Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Azza Hilal Hamad (15 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia bajeti ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kazi kubwa wanayoifanya katika Wizara hii, hongereni sana na nianze na hotuba ya Mheshimiwa Waziri ambapo katika ukurasa wa 113 anasema, naomba kunukuu; “Mikoa na Wilaya zenye maeneo tete ya chakula mwaka 2015/2016. Mkoa wa Shinyanga na Wilaya zake zote zilikuwa na hali mbaya ya chakula.”
Kwa taarifa hii tu ilikuwa inatosha kabisa kuona ndani ya kitabu cha bajeti cha Waziri, Shinyanga wameitizama kwa jicho gani. Kwa masikitiko makubwa baada ya miaka mfululizo Shinyanga kuwa na hali tete ya chakula hakuna mpango wowote ambao Serikali imeupanga kutuondoa katika hali hiyo. Ukiusoma ukurasa ule Mkoa wa Shinyanga na Wilaya na Majimbo yake yote hali ilikuwa tete. Nilitegemea basi katika bajeti hii ningeona kuna kitu tofauti. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka wa bajeti 2015/2016, Wabunge wote wa Mkoa wa Shinyanga tuligomea bajeti ya Wizara ya Kilimo na Waziri aliposimama kujibu alisema kuwa Wizara itatekeleza ahadi aliyoitoa aliyekuwa Waziri Mkuu kwenye ziara yake Wilaya ya Kahama kwamba Wilaya ya Kahama itakuwa Wilaya ya kimkakati kuuokoa Mkoa wa Shinyanga kwa kilimo kwa sababu ndiyo Wilaya pekee inayopata mvua za kutosha. Nilitegemea kuona Wilaya ya Kahama kuna jambo limefanyika, sijaona kitu chochote.
Naomba Waziri utakaposimama kuhitimisha uniambie ile ahadi iliyotolewa kwenye bajeti mwaka 2015/2016 ya kuifanya Wilaya ya Kahama kuwa ni Wilaya ya kimkakati kwa ajili ya kilimo kuokoa Mkoa wa Shinyanga iko wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wizara hii hii ya Kilimo, nilitegemea basi, Mikoa kama Mkoa wa Shinyanga ambao tunategemea maji ya juu, ningeona kuna bajeti ambayo imetengwa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji. Sijaona hata Wilaya moja kwamba tunajikwamuaje na kilimo hiki kutoka kutegemea maji ya juu na kuwa tunavuna maji; sijaona ni wapi walipoonesha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, kwa mara nyingine naiamini Serikali yangu, hebu naomba muutazame Mkoa wa Shinyanga kwa macho mawili. Hatuwezi kuwa tunasoma kwenye vitabu tu, lakini utekelezaji hauonekani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, katika Mabwawa ya Umwagiliaji, kuna bwawa ambalo lilikamilika mwaka 2015, Bwawa la Ishololo katika Jimbo la Solwa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga; lakini nasikitika kusema bwawa lile sasa hivi limeshakatika, maji yote yametoka. Kwa hiyo, kwa mwaka huu bwawa lile hatujavuna maji. Sasa hawa wakulima tunaotegemea kwamba tumewatengenezea bwawa na hatimaye waweze kulima kwa umwagiliaji, bwawa hili limekatika na maji yote yametoka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia kusema kwa mara nyingine, nilishasema tuna miradi mingi ya umwagiliaji, naomba tuitengenezee mikakati miradi hii iweze kuhifadhi maji kwa wingi ili tuwe na kilimo chenye tija. Naomba nipate maelezo, miradi yetu ya umwagiliaji kwa nchi nzima, Wizara ya Kilimo mmejipanga vipi kuhakikisha miradi hii inavuna maji ya kutosha na kuwa na kilimo cha umwagiliaji chenye uhakika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwa na Mikoa au Wilaya ambazo hazina mvua za kutosha isiwe sababu ya kutuadhibu tunaotoka katika maeneo yale, kwa sababu inavyoonekana wale wanaopata mvua mara mbili kwa mwaka ndio pia wanaotengewa fedha nyingi katika mradi wa kilimo. Naomba mtutazame, mwone tunawezeje kutoka hapo tulipo na kuweze kuwa na chakula cha kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niingie kwenye mifugo. Nasikitika kwa mara nyingine, Mkoa wa Shinyanga tulikuwa na Kiwanda cha Kusindika Nyama. Kiwanda hiki mpaka leo hakifanyi kazi, kiwanda hiki kilibinafsishwa. Mheshimiwa Waziri naomba uniambie, toka mlipobinafsisha kiwanda hiki, mpaka sasa hivi kuna hatua gani? Maana zimekuwa ni hadithi. Kitaanza kazi mwezi ujao, kitaanza kazi kesho kutwa, hatuoni kazi inayofanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Shinyanga tuna ng‟ombe wa kutosha, lakini ng‟ombe hawa wamekuwa wakinunuliwa kwa bei ya chini kusafirishwa kwenda Dar es Salaam, hali ambayo inawafanya wafugaji wetu kutokufuga kwa ubora na kupata fedha ambayo haistahili kwa mifugo yao. Mimi nadhani ni muda muafaka sasa, tuangalie kwa maeneo ya wafugaji, basi viwepo viwanda ili mifugo hii iweze kuwa na thamani. Nilikwishawahi kusema, hata kwenye minada ambako ng‟ombe zetu zinanunuliwa, basi kuwepo na utaratibu wa kuweza kuuza mifugo hii iwe na thamani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu huo naomba basi na naishauri Serikali angalau ng‟ombe hawa wawe wanapimwa kwa kilo ili wafugaji waweze kunufaika na kuuza ng‟ombe hao wapate faida. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa mifugo, katika hotuba ya Waziri sijaona popote ambapo kuna mabwawa au malambo ya kunyweshea mifugo yetu katika Mkoa wa Shinyanga. Ninapata shida, tunapowaambia wafugaji wasihame, tumewaandalia mazingira gani ya kuweza kukaa na hii mifugo ili wasiweze kuhama? Naomba Waziri aniambie, tunapotoa tamko wafugaji wasihame, ni mazingira gani tuliyowawekea ili wasiendelee kutangatanga na mifugo hii? Naomba sana mniambie, kwa Mkoa wa Shinyanga ni malambo mangapi ambayo mmepanga na ni mabwawa mangapi kwa ajili ya wafugaji? (Makofi)
Mheshimiwa mwenyekiti, naendelea kujikita katika Mkoa wangu wa Shinyanga. Katika hotuba ya Waziri na katika Kitabu cha Maendeleo pia. Nilijaribu kutazama hata viwanda vya kutengeneza/vya kuchakata ngozi, Mkoa wa Shinyanga hatuna hata kimoja. Sasa sijui mmetuweka katika fungu gani. Naomba myatazame muone kama kweli mnatutendea haki au kuna jambo gani la ziada ambalo mnaona litastahili kwetu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusema mvua za mwaka huu zimekwa ni nyingi, za kutosha lakini haitoshi kuwa na mvua nyingi, hatukuwa na miundombinu ya kujiandaa ili mvua zile ziwe na tija kwetu. Kwa kiasi kikubwa mazao mengi yameharibiwa na mvua, maji mengi tuliyoyapata yamepotea bure.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali na kuishauri, hebu kakaeni mjipange vizuri, hatuna sababu ya kuwa tunayapoteza maji haya bure, tutafute namna ya kuyahifadhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Wizara ya Kilimo itoe tamko. Pamoja na chakula kidogo walichokipata wananchi wetu, kuna wafanyabiashara ambao wanatoka nje wanakwenda mpaka mashambani kununua zao la mpunga kwa wakulima wetu. Wananunua mpunga ambao hata haujavunwa kwa bei ya kutupwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inakatisha tama! Wananchi wetu wanauza kwa sababu wana shida. Yote hii ni kwa sababu soko la mchele limekuwa likishuka mara kwa mara na hivyo mpunga wao umekuwa ukinunuliwa kwa bei ya chini, kwa bei ya kutupwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi binafsi niseme ni mkulima wa mpunga, kwa hiyo hili ninalolisema nalitambua vizuri na inanisikitisha sana kuona wakulima wenzangu wananunuliwa zao lao likiwa shambani kwa bei ambayo ni ndogo, baada ya miezi miwili watakuwa…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema na hatimaye kusimama katika ukumbi wako wa Bunge kuweza kuchangia Bajeti ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, nakumbuka mwaka 2015 wakati wa uchaguzi alisema kodi kero zimezidi na hatimaye leo ndani ya mwaka mmoja na nusu tunakwenda kuona kodi kero zimenakwenda kuondolewa. Mheshimiwa Rais hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Naibu wake pamoja na timu yake yote. Niwaombe basi haya waliyoyaandika kwenye vitabu hivi waende wakayafanyie kazi. Tunawaamini, tunaamini watatekeleza yale ambayo wametuletea leo ndani ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo bila afya hakiwezi kwenda na natambua kabisa mchango mkubwa wa wanawake katika sekta ya kilimo. Naomba uniruhusu nitumie fursa hii kuwashukuru sana Ubalozi wa China nchini Tanzania kwa kuweza kunisaidia kwa wanawake wa Mkoa wa Shinyanga, msaada wa vifaa vya kujifungulia akinamama, nawashukuru sana Mungu awabariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba nijielekeze sasa katika bajeti ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Maeneo yetu yanatofautiana kwa kiasi kikubwa. Ninaposema yanatofautiana nina maana gani? Mkoa wa Shinyanga kwa miaka mfululizo sasa tumekuwa hatupati mvua za kutosha na Mkoa wa Shinyanga huwezi kuwaambia wananchi waende wakalime. Yuko tayari kulima kimeungua analima, kinaungua analima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kusema kwa mwaka huu tukaouanza ambao msimu wake wa mvua umekwisha tuna upungufu mkubwa wa chakula. Mkoa wa Shinyanga ni Wilaya moja angalau inakuwa inafanya vizuri kwenye suala la chakula, lakini nayo kwa mwaka huu kidogo hapako vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Kwandikwa Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Jimbo lake ndio kidogo ndio kidogo linakuwa linaupatia Mkoa wa Shinyanga chakula, lakini kwa mwaka huu, Jimbo la Ushetu hawakuweza kufanya vizuri kwa sababu ya ukosefu wa pembejeo. Kwa hiyo, nikiuchukua Mkoa mzima wa Shinyanga hali ya chakula tuna upungufu kwa kipindi hiki tunachokwenda naomba Mheshimiwa Waziri atuangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikoa haifanani na maeneo hayafanani, Mheshimiwa Waziri ananitazama naomba hili alichukue alifanyie kazi. Hatupendi Waheshimiwa Wabunge wa Shinyanga kusimama humu tukasema haya, Wasukuma si watu wa kuwaambia kwenda shambani watu wote humu ndani ni mashahidi, Msukuma ni mtu ambaye anainuka mwenyewe anakwenda shambani, hakuna mtu wa kumwambia aende shambani, lakini hali ya hewa ilivyo, ndiyo inatulazimu kufikia hatua ya kusema tuna upungufu wa chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda sasa hivi mfuko wa sembe, wa kilo 50 unauzwa Sh70,000/=. Ninaposema tuna upungufu wa chakula naomba Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi waangalie. Ghala la chakula tunalo pale karibu, hatuhitaji chakula cha bure, tunahitaji wananchi wetu wapate chakula chenye bei nafuu. Niwaombe wafanyabiashara, niwaombe mikoa ambayo wanajinasibu wana chakula cha kutosha, watuletee chakula Mkoa wa Shinyanga watuuzie kwa bei ambayo ni nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba niseme kwamba Serikali ya Mkoa wa Shinyanga mwaka 2010/2011 ilikaa na kubaini maeneo ya kuweza kuwa na kilimo cha uhakika katika Mkoa wa Shinyanga ili kuuondoa Mkoa wetu katika kilimo cha kutegemea mvua za juu. Ilibaini eneo la bonde la Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga na Halmashauri ya Wilaya ya Msalala kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji na wataalam kutoka Wizara ya Kilimo walitembelea eneo hili, sijui hayo yaliishia wapi? Tangu mwaka 2010/2011 mpaka leo kimya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna bonde zuri kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji, matokeo yake ni nini. Hata mwaka huu ninavyoongea mvua zimenyesha za mwisho mwisho, bonde lile limejaa maji, lakini hayana kazi tena, yanapotea kwa sababu hatuna sehemu ya kuyahifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Wizara ituangalie Mkoa wa Shinyanga kwa sababu hata aliyekuwa Waziri Mkuu kipindi kilichopita, Mheshimiwa Mizengo Pinda, alikuja Shinyanga na akaiona hali ya Shinyanga akaahidi kulisimamia bonde hili na kuhakikisha Shinyanga tunakuwa na kilimo cha umwagiliaji. Tukikimbilia kusema kule kwenye milima na maporomoko ya maji ndio wapewa kilimo cha umwagiliaji, wanakuwa hawatutendei haki wale ambao hatuna maporomoko ya maji na milima inayoporomosha maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali itutazame Mkoa wa Shinyanga kwa jicho la huruma, watutazame waweze kutuwekea miundombinu na kamwe hawatatuona tunasimama na kusema tuna upungufu wa chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kilimo cha umwagiliaji nasikitika sana, najua kilimo na umwagiliaji ni vitu ambavyo vinaendana kwa pamoja, nina hakika Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji yuko hapa; suala hili lilitekelezwa kwenye umwagiliaji kipindi kilichopita. Mradi wa umwagiliaji wa Kijiji cha Ishololo, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga. Mradi huu umetumia fedha nyingi, mamilioni ya fedha, lakini ukifika kwenye mradi ule unaweza ukalia. Tumeachiwa mashimo tu. Tuta lile baada ya mwaka mmoja limebomoka na maji yanapita, hakuna kinachohifadhika kwenye bwawa lile la umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua, Mheshimiwa Waziri akisimama hapa aniambie. Nataka kujua waliokwenda kutekeleza mradi ule wa Kijiji cha Ishololo Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga wamechukuliwa hatua gani kwa sababu mradi ule ulikuwa umelenga kuwafaidisha na kuwanufaisha wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, lakini mradi ule tena hauna tija kwetu kwa sababu tumeachiwa mashimo na tuta lile limekatika na maji yanapita yanapitiliza hayana sehemu ya kukaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba majibu ya Serikali, Mradi ule wana mpango gani nao ili tuweze kuwa na tija nao, bila ya hilo Mheshimiwa Waziri kwa kweli sitamwelewa. Naomba awasiliane na watu wa Maji na Umwagiliaji wamweleze mradi huu wa Ishololo hatima yake ni nini? Yale mashimo yaliyoko pale hatuhitaji kuyaona, tunahitaji kuona mradi unafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye suala la mbegu. Tunapokwenda kwenye maeneo ya ukame kama Mkoa wa Shinyanga, tunawaambia wananchi wetu wabadilike wapande mbegu ambazo zinastawi kwa muda mfupi. Hata hivyo, kinachonisikitisha sana mbegu hizi zinauzwa bei kubwa sana. Unapomwambia mwananchi akanunue Stuka sijui akanunue Pama sijui akanunue kitu gani, kile kimfuko cha kilo moja kinauzwa mpaka 12,000, mwananchi wa kawaida hawezi kumudu kununua mbegu hizi na kwenda kupanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumewashawishi wananchi kwa kipindi hiki tutoke kwenye zao la mahindi twende tukalime mtama. Mbegu yenyewe ya mtama kwa mwaka huu ilikuwa ni adimu mno, haipatikani. Niiombe Wizara itufanyie mpango mkakati wa kuweza kutuletea mbegu hizi ili na sisi tuweze kuwa tunavuna kwa muda unaostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye soko la mazao. Miaka ya 2008/2009, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga iliweka mpango mkakati wa kuwa na soko la mazao, soko la mchele. Tunaposema mchele wa Shinyanga maana yake kweli Shinyanga kuna mchele, mchele wa Dodoma, mchele wa Arusha, unatoka Shinyanga. Tulipenda Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga tuwe na soko la mchele pale katika Kata ya Didia na mipango hii ilitoka Halmashauri ikaenda mkoani ikaja Wizarani, sijui ilifia wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri atuambie ana mpango gani wa kuhakikisha kwamba mchele sasa unakuwa na soko lake katika Mkoa wa Shinyanga na kuweza kununuliwa? Kuna watu wengi wanaokuja kununua mchele lakini hatuna soko la uhakika, tunahitaji na sisi kuwa na soko ili mchele wetu uweze kununuliwa sokoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye mifugo. Mkoa wa Shinyanga ni miongoni mwa mikoa ambayo ina mifugo ya kutosha. Kwa nini wafugaji wetu wanaondoka? Ni kwa sababu ya hali kama hii ninayoisema ya ukame, marlsho hayapo, maji hayapo, ni kwa nini Wizara haifikirii kwenda kwenye maeneo kama Mkoa wa Shinyanga ambapo wafugaji wanahangaika kuhama na mifugo, wakawapa utaalam wa kupanda zile nyasi ambazo zinapandwa Mwabuki, zinapandwa pale Mpwapwa na maeneo mengine ili wafugaji wetu wasiendelee kuhama na mifugo yao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina hakika mfugaji ukimwelisha na ukamwonesha hizo nyasi zinapandwa vipi, na zinapatikana wapi, hakuna mfugaji atakayehama kwenye eneo lake na kwenda kutafuta malisho sehemu nyingine.
