Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Dr. Jasmine Tiisekwa Bunga (7 total)

MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, napenda kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukarabati unahitaji fedha za kutosha na Chuo Kikuu cha Mzumbe kwa muda mrefu kina madai halali sana kutoka Serikalini ambapo chuo kinaidai Serikali kama vile fedha za ada kutoka Bodi ya Mikopo. Fedha hizi zingeletwa mapema zingeweza kusaidia kufanya ukarabati. Je, ni lini sasa Serikali itaweza kulipa madeni haya ili Chuo Kikuu cha Mzumbe kiweze kufanya marekebisho haya madogo madogo na kukifanya chuo hiki kiweze kuwa na muonekano mzuri kuliko ilivyo sasa hivi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kama ambavyo amezungumza Mheshimiwa Mbunge Dkt. Jasmine ni kweli kuna umuhimu mkubwa sana wa kufanya marekebisho katika chuo hiki, lakini pia katika suala la ada kuna wakati tulikuwa tumeagiza vyuo vyote kufanya uhakiki hasa kwa wale wanafunzi ambao walikuwa hawastahili kupata mikopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, Mheshimiwa Waziri wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mheshimiwa Profesa Joyce Ndalichako, alishatoa maagizo kwamba Bodi ya Mikopo ipeleke fedha hizo wakati uhakiki ukiwa unaendelea ili wasikwamishe shughuli zinazoendelea. Kwa hiyo, naamini muda wowote ule hizo fedha watakuwa wamezipata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Serikali imedhamiria kuona kwamba vyuo vyote vikuu vinaongezewa fedha ili kuongeza udahili unaostahili kwa wanafunzi ili kwenda kusoma kwenye chuo binafsi iwe ni hiyari zaidi ya mwanafunzi kuliko kuwa ni sababu ya kukosa nafasi katika vyuo vyetu vya Serikali. Kwa hiyo, naamini mpango huu ukikamilika hali itazidi kuwa nzuri zaidi kwa vyuo vyote ikiwepo Mzumbe.
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu haya, maana kwa siku nyingi sana tulikuwa tumeahidiwa na majibu yalikuwa hivi hivi, lakini haya mpaka tumepewa date kwamba Juni tutapata hiyo x-ray digital tunashukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri napenda kuuliza maswali ya nyongeza kwamba; kwa kweli pamoja na kupata hiyo digital x-ray lakini bado kuna huduma nyingine ya mashine za kisasa ambazo zitasaidia hawa majeruhi kuweza kuchunguzwa zaidi. Kwa mfano tumeshuhudia hivi majuzi Waheshimiwa wenzetu Wabunge walivyopata ajali ilibidi wakimbizwe haraka sana kwenda Muhimbili kule kwa ajili ya uchunguzi zaidi, lakini kama tungekuwa na mashine hizi tungesaidia hata wagonjwa kuokoa usumbufu na maisha yao na gharama; mashine hizo ni MRI na CT-Scan.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ninaomba kuuliza, je, Wizara ni lini sasa mtatuletea pia katika Hospitali hii ya Mkoa wa Morogoro mashine za MRI na CT-SCAN ili kupunguza hata rufaa kule Muhimbili na kupunguza msongamano lakini pia kuokoa maisha ya wagonjwa?
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia pale Morogoro kama tunavyoona ile hospitali inapokea wagonjwa wengi sana wa ndani ya mkoa lakini pia na mikoa mingine. Sasa bado kuna huu usumbufu ambao unapata wagonjwa kwamba operating theatre ya mifupa haipo wanatumia theatre moja, je, ni lini sasa pia Serikali itatenga fedha za kujenga theatre hii ili kuokoa maisha ya wagonjwa na kuondoa usumbufu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Tisekwa ambaye leo anaadhimisha siku yake ya kuzaliwa, nimpongeze kwa hilo, lakini nimpongeze vilevile kwa maswali yake mazuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali tunaendelea kujipanga; tunatambua kwamba Mkoa wa Morogoro, mikoa ya Iringa, Mkoa wa Pwani pamoja na Dar es Salam ziko katika highway na kumekuwa na ajali nyingi ikiwa ni pamoja na ambayo imetokea kwa Waheshimiwa Wabunge wiki iliyopita.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto tuna mradi ambao tunashirikiana na wenzetu wa Benki ya Dunia kuweka huduma za dharura na ajali na tumejaribu sana kulenga katika mikoa ya Iringa, Morogoro, Pwani na Dar es Salaam ambapo huduma mbalimbali za dharura zitawekwa ikiwa ni pamoja na ambulance na kuangalia sasa uwezekano wa kuweka hizo huduma za CT-Scan na MRI katika hospitali hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sambamba na hilo Serikali imetukabidhi Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto hospitali zote za rufaa za mikoa. Tumezifanyia tathmini za kina na katika bajeti ya 2018/2019 katika moja ya maeneo ambayo tutaenda kuboresha ni pamoja na kuongeza vyumba vya upasuaji. Kwa hiyo naomba sana Waheshimiwa Wabunge watuunge mkono bajeti yetu ya Wizara ya Afya itakapofika.
