Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Yosepher Ferdinand Komba (7 total)

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA (K.n.y. MHE. YOSEPHER F. KOMBA) aliuliza:-
Hospitali Teule ya Wilaya ya Muheza ilianzishwa miaka ya 1980 kwa ushirikiano kati ya Kanisa la Anglikana na Serikali imekuwa ikihudumia wagonjwa wengi ndani na nje ya Wilaya ya Muheza, hivyo kuzidiwa na uwezo wa kuhudumia na vifaa tiba:-
(a) Je, ni lini Serikali itaipatia Hospitali Teule gari la kubeba wagonjwa ili kuboresha huduma na kuokoa maisha ya Watanzania?
(b) Je, nini mkakati wa Serikali katika kumaliza changamoto ya Wahudumu wa Afya katika Hospitali hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yosepher Ferdinand Komba, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, katika mipango na bajeti Halmashauri ina mpango wa kununua gari la wagonjwa aina ya Land Cruiser Hard Top kwa ajili ya Hospitali Teule ya Wilaya ya Muheza katika mwaka wa 2017/2018 lenye thamani ya shilingi milioni 200. Kwa sasa huduma za usafiri wa dharura (Rufaa) kwa wagonjwa zinatolewa kwa kutumia magari ya kawaida yaliyopo kwenye Halmashauri.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, ili kutatua changamoto ya Watumishi Hospitalini hapo, Halmashauri katika Bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017 imeidhinishiwa kibali cha watumishi 133 wa kada mbalimbali za afya. Watumishi hawa watakapoajiriwa, baadhi yao watapangwa katika Hospitali Teule ya Wilaya ya Muheza ili kupunguza tatizo lililopo la uhaba wa watumishi. Aidha, katika mwaka wa fedha 2016/2017, Halmashauri imepanga kuwaendeleza watumishi 24 ili wapate sifa na ujuzi unaotakiwa katika utoaji wa huduma za afya katika Hospitali hiyo.
MHE. YOSEPHER F. KOMBA aliuliza:-
Tatizo la Maji Mkoa wa Tanga ni kubwa licha ya kuwa na vyanzo vingi vya maji, viongozi wa Serikali kwa nyakati tofauti wamekuwa wakitoa ahadi mbalimbali lakini hakuna hatua za makusudi za kutatua tatizo la maji:-
(a) Je, ni lini Serikali itapeleka maji kupitia mradi wa Manga/Magoroto ambao ulianza tangu mwaka 1970?
(b) Je, ni lini Serikali itatatua changamoto ya uchakavu wa miundombinu hasa mabomba na mipira katika mradi wa Kicheba na Kwemhosi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yosepher Ferdinand Komba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa maji Magoroto ulijengwa mwaka 1977 na ulilenga kuhudumia wakazi wapatao 8,000 katika Mji wa Muheza na maeneo yanayozunguka Mji wa Muheza. Hivi sasa mradi huu unahudumia wakazi wapatao 30,834 walioko katika Mji wa Muheza; idadi hii ni kutokana na sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na ongezeko kubwa la idadi ya watu mradi huu hautoshelezi mahitaji katika Mji wa Muheza. Ili kuondoa tatizo, mradi wa dharura utakaogharimu shilingi bilioni 2.6 unaendelea kutekelezwa kwa kutoa maji eneo la Pongwe. Taratibu za kumpata Mkandarasi zinaendelea na kazi inatarajiwa kuanza mwezi Juni, 2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa maji katika Kijiji cha Kwemhosi ulitekelezwa na Serikali kwa gharama ya shilingi milioni 225 na ulikamilika mwezi Juni, 2013. Mradi huu unafanya kazi kama ulivyosanifiwa, ila kwa sasa mradi huo umeharibiwa kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha. Aidha, Mradi wa maji wa Kicheba ulijengwa mwaka 1999 na Kanisa Katoliki ambapo hivi sasa miundombinu yake imechoka. Mradi huu utaendelea kukarabatiwa na Serikali kwa kushirikiana na Jumuiya ya watumiaji maji katika eneo la Kicheba, kadri fedha zitakavyopatikana.
MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y MHE. YOSEPHER F. KOMBA) aliuliza:-
Ni dhamira ya Serikali kutekeleza mpango wa elimu bure kuanzia chekechea hadi kidato cha nne, lakini mpango huu una changamoto ambazo zisipotatuliwa zitasababisha kushuka kwa ubora wa elimu.
(a) Je, ni nini tamko la Serikali juu ya wanafunzi wanaoanza kidato cha kwanza kwa kigezo cha kutofaulu kwa kiwango cha kianzia alama 100 na kuendelea?
(b) Je, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha ujenzi wa maabara unakamilika kwa wakati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yosepher Ferdinand Komba, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, tamko la Serikali ni kwamba mwanafunzi anahesabiwa kufaulu mtihani wa Taifa wa darasa la saba endapo atapata alama kuanzia 100 hadi 250 katika masomo yote aliyoyafanya. Hata hivyo, wanafunzi walio na alama chini ya 100 huhesabika kuwa ni miongoni mwa waliokosa sifa za kujiunga na kidato cha kwanza katika shule za Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, wanafunzi walioshindwa kufikia alama 100 na kuendelea, hushauriwa kujiunga na mfumo usio rasmi wa Elimu Masafa (Open Distance Learning) unaosimamiwa na Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima, vyuo vya ufundi au shule za sekondari za binafsi. Wanafunzi wanaojiunga na mfumo huo wa elimu hawamo katika utaratibu wa utekelezaji wa mpango wa elimu msingi bila malipo, lakini wanafunzi wanaosoma katika utaratibu huo watakaofaulu mtihani wa Taifa wa kidato cha nne huchaguliwa kujiunga na kidato cha tano katika shule za Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la (b); ujenzi wa maabara katika Halmashauri zote unaendelea ili kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia masomo ya sayansi. Kati ya maabara 10,387 zinazohitajika nchini, ujenzi wa maabara 6,287 sawa na asilimia 60.5 ya mahitaji umekamilika.
Nazikumbusha Halmashauri zote kukamilisha mapema ujenzi unaoendelea kwa kushirikisha wadau na nguvu za wananchi.
MHE. YOSEPHER F. KOMBA aliuliza:-

