaka 1966, ilichukua mbegu kwetu, sasa hivi Malawi wanazalisha tumbaku karibu kilo milioni 200; sisi ambao walichukua mbegu kwetu tumewahi kufika mwaka 2010, tulifika kilo milioni 120, sasa mwaka huu tunategemea kilo milioni 54 kutoka kwenye milioni 120 mpaka kilo 54. Kuna tatizo gani? Kwa nini uzalishaji unashuka namna hii wakati ardhi tunayo Watanzania? Watu ni walewale na watu tunaongezeka?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ningetegemea kwamba, uzalishaji ungekuwa unaongezeka, uzalishaji unashuka, ina maana kuna tatizo tena tatizo kubwa. Namuomba sana Mheshimiwa Waziri na timu yake, naomba tutumie Chuo Kikuu cha Sokoine, tutumie SUA; wenzetu Afrika hii, wenzetu duniani wanatambua umuhimu wa wataalam waliopo hapo Sokoine. Wanawaita, wanakwenda Ethiopia, wanakwenda Southern Africa huku kwenda kutoa taaluma yao. Naomba tutumie Chuo Kikuu cha Sokoine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano kuna miradi mingi ambayo huko Wizarani wamepata fedha kwa mfano Miradi ya Sumu Kuvu ambayo wameipata. Wawatumie wataalam wa Chuo Kikuu cha Sokoine ili tuweze kujua kwenye tumbaku kuna tatizo gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zao la tumbaku mwaka huu, Mheshimiwa Waziri anajua, kuna makampuni ambayo, tuna makampuni kama manne au matano ambayo yananunua tumbaku hapa nchini. Kampuni moja imeamua kujitoa, nadhani limetoa nia ya kujitoa, kwa hiyo, hawajatoa makisio mpaka sasa. Kwa hiyo, kuna Vyama vingi vya Msingi Wilayani Chunya, Tabora, Mpanda, Songea ambavyo havina kwa kuuza tumbaku ya mwaka kesho. Mheshimiwa Waziri anajua, naomba isije ikawa korosho ya pili, naomba Mheshimiwa Waziri achukue hatua stahiki tupate kampuni nyingine za kuja kununua tumbaku kwa wakulima ili tuweze kuinua kipato cha wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii adimu ili na mimi niweze kuchangia hoja hii iliyo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupanga ni kuchagua. Naona Serikali yetu imejipanga vizuri, imechagua vipaumbele ambavyo vitasukuma gurudumu la maendeleo la nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kitabu hiki cha Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, ukurasa wa 31 namba (xi), kwa ruhusa yako, naomba nisome anasema; “Aidha shughuli za kiuchumi pia zimeongezeka; vilevile, ujenzi wa mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia nguvu za maji Mto Rufiji - MW 2100.” Hili ni jambo hili ni zuri sana kwa sababu nishati ndiyo dereva mkubwa wa maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshauri Mheshimiwa Waziri kwamba Tanzania imebarikiwa kuwa na vyanzo vingi sana vya nishati, naomba aangalie huko. Ukichukua chanzo cha joto ardhi katika Rift Valley, Kenya ina potential ya kuwa na MW 1000 mpaka 1500, Tanzania tuna potential ya kuwa na MW 5000 kwa joto ardhi. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri badala ya kuangalia tu kwenye maji na sehemu nyingine, aangalie kwenye joto ardhi ili tuweze kuwa na nishati ya kutosha kuweza kuendesha viwanda vyetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja upande wa udhibiti wa matumizi ya fedha za umma, ukurasa wa 42 ameandika pale kwa ruhusa yako nasoma; “Kuhakikisha thamani halisi ya fedha inazingatiwa katika ununuzi wa bidhaa, huduma na kandarasi za ujenzi kwa kuzingatia misingi ya Kanuni za Ununuzi wa Umma kama Force Account.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ndiyo pana mgogoro. Inaonekana kwenye unit ya uzalishaji tuna kawaida ya kumuangalia Mhasibu, Mkaguzi wa Hesabu (Auditor) na General Manager, hatumwangalii mnunuzi na hapa ndiyo kuna hasara kubwa sana. Hatumwangalii mnunuzi kwa kumpa mafunzo ya kutosha na hatumwangalii kwa makini hasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe mfano, sasa hivi Serikali imeamua kutoa fedha za kujenga Vituo vya Afya, Serikali ikatumia ujanja mzuri sana wakawaambia Halmashauri fungueni account tofauti, twende kwenye manunuzi tofauti, wakafungua Force Account, fedha imetumika vizuri sana, ina maana kuna tatizo kwenye ununuzi. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali angalieni kada (profession) ya ununuzi muifundishe na kuiangalia vizuri ili tusipoteze fedha za umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakwenda kwenye ukurasa wa 46 kuhusu ujenzi wa mazingira wezeshi kwa uendeshaji wa biashara na uwekezaji, kwa mfano, reli na nishati. Wazo la kujenga Standard Gauge Railway ni zuri sana, litasaidia kwenye bandari yetu na biashara na nchi jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiangalia kwenye kitabu hiki, Mheshimiwa Waziri amesema reli hii inatoka Dar es Salaam kwenda Tabora, Tabora kwenda Mwanza, Tabora kwenda Kigoma na Isaka kwenda Rwanda. Naona Mheshimiwa Waziri amesahau ya Uvinza kwenda Msongati. Naomba tuiangalie sana reli hiyo, kwa sababu nchini Burundi kuna madini mengi sana, kuna nicol, platinum ambapo reli hiyo italeta biashara kubwa sana Tanzania. Kwa hiyo, naomba kama Burundi haina fedha, basi Serikali i-invite Burundi, m-negotiate naye ili reli hii ya kutoka Uvinza kwenda Msongati na kwenda Bujumbura ijengwe sambamba na hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika ujenzi wa reli kwa kuitumia bandari yetu ya Dar es Salaam, reli ya TAZARA tusiisahau, haihitaji kujengwa upya, inahitaji kuboreshwa tu ili sasa tuitumie vizuri bandari yetu ya Dar es Salaam. Tunapoiboresha reli ya TAZARA kwa kuipa umeme na kadhalika, tuangalie bandari kavu ya Inyala pale Mkoani Mbeya ili kutoka pale sasa tuiite Malawi tujenge pamoja reli ya kutoka Inyala kwenda Ziwa Nyasa kwenda Malawi kufanya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mbunge mwenzangu wa Mbeya Vijijini jana alisema nchi za Msumbiji, Namibia na Angola zinaboresha bandari zao kwa kuziangalia nchi ambazo ziko land locked za Zambia, Congo na Zimbabwe na sisi tunaangalia huko huko.

