Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Maryam Salum Msabaha (18 total)

MHE. CECILIA D. PARESSO (k.n.y. MHE. MARYAM SALUM MSABAHA) aliuliza:-

Kumekuwa na ongezeko la watoto wanaoishi katika mazingira magumu katika miji mikubwa kama Dar es Salaam, Arusha, Mbeya, Dodoma, Mwanza na kadhalika. Watoto hawa wengi wao hawaendi shule na kazi yao ni kuomba omba barabarani:-

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha watoto hao wanarudishwa shuleni kusoma?

(b) Je, ni lini Serikali itawachukulia hatua wale wote wanaowatumia watoto hao kuombaomba?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza Mpango Kazi wa II wa Taifa wa huduma kwa watoto walio katika Mazingira hatarishi wa mwaka 2013/2017, ambao umeainishwa majukumu ya Serikali Kuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa pamoja na wadau wengine.

Mnamo mwaka 2011, Wizara yetu ilifanya utafiti ili kubaini ukubwa wa tatizo la watoto wanaoishi na kufanyakazi mitaani, katika Mkoa wa Dar es Salaam ambapo watoto wapatao 5,600 walibainishwa. Baada ya utafiti huu uliandaliwa mradi wa majaribio wa namna ya kuwaondoa watoto hao mitaani kati ya mwaka 2011 hadi 2014 ambapo watoto wapatao 226 waliweza kuunganishwa na familia zao.

Mheshimiwa Spika, watoto 179 waliweza kurudishwa mashuleni, watoto 196 walipatiwa huduma za afya na 1,000 walipatiwa unasihi. Aidha, mradi huu ulibainisha Mikoa tisa (9) ambayo inaongoza kwa kuleta watoto katika jiji la Dar es Salaam. Mikoa hii ni Pwani, Iringa, Lindi, Morogoro, Dodoma, Mwanza, Kilimanjaro, Tanga na Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, baada ya utafiti, Wizara yetu iliandaa mpango kazi unaolenga kuzuia watoto kuingia mitaani, kuwarejesha na kuwaunganisha na familia zao na kufanya ufuatiliaji.

(b) Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali kuondoa ombaomba mijini wakiwemo wanaowatumia watoto kwa mfano, kwa Mkoa wa Dar es salaam mwezi Septemba, 2013 ombaomba 253 na watoto 135 walirejeshwa makwao kati ya watoto 33 walirejeshwa shuleni katika Mikoa walikotoka. Zoezi hili linaendelea katika mwaka huu wa fedha 2015/2016 ambapo watoto 47 wameunganishwa na familia zo na kati yao 35 wamerejeshwa shuleni.