Kuna uhaba wa watumishi na vitendea kazi katika Idara ya Ardhi na Maliasili – Wilaya ya Muheza kunakosababisha kuazima watumishi na vifaa kutoka Halmashauri nyingine:-

(a) Je, ni lini Serikali itaajiri watumishi na kununua vitendea kazi katika Idara hiyo?

(b) Je, Serikali iko tayari kuwawekea wananchi Wanasheria ili kusaidia kutatua migogoro ya ardhi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yosepher Ferdinand Komba, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Idara ya Ardhi na Maliasili katika Halmashauri ya Wilaya ya Muheza inao watumishi 12 kati ya 20 wanaohitajika. Halmashauri imeendelea kuomba vibali kwa ajili ya kuajiri watumishi hao. Hata hivyo,ili kukabiliana na upungufu huo Halmashauri imeajiri watumishi watatu (3) wa Ardhi kwa mkataba ili kutatua changamoto mbalimbali za ardhi. Vile vile katika mwaka wa fedha 2017/2018, kupitia mapato yake ya ndani Halmashauri ilinunua GPS- RTK (Real time Kinematic) kwa ajili ya upimaji ardhi kwa gharama ya shilingi milioni 37. Aidha, Halmashauri imetoa gari Toyota Land Cruiserkwa ajili ya Idara ya Ardhi na Maliasili. Halmashauri itaendelea kununua vitendea kazi kwa awamu kadri ya upatikanaji wa Fedha.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inao mfumo wa kisheria wa utatuzi wa Migogoro ya Ardhi kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa ambao umeainishwa katika Sheria ya Utatuzi wa Migogoro ya Ardhi, Na. 2 ya mwaka 2002 na Kanuni zake. Migogoro ya ardhi iliyopo Wilayani Muheza imegawanyika kwenye makundi makuu matatu; migogoro ya kiwilaya ambayo inahusisha mipaka ya vijiji vya Wilaya ya Muheza na Tanga Jiji pamoja na Vijiji vya Muheza na Pangani. Migogoro hii inashughlikiwa katika ngazi ya Mkoa na itapatiwa ufumbuzi wakati wowote.

Kundi la pili la migogoro ni migogoro ya mipaka ya vijiji iliyotokana na zoezi la upimaji wa mipaka nchi nzima uliofanyika mwaka 2007. Vikao kwa ajili ya kumaliza migogoro hii vinaendelea na vimefikiwa hatua nzuri. Migogoro mingine ni migogoro ya viwanja ambayo hupokelewa na kutatuliwa kwa utaratibu wa kawaida wa Mamlaka za Serikali za Mitaa. Suluhisho la kudumu kwa aina hii ya migogoro ni kukamilisha mpango wa matumizi bora ya ardhi, kupima viwanja na kurasimisha makazi ambapo mpaka sasa makazi 4,768 yamerasimishwa Wilayani Muheza. Serikali itaendelea kutekeleza Mpango waMatumizi Bora ya Ardhi, kurasimisha makazi, kupima viwanja na mashamba ili kumaliza migogoro ya ardhi.
MHE. YOSEPHER F. KOMBA aliuliza:-

Katika Kijiji cha Sakale, Kitongoji cha Kwempasi, Tarafa ya Amani katika Wilaya ya Muheza wananchi waligundua uwepo wa madini na shughuli za uchimbaji zilianza, lakini baada ya muda Serikali imefunga machimbo yale:-