Kwa hiyo, naomba tunapojenga reli ya Standard Gauge tuboreshe reli ya TAZARA ili tuwe na reli tatu. Tutakuwa na bahati kuwa na aina tatu ya reli, tuna Standard Gauge, Metre Gauge na Cape Gauge. Kwa hiyo, mzigo wowote ule tunaweza kuumudu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili naomba nimshauri Mheshimiwa Waziri, tunaponunua engine na mabehewa ya Standard Gauge, tununue mabehewa na engine ambazo ni adjustable ambazo zinaweza zikatumika kwenye reli ya Standard Gauge na kwenye reli ya Metre Gauge ya TAZARA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa compliment hiyo. You have made my day na leo ni birthday yangu, nina miaka 66, ahsante sana. (Kicheko/Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoiboresha reli ya TAZARA na Reli ya Kati, naomba tuangalie vilevile uwanja wa ndege wa Songwe. Nimeona kuna sehemu nyingi kuna viwanja vya ndege, tuangalie uwanja wa ndege wa Songwe ambao uko kimkakati sana kwa nchi za Kusini na Mikoa yote ya Kusini. Uwanja ule umekamilika, ni mzuri, lakini bado tu uzio, taa za kuongezea ndege, kumalizia na jengo la abiria. Naomba Mheshimiwa Waziri aangalie uwanja huu tuukamilishe ili uweze kuleta value for money kwa biashara za Mikoa ya Kusini na nchi za jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna mtandao mkubwa wa barabara ambao uko kwenye kitabu hiki. Naomba tunapojenga barabara hizi ambazo ni driver kwa uchumi wetu, tuiangalie sana barabara ya mchepuko ya kutoka Inyala kwenda kuingia kwenye barabara Kuu ya Tanzania - Zambia pale Mbalizi. Sasa hivi kwa barabara hii inapopita Mkoani Mbeya kuna congestion kubwa sana, kwa hiyo, kuna kupoteza muda mrefu sana. Naomba tuiangalie barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, lakini nakushukuru sana kwa kunipa compliment ambayo you have made my day, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja hii iliyo mbele yetu. Napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake hii nzuri sana, ya kitaalamu. Pia napenda niwapongeze Mawaziri wa Nchi, Mheshimiwa Jenista Mhagama na Mheshimiwa Angellah Kairuki, Naibu Mawaziri Mheshimiwa Antony Mavunde na Mheshimiwa Stella Ikupa, Makatibu Wakuu Bibi Maimuna Tarishi, Bwana Andrew Massawe na Bibi Dorothy Mwaluko, hotuba yenu hii ni ya kitaalamu sana, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ruhusa yako, naomba kunukuu sehemu chache sana, ukurasa wa sita ambapo hotuba inasema: “Mheshimiwa Spika, katika mpango wa maendeleo na bajeti ya 2019/2020, Serikali itaendelea kutekeleza Mradi wa Umeme wa Maji yam to Rufiji, ujenzi wa miundombinu ya reli ya kisasa, barabara pamoja na kukuza sekta ya anga. Utekelezaji wa miradi hiyo ya miundombinu wezeshi ya kiuchumi una lengo la kufungamanisha ukuaji wa sekta hizo na sekta nyingine hasa hasa za biashara, kilimo na utalii”.

