Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Richard Mganga Ndassa (8 total)

MHE. RICHARD M. NDASSA aliuliza:-
Je, ni lini barabara ya Magu - Bukwimba - Ngudu - Hungumalwa itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kuchukua nafasi hii kujibu swali la Mheshimiwa Richard Mganga Ndassa, Mbunge wa Sumve, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2010/2011 na 2011/2012, Wizara kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) ilitenga jumla ya shilingi milioni 1200 ambazo zilitumika kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami barabara ya Magu - Ngudu - Jojiro sehemu ya Ngudu Mjini yenye urefu wa kilometa 1.9
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2014/2015 na 2015/2016, Serikali ilitenga jumla ya shilingi milioni 200 kwa ajili ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa barabara hiyo yenye urefu wa kilometa 70 na taratibu za kumtafuta Mhandisi Mshauri zinaendelea. Baada ya kukamilika kwa usanifu na gharama za mradi huo kujulikana, Serikali itatafuta fedha za kuanza ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami.
MHE. RICHARD M. NDASSA aliuliza:-
Miradi ya umeme ya REA Awamu ya Kwanza na ya Pili inaendelea vizuri.
Je, ni lini miradi ambayo haijakamilika itakamilika hasa ikizingatiwa kuwa Serikali iliahidi kukamilika kwa miradi hiyo kabla ya tarehe 30 Juni, 2015?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Richard Mganga Ndassa, Mbunge wa Sumve, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilifadhili utekelezaji wa mradi kabambe wa kusambaza umeme vijijini, Awamu ya Kwanza na ya Pili kupitia Mfuko wa Nishati Vijijini (REA). Miradi ya awamu ya kwanza imeshakamilika kwa asilimia mia moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya fedha iliyotengwa kutekeleza miradi ya REA Awamu ya Pili ni shilingi bilioni 877.3 na hadi sasa Serikali imeishalipa asilimia 75 na inaendelea kutoa fedha ili miradi ikamilike kabla ya mwezi Juni, 2016.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Awamu ya Pili, katika Mkoa wa Mwanza ikiwemo Jimbo la Sumve Wilaya ya Kwimba unatekelezwa na Mkandarasi Chico-CCC (BV) JV. Wigo wa kazi wa Mkoa wote kwa Mwanza ni ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 wenye urefu wa kilomita 463. Kadhalika ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 365 na kuunganisha umeme wateja wa awali wapatao 8,990. Utekelezaji wa kazi wa Mkoa wa Mwanza umefikia asilimia 78. Gharama ya Mradi wote wa REA Phase II ni shilingi bilioni 25.36. Mradi unatalajiwa kukamilika kabla ya mwezi Juni mwaka huu.
MHE. RICHARD M. NDASSA aliuliza:-
Je, ni lini mradi wa ujenzi wa bomba la maji ya Ziwa Victoria kutoka Magu - Sumve - Malya utaanza?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Mganga Ndassa, Mbunge wa Sumve kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Uwekezaji ya Ulaya (EIB) na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA) inatekeleza miradi ya maji safi na maji taka kwa Jiji la Mwanza pamoja miradi ya maji safi katika miji mitatu ya Magu, Misungwi na Lamadi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mji wa Magu mradi huu unakadiriwa kugharimu kiasi cha Euro milioni 5.3 na Mkandarasi anatarajiwa kuanza ujenzi wa mradi ifikapo mwezi Julai, 2016. Idadi ya wananchi watakaonufaika na mradi huu inakadiriwa kuwa wananchi 73,363 ifikapo mwaka 2040.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa miji ya Sumve na Malya, Serikali inaendelea kufanya uchunguzi wa awali ili kubaini gharama za eneo la kupitisha mradi. Kazi ya upimaji pamoja na usanifu itakamalika mwezi Aprili, 2016 na ujenzi wa mradi unatarajiwa kuanza mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. RICHARD M. NDASSA aliuliza:-

Usanifu wa kina wa barabara ya Isandula (Magu) – Bukwimba Station – Ngudu hadi Hungumalwa ambayo ni kilometa 74 umeshakamilika:-