Naomba Wizara watuambie mna…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusema kwamba, naomba pia Wizara iongee na Wizara ya Maji na Umwagiliaji ili ule mradi wa umwagiliaji... (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwa haraka haraka, naomba niungane na Mheshimiwa Bura kusema kwamba Wizara ya TAMISEMI siyo rafiki kwa Wizara ya Afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti na Wabunge wenzangu, katika kitabu cha TAMISEMI hiki chenye majedwali kina kurasa 81, lakini kuanzia ukurasa wa 33 mpaka wa 81 wanaongelea elimu. Naomba Kamati ya Bajeti ikakae tujue hatma ya Wizara ya Afya ipo wapi kwenye ujenzi wa vituo vya afya na zahanati? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye vifo vya mama na mtoto; taarifa inasema wanawake 42 kila siku wanakufa au wanapoteza maisha. Kwa nini wanapoteza maisha? Wanawake hawa wanapoteza maisha kwa sababu vituo vyetu vya afya havina majengo ya upasuaji, havina damu ya kuwaongeza akinamama hawa; akinamama wanapoteza maisha kwa kumwaga damu nyingi na kwa kukosa huduma ya upasuaji. Ndiyo maana nasema, naomba Kamati ya Bajeti ikakae tujue, waje na mpango wa kuhakikisha kwamba vituo vyote vya afya hata kwa kuanzia kila Jimbo tuambiwe watajenga vituo vingapi vya upasuaji katika vituo vyetu vya afya? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kufanya hivyo, Mheshimiwa Waziri wa Afya na Naibu wake, nawapenda sana, lakini nawaambia hawatafanya kazi vizuri kwa hilo kwa sababu vifo vitaendelea kuwepo na suluhu yake ni kuwepo kwa majengo ya upasuaji na upatikanaji wa damu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende katika Mkoa wangu wa Shinyanga. Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga inatakiwa kuwa na watumishi 680, lakini mpaka hivi ninaposimama hapa ina watumishi 341, ina upungufu wa watumishi 155, hiyo ni Hospitali ya Rufaa, lakini ina Madaktari Bingwa watatu tu, ina upungufu wa Madaktari 24. Katika upungufu wa Madaktari waliopo, hatuna Daktari Bingwa mwanamke hata mmoja! Hatuna Daktari Bingwa wa upasuaji hata mmoja! Naomba Mheshimiwa Waziri alifanyie kazi haraka iwezekanavyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu ujenzi wa hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga. Mkoa wa Shinyanga uliomba shilingi bilioni tano kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Rufaa lakini mmetupa shilingi bilioni moja tu. Hivi kweli kuna dhamira ya dhati ya ujenzi wa hospitali hii? Tunategemea hospitali hii tunaijenga kwa shilingi bilioni moja? Hili halikubaliki! Naomba kama Serikali imedhamiria kweli kujenga Hospitali za Rufaa, basi wahakikishe wanatoa fedha ya kutosha, lakini siyo pesa kiduchu ambayo wanatupa, haiwezi kutufikisha popote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bado naendelea katika Mkoa wangu wa Shinyanga. Duka la MSD katika Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga mpaka sasa hivi tunavyoongea halipo. Naiomba sana Wizara, nimwombe Mheshimiwa Waziri, amefika Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga lakini sijui hili wanaliwekaje?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la dawa ni kubwa, ukienda pale Manispaa ya Shinyanga hata kwa wale wenye Bima ya Afya, ni maduka mawili tu ambayo wanatoa huduma hii. Sasa linakuwa ni tatizo kubwa na inafika mahali watu hawaoni sababu ya kuwa na Bima ya Afya, kwa sababu hata wanapokwenda kutafuta dawa, hawazipati. Naiomba Serikali iende ikafungue duka. Naomba MSD waende wakafungue duka pale Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, natumia fursa hii kuipongeza sana Serikali kwa sababu asiyeshukuru kwa kidogo, hata kwa kikubwa pia hawezi kushukuru. Naipongeza kwa nini? Naipongeza kwa sababu Bunge lililopita kila siku tulikuwa tunaimba humu ndani, MSD wanadai, lakini bajeti ya mwaka huu imeonyesha dhamira ya dhati ya kulipa deni la MSD. Kwa hiyo, niseme nawapongeza sana, naomba mkalipe fedha hizo haraka iwezekanavyo, nina hakika tatizo la dawa kwa kiasi fulani litapungua.
Kwa hiyo, nawaomba sana madawa haya yaweze kupatikana. Vile vile naomba sana tunapokuwa…
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kupata nafasi hii ili nitoe mawazo yangu katika Wizara hii ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara hii iangalie suala la maji upande wa mifugo yetu. Tunaishukuru Serikali yetu ya Awamu ya Tano kwa mradi mkubwa wa maji wa Ziwa Victoria ambao utatoka Solwa – Tinde – Nzega – Igunga
– Tabora na maeneo mengine. Naomba Wizara itambue kwamba matumizi ya maji si kwa binadamu tu, ni nyema wakajenga mabirika kwa ajili ya kunyweshea mifugo yetu ili tatizo la maji lipungue au liishe kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Wizara ya Kilimo izingatie mradi wa umwagiliaji wa Kijiji cha Ishololo katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga. Serikali imetumia fedha nyingi katika mradi huu lakini hauna tija kwa kuwa ndani ya mwaka mmoja tuta lilishabomoka na hivyo kufanya bwawa hilo kutokuhifadhi maji kama ilivyokusudiwa. Hata hivyo mkandarasi aliyefanya kazi hiyo ameacha mashimo mengi katika eneo hilo la bwawa na kuonekana kama uchafu na ni hatari kwa watoto wadogo hata watu wazima pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunijalia afya njema na hatimae nimesimama humu ndani kuweza kuchangia bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan; Mheshimiwa Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa; na Baraza lote la Mawaziri na Watendaji wote wa Serikali kwa kazi kubwa wanayoifanya. Hongereni sana, kazi inaonekana, chapeni kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo naomba nianze na kituo cha Buhangija, Kituo cha Watoto wenye Ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru sana Serikali mwaka huu wa fedha wametupa shilingi milioni mia mbili themanini na sita na laki sita ambazo zimeweza kujenga madarasa manne, mabweni mawili na matundu 18 ya vyoo. Tunaishukuru sana Serikali kwa kukiona kituo hiki, lakini kituo hiki bado kina upungufu mwingine ambao unahitaji kukamilishwa na hata mwaka jana nilivyokuwa nachangia nilisema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo cha watoto wenye ulemavu Buhangija kina upungufu wa watumishi. Kina upungufu wa Walimu wa watoto wasiosikia. Kituo hiki mahitaji yake ni Walimu nane lakini kina Walimu wawili tu. Mheshimiwa Jenista hata mwaka jana nilisema naomba akitazame kituo hiki. Walimu wawili tu hawatoshelezi kuwafundisha watoto hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo hiki kina walezi wawili tu wakati mahitaji ni walezi nane. Kituo hiki cha Buhangija hakina Mpishi hata mmoja, wapishi wanaopika pale ni kwa kujitolea na wanalipwa kama vibarua. Kwa hiyo, naiomba Serikali iweze kulifanyia kazi pamoja na kuboresha mazingira hayo lakini watumishi hawa waweze kuajiriwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie sekta ya afya; niishukuru sana Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa ambayo imeendelea kufanya katika sekta ya afya. Katika Mkoa wangu wa Shinyanga imeweza kuwezesha ujenzi na uboreshaji wa vituo sita vya afya. Kituo cha Afya cha Iyenze kilichopo Halmashauri ya Mji Kahama, Kituo cha Afya cha Chela kilichopo Halmashauri ya Msalala, Kituo cha Afya cha Ukune kilichopo Halmashauri ya Ushetu na Kituo cha Afya Tinde na Samuye Halmashauri ya Shinyanga Vijijini pamoja na Kituo cha Afya cha Songwa kilichopo Halmashauri ya Kishapu. Tunaishukuru Serikali na tunaipongeza kwa kazi kubwa wana kazi inaonekana, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na uboreshaji wa vituo hivi, kuna matatizo mengine ambayo yanastahili wagonjwa hawa kupewa rufaa. Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu haina Hospitali ya Wilaya. Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga Vijijini huu ni mwaka wa nane sasa naiongelea Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga Vijijini. Tulishaanza ujenzi lakini ujenzi huu umekuwa ukisuasua kwa sababu hatupewi fedha za kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali yangu sikivu, nimemsikia asubuhi Mheshimiwa Naibu Waziri akisema kwa mwaka huu wa fedha kuna hospitali za Wilaya 67 ambazo zitakwenda kujengwa. Namwomba na nina hakika kwamba Hospitali ya Wilaya ya Shinyanga Vijijini na Hospitali ya Wilaya ya Ushetu zitakuwepo katika orodha hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa sijatendea haki Mkoa wangu wa Shinyanga nisipoongelea Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga. Ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga unakwenda taratibu na hii ni kwa sababu fedha ambayo inatengwa imekuwa ikitengwa fedha kidogo na hivyo kufanya ujenzi huu usikamilike kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga kuna upungufu mkubwa wa watumishi. Mahitaji ya Hospitali ya Mkoa wa shinyanga watumishi ni 474, lakini waliopo ni 285 tu. Kwa takwimu zilizopo watumishi 30 ndani ya miaka miwili hii wanakwenda kustaafu, hivyo niiombe Serikali kuweza kuongeza watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia tena kusema na mwaka jana kwenye bajeti nilisema Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga ina uhitaji wa Madaktari Bingwa 21, lakini mpaka hivi ninavyoongea kuna Madaktari Bingwa wanne tu. Daktari Bingwa wa Magonjwa ya akinamama mmoja, Daktari wa Watoto mmoja, Daktari wa Upasuaji mmoja na hivyo kufanya tatizo la Madaktari Bingwa katika hospitali hii linakuwa ni sugu, niombe hospitali iweze kuletewa Madaktari hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende upande wa elimu. Nitumie fursa hii kuishukuru sana Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, Serikali sikivu ya Awamu ya Tano imeweza kufanya mambo makubwa katika Mkoa wa Shinyanga. Nianze na Halmashauri ya Wilaya ya Msalala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Msalala ilipata milioni mia moja sabini na kwenda kujenga hosteli ya Sekondari ya Burige na Sekondari ya Ntobo Sekondari, tunaishukuru sana Serikali. Halmashauri ya Ushetu imepeleka fedha katika Shule ya Msingi Nonwe milioni mia moja tisini na mbili na Shule ya Msingi Bugomba milioni mia moja tisini na mbili na hivyo kufanya mazingira ya shule hizi kuwa mazuri na kuwavutia watoto na uandikishaji kuendelea kuwa mkubwa katika shule zetu hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba niingie katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga Vijijini, Halmashauri ambayo Mimi ni Diwani na ni Halmashauri ambayo nahudhuria vikao vyake vya Baraza la Madiwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Shinyanga Vijijini ina Shule ya Sekondari ya Zunzuri, shule hii ni kongwe, shule hii ina kidato cha kwanza mpaka kidato cha nne lakini Halmashauri tulikaa kwenye Baraza la Madiwani tukakubaliana shule hii tuweke kidato cha tano na cha sita. Baadhi ya miundombinu tumekwishaiweka katika shule hii, vimebaki vitu vichache ambavyo havijakamilika bwalo la chakula, bweni moja, ukarabati wa maabara tatu pamoja vifaa vyake na vitanda 48.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa naomba niseme kwenye shule hii ya sekondari. Hazina walikuwa wanapeleka fedha katika shule moja inaitwa Tinde Day wakifikiri kwamba ile shule ni ya Boarding. Kwa hiyo fedha zile zilikuwa zinakwenda pale kimakosa, Halmashauri na Mkurugenzi wakachukua jukumu la kuiandikia barua Hazina kuomba kubadilisha fedha zile kuzipeleka kwenye Shule ya Sekondari ya Zunzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TAMISEMI walijibu barua ile wakakubali kuruhusu kubadilisha fedha hiyo na baada ya TAMISEMI kutoa barua kuruhusu kubadilisha fedha hiyo Halmashauri ilianza kutumia fedha hizo. Kwa masikitiko makubwa Hazina wameandika barua kumzuia Mkurugenzi asiendelee kutumia fedha hizo kwa matumizi ya Shule ya Sekondari Zunzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashangaa Hazina ni nani na TAMISEMI ni nani! TAMISEMI wameruhusu na fedha ile ikaanza kutumika ili kuboresha maeneo haya na kidato cha tano kiweze kuanza kufanya kazi, lakini leo hii Hazina wameandika barua kumzuia Mkurugenzi na wanamtaka Mkurugenzi arudishe fedha ile. Naomba majibu ya Serikali, Serikali ni moja, Halmashauri ni moja ni kwa nini wanazuia matumizi ya fedha hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusemea Shule ya Sekondari ya Zunzuri, naomba niisemee Shule ya Sekondari ya Wasichana iliyopo Tinde. Shule ya Wasichana ya Tinde ni ya kidato cha tano na sita. Shule hii ina miundombinu mizuri, nyumba za Walimu za kutosha, madarasa ya kutosha, maabara, lakini shule hii haina bwalo wala ukumbi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha unapokuwa katika mazingira yale kama mvua inanyesha wanafunzi wanakula nje wakati mwingine wananyeshewa na mvua. Mheshimiwa Waziri wa Elimu nilimwomba na narudia tena kumwomba leo hii humu, chonde chonde aitizame Shule ya Wasichana ya Tinde. Yeye ni mama nina hakika anajua akimwelimisha mwanamke, akimwelimisha binti atafika na yeye hapo alipofika yeye, naomba aitizame Shule ya Wasichana ya Tinde.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado niko katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga. Sasa naomba niongelee Shule ya Msingi Masunula iliyopo katika Kata ya Usule. Shule ya Masunula ipo katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga. Shule hii imekuwa ikifanya vizuri kwa miaka mitatu mfululizo, imekua ikiongoza ya kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa shule hii haina nyumba hata moja ya Mwalimu. Hivi tunawatazamaje Walimu hawa ambao kwa miaka mitatu mfululizo wameweza kutufundishia watoto wetu na shule ile kuweza kuongoza kwa ufaulu. Niiombe sana Serikali tunaomba waitizame shule ya Msingi ya Masunula waweze kutujengea nyumba za watumishi kwa sababu shule hii haina nyumba hata moja ya mtumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga fedha za maendeleo, kwa masikitiko makubwa hili naomba niliseme. Mwaka 2016/2017 tuliidhinishiwa fedha za maendeleo bilioni 1.6, lakini fedha ambayo Halmashauri ilipokea ni milioni 420 tu. Fedha zingine zote hazikuweza kufika. Mwaka wa fedha 2017/2018 tuliidhinishiwa bilioni 1.7; mpaka hivi ninavyoongea Halmashauri haijapokea kiasi chochote cha fedha ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili naomba sana Serikali ilitazame kwa macho mawili, ni kwa nini halmashauri yetu tunakuwa tunaidhinishiwa pesa, lakini fedha hizi hazifiki. Naomba nipate majibu ya kutosha ni kwa nini Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga mpaka sasa hivi hatujapata fedha ya Maendeleo hata shilingi moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nisemee suala la Watendaji. Suala la Watendaji...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia bajeti hii ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye amenijalia afya na uzima na hatimaye nimeweza kusimama ndani ya ukumbi huu kuweza kuchangia hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, kwa kazi kubwa ambayo anaifanya na anaendelea kuifanya katika kuwatumikia Watanzania. Niwapongeze pia wasaidizi wake wa karibu; Makamu wa Rais mama Samia Suluhu Hassan na Mheshimiwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Majaliwa, wamekuwa karibu sana na Mheshimiwa Rais kuhakikisha kwamba masuala yote ambayo wanakuwa wamekusudia kuyafanya yanafanyika kikamilifu na yanaonekana mbele za Watanzania, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii pia kumpongeza Waziri, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Mheshimiwa Jafo, Manaibu wako na watendaji wote wa TAMISEMI, hakika mmeitendea haki Wizara hii; hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwanza kwa kushukuru kwa yale makubwa ambayo yamefanyika ndani ya Mkoa wa Shinyanga. Ninaanza kwa kushukuru kwa sababu kuna mambo ambayo niliyasema sana ndani ya Bunge hili, lakini kwa sababu Serikali ya Awamu ya Tano, Serikali sikivu inayoongozwa na Jemedari, Dkt. John Pombe Magufuli, wamekwenda kuyafanya kikamilifu na wananchi wa Shinyanga wanayaona, naomba nitumie fursa hii kuishukuru sana Serikali na kumshukuru sana Rais wetu kipenzi, Dkt. John Joseph Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga unaendelea na uko katika hatua nzuri; ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Shinyanga umekwishakamilika, hospitali ambayo nimeipigia kelele toka nimeingia mwaka 2010 ndani ya ukumbi huu, sasa hivi imekwishakamilika. Ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Ushetu umekwishakamilika, ujenzi wa mabweni katika shule zetu za sekondani, nizitaje baadhi ya shule hizo; Shule ya Sekondari Saba Sabini, Ulowa, Kinamapula, Nyashimbi, Bukamba, Busoka Sekondari. Hiyo yote ni kazi ya Serikali ya Awamu ya Tano ndani ya kipindi cha miaka minne; hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii pia kuipongeza sana Serikali kwa ujenzi wa vituo vya afya sita katika Mkoa wa Shinyanga. Vituo hivyo vimekamilika na vinafanya kazi na wananchi wetu wanapata huduma kwa ukaribu zaidi, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niingie katika sekta ya elimu, nilikuwa najaribu kusikiliza hotuba ya Kambi ya Upinzani; wanasema miundombinu haitoshi hawajaona chochote, miundombinu haitoshi; lakini niwapitishe tu kwa harakahara. Kwenye suala la miundombinu katika shule za msingi Mheshimiwa Waziri Jafo hapa amesema vyumba vya madarasa 19,808 vimejengwa ndani ya miaka mine; vyumba vya maabara 227 vimejengwa ndani ya miaka mine; vifaa vya maabara shule 1,258 vimesambazwa katika shule zetu; matundu ya vyoo 7,922 yamejengwa katika shule zetu; na ukarabari wa shule kongwe 73 umefanyika kwa kiasi kikubwa kwa kiwango cha juu katika shule zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda tu Mkoa wa Shinyanga vyumba vya madarasa 276 vimejengwa; matundu ya vyoo 155; nyumba za Walimu 23; maabara 10; na mabweni 16. Kwa nini nisiseme hongera Daktari John Joseph Pombe Magufuli kwa kazi kubwa ambayo umeifanya ya kuwatumikia Watanzania na kutekeleza ahadi ambazo umekuwa ukizitoa?

