Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Eng. Gerson Hosea Lwenge (124 total)

MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Spika, asante sana. Tatizo la maji Tanzania ni kubwa na ndiyo maana kwenye Bunge letu kila Mbunge akiulizwa atakueleza hilo. Sera ya Maji ya Taifa inataka mwananchi wa kawaida apate maji umbali wa mita 400 toka makazi anayoishi. Sasa Mheshimiwa Waziri, na Naibu Waziri atueleze ni lini Sera hiyo ya Taifa itaanza kutekelezwa kikamilifu ili Watanzania waondokane na hii kero ya maji?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Silinde kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli Sera ya Maji ya mwaka 2002 tunasema kwamba umbali wa mtu kupata maji kwenye kichoteo ni mita 400. Kazi hii tulishaianza kuitekeleza kuanzia mwaka 2007 katika awamu ya kwanza ya programu ya maji ambayo imeishia Disemba, 2015.

Mheshimiwa Spika, matokeo ya awamu ya kwanza ni mazuri ijapokuwa hatukufikia lengo ambalo tulitaka kufika, sasa ile miradi ambayo tayari imeshanza kwenye programu tunaiingiza kwenye programu ya pili ambayo inaanza Januari mwaka huu. Ili kukamilisha miradi ile iliyokwisha kuanza ili tuweze kufikia azma hiyo ambayo kila mwananchi atapata maji kutoka umbali wa mita 400.

Mheshimiwa Spika, nikuhakikishie wakati wa kampeni Dkt. John Pombe Magufuli aliahidi adhima hiyo maeneo mengi na Serikali ya awamu ya tano itahakikisha kwamba suala la maji ni ajenda ya kwanza, na kuhakikisha kila mwananchi atapata maji, ijapokuwa tunasema asilimia 95 Mijini na asilimia 86 Vijijini, azma ya sasa ni kwamba tunataka tupate maji kwa asilimia 100 katika miaka mitano ijayo.
MHE. GIMBI D. MASABA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Kwa kuwa mpango au ahadi ya kuwapatia maji safi na salama kutoka Ziwa Victoria wananchi wa Mkoa wa Simiyu uliahidiwa tangu mwaka 2005 katika Kampeni za Uchaguzi wa Rais wa Awamu ya Nne. Swali, je, ni lini Serikali ya Chama cha Mapinduzi itaacha kuwachukulia wananchi wa Mkoa wa Simiyu kana kwamba hawana kumbukumbu na ahadi zinazotolewa na Serikali yako?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni lini Serikali yako itakamilisha ujenzi wa Bwawa la Habia lililoko Wilayani Itilima, Mkoani Simiyu uliosimama kwa muda mrefu? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa inatekeleza ahadi zake kama tunavyoainisha kwenye utekelezaji. Anachokiongea ndugu yangu kwanza akubaliane na mimi kwamba tumeeleza kwenye jibu la msingi kwamba katika Mkoa wa Simiyu, tumekuwa na miradi kadhaa kila Wilaya katika utekelezaji wa Awamu ya Kwanza ya programu ya maji. Sasa huwezi kusema kwamba hakuna kilichofanyika, kuna kilichofanyika ila hitaji la maji ni kubwa zaidi na ndiyo maana Serikali sasa inakuja na mpango mkubwa wa kutoa maji kutoka kwa Ziwa Victoria ili wananchi wote wa Mkoa wa Simiyu wapate maji, hiyo ndiyo kazi ya Serikali ya Awamu ya Tano ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa miradi unaenda kwa hatua hapa tumesema hatua ya kwanza lazima tufanye usanifu…
Ili tuweze kujua hitaji la kila mwananchi wa Simiyu ni kiasi gani kwa sababu maji ya kutoka Ziwa Victoria kwanza...
Kwa hiyo, lazima niwaahidi wananchi wa Simiyu kwamba Serikali itatekeleza ahadi yake ndani ya miaka mitano mradi huu utakuwa umekamilika. (Makofi)
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tatizo la maji ni tatizo kubwa tuseme nchi nzima, lakini hata Karagwe tuna shida sana ya maji. Wakati wana-Karagwe wanasubiri mradi wa Rwakajunju, Serikali ina miradi ya Benki ya Dunia, lakini kote Jimboni hii miradi haijakamilika. Napenda kuiomba Serikali ieleze wananchi wa Karagwe hii miradi itakamilika lini?
Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri sana.
Mheshimiwa Spika, kuhusu miradi ya Benki ya Dunia, tulikuwa na hiyo awamu ya kwanza ya program ambayo imekwisha Disemba tarehe 30. Sasa tunaingia awamu ya pili ya program ya miaka mitano katika kutekeleza vijiji vile ambavyo havikupata awamu ya kwanza na ile miradi ambayo iko inaendelea. Sasa hivi Serikali imeshapata fedha za kuweza kusukuma miradi ya kwanza ile iliyokuwa imeanza ili iweze kukamilika.
Mheshimiwa Spika, naomba nikuhakikishie na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, azma ya Serikali ni kuhakikisha vijiji vyote vilivyokuwa ndani ya program tunakamilisha ili wananchi wetu waweze kupata maji.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza ni kwamba hili bwawa lilitengenezwa maalum kwa ajili ya wafugaji kutokana na kwamba walihamishwa kutoka mbuga ya wanyama ya Mkomazi, na kazi ya pili ilikuwa uvuvi, ya tatu ilikuwa yale maji yanayo-spill over ndiyo yaende kwa wakulima. Tatizo ni kwamba huu mradi wote umegeuzwa kwamba unalenga wakulima zaidi kuliko wafugaji, matokeo yake nina wasiwasi kwamba hata Mtaalam (Consultant) mwingine akipatikana wa kutengeneza huu usanifu atakosea, kama alivyokosea mara ya kwanza ambapo huu mradi ulipotangazwa zile Terms of Reference hazikueleweka. Matokeo yake yalivyoenda UN Capital Development Fund, yakarudi kwamba haikukidhi matakwa ya ule mradi ungetengenezwaje. Sasa ninavyoliona hapa litarudia tena, because focus pia imebadilika kutokana na majibu ya Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Spika, swali langu ni hivi huoni ni wakati muafaka sasa mradi huu ukasimamiwa na Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ili pia tupate technical assistance ya kusaidia ku- frame huu mradi vizuri? Because kuharibika kwa huu mradi, I mean kujaa tope ni kwamba wafugaji walikuwa wanaleta ng‟ombe kwenye bwawa na hili bwawa ni kubwa sana, square kilometer kuna takwimu mbili, inaonesha 32 square kilometers, nyingine inaonesha square kilometers 24, ni mradi mkubwa sana. Kwa hiyo, ninachoomba au ninachoshauri ni kwamba huu mradi haionekani kwamba unatakiwa uendeshwe au usimamiwe na Wizara ya kilimo ili uweze kupata technical assistance inayotakiwa?
Swali la pili, sasa hivi wananchi wanapata shida sana, wanaolima hapa, licha ya kwamba mbolea na msaada wa kitaalam unakosekana, lakini ndege aina ya kweleakwelea, wanavamia sana mashamba ya wakulima na sasa hivi ndiyo kipindi ambacho mpunga wa eneo lote hilo la kwanzia Maore, Ndungu, Kihurio mpaka Bendera, linavamiwa na hawa ndege waharibifu. Je, Serikali inaweza kusema nini kuhusu kutatua tatizo la kuua hawa ndege waharibifu? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, ombi lake ni kwamba anataka bwawa lile lisimamiwe na Serikali Kuu badala ya Halmashauri. Naomba niwahakikishie, mwaka jana kwenye Bunge la Kumi tulipitisha Sheria ya Umwagiliaji na tukaanzisha Tume ya Umwagiliaji, Tume hii ndiyo itakayosimamia ujenzi wa mabwawa yale makubwa ambayo yataongeza eneo la umwagiliaji. Kwa hiyo, nikuhakikishie Mbunge suala la utaalam lipo katika Wizara ya Maji na Umwagiliaji kuhakikisha mabwawa haya yatatengenezwa inavyotakiwa, kwa hiyo usiwe na wasiwasi.
Swali la pili kuhusu ndege, hilo nafikiri labda Waziri wa Kilimo yupo hapa, anaweza akajibu. Ahsante sana.

WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, hilo swali la ndege waharibifu nimeshalipokea pia swali la aina hii kutoka kwa Mheshimiwa Elibariki Kingu, Mbunge makini wa kutoka Jimbo la Singida Magharibi, kuna ndege waharibifu wa aina hiyo hiyo. Niwaambie tu Waheshimiwa Wabunge kwa maeneo hayo ambayo yamepata uharibifu wa aina hiyo, nimewaelekeza wataalam wangu ili waweze kutumia utaratibu ambao Serikali huwa inatumia wa kutumia ndege kwenda kushughulika na ndege waharibifu wa mazao katika maeneo hayo husika.
Kwa hiyo, kama kuna eneo lingine ambalo Wabunge hawakupata fursa ya kuuliza lina matatizo ya aina hiyo, naomba baada ya kuahirisha Bunge nipate taarifa za aina hiyo ili niweze ku-communicate na wataalam wangu waweze kuchukua hatua zinazostahili.
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii adimu ya kuuliza swali moja la nyongeza. Kama ilivyo Wilaya na Mlalo, Wilaya ya Hanang‟ ina bwawa ambalo lilikuwa likikusanya maji ya Mlima Hanang‟ kwa scheme ambazo zinaweza zikatumika kwa umwagiliaji. Ni miaka mitano sasa tumekuwa tukiomba bwawa hilo likarabatiwe na bado hatujafanikiwa.
Mheshimiwa Naibu Waziri anaweza kunisaidia kuwahakikishia wananchi wa Hanang‟ kwamba kama anavyoomba Mbunge wa Mlalo na Mbunge wa Jimbo la Hanang‟ analiomba hilo.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba nimjibu Mheshimiwa Mary Nagu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nilikumbushe Bunge lako kwamba kupitia Bunge hili tulipitisha Sheria Namba 5 ya mwaka 2013, Sheria ya Umwagiliaji na pia tulianzisha Tume ya Umwagiliaji. Katika mwaka wa fedha 2015/2016, Serikali imetenga bilioni 53 kwa ajili ya kuendeleza na kukarabati mabwawa ambayo yanajihusisha na shughuli za umwagiliaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafanyia mapitio, mabwawa haya yote ambayo yanaweza kuongeza maeneo ya umwagiliaji, lakini pia mabwawa mengine ambayo yatasaidia wananchi wetu kuweza kupata maji. Ni azma ya Serikali ya Awamu ya Tano kwamba tunataka tuongeze kiwango cha upatikanaji wa maji vijijini na mijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, sehemu zingine tutatumia mabwawa, sehemu zingine tutatumia mito na sehemu nyingine tutatumia maziwa. Kwa hiyo, kazi hii tutakwenda kufanya, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba nitafika huko kwenda kuangalia bwawa analoliomba ili kusudi tuweze kuona nini kifanyike. Ahsante.
MHE RISALA S. KABONGO: Mheshimiwa, Naibu Spika nakushukuru. Nakushukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yako.
Kwa kuwa, mradi huu ni Mkubwa na ni wa miaka mitano; je, Serikali inavipa vipaumbele gani vijiji hivi vya Oldadai na Sokoni II na Ngilesi, kwa kuwa wamekuwa na kero kubwa na ya muda mrefu ya kupata maji?
Eneo la pili, nitaomba Mheshimiwa Waziri, atakapopata nafasi baada ya Bunge hili, aweze kutembelea maeneo haya na kujionea hali halisi katika vyanzo hivi ambavyo vinatunza maji yanayosaidia katika Mkoa wa Arusha. Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa ni kweli tumepata ufadhili wa mradi mkubwa ambao utekelezaji wake utachukua miaka mitatu. Jana tulikuwa na Mkurugenzi wa Jiji la Arusha, amekuja ofisini kwangu pamoja na Meya, pamoja na Mbunge na tumekubaliana kwamba, tutatengeneza mpango wa muda mfupi ili hivyo vijiji unavyovisema tuweze kuvitafutia angalau wapate maji wakati tunatekeleza huu mradi mkubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa kulikuwa na Mradi wa Vijiji Kumi, tumekubaliana kwamba Jiji la Arusha litakabidhi kwenye mamlaka yetu ya Arusha ili kusudi waweze kuunganisha kwenye mtandao baadhi ya maeneo ambayo Arusha hayapati maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana pia kwamba na mimi nitakuja kuangalia utekelezaji wa mpago huu. (Makofi)
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza naomba nisahishe jina langu hapa inasomeka Ngassa, siyo Ngassa ni Ndassa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na maelezo mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini naomba Serikali itambue kwamba suala la maji ni suala kila Mtanzania, kila mwananchi anahitaji maji na ndiyo maana unaona Wabunge wote wanasema kuhusu maji.
(a) Swali langu, kwa sababu Serikali katika mwaka 2000 na 2004 iliamua, maamuzi magumu yenye tija, kuyatoa maji ya Ziwa Victoria kuyapeleka Kahama, Shinyanga. Je, Serikali ina mpango gani mrefu wa kupeleka maji ya Ziwa Victoria katika Mikoa tisa ili maji hayo yawanufaishe Watanzania na mikoa hiyo ni Mwanza, Mara, Kagera, Simiyu, Singida na Dodoma. Serikali ina mpango gani kwa sababu mahitaji ya maji ni makubwa na maji ya Ziwa Victoria yapo hayana kazi nyingine. Je, Serikali ina mpango mkakati gani wa kuhakikisha kwamba maji yanafika katika maeneo hayo?
(b) Mheshimiwa Waziri wa Maji, wananchi wa Jimbo la Sumve katika Kata ya Nkalalo na Mabomba wanashida kubwa ya maji, naomba nikuombe pamoja na maelezo haya utembelee tuende ukajionee mwenyewe jinsi wananchi wa Tanzania wa Jimbo la Sumve wanavyopata taabu ya maji katika Jimbo langu.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimezungumza jana kwamba tumeleta mapendekezo ya mwongozo kwa kutengeneza mpango wa miaka 2016/2017 na nilisema katika sekta ya maji tumetoa ahadi kwamba katika miji yote ya Mikoa inayozungukiwa na Ziwa Victoria tutahakikisha tunachukua maji ya kutosha kuyafikisha kwenye maeneo husika kwa kiwango ambacho tumeshasema kwenye Ilani, kwamba Miji Mikuu ya Mikoa ipate asilimia 95 ikifika 2020 na ipate asilimia 100 ikifika 2025.
Kwa hiyo, naomba nilihakikishie Bunge hili kwamba azma hiyo ambayo pia Mheshimiwa Rais wetu ameahidi tutakwenda kufanya, tutaomba Waheshimiwa Wabunge muweze kutuunga mkono katika kupanua vyanzo vya upatikanaji wa fedha hasa kuongeza Mfuko wa Maji ili tuweze kutekeleza miradi yote hii ambayo kila Mbunge ameomba Serikali iweze kufanya, ahsante. (Makofi)
MHE. DEVOTA M. MINJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Pamoja na majibu mazuri aliyotoa Naibu Waziri kuhusu kushughulikia tatizo la maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa Serikali imekuja na mpango wa kuanzisha Bwawa jipya la Kidunda ambalo litakuwa likitoa huduma ya maji katika mikoa mingine lakini siyo kwa Mkoa wa Morogoro. Serikali haioni kama si vyema kuanzisha bwawa hilo pasipo kwanza kushughulikia kero ya maji ya wananchi hasa wa Manispaa ya Morogoro kuliko kuitumia mito yao kuendelea kutoa huduma katika mabwawa ambayo yatahudumia mikoa mingine nje ya Mkoa wa Morogoro? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, anasema si vyema kuanzisha Bwawa la Kidunda, Serikali iliona ni muhimu sana tuwe na Bwawala Kidunda kwa ajili ya kuhakikisha kwanza wananchi wa Dar es Salaam watapata maji ili muda wote Mto Ruvu uwe unakuwa na maji ya kutosha. Bwawa lile pia tumeshalifanya usanifu siyo kwa ajili ya maji tu lakini pia pamoja na kuzalisha umeme. Kwa hiyo, lina manufaa mengi na hivi sasa tupo mbioni kupata wawekezaji tunaoweza kushirikiana nao tuweze kujenga bwawa lile. Maeneo yale mengine ambayo hayana maji, Naibu Waziri ameshasema vizuri kwamba kwenye programu yetu awamu ya pili tunakwenda kushughulikia tatizo la maji katika maeneo hayo.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo ambalo lipo kwenye maeneo mengi katika nchi yetu ni miradi ya maji ambayo Serikali ilianzisha kushindwa kutekelezwa. Jimboni kwangu kuna miradi ya maji katika Kijiji cha Majalila na Igagala na imeanza kufanyiwa kazi na imefikia asilimia 70. Sasa hivi miundombinu ya miradi ile imeanza kuharibika kwa sababu ya ukosefu wa fedha. Je, Serikali ina mpango gani wa kumalizia ile miradi ambayo kimsingi ingewasaidia wananchi kwenye maeneo hayo?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli ipo miradi mingi, tuna miradi zaidi ya 508 ambapo katika awamu ya kwanza ya programu haijakamilika. Hivi sasa ipo katika hatua mbalimbali, ipo kwenye asilimia 99 na mengine 60. Sasa hivi tumeingia awamu ya pili ya programu lakini lazima kwanza tukamilishe ile miradi ambayo ipo mbioni kukamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi fedha zimeshaanza kupatikana kwa ajili ya kuwalipa wakandarasi ambao walikuwa katika hatua mbalimbali na maeneo mengine walikuwa yamesimama, kwa hiyo, tunawalipa ili kusudi wakamilishe miradi hiyo. Nilihakikishie Bunge lako kwamba Serikali itakwenda kukamilisha miradi yote ili wananchi wetu waweze kupata maji kama ilivyokusudiwa.
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona na kunipa nafasi. Napenda kumuuliza swali la nyongeza Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upo mradi wa umwagiliajii wa Bonde la Bigombo ambao ulianza 2012 na ulitakiwa kukamilika 2013, ulifadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika chini ya ASDP, mpaka sasa mradi huo haujakamilika. Mradi huu ilikuwa ni tegemeo kwa wananchi wa Jimbo la Ngara hususani wananchi wa Kata ya Rulenge, Keza na Nyakisasa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji. Ni lini sasa mradi huu utaweza kukamilika?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, jana nilisema kwamba miradi yote ya umwagiliaji inasimamiwa na Tume ya Umwagiliaji. Nikasema katika bajeti ya mwaka huu wa 2015/2016, tumepanga fedha kiasi cha shilingi bilioni 53 katika kuendeleza sekta hii ya umwagiliaji. Miradi hii ilikuwa imeanzishwa chini ya programu ya ASDP ambapo wafadhili ni African Development Bank na mingi ilikuwa haijakamilika. Kwa sababu tumeunda Tume, tutakwenda kufuatilia tuone tunaweza kukamilisha kwa namna gani mradi ambao tayari ulikuwa umeshaanza.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa sababu matatizo ya maji katika jimbo langu yanafanana sana na Jimbo la Kigoma Kaskazini, ninapenda nimuulize Mheshimiwa Waziri swali la nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini Serikali hii itakamilisha Mradi wa maji katika Mji wa Tunduma kwa sababu imekuwa inaahidi mara nyingi kwamba itatengeneza maji na hata wakati Mheshimiwa Rais anaomba kura kwa wananchi pia alisema kwamba ataweza kuwaletea maji haraka iwezekanavyo ndani ya mwaka mmoja mradi utaanza kutekelezwa. Leo hii kuna kampuni ambayo tayari imekubali kujenga…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwakajoka, swali si umeshauliza? Nadhani swali umeshauliza, kwamba huo mradi utakamilika lini?
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nataka nikumbushe kidogo kwa sababu kuna kampuni leo imekuja hapa na mradi ule umeshapitishwa na Wizara lakini tunashangaa Wizara ya Fedha hawataki kukubali mradi ule uanze kujengwa haraka. Kwa sababu mradi ule ulitakiwa uanze kujengwa mwanzoni mwa mwaka huu lakini mpaka sasa hivi hakuna kinachoendelea. Tunataka kupata majibu.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kuwapatia wananchi wote maji safi na salama kwa kiwango cha asilimia 85 ifikapo mwaka 2020. Kwa hiyo, naomba nikuhakikishie, hayo unayoyazungumza ni historia, Serikali inakwenda kutekeleza Mradi wa Maji Tunduma ambao nina uhakika na tuwashauri wananchi wa Tunduma waiamini Serikali ya Awamu ya Tano. Ahsante.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri yenye kutia moyo wananchi wa Wilaya Meatu. Mradi huu ni wa muda mrefu wa mwaka 2009, yapata sasa miaka sita, wananchi walitoa eneo hilo na kuacha kufanya shughuli zao pasipo malipo, matokeo yake bwawa hilo limekuwa likijaa na kusababisha uharibifu wa mazingira ikiwa ni pamoja na mmomonyoko wa udongo. Naomba Mheshimiwa Naibu Waziri aniambie Wizara katika mpango mkakati wake wa mwaka 2016/2017, imepanga ni lini mradi huo utakamilika na uanze kutumika?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, nimekuwa nikishuhudia miradi kama hii, Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kwa ajili ya kuchimba mabwawa, lakini yamekuwa hayakidhi mahitaji kama ilivyokusudiwa, kwa mfano mradi wa maji Mjini Mwanuhuzi, naomba Serikali iniambie je, inaniahidi nini kukamilisha mradi huo na kuusambaza katika Vijiji vya Jinamo, Paji, Mwanjolo, Koma na Itaba?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ameuliza ni lini bwawa la Mwanjolo litakamilika; katika bajeti yangu ambayo nitawasilisha hapa Bungeni muda siyo mrefu, tumeliwekea bwawa hili mpango wa kuweza kulikamilisha, kwa hiyo, tutaleta maelezo na kazi ambazo zitafanyika ili tulikamilishe bwawa hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili kuhusu mradi wa maji anaoelezea, lini tutakamilisha katika vijiji vingine; mambo yote haya tumeyaweka kwenye mpango, kwanza tunakamilisha miradi yote ambayo inaendelea iliyokuwa kwenye program ya maji awamu ya kwanza, halafu tunaingia awamu ya pili. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge nia ya Serikali ni kwamba, miradi yote ambayo ipo tutaikamilisha na tutakwenda kuikagua kuhakikisha kwamba inafanywa jinsi inavyotakiwa. Ahsante.
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona na kunipa nafasi hii. Asilimia 90% ya wakazi wa Mkoa wa Singida wanategemea maji ya visima ambapo vingi vya pump za mkono na wengine wanachota maji kwenye malambo na mabwawa na hasa maeneo ya vijijini, lakini maji hayo hayakidhi viwango na pia hayatoshelezi mahitaji. Je, Serikali haioni imefika wakati wa kutafuta wawekezaji wakubwa ili kupunguza adha hii ya maji katika Wilaya zote za Mkoa wa Singida na hasa ikizingatiwa Wilaya ya Singida ni wilaya ambayo ina hali ya ukame kijiografia? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza sitaki nibishane naye kuhusu takwimu anazosema kwamba asilimia 90% ya wananchi wa Singida wanatumia pump za mkono. Hili ni jambo ambalo kitakwimu itabidi tulizungumze na nitalileta wakati nawasilisha bajeti yangu, atajua ni wangapi wanatumia pump za mkono na wangapi wanatumia taratibu zingine ili kupata maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la msingi ni kwamba katika Programu ya Maji, wa kuamua chanzo cha maji cha kutumia tuliwaachia wao wenyewe wananchi hasa halmashauri kulingana na teknolojia na gharama za mradi, kwa hiyo, maeneo mengi walichagua visima lakini katika programu hii tulikuwa hatutumii pump za mkono. Pump za mkono ni katika miradi ile ambayo inafadhiliwa na wafadhili kama Water Aid na mashirika madogo madogo kama yale au NGO’s, ndiyo wamekuwa wanatoa pump za mikono. Kama Tigo nimekwenda juzi Singida nimefungua mradi wa vijiji 12 kwa pump za mkono.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Programu ya Maji tunatumia aidha ni pump za umeme wa generator au kama kuna grid karibu ndiyo wanaunga, kitu cha namna hiyo. Kwa hiyo, tutajaribu kuangalia, kuna baadhi ya maeneo ambayo wako karibu na mito, tunaweka mradi mkubwa ambao unaweza kwenda kusambaza maji katika vijiji vingi. Sasa ili kusudi Mheshimiwa Mbunge upate jibu zuri, naomba unisubiri nitakapowasilisha bajeti yangu, nitaonesha ni miradi ya namna gani inakuja kwa Mkoa wa Singida kuangalia vyanzo na nini tutatumia.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante. Pamoja na majibu mazuri yenye matumaini ya Naibu Waziri kwa wananchi wa Mji wa Kasulu, ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali langu la kwanza nataka kujua, hilo andiko la mradi kama Naibu Waziri anaweza akakumbuka, ni lini limepelekwa Tume ya Mipango ili tuweze kuwa na comfort kwamba jambo hili linashughulikiwa? Kama atakumbuka!