Je, ni lini barabara hiyo itaingizwa kwenye bajeti ili ijengwe kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Richard Mganga Ndassa, Mbunge wa Sumve, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Isandula hadi Hungumalwa yenye urefu wa kilometa 71 ni Barabara ya Mkoa inayohudumiwa na Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS). Barabara hii inapita katika Mji wa Bukwimba, Nyambiti na Ngudu na ni barabara muhimu katika kukuza uchumi wa Wilaya za Magu, Sumve na Ngudu. Barabara hii pia ni kiungo kati ya barabara kuu ya Mwanza – Sirari na Mwanza – Shinyanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua umuhimu huo, Wizara yangu inaifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina barabara hiyo kwa lengo la kuijenga kwa kiwango cha lami. Kazi ya usanifu wa kina inatarajiwa kukamilika mwezi Mei, 2019. Baada ya usanifu huo kukamilika na gharama kujulikana, barabara hiyo itaingizwa kwenye mpango wa ujenzi kwa kiwango cha lami kutegemeana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati ujenzi huo wa kiwango cha lami ukisubiriwa, Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS) itaendelea kuifanyia matengenezo barabara hiyo kuhakikisha kuwa inapitika majira yote.
MHE. RICHARD M. NDASSA (K.n.y. MHE. KISWAGA B. DESTERY) aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutumia mtandao wa maji Magu kupeleka Tarafa ya Ndagalu, Kata za Shishani, Njinjinili, Kabila, Nkungulu, Ng’haya, Sukuma, Buhumbi na Mwamabanza zenye jumla ya vijiji 24?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiswaga, Mbunge wa Jimbo la Magu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji Magu Mjini ambao tayari umekamilika, una uwezo wa kuzalisha maji kiasi cha lita milioni 7.25 kwa siku, ukilinganisha na mahitaji ya sasa ya lita milioni 3.54 kwa wakazi wa Magu Mjini na Vijiji vya Kipeja, Sagani, Nyashimba na Ilungu. Hivyo Mradi huu una ziada ya maji ya lita milioni 3.71 kwa siku kwa sasa kutokana na ziada hiyo, Serikali kupitia Programu ya lipa kwa matokeo yaani Programme for Results (P4R) itajenga miundombinu ya usambazaji wa maji kutoka kwenye Mradi wa Magu mjini kupeleka kwa baadhi ya vijiji vilivyopo tarafa ya Ndagalu ikiwa ni pamoja na Vijiji vya Misungwi, Kitongo, Lumeji, Buhimbi, Iseni, Nyang’hanga na Nyashoshi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha kuwa azma ya upatikanaji wa maji katika vijiji vingine vya Tarafa ya Ndagalu inapatiwa ufumbuzi wa kudumu, Serikali itahakikisha kuwa imetenga fedha katika bajeti ya Mwaka 2020/2021 ili vijiji vilivyobaki viweze kupata huduma ya maji kupitia Mradi wa Ziwa Victoria.
MHE. RICHARD M. NDASSA aliuliza:-

Kupitia Mifuko ya Jamii tayari tathmini ya kukijenga Kiwanda cha kuchambua pamba Nyambiti Ginnery kilichopo Kwimba umeshafanyika, kilichobaki ni uamuzi wa Serikali kuliongezea thamani zao la pamba.

Je, ni lini Kiwanda hicho kitaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. ANTHONY P. MAVUNDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri napenda kujibu swali la Mheshimiwa Richard Mganga Ndasa Mbunge wa Sumve kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Jumuiya ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii Nchini inayoundwa na Mifuko ya NSSF, PSSSF, NHIF, WCF na ZSSF imekamilisha mapitio mapya ya upembuzi yakinifu ya ufufuaji wa vinu vya kuchambulia pamba vya Ngasamo, Nyambiti na Kasamwa vilivyoko Mkoani Simiyu, Mwanza na Geita baada ya takwimu za uzalishaji wa kilimo cha pamba kuongezeka hususan katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Mifuko inakamilisha taratibu muhimu zinazohusiana na Miongozo ya Uwekezaji kwa kushirikiana na Vyama vya Ushirika vya Mwanza, Simiyu na Geita ili kuwezesha uwekezaji wenye ufanisi na tija taratibu zitakapokamilika.

Mheshimiwa Spika, Utaratibu maalum wa namna ya kuwezesha ufufuaji wa viwanda hivyo unatarajiwa kukamilika ndani ya mwezi Februari, 2020.
MHE. RICHARD M. NDASSA aliuliza:-

Mradi mkubwa wa maji kutoka Ziwa Victoia kwenda katika Miji ya Sumve, Malya hadi Malampaka ni ahadi ya Mheshimiwa Rais ambao usanifu wake umeshakamilika.

Je, ni lini mradi huo utatekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Mganga Ndassa, Mbunge wa Jimbo la Sumve kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria kwenda katika Miji ya Sumve, Malya na Malampaka ni ahadi ya Mheshimiwa Rais katika Awamu ya Nne. Tayari Wizara ya Maji kupitia mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Mwanza ilinza mchakato wa kufanya upimaji ili kujua ni eneo gani lipo karibu kutoka Ziwa Victoria, ili iwe rahisi kufikisha maji kwenye miji hiyo.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2019/ 2020, Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 200 kwa ajili ya kufanya usanifu wa kina ili kuanza na maandalizi ya utekelezaji wa mradi wa maji katika miji hiyo baada ya gharama halisi kufahamika.
MHE. RICHARD M. NDASSA aliuliza:-

Wananchi wa Halmashauri ya Kwimba waliombwa kutafuta eneo la kujenga Chuo cha VETA ambapo eneo la ekari 60 lilishapatikana zaidi ya miaka 10 iliyopita na Serikali imekuwa ikiahidi kutenga fedha za ujenzi wa chuo hicho:-

Je, ni lini Serikali itatenga fedha za ujenzi wa chuo hicho?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Mganga Ndassa, Mbunge wa Sumve, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa nchi kuwekeza katika elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi, hasa katika kipindi hiki ambacho Serikali ipo katika jitihada za kuelekea uchumi wa kati kupitia viwanda ifikapo mwaka 2025.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na mpango wa kujenga Vyuo vya Ufundi Stadi ikiwa na lengo la kutimiza azma ya kuwa na Chuo cha Ufundi Stadi katika kila mkoa na wilaya. Ujenzi wa vyuo hivi unafanyika kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Kwimba ni moja ya Kata ya Wilaya zilizopo katika awamu ya pili inayotarajiwa kuanza kutekelezwa mwaka wa fedha 2019/2020. Kwa sasa wananchi wa Kwimba wanashauriwa kutumia Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Malya kilichopo Wilaya ya Kwimba na vingine vilivyo mkoa na wilaya za jirani.