Mheshimiwa Spika, suala la ombaomba ni mtambuka, linazihusisha mamlaka za Serikali Kuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Taasisi zisizo za Kiserikali, jamii na familia. Nachukua fursa hii kutoa wito kwa kila mdau kutekeleza wajibu wake katika suala hili.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-
Kazi ya Vikosi vya Ulinzi na Usalama ni kulinda raia na mali zao pamoja na kulinda mipaka ya nchi; lakini baadhi yao wamekuwa wakienda kinyume na sheria kama vile kuwapiga na kuwasababishia wananchi ulemavu au vifo:-
a) Je, mpaka sasa ni Askari wangapi wameshachukuliwa hatua?
(b) Je, ni Askari wangapi mpaka sasa wamekutwa na hatia na kufukuzwa kazi?
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Vikosi vya Ulinzi na Usalama kazi yake ni kulinda raia pamoja na mipaka ya nchi kwa mujibu wa Sera ya Ulinzi wa Taifa. Vile vile ni kweli wapo baadhi ya Askari ambao wamekuwa wakienda kinyume cha sheria za nchi kama vile kuwapiga raia. Hata hivyo, jeshi limekuwa likichukua hatua stahiki kwa Askari ambao wamekuwa wakienda kinyume na sheria, mila na desturi za nchi na za kijeshi katika kipindi chote tangu jeshi letu lianzishwe mwaka 1964. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa swali la Mheshimiwa Mbunge halikulenga kipindi maalum, itakuwa ni vigumu kubainisha idadi ya Askari hao tangu jeshi lianzishwe. Kimsingi, jeshi limekuwa likichukua hatua stahiki za kijeshi dhidi ya wakosaji kwa mujibu wa taratibu zake na wengine kupelekwa katika Mahakama za kiraia kulingana na aina ya kosa alilolitenda mhusika. Waliopatikana na hatia walipewa adhabu stahiki kulingana na uzito wa makosa waliyotenda, ikiwa ni pamoja na vifungo vilivyoambatana na kufukuzwa utumishi jeshini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe kwamba Jeshi la Wananchi wa Tanzania wakati wote linasisitza nidhamu kwa Wanajeshi wake. Pale ambapo kunajitokeza utovu wa nidhamu, hatua madhubuti huchukuliwa mara moja.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-
Baadhi ya Kambi za Jeshi la Wananchi nchini (JWTZ) zina majengo chakavu sana ikiwemo Kambi ya Nyuki Zanzibar:-
Je, ni lini Serikali itatenga fedha za kutosha kwa ajili ya ujenzi wa Kambi hizi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI (K.n.y. WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Msabaha, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Kambi za Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania zina majengo chakavu ikiwemo Kambi ya Nyuki, Zanzibar. Hali hii imetokana na ukweli kwamba, Kambi nyingi za Jeshi zilirithi majengo yaliyokuwa yanatumiwa na Taasisi nyingine. Hata hivyo, Jeshi lina utaratibu wa kufanyia matengenezo majengo yake mara kwa mara kwa kadri ya upatikanaji wa fedha za bajeti za maendeleo.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-
Wapo baadhi ya wafanyabiashara wasiokuwa waaminifu ambao wamekuwa wakitumia bandari „bubu‟ ili kukwepa kodi na kusababisha Serikali kukosa mapato:-
(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kudhibiti wafanyabiashara hao wanaotumia bandari bubu?
(b) Je, ni wafanyabiashara wangapi waliokamatwa katika bandari bubu na kufikishwa Mahakamani?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu(a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua uwepo wa wafanyabiashara wasio waaminifu, wanaotumia bandari zisizo rasmi, yaani bandari bubu kupitisha biashara za magendo, madawa ya kulevya, maliasili, uhamiaji haramu, uvuvi haramu na matumizi ya vyombo vya majini visivyo salama ili kukwepa kodi na pia kuhatarisha usalama wa nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kulipatia ufumbuzi suala hili, Serikali imeanzisha utaratibu wa kufanya vikao vya Wakuu wa Mikoa ya Mwambao wa Bahari ya Hindi na Zanzibar, Kamati za Ulinzi na Usalama na kushirikisha Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Taasisi zinazoshughulikia usafiri majini ambayo ni Mamlaka ya Udhibiti Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA), Mamlaka ya Usafiri Baharini Zanzibar (ZMA), Shirika la Bandari Zanzibar (ZPC) na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA).
Mheshimiwa Naibu Spika, vikao hufanyika kila robo mwaka. Lengo la vikao hivyo ni kutambua na kurasimisha bandari bubu ambazo kulingana na vigezo vya wingi wa biashara inayopita katika bandari hizo na umuhimu wa bandari hizo kijamii, zinastahili kuendelea kuwepo na kusimamiwa na Halmashauri za maeneo husika. Bandari ambazo hazikidhi vigezo hivyo zinatakiwa kufungwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, bandari bubu zilizoamuliwa kurasimishwa katika mwambao wa Bahari ya Hindi kwa upande wa Tanzania Bara ni hizi zifuatazo:-
Mkoa wa Dar es Salaam ni Mbweni, Pwani ni Mlingotini, Kisiju na Nyamisati. Kwa Mkoa wa Tanga ni Jasini, Kigombe, Kipumbwi, Mkwaja na Pangani. Kwa Mkoa wa Mtwara ni Kilambo na kwa Mkoa wa Lindi ni Rushungi na Kilwa Kivinje.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, utaratibu wa kurasimisha bandari binafsi umefanyika katika Ziwa Victoria, Halmashauri ya Ilemela na Nyamagana. Bandari tisa binafsi zimetambuliwa na kurasimishwa. Utaratibu huo utaendelea pia katika Ziwa Tanganyika na Ziwa Nyasa.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wema wamekuwa wakiisaidia Serikali kupitia Kamati za Ulinzi na Usalama katika maeneo yenye bandari bubu kutoa taarifa kwa vyombo vya doria kuhusu kuwepo kwa wafanyabiashara wasio waaminifu katika bandari bubu na hivyo kuwezesha kukamatwa.
Katika mwaka wa 2015 walikamatwa wafanyabiashara 81 na kuanzia mwezi Januari hadi Machi, 2016 wafanyabiashara 17 wamekamatwa na kufikishwa Mahakamani. Aidha, kuna bidhaa nyingi zilikamatwa ambazo wamiliki hawakufahamika, hivyo kuzitaifisha moja kwa moja.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-
Kazi za Vikosi vya Ulinzi na Usalama ni kulinda raia, mali zao pamoja na mipaka ya nchi, lakini kuna baadhi yao wanakwenda kinyume na sheria kwa kuwapiga wananchi na kuwasababishia ulemavu au vifo:-
