Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Raisa Abdalla Mussa (5 total)

MHE. AMINA S. MOLLEL (K.n.y. MHE. RAISA ABDALLAH MUSSA) aliuliza:-
Mfumo wa Elimu ya Tanzania kwa kiasi kikubwa haimwandai mwanafunzi kuwa mbunifu na kuweza kujiajiri:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kubadili mfumo wetu wa elimu ili kuchochea mwanafunzi kuwa mbunifu na kuwa na uwezo wa kujiajiri?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha mtaala wa elimu utakaotoa mafunzo yanayozalisha ajira?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Raisa Abdallah Mussa, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014, Dira ya Elimu ni kuwa na Mtanzania aliyeelimika na mwenye maarifa, stadi, umahiri, uwezo na mtazamo chanya ili kuweza kuchangia katika kuleta maendeleo ya Taifa. Mitaala inayotumika katika elimu ya awali, misingi na sekondari kwa sasa inaweka msisitizo katika kuwajengea uwezo wanafunzi kiutendaji na utumiaji wa maarifa wanayopata darasani.
Mheshimiwa Naibu Spika, mitaala hii ni ya kujenga umahiri ambapo katika tendo la kufundisha na kujifunza mwanafunzi anakuwa ndiye kiini cha somo na mwalimu anawajibika kutumia mbinu shirikishi wakati wa kufundisha. Matumizi ya mbinu shirikishi yanamfanya mwanafunzi ajifunze kwa kina na kujenga udadisi ambao unamwezesha kuwa mbunifu.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, mafunzo kazini kwa Walimu yanafanyika ili kuwajengea uwezo, ikiwemo mafunzo ya KKK yanayozingatia kuwashirikisha wanafunzi kwa njia ya zana za kufundishia na michezo, mafunzo ya sayansi kwa nadharia na vitendo na mbinu shirikishi kwa masomo mengine pamoja na matumizi TEHAMA katika ufundishaji na ujifunzaji. Pia mafunzo kwa Walimu tarajali unazingatia mbinu zinazojenga umahiri.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na maboresho katika mtaala wa elimu msingi na sekondari, Serikali imeandaa mkakati wa kujenga stadi na ubunifu kwa vijana kupitia Mkakati wa Kitaifa wa Kuendeleza Ujuzi (Skills Development Strategy). Kwa utekelezaji wa mkakati huo, katika mwaka 2016/2017, mradi ujulikanao kama Education and Skills for Productive Jobs (ESP) utaanza. Lengo la mradi huo ni kupanua fursa na kuboresha stadi za kazi katika ngazi za ufundi stadi, ufundi na elimu ya juu pamoja na vijana nje ya mfumo rasmi wa elimu kwa kushirikiana na taasisi binafsi, waajiri na sekta binafsi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu kubwa ya mradi italenga kuwapatia wanafunzi ufadhili ili kujipatia fursa za stadi za kazi katika taasisi za mafunzo na pia katika sehemu za kazi (apprenticeship and internship). Aidha, vyuo vikuu mbalimbali nchini vinatekeleza programu za kuwaandaa wahitimu kuweza kujiajiri. Kwa mfano, Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine, Nelson Mandela Arusha na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam vimeanzisha vituo viatamizi (incubators) katika fani mbalimbali. Vilevile Chuo cha Afya na Sayansi Shirikishi cha Muhimbili kitaanza kutoa mafunzo katika fani ya afya na sayansi shirikishi kwa kampasi mpya ya Mlonganzila kuanzia Oktoba, 2016.
MHE. RAISA ABDALLAH MUSSA Aliuliza:-
Ofisi za Balozi za Tanzania hazipo katika hali nzuri na hii inatokana na ukosefu wa upatikanaji wa fedha ambazo zingewezesha kuimarisha Balozi hizi.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha tatizo hili linapatiwa ufumbuzi wa haraka ili kuendana na maendeleo ya dunia?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFIKA MASHARIKI Alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako na kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Raisa Abdallah Mussa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuendelea kukarabati na kujenga majengo ya ofisi na makazi ya watumishi Balozini na imekuwa ikitekeleza jukumu hilo kwa kutumia fedha za bajeti ya maendeleo zinazopangwa kwa kila kipindi cha mwaka wa fedha.
Mheshimiwa Spika, kupitia mpango wa Wizara wa miaka kumi na tano wa ujenzi, ununuzi na ukarabati wa majengo ya ofisi na makazi ya watumishi wa ubalozini ulioanza kutekelezwa mwaka wa fedha 2012/2013, Wizara imefanikiwa kutekeleza miradi mbalimbali kwenye Balozi zetu kama vile kufanikisha ujenzi wa jengo la Ubalozi wa Tanzania - New Delhi (India); ununuzi wa jengo la Ofisi ya Ubalozi Tanzania - Washington D.C (Marekani); ununuzi wa jengo la Ofisi ya Ubalozi wa Tanzania - New York (Marekani); ununuzi wa jengo la Ofisi na makazi ya Balozi, Ubalozi wa Tanzania - Paris (Ufaransa); ukarabati wa makazi ya Balozi, Ubalozi wa Tanzania - Nairobi (Kenya) na ukarabati wa makazi ya Balozi, Ubalozi wa Tanzania - Tokyo (Japan).