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, napenda kujua, naona fedha hizi shilingi bilioni 9.89 takriban shilingi bilioni 10 sasa, zinaombwa toka ufadhili wa Serikali ya India. Sasa kwa sababu zinaombwa toka Serikali ya India, napenda kujua kupitia kwako: Je, Serikali ina fallback yoyote endapo Serikali ya India haitatoa fedha hizi? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia masuala ya maji katika Mji wa Kasulu. Ni kwamba andiko hili tulishalipeleka Serikali ya India, kwenye Tume ya Mipango ilishapita, tumeshalipeleka tayari na muda siyo mrefu tunategema kwamba tuta-sign mkataba wa makubaliano ya kutekeleza mradi huu. Kwa hiyo, hali ni nzuri. Kama kutatokea kwamba kutakuwa vinginevyo, Serikali ipo. Serikali ya Awamu ya Tano katika vitu vyote ambavyo tayari tumeshavipanga, tutaweza kutumia fedha za ndani, kuweza kutekeleza mradi wa Kasulu.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwa vile suala hili la maji ni suala la kisera; na kwa vile miraji mingi ya maji inayotekelezwa kwa kupitia Halmashauri za Wilaya inakwama; na kwa vile ni Wizara inayohusika na maji ndiyo inayopeleka miradi hii isimamiwe na Halmashauri za Wilaya; na Halmashauri za Wilaya hizi hazitekelezi majukumu yake vizuri na kukwamisha Wizara kufikia yale malengo waliyojiwekea. Na kwa vile Wilaya ya Songea katika kijiji cha Maweso na Lilondo, miradi hiyo imekwama kwa sababu tu certificate za wakandarasi hazijafikia Wizara mpaka leo;
Ni hatua gani Wizara ya TAMISEMI inachukua pale ambapo miradi inakwamishwa na Halmashauri, ni miradi ambayo kimsingi inatoka kwenye Wizara zingine? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa kujibu vizuri sana maswali aliyoulizwa ya nyongeza kwenye sekta ya maji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu spika, tumetoa maelekezo kwenye Halmshauri wakiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Programu ya Sekta ya Maji kwamba kwa sasa hivi tunapeleka fedha baada ya kuletwa certificate. Sasa Mheshimiwa Mbunge kama unayo certificate ya kazi ambayo imeshafanyika naomba uniletee hata leo, tutakwenda kulipa. Kwa sababu wanasema certificate zipo lakini tumeangalia uhalisia kule Wizarani certificate hazipo, sasa kama ipo certificate na kazi imefanyika tunakwenda kulipa ili kusudi wakandarasi warudi wafanye kazi miradi ya maji iweze kukamilika.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE:Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali moja la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri ya Maji.
Kwa kuwa tatizo la maji ni kubwa sana karibu nchi nzima na Majimbo matatu haya ya Kibakwe, Mpwapwa na Kongwa ni tatizo kubwa. Kuna visima ambavyo vilianzishwa kuchimbwa vya Benki ya Dunia mpaka sasa havijakamilika. Mpaka sasa hivi Mjini Kongwa, dumu moja la maji wananchi wananunua shilingi 1,000;
Je, Mheshimiwa Waziri, utakuwa tayari kutembelea maeneo hayo kuhakikisha kwamba miradi hii ya Benki ya Dunia ambayo haijakamika sasa ikamilishwe?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli yapo maeneo ambayo tunayo hii miradi ya vijiji kumi ambayo haijakamilika na tumesema tu katika Awamu hii ya Pili kwanza tunakaribisha miradi ambayo imeshaanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo suala la kutembelea kuangalia hiyo miradi ambayo inasuasua, kwa sababu kusuasua inawezekana ikawa tatizo ni mkandarasi ambaye amewekwa. Sasa kama itaonekana ni tatizo la mkandarasi tutachukua hatua kulingana na mkataba wenyewe.
Kwa hiyo, kama tatizo ni fedha nimeshasema fedha sasa hivi Awamu ya Tano imeshajipanga vizuri, fedha zipo za kuweza kukamilisha miradi hii ambayo tayari iweze kupata huduma ya maji kwa wananchi wetu.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Matatizo ya maji kwenye maeneo ya Shinyanga na Korogwe ni sawa na matatizo kwenye maeneo yetu. Naomba Serikali ituambie na iwape matumaini wananchi wa Tarafa za Sikonge, Kiwele, Inyonga mpaka Kwilunde ambako yeye Mheshimiwa Kamwelwe anawakilisha; ni lini sasa shida za maji za wananchi hao zitapungua au zitaisha kabisa? Ahsate sana.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Sikonge, niseme kwamba tulikuwa tumetoa nafasi kwamba kila halmashauri ilete vipaumbele ya vijiji ambavyo wataanza navyo katika kutekeleza programu ya maji. Kwa hiyo, hayo maeneo anayoyasema Mheshimiwa Mbunge naamini kabisa halmashauri yake imeweka ndivyo vipaumbele.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunasema katika miaka mitano tunataka tupeleke miradi ya maji, kwa maana ya upatikanaji wa maji na ule mtawanyiko utakuwa kwa asilimia 85 ikifika mwaka 2020. Katika kutekeleza miradi hii ndiyo wao watachagua ni ipi tuanze na maeneo yale ambayo hayana maji kabisa wangeweka ndiyo kipaumbele ili kusudi tufikie asilimia hii tunayotaka kuifikia tukifika mwaka 2020. Kwa hiyo, yeye ndiye anajua vizuri zaidi majina ya vijiji na zile kata na wao ndiyo wanatakaoweka vipaumbele, Serikali tutaviwekea bajeti ili tuweze kufikia lengo na wananchi wetu waweze kupata maji.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru na mimi kupata nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa kijiji cha Ikelu kinafanana kabisa na swali la Korogwe; kuna mradi wa kutoka Tove kuja Mtwango mpaka Ilunda, bomba la maji limepita lakini kijiji cha Ikelu ni kilometa mbili tu hakina maji. Serikali ina mpango gani wa kuwapelekea maji wananchi hawa hasa ikizingatiwa kuwa wako kilometa mbili tu toka bomba lilipo?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Sanga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tuna mradi wa Tove-Mtwango ambao unapita karibu na kijiji hicho anachokisema. Awamu ya kwanza hatukuwa tumefikiria kijiji hicho kupata maji lakini sasa kwa jinsi tunavyotanua mtandao wananchi wale walioko umbali wa kilometa mbili toka bomba lilipopita tutaweza kuwaunganishia ili wapate maji.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yenye matumaini, hata hivyo, nina swali moja la nyongeza. Kwa kuwa, tatizo la maji ni sugu katika Kata ya Saja, Kijombe, Wanging‟ombe na Njombe Mjini, je, Serikali itatatua lini tatizo hili nimekuwa nikiulizia mara kwa mara swali hili katika Bunge lililopita? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, naomba niongezee kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Mgaya kama ifuatavyo:-
Kwanza tunakiri kweli kuna upungufu mkubwa wa maji maeneo hayo unayoyataja, Njombe Mjini kuna tatizo kubwa, Makambako kuna tatizo kubwa, hizo Kata za Saja, Kijombe na Wanging‟ombe zote zina matatizo makubwa. Ndiyo maana Serikali imeshafanya usanifu wa kukarabati miradi iliyopo na kuongeza miradi mipya.
Mheshimiwa Naibu Spika, tayari Serikali imepata milioni 500 US dollar sawasawa na shilingi za Kitanzania trilioni moja kwa ajili ya kuweza kukarabati miradi pamoja na Miji mingine 17. Kwa hiyo, kazi hii tuko kwenye hatua ya mwisho ya kuanza kutekeleza na tutafanya hivyo kwa kuanzia mwaka wa fedha 2016/2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana wananchi wa huko wawe na imani na Serikali ya Awamu ya Tano kwamba tunakwenda kumaliza tatizo hili. Mheshimiwa Rais alipokuwa Makambako, nakumbuka kabisa alisema nipeni Urais, nitakwenda kumaliza tatizo la maji Makambako. Mheshimiwa Sanga alikuwepo nataka nikuhakikishie tatizo la maji Makambako tunakwenda kulimaliza. Ahsante. (Makofi)
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii, vilevile niishukuru kauli ya Serikali kwa kunipa matumaini kwamba sasa wananchi wangu wangu wa Makambako watapona.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tatizo la Makambako ni la muda mrefu takribani zaidi ya miaka 30 na kitu, mradi ambao tunao pale ulikuwa unahudumia watu 15,000 na sasa tumeshaongezeka na tumefikia zaidi ya watu 160,000. Je, Serikali imejipangaje kuona sasa tatizo hili linatatuliwa mapema na kama Rais alivyokuja alituahidi kwamba tatizo hili atalitatua?
Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri Waziri mwenye dhamana alikuwepo siku ile wakati Rais anazungumza kwamba, atakapomteua Waziri aanzie Makambako leo unawaambiaje watu wa Makambako?
La pili…
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyotoa maelezo ya nyongeza kwa muuliza swali la msingi niseme tu kwamba, nitakachofanya sasa baada ya Bunge hili mimi nitatembelea Makambako, tutakwenda kuongea na wananchi ili tuwape mpango ambao tunao wa kutekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Tatizo la maji la Makambako kwa asilimia kubwa linafanana na Jimbo la Bunda Mjini. Natambua Serikali ya Awamu ya Nne ilianza mradi mkubwa wa maji tangu mwaka 2006 ni wa muda mrefu sana na ulikuwa ukamilike, lakini mpaka sasa hivi haujakamilika.
Mheshimiwa Naibu spika, mradi ule unaanzia Kata ya Guta lakini hauna vituo na kama mradi ule wa kupeleka maji katika Mji wa Bunda ukiwa na vituo, vile vijiji jirani Kinyambwiga, Tairo, Guta A, Guta B, Gwishugwamala, vyote vitanufaika na mradi wa maji. Sasa je, Mheshimiwa Waziri haoni kwamba kuna haja ya kuweka vituo ili vijiji hivyo vinavyopita mradi kwenda Mji wa Bunda vinufaike na mradi huo? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kuna mradi ambao tumetekeleza katika Mji wa Bunda tumeweza kujenga bomba kubwa kutoka Ziwa Victoria, tumeweza kujenga matanki, hiyo ni awamu ya kwanza. Sasa awamu ya pili tutakwenda kusambaza katika maeneo yale ambayo bomba hilo limepita. Kwa hiyo, naomba niseme tu kwamba, kazi hiyo tutakwenda kuifanya kwa manufaa ya wananchi wa Bunda. Ahsante. (Makofi)
MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza
swali.
Mheshimiwa Spika, hali ya ukame wa chakula katika nchi yetu, kimsingi inasababishwa
na matatizo mawili makubwa. Tatizo la kwanza na matatizo yote mawili yanatokana na maji.
Aidha, kunakuwa na ukame kwa maana ya kukosekana kwa maji, ama kunakuwa na mafuriko
kwa maji kuwa ya ziada. Suluhisho la kudumu la tatizo la chakula katika maeneo mengi ya nchi,
mbali na Serikali kuendelea kutoa misaada ufumbuzi wa kudumu wa tatizo la muda mrefu ni
kufanya water management kwa njia mbili.
Mheshimiwa Spika, kwenye maeneo yenye mafuriko kufanya flood management na
kwenye maeneo yenye ukame wa maji kufanya water conservation yaani hifadhi ya maji
hususani wakati wa mvua.
Mheshimiwa Spika, sasa swali ni hili, kwa nini Serikali isiweke mpango maalum kupitia
Halmashauri za Wilaya mbalimbali kwa kila Halmashauri kuwa na mpango wake wa kuangalia
namna bora ya uhifadhi wa maji kwa wakati wa mafuriko, vilevile uhifadhi wa maji wakati wa
msimu wa mvua ili yatumike kwa ajili ya unyweshaji maji. Vilevile utaratibu wa uzuiaji wa
mafuriko (flood management) wakati wa mafuriko ili tuepukane na hili tatizo la chakula kwa
utaratibu wa kudumu zaidi?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri Mkuu
naomba nijibu swali la Mheshimiwa Mbowe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, wazo la kuvuna maji ya mvua tutalileta kwenye awamu ya pili
ya programu ya maji. Ni wazo la msingi kwamba ni lazima sasa tuelekee kuvuna maji ya mvua.
Pia masuala ya kuweza kuzuia mafuriko ni jambo ambalo tutalifanya kwenye program ya pili.
Kwa hiyo, tutaleta mpango huo ambao kila Halmashauri tutaangalia kwamba kila mwaka
ikiwezekana wawe na mpango wa kuweza kujenga mabwawa madogo madogo ambayo
yako chini ya uwezo wao. Wizara ya Maji itakwenda kusimamia na miradi mikubwa ya strategic
dams hiyo itasimamiwa na Wizara ya maji.
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa maji ya kijito cha Endagaw yamekuwa mengi kuliko utaalamu ulivyoona na kwa hivyo mfereji mmoja unaweza ukafanya ukuta uliojengwa kubomoka.
Je, Waziri anaweza kuwahakikishia watu wa Endagaw na wa Hanang kwamba huu upande wa pili utajengewa mfereji mara moja?
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, palipokuwa na kijito cha Endagaw kulikuwa na wananchi ambao walikuwa na shughuli zao na makazi yao na wakaondolewa kwa ajili ya skimu hiyo.
Je, Serikali inaweza kutusaidia kuwapa fidia wale watu ambao wameondoka pale kwa ajili ya mradi huu? Namuomba Mheshimiwa Waziri aweze kutembelea eneo hilo na kuona umuhimu wa maswali haya mawili ya nyongeza niliyoyauliza, ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze kwa kuibua swali hili. Tunasema kwamba ili tuweze kupata chakula cha kutosha lazima tuende kwenye kilimo cha umwagiliaji. Sasa hivi Taifa letu tumeshaanzisha Tume ya Umwagiliaji itakayosimamia eneo hili. Mpaka sasa Taifa linalima hekta 461 tu tunataka katika miaka mitano ijayo tufikishe hekta milioni moja. Sasa kwa kuanzia na hiki Kijiji cha Endagaw ambapo tayari tumeahidi kuendelea kujenga skimu ile, hizo laki nne tutazipeleka lakini tutaboresha kwa namna ambavyo anashawishi Mheshimiwa Mbunge ili wananchi wale waweze kupata faida ya kilimo cha umwagiliaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili nitakwenda kuangalia katika kuwahamasisha wale wananchi tutaona namna gani ya kuwafidia. Jambo moja zuri ni kwamba fidia nzuri ni ile kuwajengea skimu ambayo wataweza kuendelea kulima kuliko wakipewa fedha lakini wasiendelee kulima. Kwa hiyo, tutaangalia namna bora ya kuwafidia kwa kujenga skimu ili walime kilimo cha umwagiliaji.
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali moja la nyongeza. Kwa kuwa, tatizo la Karagwe linaendana sana na tatizo la maji lililopo Jimboni Busokelo, Wilaya ya Rungwe. Je, Serikali ina mpango gani hasa katika Kata za Ntaba, Itete, Isange pamoja na Kandete kuwapelekea maji ukizingatia Kata ya Ntaba kuna bwawa la asili ambapo wananchi 12 wameuawa kwa sababu ya kutafuta maji?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge pamoja na Wabunge wengine ambao wangeweza kusimama kuuliza Kata zao, Vijiji vyao ambavyo vipo tofauti na swali la msingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwamba, anayeamua ni kijiji kipi tuanze nacho ni ninyi wenyewe kwenye Halmashauri yenu. Kwa hiyo, katika Bajeti ya mwaka huu, wamesema ni Kata ipi tunaanza halafu tutaendelea na Kata nyingine. Tulisema kwenye mradi huu wa Vijiji 10, kwanza tunakamilisha miradi ambayo tayari ilishakuwa imeanza au ina mikataba haijaanza, tukamilishe ile halafu tutaingia kwenye mikataba mipya. Sasa katika kuingia vijiji vipi, mnachagua ninyi kule kule, Waziri hawezi kuwachagulia.
Kwa hiyo, naomba sana ndugu zangu tushirikiane na Halmashauri zetu kuweka vipaumbele vijiji vile ambavyo vina shida kubwa ya maji ndivyo tuanze navyo. Vile vyenye shida au miradi ilishakuwepo labda imechoka iwe ni phase ya pili. Kwa hiyo, naomba sana tushirikiane ili tuchague Vijiji vile ambavyo vina shida zaidi ya maji, tuanze navyo katika Bajeti ya Mwaka 2016/2017.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza.
Kwanza naipongeza Serikali kwa kutenga fedha kwa ajili ya upembuzi yakinifu, lakini kutokana na uhaba mkubwa wa maji unaowakabili wananchi wa Urambo, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Swali la kwanza la nyongeza, kwa kuwa mradi huu ndio kwanza mradi wa maji ya kutoka Malagarasi uko katika awamu ya upembuzi yakinifu; na kutokana na umbali wa Mto Malagarasi kutoka Urambo, na shida iliyopo pale Urambo. Nilikuwa nataka nimuulize Mheshimiwa Waziri kwamba hivi Serikali haioni wakati huu wanapoendela na upembuzi yakinifu wakachimba bwawa la maji Mto Ugala ili bwawa hilo lipate maji kutoka Mto Ugala, pia na maji ya mvua ambayo yanapotea bure ili yawasaidie wananchi kupata maji wakati bado huu mradi ambao utachukua muda mrefu unaendelea kushughulikiwa.
Swali la pili la nyongeza, ningependa kujua hizo lot, au awamu ambazo zitatekelezwa katika upatikanaji wa maji kutoka Malagarasi na kuhakikishiwa kwamba Tarafa ya Usoke imo pia?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wakati tunashughulikia huu mradi mkubwa tumetenga fedha kwa ajili ya Halmashauri ya Wilaya ya Urambo kwa ajili ya kuweza kuhakikisha wananchi wa Wilaya ya Urambo kwa ajili ya kuweza kuhakikisha wananchi wa Urambo wana endelea kupata maji wakati tunasubiri huu mradi mkubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia katika kufanya usanifu wa Miradi hii tunaangalia kitu kinaitwa cost na benefit. Yaani kuchukua maji Mto Malagarasi itafaidisha vijiji 68 katika Wilaya ya Uvinza, Uyui, Kaliua, kwa hiyo ni mradi ambao una-benefit watu wengi zaidi na ndio maana Serikali ikaona kwamba tuweke, badala ya kuchukua Mto Ugala ambao kiangazi unakauka tuweze kuuchukua huu mradi mkubwa ambao wananchi wengi watapata maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu suala la bwawa, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwanza tutatembelea eneo lile ili tuone uwezekano kwamba bwawa hili lifanyiwe usanifu kwa ajili ya maji ya umwagiliaji kwa ajili ya wananchi wanaoishi maeneo yale.
MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Naibu Spika, matatizo ya maji katika Jimbo langu la Rufiji ni makubwa na hatuwezi kuyafananisha na Morogoro. Eneo dogo la Rufiji ambalo linapata maji safi ni Tarafa ya Ikwiriri, lakini tumeharibikiwa motor pump huu sasa mwezi wa Nane. Tuliwasilisha maombi kwa Mheshimiwa Waziri lakini mpaka leo hii hatujapata motor pump hiyo au kupata fedha kwa ajili ya ununuzi wa motor pump ili kuweza kuwasaidia wananchi wa Jimbo langu la Rufiji.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nipate taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, ni lini sasa fedha hizi zitatoka kwa ajili ya ununuzi wa motor pump ili kuweza kuwasaidia wananchi wa Jimbo langu la Rufiji hususan Tarafa ya Ikwiriri? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa ni mwezi wa Sita na mmepitisha bajeti ya Wizara ya Maji ambayo utekelezaji wa bajeti unaanza Julai. Sasa naomba tusubiri fedha za Mwaka wa Fedha wa 2016/2017 itakapotoka ndipo tuweze kumpatia Mheshimiwa Mbunge.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, Jimbo la Rombo kama yalivyo Majimbo mengine tuna shida kubwa sana ya maji, shida yetu hasa inatokana na kampuni ambayo inasambaza maji katika Jimbo letu Kili Water kuwa na ukata mkubwa baada ya GTZ waliokuwa wafadhili wake kujiondoa. Halmashauri tangu awamu iliyopita imeleta maombi katika Wizara ya Maji ili tuweze kuanzishiwa mamlaka kwa sababu mamlaka ina uwezo wa kukopa kuanzisha vyanzo vipya vya maji ili iweze kusimamia vizuri hali ya maji katika Jimbo letu. Hivi majuzi nimemkumbusha Waziri kuhusu hitaji hilo.
Sasa nataka nijue, je, Serikali ni lini watatusaidia kwa kushirikiana na TAMISEMI ili tuweze kuwa na mamlaka ya maji katika Wilaya ya Rombo itakayoweza kusimamia vizuri usambazaji wa maji yaliyopo na kuanzisha vyanzo vipya vya maji?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwenye Sera yetu ya Maji ya mwaka 2002 miradi ya maji ni shirikishi kati ya Serikali na wananchi, Serikali inajenga wananchi wanaiendesha kwa mfumo wa kutengeneza hizi mamlaka ndogo ndogo na mamlaka kubwa.
Kwa hiyo, zipo taratibu naomba nimhakikishie Mheshimiwa Selasini kwamba tutakwenda kuliangalia ombi lake viability ya Halmashauri yake kuweza kuendesha huo mradi badala ya Kili water. Kwa hiyo, hilo tunalichukua na tutakwenda kulifanyia kazi. (Makofi)
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali moja la nyongeza.
Kwa kuwa, Wilaya ya Mpwapa na Kongwa kuna mabonde mazuri sana ya maji na yanatiririsha maji mwaka mzima. Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga scheme ya umwagiliaji katika vijiji vya Godegode, Nzovu, Bori, Msagali, Tambi, Mang’weta, Chamkoroma, Mseta na maeneo mengine ili scheme hii iweze kusaidia kilimo cha umwagiliaji na kusaidia kuondoa tatizo la njaa, katika maeneo hayo?(Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, mapendekezo yake ya kutaka scheme hizo za Godegode na zingine mara nyingi tunaziandaa wakati tunatayarisha bajeti, kwa mwaka huu katika mapendekezo ambayo tulikuwa tumeyapitisha kwenye bajeti kwanza ni kuendeleza na kukamilisha scheme ambazo tayari zilikuwa zinaendelea na zina makandarasi, tukasema awamu hii tutaendelea kwanza tufanye usanifu katika miradi mingine itakayofuata baada ya kukamilisha hii ambayo inaendelea. Kwa hiyo Mheshimiwa, Godegode kwanza tuangalie zile scheme ambazo tayari tunazikamilisha halafu tutaanzisha na hizo zingine mpya. Tutazifanyia usanifu Tume ya Umwagiliaji ndiyo kazi kubwa itakayofanya mwaka huu wa fedha katika kuhakikisha maeneo mengi ambayo yanaweza kufanyiwa umwagiliaji tuweze kuyafanyia kazi.
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Chanzo cha maji Masokeni kuimarishwa kwa shilingi milioni 759 na miundombinu ya kuhakikisha Vijiji vya Mande na Tella katika Jimbo la Moshi Vijijini ni fedha kidogo kwa kuwa eneo lenyewe ni kubwa, mahitaji ni makubwa. Serikali inaji-commit vipi kuhakikisha kwamba pamoja na fedha hizi watatafuta chanzo kingine cha fedha ili mradi huu ukamilike kama walivyoahidi hapa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Moshi Vijijini, Kata nyingine za Kirua Kusini, Mamba Kusini, Mwika Kusini, Kahe Mashariki, Kahe Magharibi pamoja na Makuyuni ambayo ni Mji mdogo wa Himo ambao unapanuka kwa kasi kubwa tatizo la maji ni kubwa sana na Kata ya Mamba Kusini imebidi Diwani aanze kufanya harambee... (Makofi)
MHE. JAMES F. MBATIA: Ndiyo nauliza swali, Serikali inaji-commit vipi kwenye maeneo haya mengine niliyoyataja ambayo maji ni muhimu kwa uhai wao ili waweze kupata maisha endelevu kama raia wengine wa Jamhuri ya Muungano? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri aliyoyatoa kwamba kwanza walitangaza tenda, halafu mradi ule haujaanza. Hata hivyo, tumeshatoa maelekezo kwa Halmashauri zote ile miradi ambayo haikuanza kwa sababu ya ukosefu wa fedha kwamba miradi hii ndio viwe vipaumbele kwa awamu hii tunavyoanza katika utekelezaji wa bajeti ya 2016/2017, hayo ndiyo maelekezo tuliyoyatoa. Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwamba fedha ni kidogo, ni kweli shilingi milioni 759 haiwezi kumaliza mradi kwa mara moja, lakini ni fedha ambayo unaweza ukatangaza ukampa advance mkandarasi akaanza kujenga. Sasa hivi tunazo fedha za Mfuko wa Maji ambazo tunapeleka kukwamua miradi yote inayoendelea. Kwa hiyo, naomba sana Halmashauri wakaanze kazi fedha hizi zinatosha kupeleka Vijiji vya Tella na Mande. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu yale maeneo mengine ambayo umesema yana matatizo makubwa. Nayo pia tumetoa maelekezo kwamba kila Halmashauri iweke mpango wake katika kutekeleza awamu ya pili ya program ya maji kwamba tukimaliza vijiji kadhaa tunaendelea na vijiji vingine ili tufikishe ile azma kwamba Serikali inataka tukifika mwaka 2020 tuwe na 85% wananchi wanaokaa Vijijini wanapata maji na wanaokaa mijini wanapata kwa 95%. Kwa hiyo, tumeshatoa maelekezo usiwe na wasiwasi Mheshimiwa Mbatia tutakwenda kupeleka maji katika maeneo yote kulingana na namna tulivyopanga bajeti. (Makofi)
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Matatizo yaliyopo katika Jimbo la Moshi Vijijini yanafanana na matatizo yaliyopo katika Jimbo la Ubungo maeneo ya Kilungule, Kimara Baruti, Korogwe na Golani, Kata ya Kimara pamoja na Makoka, Kajima na Nova Kata ya Makuburi. Je, Serikali ni lini itawapatia maji wananchi wa maeneo hayo? Ahsante sana.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ya Ubungo maeneo mengi tunategemea yatapata maji baada ya kukamilisha huu mradi wa Ruvu Juu ambao tayari umeshakamilika. Tatizo lililopo ni kwamba umeme uliopo pale Ruvu Darajani ni mdogo tuna pump kubwa sana ya kuleta maji Dar es Salaam; tumeshaanza kuvuta line ya umeme kutoka Chalinze kuleta pale. Tutakapomaliza line ya umeme maeneo yote ya Ubungo yale yatapata maji kutoka Ruvu Juu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge asiwe na shaka.
MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza naomba nitoe pole kwa wananchi wangu wa Lupilo wanaopata misukosuko ya kubambikiziwa kesi na Jeshi la Polisi, nalaani vikali matumizi mabaya ya nguvu za Jeshi la Polisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali, mradi huu tangu uanze una miaka mitatu sasa hivi; upembuzi yakinifu sijui nini vinafanyika. Sasa Mheshimiwa Waziri anawaambia nini wananchi wa Lupilo wanaotarajia mradi huu uwe mkombozi wa maisha yao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, Mheshimiwa Waziri haoni umuhimu wa kuiunganisha ofisi yake ya kanda na Mkurugenzi wangu wa Ulanga ili iwe rahisi kwa ajili ya ufuatiliaji na utekelezaji wa mradi huu?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kuweka uzito katika masuala ya umwagiliaji kwa sababu huu ndiyo ukombozi wa huko tunakokwenda kuhakikisha Watanzania watakuwa na chakula cha uhakika kwa kilimo cha umwagiliaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuhusu mradi huu, ni kweli kwa mwaka huu wa fedha tumeamua kwamba katika bajeti iliyokuwa imetengwa ya bilioni 35, bilioni sita ndizo fedha za ndani. Sehemu kubwa ya kazi hii ilikuwa ni kufanya upembuzi yakinifu na kufanya mapitio ya mabwawa mbalimbali ambayo tumelenga katika miaka mitano tufikishe hekta milioni moja. Kwa,hiyo, ni pamoja na bwawa hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa fedha zinazohitajika kwa bwawa hili peke yake ni bilioni 40, bajeti ya Wizara kwenye umwagiliaji ni bilioni 35. Kwa hiyo, ni fedha nyingi tunahitaji tu-mobilize fedha kutoka kwa wafadhili mbalimbali ili tuweze kupata fedha za uhakika. Naomba niwahakikishie wananchi wanaoishi kwenye eneo hili la Lupilo kwamba mradi huu Serikali itakwenda kuutekeleza na katika mwaka wa fedha 2017/2018 tutaweka fedha kuanza kujenga skimu hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali la pili, mapendekezo yake kwamba Ofisi ya kanda iweze kuunganishwa, naomba hili nilichukue tutakwenda kuangalia uwezekano wa kufanya hivyo.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kwa kuwa Wilaya ya Longido Mkoa wa Arusha ni mojawapo kati ya Wilaya ambazo zina changamoto kubwa ya maji, wakazi wa eneo hili wamekuwa wakitumia asilimia 90 ya muda wao kwenye kutafuta maji na kuna tuhuma ya kuwa kuna pesa zaidi ya milioni 400 zilitolewa lakini hazijulikani zimeenda wapi na wananchi wa Longido wanaendelea kuteseka. Je, ni lini Serikali sasa itatekeleza ahadi yake ile ya mradi mkubwa wa maji wa bilioni 13 katika Wilaya hii ya Longido?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli katika bajeti ya mwaka huu tumeweka fedha kwa ajili ya kuanza kujenga mradi huo mkubwa wa kupeleka maji katika Wilaya ya longido. Naomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira, Serikali inaendelea na taratibu za manunuzi ili tuweze kupata mkandarasi wa kujenga mradi huu.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri ningeomba niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa tatizo la maji pale Ilula, Wilaya ya Kilolo ni kubwa na Mheshimiwa Rais aliahidi kwamba anataka kuwatua akinamama ndoo kichwani, ni la muda mrefu. Je, Waziri anaweza akatoa majibu mazuri ambayo yatawafanya wananchi wa Ilula wapate moyo na kuacha sasa kuniita mimi Mwamaji badala ya Mwamoto?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikuhakikishie Mheshimiwa Mwamoto kwamba Serikali itapeleka maji ya uhakika kwa wananchi wa Ilula. Serikali bado inaendelea kushughulika kuweza kutafuta fedha za kugharamia mradi huo na tupo kwenye hatua nzuri. Serikali ya Austria imeonesha nia ya kusaidia mradi ule, bado hatujakamilisha tu makubaliano ya fedha ambazo tutaweza kugharamia mradi huo, lakini mazungumzo yanaendelea vizuri. Nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge hutaendelea kuitwa Mwamoto utaitwa Mwamamaji ili kusudi wananchi wa Ilula waweze kupata maji.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kunipa nafasi ili kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, shida ya maji katika Jimbo la Ludewa inafanana sana na shida ya maji katika Jimbo la Ukonga. Ukitembelea kata za Kivule, Msongola, Chanika, Buyuni, Zingiziwa, Pugu, Pugu Station, Ukonga, Gongo la Mboto na Kipunguni. Kata hizi zote hazina maji kabisa na hasa maji ambayo yanasimamiwa na Serikali ambayo ni maji safi na salama.
Sasa nilikuwa naomba kuuliza, kwa sababu nimezungumza mara nyingi Bungeni hapa kuuliza shida ya maji Dar es Salaam na hasa Jimbo la Ukonga ni nini kauli ya Serikali na hasa Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana kwamba baada ya Bunge hili tuongozane kwenda Ukonga akashuhudie watu wa Ukonga wanavyokunywa maji machafu na hasa kwenye shule, zahanati na vituo vya afya?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Jimbo la Ukonga lina changamoto ya upatikanaji wa maji. Lakini tunayo mipango ambayo inayoendelea katika Mpango wa Utekelezaji wa Programu Phase II ipo miradi ambayo Jimbo la Ukonga wametengewa fedha. Lakini katika mpango wa muda mrefu, maeneo ya Ukonga, Mkaranga na maeneo ya Kigamboni, maji yatapatikana kutoka chanzo cha Mpera na Kimbiji. Ambapo sasa utekelezaji wake tumeanza kuchimba visima karibu visima 20 vinakamilika. Baada ya hapo tunajenga miundombinu ambayo tutapeleka maeneo hayo ya Ukonga na kutakuwa hakuna tatizo kubwa na nikuahidi kwamba katika kipindi cha miaka hii minne ambayo imebakia katika Seriali ya Awamu ya Tano, tutahakikisha kwamba Ukonga inakuwa na maji ya kutosha.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mradi wa maji ni tatizo kweli, katika Wilaya ya Morogoro Vijijini, katika vijiji vya Furwe, Mikese, Gwata waliahidiwa mradi wa maji kwa muda wa miaka mingi, na wananchi wanateseka kwa maji kwa muda mrefu. Je, naomba kuuliza wananchi hawa ambao wameteseka kwa muda na wameahidiwa mradi wa maji watapata lini maji na mradi huu utatekelezwa lini?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshatoa maelekezo katika kila Halmashauri namna ya kupanga vipaumbele katika vijiji ambavyo havina maji; sasa awamu hii ya kwanza siwezi kusema ni vijiji vipi vimepangwa, lakini Halmashauri yake inafahamu na wameleta vipaumbele na tumeweka kwenye bajeti na fedha zimetengwa. Kwa hiyo, sasa hivi ni ufuatilia tu utekelezaji, naomba nimuahidi Mheshimiwa Mbunge nitakaa naye ili kusudi niweze kuona hivyo vijiji anavyovisema vipo kwenye mpango wa mwaka huu au vipi, ili tuweze kuona namna ya kufanya.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tatizo la maji katika Jimbo la Kyerwa ni kubwa sana na wananchi wake hawapati maji, hata asilimia 20 haifiki: Je, Serikali inawaahidi wananchi wa Jimbo la Kyerwa kama alivyojibu, “upembuzi yakinifu unaoendelea utakapokamilika mwaka 2017/2018;” Serikali inaahidi kutenga pesa ya kutosha kwa ajili ya kukamilisha mradi huu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; ili miradi hii iweze kusimamiwa vizuri, ni vizuri tukawa na wataalam. Wilaya yangu ya Kyerwa hatuna wataalam wa kutosha, lakini wataalam wenyewe hao waliopo hawana vitendea kazi kama gari na vifaa vingine. Je, Serikali ipo tayari kutuletea wataalam wa kutosha na vitendea kazi ili kazi isimamiwe vizuri?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza alitaka kujua kama katika bajeti ya mwaka 2017/2018 tungeweza kuweka fedha kwa ajili ya ujenzi wa mradi huu ambao unaendelea kufanyiwa usanifu. Namwahidi kwamba kazi hiyo tutaifanya ili wananchi wetu kule waweze kupata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la pili, kwamba Wilaya yake ina wataalam wachache; ni kweli wilaya nyingi hazina Wahandisi wala vifaa. Katika Program ya Sekta ya Maji Awamu ya Pili, tumeweka bajeti kwa ajili ya kununua magari na vifaa muhimu, lakini pia tumeomba vibali kwa ajili ya kuajiri Wahandisi wa kutosha ili tuweze kuwapeleka kwenye wilaya mbalimbali.
MHE. ALLY S. UNGANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Je, Serikali ina mpango gani wa kutumia Mto Rufiji kutoa maji ili wananchi wa Kibiti, Bungu, Ikwiriri, Kimanzichana na Mbagala wafaidike na mto huo?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ungando, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kutumia Mto Rufiji au vyanzo vingine; haya tunafanya maamuzi baada ya kufanya usanifu wa maeneo yale tunayotaka kupeleka yale maji. Kwa hiyo, tunalinganisha gharama kwa wakati ule. Uwezo wa Serikali; kwa mfano, ukichukua maji kwenye mto na ukapeleka vijiji vingi au kilometa 100, gharama yake ni kubwa. Kwa hiyo, lazima uangalie uwezo pia wa Serikali. Kwa hiyo, kama kuna uwezekano wa kupata vyanzo ambavyo ni nafuu kwa gharama, tunaanza navyo hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mipango ya muda mrefu, tulishajibu hapa Bungeni kwamba tunafanya usanifu wa kuona uwezekano wa kuchukua maji ya Mto Rufiji na kuleta maeneo ya mpaka Mkuranga. Kwa hiyo, jambo hilo linafanyiwa kazi na Serikali. Muda utakapofika, basi tutawajulisha Waheshimiwa Wabunge kama hilo linawezekana kwa bajeti inayokuja au baada ya hapo.
nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tatizo Kyerwa linafanana moja kwa moja na tatizo lililopo katika Halmashauri ya Wilaya Masasi. Tatizo letu kubwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Masasi ni masuala ya miundombinu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tuna maji ya kutosha. Serikali iliahidi kutenga shilingi bilioni moja kwa ajili ya kuleta miundombinu itakayofikisha maji katika Vijiji vya Mbemba, Mbaju, Maparagwe pamoja na Chikunja. Je, Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kupeleka pesa angalau kidogo kidogo katika hii miradi ili iweze kutekelezwa mara moja?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ya mwaka 2016/2017, kila Halmashauri imetengewa fedha kwa ajili ya kuendeleza miradi ambayo ilishakuwa imeanza. Hii ni pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Masasi. Fedha hizo hatutapeleka moja kwa moja; tumeagiza kwamba walete certificate kwa sababu nyingi wameshakuwa na Wakandarasi. Walete certificate ili tuweze kuwalipa wale Wakandarasi waweze kuendelea na utekelezaji wa miradi hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama Mheshimiwa Mbunge kuna Mkandarasi na kuna certificate ambayo haijalipwa, niletee ili tuweze kulipa, fedha zipo. Hatuwezi kupeleka fedha zikakae tu, tunataka fedha ziende na zifanye kazi.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii nami niulize swali dogo tu kwa kifupi. Kwa kuwa matatizo yaliyopo huko Kyerwa yanafanana sana na yaliyopo katika Jimbo langu la Manyoni Magharibi katika Mji wa Itigi ambao hauna maji kabisa toka nchi hii imepata uhuru. Je, sasa Serikali iko tayari kusaidiana na Halmashauri ya Itigi ili wananchi wa Itigi Mjini pale wapate maji?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali imeahidi kupeleka maji katika Mji wa Itigi na mpango huo upo. Kwa hiyo, tunaendelea kufuatilia utekelezaji wa yale mambo ambayo tulishakubaliana kwa mwaka huu tunafanya nini. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira, Serikali itahakikisha kwamba Mji wa Itigi unapata maji.
MHE. KABWE Z. R. ZITTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu kwamba, moja ya gharama kubwa sana ya miradi ya maji ni gharama za kusukuma maji, pampu za maji na kwa mujibu wa mradi huu tunategemea kutumia pampu za umeme wa mafuta kwa kuweka jenereta na kununua umeme kutoka TANESCO ambapo gharama zitakuwa ni kubwa zaidi kwa wananchi katika kuyalipia hayo maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri haoni kwamba, itakuwa ni jambo la busara na economical kutumia hizi liquidated damages ambazo wamempa Mkandarasi kufunga solar pumps, ili ziweze kupunguza gharama za uendeshaji wa mradi kupelekea wananchi waweze kupata maji kwa gharama nafuu?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli mradi huu kwa usanifu wake tumesanifu kutumia pump kwa kutumia nishati ya umeme. Naomba nipokee ushauri wake kwamba, tuweze kuangalia uwezekano wa kubadilisha. Tukishakuwa tumekabidhiwa huu mradi Serikali tunaweza tukabadilisha sasa pampu zile tutumie solar kwa maana ya kutaka kupunguza gharama za uendeshaji wa mradi ule.
MHE. PETER J. SERUKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majawabu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, mradi huu wa maji wa Kigoma Mjini utakuwa unazalisha zaidi ya lita milioni 42 kwa siku, Matumizi ya Mji wa Kigoma haitazidi zaidi ya lita milioni 24, wanasema mpaka 25. Mheshimiwa Waziri haoni sasa na hili swali naliuliza mara ya tatu kwamba, mradi huu sasa waongeze vijiji vya jirani ambavyo ni Vijiji vya Mwandiga, Kibingo mpaka Bigabiro pamoja na kwenda Msimba ili na sisi tufaidike kwa sababu, tatizo la maji kwa Jimbo la Kigoma Kaskazini ni kubwa sana?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli mradi huu utazalisha maji mengi zaidi ya lita milioni 42 kwa siku, zaidi ya mahitaji ya wananchi wa Kigoma Mjini. Lengo la Serikali la kuweka mradi huu ni kwamba, lazima tusambaze katika vijiji ambavyo vinazunguka mji ule, ikiwepo na Mwandiga. Kwa hiyo, naomba nimwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali itazingatia ombi lake na tutahakikisha kwamba, maji haya yanafika mpaka maeneo hayo aliyoyataja.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa mradi wa maji unaoendelea Manispaa ya Sumbawanga umechukua muda mrefu na wananchi wa Manispaa ya Sumbawanga mpaka sasa hawajui huo mradi utaisha lini: Je, Serikali inawaambiaje wananchi wa Manispaa ya Sumbawanga ikiwepo wanawake ambao wanapata athari mpaka sasa na wengine kupata vifo kwa ajili ya kufuata maji kwenye umbali mrefu?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Serikali ina mradi mkubwa wa maji pale Manispaa ya Sumbawanga. Mradi ule ulikuwa umalizike toka Septemba, 2015, sasa yalitokea matatizo; kwanza, ilikuwa ni kuchimba visima 12; visima sita virefu upande wa kusini na visima sita upande wa kaskazini. Kwa hiyo, ikabidi baada ya kuanza kuchimba tukakosa, visima vyote havikuwa na maji. Kwa hiyo, tukatafua upande wa Kaskazini, ikabidi tuongeze sasa idadi ya visima kutoka sita mpaka 17, hii ikasababisha muda kuongezwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwahakikishie wananchi wa Sumbawanga, kwanza mradi kwa sehemu kubwa umeshakamilika, kilichobaki ni kujenga mtandao. Ikifika mwezi Desemba mwaka huu mradi ule utakuwa umekamilika na wananchi wa Manispaa ya Sumbawanga watakuwa wanapata maji.
MHE. MBARAK S. BAWAZIR: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Nataka nimwulize Mheshimiwa Waziri, ni lini atamalizia mradi wa maji wa Kilosa, hasa akizingatia kwamba hivi sasa Kilosa kuna kipindupindu? Imebakia pesa kidogo ili wamalizie mradi huo wa maji endelevu.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kwenye maji, kwa kweli maji yako mengi sana Kilosa na kuna mabwawa yanahitajika yachimbwe kama Kilimagai, Godegode na Kidete. Haya mabwawa yatasaidia hata kuleta mafuriko ndani Kilosa yangu na vile vile katika…
Duh, ahsante
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nirejee pia kwa Waheshimiwa Wabunge wote. Hii miradi ya maji katika mwaka wa fedha 2016/2017 tumeainisha kila Wilaya ni miradi ipi ambayo ni vipaumbele inakwenda kufanywa na fedha zimetengwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba sana Mheshimiwa Mbunge aseme specifically ni mradi upi anaoulizia? Kwa sababu ndani ya Kilosa ipo miradi mingi, ili tuweze kujua hasa ni upi na ni hatua gani ambazo tunaweza kuzichukua. Kwa hiyo, naomba tuwasiliane na Mheshimiwa Mbunge, tukae ili tuweze kubadilishana mawazo tuone ni namna gani huo mradi ambao anauulizia, nimpe majibu ambayo ni sahihi.
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, majibu ya Mheshimiwa Waziri hayaridhishi. Anaongea habari ya gesi asili Shinyanga yaani mpaka gesi asili ije kufika hizi ni ndoto na kwa kweli tutaendelea kuumia na bei ya maji. EWURA hawajaenda kufanya consultation, hawajaenda kuongea na wananchi, wamepandisha bei ofisini. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Maji ya Shinyanga na Kahama wametengeneza muungano wakaweka kitu kinaitwa SHUWASA na kazi ya SHUWASA ilikuwa ni kuboresha usambazaji wa huduma ya maji katika Wilaya hizi mbili. Badala yake SHUWASA sasa hivi wanauzia maji Mamlaka ya Kahama na ya Shinyanga ambapo watumiaji wa mwisho wanaumizwa na bei kubwa kwa sababu ya kuwepo na mtu wa katikati. Waziri ana mpango gani wa kujaribu ku-standardize suala la bei ya maji katika wilaya hizi mbili kwa sababu hali hii inawaumiza wadau na wawekezaji wanakimbia kwa sababu hakuna huduma? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, nikimnukuu Mheshimiwa Rais Magufuli kwenye kampeni zake alisema atahakikisha akiingia madarakani nchi nzima tutapata maji na kama tukikosa maji atawageuza ninyi Mawaziri kuwa maji, lakini mpaka leo hamjawa maji. Shinyanga ni Kata nane tu za Wilaya ya Kahama Mjini ndiyo zina maji wakati Kata 12 zote mpaka leo hazijapata maji, watu wanahangaika wanatumia maji taka na inatishia kuleta milipuko ya magonjwa. Ni lini watatimiza mpango wa kutandaza mtandao wa maji katika Wilaya hizi mbili ili watu waepukane na magonjwa? Ahsante sana.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge pamoja na jazba aliyokuwa nayo wakati akiongea, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba nimfahamishe kwamba masuala ya kupandisha bei yapo kisheria. Huyu mdhibiti ambaye anaitwa EWURA ipo procedure ambayo lazima aifuate. Kwa hiyo, procedure ya kupandisha bei ilifuatwa, hilo ni la kwanza.
Mheshimiwa Spika, pia naomba afahamu kwamba jurisdiction ya SHUWASA ni katika Mji wa Shinyanga kule Kahama wana mamlaka nyingine ambayo inashughulikia Kahama. Kwa hiyo, tunayo mamlaka ambayo inaleta maji SHUWASA kwa bulk halafu SHUWASA sasa ndo inafanya distribution.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hoja kubwa hapa ungesema tu kwamba unaona bei iliyowekwa ni kubwa, hilo ni jambo ambalo tunaweza tukazungumza. Ndiyo maana kwenye majibu tumesema kwamba nusu ya gharama za uendeshaji wa SHUWASA ni kulipa bili za umeme. Kwa hiyo, bili za umeme zikishushwa definitely na bili ya maji itashuka. Tukasema kwamba uzalishaji wa umeme kwa mfano kama tunatumia nishati ambayo inalazimisha bei ya umeme ishuke basi hata bei ya maji itashuka, ndiyo hoja ambayo ulikuwa umeuliza kwenye swali la msingi.
Mheshimiwa Spika, lakini pia ukielezea suala la kwamba mpaka sasa upatikanaji wa maji maeneo mengi hakuna, lakini ni lazima Mheshimiwa Mbunge afahamu tulipitisha bajeti mwaka huu na tumepanga fedha za kutekeleza miradi na kila Wilaya inaendelea kutekeleza. Sasa akilizungumza kwa ujumla inakuwa vigumu kuelewa swali lake tulijibu vipi. Nataka awe specific na swali kwamba ni Wilaya ipi na ni mradi upi ambao haujakamilika. Serikali inaendelea kukamilisha miradi kulingana na mpango ambao Wabunge mlipitisha.
Mheshimiwa Spika, naomba nitambue Mheshimiwa Masele ndiye aliyeuliza swali kwa Mheshimiwa Rais kuhusu bei za maji.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye (b) ya swali langu niliuliza, ni miradi gani inayotarajia kutekelezwa, muda wa utekelezaji, gharama za kila mradi na nani anayewajibika katika utekelezaji? Sasa majibu ya Serikali hayajanielezea mradi, ila ameelezea maeneo ambayo mradi utatekelezwa. Sasa nataka niambiwe katika maeneo haya ambayo miradi itatekelezwa, kuna miradi gani specifically, kuna Kampuni gani specifically? Hilo la kwanza.
La pili, zimetajwa dola bilioni 32, nami nilivyouliza swali, nilikuwa nataka nijue gharama za kila mradi kwenye Jimbo langu. Sasa swali langu la pili: Je, hizi bilioni 32 ndiyo zote zinaenda kwenye mradi wa Jimbo la Kawe na kama siyo, nataka nijue Jimbo la Kawe specifically katika hii dola bilioni 32 mgao wake ni kiasi gani na kwa miradi ipi? Nadhani nimeeleweka.
Swali langu nataka uchambuzi ili wananchi wangu wanaosikia kila mmoja ajue kwake anastahiki gani. Sasa Serikali ikinipa kiujumla jumla nitashindwa kuja kuwabana.
Kwa hiyo, nataka uchambue, siyo unajibu kiujumla jumla.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa katika jibu la msingi, tumeshasema mradi ambao unaendelea, Mkandarasi anaitwa Jain Irrigation Company na tumesema gharama ya mradi ni US Dollar milioni 32. Tunapokuwa tunapanga miradi, huwa hatupangi Kijimbo. Tunapanga mradi kwa ajili ya Jiji la Dar es Salaam na sehemu kubwa ya mradi huu uko kwenye Jimbo lake.
Ndiyo maana tumetaja hayo maeneo ya Kawe, Mabwepande, yote yote yako kwenye Jimbo la Kawe. Kwa hiyo, tumelijibu kikamilifu kama alivyouliza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sehemu yake ya pili alikuwa anataka kujua kama hizo US Dollar milioni 32 ni kwa Jimbo la Kawe tu peke yake? Hapana, siyo kwa Jimbo la Kawe peke yake, ni pamoja na bomba kubwa ambalo litaenda baadhi ya maeneo ya Wilaya ya Bagamoyo.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya kiufundi yaliyotolewa na Naibu Waziri, nina maswali madogo tu ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ikolojia ya Mto Malagarasi ina athari ya moja kwa moja kwa maji katika Mji wa Kasulu, nilitaka kufahamu ule mradi mkubwa unaofadhiliwa na Serikali ya India kwa takriban shilingi bilioni 9.89, ni lini mradi huo sasa utaanza kutekelezwa katika Mji wa Kasulu ili Kasulu yote na viunga vyake na miji midogo inayozunguka Mji wa Kasulu iweze kupata maji ya uhakika?
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, nataka kujua mkandarasi aliyekuwa anashughulikia mradi wa kutoa maji Ziwa Tanganyika kuyaleta katika Mji wa Kigoma amefilisika, na mmetangaza kwamba sasa anatafutwa mkandarasi mwingine, napenda pia kujua juhudi za kumpata mkandarasi mwingine badala ya huyu aliyefilisika kwa mradi wa Kigoma Mjini zimefikia wapi?
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, ahsante.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, majibu.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, suala la miradi kwa ufadhili wa Serikali ya India, hatua tuliyoifikia sasa tunafanya shortlisting kupata mhandisi mshauri atakayefanya usanifu wa kina kuweza kujua ni shughuli zipi zitafanyika katika Mji wa Kasulu, ndiyo fedha ziweze kutoka. Kwa hiyo, tupo kwenye hatua hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili kuhusu mkandarasi ambaye ana mradi mkubwa wa maji pale Kigoma Mjini, naomba nisiseme kwamba tunatafuta mkandarasi mwingine kwa sasa, kwa sababu bado hiyo kandarasi haijafutwa.
Kwa hiyo, hayo ni mambo ambayo tunafikiria may be tunaweza tukafanya, lakini tukisema sasa, inaweza ikaathiri utekelezaji wa mradi huu. Serikali itahakikisha kabisa kwamba mkataba uliyokuwepo utakamilisha ili wananchi wetu wa Kigoma waweze kupata maji.
MHE. STEPHEN J. MASELE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mwezi uliopita Mheshimiwa Rais alifanya ziara kwenye Manispaa ya Shinyanga, Jimboni kwangu na aliagiza Waziri wa Maji aje Shinyanga akiambatana na mimi tukae tujadiliane mgogoro wa bei ya maji baina ya KASHUWASA ambao ni Mradi wa Maji wa Kitaifa na SHUWASA ambayo ni Mamlaka ya Maji ya Manispaa ya Shinyanga na wananchi wa Shinyanga:-
Je, Waziri wa Maji yuko tayari kuambatana na mimi mara baada ya Vikao hivi vya Bunge ili tukakae na wadau wote hao husika tutatue mgogoro wa bei kati ya KASHUWASA, SHUWASA na wananchi wa Shinyanga? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Mradi wa KASHUWASA ni Mradi wa Kitaifa, siwezi kukubali kama Mbunge, wananchi wa Shinyanga wabebeshwe adhabu ya kugharamia mradi wa Kitaifa kwa kubebeshwa bei kubwa ya maji. Nahitaji majibu leo, Waziri kama yuko tayari twende tukashughulikie mgogoro huu.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mhweshimiwa Spika, kwanza kabisa, kwenda Shinyanga siyo tatizo, tunaweza tukaenda, lakini tunapokwenda kule lazima tuelewane tunachokwenda kufanya. Tunakwenda kule kwanza tunarejea Sheria Namba 12 ya mwaka 2009 inayohusu uendeshaji na utoaji wa huduma ya maji. Ndani ya Sheria ile tuliweka Mamlaka ya Udhibiti inayoitwa EWURA, hii ndiyo imepewa mamlaka ya kupanga bei za maji.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais alichokielekeza ni kwamba, ni lazima tufanye ulinganifu kuangalia, je, maeneo mengine watu wanachangia maji kwa kiasi gani? Kwa Shinyanga Mamlaka ile bado ni changa. Bei ya maji inaweza ikaonekana kwamba ni kubwa kwa sababu ya wachache amboa ndio wanaochangia. Kwa hiyo, Serikali tuna jukumu la kuongeza mtandao ili wananchi wengi waingie kwenye mtandao waweze kuchangia huduma ya maji ili iweze kuwa endelevu.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tutakwenda Shinyanga, lakini nataka twende huku wakijua kwamba, siyo kwamba tunakwenda kushusha bei. Tunakwenda kufanya ulinganifu wa kuona ni kipi kifanyike kwa ajili ya kuboresha huduma ya maji.
MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kutokana na ukubwa wa tatizo la maji, Bunge lako liliidhinisha Sheria hapa ya kuweka zuio la fedha ambazo Mheshimiwa Naibu Waziri hapa amekiri kwamba fedha zipo, lakini maji hakuna. Sasa swali ambalo nataka watupatie majibu, tumewapa fedha, lakini kwenye miji na vijijini kwetu kule maji hakuna. Nini kinachowafanya wanakwamisha miradi ya maji mpaka sasa hivi inashindwa kukamilika? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, ni kweli tulipitisha Sheria ya Mfuko wa Maji; na fedha hizi huwa zinatolewa kila mwezi; lakini ili fedha hizi zitumike tulipeleka mwongozo kwenye Halmashauri zetu za Wilaya. Pamoja na mwongozo, tumefanya semina nchi nzima na Wakurugenzi pamoja na Wahandisi wa Maji kwamba fedha hizi zitatolewa kwa mfumo wa certificate. Kwa sababu tulishakubaliana katika bajeti ya mwaka huu kwamba kwanza tukamilishe miradi inayoendelea.
Mheshimiwa Spika, nimetembelea baadhi ya Halmashauri, unakuta fedha wanazo zilizo-carry forward kutoka mwaka uliopita, lakini hawajafanya jambo lolote, wanasubiri wapelekewe fedha. Mwongozo tumewapa na tumewaelekeza. Kwa hiyo, kuna baadhi ya Halmashauri ziko na ile hali ya ufanyaji kazi wa kimazoea, hawataki kwenda na kasi ya Awamu ya Tano tunavyotaka matokeo.
Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge, awe karibu sana na Halmashauri yake kuweza kuona kwa nini hiyo miradi haiendelei? Kwa sababu, wakileta certificate, hakuna certificates ambazo zimebaki, tumeshapeleka fedha. Sasa hivi tuna certificates chache sana. Kila mwezi zikija, tunapeleka fedha. Kwa hiyo, nashauri tukae tuweze kuona kwa Halmashauri yako hasa ni nini kinachoendelea?
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Spika, nakushukuru nami kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kijiji cha Ishololo katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga kilitengewa fedha kwa ajili ya Mradi wa Umwagiliaji, zaidi ya shilingi bilioni moja. Mradi huu haujaweza kukamilika na Mkandarasi kuweza kuondolewa na Serikali kwa sababu, mradi huu haukuisha kwa wakati. Je, Mheshimiwa Waziri, uko tayari sasa kuja katika Kijiji cha Ishololo na kuona mashimo tuliyoachiwa na mkandarasi yule na mradi huu kuwa hauna tija kwa wananchi wetu?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza niko tayari kutembelea miradi yote ya kilimo cha umwagiliaji. Labda niseme tu, hii miradi ya kilimo cha umwagiliaji katika sehemu kubwa, mingi ina matatizo. Kwa sababu ya matatizo, kweli tumekwenda tumekuta miradi mingi haifanyi kazi jinsi inavyotegemewa.
Mheshimiwa Spika, ili tuweze kurekebisha hivi, ndiyo maana Serikali tulianzisha Tume ya Umwagiliaji. Kazi yake ya kwanza ilikuwa kurekebisha miradi yote iliyokuwa imeanzishwa kwa ufadhili mbalimbali huko nyuma ikiwa chini ya Wizara ya Kilimo, tuweze kurekebisha.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimwahidi Mheshimiwa Azza, fedha hata zikipatikana katika bajeti ya mwaka huu, tutaweza kuona nini tufanye katika kurekebisha mradi huu ambao Mheshimiwa Mbunge anauelezea.
MHE. SOFIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Tuliku-miss hekima zako.Kwa kuwa tatizo la wana Ngara linafanana kabisa na tatizo la watu wa Rungwe. Rungwe kuna vyanzo vingi sana vya maji, lakini tuna shida ya maji katika Vijiji vya Mpandapanda, Ikuti na sehemu nyinginezo. Je, Mheshimiwa Waziri anatusaidiaje tuweze kupata maji ukizingatia tunavyo vyanzo lakini watu bado wanahangaika kupata maji salama? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, nimesimama kwa kutoa majibu ya ujumla kwa wale wengine ambao pengine watauliza swali linalofanana na la Mheshimiwa Sofia.
Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya mwaka huu, kama alivyosema Naibu Waziri kwamba kila Halmashauri tumepanga fedha kwa ajili ya kuendelea kutoa miradi ya maji. Sasa katika Halmashauri yako, ninyi ndio mlipanga vipaumbele kwamba kwa mwaka huu mtapeleka maji kwenye Vijiji vipi?
Mheshimiwa Spika, tumetoa mwongozo kwamba kama mmeshapanga vipaumbele, tangazeni tenda ili tupate Mkandarasi aweze kufanya. Waziri wa Maji anafanya kazi ya uratibu, mtekelezaji ni Mkurugenzi wa Halmashauri ambayo wewe unatoka kule. Naomba tusaidiane kusimamia hawa Wakurugenzi kwenye Sekta ya Maji ili waweze kufanya kazi inayotakiwa wananchi wetu wapate maji.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii adimu. Mbulu Vijijini tuna tatizo linalofanana na Ngara.
Mheshimiwa Spika, tuna Bwawa la Dongobesh ambalo limejengwa zaidi ya shilingi bilioni mbili; na kwa kuwa limekaribia kukamilika na Naibu Waziri ameshafika; kilichobaki ni njia tu ya maji ya kwenda kuwafikia watumiaji. Je, Mheshimiwa Waziri atuambie lini anapeleka fedha kwa ajili ya kumalizia tu hilo bwawa ambalo kimsingi limekamilika bado tu njia ya kwenda kupeleka maji kwa watumiaji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza ni kweli kwamba Mheshimiwa Flatei Massay Jimbo lake nimelitembelea, Bwawa la Dongobesh nimeliona na limekamilika kwa zaidi ya asilimia 90. Kilichobaki ni spillway ambayo itakuwa inatoa maji yale yanayozidi ili yasije yakabomoa ule ukuta mkubwa uliojengwa kwa gharama kubwa.
Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Flatei kwamba fedha imeanza kutoka. Mwezi uliopita tumepata shilingi bilioni moja na fedha zitakazotoka mwezi huu nitahakikisha napanga kwa sababu hela iliyobaki ni ndogo sana ili tulikamilishe hilo Bwawa la Dongobesh liweze kufanya kazi iliyotarajiwa.
MHE. STEPHEN H. NGONYANI: Mradi huu unagusa hasa sehemu za tambarare peke yake, ni lini sehemu za milimani kama vile Suji, Mkomazi, Manga Mtindilo, Mikocheni na Bwiko mradi huu nao utatekelezwa huko kwa sababu wakati wa mwanzo tuliambiwa hela zipo na mradi unaanza? Naomba kujua ni lini sehemu zile za milimani na zenyewe zitapata maji?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji ambavyo vitapewa maji katika mradi huu wa Same-Mwanga ni Bwiko, Mkomazi, Nanyongie, Manga Mtindilo na Manga Mikocheni, hii ndiyo ipo kwenye mpango. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba mradi umechukua muda mrefu na sababu kubwa ni kwamba mradi huu unategemea ufadhili wa nchi za Kiarabu. Sasa fedha ambazo unategemea mtu mpaka akupe huwa inachukua muda mrefu. Hata hivyo, Serikali tumeamua katika mwaka wa fedha unaokuja ule upungufu wa bajeti ambao upo tutaweka kwenye fedha zetu za ndani. Kwa hiyo, nitaomba sana Waheshimiwa Wabunge tuweke fedha za kutosha kwenye fedha za ndani ili mradi huu tuweze kuukamilisha.
MHE. SAVELINA S. MWIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kuwa matatizo ya maji ya Tabora ni sawa sawa na matatizo ya maji ya Mkoa wa Kagera hasa Bukoba Mjini. Kwa sasa hivi ukame umechukua muda mrefu mito mingi imekauka. Je, ni lini Serikali itatuweka kwenye Mpango wa Ziwa Victoria angalau hizi kata zilizoko karibu na Bukoba Mjini zipate maji?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge anazungumza kuhusu maji ya Ziwa Victoria kupelekwa Kata za Mjini Bukoba. Hivi sasa Serikali imejenga mradi mkubwa sana wa kutoa maji Ziwa Victoria kusambaza katika Mji wa Bukoba. Tatizo lililopo tu ni kwamba baadhi ya maeneo yako juu. Kwa hiyo, Serikali itaweka pump za kuweza kupandisha maji zaidi kwenye yale maeneo ambayo yako juu kuliko yale ya chini ili tuweze kuona kwamba wananchi wetu wa Manispaa ya Bukoba watapata maji ya kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ni kazi ambayo inaendelea na kila mwaka tumeweka fedha kila Halmashauri na tumetoa mwongozo kwamba kwa kulingana na fedha ambazo zipo tumetenga kwenye Bajeti yetu kila halmashauri ianze kufanya manunuzi ili kusudi maeneo yale ambayo hayakuwa yamefikiwa maji yaweze kufikiwa maji kulingana na malengo ya Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tunataka maeneo yote ya mijini tufikishe maji kwa 95% ikifika mwaka 2020; kwa hiyo Wabunge ni sehemu ya Baraza la Madiwani, tuwe karibu sana katika mipango ya maendeleo ya sekta maji kuhakikisha wananchi wetu wanapata maji.
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza swali langu limejibiwa nusu, mimi nimeuliza ni lini ujenzi wa chujio na usambazaji wa maji utakamilika? Kwa hiyo, yeye amejibu upande mmoja wa ujenzi wa chujio, hajajibu upande wa usambazaji wa maji. Na ujenzi wa chujio hili unasimamiwa moja kwa moja na Wizara ya Maji pengine ndiyo maana Mheshimiwa Naibu Waziri hana picha halisi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nina maswali mawili ya nyongeza; la kwanza ni kuhusu usambazaji wa maji katika Mji wa Mugumu baada ya kukamilika kwa ujenzi wa chujio hili. Nataka kumuuliza Naibu Waziri, bahati nzuri ulikuja mwaka jana pale Jimbo la Serengeti pale Mugumu na uliyaona yale maji, ninataka kujua kama kata zote za Mamlaka ya Mji mdogo wa Mugumu, kata saba Kata ya Morotonga, Kata
ya Mugumu, Kata ya Stendi Kuu, Kata ya Getaisamo, Kata ya Kisangura kama zote zitapata maji, pamoja na vijiji vinavyozunguka lile bwawa, Kijiji cha Miseke, Kijiji cha Rwamchanga na Kijiji cha Bwitengi. Hilo ni swali la kwanza, ningependa kujua kwamba wakati wa usambazaji wa maji
haya maeneo yote yatapata?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; huyu mkandarasi ambaye anajenga chujio hili (PET) anadai sasa hivi ana certificate ambayo iko Wizarani ya zaidi ya milioni 200 na kimsingi mradi ule unasuasua pengine kwa sababu hana fedha. Je, Wizara iko tayari kumlipa certificate anayodai ili aendelee na hii kazi mradi ukamilike haraka huo mwezi wa sita?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa hii awamu tulianza kujenga chujio ili kuongeza uzalishaji wa maji ifikie lita milioni tano kwa siku, ambazo zinatosha kwa wakazi kwa sasa kwa wale wa mjini, lakini Serikali kwa kutumia mkopo wa dola milioni 500 tumetenga milioni nane US dollars ambazo ni sawasawa na shilingi bilioni 19 kwa ajili ya kuboresha usambazaji katika maeneo ya vitongoji vya Mji wa Mugumu. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge asiwe na shaka, tatizo la kupata maji ya uhakika kwa Mji wa Mugumu na vitongoji vyake linashughulikiwa na Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili kuhusu madai ya mkandarasi; madai hayo tutamlipa mara tu baada ya kupata hizo certificates, hakuna shaka ya fedha, fedha tunazo.
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwanza naomba nimpongeze Naibu Waziri, alipotembelea Wilaya ya Korogwe aliweza kuona hali halisi ya tatizo la maji lililopo katika mji wetu wa Korogwe. Hata hivyo aliahidi kutuletea shilingi bilioni mbili ili angalau tatizo la maji lile liweze kuondoka pale, swali; kwa kuwa
wameshatuletea milioni 500 kwa ajili ya kutoa maji kutoka kwenye Mto Ruvu, je, sasa Serikali zile fedha wameshaziingiza kwenye bajeti ili kusudi ziweze kutusaidia katika kutengeneza miundombinu ile ambayo ni mibovu maana yake
tutakapokuwa tumejenga matenki au tumejenga ule mkondo wa maji bila ya kuwa na matenki ya maji makubwa bado tatizo la maji litakuwa lipo pale Korogwe. Je hizi fedha shilingi bilioni mbili alizosema zimetengwa katika bajeti hii? Nashukuru.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tulitenga shilingi bilioni mbili kwa ajili ya kuboresha maji katika Mji wa Korogwe na tulitoa maelekezo kwamba usanifu ukikamilika tunatangaza tender kwa hiyo ikishatangazwa tender na wakianza kufanya kazi tutakuwa tunalipa kwa certificate jinsi zinavyokuja. Kwa hiyo, naomba nimuondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba mradi ule utatekelezwa na fedha zipo kwenye bajeti. Ahsante sana.
MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza pamoja na kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri ya mwanzo lakini pili nimpongeze pia na kumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuja kuyaona
mambo yanayoendelea Chalinze.
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Chalinze
wamechoka kusubiri maji na kwamba sasa imefikia sehemu sijui nisemeje maana yake Waziri yeyé mwenyewe ameyaona. Sasa je, Serikali pamoja na kutoa notice ya siku 100 imejipangaje kusimamia utekelezaji wa kusitisha mkataba
huu, kwa sababu tunavyofahamu sisi kwa mahitaji ya matanki 19 ujenzi wa vituo tisa na vioski vya kuchotea maji 351 sina hakika sana kama huyu mjenzi anaweza akamaliza. Pamoja na hilo pia naomba nimkumbe Mheshimiwa Waziri
kwamba mjenzi huyu ndiye yule ambaye amenyangwa passport na Mheshimiwa Rais kule Lindi, sasa je, Serikali imejipangaje juu ya wayforward baada ya kusitisha mkataba na mjenzi huyu? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa tunapokea pongezi ambazo anazitoa kwa Waziri Mkuu kwa kuweza kutembelea mradi huu. Kuhusu suala la notice tuliyoitoa kitu kinachofanyika sasa kwanza tulitoa barua kwa mfadhili ili kuomba no objection kwa sababu ni miradi ambayo ina ufadhili lazima
wao waidhinishe kama unataka kusitisha mkataba na kwamba wao watakuwa tayari kuendelea kufadhili kazi zilizobaki.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tulichokifanya
kwamba tumetoa notice ya siku 100 na tunafanya monitoring kufatilia kila siku kazi ambazo nazalisha, na sasa hivi na yeye mwenyewe anaweza kushuhudia ameongeza kasi ambayo
wala hatukutarajia, kazi inakwenda kwa nguvu sana. Ikifika tarehe 31 Mei tutafanya tathmini kuangalia kwa speed hii anayofanya je, anaweza akamaliza katika muda mfupi, lakini kwa wakati huo huo Serikali imechukua hatua kwamba
malipo yote ambayo yatakuwa yanatolewa anakatwa tozo ya ucheleweshwaji wa kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumeweza kumwagiza Mhandisi Mshauri kwamba aandae makabrasha ya zabuni ikifika tarehe 31 Mei kama itakuwa kasi ile hairidhishi tunaajiri mkandarasi mwingine kwa sababu fedha zile za kufanya ile kazi zipo na hakuna fedha ambayo imelipwa kwa kazi ambayo haijafanyika. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie wananchi wa Chalinze kwamba Serikali ina dhamira ya dhati ya kukamilisha mradi huu wa maji Chalinze.
MHE. STEPHEN J. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Siku nne ama tano zilizopita mradi mkubwa wa kitaifa wa maji wa KASHWASA Shinyanga ambao unasupply maji Manispaa ya Shinyanga pamoja na mji wa Kahama ulikatiwa umeme na TANESCO kwa sababu ya kutolipa bili za umeme.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kumuuliza Waziri wa Maji nimekuwa nikishauri hapa kwamba Serikali itenge ruzuku ya kusaidia mradi huu ili kuwaondolea mateso wananchi wa Shinyanga, Kahama na Maswa, je, Waziri yuko tayari kutenga
fedha kwenye bajeti ya mwaka huu kuhakikisha kwamba KASHWASA inasaidiwa ruzuku ya kuendesha mradi huo na kuwaondolea mzigo wananchi wa Shinyanga, Kahama na Maswa?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa kwa utaratibu mamlaka za maji tumeziweka kwenye makundi daraja A, B, na C. KASHWASA ni daraja A, kwa maana kwamba inatakiwa iwe inalipa maji
kutokana na mauzo ya maji. Sasa TANESCO wamekata deni ambalo walikuwa wanadaiwa na tatizo ni kwamba taasisi nyingi zilikuwa hazijaweza kulipa kwa wakati. Tunaendelea kusisitiza kwamba taasisi zote za umma lazima zilipe bili za
maji ili kusudi kuwezesha mamlaka zetu zilipe TANESCO. Kwa hiyo, hilo lililotokea, limetokea lakini kwa hivi tunasema wasiyazalishe madeni mapya na tutafika mahali tutaanza kukatia hata hizo taasisi za umma ambazo hazilipi bili za maji.
(Makofi)
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi uliyonipatia.
Mheshimiwa Naibu Spika, miradi mingi ya maji inayosimamiwa kitaifa inasuasua katika maeneo mengi, katika Jimbo langu la Rombo kuna miradi miwili, Mradi wa Leto na Mradi wa Shimbi Mashariki ni ya muda mrefu sana na upatikanaji wa fedha umekuwa unasuasua. Katika kipindi hiki ambacho hali ya ukame imekuwa kubwa sana ukanda ambao hii miradi ipo una shida kubwa sana ya maji. Sasa je, Serikali iko tayari kupeleka fedha zote za hii miradi ili ipate kukamilika wananchi wa eneo lote la ukanda wa chini katika
Jimbo la Rombo waweze kunufaika na miradi hii ambayo imechukua muda mrefu sasa kukamilika?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza anaelezea kwamba miradi kwenye eneo lake inasuasua, lakini tulishatoa maelekezo na nimetoa muongozo namna gani tutakwenda kutekeleza hii miradi hasa kwenye maeneo ya vijijini kwa maana ya utekelezaji wa Programu
Awamu ya Pili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa tunakamilisha miradi inayoendelea na utaratibu ni kwamba wakandarasi wengi wamesharudi sasa, walikuwa wamesimama kwa sababu ya fedha zilikuwa hazipatikani kwa wakati, lakini sasa wamerudi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, na sasa hivi kila mkandarasi aliyerudi akileta certificate tumekuwa tunalipa kwa wakati kwa hiyo, tunataka tupate matokeo ya haraka miradi ikamilike kwa sababu hatuwezi kuleta fedha tu zikae kwenye Halmashauri ya Rombo wakati hakuna kazi inayofanyika. Tunapeleka mahali ambapo kazi inafanyika, ili tupate matokeo ya haraka wananchi wetu waweze kupata maji.
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, asante sana kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa nikazie kusema kwamba, Mradi wa KASHUWASA wa Shinyanga sio mamlaka ni mradi na vilevile wananchi wa Mji wa Maswa leo sasa wanakwenda wiki ya tatu wanakosa maji kisa TANESCO imewakatia umeme kwa sababu hawajalipa bili ya umeme na wananchi wa Maswa wanalipa bili zao kwa muda unaostahili na maji wamekatiwa kwa sababu ya makosa sio ya kwao. Je, Mhesimiwa Waziri unawahakikishia ni lini wananchi wa Maswa na Shinyanga watapata maji? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu swali la Mheshimiwa Masele, tunaposema Mamlaka za Maji, KASHUWASA ni Mamlaka ya maji katika daraja la kwanza ambalo kwamba, linatakiwa lisipate ruzusu ya kulipa bili ya maji kutoka Serikalini, anatakiwa alipe kutokana na makusanyo ya madeni, yaani ya watu wanaotumia maji yale. Kwa hiyo, huo ndio utaratibu ambao tumepanga, tunazisaidia hizi mamlaka za daraja la C ambazo
hazina wananchi hawawezi kuhumili gharama za uendeshaji wa miradi ile. Kwa hiyo, katika hii miradi midogo midogo, hii tunatoa ruzuku na kwenye bajeti tunatenga fedha na mwaka
huu wa fedha tulitenga fedha, lakini na mwaka unaokuja tutatenga fedha kwa ajili ya kulipia ruzuku katika hizi mamlaka ndogo za daraja la C na B ambazo hazina uwezo wa kuweza kujiendesha.
MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Mamlama ya Maji ya Mji wa Karatu (KARUWASA) ina zaidi ya umri wa miaka mitatu, lakini uendeshaji wake umekuwa ukisuasua kwa sababu mamlaka hiyo bado haina
bodi ya usimamizi; majina ya wajumbe waliopendekezwa kwenye bodi hiyo yalishapita kwenye ngazi ya Baraza la Madiwani zaidi ya miezi sita. Ni lini bodi hiyo itaundwa ili isaidie uendeshaji wa mamlaka hiyo? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, tuna hizi mamlaka za bodi katika miji midogo zinaundwa chini ya TAMISEMI na ile miji ya mikoa na miradi ya kitaifa zinaundwa chini ya Wizara ya Maji. Sasa naomba nilichukue kwamba suala hili tuliangalie ni kwa nini mpaka leo bodi haijaundwa. Labda kutakuwa na tatizo, sasa siwezi kuwa na jibu sasahivi, nitakwenda kulifanyia kazi na nitamjulisha Mheshimiwa Mbunge ni wapi tumefikia kuhusu kuunda Bodi ile ya Maji katika Mji wa Karatu.
MHE. MAHMOUD H. MGIMWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja na ombi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na maelezo mazuri ya Serikali, naomba kupata commitment ya Serikali, lini mradi huu utaanza kufanya kazi kwa sababu vijana wengi waliopo katika Kijiji cha Ikweha wanategemea sana kupata ajira katika eneo hili ukichukulia kwamba muda wa matarajio ya kukamilika kwa mradi huu uliishia mwezi Agosti, 2016 na sasa hivi Serikali imesema wataanza rasmi Aprili 17. Sasa ni lini mradi
huu utakamilika?
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu ulikuwa
unashughulikiwa kati ya Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi pamoja na wafadhili, Serikali Kuu ilikuwa bado haijajiingiza. Naomba nichukue fursa hii kumuomba Mheshimiwa Waziri, wakati wa Bunge lako hili tukufu tuambatane nae aende akaone hali halisi na umuhimu wa mradi huu kwa ajili ya wananchi wa Kijiji cha Ikweha.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Mgimwa kwa kufuatilia miradi hii ya umwagiliaji. Pili, lini anasema utakamilika. Kama tulivyoeleza kwenye jibu la msingi, kwa sababu fedha hizi zilikuwa zimetolewa na wafadhili na ndio maana kulichelewesha kukamilisha marekebisho yanayotakiwa. Na kwa sababu wamekubaliana na Halmashauri waanze mwezi wa nne kwa hiyo, tunafikiria kulingana na kazi zenyewe ni ngapi
zinazotakiwa kurekebishwa, siwezi kusema muda hasa, lakini natarajia kwamba, katika miezi 12 iliyokuwa imepangwa mwanzo ndio hiyo ina-carry forward kwamba tutaanza mwezi wa nne kurekebisha marekebisho ambayo yamefanyika ili
kusudi mradi ule uweze kufanya kazi. Lakini pia mwaliko wa kutembelea mradi huo naupokea na tutakwenda kuutembelea na kuona hali halisi jinsi ilivyo.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, tatizo la mradi wa umwagiliaji la Mufindi Kaskazini linafanana kabisa na tatizo la mradi wa umwagiliaji uliopo katika Halmashauri ya Songea katika Kata ya Subira na katika Mtaa wa Subira. Mradi huu ni
wa muda mrefu, umeanza tangu mwaka 2008 na mpaka sasa hivi bado haujakamilika, pesa zilizotumika mpaka sasa hivi ni shilingi milioni 585 na bado panatakiwa zaidi ya shilingi bilioni moja ili kukamilisha mradi huu. Je, Serikali imetenga kiasi gani kwa ajili ya kukamilisha mradi huu kwa kipindi hiki cha Bajeti ya mwaka 2017/2018?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli miradi mingi ya umwagiliaji ina matatizo. Na ina matatizo kwa sababu, kwanza kulikuwa na udhaifu katika usimamiaji katika sekta hii, hii miradi ya kilimo. Na miradi mingi ilikuwa ina ufadhili wa JICA. Kwa hiyo, kulikuwa na weakness katika usimamizi, yaani ulikuwa dhaifu na ndio maana utekelezaji wake haukwenda kwenye viwango vinavyotakiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nikiri tu kwamba katika bajeti ya mwaka huu wa fedha tulitenga fedha kwa ajili ya kufanyia mapitio ya miradi yote ya umwagiliaji, ili kwanza tuweze kuirekebisha iweze kufanya kazi iliyokusudiwa, hiyo ndio kazi ambayo inaendelea sasa hivi.
Lakini pili, tulikuwa tunafanya usanifu wa miradi mipya ya umwagiliaji, sasa kwa sasahivi siwezi kukwambia bajeti ya mwaka 2017 ni kiasi gani, lakini nitakapowasilisha bajeti yangu najua utaunga mkono ili kusudi tuweze kukamilisha huu mradi wa Halmashauri ya Wilaya ya Songea.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa vile Waziri amekiri kwamba, miradi mingi ya umwagiliaji ilikuwa na matatizo sasa je, ni nini kauli ya Serikali kuhusu wakandarasi na wote waliohusika kufanya ubadhirifu wa pesa hizo nyingi, hasa ukizingatia kuna mradi wa umwagiliaji kule Kitele, Jimbo la Mtwara Vijijini mkoani Mtwara, ambalo kwa kweli wananchi walijitolea eneo lao, lakini mradi umejengwa chini ya kiwango, mifereji ina nyufa
na ule mradi haujaanza kutumika. Nini kauli ya Serikli kuhusu miradi hiyo? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa
Naibu Spika, kama nilivyosema hii miradi tunaifanyia mapitio, lakini pale itakapoonekana mkandarasi au kuna mtu yeyote amefanya ubadhirifu, Serikali itachukua hatua zinazostahiki kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo, naomba asiwe na wasiwasi, lakini lengo kubwa hasa la Serikali ni kuhakikisha kwamba miradi hii tunaikamilisha ifanye kazi iliyokusudiwa kwa wananchi.