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante Naibu Waziri kwa majibu mazuri, napongeza Serikali kwa mpango mzuri ambao wameueleza. Hata hivyo, kama alivyozungumza kwenye majibu yake, ameonesha kabisa kwamba milima hii ina ikolojia ya pekee, bioanuai adhimu, lakini kuna mifuko ambayo imeanzishwa kwa Hifadhi ya Tao la Mashariki na utekelezaji wa mradi wa miaka mitano kuanzia 2016 – 2021 pamoja na vijiji vinavyozunguka, napongeza kwa hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia sasa kwenye hii Milima ya Uluguru, kwa sababu uhifadhi sio lazima uwe pale kwenye chanzo, maana yake pamoja na hills yaani vijilima vyake. Lakini ukiangalia kwa sasa hivi pale Manispaa ya Morogoro ile milima iliyozunguka kuanzia maeneo ya Kilakala, Bigwa, Kigurunyembe na Pangawe ambayo hapa kuna vyanzo vikubwa sana vya maji ambao wakazi hawa wote niliowataja wa Bigwa, Kigurunyembe na Kola tunategemea maji kutoka kwenye milima hii, lakini mito hii imekauka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inasababishwa na uharibifu mkubwa ambao unaendelea sasa hivi kwenye milima hii ya Bigwa, Kigurunyembe, Pangawe ambapo sasa watu wanajenga kwa kasi kubwa sana ndani ya ile misitu, wanakata ile misitu yaani… (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba kwa sababu pia pale kuna Mbega wale weupe na ndege ambao ni adimu. Je, Serikali imechukua hatua gani kusimamisha na kudhibiti ujenzi huu holela ambao unaendelea katika milima hii ambayo ni vyanzo vikubwa vya maji? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa tarehe 5 Aprili, nilifanya ziara ya kukagua uharibifu wa mazingira kwenye maeneo ambayo Mheshimiwa Mbunge ameyasema. Maeneo hayo ndiyo ambayo Mheshimiwa Mbunge kwa juhudi kubwa aliweza kuyafuatilia na wakashirikiana na Serikali ya Mkoa na Serikali ya Wilaya wakawaondosha wale watu ambao walikuwa wanajenga kiholela.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maagizo ambayo niliyatoa kwa Manispaa ya Morogoro ni kuhakikisha kwamba wanatengeneza mpango mkakati wa namna ambavyo watashughulikia uharibifu huu wa mazingira. Mheshimiwa Tisekwa ile climate change strategy niliyomwahidi, nitampatia hapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ambalo ningependa Wabunge waelewe, masuala ya uharibifu wa mazingira au uchafuzi wa mazingira wamekuwa wakidhani ni vyanzo vya maji kuviharibu au kukata miti, ni pamoja na upigaji wa makelele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi hapa, Hajji Manara wakati anatangaza kwamba mechi yao na Simba wacheze ili mapato yale yatakayopatikana waweze kuisaidia Yanga watu walipiga makelele sana, nikaulizwa haya makelele kwa mujibu wa mazingira yana mahusiano gani. Nikasema kwa mujibu wa kifungu cha 106, makelele yanazuiwa lakini yale makelele ya kushabikia kama matamko ya Hajji Manara yale yanaruhusiwa kwa mujibu wa mwongozo. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri bado kidogo ayajaniridhisha kwa sababu mimi nilitembelea Mikumi pale 2016 na majibu niliyopewa ni haya haya kwamba mwekezaji amepatikana na ukarabati unaendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa namwomba Mheshimiwa Naibu Waziri anihakikishie hapa huu ukarabati utamalizika lini ili tuweze kupata mapato ya uhakikika? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili ni kwamba mbuga hii ya Mikumi ipo katikati ya barabara ambayo inaenda mikoani na nje ya Tanzania. Kulikuwa na mpango wa kuanzisha road toll ili kuweza kupata mapato zaidi katika mbuga hii ambayo inakumbana na changamoto nyingi, miundombinu na hata magari ya kuzuia ujangili.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujua, ni lini Serikali itaanzisha ushuru huu kwa sababu mchakato ulishaanza, sasa kuna kigugumizi gani? Hii itasaidia mbuga hii iweze kupata mapato na kukabiliana na changamoto ili iweze kuboresha na kuongeza mapato zaidi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nichukue nafasi hii kumpongeza kwa jinsi ambavyo amekuwa akifuatilia na ni kweli kabisa kwamba mwaka 2016 alifika pale kuangalia ni namna gani hoteli zinaweza kuongezeka katika lile eneo ili kukabiliana na hii changamoto ya uhaba wa vyumba vya watalii kulala pale Mikumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie kwamba ni kweli kabisa kwamba yule mwekezaji alipatikana siku nyingi toka mwaka 2016, lakini baada ya kupatikana, kwa mujibu wa taratibu za uwekezaji, lazima kwanza EIA ifanyike ili aweze kuendelea na huo mradi. Huo mradi baada ya kufanya hiyo tathimini ya mazingira, imekamilika mwezi Novemba, 2017. Baada ya kukamilika, mwezi Februari, 2018 ndipo mwekezaji amekabidhiwa rasmi lile eneo.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kukabidhiwa lile eneo, sasa hivi ametoa mpango kazi, na mimi mwenyewe nilienda pale nikaona, sasa hoteli yenyewe inategemea kukamilika mwezi Novemba mwaka ujao yaani mwaka 2019. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la kuweka road toll kule Mikumi, ni kweli hili suala limekuwepo na tumekuwa tukiliangalia ndani ya Serikali kuona kama kweli linaweza likatusaidia na kama linaweza likafanya kazi. Bado tuko kwenye hatua za majadiliano na kuona namna bora ya kuweza kulitekeleza hilo ili kusudi tusilete usumbufu kwa wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, wazo la Mheshimiwa Mbunge ni zuri na ninaomba niseme kwamba Serikali bado inaendelea kulifanyia kazi.
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mheshimiwa Naibu Waziri nakushukuru sana kwa majibu mazuri. Kwa kweli hicho ni kilio cha muda mrefu kwa wananchi kuhusu bili na kuhusu upatikanaji wa hizi pre-paid meters.