Mheshimiwa Naibu Spika, nikirudi kwenye…

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Azza kuna Taarifa.

MHE. FRANK G, MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpa Taarifa mzungumzaji, Mheshimiwa Azza kwamba, kwa mujibu wa taarifa ya tafiti ya Haki Elimu baada ya tangazo la elimu bure ongezeko la watoto kujiandikisha ni 17%, lakini ongezeko la miundombinu katika nchi hii ni 1% peke yake.

Kwa hiyo, ni kweli anazungumza kwamba, yamefanyika na Mheshimiwa Waziri ameonesha kwenye bajeti, lakini ukweli ni kwamba, bado tuna upungufu mkubwa na ndio maana bado hawakuweka mahitaji na upungufu uliopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nafikiri Mbunge ajue kabisa kwamba, bado tuna upungufu mkubwa na tumshauri tu Mheshimiwa Jafo aendelee kuhakikisha kwamba, wanaongeza vyumba kwa kasi na wapange fedha nyingi kwa ajili ya kuongeza vyumba vya madarasa. Ahsante.

NAIBU SPIKA: Kuhusu ushauri kwenye hiyo taarifa utatoa wakati wako wa kuchangia, lakini pale ulipoishia kwenye Taarifa, ndio nitakapomuuliza Mhesimiwa Azza kama anaikubali hiyo Taarifa au anaikataa?

MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa yake siipokei na wala siikubali. Namwambia kwamba, maendeleo ni hatua kwa hatua, huwezi ukafanya mambo yako yote ukayakamilisha kwa wakati mmoja. Hata sisi humu ndani leo hii ukipewa pesa begi zima hutamaliza yale yote ambayo umeyakusudia katika nafsi yako. Kwa hiyo, Serikali inafanya awamu kwa awamu, infanya hatua kwa hatua, hongera Daktari John Joseph Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ambayo ameisoma Mheshimiwa Jafo leo nimeangalia na nimesikiliza kwa makini kwa mwaka huu wa fedha Mkoa wetu wa Shinyanga tumetengewa shilingi milioni 840 kwa ajili ya ukamilishaji wa vyumba vya madarasa. Taarifa hiyo iko ukurasa wa 339, kwa nini nisiseme maendeleo ni hatua kwa hatua? Hatua moja huanzisha hatua nyingine. Hongereni sana. Ukamilishaji wa maabara. Mkoa wa Shinyanga peke yake tumetengewa shilingi bilioni 1.3 kwa ajili ya ukamilishaji wa maabara 44 ndani ya Mkoa wa Shinyanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudi upande wa afya katika kazi ambazo zimefanyika ndani ya miaka hii minne. Ujenzi na ukarabati wa hospitali za Halmashauri zetu umefanyika kwa Halmashauri 98. Vituo vya afya 433, zahanati 368 ambazo zimejengwa na kufanyiwa ukarabati, lakini kwa Mkoa wa Shinyanga pekee vituo vya afya sita vimejengwa vyenye thamani ya shilingi bilioni 7.4, tunashukuru sana wananchi wa Shinyanga kwa kazi kubwa ambayo imefanywa. Hospitali za Halmashauri katika Mkoa wetu zimejengwa hospitali tatu ambazo ni Hospitali ya Wilaya ya Shinyanga Vijijini, Hospitali ya Wilaya ya Ushetu na Hospitali ya Halmashauri ya Msalala ambayo bado haijakamilika na mwaka huu nimeona imetengewa tena bilioni moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika upande wa afya ukamilishaji wa zahanati nimeona Mheshimiwa Waziri ametuambia hapa katika bajeti ya mwaka huu kila Halmashauri itapata zahnati tatu. Kwa Mkoa wa Shinyanga peke yake tuna bilioni 3.9 kwa ajili ya zahanati, sina sababu ya kukaa hapa kuanza kutaja kwamba, naomba zahanati fulani, naomba zahanati fulani, naamini hizi bilioni 3.9 zitakwenda kukamilisha zile zahanati zetu ambazo zimeanzishwa na wananchi na wananchi sasa kwenda kupata huduma ambayo inastahili, tunawashukuru sana; lakini pia nitumie fursa hii kuishukuru Serikali kwa Halmashauri ya Wilaya ya Msalala tumetengewa bilioni moja kwa ajili ya ukamilishaji wa hospitali ya Halmashauri ya Msalala.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona katika bajeti ya mwaka huu katika ujenzi wa nyumba za watumishi na majengo ya utawala. Nitumie fursa hii tena kusema kwa Mkoa wa Shinyanga tuna bilioni 2.5 ambazo zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya utawala na majengo haya yanakwenda kujengwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, Halmashauri ya Wilaya ya Msalala na Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu. Naishukuru Serikali kwa kuona kwamba, watumishi wetu wanatakiwa sasa kuwa na sehemu nzuri ya kufanyia kazi ili waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii pia kuwashukuru sana wanawake wa Mkoa wa Shinyanga na Wananchi wa Mkoa wa Shinyanga kwani kwa muda wote wameniamini na kuweza kufanya nao kazi ndani ya miaka minne.