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo la Ngara yapo mabonde matano ambayo Serikali iliyaainisha kwa ajili ya kuanzisha skimu ya umwagiliaji. Upo mradi katika Bonde la Vigombo ambao mradi huo ulianza kutekelezwa na ulitakiwa ukamilike mwaka 2014, lakini mpaka sasa haujakamilika. Haitoshi, katika Bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali ilitenga takribani shilingi bilioni 2.1 kwa ajili ya kutekeleza
miradi katika mabonde mawili, Bonde la Mngozi, Kata ya Nyakisasa na Bonde la Muhongo katika Kata ya Bukiliro, lakini mpaka dakika hii tuko quarter ya nne hakuna hata senti moja ambayo ilishapelekwa kwa ajili ya kutekeleza miradi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, nini kauli ya Mheshimiwa Waziri kwa wananchi wa Jimbo la Ngara kuhusu upelekaji wa fedha na ili kuweza kutekeleza miradi hii kama ilivyopangwa katika bajeti?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa
Naibu Spika, kwanza ni kweli kuna miradi ambayo
inaendelea kwenye mabonde hayo anayoyaelezea. Lakini kwa sababu wanataka kujua lini ni vizuri hata mimi nikapata nafasi ya kuingia kuuangalia mradi maana siwezi kujua miradi yote lini itakamilika. Lakini lengo la Serikali ni kwamba, miradi yote tutaikamilisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, na suala la kupeleka fedha; fedha hatuzipeleki tunalipa certificate. Tumeshafanya mambo ya kupeleka fedha halafu unakuta fedha zinakaa hazishughuliki vyovyote. Tunataka matokeo kwa hiyo, fedha tutapeleka kulingana na utekelezaji wa mradi.
MHE. HUSSEIN M. BASHE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa dhamira ya Serikali ni kujenga Taifa la Viwanda na sekta ya kilimo kuwa ni muhimu. Katika Halmashauri ya Mji wa Nzega tumekuwa na mradi uliokuwa unasimamiwa na Shirika lililokuwa linaitwa NZEDECO miaka ya 1970 na miaka ya 1980 la umwagiliaji katika Kata ya Idudumo, mradi huu sasa hivi umekufa. Vilevile katika Halmashauri ya Mamlaka Ndogo ya Mji wa Igunga nako katika Bwawa la Imamapuli limejaa tope.
Mheshimiwa Naibu Spika, je, Serikali iko tayari
kuhakikisha kwamba miradi hii miwili katika Halmashauri hizi mbili katika mwaka wa fedha wa 2017/2018 wanatenga fedha kwa ajili ya kuifufua miradi hii ili wananchi wa maeneo hayo waweze kufaidika?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli ipo miradi mingi ambayo inaendelea nchi nzima na ni kwamba ni suala la Wizara yenyewe kuweka vipaumbele kwa sababu katika miradi huwezi ukatekeleza yote kwa wakati mmoja kutokana na upatikanaji wa fedha.
Na kama anasema kwamba je, tuko tayari kutenga fedha kwa mwaka huu wa fedha unaokuja; itategemeana na mawasilisho ya Wilaya ya Nzega, kwa sababu ninyi ndio mnaleta mapendekezo na vipaumbele katika Wilaya yenu.
Kwa hiyo, kama mkiweka hii ndio kipaumbele Serikali basi itaangalia namna ya kutenga fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi hiyo.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa kweli nimesikitishwa sana na majibu wa Waziri ambaye naamini ni msomi na najua ni mtaalam wa mambo ya maji. Nimesikitika sana, kwanza mradi huu ambao uligharamiwa na Serikali ya Japan ulipelekwa Wizarani tangu 2012. Mwaka jana mwezi Novemba nikamwona Waziri nikamweleza, akaniomba nilete ile proposal na maombi nikampelekea.
Mheshimiwa Spika, licha ya kwamba hata hakunipa majibu, nashangaa leo akisema bwawa hili ni dogo ambalo
gharama zake 2012 ilikuwa milioni 800 na linahudumia wananchi ambao ni zaidi ya 40,000. Hata hivyo, kibaya zaidi amejichanganya tena na huo mradi wa Kalema dam ambao mwenyewe mwaka jana tukiongea juu ya bwawa hili. Nilimweleza wazi kwamba hawa UN-CDF wamekuwa tayari kulihudumia bwawa hili, nilichokuwa nimekosa kwenye Halmashauri ilikuwa utaalam.
Mheshimiwa Spika, mpaka sasa Umoja wa Mataifa, wamekuwa tayari na Serikali ya Norway imeonesha kwamba
iko tayari kusaidia mradi huu, leo anajichanganya hapa na kusema anarudisha Halmashauri. Mradi huu wa Kalimawe ni square kilomita 24; Je, hilo ni bwawa la kati? Hapo nilikuwa nazungumzia masikitiko yangu. Swali langu ni kwamba kama Waziri aliona hili lingerudishwa kwenye Halmashauri, kwa nini hakunijibu hivyo, tangu mwaka jana Novemba?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, Wizara hii kutokana na ripoti ya Mkaguzi wa Ufanisi katika Ujenzi wa Miradi ya
Maji Mijini, imeonesha uzembe mkubwa sana na upotevu mwingi wa hela za miradi, kiasi kwamba naamini ndio
maana wanashindwa hata kujenga miundombinu ya kumwagilia maji ili wananchi wetu, wakulima waweze
kuvuna….
Mheshimiwa Spika, nauliza je, kama Wizara inaona haiwezi kufanya mambo ya umwagiliaji badala yake walijua kuchakachua tu miradi ya maji, kwa nini wasiachie kazi hiyo au watumishi wake wakafukuzwa?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge
kwamba jinsi tunavyojibu maswali haya inategemea na namna ulivyouliza. Wewe umeuliza kwamba hili bwawa
umeleta maombi kwa muda mrefu, sasa na sisi tunatengeneza majibu kulingana na swali ulilouliza. Kwa hiyo,
hatujafanya uzembe wa aina yoyote katika kujibu.
Mheshimiwa Spika, pia naomba nimpe taarifa pia kwamba miradi hii ya mabwawa ya umwagiliaji ilikuwa ina
wafadhili mbalimbali ikiwepo JICA ndiyo walioweza kufadhili. Hatukuwa tumeiweka katika mipango ya bajeti ya Serikali ambayo sisi tunasimamia moja kwa moja. Sasa maombi yake tumesema kwamba sasa tunafanya mapitio, siyo kwa bwawa lake tu yako mengi nchi nzima, ili tuweze kuona ni namna gani tutayashughulikia.
Mheshimiwa Spika, pia swali la nyongeza la pili, kwamba kuna mradi ambao una uzembe, ambao haridhiki na utekelezaji wake. Naomba atuletee ili tuweze kuona nini kifanyike na kama kuna watu waliofanya uzembe basi
tuwachukulie hatua.
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Pamoja na hayo naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vijiji hivi ambavyo vimewekwa kwenye kundi la vijiji vilivyoko katika kilometa 12, infact viko vijiji vingine ambavyo viko ndani kabisa ya kilometa moja kwa maana kwamba vilisahaulika wakati wa usanifu wa mradi mwanzo hasa vijiji kama Matinje na Izuga. Kwa mfano pale Izuga lile bomba limepita kabisa kwenye uwanja wa shule ya msingi Izuga.
Sasa katika mazingira haya ambapo jibu linasema vitaunganishwa kutegemea upatikanaji wa fedha. Hivi ni sawa katika mazingira hayo ambayo bomba limepita pale pale kijijini halafu wanaendelea kukaa bila kujua? Nilitaka kujua Mheshimiwa Waziri atuambie ni lini hasa vijiji hivi ambavyo bomba limepita pale pale kijijini kama Izuga na Matinje vitafanyiwa angalau mpango wa dharura wa kuunganishwa badala ya kusubiri mpango au lugha ya kwamba fedha zitakapopatikana? Nilitaka kujua lini katika hali ya dharura.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; katika maeneo haya ambapo bomba kuu la Ziwa Victoria kutoka Mwanza kwenda Kahama na Shinyanga limepita hapakuwepo utaratibu wa kutengeneza mabirika ya kunyweshea mifugo (water traps); na mwaka 2014 tulikubaliana kwamba uwepo mpango wa kutengeneza water traps kwa ajili ya mifugo. (Makofi)
Je, ni lini Serikali sasa itafanya mpango huo ili maeneo haya pia mifugo iweze kupata maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, amesema ndani ya kilometa 12 kuna baadhi ya vijiji ambavyo vimesahaulika. Nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hatutaacha kijiji hata kimoja, tunachotaka ni ushirikiano na Halmashauri husika kama kuna kijiji ambacho kimesahaulika basi tunaomba tupeane taarifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia umependa kujua ni mpango gani wa haraka, kwa mfano kama kijiji cha Mitinje, kijiji cha Izuga ambacho kina kilometa moja tu kutoka kwenye bomba. Tushirikiane Mheshimiwa Mbunge, Wizara ya Maji na Umwagiliaji kila mwaka inatenga fedha kwa kila Halmashauri. Basi ningeomba Halmashauri husika ijaribu kuangalia uwezekano wa kuunganisha kutokana na fedha tuliyotenga Wizara ya Maji na kama wanaona hawawezi basi wawasiliane na Wizara ili tufanye hiyo kazi haraka kuhakikisha kwamba wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuhusu mabirika. Mimi tu niseme Mheshimiwa Mbunge kwamba haya Mabirika tumepokea hii tutalifanyia kazi ili kuona ni namna gani tunaweza tukatumia maji haya ili kuweza pia kusaidia mifugo iliyo karibu na hilo bomba.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante sana kwa kuniona ili na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mahitaji ya Jimbo la Msalala yanafanana kabisa na mahitaji ya Jimbo la Ushetu, na kwa kuwa maji haya ya Ziwa Victoria yamefikishwa Kahama Mjini na hayajawafikia kabisa wananchi wa Jimbo la Ushetu, je, Serikali inawaambia nini wananchi hawa ambao wanayasubiria maji haya?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari tuna bomba, na juzi tumesaini mkataba tarehe 22 Aprili kwa ajili ya kufikisha maji Nzega, Igunga na Tabora. Kama bomba limeshapita karibu na eneo lako, tutaendelea, na kama topography inaruhusu tutaendelea kuweka fedha ili kuhakikisha kwamba na maeneo kama haya ya Ushetu na nikuhakikishie tu kwamba bado capacity ipo kubwa, yapo maji ya kutosha, tutaendelea kutenga fedha kuhakikisha kwamba na hili eneno la Ushetu tuhakikishe tunalipatia maji. Na nikuombe Mheshimiwa Mbunge kwamba naomba tuwasiliane ili tuweze kupanga tuone namna gani tunaweza tukahakikisha kwamba maji yanafika haraka Ushetu.
MHE. STEPHEN H. NGONYANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kazi nzuri anayofanya. Mimi nilikuwa nataka kujua ule Mradi wa Vuga - Mlembule - Mombo ambao yeye ameutembelea kwa muda mrefu sana na kuona matatizo yake na kuwaahidi wananchi wa Mombo kwamba ikifika mwezi wa sita watapata maji. Ni lini Mradi huu utakuwa umekamilika na wananchi wale wafurahie mradi ule mkubwa wa maji ambao unagharimu zaidi ya shilingi 900,000,000?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuhakikishie kwamba wananchi wa Mombo watapata maji. Nilifanya ziara nimeenda Vuga, nimeongea nao na tumekubaliana kwamba sasa tuongeze fedha pamoja na hiyo milioni mia tisa, tunaongeza fedha katika bajeti ya 2017/2018. Na tumeweka utaratibu, eneo lolote lenye chanzo tunapofanya mradi lazima tuhakikishe kwamba wananchi wanaozunguka hilo eneo wapate maji kabla ya kupeleka Kijiji cha mbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunatenga fedha itakayohakikisha kwamba wananchi wa Vuga wanapata maji, na bomba lingine linakuja moja kwa moja mpaka eneo la Mombo na maeneo mengine yatakayopitiwa na hilo bomba. Kwa hiyo nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunaendelea na juhudi kuhakikisha kwamba wananchi wa Mombo wanapata maji kutoka Vuga.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Naibu Waziri na Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri wanayofanya katika utendaji wao wa kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maswali yangu mawili ya nyongeza ni kama yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa Lwakajunju, imekuwa ni ahadi ya muda mrefu sana zaidi ya miaka 15. Kwa maana hiyo tumewaahidi sana akina mama wa Karagwe na wananchi kuwatua ndoo kichwani kwa muda mrefu sana. Kama unavyojua akina mama ule muda ambao wanautumia kwenda kuchota maji umbali mrefu ndio muda huo huo ungeutumia kufanya kazi za maendeleo. Sasa swali la kwanza, Mheshimiwa Naibu Waziri naomba unipe comfort, je,huu mradi wa Lwakajunju utatekelezwa lini? Ni lini wananchi wa Karagwe watapata hii huduma ya maji?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na changamoto za kibajeti za Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe, je, Wizara ipo tayari kushirikianan na Halmashauri kuhakikisha fedha ambapo tunahitaji kwa ajili ya kuchimba mabwawa katika Kata za Kanoni, Igulwa Ihanda, Chonyonyo na Nyakahanga zinapatikana ili wananchi wapate huduma ya maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kuhusiana na Mradi wa Lwakajunju, ameomba apate confort na wananchi wake pia. Comfort ya kwanza ni kwamba mradi huu umetengewa dola milioni 30 kutokana na mkopo wa India, ni mkopo wenye uhakika na sasa hivi tupo kwenye taratibu za kukamilisha usanifu ili tutangaze tender. Kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba mradi huu unatekelezwa kwasababu tayari una fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili linalohusiana na ushirikiano na Halmashauri, Mheshimiwa Mbunge nikuhakikishie kwamba tutaendelea kushiriakana na Halmashauri zote kuhakikisha kwamba miradi ya maji inatekelezwa, mabwawa, mserereko, visima na mingine ili kuhakikisha kwamba wananchi wanapata maji. Kuhusu suala la fedha upungufu wa fedha tutaenda nalo sabamba, lakini suala la msingi ni kuhakikishe kwamba wananchi wanapata maji.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Katavi kuna miradi ya umwagiliaji ambayo imeanzishwa na Serikali na imetumia fedha nyingi sana. Miradi hiyo ni mradi wa Karema, Kabage na Mwamkulu. Miradi hii ya Serikali imetolewa fedha nyingi, bahati mbaya sana Serikali inapoanzisha haiwezi kuikamilisha hiyo miradi. Nilikuwa nataka kujua ni lini Serikali itakamilisha hiyo miradi ya Karema, Kabage na Mwamkulu ili iweze kuwanufaisha wananchi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hiyo ilianza, ni kweli ilichelewa kukamilishwa lakini sasa hivi tumeandaa timu ambayo inakwenda kupitia ili kuainisha changamoto ambazo zimefanya isikalimike ili tuweze kutoa fedha tuhakikishe kwamba miradi hiyo yote mitatu Karema, Kabage na Mwamkulu inakamilika.
Kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba tayari, na mimi mwenyewe nimeshakwenda kutembelea Mradi mmojawapo pale na huo mradi sasa hivi tayari kazi inaendelea mkandarasi amerudi site ili kuhakikisha kwamba miradi yote hii inakamilika.
MHE. RHODA E. KUNCHELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nilitaka nimuulize Mheshimiwa Waziri. Imekuwa ni kero kubwa kwa wananchi wa Manispaa ya Mpanda kuendelea kusubiri miradi ambayo haitekelezeki, lakini pia ni wiki sasa maji hayatoki. Sasa ni nini tamko la Serikali ili kuhakikisha wananchi hao wanapata maji lakini pia wasiendelee kulipa bili ambazo hawapati maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, Mji wa Mpanda mahitaji ya maji ni lita 10,200,000 kwa siku. Hadi sasa kwa mradi uliopo unatoa maji lita 3,150,000 kwa siku. Sasa hivi kuna miradi miwili ambayo wakati wowote itasainiwa, miradi hiyo ikikamilika basi itaongeza kiwango cha maji hadi kufikia lita 6,000,000. Kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba utekelezaji unaendelea. Changamoto kama maji hayajapatikana, kwanza tufahamu kwamba maji yaliyopo yanatosheleza kwa asilimia 30 tu. Kwa hiyo, si suala kwamba maji hayapo, hapana, ni kidogo. Serikali inaendelea kujitahidi kuhakikisha kwamba yale mahitaji ya lita 10,200,000 yanafikiwa na tatizo la maji kutokupatikana halitakuwepo tena.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kilimo cha mabondeni ni kilimo ambacho ni cha asili na kimezoeleka na wananchi, hasa wa Mikoa ya Iringa, Njombe, Songea na kinajulikana kwa jina la ukulima wa vinyungu, sasa hivi kimezuiwa kutokana na kuzuia uharibifu wa vyanzo vya maji; na kwa kuwa, kilimo hicho ndiyo kimekuwa kikitumika kwa muda mrefu.
Je, Serikali ili kuwanufaisha wananchi wa vijiji vya Lukani, Kihesa Mgagao, Lulanzi, Idete, Kimala, Boma la Ng’ombe, wameweka mikakati gani mbadala kuhakikisha kwamba hawa wananchi wanaendelea kulima kilimo kisasa? Imejipangia mikakati gani? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa lazima tukubaliane kwamba ili tuwe na maji endelevu ya kuweza kuwatosheleza Watanzania ni lazima tutunze vyanzo vya maji. Katika utunzaji wa vyanzo vya maji, kuna watu ambao kwa miaka mingi kama anavyosema wamekuwa wanalima kilimo cha vinyungu; maana yake wanalima kwenye vyanzo vya maji. Sasa mikakati ya kuweza kuwatafutia shughuli mbadala ni lazima muwe shirikishi kati ya Halmashauri na Serikali. Haiwezi kuwa Serikali tu inawapelekea kwamba mtafanya hiki, kwa hiyo, ni lazima iwe shirikishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakwenda kukaa na Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo tuweze kuona shughuli nyingine ambayo wanaweza wakafanya nyingine tofauti na uharibifu wa vyanzo vya maji. Kulingana na sheria yetu, ndani ya mita 60 kutoka kwenye vyanzo vya maji, haturuhusiwi kufanya kazi yoyote, kufuga mifugo au kulima ili tuwe na maji na rasilimali ya kutosha kuwapelekea Watanzania.
MHE DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kukuniona. Licha ya Mkoa wa Morogoro kuwa na mito mingi na hatimaye kuweza kulisha Mikoa mingine kama Pwani, Dar es Salaam na Mkoa wa Tanga lakini Mkoa wa Morogoro hauna maji safi na salama. Sasa ni lini Serikali itahakikisha Manispaa ya Morogoro hususan katika Kata za Bingwa, Kiegea A na B, Mkundi, Kingolwira na Kihonda zinapata maji safi na salama?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza swali lake linazungumza kiujumla kwamba Mkoa mzima hauna maji salama hili si kweli, si kweli kabisa. Ni kweli kuna upngufu wa maji lakini huwezi kusema Mkoa mzima hauna maji salama, watu wangekuwa wameshakufa. Kwa hiyo, kazi ziko na kuna miradi inayoendelea na eneo analolizungumza pale Manispaa ya Morogoro tunao mradi mkubwa wa kupanua mradi ule ambao upo. Tutaongeza ukubwa wa lile bwawa la Mindu tutaongeza mtandao; hivi sasa kazi imeshaanza kwa awamu ya kwanza ya kupeleka hayo maeneo ambayo Mheshimiwa Mbunge anayasema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumepata fedha kutoka Benki ya Ufaransa ya kuweza kuweka miundombinu ya kutosha kabisa kuongeza upatikanaji wa maji, huu wa sasa mara mbili zaidi. Kwa hiyo, Serikali inatambua tatizo hilo na inalifanyia kazi. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge asiwe na shaka, Serikali ya Chama cha Mapinduzi inafanya kazi.
MHE. BALOZI ADADI M. RAJAB: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ili niulize swali moja la nyongeza. Matatizo ya maji salama na safi Muheza ni makubwa sana. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa juhudi ambazo wanafanya jinsi walivyoweza kubuni mradi wa kutoa maji Pongwe mpaka Muheza. Mradi huo upo karibu kuanza, nashukuru sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ni kwamba, ukombozi mkubwa ambao tunautegemea Wilayani Muheza ni maji yale yatakayotoka Zigi mpaka Mjini Muheza na vitongoji vyake. Sasa huu mradi upo kwenye mkopo wa Benki kutoka India wa dola milioni mia tano na ni mradi mmojawapo kati ya miradi 17 ambayo inategemewa kuanza. Sasa nataka kujua, kwa sababu wananchi wa Muheza wana shauku kubwa sana wa huu mradi. Huu mradi unaanza lini ili wananchi wa Muheza waweze kujua?Nakushukuru sana. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niwatoe wasiwasi Wananchi wa Muheza, ni kweli fedha imeshapatikana ya kuweza kujenga mradi mkubwa kutoka Mto Zigi kupeleka Mji wa Muheza. Taratibu ambazo tunazifanya sasa, kwanza tunakwenda kusaini mkataba wa financial agreements, wa fedha, tunasaini mkataba ule halafu tunaanza kufanya manunuzi ya kupata Mhandisi Mshauri atakayekwenda kufanya usanifu wa kina kwa ajili ya kuhakikisha kwamba maeneo yote ya Muheza pale yanapata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili tumepanga kulifanya katika mwaka wa fedha 2017/2018. Kwa hiyo, naomba niwahakikishie wananchi wa Muheza watakwenda kupata maji safi na salama.
MHE. SULEIMAN M. NCHAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, wabeja sana. Kwa niaba ya wananchi Shapu wa Jimbo la Kishapu, kwanza naomba nitoe shukrani za dhati kwa Wizara kwa kutekeleza mradi kabambe wa maji ya ziwa victori katika Jimbo la Kishapu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, naomba nije na scenario tofauti baada ya mradi huo kufika katika Mji Mdogo wa Muhunze, Mbunge wa Kishapu kushirikiana na viongozi wa Kishapu tumeshafanya mkakati kabambe wa kutafuta mkandarasi ambaye anaweza kutupatia fedha kwa vigezo vile ambavyo Serikali inaweza ikaridhia. Je, Mheshimiwa Waziri je, yuko tayari kukaa na uongozi wa Kishapu ukiongozwa na Mbunge wa Kishapu ili tumweleze kuwa tumeshapata fedha ambazo zinaweza zikayasambaza maji katika Jimbo lote la Kishapu katika vitongoji vyote vya Kishapu iwapo utaridhia tena kwa masharti yale ambayo Serikali inaya…(Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inakubaliana naye kama kuna mwekezaji ambaye anataka kuja kuwekeza katika sekta ya maji na iko ndani ya sera yetu ya maji, maji ni shirikishi ni Serikali pamoja na washirika wa maendeleo mbalimbali. Kwa hiyo, sisi tunamkaribisha yeye aje tuzungumze tuweze kuona namna gani tunaweza kwenda naye katika jambo hili.
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza sikubaliani na majibu ambayo yametolewa na Mheshimiwa Naibu Waziri, hayaridhishi kabisa. Ukiangalia kwa mtiririko ulioko kwenye majibu haya imesema wazi mwaka 2006/2007 walifanya upembuzi na kugundua kwamba shilingi bilioni kumi na tatu ilihitajika kwa ajili ya mradi huu lakini wakafanya upembuzi tena mwaka 2014/2015 ikaonekana shilingi bilioni 1.54 zilitakiwa kwa ajili ya ujenzi wa bwawa hili lakini bado wakafanya mwaka 2015/2016 wakatenga milioni 800.
Mheshimiwa Mwenyekiti, najenga hoja naomba utulie. (Kicheko) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]
Mheshimiwa Mwenyekiti, walitenga fedha hizi shilingi milioni 800 hazikutoka, halafu mwaka 2016/2017 hawakutenga fedha…
… 2017/2018 hawakutenga fedha, sasa ni kwa nini wanazungumza uongo? Kwa nini hawakutenga fedha katika miaka miwili hii ambayo imo mpaka bajeti ya safari hii wanazungumza…
Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna mtu ambaye amekamilika, ulimi inawezekana umeteleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Serikali haioni sasa kwamba kutokutekeleza mradi hii hawawatendei haki wananchi wa Wilaya ya Korogwe hususan Manga Mkocheni?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya shemeji yangu Mheshimiwa Mary Chatanda kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jibu langu la msingi nimeonyesha taratibu mbalimbali zilizofanywa na Serikali na kwamba utendaji lazima tufuate tathmini ya wataalam. Sisi kazi yetu ni kutunga sera na kupitisha bajeti, lakini utekelezaji unazingatia taarifa za wataalam.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jibu la msingi nimesema kwamba utafiti wa awali ulionesha kwamba bwawa lingejengwa kwa shilingi bilioni 13; lakini tathmini ya kimazingira ikaonyesha kwamba bwawa hilo lingejengwa lingezamisha baadhi ya maeneo na vijiji vya wananchi wa Manga, tusingeweza kufanya hivyo. Kwa hiyo, Tume ya Umwagiliaji kupitia Mkoa wa Kilimanjaro wakafanya tathmini nyingine upya ambayo kama ingetekelezwa basi hayo maeneo ambayo yangeathirika na bwawa yasingekuwemo, ndiyo maana bajeti sasa ikaja shilingi bilioni 1.5, hilo ndilo jibu la msingi. Lakini bado tumetenga shilingi milioni 800 mwaka uliofuata 2014/2015 lakini kwa bahati mbaya bajeti haikutoka ndio maana utekelezaji haukufanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba malengo yetu ni kuhakikisha tunajenga hili bwawa na ndio maana Serikali ya Chama cha Mapinduzi...
