Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Zainabu Mussa Bakar (7 total)

MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR (K.n.y. MHE. ZAINAB MUSSA BAKAR) aliuliza:-
Vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa kijinsia unaendelea kushamiri Tanzania hususan Mikoa ya Dar es Salaam, Pwani na Visiwa vya Zanzibar, watoto wengi wanakataa kwenda shule kutokana na udhalilishaji huo. Aidha, wengi wao wanaogopa kunyanyapaliwa ama kuona haya au aibu juu ya vitendo wanavyofanyiwa watoto wa kiume na wa kike:-
(a) Je, Serikali ina mikakati gani kuhakikisha suala hilo linapungua au linaondoka kabisa?
(b) Je, Serikali ya Tanzania ikishirikiana na Serikali ya Zanzibar inawasaidiaje watoto hawa ili waendelee na masomo bila kunyanyapaliwa?
(c) Je, Serikali haioni kuwa haiwatendei haki watoto hawa kwa kuonekana watuhumiwa nje wakati wamewavunjia utu na maisha yao kwa kisingizio cha ushahidi haujakamilika?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Mussa Bakar, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatekeleza Mpango wa Taifa wa kudhibiti ukatili dhidi ya watoto wa mwaka 2013 - 2016, malengo ya mpango huu yakiwa ni pamoja na kuanzisha na kuimarisha mifumo ya ulinzi wa mtoto, kuanzisha na kuimarisha Dawati la Jinsia na Watoto katika vituo vyote vya Polisi nchini, kuendelea kutoa mafunzo ya elimu ya malezi chanya kwa wazazi, Walimu na wanajamii, kuendesha mafunzo kuhusu Sheria ya Mtoto Namba 21 ya mwaka 2009 kwa wasimamizi wote wa sheria na kusimamia utekelezaji wake na kuhamasisha utumiaji wa huduma ya mtandao wa simu ya kusaidia kutoa taarifa za ukatili dhidi ya mtoto kwa kutumia Child Help Line Number 116.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali zikiwemo Serikali za Mitaa inaziwezesha Kamati za Ulinzi na Usalama wa Mtoto kutambua na kutatua matatizo ya watoto yakiwemo ya kisheria, kisaikolojia na kielimu.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaendeshwa kwa mujibu wa sheria ambapo haki za raia wote ikiwemo haki za watoto zinalindwa na kusimamiwa kikamilifu. Mtuhumiwa wa vitendo vya ukatili anapokamatwa na kufikishwa katika vyombo vya sheria, taratibu za uendeshaji kesi hufuatwa ikiwa ni pamoja na kuithibitishia Mahakama kuwa kweli mtuhumiwa katenda kosa ua la. Hivyo, Serikali haipendi kuwaachia watuhumiwa wa vitendo vya ukatili punde wanapokamatwa na kufikishwa katika vyombo vya sheria, bali mara nyingi kunakosekana ushirikiano wa jamii katika kutoa ushahidi wa kumtia hatiani mtuhumiwa.
MHE. FAIDA MOHAMED BAKAR (K.n.y. MHE. ZAINAB MUSSA BAKAR) aliuliza:-
Suala la Madaktari feki limezoeleka nchini Tanzania na linazidi kuendelea siku hadi siku katika hospitali zetu:-
(a) Je, Serikali haioni kuwa suala hili ni kuhatarisha maisha ya Watanzania kutokana na uzembe na usimamizi mbovu wa hospitali zetu?
(b) Je, Serikali imechukua hatua gani kuondoa kadhia/ kero hii isiendelee?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zainabu Mussa Bakar, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa suala hili la madaktari feki linahatarisha afya na maisha ya Watanzania. Mara nyingi tatizo hili linatokea katika hospitali zenye idadi kubwa ya Madaktari, hali inayowapa urahisi Madaktari feki kutotambulika upesi. Kwa kutambua hali hii Serikali imeweka utaratibu wa kudhibiti uwezekano wa kuwepo kwa Madaktari feki kwa kufanya mambo yafuatayo:-
(1) Kuimarisha utendaji wa Baraza la Madaktari na Madaktari wa Meno linalosajili na kusimamia utendaji kazi wa Madaktari na Madaktari wa Meno. Baraza hili linahakikisha kuwa Madaktari na Madaktari wa Meno wenye sifa zinazostahili ndio wanasajiliwa na kuruhusiwa kutoa huduma. (Makofi)
(2) Kuimarisha usimamizi wa watumishi ikiwa ni pamoja na Madaktari katika vituo. Utekelezaji wake unajumuisha kuvaa vitambulisho vinavyoonesha majina ya watumishi na kwamba Daktari ambaye ni feki itamuwia vigumu sana kuvaa kitambulisho feki na hivyo kumfanya aonekane kwa haraka.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ambazo Serikali imechukua kuondoa kadhia/ kero hiyo ni pamoja na kuhakikisha kuwa:-
(1) Madaktari wote walio kazini wanavaa vitambulisho vinavyoonesha majina yao.
