Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Suzana Chogisasi Mgonukulima (8 total)

MHE. SUZANA C. MGONOKULIMA aliuliza:-
Je, Serikali imeshalipa stahiki za wastaafu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki iliyovunjika?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Suzana, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeshalipa stahili za wastaafu wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki iliyovunjika Juni, 1977.
Mheshimiwa Naibu Spika, kati ya 2005 na 2010, Serikali iliwalipa wastaafu 31,519 kati ya wastaafu 31,831 wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Serikali ililipa jumla ya shilingi bilioni 115.3. Wastaafu waliolipwa stahili zao ni wale ambao walijitokeza na kuthibitishwa na waliokuwa waajiri wao yaani mashirika waliyokuwa wakiyafanyia kazi. Aidha, katika kipindi cha 2011 mpaka 2013, Serikali iliendelea kuwalipa wale ambao walikuwa hawajalipwa (on a case by case basis) ambapo wastaafu 269 walilipwa kiasi cha shilingi bilioni 1.58 na kufanya jumla ya wastaafu waliolipwa kufikia 31,788 na kiasi kilicholipwa kufikia shilingi bilioni 116. 88.
Mheshimiwa Naibu Spika, zoezi la kupokea madai mapya lilisitishwa tarehe 13 Desemba, 2013 kwa mujibu wa makubaliano kati ya wawakilishi wa wastaafu wakiwa na Wanasheria wao kwa upande mmoja na Serikali kwa upande mwingine.
MHE. NEEMA W. MGAYA (K.n.y. MHE. SUSAN C. MGONOKULIMA) aliuliza:-
Mfumo wa mashine za EFDs hauchanganui kwa uwazi fedha ipi ni mapato ya kodi na ipi ni faini au ni gharama za uendeshaji:-
Je, ni lini kutakuwepo ushirikishwaji kati ya waandaaji mfumo wa TRA na viongozi wa wafanyabiashara ili kodi inayotozwa iwe halali na isiwe inayoua mitaji ya wafanyabiashara?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Susan Chogisasi Mgonokulima, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo wa matumizi ya mashine za kutunza hesabu za kodi za kielektroniki ulianzishwa kwa lengo la kurahisisha na kuboresha utunzaji wa kumbukumbu za biashara za walipa kodi. Mfumo wa EFD ulianzishwa ili kupata ufumbuzi wa matatizo ya utunzaji kumbukumbu za mauzo na utoaji wa risiti za mauzo zinazoandikwa kwa mkono. Mfumo huu umerahisisha usimamizi na ukadiriaji wa kodi kwa kuwa kumbukumbu zote za mauzo na manunuzi huhifadhiwa na kutunzwa kirahisi kwenye mashine za EFD na taarifa za mauzo ya mlipa kodi hutumwa kwenye saver ya Mamlaka ya Mapato moja kwa moja kwa njia ya mtandao kupitia mashine husika ya EFD kila siku.
Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo wa EFD haukuundwa kwa ajili ya kutoa mchanganuo wa fedha kwa mapato ya kodi, faini au gharama za uendeshaji wa biashara. Mfumo wa EFD ni kwa ajili ya kutunza kumbukumbu sahihi za mauzo na manunuzi ya mfanyabiashara pamoja na kutoa risiti. Mchanganuo wa mapato ya kodi na gharama za uendeshaji hufanywa kwa njia ya kawaida ya kiuhasibu kwa kutumia kumbukumbu za mauzo na manunuzi ya biashara zinazotunzwa katika mashine za EFD.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mamlaka ya Mapato Tanzania ina jukumu la kukadiria, kukusanya na kuhasibu mapato ya Serikali yanayotokana na kodi, ada, na tozo mbalimbali pamoja na kusimamia sheria zote za kodi zilizotungwa na kupitishwa na Bunge lako Tukufu. Aidha, Wizara ya Fedha na Mipango ina utaratibu wa kushirikisha wadau mbalimbali wakati wa maandalizi ya bajeti ambao hutoa michango yao na ushauri kwa kupitia kikosi kazi yaani task force kilicho chini ya Idara ya Sera ambacho kazi yake ni kuchanganua maoni na ushauri uliotolewa na kuainisha mambo muhimu ya kuingiza katika bajeti ya Taifa. Utaratibu huu hutoa fursa kwa viongozi wa wafanyabiashara na wengine kutoa maoni na ushauri ili ufanyiwe kazi na kuingizwa katika mipango ya Serikali. Hakuna kodi inayotozwa kwa nia ya kuua mitaji ya wafanyabiashara wetu, kwani kiwango cha juu cha kodi ya mapato ni asilimia 30 ya mapato baada ya kuondoa gharama za biashara yaani net profit. Pale ambapo mfanyabiashara hakupata faida, hakuna kodi ya mapato itakayotozwa. Hivyo basi, kodi zinazotozwa na Mamlaka ya Mapato ni halali na haziui mitaji ya wafanyabiashara wetu.