Nawashukuru sana kwa ushirikiano mkubwa ambao wamenipa, lakini pia nitumie fursa hii kuwashukuru sana wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga ambayo ndio Halmashauri Mama ninayoishi kwa kuweza kunilea na kunifikisha hapa nilipofika. Niko pamoja na ninyi na nitaendelea kuwa pamoja na ninyi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naona unanitazama kengele imegonga, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia hotuba ya Wizara ya TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora.
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa yote. Amenipa afya njema na hatimaye kusimama katika Bunge lako Tukufu. Kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kuchangia katika bajeti hii, natumia fursa hii kuwashukuru wanawake wa Mkoa wa Shinyanga kwa kuniamini kwa mara nyingine kuweza kuwatumikia. Nawaahidi sitowaangusha kama kawaida yangu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Magufuli. Mheshimiwa Rais hongera sana pamoja na Baraza lako la Mawaziri, chapeni kazi, tuko bega kwa bega na ninyi mpaka kieleweke. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nijielekeze katika hotuba ya Waziri wa TAMISEMI. Ukurasa wa 65 anasema ujenzi wa miundombinu ya Mikoa na Wilaya mpya. Baada ya kusoma hotuba ya Waziri wa TAMISEMI nimesikitika sana kwa sababu maeneo ambayo yanatazamwa ni maeneo mapya ya utawala, wakati kuna maeneo yaliyopo ya zamani hayana miundombinu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na mfano wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga. Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga ni Halmashauri mama kwa Mkoa wa Shinyanga, ni Halmashauri ambayo imezaa Wilaya zote na Halmashauri zote za Mkoa wa Shinyanga. Hivi sasa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga iko ndani ya Manispaa ya Shinyanga, majengo yake yako ndani ya Manispaa ya Shinyanga. Halmashauri za Wilaya ya Shinyanga ina Tarafa tatu, Kata 26, Vijiji 126, ina watu laki 355,930.
Mheshimiwa Naibu Spika, lilitoka agizo kwa Mkuu wa Mkoa kwamba tunapaswa kuhamia kwenye maeneo yetu ya utawala, tusifanyie vikao Manispaa ya Shinyanga. Kinachonishangaza unapotuambia tuhamie kwenye maeneo yetu ya utawala hatuna chumba hata kimoja cha ofisi, vikao vyote vya Baraza la Madiwani kwa sasa hivi vimehamia eneo moja la Iselamagazi ambapo ndiyo tulitenga kuwa Makao Makuu ya Wilaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunafanyia wapi vikao vyetu? Tunafanyia kwenye majengo ambayo ni ujenzi wa hospitali ya Wilaya. Inasikitisha na inakatisha tamaa, kama tunasema tunataka kupunguza matumizi, unapunguzaje matumizi kwa kuondoa gari za Halmashauri zaidi ya sita kutoka Manispaa ya Shinyanga halafu zikafanye vikao zaidi ya kilometa 80, hayo matumizi unayapunguzia wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Waziri wa TAMISEMI aliangalie hilo. Hoja siyo kuangalia maeneo mapya, angalieni na maeneo ambayo ni ya muda mrefu ambayo yanahitaji miundombinu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kulisema hilo, naomba sasa nijielekeze upande wa afya. Nimepitia bajeti yote ya TAMISEMI katika vitabu vyote lakini sijaona, Mkoa wa Shinyanga tuna ujenzi wa hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, sijaona tumepangiwa kiasi gani cha fedha. Siku zote nimekuwa nikisimama humu ndani nasema hospitali ya Mkoa wa Shinyanga ina msongamano mkubwa wa wagonjwa, ukizingatia Wilaya zetu zote hazina hospitali za Wilaya isipokuwa Wilaya ya Kahama. Nilitegemea basi katika bajeti hii nitaona bajeti ya ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, lakini sijaona! Kama ipo naomba Waziri uniambie iko wapi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa hospitali ya Wilaya ya Shinyanga Vijijini gharama yake ni zaidi ya bilioni 10. Toka ujenzi huu umeanzishwa kwa nguvu za wananchi, Serikali imechangia milioni 270 tu mpaka hivi tunavyoongea, bado mnatuambia turudi kwenye maeneo yetu ya kazi, tunarudi kwenda kufanya kazi gani wakati hata miundombinu haituruhusu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunategemea nini iwapo hospitali hizi hatujazikamilisha, bado naendelea kusema hospitali ya Mkoa wa Shinyanga itakuwa na mrundikano wa wagonjwa kwa sababu hatuzitazami Wilaya zetu, miundombinu yake ikoje na wale ambao wameanzisha ujenzi wa hospitali hizi hamjatutengea fedha hata kidogo. Inasikitisha, naomba mtutazame Mkoa wa Shinyanga na mtazame Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, imeanzisha ujenzi wa hospitali ya Wilaya. Kwa sasa hivi taratibu imeanza kufanya kazi lakini kuna baadhi ya majengo hayajakamilika na Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu imeomba ombi maalum la shilingi milioni 600 angalau kujaribu kusogeza tu zile huduma, sijui ombi hilo mpaka sasa hivi limefikia wapi? Hiyo yote ni kujaribu kuondoa msongamano mkubwa uliopo katika hospitali ya Mkoa wa Shinyanga. Naiomba Serikali, Mheshimiwa Waziri namwomba sana atutazame kwa jicho la huruma Mkoa wa Shinyanga kwa sababu hatuwatendei haki wananchi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, maombi yanayotakiwa katika hospitali ya Wilaya ya Kishapu ni bilioni tatu, lakini tumeomba milioni 600, sijui imefikia wapi, nitaomba majibu Waziri utakapokuwa umesimama.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kuishauri Serikali, huu utaratibu wa kila mwaka kuanzisha majengo mapya kama Wilaya imeanza mpya, Halmashauri mpya, mnaanzisha majengo, hebu tuusitishe, tumalize kwanza miradi iliyopo. Hakuna sababu ya kila siku kuanzisha miradi wakati tuna magofu mengi hayajakamilika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kila ninaposimama humu ndani huwa nasema, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga tuna zaidi ya zahanati 28 ambazo tumeanza kujenga ambazo hazijakamilika. Tuna zaidi ya vituo vya afya nane ambavyo havijakamilika, sijaona kwenye bajeti hii tunafanya nini. Niombe tusianzishe miradi mipya, tukamilishe kwanza ile iliyopo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, upungufu wa watumishi katika Wizara ya Afya. Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, mahitaji yake katika watumishi wa afya ni 726, watumishi waliopo ni 227, upungufu ni 499. Tunategemea watu hawa wanafanya kazi kwa kiasi gani? Nawaomba sana tuangalieni muweze kutuongezea watumishi ambapo tuna upungufu mkubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nielekee upande wa maji. Nasikitika sana Bunge lililopita la mwezi wa Pili Mheshimiwa Naibu Waziri Suleiman Jafo alijibu swali langu la Mradi wa Maji wa Mji Mdogo wa Tinde, alisema ndani ya Bunge kufikia mwezi wa Nne Mradi wa Maji wa Mji Mdogo wa Tinde utakuwa umekwishaanza kufanya kazi, lakini mpaka hivi ninavyoongea hapa mradi haujakamilika na SHIWASA hawajapewa fedha ambayo ilikuwa imebaki. Nawaomba sana mtakaposimama kujibu, Waziri wa Fedha aniambie ni kitu gani ambacho kimesababisha mradi huu ulikuwa ukamilike kutoka 2014 na mpaka leo ni milioni 100 tu inayosumbua ili mradi ukamilike. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo, nijielekeze katika mradi wa TASAF. Mradi wa TASAF wa awamu ya tatu ni mradi mzuri sana, kinachosikitisha Kamati zilizowekwa pamoja na baadhi ya watendaji wanautumia mradi huu kwa kudanganya, kuweka watu ambao hawastahili kupata ruzuku hii. Niombe ukafanyike uhakiki wa kila kaya kwa wale ambao wamechukua ruzuku hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, niwashauri Serikali, Mheshimiwa dada yangu Kairuki, kwa sababu TASAF imeazimia kuwasaidia watu hawa upande wa afya, isiwe ombi, iwe ni sheria kwa watu wote wanaopewa ruzuku kutoka TASAF wakatiwe bima ya afya moja kwa moja na wasipewe zile pesa wapewe huduma ya afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na Mheshimiwa Subira upande wa Wabunge wa Viti Maalum. Imekuwa ni mazoea Wabunge wa Viti Maalum hawaruhusiwi kuingia kwenye Kamati za Fedha. Ukienda Halmashauri zingine wanaingia. Namwomba sana Waziri Mkuu atuangalie Wabunge wa Viti Maalum, mnatuogopa nini kuingia kwenye Kamati za Fedha? Kila unapokwenda Wabunge wa Viti Maalum hawaruhusiwi kuingia kwenye Kamati za Fedha, naomba sana Wabunge wa Viti Maalum turuhusiwe kuingia kwenye Kamati za Fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kuwaomba Wenyeviti wa Vijiji waweze kulipwa posho ukizingatia asilimia 20 haifiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema na kuuona mwezi Mtukufu wa Ramadhani. Nitumie fursa hii kuwatakiwa heri wale wote waliojaaliwa kufunga mwezi Mtukufu wa Ramadhani.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuchangia katika hotuba hii ya Waziri wa Wizara ya Fedha, Ofisi ya CAG, binafsi sioni kama tumeitendea haki Ofisi ya CAG kwa sababu pesa zote tunazozipeleka katika Halmashauri zetu bila kumuwezesha CAG hakuna tunachokifanya. Kwa sababu hatafanya kazi yake kwa uhakika, atafanya pale ambapo atakuwa amepafikia vinginevyo kama tunasema labda fedha hizi tunazozipeleka kule ziende zikaliwe na wale ambao wamezoea kula fedha za Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kulisema hilo naomba nisemee mafao ya Wabunge. Mbunge ninakatwa kodi kila mwezi shilingi 1,063,000; inanishangaza sana kuona mafao yangu ya mwisho ninakwenda tena kukatwa kodi. Wakati ninapomaliza Ubunge mimi silipwi tena ile pensheni wanayolipwa watumishi wengine. Nimuombe Waziri wa Fedha atakapokuja hapa atuambie ni kwa nini na kwa nini iwe kwa Wabunge tu na kwa nini iwe ni mwaka huu? Kwa hilo Waziri wa Fedha naomba utupe mchanganuo mzuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninajikita zaidi leo katika hotuba ya Waziri wa Fedha ukurasa wake wa 30 mpaka ukurasa wa 31.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kusema Ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi tulisema kwenye majukwaa tutajenga vituo vya afya kila kata na tutajenga zahanati kila kijiji.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikichukua kitabu cha Mheshimiwa Waziri cha hotuba yake ukurasa wa 31 naomba nimnukuu anasema; “Tutaimarisha mifumo, majengo na miundombinu mingine katika shule za awali, shule za misingi, za sekondari, upanuzi wa vyuo vikuu, ukarabati, ujenzi wa vyuo vya elimu ya juu, upanuzi wa vyuo vya ufundi, miradi ya kuboresha Hospitali za Rufaa, Taasisi ya Saratani ya Ocean Road, Hospitali ya Magonjwa Kuambukiza Kibong’oto na kuanzisha programu ya kuzalisha ajira na programu ya maendeleo ya ujuzi, mazingira na mabadiliko ya tabianchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna sehemu yoyote ambayo ametuambia upande wa afya tunakwendaje kutekeleza ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya kujenga kituo cha afya kwa kila kata, hakuna kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Afya. Haitoshi kwenye Wizara ya TAMISEMI nilichangia nikasema hakuna sehemu yoyote ambapo TAMISEMI wameonesha kwamba ni wapi tunakwenda kutekeleza ujenzi wa vituo vya afya na zahanati katika vijiji vyetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninamtaka Waziri aniambie, tunaposema tunakwenda kujenga vituo vya afya, tunategemea Halmashauri ikajenge vituo vya afya kwa mapato ya ndani? Halmashauri inayokusanya milioni 300 itakwenda kujenga vituo vya afya kwenye Kata zake? Hili haliwezekani! Sijui ni kwa nini Serikali yote kuanzia TAMISEMI mpaka Waziri wa fedha hawakuitizama Wizara ya Afya.
Mheshimwia Naibu Spika, tunaposema tunataka vituo vya afya kila kata. Tuna kata 3,963, vituo vilivyopo vya Serikali ni vituo 497 tu ambavyo vinatoa huduma ya afya na vituo hivi havijakamilika. Katika vituo 497 vinavyotoa huduma, ni vituo 106 tu vinavyotoa huduma ya upasuaji, sasa tunapokwenda kusema, tunataka kuondoa vifo vya mama na mtoto, tunaviondoaje wakati vituo vyetu vya afya havina majengo ya upasuaji? Tunaposema tunaboresha afya kwa wananchi wetu, tunaboreshaje wakati hata vitu vilivyopo havijakamilika?
Naomba Waziri wa fedha atuambie kama kwa mwaka huu hakuna
kitu chochote kinafanyika katka ujenzi huu, nina hakika Halmashauri hatuwezi kujenga vituo vya afya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano tu; Wilaya ninayotoka tuna kata 26, unakwendaje kujenga vituo vya afya vyote kwa kutegemea mapato ya ndani? Hili Wizara ya Fedha waliangalie halijakaa vizuri kabisa, hatutakwenda kutekeleza Ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. Ninaomba atakaposimama, ajibu wamejipanga vipi kuhakikisha kwamba tunakwenda kujenga vituo vya afya kwa kila kata ili kuhakikisha kwamba tunapunguza au tunaondoa kabisa vifo vya mama na mtoto. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vifo vya mama na mtoto vinatokea kwa sababu gani? ukienda kwenye Kituo cha afya, huduma ya upasuaji haipo, huduma ya damu salama haipo. Vifo vya Watoto vinatokea ni kwa sababu ya upungufu wa damu. Ukienda kwenye kituo cha afya, damu salama haipo. Tunasemaje tunatapunguza vifo vya mama na mtoto wakati majengo ya upasuaji na huduma ya damu salama haipo kwenye vituo vyetu?
Mheshimiwa Naibu Spika, niishauri Serikali, badala ya kusema tunakwenda kujenga vituo vipya vya afya, tuvichukue hivi 497 ambavyo vipo na vinatoa huduma, tuhakikishe vinatoa huduma zote zinazostahili katika vituo vya afya, kuliko kwenda kuanzisha majengo mapya ya ujenzi ambao pia tunaacha yale ambayo yanatoa huduma na hayajakamilika. Hayajakamilika kwa sababu gani? Unakuta hakuma wodi ya mama, hakuna wodi ya watoto, hakuna wodi ya akina baba, hakuna wodi ya akina mama wala hakuna jengo la upasuaji. Kwa hiyo, niishauri Serikali iende ikakamilishe kwanza vile vituo 497 wahakikishe kila kituo kinapata jengo la upasuaji, ndipo hapo tutakaposema kwamba huduma ya afya sasa tunakwenda kuiboresha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hilo, niende kwenye shilingi milioni 50 za kila kijiji. Imetengwa kwenye bajeti, asilimia sita tu ya asilimia 50 kwenye kila kijiji. Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015, tulisimama tukasema kila kijiji kitapata shilingi milioni 50. Tuna maswali mengi kwa wananchi wetu, nikitizama kwenye bajeti hii ni shilingi bilioni 59 tu ambazo zimetengwa kwenye bajeti hii ambayo ni sawa na asilimia sita. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, inanitia hofu kama tutakwenda kwa asilimia sita mwaka huu, ndani ya miaka mitano, tutakuwa hatujafikia lengo ambalo tumelikusudia kwa wananchi wetu. Niungane na Kamati, niishauri Serikali badala ya kutoa asilimia sita, itoe asilimia 20 kwa mwaka huu wa fedha. Tukijipanga kwa kutoa asilimia 20 kwa mwaka huu wa fedha, maana yake utatoa shilingi bilioni 196, ndani ya miaka mitano tutakwenda kuvifikia vijiji vyote tulivyonavyo, bila kufanya hivyo tutafikisha miaka mitano na hatutakuwa tumevifikia vijiji vyote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu muda bado unaniruhusu, naomba niongelee suala la maji. Tatizo la maji ni kubwa sana. Nimuombe Waziri wa Fedha, kuna miradi mingi ya muda mrefu ambayo bado inadai fedha, wakandarasi wanadai fedha. Hebu nendeni mkakamilishe miradi hiyo, walipwe wakandarasi hao na miradi iweze kufanya kazi. Nitoe mfano mdogo tu, kuna mradi wa maji wa Mji Mdogo wa Tinde ambao mpaka leo haujakamilika kwa shilingi milioni 100 tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na ninaunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii, lakini naomba niseme ninaitwa Azza Hillal Hamad.
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na kuweza kusimama ndani ya ukumbi wako kuweza kuchangia Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe kwa ruhusa yako, nitumie fursa hii kuwapa pole ndugu, jamaa na marafiki ambao wameondokewa na wapendwa wao katika ajali ya gari ya aina ya Noah iliyotokea tarehe 6 Novemba, siku ya Jumapili katka Mji mdogo wa Tinde poleni sana Mwenyezi Mungu awape subira niko pamoja na ninyi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kuchangia katika Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa. Ukiangalia katika ukurasa wa 40 wa Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa mfuko wa wanawake na vijana asilimia kumi katika Halmashauri ambazo zimekafuliwa, tumekagua Halmashauri 164 katika Halmashauri 164, Halmashauri 112 hazikupeleka fedha ipasavyo katika mfuko wa wanawake na vijana.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri 112 halmashauri 6 ziliagizwa na Kamati kuandika barua ya kuji-commit kulipa fedha hizo kabla ya tarehe 30 Septemba. Cha kusikitisha Halmashauri hizo mpaka hivi ninavyoongea au mpaka Kamati inaleta taarifa ndani ya Bunge hazijaleta barua hizo. Halmashauri hizo ni Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo, Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru, Halmashauri ya Jiji la Tanga na Halmashauri ya Ruangwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri hizo zilizokaguliwa kuna Halmashauri ambazo hazikuchangia kabisa hata shilingi moja kwa mwaka 2014/2015 ziko ukurasa wa 43. Halmashauri hizo ni Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo, Halmashari ya Tunduru, Halmashauri ya Mpanda, Halmashauri ya Tunduma, Halmashauri ya Ludewa, Sengerema na Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam.
Mheshimiwa Naibu Spika, mfuko wa wanawake na vijana umekuwa kama ni hisani kwa halmashauri. Watu wanafanya pale ambapo wanaona kwamba inafaa na Wakurugenzi wengi katika Kamati wamekuwa wakijibu kwamba wanatumia fedha hizi kwa sababu ya maagizo yanayotoka juu. Wengi wanasema wanatengeneza madawati, wamejengea maabara. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini fedha hizi zimekuwa kama shamba la bibi? Ni kwa sababu tu hakuna sheria ambayo ipo katika Halmashauri zetu inayowaelekeza Wakurugenzi kupeleka fedha hizi kwa wanawake na vijana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa tukilisema kwa muda mrefu hili ni tatizo sugu kwa Halmashauri. Wanafanya hivi kwa sababu tu wanawake hawa na vijana hawawezi kwenda kwenye Halmashauri kudai haki yao kwa sababu haipo kisheria. Lakini kama Halmashauri inafikia kupewa maagizo na Kamati, kuandika barua ndani ya Kamati na Halmashauri inakaidi maana yake ni nini? Maana yake ni kwamba Halmashauri hizi haziheshimu wala hazitambui mamlaka zilizopo juu kwa maana ya kwamba waraka huu wa kupeleka mfuko wa akina mama na vijana asilimia kumi ulipelekwa kutoka TAMISEMI. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niombe na niishauri Serikali kwa kuwa Halmashauri zimekuwa hazipeleki fedha hizi, ni vyema basi Serikali ikaleta Muswada wa Sheria wa Mfuko wa Wanawake na Vijana ili wanawake na vijana hawa ambao wako kule na wanakosa nafasi ya kupata mikopo katika mabenki kwa sababu ya masharti yaliyopo ya mabenki waweze kukopeshwa fedha hizi kama haki yao ya msingi. Vinginevyo tutabaki kulalamika lakini fedha hizi hawatazipata.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ninaishauri Serikali mlete muswada wa sheria kwa ajili ya mfuko wa wanawake na vijana ili tuweze kuwakomboa wanawake na vijana waliopo kule majimboni kwetu. Katika taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa, Halmashauri pia ina tatizo sugu. Tatizo hili ni kwamba asilimia 20 ya vyanzo vya mapato zilivyofutwa Halmashauri haipeleki kwenye mitaa na vijiji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia ukurasa wa 45 wa taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa utaona kuna Halmashauri ambazo tumezitolea mfano hazijapeleka kwa miaka mitatu mfululizo fedha za vijiji na mitaa. Halmashauri hizo ni Halmashuri ya Kilwa, Halmashauri ya Ngara, Halmashauri ya Hai, Halmashauri ya Rombo, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiwauliza hata fedha hizi kisingizio ni hicho hicho; maagizo kutoka juu. Sasa najiuliza, kwa Halmashauri ambazo wanaweza kupeleka fedha hivi wao wanafanya nini kutengeneza madawati? Kama siyo kwamba ni uongozi mbovu uliopo katika Halmashauri hizi wanashindwa kukaa na kuamua watatengeneza vipi madawati wanakwenda kuchukuwa haki ambayo siyo ya kwao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hatutaondoa tatizo la rushwa katika ofisi za Serikali za Mitaa katika ofisi za vijiji kwa sababu ofisi za Serikali za mitaa na ofisi za vijiji hawana nyenzo za kufanyia kazi. Ile haki yao ambayo wanatakiwa kuipata hawaipati; unakuta Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji na Mtaa, hana hata fedha ya kununua karatasi, unategemea nini kwa mwananchi aliyekwenda ana shida yake? Kama siyo kwamba ataombwa fedha ili aweze kukamilishiwa shida iliyompeleka ofisini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niishauri Serikali badala ya fedha hizi kuzipeleka kwenye Halmashauri zetu na Halmashauri zinafanya ni shamba la bibi basi fedha hizi zipelekwe moja kwa moja katika vijiji na mitaa ziweze kuwafikia walengwa vinginevyo kila siku tutapiga kelele Wenyeviti wa Serikali za Vijiji na Mitaa hawawezi kupata haki yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa haraka haraka nikitoka hapo niende, suala la Wakuu wa Idara na Vitengo kukaimu. Halmashauri nyingi zimekuwa zikikaimiwa nafasi hizi lakini cha kusikitisha wengine makuwa wakikaimu kwa muda mrefu na matokeo yake nafasi ile anakuja kupewa mtu mwingine, yeye aliyekaimu hapewi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema aliyenijalia afya njema nikaweza kuchangia Wizara ya Afya kwa siku ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa inayoifanya. Niseme, maendeleo ni hatua kwa hatua. Kama ambavyo kwenye familia zetu huwezi kufanya kila kitu kwa siku moja, leo hii hata ukipata mabilioni ya pesa ukinipa siwezi nikamaliza matatizo niliyonayo na ndivyo ambavyo Serikali ya Awamu ya Tano inavyokwenda kutekeleza miradi ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitaje hatua kwa hatua ambayo yamefanyika katika Wizara ya Afya. Hatua ya kwanza, upandikizaji wa kifaa cha usikivu kwa watoto; hatua ya pili, upandikizaji wa figo na hatua ya tatu, chanjo ya saratani. Hizi ni hatua ambazo Serikali ya Awamu ya Tano imezifanya katika Wizara ya Afya kuhakikisha kwamba afya zetu zinakwenda kuimarika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hatua hizo, kipekee kabisa naipongeza Wizara ya Afya, Mheshimiwa Ummy na Naibu wake na watendaji wake wote kwa kushirikiana na TAMISEMI kuhakikisha kwamba tunakwenda kuboresha na kujenga vituo vyetu vya afya katika kata zetu. Yeye kama mama ameweka historia katika Wizara ya Afya, kama mama ameweka historia katika Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisiishie kupongeza watu walioko juu tu, nampongeza RMO wangu wa Mkoa wa Shinyanga kwa kazi kubwa anayoifanya kwa sababu mpaka sasa hivi chanjo ya saratani ya shingo ya kizazi kwa Mkoa wa Shinyanga semina imekwishaanza. Wananchi wa Shinyanga wanapewa semina na hivi tunavyoongea, leo kuna semina inaendelea kwa ajili ya chanjo ya saratani ya kizazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie moja kwa moja sasa katika hoja nilizonazo. Katika hatua ambazo wamepitia Wizara ya Afya, niwaombe NHIF ni kwa nini yale malipo ambayo mmeyaweka kwa vikundi hamtaki kuyaweka kwa mtu mmoja mmoja? Watu wengi hawapo kwenye vikundi,
lakini wana utayari wa kuchangia hiyo shilingi 76,000 kwa ajili ya Bima ya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashauri NHIF ruhusuni Bima ya Afya shilingi 76,000 ichangiwe kwa mtu mmoja mmoja na isiwe kwa vikundi. Tunakwenda kuwanyima haki wananchi ambao wako tayari kuchangia Bima ya Afya, kwani vikundi na mtu mmoja mmoja vina tofauti gani? Kwa sababu kama kikundi kina watu 20, mwisho wa siku watu watabaki 20 wale wale. Kwa hiyo, nawashauri muibadilishe iende ikachangiwe na mtu mmoja mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashauri NHIF siyo kwamba wananchi wetu ni wagumu kulipa Bima ya Afya, tatizo elimu haipo. Shukeni mpaka kule chini, katoeni elimu kwa wananchi wetu, nini maana ya Bima ya Afya? Mtu akishaugua, ukishaenda hospitali, kama una Bima ya Afya ndiyo utatambua nini maana ya Bima ya Afya na kama hauna, utajuta kwa nini hukuwa na Bima ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nawashauri NHIF, shukeni kule chini kwa wananchi wetu na ninawakaribisha Mkoa wa Shinyanga, njooni mtoe mafunzo kwa wananchi wa Mkoa wa Shinyanga ili waweze kujiunga na Bima ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nijielekeze katika kitabu cha Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 118. Ni mwaka wa nane niko ndani ya ukumbi huu wa Bunge, hakuna mwaka ambao sijawahi kusemea Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga. Nimeangalia katika kitabu cha Mheshimiwa Waziri; ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga haimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa, Mheshimiwa Ummy ni ndugu yangu na rafiki yangu, lakini kwa hili nitakamata shilingi. Ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga una miaka zaidi ya mitano toka umeanza. Jengo lililokamilika pale ni jengo la utawala na wagonjwa wa nje. Unawezaje kusema kwamba pale tumekamilisha ujenzi? Nawashauri Wizara ya Afya, hakuna sababu ya kwenda kuanzisha majengo mapya wakati yale ambayo yameshaanza hamjayakamilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili iitwe Hospitali ya Rufaa kuna mambo mengi ambayo yanatakiwa kukamilishwa. Kuna jengo la mama na mtoto linatakiwa lijengwe ambalo hatujaanza hata msingi, jengo hili la mama na mtoto litakuwa na maabara na chumba cha upasuaji ndani yake. Kwa nini msitupe angalau shilingi bilioni tatu tukaenda kujenga jengo hilo la mama na mtoto ndani yake kuna chumba cha upasusaji, kuna maabara, ili huduma zikawa zinafanyika pale? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jengo ambalo wanasema kwamba liko tayari la utawala, halina hata furniture moja. Sasa tunakwendaje kutoa huduma za Hospitali ya Rufaa wakati tuna jengo la utawala peke yake? Hapo utasema kuna huduma inafanyika? Hapana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hili naomba Wizara ya Afya litizameni, mkakamilishe ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Shinyanga ili nisisimame tena hapa kila siku kusema Shinyanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Shinyanga una upungufu mkubwa wa watumishi. Nianze na Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga. Halmashauri hii watumishi wanaotakiwa ni 571; watumishi waliopo ni 196 tu; upungufu ni 375; Halmashauri ya Mji wa Kahama ina upungufu wa watumishi 214; Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga ina upungufu wa watumishi 189.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaomba Wizara ya Afya, upungufu huu wa watumishi unasababisha kwenda kutukanwa watumishi wetu wa afya kwamba hawafanyi kazi inavyotakiwa. Hii ni kwa sababu wanafanya kazi kwa kiwango kikubwa. Unakuta mtu mmoja anaandika, anakwenda kutoa dawa, anakwenda kuzalisha mtu huyo huyo mmoja. Matokeo yake, wale ni binadamu, kuna muda unafika mtu amechoka, anaweza akakujibu vibaya mgonjwa ukachukia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hili lote lipo ndani ya Wizara ya Afya, liangalieni suala la upungufu wa watumishi katika sekta ya afya, limekuwa ni tatizo kubwa na hivi tunavyokwenda kujenga na kuboresha vituo vyetu vya afya ni lazima tuhakikishe kwamba tuna watumishi wa kutosha, kwa sababu huduma nyingi zaidi zitakuwa zimeongezeka katika vituo vyetu vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho lakini siyo kwa umuhimu, naomba nisemee delivery pack. Kwa uelewa wangu, huduma ya mama na mtoto siyo kwamba imeondolewa kwenda kutolewa bure kule kwenye zahanati zetu na vituo vyetu vya afya kwa sababu ile dawa wanayochomwa akina mama wakati wa kujifungua bado itatoka kama kawaida na gloves zitapatikana kama kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilivyoielewa, sijui kama niko tofauti, Mheshimiwa Waziri atasema; nilivyoielewa delivery pack, ni ule mfuko uliobeba vitu vyote ambao unamfanya mama huyu mjamzito aende nao hospitali siku ya kujifungua ukiwa na vifaa vyote tofauti na kubeba kanga na vitenge na vitu vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata fursa hii ya kuchangia bajeti iliyopo mbele yetu ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.Kwanza naunga mkono hoja iliyo mbele yetu na nitumie fursa hii kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa inayofanya katika shughuli za maendeleo. Hongera sana Mheshimiwa Rais, Dokta John Pombe Magufuli, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na bila kumsahau Mheshimiwa Waziri Jafo na Manaibu wake wote wawili, hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali kwa kuamua kwa dhati kuboresha huduma za Mama na mtoto katika vituo vyetu vya afya Mkoa wa Shinyanga. Tumepata vituo sita ambavyo kwa sasa kazi ya ujenzi inaendeleea ukingoni. Tunashukuru sana kwa niaba ya wanawake wa Shinyanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, pamoja na shukurani zangu hizo kwa sekta ya afya, nina ombi maalum ambalo kila ninapopata nafasi ya kuongea lazima niseme chondechonde, Mheshimiwa Waziri naomba sana mwaka huu wa fedha Serikali iweze kuiona Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga kwa jicho la huruma. Naomba tupatiwe fedha ya kutosha katika ujenzi wa hospitali ya Wilaya ambao umeanza kwa muda mrefu sana ili kuweza kuunga mkono jitihada na nguvu za wananchi hatimaye hospitali hii ianze kutoa huduma zilizokusudiwa. Mheshimiwa Naibu Waziri, TAMISEMI wakati anajibu swali humu Bungeni alisema, kwa mwaka huu wa fedha 2018/2019, hospitali 67 zitajengwa; naomba sana miongoni mwa hizo 67 na hospitali ya Wilaya ya Shinyanga iwekwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu ipatiwe fedha za ujenzi wa hospitali ya Wilaya kwa kuwa ni Halmashauri mpya hivyo, huduma hii ni muhimu kwa wananchi wa Ushetu na kuwa na hospitali za Wilaya itasaidia kupunguza msongamano katika hospitali ya mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu pia, naomba mnapotoa fedha za kutosha katika ujenzi wa hospitali ya Wilaya, nashauri utumike utaratibu wa force account ambao unaonekana kuwa na tija kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Shinyanga ipatiwe fedha za kutosha ili iweze kukamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe pia kilio changu katika sekta ya elimu, Halmashauri ya Shinyanga ina shule moja ambayo kwa miaka mitatu mfululizo imekuwa ikifanya vizuri katika mitihani ya darasa la saba. Shule hii inaitwa Shule ya Msingi Masunula. Shule hii haina nyumba hata moja ya mtumishi, Walimu wanaishi katika nyumba za kupanga huko mtaani. Naomba sana shule hii itazamwe kwa jicho la huruma ili Walimu hawa tuwape nguvu ya kuendelea kufundisha watoto wetu vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuwapongeza wananchi wa Kata ya Solwa wakiongozwa na Diwani wao, wamekubaliana kwa pamoja, wameanza kampeni na wameweza kujenga vyoo katika shule zote za msingi katika kata yao na wamejenga madarasa matano, Ofisi ya Walimu na wamejenga na kuchimba vyoo matundu sita na Halmashauri imechangia upauaji wa majengo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa uamuzi huu wa wananchi wa Kata ya Solwa, naiomba Serikali iwaunge mkono wananchi hawa ili waweze kukamilisha ujenzi huo wa shule mpya ya msingi inayoitwa Solwa B ambapo ndiyo wamejenga madarasa matano, Ofisi ya Walimu na vyoo matundu sita. Naomba wananchi hawa wapewe fedha ya kutosha ili panapo majaliwa 2019 shule hii iweze kupokea watoto wa darasa la kwanza kwani wameonesha kilio chao kwa kufanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nitoe ushauri upande wa fedha za wanawake na vijana; naomba vikundi hivi wapewe vitendea kazi na siyo fedha. Hii inaweza kuwa na matokeo mazuri zaidi katika utekelezaji wa mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kuiomba Serikali iweze kuajiri watumishi zaidi hususani sekta ya afya kwa Mkoa wa Shinyanga, kwani kuna upungufu mkubwa sana kuanzia hospitali ya mkoa hadi zahanati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi hii na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii. Awali ya yote, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema aliyenijalia pumzi na uzima na hatimaye kuweza kuchangia hotuba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, niipongeze Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi kubwa ambayo inaifanya hususani katika usambazaji wa maji ingawa kuna kasoro ndogo ndogo ambazo zipo katika usambazaji wa maji. Naamini Waziri,