(2) Viongozi wote wanaosimamia sehemu za kutolea huduma wanawafahamu vyema watumishi walio chini yao ikiwa ni pamoja na Madaktari.
(3) Viongozi wa vituo vya kutolea huduma (hospitali za ngazi zote, vituo vya afya na zahanati) wanahakiki kila mtumishi anayefika kituoni kuanza kazi baada ya kuajiriwa au kuhamishiwa katika kituo husika kutoka sehemu nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua hizi zinachukuliwa ili kudhibiti hali hiyo kwa sababu kila siku Madaktari feki hawa wanakuja na mbinu mpya za kujificha wakati wakifanya vitendo vyao viovu.
MHE. ZAINAB MUSSA BAKAR aliuliza:-
Zanzibar ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Je, ni kwa nini plate number za vyombo vya moto ambazo ni za Tanzania Bara hazitumiki au haziruhusiwi Zanzibar, na ni kosa ambalo linatozwa faini ya shilingi 300,000?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Mussa Bakar, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Usalama Barabarani ambayo husimamia usajili wa vyombo vya moto siyo sheria ya Muungano. Kwa upande wa Tanzania Bara usajili wa vyombo vya moto unasimiwa na Sheria ya The Road Traffic Act ya mwaka 1973 na Kanuni ziitwazo The Traffic Foreign Vehicles Rule za mwaka 1973. Kwa upande wa Tanzania Bara sheria hizi zinasimamiwa na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na kwa upande wa Tanzania Zanzibar usajili wa vyombo vya moto unasimamiwa na Sheria ya The Road Transport Act namba 7 ya mwaka 2003. Majukumu ya usajili wa vyombo vya moto Zanzibar husimamiwa na Bodi ya Mapato Zanzibar tangu mwaka 2008.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria ya Usajili wa Vyombo vya Moto Tanzania Zanzibar (The Road Transport Act No. 7) ya mwaka 2003, chini ya kifungu cha 43, magari yasiyosajiliwa Zanzibar hutumika Zanzibar bila kufanyiwa usajili upya wa siku 90 pale ambapo magari hayo yanakibali cha kukaa na kutumika Zanzibar. Hata hivyo, baada ya kupita muda wa siku 90, mmiliki wa magari hayo hutakiwa kuomba kusajili magari yao kwa namba za Tanzania Zanzibar au kuomba muda zaidi wa kutumika Zanzibar bila usajili wa Tanzania Zanzibar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, chini ya kifungu cha 201 cha
The Road Transport Act Namba 7 ya mwaka 2003, mmiliki wa chombo cha moto akishindwa kusajili chombo cha moto baada ya siku 90 na kushindwa kuomba kuongezewa muda wa kutumia gari bila usajili, anakuwa amefanya kosa na faini yake ni dola za kimarekani 50 au shilingi zenye thamani ya dola hizi, na siyo shilingi 300,000.
MHE. TUNZA I. MALAPO (K.n.y. MHE. ZAINAB M. BAKAR) aliuliza:-
Maji ni muhimu katika maisha ya mwanadamu na bila maji safi na salama afya za wananchi zinaweza kuwa hatarini:-
Je, Serikali inachukua hatua gani kwa vijiji ambavyo havina vyanzo vya maji, hasa ikizingatiwa kuwa, bila maji safi na salama ni kuhatarisha afya na maisha ya wananchi hao?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Mussa Bakar, Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatekeleza Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji iliyoanza mwaka 2006 na awamu ya kwanza ilikamilika mwezi Juni, 2016. Kwa sasa Wizara inatekeleza awamu ya pili ya programu hiyo iliyoanza mwezi Julai, 2016 ambayo inatekelezwa kwa miaka mitano. Mpaka sasa jumla ya miradi 1,469, kati ya miradi 1,810 imekamilika na miradi mingine iliyobaki inaendelea kujengwa na ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika halmashauri zilizokamilisha ujenzi wa miradi ya awamu ya kwanza tayari ujenzi wa miradi ya awamu ya pili unaendelea. Aidha, Serikali inatekeleza miradi ya kimkakati katika maeneo mbalimbali yenye lengo la kutoa huduma kwa wananchi wengi zaidi ili kufikia malengo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Serikali imeweka kipaumbele katika maeneo ambayo ujenzi wa miradi haukukamilika kwenye awamu ya kwanza na maeneo ambayo miradi haikutekelezwa kutokana na kukosa vyanzo vya maji vya uhakika. Serikali inaendelea kutoa elimu ya utunzaji wavyanzo vya maji, ili kuhakikisha vyanzo vilivyopo vinahifadhiwa ili kutoa huduma endelevu, ikiwa ni pamoja na elimu juu ya uvunaji wa maji ya mvua, hasa kwenye maeneo yenye uhaba wa vyanzo vya maji.
MHE. ZAINAB MUSSA BAKAR aliuliza:-

Vitendo vya ukatili kwa watoto vimezidi kuendelea kwa kasi siku hadi siku kama vile ubakaji, kunajisiwa kwa watoto wa kiume na kuingiliwa kinyume na maumbile watoto wa kike:-

Je, ni lini Serikali italeta Muswada wa Sheria Bungeni ili kurekebisha sheria hiyo iwe kali zaidi?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Mussa Bakar, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ujumla sheria zilizopo zinajitosheleza kabisa kuwashughulikia wale wote wanaokutwa na hatia katika makosa ya ubakaji, kunajisi watoto wa kiume na wa kike. Sheria ya Makosa ya Jinai ya mwaka 1985, kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002, imeelekeza adhabu kali kwa yeyote atakayebainika kutenda kosa la kumdhalilisha mtoto au kumbaka mtoto ikiwemo kifungo cha miaka 30.

Hata hivyo, imekuwa vigumu kuwatia hatiani wakosaji hawa kwa sababu wengi wanatoka ndani ya familia na kwa kukosekana ushahidi ikizingatiwa matukio mengi hufanywa na watu walio karibu na familia. Wengi wao wanaogopa kutoa ushahidi kutokana na hofu ya kupoteza mmoja wa wanafamilia kutokana na adhabu za vifungo vya maisha. Aidha, kutokana na mtazamo hasi wa jamii, familia nyingi huhofia kudhalilika na kunyanyapaliwa baada ya kubainika mkosaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inajitahidi kuweka mikakati ya kusaidia kupunguza au kumaliza kabisa tatizo hili, lakini bila ushirikiano katika ngazi zote kuanzia familia haitakuwa rahisi. Serikali inatoa rai kwa jamii kutomaliza masuala ya ukatili wa kijinsia ndani ya familia na badala yake ishirikiane na Serikali ili sheria ichukue mkondo wake.
MHE. ZAINAB MUSSA BAKAR aliuliza:-

Walimu wote nchini wameingia katika Mkataba na Mwajiri ambao pamoja na mambo mengine unaonesha uwepo wa increment kila ifikapo mwezi Julai; tangu iingie madarakani Serikali ya Awamu ya Tano Walimu hawajapewa stahiki hiyo.

Je, ni lini Walimu watalipwa stahiki hiyo kama malimbikizo au haki hiyo imeshapotea?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA - MHE. MWITA M. WAITARA (K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Zainab Mussa Bakar, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikitekeleza miongozo mbalimbali iliyowekwa kuhusu maslahi ya walimu ikiwa ni pamoja na kutoa nyongeza za mwaka za mishahara kulingana na utendaji mzuri wa kazi na kwa kuzingatia tathmini ya utendaji kazi ya kila mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa kanuni E.9(1) ya kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za mwaka 2009 Toleo la Tatu, Nyongeza ya Mwaka ya Mishahara haipaswi kuombwa au kudaiwa na Walimu, bali Serikali ndiyo yenye uamuzi wa kutoa au kutotoa nyongeza hiyo kutokana na Sera za kibajeti kwa mwaka husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Watumishi wa Umma wakiwemo walimu wanastahili kupewa nyongeza ya mwaka ya mshahara iwapo bajeti ya mishahara inaruhusu. Kutokana na ufinyu wa bajeti, nyongeza hiyo haikutolewa kwa watumishi katika mwaka wa fedha 2003/2004, 2004/2005, 2008/2009, 2011/2012, 2012/2013 na 2016/2017. Hata hivyo,
kwa kutambua utendaji mzuri wa kazi, Serikali ya Awamu ya Tano ilitoa nyongeza ya mwaka ya mshahara kwa watumishi wote wakiwemo walimu katika mwaka 2017/2018.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa Serikali itaendelea kutoa nyongeza ya mwaka ya mshahara kwa watumishi wote kadri uwezo wa kulipa utakavyoruhusu. Hata hivyo, walimu hawapaswi kudai malimbikizo ya nyongeza ya mwaka ya mshahara kwa miaka ambayo nyongeza hiyo haikutolewa. Ahsante.
MHE. ZAINABU MUSSA BAKARI aliuliza:-

Yamejitokeza maradhi katika mimea ya mipapai nchini ambayo yanahatarisha kupotea kwa mimea hiyo:-

(a) Je, Serikali imechukua hatua gani ya kuweza kudhibiti maradhi hayo?

(b) Je, kuna utafiti wowote uliofanywa juu ya maradhi hayo ili kugundua yanasababishwa na nini?

(c) Kama bado; je, Serikali haioni kuna hatari ya kupoteza mimea ambao ni muhimu sana?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainabu Mussa Bakari, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara ya Kilimo imefanya utafiti na kugundua kuwa ugonjwa wa Ubwili unga ndio unaoathiri mipapai kwa kiwango kikubwa. Baada ya kugundulika ugonjwa huo, Wizara ya kilimo imechukua hatua za kuudhibiti kwa kutumia viuatilifu vyenye viambata vya croripynfos (udhibiti wa kwenye udongo), Profenophos na Dichlorovosch (udhibiti kwenye majani). Aidha, njia nyingine ya uthibiti ni kwa kutumia mbinu bora za kilimo (Cultural Control) kwa kupanda miche wakati wa kiangazi ili mimea isishambuliwe ikiwa michanga, kupalilia shamba kwa wakati na kung’olea miche iliyoathirika na utumiaji wa wadudu marafiki (Biological Control).

Vilevile Serikali inaendelea kutoa elimu kwa wakulima kuhusu kufuata kanuni bora za kilimo ili kuepuka magonjwa mbalimbali yanayoweza kuathiri mimea ikiwemo mipapai.

(b) Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Kituo cha Utafiti cha TARI-Horti Tengeru imeendelea kufanya utafiti magonjwa na wadudu wanaoathiri mazao ya bustani ikiwemo mipapai. Utafiti huo umegundua kuwa ugonjwa wa Ubwili unga unaoathiri mipapai unaosababishwa na vimelea vya kuvu (fungus) vijulikanavyo kitaalam kama Oidium caricae papaya.

(c) Mheshimiwa Spika, mipapai haiwezi kupotea nchini kwa kuwa tayari njia za kudhibiti magonjwa na wadudu wanaoshambulia mimea hiyo zipo. Aidha, Wizara itaendelea kuwaelimisha wakulima na wadau mbalimbali juu ya udhibiti wa ugonjwa na wadudu wanaoshambulia mimea na mazao ikiwemo mipapai ili kuongeza uzalishaji na tija ya mazao hayo.