Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Rhoda Edward Kunchela (11 total)

MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA (K.n.y. MHE. RHODA E. KUNCHELA) aliuliza:-
Kumekuwa na sintofahamu katika eneo la Kata ya Misunkumilo, Wilaya ya Mpanda Mjini, Wanajeshi wanadai eneo hilo ni la Jeshi, lakini makazi ya wananchi yalitangulia na wana hati ya maeneo yao:-
Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kutatua jambo hili ikiwa Jeshi limewakuta wananchi katika eneo hili?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na sababu za kistratejia, JWTZ lilipewa eneo la Misunkumilo lililopo Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda mwaka 1985 lenye ukubwa wa hekta 3195. Serikali ililipa fidia kwa wananchi waliokuwepo katika eneo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 1992 Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania lilihamisha kombania yake kutoka katika eneo hilo ila eneo alikabidhiwa Mkuu wa Wilaya kwa uangalizi. Kutokana na sababu za kiusalama hasa ukanda wa Ziwa Tanganyika, imebidi Jeshi lirejee kwenye sehemu hiyo tena. Hata hivyo, sehemu ya eneo hili sasa limevamiwa na kupangiwa matumizi mengine na uongozi wa Manispaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe 16 Novemba, 2015 kilifanyika kikao cha pamoja kati ya JWTZ na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Katavi. Maamuzi yaliyofikiwa katika kikao hicho ni kulipima upya eneo hilo kwa kuzingatia maendeleo yaliyopo, lakini vile vile na mahitaji ya JWTZ.
Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi eneo hili litapungua kutoka ekari 3,195 za awali hadi 2,235. Zoezi la kupima upya litakuwa shirikishi na litatekelezwa mara fedha zitakapopatikana katika mwaka wa fedha wa 2016/2017.
MHE. DEVOTHA M. MINJA (K.n.y MHE. RHODA E. KUNCHELA) aliuliza:-
Tatizo la umeme katika Mkoa wa Katavi hususan Wilaya ya Mpanda Mjini limekuwa kero kwa wananchi; tatizo hili linafanya maendeleo kuwa duni katika Manispaa ya Mpanda:-
(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuachana na matumizi ya jenereta ambalo ni bovu linalosababisha ukosefu wa umeme kila mara?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua kero hii ya umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kutekeleza ujenzi wa Mradi wa Umeme wa Gridi ya Taifa inayounganisha Mikoa ya Rukwa, Katavi pamoja na Kigoma. Ujenzi wa mradi huo utasaidia mikoa hiyo kuondokana na matumizi ya mitambo ya mafuta pia na gharama kubwa. Kwa maana hiyo ujenzi huo unahusisha njia ya umeme msongo wa kilovolti 400; ambao pia ambao pia wameanza kuunganisha katika mikoa Mbeya - Sumbawanga - Mpanda - Kigoma hadi Nyakanzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kuhuisha upembuzi yakinifu wa mradi kutoka kilovoti 220 za awali na kuwa kilovolti 400 zinazoendelea hivi sasa inaendelea. Awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mradi (Mbeya - Sumbawanga) itakamilika mwaka, 2018 na awamu zote tatu za mradi zinatarajiwa kukamilika mwaka 2022; gharama za mradi huu zinakadiriwa kuwa dola za Marekani milioni 664.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu utakapokamilika utaupatia umeme wa uhakika Mji wa Mpanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa ujenzi wa umeme wa Gridi ya Taifa unaendelea, Serikali kupitia TANESCO imeanza ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme kwa kutumia jenereta mbili zenye uwezo wa kuzalisha umeme wa megawati 1.25; kila moja katika Mji wa Mpanda kupitia mradi wa ORIO. Mradi huu unafadhiliwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania na Uholanzi kwa gharama ya shilingi bilioni 12.21. Kazi za ujenzi wa kituo hicho zimeanza mwezi Oktoba, 2016 na zitakamilika mwezi Julai, 2017.
MHE. RHODA E. KUNCHELA aliuliza:-
Ipo changamoto kubwa ya ukosefu wa ajira kwa vijana wa Mkoa wa Katavi. Na hii ni kutokana na miundombinu mibovu inayosababisha wawekezaji kushindwa kuwekeza.
Je, Serikali ina mikakati gani ya kusaidia vijana hao wapate ajira na kuwa na mazingira ya kuwawezesha kujikwamua kiuchumi?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, mikakati ya Serikali kusaidia vijana
wa Katavi pamoja na maeneo mengine kupata ajira na kuwa na mazingira wezeshi ya kujikwamua kiuchumi ni kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwanza ni kuzielekeza Mamlaka
za Serikali za Mitaa kuzingatia masuala ya ukuzaji ajira katika mipango ya maendeleo, hususan kutambua na kubaini mahitaji ya nguvu kazi katika maeneo husika. Kutenga na kuendeleza maeneo ya uzalishaji wa biashara kwa vijana, kuwezesha nguvu kazi kuwa na ujuzi wa kujiajiri, kuwezesha upatikanaji wa mitaji na vitendea kazi kwa makundi ya vijana, kukuza soko la bidhaa na huduma za wajasiriamali hasa vijana.
Mheshimiwa Spika, pili, kutekeleza programu ya miaka mitano ya kukuza ujuzi inayolenga kuwawezesha vijana takribani 4,419,074 kupata ujuzi wa kuajiriwa au kujiajiri katika sekta mbalimbali. Aidha, kwa mwaka wa fedha 2016/2017 vijana 1,469 wamepatiwa mafunzo ya ushonaji wa nguo kupitia viwanda vya Mazava Fabrics na Took Garment. Vijana 3,900 wametambuliwa na watapata mafunzo ya kurasimisha ujuzi wao kupitia VETA. Vijana 100 kati ya 1,001 wameanza mafunzo ya ujuzi kwa kutengeneza bidhaa za ngozi katika Chuo cha DIT, Mwanza.
Mheshimiwa Spika, tatu ni kuandaa na kuana kutekeleza Mkakati wa Kitaifa wa Kukuza Ajira kwa Vijana katika Sekta ya Kilimo (National Strategy for Youth Involvement in Agriculture) ambao unaweka mazingira wezeshi ya kuvutia vijana kujishughulisha na kilimo kwa kuwezesha upatikanaji wa ardhi, mitaji, pembejeo za kilimo, masoko, mafunzo ya ujuzi wa kilimo na ujasiriamali.
Mheshimiwa Spika, mikakati hiyo itasaidia pia kushirikisha vijana wote wa Tanzania, wakiwemo vijana wa Katavi kupata mazingira wezeshi ya kujikwamua kiuchumi. Aidha, Serikali itaendelea kuwekeza katika miundombinu ya barabara inayounganisha mikoa yote nchini ikiwemo Mkoa wa Katavi kwa lengo la kuchochea uwekezaji na kukuza fursa za ajira nchini.
MHE. RHODA E. KUNCHELA aliuliza:-
Pamoja na lengo la Serikali kuhakikisha Manispaa zinakuwa safi na kuzuia magonjwa ya mlipuko, Manispaa ya Mpanda ina changamoto ya ukosefu wa vifaa kama magari ya taka.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha Manispaa zinakuwa safi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Manispaa ya Mpanda ina maroli mawili kati ya manne yanayohitajika kwa ajili ya kuzolea taka ngumu. Kutokana na changamoto hiyo, uongozi wa Manispaa umejiwekea mikakati ifuatayo:-
(i) Manispaa ya Mpanda imebinafsisha (outsource) shughuli ya uzoaji na udhibiti wa taka kwa mzabuni anayelipwa kupitia mapato ya ndani ya Halmashauri, mMzabuni huyu ana magari mawili na hivyo kufanya jumla ya magari kuwa manne.
(ii) Manispaa ya Mpanda imeanzisha mpango shirikishi jamii wenye jumla ya vikundi vya uzoaji na udhibiti wa taka ngumu katika mitaa 17, vimejengwa vizimba vitano kwa ajili ya kuhifadhia taka na vitakabidhiwa mikokoteni 17 tarehe 21/06/2017 siku ya uzinduzi.
(iii) Kila siku ya Jumamosi kuanzia saa 1:00 asubuhi hadi saa 4:00 asubuhi wananchi wote hushiriki kufanya usafi katika maeneo ya makazi, biashara na maeneo mbalimbali ya kufanyia kazi.
(iv) Kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi kuanzia saa 1:00 asubuhi hadi saa 4:00 asubuhi usafi wa kina hufanyika ambapo wananchi pamoja na viongozi mbalimbali hushiriki kufanya usafi katika maeneo yao.
(v) Siku hiyo ya Ijumaa kuanzia saa 1:30 asubuhi hadi saa 3:30 asubuhi watumishi wa Manispaa hushiriki kufanya usafi katika maeneo ya Ofisi ya Manispaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuhamasisha usafi nchini ili kuepuka mlipuko wa magonjwa na kuongeza unadhifu wa miji yetu.
MHE. RHODA E. KUNCHELA aliuliza:-
Ujenzi wa reli ya kati ni hatua inayochukuliwa kuboresha miundombinu katika nchi hii.
Je, Serikali inawasaidiaje wananchi wanaokumbwa na bomoabomoa kupata fidia zao kwa wakati hasa ukizingatia kuwa wananchi wengi ni maskini na hawawezi kumudu gharama za kujenga makazi upya?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kuendeleza mtandao mzima wa reli kwa kiwango cha kimataifa (standard gauge) ukiwa na jumla ya urefu wa kilometa 4,886. Mtandao huu wa reli unajumuisha Ukanda wa Kati ambao una kilometa 2,561 amabao unajumuisha reli ya kutoka Dar es Salam - Isaka – Mwanza (kilometa 1,219), Tabora – Uvinza – Kigoma (kilometa 411), Kaliua – Mpanda – Karema (kilometa 321), Isaka – Rusumo (kilometa 371), Keza – Ruvubu (kilometa 36) na Uvinza – Kalelema kuelekea Msongati (kilometa 203). Ukanda wa Kusini ambao unajumuisha reli ya kutoka Mtwara hadi Mbamba Bay na matawi yake ya kuelekea Liganga kwa ajili ya chuma na Mchuchuma kwa ajili ya makaa ya mawe yenye jumla ya urefu wa (kilometa 1,092) na Ukanda wa Kaskazini ambao unajumuisha reli kutoka Tanga – Arusha – Musoma yenye jumla ya urefu wa kilometa 1,233.
Mheshimiwa Spika, inakadiriwa kuwa asilimia 75 ya njia ya reli mpya itapita katika hifadhi ya reli iliyopo. Wananchi waliopo katika hifadhi ya reli wanapaswa kuondolewa bila kulipwa fidia kwani wamevamia maeneo ya reli. Aidha, zoezi la ubomoaji linaloendelea sasa linalenga kuwaondoa wavamizi wa hifadhi ya reli na maeneo ya uendeshaji yaliyotengwa tangu reli ya kwanza ilipoanza kujengwa kati ya mwaka 1904 na kuendelea.
Mheshimiwa Spika, mpaka sasa hakuna mgogoro wala athari zilizojitokeza katika utwaaji ardhi mpya ili kupisha mradi wa reli ya kisasa kwa sababu usanifu utakaoonyesha wananchi watakaopitiwa unakamilishwa.
Aidha, Kampuni Hodhi ya Rasilimali za Reli (RAHCO) imeajiri Mshauri Mwelekezi kutoka Chuo Kikuu cha Ardhi kwa ajili ya kufanya kazi ya utwaaji wa ardhi na tathmini kwa wananchi watakaolazimika kupisha reli hiyo. Ushirikishwaji wananchi, sheria na taratibu zote za nchi zitafuatwa ipasavyo katika kutekeleza zoezi la fidia, ahsante.
MHE. RHODA E. KUNCHELA aliuliza:-
Pamoja na lengo la Serikali kuhakikisha Manispaa zinakuwa safi na kuzuia magonjwa ya mlipuko, Manispaa ya Mpanda ina changamoto ya ukosefu wa vifaa kama
magari ya taka.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha Manispaa zinakuwa safi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Manispaa ya Mpanda ina maroli mawili kati ya manne yanayohitajika kwa ajili ya kuzolea taka ngumu. Kutokana na changamoto hiyo, uongozi wa Manispaa umejiwekea mikakati ifuatayo:-
(a) Manispaa ya Mpanda imebinafsisha (outsource) shughuli ya uzoaji na udhibiti wa taka kwa mzabuni anayelipwa kupitia mapato ya ndani ya Halmashauri, mMzabuni huyu ana magari mawili na hivyo kufanya jumla ya magari kuwa manne.