Naibu Waziri na watendaji kwa sababu wako hapa watajipanga kuona wanatatuaje changamoto hizo zilizopo hususani katika Mkoa wa Shinyanga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nianze na mradi mkubwa wa maji ya Ziwa Victoria ambao ulianza Mkoa wa Shinyanga kwa mwaka 2014. Kulikuwa na utaratibu wa vijiji vilivyopo ndani ya kilometa 12 kupatiwa maji, hiyo ni toka mwaka 2014, lakini mpaka hivi tunavyoongea imekuja awamu nyingine ya usambazaji wa maji ya Ziwa Victoria kuna vijiji ambavyo havijapata maji. Naomba nitaje baadhi ya vijiji hivyo, vijiji vya Ntobo, Nyamigege, Kula, Buchambaga, Busangi na vingine vingi ambako bomba la Ziwa Victoria limepita kwa mara ya kwanza. Niiombe Wizara ya Maji waangalie wanakwendaje kumaliza vijiji hivi vilivyopo ndani ya kilometa 12 kwa mradi wa awamu ya kwanza ya Ziwa Victoria ambavyo mpaka leo hii hawajapata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiwa katika Mkoa wangu wa Shinyanga, naomba niizungumzie Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu. Mkoa wa Shinyanga mradi mkubwa wa maji ya Ziwa Victoria ndiyo unakwenda kupeleka maji Mkoa wa Tabora. Nasikitika kusema kwamba Halmashauri ya Ushetu haina kijiji hata kimoja ambacho kinapata maji ya mradi wa Ziwa Victoria. Ukiangalia Kahama Mji na Ushetu ni jirani sana na Ushetu imetokana na Kahama Mji inanipa taabu ni kwa nini Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu hamjaiweka kwenye mpango wa mradi wa maji ya Ziwa Victoria na ukiangalia Ushetu imezaliwa kutoka Kahama. Niiombe Wizara mjipange muangalie Halmashauri ya Ushetu wanawezaje kupata maji ya Mradi wa Ziwa Victoria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niingie katika Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu. Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu ina mradi mkubwa wa maji wa Ziwa Victoria ambao mpaka sasa hivi unatekelezwa na baadhi ya maeneo yanapata maji. Vijiji vinavyopata maji ni Kolandoto, Maganzo, Mwadui na Munze ambapo ni Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nimesema katika utekelezaji wa mradi huu, kuna matatizo ambayo yanajitokeza. Ukiangalia pia katika Halmashauri Wilaya ya Kishapu sehemu ambapo bomba kuu linapita kuna vijiji ambavyo viko ndani ya kilometa tatu mpaka tano yaani wanatizama bomba lakini hawana maji, haipendezi. Anawezaje mwananchi wa kawaida kuangalia yeye anahangaikia ndoo moja ya maji lakini bomba analitizima linapita kilometa tatu kutoka hapo yeye alipo? (Makofi)