(a) Je, mpaka sasa Serikali imeshawachukulia hatua gani?
(b) Je, mpaka sasa ni askari wangapi wamekutwa na hatia na kufukuzwa kazi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi hufanya kazi kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu zilizopo. Hata hivyo, kuna askari wachache ambao wamekuwa wakikiuka maadili na mwenendo mwema wa Jeshi la Polisi kama ambavyo imeainishwa katika Kanuni za Kudumu za Jeshi la Polisi, namba 103.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kinidhamu kwa watumishi wanaoonekana kwenda kinyume na maadili ya kazi za Jeshi la Polisi ikiwemo kuwapiga wananchi wasio na hatia. Mathalan, katika kipindi cha kuanzia mwaka 2015 hadi 2016 Juni, askari 200 walichukuliwa hatua za kinidhamu.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya askari 152 walikutwa na hatia na kufukuzwa kazi.
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM (K.n.y. MHE. MARYAM SALUM MSABAHA) Aliuliza:-
Tangu mwaka 2005 kumekuwa na changamoto nyingi katika kero za Muungano:-
Je, mpaka mwaka 2016 ni kero ngapi zimeshapatiwa ufumbuzi wa kudumu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA Alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2016/2017 hoja 15 ziliwasilishwa kutafutiwa ufumbuzi. Kati ya hoja 15 zilizowasilishwa ni hoja 11 zimeshapatiwa ufumbuzi.
Mheshimiwa Spika, Serikali zote mbili yaani Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zinaendelea kushughulikia kero za Muungano kadiri zinavyojitokeza.
MHE. ALLY SALEH ALLY (K.n.y. MHE. MARYAM SALUM MSABAHA) aliuliza:-
Wafanyakazi wa Kampuni mbalimbali nchini wamekuwa wakipata ajali wawapo kazini na baadhi yao kutopewa huduma ya matibabu na waajiri wao na kuishia kupata ulemavu wa kudumu:-
Je, ni wafanyakazi wangapi wamepata stahiki zao baada ya ajali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Bunge lako Tukufu lilipitisha Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi Na. 8 ya mwaka 2008 (Sura 263 marejeo ya mwaka 2015). Sheria hii ilifuta sheria iliyokuwa inamtaka mwajiri kumlipia mfanyakazi wake matibabu na fidia ya ulemavu wa kudumu baada ya kuumia, kuungua au kufariki kutokana na kazi na hivyo kuanzisha Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (Workers Compensation Fund).
Mheshimiwa Spika, Mfuko huu wa Fidia kwa Wafanyakazi unashughulikia masuala ya fidia kwa wafanyakazi waliopo katika sekta ya umma na sekta binafsi Tanzania Bara na umeweka utaratibu katika utoaji huduma za matibabu na fidia ya ulemavu wa muda, malipo ya ulemavu wa kudumu, malipo kwa anayemhudumia mgonjwa, huduma za ukarabati na ushauri nasaha, msaada wa mazishi na malipo kwa wategemezi endapo mfanyakazi atafariki.
Mheshimiwa Spika, hadi kufikia tarehe 31 Machi, 2017, Mfuko umehudumia jumla ya wafanyakazi 478 waliopata ajali wakiwa kazini. Wafanyakazi hawa wamepatiwa huduma za matibabu katika hospitali mbalimbali nchini zilizoingia mkataba na mfuko na wamepatiwa mafao ya fidia kwa mujibu wa sheria. Aidha, Mfuko pia umerudisha gharama za matibabu kwa waajiri ambao waliwatibu wafanyakazi waliopata ajali na kuhudumiwa katika hospitali ambazo hazijaingia mkataba na Mfuko.
Mheshimiwa Spika, Mfuko ulianza kupokea madai ya fidia rasmi tarehe 1 Julai, 2016 na kuanza kulipa fidia kwa mujibu wa Tangazo la Serikali Na. 212A la tarehe 30 Juni, 2016.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-
Kumekuwa na uuzwaji wa silaha kiholela kama vile mapanga na visu katika barabara zetu ikiwemo Ubungo kwenye mataa hali ambayo inaleta hofu kwa raia wema.
Je, Serikali inalichukuliaje suala hilo ambalo ni hatari sana kwa usalama wa raia?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kumekuwepo na uuzaji holela wa silaha za jadi katika maeneo mbalimbali ya barabara zetu ikiwemo katika makutano ya barabara ya Mandela na Morogoro eneo la Ubungo, Jijini Dar es Salaam.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi inatambua uwepo wa tatizo hilo na tayari hatua mbalimbali za kudhibiti hali hiyo zimechukuliwa ikiwa ni pamoja na kufanya operesheni za mara kwa mara na kukamata wauzaji wa silaha za jadi barabarani kama vile mapanga, mikuki, upinde na mishale. Aidha, elimu inaendelea kutolewa kwa wafanyabiashara wa bidhaa za silaha hizo kutowapatia wauzaji wasio na eneo maalum la kufanyia biashara hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na mamlaka nyingine za Serikali linaandaa utaratibu maalum wa uuzaji wa bidhaa za aina hii na kutoa elimu kwa umma kuhusu madhara ya biashara hii na kuwashauri wananchi waipige vita na kuepuka kujihusisha nayo.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-
Majengo ya Kituo Afya cha Kambi ya Jeshi Migombani Unguja ni chakavu na pia ni siku nyingi sana.
Je, ni lini Serikali itajenga kituo hicho ili kiwe cha kisasa na kiendane na wakati?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANO YA NCHI (K.n.y. WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum kwa niaba ya Waziri wa Ulinzi wa Jeshi la Kujenga Taifa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Afya cha Jeshi cha Migombani Zanzibar ni moja ya vituo vya tiba ambavyo huanzishwa katika kila Kikosi cha JWTZ ili kutoa huduma ya mwanzo ya tiba kwa Wanajeshi na familia zao, watumishi wa umma ikiwa ni pamoja na wananchi wanaishi jirani kabla ya kupelekwa katika hospitali za rufaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni, kweli majengo ya kituo hicho na vituo vingine vya JWTZ yamechakaa na kwa sababu ni ya muda mrefu. Kutokana na uchakavu huo wa Kituo cha Kambi ya Migombani na sehemu nyingine, ni matazamio ya Wizara kuvi karabati upya vituo vyote katika mwaka wa fedha 2018/2019 kadri hali ya upatikanaji wa fedha itakavyoruhusu.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-