Mheshimiwa Naibu Spika, kukuza sekta za miundombinu ni kukuza uchumi. Nchi ya Tanzania imebahatika kuwa na bandari nyingi na tumezungukwa na nchi nyingi ambazo hazina bandari. Tumezungukwa na nchi za Malawi, Zambia, Congo hasa upande wa Mashariki, Burundi, Rwanda na Uganda na Jamhuri ya Kati ambazo hazina bandari. Kwa hiyo, bahati hii ambayo ametupa Mwenyezi Mungu kuwa na bandari tuitumie vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimefurahishwa sana kwamba Serikali sasa inaboresha bandari zote, imeanza na bandari ya Dar es Salaam, inakwenda bandari ya Tanga na bandari ya Mtwara na kujenga bandari mpya hapo Bagamoyo. Tunapozitumia bandari hizi, tujue kwamba kuna wenzetu nao ambao wana bandari, Msumbiji wana bandari ya Beira, Afrika Kusini wana bandari ya Durban kubwa sana, Angola kuna bandari ya Luanda, zote hizi zinaangalia nchi hizi ambazo ziko landlocked. Kwa hiyo, naomba tunapoziboresha bandari zetu tujue kwamba kuna ushindani wa kibiashara, wataalamu wetu wahakikishe wanaweka vivutio vizuri vya kuweza kuzivutia nchi hizi zije kupitisha mizigo yao kwenye bandari zetu kuliko bandari za wenzetu, tulitilie maanani sana suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukichukua reli ya kati, hii mpya ambayo inajengwa ya Standard Gauge, tulikuwa tunakazania sana kutoka Dar es Salaam, Tabora, Isaka kwenda mpaka Kigali ambako na nchi ya Rwanda nayo inajenga kipande kile kule na hii inayokwenda mpaka Kigali inalenga mizigo ya Rwanda, Uganda na Jamhuri ya Kati. Nchi ya Burundi ina madini ya platinum zaidi ya tani milioni 6,7,8, sasa reli yetu tukitoa Uvinza, Msongati tuongee na nchi ya Burundi na yenyewe ijenge kutoka Bujumbura kuja Msongati, tuongee na nchi ya Congo ijenge reli kama hii kutoka bandari ya Uvira ije mpaka Bujumbura ili tuweze tuweze kuidaka ile mizigo ya Congo kwani ina madini mengi sana. Tukiacha sisi wenzetu wa Angola watajenga reli kutoka Rwanda kuja Lubumbashi au Lusaka.

Kwa hiyo, naomba sana tulenge mizigo ya Congo, Burundi na Jamhuri ya Kati kwa sababu reli yetu hii ya Standard Gauge itakapokuwa tayari ina uwezo wa kubeba tani karibu milioni 20 za mizigo kwa mwaka, naomba tulenge kuelekea huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na reli hii ya kati ya Standard Gauge, nimefurahishwa sana bado Serikali inaendelea kuikarabati hii reli ambayo ipo sasa hivi ya Metre Gauge. Kwa hiyo, hapa kati tutakuwa na reli mbili, Reli ya Standard Gauge na Metre Gauge. Mwaka jana nilisema kwamba tunaponunua rolling stock tuhakikishe tunanunua rolling stock ambayo unaweza ukatumia kwa reli zote mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuna reli yetu ya TAZARA, yenyewe haihitaji kuboreshwa katika miundombinu mingi, inahitaji umeme tu. Reli ya TAZARA yenyewe ni Cap Gauge inaoana na reli za Afrika Kusini na Zambia. Naomba na hii reli tuiboreshe kwa kuiwekea umeme ili reli zetu zote tatu, Standard Gauge, Metre Gauge na hii Cap Gauge zifanye kazi za kuhudumia nchi ambazo ziko Landlocked.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo naipongeza sana Serikali kwamba imenunua meli mbili au tatu kwenye Ziwa Nyasa ambazo zinafanya biashara nzuri sana ya kusafirisha binadamu na mizigo katika nchi ya Tanzania, Malawi na Msumbiji. Naomba sasa pale Inyara tuweke bandari kavu na vilevile Serikali ifikirie kujenga sasa reli kutoka hapo Inyara kuelekea bandari ya Itungi ili tuweze kuihudumia nchi ya Malawi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu ulikuwa ni huo tu katika hotuba hii, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye hoja hii iliyo mbele yetu. Nataka kuchukua nafasi hii kumpompngeza sana Mheshimiwa Waziri, Manaibu Waziri, Makatibu Wakuu, Watendaji wote walioko kwenye Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii imechukua moja ya sita ya bajeti ya Serikali, moja ya sita, karibu trioni tano katika trioni 30, hii inaonyesha umuhimu wa Wizara hii. Wizara hii ndiyo inayoweza kutupeleka kwenye uchumi wa kati, Wizara hii ndiyo ina miundombinu yote ambayo inachochea kukua kwa uchumi. Kwa hiyo, naomba Wizara hii wajue kwamba wanadhamana kubwa sana ya kuivusha nchi hii kwenda kwenye uchumi wa kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaongelea vipengele vitatu, vinne, cha kwanza niongelee Bandari, naipongeza sana Serikali kwa kuamua kuboresha Bandari zetu, Bandari ya Dar es Salaam, Bandari ya Mtwara, Bandari ya Tanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kiongozi mmoja wa nchi jirani amewahi kutania, akasema, Tanzania nipeni Bandari ya Dar es Salaam niiendeshe, nitawapeni bajeti yenu yote. Hakuwa anatukejeri, ana maana kwamba, kwa jinsi ya uchumi wa jiografia ulivyo, Bandari zetu zimekaa kimkakati sana. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali kwa kuziboresha bandari hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali, Wizara, tusiboreshe miundombinu peke yake, tuboreshe na huduma. Wizara hii imejaa wasomi wengi waliobobea, wana taaluma, tufanye utafiti, tuangalie je, kwenye bandari ambazo tunashindana nazo, Mombasa, Beila, Duban, vitu gani ambavyo wafanyabishara wanakimbilia kule ili na sisi tuviboreshe kwetu? Kwa hiyo, naomba tusiboreshe miundombinu peke yake, tuboreshe na huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee reli. Naishukuru tena vilevile Serikali kwa kujenga reli mpya Standard Gauge na kuboresha reli ya zamani Miter Gauge, naishukuru sana. Naishauri Wizara kila inapowezekana wanunue rolling stock ambayo unaweza ukatumia kwenye reli zote ili kuweza kupunguza gharama. Wanunue rolling stock ambayo unaweza ukatembeza kwenye Standard Gauge na vilevile rolling stock ambayo unaweza ukatembeza kwenye Meter Gauge na vilevile hata unaweza kutembeza kwenye Cape Gauge kwa reli yetu ya TAZARA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii reli ya kati Standard Gauge ikitumiwa vizuri inaweza kubeba tani ya mizigo zaidi ya milioni 20 kwa mwaka na hapo ndiyo itachochea kukua kwa uchumi wetu. Sasa nimefurahi sana kuona kwenye bajeti ya mwaka huu Mheshimiwa Waziri amesisitiza reli hii ya kutoka Uvinza kwenda Msongati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Msongati Burundi kuna Nickel zaidi ya tani milioni tano, tuna Platinum zaidi ya tani milioni sita, saba, reli hii itabeba mizigo hiyo. Namshauri Mheshimiwa Waziri aanze kuwa-engage Mawaziri wenzake wa Burundi na Kongo ili reli ya ina hiyo ijengwe kuto Msongati kwenda kwenye bandari ya Uvira. Hapo tutakuwa tume- capture mizigo ya Burundi na mizigo ya Kongo, wakati hii ya kutoka Isaka kwenda Kigali ina-capture mizigo ya Rwanda na mizigo ya Central African Republic. Umuhimu wa reli hii ni katika kubeba mizigo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee reli ya TAZARA. Reli hii inahitaji maboresho madogo sana, lakini shida ya reli ya TAZARA nadhani ni sheria. Reli hii ilijengwa na Serikali ya Awamu ya Kwanza, lengo lilikuwa kuisaidia Zambia ambayo ilikuwa Landlocked wakati tunapigania uhuru wa nchi za Kusini mwa Afrika, ilikuwa ya muhimu mno, lakini leo inaonekana kwa majirani zetu reli hiyo haina umuhimu, ndiyo maana inatusumbua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri aiangalie sheria na mkataba kwa reli hii ili ikiwezekana alete sheria hapa Bungeni tuweze kuirekebisha iende na wakati ambao tunautaka kwa sababu Tanzania tunaitaka kwa kukuza uchumi wetu. Wenzetu sasa hivi wanategemea Bandari ya Durban na Bandari ya Beira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nakuomba sana Mheshimiwa Waziri aiangalie sheria ailete Bungeni tuweze kuiboresha kwa manufaa ya Tanzania zaidi. Ilikuwa kwa manufaa ya wenzetu, naona wenzetu hakuna umuhimu, sasa tuiboreshe kwa manufaa ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hilo hilo la reli ya TAZARA pale Inyara, Mheshimiwa Mbunge wa Mbeya Vijijini anaiongelea sana. Naiomba Serikali iweze kujenga pale bandari kavu ili mizigo ifike pale, ili baadaye tuweze kujenga reli kutoka Inyara kwenda Itungi Port kwa ajili ya mizigo ya Malawi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alifanya ziara nchini Malawi hivi karibuni. Namshukuru sana, maana yake ziara yake hiyo imerudisha mahusiano ya kibiashara kati ya Tanzania na Malawi kwenye reli nzuri. Ninamshukuru sana. Akiwa huko pamoja na Rais mwenzie walishauri kwamba Mawaziri waunde tume ya mashirikiano ya pamoja. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri anayehusika waunde haraka tume hiyo kwa sababu Awamu ya Kwanza iliisaidia sana Malawi, ilijenga Cargo Centers; Dar es Salaam, Cargo Centers, Mbeya, lakini hizo Cargo Centers hazifanyi kazi. Kwa hiyo, biashara kati ya Tanzania na Malawi imekufa kinyemela nyemela.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Serikali ifufue hizo Cargo Centers haraka ili biashara kati ya Tanzania na Malawi iweze kuendelea kama kawaida. Kuna wenzetu nchi za majirani ambao bandari zao zimepata msuko msuko kidogo. Kwa hiyo, naomba bandari zetu zichukue hiyo kama ni opportunity ili kuweza ku-capture biashara hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee barabara kidogo. Mheshimiwa Rais akiwa Mkoani Mbeya aliongelea barabara ya mchepuko, kutoka mlima Nyoka kwenda Mbalizi, aliongelea na uwanja wa ndege wa Songwe na aliona umuhimu wa barabara hiyo, maana yake aliona msongamano uliopo Mbeya Mjini ni mkubwa sana. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa aweke umuhimu sana kwa barabara hiyo ya mchepuko ya kutoka Mlima wa Nyoka kwenda Mbalizi na vilevile kuboresha barabara ya kati ambayo sasa hivi ina lane mbili aiboreshe iwe lane nne kuweza kupunguza msongamo pale Mbeya Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ziara ya Mheshimiwa Rais nilibahatika sana, Mheshimiwa Rais alifika Chunya kufungua barabara ya Mbeya - Chunya na pia kuweka jiwe la msingi barabara Iinayojengwa sasa hivi kwa kiwango cha lami ya kutoka Chunya kwenda Makongorosi. Wananchi wa Chunya wanamshukuru sana Mheshimiwa Rais, wanamshukuru sana Mheshimiwa Waziri na wanawashukuru sana Watendaji wote wa Wizara hii ya Ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ziara hiyo Architect Mwakalinga na Engineer Mfugale nilikuwa nao pale tukanywa nao chai, waliiona barabara hiyo ambayo wamenizawadia, lakini pale mlimani waliona kuna matundu mawili, matatu ambayo yanachafua barabara hiyo ambayo ni nzuri sana ambayo kwetu sisi ni mboni ya jicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Architect Mwakalinga na Eng. Mfugale watununulie weighbridge, hata kama ni mobile weighbridge kwa sababu huko Chunya tuna mazao mengi ya misitu, tuna mazao mengi ya tumbaku. Wafanyabiashara huwa wanaweka malori makubwa ya lumbesa usiku, wanapita kwenye barabara hiyo wanaiharibu, wakifika Mbeya ndiyo wanagawa kwenye malori mawili matatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawaomba sana hawa Mainjia wanisaidie sana, watusaidie Chunya, watununulie hata mobile weighbridge kuweza kuiokoa barabara hii idumu kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami nichangie kwenye hoja iliyopo mbele yetu ambayo imewasilishwa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha. Nampongeza sana, amewasilisha vizuri sana utekelezaji wa Mpango wa mwaka 2018/2019 na Mapendekezo ya 2021. Hongera sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kwenye uso wa dunia wanadamu tuko zaidi ya bilioni saba; na kadri miaka inavyosogea kwenda mbele, wanadamu tutazidi kuongezeka sana. Wanafalsafa wanasema, vitu ambavyo vitakuwa adimu sana miaka ijayo kwa kuanzia ni viwili; maji na chakula. Kwa hiyo, wanaendelea Wanafalsafa wanasema, mtu anayetaka kuwa tajiri miaka 20 ijayo, aingie kwenye kilimo leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naipongeza sana Serikali kwa kuweka kipaumbele kwenye uchumi wa viwanda. Naipongeza sana. Naomba kwa kuwa Tanzania tuna ardhi kubwa sana na nzuri sana, tuna mito na mabonde, naomba tuupe kipaumbele sana uchumi wa viwanda kwenye kilimo. Tuige mfano wa kile kiwanda cha sukari ambacho kitajengwa hapo Morogoro. Tuige, tuwe na uchumi wa viwanda kupitia kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna vyuo vya kilimo vingi sana. Tuna Chuo Kikuu cha Kilimo SUA ambacho kina wataalam wabobezi wengi sana ambao wanaheshimika Afrika na dunia nzima. Afrika ya Kusini wanawapenda sana wataalam wanaostaafu kutoka hapa SUA. Naomba Serikali iwatumie wataalam hawa. Tuwachukue, tuwafungie ndani, watupe Blueprint ya namna gani tutatumia ardhi yetu hii tuweze kupata mazao ya kilimo na kuweka viwanda vya kuchakata mazao yetu. Naiomba sana Wizara ya Kilimo, Wizara ya Uwekezaji, Wizara ya Viwanda, Wizara ya Fedha tuwatumie sana hawa wataalam wetu wa Chuo Kikuu cha SUA waweze kutupa Blueprint ya namna ya kutumia ardhi na maji yetu tuliyonayo tuweze kujikomboa kwa viwanda kuanzia kwenye kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwenyezi Mungu tena ametupa neema ya bandari. Naipongeza sana Serikali, sasa hivi Serikali inaboresha Bandari ya Dar es Salaam, Mtwara na Tanga. Bandari zetu hizi zinahudumia nchi karibu nane au tisa za Uganda, Rwanda, Burundi, Congo, Zambia, Zimbabwe, Malawi na zinginezo. Kwa hiyo, naomba uboreshaji huu tunaokwenda nao ulenge kushindana na bandari zingine ambazo ziko kwenye ukanda wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umeona nchi jirani hapa juzi imeona Bandari ya Dar es Salaam inaboreshwa na mizigo mingi inapitia Bandari ya Dar es Salaam wakapunguza ushuru kwenye mafuta ili tuweze kushindana. Kwa hiyo, naomba uboreshaji huu wa bandari uendane na kujipanga sawasawa kwa kushindana na nchi ambazo tuanshindana nazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliona mwaka au miaka miwili iliyopita Bandari ya Dar es Salaam TPA waliweka ofisi yake kwenye nchi jirani ya Congo, jambo zuri sana. Hii inasaidia kufanya marketing ya shughuli zetu. Naomba hii iendelee kwa nchi nyingine zote ambazo tunazihudumia kibandari, tuweke ofisi zetu kule ili tuweze kuwahudumia, tuweze kushindana na wenzetu ambao tunashindana katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona vilevile kwenye mpango, Serikali inaendeleza ujenzi wa reli ya kati (Standard Gauge), inaendeleza kuboresha reli iliyopo ya meter gauge na vilevile ina mpango wa kuanza kujenga Standard Gauge ya kutoka Dar es Salaam kwenda Mtwara na kutoka Tanga kwenda Arusha mpaka Musoma, ni jambo zuri sana hilo. Hii Standard Gauge ya reli ya kati mwisho wa mwaka huu itakamilika kutoka Dar es Salaam mpaka Morogoro na inaanza Morogoro kuja Makutupora na itaendelea huko mpaka Tabora – Mwanza – Kigoma. Wenzetu nchi jirani ya Rwanda imeingia kwenye bandwagon hii, imeamua nayo kutafuta njia za kujenga kutoka Kigali kuja mpaka Isaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali sasa tui- entice Burundi nayo iingie kwenye mpango huu ili na wao wajenge kutoka Msongati kuja mpaka Uvinza halafu wajenge kutoka Msongati – Uvira kwenye nchi ya Congo. Hii reli ya SGR ili ilete faida kubwa kwa nchi yetu inahitaji kusafirisha mizigo zaidi ya tani milioni 20 kwa mwaka. Sasa tusipoitumia nchi ya Congo, itakuwa ni hasara. Kwa hiyo, naomba Serikali tuwa-engage Burundi nao waweze kutafuta fedha wajenge kutoka Msongati mpaka Uvinza na kutoka Msongati kwenda Uvira katika nchi ya Congo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuboresha hii SGR na meter gauge, ipo hii reli ya TAZARA ambayo yenyewe ni cape gauge. Naomba ili tuweze kuitumia vizuri bandari yetu tuiboreshe reli hii ya TAZARA na katika kuiboresha hii inahitaji tu kuiwekea umeme ili treni ziende kwa kasi. Naomba tuiboreshe reli hii na vilevile Serikali iwe na mpango wa kujenga Bandari Kavu pale Inyara ambapo tumekuwa tunaiongelea mara kwa mara. Bandari kavu ikiwepo Inyara unaweza kujenga reli ya mchepuko kutoka pale Inyara ikaenda mpaka Lake Nyasa tukatumia vizuri meli ambazo Serikali imezinunua kusafirisha mizigo kutoka Bandari ya Dar es Salaam kwenda Malawi na Msumbiji. Kwa hiyo, naomba reli ya TAZARA na yenyewe iwemo katika mpango huu wa kutumia reli zetu na uchumi wetu wa jiografia kuweza kujiletea maendeleo hapa Tanzania na kuwahudumia jirani zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yangu yalikuwa hayo machache, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Spika, nakushuru sana kwa kunipa fursa ili niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ambayo ipo mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, napenda kuungana na wenzangu kumpongeza Mheshimwa Waziri Mkuu kwa kuwasilisha hotuba yake ya bajeti kwa umahiri mkubwa sana. Pia napenda kuungana na wenzangu kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa ambayo amefanya kwa miaka minne hii. Serikali hii mtu atabeza atafanya nini lakini kazi waliyofanya ni wamefanya mapinduzi. Mapinduzi ambayo mtakapomaliza hii kazi nchi yetu hii itaingia kwenye uchumi wakati. Mungu awabariki muendelee kupiga mzigo namna hiyo.

Mheshimiwa Spika, pia naomba niungane na wenzangu kwanza kukushukuru wewe, pamoja na uongozi wote wa Bunge, Naibu Spika, Katibu wa Bunge na viongozi wengine, kwa tahadhari ambayo mmeichukua hapa Bungeni kuhusu ugonjwa huu wa corona, nawashukuru sana sana. Mmetukinga Wabunge na Wafanyakazi wa Bunge, tuchukue tahadhari kubwa kwa sababu ugonjwa huu upo.

Mheshimiwa Spika, pili, napenda kuishukuru Serikali, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano, Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Waziri wa Afya kwa maelekezo ambayo wanatupa na wanawapa wananchi kuhusu ugonjwa huu, nawashukuru sana. Nawaomba wananchi wa Chunya, wananchi wa Mkoa wa Mbeya na Watanzania, tufuate maelekezo ambayo viongozi hawa wanatupa. Tuyafuate kweli kweli uongojwa huu upo na unaua. Nawaomba sana yote ambayo wamesema tuyatuate kwa umakini sana.

Mheshimiwa Spika, nataka katika hayo ambayo viongozi wetu wametupa niongeze kimoja kidogo nacho nisimu ya mkononi. Nawaomba sana simu ya mkononi kuanzia sasa ibaki yako wewe mwenye simu usiseme shika mwenzangu shika kidogo angalia clip hii hapana, ibaki kwako mwenyewe kwa sababu nayo inaweza kuwa njia ya kuambuakiza. Unaponawa mikono unatumia sanitizer chukua kitambaa cheupe safi na simu uisafishe kwa sababu nikwambie mimi nakuapia Watanzania tungekuwa tunashika dini zetu kama tunavyoshika simu, moto wa huko ungeishia kuchoma mahindi, nakwambia kweli kabisa. Kwa hiyo naomba niongezee hapo kwamba tuwe makini sana na simu, simu yako ibaki yako, usimpe mwenzie, aangalie clip au apige salio limeisha, ubaki nayo na uisafishe mara kwa mara.

SPIKA: Waheshmiwa Wabunge mmemsikia Senator ushauri wake? Simu ibakie yako na watanzania pia kwa ujumla hasa wanawake wanapenda simu za wenzao. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwambalaswa endelea.

MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunisaidia na kuniongezea uzito kwenye hoja hii. Nikiongelea hilo la simu Mheshimiwa Rais wetu katika ushauri wake ameongezea kwamba tutubu kwa Mwenyezi Mungu, tumfuate Mwenyezi Mungu tutubu dhambi zetu. Ukiona huko Italia wanateseka sasa hivi, wanaoana wanaume kwa wanaume, mtu jitu zima linamwingia mtoto wa miaka mitato wakati watu wakubwa wapo chungu nzima, ni dhambi ambazo Mungu amekasirika.

Mheshimiwa Spika, naomba uniruhusu nikiwa katika hilo niende kwenye kitabu cha Mungu. Nachukua Biblia watu nasikia wanasema bibilia, hapana, ni Biblia, katika wafalme wa zamani mfalme wa zamani mwana wa Daud. Baada ya kutawazwa kuwa mfalme alifanya vitu vingi vizuri unique.

Mheshimiwa Spika, cha kwanza alienda kuteketeza sadaka kumshukuru Mwenyenzi Mungu na Mungu akaongea naye akamwambia nikupe nini? Akamwambia unipe maarifa na uelewa ni waatawale watu wako vizuri. Hakuomba nguvu za kijeshi hakuomba utajiri, Mwenyenzi Mungu kampa vyote kampa hekima, kampa nguvu za kijeshi kampa na utajiri.

Mheshimiwa Spika, cha pili, alimjengea Mungu nyumba nataka nianzie hapo. Sasa ukienda kwenye kitabu cha Mambo ya Nyakati wa pili nianzie sura ya saba, aya kumi na moja baada ya Suleiman kumjengea nyumba Mungu. Hivyo basi, Suleiman akaimaliza nyumba ya bwana na nyumba ya mfalme na yote yaliyomwingia Suleiman moyoni mwake ayafanye mwa bwana. Bwana akamtokea Suleiman usiku akwamwambia nimesikia uliyoyaomba na mahali hapa nimejichagulia kuwa nyumba ya dhabihu anasema Mungu sasa na Suleiman.

Nikizifunga mbingu isiwe mvua, tena nikiamuru nzige kula nchi au nikiwapelekea watu wangu tauni kama corona nikiwapeleka watu wangu tauni ikiwa watu wangu walioitwa kwa jina langu watajinyenyekesha nakuomba na kunitafuata uso na kuziacha njia zao mbaya, basi nitasikia toka mbinguni na kuwasamehe dhambi yao na kuiponya nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba tumuunge Mheshimiwa Rais ametuambia hili tumrudie Mungu tuache dhambi ugonjwa huu utapita. Baada ya hilo naomba ningelee hilo ambalo wachimbaji wangu wa dhahabu wadogo wadogo wa Chunya wamenituma.

Mheshimiwa Spika, kwanza wachimbaji hawa wanaishukuru sana Serikali kwa kuweka soko la dhahabu pale Chunya, soko lipo vizuri, linaenda vizuri, wachimbaji wanapata pesa yao, Serikali inapata pesa yake na halmashauri inapata pesa yake. Sasa hii tafrani ambayo imetukuta sasa hivi wachimbaji wadogo wamekaa na dhahabu mkononi hawana kwa kuuza kwa sababu broker wa pale Chunya ni wale wenye mitaji midogo midogo na kwa kuwa sasa hivi ndege haziendi nje, kwa hiyo kwamba anunue dhahabu akauze Dar es Salaam arudi kununua tena hawana uwezo huo. Naiomba Serikali iingilie kati, hili kuna dhahabu nyingi sana zipo mikononi mwa wachimbaji wadogo wadogo naomba tuchukue hatua interim period, ijue aidha benki ziwakopeshe wale brokers au benki kuu iende kununua in the interm period ili wananchi wetu waende kufanya biashara kama kawaida.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, nimeona kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri Mkuu kufufua kilimo na ushirika. Naongelea ushirika kwa kifupi, nimeshukuru sana nilipoona Serikali imemtuma TAKUKURU kwenda kukagua ushirika nchi nzima, nimefurahi sana. Kwa sababu ushirika ndio umeua kilimo upo wapi ushirika wa zamani KNCU, upo wapi ushirika wa Nyanza Co-operative wa zamani, upo wapi ushirika wa Bukoba au wa Mbeya? Viongozi wa ushirika wameua ushirika, kwa hiyo umeua kilimo chetu. Nimefurahi sana kwamba Serikali imeliona hilo, imeanza kulishughulikia. Naomba Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na Naibu Waziri wakomae sana katika hili, vilevile kumuachia COASCO yeye ndiye anakagua ushirika, hapana, naomba akague lakini na CAG naye aende kukagua ili kujiridhisha.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Huduma ya Msaada wa Kisheria wa Mwaka 2016