Wizara ya Maji kaeni mjipange, haipendezi na kutakuwa na uharibifu tusipokuwa makini, mtu hawezi kupata shida ya maji wakati bomba analiona linapita kwenye eneo lake. Vijiji hivyo vilivyopo katika Halmashauri ya Kishapu ni Kijiji cha Songwa, Seseko, Nyenze, Kakola, Igaga, Lubaga, Uchunga na Mwadui Luhombo. Naomba Wizara ya Maji mjipange muone vijiji hivyo vinakwendaje kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sasa niingie katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga ambayo mimi ndiyo naihudumu na ninakoishi. Nianze moja kwa moja na sehemu ninayotoka, msahau kwao ni mtumwa.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana wakati wa bajeti nilisimama ndani ya ukumbi huu nikaipongeza Serikali na nikaishukuru Wizara ya maji kwa mradi mkubwa wa maji ambao kwa kitabu cha bajeti cha mwaka jana, ninacho hapa, ukiangalia ukurasa wa 70 kitabu cha mwaka jana mradi mkubwa wa Ziwa Victoria ulikuwa unasomeka kwa ajina la Solwa, Tinde, Nzega, Igunga, Uyui na Tabora. Nilisimama hapa na kuishukuru Serikali, lakini naomna kusema sijui Wizara wameepitiwa, Mheshimiwa Waziri na Naibu wako na watendaji wenu mpo hapa. Mimi naomba mnijibu, kitabu chenu cha mwaka huu cha bajeti jina la mradi limebadilika, mradi huu umeenda kuondoa jina la Tinde, Mheshimiwa Waziri naomba nipate majibu. Ni kwa nini jina la mradi limebadilika? Katika hotuba yako ya mwaka huu ukurasa wa 46 mradi unasomeka Solwa, Nzega, Uyui, Igunga na Tabora; Tinde tena haimo, kama mmepitiwa naomba muangalie.

Mheshimiwa Spika, ukizingatia Mheshimiwa Rais alisimama Tinde na akasema, mradi mkubwa wa maji unatoka Solwa, Tinde, Nzega na kwenda mpaka Tabora. Lakini nashangaa hotuba ya mwaka huu labda bajeti ya mwaka huu mmekwenda mradi wa maji wa Tinde. Ninaomba nipate majibu, Mheshimiwa Waziri tumeshasema sana na wewe, nimekufata mara nyingi, lakini kunyamaza si majibu, watendaji wako hapa naomba nipate majibu, wananchi wa Tinde wapate majibu, mradi wa maji wa Ziwa Victoria ni kwa nini mwaka huu wa fedha haupo katika mradi wenu ambao unasomeka? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiwa hapo hapo Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga naomba nisemee mradi wa maji tena mwingine wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga ambao ni mradi wa Ziwa Victoria wa Kijiji cha Masengwa.

Mheshimiwa Spika, kuna fedha ambazo mradi huu ilikuwa imesha pata, lakini mradi huu unatoka Manipsaa ya Shinyanga na mradi huu ukifika katika kijiji cha Masengwa unaweza ukahudumia Kata zingine ambazo hazina maji. Ikiwemo Kata ya Samuye, Kata ya Usanda pamoja na Kata ya Mwamala. Kata hizi zinaweza kupata maji kupitia kijiji cha Masengwa.

Mheshimiwa Spika, na niseme mradi huu halmashauri yangu imesha andika barua nyingi Wizara ya Maji, kuanzia mwezi wa tatu mpaka hivi ninavyoongea Wizara ya Maji haijajibu. Kuna matatizo matatu ambayo yanaonekana yapo, Halmashauri imeomba Kibali cha kutumia maji ya SHUWASA kutokana na kwamba, Masengwa ipo nje na Manispaa ya Shinyanga, hivyo hawarushusiwi kutumia maji kwa sababu wao wapo vijijini. Halmashauri imeomba kibali Wizara ya Maji lakini mpaka hivi leo ninavyoongea kibali hakijapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kikwazo kingine cha pili, wizara haijatoa maelekezo ya namna ya usimamizi kutoka Wizara ya Maji kwenye Halmashauri husika, Halmashauri imeandika barua wameshapiga simu wamekuja wenyewe mpaka ofisini kwenu lakini majibu hayajapatikana mpaka sasa hivi.

Mheshimiwa Spika, kikwazo cha tatu katika mradi huu, vetting kutoka katika Mwanasheria Mkuu wa Serikali haijapata majibu Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga. Kwahiyo naiomba Wizara mtuambie, mradi huu wa Masengwa mna mpango nao gani? Kwa sababu mna utaratibu wenu wa matumizi ya fedha hizi za maji mna siku 21 sijui siku 35 siku hizi zikiisha manakwenda kuwanyang’anya Halmashauri fedha. Naomba majibu kwa nini wizara haitekelezi wala haijibu maandiko yanayoletwa na Halmashauri.

Nakushukuru naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kunijaalia afya na uzima na hatimaye nimeweza kusimama ndani ya ukumbi wako huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nami nianze kuchangia bajeti ya Ofisi ya Rais TAMISEMI. Leo nitakuwa tofauti sana na mlivyonizoea, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi kubwa ya utekelezaji wa miradi mikubwa ya Kitaifa ndani ya miaka mitatu. Ununuzi wa ndege, reli ya standard gauge, mradi mkubwa wa umeme wa Mto Rufiji, Vituo vya Afya 352 na elimu bure shilingi bilioni 20.8 kila mwezi. Mheshimiwa Rais anastahili pongezi kubwa. Kikubwa kwake tumwombee dua kwa Mwenyezi Mungu, ampe afya njema, umri mrefu aende kuwatumikia wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Jafo, Naibu Mawaziri na Watendaji wote katika ofisi yake. Mmekuwa mkifanya kazi kubwa ndani ya ofisi ya TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimejionea mambo makubwa ambayo yamefanywa katika Mkoa wa Shinyanga na Serikali ya Awamu ya Tano. Nianze kwenye elimu. Mkoa wa Shinyanga katika Shule za Sekondari na Shule za Msingi kila mwezi tunapata shilingi milioni 594, kwa nini nisisimame na kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania? Mkoa wa Shinyanga kwa mwaka huu wa fedha uliokwisha tumepata fedha za kujenga na kukamilisha maboma shilingi bilioni tatu ndani ya Mkoa wa Shinyanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haitoshi, nimetazama ndani ya kitabu cha Mheshimiwa Jafo, hata mwaka huu tumepangiwa fedha tena kwenda kukamilisha maboma kwenye shule zetu, shilingi milioni 425. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye ujenzi wa Vituo vya Afya. Katika vituo 352 vilivyojengwa nchi nzima, Mkoa wa Shinyanga tumepata vituo tisa ambavyo vimejengwa. Thamani yake ni shilingi bilioni 3.9. Naishukuru sana Serikali na ninampongeza sana Mheshimiwa Rais. Mheshimiwa Jafo, peleka salamu za wananchi wa Shinyanga kwa Mheshimiwa Rais. Wananchi wa Shinyanga na wanawake wa Mkoa wa Shinyanga tunamshukuru sana kwa kazi kubwa ambayo ameifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kusema kwamba toka nimeingia ndani ya ukumbi huu wa Bunge, mitaa hii hapa ninayokaa nilikuwa nikisimama tu kuchangia TAMISEMI wanasema, Hospitali ya Wilaya. Hilo ndilo lilikuwa neno langu kubwa. Hakuna mwaka ambao nilisimama na nisiseme ujenzi wa hospitali ya Wilaya ya Shinyanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natumia fursa hii kuishukuru sana Serikali, imetupatia fedha, shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Shinyanga. Haitoshi, katika Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu tumepatiwa pia shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. Haitoshi, Halmashauri ya Msalala tumepewa shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya Wilaya ya Shinyanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini bado nimetazama katika kitabu cha Hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, tumetengewa shilingi milioni 400 kwa mwaka huu wa fedha kwa ajili ya kwenda kuboresha Vituo vyetu vya Afya. Nitumie fursa hii kuishukuru Serikali na kuipongeza kwa kazi kubwa ambayo wameifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, aombaye hupewa na abishae hufunguliwa. Baada ya shukurani zangu hizo, namwomba sasa Mheshimiwa Jafo, kwa yale mambo yote makubwa ambayo wameyafanya ndani ya Mkoa wa Shinyanga na Halmashauri zake zote, kuna zahanati ambazo zilianzishwa kwa lengo la kuwa Vituo vya Afya; na alipokuja Makamu wa Rais, Mheshimiwa Mama Samia nilizisema zahanati hizi katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga; Zahanati ya Solo na Zahanati ya Ihalo. Wananchi kwa nguvu zao wamejenga majengo mengi, wodi za wazazi na watoto. Tunaomba angalau tupate hata shilingi milioni 200 ili zahanati hizi ziende zikafanye kazi kubwa ya kuwahudumia wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado haitoshi, alipokuja Mheshimiwa Waziri Mkuu mwaka 2018 niliomba katika Halmashari ya Wilaya ya Kishapu Kituo cha Afya cha Nobola. Kituo kile kinahudumia Tarafa nzima katika Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu. Naombe nao muwafikirie waweze kupata fedha kile kituo kiweze kuboreshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa elimu kwa Mkoa wa Shinyanga, namwomba sana Mheshimiwa Jafo, katika Shule za Sekondari, tuna shule ambazo nimekuwa nikizisemea; Shule ya Sekondari Samuye, shule hii iko katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga. Tatizo kubwa la shule hii, hii ni Shule ya Kitarafa, wanafunzi wengi wanatoka mbali. Ombi langu kwako ni bweni tu wala sina ombi lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kuiombea Shule ya Sekondari ya Ukenyenge ambayo pia ni Shule ya Kitarafa iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu. Ombi kubwa katika shule hii ni bweni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwekiti, haitoshi. Katika Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga nitumie fursa hii kuiombea fedha Shule ya Sekondari ya Old Shinyanga ambayo pia ni Shule ya Kitarafa. Ombi langu kubwa ni ujenzi wa bweni ili tuwaondoe wasichana kurubuniwa barabarani wanapokuwa wanaenda shule na kurudi majumbani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kuzisemea shule zetu za msingi. Alipokuja Mheshimiwa Waziri Mkuu tukiwa Kishapu niliiombea Shule ya Msingi Beredi na Shule ya Msingi Mwangili. Mheshimiwa Waziri Mkuu alilipokea na aliyekuwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Kakunda aliahidi kwamba shule hizi zitaletewa fedha. Shule hizi zina msongamano mkubwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii. Awali ya yote, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema aliye nijalia afya na uzima na hatimaye nimeweza kusimama kuchangia bajeti ya Wizara ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kwa pongezi katika Wizara ya Maji. Nisipolisema hili, Waziri, Naibu Waziri na Watendaji wao watanishangaa sana, kwa sababu nimezunguka sana, katika Ofisi za Wizara ya maji na hatimaye kile nilichokuwa nakifuata kimekamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii, kuwashukuru sana, Wizara ya Maji na Watendaji wote, Kata ya Tinde na vijiji vyake vyote vilikuwa vimesahaulika kwenye Mradi wa Maji ya Ziwa Victoria. Nilisimama humu ndani nikasema, namshukuru sana Mheshimiwa Eng. Kamwelwe, alilipokea, tukaa kikao Ofisini kwake na Watendaji wake na hatimaye mradi ule sasa unakwenda kuanza kutekelezwa mwezi huu wa Mei. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana kwa kazi kubwa ambayo mmeifanya, vijiji vyote vilivyopo Kata ya Tinde, vinakwenda kupata maji ya Ziwa Victoria. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri Prof. Mbarawa, yale yaliyofanywa na Mheshimiwa Eng. Kamwelwe uyaendeleze na mradi ule uende kukamilika. Mradi ule unaenda kutekelezwa kuanzia mwezi huu wa Mei na utafanya kazi ndani ya miezi saba, nikuombe sana, uende ukasimamie na mradi huu uweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nisiishie mradi huo, nilisimama ndani ya Bunge hili lakini nimezunguka sana Ofisi za Wizara ya Maji kwa ajili ya mradi wa maji Kata ya Masengwa. Mradi huu umeanza kufanya kazi na unaendelea vizuri. Niwashukuru sana Wizara ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo kubwa lililopo, fedha kwa Timu iliyoundwa kwa ajili ya kufuatilia mradi huo wa maji hazijapelekwa hata senti tano. Hivyo, tunaipa kazi kubwa Timu ya ufuatiliaji kufanya kazi kwa kutumia pikipiki kwa sababu hawajawezeshwa kwenda kusimamia mradi huu. Niwaombe sana Wizara ya Maji wapeni Halmashauri fedha hizo ili waweze kuusimamia Mradi wa Masengwa kama ambavyo ilikuwa imepangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, akini Mradi wa Masengwa wameleta hati ya madai ya shilingi milioni 94 kwa ajili ya mradi huu, malipo hayo bado hayajafanyika. Niwaombe mtoe malipo hayo ili kazi hii iweze kuendelea na kuweza kukamilika mapema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu katika Mradi wa Maji wa Masengwa. Mradi huu una zaidi ya shilingi bilioni nne, ni mradi mkubwa sana na kuna tenki kubwa ambalo linakwenda kujengwa. Kulikuwa na mradi awamu ya kwanza, awamu ya pili na awamu ya tatu. Awamu ya kwanza, ndiyo huu ambao unatekelezwa. Niwaombe sana Wizara ya Maji, toeni pesa kwa ajili ya usanifu kwa awamu ya pili ya Mradi wa Maji wa Masengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, awamu ya pili ya Mradi wa Masengwa utakwenda kutekeleza Vijiji vya Ishinaburandi, Isela, Idodoma na Ibingo. Hawa watu vijiji vyote hivi watanufaika kupata maji katika mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuzungumzia Mradi wa Maji wa Masengwa, naomba nijikite katika vijiji ambavyo vipo nje na Mradi wa Maji ya Ziwa Victoria. Vijiji hivi ambavyo haviko ndani ya kilomita 12, haviguswi popote na Mradi wa Maji ya Ziwa Victoria lakini hakuna namna yoyote ya vijiji hivi kuvipatia maji. Vijiji hivi viko 23, naomba nivitaje baadhi. Vijiji vya Mwasenge, Nyang’ombe, Nyaligongo, Bushoma, Kilimawe, Mwamala, Bugogo, Masonula, Igalamya, Singita, Chabuluba, Mwamkanga, Msalala, Supigu na Masokelo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vijiji hivi 23, vina idadi ya watu 59,241. Wizara ya Maji mmejipangaje kuhakikisha kwamba vijiji hivi 23 tunaleta mpango mkakati wa kuhakikisha kwamba watu hawa na wao wanakwenda kupata maji. Akina mama wanahangaika, hawawezi kufanya shughuli zozote za kiuchumi kwa kutafuta maji, ukiangalia Mradi wa Maji wa Ziwa Victoria uko mbali nao, je, Wizara ina mpango gani wa kuhakikisha vijiji hivi na wao sasa wanakwenda kupata maji ya uhakika ili na akina mama hawa waweze kufanya kazi zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hilo, niingie katika vijiji ambavyo viko ndani ya kilomita 12 lakini havijapata maji mpaka leo. Toka awamu ya kwanza ya Mradi wa Maji ya Ziwa Victoria vijiji hivi havijapata maji na viko ndani ya kilomita 12. Kila nikisimama ndani ya Bunge hili huwa nasema, naomba pia nivitaje tu. Vijiji hivi viko 22 toka awamu ya kwanza ya Mradi wa Maji ya Ziwa Victoria. Vijiji hivi vina idadi ya watu 58,465 ambao wako ndani ya kilomita 12 lakini hawapati maji ya Ziwa Victoria wanayaona yanakwenda kwa wenzao. Vijiji hivi ni Mawemilu, Buduhe, Azimio, Mwandutu, Ibubu, Mapingiri, Mwashagi, Mwamala, Mwabagehu, Mwashilugura, Mwambasha, Mwalukwa, Bulambila na Shatimba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haipendezi toka awamu ya kwanza ya Mradi wa Maji ya Ziwa Victoria, hawa watu wanapewa matumaini kwamba watapewa maji, wako ndani ya kilomita 12, lakini mpaka tunakwenda awamu nyingine sasa hawajapata maji.