Bagamoyo ni mji mkongwe wenye vivutio vya kitalii kama ilivyo miji mingine nchini kama vile Zanzibar, Kilwa na Mapango ya Amboni, Tanga.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha vituo vya kitalii nchini ikiwemo Bagamoyo ili kupata wageni wengi zaidi na kukuza pato la Taifa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wa Bagamoyo ni moja ya miji mikongwe katika historia ya utamaduni na maendeleo ya Tanzania ukiwa kando kando ya Bahari ya Hindi. Bagamoyo ni moja ya vituo vya Malikale ambavyo ni mojawapo ya vivutio vya utalii hususani wa utamaduni hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, vivutio hivyo havitumiki ipasavyo katika kukuza utalii kutokana na changamoto mbalimbali ambazo ni ufinyu wa bajeti, ukosefu wa huduma muhimu kwa watalii, kutofikika, kuchakaa kwa vioneshwa na kutotangazwa ipasavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatia changamoto hizo, Wizara imeandaa mkakati wa kuvitambua na kuvitangaza vivutio vyote nchini ukiwemo Mji wa Bagamoyo. Mpango huu unalenga kushirikisha mashirika yaliyo chini ya Wizara, yaani Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA), Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS).
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, vivutio vya malikale vilivyo Bagamoyo ni miongoni mwa maeneo yatakayoendelezwa kwa ushirikano na mashirika hayo. Aidha, vivutio vyote vya utalii nchini vitaendelea kutangazwa kupitia taasisi zinazohusika ikiwemo Bodi ya Utalii Tanzania (TTB). Kazi zitakazotekelezwa na mashirika hayo ni pamoja na kuweka huduma muhimu kwa watalii, kuboresha miundombinu ya vituo hususani majengo na barabara ili kuwezesha kufikika kwa urahisi na kuwa na mwonekano unaovutia; kujenga vituo vya kumbukumbu na taarifa pale ambapo vinahitajika, kuboresha vioneshwa na kuvitangaza na kuhamasisha wawekezaji wa hoteli, michezo na vivutio vingine vya watalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mkakati huu, Wizara itaendelea kusimamia majukumu yote ya uhifadhi, utafiti na kuandaa taarifa zitakazosaidia kuboresha na kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo nchini, kwa kutoa elimu kwa umma juu ya uhifadhi na matumizi endelevu ya malikale na maliasili za nchi yetu. (Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO (K.n.y. MHE. MARYAM SALUM MSABAHA) aliuliza:-
Mradi wa TASAF ni mradi wa kusaidia kaya maskini nchini. Je, ni wananchi wangapi ambao wananufaika na mradi huo katika Visiwa vya Pemba na Unguja?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini ulianza rasmi januari 2013. Mpango huu ni wa miaka 10 iliyogawanyika katika vipindi viwili vya miaka mitano mitano na unatekelezwa hadi 2023 katika Halmashauri zote Tanzania Bara na Zanzibar. Jumla ya kaya maskini milioni 1.1 zenye jumla ya watu takribani milioni tano zimeandikishwa katika jumla ya vijiji, mitaa na shehia 9.986.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Zanzibar, Unguja na Pemba kaya zilizonufaika na mpango huu kwa kupatiwa ruzuku na ajira kwa kushiriki kwenye kazi katika miradi ya kutoa ajira ya muda mfupi na vikundi vya kuweka akiba na kuwekeza kwa lengo la kukuza uchumi wa kaya ni 32,262 kutoka katika shehia 168. kati ya idadi hiyo kaya 18,092 ni kutoka Unguja na kaya 14,164 ni kutoka pemba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya shilingi bilioni 32 zimetumika tangu mpango uanze kama ifuatavyo:-
(a) Miradi ya kutoa ajira za muda shilingi 7,240,498,800;
(b) Ruzuku kwa masharti ya elimu na afya ni shilingi 25,24,002,721; na
(c) Vikundi vya kukuza uchumi wa kaya zilizotolewa ni shilingi 464,000,000.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-
Sekta ya Utalii imekuwa ikitoa ajira kwa vijana wetu wa Visiwani na Tanzania Bara; kutetereka kwa sekta hii kumesababisha kupungua kwa ajira kwa kiasi kikubwa na vijana kurudi mitaani;
Je, Serikali ina mpango gani wa kuimarisha na kuboresha sekta hii ili ajira zipatikane kwa wingi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, sekta ya utalii ni miongoni mwa sekta muhimu katika uchumi wa Taifa ambapo sekta hii huchangia zaidi ya asilimia 17 ya Pato la Taifa (GDP) na asilimia 25 ya fedha za kigeni nchini. Sekta hii inatoa ajira nyingi za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja hapa nchini ambapo kwa sasa sekta ya utalii huchangia ajira takriban 1,500,000.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mchango mkubwa wa sekta ya utalii katika kuchangia ajira nchini, Wizara inaendelea na mikakati mbalimbali ya kuongeza fursa za ajira ikihusisha:-
(a) Kupanua wigo wa mazao ya utalii ili kuongeza fursa za ajira kama vile; utalii wa mikutano, utalii wa fukwe, utalii wa matamasha mfano urithi festival, utalii wa miamba (geo-tourism), utalii wa meli, utalii wa reli, mfano TAZARA na Tanga Line, utalii wa michezo, utalii wa matibabu na kadhalika.
(b) Kuhamasisha uwekezaji katika Sekta ya Utalii. Katika kutekeleza hili, Wizara imekamilisha zoezi la kubaini maeneo ya fukwe katika mwambao wa bahari ya Hindi kwa ajili ya uwekezaji wa shughuli za utalii.
(c) Wizara inaendelea kuhamasisha wananchi kuanzisha miradi ya utalii wa utamaduni (Cultural Tourism Programme) ambapo mpaka sasa miradi 66 imeshaanzishwa katika mikoa mbalimbali nchini.
(d) Wizara kupitia Wakala wa Chuo cha Taifa cha Utalii hutoa mafunzo ya kozi za utalii na ukarimu katika ngazi ya astashshada na stashahada. Kozi hizo zimesaidia kupata wahitimu wenye ujuzi unaohitajika katika soko la ajira za sekta ya utalii.
(e) Kuimarisha miundombinu ya usafiri wa anga, nchi kavu na baharini, kuanzisha channel na studio mahsusi kwa ajili ya kutangaza utalii, kuhamasisha wawekezaji kwenye maeneo ya utalii na kuandaa na kutangaza utambulisho wa Taifa (destination branding).
(f) Aidha, Sheria ya Utalii ya mwaka 2008, kifungu cha 58(2), imetenga shughuli mahsusi za biashara ya utalii kwa ajili ya Watanzania. Vile vile, Wizara imepunguza ada ya leseni za biashara ya utalii kwa lengo la kuwawezesha Watanzania wengi kushiriki kufanya shughuli za utalii.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-