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii niwe mchangiaji wa kwanza kwenye Muswada huu ambao nauona ni wa muhimu sana kwa mustakabali wa wananchi maskini wa Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka ku-declare interest, Mheshimiwa Waziri aliyeleta Muswada huu hapa Bungeni leo ni ndugu yangu mimi wa damu, ni pacha wangu lakini kwa hili natofautiana nae. Sasa hivi amekuwa Waziri karibu mwaka mmoja na mwezi, alikuwa wapi kuleta Muswada huu toka mwanzo na Mawaziri wengine waliomtangulia walikuwa wapi kuleta Muswada mzuri kama huu hapa Bungeni? Naomba nitofautiane naye ndugu yangu na Mawaziri wote waliotangulia, walikuwa wapi kuleta Muswada mzuri kama huu? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa Mheshimiwa Tundu Lissu mdogo wangu anasema hizi Taasisi za kujiandikisha amezitaja nyingi Chuo Kikuu wapi na wapi lakini kwangu mimi Chunya kijijini Taasisi hazipo, hamna Taasisi hizi Chunya kwa hiyo Mkombozi ni Muswada huu, sasa Waziri Mwakyembe alikuwa wapi nimetofautiana naye kweli kweli, ulikuwa wapi ndugu yangu?(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nitoe experience yangu kwenye masuala mawili, matatu. Kwenye uchaguzi uliopita huu, nimekwenda Kata ya Matwiga naenda kuomba kura kwa wapiga kura. Nimekuta hapo mtu ananikimbilia wa jamii ya wafugaji anasema baba yake amekamatwa amewekwa ndani na Mtendaji. Anasema umeweka mifugo yako mahali ambapo haparuhusiwi (tresspass), anasema Mtendaji, kama hukutoa shilingi milioni tano kwa mifugo yako hii nakupeleka Polisi kesho uende Mahakamani sasa dawa yake ni Muswada huu. Nilimfuata huyu Mtendaji kwenda kumuomba amuachie yule mfugaji kwa sababu mfugaji hana kosa na mfugaji hajui sheria akamtoa, hilo la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, juzi hapa niko Wilayani Chunya natekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, niko na Mkuu wa Wilaya anaitwa Bi. Rehema Madusa mchapakazi kweli huyu mama. Kuna Ma-DC ambao wanagongana na Wabunge lakini mimi na DC huyu tuko kitu kimoja. Ameniita anasema, Mbunge njoo kuna tatizo, tatizo gani? Anasema kuna wafugaji wametoka wilaya nyingine wamekuja huku, wanakula mazao ya wakulima, wameshikiana mikuki wanataka kupigana, tumeita Kikao mimi niko pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nikamwambia Mkuu wa Wilaya tatizo hapa ni Mwenyekiti wa Kijiji. Mwenyekiti wa Kijiji anawaita wafugaji njooni wekeni mifugo yenu hapa, wanampa chochote, anawaruhusu. Kumbe ardhi ile siyo ya wafugaji ni ya wakulima. Kwa hiyo, tatizo kubwa katika ugomvi ambao nimeuona hapa nchini wa wakulima na wafugaji ni aidha Mtendaji au Mwenyekiti wa kijiji. Sasa hawa wakulima wetu, wafugaji wetu sheria hawajui, huu ndiyo tiba yake, muarobaini wake ndiyo huu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakwambia vijijini kama kwangu mimi Chunya, mfugaji awe wa kabila lolote awe Msukuma au awe nani hajui sheria kabisa kabisa. Anachoambiwa na Mwenyekiti, anachoambiwa na Mtendaji ndiyo hicho hicho. Sasa huu ndiyo tiba yake hiyo. Nakushuru sana Mheshimiwa Mwakyembe umeuleta pamoja na kwamba nimekulaumu, lakini pia nakushukuru sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, haki za binadamu, Mheshimiwa Ritta leo asubuhi alikuwa analalamika anasema Mkoani Iringa watoto wadogo wanabakwa sana. Kwanza Mungu alivyomuumba mwanadamu, Mungu akatofautiana na Malaika mmoja. Huyo Malaika amekuwa Shetani. Imefika Watanzania siku hizi wanatenda mambo ambayo hata Shetani anashangaa. Unaendaje kubaka mtoto wa miaka mitatu? Shetani mwenyewe hajawahi kutenda dhambi kama hiyo, hajawahi anawashangaa wanadamu na ndiyo maana labda hata mvua tunakosa kwa sababu tunatenda mambo ambayo hata Shetani hatendi. Sasa wanaobaka watoto muarobaini wao ndiyo huo umefika. Wanawaonea wananchi, haki za binadamu, muarobaini wao umefika. Wanaowaonea akinamama kwenye mirathi muarobaini wao umefika, wanaowaonea wakulima na wafugaji kwenye ardhi yao, muarobaini wao ndiyo huu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimefurahi sana, nasema hawa watakaoteuliwa kwangu mimi, hawa wasaidizi watoa msaada bila malipo, Mawakili bila malipo; watakaokuwa kwangu Chunya nimefurahi Mheshimiwa Waziri amesema tayari wameshapata mafunzo kwa hiyo, iliyobaki ni kusajiliwa na waanze kazi. Mimi kwangu Chunya watakaoanza, nina mambo mawili; la kwanza nitaomba Kamati yangu ya mfuko wa Jimbo tuwanunulie pikipiki ya kuweza kusambaa vijijini kwenda kutoa msaada kama huu. Kama haitawezekana mfuko wa Jimbo kutoa fedha hizi, mimi nitatoa hela yangu ya mshahara niwanunulie pikipiki ili waweze kutoa msaada huo wa sheria kwa wananchi wote wanaotaka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli hata sura yangu inaonesha nimefurahi sana Muswada huu kuja sasa hivi. Naomba Wabunge wenzangu wa vyama vyote tuunge mkono upite haraka iwe sheria ili tuweze kuwasaidia wananchi ambao wananyanyaswa, wanateswa kwa sababu tu hawajui sheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana.