Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Suzana Chogisasi Mgonukulima (8 total)

MHE. SUZANA C. MGONOKULIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, sijaridhika na majibu ya Mheshimiwa Waziri hasa kwa baadhi ya wastaafu hao kusitishiwa zoezi wakati walikuwa watumishi wa halali. Hii inaashiria kuwa Serikali haikuwa na orodha sahihi ya wastaafu hao. Pia stahiki walizolipwa ilikuwa ni kusafirishia mizigo na wala siyo kiinua mgongo. Je, Serikali itawalipa lini kiinua mgongo?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali imeomba fedha ya kulipa madeni kwenye bajeti ya mwaka 2016, je, madeni hayo ni pamoja na ya wastaafu hao?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niseme kwamba hawa watumishi wa iliyokuwa Afrika Mashariki walipokuwa wanastaafu kazi, mafao yao ya kustaafu yalikuwa yanakokotolewa na kuunganishwa na kipindi ambacho walikuwa wanafanyia kazi Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa kipindi chote walichofanyia kazi kwenye mashirika husika. Pamoja na kulipwa mafao yao kwa namna hiyo, walikwenda wakafungua kesi Na.93 ya 2003, wakidai walipwe mafao ya utumishi waliyotumikia kipindi wakiwa Jumuiya ya Mashariki. Serikali iliwaomba tufanye mazungumzo nje ya Mahakama wakakubali na tulifanya mazungumzo na 2005 Serikali ndipo ilikubali kuwalipa wafanyakazi 31,831. Mwezi wa Septemba, tulifikia makubaliano (Deed of Settlement) kwamba baada ya kuwalipa wastaafu hao hapatakuwa na madai mengine tena na ndiyo tuliwalipa kama nilivyoeleza katika jibu la msingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, swali la ni lini tutawalipa kiinua mgongo tulishamaliza na Serikali haidaiwi tena. Pia ni muhimu nieleze kabisa kwamba pamoja na kufikia Deed of Settlement bado tulitoa muda wa zaidi ya miaka saba ambapo wastaafu walikuwa wanakuja wanalipwa on a case by case basis. Kwa hiyo, Serikali hatudaiwi tena na wastaafu hao.
MHE. SUZANA C. MGONUKULIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na
majibu ya Waziri, Manispaa ya Iringa ina miradi mikubwa ya Machinjio ya Kisasa
ya Ngelewala, Soko la Ngome, Sekondari ya Mivinjeni, Nyumba za Waganga na
Wauguzi wa Zahanati ya Njiapanda na Nduli. Katika Baraza la Madiwani, kupitia
bajeti ya mwaka 2016/2017, Manispaa ya Iringa ilikadiria kukusanya mapato ya
ndani Sh. 4,532,000,000 ili kuweza kumalizia miradi midogo iliyokuwa inaikabili
Manispaa hiyo. Manispaa ya Iringa, vyanzo vikuu vya mapato vinatokana na
kodi ya majengo, Serikali ikaamua kodi hizi za majengo zikusanywe na TRA, je, ni
lini Serikali itaona umuhimu wa kupeleka hela za miradi hii kwa wakati ili kuweza
kumalizia miradi ambayo haijamalizika hadi sasa?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika,
napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kwamba Serikali inaona umuhimu wa
miradi yote ya maendeleo kama ilivyopitishwa katika bajeti yetu mwezi Juni.
Hivyo, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, kinachopelekea kupeleka
fedha hizi ni upatikanaji wa fedha hizi. Kwa kuwa Mheshimiwa Mbunge
ameongelea kuhusu kodi ya majengo, naomba nimwambie kwamba TRA
imekusanya kodi ya majengo mwezi wa Kumi, baada ya quarter ya kwanza
kupewa Halmashauri zenyewe kukusanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Mbunge,
anapuhudhuria Baraza la Madiwani aweze kusimamia mapato yaliyopatikana ili yaweze kutumika katika miradi aliyoitaja. Serikali yetu baada ya kukusanya
kuanzia mwezi wa Kumi, fedha zote tulizoahidi zitarejeshwa katika Halmashauri
husika kutokana na bajeti zilizopitishwa.