Wachimbaji wadogo wadogo wa madini nchini wamekuwa wakipoteza maisha mara kwa mara kwenye mgodi:-

Je, ni lini Serikali itawapatia zana za kisasa pamoja na elimu ya kutosha wachimbaji hao?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum; kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha kwamba uchimbaji wa madini nchini unafuata taratibu za usalama, afya na utunzaji wa mazingira, Serikali imeanzisha Tume ya Madini ambayo ina Ofisi za Afisa Madini Wakaazi (RMO’s) takribani mikoa yote nchini. Vilevile kila eneo lenye shughuli za uchimbaji madini, Wizara imeanzisha Ofisi za Maafisa Migodi Wakaazi kwa lengo la kuimarisha shughuli za utoaji elimu kwa wachimbaji wadogo, ukaguzi wa migodi na ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wachimbaji wengi katika migodi ya wachimbaji wadogo wamekuwa hawazingatii tahadhari za usalama wakati wa shughuli za za uchimbaji. Serikali itazidi kuweka msisitizo kwa wachimbaji wadogo kuzingatia Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na marekebisho yake ya mwaka 2017 na Kanuni zake za Usalama, Afya na Utunzaji wa Mazingira wakati wa uchimbaji. Aidha, Serikali haitasita kuyafunga maeneo yatakayobainika kuwa ni hatarishi na yanakiuka kanuni za usalama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Madini ilikuwa ikitoa ruzuku kwa wachimbaji wadogo wa madini. Hata hivyo, ilibainika kuwa baadhi ya wachimbaji waliopatiwa ruzuku walitumia ruzuku hiyo kinyume cha maelekezo na makubaliano. Serikali inaanglia utaratibu mzuri wa kuwasaidia wachimbaji wadogo, ikiwa ni pamoja na kuzishawishi taasisi za fedha kuwakopesha wachimbaji wadogo. Wachimbaji wadogo wanashauriwa kutunza kumbukumbu za uzalishaji na mauzo ya madini ili kuzishawishi taasisi za fedha kuweza kuwakopesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-