MHE. SUZANA C. MGONUKULIMA aliuliza:-
Miradi mingi ya maendeleo inashindwa kumalizika kwa wakati kutokana
na Serikali Kuu kutokuleta fedha za miradi kwa wakati:-
Je, ni lini Serikali itapeleka fedha kwa wakati kwenye Halmashauri ili miradi
ya maendeleo itekelezwe kwa kipindi kilichopangwa?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango,
napenda kujibu swali la Mheshimiwa Suzana Chogisasi Mgonukulima, Mbunge
wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa
kutumia fedha za makusanyo ya ndani, mikopo ya ndani na nje, misaada kutoka kwa washirika wa maendeleo pamoja na makusanyo ya Mamlaka ya Serikali za
Mitaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, mapato ya fedha za ndani (tax revenues and
non tax revenues) hupelekwa katika Wizara, taasisi na idara mbalimbali za Serikali
pamoja na Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa ajili ya
utekelezaji wa miradi ya maendeleo kulingana na upatikanaji wa fedha kutoka
katika kila chanzo. Aidha, asilimia 60 ya makusanyo ya Mamlaka ya Serikali za
Mitaa hubakishwa katika Halmashauri husika kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya
maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa miradi inayotekelezwa kwa kutumia fedha
za mikopo ya ndani au nje, pamoja na fedha za washirika wa maendeleo, fedha
hizo hupelekwa kwenye Halmashauri zetu mara tu zinapopatikana. Hivyo basi,
uhakika wa mtiririko wa fedha kutoka vyanzo vyote vya mapato ndiyo msingi wa
kupeleka fedha kwenye Halmashauri zetu kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya
maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni wajibu wetu Waheshimiwa Wabunge
kushirikiana na Waheshimiwa Madiwani katika Halmashauri zetu kupanga
mipango stahiki, kuainisha vyanzo vya mapato na kusimamia ukusanyaji na
matumizi ya mapato hayo ipasavyo ili kuziwezesha Halmashauri zetu kujenga
uwezo wa kifedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo na hivyo
kupunguza utegemezi kutoka Serikali Kuu.
MHE. GODFREY W. MGIMWA (K. n. y. MHE. SUZANA C. MGONOKULIMA) aliuliza:-
Tangu kutangazwa sheria ya kuzitaka Halmashauri zote nchini kutenga asilimia 10 ya mapato yake kwa ajili ya wanawake na vijana.
Je, ni nini kinaifanya Serikali kutokuwa na taarifa ya mfuko huo kujua una kiasi gani cha fedha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Suzana Chogisasi Mgonokulima, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, chimbuko la maelekezo yanayozitaka Halmashauri zote nchini kutenga asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa ajili ya mikopo ya wanawake asilimia tano na mikopo ya vijana asilimia tano ni Azimio la Bunge la Agosti 1993, chini ya kifungu cha 17(1) cha Sheria ya Exchequer and Audit Ordinance ya mwaka 1961; likiazimia kuanzishwa kwa Mifuko Maalum ya Mikopo kwa Vijana na Wanawake kwa kuchangiwa asilimia 10 ya mapato ya ndani ya kila halmashauri kila mwaka. Baada ya azimio hilo Serikali ilitoa maelekezo mahsusi kwa Halmashauri zote nchini kutenga fedha hizo kuanzia mwaka wa fedha 1993/1994.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na changamoto kadhaa za kiutekelezaji ambazo zimekuwa zikisababisha utekelezaji wa azimio hilo usifikie asilimia 100. Miongoni mwa changamoto hizo ni kutofikia viwango vya makusanyo ya ndani vilivyopangwa kwa mwaka husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, mfano katika mwaka wa fedha 2016/2017 jumla ya shilingi 665,414,828,000 za mapato ya ndani zilipangwa kukusanywa na Halmashauri zote nchini; lakini mapato halisi yaliyokusanywa ilipofika mwisho wa mwaka yalikuwa ni shilingi 544,897,803,696 tu. Kutokana na ukusanyaji kutotabirika na hivyo kutofikia viwango tarajiwa, badala ya kiasi cha shilingi bilioni 56.8 kukopeshwa wanawake na vijana kama ilivyokuwa imetengwa, ni shilingi 17.5 tu sawa na asilimia 31, ndizo zilizotolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwakumbusha wakurugenzi wa halmashauri zote 185 Tanzania Bara kwamba kutotoa asilimia 10 ya mapato ya ndani ni tabia ambayo husababisha waandikiwe deni kwenye taarifa za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali. Kupitia Bunge lako Tukufu, naagiza kuanzia sasa ni lazima kila Halmashauri itoe asilimia 10 ya mapato halisi ya ndani kama ilivyoelekezwa na Serikali ili kutokusababisha madeni ya aina hiyo.
