Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Susan Anselm Jerome Lyimo (1 total)

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi, nchi yetu takribani asilimia 70 ya wananchi wake wanategemea kilimo na Mheshimiwa Waziri Mkuu kilimo hiki kimekuwa na matatizo makubwa kutokana na mabadiliko ya tabianchi. Hivyo basi kilimo cha umwagiliaji kimeonekana ndiyo chenye tija na chenye uhakika wa chakula lakini Mheshimiwa Waziri Mkuu utakubaliana nami kwamba kilimo hiki bado hakijapewa kipaumbele na hasa ukizingatia sasa hivi kuna maeneo mengi sana yana njaa hata Dodoma mazao yamekauka na maeneo mengine mengi.

Nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba kilimo cha umwagiliaji sasa kinapewa kipaumbele ili tuwe na uhakika wa chakula lakini vilevile viwanda vyetu viweze kupata hiyo malighafi? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Susan Lyimo, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nataka nikiri kama ulivyosema kwamba hatujaona tija ya kilimo cha umwagiliaji nchini. Serikali hilo imeliona na mwenyewe nimechukua hatua wiki moja iliyopita, tumeivunja Tume ya Umwagiliaji yote, kwanini tumeivunja? Ni kwa sababu kilimo chetu nchini ambacho kinategemea sana mvua na Serikali ilipopanga kuboresha kilimo na kuongeza uzalishaji kwa kuwa na Sekta ya Umwagiliaji, tumegundua kwamba mpaka leo hii Taifa haliwezi kuringia usalama wa chakula nchini kutegemea umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, kwanza tumeiondoa Tume ya Umwagiliaji kutoka Wizara ya Maji ambayo Wizara ya Maji yenyewe inashughulikia zaidi kwa Watanzania na kuihamishia Kilimo ili napo sasa iweze kusimamia vizuri Sekta ya Umwagiliaji kwa mipango waliyonayo ya uzalishaji wa chakula nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbili, tumegundua fedha yote tunayoipeleka pale kwa ajili ya kutengeneza miradi ya maji haijafanya kazi yake, miradi mingi ya umwagiliaji haijaleta tija, hiyo ndiyo imetusababisha tumevunja tume. Tumepitia tumegundua tuna hasara, tayari tumepeleka timu ya kuchunguza; wakurugenzi sita tumewasimamisha, watendaji 25 tumewahamisha na sasa tunaijenga upya tume ile ili iweze kuleta tija kwa maelekezo mapya kabisa ya Serikali chini ya usimamizi wa Wizara ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka niwahakikishie Watanzia kwamba miradi yetu yote iliyopo huko ambayo inasuasua, itaratibiwa upya na timu mpya inayoundwa sasa na Waziri atakuja kutangaza tume na bodi muda mfupi ujao ili ianze kusimamia miradi yote iliyopo nchini. Na sasa ile structure ya utawala wa Tume ya Umwagiliaji ilikuwa wanaishia kwenye kanda, tumetoa utaratibu mpya waende mpaka wilayani. Tutakuwa na Afisa wa Umwagiliaji Mkoani, atakayekuwa anasimamia wilaya zote zenye miradi lakini tutakuwa na Afisa wa Umwagiliaji kila halmashauri asimamie mradi uliopo kwenye halmashauri badala ya kuishia kanda ambako walikuwa hawana uwezo wa kutembelea kwenye wilaya zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, marekebisho haya, yanakuja kuleta tija sasa ya umwagiliaji nchini na tutasimamia kikamilifu kuhakikisha kwamba mabadiliko haya yanaleta tija kwa Watanzania, ahsante sana. (Makofi)