Kumekuwa na baadhi ya Askari wa barabarani wanaosimamisha magari hasa yale ya safari ndefu wakitokea vichakani (kujificha) na hatimaye wakati mwingine kusababisha ajali:-

Je, ni Askari wangapi kama hawa wameshachukuliwa hatua za kinidhamu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi nchini chini ya Sheria ya Usalama Barabarani Sura 168 iliyorejewa mwaka 2002, inamtaka Askari wa Polisi kuhakikisha usalama wa watumiaji wote wa barabara. Katika kutekeleza hilo, Polisi wanatumia mbinu mbalimbali kwa mujibu wa sheria na taratibu ambazo zinawaongoza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge lako Tukufu litakumbuka kuwa wakati Serikali ya Awamu ya Tano inaingia madarakani kulikuwa na mfululizo wa ajali nyingi barabarani hususan zile ambazo zinahusisha magari ya abiria. Kwa kuzingatia hilo, Baraza la Usalama Barabarani lilibuni mkakati maalum uliofanikisha kupunguza ajali kwa asilimia 43 mpaka sasa. Mkakati huu ulihusisha mbinu mbalimbali zenye lengo la kuwalazimisha madereva kufuata sheria za usalama barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haina ushahidi wa matukio ya askari waliowahi kusababisha ajali barabarani kwa sababu ya kujificha. Hata hivyo, Serikali kupitia Baraza la Taifa la Usalama Barabarani limejiwekea utaratibu wa kufanya uchunguzi wa kina kwa kila ajali kubwa inayotokea na kuchukua hatua stahiki inapobainika kuna uzembe wa usimamizi wa sheria au uvunjifu wa Sheria za Usalama Barabarani.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-