MHE. SUZANA C. MGONUKULIMA aliuliza:-
Lengo la Serikali ni kuingiza fedha zote za kodi kwenye mfuko mmoja na baadaye asilimia fulani ya fedha hizo zirudishwe kwenye Halmashauri:-
Je, kwa nini isitungwe sheria ya kuibana Serikali ikiwa haitarejesha fedha hizo kwenye Miji, Halmashauri, Manispaa na Majiji?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Suzana Chogisasi Mgonukulima, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria ya Bajeti ya mwaka 2015, kifungu cha 58 usimamizi wa mapato utazingatia misingi ifuatayo:-
• Mapato yote ya Serikali kuingizwa kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali;
• Yeyote aliyepewa mamlaka ya kukusanya mapato ya Serikali atawajibika ipasavyo katika ukusanyaji wenye ufanisi, utunzaji wa hesabu, utoaji wa taarifa na kuzuia ufujaji wa mapato; na
• Mapato yote kuingizwa kwenye Sheria ya Kuidhinisha Matumizi ya Fedha za Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa mujibu wa kifungu cha 44 cha Sheria ya Bajeti, mgawo wa fedha utazingatia bajeti iliyoidhinishwa, upatikanaji na mtitiriko wa fedha, utekelezaji wake, mpango wa manunuzi na mpango wa kuajiri. Aidha, hakuna fungu litakaloruhusiwa kufanya matumizi ya aina yoyote mpaka kuwe na fedha za kulipia matumizi husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa vifungu vya 44 na 58 vya Sheria vya Bajeti vya Mwaka 2015, usimamizi wa mapato na matumizi ya Serikali umebainishwa vizuri na hivyo hakuna haja ya kutunga sheria nyingine ya kuibana Serikali ikiwa haitapeleka fedha kwenye Miji, Halmashauri, Manispaa na Majiji.
MHE. SUZANA C. MGONUKULIMA aliuliza:-
Serikali inamhudumia Faru Fausta kwa gharama ya shilingi milioni 64 kwa mwezi na ambae hazalishi kutokana na kuwa ni mzee sana lakini Serikali hiyo haiwezi kumhudumia mwananchi aliyezeeka ambae hawezi kufanya shughuli zozote za kujikimu maisha na hana mtu wa kumsaidia.
Je, ni kipi kilicho muhimu zaidi kwa Serikali kati ya Faru Fausta au mwananchi mzee asiyeweza kufanya lolote na hana wa kumsaidia?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Suzana Chogisasi Mgonukulima, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Faru Fausta amekuwepo eneo la Hifadhi ya Ngorongoro tangu mwaka 1965. Kwa sasa Faru huyu ndiyo mwenye umri mkubwa kuliko wote duniani. Kutokana na uadimu wa wanyama hao, uwepo wa Faru Fausta umekuwa kivutio kikubwa kwa watalii na watafiti wa ndani na nje ya nchi na hivyo kuchangia kwa kiwango kikubwa mapato ya hifadhi ya Ngorongoro na Serikali kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na uzee, Faru Fausta alijeruhiwa na fisi tarehe 9 Septemba, 2016 hivyo kulazimisha atunzwe kwenye kizimba (cage) kwa ajili ya uangalizi maalum ambao unahusisha matibabu, chakula na ulinzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama kubwa iliyokuwepo kipindi ikilichopita ilitokana na hali ya dharura iliyohitajika ikiwemo miundoimbinu, ulinzi, matibabu na malisho maalum ambapo matumizi kwa mwezi yalikuwa ni takribani shilingi 1,435,571. Kwa sasa afya ya Faru Fausta inazidi kuimarika kadri siku zinavyozidi kwenda hivyo gharama za uangalizi zimeshuka hadi kufikia shilingi 285,000 kwa mwezi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo Faru Fausta si kwamba ni muhimu kuliko binadamu wazee bali uamuzi wa kumtunza kwenye kizimba ulifanyika kwa lengo la kunusuru maisha yake ili hatimaye aendelee kuwa kivutio cha utalii na kuingiza fedha za kigeni nchini. Fedha zote hizo zinaingia kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali.