(b) Manispaa ya Mpanda imeanzisha mpango shirikishi jamii wenye jumla ya vikundi vya uzoaji na udhibiti wa taka ngumu katika mitaa 17, vimejengwa vizimba vitano kwa ajili ya kuhifadhia taka na vitakabidhiwa mikokoteni 17 tarehe 21/06/2017 siku ya uzinduzi.
(c) Kila siku ya Jumamosi kuanzia saa 1:00 asubuhi hadi saa 4:00 asubuhi wananchi wote hushiriki kufanya usafi katika maeneo ya makazi, biashara na maeneo mbalimbali ya kufanyia kazi.
(d) Kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi kuanzia saa 1:00 asubuhi hadi saa 4:00 asubuhi usafi wa kina hufanyika ambapo wananchi pamoja na viongozi mbalimbali hushiriki kufanya usafi katika maeneo yao.
(e) Siku hiyo ya Ijumaa kuanzia saa 1:30 asubuhi hadi saa 3:30 asubuhi watumishi wa Manispaa hushiriki kufanya usafi katika maeneo ya Ofisi ya Manispaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuhamasisha usafi nchini ili kuepuka mlipuko wa magonjwa na kuongeza unadhifu wa miji yetu.
MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y RHODA E. KUNCHELA) aliuliza:-
Kuna mgogoro kati ya Manispaa na wafanyabiashara wanaomiliki vibanda katika masoko ya Buzogwe Soko Kuu na Mpanda Hoteli ambapo Manispaa inawaongezea kodi wafanyabiashara hao bila makubaliano ya pande zote mbili:-
Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kumaliza mgogoro huo maana ni muda mrefu sasa na wafanyabiashara wamefunga vibanda vyao wakisubiri muafaka na hivyo Serikali kushindwa kukusanya kodi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Halmashari ya Manispaa ya Mpanda imejenga vibanda vya biashara katika masoko kwa ubia baina ya Halmashauri na wafanyabiashara (wamiliki/ wajenzi). Masoko ambayo yaliongezewa ushuru wa pango ni masoko yanayomilikiwa na Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda ambayo ni soko kuu la Buzogwe na Azimio.
Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda iliamua kufanya mabadiliko ya ushuru baada ya kubaini kuwa wamiliki/wajenzi walikuwa wakinijufaisha wenyewe kwa kuwapangisha wafanyabiashara na kuwatoza kodi kati ya Sh.100,000 hadi Sh.150,000 na kuwasilisha kodi ya Sh.15,000 tu kwa mwezi kwa Halmashauri.
Mheshimiwa Spika, mabadiliko ya kodi yaliyofanyika kwa wamiliki/wajenzi ni kutoka Sh.15,000 hadi Sh.40,000 kwa mwezi. Wadau wote walishirikishwa na makubaliano yaliridhiwa katika vikao vya kisheria vya Halmashauri. Aidha, hakuna maduka yaliyofungwa, huduma zinaendelea kama kawaida na Halmashauri imeendelea kukusanya mapato.
Mheshimiwa Spika, Halmashauri zinaweza kufanya marekebisho ya kodi wakati wowote. Utaratibu unaotumika katika kuibua na kuongeza kodi/tozo huanzishwa, huchakatwa na kuamuliwa na kikao cha Kamati ya Fedha, Uchumi na Mipango ya Halmashauri husika.
MHE. RHODA E. KUNCHELA aliuliza:-
a) Je, ni lini Serikali itatatua mgogoro wa ardhi kati ya Hifadhi na wananchi katika Kata ya Kapalamsenga, Isengule na Ikola?