Kwa mwaka wa fedha 2016/2017, Wizara itakamilisha ukarabati wa jengo la ghorofa tisa la ofisi na makazi lililopo Ubalozi wa Tanzania Maputo (Msumbiji); ukarabati wa makazi ya Balozi na nyumba za watumishi zilizopo Ubalozi wa Tanzania Stockholm (Sweden); na ukarabati wa jengo la Ofisi na makazi ya Ubalozi yaliyopo Khartoum (Sudan).
Mheshimiwa Spika, hivi sasa Wizara inaandaa mpango mwingine wa miaka kumi na tano wa ujenzi, ununuzi na ukarabati wa majengo ya ofisi na makazi ya watumishi Ubalozini utakaoanza kutekelezwa mwaka 2017/2018.
Mheshimiwa Spika, baadhi ya miradi itakayotekelezwa ni ukarabati wa jengo la ofisi na makazi ya watumishi kwenye Balozi za Tanzania Harare (Zimbabwe); Kampala (Uganda); Beijing (China); Pretoria (Afrika Kusini); na Cairo (Misri); ukarabati wa nyumba za Ubalozi zilizopo kwenye Ubalozi wa Tanzania Lilongwe (Malawi); Kinshasa (DRC); ukarabati wa jengo la zamani la Ofisi ya Ubalozi lililopo Washington DC; ukarabati wa miundombinu ya Chuo cha Diplomasia kilichopo Kurasini na ujenzi wa Ubalozi wa Tanzania - Addis Ababa (Ethiopia) na Ofisi ya Ubalozi wa Tanzania - Muscat (Oman).
Mheshimiwa Spika, mikakati ya kutekeleza mpango huu ni kuendelea kutumia bajeti ya maendeleo ya Serikali, kuishirikisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kama vile Taasisi ya Miradi ya Maendeleo ya Miundombinu na kwa kutumia utaratibu wa karadha katika kutoa mikopo ya kutekeleza miradi ya maendeleo Ubalozini kwenye nchi za uwakilishi ambapo utaratibu huo unatumika.
MHE. RAISA ABDALLAH MUSSA aliuliza:-
Wapo wanawake ambao wamefungwa kwenye magerezani wakiwa na watoto wachanga/wadogo ambao bado wanahitaji uangalizi au huduma za mama zao.
(a) Je, Serikali imejipanga vipi katika kuwanusuru watoto hao ambao hawana hatia?
(b) Je, Serikali haioni kuwa inavunja haki za binadamu kwa kuwaweka gerezani watoto hao wasio na makosa?
(c) Je, Serikali inaweza kulipa Bunge takwimu za wanawake waliokinzana na sheria na wamefungwa kwa miaka mitano iliyopita?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Raisa Abdallah Mussa, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b), na (c) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli yapo mazingira ambayo watoto wadogo na watoto wachanga huingia gerezani wakiwa wameambatana na mama zao kutokana na mama zao kufungwa gerezani au kuingia mahabusu, ama mama zao kuingia wakiwa wajawazito na baadae kujifungua gerezani. Watoto hao hupokelewa na kuruhusiwa kuwepo gerezani na mama zao kwa mujibu wa Kifungu cha 144(1) cha Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 na Kanuni 728 ya Kanuni za Kudumu za Jeshi la Magereza za mwaka 2003.
Mheshimiwa Mwenyekiti, msingi wa kuruhusu watoto kuwa na mama zao magerezani unatokana na kuzingatia maslahi ya mtoto kama inavyohimizwa katika Mkataba wa Kimataifa wa Haki ya Mtoto (The Convention of Rights of the Child) na mikataba mbalimbali ya kikanda inayohusiana na haki za mtoto. Kwa kuwa mtoto mchanga huwa bado ananyonya, hivyo himaya stahiki ya malezi na makuzi ya awali huwa ni ya mama yake. Hata hivyo Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 imetoa nafasi kwa mtoto ambae mzazi wake wake yuko katika ukinzani wa sheria kuweza kupata malezi mbadala ambayo yanazingatia mahitaji yote ya mtoto kama ilivyo kwa mtoto yeyote yule chini ya uangalizi wa uongozi wa magereza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2012 hadi mwaka 2016, idadi ya wanawake waliofungwa magerezani kutokana na kukinzana na sheria ilikuwa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2012 ni 364, mwaka 2013 ni 321, mwaka 2014 ni 373, mwaka 2015 walikuwa ni 334 na mwaka 2016 ni 616. Hivyo kufanya jumla yake wote kuwa ni 2008.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN (K.n.y. MHE. RAISA ABDALLAH MUSSA) aliuliza:-
