Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Ester Alexander Mahawe (1 total)

MHE. ESTER A. MAHAWE:
Mheshimiwa Spika, ahsante.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, sera ya elimu ya nchi yetu sasa inasema ni kupata elimu bure lakini hii bure ina maana inalipiwa na Serikali. Lakini kumekuwa na kundi dogo la wazazi wengine ambao kwa kuchangia kupitia kodi zao ndizo ambazo zinatumika kusomesha watoto wao ama kugharamia elimu lakini kundi hili limekuwa likilipa kodi zote zinazotakiwa kulipwa lakini wamekuwa wakichajiwa mara mbili (double taxation) kupitia watoa huduma wa elimu katika taasisi binafsi.
Je, nini kauli ya Serikali ili kwamba na hawa wananchi amba tayari walikwisha kulipa kodi na kuchangia elimu bure na wenyewe waweze kufurahia keki hii ya elimu bure? (Makofi)
WAZIRI MKUU:
Mheshimiwa Spika, kama ambavyo umesema, kwamba swali limechanganywa sana haliko wazi mno na haya ni maswali ya papo kwa papo inatakiwa liwe-clear ili na mimi niweze kujibu kitu halisi ili pia naye aweze kunufaika na majibu lakini pia Watanzania ambao wanasikia kipindi hiki waweze kujua jambo gani limeulizwa na jambo gani ambalo linatakiwa kujibiwa.
Lakini pia, amezungumzia suala la elimu bure na ni jambo ambalo watu wengi limekuwa likiwachanganya na wengine kupotosha, naomba nitoe ufafanuzi huu ufuatao ili Watanzania wajue kwamba elimu bure ni mkakati unaolenga Kurugenzi ya Msingi na Sekondari na hasa katika kuwapunguzia mzigo wazazi wa kuchangia changia michango mbalimbali shuleni.
Mheshimiwa Spika, Serikali tumeanza na maeneo ambayo tumeona wazazi walikuwa wanakwazwa sana. Tumezungumza mara kadhaa lakini narudia kwamba moja kati ya maeneo hayo tumeondoa yakle malipo yaliyokuwa yanaitwa ada kwa sekondari, shilingi 20,000 na shilingi 70,000. Pia kulikuwa na michango ya ulinzi, maji, umeme pale shuleni michango ile yote ile sasa Serikali imetenga fungu kwa ajili ya kuipa shule ili iweze kulipia gharama hizo, lakini suala la mitihani mbalimbali nayo pia ni eneo Serikali imeamua kulichukua kwa sababu gharama za mitihani zitafanywa na Serikali ili wazazi
wasiingie kwenye michango hiyo.
Mheshimiwa Spika, lakini pia tunaendelea kuona ni maeneo gani mengine ambayo wazazi yanawakwaza zaidi katika kuchangia, sasa kama kuna mzazi anachangia huku nje hata kama analipa kodi maeneo mengine, ni jukumu tu la kuona kwamba kuna umuhimu wa kuchangia sekta ya elimu na kwamba yeye kama Mtanzania anayo nafasi ya kuchangia mahali popote bila kujali kama mchango huo pia unagusa kodi ambazo alikuwa anazilipa kule awali.
Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo, tutoe wito kwa Watanzania, kwanza tupe subira Serikali kuona maeneo mengine zaidi ambayo tunaweza tukaboresha ili kumpunguzia mzazi mzigo wa kuweza kusomesha watoto hawa.
Sasa lawama inakuja pale ambako tumetoa nafasi hizi tumegundua kwamba kuna watoto wengi wa Kitanzania walikuwa hawapelekwi shuleni na kwa kuondoa hizi gharama, gharama watoto wengi wanapelekwa shule na sasa tumeanza kuona uzoefu wa kwamba watoto wengi wameendelea kusajiliwa shuleni, idadi imekuwa kubwa na kumekuwa na changamoto nyingine kama madawati na vyumba vya madarasa.(Makofi)
Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishi e Watanzania, kwamba Serikali inaendelea kuweka utaratibu wake kwa ajili ya kuongeza madawati lakini pia miundombinu ya vyumba vya madarasa ili watoto wetu ambao sasa tumebaini kuwa wamekuwa wengi waweze kupata mahali pa kukaa na chumba ambacho wanaweza kupata taaluma yao. Lakini hatuzuii mlipakodi yeyote wa sekta nyingine kuchangia kujenga madarasa kwa haraka ili watoto wetu waingie ndani, kutoa madawati kama ambavyo tumeona Watanzania wengi
wamejitokeza, makampuni mengi yanachangia lakini pia hata baadhi ya Wabunge tumeona mkitoa mchango wenu, na mimi nataka nitumie nafasi hii kuwapongeza sana Wabunge ambao pia mmeanza kuunga mkono jitihada za Serikali kuchangia madawati. Jambo hili ni letu sote, watoto ni wetu sote hebu twende pamoja, tutoe elimu hiyo ya kuchangia kwa namna mtu anavyoweza kwenye madawati, kama una uwezo wa kujenga chumba cha darasa ili watoto wetu waweze kusoma ndani, lakini Serikali inaendelea na mkakati pia
wa ujenzi wa maeneo hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ningependa nitamke hili ili wale wote wanaodhani kulundikana kwa watoto sasa ni jambo la makusudi, hapana, ni jambo ambalo tuliona ni muhimu tupunguze michango, lakini Wazazi ambao walikuwa wanashindwa kuleta watoto nao wapate kupeleka watoto, wamepeleka watoto wengi ni jukumu letu sasa kujenga vyumba na kupeleka madawati. (Makofi