MHE. SUZANA C. MGONUKULIMA aliuliza:-

Je, Serikali inasema nini kuhusu Mradi wa Maji kutoka Ibofye kwenda Magulilwa, Kuhota, Lyamgun’we, Ifunda ambao ulipitishiwa bajeti na Bunge?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Suzana Chogisasi Mgonukulima, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Iringa, kama ifuatavyo:-


Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka 1982, kupitia ufadhili wa DANIDA, Halmashauri ya Wilaya ya Iringa ilifanya upembuzi yakinifu wa Mradi wa Maji wa Mtitiriko (Gravity Scheme) utakaotumia chanzo cha maji cha Mto Mtitu ili kuweza kuhudumia vijiji 34 vilivyopo katika Kata sita za Magulilwa, Kuhota, Mseke, Ifunda, Mgama na Maboga ambazo zilikuwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa kabla ya kugawanyika na kuundwa kwa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo. Mradi huo ulikadiriwa kugharimu kiasi cha shilingi milioni 596.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya utekelezaji wa mradi huo kuanza kuligundulika chanzo kingine cha Mto Ibofye katika Kijiji cha Ihimbo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo ambacho kingeweza kutumika kwa ufanisi zaidi na kutatua tatizo la maji kwa kata hizo. Hata hivyo, usanifu wa mradi huu haukukamilika na unategemewa kutekelezwa katika mwaka wa fedha 2019/2020. Mradi huu unatarajiwa kuhudumiwa vijiji 17 na kati ya hivyo vijiji 15 vipo katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa na vijiji viwili katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha wananchi wa maeneo hayo wanapata huduma ya maji wakati wakisubiri Mradi wa Ibofye, Serikali kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Iringa pamoja na wadau wa maendeleo ilichimba visima 53 ambavyo vimewezesha wakazi 8,200 wa kata hizo kupata huduma ya maji. Aidha, ukarabati wa visima katika Kata za Ifunda na Mgama umekamilika na tayari vinatoa huduma kwa wananchi.
MHE. SUZANA C. MGONUKULIMA aliuliza:-

Watu wenye ulemavu wa macho wanakosa haki ya kuchagua viongozi wanaowataka kutokana na kusaidiwa kupiga kura na watu wengine ambao wanaweza kuwapigia kura kinyume na ridhaa zao, hivyo kura zao kwenda kwa watu ambao si chaguo lao:-

Je, Serikali iko tayari kuchapisha karatasi maalum za kupiga kura kwa kutumia mfumo wa nukta nundu kwa ajili ya watu wenye ulemavu wa macho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI,VIJANA NA AJIRA (MHE. ANTONY P. MAVUNDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Suzana Chogisasi Mgonukulima, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kifungu cha 61(3)(b) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi Sura ya 343 na Kifungu cha 62H cha Sheria ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa Sura ya 292 vinafafanua kuwa ikiwa Mpiga kura ni mlemavu wa macho au ana ulemavu wa viungo (mfano, ulemavu wa mikono), au hawezi kusoma na kuandika anaweza kumchagua mtu anayemwamini amsaidie kupiga kura. Mtu huyo anapaswa asiwe Msimamizi wa Kituo cha kupigia Kura, Msimamizi Msaidizi wa Kituo au Wakala wa Chama cha Siasa. Aidha, Kanuni ya 53 ya Kanuni za Uchaguzi wa Rais na Wabunge za Mwaka 2015 na Kanuni ya 46 ya Kanuni za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa za (Madiwani) zimeweka utaratibu kuwa iwapo Mpiga Kura mwenye ulemavu wa macho ataomba kupewa karatasi ya kupigia kura ya nukta nundu (tactile ballot paper), Msimamizi wa Kituo atapaswa kumpatia Mpiga Kura karatasi hiyo ili aweze kupiga kura.

Mheshimiwa Spika, katika Uchaguzi wa mwaka 2015, Tume iliandaa karatasi maalum za kupigia kura kwa mfano wa nukta nundu kwa ajili ya Uchaguzi wa Rais pekee. Hivyo, katika chaguzi zijazo, Serikali kupitia Tume ya Taifa Uchaguzi, itaandaa karatasi hizo maalum wa kutumia mfumo wa nukta kwa ngazi zote za uchaguzi.