Mheshimiwa Spika, katika jibu la Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba Serikali imeagiza Mamlaka zote nchini kuendelea kuwafungia wananchi; swali langu ni kwamba: Je, ni lini sasa wamewaagiza muda wa kumaliza kufunga hizi meters? Maana isije ikachukua muda mrefu, tuweze kuwapunguzia adha hii ya bili kubwa na wananchi waweze kupata maji kwa bili ambayo ni ya uhakika.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, hii ni changamoto, lakini sisi kama Wizara tumeliona. Nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa kuwatetea wananchi wake wa Morogoro pamoja na Watanzania kwa ujumla kutokana na changamoto hii.

Mheshimiwa Spika, kwanza tumewaita Wakurugenzi wote katika Wizara yetu kwa maana ya Mamlaka za Maji na Mheshimiwa Waziri akawapa agizo hili kutokana na changamoto hii. Kikubwa, sisi katika kuhakikisha tunaongeza utendaji, tumewasainisha mikataba (performance agreement) kwa maana ya utendaji wao. Huwezi ukawa Mkurugenzi wa Maji halafu kumekuwa na changamoto katika suala zima la upatikanaji wa maji. Kwa hiyo, ninachotaka nimhakikishie, sisi kama viongozi wa Wizara tutawapima kwa yale maagizo tuliyowapa kuhakikisha wanatekeleza kwa wakati ili kuweza kuondoa changamoto hizi za bei pamoja na maeneo mengine ambayo hayajafikiwa na usambazaji wa maji.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri yenye matumaini hasa kwa mwaka huu kutengewa hizo shilingi milioni 34, lakini hii barabara ya Kidiwa - Tandali imeshafanyiwa upembuzi yakinifu, ingawa sasa hizo fedha zitatafutwa mpaka lini? Hapo sasa napenda kufahamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri kwamba Tarafa ya Mgeta kama alivyotembelea miaka ya nyuma, landscape yake bado ni ile ile ya milimani na watu wanaishi milimani. Kwa sasa tunategemea barabara hii kubwa moja toka Sangasanga kwenda mpaka Nyandila - Kikeo. Barabara hii ni mbovu sana hasa wakati wa masika; na tulishaahidiwa. Nakumbuka miaka ya 1970s alipokuja Mheshimiwa Abdu Jumbe aliahidi kwamba tutatengenezewa kwa kiwango cha lami. Ni kweli naweza nikalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Rais Mstaafu, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Kikwete alipokuja aliahidi kwamba barabara hii itatengenezwa kwa kiwango cha lami kulingana na ubovu wake na nauli inakuwa kubwa: Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi yake ya kujenga barabara hii ya Sangasanga mpaka Nyandila kwa kiwango cha lami?