b) Kwa kuwa migogoro hiyo imechukua muda mrefu bila suluhu hivyo kusababisha usumbufu na hasara kwa wananchi; Je, Serikali haioni kuwa migogoro hiyo imesababisha umaskini mkubwa kwa wananchi kushindwa kuendeleza shughuli za kiuchumi kwenye maeneno yao hivyo ifanye haraka kutafuta ufumbuzi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Kapalamsenga, Isengule na Ikola zipo katika Wilaya ya Tanganyika na zinajumuisha maeneo ya ushoroba wa wanyamapori ujulikanayo kama Katavi – Mahale. Ushoroba huu ni njia kuu ya wanyamapori kutoka Hifadhi ya Taifa Katavi kwenda Hifadhi ya Taifa Mahale. Kutokana na wanyamapori hususani tembo kupita katika maeneo hayo, wenyeji wanautambua ushoroba husika kama “Tembo na Mwana.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na ushoroba huu kufahamika kwa baadhi ya wananchi kulikuwa na mkanganyiko kuhusu eneo sahihi la (mipaka), yaani mipaka ya mapito ya wanyamapori na hii inatokana na baadhi ya wananchi na hasa wahamiaji na wafugaji kutoka mikoa ya jirani, kuvamia na kuharibu maeneo ya mapito ya wanyamapori bila kufuata taratibu na kujichukulia ardhi kiholela.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutafuta ufumbuzi wa migongano hii iliyopo juu ya matumizi ya ardhi, Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika ilichukua hatua mbalimbali kama ifuatavyo:-
• Kuhakikisha kuwa mipaka ya ushoroba inajulikana kwa wananchi kwa kutenga na kuainisha maeneo kwa ajili ya uhifadhi wa wanyamapori kama vile Sokwe. Sokwe hao wanapatikana katika Kata za Kapalamsenga, Ikola, Isengule, Mwese na Kasekese hasa katika safu za milima ya Mwansisi na Mgengebe.
• Kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi ya vijiji na kutunga sheria ndogo za usimamizi wake kwa mwaka wa fedha 2015/2016 na 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa vijiji vyote vilivyopo katika Kata ya Kapalamsenga, Ikola na Isengule vimeshafanyiwa mpango shirikishi wa matumizi bora ya ardhi. Pia, eneo la ushoroba wa wanyamapori limebainishwa na kutengwa hivyo kuondoa mkanganyiko uliokuwepo awali. Aidha, kwa kutumia Kanuni ya usimamizi wa shoroba na maeneo ya mtawanyiko zimeshaandaliwa (GN 123 ya mwaka 2018).
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mpango wa kutafuta suluhu ya kudumu kwa wananchi katika vijiji vyote vinavyopitiwa na shoroba za wanyamapori, vinavyopakana na maeneo ya hifadhi na vyanzo vya maji ili kuondoa migongano inayohusiana na umiliki wa matumizi ya ardhi. Hivyo, tunawaomba wananchi wote kuheshimu mipaka ya matumizi bora ya ardhi pamoja na kanuni mpya za ushoroba.
MHE. RHODA E. KUNCHELA aliuliza:-

Serikali iliahidi kumaliza migogoro ya ardhi kwa kupima maeneo ya wananchi mapema ili kuepuka bomoa bomoa bila fidia:-

Je, ni lini jambo hilo litafikia mwisho?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba kila kipande cha ardhi nchini kinatambuliwa, kinapangwa na kinapimwa. Katika kutekeleza azma hiyo, Wizara imenunua vifaa vya kisasa vya upimaji ambavyo vimesambazwa katika kanda zote nane na vinatumiwa na Hamashauri zote ili kurahisisha na kuharakisha upimaji wa maeneo ya wananchi na kutoa hatimiliki za ardhi. Vile vile Wizara inaendelea na utekelezaji wa mkakati wa kupima kila kipande cha ardhi nchini ambapo awamu ya kwanza ya mkakati huu inatekelezwa kupitia Mradi wa Majaribio wa Kuwezesha Umiliki wa Ardhi (Land Tenure Support Programme) unaotekelezwa katika Wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi katika Mkoa wa Morogoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imetoa kiasi cha shilingi 6,400,000,000 kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa 25 kwa ajili ya kupima, kupanga na kumilikisha ardhi. Halmashauri hizo ni Halmashauri ya Jiji la