...imeunda Tume ya Umwagiliaji ambayo sasa kazi yake itakuwa ni kusimamia moja kwa moja suala la utekelezaji wa miradi ya umwagiliaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge usiwe na wasiwasi hakuna haja ya hasira kazi hii tutaifanya na wananchi wa Manga watapata huduma wanayoihitaji. (Makofi)
MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa tatizo la maji nchini ni kubwa na Tanzania ni moja ya nchi ambayo tuna sifa ya kuwa na Maziwa makubwa pamoja na mito mingi; yaani ni nchi ya Maziwa Makuu tofauti na zile nchi za kwenye jangwa kule kama Libya ambao wana maji zaidi ya asilimia 80. Sasa ni kwa nini Serikali isione aibu ya kushindwa kutatua hili tatizo kwa muda mrefu ilhali tuna maji mengi? Sasa hivi ukiangalia moja ya sifa ya nchi yetu ambayo tumekuwa tukijitamba na Serikali mmekuwa mkijisifu kwamba mmekuwa mkikusanya mapato mengi. Ni kwa nini sasa…
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imejitahidi, kila mwaka inatenga fedha na inazipeleka kwenye Halmashauri. Ni kazi ya Halmashauri kuhakikisha inatumia hiyo hela kuwapatia wananchi maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeandaa kitabu kinachoonesha bajeti iliyotengwa katika Halmashauri na kiasi cha fedha ambacho Halmashauri imetumia. Halmashauri nyingi zimeshindwa kutumia fedha zilizotengwa kwenye bajeti. Sasa lawama hii iende kwa nani wakati sisi wenyewe ni Madiwani kwenye hizo Halmashauri?
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba nchi yetu ina maji ya kutosha kilichobaki ni kuweka fedha na kusambaza na Serikali inaendelea kuweka fedha. Imeweka fedha mwaka uliopita na mwaka huu fedha tayari ipo kwa ajili ya Halmashauri kuhakikisha kwamba mnatumia zile fedha kuwapa wananchi maji na Wizara ya Maji na Umwagiliaji imeshatoa maelekezo ya jinsi ya kufanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niwaambie Waheshimiwa Wabunge Halmashauri yangu tayari imeshatengeneza mpango kazi leo tarehe 3 Julai, hebu jiulize wewe kwenye Halmashauri yako kwenye bajeti mpya je, mpango kazi umeshaanza kufanya? Ndugu zangu naomba sana bajeti ipo tusimamie Halmashauri waweze kutekeleza miradi ya maji hakuna haja ya kulaumiana.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Maji, hivi sasa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu katika majimbo yote mawili tulikuwa na mradi wa maji takribani zaidi ya miaka minne na hao wamekosesha Halmashauri zetu kupata mpya za miradi ya maji. Ni kwa nini sasa Serikali isitoe maelekezo ya Waraka kwa Halmashauri za Wilaya kwa jinsi ambavyo watajiondoa katika mikataba ya awali ili wananchi wetu waweze kupata huduma bora na kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Halmashauri yake naijua, tena mikataba hiyo imeingiwa wakati na yeye mwenyewe akiwa ni Mwenyekiti wa Halmashauri. Tumeanza kutoa fedha na tumetoa maelekezo kwamba kwanza tukamilishe ile miradi ya awali ambayo ilikuwepo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala la mikataba ni la Mkurugenzi mwenyewe aliyeingia mikataba, clauses za kuhudumia mikataba ziko ndani, termination ziko ndani namna gani ziko ndani, suala la mikataba haliwezi kujadiliwa Bungeni, ni la yeye mwenyewe Mkurugenzi ambaye aliingia mikataba hiyo; na condition ya mikataba ipo pale na taratibu zote zipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Mbunge amwambie Mkurugenzi wake aiangalie mikataba vizuri, madirisha ya jinsi ya kutoka yapo ili kuachana na huyo mkandarasi ambaye ameshindwa kazi ili kuweza kuingia na mkandarasi mwingine.
MHE. SAUMU H. SAKALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Pamoja na majibu haya ambayo amejibu Naibu Waziri tatizo la maji ambalo lipo Makambako ni sawa kabisa na tatizo la maji ambalo kwa sasa limejitokeza katika Jiji la Tanga na linaendelea kujitokeza ambapo licha tu ya maji kukatika mara kwa mara bila ratiba na bila taarifa lakini pia maji yale takribani mwezi mmoja sasa yamekuwa yakitoka machafu yenye tope.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo hili nilimfikishia Mheshimiwa Waziri wa Maji, nilimwandikia barua lakini pia nilikwenda kumwona mimi mwenyewe lakini bado linaendelea na majibu ya uhakika bado hatujapata. Maji yamekuwa yakiendelea kutoka machafu, yakiwa na tope na bado pia yanaendelea kukatika mara kwa mara. Serikali itoe tamko sasa ni lini watu wa Tanga watapata maji safi kama walivyozoea na maji ambayo hayakatikikatiki?Ahhsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Mbunge alikuja kwangu akilalamikia hali ya maji kuwa na tope katika Jiji la Tanga. Jiji la Tanga ni mojawapo la mamlaka katika nchi ambayo imekuwa siku zote inatoa maji safi na salama.
Mheshimiwa Naibu Spika, kilichojitokeza ni kwamba kumetokea hitilafu katika mtambo wa uchujaji maji na hii imetokana na uchafuzi mkubwa wa maji kule kwenye vyanzo kwa sababu wamevamia wachimbaji wa madini kwa hiyo maji yanakuja na tope na rangi. Kwa hiyo, imebidi sasa tutengeneze design nyingine ya kuchuja maji yale na tatizo lile tumeshalimaliza sasa hivi Tanga wanapata maji safi kama walivyokuwa wanapata zamani.
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii. Kama ilivyo kwa Bwawa la Makambako, Wizara ya Maji iliahidi Wilaya ya Hanang’ kuchimba Bwala la Gidahababieg kwa miaka saba. Naomba niulize ni lini bwawa hilo litachimbwa ili wale watu waliopata matatizo kwa miaka mingi waweze kupata maji?Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge ambaye pia ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji, Kilimo na Mifugo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli bwawa hili amekuwa analipigania kwa muda mrefu lakini katika bajeti ya mwaka huu tutaanza kwanza kufanya usanifu ili tuweze kujenga bwawa hilo. Baada ya kujua gharama ya ujenzi ni kiasi gani na michoro itakuwa namna gani, basi tutajenga bwawa hilo kwa mwaka huu wa fedha unaokuja 2017/2018.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri napenda kumuuliza swali moja la nyongeza.
Kwa upande wa Tanzania Bara maeneo yatakayohusika ameyataja, je, kwa upande wa Tanzania Zanzibar ni maeneo gani yatakayohusika na mradi huu?(Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa kama unavyofahamu fedha zile zimetolewa dola milioni 31 kwa ajili ya Zanzibar, lakini atakayeamua kwa upande wa Zanzibar fedha zile zinaenda kipande gani cha nchi ya Zanzibar ni Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Kwa hiyo, tumeshawasiliana nao wamesema wanafanya majadiliano na Serikali kwa ngazi za juu ili kuweza kuamua kwamba fedha hizi zitakwenda kuhudumia sehemu gani ya Zanzibara. (Makofi)
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nashukuru sana kwa kujali hilo.
Ningependa kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri wa maji kwamba kuna mradi ule mwingine wa Ziwa Victoria unaopita hadi maeneo ya Kolandoto kwenda Wilaya ya Kishapu. Nilishawahi kuuliza siku za nyuma kwamba kuna vijiji vya Mwamashindike, Mwabalatulu, Mwakidiga, Lalago hadi Budekwa viko karibu na eneo la Kishapu. Je nini kauli ya Serikali kwa maeneo hayo kupata maji kutoka ule mradi wa Kolandoto kuja maeneo hayo? Ahsante sana.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri aliyoyatoa. Katika utekelezaji wa mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria kupeleka Kishapu tulichokifanya ni kwamba maeneo yote ambayo lile bomba limepita tumetoa matoleo ya kupeleka kwenye vile vijiji ambavyo vipo ndani ya kilometa 12 kila upande. Sasa tumetoa maelekezo kwa Wakurugenzi, kwamba sasa wanapopanga mipango yao ya kupeleka maji kwenye vijiji vyao pale ndipo patakapokuwa chanzo cha kuchukulia maji. Kwa hiyo, mipango ya halmashauri na vipaumbele vyao tumeshawazogezea sasa kwenye lile bomba kubwa. Lakini pia tutaweza kuendelea na bajeti ya Serikali maeneo yale mengine kulingana na bajeti ambayo mmeipitisha hivi karibuni. Tukipata fedha hizo basi tutaendelea nasi kusaidiana na Halmashauri kupeleka maji maeneo mengi jinsi itakavyokuwa inawezekana.
MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, nina maswali mawili madogo ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, la kwanza, maji yanapokuwa ni adha kubwa waathirika wakubwa kwa kiwango kikubwa wanakuwa ni wanawake. Katika Wilaya hii mpya ya Songwe iliyoko Mkwajuni ni kilometa kumi tu kutoka katika Ziwa Rukwa, sasa nataka kujua, nini mpango wa Serikali katika kuvuta maji kutoka Ziwa Rukwa ambalo Mheshimiwa Mulugo amekuwa akililia kwa muda mrefu? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, Wilaya hii mpya ya Songwe, matatizo yake yanafanana sana na Wilaya ya Chunya ambayo ilikuwa ni Wilaya moja katika Mkoa wa Songwe. Katika Wilaya hii ya Chunya kuna Kata za Makongolosi, Matundasi na Bwawani hazina maji kwa muda mrefu sana. Nini mkakati wa Serikali katika hilo? Nashukuru.(Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze kwa swali zuri ambalo ameliuliza kwa niaba ya Mulugo. Kuhusu kwamba Mkwajuni iko kilometa kumi kutoka Ziwa Rukwa na angependelea kwamba maji yale yangepelekwa kwenye Mji wa Mkwajuni, jibu ni kwamba, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi kwamba tumetenga milioni 100 kwa ajili ya kufanya usanifu. Sasa usanifu ndiyo utaelekeza ni wapi tuchukue maji. Kama tutaona maji ya Ziwa Rukwa yanafaa basi tutachukua hapo na kuweza kupeleka maji katika Mji wa Mkwajuni. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu mkakati wa hizo
Kata za Makongolosi na zingine katika Halmashauri ya Wilaya ya Chunya, mkakati wa Serikali ni kwamba katika bajeti kila Halmashauri tumeitengea fedha na tumetoa mwongozo kwamba wao watoe vipaumbele kulingana na zile bajeti. Inasikitisha kwamba unaweza kufika mahali kwenye Halmashauri ikiwepo hata hii ya Songwe, katika bajeti ya mwaka uliotangulia walitengewa milioni 752, lakini mpaka leo tunamaliza mwaka fedha zipo lakini hakuna kazi iliyofanyika.
Mheshimiwa Spika, nitakwenda kule kuangalia matatizo yao ni yapi ili tuweze kuwasaidia tuweze kutatua matatizo ya wananchi. (Makofi)
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Mji wa Mkwajuni hauna tofauti na Mji wa Kasulu. Mji wa Kasulu sisi tuna maji mengi tu, tatizo letu ni maji machafu yanayotoka kwenye bomba. Sasa Mheshimiwa Waziri, ni lini atatujengea treatment plant ili tupate maji masafi kama sera za nchi yetu na Sera za CCM zinavyoagiza?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kama anavyosema kwamba Mji wa Kasulu unapata maji ambayo ni machafu, lakini mkakati wa Serikali tumeshatoa maelekezo kwamba kuanzia sasa hatutatoa maji ambayo si salama kwa wananchi. Kwa hiyo, kitu cha kwanza tutaanza na mitambo midogo ya kuweka dawa, lakini jinsi hali ya uchumi inavyoboreka, tutapeleka mitambo ya kuweza kusafisha maji kubadilisha rangi kuwa rangi ya tope yawe maji meupe. Kwa hiyo, huu ndio mkakati wa Serikali katika kuhakikisha wananchi wetu wanapata maji safi na salama na ni meupe, mazuri.
MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, nafahamu kwamba lengo la Serikali ya CCM ni kuwapatia Wananchi wengi maji safi na salama kwa gharama nafuu na ndiyo maana kuna miradi ya vijiji vingi nchi nzima kila Halmashauri ya kupeleka maji kwa wananchi na miradi hii inagharimu takribani kila mradi shilingi milioni 700 au 800. Mradi huu ninaoulizia swali, ulikuwa unahudumia vijiji sita; vijiji hivyo ni Maruku, Butairuka, Bwizanduru, Bulinda, Butayaibega na Buguruka. Mradi huu kama ungekarabatiwa haraka ungegharimu kama shilingi milioni 500 au 400 kwahiyo ni gharama nafuu na maji yangepatikana kwenye vijiji vyote hivi pamoja na Chuo cha Kilimo cha Maruku, shule kadhaa zipo pale za sekondari na za msingi. Sasa Serikali haioni kama ni busara mradi huu ukarabatiwe haraka wananchi wapate maji safi na salama?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza ni kweli kwamba kuna umuhimu wa huo mradi kukarabatiwa ili uweze kutoa maji kwa namna jinsi ulivyokuwa umepangwa na kwenye jibu la msingi nimeeleza kwamba nia hiyo ipo na tayari Serikali imetenga fedha shilingi bilioni katika kuetekeleza miradi ya Halmshauri ya Bukoba lakini vipaumbele ni mradi upi wanaanza nao, wanaamua kule kule kwenye Halmshauri na kwa kuwa Waheshimiwa Wabunge ni sehemu ya Baraza la Madiwani katika kuweka vipaumbele na kwa sababu mradi huu tayari umeshakubaliwa na Serikali, kwa hiyo mimi ningeshauri kwamba uupe kipaumbele ili tukarabati na hivyo vijiji anavyosema viweze kupata maji.
MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, nikushukuru na mimi kupata nafasi ya kuuliza swali la nyongeza kuwa matatizo waliyonayo wananchi wa Bukoba Vijijini yanafanana moja kwa moja na matatizo waliyonayo Wananchi wa Chalinze na kwa kipindi kirefu sana wamesubiri maji na sasa hivi hawaoni kinachoendelea. Sasa swali langu, Mheshimiwa Waziri ni lini mkandarasi yule utamfukuza ili wananchi wa Chalinze wajue wanaanza upya? Swali langu la kwanza na swali la pili, nini mpango mkakati sasa wa kuwakwamua wananchi wa Chalinze? Ahsante sana.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, ni kweli pale Chalinze kuna mradi Awamu ya Tatu ambao unatekelezwa na Kampuni moja kutoka India (OIA) na utendaji wake wa kazi hauridhishi na tulikuwa tumetoa muda kwamba mpaka mwezi wa kumi awe amefikisha mahali ambapo Serikali inaweza kumruhusu au kufuta mkandarasi yule. Tunafuatilia kazi hiyo kwa karibu sana, naomba nikuhakikishie Bunge hili kwamba ikifikia mwezi wa kumi na hakuna kazi ya maana inayoendelea pale, tutachukua hatua zaidi za kimkataba.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Katika jibu lake la msingi amekiri kwamba kuna miradi 114 ambayo imekuwa haiendelei au imeharibika kabisa na katika miradi hiyo 114 mmojawapo ninaoufahamu mimi ni ule wa Kili Water kule Mkoani Kilimanjaro.
Mheshimiwa Spika, ni lini sasa Serikali itahakikisha imeukarabati mradi huo ili kuondoa adha ya Wanawake wa Tambarare ya Rombo kubeba ndoo za maji Alfajiri na mapema walio katika Kata ya kule Ngoyoni, Mamsera chini pamoja na wale ambao wako kule pembeni ya Ziwa Chala?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, tambarare yote ya Mkoa wa Kilimanjaro imekumbwa na adha hii ikiweko Wilaya ya Mwanga, Same Mjini mpaka kule Hedaru. Ni lini sasa Serikali itakamilisha ule mradi wa maji wa Ziwa la Nyumba ya Mungu ambao utapeleka maji kupitia Mwanga, Same, Hedaru mpaka Mombo?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nichukue fursa hii kwa niaba ya Serikali kumpongeza sana Mbunge kwa maana kwamba anafuatilia kuona namna gani miradi hii inawea kuathiri matumizi ya wananchi kwa maana kwamba maji yamekuwa yanapungua kwa namna hali ya hewa inavyobadilika. Kwa hiyo ni jambo ambalo ni la msingi lakini pia ni lazima tuchukue hatua. Hatua mojawapo ni lazima sisi sote tuhakikishe kwamba tunalinda vyanzo vya maji lakini pia tupande miti ambayo ni rafiki lakini pia tuvune maji ya mvua kwasababu rasilimali za maji zinapungua mwaka hadi mwaka kama hatuchukui hatua yoyote ya kukabiliana na tatizo hilo. (Makofi)
Sasa kuhusu mradi ambao unasema ni lini utakarabatiwa, Mkoa wa Kilimanjaro Serikali kwa mwaka huu wa 2017/2018 tumetengea shilingi bilioni 8.95 kwa ajili ya kumaliza miradi inayoendelea lakini pia kukarabati miradi ambayo ipo haifanyi kazi katika kiwango kwahiyo watumie fddha zile katika kuangalia vipaumbele na kuona kama wanaweza kukarabati kwa mwaka huu wa fedha vinginevyo wapange katika mwaka wa fedha unaofuata.
Kuhusu swali lake la pili, mradi wa Nyumba ya Mungu kupeleka maji Mwanga mpaka Same, sasa hivi mkandari huko mwanzo alikuwa anusua sua lakini sasa hivi anakwenda kwa kasi na nina uhakika kwamba mradi ule utakuja kukamilika lakini pia tumeanza na awamu nyingine ya kupeleka maji kule Same nayo Mkandarasi yupo site na kazi inakwenda vizuri. Serikali inafuatilia kwa nguvu zote ili miradi hii iweze kukamilika.
MHE. LEONIDAS T. GAMA: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii kwa niaba ya wananchi wa Songea Mjini katika maeneo hayo niliyoyataja niishukuru sana Serikali kwa kutupa matumaini kwamba fidia hiyo italipwa kipindi cha bajeti ya fedha mwaka 2018/2019. Sasa naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, la kwanza, katika eneo hilo wapo wananchi 157 ambao wanadai kwa namna moja ama nyingine majina yao yaliondolea kwenye eno la fidia. Sasa naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, je, Serikali iko tayari kufuatilia ukweli juu ya wananchi hawa 157 ili ukweli ukijulikana walipwe fidia zao?
Mheshimiwa Spika, la pili, naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, kwa sababu wananchi wa aneo hilo pamoja na kupata maji kutoka hilo bwawa lililotengenezwa lakini bado kuna migogoro mingi kati yao na SOUWASA. Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kwenda Songea ili kukutana na wananchi wa eneo hilo ili kuwasikiliza matatizo yao na kutatua? Naomba kuwasilisha.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza Serikali inaipokea hiyo shukurani aliyoitoa, lakini kuhusu wananchi 157 ambao inaonekana wako nje ya wale 872 tutakwenda kufuatilia na ninamuomba nimuahidi Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge hili nitakwenda Songea, nitakwenda kuona hali halisi na tuweze kuchukua hatua kwa Wananchi wale ambao bado wanadai hiyo fidia.
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize maswali madogo mawili ya nyongeza. Kwa kuwa, visima vilivyopo Kibiti vinazalisha maji kidogo tu, lita 4,000; na kwa kuwa, mahitaji ya maji kwa sasa kwa wananchi wa Kibiti ni zaidi ya lita 8,000 hivi ni kwa nini Serikali isianzishe mradi mkubwa wa maji kutoka Mto Rufiji ili uwafae wananchi wa Rufiji, Kibiti, Kisarawe, Mkuranga na Dar-es-Salaam?
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia, kuungua-ungua kwa mota mara kwa mara husababishwa na kukatika kwa umeme mara kwa mara. Nini sasa mpango wa Serikali katika kumaliza kadhia hiyo ili wananchi wa Kibiti waweze kunufaika na mradi huo wa Kibiti? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kweli anavyosema kwamba uzalishaji ni mdogo kuliko mahitaji na hili ni jambo ambalo liko maeneo mengi; lakini tunayashughulikia yote haya kwa awamu kulingana na bajeti inayotengwa na Serikali. Kwa hiyo, Serikali itaendelea kuangalia namna ya kuongeza uwezo wa uzalishaji wa maji, ili kukidhi mahitaji yaliyopo. Hata hivyo, tumeipangia kwamba, kwa sasa hivi uzalishaji wa pale unakidhi asilimia 70 ya wananchi wa Kibiti.
Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la Serikali tunataka ikifika mwaka 2020 tufikishe asilimia 85 kwa hiyo, tutaongeza vyanzo vingine ili kusudi tuweze kufikisha lengo ambalo tumelipanga.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili la kuungua-ungua kwa mota. Hili ni tatizo la mahitaji na uendeshaji ni lazima vitu kama hivyo vinaweza vikatokea. Kuungua kwa mota inawezekana pengine ni matatizo ya umeme unapo-flactuate kuwa mkubwa sana kuliko capacity ya zile mota, zitaungua. Kwa hiyo, tutaendelea kushirikiana na Wizara ya Nishati kurekebisha ule umeme unaopatikana pale uwe angalau hauleti madhara ya kuunguaungua kwa mota ambazo zimewekwa.
MHE. IGNAS A. MALOCHA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Serikali imejenga mradi wa maji katika Mji Mdogo wa Laela ulioanza mwaka 2014 na umetumia takribani shilingi bilioni moja na milioni mia nne; na mradi huu unaonekana umekwisha, lakini cha ajabu hautoi maji, jambo ambalo limeleta taharuki kubwa sana kwa wananchi wa Mji Mdogo wa Laela. Je, ni lini Serikali itahakikisha maji yanatoka katika mradi huo?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, huu Mradi wa Mji wa Laela ambao Mheshimiwa anauzungumzia nimeutembelea na nimeona umefikia hatua za mwisho, walikuwa katika ufungaji wa zile solar panels. Sasa katika ufungaji wa solar panels kukatokea kwamba ile mota ambayo iliwekwa haiendani na ukubwa wa zile panels. Kwa hiyo nimetuma wataalam waende kule wakaangalie namna ya kutatua tatizo hilo. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tutahakikisha mradi ule ambao umetumia fedha nyingi za Serikali unafanya kazi kwa manufaa ya wananchi.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize swali la nyongeza. Kunakuwa na matatizo mengi ya miradi mingi ya maji nchini ambayo haikamiliki kutokana na matatizo ya fedha, lakini mara nyingi tukiuliza hapa, nakumbuka Bunge lililopita, Mheshimiwa Naibu Waziri wa Wizara hii alikuwa anasema kwamba Wakurugenzi wetu wakamilishe taratibu za manunuzi, pesa zipo kwenye Wizara.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilipokwenda kwenye halmashauri yangu kwa mfano, nilienda kuulizia suala hili wakasema wameshaandika maandiko mengi kupeleka Wizarani, lakini mpaka leo hawajaletewa hizo pesa na miradi mingi imekwama . Sasa naomba kupata Kauli ya Serikali; ni nini Kauli ya Serikali kwa miradi ile ya maji iliyokwama kwenye halmashauri zetu mbalimbali hapa nchini?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza; kulingana na fedha za utekelezaji wa miradi zinazopelekwa kwenye halmashauri; tumetoa mwongozo kwamba katika bajeti ambayo kila halmashauri imetengewa wanaweka vipaumbele, wakishaleta andiko Wizarani sisi tunaidhinisha wafanye manunuzi. Wakishafanya manunuzi wakaajiri mkandarasi au mhandisi mshauri tunapeleka fedha kulingana na certificate. Maeneo mengi, halmashauri nyingi zimefuata mwongozo huu na miradi inbaendelea kutekelezwa. Sasa namwomba Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge hili tukutane tuweze kuona, labda kuna tatizo mahususi katika halmashauri ya wilaya yake.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali moja la nyongeza. Kwa kuwa, nilishamwomba Mheshimiwa Waziri kwamba, wataalam wa utafiti wa visima vya maji, visima ambavyo vitatoa maji baridi wafike na kufanya utafiti wa visima hivyo. Kwa sasa wananchi wa Mji wa Mpwapwa wanatumia maji ya chumvi. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri kuhusu ombi langu hilo la kutafiti visima vingine vya maji baridi, ni lini atalitekeleza?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli, ameomba kupata watafiti wa kuweza kugundua maji yaliyoko chini ya ardhi kama yana chumvi au hayana chumvi. Utaalam wa namna hiyo, kwanza haupo. Ni kwamba, lazima kwanza tuchimbe, tuyapate yale maji tukayapime ndipo tutajua yana chumvi na chumvi kiasi gani na kama inahimilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sisi tutakachofanya ni kwamba, tunakwenda kufanya tu tafiti kuona kwamba maji yapo mahali fulani, yatachimbwa halafu tutayapima na kuweza kuona. Kwa hiyo, wataalam hawa tutawapeleka kama anavyoomba, lakini kwa maana ya kujua maji yaliyopo pale, ni lazima kwanza tuyachimbe ndiyo tuweze kujua kama yana chumvi au hayana chumvi.