Je, ni lini Serikali itaandaa utaratibu wa kufungua machimbo hayo ili wachimbaji wadogo hususan vijana wazawa waweze kunufaika.
WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Yosepher Ferdinard Komba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini (GST) ikishirikiana na wadau wa maendeleo ilifanya utafiti na ulibaini uwepo wa madini ya dhahabu katika Vijiji vya Mindu, Amani, Tengeni, Segoma, Mbambara, Sakale, Muheza na Korogwe. Pia Wilaya ya Muheza ina madini ya ujenzi kama vile mchanga na mawe katika Vijiji vya Magila, Kilapula, Kwakifua, Mhamba, Furaha na Tanganyika na madini ya garnet, ruby na sapphire katika Kijiji cha Misozwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli machimbo yaliyokuwa yakiendelea katika Kijiji cha Sakale yalifungwa tarehe 2 Oktoba, 2018 baada ya timu ya watalaam kubaini uchimbaji huo kutokuzingatia Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 na Marekebisho yake ya mwaka 2017. Aidha, Sheria ya Mazingira ya Mwaka 2004 na kanuni zake haziruhusu kufanya uchimbaji katika vyanzo vya maji ili kuzuia kemikali ya zebaki na uchafu utokanao na uchenjuaji kuingia kwenye mito ambayo inamwaga maji kwenye Bwawa la Bayani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchimbaji huo ulikuwa unafanyika katika vilima vya Kwempasi na Nelusanga ambapo uchimbaji unaweza kutiritirisha majitaka na udongo kutoka juu ya vilima na kuingia katika bonde la Mto Kihara ambao ni moja ya chanzo cha Bwawa la Bayani linalotumiwa na wakazi zaidi ya laki 500 katika Wilaya ya Korongwe, Muheza na Jiji la Tanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, timu ya watalaam ilishauri mwekezaji mzawa au mgeni anaweza kuruhusiwa kuchimba madini hayo kwa kutumia leseni ya uchimbaji mkubwa na kuweza kufanya tathimini ya kimazingira (EIA) na kuwashirikisha wadau wote muhimu kabla ya kuanza uchimbaji ili kuzuia uharibifu huo wa mazingira.
MHE. YOSEPHER F. KOMBA aliuliza:-

Nyumba za makazi pembezoni mwa reli Wilayani Muheza zimewekewa alama ya ‘X’ zikisubiri kubomolewa kwa kigezo cha kujenga kwenye eneo la reli wakati walipewa maeneo hayo kIhalali na Serikali.

Je, ni nini hatma ya wananchi hao ambao wanaishi kwa mashaka?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Yosepher Ferdinand Komba, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo;-

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa Serikali ni kuendelea na ujenzi wa mtandao wa reli nchi nzima. Hata hivyo, umejitokeza uvamizi mkubwa wa maeneo ya reli katika maeneo mbalimbali yanayopitiwa na reli.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Serikali kupitia Shirika la Reli Tanzania (TRC) iliendesha zoezi la kutambua maeneo ya reli nchi nzima na kubaini uvamizi huo na hivyo kuchukua hatua ya kuweka alama ‘X’ na kutoa notisi ya kuwataka wananchi hao kupisha katika maeneo hayo. Kufuatia zoezi hilo TRC imekuwa ikipokea malalamiko kutoka kwa wananchi mbalimbali wakiwemo wananchi wa Muheza. Shirika la Reli Tanzania (TRC) limeanza kukutana na viongozi wa mikoa mbalimbali husika ili kufahamu sababu za madai hayo katika maeneo ambayo ni hifadhi ya reli.

Mheshimiwa Naibu Spika, ifahamike kuwa maeneo yote yaliyowekwa alama ‘X’ ni hifadhi halali ya reli na mipaka yake iiwekwa tangu mwaka 1967 kupitia ramani ya mipaka ya reli.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo nimuombe Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Muheza kuwa na utaratibu wa kupata taarifa za kina za matumizi ya maeneo husika kabla ya kuyatwaa na kuanza kuyaendeleza kwani husababisha usumbufu kwa Serikali na hasara kwa mali zilizoendelezwa katika maeneo hayo.
MHE. YOSEPHER F. KOMBA aliuliza:-

Sekondari ya Lanzoni iliyopo Wilayani Mkinga ilianzishwa mwaka 1995 kwa lengo la kuchukua wanafunzi wa chaguo la pili lakini inakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa umeme, maji, usafiri pamoja na makazi ya watumishi:-

Je, Serikali ina Mikakati gani ya kushirikiana na Halmashauri ya Mkinga katika kutatua changamoto hizo?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yosepher Ferdinand Komba Mbunge wa Viti maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa Shule ya Sekondari ya Lanzoni ina changamoto nyingi za kimazingira ikiwemo kutokuwa na umeme wa grid, maji na uhaba wa nyumba za walimu. Pamoja na changamoto hizo, Serikali kwa kushirikiana na Halmashauri kupitia Mpango wa MMES II, ilifanikiwa kujenga nyumba mbili (2) mpya za walimu, vyumba viwili vya madarasa na maabara moja ya kisasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga imefanya tathmini ya kupeleka maji katika shule ya Lanzoni kutoka katika Mto Zigi na kubaini kuwa kiasi cha shilingi milioni 7.6 zinahitajika. Halmashauri kwa kushirikiana na wadau inaendelea kutafuta fedha ili kukamilisha kazi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Shule ya Sekondari Lanzoni haina umeme wa grid na inatumia umeme wa jua. Hata hivyo tayari imeshaingizwa kwenye Mpango wa REA III hivyo muda wowote itaunganishwa kwenye umeme wa grid Taifa, ahsante.