Kumekuwa na matukio ya mara kwa mara ya watoto wachanga kutupwa majalalani, mitaroni na katika mifuko ya rambo:-

(a) Je, nini kauli ya Serikali kuhusu matukio hayo?

(b) Je, ni watuhumiwa wangapi walishakamatwa na kuchukuliwa hatua za kisheria?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, vitendo vya kutupa watoto majalalani, mitaroni na maeneo mengine ni kinyume na sheria za nchi na haki za binadamu. Kwa mujibu wa Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16 kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002 chini ya kifungu cha 218 na 219, adhabu ya makosa hayo ni kifungo cha maisha. Aidha, Serikali inalaani vikali vitendo hivyo na itaendelea kuchukua hatua kali dhidi ya wale watakaopatikana na hatia.

Mheshimiwa Naibu Spika, takwimu za matukio ya kutupa watoto wachanga zinaonesha kuwa katika kipindi cha mwezi Januari hadi Juni, 2019 kumekuwa na jumla ya matukio 66 ya watoto waliopatikana wakiwa wametupwa, 43 kati yao waliokutwa hai na 23 walikutwa wamefariki. Aidha, watuhumiwa 18 walikamatwa na kufikishwa mahakamani na kesi zao zipo katika hatua mbalimbali.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-

Shirika la Mzinga limekuwa likifanya kazi zake kwa weledi na uaminifu mkubwa lakini lina changamoto za vifaa kama vile mashine za ramani:-