MHE. PHILLIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nami ningependa kumuuliza Mheshimiwa Waziri swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kila siku nimekuwa nikilalamika hapa kwamba Wilaya ya Songwe, Mkoa mpya wa Songwe na hasa Jimbo langu lina Vijiji sita tu vyenye kutoa maji, vijiji vingine vyote 28 hakuna maji. Je, ni lini yeye mwenyewe kama Waziri anakuja Songwe mimi na yeye tutembee siku nzima nimwoneshe sehemu ambazo wananchi wa Songwe wanalalamika maji, hususan ni maeneo ya Mbangala, Mbotoe na Mkajuni. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini nitatembelea Wilaya ya Songwe, nimepanga kuanzia Jumatatu kufanya ziara katika Mikoa ya Ruvuma na Songwe. Kwa hiyo, nitakwenda Songwe kwenda kuangalia malalamiko ya Mheshimiwa Mbunge na tuweze kuona namna ya kusaidiana. (Makofi)
MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Scheme ya Umwagiliaji ambayo ipo Kijiji cha Mbala Wilaya ya Mbozi, imetengenezwa tangu mwaka 1971 na miundombinu ya scheme hii imeharibika sana na hadi sasa haifanyi kazi. Naomba nijue Mheshimiwa Waziri atakapokuja Songwe yupo tayari kuongozana na mimi kuelekea kwenye scheme hiyo ya umwagiliaji na baada ya hapo sasa Serikali iweze kutengeneza miundombinu miundombinu ya scheme umwagiliaji ili wananchi hao waweze kunufaika na scheme hiyo? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba zipo scheme nyingi ambazo hazifanyi kazi, lakini tumesema mara nyingi kwenye Bunge hili kwamba tumeshatuma watu wanafanya mapitio ya scheme zote ili kuweza kuainisha mahitaji yake. Kwa hiyo, kwenda tu bila kuwa na jibu haisaidii, kwa sababu ameshasema kwamba haifanyi kazi. Kwa hiyo, tunaleta watu wataalam ili waainishe ni vitu gani vinatakiwa vifanyike kwa ajili ya kufanya ile scheme ifanye kazi. Kwa hiyo, naomba tusubiri ripoti ile itakavyoandikwa halafu tutaona hatua za kuchukua. (Makofi)
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa, utaratibu wa kuanzisha miradi ya scheme ya umwagiliaji na kutoimaliza sasa unaonekana kama ni utaratibu wa kawaida, ukiacha kwamba uzalishaji hautafanyika lakini pana pesa ile ambayo ndiyo imeanzisha hiyo miradi, hiyo pesa itapotea. Mfano mzuri ni miradi ya umwagiliaji katika Jimbo la Mtama, katika Vijiji vya Utimbe, Kiwalala na Mbalala ambayo imeanzishwa karibu miaka mitano mpaka saba iliyopita, imeishia katikati na haijamalizwa. Je, ni lini sasa Serikali itatenga fedha kuimalizia miradi hii ili tufaidike na miradi hii? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli ipo miradi mingi ambayo ilikuwa imeanzishwa na haikukamilika. Huko nyuma miradi hii katika Program ya Maendeleo katika Sekta ya Kilimo, sehemu kubwa ya miradi ile ilikuwa inaendelezwa na wafadhili kwa fedha za nje. Sasa tumeona kwamba ni lazima sisi kama Serikali tuwekeze fedha za ndani na kusimamia ili miradi iweze kukamilika na ndio maana tumeunda Tume ya Umwagiliaji ili iweze kusimamia miradi ya umwagiliaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuunda Tume hii, mwaka huu tumeamua kwanza kuipitia miradi yote na kuainisha mahitaji yake. Kwa hiyo, Serikali itatenga fedha kulingana na yale mahitaji yatakayokuwa yameainishwa ili miradi hii ambayo tumeipanga iweze kutekelezwa.
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri. Sambamba na hilo naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Ngara.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwepo na miradi ya vijiji kumi ambayo imechukua muda mrefu bila kukamilika. Kwa mfano, mradi wa Kijiji cha Mbuba, Munjegwe, Kanazi, Kabarenzi na Mkibogoye, je, ni lini miradi hii itakamilika?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, nichukue nafasi hii kwanza kumpongeza Mheshimiwa Waziri, kwamba tumepata shilingi milioni 24 kwa ajili ya pampu ya K9, lakini kwa namna ya kipekee nampongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tarehe 20 alipokuwa Ngara alitupatia shilingi milioni 13 kwa ajili ya kununua pampu ya maji ili kuboresha huduma ya maji katika Mji wa Ngara. Imeshafungwa na maboresho yamefanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na ahadi yake ni pamoja na kuanzisha mradi ambao unaweza ukawa suluhisho kwa Vijiji vyote vya Wilaya ya Ngara na Wilaya ya jirani kwa kutumia mradi wa vyanzo vya maji, Mto Kagera, Mto Luvubu na Mlima Shunga na akaahidi kwamba ataagiza Waziri na watendaji kufika kwa ajili ya kuangalia namna ya kufanya usanifu wa mradi huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, je, Waziri na timu yake ya wataalam yupo tayari baada ya Bunge hili kuambatana nami kwenda Ngara ili kuona uwezekano wa kusanifu mradi huu ambao utakuwa ni suluhisho kwa vijiji vyote vya Wilaya ya Ngara na Wilaya jirani? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa
Naibu Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia huduma ya maji katika Wilaya yake ya Ngara na hasa Mji wa Ngara ambapo Mheshimiwa Rais alipatembelea na akaweza kutoa fedha za kutengneza pampu ili wananchi wa pale waweze kupata maji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika maswali yake ya nyongeza, Mheshimiwa Mbunge ameulizia baadhi ya Vijiji ambavyo anasema havijakamilika. Nitoe tu taarifa kwamba Serikali imetenga shilingi 1,500,000,000 katika bajeti yake ya mwaka 2017/2018 kwa maana ya kuendelea kukamilisha miradi hiyo inayoendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili kama nipo tayari kwenda naye Ngara, mimi nipo tayari na nimepanga baada ya Bunge hili nitakwenda Ngara kuangalia huduma ya maji katika Mkoa mzima wa Kagera. (Makofi)
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Natambua kwamba tatizo la uhaba wa maji linawakumba sana wanawake wote Tanzania. Nilikuwa naomba Mheshimiwa atusaidie hasa kwenye Mkoa wetu wa Singida, hakuna mradi wowote mkubwa wa maji ambao umeanzishwa kwa ajili ya kuokoa tatizo la maji katika Mkoa wa Singida.
Je, ni lini sasa Serikali itaenda kuwakomboa wanawake wa Mkoa wa Singida kwa tatizo la maji? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli watu wanaopata adha kubwa katika suala la maji hasa vijijini ni akina mama na Serikali inatambua jambo hilo na ndiyo maana katika mwaka huu wa fedha 2017/2018 tumetenga shilingi bilioni 237. Hizi zinakwenda kwenye Halmashauri zote katika kutekeleza miradi ambayo iko vijijini na hususan miradi hiyo ikikamilika itakuwa imeondoa hii adha ya akina mama wanaopata shida ya maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali kama tuna mpango wa kupeleka mradi mkubwa, katika bajeti ambayo imetengwa hiyo ya shilingi bilioni 237, kwanza tunataka tukamilishe miradi ambayo tayari Serikali ilishawekeza. Kwa hiyo, ikishakamilika miradi hii tutaangalia mahitaji sasa ya ziada na tutaona namna gani tuweze kutafuta mradi mkubwa wa kuweza kuwafikishia wananchi wa Mkoa wa Singida. (Makofi)
MHE. LUCIA M. MLOWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Mheshimiwa Waziri amekuwa akiahidi kila siku juu ya bili kupanda kwa wananchi wetu. Hapa ninavyoongea nina bili ya maji ya shilingi 700,000 ambapo maji hayatoki lakini unaletewa bili.
Sasa naomba kujua, je, ni lini, tunaomba ututajie kabisa Mheshimiwa Waziri utatekeleza ahadi hii kwa wananchi wetu kwa sababu wanaumia sana? Ahsante sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Bili hii ni ya miezi mitatu, lakini maji hayatoki kabisa. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimeshatoa maelekezo kwenye mamlaka zote kwamba haiwezekani mtu akalipa bili ya maji ambayo hajatumia. Kwenye mamlaka zote tumeweka bodi za kusimamia uendeshaji wa mamlaka zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba sana ndugu zangu, kama kuna mtu ambaye kapelekewa bili ambapo hakupata maji, basi mahali pa kupeleka ni pale kwenye bodi, maana hili ni suala mahususi ili liweze kushughulikiwa. Hatuwezi kuwa na jibu la moja kwa moja kwa sababu siyo wote wanaopata bili ya maji ambayo hawajatumia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama kuna special case, naomba uniletee. Pia Mheshimiwa Mbunge akiwa kwenye Jimbo lake apeleke kwenye mamlaka ile, hasa kwenye Bodi ya Wakurugenzi inayosimamia uendeshaji wa mamlaka hizi ili mtu alipie maji aliyotumia tu, kulingana na Sera yetu ya Maji ya mwaka 2002 na Sheria Namba 12 ya mwaka 2009, kwamba ni lazima wananchi tutachangia huduma ya maji. Sasa katika kuchangia ni pamoja na kulipa bili, lakini kama bili ina mzozo, basi tutalishughulikia jambo hili na kuweza kulimaliza.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mradi wa Maji wa Haydom unafanana kabisa na jinsi ambavyo matatizo ya Ngara yalivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi huu wa Haydom umekaa miaka saba, mkandarasi amechukua pesa na muda wa kukabidhi mradi umeshafika. Mkurugenzi kafanya jitihada mpaka leo mradi haujaisha.
Je, Mheshimiwa Waziri atanisaidiaje sasa kuisaidia Halmashauri yangu ule mradi wa Haydom ukaisha na wananchi wakapata maji?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa
Naibu Spika, ni kweli, ipo miradi mingi ambayo ukamilishaji wake umechukua muda mrefu na sababu mojawapo ni ama kulikuwa na matatizo ya mkandarasi au kulikuwa na matatizo ya vyanzo au kulikuwa na matatizo ya kutokulipwa. Sasa tulipoingia awamu hii, maana hii ni miaka saba, sisi tuna miaka miwili, tumeanza kwanza kufuatilia miradi mmoja baada ya mwingine na kuhakikisha kwanza Wakandarasi wanarudi. Miradi mingi wakandarasi walikuwa wameondoka kwenye utekelezaji ikiwa ni pamoja na huo mradi wake ambao umechukua miaka saba.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Mkandarasi amerudi na sasa hivi tunawapa fedha kwa kazi ambazo wamefanya. Kwa hiyo, nitafuatilia huu mradi anaousema ili niweze kuona nini kinachoendelea na tuweze kumwambia Mheshimiwa Mbunge ni lini kazi ile ingeweza kukamilika? (Makofi)
MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii. Nina maswali mawili ya ngongeza. Hali ya upatikanaji wa maji hasa katika eneo la Bonde la Ufa katika Jimbo la Manyoni Mashariki ni ngumu sana, hivi ninavyozungumza mifugo inahangaika, watu wanahangaika, akinamama wanalala kwenye visima ambavyo havina uhakika wa kupatikana kwa maji, hali ni ngumu sana kwa kweli. Mheshimiwa Waziri amejibu kwamba litawekwa katika kipaumbele cha bajeti inayokuja, ninaomba tu ni ombi, kwa emergency, kwa hali ambayo nimeielezea hii, hali ni ngumu, naomba liingizwe kwenye bajeti ya mwaka unaofuata.
Mheshimiwa Spika, swali la pili, katika Kata ya Sorya Wilayani Manyoni, kwenye Jimbo langu katika harakati za kuhangaika kuwatafutia ajira vijana na akina mama tumetenga eneo, zaidi ya eka 400 kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji na tumechimba visima vitatu kwa fedha yetu wenyewe. Tuna shida ya umeme kwa ajili ya kufunga pampu za kutoa maji ili tuweze kumwagilia.
Je, Serikali inaweza kutusaidia sasa kupeleka umeme kwenye visima vile ili kunusuru wananchi hawa wanaohangaika, hasa vijana, tuweze kumwagilia maeneo haya na tuweze kujinusuru kwa suala la njaa? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimhakikishie kama tulivyoji-commit kwenye jibu la msingi, kwamba tutaweka kwenye bajeti ya mwaka 2018/2019 kwa hiyo naomba nimhakikishie kwamba tutafanya hivyo kwa sababu tumeshatoa jibu la namna hiyo.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusu ekari 400 ambazo mmepanga kuendeleza kilimo cha umwagiliaji; nilipokee ombi lake lakini tutaangalia uwezo wa bajeti iliyotengwa kwa mwaka huu wa fedha, kama itawezekana tutasaidia, lakini vinginevyo tutaangalia katika bajeti ya mwaka utakaofuata.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali ilitenga shilingi bilioni moja kwa ajili ya Mradi wa Maji Sumve, Madya na Malampaka, mwaka 2017/2018 ilitenga shilingi bilioni mbili kwa ajili ya mradi huo. Sasa Mheshimiwa Waziri katika majibu yake, kwa sababu ili maji yafike Mji wa Malampaka ni lazima yafike Sumve na Malya. Sasa nataka kujua, tulitegemea kwamba ungetaja, angalau kwamba Serikali imetenga shilingi bilioni mbili kwa ajili ya mradi huo, lakini hukutaja hata kidogo. Sasa swali Mheshimiwa Waziri, pesa zilizotengwa sasa hivi hazipo tena au mradi huo umeshakufa?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, majibu niliyoyatoa haya yanalingana na swali lilivyoulizwa na Mheshimiwa Mashimba. Lakini kwa maana ya kutaka afahamu mradi wa kupeleka maji Sumve mpaka Malampaka, tumetenga fedha hizo, mwaka huu, shilingi bilioni mbili, kwanza kwa ajili ya kukamilisha usanifu na makabrasha ya zabuni ili kusudi tuweze kutangaza tender ya kupeleka maji Sumve mpaka Malampaka. Nia ya Serikali ipo palepale, hakuna mabadiliko, hata kama tungesema tu hapa bila utekelezaji ingekuwa haitusaidii, lakini nia ya Serikali ipo na lazima tupeleke maji Sumve, Malya na Malampaka.
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Ninapenda kujua kwamba Maswa tumekuwa na tatizo kubwa sana la maji, kwa kweli hali ni mbaya na inahitajika hali ya dharura kutatua tatizo la maji katika Mji wa Maswa na maeneo yake. Sasa ninaomba Mheshimiwa Waziri atusaidie, anatuhakikishia vipi kwamba kuna njia mbadala ya kupata maji katika Mji wa Maswa kwa sababu bwawa tunalolitumia limekauka kabisa? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza, nikiri, ni kweli bwawa ambalo Mji wa Maswa ulikuwa unategemea limekauka, na hii inatokana na matumizi yasiyokuwa endelevu ya wafugaji ambao walikuwa wanafuga jirani na lile bwawa kuweza kuzalisha matope na hivyo kufanya lile bwawa kujaa matope na maji kukauka. Kwa hiyo, Serikali tumetenga bilioni 1.1 katika Halmashauri ya Maswa, sasa katika fedha zile wanaweza wakatumia sehemu ya fedha hiyo katika kutafuta mpango wa dharura ili kuhakikisha kwamba wananchi wa pale wanapata maji.
Mheshimiwa Spika, lakini kwa ujumla, Mkoa wa Simiyu, tunao mpango mkubwa wa kupeleka maji kutoka Ziwa Victoria kupeleka Bariadi na wilaya hizo zote ambao unafadhiliwa na KfW pamoja na Global Climate Fund, huu ni Mfuko wa Mazingira Duniani, kwahiyo fedha hizo, Euro milioni 100 na Euro milioni 25 tayari tumezipata. Sasa hivi tunakamilisha tu usanifu wa kina na muda si mrefu tutatangaza tenda ili tuweze kuujenga mradi ule, huo ndio utakuwa jibu la Mkoa huu wa Simiyu kuliko hivi visima ambavyo kwa muda mfupi vinakuwa vinakauka.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa huu ni mwaka wa nne tangu Serikali ilivyokuja na mpango wa kutoa maji Malagarasi lakini bado mradi uko kwenye upembuzi yakinifu na hata fedha iliyotengwa, shilingi bilioni mbili mwaka huu ni kwa ajili ya upembuzi yakinifu, wakati huohuo wananchi wa Kaliua wanaendelea kuteseka kupata maji na akina mama wanateseka na watoto hawaendi shule kwa wakati.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa huu ni mpango wa muda mrefu, Serikali ina mpango gani wa muda mfupi wa kuwapatia wananchi wa Kaliua maji ya uhakika na masafi? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Kampuni ya GTI imefanikiwa kuchimba kisima cha maji kwenye Kata moja ya Usindi na ikapata maji mengi pamoja na kuwa ardhi ya Kaliua haina maji kwenye water table, Serikali sasa ina mpango gani wa kupeleka wataalam wenye uwezo mkubwa Kaliua waweze kugundua maeneo yenye maji ya uhakika kwenye ardhi ili angalau tupate visima vyenye maji ya kutosha wananchi wapate maji ya kutosha waache kuteseka na adha kubwa ya maji Jimbo la Kaliua? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza Mheshimiwa Sakaya alikuja ofisini na tukazungumza matatizo ya maji katika Wilaya yake na nikamueleza kwamba nitapeleka wataalam kupitia TUWASA ili wakasaidiane na Mhandisi wa Wilaya, inaonekana kidogo Mhandisi wa Wilaya hana uwezo wa kuweza kufanya usanifu wa miradi maana mpaka sasa ametengewa shilingi milioni 692 anataka azitumie zote kufanya usanifu, nimekataa kwamba haiwezekani ukatumia shilingi milioni 600 kwa usanifu, tunataka tupate matokeo.
Kwa hiyo, napeleka wataalam ili wakashirikiane angalau hata hicho kisima anachokizungumza tuweze kukiendeleza wananchi wa pale waweze kupata maji.(Makofi)
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Katika maeneo ya Mkoa wa Manyara hasa Wilaya ya Kiteto na Simanjiro katika Kata za Makame, Ndedo, Lolera kwa upande wa Kiteto na Kitwai, Naberera na vijiji vya Namalulu hali ni mbaya, ule ukanda ni wa wafugaji.
Naomba tu kumuuliza Mheshimiwa Waziri ni lini sasa watu hawa wataweza kupata huduma hii ya mabwawa kwa ajili yao wenyewe pamoja na wanyama?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba tuelewane, suala la vijiji anavyovisema na hayo mabwawa anayoyasema tumetoa mwongozo. Naomba sana Waheshimiwa Wabunge tushiriki katika kuweka vipaumbele katika wilaya zetu kulingana na bajeti ambazo tunaziweka kwamba mwaka huu tunapeleka maji katika vijiji kadhaa na mwaka unaofuata vijiji kadhaa. Pia tumesema kwamba kila Halmashauri iweke katika mapato ya ndani mipango ya kujenga mabwawa.
Kwa hiyo, mambo yote haya yanaibuliwa kwenye Wilaya na Halmashauri husika, ukiniuliza swali la nyongeza hapa nitakujibu kiujumla. Kwa hiyo, mimi nilifikiri ni vizuri sana tukashiriki kuibua miradi kwenye Wilaya ili hivyo vijiji anavyovisema viweze kuwekwa kwenye mipango.
MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kuwa mji mdogo wa Mlowo uliopo Jimbo la Mbozi ambao una idadi ya watu karibu 60,000 tangu uhuru hawajawahi kupata maji safi na salama ya kunywa licha ya kwamba Marais wote wanaopita huwa wanaahidi kutatua tatizo hili la maji.
Je, ni lini Serikali itatatua tatizo hili la maji katika Mji Mdogo wa Mlowo ambapo mwaka jana wametangaza tenda lakini hadi sasa hakuna kinachoendelea katika Mji ule wa Mlowo? Ahsante sana.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza si kweli kwamba wananchi wale hawajawahi kupata maji toka uhuru. Sema maji yaliyopo pale Mlowo hayatoshelezi kwa wingi wake lakini wanapata maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nikupe taarifa kwamba sasa hivi Serikali imeamua kuanzisha huu Mkoa wa Songwe na tutakuwa na mamlaka moja. Kwa hiyo, Mlowo na Mbozi tutaunganisha mamlaka moja ya maji na tutaipa uwezo zaidi wa kuweza kusambaza maji ya kutosha. Sasa hivi tayari tender imeshatangazwa katika kuboresha upatikanaji wa maji Mlowo pamoja na Mbozi.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru Mheshimiwa Waziri amejibu vizuri. Swali langu lilikuwa ni kuhusu vipingamizi ambavyo vimekuwa vikitumika vya wanyama kwamba ni Mbunga ya Wanyama; na pili suala la misitu. Mimi naomba Serikali itoe kauli yake kwamba hivyo vipingamizi havitakuwepo.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Pia nampongeza Mheshimiwa Sitta kwa namna anavyofuatilia tatizo la maji kwa wananchi wa Urambo. Amekuja Wizarani, tumeongea naye na kimsingi tumekubaliana kwamba maji ya wananchi wa Urambo tutayatoa Mto Ugalla. Suala la kufanya upembuzi yakinifu ni jambo la msingi katika miradi yote. Ni lazima tufanye haya maana kule Ugalla ni Hifadhi. Sasa ni lazima tufanye mawasiliano nao kwamba tutapitisha mabomba sehemu zipi na itaathiri vipi! Masuala haya ni ya msingi lakini haitazuia mradi ule kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nikuhakikishie kwamba tutapeleka maji kupitia kwenye Hifadhi, lakini mawasiliano ya kimsingi kati ya Wizara husika; Maliasili na Utalii pamaja na Ofisi ya Rais, Mazingira, lazima tuyafanye ili tuweze kukubaliana vigezo vipi tuvifanye na mradi uweze kuwa endelevu kwa ajili ya faida ya nchi hii. Ahsante sana.
MHE. ABDULAZIZ M. ABOOD: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Spika, tatizo la Urambo linafanana na tatizo la Morogoro Mjini, wananchi wa Morogoro Mjini wanategemea maji Bwawa la Mindu. Vyanzo vingi vinavyomwaga maji katika bwawa la Mindu vimekauka. Kuna Mto Mgeta kilomita 60 kutoka Bwawa la Mindu.

Je, Serikali haiwezi ikaanzisha mradi wa maji kutoka Mto Mgeta ili kuweza kujaza Bwawa la Mindu na wananchi wa Morogoro wakaondokana na kero ya maji?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, tutaangalia mapendekezo yake. Kwa sasa hivi tumeanzisha Awamu ya Pili ya Programu ya Maji katika nchi nzima.

Kwa hiyo, tutaangalia vyanzo vya maji vilivyopo na vingine vipya ili kuhakishisha kwamba azma ya kupeleka maji kwa wananchi wote inatekelezeka. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge ushauri wako tutauzingatia.

MHE. JUMA S. NKAMIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali moja tu la nyongeza. Mji wa Dodoma ni Mji unaokua kwa haraka sana na leo tunategemea asilimia mia moja ya maji kutoka katika visima vilivyoko pale Mzakwe. Moja kati ya juhudi zilizokuwa zimebuniwa na Serikali ni pamoja na kutengeneza bwawa la Farkwa, ambalo litaleta maji hapa Dodoma kupeleka Bahi, Chemba na maeneo ya jirani.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri awahakikishie Watanzania na wananchi wote wa Dodoma, kwamba ni lini mradi huu wa bwawa la Farkwa utaanza kujengwa kwa sababu sasa hivi tayari wananchi wameshaambiwa wasiendeleze nyumba zao na miradi yao mingine wakisubiri ujenzi uanze. Naomba Mheshimiwa Waziri atuhakikishie ni lini bwawa hili litaanza kujengwa na lini wananchi wataanza kulipwa fidia?
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Nkamia, kwanza umeuliza swali mara mbili lakini naona kama kuna maswali matatu.
MHE. JUMA S. NKAMIA: Mheshimiwa Naibu Spika, basi unisamehe tu kwa leo.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba ujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Nkamia.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba sasa hivi maji tunayoyapata tunayapata kutoka visima vya Mzakwe, lakini Serikali tayari imeishafanya upembuzi yakinifu, na usanifu wa kina kuhusiana na ujenzi wa bwawa la Farkwa. Sasa hivi Serikali inachofanya ni kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa bwawa hili ili kuhakikisha kwamba Mji wa Dodoma sasa hautakuwa na matatizo ya maji. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, suala hili tunalitekeleza katika Program ya pili ya Maendeleo ya Sekta ya Maji.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Mamlaka ya Maji ya Tabora Mjini (TUWASA) ina matatizo makubwa ya malimbikizo ya madeni zaidi ya bilioni mbili ambayo inawadai Taasisi za Serikali na hasa majeshi yetu na kwa kuwa Mheshimiwa Waziri amesema katika majibu yake ya msingi kuna pesa zimetengwa kulipa katika miradi mbalimbali. Je, ni lini Mamlaka ya Maji Tabora watalipwa pesa zao ambazo zinawafanya sasa wasifanye kazi kwa ufanisi?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, madeni ya maji ambayo Taasisi za Serikali zinadaiwa katika mwaka wa fedha zitalipwa moja kwa moja kwenye Fungu la Hazina. Kwa hiyo, tutakapoanza kutekeleza Bajeti hii ambayo mmeipitisha tutaangalia tuweze ku-manage fedha zile, tuweze kulipa kwenye mamlaka husika ili waweze kuendelea kutoa huduma za maji.
MHE. ESTER M. MMASI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa upande wa Dar es Salaam na hususani kwa Jimbo la Kawe, ni dhahiri kwamba tumekuwa na changamoto za maji. Changamoto hizi zinatokana na kodi kubwa inayowekwa kwenye madawa ya kutibu maji, pamoja na kuhifadhi maji.
Pia tumekuwa na tatizo la miundombinu chakavu kwa upande wa DAWASA na vile vile tumekuwa na bajeti isiyokidhi mahitaji ya suala zima la upatikanaji wa maji kwa Mkoa wa Dar es Salaam. Je, Serikali imejipangaje katika kutatua changamoto za maji, kwa Jimbo la Kawe zaidi sana pale Boko, Tegeta na Bunju. Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, mradi wa mkubwa wa maji kutoka Ruvu Chini umekamilika na sasa hivi maji yameongezeka sana katikaJiji la Dar es Salaam. Tatizo tulilokuwa nalo ni ule mtandao. Tunao ule mtandao wa zamani ambao ni chakavu, kazi ya ukarabati inaendelea. Pia tayari tuna mkandarasi ambaye anafanya mtandao mpya maeneo hayo ya Kawe kwenda Bunju mpaka Bagamoyo, baada ya muda siyo mrefu maeneo yale upatikanaji wa maji utaongezeka sana. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge na suala la kodi ya VAT kwenye madawa ya maji, Serikali imeshakubali kuondoa kodi ya VAT kwa hiyo, tunatarajia bei ya maji itapunguzwa kwa sababu itakuwa ni kigezo cha kupunguza bei maji wakati gharama za kununua madawa yale zimepunguzwa.
Mheshimiwa Mbunge uwe na imani kwamba baada ya muda siyo mrefu bei ya maji itapungua, lakini pia upatikanaji wa maji utaongezeka katika Jiji la Dar es Salaam.
MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niulize swali la nyongeza. Wananchi wa Vijiji vya Kitulila, Mwatola, Luponde, Njomlole, Lusitu na Uwemba walichanga fedha kama asilimia 10 ya mradi wa maji ya mtiririko kutoka katika milima ya Igongwi
Ludewa: Je, ni lini mradi huu sasa utaanza kutekelezwa ili wananchi hawa waweze kupata maji?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, tulivyoanza mradi wa WSDP tulisema kwamba mradi huu ni shirikishi na wananchi ilibidi wachangie, lakini sasa tumeamua kwamba fedha zile ambazo wanachangia wananchi hazitatumika wa kujenga miradi ila watazitumia katika kuiendesha miradi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, asilimia ambayo vijiji wameweza kujenga, watatumia katika kuendesha ile miradi itakapokamilika. Lini miradi ile itaanza? Tumetoa program na bajeti tumepitisha, tumeeleza utaratibu. Kwa hiyo, kila Halmashauri ilileta vijiji vya kipaumbele, kwa hiyo, naamini vijiji anavyovisema, Halmashauri yake iliviweka kwenye kipaumbele, tutaanza katika mwaka wa fedha wa 2016 /2017.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Nakushukuru sana Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumuuliza Waziri wa Maji, kumekuwa na miradi ya World Bank ambayo ilianza mwaka 2013 na miradi hii baadhi yake huwa inatolewa ripoti kwamba tayari imekamilika ilhali maji hayatoki katika maeneo hayo. Napenda kuainisha maeneo ambayo maji hayatoki ikiwa ni pamoja na kumwomba Waziri mwenye dhamana akubaliane nami baada ya Bunge hili twende pamoja kwenye maeneo hayo ili akajionee yeye mwenyewe adha ambayo wanaipata wanawake kuhusiana na miradi hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo haya ni yafuatayo: Litola na Kumbara ni baadhi tu ya maeneo katika Wilaya ya Namtumbo; Wilaya ya Mbinga kuna mradi wa Mkako na Litoha; Wilaya ya Tunduru kuna Nanembo na Lukumbule; lakini pia katika Manispaa ya Songea kupitia SOWASA Kata ya Ruvuma, Subira, Luwiko, Bombambili, Msamala na Matalawe ni maeneo ambayo maji hayapatikani. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ningependa baada ya Bunge hili tuweze kuongozana akaone mwenyewe kwa macho. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili…
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Nahitaji Waziri niongozane na yeye akaone mwenyewe.
Swali la pili, katika Kituo cha Afya cha Lipalamba hakuna maji kabisa na wananchi sasa wameshaanza kujichangisha kwa ajili ya kuchimba mitaro kwa ajili ya kutandika mipira ya mabomba. Je, Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari kutoa fedha kwa ajili ya kununua roll mita 30 kwa ajili ya kutandika pamoja na vifaa vyake vya kuungia?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ameomba kama niko tayari kuongoza naye kwenda kuona maendeleo ya utoaji wa huduma ya maji katika Mkoa wa Ruvuma. Nakubali ombi lake, nitafanya hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili na katika jibu la msingi, tumesema kweli katika vijiji 80 vipo vijiji ambavyo bado miradi haijakamilika na kwamba iko katika hatua mbalimbali. Sasa kuwa na jibu ambalo ni mahususi kujua kijiji gani tumesema imekamilika na maji hayatoki, hii inabidi tuifanyie verification. Haya majibu yanayoletwa inawezekana yakawa sio sahihi, lakini naomba sana Waheshimiwa Wabunge katika vikao vya Halmashauri za Wilaya taarifa hizi za maendeleo ya huduma za maji katika maeneo yale huwa zinatolewa kila robo mwaka, naomba sana tuwe tunahudhuria vikao vile ili tuweze kujua.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, kama kuna tatizo la msingi la kisera ambalo Waziri inabidi nijue, naomba Mheshimiwa Mbunge tuendelee kuwasiliana ili tuweze kuona namna gani tutamaliza matatizo ya maji kwa wananchi wetu.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa Rais alipotembelea Mji wa Makambako aliwaahidi Wanamakambako kwamba atatoa fedha kwa ajili ya kutatua tatizo la Mji wa Makambako kupatiwa maji; naishukuru Serikali kwamba na kwenye bajeti zilitengwa fedha za kutoka India: Mheshimiwa Waziri anawaambia nini Wanamakambako kuhusu fedha ambazo zimetengwa kutoka Serikali ya India kutatua tatizo la Mji wa Makambako kupata maji?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli wakati wa kampeni aliahidi kwamba tutaboresha upatikanaji wa maji katika Mji wa Makambako. Tayari Serikali ya Tanzania pamoja na Serikali ya India imeweza kupata fedha za kuchangia uboreshaji wa huduma za maji katika Mji wa Makambako. Taratibu za kupata Mhandisi Mshauri atakayefanya usanifu wa kina ili kuweza kujua ni maeneo yapi na usambazaji wake ukafanyika zinaendelea kufanyika na hatua hizo zitakapokuwa tayari, tutamjulisha Mheshimiwa Mbunge.
MHE. RASHID M. CHUACHUA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Napenda kumwuliza Mheshimiwa Waziri maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, kwa kuwa Kata nyingi katika Kata alizozitaja hakuna hata kijiji kimoja chenye maji ya bomba, na kwa sababu Serikali imetenga fedha katika mwaka uliopita wa bajeti, shilingi milioni 599 na fedha hizi bado hazijakwenda katika Halmashauri yangu wakati wananchi wameshachimba mifereji kwa ajili ya maandalizi.
Je, Serikali itapeleka lini fedha hizi?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Halmashauri yangu imeandika barua ya kuomba uchimbaji wa visima katika vijiji kumi vya Halmashauri yangu vilivyopo pembezoni, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya uchimbaji wa visima hivi? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Chuachua kwa namna alivyoweza kuwahamasisha wananchi wa Masasi kujitolea kuchimba mitaro ili ile Mamlaka ya MWANAWASA iweze kuunganisha. Nilifika pale na nikaona hiyo kazi, tukacheza na ngoma. Kwa hiyo, nakupongeza sana Mheshimiwa Chuachua na nataka huu mfano uigwe na Waheshimiwa Wabunge wengine, kwamba ni vizuri tukahamasisha wananchi pale inapowezekana, kujitolea kuchimba mitaro ili kazi iweze kwenda haraka na wananchi waweze kupata maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake kwamba ni lini fedha zitapelekwa? Tayari nimeshaidhinisha kupelekwa fedha, hasa kuanzia Masasi Mjini kwa ile kazi ambayo niliona inaendelea. Kwa hiyo, nimeshaidhinisha fedha, kwa hiyo, sasa hivi ziko njiani, muda siyo mrefu watazipata ili waweze kuunganisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili kuhusu ombi la visima, hili naomba nilipokee kwa sababu ameliuliza kama swali la nyongeza, nilipokee, nitakwenda kuangalia tuone namna gani tutasaidia kuweza kuchimba visima hivyo.
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kazi iliyofanyika Masasi ya kuchimba mitaro, kazi hiyo iliyofanyika pia katika Wilaya ya Nachingwea katika Kata za Naipanga, Chiwindi, Rahaleo, Mkotokweana pamoja na Stesheni. Kupitia nguvu za Mbunge na wananchi tumechimba zaidi ya kilometa 15. Sasa fedha iliyoletwa ni chache na sasa hivi ni mwezi, mabomba yaliyoletwa kwa ajili ya mradi huu yameshindwa kukidhi mahitaji ya mradi mzima. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kupata jibu la Mheshimiwa Waziri, ili nguvukazi za wananchi zilizotumika zisipotee, ni lini fedha hii ambayo imeombwa kwa ajili ya mradi huu italetwa ili tuweze kukamilisha kazi ambayo tumeianza? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naye nimpongeze kama ameweza kuhamasisha wananchi kuchimba mtaro wa kilometa 15 ili iwe kazi rahisi kwetu sisi kuweka mabomba. Tayari mabomba mengi yameshapelekwa, yapo Masasi na Nachingwea kwa ajili ya kuyalaza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la fedha, fedha tunazipeleka kulingana na namna tunavyopokea. Kwa hiyo, fedha za Mfuko wa Maji zinazokuja kwa mwezi ni kama shilingi bilioni kumi. Kwa hiyo, hizi ndizo tunazogawana kuwapelekea kila Halmashauri, pale ambapo inaonekana kuna kazi inayoendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kazi ambayo imeanza haitaachwa, tutapeleka hiyo fedha mapema iwezekanavyo.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, matatizo yaliyopo huko Masasi, yanafanana kabisa na matatizo yaliyopo katika Mji wa Itigi wenye vijiji saba vya Kihanju, Songambele, Tambukareli, Majengo, Ziginari, Itigi Mjini na Mlowa, hakuna kabisa mtandao wa maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tulishaandika barua kwa Wizara kuomba wataalam wa Wizara waje watufanyie upembuzi yakinifu na Wizara ikatujibu kwamba haina wataalam kwa sasa na kwamba tushirikiane na Mkoa, na tukaandika barua ya kuomba kiasi kidogo tu, shilingi milioni 40 kwa ajili ya kutusaidia bajeti ili wataalam hawa wa Mkoa na wale wa Halmashauri waweze kufanya upembuzi yakinifu ili tuwapatie maji wananchi wa Itigi.
Je, ni lini sasa Serikali itaisaidia Halmashauri ya Itigi hizo hela kidogo tu ambazo zitafanya nasi tupate mchanganuo wa kujua ni nini tunahitaji ili Wizara iweze kutupa pesa za kujenga miundombinu ya maji?
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa kuhusu fedha za uendeshaji au kufanyia usanifu wa kazi kwenye Halmashauri yake, katika hii bajeti ya shilingi bilioni 237 tuliyoitoa, kazi yake kubwa kwanza ni kujenga miundombinu kama ipo lakini pia fedha hizo zinatumika kwa usanifu, usimamizi na kadhalika; lakini pia na uendeshaji wa ofisi ni fedha hiyo hiyo. Kwa hiyo, katika bajeti ambayo Halmashauri yake ya Itigi imetengewa kwa mwaka 2017/2018 naomba watumie sehemu ya hiyo fedha ili waweze kufanya hiyo kazi ambayo Mheshimiwa Mbunge anaizungumzia. Kama wanaleta maombi, maana tutawapa hizo fedha, lakini tutakata kwenye allocation ambayo wametengewa kwa mwaka 2017/2018.
MHE. CATHERINE N. RUGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Napenda nimuulize Mheshimiwa Waziri swali dogo la nyongeza. Tatizo la uhaba wa maji katika Wilaya ya Serengeti hasa vijijini, limekuwa ni kubwa na la muda mrefu na kuanzia mwaka 2007 mpaka sasa hivi Serikali bado inatekeleza mradi wa maji katika vijiji kumi, ila mpaka ninavyozungumza kuna miradi miwili katika vijiji vya Kenyana, Nyamitita na Kibanjabanja haijakamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujua, ni lini sasa miradi hii itakamilika ili wananchi wa maeneo husika waweze kupata maji safi na salama?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Catherine amezungumzia baadhi ya miradi ambayo ipo kwenye Halmashauri yake na kuniuliza ni lini miradi ile itakamilika?
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme tu kwamba itabidi nifuatilie niweze kujua, kwa sababu hili ni swali la nyongeza, siwezi kuwa najua kila kijiji katika nchi nzima, mradi ule uko katika status gani? Kwa hiyo, naomba sana tuonane naye, anakaribishwa ofisini ili tuweze kuangalia. Nitampa status na taarifa kamili ni lini miradi ile itakamilika.
MHE. LUCY T. MAYENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa tatizo hili la maji lipo kwenye categories mbalimbali kwa nchi nzima, wapo watu ambao hawana kabisa miradi katika maeneo yao kwa sisi Wabunge hapa ndani Bungeni, lakini pia yapo maeneo ambayo miradi ipo lakini haijakamilika kutokana na sababu mbalimbali, lakini yapo maeneo katika nchi yetu ambayo maji yanapatikana lakini kumekuwa na manung’uniko ya chini chini ya wananchi kwamba jinsi bili zinavyotoka kunakuwa hakuna usawa.
Mheshimiwa Naibu Spika, matatizo haya yamekuwa yakisemwa kwa wananchi kwa muda mrefu na yamekuwa takribani kila Mbunge anaposimama hapa wengi wamekuwa wakigusia kuhusu tatizo la kutokuwa na usawa wakati wa kutoa bili.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara badala ya kusema kwamba wananchi au sisi Wabunge twende kwenye bodi kutoa malalamiko au wananchi waende kule kwenye taasisi za kutoa huduma ili kwenda kupeleka malalamiko yetu.
Je, Wizara hii haioni sasa umefika wakati kuchukulia tatizo hili kwa ukubwa wake kama tatizo la kitaifa, kuunda timu maalum itakayopita kila maeneo na kuweza kujua kwamba maeneo haya yana matatizo haya tuweze kuyatatua vipi na eneo hili matatizo yake tuweze kutatua vipi? (Makofi). Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Lucy Mayenga ameuliza swali zaidi ya moja; anazungumzia habari ya matatizo ya upatikanaji wa maji, lakini pia anachanganya tena na masuala ya bili. Sasa ni vitu viwili tofauti. Masuala ya upatikanaji wa maji, Serikali inaendelea kutekeleza.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili la matatizo ya bili nimeshalitolea majibu, labda nirudie kwa kuweka msisitizo. Ni kwamba Wizara inatambua yapo maeneo ya mtu mmoja mmoja kulalamikia bili, siyo kwamba kila mmoja analalamikia bili. Sasa nasema, kama ni isolated cases, hatuwezi kuchukulia kama ni tatizo la Kitaifa. Hili ni tatizo la mtu mmoja ambaye ana tatizo, amepewa bili ya miezi mitatu hajapata maji.
Sasa hili naomba tulifuatilie kwa maana ya kwa huyo mtu ambaye anatuletea ni isolated case tuishighulikie. Siyo jambo la kusema tulitolee mwongozo kama Taifa kwa maana ya kwamba tumeshakubaliana kwamba maji ili yawe endelevu, upatikanaji wake ni lazima tuchangie.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kulipa bili ni lazima ili tuwe na uhakika wa kuwa na maji. Sasa kama kuna matatizo mahali, tutayashughulikia kwa mujibu wa sheria na kwa mujibu wa taratibu tulizojiwekea.
MHE. MARY D. MURO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa miradi yote iliyojengwa katika Wilaya ya Kibaha Mjini iko chini ya viwango na imetokana na kwamba Wilaya ya Kibaha haina Mhandisi wa Maji anayetumika pale ni Mhandishi wa Mazingira. Je, ni lini Kibaha italetewa mtaalamu wa maji?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa ametaja kwamba Pangani iko miongoni mwa kata zitakazopata maji, lakini Pangani ina mradi ambao umegharimu shilingi milioni 531 ambao umejengwa chini ya kiwango kwa mabomba kuunganishwa na moto badala ya connector. Je, yuko tayari kufuatana na mimi kwenda kujionea ubadhirifu uliofanyika?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri aliyoyatoa kuelezea mafanikio ya mtambo wa Ruvu Juu maana ndio lilikuwa swali la msingi, kuona kwamba maeneo yale ambayo mtambo ule umepitisha maji yanapata maji kwa sasa baada ya kuwa umekamilika. Haya maswali mawili anayoongezea ni tofauti na lile swali la msingi. Maswali anayoyauliza ni miradi inayotekelezwa na Halmashauri ya Kibaha.
Mheshimiwa Spika, hii ni sehemu nyingine lakini hata hivyo tutakupa majibu kwamba kama miradi ya Kibaha Mjini anasema yote imetekelezwa chini ya kiwango, hii ni kazi ambayo inabidi twende tukaiangalie, hatuwezi kuwa na jibu hapa, maana yake hatuelewi hilo. Mimi taarifa niliyonayo kwamba kazi zimefanyika lakini kama ni kweli iko chini ya kiwango tutakwenda kuliangalia.
Mheshimiwa Spika, pia huo mradi wa Pangani anaousema ana wasiwasi wa utekelezaji wake, nao naomba pia tupewe nafasi tutakwenda kuangalia na kama kuna tatizo tutachukua hatua kulingana na taratibu zetu za kusimamia miradi ya maji.
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Katika majibu yake Mheshimiwa Naibu Waziri amesema mradi wa Ruvu Juu umekamilika na kwamba maeneo ya ndani ya kilometa 12 kutoka bomba kuu yanapata maji hivi sasa na ameyataja maeneo ya Kibamba, Mbezi, Msigani na kwingineko ambayo yako ndani ya Jimbo la Kibamba. Ukweli ni kwamba ule mradi haujakamilika, yapo maeneo ambayo yana mabomba ya Mchina ambayo maji bado hayatoki.
Mheshimiwa Spika, napenda Mheshimiwa Naibu Waziri ajibu ukweli, kwa maeneo ambayo yana mabomba ya maji lakini maji hayatoki mpaka sasa, ni lini maji yatatoka kama anavyosema mradi umekamilika? Je, yuko tayari baada ya hapa twende tukakague huo mradi anaosema umekamilika lakini maji hayatoki?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, tunaposema kwamba mradi umekamilika ni kwamba sasa maji yameanza kutoka na tumeanza kusambaza. Kwenye jibu la msingi tumeelezea kwamba tutakwenda kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Awamu ya kwanza tumeeleza maeneo ambayo tayari yameanza kupata maji.
Mheshimiwa Spika, maeneo hayo anayosema ya mabomba ya Mchina ni sehemu ambayo maji yale yatakwenda. Yamechelewa kufika kwa wakati kwa sababu kulikuwa kuna tatizo la umeme pale Ruvu Juu. Sasa hivi tayari mitambo imeshawashwa na imeshajaribiwa tayari maji yameanza ku-flow mpaka tanki la Kibamba, kwa hiyo, tunaendelea kuunganisha. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge tutakwenda kuangalia hayo maeneo unayosema yana mabomba ya Mchina kwamba yameanza kupata maji au vipi lakini lengo letu ni maji yale yafike kule.
Mheshimiwa Spika, kwa sababu sasa hivi kwa mitambo hii miwili, ya Ruvu Chini na Ruvu Juu tunazalisha lita milioni 466 kwa siku, ni maji mengi sana. Kwa hiyo, kazi yetu kubwa ni kuhakikisha kwamba mitandao ile ambayo ina mabomba inapata maji lakini maeneo mengine yale ambayo hayana mitandao, Serikali inaweka bajeti yake. Hata bajeti ambayo nitaisoma baada ya wiki moja nitaelezea mipango ambayo tumeiweka kwa ajili ya fedha za ndani kuweza kusambaza maji zaidi maeneo ambayo hayana mtandao.
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Wanawake wa Kongwa, Singida na wa nchi nzima wanasubiri utekelezaji wa kauli ya kumtua mwanamke ndoo. Leo hii Mheshimiwa Waziri anajibu swali kwa kusema kwamba mkandarasi alipata mkataba mwaka 2014 mpaka sasa eti wana mazungumzo. Naomba Mheshimiwa Waziri aendane na kauli ya kumtua mwanamke ndoo kwa kusitisha kwa haraka mikataba inayosuasua ili tuwaokoe wananchi wa Tanzania. Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa katika utekelezaji wa kuhakikisha kwamba Watanzania wanapata maji, tulianzisha hii Programu ya Maji na tukawapa hawa Wakurugenzi wa Halmashauri kusimamia miradi mingi. Toka tumeingia Awamu ya Tano, kitu cha kwanza tulichofanya tumeikwamua miradi mingi iliyokuwa imesimama baada ya fedha kuanza kwenda.
Mheshimiwa Spika, hatua ya pili, tunafanya mapitio ya mikataba yote ya hovyo ambayo ilikuwa imeingiwa halafu wanafika mahali wamekwama. Kwa hiyo, mikataba ile ambayo ilikwenda vizuri miradi imekamilika na sasa hivi kati ya miradi 1,800 miradi 1,300 imekamilika, bado hii 400 ambayo inaendelea kwa hatua mbalimbali.
Kwa hiyo, katika hii 400 kuna baadhi ya mikataba ambayo tunafanya mapitio kama huo mradi wa Nyang’wale ambao kidogo una figisu figisu kwamba mkataba wa kujenga matanki na kupeleka mabomba ni watu tofauti. Sasa mikataba ikiwa ya namna hiyo unakuta mmoja akizembea, utekelezaji unakuwa hafifu. Kwa hiyo, azma ya Serikali ya kuhakikisha kwamba tunamtua mama ndoo iko pale pale.
MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza, lakini kabla sijauliza maswali mawili ya nyongeza ninaomba kufanya marekebisho kidogo. Jimbo sio la Mbozi Mashariki ni jimbo la Mbozi, kwa hiyo, naomba liingie vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, Skimu za Umwagiliaji za Wilaya ya Mbozi zimechukua muda mrefu sana, kwa mfano Skimu ya Mbulu Mlowo imechukua zaidi ya miaka mitano haijakamilika na skimu hii ina urefu wa mita 1,125, zimejengwa mita 700 tu bado mita 400 kukamilika, miaka mitano mita 700, hizi zilizobaki 400 sijui zitakamilika lini. Sasa ninaomba Mheshimiwa Waziri aniambie ni lini hizi mita 400 zilizobaki zitakamilika katika Skimu hii ya Umwagiliaji ya Mbulu Mlowo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Wilaya ya Mbozi ni maarufu sana kwa uzalishaji wa zao la kahawa aina ya Arabica, ni kahawa ambayo ni tamu sana na ina soko sana duniani. Lakini kutokana na mabadiliko ya tabianchi mikahawa mingi inakauka Mbozi, hali imekuwa ni mbaya na muda si mrefu mikahawa hii inaenda kupotea Mbozi hatutakuwa na kahawa tena. Mheshimiwa Waziri, ninaomba sasa Serikali iweze kutoa commitment hapa; je, mko tayari kuweza kujenga mabwawa ya umwagiliaji wa kahawa maeneo yote yanayolima kahawa Mbozi ikiwepo Isansa, Igamba, Iyula, Msia na maeneo mengine ya Wilaya ya Mbozi? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, anasema kwamba hizo skimu zimechukua muda mrefu; ni kweli, utaratibu uliokuwepo hapo mwanzo ulikuwa kwamba washirika wa maendeleo, JICA wamekuwa wanatekeleza wenyewe moja kwa moja, sasa tumeanzisha Tume ya Umwagiliaji ambayo ndiyo itasimamia miradi yote ya umwagiliaji na tulichopanga ni kwamba kwa kuanzia tutafanya mapitio ya miradi yote ya umwagiliaji tuikamilishe ile ambayo inaendelea.
Kwa hiyo, na huo mradi ambao tayari unaendelea tutaukamilisha kwanza kwa fedha ambazo tumezitenga kwenye bajeti. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali lako la pili kuhusu tabianchi; tabianchi haina jibu la moja kwa moja ila ni lazima sisi tuchukue hatua kwanza ya kukabiliana nalo. Kwanza, tuweze kuona namna gani tutatunza mazingira, hii ni kazi ambayo lazima hata Halmashauri ya Mbozi ishughulike, ukataji wa miti, uchomaji wa mikaa ni lazima uachwe kwa sasa hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia suala la kujenga mabwawa, tulichokipanga ni kwamba kwanza tutafanya kila Wilaya imeainisha maeneo ya kujenga mabwawa, tunafanya usanifu kwanza tuweze kujua gharama na tuweze kuona mahitaji jinsi bwawa lile linaweza kuwasaidia wananchi kwa kilimo cha umwagiliaji. Kwa hiyo, suala lake tunalishughulikia na Serikali kupitia Tume ya Umwagiliaji. (Makofi)
MHE. JOYCE B. SOKOMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nashukuru pia kupata swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mara umezungukwa na Ziwa Victoria lakini cha ajabu Ziwa hilo hilo lime-supply maji kutoka Ziwa Victoria kuja Shinyanga, Tabora na Dodoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mara hasa Musoma Vijijini na Wilaya ya Bunda haina maji. Je, Mheshimiwa Waziri ni lini Wilaya hizo zitapata maji? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mara ukianzia na Mji wa Mara tumechukua maji kutoka Ziwa Victoria pamoja na vijiji vyote vinavyozunguka ule Mji wa Musoma kwahiyo siyo kwamba hakuna mahali tumechukua maji kutoka kwenye Ziwa Victoria. Pia katika maeneo mengine, unajua hatuwezi kusema tutapeleka maji ya Ziwa kupeleka kila Kijiji katika mradi huu wa WSDP tulikubaliana kwamba ili tuweze kufika maeneo mengi lazima tutafute teknolojia ambayo ni rahisi ili kila Kijiji kiweze kupata maji kwa haraka na ndiyo maana tulianza na concept ya visima. Sasa baada ya kuona kwamba visima maeneo mengine havijakuwa endelevu ndiyo tumeanza kurudi sasa kubuni miradi mikubwa zaidi ambayo teknolojia Wananchi hawawezi kuendesha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukichukua maji kwenye bahari au kwenye ziwa utahitaji umeme mkubwa, mitambo mikubwa na wananchi hawawezi kuendesha na ndiyo maana sasa tunafikiria kwamba katika awamu inayokuja hii awamu ya tano ili tuwe na uhakika kwamba miradi yetu inakua endelevu tunataka tusimamie chini ya Wakala wa Maji Vijijini, hawa watakuwa na mfumo unaokuwa ni sahihi kwa nchi nzima kuliko sasa kila Halmashauri, unakuta Halmashauri nyingine umewapelekea fedha mpaka inafika mwezi Juni hawajafanya kitu chochote, fedha wanazo lakini hawafanyi chochote sasa nataka tuingize kwenye Wakala wa Maji ambao watasimamia ujengaji wa hii miradi, halafu hawa TAMISEMI, hizi Halmashauri zitakuwa zinaendesha pale ambapo wanaweza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukichukua kwa mfano Nansio, tumejenga mradi mkubwa wa maji, Halmashauri haiwezi kuendesha kwahiyo imebidi Wizara tuendelee kuendesha kwahiyo maeneo mengine tutafanya hivyo. Ukichukua mradi mkubwa kutoka kwenye mto ni lazima pia uendeshaji wake uwe sasa chini ya Wizara maana yake Halmashauri haziwezi kuendesha kwahiyo hili jambo tutalifanyia kazi…