Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Suleiman Ahmed Saddiq (1 total)

MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nina swali moja kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa waziri Mkuu, kwa kuwa mwaka 2016 miezi kama hii kulitokea upungufu mkubwa wa sukari nchini na Serikali ya Awamu ya Tano ilifanya jitihada kubwa sana kukabiliana na hali ile na hatimaye nchi yetu ikapata utulivu mkubwa katika suala zima la sukari.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba nikupongeze wewe na Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa mliyofanya mwaka 2016 katika suala zima la upungufu wa sukari nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa kipindi hiki, viwanda vyetu vya ndani vinakamilisha msimu, vingine vinamaliza mwezi wa Tatu, vingine vinamaliza mwezi wa pili; na kwa kuwa vikikamilisha msimu, uzalishaji unaanza tena mwezi wa sita na kuendelea. Je, hali ilivyo sasa ya sukari nchini ikoje? Serikali imechukua juhudi gani kuhakikisha kwamba yale yaliyotokea mwaka 2016 hayatatokea?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saddiq, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka niwahakikishie Watanzania kwamba hakutakuja kutokea upungufu wa sukari, kwa sababu viwanda vyetu vya ndani vilishaanza uzalishaji na sasa vinaendelea na uzalishaji. Tunavyo viwanda vitano ambavyo tumevitembelea, tumehakiki utendaji kazi wake na uzalishaji upo na sukari ambayo inatumika nchini inatokana na uzalishaji huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaaamini kufikia mwishoni mwa msimu ambapo ni mwezi wa tatu mwaka huu wa 2017 tunaweza kuwa tumezalisha na kufikia malengo. Kwa sababu kwa taarifa za mwisho, mpaka mwishoni mwa Januari, uzalishaji kwa malengo waliokuwa wamejiwekea wamefikia asilimia 86. Asilimia iliyobaki inaweza kuzalishwa kwa kipindi kifupi kilichobaki.
Mheshimiwa Naibu Spika, na kama itajitokeza upungufu kwa sababu ya mahitaji ya sukari, pia kutozuia upandaji wa bei, Serikali itakuwa iko tayari kutafuta namna nzuri ya kupata sukari tukishirikiana na viwanda vyenyewe ikiwa ni mkakati wa kuvilinda viwanda vya ndani vinavyozalisha sukari ili viweze kuongeza uwezo wa uzalishaji wa sukari nchini. Huo ndiyo mpango wa Serikali.