Mbeya, Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela, Halmashauri ya Sumbawanga, Manispaa ya Shinyanga na Iringa, Halmashauri za Miji ya Makambako, Njombe, Kondoa, Nzega, Kahama, Bariadi na Halmashauri za WIlaya za Misungwi, Sengerema, Geita, Nzega, Bukombe, Magu, Chato, Ukerewe, Busega, Simanjiro, Gairo, Songea, Namtumbo na Itilima. Serikali inaendelea kutafuta fedha katika vyanzo mbalimbali ili jambo hili lifikie mwisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na utekelezaji wa kupima kila kipande cha ardhi nchini, Wizara imeendelea na utekelezaji wa Programu ya Kurasimisha Makazi yasiyopangwa katika maeneo mbalimbali nchini kwa kushirikiana na makampuni binafsi ya kupanga na kupima ardhi yaliyosajiliwa kwa mujibu wa sheria. Lengo la Serikali ni kuhakikisha maeneo yote yanapangwa na kupimwa ili kukidhi mahitahi ya sasa na ya baadaye na hivyo kuzuia uendelezaji holela ambapo husababisha migogoro na adha kwa wananchi ikiwemo bomoa bomoa ya makazi yasiyo rasmi.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA (K.n.y. MHE. RHODA E. KUNCHELA) aliuliza:-

Ujenzi wa Chuo Kikuu cha Kilimo Mkoa wa Katavi ni jambo ambalo linaleta sintofahamu kwa maana ya umiliki wa eneo (Hati) na ujenzi wa Chuo ambao ni miaka sasa bado hakijajengwa na kusababisha jambo hili kuleta usumbufu kwa wanafunzi kwenda Mikoa mingine kutafuta vyuo vya kilimo:-

Je, Serikali ipo tayari kuondoa sintofahamu hii ya ujenzi wa Chuo hicho cha Kilimo?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inatambua kuwa ujenzi wa Chuo Kikuu cha Kilimo Katavi lilikuwa ni wazo la Halmashauri ya Mji wa Mpanda. Halmashauri iliingia makubaliano na Chuo cha Royal Agricultural University cha Uingereza kwa ajili ya utekelezaji wa azma hiyo.

Mheshimiwa Spika, mnamo mwaka 2013 Halmashauri ya Mji Mpanda ilileta ombi la kukabidhi mradi huo kwa Wizara na walielekezwa kuwasilisha taarifa rasmi ya maendeleo ya mradi kwa ajili ya hatua stahiki. Hadi sasa Wizara haijapokea taarifa hiyo. Aidha, umiliki wa eneo hilo la chuo bado uko chini ya Halmashauri ya Mji Mpanda.
MHE. RHODA E. KUNCHELA aliuliza:-

Sekta ya Madini inaongeza pato kubwa katika uchumi wa nchi.

Je, Serikali iko tayari kutatua kero kwa wachimbaji wadogo na vibarua ambao wananyanyasika katika migodi mbalimbali hapa nchini?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Wizara kupitia Tume ya Madini imeendelea kuweka mikakati ya kuwatambua wachimbaji wadogo kwa kuwapatia leseni za uchimbaji. Aidha, Wizara ya Madini imeendelea kuhamasisha watanzania kote nchini kujiunga latika vikundi kwa mujibu wa sheria ya vyama vya ushirika, ili waweze kupatiwa elimu kiurahisi kuhusu uchimbaji salama, utunzaji wa kumbukumbu na uzalishaji na namna ya kupata mikopo kwa riba nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wizara imedhamilia kuondoa kero za wachimbaji wadogo hasa za maeneo ya kuchimba ili kuwawezesha kujiajiri katika sekta ya madini. Aidha, nimeagiza Tume ya Madini kuhakikisha wamiliki wote wa leseni za utafiti ambazo hazifanyiwi kazi zifutwe ili maeneo hayo yamilikishwe wachimbaji wadogo wenye lengo la kuviendeleza ili kuongeza mchango kwa sekta ya madini katika pato la Taifa na kujenga uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, migodi yote hapa nchini, inaendeshwa kwa mujibu wa Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 na marekebisho yake ya Mwaka 2017 na kuzingatia kanuni za uchimbaji salama, mazingira na afya kwa wafanyakazi. Suala la unyanyasaji wa aina yoyote halikubaliki na mmiliki anayefanya hivyo atakuwa anavunja Sheria ya Madini na Sheria za Kazi Mahali pa Kazi. Aidha, natoa wito, kwa yeyote mwenye malalamiko ya msingi kutoa taarifa kupita ofisi za madini zilizoko mikoani mwao ili yaweze kushughulikiwa kwa mujibu wa sheria.