Je, kwa mwaka 2019/2020 Serikali ilitenga kiasi gani cha fedha kwa ajili ya Shirika hilo?
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mwaka wa Fedha 2019/2020, Shirika la Mzinga limetengewa jumla ya shilingi 2,000,000,000.00 kwa ajili ya kutekeleza Miradi ya Maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha shirika linatekeleza majukumu yake kwa ufanisi, shirika limeanza kutekeleza Mpango Mkakati wa Miaka Mitano (2017/2018 – 2021/2022) ambao unakusudia kupanua wigo wa uzalishaji wa mazao ya kijeshi. Aidha, shirika limepanga kuanzisha kiwanda cha kutengeneza baruti kwa ajili ya matumizi yasiyo ya kivita (civil explosives) na kupanua mradi wa kutengeneza mashine ndogo ndogo zitakazowezesha wajasiriamali kuongeza thamani ya mazao ya kilimo na misitu.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-

Kuna baadhi ya Bar na Club ambazo zimejengwa kwenye makazi ya watu ambazo zimekuwa kero kwa jamii:-

Je, ni nini kauli ya Serikali kuhusu Bar na Club hizo ambazo zinakiuka sheria na maadili ya jamii?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba biashara nyingi, zikiwemo za uendeshaji wa bar na club zipo kwenye maeneo ya makazi ya watu. Serikali inawaelekeza wamiliki wote wa bar na club kuwa wanapaswa kuzingatia maelekezo ya Sheria ya Vileo Sura Na. 28 ya mwaka 1968, kifungu cha 14(1) katika uendeshaji wa shughuli zao. Aidha, Serikali haitasita kuchukua hatua kwa vitendo vyovyote vitakavyobainika kukiuka sheria na kusababisha kero kwa wananchi wengine.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-

Kumekuwa na kero kubwa sana kwa abiria wanaotumia bandari kwenda Zanzibar kwa boti ambapo hulipishwa ushuru wa bandari kwa mizigo hata boksi la kilo kumi tu au mchele kilo 20 kwa malipo ya shilingi 9,750.

Je, ni mizigo gani ambayo abiria anapaswa kulipia ushiri huo wa bandari (Wharfage)?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kufuatana na mwongozo wa tozo (tariff book) kifungu kifungu 29 wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA), tozo ya wharfage inatozwa inatozwa kwa mizigo ya biashara yenye uzito zaidi ya kilo 21 na yenye zaidi ya mita moja ya ujazo inayopita kwenye gati, jeti na maboya yaliyo chini ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA).

Mheshimiwa Spika, TPA haikusanyi tozo yoyote kwa abiria ambao wana vifurushi binafsi (personal effects) vyenye uzito au ujazo mdogo chini ya kilo 21 au mita moja ya ujazo wanaotumia bandari kwenda Zanzibar kwa boti kwenye eneo la baggage room. Aidha, abiria wanaotumia bandari kwenda Zanzibar kwa boti ambao hutozwa ushuru wa bandari katika eneo la baggage room ni wale tu wanaokuwa na mizigo mikubwa tena kwa madhumuni ya kibiashara.

Mheshimiwa Spika, TPA inapenda kuwasisitiza wateja/ abiria wote wenye mizigo ya kibiashara kwenda au kutoka Zanzibar kutumia eneo la Azam Sea Link lililotengwa kwa ajili ya shughuli za kibiashara ili kuondokana na usumbufu kwenye eneo la baggage room ambalo limetengwa mahsusi kwa ajili ya abiria wenye mizigo yao binafsi (personal effects).

Mheshimiwa Spika, tunapenda kutoa wito kwa wateja wetu wote wanaotumia bandari kwenda Zanzibar kwa boti wahakikishe kuwa mizigo yao inapimwa kabla ya kupakiwa ili wajue kama uzito wake unastahiki kutozwa ushuru wa bandari au la, kuepuka usumbufu unaoweza kujitokeza.