Kutokana na umuhimu wa misitu hapa nchini na kwa kuzingatia kuwa theluthi moja ya ardhi ya Tanzania ni misitu; na kwa kuwa, Serikali ina Chuo kimoja tu cha Misitu cha Olmotonyi ambacho sasa kinakaribia kufikisha karne moja tangu kianzishwe:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha vyuo vingine vitakavyotoa taaluma zaidi ya misitu kwa Watanzania?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Raisa Abdallah Mussa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania Bara ina eneo la takribani hekta milioni 48 za misitu sawa na 55% ya eneo lote la nchi kavu lipatalo hekta milioni 88.1. Kwa mujibu wa viwango vinavyoratibiwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo, inakadiriwa kuwa Afisa Misitu mmoja husimamia wastani wa hekta 5,000 za misitu hivyo, kwa ukubwa wa eneo la misitu katika nchi yetu kiasi cha wataalam wa misitu 9,600 wenye jukumu la kusimamia misitu moja kwa moja ukiondoa watawala na watumishi wa viwandani na kadhalika wanahitajika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina vyuo vitatu vinavyotoa taaluma ya misitu. Vyuo hivyo ni pamoja na Chuo Kikuu cha Sokoine kilichoko Morogoro ambacho kinatoa Shahada ya Kwanza, Shahada ya Uzamili na Shahada ya Uzamivu katika Fani ya Misitu; Chuo cha Viwanda vya Misitu kilichopo Moshi, ambacho kinatoa Astashahada ya Teknolojia ya Viwanda vya Misitu na Astashahada ya Teknolojia ya Viwanda vya Misitu na Chuo cha Misitu kilichopo Olmotonyi, ambacho kinazungumziwa na Mheshimiwa Mbunge muuliza swali, nacho kinatoa mafunzo ya Astashahada na Stashahada ya Misitu.
Mheshimiwa Naibu Spika, bila kujali vyuo walivyosoma, taaluma mahsusi ya misitu na ngazi za shahada walizohitimu, katika kipindi cha miaka 10 vyuo nilivyovitaja hapo juu vimeweza kuzalisha jumla ya wataalam 3,500 ambao wameingia kwenye soko la ajira. Kufikia mwaka 2020, Serikali inao mpango wa kuongeza udahili, mara mbili ya viwango vya sasa, katika vyuo vilivyopo kwa kutekeleza, pamoja na mambo mengine, uboreshaji miundombinu ya kufundishia, kuongeza ubora na idadi ya wakufunzi na vifaa vya kufundishia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, mipango ya Serikali inaonesha uwezekano mkubwa wa kufikiwa kwa malengo ya kupatikana kwa wataalam wa kutosha kwa idadi na uweledi, kwa sasa Serikali haioni umuhimu wa kuongeza vyuo vingine kwa madhumuni hayo.
MHE. RAISA ABDALLAH MUSSA aliuliza:-
Wapo wanawake ambao wamefungwa kwenye magerezani wakiwa na watoto wachanga/wadogo ambao bado wanahitaji uangalizi au huduma za mama zao.
(a) Je, Serikali imejipanga vipi katika kuwanusuru watoto hao ambao hawana hatia?
(b) Je, Serikali haioni kuwa inavunja haki za binadamu kwa kuwaweka gerezani watoto hao wasio na makosa?
(c) Je, Serikali inaweza kulipa Bunge takwimu za wanawake waliokinzana na sheria na wamefungwa kwa miaka mitano iliyopita?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Raisa Abdallah Mussa, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b), na (c) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli yapo mazingira ambayo watoto wadogo na watoto wachanga huingia gerezani wakiwa wameambatana na mama zao kutokana na mama zao kufungwa gerezani au kuingia mahabusu, ama mama zao kuingia wakiwa wajawazito na baadae kujifungua gerezani. Watoto hao hupokelewa na kuruhusiwa kuwepo gerezani na mama zao kwa mujibu wa Kifungu cha 144(1) cha Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 na Kanuni 728 ya Kanuni za Kudumu za Jeshi la Magereza za mwaka 2003.
Mheshimiwa Mwenyekiti, msingi wa kuruhusu watoto kuwa na mama zao magerezani unatokana na kuzingatia maslahi ya mtoto kama inavyohimizwa katika Mkataba wa Kimataifa wa Haki ya Mtoto (The Convention of Rights of the Child) na mikataba mbalimbali ya kikanda inayohusiana na haki za mtoto. Kwa kuwa mtoto mchanga huwa bado ananyonya, hivyo himaya stahiki ya malezi na makuzi ya awali huwa ni ya mama yake. Hata hivyo Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 imetoa nafasi kwa mtoto ambae mzazi wake wake yuko katika ukinzani wa sheria kuweza kupata malezi mbadala ambayo yanazingatia mahitaji yote ya mtoto kama ilivyo kwa mtoto yeyote yule chini ya uangalizi wa uongozi wa magereza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2012 hadi mwaka 2016, idadi ya wanawake waliofungwa magerezani kutokana na kukinzana na sheria ilikuwa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2012 ni 364, mwaka 2013 ni 321, mwaka 2014 ni 373, mwaka 2015 walikuwa ni 334 na mwaka 2016 ni 616. Hivyo kufanya jumla yake wote kuwa ni 2008.