Je, Wizara mna mpango gani kuhakikisha vijiji hivi 22 vinakwenda kupata maji kwa sababu wanaishi kwa matumaini wakitegemea kwamba siku moja na wao watapata maji kwa sababu utaratibu unawaruhusu wako ndani ya kilomita 12. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusemea hilo, naomba niingie katika Manispaa ya Shinyanga, Mradi wa Maji wa Galamba. Mradi huu umeanza kutekelezwa ndani ya Manispaa ya Shinyanga lakini kwa masikitiko makubwa, toka Agosti, 2018, Halmashauri imeleta hati ya malipo ya shilingi milioni 131 mpaka sasa hivi fedha zile hazijalipwa na mradi ule umesimama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tunaposema Wizara ya Maji kuna tatizo huko chini angalieni. Inawezekana huku juu mko vizuri sana lakini Mheshimiwa Waziri hebu jaribu kuangalia Ofisini kwako kuna shida gani kwa sababu Wabunge wengi pia wanalalamika hati hizi zikiletwa fedha hazitolewi kwa wakati. Fikiria toka Agosti, 2018, fedha hizi hazijalipwa mpaka leo, kuna tatizo gani katika Mradi wa Maji wa Kijiji cha Galamba katika Manispaa ya Shinyanga? Nimuombe sana Waziri alifanyie kazi suala hili na nitafurahi kama nitapata majibu kabla hujahitimisha mjadala wako kujua Mradi wa Maji ya Galamba mmewapelekea pesa au unanipa majibu gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa. Tunazunguka kukagua miradi mingi katika Halmashauri hapa nchini lakini katika miradi mibovu ambayo tunakutana nayo ni miradi ya maji. Sijui kuna tatizo gani, miradi mingi unakuta ama maji yanatoka lakini tenki linavuja. Serikali imewekeza fedha nyingi lakini unakuta mradi ule hauna tija kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mimi najiuliza miradi ile inasimamiwa na Wahandisi haya matatizo yanatokea wapi? Mheshimiwa Waziri jaribu kuangalia, fedha nyingi ya Serikali inakwenda kule lakini miradi mingi ina matatizo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Azza, muda wako umekwisha.

MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, naunga mkono. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa fursa hii. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya na uzima na hatimaye nimeweza kusimama na kuweza kuchangia bajeti ya Wizara ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa pongezi nyingi kwa Wizara ya Afya, kwa Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wao wote katika Wizara ya Afya. Kazi mnayoifanya ni kubwa na hakika mmeleta mabadiliko makubwa katika Sekta ya Afya. Hongereni sana. Mwenye macho haambiwi tazama, yanaonekana yale yote ambayo mmeyafanya katika Sekta ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza pia kwa uboreshwaji wa huduma katika hospitali zetu maalum; Hospitali ya Ocean Road, Hospitali ya Jakaya Mrisho Kikwete ya kitengo cha Moyo na hospitali zote za mikoa, Wilaya na uboreshwaji wa vituo vya afya. Hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu muda ni mfupi, niende moja kwa moja katika Mkoa wangu wa Shinyanga ili niwasemee wananchi walionileta ndani ya ukumbi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuisemea Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga. Mwaka 2018 nilisimama humu ndani nikasema kuhusu ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga. Ujenzi huu umeanza bajeti ya mwaka 2013/2014; kuna jengo moja kubwa ambalo limekamilika, jengo la utawala. Jengo hili wanaishi popo, halina kazi yoyote. Namshukuru Mheshimiwa Waziri, tarehe 24/01/2019 alitembelea ujenzi wa hospitali hii katika Mkoa wa Shinyanga na baada ya kutembelea alitoa ahadi kwamba atatoa fedha, shilingi bilioni 2.5 kwa ajili ya maternity block ili hospitali ile ianze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namkumbusha Mheshimiwa Waziri wa Afya, ahadi yake Wana-Shinyanga tunaisubiri kwa sababu ulisema jengo lile litakamilika na mwishoni mwa mwaka huu hospitali ile itaanza kufanya kazi, sijui umekwamishwa na kitu gani? Nakuomba sana, nakusihi sana, ahadi ni deni. Vitabu vya dini vinasema, ukiahidi halafu bahati mbaya Mwenyezi Mungu ikatokea lolote, umekufa deni. Naomba ahadi hii uitekeleze Wana-Shinyanga tunaisubiri kwa hamu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa bajeti mwaka 2018 nilisimama nikasema ubovu wa X-Ray machine katika Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga. Namshukuru Mheshimiwa Waziri pia alipokuja Shinyanga alituahidi wana Shinyanga kwamba atatuletea X-Ray machine ya kisasa, lakini mpaka sasa hivi hatujapata X-Ray machine ile.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado namkumbusha Mheshimiwa Waziri, aliahidi mwenyewe na Wana-Shinyanga tunasubiri na watendaji wake wanamsikia. Ahadi ni deni, tunasubiri X-Ray machine ya kisasa kwa sababu tuliyonayo ni mbovu na haifanyi kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, niendelee kukumbusha ahadi za Serikali. Wakati wa ziara ya Mheshimiwa Waziri Mkuu katika Mkoa wa Shinyanga, nilisimama katika Jimbo la Ushetu nikaomba ambulance kwa ajili ya Jimbo la Ushetu. Bahati nzuri Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokea ombi hilo na akatuahidi kwa Mkoa wa Shinyanga kutuletea ambulance nne na Mheshimiwa Waziri mwenyewe akiwepo. Tunahitaji Ambulance kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Tinde, kwa ajili ya Jimbo la Ushetu, Jimbo la Msalala na Jimbo la Kishapu. Ahadi hizo hazijakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kusemea kuhusu watumishi katika Mkoa wa Shinyanga. Watumishi wa Idara ya Afya katika Mkoa wa Shinyanga mahitaji ni 3,606, waliopo ni 1,446 na upungufu ni 2,160. Naomba Wizara, tutazameni, mmeboresha vituo vya afya lakini vituo hivi kama havina watumishi bado vitakuwa haviwezi kufanya kazi vizuri. Upungufu tulionao ni mkubwa, watumishi waliopo wanalazimika kufanya kazi kwa shida kwa sababu wanafanya kazi ambazo zinawazidi uwezo. Watumishi ni wachache katika vituo, kwa hiyo, tunawaomba sana fanyeni utaratibu muweze kutuongeza watumishi katika idara ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali katika ujenzi wa vituo vya afya 11 ndani ya Mkoa wa Shinyanga. Vituo hivi vimekamilika, lakini kinachonisikitisha mpaka sasa hivi hatujapata vifaa tiba. Kwa hiyo, niwakumbushe Wizara ya Afya, vituo hivi vinahitaji kufanya kazi ili viende vikatimize lengo ambalo mmelikusudia.

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo hili ni zuri na linapendeza hata ukiangalia hali ambayo inaonekana katika vituo vyetu vya afya, lakini haviwezi kufanya kazi kwa sababu lengo lililokusudiwa halijaanza kufanya kazi. Hakuna vifaa ambavyo vimeletwa katika vituo vyetu vyote 11 vilivyopo ndani ya Mkoa wa Shinyanga na hivyo lengo lile la kwenda kufanya upasuaji bado halijaanza kufanya kazi. Kwa hiyo, niwaumbushe mtuletee vifaa tiba katika vituo 11 ambavyo mmetujengea katika Mkoa wetu wa Shinyanga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudie kusema kwamba naipongeza sana Serikali, nilikuwa nikisema sana kuhusu Hospitali ya Wilaya ya Shinyaga, hospitali sasa hivi inaendelea. Nawashukuru sana kwa kazi kubwa ambayo mmeifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naona unanitazama, nakushukuru na ninaunga mkono hoja. (Makofi)