MHE. SUZANA C. MGONUKULIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitauliza maswali mawili ya nyongeza kwa niaba ya Mheshimiwa Susane Maselle, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, kutokana na majibu ya Naibu Waziri kuwa wachimbaji hawa wadogo walipata leseni, je, Serikali inatoa kauli gani juu ya Jeshi la Polisi lililotumia nguvu kupiga mabomu wachimbaji hao wadogo na kuwanyanyasa wenyewe na familia zao na kufanyiwa vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia wanawake na watoto? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, je, Naibu Waziri yupo tayari kuongozana na Mheshimiwa Susane Maselle kwenda eneo hilo kuongea na wananchi hao kuhusu vitendo walivyofanyiwa na Jeshi la Polisi kuwa hawakufanyiwa kiusahihi kwa sababu walikuwa na leseni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na swali la pili, niko tayari kufuatana na Mheshimiwa Susane na kwa ridhaa yako kama itapendeza basi nitafuatana naye, nitembelee maeneo yale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na wachimbaji hao kupigwa mabomu pamoja na kufanyiwa harassment ni suala ambalo linatakiwa litazamwe kwa kina sana unaweza usiwe na jibu la moja kwa moja. Ninachoweza kusema ni kwamba pale inapotokea kunakuwa na vurugu katika maeneo ya uchimbaji kazi ya Jeshi la Polisi ni kutuliza ghasia ili kuhakikisha kwamba kunakuwa na amani na utulivu katika maeneo yale. Inawezekana ilifanyika katika hatua hiyo, lakini Mheshimiwa Mbunge tutakaa pamoja tuone ni hatua gani zilichukuliwa ili tushirikiane na wenzetu wa Mambo ya Ndani tuone nini cha kufanya zaidi.
MHE. SUZANA C. MGONOKULIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tatizo la barabara la Makambako - Songea yanafanana na matatizo ya barabara inayotoka Mwatasi -Kimara – Idete - Idegenda ambako uzalishaji wa mbao pamoja na matunda aina ya pears ni wa kiwango kikubwa sana lakini hali ya barabara hii siyo nzuri. Ni lini Serikali sasa itafanya mpango mkakati kuhakikisha hizi barabara zinatengenezwa kwa kiwango cha lami ili kupelekea usafirishaji wa mbao uwe salama na safi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Songea - Makambako ni trunk road wakati barabara anayoongelea ni ya district. Ni kweli zinafanana kwa sababu zote ni barabara lakini zina hadhi mbili tofauti na district road zinashughulikiwa na Halmashauri chini ya TAMISEMI.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana na hoja yake lakini naomba Watanzania wote tuungane kama watu wamoja, tuweke vipaumbele vya hizi barabara na vile ambavyo tunakubaliana tuanze navyo, tuanze navyo, kwa sababu hatimaye fedha zinahitajika na hatuwezi kujenga barabara zote kwa wakati mmoja, ni lazima tuanze hizi, baadaye tunafuata hizi, hatua kwa hatua. Kwa hiyo, nimuombe avute subira itafika wakati baada ya kukamilisha zile ambazo tumekubaliana ni vipaumbele chini ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya 2015 - 2020 tutakuja huku ambako Mheshimiwa Mgonokulima anakuongelea.
MHE. SUZANA C. MGONUKULIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya majibu ya Mheshimiwa Waziri, nina maswali ya nyongeza mawili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, makusanyo ya kodi za majengo katika Manispaa ya Iringa katika mwaka wa fedha 2015/2016, TRA iliweza kukusanya shilingi milioni 800. Katika upangaji wa bajeti wa Halmashauri ya Manispaa Iringa fedha za kodi ya majengo zilikuwa zimekadiriwa zisaidie miradi ya Manispaa ya Iringa. Hadi navyozungumza hapa hakuna hata senti tano iliyorudishwa. Je, nia ya Serikali ni kutaka kukwamisha maendeleo ya Manispaa ya Iringa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mjumbe wa vikao vya RCC. Halmashauri saba za Mkoa wa Iringa zilipeleka barua ya maombi maalum kama sheria inavyotaka, kuomba fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali za Wilaya. Wilaya ya Kilolo imefanikiwa kupewa shilingi bilioni moja na point, Wilaya ya Iringa vijiji imefanikiwa kupewa milioni moja na point, Wilaya ya Mufindi imefakiwa kupewa shilingi bilioni moja na point, Mafinga Mjini imefanikiwa kupewa shilingi milioni 400; Manispaa ya Iringa ilikuwa imeomba kibali maalum cha shilingi milioni 700, haikuweza kupewa fedha hizo. Je, fedha hizi zinalipwa kisiasa hasa ukizingatia Majimbo yaliyopewa fedha ni ya CCM na Jimbo la Manispaa ya Iringa ni la CHADEMA? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Suzana Chogisasi Mgonukulima, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza, napenda kumwambia kwamba siyo nia ya Serikali kukwamisha maendeleo ya Halmashauri yoyote ile na ndiyo maana tarehe 5 Mei, 2018, Serikali imezindua Mpango Mkakati wa Kuziwesha Halmashauri kubuni miradi ya maendeleo itakayo-generate mapato kwa ajili ya Halmashauri husika na hatimaye kuhakikisha shughuli zote za maendeleo zinaendelea kutekelezwa ndani ya kila Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili, napenda kwanza kumshukuru kwa kuweza kusema ndani ya Mkoa wa Iringa, Wilaya nne ndani ya miaka miwili ya Serikali ya Awamu ya Tano ya Mheshimiwa Dkt. Magufuli zimepewa fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali za Wilaya. Hilo ni jambo la msingi, naamini angetupongeza kama Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swaIi lake la pili amesema kwamba pesa zinatolewa kisiasa. Napenda kumwambia Mheshimiwa Mgonukulima kwamba Mheshimiwa Msigwa Mbunge wa Iringa Mjini yeye mwenyewe amekiri mbele ya Mheshimiwa Rais kwamba miradi mingi ya maendeleo inapelekwa kwenye Majimbo yote. Kwa hiyo, hakuna siasa kwenye utelekelezaji wa miradi ya maendeleo. (Makofi/Kicheko)
MHE. SUZANA C. MGONUKULIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na majibu ya Waziri naomba niulize maswali ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa majibu ya Waziri, utunzwaji wa Faru Fausta umewezesha kulitumikisha taifa kwa gharama kubwa kuliko wazee wa Tanzania waliofanyakazi ya kuleta haki na amani katika Taifa hadi Faru Fausta kuonekana ni wa muhimu ni kwa ajili ya amani iliyopatikana kwa wazee hawa. (Makofi)
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali haioni ni wakati sasa wa kuhakikisha wazee wa taifa hili wanatunzwa kama vile gharama zote anavyotunzwa faru Fausta ili waweze kuleta amani katika nchi hii?
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa kuwa kwa majibu ya Waziri amesema anahifadhiwa na ana ulinzi mkali, hivyo hata watalii hawamuoni, hizo fedha za kigeni zinazopatikana zinatokana na nini na wakati amehifadhiwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba niweke record vizuri kwa dada yangu Mheshimiwa Mbunge kwamba wanyama wana haki sawa kama binadamu wengine na huyu mnyama kutokana na uadimu wake, na kwamba ni moja ya wanyama ambao wapo hatarini kutoweka ndiyo maana tumemweka kwenye ulinzi maalum. Kutokana na umuhimu wake huo na kutokana na jinsi ambavyo ameliingizia Taifa fedha nyingi za kigeni na kutokana na kwamba watu wengi wanataka kujua maisha yake kwamba ataishi miaka mingapi, maana mpaka sasa hivi ana miaka 53 ndio maana tumeamua kumweka kwenye ulinzi huo sawa na binadamu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo Ilani ya Chama cha Mapinduzi inasema Wazee wote sasa hivi tunawatambua ili kutengeneza sera nzuri ya kuweza kuwasaidia na kuwalipa pensheni. Kwa hiyo, watalipwa sambamba na faru huyu, Faru Fausta ambaye ndiyo sera inavyosema ya Chama cha Mapinduzi, nashukuru. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii naomba niongeze maelezo kidogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sera ya Afya ya mwaka 2017 Serikali inatambua mchango na kuthamini mchango wa wazee na tumeweka utaratibu wazee wote ambao wako zaidi ya miaka 60 watapata matibabu bure.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeweka mkakati sasa hivi kuhakikisha kwamba wazee wanatambuliwa na kupewa vitambulisho vya kupewa matibabu na tumeweka utaratibu wa kuhakikisha kwamba, katika vituo vyetu vyote vya kutolea huduma za afya wazee wanapewa kipaumbele cha kwanza. (Makofi)
Kwa hiyo pamoja na majibu yote ambayo ametoa Naibu Waziri mchango huu ambao unapatikana katika mapato ya utalii katika sekta hii ya utalii ndio haya yanayoingia kwenye Mfuko Mkuu wa Taifa na kwenda kuwahudumia wazee hawa. (Makofi)
MHE. SUZANA C. MGONUKULIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya majibu ya Serikali, nina maswali ya nyongeza mawili.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kutokana na majibu ya Serikali kuwa Halmashauri ya Iringa na wadau wa maendeleo walichimba visima 53, naomba kujua ni visima vingapi vimetatua matatizo ya maji kwa wananchi wa vijiji hivyo nilivyouliza?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa maelezo ya Serikali Mradi wa Maji wa Ibofye utatekelezwa mwaka wa fedha 2019/2020. Mradi huu una miaka 37 umeshindwa kutekelezeka. Naomba kujua ni muujiza gani utakaotumika kwa Serikali kutekeleza mradi ndani wa mwaka mmoja?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kuhusu idadi halisi ya visima ambavyo vipo katika vijiji hivyo alivyovitaja. Nimwombe Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge saa saba tukutane ili tuweze kumpa kwa maandishi visima halisi katika vijiji anavyohitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala zima la Mradi wa Ibofye, hii ni Serikali ya Awamu ya Tano, inapoahidi inatekeleza na hata kama haijatekeleza inakuwa na sababu ya msingi na maalum katika suala zima la utekelezaji. Ssisi ni Wizara ya Maji siyo Wizara ya Ukame, tutahakikisha Mradi huu wa Ibofye tunautekeleza ili wananchi wake waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. SUZANA C. MGONUKULIMA: Mheshimiwa Spika, kutokana na majibu ya Mheshimiwa Waziri nitakuwa na maswali ya nyongeza mawili. Swali la kwanza, kutokana na maelekezo ya kuwa mtu mwenye ulemavu wa macho atamwomba Msimamizi wa Uchaguzi karatasi ya nukta nundu. Je, Serikali imetoa elimu kiwango gani kwa watu wasioona ili wajue wakifika kwenye kituo hicho wamuone huyo mtu atakayetoa karatasi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni miaka 58 ya uhuru wa nchi yetu, ni mwaka 2015 kama Mheshimiwa Naibu Waziri alivyokiri Serikali iliweza kutoa makaratasi ya nukta nundu kwa watu wenye ulemavu wa macho napo kwa kumchagua Rais tu. Je, Serikali haioni haiwatendei haki watu wenye ulemavu wa macho kutokumchagua Mwenyekiti, Diwani na Mbunge hatimaye kupata set ya Serikali ambayo anaitarajia imuongoze?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI,VIJANA NA AJIRA (MHE. ANTONY P. MAVUNDE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Suzana Mgonukulima, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza la kuhusu elimu kwa watu wenye ulemavu, Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa kushirikiana na Shirikisho la Vyama vya Watu wenye Ulemavu kwa pamoja, tutafanya kazi ya kutoa elimu kwa makundi mbalimbali likiwemo kundi hili la watu wenye ulemavu ili waweze kutimiza haki yao ya Kikatiba ya kupiga kura. Hivyo nichukue fursa hii kuwaondoa hofu watu wote wenye ulemavu wa macho, kwamba wakati wa uchaguzi wa mwaka 2020 watapata fursa ya kupiga kura kwa kupata elimu kupitia Tume ya Taifa ya Uchaguzi pamoja na shirikisho ambao tunafanya nao kazi kwa pamoja.

Mheshimiwa Spika, suala la pili, kuhusu haki za watu wenye ulemavu kuwapigia kura wagombea wengine zaidi ya mgombea wa urais. Katika majibu yangu ya msingi nimeeleza kwamba mwaka 2015 ilikuwa ni fursa hiyo tu ya kuweza kumchagua mgombea wa urais, lakini kwa mwaka 2020 nataka nilihakikishie Bunge lako kwamba tunaweka utaratibu mzuri ili pia watu wenye ulemavu wawe na haki ya kuchagua viongozi wote kwa ngazi zote kama majibu yangu ya msingi yalivyosema.