Swali la pili. Katika kutatua changamoto za usafiri katika Tarafa hii ya Mgeta, wananchi wamejitolea kutengeneza barabara nyembamba za kupita pikipiki, lakini wanakutana na changamoto ya utaalamu; wakati mwingine hawajui barabara iende hivi, kwa hiyo, wanakutana na changamoto hizo, lakini pia wanakutana na changamoto sehemu nyingine inabidi ijengwe madaraja au karavati.

Je, Serikali sasa iko tayari kuungana na wananchi hawa wa Tarafa ya Mgeta ili kupeleka wataalam pamoja na kuwajengea madaraja ili tuweze pia kutumia usafiri wa pikipiki kuunganisha vijiji na Kata? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, machozi tuliyoshuhudia yakitoka kwa Mheshimiwa Mbunge wa Mlimba pale, yanatosha kwa Mkoa wa Morogoro. Kwa hiyo, isingependeza tukapata machozi mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Dkt. Tisekwa akubaliane nami kwamba ahadi zote zinazotolewa na Viongozi Wakuu kwa maana ya Marais, hata kama Rais aliyetangulia ndio aliyetoa ahadi, sisi kama Serikali, ahadi hizo tunazitunza na ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba ahadi za viongozi wetu tunazitekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni Mheshimiwa Mbunge atakuwa shuhuda, katika ahadi ambazo zimetolewa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, katika bajeti ambayo tumepitisha, tumeanza kutekeleza katika maeneo yote ambayo ahadi zimetolewa. Tumeanza kujenga lami kwa kilometa moja moja. Kwa muungwana ahadi ni deni, naomba nimtoe mashaka Mheshimiwa Mbunge, tutatekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili suala la pili ambapo wananchi wameanza kutengeneza barabara kwa ajili ya kupita angalau kwa pikipiki, lakini kinachokosekana ni utaalam, naomba nichukue fursa hii kumwagiza coordinator wa Mkoa wa Morogoro ahakikishe kwamba anamwagiza Meneja wa Wilaya husika ili kwenda kutoa utaalam ili wananchi pale ambapo wanatoa nguvu yao isije ikapotea na aone namna ambavyo na Serikali tunaweza tuka- complement ili kazi nzuri iweze kuonekana.
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake kuonyesha kwamba Serikali inatambua mchango wa wazazi ambao wamehangaika kutulea hadi kufikia hapa tulipo. Tukumbuke kwamba hata vitabu vitakatifu vya Mungu, kwa mfano amri kumi za Mungu ni amri ya nne pekee ambayo inatoa na ahadi kwamba ukiheshimu wazazi utapata baraka na utaishi miaka mingi duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kutatunza wazazi, wenzetu ambao wazazi wapo hai ni vizuri, it is a blessing. Tuendelee kuangalia wazazi wetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nina maswali mawili ya nyongeza kwamba Je, Serikali ipo tayari kutunga sheria itakayowabana watoto hawa wanaotelekeza, ili waweze kuwatunza wazazi wao?

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Je, wakati tunasubiri hiyo sheria kutungwa, Serikali ipo tayari kuweka Dawati la Wazee ili waweze kusikilizwa katika malalamiko yao, hasa kwa wale ambao wanatelekezwa na watoto wao? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa maswali mawili ya Mheshimiwa Jasmine Tisekwa Bunga. Swali lake la kwanza ameuliza kwamba, je, Serikali iko tayari kutunga sheria ya kubana watoto ambao wanawatelekeza wazee? Niseme tu kwamba kwa sasa hivi hatuna mpango huo kama Serikali. Tunajikita na kujielekeza zaidi katika kutoa elimu kwa jamii kuhakikisha kwamba wanatambua wajibu wao na kutimiza majukumu yao ya kutunza na kulea wazee.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ameuliza kwamba, je, tuko tayari kuanzisha Dawati la Wazee? Niseme kwamba tunayo mifumo kupitia Maafisa Ustawi wetu wa Jamii ambao majukumu yao ni pamoja na kuhakikisha kwamba huduma kwa wazee zipo. Kwa hiyo, wale wazee ambao wanaona kwamba matunzo au zile haki za msingi hawazipati, ni vizuri wakafika kwa Maafisa Ustawi wa Jamiii ili kupata msaada wa kuwaunganisha na watoto wao.

Mheshimiwa Spika, sisi kama Serikali tuna nyumba za kuwatunza wazee 17 na tuna wazee takribani kama
500. Nasi Serikali tunachukua tu wale wazee ambao imedhibitika kwamba hawana watoto, hawana ndugu, jamii ile inayowazunguka haiwezi kuwatunza, ndipo pale Serikali inawachukua na kuwatunza.